Search This Blog

Sunday 19 June 2022

USINIBANIE - 2

 





    Simulizi : Usinibanie

    Sehemu Ya Pili (2)





    HASIRA zilinipanda kichwani nikajiona nadhalilika mwanamume mimi, niliona wazi kuwa nakosewa adabu. "Nimchape vibao nini?" Nilijikuta nikiwaza kwa haraka haraka.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Bahati nzuri akaingia mmojawapo wa watumishi wa mule ndani,

    cha kushangaza Tausi hakuufurahia ujio ule. Akamdakia,

    "sihitaji usumbufu, nina shauri muhimu na Hoza. Waambie na

    wenzio!"



    Yule mtumishi akatoka harakaharaka na kuishia zake

    nje. Nikashusha pumzi ndefu kisha nikatulia kwa muda ili kuipa

    nafasi hekima ichukue mkondo wake. Akili ilipotulia

    nikamjibu. "Mimi sio mtunzi wa mashairi, huwa naandika

    kilichopo moyoni wangu. Samahani kama nimekukwaza" nilimjibu kwa upole lakini kwa chuki kubwa.



    Niliojiona nimedharaulika sana mwanamume mimi, lakini Tausi

    hakuonyesha kujali kabisa. "Unaweza kuniambia

    uliyemwandikia?" aliniuliza akiniangalia usoni.



    Mapigo ya moyo yalibadilika ghafla. Laiti kama angetokea

    daktari pale na kunipima presha, kwa hakika ningepelekwa

    wodi ya wagonjwa mahututi kwa jinsi mapigo hayo

    yalivyoongezeka.



    Huyu mtoto sijui vipi? Anaongea na mwanamume akimtazama

    usoni. Sijui kaitowa wapi tabia hii, ila kwa mimi

    sikumshangaa kutokana na kusafiri nchi kadhaa. Ni tabia za

    kizungu!



    Nilishusha pumzi ndefu nikamkazia macho na kumjibu kwa upole lakini kwa kujiamini. "Sidhani kama itasaidia nikikwambia Tausi, niliyemwandikia ameshayasoma na anajijua ila sitamruhusu anijibu kwa maneno kwa kuwa hataweza

    kunitamkia!"



    Mchezo ukageuka ghafla, nikamwona Tausi anapoteza ujasiri

    wake. Macho yake yalianza kubadilika rangi na kuwa mekundu

    yakifunikwa na utando wa machozi. Nikaacha kumtazama kwa

    kuwa alishindwa kuendelea kuangaliana na mimi wakati

    nilitaka aniangalie nikimpa vidonge vyake.



    Nikaendelea kumwambia "Nahisi ana mwingine ampendaye, moyo unaniuma lakini nafurahi kwa kuwa ameshazijua hisia zangu kwake. Mara zote nikimwangalia, natamani nimkumbatie lakini sidhani kama nitakuja kupata ruhusa yake!" .



    Tausi akanikatisha "Nenda tafadhali Hoza, naomba uniache

    nipumzike."



    Kwa sauti aliyoitoa nilijihisi mwili unasisimkwa

    na kupoteza ujasiri wake. Nikamwangalia usoni, hakuwa akionyesha kuwa ananiambia niondoke kwa nia mbaya, ila maneno yangu yalikuwa yakimchoma. Akageuka na kuanza kuondoka akiniacha nimesimama.



    Nilijikaza mtoto wa kiume nikamuita. "Tausi!"



    Akasimama bila kunigeukia, "unasemaje?"



    "Nahitaji bado kuongea na wewe, ukipata muda naomba unifikirie!"



    Tausi akageuka kuniangalia. Akasimama kwa muda akinitumbulia macho. Baada ya kimya kifupi, mrembo Tausi alishusha pumzi ndefu akaniuliza kwa sauti yake laini. "Huogopi?"



    "Naamini sifanyi kosa, sidhani kama natakiwa kuogopa!"

    nilimjibu kwa kujiamini.



    Tausi alitabasamu, kisha akageuka na kunijibu akiwa

    anaondoka. "Nishakuelewa unachotaka kuniambia."



    Akaishia na kuniacha nimesimama kama sanamu ya kwenye duka la nguo kasoro sikutoa pozi. Mwanamume nikatoka taratiiibu nikiwapita watumishi na wambeya

    wengine waliokuwa wakisubiri nje ili waniulize kuwa

    nimeitiwa nini na Tausi.



    Kweli watu wanapenda wenzao wakipatwa na matatizo,

    walifurahi sana nilipowaambia kuwa niliitwa kusemwa kutokana

    na kuchelewa kufanya usafi.



    Nilipotoka pale nikaanza kufanya usafi haraka haraka, kisha

    nikarudi kibandani kwangu na kujifungia ili nipate

    kuutafakari mwenendo mzima wa maongezi yangu na Tausi.



    Nilihisi mambo kama vile yameharibika, mara nyingi msichana

    akishajua kama umemzimia inakuwa ngumu sana kumnasa kama yeye hakutaki. Nilijiona kuwa natakiwa kufanya uamuzi wa hatari sana na wa haraka, nilijua wazi kuwa Tausi hawezi

    kuamua kunikubali hata kama ananipenda kutokana na hali

    yangu.



    Inabidi nifosi goli! Hakika Tausi alikuwa ameanza kuuogopa

    ujasiri wangu, nilimuona kuwa katikisika hivyo sikutaka

    kumpa nafasi ya kuutafuta tena ujasiri wake ulioyeyuka.



    Usiku ulivyoingia, nilienda moja kwa moja hadi dirishani

    kwake na karatasi langu mkononi, wakati huo hakuwa ameingia

    chumbani kwake, nikampenyezea. Karatasi hiyo niliiandika

    hivi....



    ‘Nitaingia humu chumbani usiku sana tupige stori’

    Karatasi lile lilipeperukia pembeni kidogo ya kitanda,

    karibu na dirishani. Nilitulia pale nikisubiri kumwona

    atalichukuliaje suala lile.



    Tausi alipoingia chumbani, akalikuta lile karatasi. Moja kwa

    moja akaliendea na kuliokota, akawa analisoma. Nilimuona

    akiwa na hofu kubwa akiangaza angaza huku na kule ili ajue

    karatasi lile limeingiaje mule ndani.



    Alikuja hadi dirishani, nikainama chini ili asinione.

    Akaanza kulikagua, alijisahau kuwa dirisha la kuzuia mbu

    halikuwa limefungwa vizuri nami nilitumia upenyo huo

    kupenyeza lile karatasi kisha nikalifunga.



    Baada ya kushindwa kujua karatasi lile limeingiaje akabaki

    pale kitandani akiwaza. Sikujua alikuwa akiwaza nini.

    Nilikuwa nataka kuusoma mwenendo wake, kama angetoa taarifa kwa walinzi au angeuchuna.



    Kuuchuna kwake kulimaanisha kuwa yuko tayari kuhifadhi siri.

    Lakini vile vile yawezekana kuwa amekaa kimya kwa kujua

    kwamba sina uwezo wa kufanya nilichoandika.



    Ilipofika saa nane kasoro, myumba yote ilikuwa kimya. Ni

    mbwa na walinzi tu waliokuwa wakiranda randa. Inaelekea hata

    wale mbwa walikuwa wananishangaa kutokana na mizunguko yangu ya usiku kwa usiku, wangekuwa binadamu wamgeshatoa umbeya.



    Sijui mapenzi yana nini? Nilikuwa na ujasiri wa ajabu kuweza

    kufikiria kufanya lile nililokusudia. Nilimchungulia Tausi,

    hakuwa amelala. Ananisubiri? Mwanaume nikaanza kunyata

    nikiizunguka nyumba, nikaliendea bomba linalopandisha maji

    kwenye tenki.



    Nikaanza kulikwea taratibu hadi juu. Juu ya nyumba ya Mzee

    Nurdin kuna sehemu ya kupumzikia, pia kuna mlango ambao

    nilipoufungua kitasa chake kwa kutumia waya nilikutana na

    sehemu yenye gazi.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Niliteremka na ngazi taratibu nikatokea kwenye chumba kimoja

    chenye giza nene. Nilitulia kwanza ili macho yangu yazoee

    lile giza. Japo nilikuwa nina tochi ndogo, lakini huwezi

    kuwasha katika mazingira yale.



    Macho yalipolizoea giza, niliona sehemu ulipo mlango mdogo.

    Nikanyata kuulekea huo mlango, nilipotoka nikakutana na

    korido ndefu ambapo mbele yake kulikuwa na mlango mkubwa

    sana. Hakukuwa na mlango mwingine wowote ulioonekana katika mwanga ule hafifu.



    Nilipotazama kwa makini niliona dalili za kuwepo mlango

    mwingine mdogo mita chache kutoka pale niliposimama.

    Nikatabasamu! "Huyu mzee ni mjanja sana!" nilijisemea

    moyoni.Unajua katika mazingira ya kawaida ukitokea tu lazima

    mawazo yote yatakuwa kwenye mlango ule mkubwa na ndipo huwa kunawekwa ulinzi mkubwa.



    Nilicheza na kitasa cha kale kamlango nikaufungua,

    nikatokeza kwenye kikorido kifupi chenye milango minne

    tofauti. Nikajua ni vyumba vya kulala. Nilianza kupiga

    hesabu kutokana na madirisha yalivyokaa kwa nje nikakihisi

    chumba cha Tausi. Nikaanza kutembea nikinyata kuuelekea

    mlango niliouhisi kuwa ni wa chumba cha Tausi.



    Hapo sasa ndio akili ikaanza kunirudia. Wasiwasi ulinijaa,

    jasho jembamba likaanza kunitoka lakini nikajipa moyo kuwa

    hata nikishtukiwa poa tu, nitamwambia mkuu kuwa nilikuwa

    naichunguza ile nyumba.



    Nilipougusa mlango wa Tausi, nikagundua kuwa uko wazi.

    Nikausukuma polepole na kuchungulia, Tausi alikuwa amepitiwa na usingizi akiwa kakaa kwenye kitanda huku amejiegemeza ukutani. Niliingia taratibu na kujiegemeza pembeni ya mlango nikimwangalia.



    Mapigo ya moyo wangu yalienda kwa kasi ya ajabu, nilikuwa

    sijui nifanyeje. Kwa akili ya haraka haraka nilijua kuwa

    endapo angeshtuka, cha kwanza angepiga kelele. Nikajivua

    kamba ya urembo ambayo nilikuwa napenda kuivaa mkononi,

    nikaidondosha chini kisha nikaondoka.



    Ilipofika asubuhi niliendelea na taratibu zangu kama

    kawaida. Nilifanya kama vile hakikutokea kitu usiku wake.

    Nilipomaliza usafi nikakaa kwenye eneo langu la kujidai na

    paka wa Tausi. Kila nilipochungulia pale dirishani kwenye

    eneo la Tausi, sikumuoana Tausi.



    Nilianza kuingiwa na wasiwasi. Baada ya muda kidogo

    nilimuona Tausi akiwa anajongea mbele yangu. Niliingiwa na

    hofu sana lakini nilijikaza kwa kutabasamu ili kuficha hofu

    niliyokuwa nayo. "Hivi wewe Hoza, una akili kweli?"

    Alinianza kwa swali la kebehi.



    "Sina akili hata moja Tausi," nilimjibu bila kusita hata

    nukta. Tausi alikaa kimya kwa muda kabla ya kutoa kicheko

    kilichoambatana na mhemo.



    "Ulimtuma nani kuleta hii kamba yako?"



    "Niliileta mwenyewe!"



    "Thubutuuu!" Tausi alisema huku akicheka kwa kebehi

    akinirushia kamba yangu. Niliiona kama bahati ya mtende,

    nikamwambia kuwa kama anabisha aende nayo, usiku nitaifuata

    kama nilivyoileta. Naye eti akakubali, sasa sijui nae

    alikuwa na hamu tuonane usiku au alikuwa anabisha kiukweli

    ukweli.



    Malaika ’mzima jua’ akafanya kazi yake, giza likatawala

    katika uso wa dunia na watu katika himaya ya Mzee Nurdin

    wakawa wamelala. Kitu ambacho nilikuwa nimekigundua wakati nikiongea na Tausi asubuhi ni kwamba alikuwa ameondoka kabisa ile hali ya kuwa mimi ni mfagizi wao. Alikuwa akinichukulia kama mwanamume anayemfukuzia.



    Jambo hilo lilinipa mzuka sana, nikajiona nimepiga hatua kubwa sana kuelekea kumpata Tausi.



    Usiku ulipoingia, mwanamume nikapitia njia yangu ile ile.

    Ila kabla sijaianza safari yangu nilimchungulia Tausi

    nikamkuta yuko macho anasubiri aone ’uongo wangu’.



    Nilipofika mlangoni, sikuhangaika na kuufungua mlango wake,

    niligonga taratibu. Mlango ukafunguliwa, tukakutana uso kwa

    uso na Tausi. Tausi hakuweza kuuficha mshangao wake, nami

    nilijihisi kuwa mzunguko wa damu umeongezeka kasi mara dufu.





    Tukabaki tunatazamana kwa muda.



    Ghalfa akili ikamrudia Tausi akanivutia kwa nguvu ndani.

    "Una hatari sana wewe! Umeingiaje?" Nilikuwa natabasamu tu

    nikimuangalia Tausi. Alikuwa kavalia suruari ya kulalia na

    shati lake vilivyomkaa sawa sawa. Nikamuuliza kimoyomoyo,

    "Mbona hujanivalia lile gauni lako la hudhurungi

    linaloonyesha yaliyomo?"



    Tausi alibaki kimya akinishangaa, nami nilibaki nikimtazama

    usoni. Nadhani alishangaa nilivyovaa, nilivaa suruali ya

    ’traksuti’ nyeupe, juu nilivaa fulana nyepesi nyeupe ya

    mikono mirefu ambayo ilionyesha mabonde na milima ya mwili

    wangu.



    Nilikuwa msafi haswa tena wa kukaribishwa kitandani.

    Tulikaa kimya kwa muda tukitazamana, sio yeye wala mimi

    ambaye alipata kauli ya kutamka. Taratibu tabasamu lilianza

    kutoweka usoni kwa Tausi, nami nikafunika meno yangu

    yaliyopangana mithili ya punje za mahindi.



    Nilishusha macho yangu kuitazama midomo yake nikahisi kuwa

    inahitaji kitu fulani. Nikasogea hatua moja mbele, tukawa

    tunatazamana kwa ukaribu sana. Nikaupeleka mkono wangu

    kumshika shavuni, nikimpapasa. Midomo yetu ikakutana kisha

    ndimi zikasabahiana.



    Niliuzungusha mkono wangu kiunoni kwake, nikauhisi mwili

    wake ukitetemeka, ukivaibreti kama uliopigwa na shoti ya

    umeme. Miili yetu ilikuwa ikibadilishana joto na kuifanya

    akili yangu ishindwe kufikiri wala kuiona hatari ya mimi

    kuwa mule ndani usiku ule.



    Ghafla Tausi akanisukuma na kujitoa kwenye mikono yangu,

    alibaki akinitazama huku anatweta. Akaniambia kwa sauti

    laini iliyojaa mihemo. "Ondoka Hoza!"



    Nilimwangalia kwa sekunde kadhaa, kisha nikageuka na kuanza

    kuondoka. Tausi akanishika bega nikageuka na kumwangalia.



    "Umekasirika?"



    Sikumjibu kitu, nilibaki nikimwangalia tu kwa

    upole, akanivuta na kunipiga busu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nami sikufanya ajizi nikampelekea, tena zima-zima. Baada ya

    muda tukawa tunatazamana. "Ahsante kwa busu lako, mimi

    naenda!" Nilimwambia Tausi nikigeuza na kuanza kuondoka.



    Wakati navuka mlango nikamsikia akisema kwa sauti ya

    kunong’ona "I love you." Nikarudi ndani. "Unasema?" Akabaki

    akiniangalia huku akitabasamu. "Toka hapa! Kama hujasikia

    basi!" Nilicheka kidogo na kutoka kupitia njia yangu ile

    ile.



    *********



    Naukumbuka usiku ule, kwa kweli sikupata usingizi wa moja

    kwa moja. Na hata nilipopata usingizi ndoto zilikuwa ni

    kuhusu mabusu ya Tausi tu.



    Najua unaweza kuniona bwege kwa kutofanya kweli katika usiku ule, lakini ngoja nikudokolee siri za wanawake hasa warembo kama Tausi.



    Hutakiwi kuwa na papara, kuuteka moyo wa Tausi ni kitu

    kikubwa kuliko kufanya nae mapenzi. Wanaume wengi hudhania kufanya mapenzi ndiyo uhakika kuwa unapendwa. Mtachekwa!



    Siku iliyofuatia Mzee Nurdin, baba yake Tausi alirejea toka

    safari yake akiwa na msafara wake kamili. Ulinzi

    uliimarishwa mara dufu na sheria zikaanza kuzingatiwa,

    ilikuwa ngumu sana.



    Zilipita siku kadhaa bila ya mimi kumuona Tausi, moyo wangu uliniuma sana.Nilihisi kuwa hata yeye alikuwa na wakati mgumu kama mimi.



    Mawazo kuhusu kazi iliyonipeleka pale hayakuweza kabisa

    kuitoa akili yangu katika fikra juu ya Tausi. Nikaanza na

    kuingiwa na woga wa kuharibu kazi, nikakumbuka mambo ya

    Ngoswe katika kitabu cha ’Penzi Kitovu cha Uzembe’.



    Lakini nilijipa moyo kutokana na uwezo wangu mkubwa wa

    kuutumia upungufu wangu kama njia ya kupatia ushindi. Kila

    mpango nilioupanga sikuona kama ungeleta manufaa au katika

    kazi yangu ya kumpeleleza Mzee Nurdin ama katika kumsogeza

    karibu tabibu wa moyo wangu, Tausi.



    Siku moja baada ya kufikiria kwa kina, nikaamua kufanya

    jambo la hatari, nikaamua kuwa liwalo na liwe. Lazima

    nionane na Tausi! Siku hiyo niliamua kuwa katika hali ya

    kivita haswa, nilivaa pajama jeusi, fulana nyeusi na raba

    nyeusi.



    Niliamua kuwa mtu wa gizani. Niliamua pia kuifanya

    safari hiyo mapema sana mara baada ya giza kuingia.

    Nilitembea taratibu kuielekea njia yangu ya kuingilia ndani

    kwa Mzee Nurdin.



    Nilipanda taratibu kwenye bomba kuelekea

    juu. Nilipofika tu juu nikashtushwa na sauti ya miguu

    inayotembea, nikatulia na kuangaza katika giza lile.

    Nilimuona mlinzi mmoja akirandaranda huku mkononi amekamata bunduki.



    Nikatulia kwanza!





    Yule mlinzi alizunguka zunguka kisha akawa anaelekea kwa mbele ya sehemu ile ya kupumzikia ambayo ukisimama unaona hadi getini, akawa kanipa mgongo.



    Nilinyata kwa haraka hadi kwenye kigeti cha kuingilia ndani,

    nikakuta kimeegeshwa tu. Nikakifungua taratibu na kuanza

    kushusha ngazi kwa tahadhari kubwa. Sikufika moja kwa moja

    kwenye kale kachumba ka giza, niliishia kwenye gazi nikawa

    nakikagua kwa macho kwa kukichungulia. Nikakiona kuwa ni

    kitupu. Nikasimama kulitazama lango kubwa, safari hii

    lilikuwa wazi.



    Nilimuona mlinzi mmoja akiwa kasimama sambamba na ukuta

    karibu na lango lile. Pia kutoka pale niliweza kuwaona

    watumishi wa ndani wakizunguka huku na kule. Nikabaki

    nikipiga hesabu za kuweza kuufikia ule mlango mdogo ambao

    huwa ninapitia. Tena kuufikia bila ya kuonekana na yule

    mlinzi na watumishi.



    Kwa kuangalia zile pilika pilika za watumishi nikajua kuwa

    yalikuwa ni maandalizi ya chakula cha jioni, kwa hiyo nikawa

    nasubiri kuwaona Mzee Nurdin na familia yake wakipita. Baada

    ya muda pilika zilitulia, nikamuona Tausi akipita.



    Nilijikuta nikitabasamu! Kisha mama yake na Mzee Nurdin nao

    wakipita.



    Macho ya mlinzi yalikuwa yakiwasindikiza, nikapita haraka kuuendea mlango wangu. Kuugusa ukawa umefungwa!



    Nikarudi spidi na kujituliza pale gizani nikitafakari cha kufanya.

    Akili moja iliniambia nirudi, nyingine iliniambia nisonge

    mbele.



    Wakati nimekaa nafikiria cha kufanya, niliuhisi ubaridi

    fulani kwenye ule ukuta niliouegemea ambao ni tofauti na

    ubaridi wa ukuta wa kawaida. Nikajaribu kuugonga-gonga.



    Ulikuwa ni ukuta wa chuma!



    Nikatoa tochi ndogo yenye mwanga hafifu na kuanza kuukagua

    ukuta ule wa chuma. Nikaviona vitufe kadhaa kama vya lifti

    za kwenye majengo marefu. Baada ya kuvisoma kwa muda

    nikagundua kuwa ule ni mlango, nikajawa na shauku ya kuujua

    ni mlango wa kuelekea wapi?



    Nikabonyeza kitufe cha kufungulia, lango likafunguka. Mbele

    kulikuwa na ngazi kadhaa, nikashuka taratibu kuzifuata hizo

    ngazi. Chini nikakutana na korido ndefu sana, nikatulia kwa

    muda ili kuona kama kuna harakati zozote. Kulikuwa kimya

    mno!



    Nikaanza kutembea kuifuata ile korido kwa uangalifu. Baada

    ya kutembea kwa takribani dakika tano nikatokea kwenye

    chumba chenye milango mitatu tofauti. Mmoja ulikuwa ni

    mkubwa, miwili ilikuwa ni midogo.



    Nikaanza kuvichunguza vitasa, nikauhisi mlango mmojawapo

    kati ya ile midogo miwili una hadhi ya juu na haufunguliwi

    mara kwa mara. Nikauchagua huo, nikaukorokochoa na funguo

    zangu malaya, ukafunguka. Nikaingia kwa tahadhari kubwa,

    nikakutana na ngazi zinazopandisha juu ambako nilikikuta

    choo.



    Kilionekana kuwa ni choo cha mtu binafsi, na kilikuwa

    kimefungwa kwa ndani. Nikakifungua na kutoka nje, nikakutana

    na sebule kubwa ya kifahari. Kwa kuiangalia haraka haraka

    ile sebule haikuwa ngeni kwangu! Nikaanza kuvuta kumbukumbu.



    Jibu nililolipata sikuweza kuliamini, ni ofisini kwa Mzee

    Nurdin! Sikuamini kwa sababu kutoka ofisini kwa Mzee Nurdin hadi nyumbani kwake ni mwendo wa zaidi ya robo saa kwa gari!



    Inakuwaje? Nilianza kuikagua taratibu sebule ile kwa macho,

    nikahakikisha kuwa ndio yenyewe. Nikaanza kufanya upekuzi wa nyaraka mbalimbali pale sebuleni na ndani ya ofisi yake.



    Nilitoa kopi nyaraka kadhaa ambazo nilidhani kuwa

    zingenisaidia kwa upelelezi wangu, pia nilinyonya mafaili

    kadhaa toka kwenye kompyuta yake baada ya kufanikiwa

    kuzibomoa namba zake za siri. Nikayaweka kwenye flash diski

    yangu.



    Wakati najiandaa kuondoka nilipata wazo ambalo lilinifanya

    niingiwe na hofu kwa sekunde kadhaa. Nikaangaza kona zote za

    ofisi ile, nikakikuta nilichokitarajia. Kamera! Mambo yote

    niliyokuwa nikiyafanya yalikuwa yakirekodiwa na kamera ile!

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilifikiria njia ya kufanya bila jibu.



    Niliwaza kama kuna watu walikuwa wanafuatilia ina maana hadi pale nilishajulikana na sikuwa na ujanja wa kufanya lolote!



    Akili ikaanza kuzunguka nikipanga na kupangua namna ya

    kujinasua bila kuharibu uwepo wangu pale nyumbani kwa Mzee

    Nurdin.



    Nilijua nikiharibu tu na Tausi nimemkosa. Nikaanza kukosa

    raha. Nilishusha pumzi ndefu, nilipopata wazo. Nikarudi

    kwenye kompyuta za ofisini kwa Mzee Nurdin, nikaanza

    kuifungua moja baada ya nyingine.



    Hatimaye, nilifanikiwa kupata inayohifadhi rekodi

    zinazochukuliwa na zile kamera za ulinzi. Nikaipapachua na

    kukitoa kisehemu cha kuhifadhia kumbukumbu kisha nikaizima.



    Niliporidhika kuwa kila kitu kiko sawa nikaanza safari yangu

    ya kurudi huku nikiwa na mawazo mawili mawili, nipite kwa

    Tausi ama la! Nilifanikiwa kurudi hadi kwenye kale ka chumba

    ka giza, nilibaki pale nikipiga hesabu za kutoka.



    Kutokana na vitu nilivyobeba haikuwa busara kwenda kwa

    Tausi. Tatizo kubwa alikuwa yule mlinzi mwenye bunduki

    anayelinda sehemu ya kupumzikia iliyo juu ya nyumba ya Mzee

    Nurdin.



    Nilikuwa najaribu kupiga hesabu ili kwa vyovyote ilivyo

    niepuke mapambano, japo najiamini kwa ufiti nilionao haikuwa

    ni jambo jema kutoa ujumbe kuwa umetokea uvamizi.



    Nilianza kunyata taratibu nikizipanda ngazi za kuelekea juu,

    hadi nilipolikaribia geti. Nikamuona yule mlinzi ametulia

    katikati ya geti. Nikakaa pale ngazini nikimkodolea macho

    yule mlinzi mnoko ambaye hakuwa na dalili yeyote ya kuondoka getini.



    Zilipita takribani saa mbili ndipo mlinzi yule alipotoka

    pale getini kufanya mzunguko mdogo. Nikaitumia fursa hiyo

    kutoka kwa haraka ila kwa tahadhari kubwa. Nikatembea na

    ukuta, nikalidandia bomba na kuseleleka kushuka chini bila

    kufanya kelele.



    Nikanyata na kurudi kwenye kibanda changu nnachoishi.

    Nilikuwa nimepiga hatua moja kubwa sana! Nilitumia usiku ule

    kuzipitia nyaraka zote nilizozitoa kopi kule ofisini kwa

    Mzee Nurdin, nilivinakili vitu muhimu nilivyovitaka kisha

    makaratasi yale nikayaweka kwenye sufuria ndogo na

    kuyaunguza.



    Nilibaki na flash diski na kile kiboksi cha kuhifadhia

    kumbukumbu cha kwenye kompyuta. Inabidi hivi vifike kwa

    mkuu!



    Siku iliyofuatia kulikuwa na pilika zisizo za kawaida hivyo

    kila mtu akawa anajiuliza kuwa ni nini kimetokea ila jioni

    yake tukapata taarifa kuwa wasaidizi wa Mzee Nurdin

    wanashikiliwa na polisi.



    Wakati kila mtu akitafakari kuhusu mambo yale, ilikuja gari

    la polisi, tukakusanywa wafanyakazi wote kasoro walinzi.

    Akilini nilijua kuwa ni nini kinaendelea. Tukapelekwa hadi

    kituo cha polisi ambacho sijawahi kukijua kabla kwa

    mahojiano, akawa anachukuliwa mmoja mmoja.



    Ilipofika zamu yangu kupelekwa nilishangaa kujikuta uso kwa

    uso na chumba kitupu. Wakati nashangaa akatokea mkuu, nyuma yangu. "Umepata nini?"



    Mara moja niliitambua sauti yake, wakati huo alikuwa

    akielekea kukaa kwenye kiti kilicho mbele yangu. Nikampa

    taarifa zote. Nikamwelekeza nilipoficha flash diski na kile

    kiboksi cha kompyuta.



    "Sasa nimeanza kupata picha, nilishangaa kwa biashara

    anayoifanya anawezaje kupata fedha nyingi za kufadhili

    shughuli za chama," alisema mkuu akizunguka-zunguka kwenye

    kiti.



    Pia alinidokeza kuwa wale waliokuja kutuchukua hawakuwa

    askari wa kawaida na pale ni kituo bandia cha polisi ambacho

    huwa wanakitumia kwa operesheni kama hizo. Nikarudishwa kwa wenzangu ambako kila mtu alikuwa akilalamika kivyake.



    Biashara kubwa alizokuwa akizifanya Mzee Nurdin za magendo, kusafirisha nyara za serikali na mbaya zaidi kusafirisha watoto nje ya nchi. Ila kwa watu alikuwa akijulikana kama mfanyabiashara wa mazao ya kilimo akimiliki pia viwanda vya usindikaji.



    Ila taarifa iliyomwacha hoi zaidi mkuu ni ile kwamba kuna

    watu wazito katika taasisi nyeti ambao wako katika orodha ya

    malipo ya Mzee Nurdin. Kuna maofisa wakubwa katika jeshi,

    idara ya usalama wa taifa, mahakama, polisi, ikulu, ndani ya

    chama tawala na ofisi ya bunge. Hao wote hutumika kumlinda

    na kumfikishia taarifa zote muhimu.



    Tuliachwa pale kituoni na mapolisi feki kadhaa.

    Tukasikia

    mlio wa gari linaloondoka, nikajua kuwa wanafuata vitu

    nilivyowaelekeza. Kichekesho alikuwa yule bosi wangu mnoko,

    toka tukamatwe ye alikuwa analia tu akilalama. Eti hastahili

    kukamatwa kwa kuwa yeye ni mtumishi mtiifu wa Mzee Nurdin.

    Tuliachiwa kesho yake alfajiri kwa kurudishwa na lile lile

    gari. Wakati tunashushwa pale nje kwa Mzee Nurdin, nilimuona

    Tausi amesimama akituangalia.



    Uso wake ulikuwa umejaa huzuni kubwa, ila sikutaka hata

    kumtazama. Niliinama chini na moja kwa moja niliongozea

    kibandani kwangu ambako sikukuta chochote kati ya vile vitu

    nilivyowaelekeza. Nikajua kazi imefanyika!



    Pamoja na kufurahia kuwa nimefanikisha jambo kubwa sana,

    upande mwingine nilikuwa nasononeka kwa kuwa mazingira ya

    kumbinjukia Tausi yangekuwa ni magumu sana. Sio kwamba

    ningeshindwa kubinjuka, bali endapo ingetokea kugundulika

    mchezo wangu basi mzigo wote wa yaliyotokea ungekuwa ni juu

    yangu. Nifanyeje?



    Siku moja wakati nimekaa kwenye eneo langu la kazi,

    nikamuona Tausi amekaa sehemu ile aliyokuwa akutumia

    kunichungulia. Tukakutanisha macho. Akafungua dirisha na

    kutupa kifurushi kidogo, aliniangalia kwa muda kisha

    akaondoka pale dirishani. Nilienda kwa kasi hadi pale

    dirishani, nikakiokota na kukifungua. Ilikuwa ni simu ya

    Nokia 3310, maarufu kama nokia ya jeneza.



    Ilikuwa na chaja yake na tayari ndani kulikuwa na laini na

    salio la kutosha. Lilikuwa limehifadhiwa jina moja tu,

    ’Ndege’ alikuwa akitania kutokana na jina nililompa katika

    shairi langu nililomwandikia siku ile. Kwa shauku nikaanza

    kuipiga namba hiyo ya ’Ndege’ simu iliita hadi ikakatika.

    Ghafla akapiga yeye.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Inaelekea una kiu sana, hata dakika haijapita?" Nilijikuta

    nikiishia kucheka tu nikishindwa kutoa jibu ila nilifurahi

    kupita kiasi. Tulianza kuwasiliana karibu kila dakika labda

    kwa kupiga au kwa ujumbe mfupi, ila tuliboresha sana

    uhusiano wetu.



    Nikaanza kujihisi nahitaji penzi la Tausi, nilihisi kuwa

    naye ana haja hiyo. Ila niliogopa msemo wa ’mvumilia mbivu

    hula mbovu’. Nikaanza chombeza chombeza, naye akielekea

    kibra!



    "Lini utanipa penzi Tausi?" nilijikuta nikiulizia. Tausi

    alicheka sana hadi nikajihisi nimechemka kumuuliza swali

    hilo. Nikawa mpole, tena mdogo kuliko kidonge cha piriton.

    Siku nzima nilikosa raha kutokana na kitendo kile cha

    kikatili alichonifanyia Tausi binti Nurdin, nilijihisi kama

    nimeachwa bila nguo.



    Niliamua kuizima simu ili nipate muda muafaka wa kufikiria

    nini cha kufanya, kwa kuwa ilikuwa ni mara ya kwanza kujiona

    mjinga, ilibidi nijipe nafasi ya kujitia ujasiri.

    Usiku uliingia bila kuwasiliana tena na Tausi, nikalala

    kinyonge nikijikunyata kama kinda la njiwa. Nilikuwa Musa

    Njiwa hasa, Musa mtoto wa Njiwa. Nikawazia kuwa ni kweli

    majina huwa yanajidhihirisha.



    Asubuhi ya siku iliyofuatia, nilijidamka asubuhi sana

    nikazifanya kazi zangu zote na kurudi katika kibanda changu

    na kurudi kulala.



    Ilipofika saa nne asubuhi, mlango wangu uligongwa.

    Nikakurupuka kwenda kuufungua, nikakiona nilichokitegemea,

    kiongozi wangu wa kazi. "Twende kuna kazi, unalala lala

    sana. Mzembe sana wewe" alianza kubwabwaja bila breki.

    Niliamua kukaa kimya bila kumjibu chochote kwa maana maneno

    yote yaliyokuwa karibu na mdomo wangu ni matusi matupu, huku

    moyo wangu ukiwa umejaa chuki. "Ipo siku yake tu ataingia

    kwenye anga zangu" nilijisemea moyoni.



    Wakati najifikiria jamaa likawa linaendelea na mineno yake

    ya kukera, nilichokifanya nikurudi ndani na kuvaa raba

    zangu. Nikatoka na kumfuata kwa nyuma kwa kuwa muda wote

    alikuwa mlangoni akinisubiri utafikiri askari anayemsubiria

    mfungwa atoke mahabusu.



    Tuliongozana mkukumkuku akinipeleka hadi kwenye lango la

    nyumba kubwa. Tausi alikuwa amesimama akiwa katika hali ya

    kutoka, pembeni yake amesimama binti mmoja mtumishi wa mle

    ndani.



    "Utampeleka bosi kufanya manunuzi yake, huko acha uvivu

    uvivu wako" lile jamaa liliendeleza gubu. Nilimwangalia kwa

    jicho kali huku nikishusha pumzi ndefu, jamaa linanitoa

    nishai mbele ya mtoto bwana?



    Tausi alitangulia kwenye gari bila kunisemesha akifuatiwa

    kwa nyuma na yule mtumishi. Wakati huo dereva alikuwa

    ameshawasha gari. "Kanichunia nini?" Nilijiwazia huku

    nikilijongelea gari na kuingia.



    Safari ilianza taratibu kila mtu akiwa kimya, hakuna

    aliyekuwa na la kumwambia mwenzake japo tumetoka nyumba moja ukiondoa mawasiliano ya siri kati yangu na Tausi hakuna

    aliyekuwa na mazoea na mwenzake zaidi ya kuonana kwa juu

    juu.



    Tausi alikuwa kimya akiangalia mbele bila kusema neno wala

    kumwangalia yeyote kati yetu, na kwa jinsi ilivyokuwa

    ilionekana kuwa dereva alikuwa na ratiba kamili ya safari.

    Tulipita katika maduka mbalimbali lakini yote aliteremka

    Tausi na yule binti mtumishi. Mara ya kwanza nilitaka

    kuteremka akanizuia kwa kuniambia kuwa akihitaji niteremke

    ataniambia.



    Nilihisi ananinyanyasa kisaikolojia, ila kilichonikera zaidi

    ni kitendo cha yule dereva kunicheka kwa kuniona kuwa mimi

    ni kimbelembele.



    Nilitamani kumtukana kwa kuwa ndio lugha inayonipunguziaga

    hasira. Tukahama toka Posta, tukaelekea maeneo Mnazi Mmoja.

    Gari likaegeshwa mbele ya benki iliyokuwa mtaa wa Lumumba

    katika jengo la Ushirika, yule binti akataka kuteremka na

    Tausi.



    "We subiri kwenye gari na vitu. Hoza twende!" Mapigo ya moyo

    yaliongezeka spidi nisijue yule binti alitaka nimsindikize

    benki kwa ajili gani. Akawa ametangulia mimi niko nyuma

    yake.



    Kufika mlango wa benki akapitiliza, nikaendelea kumfuata kwa

    nyuma. Akawa kama anaelekea kupanda lifti, akakata kona

    kuzielekea ngazi lakini hakuzipanda kwenda juu akawa

    anateremka.



    Kama kawaida niliendelea kumfuata kwa nyuma kama mbuzi

    anayepelekwa machinjioni, tukafika chini tukatokeza kwenye

    maofisi mengi. Tausi aliongozea kwenye ngazi nyingine

    inazopandisha juu.



    Tulitokea nyuma ya jengo la Ushirika kwenye mtaa wa Kipata,

    akasimamisha teksi akaingia mlango wa nyuma, na mimi

    nikamfuata humo humo kwenye siti ya nyuma. "Wapi dada?"

    Dereva aliuliza.



    "Hotel yeyote iliyo karibu" akajibu Tausi.

    ’Kama hoteli yeyote si tuingie hii hapa mbele yetu?’

    nilidakia mazungumzo. Dereva wa taksi aliniangalia jicho la

    kuniambia ’acha uchawi wewe’



    "Dah kweli. Samahani kaka, lakini nitakupa hela kidogo"

    alitamka Tausi akionyesha alimwelewa. Tukaingia hotelini.

    Tukafanya taratibu za haraka haraka, tukapata chumba.

    Mpaka muda huo sikujua lengo la Tausi lilikuwa ni lipi,

    lakini cha mwisho nilichoamini ni kuwa kaamua kunisusia

    penzi lake. Nilipowaza hilo nilijihisi mwili ukisisimka

    kujiandaa na kukabiliana na zawadi ya penzi la kushtukiza,

    nguo ikawa haikai vizuri tena. Tukaingia ndani, tukajifungia

    mlango.



    Mwanamume nikaanza kutetemeka bila kujijua, nikajihisi

    napata tumbo la kuhara. "Sijui nitoke kidogo nikamnywee

    konyagi?" Nilijiuliza kwa haraka haraka. Nilijikuta mawazo

    ya kihama huku na kule.



    Kutahamaki Tausi alikuwa amenisimamia mbele yangu

    akiniangalia usoni. "Umenikasirikia?" Aliniuliza kwa utulivu

    akiwa ananitazama usoni.



    "Hapana ila nilifadhaika sana ulipoamua kuniche.."

    nikakatizwa na mdomo wake ambao tayari ulikuwa umeshafika

    mdomoni kwangu. Nilijiona dhahiri kuwa nazidiwa, Tausi

    alianza kuutawala mchezo.



    Nikaona ni jambo la hatari kumruhusu mpinzani akutawale

    mchezoni. Mwanamume nikaanza kupiga ’kaunta ataki’ au kwa

    lugha fasaha mashambulizi ya kushtukiza. Nikawa namgusa zile

    sehemu zitakazomfanya apoteze kasi yake.



    Nilianza kumtoa kitambaa cha kichwani alichokitumia

    kuzistiri nywele zake, nikaanza kuzichezea nywele zake

    taratibu nikimpiga busu masikioni na kushuka taratibu hadi

    shingoni. Nikamuona akianza kuhema kama mgonjwa wa pumu.

    Tausi alianza kuhema kwa shida akitetemeka, nikajua sasa

    nimeudhibiti mchezo. Nikamlaza pole pole kitandani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Nakupenda sana Hoza" aliniambia akihema. Nilimwangalia kwa

    makini, hakuonyesha masihara akitamka maneno yale.

    Mambo yote toka tuliache gari pale mbele ya benki

    yalituchukua takribani dakika kumi na tano, nikaona kuwa

    bado naweza kulifanya nilitakalo kwa muda uliobakia.

    Nikajipa tena dakika tano za ’shoo gemu’.





    ITAENDELEA



0 comments:

Post a Comment

Blog