Search This Blog

Monday 20 June 2022

KIZUIZI - 2

 





    Simulizi : Kizuizi

    Sehemu Ya Pili (2)



     Sauti zilizosikika pekee katika masikio ya Jose zilikuwa za wale mbwa wenye hasira, kiatu kimoja kikiwa kimechoropoka mguuni Jose alibakiwa na kiatu kimoja tu huku mguu mwingine ukiwa peku.

    Umakini wa Jose katika kuwakwepa mbwa ukamsababisha asiweze kuisikia honi iliyokuwa inapigwa na pikipiki, Jose akaifikia kona, akajaribu kuwahi kuruka upande mwingine baada ya kukutana ana kwa ana na pikipiki ikiwa katika mwendo wa kasi.

    Akili yake ya kuhama upande ikafanana na ya yule dereva nay eye akahamia upande aliorukia Jose.

    Mlio mkubwa kisha kimya kikatanda.

    Jose kimya, dereva kimya.

    Kiza kikubwa kikatanda.

    ****CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Haikuwa mara yake ya kwanza kumfungia tela mtu ili aweze kufahamu anachokihitaji. Zoezi lake alilotegemea kuwa litakuwa gumu sana lilibadilika na kuwa jepesi. Hali hii ilikuja baada ya kumuona Jose B.

    Akampigia mahesabu kuwa ni huyo ambaye atamuonyesha wapi alipo Deo na kisha wote wawili atawaangamiza aweze kubaki bila hatia inayoleta kizuizi.

    Kila hatua aliyokuwa anaenda Jose, jicho la James lilikuwa makini kumfuatilia. Na hata alipomuona akimfuatilia Deo na yeye aliendelea kufuatilia.

    Jose B hakujua kabisa kama kuna uwezekano wa kuwa anafuatiliwa na mtu nyuma yake, alijiamini kuwa ni yeye pekee anayemfuatilia kiumbe yule.

    James alijiegesha mahali ambapo hawezi kuonekana kirahisi hadi alipomuona Deo anaagana na Jose B. Alisikia maneno yao ya mwisho wakisisitizana juu ya kuwahi kesho wakutane msibani. Maneno haya yakawa na umuhimu sana kwa James.

    Akahisi zoezi lake litakuwa na wepesi.

    James alitaka kuanza na Jose B kwa wakati ule lakini akaona wa muhimu zaidi ni huyu Deo ambaye wamekuwa naye ujanani na utotoni na anamfahamu fika. Kuhusu Jose, hakumtilia sana maanani kwani alifahamu kuwa hajui lolote kubwa kuhusu yeye. Pia akaamini alikuwa na nafasi kubwa ya kumteka Jose wakiwa msibani siku inayofuata.

    Dakika kumi baada ya Jose kutoweka, James akiwa amechemkwa na hasira kichwani aliingia bila kubisha hodi katika chumba kidogo cha Deo. Taa ilikuwa inawaka, ana kwa ana na rafiki wa utotoni na ujanani.

    Deo na James.

    Deo akataharuki zaidi ya kushangaa. James akatoa tabasamu bandia kisha akamsukuma kwa nguvu akatua kitandani, kitanda kikazidiwa nguvu kikaachana na chaga kikatua chini na mwili wa Deo.

    Deo aliyezoea utotoni kuwa alikuwa mbabe kwa James, alisimama wima kibabe ili ajaribu kama anaweza kukabiliana na James. Lakini mawazo hayo yalikuwa ‘mawazo mfu’, James alikuwa mwingine kabisa wakati huu.

    Ngumi moja iliyoshiba haswa ikakutana na mdomo tepetepe wa Deo.

    Damu ikaruka.

    “Wewe na Bibiana mlitaka kwenda kumwambia nini Paroko??” James aliuliza kibabe.

    Deo kimya!!

    “Nakuuliza wewe boya, wewe na huyo Bibiana wako mlitaka kumwambia nini paroko?” sauti ya ukali ikamtoka. Deo akawa anatetemeka midomo bila kusema lolote.

    “Mnajifanya mnanijua sana eeh...” Aliuliza James huku akilazimisha tabasamu.

    “Sio mimi ni Bibiana peke yake ndo alisema.....alisema kuhusu ...Mamu...”

    “Mamu kafanyaje??” alihoji kwa ukali.

    “Mi sijui, anajua Bibiana...haki ya Mungu tena Jimmy mi sijui kitu kaka..” alijitetea Deo. James akiwa anamsikiliza.

    “Okey, kumbe haujui vizuri sana.....sasa naomba nikupe agizo moja.” Alizungumza kwa sauti ya chini kama aliyeelewa alichosema Deo.

    Amani ya Deo ikarejea kiasi.

    “Niagize tu kaka.” Deo akanyenyekea.

    James alimtazama machoni Deo, Deo akakwepesha macho.

    Likafanyika tukio la mara moja lililoambatana na maneno.

    “Sasa nakuagiza nenda ukamuulize huyo Bibiana halafu uje unieleze Mamu amefanya nini....” Jose alitoa maagizo haya huku kisu kikiwa kinazama na kutoka katika mwili wa Deo.

    Baada ya dakika kadhaa kweli Deo aliyekubali kuagizwa kwa Bibiana akawa ameagizwa. Agizo la milele lisilokuwa na majibu.

    Deo akaiaga dunia bila kumueleza Jose B juu ya kizuizi.

    Usiku ulikuwa umeingia, James akarejea kimyakimya hotelini huku mawazo yake yote yakiwa juu ya Jose B, ni huyu pekee alikuwa amesalia katika orodha ili amani ichukue nafasi.

    Asubuhi kama ilivyo ada aliwahi sana kuamka, akajiandaa na kupata kifungua kinywa kisha safari kuelekea msibani.

    Kama alivyotarajia alimkuta Jose B akiwa amewasili tayari.

    Kama ilivyokuwa siku iliyopita alifanya kumfuatilia nyendo zake ili aweze kupata upenyo wa kupata faragha na kumwondosha duniani mara moja.

    Kwa kugundua kuwa amekosa cha kumweleza mkewe mtarajiwa juu ya sababu za kuchelewa kurejea, alitumia sababu ya kuhudhuria mazishi ya Bibiana, sababu ambayo haikupingwa na mkewe huyo, taarifa hiyo akampatia pia mzee Magayane ambaye ni baba yake mzazi. Alifanya hivyo kwa kuhofia mkanganyiko iwapo ataweza kukutana naye msibani.

    Mawazo yake yalikuwa sahihi kabisa, akiwa katika kumfuatilia Jose B asiweze kumpoteza hata kwa sekunde moja, alikutana na mzee wake, alitaman i kuongea upesi ili waweze kuachana, lakini mzee yule akamvuta mwanaye pembeni na kumpatia sifa kedekede anazozipata mtaani baada ya kusikia kuwa mwanaye anaoa.

    James hakuwa makini kabisa na mazungumzo yale. Na alijitahidi kadri ya uwezo wake kuyafupisha.

    Licha ya jitihada zote hizo aliporejea hakumkuta tena Jose B. Aliangaza huku na huko lakini hata dalili haikuwepo.

    Ni katika muda huo ambao mzee alimvuta James pembeni ndipo Jose B alikuwa ameamua kumfuata Deo nyumbani kwake baada ya kuwa amechelewa sana kurudi.

    Huko anakutana na dhahama ya kukutana na maiti ya Deo, kisha kabla hajakaa sawa anakimbizwa na mbwa wakali, riadha yake haifiki mbali anakutana na ajali mbaya ya pikipiki na sasa kimya kimetanda.

    Kimya kinachotia wasiwasi.



    ***



    EMMY JOHN, hakuamini hata kidogo ile dawa aliyopewa na Lameck inaweza kufanya kazi kiasi kile alichokishuhudia, alikuwa anakauka na kurejea kawali.

    Furaha ikarejea kwa kasi, akampigia simu Lameck na kumweleza juu ya yale mabadiliko.

    Lameck akajipongeza kwa ujuaji huo alioupatia katika kambi ya jeshi. Ujuaji ambao unatumiwa na wasichana matapeli wa mjini kujikausha na kufanana na mabikira. Kisha kuwalaghai wakuja.

    “Lameck hivi inaleta kichefuchefu eeeh maana mh!!” Emmy alimuuliza Lameck.

    “Kichefuchefu? Yeah..ok..ndio inaleta lakini sio sana..” alijiumauma Lameck. Emmy hakushtukia.

    “Ndo maana dah kichefuchefu kama nini dah....” alizidi kulalamika Emmy.

    “Usijali lakini...kitaisha cha msingi kutimiza tulichohitaji au vipi?”

    “Haya masta”

    Lameck akawahi kukata simu baada ya kugundua kuwa alikuwa na dalili za kutetemeka.

    Kichefuchefu?? Alijiuliza Lameck.

    Hizo hazikuwa dalili za dawa ile kufanya kazi, mjeshi huyu akakaa kitako, kiutu uzima akatafakari kidogo kisha akafanya tabasamu ndogo yenye karaha ndani yake. Akataka kufanya ubashiri lakini akasita maana aliamini atajiumiza kwa ubashiri.

    Siku ikapita.

    Lameck na shughuli zake na Emmy akiendelea kwa juhudi zote kutumia dozi ya shabu na ndimu kuimarisha bikra feki. Kichefuchefu kikiwa rafiki yake wa karibu sana.



    ***



    Maandalizi ya harusi yalikuwa yakifanyika kwa bidii kubwa. Emmy alikuwa ana furaha sana kwani kizuizi chake aliamini amefanikiwa kukikwepa, James yeye alikuwa hamsini hamsini, jitihada zake za kumsaka Jose B zilivyogonga mwamba jijini Mwanza alikuwa katika taharuki ya kuaibika siku moja baada ya tangazo la tatu, aliamini kuwa lazima Jose B atamuharibia. Alifanya maombi katika miungu yote anayoifahamu ili imwepushe na aibu inayokaribia kumpata.

    Alipungua uzito na hakuwa na amani kabisa, hatimaye jumapili ya tangazo la tatu na la mwisho ikafika.

    Maajabu!!

    Tangazo la tatu lilipita bila kizuizi chochote kile. Hakuna kipingamizi kutoka jijini Mwanza wala Dar es salaam.

    Furaha kamilifu.



    Yule Jose B aliyekuwa anahofiwa kuleta matatizo hakuonekana kuwa na hatari yoyote tena na wala hakujulikana ni wapi alipo.

    Ile harusi babu kubwa iliyokuwa inangojewa hatimaye ikashika hatamu.

    James mwenye siri kubwa moyoni akamvisha pete Emmy mwenye siri kubwa zaidi mwilini. Kila mmoja alitoa tabasamu kwa mwenzake, tabasamu la kinafiki, kila mmoja alijiona ni mkosefu kwa mwenzake.

    Emmy akajutia kwa kufanya mapenzi na Lameck huku James naye akijutia mengi mazito.

    Nani ajuaye siri ya moyo? Hayupo!!

    Na ilikuwa hivyo, hatimaye kiongozi wa kiroho akawabariki James na Emmy kuwa mume na mke.

    Vigelegele, mbinja na makofi vikasikika.

    Harusi ya kifahari kabisa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ya ukumbini yalikuwa ni kufuru kubwa, pesa ilitumika sana, hayasimuliki kwa ambaye hakuwepo. Ni kama maigizo.

    Lameck akamkumbatia Emmy wakati akimpatia zawadi yake kama babamdogo. Msema chochote (MC) naye akawapamba sana wawili hawa kuwa walisoma pamoja na kukua pamoja.

    Laiti angejua siri waliyohifadhi wawili hawa ni heri angekaa kimya bila kusema neno.

    Siku ikamalizika, bwana na bibi harusi wakisafirishwa hadi Kampala Uganda kwa ajili ya fungate la majuma mawili na siku tatu.

    Ni huku Kampala Uganda ambapo mambo mapya kabisa yanazaliwa. Mambo yanayoleta furaha ya muda mfupi kisha linazuka la kuzuka.



    Harusi hii ya kifahari isingeweza kukosa waandishi wa habari wa kununuliwa. Na kipindi kikarekodiwa na kurushwa katika kituo kimojawapo cha luninga hapa nchini.

    Kipindi kilirushwa siku mbili baada ya harusi ile ya kifahari.

    Huenda ni maelfu walikitazama kipindi kile b ila ya kuwatambua maharusi wale, lakini kijana mmoja alivutika zaidi na kupagawa sana kwa kile alichokiona, alitambua tukio lile na alijiona kama lilikuwa linamuhusu, alitazama tabasamu la bibi harusi na kisha akachukizwa na cheko la bwana harusi.

    Alisikiliza kila kilichokuwa kinasemwa. Alitamani sana kusimama wima aweze kuangalia kwa makini lakini hakuweza, alitamani kusema neno lakini hakuweza kutokana na kufungwa vifaa maalumu katika taya zake kwa ajili ya kuzilinda, alikuwa amevaa bukta mguu wake wa kuume ukining’inia juu huku ukiwa na bandeji gumu.

    Macho na masikio pekee ndio viungo vilivyokuwa huru kufuatilia tukio hili kikamilifu. Kichwani alipitisha maswali mengi lakini akakosa majibu, aliamini kuwa laiti kama angekuwa mzima wa afya hakika angepata cha kusema juu ya ndoa ile ya kifahari. Alipokumbuka juu ya uzima wake akawalaani wale mbwa waliomkimbiza, akataka kumlaani na dereva aliyemgonga na pikipiki lakini akakumbuka kuwa dereva yule alikufa hata kabla ya kufikishwa hospitali.

    Laana zake akazihamishia kwa muuaji wa Deo.

    Nani amemuua Deo? Alijiuliza tena.

    Macho yake yakaitazama luninga akakutana na James akimlisha mkewe keki kwa kutumia midomo. Hasira ikamkamata akataka kutukana, taya lililovunjika likamsaliti akauma meno kwa uchungu, chozi likamtoka kutokana na maumivu ya taya.

    “Jose B waukweli hapa sina ujanja aisee. Ila ngoja nipone..” Alikiri kimya kimya wakati kile kipindi kikielekea ukingoni.

    Wagonjwa walivutiwa na kipindi kile, Jose B akafurahishwa na huduma bora kutoka hospitali binafsi. Laiti kama angekuwa hospitali ya serikali hata hiyo luninga asingeweza kuiona. Na hiyo ndoa ya James na mkewe asingepata fursa ya kuitazama pia.



    ***



    Ndege ilitua katika ardhi ya nchi ya Uganda katika jiji la Kampala, uwanja ndege wa kimataifa wa Entebbe. Haikuwa mara ya kwanza kwa James kutia mguu wake katika jiji hili. Lakini kwa upande wa Emmy ilikuwa mara yake ya kwanza.

    Wapambe walioandaliwa jijini hapo waliwapokea kama wanavyopokewa maraisi ama viongozi wengine wa serikali.

    Moja kwa moja wakaongozwa na kuingia katika magari kadhaa. Safari ikaanza, ilichukua takribani dakika arobaini na tano kutoka uwanja wa ndege hadi kuifikia hoteli ya kimataifa yenye nyota tano ya Sheraton.

    Safari ya wapambe ikaishia katika chumba cha mwisho kabisa cha hoteli hii yenye ghorofa kumi na tano ikiwa na vyumba mia mbili na nane.

    Emmy na James wakabaki peke yao katika chumba namba 208.

    Chumba ambacho James alikichagua kwa sababu maalumu kabisa na alikilipia miezi miwili kabla ya siku hiyo.

    Katika chumba hicho cha juu kabisa mteja anaweza kuiona kwa uwazi fahari ya Uganda, vilima vya Kololo na Nakasero ambavyo vinavutia sana kutazama.

    Ilikuwa mara ya kwanza kwa mwanadada Emmy kuingia katika hoteli ya kifahari namna hii ambayo kwa usiku mmoja ilikuwa inalipiwa dola za kimarekani 440 ambayo ni zaidi ya shilingi laki tano za kitanzania.

    Katika nafsi yake alikiri kuwa kuolewa na mtu mwenye pesa zake wakati mwingine ni jambo jema sana. Angeyaona wapi haya kama angeolewa na kapuku kama fulani?

    James hakuwa na haraka sana ya kutimiza haja yake. Haja iliyomfanya amuoe Emmy. Alikuwa mtulivu sana. Baada ya kupumzika kwa takribani nusu saa, alimuongoza Emmy wakabadili nguo zao kisha wakatoka nje na kuchukua ‘lifti’ ambayo iliwafikisha katika mgahawa mkubwa ndani ya hoteli hiyo ya aina yake katika jiji la Kampala na Afrika mashariki kwa ujumla.

    Equator Lounge. Emmy aliyasoma maandishi makubwa mlangoni.

    Huku walikula na kunywa huku James akionekana kumjali zaidi mkewe kuliko anavyojijali yeye. Hali hii ilimfanya Emmy ajute sana kwa kitendo cha kutotimiza ahadi na kufanya uzinzi na Lameck. Baada ya kula waliliendea bwawa la kyoga ambalo lipo pia ndani ya hoteli hiyo ya kimataifa.

    Hapa ndipo simulizi ya kushangaza inapoanzia.

    Emmy hakuwa mzoefu hata kidogo katika kuogelea, James alikuwa mzoefu sana katika mambo hayo. Akamchukua Emmy katika namna ya kumfundisha, Emmy alikuwa amevaa kinguo chepesi sana na James alikuwa na bukta yake maalumu kwa ajili ya kuogelea.

    Akamshika Emmy kifuani, akaanza kuogelea naye taratibu.

    Kila mara alivyojaribu kumweka sawa Emmy alifanya namna ya kuzitikisa chuchu zake ndogo za moto ambazo zilikuwa wima kama askari mkakamavu katika gwaride.

    Kadri alivyozipapasa nazo zikazidi kuwa imara.

    James akaingiwa matamanio, lakini hakusema.

    Pumzi za Emmy zikaanza kupishana kwa kasi ya ajabu kama ambaye anatapatapa

    kujiondoa katika hatari fulani ama aliyemaliza mashindano ya riadha ndefu.

    James akaganda kama kinyago. Hali ilikuwa mbaya sana.

    Juhudi za kufanya subira zikashindikana.

    Upesi kabla ya lolote la kuwatia aibu kutokea alimtwaa Emmy mpaka nje ya maji. Akamfuta hovyohovyo kisha wakakimbilia ndani katika lifti. Ikawarejesha chumbani.

    Kitanda kikubwa cha kisasa chenye mashuka meupe sana kikawapokea.

    James akamnyanyua Emmy na kumrusha kitandani.

    Emmy aliyekuwa anathema juu juu akakata ghafla pumzi hizo na kurejewa na pumzi zake za kawaida.

    “Jimmy...noooo....” akamzuia mwanaume yule aliyetaka kumvamia pale kitandani.

    James kimya. Akashangaa.

    “Naomba nipumzike kidogo mume wangu...utaniua ujue...” aliongea kwa kubembeleza huku moyoni akikiri kuwa alikuwa katika uhitaji mkubwa wa hicho anachohisi.

    Lakini asingeweza kumruhusu, kuna sharti moja alikuwa hajatimiza.

    James akiwa katika upole hakuwa na cha kupinga, akamkubalia Emmy.

    Msichana huyu akajifanya amepitiwa na usingizi, James akasinzia kweli.

    Emmy akanyanyuka na kuelekea bafuni, kwa siri kubwa akatoa kisabuni kilichopigwa lebo ya ‘KAISIKI’

    Kaisiki ni sabuni ambayo alipewa na Lameck. Alitakiwa kujiosha na sabuni hii masaa kadhaa kabla ya tendo, ni jambo hili alikuwa hajalifanya.

    Akafanya kisha akarejea kitandani baada ya kuwa ameificha.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Saa nane usiku, Jimmy akahisi anapapaswa, aliposhtuka alikuta ameelekezewa bastola mbili fupi zinazofanana. Alikuwa ametekwa.

    Hofu kuu ikatanda. Bastola zile zikamsogelea na sasa zikamgusa, mapigo ya moyo yakapanda maradufu, hakutegemea kama anaweza kutekwa kutoka usingizini bila hata dalili za kutekwa.

    Bastola zile badala ya kutoa risasi zikamchomachoma kifuani na kuunda joto kali.

    James akaamua kupambana. Akazishika zile bastola mbili kutoka katika kifua cha Emmy.

    Kilichoendelea hapo, makelele ya kuigiza yaliyopigwa na Emmy na mengine yote.

    Si mimi wala wewe anayeweza kuyasimulia lakini vilima vya Kololo na Nakasero vilishuhudia kila kitu, hata wakati muhudumu anapewa pesa ya ziada kwa ajili ya kufua mashuka yaliyotiwa doa na damu vilima vilishuhudia pia.



     Saa nane usiku, Jimmy akahisi anapapaswa, aliposhtuka alikuta ameelekezewa bastola mbili fupi zinazofanana. Alikuwa ametekwa.

    Hofu kuu ikatanda. Bastola zile zikamsogelea na sasa zikamgusa, mapigo ya moyo yakapanda maradufu, hakutegemea kama anaweza kutekwa kutoka usingizini bila hata dalili za kutekwa.

    Bastola zile badala ya kutoa risasi zikamchomachoma kifuani na kuunda joto kali.

    James akaamua kupambana. Akazishika zile bastola mbili kutoka katika kifua cha Emmy.

    Kilichoendelea hapo, makelele ya kuigiza yaliyopigwa na Emmy na mengine yote.

    Si mimi wala wewe anayeweza kuyasimulia lakini vilima vya Kololo na Nakasero vilishuhudia kila kitu, hata wakati muhudumu anapewa pesa ya ziada kwa ajili ya kufua mashuka yaliyotiwa doa na damu vilima vilishuhudia pia.

    James akatimiza azma yake.

    Hatimaye, sasa aliyangoja majibu.

    Baada ya majuma mawili. Mume na mke wakarejea nyumbani baada ya kuwa wametumbua mamilioni kadhaa katika hoteli ya kifahari ya nyota tano. Sheraton.

    Walipotua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu nyerere, walikuwa mume na mke halali kabisa.

    Likafuatia fungate la nyumbani, James akatulia na Emmy kwa siku kumi kabla ya kuanza shughuli zake.

    Katika siku hizi kumi, Emmy akaongeza baraka katika familia. Emmy alikuwa mjamzito.

    Habari hii ilipokelewa na James katika namna ya kustaajabu, hakutegemea kabisa kupokea taarifa hii mapema kiasi kile.

    Hakuweza kumueleza mtu yeyote ni kwa jinsi gani ameipokea taarifa ile. Lakini alielewa kuwa ilikuwa nzito na ya kushangaza.

    Zawadi ya kipekee kwa wakati muafaka.

    Mwisho wa Emmy kutumia SHABU, NDIMU na KAISIKI.



    ***



    Mazoea hujenga tabia. Na tabia kuibadilisha hasahasa kwa mtu mzima ni jambo gumu sana. Wanasema samaki mkunje angali mbichi, ukimngoja akauke atavunjika ukithubutu kumkunja.

    Ilikuwa hivi kwa huyu kijana ambaye mazoea yake ya kupenda kujua mengi tangu utotoni yaligeuka kuwa tabia yake ya ukubwani.

    Hakujali kama alivunjwa mguu katika ajali ya pikipiki huku taya nazo zikipisha na sasa alikuwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili jijini Dar es salaam kwa matibabu baada ya hospitali za jijini Mwanza kushindwa kumuhudumia ipasavyo.

    Akiwa katika kufanya mazoezi ya mguu wake ambao ndio ulikuwa ndio kwanza umetolewa bandeji gumu, maarufu kama P.O.P. Jose B wa ukweli anakutana na jambo ambalo linakuwa kama ndoto.

    Akajiuliza kama anaota kile kipindi alichokiona katika luninga kikionyesha ndoa ya kifahari ama anakiona kweli kikiendelea.

    Aliyapikicha macho yake lakini alipoyaacha wazi bado aliziona zile sura ambazo aliziona katika luninga zikitabasamu.

    James na mkewe. Ni siku ambayo walikuja kupima mimba na ikagundulika mwanadada yu mjamzito....Jose B anawaona.

    Ushakunaku ukampanda kichwani, akajikongoja na magongo yake ili aweze kupata mawili matatu yasiyomuhusu, aliwaza juu ya kizuizi, akahisi bado kuna nafasi ya kumpatia shilingi mbili tatu.

    Jose B waukweli akajisogeza kwa tabu hadi akalikaribia eneo walilokuwa James na mkewe, wakiwa na daktari, wote walikuwa na furaha.

    Baada ya mazungumzo James aliagana na daktari na mke wake kisha akatoweka.

    Hiyo ikawa nafasi ya kipekee iliyokuwa inasubiriwa na Jose B waukweli.

    Kutoweka kwa James kukamfanya abakie na sura ngeni zisizomtambua.

    Shida yake ikawa juu ya yule msichana mrembo ambaye alimuona katika luninga akilishana keki kwa kutumia midomo na bwana James.

    Jose B akaupima mguu wake akahisi una masalia ya nguvu za kutembea japo kwa kuchechemea kidogo.

    Akajikongoja hadi nje akiwa kama anayefanya mazoezi.

    Baada ya dakika kadhaa yule mwanamke akafika akaangaza huku na kule akamuita dereva taksi, Jose B naye akafanya vilevile.

    Mfukoni alikuwa na akiba kiasi fulani ya pesa.

    Hakuwa mwenyeji sana wa jiji la Dar es salaam, alimuagiza dereva kufuata taksi iliyoanza kuondoka.

    Jose B akaanza kumfuatilia mke wa James.

    Emmy John.



    Ilikuwa siku ya mapumziko hapakuwa na foleni kubwa barabarani. Safari ikaishia katika mitaa ambayo ilikuwa na watu wengi wakijishughulisha na biashara ndogondogo.

    “UBUNGO BUS TERMINAL” Jose B aliyasoma maandishi makubwa, kisha moyoni akajisemea. Kumbe hapa ndio Ubungo.

    “Hivi nilipotoka panaitwaje vile?” alimuuliza dereva huku akijiandaa kumlipa.

    “Muhimbili hospitali.”

    Emmy aliposhuka na yeye akashuka baada ya kulipa akaanza kumfuatilia. Alijikaza asichechemee sana lakini alilazimika kuchechemea.

    Kuna wakati alijiuliza anafuatilia ili iweje lakini tabia kamwe haibadiliki kirahisi, akajiona yupo sawa tu.

    Emmy mbele, Jose B nyuma.

    Wasiwasi ulioonyeshwa na Emmy wakati akitembea ulizidi kumvutia kijana huyu wa Mwanza. Hatimaye wakafikia mahali pakiwa na nyumba ya kulala wageni yenye hadhi ya ‘uswazi’. Jose B akaduwaa, hakuamini malaika kama Emmy anaweza kuwa anaenda kukutana na mtu katika nyumba ile isiyokuwa na hadhi ya kumuhifadhi malaika kama yeye.

    Akiwa bado anatafakari, alimuona mwanamama yule akifanya mawasiliano katika simu na baada ya dakika kadhaa kikajitokeza kipande cha mtu kikiwa na misuli iliyokakamaa na mwili wa mazoezi ambao haujatepeta.

    Jicho la Jose B likakumbwa na sintofahamu.

    Umbea wake ukamuwasha zaidi, akatamani kujua zaidi kinachoendelea.

    Hakujali kama ametoroka hospitali ama la. Alijiona yupo sawa kabisa isitoshe alikuwa amekaribia kupona.

    Roho wa kiherehere alikuwa amemteka na kumpelekesha atakavyo.

    Kipande cha mtu kikamkumbatia Emmy, binti akaona aibu lakini hakuwa na budi akapokea lile kumbatizi mwanana.

    Jose B akakumbwa na wivu asiojua ni wapi umetokea.

    Akatamani kupiga kelele, lakini hazikuwa na tija. Akajikausha.

    Wawili wale wakakokotana hadi chumbani. Jose B akachungulia kwa mbali.

    Ule uzuri wa gesti bubu ukawa faida kwa Jose B.

    Chumba namba 18!!

    Jose B akaweza kukisoma kile chumba walichoingia wawili hawa.

    Lazima nijue kunani humo ndani haiwezekani yanipite. Jose B akajiapiza huku akikumbwa na hasira kana kwamba yanamuhusu ama ni mkewe ameingizwa humo ndani.

    Uswazi ni uswazi tu. Upande wa nyuma wa ile nyumba ya kulala wageni ilikuwa ni chochoro ya kupita watu.

    Jose B akashtukia huo mchezo.

    Huku akichechemea kwa mbali akaanza kupiga mahesabu ya kupata udaku.

    Laiti kama angekuwa mwandishi wa habari hizo. Basi angekuwa maarufu sana.



    Msichana dhaifu, mwenye macho mekundu, akatokea katika chumba baada ya masaa matatu kupita. Alikuwa ana kila dalili ya kuchoka sana na ni kama alikuwa aidha katika maumivu ya nafsi ama mwili moja kwa moja.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Jicho la Jose B ambaye tayari alikuwa amedaka mawilimatatu kupitia dirishani liliweza kumuona. Kilichomfurahisha Jose B na kujiona kijana anayefanikiwa upesi sana katika harakati zake na kuzisikia namba za simu za yule binti wakati akimtajia mwenza wake katika kile chumba. Alizitaja namba zake baada ya kuwa katika uhitaji wa kupata salio katika simu yake na yule bwana bila shaka alikuwa na salio la kutosha, akatajiwa namba kwa utulivu, Jose B naye akazinakiri kwa umakini katika ubongo wake.

    Zoezi la kawaida kwa watu wenye tabia kama yake.

    Namba hizo zikamsahaulisha Jose B wivu na matamanio aliyoyapata wakati akimsikia yule binti akigumia kimahaba katika chumba kile cha uchochoroni.

    Jose B hakutaka kumfungia tela. Alimsindikiza kwa macho huku moyo wake ukiteketea kwa maumivu kadri yule binti alivyozidi kutikisika huku akipotelea mbali.

    Jose B waukweli akafanya ishara ya msalaba, katika namna ya kumshukuru Mungu.

    Sijui kwa lipi? Labda kumpatia ule umbea.

    Anajua yeye mwenyewe!!.

    Akiwa hajapoteza kumbukumbu ya kituo alichoambiwa, alipanda taksi tena ikamrejesha hospitali ya taifa ya Muhimbili.

    Bahati nzuri hakuna aliyeshtukia kutoweka kwake, kwani hakuwa chini ya uangalizi mkali kama awali.

    Jose B akakirejea kitanda chake. Akafumba macho na kuitafakari siku hiyo.

    Akamjengea picha yule bibi harusi aliyetoka kumuona katika luninga siku kadhaa nyuma lakini leo hii amemuona tena akiwa katika kuisaliti ndoa yake.

    Roho ikamuuma. Akatamani sana kuitua siri hii kwani ilikuwa nzito sana kwake.

    Ataitua kwa nani tofauti na muhusika wa mali hii. James.

    Mtihani mkubwa.



    ***



    Simu yake iliita majira ya saa nane usiku. Alipotazama aligundua kuwa alikuwa mkuu wake wa kazi. Hakuruhusu uzembe wa usingizi kuitawala sauti yake. Alipokea na kuzungumza kikakamavu.

    Baada ya mazungumzo kuisha alianza kujiuliza ni nini kimemfanya mkuu wake wa kazi kumpigia simu usiku kama huo kisha kumweleza kuwa asubuhi na mapema alikuwa anahitajika ofisini. Sheria ya jeshi ni kwamba ukiitwa huna haja ya kuuliza kwa nini umeitwa, hasahasa akiwa mkuu wako wa kazi. Cha msingi ni kutii amri.

    Bwana Lameck naye alitii amri.

    Asubuhi na mapema alikuwa katika ofisi ya aliyempigia simu.

    Cha kushangaza hakumkuta ofisini.

    Alisubiri hadi majira ya saa nne asubuhi ndipo bwana mmoja mwenye kitambi alifika, alikuwa katika mwendo wa taratibu. Lameck akasimama na kumpigia saluti.

    Akaruhusiwa kuingia ofisini.

    Baada ya salamu za awali. Likafuata kubwa aliloitiwa.

    Ilikuwa safari ya kuelekea Sudani kusini, safari ya kijeshi kwenda kulinda amani ambayo ilikuwa imetoweka kabisa kutokana na mapigano ya ana kwa ana huku waasi nao wakiwa wamechachamaa sana. Tanzania ikiwa mojawapo katika nchi zilizo katika umoja wa mataifa, kulindana ilikuwa mojawapo ya kanuni!!



    Mapigo ya moyo ya Lameck yalienda kasi lakini alijitahidi sana kujificha ili mkuu wake asiugundue udhaifu huo. Ni kosa kwa mwanajeshi kuonyesha uoga mahali popote pale.

    Kwa Lameck ilikuwa kawaida kufanya mazoezi ya kulinda amani lakini sio kuilinda kweli.

    Sasa alitakiwa kwenda kuilinda katika nchi yenye hatari kali, raia wanaomiliki bunduki hovyohovyo na pia waasi wasiokuwa na huruma na wanaowachukia sana askari wa umoja wa mataifa wanaoletwa kulinda amani.

    “Wewe na wenzako arobaini na nne mtaiwakilisha Tanzania vyema katika nchi hiyo inayokaliwa na waafrika wenzetu....mtakuwa na maandalizi ya siku saba tu. Siku mbili za kuaga wanafamilia, siku nne kwa ajili ya semina fupi ikiwemo makabidhiano kisheria katika serikali ya Sudani na siku iliyosalia ni siku ya safari” alielezea bwana yule huku akiukuna upara wake kwa kutumia kalamu.

    “Ni jambo la kifahari sana na la kujivunia kwenda kuiwakilisha nchi yako katika nchi nyingine, nakupongeza sana bwana Lameck.....” alimaliza kwa kutabasamu.

    Lameck hakuelewa kabisa hizo pongezi ni za nini hasa. Maana kilichokuwa mbele yake ni hatari tupu. Na bado anaambiwa hongera.

    Kidogo aulize swali lakini akakatishwa.

    “Wenzako nimezungumza nao tangu usiku wa jana na leo jioni mtakutana kwa pamoja kupongezana.”

    Maongezi yakaishia pale na Lameck akaruhusiwa kuondoka. Akasimama akapiga saluti ambayo haikujibiwa.

    Safari yake ya kurejea katika makazi yake haelewi kama iliongezeka masaa kadhaa ama ilikuwa imepungua. Hakuelewa kama aliwahi kufika nyumbani ama alichelewa.

    Hakika alikuwa amechanganyikiwa. Na hakuelewa kabisa ni nini kinapita katika kichwa chake.

    Alijaribu kulala lakini usingizi ukagoma kuja.

    Akiwa hana hili wala lile simu yake ya kiganjani iliita.

    Alikuwa Tino, rafiki yake ambaye walijiunga jeshi pamoja.

    “Sema kaka.....vipi nawewe umo kwenye hilo zali..” Tino aliuliza huku akiwa na kimuhemuhe cha kujua kama rafiki yake naye yumo katika orodha.

    “Nimo kaka na wewe je?” alijaribu kuchangamka Lameck.

    “Daah kaka nina furaha hapa asikwambie mtu...nimo kaka....yaani siamini ujue....kaka manyota hayo manyota yanatuangukia.” Tino alizidisha furaha yake.

    Lameck akakata simu kisha akazimisha kisha kimyakimya akamtusi Tino.

    “Mpumbavu nini huyu anachekelea kufa au...manyota manyota mshenzi kabisa....” akasonya kisha akaendelea na mawazo yake yasiyoeleweka.

    Lameck alikuwa anaogopa kufa!!

    Muda nao ukazidi kuyoyoma lameck akiwa hajui la kufanya. Kuna wakati alifikiria kutoroka lakini mwisho akagundua ni ujinga na aibu sana kwake.

    Kama rafiki zake wanafurahia kwa nini na yeye asiwe na furaha.

    Lameck akajivika ujasiri akaiwasha simu yake.

    Akampa baba yake taarifa hiyo, mzee wake ambaye zamani alikuwa jeshini akampongeza. Jambo ambalo lilimpa nguvu zaidi.

    Akiwa amechangamka kabisa alianza kupanga ratiba za kuaga watu wa muhimu ndani ya siku mbili walizokuwa wamepewa.

    Katika orodha jina la kwanza kabisa likawa Emmy wa James. Aliamini kuwa alikuwa na kila haja ya kuagana na binti huyu ambaye ni yeye aliutoa usichana wake.

    Akampigia simu ya dharula wakazungumza kwa kifupi.

    “Kesho nikitoka hospitali tukutane, lakini isiwe kwako tafadhali.” Emmy akakubaliana na Lameck.

    Siku iliyofuata wawili hawa wakakutana huku Lameck kwa kuangalia asiitie ndoa ya emmy katika utata alimtumia rafiki yake mwingine ambaye pia ni mwanajeshi kumpokea Emmy.

    Ilikuwa ni heri agundulike Emmy anamsaliti James kwa bwana mwingine lakini sio kwa baba yake mdogo.

    Zoezi likakamilika, wawili hawa wakaonana, Lameck akaagana na Emmy katika namna ya kuchukiza.

    Kufanya uzinzi!! Baba na mwana

    Walidhani kuwa ile ilikuwa siri kubwa lakini kuna kijana wa kileo ambaye amejiajiri katika kufuatilia mambo ya watu bila kujua nini faida yake.

    Jose B waukweli alikuwa shuhuda. Bahati mbaya kwao hawakuweza kugundua janja ya bwana huyu kutoka kanda ya ziwa jiji la Mwanza.

    Emmy alilia sana, kwanza kwa furaha kisha baada ya tendo akalia kwa uchungu kwa mambo ambayo alikuwa akimfanyia James.

    “Lameck...naomba hii iwe mara ya mwisho tafadhali nakuomba...James ananipenda sitakiwi kumlipa hivi ninavyofanya”

    “Usijali hata mimi nilitaka kusema hivyo hivyo...” Lameck alijibu kinafiki.

    “Isitoshe nina mimba yake tayari, sitaki kumtenda vibaya huyu mtoto...” Emmy alikazia akidhani jambo hilo litamuua nguvu Lameck. Lakini badala yake likamshtua.....

    Lameck hakutaka kuhoji sana....kuna mjadala ukazuka kichwani mwake. Mjadala ambao aliuanza tangu siku Emmy alipomwambia kuwa alikuwa na kichefuchefu baada ya kutumia dawa za kurejesha bikra iliyopotea.

    Lameck akaguna . hakusema neno zaidi.

    Baadaye waliagana huku Emmy akimtakia mema huko anapoenda.

    Jicho la Jose B lilimsindikiza binti huyu hadi alipotokomea kuelekea ambapo Jose b hakuhitaji sana kupatambua kwa wakati ule.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tayari alikuwa ana namba za simu.

    Baada ya juma moja Lameck na wanajeshi wengine walikwea ‘pipa’ wakaipasua anga kuielekea nchi ya Sudani.

    Lameck akijiahidi kuwa baada ya kurejea nchini atafuatilia juu ya hiyo mimba ya Emmy.

    Hakutaka kuweka hisia kuwa huenda anahusika nayo. Aliamua kujipa muda zaidi, pia hata kama angekuwa anahusika naye bado asingeweza kumuhitaji mtoto kwani ni skendo ya baba kuzaa na mwanaye.

    Aibu kubwa.



     Wakati Lameck anakwea pipa. Jose B yeye alikuwa katika siti ya basi akiwa ameketi na baba yake mzazi wakirejea katika jiji la Mwanza, Jose B alikuwa amepona kabisa.

    Mzee Boniphace hakujua lolote ambalo lilipita katika kichwa cha mwanaye.

    Jose B alikuwa akiliwaza jiji la Dar es salaam na kuliona kuwa jiji zuri sana kibiashara.

    Si biashara ya nguo wala vyakula.

    Biashara ya umbea. Aliona kuna kila dalili jiji hilo likatoa neema kwake.

    Hakumweleza mtu yeyote juu ya pesa alizokuwa amebakisha katika chumba chake katika godoro jijini Mwanza. Hakutaka kuulizwa maswali mengi. Akiwa katika kuwaza alizipigia mahesabu kuwa akifika anazichukua kisha anasafiri peke yake kurejea jijini Dar es salaam kwa ajili ya kufanya biashara ya umbea. Hasahasa kwa wateja wake wakuu, James na mkewe ambaye hadi wakati ule alikuwa hajalifahamu jina lake.

    Waliwasili Mwanza majira ya saa tatu usiku. Moja kwa moja wakaelekea nyumbani.

    Mama Jose aliwapokea kwa mashamushamu huku akimkumbatia Jose b ambaye aliondoka jijini Mwanza akiwa katika machela.

    Sasa alikuwa amepona.



    Jose B alipofika katika nyumba yao ndipo alipata jawabu la ni wapi ilitoka pesa ya kumsafirisha hadi jijini Dar kwa ajili ya matibabu.

    Kabati la vyombo, luninga, jozi ya sofa, kompyuta na vitanda viwili. Vyote havikuwa pale ndani. Viliuzwa Jose B aweze kutibiwa na kupona kabisa.

    Roho ikamuuma Jose. Alipoingia chumbani kwake moja kwa moja alitazama kitanda.

    Hapakuwa na lile godoro lake alilolitambua, bali palikuwa na mfano wa godoro, ambalo limechakaa na halifai tena kulaliwa.

    “Mama....godoro langu....” aliuliza huku akiwa amehamaki Jose B.

    “Godoro lako? Lipi tena na ulinunua lini?” alijibu huku dhahiri akionyesha kukereka.

    “Mama naulizia godoro lililokuwa chumbani kwangu....”

    “Mguu wako na godoro kipi bora?? Pumbavu wewe!!” mama akauliza swali na tusi juu....Jose B akauma meno kwa ghadhabu, na alikuwa ametaharuki. Ndani ya lile godoro kulisaliwa na takribani milioni moja na laki tano.

    Sasa halipo lile godoro.

    Kizuizi!!



    Mama akatoweka akimwacha Jose B akihangaika kujiuliza na kujipatia majibu. Majibu ambayo si sahihi.

    Usiku ule ulipita Jose akibakia kuwa mlinzi wa familia. Hakulala kabisa, alilia machozi kama kuna msiba ulitokea.

    Muda wote aliotumia kuzisaka pesa zile, sasa hana hata senti.

    Inauma sana.

    Harakati za Jose B kurejea jijini Dar kwa ajili ya kufanya biashara zikaanza kupotea.

    Atatoa wapi nauli, atatoa wapi pesa ya kuishi jijini Dar wakati akifuatilia biashara yake??

    Kizuizi kikubwa sana.........



    Jose B, mlinzi bila silaha alikurupuka na kuanza kufagia uwanja majira ya saa kumi na moja na nusu. Hakuwahi kufagia kwa sababu alikuwa anapenda usafi. La alikuwa amepagawa bado. Hakuamini kama milioni na ushee zilikuwa zimeuzwa sanjali na godoro.

    Huenda liliuzwa elfu hamsini. Elfu hamsini pamoja na milioni kadhaa, biashara nzuri kupita zote duniani. Lakini muuzaji ni mmoja kati ya watu washenzi kupata kutokea duniani.

    Jose B aliendelea kulalamika hovyo hovyo, mara atupe uchafu ambao ameuzoa tayari.

    Kijana alikaribia kuchanganyikiwa.

    Alijipekua mifukoni, mara arudishe alivyovitoa awali na kuvihamishia katika mfuko mwingine. Alisikitisha sana. Pesa asiyoitolea jasho ilimuhuzunisha.

    Katika kujipekuapekua mara alifanikiwa kukamata simu kutoka katika mojawapo ya mifuko yake.

    Ilikuwa simu yake.

    Kuitazama simu ile mara ikarejea na kumbukumbu ya jiji la Dar es salaam. Akazikumbuka namba zilizotajwa katika mojawapo ya chumba katika nyumba za kulala wageni jijini humo.

    Namba za mke wa James ambaye alikuwa akiisaliti ndoa yake ambayo hata haikuwa na miezi miwili, Jose B akaanza kuziimba zile namba kama mtoto mdogo anayekariri alfabeti.

    Dili!!

    Akalipuka kwa furaha Jose B, na kisha kujiaminisha kuwa huenda yeye ni mzuka uliofufuka.

    Kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu Jose B akaiwasha simu yake.



    ***



    Nyumba kubwa ya vyumba vitatu pamoja na sebule ilionekana kupwaya sana kwa kukaliwa na watu wawili. Furaha ilikuwa kubwa kutokana na kumngojea mzaliwa mpya.

    James na Emmy wote kwa pamoja waliungoja ujio wa mtoto katika nyumba yao.

    Kila mara walizungumzia juu ya mtoto, mwingine angesema atazaliwa wa kiume mwingine alisisitiza kuwa lazima awe wa kike.

    Simu iliyoita ilikatisha ubishi huu ambao haukuwa na dalili za kumalizika.

    Ilikuwa simu ya Emmy.

    James akajongea kuifuata akaitazama, ilikuwa namba mpya kabisa.

    Akamshirikisha mkewe.

    Emmy akamwomba apokee.

    “Hapana ...sio utaratibu mzuri mke wangu....je kama ni rafiki zako watajifikiriaje??”

    Jimmy akapinga.

    Emmy akakubaliana naye, lakini kabla simu haijapokelewa ikakatika baada ya kuwa imeita kwa muda mrefu.

    Walingoja huenda angepiga tena. Hakupiga.

    Wakaendelea kupata chakula huku ubishi wao ukisahaulika.



    Baada ya chakula. Emmy akiwa uani akiosha vyombo akasikia tena simu yake ikiita.

    Safari hii, James alikuwa amelala hakuisikia.

    Emmy akaitwaa. Namba nyingine tena.

    Akapokea.

    “Mambo shem....”

    “Poa vipi..” alijibu kwa mkato sana.

    “Huku kwema..mimi ni...hauwezi kunijua jina lakini nilikupokea siku ile ulipokuja kwa Lameck.....” alijitambulisha. Emmy akawa amemkumbuka. Mapigo ya moyo yakaenda kasi sana.

    “Nimekukumbuka nambie....”

    “Nilikuwa nakusalimia tu...Lameck amewasiliana na mimi akanipatia namba yako nikusalimie..alifika salama..” Simu ikakatwa wakati huyu bwana anaendelea kutoa hizo salamu.

    Emmy hakutaka kusikia chochote juu ya Lameck japo katika nafsi yake alikiri waziwazi kuwa yule bwana anajua kukipendezesha chumba kuliko mumewe.

    Lakini hakuwahi kumwonyesha mumewe kuwa anachukizwa na jambo hilo.

    Emmy akiwa bado amenuna huku akihema juu juu mara ikaingia simu nyingine.

    Namba mpya tena.

    Akaitazama na kuwaza kuwa huenda ni yule yule bwana amepiga. Lakini akapingana na hisia zake akaipokea ile simu.

    Sauti inayojiamini, ya kiume ikatawala kutoka upande wa pili.

    “Mambo shem.” Salamu kama ya awali lakini sauti tofauti.

    “Poa nani samahani.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Unaongea na......eeh samahani mumeo yupo hapo jirani?”

    “Anahusika vipi katika maongezi haya..” Emmy aliuliza huku akiizuia jazba yake kutokana na swali lile.

    “Hausiki hata kidogo ndo maana nimekuuliza kama yupo nisitishe simu hii ili tuzungumze baadaye.”

    “Ongea tu...umeniita shem halafu unamuhofia mume wangu nini tatizo?”

    “Tatizo ni haya maongezi mafupi kati yangu na wewe.”

    “Kwanza wewe nani kwa jina.

    “Sam wa pili.”

    “Mh!! Ninadhani hatufahamiani.”

    “Yeah. Lakini maongezi haya yatakuwa mwanzo mzuri wa kukumbushana wapi tulipoonana shem wangu.”

    “Wapi tumeonana?” sasa alikuwa ameshindwa kuizuia jazba, sauti kali ikamtoka.

    “Ubungo....Ubungo Dar es salaam.” Sauti ya kiume ilijibu pasipo kujiamini sana.

    “Ubungo kubwa kakangu ni mwaka gani..ongea ueleweke basi..”

    “ZamZam guest house, unapakumbuka.”

    “Nadhani umekosea namba...samahani nipo katika ndoa naomba uniheshimu tafadhali.”

    “Haya nakutakia siku njema, msalimie mumeo mwambie kuna jamaa anaitwa Sam wa pili alikuchungulia wakati unatoka hospitali, kisha ukaenda Ubungo kufanya uzinzi na jamaa....na kama ikibidi mpatie namba yangu ili nimueleze vizuri picha zima lilivyokuwa, bahati nzuri nakumbuka hadi nguo yako ya ndani ilikuwa ya rangi gani, na maongezi yenu nilirekodi......sikia dada sio siri unajitahidi sana. Japo nimefanikiwa kukuona mara moja tu nimeamini kuwa unajua sana haya mambo......amakweli James amelamba dume. Vipi bado unahitaji heshima?” alimaliza mazungumzo kwa mbwembwe huyku akimuachia uwanja mwanadada Emmy wa kujifalagua kama alivyoanza awali kwa kujiita kuwa yupo katika ndoa. Emmy kimya, pumzi zikipishana kwa kasi, miguu ikiwa imeishiwa nguvu na glasi aliyokuwa ameshika mkononi ikiwa imeanguka chini, ilikuwa bahati kuwa haikuvunjika.

    Emmy hakuwahi kutegemea kuwa anaweza kupigiwa simu kama hii na kuelezwa habari nzito kama hizi zisizokuwa na hata chembe ya uongo ndani yake.

    Binti wa watu akapagawa. Akataka kusema neno lakini atasema neno lipi.

    “Mama James nakusikiliza....” upande wa pili ukauliza kwa sauti tulivu.

    “Samahani....naomba kama unaweza tuonane pliiz.....nisaidie kaka yangu nisaidie jamani...’

    “Ndo maana nimekuomba umpe James hii namba ili niweze kukusaidia kumsimulia ile filamu ambayo umeicheza halafu ukaishiwa vocha ukamuomba kidume akurushie.....” Maneno makali na yenye kuumiza yalizidi kushambulia katika namna ya utani.

    Emmy akakimbilia katika choo cha nje akajifungia humo kisha akaendelea kuongea.

    “Jamani kakangu pliiiz...ndo kwanza nina mwezi katika ndoa yangu nakuomba tafadhali nakuomba tuonane..nitakupa utakacho tafadhali....nakuomba kaka nipo chini ya miguu yako..nakuomba kaka nisikilize kaka nakuomba....” Emmy alisihi kwa kila namna.

    “Nitakupigia......msalimie mumeo.” Aliyamaliza mazungumzo haya katika namna ya kipekee, alikuwa kijana yuleyule ambaye anafanya mambo ambayo ukisimuliwa huwezi kuamini. Lakini nani atakusimulia iwapo anayafanya bila kumshirikisha mtu?? Akili yake aliijua yeye mwenyewe. Jose B waukweli. Kijana wa Mwanza.

    Jose B baada ya kumsikia mwanadada yule akitetemeka alianza kuzisahau shida zake, kauli ya yule dada kuwa atampa chochote kwa kumuokolea ndoa yake ambayo haijakomaa bado ilimpa nguvu sana na kuamini kuwa hana haja ya kujutia zile milioni zilizouzwa pamoja na godoro.

    Jose B akajiweka katika kundi la washindi, kundi lisilojua lolote juu ya kushindwa.

    Jose B akawa kinara.

    Sasa alikuwa katika nafasi ya kumuongoza mwanadada emmy kwa namna aliyotaka yeye.

    Jioni ya siku hiyo akampigia tena simu, wakafanya mazungumzo marefu katika hali ya utulivu. Mazungumzo haya kwa maneno yalitawaliwa na Jose B. Emmy akawa msikilizaji tu.

    Wakafikia maelewano.



    ***



    Hali ya amani ilikuwa hafifu kiasi fulani. Raia hawakuwa na amani na serikali yao kabila la Dunka lilikuwa linaongoza kwa kupoteza mamia ya watu katika machafuko hayo.

    Nyumba za tope zilikuwa zimesambaratishwa kwa wingi na mamia ya watu kukosa makazi.

    Hali ilikuwa tatanishi.

    Ni familia chache sana zilisalimika bila kuwa na misiba.

    Ilikuwa afadhali kwa upande mwingine wa Sudan kuliko upande wa Sudani ya kusini. Hali ilikuwa tete zaidi.

    Maisha yalikuwa duni sana. Na asilimia kubwa hawakuijua kesho yao.

    Mindombinu haikutiliwa maanani na serikali, macho ya wanajeshi yalikuwa yakitazama hali hii.

    Lameck akiwa mmoja wao, gari la kijeshi lilikuwa linayumbayumba katika barabara mbovu kabisa katikati ya mji.

    Lameck alijiuliza kulikuwa na umuhimu gani wa kugunduliwa kwa uvunaji wa mafuta katika ardhi ya Sudani mwaka miaka ya 1978. Mafuta hayo hayakuleta mabadiliko yoyote katika ardhi ile zaidi ya raia kuendelea kugandamizwa na kuteseka.

    Lameck alifumba macho na kukumbuka maeneo mbalimbali kama mkoa wa Mara nchini Tanzania, akauweka katika rada mgodi wa Nyamongo.

    Kisha akafumbua mamcho na kusema ‘yaleyale’.

    Hakika yalikuwa yaleyale.

    Gari lilisimama, kiongozi wa msafara akawagawanya wajeshi hao waliokuja kwa lengo la kulinda amani katika vikosi mbalimbali. Kisha wakatawanyika, silaha mkononi.

    Hapo ndipo uoga ulipomuanza Lameck.

    Katika giza nene, hali tulivu inavurugwa na waasi. Milio inaanza kusikika, kila mwanajeshi anajiweka tayari huku akipokea ishara kutoka kwa mkuu wa msafara.

    Siku ya kwanza ikapita, ya pili na ya tatu....hatimaye hali ile ya waasi kutokea na kutoweka ikaanza kuonekana ya kawaida tu kwa wanajeshi wageni.

    Mazoea hujenga tabia. Lameck naye akazoea na kujiona jasiri sana huku akishangaa ilikuwaje akaijutia nafasi kama ile ya kuliwakilisha taifa kisha akirejea anakuwa na nyota ya ziada na heshima kubwa kama shujaa.

    Ikafikia siku isiyosahaulika kirahisi, siku inayotia huzuni na kuihamisha simulizi mahala pasipotarajiwa.

    Lameck alivutiwa kuitazama jamii ya watu kadhaa waliomzunguka, maisha yao yakiwa kulala nje ama katika mahema. Hawakuwa na makazi.

    Suala hili lilimgusa sana, alijisikia kama yu mmoja wao.

    Mwanamke mmoja ambaye anazeeka kutokana na shida lakini akiwa ni kijana anamtazama Lameck kwa macho makavu lakini sura inayolia.

    Lameck anamsogelea na kumuuliza anaitwa nani, anajaribu kutumia kiingereza yule binti hamjibu kitu.

    Anamkazia macho tu.

    “She’s from Nuer tribe” (Ni wa kabila la Nua). Mhanga mmoja wa vita hii, kijana wa umri usiozidi miaka kumi na tisa anamweleza yule mwanajeshi kamili.

    “So you may speak English. (Kwa hiyo unaweza kuzungumza kiingereza) ” Lameck anamuuliza yule kijana naye anakubali.

    Mazungumzo yanaanzia hapo. Yule binti anamfanya Lameck ajisahau kuwa yupo katika kulinda amani na kujikuta kama muhanga pia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Simulizi ya binti yule inamfanya Lameck kuliacha lindo lake na kuongozana na yule binti mpaka eneo la nje kidogo ya mji.

    Waliongozana na yule mtafsiri wao.

    Huku walimkuta yule mwarabu ambaye anamyanyasa yule dada kijinsia, anawanyayasa na wadogo zake ili tu aweze kuwapatia chakula.

    “Huwa ananiingilia na wenzake kadri wanavyotaka. Huwa ananipiga sana na wakati mwingine huniita sokwe. Alimuua mama yangu alivyojaribu kunitetea na alimnyonga baba....” hapa sasa hakuweza kusema lolote zaidi ya kulia.

    Yule mwarabu hakutegemea ujio wa yule dada akiwa pamoja na mwanajeshi wa umoja wa mataifa lakini ana kwa ana na Lameck.

    Lameck, hakuwa mzoefu wa vita. Na pale lindoni aliambatana na wakongwe ambao alitakiwa kujifunza kwao.

    Huku kuwa peke yake na kuweka ubinadamu mbele kulimgharimu.

    Jicho la Lameck lilishuhudia kifua cha yule dada kikisambaratishwa mara moja.

    Wakati anajiweka sawa kukabiliana na shambulizi linalofuata. Ghafla likatokea tukio asiloritarajia. Tukio lililoibadili historia ya maisha yake!!

    Alichokiona mara ya mwisho kabla ya kiza kinene ni uso wa yule mwarabu ukitabasamu.

    Kisha akausikia mlio wa bunduki.

    Kiza kinene kikatanda, harufu ya damu ikatawala.

    Kimyaa!!



     Shughuli anayoifanya akaichukulia kuwa ni moja kati ya kazi bora kabisa kuwahi kutokea duniani.

    Hakuamini kama alikuwa ni yeye ama la.

    “Na hapa hata mkiaka thelathini bado.” Aliwaza wakati wakipokea maelekezo ya jinsi ya kufunga mikanda.

    Alijiona mshamba sana kwa kudhani kuwa mikanda ndani ya ndege ni rahisi kufunga kama kwenye gari. Huku palikuwa na maelekezo tofauti kiasi.

    Jose B wa ukweli akiwa anakwea usafiri huu wa anga kwa mara ya kwanza alikuwa mwenye furaha ya kipekee.

    Hakuwa amemuaga mtu yeyote na alitegemea kufika jijini Dar na kurejea siku chache baada ya kumaliza biashara iliyompeleka.

    Jose B akiwa katika kuitafakari safari hii. Kama iliyo kawaida alianza kujipangia ni kiasi gani ambacho atamtoza mwanadada Emmy kwa kumfichia siri ambayo anaimiliki.

    Kwanza alitaka kufanyia bei chee lakini alipokumbuka kuwa alikuwa ametoka kupata hasara baada ya pesa aliyoitumia kuuza kizuizi kupotea kirahisi aliamua kumpangia bei ya juu.

    “Milioni saba...na wala sifanyi aina yoyote ya mazungumzo ya kupunguza....kama hataki aache nitaiuza pengine...” Jose B aliwaza kwa tuo, kana kwamba ilikuwa biashara halali.

    Akiwa hata hajapata wazo jingine, ndege ilitua katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa mwalimu nyerere jijini Dar es salaam.

    Jose B akafuatisha ambayo wenzake walikuwa wanafanya.

    Hatimaye akatoka nje.

    Akiwa anashangaa shangaa akijiandaa kuiwasha simu yake ambayo aliizima akiwa anakwea ndege. Mara alisita baada ya kuona kama yu katika ndoto.

    Binti mrefu wa wastani mwenye umbo lililojikata vyema na kuunda mfano wa namba nane alimkaribia huku akitabasamu.

    “Karibu Sam wa pili.” Alisema yule binti kisha akamuongoza Jose B katika gari iliyokuwa inawasubiri.

    Wakajibweteka katika siti ya nyuma.

    Dereva ambaye hapo kabla alikuwa amepewa maelezo ya wapi wanaelekea alifanya kama alivyoagizwa. Moja kwa moja hadi Kijitonyama katika hoteli ya Grand Villa.

    Chumbani.

    Jose B akiwa hana hili wala lile, Emmy akiwa na mambo mengi yanayopita katika kichwa chake.

    Mshikemshike!!



    Jose B hakuwahi kugundua kuwa ana matatizo. Alikuwa akiyasikia matatizo haya kwa wengine na aliyachukulia kama simulizi zenye mvuto lakini zisizokuwa na ukweli ndani yake, na wahanga wa simulizi hizi aliwachukulia kuwa ni viumbe dhaifu ambao hawafai kuwa mfano katika jamii.

    Sasa naye anajikuta anaangukia kulekule.

    Macho yake yalikuwa yanatazamana na macho murua yaliyojawa na aibu, midomo iliyojilazimisha kutabasamu nayo ilipendezesha uso huu usioitangaza hatia yake waziwazi.

    “Karibu Sam.” Sauti ilimwambia. Mapigo ya moyo yakapanda maradufu. Jose B mtegoni.

    “Nimekaribia nimekaribia...”

    “Nipo hapa kwa ajili ya kufanya biashara na wewe. Tafadhali nakuomba sana unachokijua ama ulichokiona kibakie kuwa siri yako pliiz...” Emmy akamsihi Jose B.

    Kijana wa Mwanza akaachia tabasamu mwanana, tabasamu lilidhihirisha ufahari wa kunyenyekewa na mtoto wa kike mwenye hadhi ya kuitwa mrembo.

    “Nakusikiliza....tangaza dau maana ni biashara hii.” Alijaribu kujilazimisha kuwa jasiri lakini hakuweza aliongea kutimiza tu wajibu.

    Emmy akafanya tabasamu la karaha lakini linalopendeza kulitazama.

    Jose B naye akatabasamu.

    Lile wazo la kumgalaliza mrembo huyu bei ya milioni saba, liliyeyuka bila kupata mbadala wake. Kuondoka kwa wazo hilo kukaingiliwa na wazo jingine matata.

    Kwanza Jose B alihisi ni jambo gumu sana kuweza kutimizwa, lakini akajipa moyo kuwa ni afadhali wazo hilo kuliko wazo la kuomba pesa.

    “Mimi ni mgeni jijini Dar natoka huko nilipotoka. Kikubwa ili tuimalize biashara hii vizuri. Nahitaji nyumba. Nahitaji mahali pa kuishi, nahitaji unipangishie nyumba inayoendana na hadhi ya siri hii nitakayoificha.” Alizungumza kwa utulivu.

    Emmy aliendelea kuwa msikilizaji. Kabla hajasema lolote, Jose B aliendelea, “Na ninakusihi usijaribu kufanya ujanja wowote, wenzangu hawana roho ya huruma kama mimi ya kumsikiliza mtu. Kwa hiyo ukifanya masihara nawaachia jukumu hili wao.” Jose akamtahadhalisha Emmy.

    Binti yule akatii.

    Biashara ikamalizika huku Jose B akimpa Emmy majuma mawili kuandaa nyumba yenye hadhi yake.

    Hadhi ipi? Ushakunaku labda.



    ****



    Gari moshi kutoka mkoa wa Kigoma liliwasili maeneo ya stesheni majira ya saa nne usiku. Abiria walikuwa wamechoshwa na safari lakini hawakuwa na jinsi kwani uwezo wa kulipia nauli ya basi kuelekea jijini Mwanza hawakuwa nao.

    Kila mmoja alishuka kwa namna yake. Mwingine alikuwa na mizigo, mwingine alikuwa na watoto huku vijana wengine wakiwa na bahasha ama vifuko vidogo.

    Tofauti na akina mama wengine ambao walikuwa na hekaheka nyingi sana wakati wa kushuka, alibaki mwanamke mmoja ambaye hakuwa na haraka.

    Huenda hakuna ambaye angekuja kumpokea ama la hakuwa imara kiafya hivyo hakutaka kusongamana mlangoni.

    Baada ya abiria wote kutelemka, na yeye alijikongoja akaikanyaga ardhi ya Mwanza. Alitazama kushoto na kulia kama vile kuna kumbukumbu anajaribu kutafuta.

    Watu walizidi kupungua, wengi wakiondoka na usafiri wa daladala kuelekea wanapopajua wao.

    Hakuwa mwanamama wa makamo sana. Lakini shida ndizo zilimfanya aonekane amezeeka. Baada ya kufanya tafakari ya muda mrefu, hatimaye alijikongoja katika kibanda kilichopo nje ya stesheni, akanunua maji ya kunywa saizi ndogo. Wakati anakunywa alimuuliza mwenye kibanda hicho. Mwenye kibanda akatoa ushirikiano wa hali ya juu.

    Mwanamama akatoweka.

    Akapanda daladala kama alivyoelekezwa

    Alikuwa mkimya sana kama anayewaza makuu.

    Ulikuwa ni usiku na barabara zilikuwa wazi sana. Aliwasili mapema sana mahali alipoelekezwa. Akatumia dakika takribani kumi kutafuta nyumba ya kulala wageni. Akalipia akaingia chumbani.

    “Umeme upo vyumbani?” alimuuliza muhudumu. Muhudumu akamjibu kuwa upo.

    Alipoingia chumbani akawasha taa, akaufunga mlango kisha akautoa mkoba wake na kunyofoa karatasi chafu lakini iliyotuzwa kwa uangalifu mkubwa.

    Alipoikunjua lilikuwa ni gazeti la Kiswahili, chakavu na ni kama lilitupwa na kusahaulika kisha kwake likawa na umuhimu mkubwa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alipolikunjua akakutana na kile kilichomtoa katika Kigoma na kumleta katika jiji ambalo hakuwahi kutegemea kufika. Ilikuwa picha inayoonyesha nyuso mbili zenye furaha. Picha hiyo ilipambwa na maandishi yaliyowasifia kwa kupendeza maharusi hao.

    James Syaga Magayane na Emmy John.

    Mwanamama yule akafanya tabasamu kisha akaikazia macho zaidi picha ya Emmy.

    Akatokwa na machozi.

    “Mzee Magayane. Huyu mzee huyu...huyu..kumbe alikuwa anajua kila kitu akanilaghai kuwa nivute subira..” alinung’unika kwa sauti yenye kila dalili ya shari. Kisha akakikunja kigazeti akalala.

    “Huyu bwege naye eti anajiita James....” lilikuwa neno lake la mwisho kabla hajasinzia.



    ***



    Jose B waukweli akiwa katika chumba kingine katika hoteli nyingine ya kifahari pia alikuwa anagalagala kitandani huku akiendelea kuifurahia kazi yake iliyomleta jijini Dar.

    Mawazo yakapita katika kichwa chake.

    Akaanza kufikiria juu ya maisha yake mapya. Akaiwaza familia yake.

    “Hapa nikishapata hiyo nyumba kitu cha kwanza namtuimia dogo nauli anakuja kusomea Dar, halafu baadaye namchukua maza na mshua....hapo heshima lazima..ujue watu wananidharau sana we ngoja yaani....” akiwa anazungumza peke yake kwa hisia kali za ukombozi. Mara simu yake ikaita.

    Ilikuwa ni namba mpya. Akapokea kwa ujivuni.

    “Jose B naongea nani mwenzangu....”

    “Fundi hapa...kuna dili kaka kama upo home....”

    “Dili gani...”

    “Ongea naye huyu hapa....”

    “Mambo vipi kaka.....” sauti ya kike ikapenyeza, Jose B akatulia kumsikiliza.

    “Mimi ni mgeni jijini Mwanza nahitaji mtu wa kunizungusha mjini kwa malipo.

    Nimeambiwa nizungumze nawe.”

    “Una bei gani....”

    “Tutazungumza mimi na wewe....”

    “Basi nitakupigia..hii namba ni ya kwako?”

    “Ndio ni yangu. Nashukuru sana.”

    Baada ya kukata simu Jose B akazidi kuhamasika na kazi yake hiyo ya kujua mengi. Tazama sasa anatafutwa kwa ajili ya kumzungusha mtu katika jiji la Mwanza.

    Naelekea kuwa maarufu. Aliwaza Jose B.

    Alipotulia aliitwaa simu yake akampigia Emmy.

    “Nimeitwa Mwanza kikazi tafadhali naomba ufanye mpango wa safari yangu kisha nikuache ukiendelea na mpango wetu wa awali.” Hakusubiri majibu. Akakata simu, alikuwa na uhakika kuwa anammiliki Emmy kwa asilimia zote.

    Kama alivyotaraji, baada ya siku mbili alikuwa katika usafiri uleule wa awali akirejea jijini Mwanza.

    Kitu cha kwanza baada ya kufika jijini akiwa tayari amepewa pesa ya kutosha na Emmy kama kishika uchumba cha biashara yao. Jose B alikuwa ana kila sababu ya kutembea huku akinesanesa.

    Wazazi ambao myumbo wa kiuchumi uliwaathiri na kuwafanya wasahau kuhusu familia waliamini kuwa Jose B ameamua kuwa analala kwa rafiki zake kisa tu nyumbani hakuna godoro.

    Mke na mume walimlaani Jose na kumuona kama mtoto asiyekuwa na staha hata kidogo huku akionekana kutaka maisha ambayo muda wake haujafika.

    Mama na baba Jose wakaamua kukaa kimya.

    Hawakuwahi kumpigia simu Jose B wala kumsisitiza mdogo wake amtafute.

    Hadi siku hii alipoingia nyumbani akiwa ameng’ara kuliko kila kitu kilichokuwa na thamani katika nyumba yao.

    Wazazi wakasahau kuwa walisema hawatamuuliza kitu chochote. Ghafla wakajikuta kwa pamoja wanapaparuka.

    “Ulikuwa wapi we Jose. Mbona kama ulikuwa umesafiri, Jose mwanangu.” Ilikuwa sauti ya mama. Baba naye akauliza.

    Hakuna aliyekumbuka kumkumbusha mwenzake.

    “Nilikuwa hapo Dar mara moja kikazi na hata hapa nimerejea kikazi tu.” Jose alianza kuweka tambo zake hadharani huku akijikuna vindevu vichache kidevuni.

    Wazazi macho yakawa yanawatoka tu.

    Jose B hakuwa na subira, mara akafungua begi lake akachomoka na kitita.

    Akajisahau kuwa wale ni wazazi wake, akawafananisha na wadogo zake na wao wakajisahau kuwa ni wazazi wakanyenyekea.

    PESA BWANA!!!



    Pesa ikamwagwa, ya kununua godoro, luninga, na madikodiko yote yaliyouzwa ili Jose B aweze kutibiwa. Amakweli mwenye nacho huongezewa, katika kusheherekea hizo pesa mara mama mtu akaingiwa na roho ya ubahili badala ya kununua godoro jipya kama bosi Jose alivyoagiza akadai kuwa anaenda kukomboa lile godoro aliloliweka kwa mkopo kwa mama Saidi.

    Lahaula! Godoro likarejeshwa kundini. Godoro lililomfanya Jose B arejee Dar kusaka pesa nyingine. Godoro la Jose B waukweli.

    Godoro lenye pesa.

    Mara waa! Pesa zilikuwemo.

    Furaha nyingine. Pesa zilikuwa zimeongezeka.

    Wazazi wakachachawa, cha ajabu hawakukumbuka kumuuliza Jose B ni kazi gani anayofanya.

    Laiti kama wangemuuliza huenda wangeweza kutoa ushauri. Bahati mbaya wakamuacha kama alivyo.

    Furaha ikarejea katika familia.



    ***



    Siku iliyofuata Jose B alimpigia mwanamama simu. Wakaonana.

    “Kwa siku utanilipa shilingi elfu sabini.” Jose B akamtangazia dau yule mwanamke aliyekuwa anataka kuzijua konakona za jiji la Mwanza.

    Wakafikia makubaliano na kuelewana kuwa watachukua siku sita katika zoezi hilo.

    Jose akapewa malipo ya utangulizi. Akatia mfukoni.

    Ama kwa hakika ulikuwa msimu wa Jose B waukweli.

    Mambo yalienda kama kawaida hadi siku hizo sita zikamalizika.

    Akamaliziwa malipo yake na mwanamke yule huku akimzidishia na nyongeza kwa kazi aliyomfanyia. Alipumzika kwa siku moja nyumbani kujiandaa na safari ya kurejea jijini Dar es salaam. Tayari kwa kuanza maisha mapya katika jiji hilo.

    Safari hii hakupokelewa na Emmy kama ilivyokuwa awali bali walifika watu walioagizwa. Alivyowauliza kulikoni Emmy hajafika ndipo alikutana na taarifa ya kusisimua.

    Msiba!

    Emmy alikuwa amefiwa na babamkwe wake.

    Waliompa taarifa hii hawakujua kama Jose B anamfahamu vyema mzee yule mwenye hekima.

    Ameuwawa kwa kupigwa na kitu kizito kichwani kabla ya kuchomwa visu tumboni na kifuani.

    Kifo cha kustaajabisha na kusikitisha sana.

    Kulikoni! Jose B alijiuliza.



    ***



    Walioagizwa kumchukua Jose B waukweli walielekezwa mahali pa kumpeleka ambapo atakaa na kumngoja mwenyeji wake.

    Jose B aliwaza kuwa huenda anapelekwa hotelini tena. Lakini haikuwa hoteli mara hii bali nyumba nzuri ambayo ilitawaliwa na samani mpya mpya.

    Akakaribishwa.

    “Sisi tunatoka kidogo amesema atakukuta hapa.” Waliaga wale wenyeji, Jose B akabaki peke yake.

    Maswali lukuki yakapita katika kichwa chake. Kuhusu kifo cha mzee Magayane pamoja na uwepo wake katika nyumba hii.

    Hakuamini kirahisi rahisi kuwa yule mtoto wa kike alikuwa ametimiza mara moja kile ambacho Jose B alikuwa amekihitaji.

    Majibu yake aliyapata usiku wa saa mbili, baada ya Emmy kuwasili nyumbani pale na kumkabidhi rasmi nyumba ile.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Imelipiwa kodi ya mwaka mzima pliiz Sam wa pili nakuomba sana usiniangushe ndoa yangu bado change sana.” Alizungumza kwa huzuni kuu huku macho yake yakiwa mekundu sana kutokana na kilio kikubwa baada ya taarifa ya kifo cha baba mkwe.

    Jose B akashikwa na imani huku udhaifu nao ukichangia akamhakikishia kuwa atakuwa naye bega kwa bega. Wakaagana, kwa mara ya kwanza Jose B akalala katika nyumba ya kifahari. Ikiwa katika milki yake.

    “Natamani mama angeniona hapa nilipo.” Aliwaza. Usingizi mwanana ukampitia.

    Alfajiri alidamka akiwa na wazo la kumpigia Emmy simu aweze kumuuliza kiundani juu ya msiba ule wa ghafla. Jose B alitaka kufahamu mawili matatu ili atii kiu yake.

    Alipopiga simu ya Emmy haikuwa inapatikana.

    Alijaribu tena na tena hali ikawa ileile.

    Wakati Jose akifanya jitihada za kumtafuta Emmy, mwanadada huyu alikuwa mkimya kabisa katika ndege iendayo Mwanza. Mambo kadhaa yakipita kichwani mwake, alikuwa akimuwazia Jose B waukweli kama ni kweli ataitunza siri ile kwa muda mrefu bila kuivujisha popote. Alimchukulia Jose B ama Sam wa pili kwa alivyojitambulisha kama mwanadamu pekee anayeweza kuiacha ndoa yake salama ama kuisambaratishia mbali.

    Kimya kimya akafanya dua huku akimwombea kijana huyu awe na moyo wa chuma.

    Kijana mtanashati aliyeketi kiti cha pembeni ya Emmy naye alikuwa amejikita katika kusoma jarida lililoandikwa katika lugha ya kiingereza, lakini cha kustaajabisha hakufunua kurasa kuendelea mbele. Alikuwa amekodolea macho ukurasa mmoja pekee. Akili yake haikuwa pale kabisa alikuwa anawaza mengi zaidi ya yule mwanamke.

    Alikiwaza kifo cha ghafla cha baba yake, tena kilichotokana na shambulio la kisu na kitu kizito.

    Atakuwa nani huyu? Alijiuliza.

    Akajaribu kufanya makisio lakini hakupata majibu. Ni sura gani ambayo mzee ameiona na kunipigia simu usiku? Alizidi kujiuliza.

    Ghafla akamkumbuka kijana aliyemuuzia siri ya kizuizi. Alimkumbuka kwa sababu alikuwa ni mpenda kujua mengi hata yale yasiyomuhusu.

    Jose B waukweli.

    Nikifika Mwanza namtafuta. Huenda anajua chochote.

    James alifikia maamuzi ya kujaribu kama atapata lolote kwa kijana yule.

    Mtu na mkewe kwa wakati mmoja wanamuwaza mtu mmoja.



     Sura iliyopita mbele yake ilifanana na sura ambayo tayari alianza kuisahau. Hakuitilia manani sana na aliamini kuwa hakuna kilichotokea zaidi ya hisia zake.

    Wakati anapata chakula cha usiku na wanafamilia akaikumbuka tena sura ile ambayo hata angewashirikisha bado wasingeweza kumtambua kwani ni yeye na mwanaye wa kiume pekee walikuwa wanaitambua sura ile ambayo ilipotea machoni mwao miaka kadhaa.

    Sura ya mwanamke.

    Baada ya kupata chakula mzee Magayane alitoka nje ili aweze kumpigia simu James na kumueleza juu ya ndoto hiyo ya mchana ya kuiona sura ile.

    Alipompigia James, kwanza alikuwa anaongea na mtu. Mzee akafanya subira kisha akapiga tena.

    Ikapokelewa. Wakapeana salamu za kila siku kisha mzee Magayane akataka kutiririka.

    “Huwezi amini bwana yaani leo nimeota ndoto ya mchana sijui ni watu wanafanana ama vipi....hebu otea nimeona kitu gani au nimeona sura ya nani hapa mjini.” Mzee Magayane alimuuliza mwanaye. Kwa kuwa usiku ulikuwa umeenda. Hata gharama za kupiga simu zilikuwa chini.

    James akakosa la kumjibu baba yake.

    “Vipi mbona kimya..we bashiri tu, nimeonana na nani leo?”

    James kimya. Akifanya tafakari bila mafanikio.

    “Samahani mzee mwanao ananiita kidogo, nikimaliza nakupigia na jibu nitakuwa nimepata...iwapo nitakosa basi nitakupa mji ili unipe jibu sahihi.” James aliaga, mzee akakubali.

    Hayo yalikuwa mazungumzo ya mwisho kati ya mzee Magayane pamoja na mwanaye. Akiwa katika kusubiri simu ipigwe, akiwa mbele ya nyumba yake.

    Mara ikapita taksi katika mwendo wa taratibu.

    “Samahani mzee naomba kuuliza..”

    “Bila shaka waweza kuuliza.” Alijibu mzee Magayane.

    “Huku mbele ni njia gani inatoka kuifikia barabara ya lami?” akauliza bwana mmoja ambaye alikuwa anaendesha ile taksi ya kukodi.

    Swali lile likamvutia yule mzee, akajisogeza tayari kwa kutoa maelekezo.

    Ghafla akadakwa, na kutupwa garini kisha wale wazoefu wa matukio wakaondoa gari kwa mwendo wa kasi huku wakionekana kuitambua njia zaidi ya mzee Magayane alivyoweza kudhani.

    Ndani ya gari lile alikuwepo mwanadada ambaye alikuwa amevaa baibui nyeusi iliyomficha hadi sura yake.

    Safari fupi mwendo wa nusu saa. Gari ikasimama.

    Lilikuwa ni pori dogo sana maeneo ya Buswelu. Taa za ndani ya gari zikawashwa, yule mwanamama akavua juba lake. Ana kwa ana na mzee Magayane.

    Ile ndoto aliyodhani ameiota ikageuka kweli, alikuwa anatazamana na mwanamke ambaye hakutegemea kuwa ipo siku watakutana katika mazingira hayo.

    Yeye na mwanaye walikuwa na hatia kubwa sana juu ya mwanamama huyu na adhabu waliyostahili haikuweza kusemekana.

    Hapakuwa na maongezi marefu sana.

    Mzee Magayane hakuwa na cha kujibu.

    Umauti ukamkumba katika namna ya kusikitisha.

    Kwanza alipigwa na rungu kichwani, akapoteza fahamu.

    Hakuweza kuzinduka tena. Visu vilipenyeza akiwa ametulia tuli.

    Hatimaye akatambulika na wanafunzi waliokuwa wanawahi shuleni kuhesabu namba akiwa mfu.

    James ambaye alikuwa ameandaa majibu kadhaa ya kumpa baba yake kwa lile swali alilouliza hakuipata tena nafasi hiyo ya kujaribu kujibu.

    Na kamwe hakujua ni jibu gani baba yake alikuwa anataka kumpa.

    Siku iliyofuata anapokea taarifa hiyo mbaya.

    Sasa yupo ndani ya ndege akikaribia kutua jiji la Mwanza kwa ajili ya mazishi.



    ***



    Kila mtu alikuwa na jibu lake juu ya kifo cha bwana Magayane, mzazi wa James, wapo waliohusisha ujambazi na wengine wakihisi kuwa kuna kisasi kimejificha.

    James na mkewe walibaki katika sintofahamu. Hawakujua waseme nini.

    Ilikuwa inasikitisha.

    Hatimaye maziko yakafanyika huku baadhi ya ndugu wa karibu wakiwa hawaamini kama ni kweli bwana Magayane amekufa.

    Akina mama walikuwa wamejitanda kanga na vitenge vyao wakiomboleza kwa kila aina ya vilio. Hatimaye mwili wa mzee Magayane ukahifadhiwa katika nyumba yake ya milele.

    Akina mama wengi walilia kwa uchungu, lakini kuna mmoja kati yao hakuwa akilia kwa uchungu bali alilia kutimiza wajibu.

    Alikuwa amevalia miwani nyeusi na alikuwa amejitanda kama wanawake wengine. Na alikuwa anafurahia jinsi shughuli ile ilivyokuwa inaendelea. Alifurahi kwa kuwa alipenda iwe hivyo na imekuwa.

    Mzee Magayane alizikwa nyuma ya mbele ya nyumba yake jijini Mwanza. Ndugu wa karibu na majirani walilala hapo kwa siku kadhaa.

    Mwanamama mwenye miwani nyeusi naye alibaki pale si kwa ajili ya kulala lakini kuna jambo alikuwa analihitaji.

    Majira ya saa sita usiku aliondoka baada ya kulitimiza.

    Waliobaki kwa ajili ya kulala hawakujua lolote. Hata mwanamama aliyemuagiza kwa jirani mdogo wa mwisho wa James hakukumbuka kama aliwahi kumtuma kwani alipitiwa na usingizi na kisha kusahau, huenda alichomuagiza hakikuwa cha msingi sana.

    Majira ya saa nne ukazuka msiba mpya kabisa wa kushtukiza.

    Castor, mdogo wa mwisho wa James alikutwa ameuwawa kwa kunyongwa shingo kisha mwili wake kutupwa mtaroni. Wasiwasi ukatanda. James akapagawa.

    Hofu ikamvagaa na kuanza kumsulubisha, swali ambalo marehemu baba yake alimuuliza bila kumpa jibu likaanza kujirudia kichwani.

    Ni nani aliyeonekana Mwanza? Je ndiye anayeua? Hakupata jibu.

    Uchunguzi wa polisi uliishia kubaini kuwa kuna alama za mikono katika shingo ya marehemu. Alama hizo zilitakiwa kutumwa jijini Dar es salaam kwa uchunguzi zaidi.

    Haikufahamika kama zilitumwa ama la.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Castor naye akazikwa huku msiba huu ukivuta watu wengi zaidi kutokana na aina yenyewe ya kifo, aliyetoka kumzika baba yake naye amezikwa. Ilileta mvuto flani wa kusikitisha.

    Emmy akaanza kukosa imani na familia iliyomuoa, akaanza kujiuliza wana kisa gani na watu gani hadi haya yanawatokea?

    Wasije wakaniua na mimi? Alijipa tahadhari lakini hakutaka kumwomba James ruhusa ya kutoweka jijini Mwanza na kurejea Dar. Alihofia kumkwaza. Mbaya zaidi alikuwa na pete kidoleni tayari.

    Eeh Mungu kwa nini haya hayakutokea nikiwa katika uchumba ili nigaili? Alisali kimya kimya.

    Emmy hakuwa amekomaa sana kiakili katika suala la mahusiano, kwanza ilikuwa ni mara yake ya kwanza kumilikiwa na mwanaume kwa ukaribu kiasi kile tofauti na baba yake mdogo, Lameck. Pili alikuwa na muda mfupi sana katika ndoa.

    Emmy akawaza kuachana na James, hofu ikamtuma kufanya hivyo.

    Alikiri katika nafsi yake kuwa katu hawezi kuamua kwa mdomo wake kumtamkia kuwa waachane, kwani hakuwa na sababu kubwa ya kufanya vile. Akiwa katika mawazo hayo akamfikiria Jose B ambaye yeye alimtambua kwa jina la Sam wa pili. Aliamini kuwa iwapo atakiuka masharti aliyoagizwa ayatii basi utakuwa mwanzo wa kijana huyu kutoboa siri ile inayomkabili. Siri ya kufumaniwa akiwa nyumba za kulala wageni na mwanaume.

    Emmy akaona kuwa hilo lilikuwa jibu sahihi.

    Akafanya tabasamu, akashika simu yake aanze kumchanganya Jose B.

    Kabla hajafanya lolote akasikia sauti ikinong’ona naye na kumwambia.. ‘Lameck ni baba yako.....aibu ya maisha’...kijasho kikamtiririka na kugundua kuwa alikuwa anataka kufanya jaribio la kujisulubu mwenyewe.

    Iwapo Lameck atagundulika kuwa ndiye mwanaume ambaye alikuwa naye katika chumba hicho wakizini, jamii itawachukuliaje ndugu hawa wa karibu.

    Mama na baba watanitazama vipi? Alijiuliza huku akiirudisha simu mahala pake na kuuvunja rasmi mpango wake wa kumtibua Jose B ili aivuruge ndoa yake.

    Jose B alikuwa ametulia tuli katika nyumba ile ambayo alikuwa ametimiza juma moja tangu aimiliki. Alikuwa akifanya utafiti wa kina juu ya vifo viwili vya mfululizo.

    Baba na mwana jijini Mwanza.

    Taarifa za msiba huu Jose B alizipata akiwa jijini Dar es salaam katika nyumba ambayo alikuwa amepangishiwa na Emmy kutokana na kumiliki siri nzito inayomuhusu mwanadada huyo.

    Jose B akaweka hisia zake kwa aidha ndugu wa karibu wa Bibiana ama ndugu wa Deo wapo katika kulipa kisasi. Aliamini hivyo kutokana na tukio la James kufanya mauaji jijini Mwanza. Baada ya kuuziwa Kizuizi.

    Jose B akatamani sana kuwajua hawa ndugu wa Deo ama Bibiana ili aingie nao katika biashara kwa sababu tayari anaijua siri ya wao kufanya mauaji.

    Alijaribu kuvuta kumbukumbu akakosa ndugu wa karibu wa wawili hawa. Akasikitika kuikosa biashara hii.

    Ghafla akamkumbuka tena James, akatamani kufanya naye biashara nyingine lakini akaingiwa hofu juu ya biashara ya kwanza ambayo haikukamilika. Pia hii misiba miwili mizito huenda hatakuwa katika nafasi ya kufanya biashara.

    Akaamua kumpuuzia na kuwaza mambo mengine.



    BAADA YA MIEZI MIWILI.



    Misiba ilianza kusahaulika, familia ikaanza kujengeka katika furaha tena. James aliondoka na mdogo wake mmoja Mwanza na kuishi naye jijini Dar es salaam. Emmy naye akamchukua binamu yake mdogo wakaishi naye.

    Ikawa familia ya watu wanne.

    Familia yenye furaha.

    Emmy alikuwa ametimiza kila kitu kwa Jose B wa ukweli ikiwemo kumfungulia banda la tigo pesa na Mpesa kandokando ya jiji.



    Jose B akajikita katika biashara muda wa kufuatilia ya watu ukapungua. Japo alipokuwa kazini pia alijaribu kujua mawili matatu.

    Jina lake likaendelea kukua japo wanaomuita hawakujua kwanini anaitwa Jose B waukweli.

    Usumbufu wake kwa mke wa James ukapungua kwa kiasi kikubwa baada ya kuwa na uwezo wa kujiingizia kipato.

    James kwa upande wake, kupita miezi miwili bila kusikia mauaji yoyote yale walau alipata amani katika moyo wake.

    Mawazo yake juu ya kisasi kinacholipwa yalianza kufutika japo maswali ya kujiuliza hayakuisha

    Kitumbo cha Emmy kilizidisha furaha ndani ya nyumba.

    Mama kitumbo. James alimtania mkewe kila mara na walicheka.

    Kasoro siku moja tu, James alimtania mkewe na wala hakucheka, mbaya zaidi alikuwa ameegemea kochi katika namna ya kuinama.

    “Mama kitumbo.” James aliita. Emmy kimya.

    “We mama kitumbo wewe....amka...” alisisitiza lakini hakupata majibu bado palikuwa kimya.

    Watoto walikuwa shuleni pale nyumbani alibakia Emmy peke yake na sasa alikuwa hazungumzi, japo alikuwa anapumua.

    James akamkabili na kuanza kumpapasa huku na kule. Emmy alikuwa na kila dalili ya mtu aliyezimia. Mwanaume akachukua maamuzi. Akambeba mkewe hadi katika gari yake, hakutaka kupaparuka wala kutaharuki maana kwa kufanya hivyo angeweza kufanya maamuzi mabovu kabisa.

    Emmy akafikishwa hospitali ya jirani.

    Baada ya nusu saa alirejewa na fahamu.

    “Mama...mama...” alianza kuita. James akashangaa kulikoni.

    Emmy aliendelea kuangaza huku na huko.

    James alidhani ni mang’amung’amu baada ya kuzinduka, lakini Emmy alizidi kuita mama.

    Alipotulia alisimulia juu ya mkasa aliokumbana nao kabla ya kupoteza fahamu, mkasa wa kustaajabisha. Mkasa wa kusikitisha. Mkasa unaoisha mama yake mzazi akiwa ameupoteza uhai.

    Kifo cha kutatanisha.

    Baada ya kupigiwa simu akaondoka na furaha bila kumweleza mtu yeyote kitu, lakini sasa yu katika jokofu linalopuliza baridi kali, baridi isiyoweza kustahimiliwa na yeyote aliye hai, bali maiti tu.

    Mama Emmy naye alikuwa maiti.



    ***



    Hali ya joto kali la jijini Dar es salaam lilimfanya aone hata pangaboi lililokuwa linazunguka kwa kasi kubwa halikuwa na msaada wowote.

    Alilitazama kwa makini jinsi linavyojitahidi kuzunguka kwa kasi ili mmiliki wake ajivunie kuwa nalo lakini jitihada ziligonga mwamba.

    Ile hali ya kufananisha lile panga boi na kitu hai zikamrudisha nyuma na kuzitazama jitihada za madaktari zilivyogonga mwamba hadi hapo alipo kuwa kama pangaboi lisilokuwa na maana.

    Alijaribu kuyatumia vyema maneno aliyoambiwa na mwanasaikolojia, kiasi fulani yalimsaidia lakini bado aliumia moyoni.

    Alijiona kuwa hana manufaa kabisa katika jamii.

    Akiwa kifua wazi alitoka nje na kwenda kujiegesha katika pembe moja chini ya mti wenye kivuli.

    Akiwa chini ya mti huo jicho lake likasafiri mita kadhaa akamuona mwanadada akiwa amejisitiri kwa kanga moja pekee akiwa anaanika nguo. Kanga yake ilikuwa imelowana na kunatiana na mwili wake katika hali ambayo inaleta matamanio kuitazama.

    Hasira zikamzidia kwa hali hiyo akajipigapiga kichwa chake ukutani. Hasira zikatulia kidogo, akahamisha macho na kutazama upande mwingine, huku akakutanisha macho yake na rafiki yake wa siku nyingi. Alikuwa amebeba mtoto.

    Mtoto alionekana kuwa katika mikono salama kabisa na alikuwa anatabasamu kila aliporushwa juu kisha kudakwa.

    Hili nalo likamuumiza zaidi. Akauma meno yake ili kuikabili hasira, akafanikiwa.

    Hakutaka kuendelea tena kukaa pale nje. Akarejea katika pangaboi lisilokuwa na msaada wa kukabiliana na joto.

    Akajifunika gubigubi akaanza kulia.

    Kilio cha mtu mzima.

    Baadaye akapitiwa na usingizi. Katika usingizi huo usiokuwa na ladha aliwaza mambo kadhaa, mambo yanayoweza kumpa amani katika moyo wake.

    Akafikiria jinsi ya kuipigania furaha yake.

    Akamkumbuka Devotha.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Devotha angeweza kuwa mwanzo mzuri wa kuirejesha furaha yake.

    Akasimama wima akavaa nguo zake nadhifu. Hakuaga mtu akatoweka.

    Alipofika mahali pazuri kabisa akatoa kitabu chake kidogo akaibuka na namba za simu akabofya zikaita. Hakujitambulisha mapema. Akatumia uumbaji wa maneno. Devotha akaingia mtegoni.

    Baada ya masaa mawili walikuwa katika mazungumzo.

    Mazungumzo yaliyoanza kwa furaha tele, lakini baadaye yakaleta msuguano. Devotha hayupo tayari kukubaliana na ukweli wakati mwanaume anasisitiza kuwa lazima iwe vile. Devotha anataharuki.

    Mwanaume anaposhindwa kuizuia taharuki ile, anaamua kuchukua hatua. Anamkubalia Devotha kwa lile analolitaka, mwisho wanaagana.

    Laiti Devotha angejua, asingefanya maagano kwa kushikana mikono.

    Kwa kutojua hili basi akaibariki safari yake.

    Hatimaye yule dereva taksi aliyemchukua kumrejesha nyumbani anatiwa hatiani, kwani Devotha alikufa akiwa katika teksi yake.

    Taarifa inamfikia Emmy, taarifa yenye utata.

    Mwanamama aliyefahamika kwa jina la Devotha John amekutwa amekufa katika taksi. Hilo jina ni sawa na la mama yake mzazi.

    Taarifa ya pili kutoka kwa ndugu wa karibu ikatoa uhakika, Devotha aliyetajwa ni yuleyule mama mzazi na rafiki kipenzi wa Emmy, mama kitumbo akazimia. James akamkuta katika hali ile.

    Sasa wapo hospitali na Emmy anasimulia.

    UTATA MWINGINE.......



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog