Search This Blog

Sunday 19 June 2022

DEMU WA FACEBOOK - 3

 





    Simulizi : Demu Wa Facebook

    Sehemu Ya Tatu (3)



    "Mh! Nina bahati kweli ya kuonana na huyu dem sasa mara ya tatu,leo mkimya hana hata kasheshe loh! Kuna watu dunia si mchezo yaani mdada kama yule anakuwa mtu wa shari kiasi kile 'anyway' umbo lake linaruhusu maana Mungu akikuumba we mbaya lazima akupe na njia ya kuutetea ubaya wako...dah! Lakini cha kufurahisha na yeye hapo eti ana boyfriend halafu pia ataolewa na atazaa dah! wanaume bwana!! Yaani mimi hata kwa dawa yaaani hata kama napewa pesa silali chumba kimoja na kontena kama lile ..bora unipasue kichwa kwa hali ile" alimaliza Peter kwa kucheka huku akigonganisha mikono yake,macho yake yalikuwa hayajakosea alikuwa amemwona Husna msichana ambaye alikuwa amepata nafasi ya kumshuhudia katika fujo mara mbili. Husna alikuwa anatembea kwa mwendo wa taratibu sana akielekea mahali ambapo Peter naye alikuwa anaelekea lakini yeye Husna alikuwa kwa mbali.

    "Sijui nimpige tena picha niweke facebook? Mh! Lakini akigundua yanaweza kunikuta nikaaibika mtoto wa kiume tena hapa mtaani kwetu wanavyonikubali itakuwa nuksi sana..kwanza likizo yangu ya facebook bado haijaisha.." alijiuliza na kupata muafaka Peter kisha akaamua kuachana na Husna na kuendelea na safari yake akaihifadhi simu yake aliyotaka kuitumia kumpiga picha.

    Peter alikiri kimya kimya kuwa hata yeye alikuwa anamuogopa yule binti!!

    *****CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Macho ya Husna yalikuwa chonjo sana yakifuatilia kila nyendo anayopitia Peter kwa umakini kabisa bila kupoteza hata sekunde tatu kukwepesha Husna alimshuhudia Peter alipogeuza shingo mara mbili kumwangalia na kuwa kama amemfananisha,kwa umakini bila kugundulika alipunguza mwendo na kujifanya amepokea simu ambayo hata ilikuwa haijapigwa.

    Lengo la Husna lilikuwa kujua mahali ambapo Peter anaishi ili aweze kuanzisha vita rasmi na baba wa mtoto aliyetegemea kuzaliwa baada ya miezi kadhaa, baba huyo akuwa mwingine bali ni Peter huyohuyo. Peter siyejua lolote!!!

    Wakati akiwa na simu sikioni aliendelea kufuatilia hatua za bwana Peter kwa mbali kabisa hadi akafanikiwa kumwona akiingia katika geti la mbao, kwa spidi kali kama mgonjwa wa kuhara anavyowahi chooni kila anapohisi mambo kuharibika ndivyo Husna alivyowahi katika lile geti na kuweka jicho lake pale mlangoni bila uoga …."VAMPIRE" lilisomeka jina hilo lililoandikwa kwa kutumia chaki katika mlango wa chumba alichoingia Peter.

    "Hongera Husna nakukubali" alijisemea Husna huku akiubetua mdomo wake na kufanana na mkongwe wa muziki wa taarabu na ngoma za asili Bi.Kidude binti Baraka.

    Husna aliondoka kwa shangwe sana katika mtaa wa Kigogo pembeni kidogo ya kata ya Magomeni, hakika alikuwa na haki ya kufurahi kwani alikuwa ameshinda tena kwa kishindo michezo miwili kwanza alifanikiwa kumzuia Peter asimsaliti kwa binti waliyekuwa naye pale Bar na pili aliweza kutambua ni wapi Peter anaweka mgongo wake kila usiku.

    Ndani ya gari litokalo maeneo ya Buguruni Husna alikuwa amesimama akiwa na furaha tele na hata viti vilipobaki wazi hakutaka kukaa aliendelea kusimama hivyo hivyo hadi alipofika Kinondoni na kushuka baada ya kuwa amelipa nauli, tayari ilikuwa imetimu saa moja na nusu usiku.

    Hakuwepo wa kumuuliza kwanini amechelewa kurudi nyumbani kwani vituko vyake vilikuwa vimewashinda na walikuwa wamevizoea tayari. Mama mwenyewe hakuwa na hofu na mwanaye kwani aliamini hakuna mwanaume wa kumzuzua na katu hakuwahi kutegemea kusikia habari za Husna amekutwa na mwanaume mahala fulani!! Hata mama alitambua kuwa wanaume hutazama kitu gani hadi kufikia hatua ya kumsumbua msichana.

    Kama malkia vile Husna alijitawala na kuingia hadi chumbani kwake na kujitupia kitandani na baadaye kujiandaa na kuingia bafuni kuoga kisha akarejea tena kilichofuata akatoka nje na kuelekea dukani aliporejea alikuwa na kinywaji aina ya Sayona mkononi, moja kwa moja chumbani mwake alipoifungua na kujipongeza kwa ushindi wake wa ugenini. Siku hiyo usiku hakujumuika na familia kwa mlo wa usiku.

    "Sina kazi ya kufanya mie nitamfatilia hadi nimjue nje ndani mwanaume huyu,kama ni nauli ni bora nigharamike lakini Peter abaki kuwa wangu yaani ni hapo tu Kigogo haki ya Mungu mara tatu kila wiki nitakuwa nahudhuria Kigogo" alijiapiza Husna huku akinywa Sayona yake taratibu. Jeuri yake ilitokana na pesa alizokuwa akitumiwa na ndugu zake ambao kimaisha wapo juu kidogo.



    ***

    Peter aliendelea na tabia ya kuacha kujibu meseji zote za Husna pia hata simu yake hakuwa tayari kupokea. Tabia hìi iliendelea hadi Husna alipokoma kutuma meseji na kupiga simu.

    "Kwisha habari yake kumbe alikuwa ananizuga tu mimba ya wapi mbona yupo kimya sasa" aliwaza Peter baada ya kuona ukimya wa Husna unazidi katika simu yake pia katika mtandao wa kijamii wa facebook.

    Kama ilivyo starehe ya Peter, leo hii alikuwa mwenye furaha na alikuwa amesahau jinsi Lucia alivyopepea na kumwacha kwenye mataa. Sasa alikuwa na kifaa kipya kutoka Mwanza ambacho ndio kwanza kilikuwa kinasubiri siku kadhaa zipite kitimize mwezi mmoja jijini Dar.

    Huyu alikuwa ni Doreen, binti aliyekuwa ametoka jijini Mwanza na kuhamia Dar es salaam kimasomo.

    Ilimchukua Peter siku tano za wiki kumlaghai na kumwonyesha binti huyo raha ya jiji la Dar es salaam ambapo ndio alikuwa amekanyaga kwa mara ya kwanza tangu azaliwe. Mara Msasani Beach, Mlimani City, Coco Beach, Chuo kikuu cha Dar es salaam, na sehemu nyinginezo. Binti kachanganyikiwa akajiona yupo katika pepo na Peter ndiye malaika mlinzi wake. Sasa malaika na mtu wake walikuwa nyumba ya kulala wageni!!! Kiliwapeleka nini? Hayo walijua wao!!

    Malaika huyu kwa jina la Peter alidumu na furaha kwa dakika takribani thelathini kabla mambo hayajaharibika. Hali ikawa tete.

    Kelele zilisikika katika chumba namba 18 alichokuwa Peter na msichana wake wa siku hiyo.

    "Mh! Hivi ni hapa au?" Peter alimuuliza yule binti ambaye alikuwanaye pale ndani. Nani amjibu mwenzake wakati mlango umefungwa.

    "Mi sijui jamani" alijibu huku akiwa ameishikilia kanga yake vyema kifuani isidondoke. Nguo nyingine hazikuwa mwilini.

    Peter kwa haraka alikimbilia katika tundu dogo lililokuwa katika kitasa cha mlango wa chumba hicho. Akachungulia!!!

    "Mama yangu we naniii wewe njoo uone mh! Njoo haraka sijui ni nini leo ndio leo" aliongea kwa sauti ya chini Peter akimwambia binti waliyekuwa naye. Jasho jembamba lilikuwa linamtoka licha ya feni kuwa inapuliza pale ndani,taulo iliyokuwa katika kiuno chake tayari ilikuwa imeanguka na hakujua imeanguka saa ngapi........

    Peter uoga ulikuwa umemkumba katika hali isiyokuwa ya kawaida kundi la watu kama saba wa jinsia ya kike walikuwa wanapiga kelele kwa fujo pale mbele ya mlango wa chumba chake,akiwa bado haamini kuwa walikuwa wanamaanisha mlango wake mara mlango ulianza kugongwa si katika hali ya shwari bali shari tena shari kubwa sana.

    Peter hakuelewa walitaka nini pale. Akawa anatetemeka, hisia za kufanya uzinzi zikawa zimetoweka tayari hakuwa na hamu tena, mapaja meupe ya msichana aliyekuwanae hapo chumbani hakuyatamani tena alimuona kama mikosi tena mikosi mikubwa kwake.

    "Umeangusha taulo Peter" binti yule alimwambia Peter aliyekuwa hajielewi bado. Haraka haraka aliinama akaikota taulo lakini hakuirudisha kiunoni bali aliitupia kitandani badala yake akachukua suruali yake akaivaa haraka haraka akawa amesahau kuvaa Boxer,yule binti naye akafanya hivyo hivyo,kisha kwa kutetemeka Peter akawa anauendea mlango

    “Umesahau kuvaa boxer baby!!” yule binti akamkumbusha Peter. Peter akageuza tena akataka kuvua suruali mara akataka kuvaa boxer juu ya suruali. Alikuwa amechanganyikiwa.

    Akaamua kuahirisha vyote akaificha boxer chini ya godoro!!! Akauendea mlango akafungua kidogo

    "Niwasaidie nini jamani!!..." alihoji Peter kwa wasiwasi huku akipepesa macho huku na huko, akiwa bado hata hajamaliza vizuri kuongea mara mmoja kati ya wanawake waliokuwa pale nje akausukuma mlango, Peter alipojaribu kumzuia na yeye alisukumwa kidogo aanguke akawahi kushika ukuta. Na kama vile msukumaji alijua kila kilichokuwa kinatendeka pale ndani alimvamia yule binti na kumbeba mzegamzega kama wafanyavyo wacheza mieleka. Akamsogeza nje, Peter alitaka kuingilia akakutana na jicho kali la mwanamama aliyemsukuma awali. Peter akaogopa!!!

    "Jamani ni nini kwani, kwani nimefanyaje…" aliuliza yule binti huku akiwa amebebwa juu juu.

    “Utaelewa tu si unataka majibu!!!” aliongea mwanamke mwingine huku akimdaka na kumweka chini

    "Mshenzi mkubwa tena mwendawazimu unajua tu kuchukua waume za watu sivyo utatueleza vizuri" alijibu kwa hasira mwanamke yule aliyekuwa amejazia mwili wake.

    "Mimi ni mgeni huku jamani!"

    "Mgeni! Eti unasema we mgeni, nyie ndio nilikuwa nawatafuta...sasa leo tunamalizana hata mimi nilikuaga mgeni" alidakia mwanamke mwingine huku akituliza kibao cha nguvu katika mgongo wa yule binti hadi akatoa kilio kikali kilichoashiria maumivu.

    Peter alikuwa ameduwaa tu hata asijue la kufanya wanawake wote mbele yake walikuwa wanasema yao tena kwa sauti ya juu huku wamemshikia viuno. Umati ulianza kuongezeka kwa kasi,tayari palihisiwa kuwa na fumanizi katika nyumba ile ya kulala wa wageni pale kigogo.

    Waswahili hawana dogo jamani!!!



    ***

    Husna alikuwa katika mizunguko ya hapa na pale katika mtaa wa Kigogo katika kutimiza wajibu wake wa kumpeleleza Peter mienendo yake na maisha yake kwa ujumla.

    Siku hii ilikuwa njema sana kwake kwani alifanikiwa kugundua kitu kingine kikubwa sana kuhusu Peter, macho yake kama kawaida yalikuwa yanaonyesha ushirikiano mkubwa sana katika msako huo kwani hayakumdanganya hata kidogo, ndani ya shati nyeupe ya mikono mirefu, tai ya bluu shingoni, suruali rangi ya bluu na kiatu cheusi ndio mavazi aliyokuwa amevaa kijana huyu aliyetelemka katika gari litokalo Mtongani kwenda Kawe katika kituo cha Kigogo au maarufu kama 'njia panda' laiti kama mavazi yake yangebaki kuwa hivyo basi angeweza kufanania na mfanyakazi wa benki ya Barclays ama hata diwani wa kata flani kijijini lakini muhuri uliokuwa katika shati lake uliosomeka Jitegemee Secondary School 'JKT' ulimshusha hadhi na heshima zote akabaki na jina la 'wakusoma' huyu alikuwa Peter akiwa ametoka shule kabla ya muda. Makubwa!!! Kumbe …kumbe…

    Peter alikuwa mwanafunzi!!!!

    "Dah! Mungu wangu kumbe ni kianafunzi! He! Watu wengine waongo jamani mh! Sasa hapo alinidanganya ili iweje!!!" aliduwaa Husna kwa sauti ya chini huku akimlaumu Peter kwa kuwa muongo na kujisahau kuwa yeye ndiye bingwa wa uongo.

    "Au ninamfananisha jamani!!" alijiuliza lakini hakuwa akimfananisha yule mbele ya macho yake alikuwa ni Peter mwenyewe.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Lakini jukumu langu ni kumfatilia huyu kiumbe hebu ngoja nitimize wajibu, awe mwanafunzi asiwe mwanafunzi huyu ndiye aliyenipa mimba na si mwinginealiapiza Husna huku akitafuta maficho ili aweze kumuona mume wake vizuri.

    Mara!!!

    "He! He! He! Peter mume wangu nani huyo uko nae tena jamani kwa nini unakuwa malaya kiasi hicho mume wangu jamani magonjwa jamani magonjwa Peter Wangu!!!" Husna alijikuta akilalamika mwenyewe baada ya kumuona Peter akiwa na msichana wanaongozana kuelekea pale anapoishi. Machozi yalimlenga!!!

    "Lazima nijue mwisho wao hawa he! Yaani mh!" aliongea Husna huku akin'gata kidole chake cha shahada

    Wivu ulichukua nafasi yake!!! Wivu kwa mtu asiyemtambua!!! Wivu kwa Peter

    Husna aliendelea kukaa pale alipokuwa hadi Peter alivyotoka ndani na yule msichana. Hawakuwa kama walivyoingia, yule binti alikuwa amebadili nguo na Peter vilevile hakuwa na nguo za shule.

    Wote kwa pamoja walikuwa na furaha sana.

    "Wanaenda wapi hawa washenzi" alijiuliza Husna huku akiwaachia nafasi watangulie kisha na yeye akaanza kufatilia kwa nyuma kama kawaida yake hakuwa na la ziada la kufanya pale Kigogo zaidi ya kumfatilia kwa ukaribu Peter aliyekuwa amemjaza mimba. Moja kwa moja Husna alitekeleza kwa umakini jukumu lake pale Kigogo.

    "Hapa namuhitaji Mwamvua kwa hili shari kumalizika vizuri" Husna alifikia uamuzi huo huku akibonyeza namba za Mwamvua (changudoa mzoefu)..bahati nzuri ziliita.

    "Niambie Husna binti mbaya wewe umekaa kimya muda wote huo hata hatuwasiliani unipe maendeleo mh! Haya niambie"

    "Mwamvua hebu achana na hayo yote upo wapi nakuhitaji sana huenda zaidi ya awali" alijibu Husna.

    "Kulikoni nipo hapa Kigogo kuna ...."

    "Wewe hata mie nipo Kigogo amakweli Mungu mkubwa wapi hapo" alihoji Husna.

    "Utulivu Bar, unaifahamu?" aliuliza Mwamvua.

    "Ndio naifahamu"

    "Hapa hapa nipo na wafanyakazi wenzangu" alijibu kwa furaha Mwamvua, tayari pombe zilikuwa zimeanza kutambaa kichwani mwake.

    Husna hakujibu kitu akawa amekata simu tayari, macho yake yalikuwa yamemaliza safari ndefu ya kumsindikiza Peter na sasa alikuwa anaingia Guest na yule dada, Husna alivyokuwa hataki kufanya kazi pasipo uhakika alihakikisha anakitambua chumba namba 18 ndicho Peter na yule msichana wameingia.

    Fundo la hasira lilijiunda kooni na kumzuia Husna asipumue vyema,jasho jembamba lilimtoka tena kwa wingi,Husna akajikuta machozi yakimlengalenga safari hii jicho moja liliangusha chozi!!!.

    "Nipeleke Utulivu Bar" Husna alimwambia mwendesha pikipiki.

    "Buku" alijibiwa. Husna hakujibu tena kitu akapanda kwenye kiti cha piki piki na safari ikaanza, hapakuwa mbali sana ndani ya dakika nne hadi tano walikuwa mbele ya geti la kuingilia Utulivu Bar, Husna pasipo malalamiko yoyote alimlipa mwenye pikipiki pesa yake naye akaenda zake.

    Wakati huo Husna tayari alikuwa amemtumia ujumbe Mwamvua kuwa yupo pale nje.

    "Mwamvua anachonitendea Peter kwa kweli sio haki hata kidogo, kwanza amenipa mimba halafu ananikwepa na kuikataa hii mimba,hiyo haitoshi anabadili wasichana kama nguo, yaani Mwamvua eti mimi ndio nafanya kazi ya kumlinda na sasa hivi yupo hapo guest na msichana mwingine, Mwamvua kwa nini ananitendea hivi lakini huyu mwanaume ah!" Husna alishindwa kujizuia na kwa mara ya kwanza Husna akatoa machozi mbele ya Mwamvua. Kwa mara ya kwanza akayalilia mapenzi!! Pombe zilizokuwa kichwani mwa Mwamvua zilikatika ghafla halikuwa jambo la kawaida hata kidogo Husna kutoa machozi.

    Machozi yale yakamcharua Mwamvua!!!

    "Husna yaani Peter ndiye wa kunilizia shoga yangu nilikuwa sijaapa siku nyingi sasa naapa atakiona cha mtema kuni,tena leo leo ninao makomandoo wangu hapa wewe nenda nipe maelekezo niwape wakashughulike na huyo malaya" aliongea kwa hasira Mwamvua.

    Mwamvua hakuwa na utani na wala hakutaka kupoteza muda hata chembe, pale pale aliwaalika shoga zake ambao wote walikuwa machangudoa katika kasheshe hilo.

    "Mimi najifanya mke wake, twende tukafanye fumanizi" mmoja wa wale wasichana alitoa wazo hilo lililopokelewa kwa mikono miwili na wenzake punde baada ya kuwa Mwamvua kuwa amewapa picha nzima

    "Mimi sitakiwi kuonana naye ananifahamu kwa sura, kasheshe la kwanza mimi ndio nilikuwa steringi" Mwamvua aliwapa wenzake sababu kuu ya yeye kutoenda kwenye hilo fumanizi.

    "Hamna shida hata sisi tunatosha na tutawapata wengine hapa hapa mtaani ili kuzua zogo zaidi" alisema mmoja wao.

    ****

    Peter kwa macho yake alishuhudia kichapo kikali kikitolewa kwa msichana waliyekuwa naye ndani. Hakumtambua hata mtu mmoja kati ya wale wanawake waliokuwa wanagawa kisago kwa msichana wake. Kila mtu aliyefika pale aliamini kweli yule binti amefumaniwa na mke wa mtu.

    "Jamani hawa wanafunzi yaani wanadanganyika haraka kweli ona sasa yanayomtokea" alisikika akisema hayo shuhuda mmoja aliyekuwa pale.

    "Nitapoteza shule hivi hivi nisipokuwa makini cha msingi ni kuiponya nafsi yangu" Peter aliwaza hayo kisha akatimua mbio kama mwizi huku akisindikizwa na miluzi mikali ya wakazi wa Kigogo walioshuhudia tukio hilo. Wale wanawake nao baada ya kuridhika na kipigo walichotoa kwa yule binti walimwacha pale wakaondoka zao, Husna alishuhudia kila kitu,moyo wake ulifarijika sana kuona kuwa Peter hatimaye ameenguliwa kutoka katika mikono ya yule msichana.

    "Asante Mungu, nadhani unajua ni kiasi gani ninampenda Peter...nisaidie eeh Bwana" alitoa ombi fupi kabla hajaondoka eneo lile na kurejea Utulivu bar alipomkuta Mwamvua akiendelea kujidunga pombe.

    "Asante Mwamvua asante sana umenisaidia kwa kiasi kikubwa sana" Husna alimshukuru Mwamvua.

    "Usijali huu ndio mwanzo na kama mimi ndio Mwamvua,basi Peter tayari amenyooka na nitasimama kidete hadi atimize unachotaka" alijibu Mwamvua huku akisitisha zoezi la kunywa zile pombe.

    "Asante Mwamvua"alijibu Husna kwa upole sana na aliamini Mwamvua ndio kila kitu kwake kwa wakati huo na ni yeye wa kuamua awe au asiwe na Peter

    Imani ya Husna ilijengeka maradufu kwa Mwamvua kutokana na msaada alioufanya kwake bila kutaka malipo yoyote. Urafiki kati yao uliongezeka zaidi na zaidi na ilichukua muda mfupi sana mtaa mzima waliokuwa wanaishi pale Kinondoni kulitambua hili,Husna hakuwa tena mtu wa visa na mikasa hakutaka shari na mtu yeyote,hata nyumbani kwao walizishuhudia hizo tofauti.

    "Husna wewe ni mke wa mtu mtarajiwa usiwe kama hawa wasichana wengine hapa mtaani sawa! Yaani usiwe hata kama mimi niliyekubuhu katika uchangudoa wewe kuwa tofauti sasa kuwa kama mama mtarajiwa unachotakiwa kuwaza ni jinsi gani utamlea mtoto na kumpenda baba yake" ilikuwa sauti ya Mwamvua akimwambia Husna,ni kauli hizo zilisaidia kumbadili kwa kiasi kikubwa binti Husna.

    "nimekuelewa Mwamvua nimekuelewa sana hata mimi sipendi tena yale niliyokuwa nafanya zamani" alijibu kwa upole Husna.

    Baada ya mwezi mmoja kupita tangu Husna akisaidiwa na Mwamvua kumfanyia Peter fumanizi,mwili wa Husna ulianza kupata mabadiliko mwili ulikuwa umeongezeka unene kiasi flani.

    "Husna mimba hiyo imeanza kuchungulia na muda si muda mtumbo huo utakuwa wazi na mwenye hiyo mimba kumbuka kuwa hakujui kwa sura bali jina sasa halahala shogangu mtoto asije akakosa baba na ulivyowatesa hapa mtaani watakucheka kweli lazima tufanye kitu hapa kuepuka hilo janga" Mwamvua alimpasha habari hizo Husna siku moja wakiwa katika maongezi yao ya siku zote.

    "Shoga hata nyumbani wameanza kushtukia sijui sasa tunafanyaje hapo mimi nahisi kuchanganyikiwa kwa kweli"CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Usichanganyikiwe na wala usiwaze kuhusu hilo vinginevyo utazaa mtoto punguani hapa cha kuwaza ni nini cha kufanya na mimi ninacho tayari" alijibu Mwamvua.

    "Ehee! Mwamvua nini tena hicho najua lazima kitakuwa kizuri" aliuliza kwa mshawasha mkubwa Husna huku akisubiri kwa hamu Mwamvua azungumze.

    "Peter anatakiwa akufahamu ulivyo na aelewe hiyo mimba ni ya kwake...yaani iwe isiwe lazima uonane na Peter kwa sababu hata tufanye vituko vingapi mwisho wa siku tutarudi palepale kuonana na Peter" alijieleza kwa utulivu Mwamvua na Husna akawa anasikiliza kwa makini yote.

    "Sasa ataanzaje kuamini eti usiku ule alilala na mimi jamani Mwamvua" alijibu Husna huku akiwa amekata tamaa kabisa.

    "Mimi naitwa Mwamvua na ninamwaga kweli mvua ya maujanja usiogope kesho tunaenda shuleni kwao mchana kweupe huo utakuwa mwanzo na mwisho wake utakuwa mzuri sana" alijitamba Mwamvua.

    "Mungu wangu! Yaani kweli Mwamvua unanipeleka kule mchana itakuwaje sasa" alipatwa hofu Husna.

    "Mimi ndio afisa mipango wewe tekeleza unachoambiwa na mambo yakiharibika ndio unilalamikie" alijibu kwa ukali kidogo Mwamvua na Husna akawa mpole

    ***



    ***

    Ilikuwa jumatano tulivu sana mvua ya rasharasha iliyokuwa inaanguka ilikuwa imewatuliza wanafunzi wote katika madarasa yao hapakuwa na mizunguko ya hapa na pale kwani wanafunzi waliogopa kulowana nguo zao. Kengere ya dharula majira ya saa tatu na nusu asubuhi ndio iliwatoa darasani tena bila ridhaa yao. Kama vile kengere ile ilikuwa ya kuzuia mvua kwani pale pale rasha rasha nazo zilikatika hivyo wanafunzi hawakulowana nguo zao. Asilimia kubwa ya wanafunzi walikuwa wakisugua mikono yao kutafuta joto huku jukumu kubwa la viranja likiwa kuwapanga vyema katika mistari iliyonyooka.

    Punde mwalimu wa zamu akitangulizana na kundi la wanawake watatu lilitokeza na kujongea mbele ya wanafunzi wale,punde mwalimu mkuu msaidizi na yeye alifika akiwa na bahasha fulani mkononi.

    KIRANJA:"mguu upande..mguu sawa...mguu upande..mguu sawa...kulia geuka...kushoto geuka...mguu upande...heshima kwa mwalimu toa"

    WOTE:Shkamoo walimu. Wanafunzi walitoa heshima hiyo baada ya kupewa maelekezo na kiranja.

    "Sina haja ya kujibu salamu zenu watoto wa kiume lakini kwa mabinti marahaba" alijibu makamu mkuu na kusababisha wanafunzi kuangua kicheko kwani walikuwa wanampenda sana japo alikuwa mkali.

    "Hivi huwa mnaona kununua condom gharama sana..sasa kama ni gharama mwenye huu mzigo ndani ya huyu binti ataijua gharama yake ni nini..yaani hamwogopi Ukimwi na kujaza mimba pia hamwogopi leo itafahamika" aliongea kwa ukali mwalimu huyo aitwaye Werema.

    "Du! Watu wana uchu jamani huyu dem mi nampata ni bonge la komandoo anatoa kichapo usipime yani leo ana mimba mh! Wanaume sio watu leo namjua sasa mwenye mali" ilikuwa sauti ya Peter akiwasimulia wenzake huku akiwa amecheka hadi machozi yamemtoka

    Peter alikuwa kati ya wanafunzi waliokuwa na furaha zaidi asubuhi ya siku hiyo kwani alikuwa alikuwa anaenda kushuhudia jambo ambalo hakulitegemea na kwake lilikuwa kama muujiza aliokuwa ameutabiri hapo kabla eti yule binti aliyezoea kumuona katika mitafaruku mbalimbali ya kibabe leo hii ana ujauzito, lilikuwa jambo la kushangaza sana.

    “Ama kweli wanasema simba hata awe mkali vipi atazaa” aliendelea kutoa vidokezo Peter huku makamu mkuu wa shule na yeye akiwa bado anaongea pale mbele.

    Tayari Peter alikuwa ameharibu kabisa suala zima la usikivu katika msitari wote wa nyuma wanafunzi wote walitega masikio yao kuweza kumsikiliza yeye na hadithi zake juu ya msichana aliyekuwa na malalamiko kuwa amepewa mimba kisha kutelekezwa na mwanafunzi wa shule hiyo (Jitegemee). Kila mmoja alikuwa na shauku ya kusikia Peter alikuwa anasema nini juu ya binti yule maana mara kwa mara Peter alikuwa mwingi wa habari jambo lililompatia umaarufu pale shuleni.

    “Peter na wewe umekuwa mwalimu huko nyuma umeanzisha kikao chako baba haya endelea babangu ukimaliza nitaendelea baba” mwalimu Werema alikatisha maongezi yake na kumuuliza Peter ambaye alikuwa maarufu sana pale shuleni kutokana na tabia yake ya kupenda sifa kupita kawaida, kwake yeye sifa ilikuwa ana thamani kubwa zaidi ya kupata alama za juu katika masomo na waziwazi alionekana kutamani sana asimalize shule ili aendelee kujichotea sifa kemkem pale shuleni. Kila walipoingia wanafunzi wapya Peter alitamani wamjue na hilo halikuwa gumu kwa upande wake alifanikiwa kirahisi sana.

    “Hapana mwalimu sijaanzisha vikao vyovyote wala mimi” alijitetea Peter kwa sauti ya kukoroma iliyojaa hatia ambayo haikusikika vyema

    “Tena cha kushangaza wewe huyo huyo muongeaji ndio unaweza kuwa muhusika wa hii mimba ya huyu binti hapa, nyie wenye maneno mengi ndio haya madhara yenu leo itafahamika!!” mwalimu Werema alimwambia Peter na shule nzima ikalipuka kwa vicheko kasoro wanawake watatu waliokuwa pale mbele na hao walikuwa ni Husna (ambaye alitambulishwa kama Mariam),Mwajuma(shoga yake Mwamvua) pamoja na mwanamke aliyeonekana kuwazidi wote umri aliyedaiwa kuwa ni mama yake na Husna lakini katika hali halisi hakuwa mama yake mzazi na Husna bali alikuwa ni mama wa kuchonga na mchongaji mwenyewe alikuwa Mwamvua ni huyu aliyemtafuta mwanamama huyu na kumwomba awasaidie katika hilo la kumpeleka Husna pale shuleni kwa jiji la Dar es salaam haikuwa ngumu kuwapata kina mama kama hawa.

    Kwa jinsi alivyokuwa ameukunja uso wake ungeweza kuamini kweli ni mama yake Husna wa kumzaa kabisa kwani uchungu wake ulionekana kuanzia usoni. Kwa haraka haraka ungeweza kusema aidha alimzaa kwa upasuaji ama ni motto wake wa pekee.

    “aaaah!!! Ticha yaani mimi tena na huyo haiwezekani hata siku moja katika maisha yangu labda niwe naota hapo sawa lakini hata ndoto pia haiwezekani kuna mtu na mtu ticha angalia” alijibu Peter kwa jeuri huku akijiamini sana. Wakati huu sauti yake ilisikika vizuri, wanafunzi bado walikuwa wanacheka kama kawaida yao jambo ambalo lilimfurahisha Peter.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Umaarufu ukawa unaongezeka!!!

    “Hayaaaa!! Tosha tosha tosha,suala lililopo mbele yetu kwa sasa ni kwamba huyu binti ambaye jina lake ni Mariam akiwa na dada pamoja na mama yake watapita mstari baada ya mstari na pote walipo wanaume watakagua kumtafuta shemeji na mkwelima wao” aliongea mwalimu Werema na kuibua kicheko kikubwa zaidi ya awali katika umati ule.

    “Eeh!! Sasa mama, dada pamoja na binti mnaweza kuanzia hapa au pale yaani popote pale na wala msisite kumtaja mtuhumiwa wenu mkimuona, msitingishwe na vitisho vyao hii ni shule ya jeshi hakuna wa kuwafanya kitu chochote kibaya labda kama mtu huyo hajipendi hivyo napenda muwe huru kabisa na kwa umakini kabisa ili zoezi hili liweze kukamilika katika hali ya kila mmoja wenu kuridhika katika nafsi yake” mwalimu Werema aliwapa hali hiyo ya kutia moyo wanawake hao watatu ambapo Mwajuma aliuongoza msafara kwa nyodo zote hadi mstari uliokuwa jirani yao, japokuwa msitari mzima ulikuwa umejaa wanafunzi jinsia ya kike bado walikagua hivyo hivyo na kuzua kituko kingine katika asubuhi hiyo ya kipekee katika shule ya Jitegemee katika jiji la Dar-es-salaam maeneo ya Kurasini. Kila mmoja alikuwa akirefusha shingo kusubiri fumanizi hilo la aina yake lisilokuwa na waandishi wa habari

    Mwajuma, Husna pamoja na yule mama wa makamo hawakujali hata kidogo vicheko na kelele za wanafunzi hawa wao walikuwa makini katika zoezi zima la kumsaka mbaya wao Husna aibu zilikuwa zimemjaa moyoni lakini kwa nje na yeye alionyesha kuwa bado ni jasiri sana.

    “Hebu na wewe tembea huko!!! Unajishaua shaua nini hapa, si mlifurahi kufanya huo ujinga” mama feki wa Husna alimzodoa Husna huku akimsukuma baada ya kuona anapunguza mwendo

    “Huyo huyo….eeeeh!! kamata huyo……ndio mwenyewe huyo dada chukua mtu wako……aaaah!!! Shemejiiiiiii” zilikuwa kelele za Peter kila akina Husna walipokuwa wakiendelea na ukaguzi wao.(Peter alikuwa anapenda sana sifa zisizokuwa na msingi wowote ule mbele ya wasichana na jinsi wasichana walivyokuwa wa ajabu eti walimpendea hizo sifa zake).

    “We mshenzi wewe mwanahizaya mkubwa” Husna alijikuta akitoa tusi hilo alipokutanisha uso wake na mwanadada ambaye alimfumania katika nyumba ya kulala wageni akiwa na Peter halafu Peter akakimbia.

    “He!! Huyu vipi??? Au mimba yake imemtuma kukuchukia wewe!!!!???” aliuliza binti mmoja aliposhuhudia hali ile ya Husna kumtukana mtu asiyemfahamu. Laiti wangejua!!!

    Ili kuepusha shari Husna alijaribu kuziongoza hasira zake zisimpeleke pabaya na akajiondokea eneo lile kwa amani kabisa.

    Hatimaye ilikuwa zamu ya mstari aliokuwa amejipanga Peter pamoja na wavulana wengine wengine

    “Haya sasa Peter zamu yako anakuja mkeo wa ndoa huyo jiandae kumpokea” wasichana walianza kumpigia Peter kelele baada ya kuona Husna (Mariam) na kundi lake wakizidi kujongea kuelekea kule alipokuwa, Peter hakuwa na la kufanya wakati huu akawajibu kwa kutoa tabasamu kali sana huku moyoni akiwa na amani kabisa kuwa haiwezekani akawa ni yeye atakayeumbuliwa na Husna.

    “Tumemuona muhusika wetu, tunampa muda wa kujirekebisha asipobadilika tu!! Kwa mara nyingine tunakuja na polisi hapa na kumchukua na kuondoka naye.

    Hatupendi hata kidogo kuyaingilia masomo yake na kuikatisha shule yake lakini akitaka iwe hivyo hata sisi tutakuwa tayari kwa shari hiyo hatutakuwa na huruma tena kama yeye ambavyo hakuwa na huruma kwa binti yetu Mariam, nadhani tumeelewana sisi tumemaliza na yetu ni hayo tu!!? Asanteni kwa ushirikiano” alitoa hotuba hiyo fupi Mama yake Husna (feki) akiwaambia wanafunzi wote.

    Peter alikuwa amejawa wasiwasi maneno ya kejeli wanafunzi waliyoyazoea kutoka kwake hayakuwepo tena, alijaribu kutabasamu lakini haikuwezekana Peter hakuwa kawaida hata kidogo.

    “Umesikia Peter hayo maneno sasa umepewa nafasi ya kujisalimisha kiustaarabu na tena kwa amani yaani ukipuuzia tu mara ya pili wakija unapelekwa polisi moja kwa moja” makamu mkuu wa shule alimtumia Peter kama utani ili kuwaburudisha wanafunzi kabla ya kuwaruhusu wote warejee darasani.

    “Vipi kaka Peter jumba bovu limekuangukia nini!!!??? Tuambiane kaka tuanze kupitisha michango ya harusi hapa” rafiki yake Peter alimtania baada ya kumuona Peter ghafla hayupo kabisa katika hali yake ya kawaida ya uchangamfu na utani mwingi.

    “Hapana kaka nina ishu nyingine tu inanichanganya” alijibu Peter huku usoni akionekana dhahiri kuwa anadanganya

    * * * *

    “Kwa nini wale watu wameniachia ujumbe huu jamani mhh!! Au wamenifananisha eeehh!! Alijiuliza maswali Peter njia nzima ndani ya gari hadi aliposhuka chini na kuanza kutembea kwa miguu kuelekea kwake, kitendo cha kupewa kiujumbe na yule mama wa mlalamikaji kilikuwa kimemchanganya.

    “ Mambo 076777909*” ujumbe ulisomeka hivyo bila kuongeza wala kupunguza neno lolote lile.

    Haikuwa namba mpya sana machoni mwa Peter lakini hakujua ni ya nani kwa uhakika lakini aliamini kuwa anaifahamu tena vizuri sana.

    Alipofika katika chumba chake pale Kigogo hata hakuvua viatu kabla ya kuingia ndani kama ilivyokuwa kawaida yake ya kudumisha usafi katika chumba chake hicho kidogo.

    Moja kwa moja aliiendea simu yake na kubonyeza namba hizo ili aweze kujua ni za nani hasa.

    “Mama yangu Husnaaaaaaa!!!!! Nimekwisha lakini mbona hakuwepo kwenye lile kundi sasa au ndio…..aaaahhhh!! hapana haiwezekani hawezi kuwa Husna yule sasa ni nani hawa tena Yesu wangu” Peter alichanganyikiwa zaidi ya kawaida alipogundua namba iliyokuwa pale ni ya Husna, binti ambaye walikutana katika mtandao wa kijamii kwa mara ya kwanza kisha mara ya pili wakakutana katika hoteli ya Lamada majira ya usiku ambapo walikutana kimwili katika chumba kilichokuwa na giza nene, Husna yule alikuwa mrembo sana tena mrembo wa kutisha ambaye macho ya Peter yalimkubali bila kipingamizi chochote kile, na maujanja yake pale kitandani yalimkosha sana na uhondo alioupata siku ile katika kitanda kile cha futi sita kwa sita kamwe haukufanania na sura zote alizoziona pale mbele walipokuwa mstarini.

    Haraka haraka Peter akafungua simu yake ili aweze kufungua ‘profile’ la Husna na kutazama kama kuna sura hata moja iliyokuwa pale shuleni huenda wana uhusiano na Husna. Alipojaribu kufanya hivyo hakuweza kupata jina la Husna Chammy.

    Husna alikuwa amemblock Peter!!!! Pabaya zaidi!! Jasho likamtiririka!!

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Husna alikuwa amemblock Peter!!!! Pabaya zaidi!! Jasho likamtiririka!!

    Hofu ikatanda, joto likamtuma kuvua shati na kujikuta kifua wazi ndani ya sekunde kadhaa, wasiwasi wa kufukuzwa shule kama jambo hilo ni kweli ukamtia baridi kali akajikuta tena analivaa shati lake.

    Peter alikuwa katika fumbo gumu kufumbua!!!

    Akataka kumpigia Husna lakini akagundua hakuwa na jipya la kumwambia.

    Kwisha jeuri yangu hapa!!!!! Aliwaza Peter!!!!

    “Sasa hii namba ya Husna wametoa wapi Mungu wangu!!!!” hilo ndilo swali kubwa walilojiuliza wajumbe katika halmashauri ya kichwa cha Peter bila kupata majibu ya uhakika na hata yale ya kubahatisha pia hayakupatikana.

    “Peter nimekaribia kuumbuka mtoto wa kiume mimi tena hadharani dah!! Au wanatania wale wanawake jamani, lakini wamejuaje kama mimi ninajuana na huyo Husna mh!!!” aliendelea kuumiza kichwa Peter huku kile kikaratasi kikiwa bado mkononi mwake alikuwa anakiangalia kama vile hajamaliza kukisoma japo tayari alikuwa amemaliza kukisoma tatizo ni kwamba hajaielewa maana hasa hasa iliyobeba maandishi yale.

    “Wanamaanisha nimpigie Husna au maana yao hasa hapa ni ipi kwa kweli nashindwa kupata picha hapa” aliendelea kujihoji Peter akiwa peke yake na viatu vikiwa bado miguuni mwake..

    “Aah!! Waachane na mimi hawaniwezi kwanza mi ndio Peter mtoto wa hapa hapa town japokuwa nimezaliwa kijijini” aliamua kujivika ujasiri wa hali ya juu Peter japo alikuwa amejawa na uoga tele.

    “Na simu wanayotaka nipige ndio sipigi ng’o!!!” alisema Peter huku akianza kuvua viatu vyake taratibu.

    Siku iliyofuata Peter aliendelea kuwa katika hali ya hofu kila alipoona wageni wakiingia pale shuleni kwao alipatwa na wasiwasi mkubwa moyoni aliamini muda wowote ule wale wanawake waliokuwa wamefika pale siku iliyopita watakuja tena na safari hii na polisi kama walivyokuwa wameahidi kwa msisitizo, hakuna kitu alichoogopa kama polisi hakuwahi kulazwa kituoni hata siku moja lakini fedheha zilizopo pale pamoja na manyanyaso vilimuogopesha sana na hakutaka hata siku moja itokee na yeye kuionja adha hiyo inayokera sana na kufadhaisha. Umaarufu wake pale shuleni pia ulizidi kumuweka matatani zaidi

    “Nitauficha wapi huu uso wangu kama nikipigwa pingu hapa halafu kisa chenyewe awe yule demu sijui Mariam dah!! Aibu aibu aibu” aliwaza Peter wakati mwalimu akiwa darasani anaendelea kufundisha, akili yake haikuwepo pale hata kidogo.

    ****

    Siku ziliendelea kukatika kwa fujo bila Peter kuona madhara ya ujumbe aliopewa na mama yake na Husna (feki).

    “Aah!! Wazinguaji tu wale wameniumiza kichwa mpaka basi kumbe hamna lolote, polisi polisi, mimba mimba wanazijua mimba hawa au!! Nani wa kuzaa na ile Scania hapa bongo labda huko bush tena usiku wa giza dah!! Demu gani sasa yule kwa akili ya kawaida tu jamani, ni heri nitoe jero (500) nikanunue malaya hapo Buguruni kuliko huyu katuni kunipa bure, angekuwa ni Husna kweli ningejisifu nimempa mimba mtoto wa maana tena wa kizito tu mambo yakiharibika baba yupo anasaidia saidia lile chizi limepotea njia jamani” yalikuwa mawazo ya Peter aliyoyatoa kwa sauti ya juu akiwa chumbani kwake zikiwa zimepita siku nane tangu tukio la binti kuletwa na mama yake eti amepewa ujauzito na mwanafunzi wa shule ya upili (sekondari) Jitegemee.

    Hali ya Peter sasa ilikuwa imerejea kuwa ya kawaida tena kama awali. Akajiona mshindi!!

    ****

    Mpango aliokuwa ameusuka Mwamvua hakuwa na wasiwasi nao hata kidogo aliamini kwa namna yoyote ile lazima azma yake ya kumtia adabu Peter lazima itimie kwa njia zozote zile zilizo ndani ya uwezo wake pamoja na shoga zake na tayari jaribio la kwanza lilikuwa lipo katika kusubiri matokeo yake ambayo Mwamvua aliamini yatakuwa mazuri sana japo siku zilikatika bila kupata simu kutoka kwa Peter.

    “Hajaukwepa msala wangu hata kidogo wala hajapunguza tatizo na badala yake amejiongezea tatizo kubwa zaidi ambalo kulitibu yataka ujasiri mkubwa sana.” Mwamvua alijiapiza baada ya kuhisi Peter amejifanya ana kiburi amepewa namba na ameacha kupiga.

    “Amenipanda kichwani huyu mtoto yaani kianafunzi kama kile kweli kinataka kunipotezea muda mimi!!! Ninapambana na mijibaba hapa mjini mwaka wa ishirini sasa hichi kitoto cha juzi juzi kinataka kunipotezea dakika zangu loh!! Ngoja sasa nimvalie njuga kabla hajanivua nguo hadharani” alijiapiza Mwamvua. Hasira zikiwa zimeanza kumpanda.

    Mwamvua alikuwa amechukizwa kweli na kitendo cha Peter kuacha kupiga simu wakati alipewa namba halisi ya Husna na yeye (Husna ) anadai hata siku moja hakuwahi kuzima simu yake. Moja kwa moja Mwamvua aliamua kwenda nyumbani kwao Husna lakini hata kabla hajafika alikutana naye njiani. Ilikuwa bahati ya kipekee!!!

    “Husna shoga hicho kitoto tumekiendekeza sana yaani kama tunakiogopa vile, hivi kina nini hasa au hii mimba ndio inasababisha hivyo” alihoji Mwamvua baada ya kusalimiana na Husna.

    “Yaani hata mimi nimefikiria sana juu ya suala hilo usiku wa jana na huu mguu ulikuwa unakuja kwako kwa shida hiyo hiyo amini usiamini” alijibu Husna huku akishika kiuno chake kwa mbwembwe.

    “Sasa tunafanyaje kwa mawazo yako!! Shoga yangu”

    “Ni kumkabiri huyo Peter kiukweli ukweli tena kwake uso kwa uso yeye atajua kama hii mimba iliingia bahati mbaya au maksudi…kama ni bahati mbaya na aitoe sasa bila kunitoa damu na kama ni maksudi ailee nisije kuzaa toto limekunja uso hapa kwa hasira za kutengwa na baba yake”

    “Wazo lako ni kama langu sasa tufanye kazi tena kazi hasa hasa haraka haraka..tukilegeza tutaaibika ujue” Mwamvua alimjibu Husna huku wakigonga mikono yao.

    *****

    Ilikuwa jioni tulivu sana japo joto la jiji la Dar es salaam liliendelea kutawala katika nafasi kubwa mno, waliozoea hawakuona tabu sana lakini kwa wageni hilo lilikuwa ni tatizo kubwa walijihisi kama vile wamelisogelea jua tena kwa ukaribu sana. Peter alikuwa mmoja wa wahanga wa hali hii ya hewa na alikuwa nje amejikalia mbele ya mlango wake kama kijana asiyependa makuu haatakidogo, muonekano wake ulikuwa mvuto tosha na ushawishi kwamba alikuwa mstaarabu sana. ilipendeza kujiburudisha kumtazama.

    Majira ya saa moja kigiza kilipoanza kuingia Peter alirudishia mlango wake na kujisogeza katika mtaa uliokuwa jirani ambapo aliingia katika mgahawa mmoja ili aweze kupata chakula chake cha jioni hiyo. Hakuwa mtu wa kupika mara kwa mara.

    “Kwani wali nyama wenyewe shilingi ngapi???” alihoji Peter baada ya kuwa ameambiwa wali mkavu ni shilingi mia nane (800).

    “Wali nyama buku kaka yangu” alijibu yule muhudumu huku akiendelea kuwahudumia wateja wengine.

    “Basi nipatie wali nyama wakushiba tafadhali.” Alisisitiza Peter na muhudumu akatii alichoagizwa. Baada ya kumaliza kupata chakula chake pamoja na maji mengi ya kunywa yasiyokuwa salama Peter tayari uchovu ulikuwa umeanza kumuandama na hapakuwa na lolote jipya eneo lile akalipa alichokuwa anadaiwa kwa kula chakula kile kisha akatoweka kurejea kwake.

    “Hivi vitoto hivi yaani kila siku nachimba mkwara kuwa sitaki wacheze mlangoni kwangu hata ndio kwanza hawasikii, na hapo ukivipiga utawasikia mama zao!!” aliongea Peter kwa sauti ya chini chini wakati akijongea katika chumba chake hiyo ni baada ya kuona kwa mbali kama watoto wakiwa jirani na mlango wake.

    “Ole wenu nikute michanga hapo mlangoni nitawachapa nyie, hivi mlishawahi kupigwa kweli” alianza kukoroma Peter akitegemea watoto wale watashtuka lakini wala hata hawakupata mtetemeko wa aina yoyote ile. Watoto wa uswahilini bana!!!

    “Shkamoo kaka” alisalimiwa Peter

    “Marahaba ehe! Nini kucheza hapa mlangoni muda huu!!” alihoji Peter.

    “Sisi hatuchezi tulikuwa tunakusubiri wewe…….”

    “Mnanisubiri ili niwawashie video muangalie…..hapana usiku umeenda sana nataka kupumzika watoto wazuri sawa eeeh!” alidakia Peter.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hamna kaka si tumetumwa kuna watu wanakuita kuleee” alijieleza mtoto mmoja. Maelezo yaliyonyooka lakini yakipindishwa na sauti ya kitoto.

    “Wakoje hao ni wavulana au wasichana??” alihoji Peter akiwa na shauku huku usingizi wote ukimpaa.

    “Ni wasichana wanasoma na wewe wamesema” alijibiwa.

    “Nishawafahamu mmesema wako wapi vile” alijifaragua Peter. Neno ‘wasichana’ kwake ilikuwa ni kama ufalme . nani hapendi kuwa mfalme!!

    “Pale chini ya mti pale mbele kidogo utawakuta” walielekeza wale watoto.

    “Hebu twende wote watoto wazuri” alishawishi Peter na watoto wale wawili hata hawakubisha wakaongozana naye hadi eneo husika.

    “Haya nimewaona nyie nendeni mnisubiri pale nje nije kuwawashia video sawa watoto wazuri”

    “Haya kaka Peter tunaenda kukusubiri!!!” waliaga wale watoto kisha wakaondoka huku wakikimbizana.

    Peter alianza kujisogeza taratibu kwa wasichana wale ambao alikuwa hajawatambua bado kutokana na kigiza cha usiku na mavazi yao ya baibui waliyovalia katika miili yao. Ni mavazi yale yalimfanya atambue kuwa ni wasichana.

    “Mh! Hivi leo kuna club gani maana najua hapa wamenipitia twende kuruka kwanja hakuna lolote, hapa wametoroka kwao na hiyo minguo halafu kwenye pochi zao kama kawaida mambo yetu yale nguo za nusu uchi kama sio uchi kabisa” alijiwazia Peter akizidi kuwasogelea.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog