Search This Blog

Sunday 19 June 2022

WANAWAKE NI WAUAJI ?! - 2

 







    Simulizi : Wanawake Ni Wauaji ?!

    Sehemu Ya Pili (2)





    Nilistuka mara baada ya kuhisi hali ya ubaridi na unyevunyevu na nilipotaka kuamka nilijihisi kichwa kuwa kizito sana lakini nilijitahidi na kukaa kitako pale njiani huku nikitazama huku na huko kuangalia kama kuna watu wanakuja niombe msaada ama sivyo nikusanye nguvu nipige mayowe raia waje wanisaidie japo nilijua kuwa pale nilipo kuna zaidi ya kilometa moja kufika kwenye makazi ya watu ambako ndiko pia alipatikana babaangu mkubwa yule mganga wa kienyeji na ndio nia ya safari ile tulikuwa tunaelekea kwake.

    Sikujua ilinichukua muda gani mpaka niliporejewa na fahamu kwani nilijikuta niko mwenyewe pale chini.



    Lakini niliponyanyua mkono wangu na kutokana na mbalamwezi kuchomoza muda ule nilishangaa kuona umetapakaa damu halkadhalika na mkono mwengine.

    Nilijikagua haraka haraka kuona wapi nimeumia lakini bado sikuhisi jeraha lolote mwilini mwangu zaidi ya jeraha dogo kichwani ambalo lilikuwa halivuji damu kivile.

    Lakini pia nilipoangalia chini vizuri nilishangaa kuliona panga usawa ule nilipolala likiwa limeloa damu pia kulionekana michilizi ya damu kuelekea kwenye kichaka kimoja eneo lile.

    Nilijikuta nikilishika lile panga kwa mshangao na kuligeuza geuza kuhakikisha kama ni kweli au macho yangu yalikuwa bado yana mawenge,! lakini nilipofanya vile akili iliniaminisha kuwa kile nikionacho ni kweli wala si mawenge na hapo ndipo nilipogutuka na kulitupa haraka chini lile panga na kujikuta nimepata nguvu za kusimama na kuanza kunyata kwa umakini kufatilia ile michilizi ya damu kujua nini kilichopo pale kwenye kichaka.

    Lakini kabla sijakifikia kile kichaka mara nilianza kusikia kelele kelele za watu wengi waliokuwa wanakuja kwa mwendo wa kasi wakitokea ile njia iliyoelekea kijijini na punde tu nilipogeuka niliona mianga ya tochi ikinimulika huku kwa mbali nikisikia baadhi ya maneno waliyokuwa wanaongea wale watu.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Mwanaharamu mwenyewe si ndio yuuleeee.."

    "Enheeeee yule yule si unaona midamu ilee.."

    "Aliyeua auaweeee hebu tupisheni sie mbona hamtembei tutamkosaaa.."



    Zilikuwa ni moja ya kauli nilizozisikia toka kwa wale watu huku wengine wakianza kukimbia kuja pale niliposimama nami nikabaki nimeganda kwanza nikiwashangaa na nilipokaza macho kutazama vizuri niliwaona wengine wakiwa wamebeba silaha za jadi na macho yao wote wakinilenga mimi hasa baada ya kunionaa.

    "Uuuuuaaaa Huyooooo.."

    "PIGA UUAAA.."

    Ukelele huu ambao uliambatana na kurushwa kwa mkuki ambao kwa bahati nzuri ulinikosa na ndipo akili ikanicheza na kunionya endapo nitachelewa sekunde kadhaa watu wale wataponikaribia zaidi wataniua kwani walionesha wazi walikuwa hawaji kwa wema wala huruma hata chembe juu yangu.

    Nilijikuta naruka na kuanza kutimua mbio huku upepo mkali ukinipitia ghafra karibu na kichwa baada ya kurushwa kwa rungu moja kubwa ambalo niliamini lingenipata huenda ningezima pale pale kama sio kufa kabisa.



    Nilikimbia kwa speed ya kunusuru maisha yangu huku nikifata kile kibarabara kilichoelekea barabara kuu kule tulipotoka na nyuma yangu bado niliandamwa na watu wale wenye hasira kali ambao sikuwa na uhakika wa moja kwa moja kuwa ni wanakijiji au ni miongoni mwa wale walionivamia awali!?

    Lakini kabla sijafika mbali mbele yangu kulisikika mlio wa gari sambamba na mwanga mkali wa taa zilizonizuia kuona vizuri na kujikuta naingia porini lakini mara ile gari ilisimama ghafraa na nilisikia vishindo vya watu wakiruka na kunizunguka huku ukelele wa mlio wa risasi ukisikika kuwatuliza wananchi waliokuwa wanakuja ndipo nilipotulia hasa baada ya kusikia kauli zao na kugundua kuwa walikuwa ni polisi.

    "tulia hivyo hivyo usikimbie zaidi mikono juu sisi ni maafsa wa polisi.."

    Ilikuwa ni sauti ya mmoja wa watu walioruka kwenye gari akinisihi na kunisogerea pale niliposimama huku nami nikitii na kuona sasa afadhali msaada umepatikana.

    Ajabu aliponifikia cha kwanza nilipigwa pingu na kugongwa mabega na kitako cha bunduki hali iliyonistaajabisha na kunikosesha kabisa nguvu.



    "Wananchi tunaomba mtulie, mshatoa taarifa kwetu hampaswi tena kuchukua sheria mkononi. kwa pamoja naomba mtusaidie kuona eneo lenyewe la tukio hasa ni lipi na jee mtuhumiwa husika ndie huyu mliyekuwa mnamfukuzaa?"



    "Ndioooooo Afande tuachieni tuliue kabisaaa linyamaa hiloo"



    Sauti hizi zilizidi kunishangaza na kunishtua kwani mpaka muda huo sikujua nini hasa nilichofanya yaaani badala ya kupewa msaada ndio kwanza nataka kuuawa?

    Nilikamatwa suruali na kuanza kutembezwa mpela mpela na wale askali wakiwafata wananchi ambao nao waliongozwa na mtu mmoja kuelekea kule niliposhambuliwa hususani eneo lile la kichaka ambako sikubahatika kuona kilichopo na ndipo mara baada ya askali kufika pale huku wakiwa na matochi makubwa yenye mwanga mkali tulishuhudia maiti mbili ya mama na mtoto mdogo zikiwa zimekatwa katwa vibaya.

    Nilijihisi kuchanganyikiwa hasa baada ya kuona nguo za kale katoto ndio zilezile alizovaa mwanangu siku hiyo.

    Nilipiga kelele kwa kumlilia zaidi mwanangu nikiamini nae wamemuua sambamba na mke wangu lakini chaajabu ndio kwanza nilizidi kuchezea vitasa na maneno makali kutoka kwa wale mapolisi huku wengine wakinipiga picha.



    "Afande Jacobo sogeza gari pia afande Dula weka hilo panga vizuri hapo mbele hakikisha mtu yeyote asilishike direct bila groves pia inabidi turisachi hili liuaji vizuri tuone kama kutakuwa na ushahidi zaidi.. hakikisheni kila tukio linapigwa picha"

    Aliongea afande mmoja alioonekana mkubwa wao, wakati huo wote mi nilikuwa nalia sana huku wananchi wakinitazama kwa hasira mno.



    Ajabu kilichonistua zaidi na kufanya nipoteze fahamu kwa mara nyengine ni mara baada ya kuanza kusachiwa kabla ya kupandishwa kwenye difenda.

    Ama kweli ukistaajabu ya Musa utayaona ya Firauni kwani kwenye mifuko yangu ya mbele ya suruali nilikutwa na kipande cha kiganja cha mkono wa mtoto kikiwa kimezungushiwa hirizi.

    Aaaaaghhh!!!!!!!!! sikuaminiiii hata chembe nikionacho na mara ndipo nilipojihisi kizunguzungu cha ghafra na network zangu zilizima palepale.



    Nilirejewa na fahamu mara baada ya kustuliwa kwa kumwagiwa maji mengi ambapo nilikuwa nimelala kifudi fudi ndani ya bodi la difenda iliyokuwa imesimama na nilipoinua kichwa niligundua nilikuwa peke yangu lakini nilipogeuka sasa kutazama vizuri ndipo nilipoona gari nyingi za polisi zikiwa zimepaki huku askali wengi sambamba na waandishi wa habari walikuwa wamesimama wakinipiga picha nikiwa kwenye ile Difenda hadi walipopanda askali wengine na kunishusha mkuku mkuku huku wakinisukuma na kuniongoza kwenye jengo moja ambalo niliponyanyua uso niliona maandishi makubwa yaliyosomeka KITUO KIKUU CHA POLISI KINONDONI



    Nilijua sasa kumbe hatukua kule polini bali tupo mjini na ni katika kituo kikubwa cha polisi ambacho awali nilizoea tu kukisikia na kukiona kwa mbali huku sikuwahi kuwaza hata siku moja kama nami ningekuja kuingia eneo lile kama mtuhumiwa tena kwa kesi mbaya mno.

    Sikujua tulichukua mda gani kutoka kule porini kutokana na kupoteza kwangu fahamu na mpaka muda ule akili zangu hazikukaa sawa kabisa na kila kilichokuwa kinaendelea niliona kama ndoto ama sinema tu na si kitu halisi japo ukweli ulibaki kuwa haikuwa ndoto wala sinema.

    Nakumbuka baada ya kuvuliwa mkanda na viatu nilisongomekwa katika selo moja huku nyuma yangu nikiandamwa na virungu mfululizo hasa pale nilipotaka kusimama kuongea chochote lakini nafasi hiyo sikuipata.

    Niliingia ndani ambapo kulikuwa na mahabusu wengine wakinishangaa kwa jinsi nilivyokuwa, nilijituliza na kukaa kitako kwenye kona ya kuta ya selo ile na kujikuta naanza kulia kwa uchungu mkubwa hasa nilipokumbuka maiti zile ambazo nilikuwa na uhakika kuwa ni za familia yangu hususani nilimlilia sana mwanangu kipenzi kwa kuuawa bila kosa lolote.



    "Oyaaa M baba mbona unaleta uduanzi sasa... hebu tukaushie usituchulie hapaa tutakunjenga ooohooo.."



    Ilikuwa ni sauti ya kiteja iliyondamana na kofi lililonikuta kichogoni na kunistua kwenye dimbwi la huzuni na mawazo na kunifanya nipunguze mdadi wa kulia kwa sauti na kubaki machozi yanaendelea kububujika yenyewe huku nikiomba kupambazuke haraka.

    Asikwambie mtu selo pabaya sana hakuna hata chembe ya raha, harufu mbaya ya kinyesi tulichokuwa tunalala nacho kikiwa kwenye ndoo mpaka asubuhi ndio mtu anaenda kumwaga, hakukuwa na vigodolo wala shuka ya kujifunika na siku watu wakiwa wengi unakosa hata sehemu ya kukaa na kubaki umesimama daaah!! ni afadhali walau maisha ya huku jera japo nayo si mazuri.

    Nakumbuka baadae asubuhi yake nilichukuliwa na kuingizwa katika chumba maalum cha mahojiano na mateso na huko nilikutana na askali watatu mmoja wao alikuwa mrefu mtu wa milaba minne ambae ndie alienikalisha kwenye kiti cha chuma na kuanza kunihoji huku wengine wakiandika na kurecord.



    "Taja lijina rako upesi.."

    Alianza kuniuliza kwa ukali kidogo yule afande baunsa.

    "Naitwa Hussein afande.. hus..sein.." Nilijibu huku nikiwa na hofu.

    "Taja vizuri bwana Lihuseni nani?"

    "Hus..sein.. Bakari..kaka."

    "Nani likaka lako wewe?! sina dogo likatiri na Riuaji kama wewe Ebo!.. haya sema kwanini uliua familia yako?"

    "Familia yangu!! hapana.. afande sijaua yeyote mbona..!!"

    "KELELE.. Tuna ushahidi wa kutosha na tumekukamata eneo la tukio. Unataka kudanganya chombo cha dora wakati vielelezo vyote tunavyo?..! lichawi likubwa wewe ngoja nikupe chai kwanza.."

    Aliongea kwa hasira yule afande huku wenzake nao wakinikandamiza zaidi kwa tuhuma za ukatili ambao sikuwahi hata kuuwaza kama kuna binaadam anaweza kufanya vile kwa familia yake mwenyewe aliyoipenda.

    Nilifungwa barabara kwa kuinamishwa nikiwa nimekaa kwenye kiti kile cha chuma kilichokuwa na mfano wa kisturi (hakina uegemeo) huku viwiko vya mikono yangu vikiwa sambamba na magoti yangu na kubananizwa pamoja hali iliyofanya nibaki nusu nimekaa nusu nimeinama na ndipo mateso makali yalipoanza sambamba na mijeredi.



    Niliumia sana na kulia mpaka sauti ikaanza kunikauka kutokana na mateso yale makali asubuhi ile. Niliwaambia na kuwaapia kadri nijuavyo kuwa sijahusika na tukio lolote baya zaidi ya kwamba mimi na familia yangu ndio tulivamiwa lakini maneno yangu ndio ilikuwa kama chachu ya kufanya mateso yaongezeke zaidi.

    Nilitamani hata kifo kije muda ule lakini nacho kilikuwa mbali na mimi. Oooh! sikuamini kama Hussein mimi ambae sikuwa na rekodi hata ya kushtakiwa kwa mjumbe tu ktk makuzi yangu wala kuwahi japo kumtishia mtu na kiwembe achilia mbali kumkata, lakini leo hii nateswa vikali kwa kosa la kuwakatakata na kuwaua vibaya mwanamke na mtoto mdogo? tena eti ni familia yangu? yaani mke wangu na mwanangu mwenyewe!!? aaaaaghhhhh!!!!! kwa mara nyengine nilizimia tena katikati ya mateso yale makali.



    Nilizinduka baada ya siku mbili na kujikuta nipo hospitali nikiwa nimetundikiwa madripu huku mkono mwengine ukiwa umefungwa pingu sambamba na kona ya kitanda nilicholalia na pembeni yangu bado kulikuwa na ulinzi mkali.

    Sikuwa na cha kuongea zaidi ya kububujikwa machozi tu huku moyo wangu ukiniambia kuwa ndio nishaangamia tena sitoweza kubadilisha ukweli labda utokee muujiza.

    Baada ya kupata ahueni nilichukuliwa tena mkuku mkuku na askali kisha nikapandishwa kwenye difenda na ndipo mlio wa toori toori (king'ora) ulisikika na safari ilianza kutokea pale hospitali mpaka tulipofika kwenye jengo moja ambalo nililijua vizuri tu kwa nnje kwani ilikuwa ndio njia yangu kubwa ya kupita pindi niendapo na nirudipo kazini, aaaah! ama kweli usilolijua ni sawa na usiku wa giza. Leo hii hussein mimi naletwa sehemu hii!!? tena kwa staili hii..? Nilijiuliza pindi niliposhushwa na kuzungukwa na askali wenye bunduki na kuanza kuelekea kwenye jengo lile huku eneo zima kukionekana watu wengi hasa waandishi wa habari.

    nakumbuka nilinyanyua kichwa kwa mara nyengine na kuyasoma vizuri maandishi yale makubwa yaliyokuwa kwenye lango kuu la lile jengo yaliyosomeka MAHAKAMA KUU YA TAIFA.

    Nilishusha pumzi na kichwani niliisikia sauti ikinambia 'Umeangamia Hussein'



    Sikuwa na chaguo zaidi ya kutii kila nilichoelekezwa mule ndani ambapo zamu yangu ilipofika niliongozwa na askali wawili na kufikishwa kizimbani kusikiliza kesi inayonikabiri.

    Niliangaza huku na kule ndani ya mahakama ile huku kila niliyemtazama alinitazama kwa jicho baya tu na hali iliyoniashiria kuwa nina kesi nzito sana na mbaya mno, nilibaki nimeinamisha kichwa na masikio yangu kuyaelekeza kwa hakimu pale juu japo akili zangu tayari zilishanambia kuwa Nimekwisha.

    Hakimu yule ambae alikuwa ni mwanamke alianza kusoma kesi yangu kama ifuatavyo.....



    .............

    '' Ndugu Hussein Bakari, Unashtakiwa na jamhuli kwa kesi inayohusu mauaji ya kikatili na ya kinyama kama ifuatavyo;.......

    Mnamo tarehe kumi mwezi wa pili mwaka huu majira ya saa tatu usiku makao makuu ya jeshi la polisi kitengo cha mawasiliano ya dharula ilipokea simu kutoka kwa msamalia mwema iliyotoa taarifa kuhusu mauaji ya kinyama yaliyokuwa yanaendelea pembezoni mwa jiji maeneo ya Kibamba karibu na kijiji cha Hakipo.

    Taarifa ilidai zaidi kuwa huyo kijana (msamalia mwema) akiwa anatoka kijijini kwa mbali aliona mwanaume akiwa na panga mkononi wakibishana na mkewe huku wakinyang'anyana mtoto mdogo ambapo alimsikia mwanamke akimlalamikia mumewe kuwa waachane na ushauli wa mganga wasimuue mtoto wao ni heri wafe masikini, lakini mwanaume alikuwa m bishi na kumtishia mkewe kuwa kama ataendelea kubisha basi atawaua wote na ndipo hapo msamalia yule alishuhudia mwanaume yule akimrushia mapanga mfululizo mkewe na kuanza kumkatakata na kwa kuwa yule msamalia hakuonwa na yule muuaji na alishindwa kusaidia chochote kuzuia mauaji yasiendelee ndipo alipokimbilia kijijini kutoa taarifa kwa wanakijiji wenzake baada ya kupiga simu polisi na hapo ndipo vijana wa polisi walipotoka haraka kuelekea eneo husika ambako walimkuta mtuhumiwa bwana Hussein Bakari akikimbizwa na raia wenye hasira kali huku akiwa katapakaa damu mwili mzima.



    Kwa uzoefu na mbinu za kiusalama, polisi waliweza kuwashawishi wananchi watulie baada ya kumkamata mtuhumiwa na kisha kupelekwa eneo husika ambako ilikutwa miili ya marehemu ikiwa imekatwa katwa vibaya sana na walilikuta panga lililogandiwa damu lililoaminika kuwa lilitumiwa kwa mauaji na kama hiyo haitoshi pia walipomsachi mtuhumiwa walimkuta na kiganja cha mkono wa mtoto kikiwa kimezungushwa kwenye kitambaa chekundu kilichofungwa kwa hirizi ikisadikika kuwa mtuhumiwa Hussein alifanya mauaji hayo kwa imani ya kishirikina.

    Mwisho wa kunukuu .. ''

    ..............CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Nilinyanyua macho na kumtazama yule mama hakimu kipindi ananisomea kesi yangu huku mwili wote ukiwa umekufa ganzi nilijikuta napiga kelele kwa sauti ya juu sana ambayo sikuwahi kuitoa toka kuzaliwa kwangu

    "HAPANAAAAAAA.... HUO NI UONGOOOOOOO"



    Hakimu aligonga nyundo baada ya kuanza minong'ono kutoka kwa mawakili na watu waliokuwepo pale mahakamani kutokana na kitendo changu cha kupiga kelele huku nikiambiwa kuwa ni kosa kisheria kwa mujibu wa katiba sikupaswa kuongea mpaka niruhusiwe na baada ya hapo ndipo mahakama ikabaki tena kimya na hakimu aliendelea kwa kusema kuwa sitakiwi kujibu chochote siku hiyo ilikuwa ni kusomewa shtaka tu ila kesi itakuja kusikilizwa rasmi baada ya miezi miwili na dhamana juu yangu ilifungwa kutokana na aina ya kesi iliyonikabiri hivyo ikalazimika nifikishwe segerea kusubiri tarehe nyengine ya kesi.

    Sikuamini hadi muda naingizwa kwenye karandinga na safari ya Segedansi (segerea) ilianza huku nikiwa nimepoteza kabisa matumaini ya kuishi na kumuomba mungu akilete kifo upesi kije kinichukue lakini bado kifo kilikuwa mbali nami.

    Nilijikuta naongea na mungu mithili ya binaadam mwenzangu ninayemuona huku nikimlaumu kwanini hanitendei haki au muujiza wa kuniokoa kwenye matatizo yale mazito yaliyonikumbuka ilihali anajua fika kwamba sijatenda kosa lolote?



    Pia nilimlaumu sana mke wangu ambae hadi muda huo imani ya kuwa nae amefariki sikukubaliana nayo kwani maiti ya yule mwanamke haikufanana na alivyokuwa mke wangu ila niliamini kuwa nimechezewa mchezo mchafu na watu walioshilikiana na mke wangu mwenyewe na kuniulia mwanangu aaaaaah!! nini kilimsibu mama watoto wangu hadi akawa tayari kuacha mwanae anauawa na yeye kuondoka na mwanaume mwengine akiniachia majanga mwanaume niliyempenda na kumthamini siku zote?

    Ina maana Zai alikuwa msaliti..!? aagh.. lakini mbona sikuwahi kuona walau chembe ya tabia yake mbaya? Daah niliishia kujiuliza maswali ambayo yalizidi tuu kuniongezea maumivu na sikuwa na chaguo zaidi ya kukubali kuwa sasa mimi ni mtuhumiwa wa kosa la mauaji na hapa segerea ndio makazi yangu mapya mpaka pale nitapohukumiwa.



    Nikiwa nimeshaanza kutumikia maisha ya kukosa uhuru ndani ya segerea nikisubiri hukumu yangu, Kumbe upande wa nje kona zote za jiji na mikoa ya jirani kesi yangu nayo ilikuwa moja ya gumzo midomoni kwa watu.

    Vyombo vya habari hususani magazeti ya udaku yaliandika na kuchapisha picha mbalimbali zilizohusu tukio langu la mauaji ya kinyama tena kwa familia yangu kwa sababu tu ya kutaka utajiri.

    Kila aliyenifahamu alishangazwa na kustushwa sana na habari zile na kutokana na mazingira niliyokutwa na vithibitisho vya uhakika vilivyoolozeshwa kwa mujibu wa habari vilifanya hata walionijua kuamini habari zile na kunilaani kuwa kumbe upole na ustaarabu niliokuwa nawaonyesha ulibeba siri nzito moyoni mwangu tena za kishirikina....!!



    Ilinichoma sana na haya niliyapata toka kwa rafiki yangu kipenzi aliyejitolea kuja kuniona segerea mara baada ya ndugu na marafiki wengine kunisusa na kutotamani kuniona huku wengine wakihofia kujitokeza na kuthibitisha kuwa wananijua huenda ikawaponza kukamatwa na wao kuisaidia polisi juu ya ukatili wangu.

    Niliangalia baadhi ya vichwa vya habari vya magazeti aliyokuja nayo rafiki yangu yule japo niliishia kuyaona kwa mbali kupitia kidirisha kidogo cha nondo kilichokuwa katikati ya ukuta uliotutenganisha huku nikiwa bado chini ya ulinzi na uangalizi mkubwa tofauti na watuhumiwa na wafungwa wengine waliokuwa pale segerea kwa muda ule.

    Sikujua ni kwa sababu tuu ya uzito wa kesi yangu ama ndio taratibu za pale kwa mtuhumiwa mpya au laah.



    Rafiki yangu hakunificha kitu kuhusu kazini na maagizo ya bosi kuwa nishafutwa kazi wala nisitegemee msaada wowote wa kiofisi. Daah!! yaani kwa jinsi nilivyoitumikia kwa moyo mmoja ile ofisi na kujituma kwangu kote tena kwa uaminifu wa hali ya juu sikuamini kama leo hii wameshindwa hata kuja kuniona na kunisikiliza ili walau waniekee hata wakili wa kunitetea juu ya tuhuma zile lakini loh! wao pia wamekuwa mstari wa mbele kwa kunitenga.

    Niliishia kutokwa machozi tu kila habari niliyokuwa naipata kutoka kwa rafiki yangu yule wa kweli na pekee aliyekuwa na moyo wa kumfariji mtuhumiwa wa kesi mbaya ya kutisha kama yangu lakini hakusita kuniamini nilichomuelekeza na kunipa moyo kuwa nisichoke kumuomba mungu kwani hakuna linalomshinda na haki yangu itasimama tu nisihofu.



    Muda mfupi baadae askali walikuja kuniondoa baada ya muda kuisha na kuwapisha watu wengine ktk kidirisha kile na nilimshuhudia rafikiangu akinitazama kwa jicho la kunisikitikia na kukata tamaa hadi nae machozi yalianza kumdondoka.

    Nilirudi ndani ya jengo lile la kujichanganya na mahabusu wenzangu lakini haukupita muda mrefu tena niliitwa na askali wawili walinichukua kwenda kuongea na mtu mwengine ambae sikujua ni nani harafu tayari muda wa kuongea na watuhumiwa ulishakwisha.

    Niliongozwa na kuelekea tena pale kwenye kidirisha na niliponyanyua macho kuchungulia ni nani mwengine aliyekuja kuniona nilijikuta napata faraja na kuangusha kilio cha matumaini baada ya kumuona mtu yule na kugundua ni baba mkubwa.

    Nilielewa wazi ni ba mkubwa pekee ndie aliujua ukweli juu ya tatizo langu na ni yeye tu ndie nilimpigia simu kumuelezea matatizo yote na vitisho vilivyokuwa vinaniandama hadi ukweli juu ya safari yetu aliujua kwani tulikuwa tunaelekea kwake.



    "Usilie mwanangu Hussein, huu ndio ukubwa baba huwezi kujiita mkubwa bila kukupitia mitihani mwanangu na unapopata mtihani inabidi utulize akili ujue jinsi ya kukabiliana nao usijiferishe kabla hujajaribu kuufanya mtihani wako hata kama utauona mgumu kiasi gani. Lakini kumbuka kauli yangu miaka ile nilikuonya kwa kukwambia kuwa 'Mpotea njia mara nyingi si muulizaji'

    laiti ungeifanyia kazi kauli yangu ile tu nadhani ungeniuliza mapema na pengine haya yote yasingekufika leo hii.

    Lakini sikulaumu sana kwa kupotea kwako kwa kuwa bado niko hai nitahakikisha nakutetea kadri niwezavyo kuhakikisha haki inatendeka kwani najua wazi huna kosa mwanangu, wewe si muuaji, wamekupakazia tuu na hata mkeo nina imani kabisa yuko hai.

    Usilie wala usihuzunike amini mungu yu nawe na ataweza kukuokoa kama utamuamini kwani kumbuka tatizo lako si kubwa mbele ya matatizo makubwa yaliyowahi kuwakuta watu na mungu akawaokoa. Usijali baba tuko pamoja nami nishajiandikisha kama shahidi wako siku ya kesi nitakupigania. "



    Maneno ya Ba mkubwa yalinitia nguvu sana na faraja lakini hayakuzuia machozi yaliyokuwa yananidondoka yaache.

    Nilishangaa pia kuona hisia zangu zimelingana kabisa na maneno ya ba mkubwa kuwa Zai si yule mwanamke aliyeuawa siku ile na kubaini kuwa kumbe ba mkubwa alikuwa na siri nyingi kuhusu mke wangu Zai..! ina maana alimjua hapo kabla ama vipi? na jee sasa hivi yuko wapi? hapo nilikosa jibu kabisa pia nilitamani kumuuliza Ba mkubwa kuhusu huyo Mr. X kama anaweza kuwa anamtambua lakini muda wa kuendelea kuongea haukuturuhusu mara baada ya askali kumtoa ba mkubwa kule nje nami kurudishwa ndani kabisa ya gereza.



    Siku zilienda hatimae ilipita miezi miwili nikiwa segerea na ilifika tarehe ya kesi yangu ambapo siku hiyo asubuhi na mapema niliingizwa kwenye karandika sambamba na watuhumiwa wengine wenye kesi tofauti tofauti na safari kuelekea mahakamani ilianza tukiwa chini ya ulinzi mkali.



    Tulifika kwenye viwanja vya mahakama kuu na kutelemshwa ambapo siku hiyo niliushuhudia umati mkubwa ulifurika huku wengi wao wakinyoosheana vidole kuelekezea kwangu ndipo nilipobaini kuwa ni kweli kesi yangu ilikuwa ni moja ya habari iliyotikisa.

    Zamu yangu ilipofika nilifikishwa kizimbani na siku hiyo sikuwa nalia kama ilivyokuwa siku ile ya kwanza.

    Nilimudu kutazamana na watu waliokuwepo mule ndani ya mahakama japo wengi wao walinitazama kwa jicho baya lakini niliwapuuza na kuwasikitikia kwa kutojua walitendao.



    Macho yangu niliyaelekeza kila pembe ya mahakama kwa umakini mkubwa nikimtafuta ba mkubwa na kweli nilimuona nae alikuwa ananitazama na kunipa kwa kuinamisha kichwa kuwa yupo pamoja nami na nilitegemea pia ushahidi wake pekee kuwa ndio utetezi mkubwa kwangu.

    Niliendelea kuangalia kona nyengine kwa makini kujua kama kuna mwengine ninayemfahamu kaja kusikiliza kesi yangu na kipindi hiko hakimu alikuwa ndio anaanza kuisoma tena ile kesi nami ktk kupepesa pepesa macho huku na kule nilimuona rafiki yangu kipenzi yule aliyenitembelea segerea na tulipokutanisha macho alitabasam kwa kunionesha ishara kuwa yuko pamoja nami.

    Nilijisikia faraja kwa namna furani na kumshukuru mungu kwa kuwajua rafiki na ndugu wa kweli kwangu kwani ni vigumu kumtambua rafiki wa kweli au ndugu wa kweli kama hujapatwa matatizo makubwa.



    Siku hiyo ndio nilizidi kuielewa na kuimbuka misemo mingi ya wahenga ambapo awali nilichukulia kama burudani tu kwa watoto lakini baada ya majanga nikakubali kuwa Akufaae kwa dhiki ndie rafiki pia umdhaniae sie ndie, kwani sikuamini kama mjombaangu aliyetoka tumbo moja na mamaangu angeweza kunisariti na kutofika ilihali nilimthamini na kumsaidia sana huku nikimpuuza ba mkubwa kuwa ana mila za kizamani lakini leo hii niliyempuuza ndie kaja kunifariji jera na mahakamani yupo ila yule niliyemtegemea awali hata salamu zake za kunifariji sikuzipata. Ina maana ameamini mimi

    ...



    Hussein bubu aliendelea kumshangaa yule kijana pindi alipokuwa anabisha kutaja jina lake na kung'ang'ana na kusema kuwa wanawake ni wauaji mpaka yule kamanda alipopewa agizo na mkuu msaidizi wa gereza kuwa amuache ndipo alipoachwa na kujumuishwa na wafungwa wenzake kisha kupewa sare zao kabla hawajachanganywa na wenzao ndani ya lile gereza.



    Muda wote cj4 alikuwa kimya na mara nyingi alionekana mtu wa mawazo sana hata walipokuwa wanatolewa na kupelekwa kwenye kazi za kuvunja kokoto ambapo Hussein bubu yeye alikuwa kwenye kitengo cha kusambaza maji ya kunywa kwa wafungwa wenzake.

    Hali ya mfungwa yule mpya kutopenda kuzungumza na kufanya kazi kwa nguvu huku akionesha ni mtu mwenye mawazo mengi ilianza kumvutia Hussein bubu na kujikuta anaweka ukaribu nae kwa siku tano tu baada ya kuja kwake na Hussein alijifariji moyoni kuwa yule ni mtu pekee anayeweza kukaa nae kwani alihisi yaliyomkuta ni makubwa kama yaliyomkuta yeye.

    Lakini kichwani kwa Cj4 alikuwa na nia moja tu ya kutimiza agizo alilopewa na Mkuu wa majeshi lililotoka kwa Amiri jeshi Mkuu mh Rais wa jamhuri a Muungano wa Tanzania.

    Ukaribu alioutengeneza kwa mbinu maalum na kumteka Hussein bubu pasi na kutarajia ilikuwa moja ya hatua kubwa aliyoidhamiria Cj4 na taratibu Hussein alianza kufunguka kumpekua Cj4 ili kujua kulikoni kilichompata japo awali Cj4 alionesha ugumu wa kutopenda ukaribu na Hussein lakini baada ya wiki moja aliamua kuwa mpole na kipindi cha mapumziko ama chakula walikaa pamoja na taratibu Cj4 alianza kumsimulia Hussein mkasa wake wa uongo lakini uliomhuzunisha sana Hussein na kujikuta nae anamsimulia mkasa wake mpaka yuko pale na ndipo walipotengeneza urafiki.



    "Laiti kungekuwa na askali muelewa na mwenye roho nzuri nadhani angesikia kilio changu na kunisaidia lakini daaah!! nawachukia sana hawa askali wetu wooote wapuuzi na makatili watupu"

    alilalama siku moja Cj4 alipokuwa anapata chakula cha jioni sambamba na Hussein bubu.

    "Dah! pole mwanangu lakini kumbuka si askali wote wabaya."

    alitetea Hussein bubu

    "Hapana mzee we kufungwa kote huku na kuteseka kwa kesi usiyoitenda hadi unafikia huko mbona hajatokea hata askali mmoja kujipendekeza walau kiuongo kwa kukuonea huruma ama kukusaidia kivyovyote?? hawa wanyama tuu usiwaamini babu"

    alizidi kukazia Cj4 lakini alifanya haya yote kwa makusudi ili kumtia katika kumi na nane zake Hussein pasi na kutambua na kuanza kufunguka ajenda kuu aliyoifata na siku hiyo ilikuwa ni siku ya kumi na mbili tangu afungwe pale na siku tano tangu wawe marafiki.



    "Sikia nikwambie mwanangu, mi mwenyewe awali niliamini hivyo na nilikaa kimya zaidi ya miaka ishirini lakini baadae alitokea askali ambae sikuwahi kuwaza hapo awali kama anaweza kuwepo askali mwenye roho ya imani tena mkubwa kama huyo bwana ambae alinihurumia na kufanya kila jitihada za kunisaidia na kuutafuta ukweli wa kesi yangu japo ni ya miaka mingi sana. aaah! usihofu mwanangu wewe kesi yako bado changa sana usijikatie tamaa hivyo naamini kama yule kijana asingepatwa matatizo na angekuwepo nadhani toka siku ile ya kwanza unaingizwa hapa angeshakwita kutaka kujua kilichokusibu na ungestaajabu mwenyewe."



    "Mh! siamini mzee kama kuna mtu kama huyo... yaani atake kukusaidia juu ya kesi yakoi ya miaka mingi? angeanzia wapi??"

    "Aaagh! baba inabidi uamini tu kwani hiki nikuambiacho si ndoto"

    "Mh! basi huenda atakuwa alikuongopea tuu kwa kuwa wewe upo ndani usingejua chochote."

    "Naamini asilimia zote hakuwahi kuniongopea kwani hata matatizo yaliyosababisha asiwepo hapa leo hii naamini ni kwasababu yangu asilimia tisini."

    aliropoka Hussein na kutupa plate ya chakula na kusogea pembeni huku machozi yakianza kumtoka baada ya kujitonesha kidonda chake makusudi na kuanza kumkumbuka Kamishna Shebby ambae mpaka muda huo hakujua anaendeleaje japo alijua kuwa alinusurika kule kwenye shambulizi Mkuyuni.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ukaribu wa Dokta Asha na Kamishna Shebby ulianza kuwavuta katika hisia moja mioyoni mwao japo kila mmoja alibaki akimuonea soni mwenzake hasa Kamishna Shebby.

    Hata mzee Mwinchande na mkewe walibaini kitu hiko na walitamani mtoto wao amuoe yule Dokta hasa walivyoona jinsi alivyokuwa anamuhudumia kwa upendo na ilikuwa kawaida halali hadi muda Shebby amelala na kabla Shebby hajaamka ye anakuwa tayari yuko macho.

    Yaani kwa jinsi Dokta Asha alivyojituma kumuhudumia Shebby hadi mzee Mwinchande akaona kile kiasi anachomlipa hakitoshi japo ilikuwa ni zaidi ya milioni kumi kwa wiki.



    * * *

    Siku moja ambapo ilikuwa siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Kamishna Shebby huku wakialikwa watu wachache sana katika hoteli maaalum waliyoikodi kwa niaba ya tafrija ile.

    Shebby akiwa bado kumbukumbu zake hazijakaa sawa aliongozwa na Dokta Asha katika kila steji wakati tafrija ilipokuwa inaendelea hadi wakati wa zoezi la kukata keki japo aliweza kusimama bila kutegemea gongo na kutembea mwenyewe lakini bado balance ya mwili ilikuwa haijakaa sawa na ndio sababu Dk, Asha hakuwa mbali nae.

    Ki ukweli dk Asha na Kamishna Shaaban walipendezana sana na hata wahudumu wa hoteli walijua kuwa ni wapenzi lakini haikuwa hivyo na kabla Shebby hajamlisha yeyote keki mc alimuomba azungumze chochote kuhusu siku yake ile ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake na ndipo taratibu baada ya kukamata kinasa sauti na kuangalia huku na huko Kamishna Shebby alianza kuzungumza na kila mtu alitulia akimtazama na kumsikiliza kwa umakini.



    "Kwa kweli kikubwa namshukuru sana Mungu kwa kunifikisha umli huu japo bado naumia moyoni mwangu kwa kushindwa kukumbuka yaliyonikuta hadi muda huu pia napenda nichukue nafasi hii kumshukuru sana tabibu wangu aliyejitoa kwa hali na mali kuhakikisha nakuwa mzima na kutembea kama zamani ila ningependa pia nimwambie kitu kilicho moyoni mwangu na kila mtu nataka asikie ili nimuaminishe pia nimuhakikishie kuwa hiki ninachoongea kinatoka kweli moyoni mwangu na si vinginevyo..."

    alipofika hapa kamishna Shebby alinyamaza kidogo na kumtazama dk Asha aliyeonesha nae kuwa na shauku kubwa ya kusikia hiko kitu ndipo Shebby alipoendelea

    "Dokta Asha.. Dokta Asha Nakupenda sana na naomba ukubali niwe wako ili tuunganike na kuwa mke na mume siku za usoni tuzidi kutengeneza ukaribu na kuzalisha familia bora pamoja. Naomba unikubali Asha na kama utanikataa naomba uthibitishe mbele ya wote wanaonisikia sasa hivi humu ndani.

    Kwanini niutese moyo wangu kwa kuficha ukweli halisi uliomo? Nakupenda sana dokta Asha nikubali tafadhali.."

    Maneno ya Shebby yalimstua kila mtu aliekuwa ukumbini na kufanya watu wote wamgeukie Dokta Asha ambae alijikuta anainamia chini kwa aibu na mshangao kwa kutoamini kama kweli mgonjwa wake ambae hata yeye mwenyewe alishaanza kuwa na hisia nae za uhitaji wa kuwa karibu zaidi lakini hakufikiri wala kuzani kama Shebby angefikia hatua ile ya kutamka maneno yale hadhalani vile.



    mzee Mwinchande alitabasamu sambamba na mkewe mara baada ya kumsikia mtoto wao wa pekee akisema yale maneno na kuanza kumpigia makofi kwa ujasiri aliouonesha na kuwafanya na watu wengine taratibu kuanza kumpigia makofi Kamishna Shaaban na hapo ndipo mc alipochombweza kidogo kwa maneno ya bashasha na kupiga wimbo mmoja wa kizungu ulioimbwa na westlife ujulikanao kama Queen of my Heart na hapo ndipo Dokta Asha alipoinuka huku uso wake ukibubujikwa na machozi mepesi ya furaha na kwenda kumkumbatia Kamishna Shebby kwa kuashilia kuwa alikubali kwa moyo mmoja ombi la kamishna Shebby.

    Na hivyo ndivyo mapenzi baina ya kamishna Shebby na Dokta Asha yalivyoanza rasmi.



    * * * * * *



    Cj4 alimsogelea Hussein bubu na kumshika bega

    "Pole sana mzee wangu lakini kwanini unaamini kuwa matatizo yaliyompata yamesababishwa na wewe"

    aliuliza kwa upole Cj4 na kumfanya Hussein akiuvunja tena mwiko wake aliojiwekea na kuanza kumuhadithia kwa ufupi kilichotokea baina yake na Kamishna Shebby kwa kuamini kuwa yule aliyekuwa anaongea nae ni mfungwa mwenzake aliyeponzwa na mwanamke na kubambikiwa kesi ya kuhuzunisha kama yeye bila kujua sivyo alivyofikiri bali alikuwa anatoboa siri kwa Komandoo aliyeletwa pale kwa kazi hiyo maalum ya kutafuta kilichomsibu kamishna Shebby hadi aende kwenye mission ya siri iliyopelekea vifo vya askali wenzake na kusababisha kupoteza kwake kumbukumbu.

    "Kwa hiyo daah! kumbe kuna mtu anajiita mr.X ndie aliyekuwa anamuumiza kichwa huyo Kamishna?"

    "We acha tu mwanangu ila nakuomba habari hii usije kuongea na mtu mwengine yeyote kwani sipendi kabisa matatizo mengine yatokee. Sina imani na huyo Mr.X huenda akawa jini ila namuomba Mungu siku moja nije kumuua mimi mwenyewe kwa mikono yangu."

    alisisitiza Hussein bubu na muda huo huo firimbi ilipulizwa na muda ulikuwa umeisha wa kupumzika hivyo walinyanyuka na kuendelea na kazi.



    Lakini baada ya siku tatu baadae Hussein bubu anastushwa na taarifa za kutoweka kimaajabu kwa mfungwa ambae ndie yule rafiki yake walietokea kuzoeana ghafra.

    Hakuzielewa haraka tetesi zile ambazo zilizuka kwa wafungwa wengine ambao walikuwa wamefungwa ukanda mmoja na yule kijana swahiba wa Hussein kutokana na yeye kuwa upande mengine ambao alihamishiwa kipindi cha nyuma kwa msaada wa Kamishna Shebby.

    "Kh!! sasa katorokatoroka vipi? au alikuwa jini yule?? "

    lilikuwa ni moja ya swali lililomuumiza kichwa Hussein baada ya kuthibitisha kuwa yule kijana hayupo tena ndani ya gereza na kuna timu ya maaskali iliyotumwa kufanya msako juu yake.



    * * * * * *



    Ndani ya kijiji cha mkuyuni stendi kuu iliyokuwa mkabala na soko alionekana kijana mmoja aliyevaa nguo chakavu akishuka kwenye roli lililotokea mjini na kuja pale mkuyuni kwa ajili ya kupakia ndizi.

    Akiwa kabeba fuko lake la rambo na mkononi kashika pingili ya mua aliokuwa anaumenya taratibu kwa mdomo huku akipiga hatua mdogo mdogo kutokea kule kwenye lile roli mara baada ya kuwashukuru wahusika waliokaa mbele akionesha dhahili alibebwa kwa msaada tu, ndipo yule kijana alianza kuchanja mbuga na kuelekea mabondeni akiifata njia moja iliyoelekea ndani kidogo ya maeneo ya soko huku watu wengi aliokuwa anapishana nao walionesha kumshangaa japo hakujua walimshangaa kwa jinsi alivyo au kutokana na ugeni wake pale Mkuyuni.



    "Samahani babu shikamoo"

    alisalimia yule kijana alipomkuta babu mmoja akiwa kabeba jembe akielekea njia ile aliyokuwa anaenda yeye.

    "Asante mzukulu, kugenda kwani?"

    aliuliza yule mzee ambae ilionesha kiswahili chake hakikuwa kizuri zaidi aliongeama kwa lugha ya kirugulu ambayo haikumpa tabu sana yule kijana.

    "natafuta sehemu mzee nitayoweza kupata chumba cha bei nafuu sana niweze kujisitiri"

    "Ng'andaaa mh! tuke huku kwani we mgeni mzukulu?"

    "Ndio babu"

    "Tapata tuke hakuna ng'anda zimema"

    aliongea yule babu na kuongozana na yule kijana hatimae wakafika kwenye kijiji kimoja ambapo kulikuwa na nyumba ambayo ilikuwa kama imetelekezwa kutokana na matukio yaliyowahi kutokea mtaa ule na alionekana mama mmoja aliyerukwa akili (chizi fresh) akiwa pekee anayeishi pale.

    "Ahano ng'anda hii mzukulu tuke kwa mjumbe ukamlongele akusaidile utawasa tu mzukulu"



    alionesha ile nyumba yule mzee kisha kwenda nae sambamba kwa mjumbe ambae hakuwa mbali na eneo lile na ndie alikuwa kama mmiliki wa haki ya nyumba ile na walipofika mzee alisalimiana na mjumbe kisha kumkabidhi mgeni wake huku akimsisitiza amsaidie.

    "sawa kijana karibu, Enhee umetoka wapi, unaitwa nani, na ipi hasa shida yako"

    "Mzee mi naitwa Ndonga ni mgeni kabisa nimetokea Kilosa nilipoenda kumtafuta kakangu ambae sikufanikiwa kumpata baada ya kutoka kwetu Kigoma na kumtafuta kwa muda mrefu hadi nikakosa muelekeo pale kilosa ndipo nilipoelekezwa kuwa alihamia hapa mkuyuni sasa naomba unisaidie sehemu ya kulala hata kwa kulipia pesa kidogo kwani uwezo wa kulipia guest sina na ndio nimeelekezwa hapa na yule mzee tafadhali sana mjumbe naomba msaada wako nihifadhi mtoto wako"



    aliongea kwa lugha ya upole na unyenyekevu yule kijana na kumfanya mjumbe amtazame huku akifikiria jinsi ya kumsaidia.

    "Mh! kijana wanguuuu kiukweli hapa mkuyuni nyumba ni gharama japo unapaona kijijini ila kuna nyumba moja ambayo inaweza kuwa rahisi kuipata kwa kuwa ilikuwa ya marehemu babaangu kabla hajamuuzia mganga furani ambae nae alishafariki, lakini sasa pale kuna matatizo kidogo yalitokea na watu wote waliikimbia ile nyumba kasoro mama mmoja ambae kidogo akili zake hazipo sawa ndio yupo pale. sasa sidhani kama patakufaa ama wewe ulionaje?"

    "Mh! mzee wangu yani mi siwezi kubagua sehemu ilimradi nihifadhi ubavu wangu kwa visiku hivi nikiendelea kumtafuta ndugu yangu"

    "Sawa sasa itabidi nikuandikishe kisha nikupeleke sehemu yenyewe hapo mbele tu ila naomba uwe muangalifu usije kuthubutu kumghubudhi yule mama japo akili zake hazipo vizuri"

    "ondoa shaka kabisa mjumbeee Aaagh! Mungu akubariki sana baba kwa msaada wako"

    alishukuru huku akipiga magoti yule kijana na kutoa noti ya shilingi elfu tano iliyochakaa sana kutokana na fundo alilolifunga sehemu za pensi lake alilofunga kwa mkwiji wa kamba ya mti.



    Baada ya kuafikiana na mjumbe alipelekwa kwenye ile nyumba iliyokuwa imepooza na kwa nje walimuona yule mama ambae aliwaangalia tu bila kusema kitu na baada ya mjumbe kumuonesha chumba cha kutumia huku akimwambia kuwa kama atakaa wiki moja pasi na kuonana na huyo nduguye itabidi ampeleke kwa mwenyekiti wa serikali ya mtaa ili atambuliwe na ikiwezekana aandikishwe kama mkazi wa eneo lile ili kila mtu aelewe ujio wake.

    Baada ya hapo Mjumbe alitoka mule ndani na kumuacha yule kijana akikung'uta mavumbi kwenye kile chumba kilichokuwa na mkeka na kigoda cha miguu mitatu tu.

    "Shabbashh Nice Step creat another good Chance"

    alijisemea mwenyewe yule kijana na kugonganisha mikono yake huku akiwa na furaha mno moyoni mpaka usoni.

    Hakuwa mwengine yule kijana bali ni Komandoo Jumanne ama Cj4.



    * * * * * *



    Baada ya siku kadhaa kupita tangu kufanyike ile tafrija ya kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwa Kamishan Shaaban na kuanza rasmi mahusiano ya kiuchumba baina yake na Dokta Asha, siku hiyo walionekana wakiwa wawili maeneo ya fukwe huku dereva ambae alikuwa ni mlinzi pia aliyetumwa na jeshi la polisi kwa niaba ya kuchunga usalama wa Kamishna Shebby alikaa sehemu moja ya juu akiwaangalia wapendanao Shebby & Asha wanavyokokotana na kurushiana maji maeneo ya fukwe huku wakiwa na nyuso za furaha.



    "Nakupenda sana Asha"

    "Hata mimi Shebby tena nilikupenda toka siku ya kwanza nilipokuona"

    "Haa acha utani Ashaa"

    "Kweliii"

    "sasa kwanini hukunambia mapema hadi nimekuanza mimi"

    "aaah! si nlikuwa naogopaa!"

    "tehtehteheee huyoo"



    Basi ilikuwa full upendo maeneo ya fukwe pindi walipokuwa wanataniana na kuchombwezana baina ya Kamishna Shebby na Dokta Asha.

    Hata jioni yake waliporudi nyumbani kwenye jengo kubwa la kifahari la mzee Mwinchande bado waliendelea na utani wa hapa na pale mpaka wanaingia kulala ambapo ulikuwa ni usiku wa tatu toka waanze kulala pamoja lakini walilala kindugu ndugu kwanza kutokana na maelezo ya Dk Asha kuwa inahitajika Shebby kujiponesha zaidi na atapokuwa sawa aende kujitambulisha kwao pindi ataporudi na wakioana ndipo watapata uhuru wa kucheza sebene pamoja muda wote hasa nyakati za giza.



    Lakini muda mwingi Kamishna Shebby anapokuwa amesinzia Dk Asha hutumia wakati huo kumuangalia vizuri Shebby na kumpekua sehemu za kichwa huku akimuonea sana huruma hadi muda mwengine machozi yalimtoka bila kujitambua Asha lakini hakuwa na chochote cha kumwambia Shebby zaidi ya kunyamaza na kumsikitikia.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    * * * * * *



    Asubuhi na mapema ndani ya Kijiji cha Mkuyuni kwenye nyumba ile ile ya mzee Mnyungunyungu ambayo shabaha na mipango ya Cj4 ilienda barabara na kutua sehemu husika kabisa na hesabu zake alizopiga awali ili kubaini kilichowakumba askali na kilichoikumba ile familia zaidi akitafuta ukweli wa huyo mr X.



    Alijinyoosha pale ndani na kutoka nje asubuhi na mapema na kuelekea kule kwenye choo ambapo njia yake ilionesha kuwa na majani majani yaliyoashilia kuwa kile choo alichokuwa anaenda yeye hakikutumiwa muda mrefu kidogo.

    Alitembea taratibu huku akipiga hesabu nyingi kichwani kutokana na maelezo aliyokuwa nayo juu ya tukio la mtu wa mwisho wa familia ile ambae inasemekana alikutwa amejinyonga ama amenyongwa pindi alipoenda chooni.

    Kwa kutumia akili za kijeshi na mbinu hadimu alizokuwa nazo Cj4 alisimama ndani ya kile choo na kuangalia juu ambapo kulikuwa na matawi makubwa ya miti yaliyokatisha na kuvuka kile kipaa cha choo ambacho kilikuwa hakijaezekwa na alitumia dakika tano kutazama vizuri kule juu na kuanza kurudi nyuma huku akivuta taswira na kutengeneza picha kichwani mwake ambapo alianza kuona yule mtu alipoingia pale chooni na aliangalia kwa juu na kuona kamba iliyotengenezwa mtindo wa kitanzi kikubwa ikishushwa taratibu na kumvaa pindi aliposimama na kabla hajafurukuta kitanzi kikapandishwa na kumkaba shingoni.



    Alizunguka kwa nyuma ya choo Cj4 harakaharaka huku ile taswira ikiwa bado kichwani mwake na kuangalia upande wa juu na kuona kuwa alilala mtu shupavu na makini aliyevaa nguo maalum na vifaa vya kininja akiwa anaivuta ile kamba kwa kuizungusha kwenye skurul aliyoifunga kwenye tawi ambayo ndio ilishikilia ile kamba maalum aliyomshushia na kumkaba yule bwana aliyekuwa chooni na kupanda juu taratibu huku akiwa anapapatika na kushindwa kutoa sauti kwa jinsi alivyokabwana na pindi alipofikishwa juu kabisa ya lile tawi alikuwa tayari ashakufa na alichofanya yule ninja aliyekuwa anamuona kwa taswira tu kuwa alichomoa skurul baada ya kuivinga kamba yenyewe kisha kumuacha yule mtu akiwa ananing'inia pasi na kumgusa mithili ya mtu aliyejinyonga mwenyewe.



    Alizunguka tena Cj4 na kuendelea kuiona taswira kuwa yule Ninja alishuka na alipofika chini akaondoka kabisa eneo lile.

    Ndipo akaanza kufata hatua alizohisi moja kwa moja alipita yule muuaji.

    Wakati huo Cj4 alikuwa makini mno na akiwa anaendelea kutokomea kabla hajafika mbali alistuka baada ya kusikia mtu akipiga chafya na alipogeuka kumtazama alimuona kwenye kichaka kilichokuwa jirani na ule mti mkubwa na ilionesha wazi yule mtu alikuwa anamtazama kwa muda mrefu tu hasa kwa jinsi nae alivyostuka baada ya kutazamana uso kwa uso na Cj4







    "Afadhali mzee nadhani wewe utanisaidia"

    aliongea Cj4 na kupiga hatua kumfata yule mtu ambae alikuwa ameshika Mundu (panga la kienyeji) na kifuko kilichokuwa na maembe ambapo alijibainisha pale pembezoni mwa mti mara baada ya kujua kuwa kaonekana pindi alipokuwa anamshangaa yule kijana.

    "Mh! mbona sikufahamu baba?"

    aliuliza kwa hofu kidogo yule babu ambae alimtazama vizuri Cj4 na kupatwa woga nae wa ghafra hasa alivyomtazama sehemu za kifua na mikono huku uso wake ukionesha ni mtu wa tofauti sana kwa jinsi alivyokuwa bussy muda uliopita kabla hajamstua kwa kupiga chafya.

    "Mi mgeni hapa mzee wangu nimeingia jana tu na nimesaidiwa na mjumbe kulala hapa lakini alinambia kuwa wenyewe waliikimbia hii nyumba na watu wengi wanaiogopa sasa ndipo nami nilipokuja chooni kujisaidia moyo umeniripuka na kujikuta nakuwa na woga sana ndio maana nilikuwa naondoka nikajisaidie kule porini."

    "Hee! baba basi mi naenda shamba we kajisaidie tu huko hata wanakijiji wengine mbona wanajisaidiaga porini."

    aliongea yule mzee na kuanza kuondoka huku moyoni mwake akiwa na hofu bado "

    "Samahani lakini babu naomba nisikilize kama utakuwa na uwezo wa kunisaidia"

    alisisitiza Cj4 na kumshika mkono yule babu aliyekuwa ameanza kuondoka eneo lile.

    "Mwe!! haya nokutegeleza"

    alijibu mtindo wa sitaki nataka yule babu na kusimama tena

    "Ni hivi babu hebu njuu kwa huku kwanza nataka tuongee kitu muhimu na nitakupa pesa nyingi ili unifichie siri hii babu, ukweli mimi ni Polisi na nimetumwa hapa kupeleleza juu ya kilichotokea hapa juu ya mtu aliyenyongwa siku za nyuma, na nimekuja kuondoa uoga uliotawala eneo hili"

    aliongea safari hii kwa sauti ya chini Cj4 na kumfanya yule mzee atulie na kusikiliza kwa umakini huku moyo wake ukifurahi ghafra kwa kujua kumbe yule ni mwanausalama.



    Ndipo yule mzee alianza kumfata taratibu kwa kunogewa na story aliyokuwa anahadithiwa na Cj4 huku wakiingia kwa msituni kidogo kukwepa watu wasiwaone pia yule mzee alimuongoza Cj4 hadi maeneo yale yalipowahi kutokea mauaji ya Askali miezi kadhaa iliyopita baada ya kuulizwa kama anapafahamu.

    "Mh! baba nakuahidi ambe hajatuona mtu tukiongea,! na eneo hili watu wengi wanaogopa kufika hadi sasa hivi, basi hatojua mtu yeyote habari zako baba Niamini."

    aliongea yule babu pindi walipofika eneo lililoshona majani mengi na miti mikubwa.

    "Ni kweli mzee, lakini tatizo hata Askali aliyekuja kupeleleza awali alifanya ujinga kwa kumuamini mzee kama wewe na mwishoe akamsaliti na kusababisha Mauaji kwa askali wengine."

    Alinena kwa sauti tofauti iliyokuwa serious zaidi Cj4 na kumfanya yule mzee astuke hadi akaangusha kile kifuko chake cha maembe na na kabla hajageuka alistukia kashakamatwa kichwa kwa mikono shupavu ya Cj4 na kuanza kubinywa hadi sehemu za taya zikaanza kupishana na hakuwa na uwezo walau wa kutoa sauti ama kupiga kelele.

    "Kawaambie huko uendako kuwa Umekumbana na mstari Mwekundu wa CJ4"

    Mara Cj4 aliponena maneno hayo tu palepale alipindua kwa nguvu kichwa cha yule babu na kuivunja shingo yake kisha kumuachia na kudondoka kwenye manyasi ambapo alianza kupapatika pale chini kwa zaidi ya dakika kumi mpaka akatulia na kuaga dunia rasmi.



    "Kama na wewe uliekwa na mr.X ufanye uchunguzi wa watu wataokuja kuchunguza hapa basi ajue kuwa mbinu zake zimezeeka"

    aliongea Cj4 na kuchukua ile mundu ya yule babu na hapo aliuvinga mkono wake mmoja kwa kile kifuko kilichokuwa na maembe baada ya kumwagika pale chini kisha akatumia mkono ule wenye mfuko wa naironi kukamata sikio la yule babu na kuanza kukata ngozi yote upande wa sikio la kulia sambamba na sikio lenyewe kisha alimgeuza na kufanya vile vile upande wa sikio la lengine na kumuacha.

    ("sasa na waje tu wakupime pindi watapojua")

    aliwaza moyoni Cj4 huku akiifuta futa damu ile mundu kwenye manyasi na kuzishika vizuri zile ngozi zenye vipande vya masikio na kuanza kupiga hatua kadhaa kuelekea kule alipotoka na alipokaribia kwenye ule mti wa awali alisimama na kuchimba kishimo cha futi moja na kuzizika zile ngozi kisha akafukia na kuweka weka nyasi juu yake ambapo ilikuwa vigumu sana mtu kubaini kama sehemu ile imechimbwa.

    Alifanya hayo yote ili hata kama wataigundua ile maiti mapema na kuja wachunguzi kupima watachojua ni kuwa amevunjwa shingo tu, lakini hawatapata alama zozote za muhusika aliyemvunja hususani zile za mikono.

    Baada ya kuhakikisha mambo safi huku akiwa makini asionekane na mtu yeyote alinyanyuka na kuelekea hadi pale kwenye kile choo kwa uangalifu na kuitumbukiza ile Mundu chooni

    lakini alipotoka chooni tu na kufunua kile kigunia kilichofungwa kama mlango alikutana uso kwa uso na mtu akiwa kasimama pale pale mlango wa choo.



    * * * * * *



    )('nashukuru nimemchunguza ananipenda na kuniamini kweli, usiwe na wasi tena tuko pamoja')(

    yalikuwa ni maneno ya ujumbe mfupi wa kwenye simu aliyokuwa anasoma Kamishna Shebby pindi alipostuka usingizini baada ya alert ya simu ya dk Asha iliyokuwa kitandani kuita na alipogeuka na kumtazama Asha alikuwa bado yupo kwenye usingizi mzito japo ilikuwa tayari ni alfajiri ya saa kumi na moja.

    Aliichukua simu na kukuta ulikuwa ni ujumbe uliorudishwa baada ya kushindwa kufika kwa mlengwa na kubaki hewani kwa zaidi ya masaa 24 na alipoamua kuufungua kuona alichokuwa ameandika mchumba wake ndipo alipokutana na hayo maneno ambayo hakujua ni nani aliyekuwa ametumiwa na Asha ujumbe huo kutokana na namba husika kutoseviwa jina.

    alianza kuipekua simu ya asha na kuangalia charting za meseji za nyuma lakini hakukuta ujumbe wowote zaidi ya ule ambao ulirudishwa na mtandao husika baada ya kushindwa kumfikia mlengwa.

    Muda huo huo Asha nae alizinduka na kumshangaa Kamishna Shebby akiwa bussy na simu yake lakini alibaki anamtazama bila kumstua wala kusema lolote na kugeukia tena upande wa pili na kuendelea kulala.

    "ukimaliza baby naomba nimtumie message mama"

    aliongea kwa sauti ya kivivu Asha na kumfanya Shebby atabasamu baada ya kujua kumbe Asha alishamuona muda mrefu kuwa anapekua simu yake na ndipo Shebby alipoacha upekuzi zaidi baada ya kuona jinsi Dk Asha alivyokuwa hana wasi hata kidogo kwa kuchezea simu yake na kuamini kuwa hakuna tatizo lolote japo awali alichanganywa kidogo na ile message.

    "Eeh! baby harafu kuna message yako imerudishwa"

    aliongea Shebby huku akimkumbatia kwa nyuma Asha pale alipolala ubavu na kumpitishia simu yake ambapo Asha alipokea na kuitazama message yenyewe.

    "Aaaagh! mamaa naee.. mh! mme wangu na wewe hupitwi?"

    "kivipi tena honey"

    "sasa hii message ulivyoisoma umeelewa nini?"

    "hahahaa Asha my love, message umeandika wewe mimi nitaielewaje wakati sijui hata uliyemtumia nani na mlianzia wapi."

    "hehehee Hiloo, oteaa sasa.."

    "Mh! nimeshindwa kuotea baby hebu nijuze..!"

    "heheheee acha wivu bwana huyu mama"

    "MAMA!!"

    "Hee! sasa unastuka nini huyu mamaangu na niliongea nae jana na kumpa habari za mahusiano yetu na ndipo aliponiuliza kuwa nina hakika unanipenda kweli? lakini nilimuahidi nitamjibu ndipo baadae nilimtumia hii massege, sasa ajabu ipi..!! sema kabla sijakuvunja mguu tehtehteheee"

    aliongea huku akiongezea utani Asha na kugeuka upande ule aliolala Shebby na kutazamana usoni na mwishoe wote waliangua kicheko hasa baada ya Asha kuzungusha zungusha macho yake na Kujitunisha mashavu kama mtu aliyetumbukiza kitu kikubwa zaidi ya uwezo wa mdomo wake.

    "ha ha hahaa Dokta mzimaaa kumbe muda mwengine kama kitotoooo hahahahaaaa"

    "tokaaa hapaaa hiloo mbona we Polisi zimaaa lakini umeshindwa kuluka mto kitandani umekuwa ovyo hata umeshindwa kuramba asali iliyotelekezwa na nyuki kwa kuhofia guu kuoza aahahahahaaaaa"

    "Asha ashaa Ashaa Ashaaaa!!!! Ngoja sasa"

    aliongea kamishna Shebby baada ya utani wa Asha kumgusa kidogo na kuanza kumchezea chezea maungo yake raini yaliyofichwa na nguo nyepesi alizovaa usiku.

    "ha ha ahaa bwanaaaaniniiiiiii..Niacheee basiiii"

    aliongea kwa sauti ya kudeka Asha kipindi hiko Shebby alikuwa serious zaidi baada ya Achumani kichwa wazi kuanza kufurukuta na kututumsha bukta aliyovaa akitaka kutoka akasalimiane na mwajuma mficha asali.



    Mchezo wao wa kutekenyana na kubimbilishana kitandani ulidumu kwa zaidi ya dakika arobaini kabla ya wote kujikuta wakiwa kama walivyozaliwa na kuanza kurambana rambana taratibu kama vitoto vya mbwa mwitu huku Achumani kichwa wazi wa shebby akizidi kudondosha mate ya uchu wa kuiramba asali ya mwajuma iliyofichwa katikati ya pachupachu ya mapaja ya Dokta Asha na kumfanya Kamishna asahau kama mguu wake mmoja ulikuwa na jeraha pia mifupa bado haikuungana vizuri na hata lile swala kuhusu message aliyoisoma na kumchanganya alfajiri ile alilisahau kabisaaa kuliulizia tena kujua ile namba ilikuwa ya nani?

    Zaidi mawazo na akili yote ya Kamishna Shebby ilihamishwa na mautamu yaliyokuwa mbele yake kutoka kwenye mwili laini wenye joto la huba wa Dokta Asha.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kilichofuata ni miguno ya kimahaba na purukushani za hapa na pale kipindi Kamishna Shebby na Dokta Asha wakivunja amri ya sita mule ndani na kuishi kwenye sayari ya ajabu kwa takribani nusu saa kabla ya kila mmoja kuridhika na kubaki hoi huku wakiwa wamekumbatiana na kuangaliana machoni kama majogoo yaliyotoshana nguvu.

    "Aaagh! siamini Asha kumbe bado mtoto kabisa?"

    aliongea Shebby na kumpelekea Asha mdomo na kuanza kunyonyana ndimi huku wakifonzana mate kwa hisia kali.

    "Nakupenda sana Shebby kumbe na wewe fundi kiasi hiki Mhh! kama Simbaa!!"

    aliongea kwa sauti ya kudeka Asha na kumlalia kifuani Kamishna Shebby.



    * * * * *

    (MKUYUNI)

    ...............



    Alistuka kidogo na kushusha pumzi Cj4 baada ya kumtazama machoni yule mtu na kugundua kumbe alikuwa yule mama mtoto wa marehemu Mnyungunyungu aliyerukwa akili na alipomkazia macho ndipo yule mama alipojichekesha na kuanza kujifunua nguo huku akikimbia na kucheka kwa sauti ya juu.

    ("Mh! huyu naeeee ok nitajua cha kufanya")

    aliwaza moyoni Cj4 wakati akielekea kwenye ile nyhumba na kuingia chumbani kwake kuendelea kurekodi kile alichokuwa anakitafiti.



    Mpaka dakika hiyo Cj4 aliweza kujua sababu zilizompeleka Kamishna Shebby pale mkuyuni na alielewa kuwa yule mfungwa Hussein bubu hakuwa na makosa yoyote ila alijua kuwa mchezo ule unachezwa na huyo mtu anayejiita Mr X ambae alikiri moyoni mwake Cj4 kuwa huyo mr X ni mtu anaetumia akili nyingi sana kuliko nguvu na ana wafuasi wengi.

    Lakini alitafakari sana mule ndani na kuona jinsi ya kumpata mr X kirahisi ni sawa na hakuna kwani atakuwa anamtafuta mtu kwenye mzunguko asioujua kwani huwezi kumshinda mtu mwenye akili kwa kumtafuta ilihali humjui ila yeye anakujua kama unamtafuta na alibaini kuwa jinsi ya kumtafuta mr X ni kumtafuta pasi na yeye kujua kama anatafutwa na njia aliyoiona ni sahihi ni kumuingiza mr X kwenye mzunguko wa mission yake ili aweze kumtambua pasi na yeye kutambulika.

    ("Yap thats is a Solution")

    alijisemea kimoyo moyo Cj4 na kunyanyuka haraka kuanza kujipachika mwilini vitu vichache muhimu na pale pale alichomoa simu na kupiga kwa mkuu wa Majeshi na kumuelekeza jibu alilolipata kwa siku moja tu baada ya kutua Mkuyuni na Mkuu wa Majeshi aliporidhika alimuamuru kuwa afanye hima arudi makao makuu na yeye ataongea na Muheshimiwa Rais ili wafanye vile alivyopendekeza.

    Na ndipo baada ya hapo kwa kutumia mbinu za Kikomandoo Cj4 aliweza kutoweka Mkuyuni baada ya kuwasili na kukaa masaa 24 pekee.



    -(IKULU~DSM)-

    .......................



    Kikao cha siri kwa dharula kilikuwa kinaendelea ambapo alionekana Mh Rais sambamba na wazili wa ulinzi na mkuu wa majeshi ya ulinzi na usalama bila kumsahau Kamanda mkuu wa jeshi la polisi huku pembeni yake akionekana Jaji mkuu wa taifa.

    Mada iliyokuwa inaendelea ni juu ya swala zima lililojiri miezi ya karibuni kule Mkuyuni juu ya shambulio la polisi na kutojulikana sababu na muhusika wa shambulio hilo huku wakiongozwa mjadala ule na ripoti maalum kutoka kwa Komandoo waliyempandikiza kufanya utafiti na kugundua kuwa chanzo cha Kamishna wao kuliingiza jeshi kwenye misukosuko ni kutaka kuujua ukweli wa kesi ya zaidi ya miaka ishirini ya mfungwa mmoja aliyekuwa kwenye gereza lake ili apate kuifufua na kumsaidia baada ya kugundua kuwa alihukumiwa kimakosa na kiuonezi.

    Ripoti ya Cj4 ilikiri kuwa ni kweli huyo mfungwa ambae aliitwa Hussein alihukumiwa kimakosa lakini si kimakusudi bali kutokana na mchezo mchafu wa akili nyingi uliokuwa unachezwa na mtu asiyejulikana jina lake halisi wala makazi na wadhfa wake zaidi ya kutumia kivuli cha jina la MR.X



    Na iliongezea kuwa mr.X bado yupo na ana mtandao mkubwa na ni vigumu sana kum baini kwa kutuma wapelelezi bali ripoti ilishauri cha kufanya ni kumuingiza Mr X kwenye mtego utaofanya atume wapelelezi na majasusi wake na hapo ndio itakuwa rahisi kumpeleleza na kupambana nae.

    Na njia ya kumuingiza mr X kwenye huo mtego ni kumtoa gerezani na kumuacha huru kwa kupitia kipengele cha msamaha wa rais mfungwa Hussein na wafanye jingo itayowawezesha watu wengi wasikie na hiyo itakuwa njia ya mr X kutuma watu wakamuue Hussein ili asiongee mengi zaidi aliyoyajua na hapo ndipo wao watapata nafasi ya kuunasa mtandao wa mr X na mr X mwenyewe kwani watapandikiza ulinzi yakinifu kwa Hussein popote atapokuwa.



    "Jaji unasemaje, unakubaliana na hiyo ripoti ya kijana wetu?"

    aliuliza muheshimiwa Rais mara baada ya wakuu wote wa jeshi kukubaliana na ripoti ile kasoro Jaji ambae bado alikuwa anafikiria kitu.



    "Mh! muheshimiwa ripoti sio mbaya sana ila nilikuwa na wazo japo najua hata nikipingana nayo itakuwa ishapita kutokana na uchache wangu na wingi wenu lakini napenda kupendekeza wazo langu kuwa kwanza tunalazimika kuonana na wastaafu wa kipindi hiko na kuwahoji kwa pamoja hasa wakuu wa usalama kwani naamini kwa akili za huyo mr.X lazima atakuwa alikuwa mmoja wa wakuu wa usalama nchini na si mtu wa kawaida na pengine alipendwa sana na wananchi na alikuwa na sifa hapa nchini ambayo hataki ipotee wala ichafuliwe. kwa hiyo napendekeza wapatikane watu kama wazili wa ulinzi mstaafu wa kipindi hiko, mkuu wa majeshi kwa bahati mbaya hatunae ila yule wa polisi uzuri bado yu hai yupo huko Morogoro."

    aliongea Jaji kauli iliyomfanya mh Rais kutikisa kichwa kwa ishara ya kukubali.



    "Enheee harafu huyu kamanda wa pilisi namkumbuka vizuri miaka ile si mzee Cyplian kama sikosei... na isitoshe tulikuwa nae katika shughuli ya kuwaaga marehemu siku ile na alinambia kuwa kumbe yule mkuu wa kituo Mkuyuni aliyeuawa alikuwa mwanae."

    alidakia kamanda mkuu wa jeshi la polisi

    "Basi vizuri Jaji itabidi tufanye hivyo pia ila kwa njia ya kijeshi na usalama zaidi tutayafanya hayo yote kwa pamoja aachiwe huyo mfungwa na kipindi hikpo hiko wastaafu muhimu tutakuwa nao faragha na itakuwa rais zaidi kubaini kama mmoja wao akawa ndie Mr X"

    aliongezea mkuu wa Majeshi na baada ya makubaliano hayo kikao kilifungwa.



    * * * * * *



    Saa zilikatika, siku zilisonga na baada ya wiki kadhaa tena mbele hatimae Kamishna Shebby alipona vizuri mguu wake na kuweza kutembea kwa ufasaha huku mapenzi baina yake na dk Asha yakipamba moto siku hadi siku hali iliyowafurahisha na kuwachochea wazazi wa Shebby kutaka kuona mtoto wao akimuoa kabisa yule daktari wa kipekee.

    Hata moyoni mwake dk Asha alizidi kumpenda Kamishna Shebby na kuwa radhi kuolewa nae.



    Siku moja majira ya usiku sana ikiwa ndio ilikuwa siku ya mwisho kwa dk Asha kuwepo pale kwenye jumba la mzee Mwinchande baada ya kumaliza shughuli ya kumtibu kijana wake na ilipaswa arejee kwao ili kama taratibu za ndoa zianze kufanywa na ataporejea awe Mke rasmi wa Kamishna Shebby, ndipo usiku huo baada ya Shebby kupitiwa na usingizi Dokta Asha alinyata na kuchomoa pakiti ya sindano kwenye moja ya mabegi yake ya dawa na kuchukua kichupa kimoja kilichokuwa na dawa maalum ya ganzi na usingizi ndani yake na kuichoma kwa kuiingiza ndani ya bomba la sindano kabla ya kumchoma taratibu Shebby ambae alikuwa kalala fofofo na baada ya dakika kadhaa ndipo alipochukua kifaa maalum mithili ya bastora ambapo ndani yake kulikuwa na bomba la sindano kubwa na nyuma sehemu ya kushikia kulikuwa na waya wa umeme ambao aliupeleka mpaka kwenye socket na kuichomeka kisha kuiwasha na kumsogelea kitandani Shebby.

    "am so sorry baby kwa kufanya haya bila ya ridhaa yako but it's all about Love"



    aliongea mwenyewe Dk Asha na kum busu kwenye paji la uso Shebby ambae tayari alikuwa ndani ya nusu kaputi na ndipo taratibu alikamata lile bomba lililo katika muundo wa bastora na kumpekua Shebby sehemu za kichwani pale alipokuwa anapenda sana kumshika na kupatazama kwa muda mwingi huku akionesha kumuhurumia muda mwengine hadi akawa analia na taratibu aliuelekeza mdomo wa lile bomba na kubonyeza kitufe furani mithili ya kile cha kuruhusu risasi itoke huku akiutuliza kwa umakini mkono wake kwa kuundamiza ule mdomo wa bomba huku akizungusha kijidude kilichokuwa pale ulipoanzia waya ulioelekea kwenye umeme na ndipo mara kwa ndani ya bomba kulianzakuonekana damu zikiingia baada ya kusikika mlio wa 'prruchuu' ndani ya bomba na kuonekana kijisindano kidogo ndani yake kilichotoka kichwani mwa Shebby.



    Alichukua pamba na kuibandika pale kichwani mwa Shebby haraka haraka na kuchukua sprit maalum na kuimwagia pindi tu alipotoa lile bomba mfano wa bunduki ili kukata vijidamu vilivyoanza kutoka kupitia kijitobo chembamba kilichosababishwa na ile sindano kubwa iliyotoka ndani yake na kufonza damu sambamba na kile kijisindano kilichotoka kichwani mwa Shebby.



    "Ohh! my God, pole sana honey hope now mambo yataanza kurudi nakuwa sawa polepole. Najua hautajua nami sitomwambia mtu honey."

    aliendelea kujisemea Dk Asha mithili ya kuwa alikuwa anaongea na Shebby ilihali Shebby hakuweza kusikia wala kuhisi chochote.

    Asha alikuwa mtaalam sana kwani aliweza kupakausha na kupashona na vijiuzi maalum vyenye rangi kama ngozi ya binaadam kabla ya kukibandika chengine kwa matilio maalum yaliyoweza kuziba kabisa na kuwa vigumu sana mtu kubaini kama sehemu ile ya kichwa cha Shebby kulikuwa na jeraha lolote.



    Baada ya hapo alisafisha vizuri na kukitoa kile kisindano kilichotoka kichwani mwa Shebby kilichokuwa ndani ya bomba na kukitazama kwa umakini kabla ya kukihifadhi kwenye matereo yake na baada ya kuhakikisha kila kitu kipo sawa alimchumu Kamishna Shebby kisha na yeye kulala.



    Asubuhi kulipambazuka na kamishna Shebby aliamka kama ilivyoada na kumkuta dk Asha akiwa anajiandaa andaa kuonesha kuwa aliamka muda mwingi

    "so baby mi mkataba wangu ndio hivyo tena, sasa kama kupona kwako ndo na mapenzi yameisha tutajua pindi nitapokuwa kwetu"

    aliongea na kufanya utani kidogo dk Asha kipindi hiko Shebby alibaki kalala chali pale kitandani akiwa kaegama kwenye mito akimuangalia Asha huku moyo wake ukitamani asiondoke.

    Lakini hakukuwa na jinsi ukweli ulibaki kuwa mkataba wa Asha kuendelea kuwapo pale ulikuwa umeisha na ni zaidi ya milioni miamoja sabini ziliingizwa kwenye account yake kwa muda ule mfupi alioutumia kukaa pale kwa mzee Mwinchande na kumuhudumia Kamishna Shebby.

    Lilikuwa ni jambo la furaha sana kwa familia nzima mara baada ya Shebby kujiandaa na kutoka sambamba na dk Asha pale kwenye sebule yao kubwa ambapo kulikuwa kumekatwa upande kwa niaba ya vikao vya dharula na kuungana na familia nzima iliyokuwa tayari eneo lile kwa dhumuni la kufanya tafrija fupi ya kumuaga dk Asha na kumshukuru kwa yote aliyofanikisha kuhakikisha Kamishna Shebby anarudi kwenye hali ya kawaida.



    Tafrija iliongozwa na mzee Mwinchande mwenyewe kwa kutoa maneno ya hekima na nasaha kwa Asha huku akimsisitiza aendelee kuwa na moyo ule wa kipekee na asije kubadilika pindi watapotuma watu kwaajili ya kujitambulisha huko kwao kwani walihitaji kuunganisha undugu na ukaribu kabisa kwa njia ya kuolewa na mtoto wao Kamishna Shebby.

    "Nashukuru sana baba nami sitoweza kubadilika kwani ukweli nampenda sana Shebby"

    aliongea kwa sauti laini Asha na kuwafanya wote watabasamu na baada ya tafrija kuisha gari maalum aina ya Lange ambayo ilikuwa ni mali ya Dk Asha iliondoka sambamba na escot kutoka kwa kamishna Shebby mpaka maeneo ya jilani kabisa na alipokuwa anaishi Asha ambapo alidai kuwa anaishi na mamaake na isingekuwa vyema Shebby kufika moja kwa moja japo ilijulikana kuwa alikuwa ni mgonjwa wake.

    Na hapo ndipo walipoachana Shebby na Asha japo mawasiliano yaliendelea kuwapo huku mawazo yao yakilenga siku ziende haraka ili waoane na kuwa pamoja.



    * * * * *

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwa mara nyengine Cj4 anaonekana akiwa kavaa mavazi ya kipolisi yenye cheo cha Inspector huku akiwa anaendeesha gari aina ya Land cruiser nyeupe ya kipolisi speed kali kwenye barabara ya vumbi na safari yake ilimpeleka hadi mbele ya kituo kikuu cha polisi Mkuyuni ambapo baada ya kushuka alipigiwa saloot na askali aliowazidi cheo mahala pale na moja kwa moja alienda kukutana na mkuu mpya wa kituo na baada ya kusalimiana alijitambulisha.

    "Naitwa Inspector Sudy kama ulivyoipata taarifa ya ujio wangu nimekuja kwa nia ya kukutana na baba wa marehemu mkuu wa kituo aliyekutangulia kwa ajili ya kwenda nae makao makuu Dar."

    aliongea kwa ukakamavu Cj4 japo ukweli hakuwa askali polisi bali ulikuwa ni mpango wa siri tu uliofanywa na viongozi wakubwa ili iwe rahisi kufanikisha zoezi la kwenda na mzee Cyplian kwa mahojiano maalum ya siri ili wapate kumvumbua huyo Mr.X

    "Sawa Inspector basi utaongozana na vijana wachache wataokupeleka mahala anapoishi mzee Cyplian"

    alijibu mkuu wa kituo na baada ya hapo amri ilitolewa na ndipo Difender moja iliyowabeba askali watatu iliongoza njia na kufuatiwa na gari ya Cj4 moaka kule ambako alikuwa anaishi baba wa marehemu Ocs John ambae ni mzee Cyplian



    Baada ya mwendo wa dakika ishirini waliingia mbele ya nyumba moja ya kifahari licha ya kuwa ilikuwa kijijini mbali na barabara kuu lakini ilitosha kumjuza mpita njia wa eneo lile kuwa mtu aliyejenga pale si mtu wa kipato cha chini.



    Mara baada ya gari kusimama na walinzi ambao pia walikuwa ni askali wa jeshi la polisi walifungua geti na kuukaribisha ule ugeni ulioongozwa na inspector fake Cj4 mpaka ndani ya sebule kubwa baada ya kukaribishwa na kuruhusiwa na mzee Cyplian kwa njia ya simu ya upepo pindi askali alipomjuza juu ya ugeni ule na muda mfupi Cj4 alipokuwa ameketi sebuleni mzee Cyplian alianza kushusha ngazi taratibu huku akiwa amevalia suti nadhifu na mkononi mwake akiwa na bluefcase ndogo na kufika pale sebureni.

    "Karibu sana kijana, nina taarifa zote za ujio wako na nilikuwa nakusubiri wewe hahahaa karibu sana mwanangu."

    aliongea mzee Cyplian na kupeana mikono na Cj4.



    Hakukuwa na muda wa Kupoteza zaidi ya Cj4 kuongozana na mzee Cyplian mara baada ya kuagana na familia nzima aliyoikuta pale akiwemo mama mzazi wa marehemu Ocs John na baada ya kutoa pole kwa mara nyengine aliaga na safari ilianza huku akiescotiwa na ile Difender mpaka morogoro mjini ambapo Difender ilirudi Mkuyuni nae kunyoosha tairi kuwahi Dar es Salaam huku kichwani mwake akipiga hesabu juu ya maswali ya kumuuliza yule mzee kabla hawajafika sehemu husika.



    * * * * * *



    Akiwa amekaa sebuleni akifatilia taarifa ya habari ikiwa ndio wiki yake ya mwisho kuendelea kuwapo nyumbani baada ya kupona vizuri, kamishna Shebby alistushwa na habari iliyokuwa inatangazwa muda huo juu ya wafungwa walioachiwa huru kwa msamaha wa rais huku kivutio kikubwa kikiwa kwa mfungwa mmoja ambae kesi yake ilitikisa miaka mingi naye si mwengine bali ni Hussein Bakari a.k.a babu bubu jina la utani alilopachikwa akiwa huko gerezani.

    Macho yalimtoka Shebby baada ya kukumbuka kitu na kujikuta anaropoka kwa sauti ya juu na kumuita babaake aje pale sebureni aone.



    "Baabaaa babaaa njoo , Nimekumbukaaa.. Aaagh!! nimekumbukaaa Nimekumbukaaa babaaa"

    aliongea kwa furaha Shebby na kuwafanya wazazi wake warudi huku wakiwa na taharuki kwa shangwe na maneno ya mtoto wao.

    "Vipi mwanangu?"

    "Nimekumbuka baba, kumbukumbu zangu sasa zimerudi aaahhh!"

    "Allahu akbaaru Allaaaah akbaaaaar"

    alishukuru na kufurahi mzee Mwinchande huku wakikumbatiana na mkewe baada ya kijana wao kuthibitisha kuwa kumbukumbu zake zimerejea sawia.

    "Kipi kimekukumbusha mwanangu?"

    aliuliza kwa furaha na kutoamini mzee Mwinchande

    "Taarifa ya habari, ngoja nimpigie Asha nimwambie nae Mungu amenisaidia nimekumbuka kila kitu sasa sina wasiwasi tena pindi nitapokutana na Kamanda kwa mahojiano aaaaah!!! masikiiini rafiki angu Kimarooo..."

    aliongea Shebby lakini mwishoe alijikuta anaanza kulia mara baada ya kumbukumbu zake kumrudisha Mkuyuni na kuliona tukio zima lililojili miezi kadhaa nyuma na zaidi alimkumbuka rafiki ake kipenzi Kimaro na kuanza kulia kwa uchungu sana.

    "pole babaa polee ndio uanaume na misukosuko ya kazi zetu hizo pole baba"



    alimfariji mwanae mzee Mwinchande huku akimkumbatia wakati huo mamaake alibaki anawatazama huku machozi nae yakimtoka

    "Babaa!! inatisha sanaaa, babaaa inaniumaa sanaa lazima nilipe KISASI"

    aliongea kwa hisia zenye uchungu sana Shebby lakini babaake alimtuliza na kumsihi asije kuthubutu kufanya hivyo

    "chonde chonde mwanangu mi mwenyewe ni askali mzoefu sana nakusihi na kukuomba sana kwa usalama wako futa kabisa hayo mawazo"

    "kivipi baba?"

    "Kwa sababu ni hatari ya maisha yako hebu fikiria unataka kulipa kisasi je unamjua huyo unaetaka kumlipizia?"

    "Nitamtafuta mpaka nimjue sitokubali ni heri nife nikiwa namtafuta hata nitapokutana na wenzangu huko mbinguni watanipokea vizuri kuliko kukaa kimya na kufa bila kufanya kitu wakati mimi ndie niliyewaponza wengine"



    alisisitiza Shebby huku akiwa amekasirika mno baada ya kumbukumbu zake kuendelea kumiminika kichwani mwake mithili ya bomba la maji lililokuwa limefungwa muda mrefu na sasa limefunguliwa koki.

    "Hee! Shebby mwanangu kumbuka hata ufanyeje huwezi badilisha ukweli kuwa rafiki zako wamekufa na mtu uliyekuwa unamtetea kaachiwa huru sasa iweje bado unang'ang'ania kumtafuta mtu usiyemjua hata jina?"

    "Namjua babaa.."





    "Unamjua!!!"

    "Hee, Nitatumia jina hilohilo analolitangaza mwenyewe na Kifo chake lazima nikishuhudie mbele ya macho yangu."

    "Hee basi tulia baba unasema unamjua jina? ndio nani sasa?"

    aliuliza mamaake wakati huo babaake alikuwa kataharuki na haamini jinsi mwanae alivyobadilika ghafra namna ile.

    "Mama, Baba nawapenda na nawaheshimu sana naomba mnisamehe kwa kubishana nanyi ila niacheni nipambane na huyu mtu anayejiita Mr x."

    "MR X!!!?"

    "Ehh! Mshenzi mwenyewe anaitwa Mr X"

    aliongea Shebby kwa hasira na kuelekea chumbani kwake moja kwa moja huku akijiapiza kulipa kisasi na kumlaani mr X akiwaacha wazazi wake wakiwa wanatazamana wasijue la kufanya au la kumwambia kijana wao.



    * * * * * *



    "Pole sana mzee wangu kwa kumpoteza shujaa akiwa bado na umli mdogo vile"

    alivunja ukimya Cj4 mara tu walipoanza kukaribia mkoa wa Pwani na kuzifufua hasira za maumivu zilizokuwa kifuani mwa Kamanda mkuu wa Jeshi la polisi mstaafu mzee Cyplia.

    "Aaagh! yaani mwanangu unavyosema hivyo unazidi kunitonesha kidonda cha mwanangu John! aaagh! mungu ampumzishe kwa amani."

    "Daah! binafsi mzee wangu nimeamua kujikita katika upelelezi wa kujua kilichotokea kwani inasemekana chanzo kabisa ni mfungwa aliyekuwa gereza alilosimamia Kamishna wetu yule mtoto wa kamanda wako msaidizi enzi zenu "

    "Aaagh! ndio mtoto wa Mwinchande!"

    "eeh, sasa kumbe alikuwa katika mpango wa kumsaidia yule mfungwa baada ya kujua story yake na ukweli halisi wa kesi ulikuwa kule morogoro lakini alipoenda kufanya tafiti na kusaidiana na askali wa kule ndo yakatokea ya kutokea"

    "Mh! sasaa kidooogo naanza kupata mwangaza"

    aliongea mzee Cyplian na kumfanya Cj4 azidi kutuliza umakini kwani tayari moyoni mwake alishaanza kumuhisi huenda yule mzee akawa ndie Mr X lakini aliamua kuongea vile ili kumpoteza na kujifanya hajamstukia kitu ili iwe rahisi kumteka kimazungumzo

    "Mwangaza gani tena mzee wangu"



    "Kwa yaliyotokea ila naamini hadithi ya huyo mfungwa ndio funguo ya kumjua muhusika aliyewafanyia unyama wanangu.,,,,"

    kauli ya mzee Cyplian ilibeep ubongo wa Cj4 wakati huo tayari walikuwa wanaingia Chalinze lakini mara ghafra kabla mzee Cyplian hajaendelea wala Cj4 hajauliza chochote ghafra walishangaa kuona basi lililokuwa linatokea njia ya Tanga likipitiliza na kuingia mkuku mkuku barabara kuu huku likiwa limewasha taa na kupiga honi mfurulizo kuashilia kuwa aidha dereva limemshinda au limekata breki na kutokana na speed aliyokuwa anakuja nayo Cj4 alijikuta anashindwa kusimama na kuhamia barabara ya pili ili apate kulikwepa lakini bahati haikuwa yake baada ya kukutana na kiuno cha tela la roli lililofunga breki za ghafra kwa kuogopa kulivaa basi lililokosa muelekeo na kusababisha tela kugeuka kuelekea usawa wa gari la kina Cj4 huku kikisikika kishindo kikubwa sambamba na milio ya breki iliyosababisha cheche kuwaka barabarani na kelele za hofu toka kwa wafanya biashara na watu mbalimbali zilizosikika Chalinze nzima.



    Hakuna aliyeelewa jinsi gani ile gari ndogo Landcruiser nyeupe iliyokuwa inaendeeshwa na Cj4 ilivyofika fika kule kwenye tawa za umeme tena ikiwa imechakazwa mno sehemu za mbele, na baada ya watu kukimbilia hususani wale wahuni na vibaka mpaka pale ilipokwamia ile gari walimshuhudia mzee mmoja kwa ndani akiwa kabanwa ipasavyo kwenye kiti na bashboard huku ule upande wa dereva kukiwa patupu na ndipo vijana wale wa kihuni walipong'ang'a kuuchomoa mlango mmoja uliojikunja ili wapate kuingia na kuitoa blufkes waliyoiona kwa ndani wakiamini lazima kutakuwa na hela tu.



    Lakini kabla hawajafanya hivyo walistushwa na sauti ya mtu akiwaamuru waondoke haraka ikitokea nyuma yao na walipogeuka kutazama walimshuhudia askali mmoja ambae mavazi yake ya juu yalichafuka kwa damu iliyokuwa inaendelea kuvuja kutokea kichwani na ndipo wale wahuni wote walipotimua mbio.

    Hakuwa mwengine bali ni Cj4 dereva wa ile gari nyeupe iliyokwamia pale kwenye matawa ya umeme akiwa na jeraha lililokuwa linavujisha damu nyingi huku ikiwa haieleweki alitokajetokaje kutokana na kubondeka vibaya hasa ule upande aliokaa yeye.

    Alimuangalia mzee Cyplian na moyo kumuuma zaidi mara baada ya kugundua kuwa alishafariki pale eneo la tukio na hapo hapo kwa speed bila kujali damu zilizokuwa zinamvuja Cj4 alianza kukimbia kuelekea barabara kuu ambapo jumla ya magari sita yalipata ajali iliyosababishwa na lile basi lililopoteza muelekeo ambalo lilianguka na kuseleleka upande wa pili hadi kwenye vibanda vya mama lishe na kusababisha maafa makubwa mara baada ya derva kulazimisha kukata kona licha ya mwendo kasi lililokuwa nao.

    Kitu cha kwanza kufanya Cj4 akiwa kama mtu aliyechanganyikiwa alisimama na kulitazama eneo lile la ajali na kuanza kupiga hesabu alizozijua yeye wakati huo maaskali ndio walikuwa wanawasili eneo lile licha ya kwamba kituo hakikuwa mbali na mahala palipotokea ajali.

    (''Hii ni ajali ya Kutengeneza kabisaaa,'')



    aliwaza Cj4 na kukimbilia kwenye ile basi na kuvunja kioo cha mbele kwa kupiga teke kali na alibahatika kumchomoa dereva ambae licha ya kwamba hali yake ilikuwa sio nzuri lakini alijitahidi kuzungumza

    "Jitahidi kuongea mimi ni askali nimekushika, nambie mara ya mwisho mlisimama wapi kwa ufasaha kabisa"

    alionga Cj4 kumuuliza yule dereva ambae alitoa maelekezo kwa shida huku akimwambia kuwa gari iliferi breki baada ya kuhisi waya maalum uliopita kwenye propela ulioshikilia vipira vilivoenda kukamata ringi za taili za mbele kuwa ulikatika ghafra na hakujua chanzo.

    maneno yale ya yule dereva yalizidi kumuaminisha Cj4 kuwa ile ajali ilitengenezwa tu sio bure lakini kama imetengenezwa wamefanyafanya vipi hao watu? hapo akakosa jibu ndipo alipotaka kumuuliza tena yule dereva mara askali wengine walifika eneo lile na kuanza kuwatoa majeruhi wa kwenye basi wakishilikiana na wananchi huku naye Cj4 akipigiwa saloot na askali aliowapita cheo na wakimsihi wampeleke nae akatibiwe kwani alikuwa kaumia sana kichwani licha ya kuwa yeye mwenye alijiona yuko sawa.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Na wakati akiwa kasimama akiangalia pilika pilika zilizokuwa zinaendelea za uokozi na wapiga picha eneo lile mara macho yake yaligongana mara mbili na macho ya binti mmoja aliyevalia kiislamu usoni mwake akifichwa na nikabu nyeusi akiyaacha macho tu huku akitembea kwa madaha bila wasi kuelekea sehemu aliyopaki gari yake ndogo lakini kila alivyokuwa anapita alipogeuka macho aliyaelekezea kule kwa Cj4 na kwa ile Landcruide iliyobondeka kwenye Tawa za umeme na hapo hapo aret ya hatari iligonga kichwani na Cj4 na kuhisi yule mwanamke ndie aliyesababisha ile ajali na kuanza kupata ufumbuzi basi huenda mzee Cyplian hakuwa mr.X kama alivyomuhisi awali ila alitia shaka kuwa huenda mzee Cyplian kuna vitu alivijua kuhusu mr X na ndio maana mr X amewatuma vijana wake kufanya ujanja wowote ili mradi wahakikishe mzee Cyplian hatoboi ukweli wala siri yoyote kuhusu mrX.

    Lakini akiwa na maswali lukuki Cj4 kila alipomtazama yule bint moyo ulimtuma amzuie tu kwani macho ya yule binti yalionesha wazi kuna kitu anataka ahakikishe kule ilipodondokea ile gari na ndipo alipowaponyoka polisi wenzake na kukimbilia upande wa pili ilipokuwa ile gari ya yule bint ambayo ndio ilikuwa inaondoka taratibu eneo lile lakini kwa bahati mbaya zaidi Cj4 alianza kujisikia kizunguzungu kabla hajafika na kujikuta anadondoka katikati ya barabara ambayo ilikuwa inazungushiwa utepe wa kuzuia magari yasipite upande ule na macho yake yaliishia kuitazama kwa mbali ile gari pindi alipokuwa anadondoka na kupoteza fahamu.



    * * * * * *



    Akiwa amekaa huku mawazo na hasira juu ya yaliyopita hususani mr X na vifo vya rafiki zake huku akiwazia kukutana na Hussein bubu, ndipo Shebby alistushwa na sauti ya babaake pindi alipokuwa anaongea kwa njia ya simu kwa mshtuko mkubwa na kumfanya atoke na kukimbilia sebuleni aliposimama mzee Mwinchande akiendelea kuongea na simu.

    "Vipi baba nini kimetokea?"

    aliuliza kwa taharuki Shebby baada ya kuuona uso wa babaake ukionesha kushangazwa na kustushwa na alichokuwa anakisikia

    "ajali mwanangu"

    "Ajali? nani tena!"

    "Mkuu mstaafu wa jeshi la polisi Kamanda Cyplian anasadikika amepata ajali mbaya wakati akiwa njiani kuja Dar"

    "Kha!! ilikuwaje sasa, si yule babaake marehemu ocs wa Mkuyuni?"



    "haswaaa, yaani aaagh! namkumbuka vizuri alikuwa mkubwa wangu na mtu wa karibu kipindi hiko daah!"

    "Daah! shit, amepona?"

    "Bado hatujapata hakika"

    Baada ya Shebby kuzipata habari zile muda ule ule alichukua simu yake na kumpigia kamanda wa mawasiliano ya idala ya dharula na alipouliza walithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na tayari kuna timu ya vijana ilikuwa njiani kuelekea huko.



    Aliingia ndani Shebby na kujiandaa kwa kuvaa gwanda zake hali iliyowashangaza wazazi wake na kumuuliza kulikoni lakini alichojibu kiliwashangaza wote.

    "Baba najua ni ajali tu imetokea lakini kuonana na mzee Cyplian ni jambo la muhimu sana kwangu ktk njia za kumjua mr X"

    alijibu Shebby na kutoka mkuku na kuchukua gari aina ya Jeep na moja kwa moja aliondoka kwa speed maeneo ya kwao mara baada ya mlinzi kufungua geti huku akiwa hataki kusikia chochote toka kwa babaake ala mamaake.



    Mwendo aliokuwa anatembea Shebby nimeshindwa hata kuuelezea mara baada ya kupita maeneo ya Kibaha na kutembea upande ambao ulikuwa haumruhusu lakini alifosi hivyohivyo huku akipiga honi mfurulizo lakini ghfra alipokuwa anapandisha kilima cha kuingia Mlandizi almanusura nae apate ajali baada ya kukosana na gari ndogo aina ya toyota creaster uso kwa uso na kusababisha wote wayumbe na yule dereva mweney wa toyota bado kidogo atumbukie mtaroni lakini nae alikuwa mtaalam sana na alifanikiwa kuidhibiti gari na kutulia tena barabarani na kuangalia nyuma kwa kutumia site mirror ambapo aliishuhudia ile Jeep nayo ikiendelea kuambaambaa pembeni ya barabara na kukaa sawa huku speed ikiwa pale pale.

    Chaajabu alitabasamu yule dereva badala ya kuchukia na kuendelea kupiga gea na hakuwa mwengine bali ni yule yule binti aliyejiziba uso kwa nikabu ambae Cj4 alimtilia shaka kule Chalinze.



    Upande wa Shebby alikuwa nusu mzima nusu kichaa kwani alipoituliza tu gari mwendo ukawa uleule tena utadhani ndio kaambiwa aongeze vile huku akizipita gari kibao zilizokuwa zinaenda polepole kutokana na foreni nae kuweza kupita barabara ya pili akisaidiwa na sare alizovaa hakuweza kusimamishwa na askali yeyote mpaka alipoukaribia msafara uliokuwa unaelekea eneo lilelile la ajali na kufika nao pamoja.



    "Wapi mzee Cyplian? wapi mzee Cyplian?!"

    aliuliza Shebby mara tu ya kusimamisha gari ambalo wengi walilikwepa kwa jinsi lilivyokuwa linakuja kasi na polisi wa pale wote walishindwa cha kufanya mara baada ya kumuona dereva wake akiwa kawazidi cheo wote waliokuwapo pale.

    "Wapi mzee Cyplian"

    aliuliza tena Kamishna Shebby safari hii akimfata Seneor Inspector ambae ndie alikuwa mkubwa wa pale kipindi shughuli za uokoaji zikiendelea.



    "mkuu ndio sasa ivi ambulance iliyobeba mwili wake imetoka."

    "Whaat! ina maana amefariki?"

    "Ndio mkuu ila ambulance ile ndio yupo inspector aliyekuwa anamuendeesha nae hali yake si mbaya sana ila amepoteza fahamu"

    aliongezea yule s.inspector huku akiionesha kwa kidole ambulance iliyokuwa inatoka na palepale Kamishna Shebby aliingia kwenye gari na kuifatilia ile ambulance mpaka hospital ya Tumbi na pindi ilipopaki alishangaa kuona yule mgonjwa ambae ndie Inspector aliyekuwa anamuendeesha mzee Cyplian akishuka mwenyewe huku akiwa na bandeji kubwa kichwani akiwakataa polisi na madaktari waliomleta pale kuingia hospitali na kuichomoa ile sindano ya dripu aliyowekewa kwenye gari na kuanza kuondoka huku akiwa kama mtu aliyechanganyikiwa lakini anajiamini mno.

    Hapo ndipo Shebby aliposhuka na kumfata yule inspector ambae ndie Cj4 huku akiwazuia askali wote waliokuwa wanajaribu kumzuia na kumuingiza hospital na kutokana na ukubwa wa Shebby wote walitii na hapo kwa mara ya kwanza Shebby alionana uso kwa uso na Cj4 huku akiwa hamjui ni nani hasa nae Cj4 alitabasam kuonana na Shebby huku akiwa anajua kila kitu ni nani hasa nyuma ya pazia.



    "Nakufahamu wewe ni Kamishna Shebby nilisimama kwenye nafasi yako kuendeleza ulichokiacha, tuwahi haraka Dar kabla hajatoweka."

    aliongea Cj4 na kuingia kwenye Jeep huku Shebby akiwa ametumbua macho akiwa haelewi nini anamaanisha yule inspector na imekuaje aongee kwa kujiamini vile ilihali yeye ni mkubwa kuliko yule inspector.

    "Twende Kamishna tuiwahi crester iliyombeba muuaji."

    Alipoongea maneno haya sasa Shebby alielewa kitu haraka na kuwahi kwenye gari na kuigeuza kwa fujo huku askali na madaktari wote wakishangaa kile kilichokuwa kinaendelea.



    Ilikuwa ni ajabu na kweli ndani ya vichwa vya watu kwa kila aliyeiona ile gari jinsi ilivyogeuzwa na kuondoka eneo lile kwa speed ya hatari mithili ya gari ya mashindano huku Cj4 akiufurahia ule mwendo ambao kwake yeye Kamishna Shebby aliona kama vile gari ilikuwa haitembei kabisa.

    "Inspector! Umesema ni Creaster nyeupe?"

    aliuliza Shebby huku akiwa makini na barabara ambapo aliwasha taa zote full mbali na kuwa haukuwa usiku.

    "Yap yap nyoosha mguu nyooshaa"

    alijibu Cj4 kwa msititizo na kikatawala kimya baina yao zilibaki kusikika tairi za gari zikilalamika honi mfurulizo na muhemo wa injini tu.



    Lakini walipofika maeneo ya Kibamba pale njia panda ya kijiji cha Hakipo walishangaa kuuona moshi mzito umetanda pia waliuona umati wa watu kwa mbali na askali wa usalama barabarani sambamba na gari ya zima moto huku askali moto wakiwa bussy kuzima moto uliokuwa unawaka na kusababisha hali ya hewa pale kuwa na ukungu uliosababishwa na Moshi.

    Walisimama na kushuka mkuku mkuku eneo lile na kuwahi kushuhudia kilichotokea wakiwa na wasiwasi isije kuwa ni yuleyule mtu aliyekisiwa na Cj4, na kweli baada ya kushuka na kusogea kuangalia kilichokuwa kinawaka walishangaa kukuta ni gari ndogo na walipoichunguza vizuri ilikuwa ni ileile Toyota Creaster aliyokosa kosa kugongana nayo Shebby na ndio ile aliyopanda yule mwanamke aliyemtilia mashaka Cj4

    "Vipi afande ilikuwaje?"

    aliuliza Kamishna Shebby kwa mmoja wa askali barabarani (trafic)aliyekuwapo maeneo yale baada ya kupokea heshima yake

    "Ni ajabu kidogo mkuu, tulipigiwa simu na raia wema kwamba kuna moto umezuka kutoka kwenye hiyo gari na umekutwa mwili wa mwanamke mmoja ambae inasadikika alikuwa dereva wa hiyo gari akiwa kaungua vibaya mno."

    alijibu yule afande na kumfanya Shebby akune kichwa na kushusha pumzi lakini Cj4 alicheka na kumvutia pembeni Kamishna Shebby.



    Vitendo vya Cj4 kutomtetemekea wala kueka nidhamu ya uoga kwa Shebby ilizidi kumshangaza Shebby na kujiuliza huyu ni askali gani mwenye cheo kidogo kuliko yeye lakini haoneshi kuogopa wala kumnyenyekea mkubwa wake na kufikia hadi hatua ya kumshika mkono na kumvutia pembeni? lakini alijikuta anashindwa kumkatalia wala kumuuliza na kukubali kusogea nae pembeni.

    "Vipi inspector?"

    aliuliza Shebby kwa taharuki mara baada ya kuvutiwa pembeni na Cj4 wakati yeye alikuwa bado anahoji kilichotokea.

    "Tushamkosa, kashatuzidi akili"

    "Kivipi?"

    "Huyu mwanamke muuaji"

    "Muuaji, lakini mbona na yeye amekufa! hapa lazima kutakuwa na mtu aliyemuua"

    aliongea Shebby kauli iliyopingwa na Cj4

    "Hapana Kamishna, huyu mwanamke ni special Killer na anajua kupoteza ushahidi. nina imani yule aliyeungua si yeye"

    aliongea Cj4 na kumfanya Shebby abaki na taharuki akishangaa maneno ya Cj4, na kuanza kuhisi huenda huyu si askali wa kawaida



    "Sikia Shebby, washa chombo twenzetu turudi taratibu eneo la tukio ukaniache hapa hakuna kitachoweza kutusaidia ila maswali yote unayojiuliza nitakujibu tukiwa njiani"

    aliongea Cj4 na kumfanya Sheby awe mpole na kuingia kwenye Jeep na kuanza kuendeesha kuelekea walipotoka huku akiwa anajiuliza mara mbili mbili kuhusu inspector wake ambae licha ya kuwa ameumia sehemu za kichwa na hata ile bandage aliyofungwa kwenye ambulance ilianza tena kuvujisha damu lakini hakuonekana kujali.

    "Enhee, kwanini Inspector unalazimisha turudi tena eneo la tukio?"

    "Kule ndipo tutapata uelekeo wa sababu za ajali na alipotokea muuaji aliyetuzidi akili."

    "Kivipi sasa katuzidi akili?"

    "Si umeona katengeneza kifo fake!!"

    "Kifo fake? kwa hiyo unataka kusema yule aliyeungua si muhusika?"





    "Ndio maana yake ni kamchezo kadogo sana, nahisi kumbukumbu zako zimerudi unakumbuka nini kuhusu Mkuyuni?"

    alijibu Cj4 na kumuunganishia swali Kamishna Shebby lililofanya amtazame na kuamua kumjibu kiunagaubaga

    "Mkuyuni nakumbuka vifo tu"

    "Nina mashaka na muuaji wa Mkuyuni anaweza kuwa yuleyule mwanamke aliyesababisha ajali"

    aliongea Cj4 maneno yaliyomfanya Kamishna Shebby kufunga breki za ghafra za gari na kupaki pembeni huku akimuangalia kwa mshangao Inspector wake.

    "Unasema??"

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    aliuliza Shebby mithili ya mtu aliekuwa na matatizo ya masikio mara baada ya kusimamisha gari.

    "Nina wasiwasi na yule mwanamke aliyesababisha ajali ndie aliyewashambulia Mkuyuni."

    "Khaaa! wewe ni Inspector kweliiiii ama umevaa sare tu?"

    aliuliza Shebby akionesha kuanza kuwa na wasiwasi na Cj4 kutokana na maneno yake kugusa mulemule

    "Hapana mimi ni Inspector kwa sasa... Naitwa Inspector Sudy kama ilivyoandikwa"

    alijibu Cj4 na kumshangaza sana Shebby

    "Sawa Inspetor hata mimi naanza kukubaliana na wewe kuwa ule mwanamke ndie aliyetushambulia Mkuyuni"

    aliongea Shebby na kumfanya Cj4 amuangalie kwa umakini na ndipo Shebby alipozidi kufunguka

    "Nilimshuhudia muuaji wa Mkuyuni kabla hajanipiga risasi ya mguu, alikuwa ni Ninja wa kike ila kwa bahati mbaya nilimjua kwa sauti tu na muonekano lakini sikubahatika kuona walau macho yake yalivyo kutokana na miwani aliyovaa"

    "So, unadhani kwanini alikuacha? wakati wenzako wote aliwaua?"

    aliuliza Cj4

    "Mh! kwakweli hata mimi sikudhani kama angeniacha ila nakumbuka alichosema kuwa eti nina bahati na kunipa agizo toka kwa mr X kwamba nisije kuthubutu kumtafuta tena mr X kwa usalama wangu. Lakini pia kuna kauli alinambia ambayo ilinichanganya sana hadi sasa"



    "Ipi hiyo?"

    "Alinambia iwapo nataka kupambana na Mr X basi inatakiwa nianze kufanya mazoezi ya kusimama juani na kupambana na kivuli changu mpaka nikikamate"

    "Aaaahaa sasa naanza kupata taswira"

    aliongea Cj4 huku akifikiria kitu na kumshangaza zaidi Kamishna Shebby.

    "Taswira gani tena Inspector!"

    "Juu ya mr X"

    "kivipi?"

    "Nina wasiwasi mr X ni mtu aliye katika mzunguko wa maisha yako ya kila siku."

    "Mhh! mbona sikuelewi unamaanisha nini?"

    "Namaanisha mr X ni mtu anayekujua vizuri na inawezekana nawe ukawa unamjua pia, na anapatikana katika sehemu kuu tatu"

    "Mbona sikuelewi wee Inspector? ni sehemu gani hizo?!"

    "Usipanic Shebby, nina wasiwasi mkubwa kuwa mr X ni mtu anayepatikana katika mzunguko wa maisha yako ya kila siku yaani kazini, serikalini ama nyumbani."

    "Nyumbani?"

    "Yap, huenda akawa na ukaribu hata na babaako mzazi, au huenda akawa moja ya wakuu wako wa kazi ama kiongozi mkubwa serikalini aidha mstaafu ama bado yupo madarakani"

    maneno ya Cj4 yalizidi kumchanganya kabisa Shebby na kabla hajauliza tena lolote ndipo Cj4 alianza kufungua vifungo vya shati ya sare ya kipolisi aliyovaa na kuisogeza pembeni vest yake na kumuonesha eneo la kifua Shebby ambae macho yalimtoka baada ya kuona mchoro wa bawa na alama za Komandoo wa Jeshi.



    "Usistuke nimeingia kwenye hii kazi kwa msaada wa kupoteza kwako fahamu, mimi si polisi ila kama unataka kazi hii ifanikiwe na tumgundue huyu mshenzi mdogo inatakiwa asijue mtu yeyote kama kumbukumbu zako zimerudi"

    aliongea tena Cj4 huku akifunga vifungo vya shati yake na wakati huo wote Shebby bado alikuwa katumbua macho akiwa haamini kuwa kumbe yule aliyekuwa anazunguka na kuzungumza nae muda wote ni Komandoo wa heshi!!

    "Zingatia Kamishna kwa usalama wako na urahisi wa kazi hii. take care twenzetu tukapate mchoro eneo la tukio lakini kumbuka hii tunajua mimi na wewe"

    aliongea tena Cj4 na ndipo Kamishna Shebby alipoanza kuondoa gari huku akiitika kwa kichwa akiwa bado haamini kilichokuwa kinaendelea hadi serekali wampandikize Komandoo katika kazi ile.



    * * *



    Baada ya Kamishna Shebby na Cj4 kufika tena Chalinze eneo la tukio na kufanya utafiti wa siri walioujua wao kabla ya Cj4 kukubali kujishusha na kuingizwa tena kwenye ambulance ambayo ilitokea ikulu pasi na mtu yeyote kujua na madaktari waliokuwa mule karibu wote walikuwa ni wanajeshi lakini walifanya hayo kwa agizo la mkuu wa majeshi kuwa wao ndio waondoke na yule dereva wa marehemu mzee Cyplian kwa lengo la kuwazubaisha hadi polisi wengine wasijue nini kinaendelea kwani isingekuwa vyema Cj4 kutibiwa na raia ama polisi wa kawaida.



    Baada ya Kamishna Shebby kuondoka eneo la tukio huku akiwasiliana na baadhi ya wakubwa zake akijifanya bado kumbukumbu zake hazijarudi kama alivyoagizwa na Cj4 alifika nyumbani huku kichwa kikiwa kinamuwaka moto akiyakumbuka maneno ya Cj4 na kuona kweli mr X anatumia akili nyingi sana na inawezekana kabisa yupo katika mzunguko wa maisha yake ya kila siku.

    ('Mh! sasa itakuwa nani? au mh Wazili? mhh sidhani.. au Kamanda mkuu anatuzunguka? Mh! !!')

    aliwaza Shebby usiku pindi alipokuwa ndani lakini mara akiwa katika mawazo mazito alipokea ujumbe wa sms kutoka kwa Dk Asha ambae alikuwa mchumbaake akimlaumu kwa kupata riport kuwa alielekea eneo la ajali iliyotokea mchana huo mbali ya kuwa bado likizo yake ilikuwa haijaisha.

    Alitabasamu na kuendelea kuchart na baby wake Asha japo ukweli moyoni alikuwa na mawazo mengine kabisa.



    * * * * *



    Siku kadhaa zilisonga huku ukweli wa chanzo cha ajali ya Chalinze ukibaki kuwa wa kubahatisha na hata kile kikao cha siri alichopanga mh Rais kifanyike kiliahilishwa kwanza na kuupisha msiba uliozuka ghafra wa Kamanda mkuu mstaafu wa jeshi la polisi mzee Cyplian na kuzidi kuwachanganya wakubwa wa serikali washindwe kuthibitisha moja kwa moja juu ya ajali ile ilikuwa imetengenezwa ama laah.

    Hii hata mkuu wa Majeshi ilianza kumpa wasiwasi mara baada ya kupokea ripoti toka kwa Komandoo waliyemchomeka na kumwambia kuwa ajali ile ilisababishwa na watu wa mr X so, ni lazima kwenye kikao cha siri walichofanya kutakuwa na spy anayevujisha siri kwa mr X ama mr X mwenyewe anaweza kuwamo kwenye vikao vyao.

    Na ripoti hii ilifikishwa kwa mh Rais tu na kukubaliana na ushauli wa mkuu wa majeshi kuwa haina haja ya kutangaza tena ile ripoti wala kueka tena kikao huku akimuahidi kuwa kijana wake shupavu ataifanya hiyo kazi na mr X atakuja kuletwa mbele ya macho yake siku moja.



    Kamishna Shebby alirudi rasmi kazini huku akiigiza bado kumbukumbu zake hazijarudi na kuwashangaza tena wazazi wake ambao awali walikuwa na uhakika kuwa mtoto wao kumbukumbu zimerudi.

    Hali hii ilimliza sana mamaake Shebby na kumuombea kila siku alipokuwa anasali akiwa haelewi inakuaje mtoto wao mara kumbukumbu zirudi mara zipotee tena?

    Hata mzee Mwinchande hii ilimshangaza sana lakini ukweli ulibaki katika moyo wa Shebby na Cj4 huku wakiendeleza mission yao ya siri ya kumnasa mr.X pasi na mtu yeyote kujua.



    * * * *



    Ilikuwa ndio siku rasmi ya kutoka kwenye makazi ambayo hakutegemea kama angetoka tena mara baada ya msamaha wake kutangazwa na kupitishwa wiki chache zilizopita na Mh Rais wa Tanzania.

    Geti kubwa lile la mwisho lilifunguliwa kwa mitambo ya umeme na oparator aliyekuwa kwenye moja ya jengo la usalama wa gereza lile na mwanga wa nje ukaanza kummulika Hussein babu bubu huku akiwa haamini kama kweli leo hii anakuwa huru kwa mara nyengine japo alikuwa hajui wapi aelekee kwani wenzake wote waliotangazwa kuachiwa walipokelewa na ndugu jamaa na marafiki kadha wa kadha waliokusanyana nje ya geti la gereza kuwasubiri isipokuwa yeye tu.

    Akiwa kava nguo mpya alizonunuliwa na serikali huku mkononi kabeba kijibegi kidogo chenye nguo za kubadilisha na shuka ikiwa ndio vitu pekee alivyoambulia kama msaada kutoka serikalini juu ya maisha yake mapya anayoenda kuyaanza huko uraiani.



    Alimshukuru mungu na kuanza kupiga hatua mdogo mdogo akiifata barabara ndogo ya lami iliyoenda kukutana na barabara kubwa katika njia panda ambapo kulikuwa na stendi ya daladala japo hakujua hata akifika hapo stendi atapanda gari ya wapi ama atafikia wapi na mfukoni alikuwa na kiasi cha shilingi elfu tano aliyorudishiwa ikiwa ni pesa aliyokutwa nayo kipindi anakamatwa miaka iliyopita ambayo kwa kipindi hiko ilikuwa haina thamani kabisa ya kumsaidia mtu walau siku tatu.

    Lakini akiwa anaendelea kupiga hatua huku kichwa akiwa kakiinamisha chini akienda huku anatafakari mara alisikia muungurumo wa gari ikitokea nyuma yake upande ule wa gereza na kuchapukia pembeni kwa kuipisha lakini alishangaa ile gari ikisimama karibu yake na kushushwa kioo na mara sauti ya mtu ambae alikuwa dereva wa ile gari ilisikika akimwita na aliposogea kuchungulia hakuamini kuona ni Kamishna Shaaban na ndipo alipoingia garini akiwa haamini kama amekutana tena na kijana aliyetokea kumuhusudu kupita binaadam yeyote tangia aanze maisha ya jera.

    "Kamishna baba!! aah, siamini mwanangu kumbe umerudi"

    aliongea huku chozi la furaha likimdondoka Hussein babu kwa kutoamini kabisa hasa mara baada ya Shebby kuvua miwani meusi aliyovaa na kofia.



    "Nimerudi baba nakaribia wiki sasa, hongera sana kwa kupata uhuru hatimae unarejea uraiani"

    alijibu Shebby kwa furaha ya kukutana tena na Hussein

    "Ahsante mwanangu leo hii nimekumbuka sana maneno yako pindi nilipokuwa natoka rasmi pale getini daah! mwanangu pole sana kwa matatizo.. Naomba unisamehe sana"

    aliongea Hussein huku akiendelea kufuta machozi yaliyokuwa yanatililika mashavuni mwake ghafa kila alivyokuwa anamuangalia Kamishna Shebby

    "Hapana baba, hupaswi kuniomba msamaha kwani ile ilikuwa ni moja ya kazi. Usijali babaangu kwakuwa leo hii upo huru hata moyo wangu umefurahi sana najua kazi niliyobakiza ni moja tu"

    "Kazi gani tena baba"

    "Nataka kumjua huyo mr X nilipe kisasi"

    "Haa! sasa kisasi cha nini tena mwanangu wakati mi nishakuwa huru! isitoshe naomba swala hilo niachie kwani mi mwenyewe nataka nilipe kisasi kwa mr.X nishasali sana miaka yote nikiwa jera kumuomba Mungu anitendee muujiza siku moja nitoke jera na nikamuue mr X kwa mikono yangu na mpaka sasa naona Mungu kashaanza kunijibu dua zangu. Futa mawazo ya mr X mwanangu sitaki nikuponze tena hii ni kazi yangu sasa ni zamu yangu"

    aliongea Hussein babu kwa hisia kali na safari hii machozi yaliacha kumtoka huku akimuangalia kwa umakini Shebby ambae sasa alianza kuiondoa gari taratibu na kuelekea kule alipokuwa anaelekea Hussein na alipoifikia ile barabara kuu alikunja upande unaoenda kutokea Kongowe.

    "hahaha, hapana baba si rahisi kama unavyofikiria lakini pia sifanyi kwa sababu ya wewe tu bali nafanya kwa sababu ya rafiki zangu wote waliokufa"



    alijibu Shebby huku akizidi kuongeza mwendo wa gari

    "Mwanangu nakuomba chondechonde mi sina ubora wowote niliobakisha wala thamani hapa duniani hivyo hata kama kumuua kwa kumpiga nisipoweza, niko tayari hata nijilipue tufe wote lakini si wewe kurudi tena kwenye matatizo baba nakuomba"

    alisisitiza Hussein lakini Shebby hakuonesha kujali sana zaidi ya kuongeza mwendo mpaka walipoipita Kongowe na kuanza kuufata muelekeo wa mbagara na walipofika Mbagala Zakiem aliingiza gari kwenye parking ya hoteli moja mpya ya kisasa iliyokuwa pale Zakiem na kumuomba Hussein waongozane kuingia kwenye ile hoteli na kumshangaza sana Hussein mara baada ya kushuhudia Kamishna Shebby akimlipia chumba na bili ya chakula cha wiki nzima pale hotelini.

    "Usijali baba utakaa hapa kwa wiki moja kipindi nikikutafutia makazi rasmi ya kuishi usiwe na wasiwasi simu hii utatumia kwa mawasiliano endapo kutatokea tatizo, line yake imeunganishwa na kifurushi cha wiki na ina namba mbili tu zilizoseviwa na zote ni za kwangu.. Kuwa na amani baba"



    Ni maneno ya Shebby pindi walipoingia kwenye chumba cha hoteli kilichokuwa ghorofa ya pili ambapo Hussein alibaki kataharuki tu akiwa haamini moyo wa yule kamishna na vile anavyojitolea kiasi kile kumsaidia ilihali hawana undugu wowote.

    "Mi nahitajika kuwahi tena gerezani baba, ila hii Elfu hamsini itakusaidia kwa matumizi madogo madogo na ya dharula"

    "Asante babaaa.. aaaah Asante sana mwanangu Mungu akuzidishieeee eeeh!! Akulinde na kila shari jamaniiii Asante babaaa"

    alishukuru hadi akapiga magoti Hussein lakini Shebby alimuinua na kumsihi asijali kabisa kisha aliagana nae na kutoka hadi ilipopaki gari yake.

    ["Hallow, yah Cj4 kazi kwako sasa tayari nishafanikisha yupo chumba namba 90 ghorofa ya pili"]

    yalikuwa ni maneno ya Shebby kwa njia ya simu akiongea na Cj4 mara baada ya kuingia ndani ya gari yake na kuanza kugeuza kuondoka maeneo yale.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ulikuwa ni mchezo wa akili nyingi waliokuwa wanaufanya Kamishna Shebby na Cj4 na muungano wao hakukuwa na mtu mwengine yeyote aliyekuwa anaujua, na kumbe Cj4 alikuwa na jukumu la kuchunga usalama wa Hussein babu na kumfatilia pale kwenye ile hoteli ama ikitokea ametoka ama kama kuna mtu yeyote atayekuja kuufatilia uwepo wake pale basi atashughulika nae.

    Naam na huo ulikuwa ni ulinzi na usalama mkubwa uliomzunguka Hussein pasi na yeye mwenyewe kujua hadi atapojulikana mr X ni nani.



    * * * * * *





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog