Search This Blog

Sunday 19 June 2022

SIONDOKI MPAKA NIFE - 1

 





    IMEANDIKWA NA : STALLONE JOYFULLY





    *********************************************************************************



    Simulizi : Siondoki Mpaka Nife

    Sehemu Ya Kwanza (1)





    CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ Mlio wa sauti kama bomu, ulileta taharuki kubwa katika hifadhi ya barabara ya Kilwa. Hakuna ambaye alitembea kwa madaha tena kama mwanzo. Hakuna ambaye alimkumbuka mwenzake. Mvulana alimuacha msichana waliyekuwa wakitembea pamoja kimahaba. Marafiki walitimua mbio, kiasi cha kumfanya mmoja wapo kudumbukia katika mtaro. Huo ulikuwa upande wa mashariki, huku magharibi upande wa pili wa barabara kituo hicho cha taksi cha ujamaa; kilipakana na shule ya jitegemee. Hivyo sauti za wanafunzi waliokuwa wakitoka shuleni kwao, zikasikika "Bomuuu!!!" hakuna ambaye alikumbuka kuyatazama magari yaliyokuwa yakilikwepa gari ambalo lilibeba takribani abiria 64. Gari hilo lilikuwa likipepesuka huku na kule kutokana na kupasuka kwa gurudumu lake la mbele. Mpira wa gurudumu hilo, ndio uliopasuka na kulia kwa sauti kubwa hivyo kufanya wapita njia kudhani kuwa ni bomu. Gari hiyo ilikuwa inatoka upande wa uhasibu baada ya kukipita kituo cha jeshi la wokovu mita chache karibu na chuo cha diplomasia. Msichana mrembo Agape, alikuwa anvuta kwa kasi bila kuliona gari hiyo iliyopoteza muhimili wake na hivyo kukaribia kuanguka. Lilikuwa likipinda kwenda kulia na kushoto. Abiria wake walikuwa wakipiga kelele za kuomba msaada "Tunakufaaa" Agape yeye akapuuza mara alipoona kuwa huenda lipo mbali. Agape ambaye alikuwa akisoma katika chuo cha diplomasia akichukua shahada yake ya kwanza. Gari hiyo ikiwa inakaribia kumgonga, ghafla alipigwa kikumbo. Kikumbo ambacho kilimfanya apae juu kama kifaranga aliyenyakuliwa na mwewe na kuzisalimia changarawe kwa ngozi yake laini. Changarawe hizo za mawe mawe, zikampokea kwa ukatili na kumchubua juu ya goti. Ikawa ni picha iliyovuta hisia za watu wengi. Picha ya kijana aliyeyaokoa maisha ya msichana mrembo. Msichana aliyetaka kugongwa na gari lililopoteza mhimili wake. Picha hiyo ilivutia kutazama, lakini gari lililoanguka kwa kishindo ndio lilivuta hisia za watu wengi zaidi. Hata wale waliokuwa wakiwatazama Titus na Agape, waliwaacha na kukimbilia eneo ambalo gari lile lilidondoka. Gari hilo lilipita na kudondosha ukuta wa shule ya jitegemee. Si Agape wala Titus ambaye alikuwa na uwezo wa kuzungumza. Agape ndiye ambaye alikuwa na uwezo wa kunyanyua japo uso wake kumtazama aliyeyaokoa maisha yake. Mikwaruzo midogo midogo juu ya paji la uso pamoja mnikononi na miguuni ikamtisha Agape. Zilimtisha kudhani huenda ameumia sana. Agape alikuwa akigugumia kwa maumivu. Alilalamika maumivu aliyoyapata kutokana na kuangukia changarawe. Umbali ambao alianguki Titus alilowa damu. Kitu ambacho kilimtisha Titus suruali yake ilitoboka. Labda ungekuwa wewe ungedhani tu imechanika. Suruali nyeupe ya linen aliyokuwa ameivaa, ililowa damu. Kitu ambacho kilimtisha sana Titus. Lakini haikuwa hivyo kama ambavyo wewe ungedhani kuwa ilitoboka tu, lakini ni mfupa uliopasuka na kutokeza nje. Ikawa ni sura ya mbaya sana kwa mguu wake. Kutokana na mshituko alioupata, alipoteza fahamu. Agape akiwa bado anagugumia katika maumivu hayo, huku akiwa nakunja sura yake, alimshuhudi yule aliyemsaidia ameikumbatia lami kwa kuibusu. Titus alipoteza fahamu. Hali hiyo ilimchanganya sana Agape. Maumivu hakuyasikia tena, akanyanyuka kwa ujasiri. Japo alikuwa akichechemea, hakuyasikia maumivu. Alimuamsha bila mafanikio. Ukimya ukazidi kumfanya kulia bila kujua sababu ya machozi kumporomoka kama mfereji. Alipokuwa akitazama huku na huko, aliona watu wakikimbilia eneo ambalo gari lile lililosababisha hayo kutokea lilipoangukia. Alijaribu kujikokota mpaka ambapo angeweza kuipasa sauti yake na kuita gari ambayo ingempeleka yeye pamoja na kijana aliyemsaidia hospitali. Taksi ya kwanza ilikuwa ni ya kijana ambaye alionekana hakuwa mpenzi sana wa kufuatiliaCHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ matukio. Kazi ya kijana hiyo kubwa ilikuwa ni kutafuta abiria, ndiyo maana ilikuwa rahisi kumuona Agape aliyekuwa akipunnga mkono huku akiita Taksi. Aligeuza gari na kuwafuata mpaka walipo. Alimsaidia Agape kumbeba Titus na kuikimbiza gari yake kuelekea eneo la bandari ikiwa eneo barabara hiyo hiyo ya Kilwa. Mwendo ulikuwa ni wa kasi huku akipiga selo za fujo kuashiria kupishwa. Ikamsaidia Agape kufika mapema hospitali akiwa na Titus. Alimlipa ujira wake dereva na kuondoka zake kwa shukrani. Kitanda cha wagonjwa kikambizwa mbio mbio mpaka katika wodi ya wagonjwa mahututi. Hospitali ya taifa ya muhimbili ilikuwa na msongamano wa watu wengi, lakini Agape akapata huduma nzuri sana. Ikawa kama bahati sana kwake. Alipewa kitanda cha kupumzika huku akisafishwa sehemu za vidonda vyake. Kutokana na uchovu mwingi naye alipoteza fahamu. Baada ya dakika chache baadaye alipozinduka, alijihisi ni mwenye nguvu za kutosha na kuweza kusimama bila tatizo. Wazo la kwanza likawa juu ya Titus, licha ya kuwa alikuwa hamfahamu hata kwa jina. Msaada aliompa ulikuwa ni mkubwa na aliuthamini kwa kuwa aliyaweka maisha yake rehani kwa sababu yake, Agape. Dokta Jenifa James, ndiye alimsindikiza mpaka wodi ambayo Titus alikuwa anahudumiwa. Wakiwa nje picha ambayo alikutana nayo alipokuwa akitazama kwa ndani ikamfanya Agape kutumbua macho kwa uoga. Picha ambayo ilimtoa jasho jingi na kumpeleka puta moyo wake. Moyo ulisukuma kwa kasi damu yake na kufanya kwenda kasi mara mbili zaidi ya mapigo yake ya kawaida. Picha ambayo ilionesha Titus kuwa ameshindwa kupumua hata kwa msaada wa pumzi ya mashine ya oksijeni. Aliwasikia madaktari wakipiga kelele huku wakikimbizana huku na huko "Shitua mapigo yake ya moyo, shitua" Muuguzi mwingine naye alikuwa akimkandamiza kifuani Titus huku akijaribu kuyarudisha mapigo yake ya moyo. Kitu ambacho kikamshitua zaidi Agape na kujiuliza ni kivunjika kwa mfupa tu kumesababisha kijana yule kukaribia kupoteza maisha yake? "Haiwezekani" Alipiga kite cha uchungu huku akitaka kuingia na kuzuiwa na dokta Jenifa James. Hali ya chumba cha wagonjwa mahututi, ilionekana kutulia. Madaktari na wauguzi, wakiwa wanazishusha pumzi zao kwa ahueni. Walitoa vitambaa vilivyofunika pua na midomo yao huku kila mmoja akifuta jasho lililokuwa likimtiririka kutokana na uoga. Titus akarudishiwa kifaa cha mashine ya oksijeni kumsaidia kupumua. 'Bila shaka anaendelea vizuri sasa' Agape akajipa moyo. Baada ya kuwasihi kwa mua mrefu, madokta waliotoka katika chumba alicholazwa Titus aingie kumuona; akaruhusiwa. Aliingia baada ya kupewa mavazi maalumu kwa ajili ya kuvaa aingiapo ndani ya chumba cha wagonjwa mahututi. Hakutofautiana na madokta waliotoka ndani ya chumba hicho. Alivaa gauni la kijani, kofia iliyofunika nywele zake pamoja na kitambaa kilichofunika pua na mdomo huku kikiacha macho tu. Vyote vikiwa vya kijani. Aliingia na kupokelewa na madhari nzuri yenye hewa safi ya chumba hicho. Chumba kilicholindwa kwa madawa kuzuia bakteria yeyote ambaye angeweza kuleta madhara kwa mgonjwa. Alikisogelea kitanda cha mgonjwa ambaye ni Titus na machozi yalianza kumtoka. Alilia kutokana na shukrani ya kuwa hai mpaka sasa ni kwa sababu ya Titus. Mwanaume aliyethubutu kuiweka roho yake hewani kwa kuyaokoa yake Agape. Hakuijua thamani aliyonayo tangu alipotelekezwa na mpenzi wake Venance. Venance ambaye alimuacha na kutembea na rafiki yake wa karibu. "Huna hadhi ya kuwa na Venance" Kila alipoyakumbuka maneno ya rafiki yake wa muda mrefu yakamliza zaidi. Lakini chozi la sasa, ni chozi la shukrani. Chozi lililoshuka mashavuni na kuishia juu ya kitambaa hicho kilichozuia pua na mdomo visionekane. Alikaa kwa muda mrefu akiutathimini uzuri alio nao Titus. Uzuri ambao haukuonesha aina yeyote ya shida na umasikini kwa Titus. Sura ambayo ilionesha kujiweza na mvuto uliomvutia kumtazama baada ya kunyamaza. Uzuri ambao ulimtia wivu na kujiuliza kwanini alichelewa kukutana na kijana huyo. "Huenda nisingejuta leo kumpa moyo wangu akauchezea yule mshenzi" Akajisemea. Alijisemea kwa uchungu mara baada ya kulazimika kukiacha chuo cha Nairobi university huko nchini Kenya na kuamua kurudi kusoma Tanzania. Venance ndio sababu. Venance mwanaume pekee aliyetokea kumpenda kuliko mwanaume yeyote duniani. Mwanaume ambaye alimuonjesha ladha ya mapenzi mara baada ya kuutoa usichana wake. Furaha yake ikaingiwa na dosari. Dosari ya kumkumbuka Venance lilikuwa ni kosa kubwa sana. Kosa ambalo lilitonesha jeraha kubwa ndani ya moyo wake lililokuwa likivujisha damu ya majuto chuki na hasira ya kuutoa usichana wake kwa mtu ambaye hakuthamini penzi lake. Aliacha kuitazama sura ya Titus na kukumbuka jinsi ambavyo Venance alianza kumlaghai. Alitumia upweke wake kama njia rahisi ya kumteka kimapenzi. Zawadi mbali mbali zilizoonesha upendo kama kadi, maapple na vyakula; vilikuwa ni miongoni mwa vitu ambavyo vilimfanya Agape kuona kuwa anapendwa. Hakuleta pingamizi hata alipoambiwa kuwa anapendwa. Kumbukumbu hiyo ikamfanya kumuona hata Titus hana tofauti na Venance. Hata mwanzo alivutiwa na Venance. Hata mwanzo Venance alikuwa mkarimu tena sana inawezekana zaidi ya ukarimu aliofanyiwa na Titus. Akaropoka "Hapana!"CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ Kilio kikaongozwa na kwikwi. Akaapa kuwa kiapo chake cha kutakuja kupenda tena kitakuwa pale pale mpaka wakati muafaka utakapofika. Alitoka ndani ya chumba hicho ikiwa imeshatimu jioni ya saa 11:45. Alielekea chumba cha daktari na kumuaga kuwa kesho angerudi mapema mara baada ya kutoka hospitali. ... Titus akiwa katika usingizi ambao wengine waliuita ni nusu kifo, yaani kupoteza fahamu; alikuwa katika ndoto ya mwezi mmoja uliopita. Ndoto ambayo sijuhi kwanini ilimjia kwa wakati ambao alishikwa kwa hisia na Agape. Wakati ule ambao Agape alikuwa akilia kutokana na maisha ya usaliti wa mapenzi aliyopitia kwa Venance. Ndio wakati ambao Agape alikuwa akimshika na kumbinya binya Titus. Bila kujua Agape alimrudishia Titus kumbukumbu kwa njia ya ndoto. Kumbukumbu ambayo ilimchanganya sana Titus. Ilimchanganya mara kwa mara na kujiuliza ni vipi atamuona tena msichana yule? ndoto yenyewe ilihusu mwezi mmoja uliopita Titus akiwa na wenzake huko Kenya. Walienda Kenya kutokana na kazi ambayo walipewa. Kazi ya kuvunja na kuiba katika benki kuu ya nchi hiyo. Ni dili ambayo walipatiwa na mmoja wa vigogo wakubwa katika benki hiyo. Ramani nzima ya kazi walipatiwa na kuwa na uhakika na kazi yao. Kikundi chao kilikuwa na watu watano. Watu waliolewa thamani ya pesa na kuwa na tamaa nayo. Si wote walikuwa watu kutoka nchi mmoja, lakini kikundi hiki kilikuwa ni zaidi ya ndugu waliozaliwa tumbo moja. Mara ya kwanza walikutana katika chuo cha Udsm hapa hapa Tanzania. Maliki akiwa kama mkubwa wao yeye alitokea Algeria, aliwapita wenzake miaka 5 yeye akiwa na miaka 30. Mwingine akiwa ni Jonathan kutoka Uganda na watatu waliobaki wakiwa ndio watanzania. Hao walikuwa ni Titus, Fadhili na Fredy. Watoto walioanza utukutu waliofundishwa na Maliki. Maliki ambaye utajiri wa baba yake ulitegemea kazi chafu za kuua na kuiba. Titus akiwa mtoto wa kimasikini aliyewapoteza wazazi wake akitegemea kiasi kidogo cha fedha kilichoitwa mkopo kiwe kama msaada kwake akalaghaika na zilizoitwa harakati za utafutaji wa maliki. Maliki alifahamiana na viongozi wengi waliofanya uharamia nchi mbali mbali na ndiye aliyeletewa mchongo wa kuiba pesa katika benki kuu ya Kenya. "Utajiri ndio huu ndugu zangu" "Acha tu!" Fadhili akatokwa na uchu baada ya kusikia mchongo huu mkubwa. Bila uoga kila mtu alipanga cha kufanya wakiwa katika hoteli hiyo siku moja kabla ya tukio. Titus yeye akasema kuwa "Yaani ile Buu.. Baa! Tumefanikiwa? Baba yako naendesha hummer" Wote wakacheka kwa furaha na kupewa muda wa kwenda kujivinjari ndani ya jiji la Nairobi "Ila hakikisheni hamfanyi fujo na msichelewa zaidi ya saa sita usiku mkaja kukwamisha kazi ya kesho" Kila mmoja alienda njia yake. Titus akiwa na Jonathan walielekea katika Club iliyokuwa ikipiga mziki karibu na chuo kikuu cha jiji hilo. Bahati nzuri kulikuwako na wanachuo wengi ndani ya club hiyo ya usiku hivyo warembo walikuwa ni wengi sana. Miongoni mwa warembo hao ndipo Titus alipomuona msichana fulani aliyemvutia. "Samahani naweza kukununulia kinywaji?" "Asante." Msichana huyo alionekana mwenye msongo mkubwa wa mawazo. Ndio maana hakupenda kujumuika na wenzake kama wengine walivyokuwa wakifanya. Hata kujibu pia alijihisi shida. Titus akiwa na Jonathan alijaribu kumshawishi msichana yule kumfahamu japo jina lake "Naitwa Isabella nasoma Muguga" bila kujua Titus alidanganywa. Jina halisi la msichana huyo si hilo na wala hakusoma shule ambayo anaitaja. Msichana huyo alichukia wavulana na kutoona thamani ya mapenzi. Hakuwa mlevi lakini alikunywa kilevi kikali kuondoa mawazo yaliyosababishwa na maumivu ya mapenzi. Titus akavutiwa sana na msichana huyo. Alitamani angekuwa mkenya ili ampate na kuishi naye. Akatamani pia labda msichana huyo angekuwa ni mtanzania basi ingekuwa rahisi kuwa naye. Angemuona kila siku huenda asingekua mgumu kama anavyomsumbua hapo. Hiyo ikawa ni siku ya mwisho kumuona msichana huyo ndani ya giza nene huku akisaidiwa kuuona uzuri wa msichana huyo kwa taa za disco. "Jonathan" wakiwa wanajiandaa kwenda kuiba bank, Jonathan alipomgeukia huku akiitazama silaha yake ndogo bastola aina ya Microvet aliyoiweka kiwambo cha kuzuia sauti, Titus akamwambia lililopo moyoni mwake "Kiukweli nimempenda sana yule msichana" Jonathan alimcheka sana huku Fredy Fadhili na Maliki wakibaki kwenye mabano ya kutofahamu. Muda wa tukio ulikuwa umetimia. Waliandaa kila kifaa kilichokuwa kikihitajika kuwarahisishia kazi ya kuchukua pesa benki. Walifahamu fika kuwa katika benki kubwa kama hiyo lazima ulinzi ungekuwa mkubwa wa kutosha. Ulinzi ambao walipaswa kuwa makini ili wasikamatwe. Kadi ya kufungua kabati lenye pesa, walikabidhiwa. Ilikuwa ni kadi ya muda iliyotengenezwa na Jackson Odhiambo. Kigogo wa benki hiyo. Njama zilizopangwa kwa muda mrefu. Njama ambazo zilianza baada ya mianya ya wazi kuonekana katika kitengo cha kuhifadhi hela kubweteka. Isingekuwa rahisi kukubali kuwa wazembe, pasipo kuwa makini ili hali wakifahamu kuwa ulinzi wa nchi ya Kenya ulikuwa mkubwa sana. Ulinzi ambao uliongezwa kutokana na tukio la shambulio la ugaidi lililotokea miezi michache iliyopita. Waliamini kila kitu kitaenda sawa lakini hawakupenda kujiaminisha kirahisi hivyo. Walitengeneza mfano wa duara huku vichwa vyao wakiviinamisha chini na kusali. Unaweza kushangaa. Unaweza kushangaa inakuwaje kwa wahalifu wakiomba Mungu. Lakini wao waliamini sana kuwa Mungu alikuwa akiwasikiliza. Waliamini kuwa Mungu ndiye alikuwa akiwalinda siku zote walipokuwa wakifanya tukio. kuwalinda wasikamatwe na kufanikiwa kupata walichokuwa wamekiendea. Hawakuchukua muda mrefu wakawa wamemaliza sala yao. Walipeana mikono na kila mmoja kubeba begi kisha kutoka nje. Ilikuwa ni majira ambayo kwa muda huo wafanyakazi walianza kupungua katika mazingira hayo ya benki. Ulinzi wa camera ulikuwa ni mkubwa pamoja na askari waliomwagwa kila kona ya jengo pana la benki hiyo. Titus akiwa na wenzake ndani ya gari lililofanana na Noah lenye rangi nyeusi tupu, walikuwa wakizima mitambo ya canmera ya benki hiyo. Walikuwa wakitumia uwezo wa rada ambayo alikuwa amepewa Maliki kama zawadi. Rada hiyo ilikuwa ni mali ya baba yake Maliki, hivyo Maliki alipewa vifaa vya kutumia na uwezo wa kuiendesha rada hiyo. Titus alimuona Maliki akibonyeza namba kadhaa kwenye kompyuta yake ya mapajani, kisha ikatokea mandhari yote ya ndani ya benki hoyo. Waliitana kwa pamoja na Maliki akawa kama akiwaongoza pa kuingia mpaka kulifikia kabati ambalo lilikuwa na pesa. Wakatabasamu na kujitia moyo kwa kugongeana mikono. Maliki akazizima kamera zote za eneo hilo hata zile maalumu zilizowekwa barabarani kwa ajili ya ulinzi wa nje. Wakavaa vinyago ambavyo si rahisi kufahamu sura zao. Kila mmoja kabla hajalikaribia jengo hilo walitoa bunduki zao zilizo na kiwambo cha kuzuia sauti kutoa mlio. Johnson na Maliki ndio waliua walinzi sita waliokuwa wakitembea tembea hapo nje. Walifanikiwa kuingia ndani huku wakiendelea kuua kwa uangalifu wa hali ya juu wasikamatwe. Ulinzi ulikuwa ni mkali sana. Walikuwa na tahadhali juu ya ulinzi wa umeme uliowekwa kabla ya kuufikia mlango wa kabati la pesa. Ulinzi ambao ulikuwa hauonekani kwa macho ya kawaida. Kila mmoja alivaa miwani maalumu iliyosaidia kuiona miale hiyo ya umeme yenye rangi nyekundu. Maliki alikuwa na uwezo wa kuikata miale hiyo. Pasword zake alikuwa nazo. Alizitumia kwa kubonyeza kwenye kifaa ambacho kilikuwa pembeni. Kifaa hicho kilikuwa kama sanamu la raisi wa nchi hiyo Bwana John Bravo. Sanamu hiyo ilikuwa imenyoosha mkono. Akakumbuka maneno aliyokuwa akiambiwa na Odhiambo, kigogo wa benki hiyo. "Ukiuzungusha mkono wa sanamu hiyo, utatokea mwanga ambao utakuonesha namba kadhaa zitakazotokea hewani kuwa kama kioo kisha wewe utabonyeza namba 911410"CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ Maliki alikumbuka vizuri maelekezo hayo ya Odhiambo. Walifanikiwa kuiona miale ile iliyokaa kwa aina ya mtindo wa zigzag ikizimika kama umeme. Waliingia mpaka katika chumba ambacho kulikuwa na kabati hilo lenye pesa. Hakuna ambaye aliamini kuwa walifika kwenye utajiri waliokuwa wakiuota. Lakini hawakuwa wazembe kukaa japo sekunde. Maliki akaitazama saa yake ya mkononi, ilikuwa imeshameza dakika kumi tangu waingie eneo hilo la chini kabisa kilipo chumba hicho. "Zimebaki dakika Tano tutoke" Hivyo Maliki alipanga watumie dakika kumi na tano tu. Maliki ndiye alifungua kabati hilo lenye pesa. Kabati lilikuwa lina milango mitatu tu peke yake. Mlango wa kwanza ulifunguliwa kwa kunyongwa kifaa fulani kilichofanana kabisa na sterling ya meli, mlango wa pili ukafunguliwa kwa kiganja cha mkono wa mtu maalumu. Mtu huyo alikuwa gavana wa benki hiyo. Odhiambo alitumia vifaa maalumu kupata alama za kiganja hicho cha bwana Saitoti Brady. Akamtumia Maliki kwa njia ya mtandao. Mtandao ambao Maliki alitoa mfuko maalumu wenye alama za kiganja hicho na kukandamiza na chake kisha kuweza kufungua mlango huo wa pili. Mlango wa tatu ulikuwa kama ule wa kwanza. Nao ukatii mlango ukawa wazi. Kilichokuwa ndani ya kabati hilo, kikamfanya Titus kupumua, Jonathan kucheka kwa nguvu na Maliki pamoja na fadhili kukenua meno kwa furaha Fredy yeye alikuwa ameshalivua begi lake maalumu kwa kuzihifadhi hela hizo. Fedha zilikuwa za nchi mbali mbali. Ziliwekwa kwa mpangilio maalumu. Ila Maliki na Titus walishughulika kujaza fedha za dubai, Riyali kwa mariyali. Mabegi yalituna kiasi kwamba hata kwao wenyewe yakawa mazito. Maliki akawaongoza njia nyingine yakutokea ambayo alielekezwa na bwana Odhiambo. Wakati wanatoka ndani ya kabati hilo la fedha, vishindo vya watu wakikimbilia eneo hilo ndio vikawafanya wasimame. Bunduki zao zikiwa mbele, mikononi mwao zimeshikiliwa kiukakamavu haswa walikuwa wakinyata kuelekea kule alipokuwa akienda Maliki. Walikuwa wakirudi kinyume nyume. Mara hapo hapo ndoto ya Titus ikakatishwa mara baada ya fahamu kumrudia taratibu akiwa ndani ya kitanda cha chumba cha wagonjwa mahututi. Alianza kushitua kwa kurusha kidole chake cha shahada kilichopeleka taarifa kwenye kifaa cha oksijeni kuonesha mtu huyo amerudiwa na fahamu zake ... Akiwa njiani kuelekea nyumbani kwao, mawazo ya Agape yalikuwa kwa Titus. Alikumbuka vyema uzuri wa Titus. Ndiyo, alishakutana na wengi vyuoni haswa alipokuwa Nairobi, lakini uzuri wa Titus ulikuwa ni wa tofauti. Kijana mwenye umbo pana kiasi kifua cha mazoezi na weusi wa kunawiri uliichanganya sana akili ya agape. Midomo yake midogo ilibebwa na kidevu kilichotota ndevu zilizokolezwa na rangi nyeusi kuleta tu uzuri zaidi juu ya kidevu cha Titus. Sura yake ya duara ilibeba pua ndefu iliyochongoka na kuleta ulakini ndani ya mawazo ya Agape na kujinong'oneza mwenyewe "Huenda akawa ni chotara" Mara akacheka alipoingia ndani ya geti lao. Alifika mpaka sebuleni alipokutana na baba yake Mzee Twaha Kimashi. "Umetoka wapi?" Mzee aliyeukataa uzee na kujivika ujana kutokana na mazoezi ya kujiweka sawa kimwili na afya yote ikiwa ni kujihakikishia kazi zake za upelelezi. Mzee aliyenyemelewa na vituta vya barafu nyeupe ambazo wewe ungeziita mvi. Basi kama asingekuwa na kazi nyingi weupe huo usingeuona. Kazi ambazo zilimfanya hata kupoteza mwili na uzee kumnyemelea tena. Ndiyo maana yeye binafsi alionmba ruhusa kwa mkuu wake wa kazi apate muda wa kulala japo kwa masaa ishirini na nne. Lakini macho yake hayakuzoea kitu kinachoitwa usingizi. Ndio maana hakukitaka kitanda, akawa sebuleni akisoma gazeti. Kazi kubwa ya kuwatafuta watanzania watatu na maharamia wawili wa kiarabu ilimchanganya sana. Hakuwa na kawaida ya kuwa mkali kwa Agape wake aliyempenda kama mboni ya jicho lake lakini mawazo yaliyomchanganya fikra zake yakasahau hata upendo alio nao kwa mwanaye. "Nakuuliza ulikuwa wapi?" Akarudia tena. Tabasamu alilokuja nalo Agape toka alipotoka, likatoweka. Uoga ukamvaa na kumueleza ukweli wote kuhusu ajali aliyoipata. Mzee Twaha akampa pole mwanaye na huruma ikamrudia ikikaribishwa na ule upendo wa dhati alio nao kwa mwanaye. Usiku ukiwa umeliathiri anga na nyota zikatawala mbingu basi Agape akalala akiwa ana ndoto tamu kuhusu Titus. Licha ya kumueleza kuwa alipata ajali, lakini alisahau kumueleza baba yake juu ya kijana aliyemsaidia. Usingizi huo ukafutika siku ya pili yake majira ya saa 2. Alipoenda mezani hakumkuta baba yake. Mfanyakazi wa ndani akamueleza kuwa mzee Twaha aliondoka tangu saa 10 alfajiri, kabla hata jua kuchomoza. Naye aliitazama saa yake akaifakamia juisi ya mchanganyiko wa parachichi na ukwaju ndani ya bilauri na kuondoka na gari yake. Gari ndogo aina tya Subaru ambayo jana aliiacha service. Safari ya kwanza ilikuwa ni kwenda kwa Titus, muhimbili hospitali. Kutoka masaki alipokuwa akiishi na baba yake mpaka muhimbili, alipoteza dakika 30 tu katika msongamano mdogo wa magari. Alikikumbuka chumba cha daktari. Alipofika tu akapokelewa kwa habari mbili na daktari Jenifa James. Dokta Jenifa James alimueleza kuwa "Kuna habari mbili yaani nzuri na mbaya, sijuhi nianze na ipi kukueleza?" Moyo wa Agape ukamuenda mbio kiasi cha kumtoa jasho jingi. Katika uchaguzi wa habari, Agape alichagua habari nzuri kwanza. Aliona ni heri asikie jambo zuri kwanza kisha baya atajua jinsi atakavyolikabili. Jenifa James akarekebisha koo yake kwa kikohozi kikavu na miwani yake kwa vidole vyake viwili. Miwani hiyo ikawa imenasa vyema juu ya pua yake ndogo iliyoendana na uso wake mdogo uliovutia. Hakuwa mweupe. Akiwa ameshika makaratasi kadhaa, baadaye Agape alifahamu kuwa yalikuwa hayana maana yeyote. "Mgonjwa wako amepona" Jenifa James alizungumza, Agape macho yakamtoka pima sanjari na tabasamu pana la furaha. Akauliza kwa pupa huku bado furaha aliyo nayo ikiwa imemganda usoni mwake. "Ninaweza kumuona? Ninaweza kumuona kabla hujanieleza hiyo habari mbaya?" Dokta Jenifa James akatabasamu kabla hajaponyokwa na kicheko hafifu. Akamueleza kuwa " Hiyo ndiyo habari mbaya" Tabasamu na furaha vikajitenga na uso wa Agape. Macho yake yakaingiwa na wasiwasi huku hasira ikiwa inamtafuna taratibu. "Una maana gani dokta" "Ndugu yako amepotea katika mazingira ya kutatanisha" alinyamaza kiasi kisha akaendelea "ilikuwa ni saa chache tu baada ya kuamka, nikamsafisha mwenyewe kidonda na kumuwekea dawa kwenye dripu yake. Kutokana dawa zilikuwa kali, ingawa alishapatiwa chai ilibidi tumpe chai nyingine ili dawa ifanye kazi. Tukiwa tunamuandalia staftahi, dakika tano zilikuwa nyingi btuliporudi wodini aklitoweka" "Ametoweka? Ametoweka vipi na yeye ni mgonjwa? Amewazaje kutembea kama ana mguu mbovu?" Agape alihamaki kwa hasira. Si kwamba alimfahamu sana Titus, cha ajabu hata jina lake hakulifahamu. Alimuuliza Dokta Jenifa James ambayo yalikuwa magumu sana kupata majibu ambayo aliyatarajia "Mguu si umewekwa antena? Na ulinieleza kuwa hataweza kutembea bila magongo au baiskeli ya vilema? Kwanini sasa unanieleza kitu ambacho unafahamu fika sitaweza kukuelewa?" "Hata mimi pia sina la kujibu kwa kuwa ninajiuliza mengi zaidi ya hayo unayoniongezea" Agape alinyanyuka kwa ghadhabu na kutoka ndani ya chumba cha dokta Jenifa James bila kuaga kwa maelewano. Alipoenda hakupajua lakini kilichokuwa akilini mwake ni kuwa anaenda kumtafuta Titus. Anamtafutaje Titus? Kijana waliyekutana barabarani baada ya kumsaidia kumuokoa katika ajali? Kama alimsaidia kutoka katika ajali na yeye alishalipa fadhila kumleta hospitali. Habari njema ni kuwa Titus ameponan kwanini anaendelea kuwa na hamu ya kumtafuta? Kwanini awe na shahuku ikiwa wao wamekutana kwa bahati mbaya na amepotea kwa makusudi? Akiwa bado anajiuliza hayo kama anayejisuta mwenyewe, akapata majibu ya hayo yote alipokuwa katika mgahawa fulani uliopo nje ya hospitali ya taifa ya Muhimbili. Aliagiza maziwa ya moto na toast(mkate uliochanganywa na mayai). Mapenzi. Jinamizi mapenzi ndio lilimpa uchizi wa kumtafuta asiyemjua. Kumtafuta na kujali kupotea kwa Titus ndio hapo akafahamu kuwa ameanza kutembelewa na ule ugonjwa wa mapenzi. Ugonjwa wa kupenda kupitiliza. Kujitoa mwili na roho kwa mwanaume yeyote bila kujali amemfahamu kwa muda upi. Hakujali kusubiri kuichunguza tabia yake kwa muda mrefu. 'Ukimchunguza bata hutamla' alijitetea kila mara alipoingia kwenye mapenzi kichwa kichwa. Mwisho wa siku aliyemuamini akamtenda asivyo tegemea. Venance. "Oh Venance!" Chai ikamkifu alipolikumbuka jina la mtu huyo. Alimuita muhudumu wa mgahawa na kumlipa pesa yake kisha akaondoka. Alitekenya ufunguo injini ikaitika akaigeuza gari yake na kuelekea Masaki.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ Akili yake ikawa imevurugika kwa kuwa alianza kumpenda mwanaume mwingine. Kiumbe ambacho alikiona kuwa hakina tofauti na mwenzake. 'Wanaume wote ni sawa' alisema mara kwa mara. Angekuwa ni katili? Basi angewaangamiza wavulana wengi kama alivyofanya Camilla. Camilla aliyekuwa akikata sehemu za siri za wanaume na kuzibanika ili zisioze. Kisha alizihifadhi katika sanduku lake. Akajaribu kukumbuka mkasa huo wa Camilla ulitokea mwaka gani? "Mwaka gani tenaaa..?" Akajisonya kwa upuuzi wa kupoteza kumbukumbu kuwa aliusoma mkasa huo katika kitabu kilichoitwa KIFO NI HAKI YANGU kama kilivyoandikwa na mwandishi mashuhuri Tanzania. Mwandishi aliyejizolea mashabiki wengi katika Tanzania na nchi za jirani. Akiwa katika kuwaza huku jinsi alivyowachukia wanaume, hakujitofautisha na Camilla. Tofauti yake yeye alikuwa ametendwa na mwanaume mmoja na si wengi kama Camilla alivyofanyiwa. Alikuwa na baba anayempenda na si yatima kama Camilla. Alipojioanisha yeye na Camilla akaona heri yeye na ana nafasi ya kupenda tena. Akajiona yupo sahihi kumpenda Titus. Lakini hida ilikuwa hamfahamu Titus. Hafahamu anapokaa na wapi amekwenda. Mwendo mfupi na foleni chache huku mawazo yakiwa lukuki kichwani mwake, alikuwa tayari amefika nje ya geti la nyumbani kwao. Alipiga selo mlinzi Maseko afungue geti jeusi la chuma. ... Titus akiwa ndani ya chumba cha wagonjwa mahututi, fahamu zikiwa zimemrudia; Maliki na Fredy walikuwa mbele yake. Sura zao zikiwa zimejikunja kwa hasira, binafsi hakuelewa wamejuaje kuwa yupo hapo ndani ya chumba hicho. "Pole sana kamanda" Fredy ndiye alizungumza. Titus hakujibu kitu. Hakujibu kwa kuwa hakuelewa sababu ya ujio wao. Sawa walikuwa ni washiriki wake wakubwa, lakini kwenye mavazi ya kiuguzi? Hila zote za nini ikiwa bado anapata matibabu? "Wapelelezi wa kimataifa wameletwa kutoka nje ya nchi kutafuta watu watatu ambao ni mimi wewe na fredy walioiba kiasi kikubwa cha fedha katika benki kuu ya kenya. Unalijua hilo?" Macho ya wasiwasi yakawa sambamba na mapigo ya moyo yaliyomuenda kasi Titus. Jonathan na Fadhili walipoteza maisha katika tukio lile la kurushiana risasi. Hawakufanikiwa kuondoka nao kutokana na kuzungukwa na lundo la askari waliomwagwa katika jiji zima la nairobi kuendesha msako wa wezi wa benki. Maliki akamwambia "basi kama ulikuwa hufahamu licha ya wenzetu kupoteza maisha pale benki na vivuli vyetu pia vimekamatwa" Titus akahamaki "vivuli? Sijakuelewa!?" "Ndiyo unaweza ukawa hujaelewa kwa kudhani kuwa nilipozima zile kamera za ulinzi ndio nilimaliza. Ulinzi wa eneo kama lile ni mkubwa sana hivyo hata kamera zao zina nguvu kuliko nilivyodhani. Kamera zile hata ukichomoa waya wake zina uwezo wa kunakili kivuli cha muhusika. Licha ya mimi kuzizima walifanikiwa kuvipata vivuli vyetu. Wapelelezi hao kutoka nje ya nchi(interpol) hutumia vivuli hivyo kutafuta wahusika. Wamefanikiwa Nairobi kwa michoro waliyoibuni wao wenyewe kutoka kwa mashuhuda huku wakitumia vivuli hivyo kutatumbua na kuelezwa kuwa tupo Tanzania" Titus alikatishwa na Fredy "Hakuna sababu ya kumueleza mambo ambayo tunaweza kumueleza nyumbani. Tumchukue haraka na tutokomee eneo hili" "Sawa" Maliki hakupinga na kutokana na hali halisi alivyoelezwa, Titus alikubali kuendeshwa kwenye baiskeli ya vilema na kutokomea eneo la hospitali. aliingizwa ndani ya gari la wagonjwa kwa hila za Maliki na Fredy ikiwa njia rahisi ya kutolewa eneo hilo la hospitali bila vizuizi vya maswali ya walinzi wazembe getini. Maliki na Fredy walitumia pesa kuhakikisha Titus anapona. Titus alikuwa kiungo muhimu katika shughuli zao. Titus ndiye mlenga shabaha mashuhuri na asiyekosa anachokilenga. Waliwatumia baadhi ya madaktari bingwa huku wakiwahonga kiasi kikubwa cha pesa kumtibu Titus. Kipindi cha nusu mwezi, Titus alionesha uhafadhali wa afya. Alikuwa akitembea kwa kuchechemea baadaye, yaani mwezi mmoja ulipopita akapona kabisa na kuweza hata kukimbia. Lakini mguu wake ulikuwa na jeraha kubwa sana. Jeraha ambalo alishonwa nyuzi ishirini kwenye ugoko wake baada ya kuunganishwa mfupa wake na vyuma ili kuurudisha mguu kuwa katika hali ya kawaida. Nafuu hiyo ya Titus, ikamtia faraja Maliki. Salamu zikatumwa kutoka kwa baba yake Maliki, huko Algeria. Salamu za kumuangamiza mpelelezi mkuu aliyeshikilia kesi hiyo. Kesi ya kufuatilia vibaka waliopora mabilioni ya pesa katika benki kuu ya Kenya. ".. Ni mtanzania" Maliki alikuwa akizungumza na baba yake katika mtandao wa skype, akimpa maelekezo juu ya mpelelezi huyo. "Sawa baba tutamshughulikia" Maliki akahitisha kikao. Kikao kilichowekwa katika mgahawa mdogo katika hoteli ya JB bellmont pale katikati ya mji. Pesa walikuwa nazo hivyo walikunywa na kula walichokitaka. Kiasi cha pesa walizoziiba benki, kilitosha kukaa bila kufanya kazi kwa zaidi ya miaka mitatu. Ni kiasi kikubwa cha pesa. Kiasi ambacho kilitosha kufanya starehe za kila aina bila kujali gharama za starehe waliyokuwa wakifanya. Kikao kilihudhuriwa baada ya kutumiwa ujumbe mfupi kwenye simu zao, Titus na Fredy kutoka kwa Maliki. Walikutana majira ya saa tano usiku. Katika mgahawa huo kulipigwa mziki laini kutoka katika bendi maarufu nchini. Wakwanza kufika alikuwa Maliki Al-jamal aliyeagiza wine tamu huku akisindikiza kinywaji hicho na moshi mzito wa sigara. Alikuwa akiangalia wahudumu waliovutia kwa utembeaji wao wa madaa waliwazidi hata walimbwende walioitwa 'Miss Tanzania' Alikwisha mfahamu mmoja wao kuwa aliitwa Tausi. Alipokuwa akiitazama saa yake, ilitimu saa 5:45 usiku. Akapiga kite cha hasira "Shenzi!" Kabla hasira zake hazijaisha hata mikunjo juu ya paji lake la uso kukunjuka, Mbele yake akasimama Titus na Fredy wakimsalimu. "Mna bahati, ilikuwa nimalize hiki kinywaji" akiinua glass yake juu kuonesha kinywaji kilichokaribia kuisha. "Niondoke" Kisha akaipiga funda moja na kuimaliza yote. Fredy na Titus walipokaa, alinyoosha mkono wake wa kushoto juu kumuita Tausi. Tausi alikuja kumsikiliza. "Lete mzinga mwingine mrembo" Akampiga ukope. Akakohoa kidogo na kuwageukia Titus na Fredy, aliwakuta wakicheka. "Mnacheka nini?" Naye akaunda tabasamu. "Tuendelee na jambo la msingi" Titus alizungumza "Any way kuna kizuizi"CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ "Kizuizi?" Fredy aliuliza "Kipi?" Titus akapigilia msumari. "Kuna mpelelezi mkubwa wa Tanzania amepewa kazi ya kututafuta. Halali, hali mpaka atupate" "Kwa hiyo?" Fredy akauliza kwa kiherehere kilichokamata shahuku yake. Maliki alikenua kwa kuudhika na kumjibu "Una uliza kwa hiyo hujui misingi ya kazi zetu?" "Mimi pia siifahamu?" Titus ndiye alizungumza "unaonaje ukiacha mafumbo kama tupo kwenye taarabu ukaenda moja kwa moja kwenye main point?" Titus akamaliza "Auawe haraka kabla hatujaanza kushukiwa na kusumbuliwa" Maliki akamaliza. Tausi alileta kinywaji mezani na kuwafungulia hatinaye kuwamiminia kwenye glass zao. Aliwakaribisha kwa sauti nyororo. "Karibuni" "Ahsante" ni Maliki ndiye alijibu. Fredy na Titus walikuwa wakimtazama tu. "Nadhani nimeeleweka?" Maliki akauliza teana, mara baada ya ukimya uliopita kitambo. "Wala haikuwa na sababu ya kukutana tungezungumzia nyumbani" Fredy alionekana kukerwa na kutoka siku hiyo. Walipiga kilaji na chakula kizito kutoka katika menu ya leo ndani ya hotel hiyo. Baada ya muda kwenda sana, Titus aliaga kwenda chooni. Choo kilikuwa hatua chache kutoka kwa watu waliokuwa wakitazama na kusikiliza mziki wa bendi hiyo na ni lazima upite eneo la watu waliokuwa wakicheza. Pombe haikuwa nyingi kichwani mwa Titus, lakini alichechemea kiasi kutokana na ubovu wa mguu wake. Hivyo hata ungekutana naye eneo hilo ungedhani huenda ni pombe. Si unafahamu hilo ni eneo la kustarehe? Akaingia chooni vizuri na kumaliza shughuli zake ndani ya choo hicho. Akawa anatoka kurudi alipokuwa amekaa. Kabla hajalipita eneo la watu waliokuwa wakicheza, alikutana na msichana anayemfahamu. Msichana yule yule ambaye walikutana Kenya. Alikutana na Agape ambaye alimsaidia katika ajali ya Gari katika barabara ya Kilwa. Ndiye aliyesababisha mguu wake kupata kovu na kilema cha maisha. Lakini yeye hakumkumbuka wala hakumfahamu hivyo. Alimfahamu msichana huyo alikutana naye kenya siku moja kabla ya kwenda kufanya tukio. Alikutana naye ndani ya club ya usiku iliyopo karibu na chuo kikuu cha Nairobi. Moyo wake ukalipuka kwa furaha. Ndiye huyo huyo aliyemuona eneo lile. Ndiye huyo aliyemuwaza akamkumbuka na hata kumuota alipopata ajali. Hakuiona vyema sura nzuri ya msichana aliyemsaidia ndio maana hakuweza kumfananisha huyu na yule. Akaita jina lake "Isabella!" Hakuna aliyegeuka kati ya wasichana watatu waliokuwa wakicheza pamoja mziki wa bendi hiyo, Agape akiwa miongoni mwao. Titus akaita tena. Bado hakuna aliyeshitushwa wala kujisumbua kama kuna aliyekuwa anaitwa kati yao. Ni hapo Titus alipoamua kumfuata Agape na kumshika mkono. "Isabella!" Alimvuta mpaka eneo fulani lenye mwanga wa kutosha. Rafiki zake Agape nao walikuwa wakimfuata. "Ina maana umenisahau?" "He! We kaka vipi?" Agape Aliongea kilevi huku akiwa amelegea sana "mi sikujuhi bwana" Ulevi wa Isabella ulianza siku ile club. Siku ambayo alikutana na Titus. Ndiyo siku ambayo alianza ulevi ambao pombe yake alimnunulia Titus mwenyewe. Ya kwanza haikuwa tamu lakini kadri alivyoweka nia na nguvu katika kupoteza mawazo juu ya Venance, aliamua awe mlevi aliyekubuhu. Titus akadhani ndiyo tabia yake. Akajaribu kumkumbusha lakini akaambulia matusi na sonyo la mwisho lililomlazimu kumuachia mkono wake na Agape kuondoka akiwa na rafiki zake. Lakini yeye binafsi, aliamua usiku huo uywe usiku wa kumfuatilia Agape aliyemjua kama Isabella. Alirudi kwenye meza ya rafiki zake huku macho yae yakiwa kwenye meza aliyokaa Agape. ... Aliporudi nyumbani hakukuta mtu. Ilikuwa ni hali ya kawaida baba yake anapokuwa busy na kazi fulani. Hakuifahamu kazi ya baba yake na wala hakujisumbua kutaka kuijua. Kuna siku alijaribu kuuliza, jibu alilopewa ndio jibu lililomfanya asiulize. Aliambiwa "Kuna unachokikosa?" Basi akaamua kunyamaza kwa kuwa ni kweli alipata kila alichokihitaji. Kazi ya baba yake ni kazi ngumu inayohitaji usiri mkubwa. Agape akaingia moja kwa moja mpaka chumbani kwake na kukisoma kitabu cha ROHO ZA WAFU yeye ni mpenzi sana wa hadithi za stallone. Muandishi mdogo aliyemezwa na simulizi za kutisha. Nani asiyemfahamu na kile kitabu chake kilichokamata wengi kilichoitwa Kivuli cheusi? Akawa teja wa simulizi zake kila alipotoa nakala mpya. Lakini kitu cha kushangaza kikaibuka. Leo hakutamani kabisa kusoma kitabu hicho kipya kilichotoka hivi karibuni. Akajiuliza kwanini? 'Mawazo' nafsi fulani ikamnong'oneza. Ni kweli alikuwa na mawazo sana lakini alipojiuliza alikuwa akiwaza nini bado nafsi ile rafiki, ikamjibu 'unawaza kuhusu mapenzi' "Mapenzi? Hapana. Nampenda nani kiasi cha kunifanya nikose raha kiasi hiki?" Akazungumza kwa nguvu huku akijaribu kuunda kitu kama tabasamu. Akajaribu kufungua kurasa katika kitabu kile cha roho za wafu, bado hakuiona ladha ya kitabu hicho licha ya kuwa ni stori iliyokamata ubora wa hadithi zote za kichawi tanzania na nchi kadhaa za Afrika. 'Unamuwaza yule kijana' hapo ile nafsi ikazungumza kana kwamba alikuwa akijiambia mwenyewe. Akakishika kichwa chake kama kilikuwa kinauma hivi. Akaudhika na hisia hizo. Akaona ni heri atoke. "Nitoke niende wapi?" Likawa ni swali jingine alilojiuliza. Likamuumiza kichwa. Punde akakumbuka ilikuwa ni jumamosi siku hiyo. Akajiuliza "Kwanini nisiende club? Hapana club si vyema hakuvutii kwa leo" akakumbuka kuwa kulikuwa na tangazo kuwa ile bendi anayoipenda sana ilikuwa ikipiga katika ukumbi wa JB bellmonte hotel. Akampigia rafiki yake Salsha na Nadia. Hawakukataa kwa kuwa kuhusu usafiri na gharama zote zilikuwa juu yake.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/ Waliingia ndani ya ukumbi huo majira ya saa nne. Saa moja kabla ya Titus. Hivyo masaa mawili baadaye hadi wanakuja kukutana na Titus, alikuwa ameshalewa mvinyo. Alikumbuka kuwa kuna mtu alimuita kwa jina la Isabella saa chache baada ya kutoka katika hotel ya JB bellmonte. Hakujua ni kwanini alimuita hivyo. Hiyo ilikuwa ni saa nane usiku. Ndani ya hostel za chuo cha uchumi IFM huko katikati ya jiji. Alipuuza jambo hilo la kuitwa Isabella akidhani huenda mtu huyo alimfananisha tu kama wengine walivyokuwa wakimfananisha na Hanna montana yule muigizaji wa kimarekani. Akapitiwa na usingizi bila kufahamu kuwa yule aliyekuwa akimuita Isabella ni yule aliyemsaidia alipotaka kugongwa na gari karibu na chuo cha diplomasia alichokuwa akisoma. Hakujua kuwa aliwahi kukutana naye nchini Kenya siku chache tangu alipoachwa na Venance. Hakujua pia kama mvulana huyo alimfuatilia hadi mahali hapo na kudhani kuwa yeye ni mwanafunzi wa chuo cha Ifm.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    ITAENDELEA



0 comments:

Post a Comment

Blog