Search This Blog

Sunday 19 June 2022

USINIBANIE - 5

 





    Simulizi : Usinibanie

    Sehemu Ya Tano (5)





    Muda mfupi baadae tukawa tukiingia barabara ya Bagamoyo

    ambako jioni ile hakukuwa na foleni kabisa. Kagiza kalikuwa

    kameshamiri.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Niliingia barabara hiyo kuu nikiendesha huku mpenzi wangu

    Tausi kanilalia begani na mkono wake ukiwa pajani kwangu

    akinifariji, dunia yote ilikuwa yangu. Muziki laini ulikuwa

    ukiunguruma garini huku Lionel Richie akifanya vitu vyake

    vya kiutu uzima. Kwa kweli ukijipanga pepo inashuka hapa

    hapa bongo!



    Ghafla wakati nalipita eneo la Tegeta, nikakutana na lori

    lililokuwa likija kwa kasi usawa wa gari nililokuwa

    nikiliendesha. Lilikuwa likilikwepa daladala lililokuwa

    limeharibika na kusimama njiani.



    Nikajaribu kulikwepa kwa kutoka nje ya barabara. Japo

    tulikosa kugongwa uso kwa uso, gari langu likaserereka na

    kupinduka kisha sikujua ni nini kiliendelea.



    *****

    Nilipokuja kuzinduka nikajikuta nimelala kitandani

    hospitalini nikiwa na maumivu makali ya kichwa. Pembeni

    yangu alikuwa amekaa mtu nisiyemfahamu, lakini hakuonekana

    kama ni mtu mwenye masihara.



    Hakukuwa na dalili yeyote ya kuwepo Tausi mule nilikolazwa,

    nikaanza kuvuta kumbukumbu kuhusu kilichotokea lakini

    sikuweza kukumbuka chochote cha ziada. Nikatulia pale

    kitandani nikimkagua yule mtu ambaye muda wote alikuwa

    akiniangalia bila kupepesa macho.



    Japo sikuwa nikisikia pilika pilika zozote, mwanga uliokuwa

    ukipenya dirishani ulikuwa ukiashiria kuwa ulikuwa ni muda

    wa mchana. Akili yangu ilianza kufanya kazi haraka haraka

    kujua la kufanya, lakini sikulipata.



    Na hata ningelipata nisingeweza kulitekeleza kutokana na hali yangu ya kiafya.



    Mtu yule hakuwa hata na utu wa kuniuliza kuwa najisikiaje,

    na nilipomkagua vizuri nikaiona bastola imetulia kiunoni

    mwake. Ni askari au mtu wa Mzee Nurdin?



    Nilikuwa nimefunikwa shuka lakini nikaanza kuhisi ubaridi,

    kwa kuwa nilifikiri kuwa hata kama ni askari bado kuna

    uwezekano akawa ni mmoja kati ya wale wanaotumiwa na Mzee

    Nurdin.



    Kidogo akaingia daktari, alionekana ni muungwana sana

    machoni na uso wake wa kilevi lakini sikutaka kumuamini

    kijinga. Nikatulia kumwangalia ni nini anachotaka kukifanya

    au kunifanyia.



    "Habari yako bwana Musa Njiwa?" Aliniuliza kwa kulitamka

    jina langu kwa ufasaha huku akitabasamu kipombe pombe.



    "Najisikia vyema kidogo" nilijibu kwa upole katika sauti ya

    utata ambayo isingemfanya ajue hali yangu kwa uhakika.



    "Pole sana, ulijigonga tu kichwani lakini bahati nzuri

    hukuumia kwa ndani" alinijibu akiniangalia kwa huruma.



    Nilitamani kumuuliza kuhusu hali ya Tausi lakini nilisita

    kwa sababu ya yule bwege pembeni yangu, sikumjua alikuwa

    pale kwa sababu gani. Pia sikutaka kumuuliza daktari kuwa

    lile jamaa ni nani na linafanya nini pembeni ya kitanda

    changu na ni kwa nini hakumsalimia hata daktari.



    Daktari akaondoka bila kunigusa wala kuongea lolote la

    maana. Alipofika mlangoni alisimama kidogo, aliingia kiumbe.

    Kisha yule daktari akaondoka zake baada ya wawili hao

    kusalimiana kwa uchangamfu. Jua tu kuwa kiliingia kiumbe!



    Alikuwa ni dada mrefu, mwenye sura nyembamba lakini alikuwa

    na figa la kufa mtu, japo hakuwa mnene sana. Yaani kwa wale

    wagonjwa wa mifiga ya kuchorwa vitabuni pale wangeweza

    kuhonga hadi roho, manake mali tu zisingetosha kuwaridhisha

    kama wamehonga. Alikuwa amevaa suti ya sketi fupi,



    iliyoonyesha ni kwa namna gani kiumbe huyu amejaaliwa miguu.

    Kifupi tu ni kuwa hakuna fundi wa mahesabu kama Mwenyezi

    Mungu. Yaani kama binadamu mwili wake unapigwa kwa mahesabu

    hapa vifaa vyote vya kupigia mahesabu vilikamilika, vibikari

    bikari, rula bila kusahau kikokotozi cha kisayansi!



    Alipofika tu yule, jinamizi aliyekaa pembeni yangu aliinuka

    na kusimama mbali kidogo na kukipisha kiumbe kikae karibu

    yangu. Sijui alikuwa akinifanyia makusudi? Aliingiza mkono

    wake kunishika shingoni kwa karibu na kifua, sasa sijui

    alikuwa ananipima joto tu au wazimu wake? Labda alitaka

    nihisi mikono yake ilivyo laini.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Pamoja na yote lakini bado akili yangu ilitaka kujua alipo

    Tausi na hali yake. "Yule msichana niliyepata naye ajali ana

    hali gani?" Nilimuuliza bila kumsalimia wala kutaka kumjua

    kuwa ye ni nani.



    "Tausi binti Nurdin?" Aliniuliza swali ambalo lilizidi

    kunichanganya. Kwa swali aliloniuliza, na kutokana na uzoefu

    wa kazi yangu, pamoja na ujuzi nilionao sikuwa na shaka kuwa

    jibu atakalolitoa halingekuwa na ukweli wowote.



    Niliamua kutotilia maanani jibu lenyewe, lakini kutokana na

    jibu lenyewe ningeweza kuhisi kuwa wale ni kina nani na wana

    lengo gani. Baada ya kujishaua shaua pale alipokaa huku

    akijifanya kuwa ana huzuni sana, aliniangalia mithili ya

    atafutaye namna ya kuongea.



    Nilipomwangalia machoni nilijua wazi kuwa anajifanyisha,

    aliniwekea ’uso wa plastiki’ huzuni ile haikuwa ya kutoka

    moyoni. Akanieleza jibu nililolitarajia, "Tausi tumempoteza,

    pole sana"



    Japo nilitambua kuwa halikuwa jibu la ukweli, lakini mapigo

    ya moyo yaliongezeka na nikajihisi kutetemeka mwili mzima

    nikijiuliza, "vipi kama itakuwa ni kweli?"



    Nilitaka kuwaridhisha na pia kujua hasa ni nini lengo lao,

    hivyo baada ya kuniambia habari hiyo nikapiga ukelele kisha

    nikafumba macho kujifanya nimepoteza fahamu.



    Nikaanza kuzisikia pilika pilika zao, wakimkimbilia daktari.

    Yule kiumbe ambaye nilikuja kulijua jina lake baadae, kuwa

    ni Yolanda akawa akijitetea. "Mi nimemwambia tu yale maneno

    ndio ikawa hivi" alirudia rudia sentensi hiyo mara nyingi,

    hivyo ikanihakikishia kuwa taarifa aliyonipa haikuwa sahihi.



    Ina maanisha kuwa alitumwa tu kuniambia maneno na sio kunipa

    taarifa ya msiba wa Tausi. Moyoni nilifarijika kugundua kuwa

    taarifa zile hazikuwa za kweli. Daktari aliwaambia waniache

    kwanza kwa muda, hiyo ilikuwa ni nafasi nzuri ya kutafakari

    kuhusu hatua za kuchukua.



    Ila nilibaki na wasiwasi mmoja, wale ni akina nani na

    wametumwa na nani? Pia nilikuwa na hamu ya kujua alipo

    Tausi. Nilimsikia Yolanda akiaga, nikasikia pia miguu

    mingine ikitoka. Nilijua wazi kuwa wametoka wawili bado

    mmoja yupo na bila shaka ni yule jamaa.



    Muda ulipopita sana nikafumbua macho, nikaliona lile jamaa

    linazunguka zunguka huku limenipa mgongo. Nilijikohoza kama

    nimepaliwa na mate ili ajue kuwa nimezinduka.



    Jamaa liliruka ile mbaya likanigeukia, likichomoa bastola

    yake kisha likawa limeishika mkononi kwa nguvu. Akabaki

    kuniangalia huku akiwa katika taharuki, kwa hesabu za haraka

    haraka nikagundua kuwa kuna jambo moja kati ya mawili. Labda

    huyu jamaa ni mwoga sana au alipewa sifa zangu.



    Nilimaliza kujikohoza nikatulia pale kitandani, akaniangalia

    kwa muda kisha akaenda kujiegemeza kwenye kona fulani

    akiichezea bastola yake mkononi.



    Nikajua alikuwa anamaanisha nini. Ile ni ishara ya kuniambia

    kuwa nitulie vile vile kwa kuwa yeye alichoamriwa ni

    kuitumia bastola yake kwa lolote litakaloenda tofauti na

    mpango uliopangwa.



    Nikalihisi jasho jembamba likinichuruzika. Baada ya muda

    mchache nililetewa chakula, ulikuwa ni mkate mkavu na soda,

    fanta. Nilichekea moyoni kwa kuwa mlo ule ulinikumbusha

    wakati nikiwa sekondari.



    Ila nilielewa maana ya mlo ule, aliyekileta alikuwa anataka

    kunihakikishia kuwa natakiwa bado niendelee kuishi. Alijua

    kuwa angeleta kilichopikwa ningesita kula kwa kuhofia sumu.



    Ila pia nilijua wazi kuwa kulikuwa na uwezekano wa kuweka

    sumu ndani ya soda au kwenye mkate. Kitu ambacho kilinipa

    moyo ni kuwa pale niko chini ya himaya yao hivyo hawana

    sababu ya kuniwekea sumu kama kweli walikuwa na nia ya

    kuniua.



    Baadaye waliingia watu watatu walioonekana kuwa wameingia

    kishari haswa. Yule jamaa aliyekuwa mule ndani alijiweka

    sawasawa na bastola yake mkononi.



    Nilikula haswa kwa kuwa njaa ilikuwa ikinitandika ila

    sikutaka kuwaeleza watu wale nisiojua lengo lao. Nikabaki

    pale kitandani nimejilaza, sikuweza kufanya ujanja wowote

    kwa kuwa bado nilihisi maumivu mwilini pia sikujua pale

    nilikuwa wapi na kulikuwa na ulinzi wa aina gani.



    Nilitumia muda mwingi kujiuliza kuwa wale wametumwa na nani

    japo kutokana na taarifa za kuhusu kifo cha Tausi nikahisi

    kuwa wana lengo la kuniachanisha na Tausi.



    Baadaye waliingia watu watatu walioonekana kuwa wameingia

    kishari haswa. Yule jamaa aliyekuwa mule ndani alijiweka

    sawasawa na bastola yake mkononi.



    Nilipomsoma yule jamaa mwenye bastola nikajua kuwa alikuwa

    na taarifa ya ujio ule kwa kuwa hakuonyesha mshtuko wowote

    wale jamaa walipoingia. Walinivamia pale kitandani

    walinikamata kwa nguvu, mmoja akinibana miguu huku mwingine

    akinishindilia sehemu ya kifuani.



    Sikutumia nguvu yeyote kuwazuia. Sio kwamba sikuwa na uwezo

    wa kushindana nao bali matumizi ya nguvu katika sehemu kama

    ile hayakuwa na tija, sana sana ningesababisha waniumize.

    Walipoona sishindani nao wakajilegeza, ila ghafla mmojawapo

    akatoa sindano na kunichoma.



    Nikaona kiza kinene kisha nikapoteza fahamu. Sikukumbuka

    tena kilichoendelea baada ya kuchomwa sindano ile.



    Nilipokuja kuzinduka nilijikuta katika chumba chenye mwanga

    hafifu, na pindi macho yalipozoea nikawa naona kila kitu kwa

    ufasaha. Nilikuwa katika sehemu ambayo naifahamu fika na

    nimeizoea. Kila ambacho nilikuwa nakiona kilikuwa vile vile

    nnavyokijua.



    Nilichanganyikiwa na mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi,

    sikujua hasa ni nini kilikuwa kikiendelea. Pamoja na uzoefu

    wangu katika kazi ya upelelezi hali ile ilikuwa inanitatiza,

    na sikuweza kujua haswa ni nani aliyekuwa nyuma ya yale

    niliyokuwa nikifanyiwa.



    Lakini niliamini kuwa aliyekuwa akinifanyia vile hakuwa na

    lengo zuri juu yangu na alikuwa ni mtu aliyenifuatilia kwa

    muda mrefu na sasa niko chini ya himaya yake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakuna kitu ambacho kinaniudhi kama mtu kuniendesha kwa

    rimoti kontroo! Nilikuwa nyumbani kwangu, tena katika chumba

    changu cha kulala. Nilikurupuka na kukagua sehemu zote mule

    ndani.



    Hakukuwa na chochote kilichoguswa kwa maana hiyo ni kwamba

    nyumba yangu haikuwa imefanyiwa upekuzi wa aina yeyote.

    Kilichofuata ni kwenda kwenye simu na kuangalia rekodi mbali

    mbali.



    Nikakuta Mkuu amenitafuta sana katika kipindi ambacho

    nilikuwa kule nisikokujua bado kama ilikuwa ni hospitali ama

    nyumbani kwa mtu.



    Mara ya kwanza nilitaka kuamini kuwa Mkuu alinitafuta kweli

    lakini kichwani mwangu kuna kitu kilikataa. Kilichonifanya

    nisite kuamini ni jambo kuwa, Mkuu alinitafuta tu katika

    kipindi ambacho sikuwepo.



    Hii iliniashiria kuwa alijua nilipo na pia alijua

    kilichokuwa kikiendelea. Nikaanza kukumbuka mambo mbali

    mbali, kuhusu mkuu na maswali aliyokuwa akiniuliza hasa

    baada ya utekwaji nyara wa Tausi.



    Picha ikaja wazi kuwa haya yote yaliyonitokea yana mkono wa

    Mkuu, ila ambalo bado lilinitatiza ni kujua sababu hasa ya

    Mkuu kunifanyia vile.



    Muda ulipita wa takribani saa sita, nikapokea simu toka kwa

    Mkuu. Mkuu alinipa pole kwa ajali iliyotokea na akanieleza

    wazi kuwa ni yeye aliyetuma watu wanitibie na kunirudisha

    nyumbani. Alidai kuwa sababu kubwa ya kufanya hivyo ni

    kunilinda.



    Eti kwa kuwa kesi ya kumteka Tausi ilikuwa iko polisi

    aliniepusha kuhusishwa na hivyo kunifanya nichafue faili

    langu. Sikujua kama alikuwa ananiambia ukweli ama alikuwa

    akitaka tu kunifariji kwa kuniweka roho juu juu kwa muda

    mrefu.



    Mwisho aliongea neno ambalo kwa kweli lilinikera. Kama neno

    hilo lingetoka kwa mtu nisiyemheshimu, jibu lake lingekuwa

    ni tusi la nguoni. Mkuu alinipa pole kwa kufiwa na Tausi,

    eti anajua ya kuwa nilimpenda ila Mungu alimpenda zaidi.



    Nilijikaza sana kumuitikia, sio tu nilijikaza kwa kuwa

    namheshimu bali nilijikaza ili nimfanye aone ya kuwa

    nimeamini kuhusu kifo cha Tausi.



    Baada ya propaganda za Mkuu, niliamua kwenda ufukweni kukaa.

    Sikuweza kuendelea kukaa mule ndani kutokana na kupata hisia

    za Tausi kila mara. Niliazimia kumtafuta Tausi kwa udi na

    uvumba hadi nimpate, lakini sikutaka kufanya papara.

    Nilitaka wote waamini kwanza kama nalia msiba.



    Nikaenda kujilaza ufukweni baada ya kutandika kagodoro

    kangu, punde nikawa nimepitiwa na usingizi na mawazo

    niliyokuwa nayo yakawa yakiendelea kwa njia ya ndoto.

    Nilipata picha nzuri za Tausi ndotoni tena alikuwa amelala

    kifuani kwangu tukipanga maisha.



    Tena tulikuwa tukipanga kuondoka nje ya nchi ili kuondoa

    gozi gozi. Nilihisi mipapaso ya Tausi. Lakini kadiri muda

    ulivyokuwa ukienda mipapaso hiyo ilikuwa ikihisika

    kiuhalisia. Nikashtuka!



    Kuangalia pembeni yangu alikuwa mtu, mwanamke mwenye

    mipapaso ile niliyodhania kuwa ni ya ndotoni. Lakini hakuwa

    Tausi. Na maeneo yake nilikuwa peke yangu, nikajua sasa ni

    mambo yale yale ya mpenzi jini! Nikainua uso kumtazama.

    Alikuwa Yolanda, yule binti mwenye figa iliyofigika!



    Nikakurupuka na kukaa chini, akabaki ananiangalia huku

    akitabasamu. "Umeshtuka?" aliuliza swali ambalo jibu lake

    aliliona kwa macho yake. Sikumjibu chochote.



    Sio tu kwamba sikumjibu chochote kwa sababu jibu analo bali

    kuna kingine cha ziada! Sijui alivaaje yule binti! Jamani

    wakina dada wengine ni wachokozi, huwezi kuamini.

    Si unakumbuka nilikudokeza kuhusu figa yake? Bali alikuwa

    amenivalia kiufukweni ufukweni, japo alipendeza sana lakini

    zaidi alikuwa anatamanisha.



    Nikajikuta nikimuomba baba aliye mbinguni aniepushe na

    kikombe kile ila siyo kwa mapenzi yangu bali nilitaka

    mapenzi yake yatimizwe. Nikajikuta akili inanizunguka

    zunguka kama saa mbovu, mara inatembea, mara inasimama.



    "Unanitakia nini mwali wewe?" nilijikuta nikimuuliza kizee

    zee.



    Alibakia akicheka bila kutoa jibu la uhakika. Nikajikuta

    nikimuuliza tena swali ambalo hata mwenyewe nilikuja

    kujistukia baadae kuwa lilikuwa ni la kibwege. Eti

    nilimuuliza amefikaje pale. Yaani ni kama vile nilikuwa naye

    sehemu kisha nikamtoroka!



    Mwisho nikaamua kukaa kimya ili akili ikae kwenye mzunguko

    wake wa kawaida maana nilijiona kuwa nazidi kuchemka. Baada

    ya muda kidogo kupita, akanieleza sababu ya yeye kuwa pale.

    Kwa haraka haraka sikuweza kujua Mkuu ananitakia nini?



    Eti yule binti ndio kateuliwa ili awe msaidizi wangu na

    kaamriwa aje kunisaidia pale nyumbani hadi nitakapopona

    vizuri.



    Yolanda kumbe ni askari mpya ambaye yuko katika hatua za

    mwisho za mafunzo ya upelelezi, na kutokana na alivyo

    anaandaliwa kwa ajili ya kupewa kazi maalum.



    Najua lengo la Mkuu sio kwamba mimi nianzishe uhusiano wa

    kimapenzi na binti huyu bali anafikiri kuwa nimeathirika

    kisaikolojia kwa ajili ya Tausi.



    Nikatupa tena jicho kumtazama Yolanda, nikajikuta

    nikimuamrisha. "Twende kwanza nyumbani."



    Yolanda alinitazama kwa jicho la kurembua, kisha akajiinua

    taratibu tukaanza kuondoka kuelekea nyumbani kwangu ambapo

    ni hatua chache toka pale ufuweni nilipojilaza.



    Tukaongozana kimya kimya huku akili yangu ikiwa haijui

    inafikiria kitu gani. Tukafika kwangu, nilikuwa mbele ya

    Yolanda. Wakati naelekea mlangoni nilishtushwa na jambo.



    Kulikuwa na mtu amekaa katikati ya bustani iliyoizunguka

    nyumba yangu. Alikuwa ni mgeni machoni pangu lakini

    hakuonyesha kama yuko kishari au kiheri, alikuwa yupo yupo

    tu haeleweki.



    Wakati nikimshangaa, Yolanda alikurupuka na kumkimbilia.

    Jamaa akasimama kumpokea, na kilichofuata ni mmiminiko wa

    mabusu mithili ya waigizaji wa filamu za wamarekani weusi.

    Nikabaki nawashangaa.



    Kimsingi nilikereka. Sikukereka kwa sababu wanayafurahia

    mapenzi yao, bali ilikuwa kama wananikoga kwa kuwa niko

    mpweke bila Tausi.



    Yolanda akanigeukia, "bosi huyu anaitwa Jovin, ni boifrendi

    wangu. Yeye anakujua". Nikamkenulia meno kumuonyesha

    tabasamu feki, ’la kichina’, lakini laiti angujua moyoni

    nimekereka namna gani, asingethubutu kunijibu kwa kukenua

    meno yake.



    "Kwa hiyo bosi mi naomba niende, nitaripoti kesho asubuhi"

    aliniaga Yolanda utafikiri mi ndiyo nilimpa kazi ya kuja

    pale kwangu kuleta gozi gozi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Nadhani usije tena, nahitaji kuwa peke yangu kwa siku mbili

    tatu ili nipate muda wa kutafakari mambo yangu" nilimwambia

    kikauzu kauzu mbele ya bwana ’ake.



    "Samahani bosi, mkuu aliniambia nisiache kuja hata siku moja

    hadi pale atakaponipa maagizo mengine." Alitoa maelekezo

    utadhani nilitaka kuyajua yote hayo.



    Usiku wa siku hiyo sikupata usingizi kabisa kutokana na

    panga pangua iliyokuwa ikiendelea kichwani mwangu. Yote

    ilikuwa ni katika mpango wa kumrudisha Tausi kwenye himaya

    yangu. Ilipofika saa kumi alfajiri, kausingizi katamu kakanipitia.





    Saa nne kasoro dakika chache usingizi ulikatika.

    Nikakurupuka na kuingia bafuni, kisha nikajiandaa fasta

    fasta kwa ajili ya kutoka japo sikujua nataka kuelekea wapi.

    Nilipotoka kitu cha kwanza kukiona ni mapaja ya Yolanda.



    Alikuwa kajilaza kwenye kochi dogo lililo nje ya nyumba

    yangu kainyanyua miguu juu kiasi cha kuifanya sketi yake

    ipande.



    Kwanza nilidhani amepitiwa na usingizi hadi niliposogea

    karibu yake, alikuwa akiniangalia akitapasamu. Kwa tabia

    zetu wanaume ningeweza kubadili mawazo pale pale na kuanza

    kuchombeza, lakini kutokana na weledi wangu nilijua kuwa

    anataka kucheza na akili yangu.



    "Natoka, na unisubiri hapa hapa" nilimwambia nikichomoka

    haraka haraka kuongozea njia ya kuondokea bila gari. Kabla

    hajajiinua pale chini nikawa nimeshatoweka. Nikaenda

    kujibanza sehemu.



    Baada ya dakika kama mbili tatu, nikamuona Yolanda akipita

    kwa kasi. Alipopita tu, nikarudi nyumbani haraka, nikabadili

    nguo kisha nikajilaza kitandani nikiendelea kupanga mikakati

    ya kumrudisha Tausi wangu.



    Yalipita takribani masaa saba ya utulivu. Ghafla nikasikia

    pilika pilika za miguu zikiingia nyumbani kwangu, nikafunua

    dari nikadandia na kuingia humo. Mara miguu ikaingia

    chumbani kwangu.



    "Jamani huyu Musa ana nini?" aliuliza mtu mmoja huku wenzake

    wakikaa kimya bila kumjibu. Baada ya kuridhika na upekuzi

    wao wakaondoka huku wakishauriana kwa kunong’ona.

    Nikateremka na kurudi kitandani.



    Ilipofika moja kasoro, giza likianza kuingia nikawa nasikia

    sauti kwa mbali kama mtu anayelia. Nikatoka nje kwa

    tahadhari kubwa, nikamkuta Yolanda kajiinamia akilia.

    Nikamuangalia kwa muda.



    "We binti!" nilimuita kwa sauti ya upole. Yolanda alishtuka

    sana akageuka kuniangalia.



    "Pole, nilikuwa nakukuza katika kazi yako" Yolanda

    akakurupuka na kunikumbatia kwa muda, akilia.



    "Wameniambia kuwa nisingekupata wangenipa adhabu na

    ingenichafulia faili langu. Nashukuru umerudi, ulikuwa

    wapi?" aliniuliza akiwa kama aliyepagawa.



    Nilimruhusu aende baada ya kuongea naye kwa muda nikimueleza

    kuhusu masuala ya kazi na namna ya kukabiliana na hali kama

    ile. Tuliongea mengi kwa kuwa nilishayakomesha maigizo yake

    ya kujifanya kahaba, ’kujikahabisha’.



    Zilipita siku kadhaa za kuelewana na Yolanda, sasa tulikuwa

    kama mtu na kaka yake. Heshima ilichukua mkondo wake,

    nikatumia siku hizo kumuelezea namna Tausi alivyo na nafasi

    katika maisha yangu.



    Alinionea huruma sana, lakini hakuwa na namna ya kunisaidia

    kwa kuwa kumbe hata Tausi mwenyewe hamjui. Alikuwa

    akishindiliwa maneno tu ya kuropoka naye akawa anayatoa kama

    kasuku.



    Kutokana na mazoea yangu na Yolanda na kwa sababu niliamua

    kumsaidia katika kumuimarisha katika kazi hii ngeni kwake,

    akawa ananisaidia kutafuta taarifa za Tausi. Na hata

    nilipokuwa natoka kufuatilia baadhi ya taarifa kuhusu Tausi,

    hakuwa akinitilia umbeya.



    Baada ya siku kadhaa, nikawa nimepata taarifa kuwa Tausi

    alikatiwa tiketi ya kuelekea Ujerumani kupitia Kenya, lakini

    nilipofuatilia nikapewa taarifa kuwa alipofika Kenya alirudi

    Tanzania kupitia njia ya barabara akitumia jina la bandia.



    Hatimaye kwa kuunganisha unganisha taarifa mpya na zile

    nilizozipata kwa Mzee Nurdin nikagundua kuwa Tausi atakuwa

    kati ya miji ya Kilosa au Iringa. Huko ndiko kuna nyumba za

    kisasa zaidi za Mzee Nurdin ambazo hata mwenyewe huzitumia

    kwa mapumziko.



    "Lazima nifunge safari nikamtafute" nilimwambia Yolanda

    jioni moja tukiwa pale nyumbani kwangu. Yolanda aliniambia

    ugumu wa mimi kuondoka pale nyumbani kutokana na amri

    iliyotolewa na Mkuu.



    "Huwezi kwenda popote Musa Njiwa. Ni amri!" alinijibu Mkuu

    baada ya kumvaa kuomba ruhusa ili nisafiri kwa mapumziko

    mafupi japo moyoni nilijua ninapotaka kwenda.



    Kwa mara ya kwanza nikaiona kazi ya upelelezi ni kazi ya

    kitumwa, na sikuweza kuvumilia tena kuishi katika hali ile.

    Nikafanya uamuzi ambao hakuna aliyeutegemea.



    Niliandika barua ya kuacha kazi kwa masaa ishirini na nne,

    nikalipa na mshahara wa mwezi mmoja. Toka hapo vikaanza

    vikao mfululizo kujadili kuhusu uamuzi wangu huo.



    Baada ya kukabidhi kila kitu nikarudi nyumbani kwangu na

    kujiandaa kwa safari. Ghafla gari mbili zikawasili nyumbani

    kwangu, nikachukuliwa msobe msobe nikaenda kutupwa rumande.

    Niliwekwa ndani kwa takribani siku saba nikitolewa kwa

    vipindi tofauti kwa mahojiano, lakini haikusaidia kitu.



    Katika kipindi chote hicho kwa msaada wa Yolanda, ofisini

    walijua kuwa nishaachana na habari za Tausi.



    Siku niliyotolewa rumande, niliambiwa na wasaidizi wa Mkuu

    kuwa naruhusiwa kusafiri kwa siku zisizozidi saba lakini

    niliwajibu kuwa sisafiri kokote na hatanikisafiri sitahitaji

    ruhusa ya mtu yeyote kwa kuwa nimeshaacha kazi.



    Mkuu alipofikishiwa taarifa, aliwaambia waniache nifanye

    ninavyotaka kwa muda fulani ila waangalie mienendo yangu.

    Kama kawaida umbeya ukanifikia kupitia kwa Yolanda. Ilikuwa

    rahisi kwa Yolanda kupata taarifa kutokana na urembo wake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya siku kama nane za kufanya mazoezi ya nguvu,

    nilijifunga kwa safari. Kwanza nilitengeneza utaratibu

    fulani ambao uliwarahisishia wanaonifuatilia, niliwataka

    wajue naamka saa ngapi naelekea wapi na usiku nalala saa

    ngapi.



    Siku niliyosafiri niliingia kulala kama kawaida, ilipofika

    saa nane za usiku nikafungua dirisha langu ambalo huwa

    nalitumia kama mlango wa dharura. Nikatoka na kulifunga.



    Nilipita njia ambayo niliibuni kwa ajili ya kuitumia kwa

    safari za dharura ambazo sikutaka yeyote ajue. Nikatokea

    barabarani na kuianza safari yangu nikianzia na Kilosa.



    Usiku mmoja tu ulitosha kujua kuwa Tausi hakuwepo katika mji

    ule. Alfajiri nikasafiri hadi Mikumi ambapo nilidandia lori

    mpaka njia panda ya kwenda Iringa mjini. Nikakaa pale hadi

    usiku, nikakodi taxi hadi mjini.



    Ilikuwa yapata saa nne za usiku wakati napita maeneo ya

    stendi kuelekea Makanyagio. Taxi likaniacha karibia na geti

    la Chuo Kikuu kishiriki cha Ualimu Mkwawa. Lengo lilikuwa ni

    kumfanya dereva ahisi kuwa mimi ni mwanachuo.



    Ilinichukua takribani masaa kumi na nane kuitambua nyumba ya

    Mzee Nurdin sehemu za Kihesa. Kwanza niliihisi nyumba fulani

    iliyoko katika mlima wa Wilolese, ikanipotezea karibia masaa

    mawili kabla sijagundua kuwa sio yenyewe.



    Baada ya kuhakikisha kuwa nyumba niliyoihisi ndiyo ya Mzee

    Nurdin nikaanza kupeleleza mambo kadhaa ya msingi. Baada ya

    kupata kila nilichokihitaji, niliondoka ili nikajipange.



    Nilichukua chumba katika gesti moja ya uchochoroni sana

    ambako ni mwenyeji tu anayeweza kupajua. Nikatumia muda

    mrefu kulala kisha nikaamka na kuanza maandalizi nikijiweka

    tayari kwa lolote.



    Niliporidhika na maandalizi, nikaanza safari ya kwenda kwa

    Tausi. Baada ya dakika kama kumi na mbili hivi nikawa mbele

    ya nyumba ya Mzee Nurdin. Nikawaona walinzi wawili wakiwa

    getini.



    Nikaizunguka nyumba, nikaruka ukuta kuingia ndani. Nikatulia

    kwa muda kisha nikatambaa hadi nikaufikia mlango wa uwani,

    nikauchokonoa ukafunguka, nikaingia na kuurudishia.



    Nikatulia kimya kwa muda kusoma mizunguko ya mule ndani.

    Ilionekana kuwa kuna watu wasiozidi watatu akiwemo Tausi

    mwenyewe na wote walikuwa ni wanawake. Nikanyata taratibu na

    kuingia chumba kimojawapo nikaacha barua niliyoianda, juu ya

    bahasha nikaandika jina la Tausi.



    Nikatoka taratibu nikaondoka zangu. Katika barua ile

    nilimjuza kuwa nipo katika mji ule kwa ajili ya kumfuata

    yeye. Nikamuelekeza nilipofikia, japo nilimdanganya lakini

    angekuja angenikuta.



    Baada ya masaa kama mawili, lilifika gari moja lenye namba

    za serikali. Wakashuka jamaa wawili waliovalia suti nadhifu,

    wakaingia ndani kisha wakatoka baada ya dakika kama kumi

    hivi wakiongozana na Tausi na mlinzi mmoja.



    Wakaingia ndani ya gari kisha gari likaondoka. Nikaanza

    kulifuatilia kwa nyumba nikitumia taxi nililokodi.



    Mwisho wa safari ya gari la kina Tausi ilikuwa pale

    nilipomwelekeza. Walitangulia kuteremka mlinzi na mmojawapo

    wa wale jamaa wakaenda kukaa sehemu ya baa ya ile hoteli

    niliyomwelekeza, kisha akateremka Tausi.



    Nikaliruhusu taxi liondoke, nikaandaa ujumbe mwingine haraka

    na kuuweka katika bahasha. Wakati huo Tausi alikuwa

    akielekea mapokezi ya hoteli ile, akaulizia akaambiwa kuwa

    ni kweli nimechukua chumba pale ila nimetoka.



    Tausi akatafuta sehemu ya kunisubiria akaenda kukaa. Nikampa

    mtu ampelekee mhudumu mmoja aliyeko mapokezi kisha nikatuli

    a sehemu nikiangalia mchezo.



    Yule mhudumu alielewa maagizo akampelekea Tausi moja kwa

    moja. Nikaondoka baada ya kuona Tausi anakabidhiwa ile

    bahasha na anaifungua. Niliandika..



    ’Mpenzi Tausi, nimefurahi kwa kuwa nimekuona tena ukiwa na

    afya njema. Ila nimefurahi zaidi kwa kuwa umeitikia mwito

    wangu japo msafara uliokuja nao sikuupenda. Sina na wala

    sijawahi kuwa na nia ya kukudhuru, huna sababu ya kuniwekea

    mitego. Nakupenda sana’



    Sijui alifanyaje lakini baada ya kuupata ule ujumbe.

    Nilitoka pale haraka haraka nikarudi nyumbani kwa Tausi,

    nikaingia ndani. Nikakagua vyumba vyote wakati huo wale

    watumishi walikuwa sebuleni wakiangalia TV.





    Kitu ambacho nilikisoma na kikawa kikiniumiza kichwa ni

    kuwa, Tausi anaonekana yuko tofauti mno. Yaani muonekano

    wake ni kama wa mwanamke aliyekuwa anamuamini mumewe kisha akamfumania, tena na shoga yake.



    Nilikigundua chumba cha Tausi mule ndani, nikaingia na

    kutulia kimya mule ndani. Harufu ya mule ndani ilirudisha

    kumbukumbu zangu mbali mno, nilikumbuka siku za mapenzi

    yangu na Tausi. Nikajikuta nasinzia.



    Mlio wa gari ulisikika nje, kisha pilika pilika za watu

    zikaendelea kwa muda. Baada ya hali kutulia, mlango wa

    chumbani kwa Tausi ulifunguliwa.



    Niliruka na kujibanza sehemu. Tausi akaingia na kuufunga

    mlango kwa ndani. Alionekana kuwa na wasiwasi sana,

    akajitupa kitandani kukaa. Nikajitokeza na kuwahi kumziba

    mdomo ili asije akapiga kelele kwa woga.



    Tulibaki tunaangaliana kwa muda, ila kwa mitazamo tofauti.

    Tausi alionekana kuniangalia kwa chuki ya hali ya juu

    tofauti na mimi niliyekuwa nikimwangalia kwa mapenzi.



    "Kuna nini mpenzi wangu?" niliufunua mdomo wangu na kuuliza kwa sauti ya upole. Tausi alibaki kimya akiniangalia huku machozi yakianza kumtiririka. Nilimsogelea na kukaa karibu yake.



    "Kaa mbali na mimi tafadhali. Sipendi kujihusisha chochote

    na wewe, nakuchukia Musa," alitamka maneno ambayo yaliuchoma moyo wangu hasa. Nilikaa kimya kwa muda nikiyatafakari maneno yale ambayo kwa

    hakika yalionekana kumtoka moyoni.



    "Sumu gani umelishwa mpenzi wangu?" niliufungua mdomo hatimaye.



    "Sikiliza Musa, najua kama ulikuwa pale kumpeleleza baba

    yangu na ulianzisha uhusiano na mimi ili upate urahisi wa

    kutimiza kazi yako, bahati mbaya ukanogewa na mimi. Kazi

    yako imeisha unanifuatia nini? Ukipata kazi nyingine,

    utapata mwanamke mwingine." aliongea huku akitokwa na

    machozi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Ni kweli nilikuwa nikimpeleleza baba yako. Na ni kwa sababu

    anahusika na usafirishaji wa watoto nje ya nchi, watoto

    ambao wanaenda kutumikishwa kitumwa na wengine kuuliwa na kuchukuliwa viungo vyao kwa ajili ya matibabu ya matajiri.

    Kwa hilo hata ningeamriwa nimpige risasi baba yako

    Ningemuua," nilimwambia kwa sauti ya kumaanisha.



    Niliendelea kumwambia, "bahati mbaya niliangukia penzini

    kwako nikiwa kazini. Nilijitahidi kupuuza hisia zangu lakini

    nilishindwa na hadi leo nashindwa kuzipuuza hisia zangu

    ndiyo maana niko hapa. Nakupenda sana Tausi na nahitaji

    nimalize maisha yangu na wewe."



    "Kwa kifupi fanya kama hakijawahi kutokea kitu kati yetu na

    nataka uondoke sasa hivi kama ulivyoingia. Neno lolote

    utakaloongeza nitapiga kelele, na usidhani kuwa natania"

    aliongea kwa sauti ya upole iliyojaa chuki akiwa

    haniangalii.



    Nilimwangalia binti yule mrembo kwa muda, akageuka

    kuniangalia, moyo wangu ulikuwa unalia lakini tabasamu

    lilikuwa halijafutika usoni. Nikajiinua taratibu na kuanza

    kuondoka bila kusema neno.



    Siku hiyo ilikuwa ngumu sana kwangu. Nilirudi nilipofikia

    kama nimetoka msibani, tena kwenye msiba wa mtu anayenihusu kwa karibu. Usiku huo huo wa siku hiyo ndipo nilienda kumrushia maneno Tausi.



    *********



    Nilikaa, nikatafakari kwa muda mrefu. Nikaamua kusafiri

    kuelekea sehemu yenye utulivu ili niweze kupata akili mpya,

    niweze kujitafuta.



    Nilichagua kwenda Kilwa ambako nilikaa kwa takribani wiki

    tatu. Iliniwia vigumu kuweza kumsahau Tausi lakini hatimaye

    nilimchukulia kama historia.



    Nilirudi jijini Dar es Salaam nikiwa mpya kabisa. Sikutaka

    tena kuendelea na kazi lakini kichwa changu kilikuwa

    kimetulia tayari kwa majadiliano yeyote.



    Niliporudi nikaripoti makao makuu ili kujua hatma ya barua

    yangu, lakini nilichokikuta pale kilinistaajabisha. Nilikuta

    barua ya likizo ya miezi sita, mshahara niliolipia notisi,

    na malipo mbalimbali yanayoambatana na likizo.



    Kwa kweli sikuweza hata kujaribu kupinga, nilijua kuwa

    endapo ningeleta ubishi wowote ningeonekana mkorofi na hatua

    zozote za kinidhamu ambazo zingechukuliwa dhidi yangu

    zingekuwa sahihi.



    Upweke ndugu yangu,upweke! Nilianza kuhisi upweke wa hali ya juu, nikaamua kutafuta binti wa kuniondoa upweke ikiwezekana kuoa kabisa japo kutokana na majukumu ya kazi yangu ilibidi nimpate mke ambaye ni mwelewa hasa.



    Yolanda?! Hapana. Pamoja na urembo wake wote lakini Yolanda hakuwa ananivutia kimapenzi, sijui ni kwa nini. Ila nahisi kwamba ana tabia feki, hayuko halisia na mimi na wanawake ‘waigizaji’ ni vitu viwili tofauti.



    Nilianza kupanga orodha ya wasichana ambao nimewahi kuwa nan uhusiano nao, nikaanza kuwahakiki mmoja baada ya mwingine.



    Nikajikuta kama Marehemu John Mgema na wimbo wake wa

    wachumba thelethini.



    "Nimeamua kuwa mpya, nataka mahusiano mapya" nilihitimisha na kuanza kujiandaa kutoka. Nilipanga kutembelea sehemu mbalimbali na kujichanganya na watu ili nizidishe fursa za kuanzisha uhusiano mpya.



    Baada ya miezi kama miwili hivi ya kutoka na wasichana

    mbalimbali nikajionea upuuzi, nikaamua kuachana ma kwenda

    mbio. Niliamua kuweka akili yangu yote katika hali kufikiria

    masuala ya kiuchumi zaidi.



    Jioni moja nilikuwa ufukweni karibu na nyumba yangu,

    nilikuwa nimejilaza kwenye kigodoro changu cha ufukweni

    nikitafakari mambo yangu. Ilikuwa yapata mwaka mmoja toka

    nilipoamua kuachana na habari za kutafuta mwenza.



    Simu yangu iliita. Alikuwa ni Omar, moja kwa moja nikajua

    kuwa ni kimeo maana urafiki wetu na Omar ni wa kukumbukana

    kwenye vimeo tu.



    Toka siku ile nilipomhadithia kuhusu Tausi, tulikuja kuonana

    siku moja tu makao makuu na hatukupata muda wa kuongea kwa kuwa kila mmoja alikuwa bize na ishu zake. Nikaipokea!



    "Njoo haraka Uwanja wa Ndege" alisema Omar na hapo hapo simu ikakatika. Sikuwa na muda tena wa kupoteza, nilijua kuwa

    Omar yuko kwenye tatizo kubwa kwa kuwa simu yake haikuwa

    ikipatikana tena. Nilikurupuka kujiandaa, baada ya dakika ishirini na tano nilikuwa uwanja wa ndege. Nikaulizia kama kuna tukio lolote lisilo la kawaida, nikaambiwa hakuna.



    Nikaanza kumtafuta Omar kwenye sehemu ambazo nilihisi angekuwepo. Baada ya kuchoka nikakaa sehemu ya kusubiria wageni nikifikiria cha kufanya. Mara nikaguswa begani, kuinua uso nikamwona Omar.



    "Umenitisha sana Omar, kuna nini?" Nilimuuliza kwa shauku

    kubwa.



    "Nina tatizo kubwa sana ndugu yangu, nimepokea mgeni lakini

    nahitaji ukampe hifadhi kwa usiku huu. Wewe ndiyo

    ninaekuamini Musa" alisema Omar akionyesha kweli ni jambo

    linalomtatiza.



    "Ondoa shaka Omar! Yuko wapi?" nilimuuliza kwa kuwa

    sikumuona akiwa na mtu yeyote pembeni.



    "Nimemtanguliza kwako, yuko kwenye chumba cha wageni. Ila

    ukimkuta amepumzika usimuamshe, ameshakula chakula cha

    jioni. Ni mwanamke, na ni ndugu yangu lakini wewe

    nakuamini." alisema Omar akitabasamu.



    Sikumuuliza kuwa aliingiaje kwa kuwa tunajuana michezo yetu

    hivyo hata kama una kitu unataka kukifaya siri unatakiwa

    kukifichia nje ya nyumba, sio ndani. Niliagana na Omar na

    kurejea nyumbani.



    Nilipofika nyumbani, kweli nilikuta dalili za mgeni tena wa

    kike kutokana na marashi yanayonukia. Nilimkuta kajifungia

    ila sikumtilia maanani, niliamini kuwa Omar hakutaka aende

    kwake usiku ule kutokana na vimeo vyake.



    Omar huwa anapenda sana wanawake wasio na adabu, mwenyewe anadai ndio anaokuwa nao huru zaidi. Kwa kifupi anapenda wanawake malaya.



    Nilimpotezea mgeni wa Omar usiku ule, japo kwa vipindi

    fulani nilijihisi mzuka wa kumgongea mlango. Halmashauri ya

    kichwa changu ilikuwa makini katika kuidhibiti tamaa yangu

    ya mwili.



    Ilipofika saa kumi alfajiri niliamka kwa ajili ya mazoezi.

    Kwa kawaida mimi hufanya mazoezi kuanzia muda huo na huwa namaliza mara tu mwanga unapoanza, kwa wale watu wa mazoezi yanayohusisha hisia watakuwa wananielewa zaidi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya kumaliza na kuoga nikawa chumbani nikisikiliza

    muziki kwa mbali huku nikisoma kitabu changu. Nilitoka nje

    kwenye saa mbili hivi, nikaona kitu cha kunishangaza.



    Mezani kulikuwa kumeandaliwa kifungua kichwa na mgeni wa

    Omar. Kabla sijawaza vyema, mgeni alitokea chumbani kwake.

    Nilimtambua na sikujua niwaze nini, alikuwa ni Tausi.



    "Nimefurahi kuwa una heshima kwa wageni, naomba uendelee

    hivyo hivyo" alisema akitabasamu.



    Sikuweza kumjibu wala kusema chochote. Nilidhani kuwa

    nimemsahau na simpendi tena, lakini nilikuwa ninajidanganya.

    Hisia zilirudi ghafla kama mwanzo.



    Baada ya muda nikapata swali la kumuuliza, "umefika au

    unaendelea na safari?"



    "Fungua kwanza kinywa" alinijibu kwa upole ila sikuweza

    kutulia nikaendelea kum’bembeleza aniambie. Akanijibu kuwa

    atakuwa amefika kama bado nafasi yake ipo.



    Nilimnyanyua ghafla na kumuingiza chumbani kwangu ili

    nimuonyeshe nafasi yake ilipo, ila yeye alinisisitiza

    nifungue kinywa kwanza.



    Kumbe operesheni yote ya kunitenganisha na Tausi ilikuwa

    inaendeshwa na Omar kwa amri ya Mkuu, lakini alipoona mambo yametulia ilibidi akamueleze kila kitu Tausi. Ndipo

    wakakubaliana aje.



    Na pia hakukuwa na kikwazo tena kwa kuwa Mzee Nurdin

    alihukumiwa kifungo cha maisha baada ya Rais kukataa kusaini

    hukumu ya kifo.



    Mwisho wa yote nilimkubalia kwa masharti Tausi kuwa

    nitafungua kinywa kwanza lakini nikamwambia nikimaliza

    kufungua kinywa, USIN’BANIE!



    Leo hii yuko mbele yangu, tukijiandaa kufurahia fungate yetu

    baada ya kufunga ndoa takatifu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ***MWISHO***



0 comments:

Post a Comment

Blog