Search This Blog

Sunday 19 June 2022

AHADI YA NDOTONI - 5

 





    Simulizi : Ahadi Ya Ndotoni

    Sehemu Ya Tano (5)





    Baada ya kuoga na kupata chakula, hakuwa na muda wa kupumzika, aliingia madukani kama alivyotuma oda ya vitu. Alikuta vitu vipo tayari, alilipa pesa na kuchukua mizigo yake. Hakutaka kukaa nchini Dubai kwa muda mrefu kama alivyopanga kupumzika kutokana na mauzauza yaliyomtokea. Uwepo wa Lakashi kule ulimfanya aamue kuondoka haraka.



    Akiwa kwenye moja ya maduka makubwa jiji pale, wakati akifanya manunuzi kijana mmoja wa Kiarabu ambaye alionekana si mgeni wa Afrika Mashariki kutokana na kuzungumza Kiswahili safi alimchangamkia sana Lakashina.



    Kutokana na uchangamfu wake, mavazi ya heshima aliyoyavaa na jinsi alivyojiweka alimvutia yule kijana ambaye alikuwa mtoto wa tajiri mkubwa pale Dubai.



    “Samahani dada umeolewa?”



    “Kwa nini unaniuliza swali hilo?”



    “Dada nimekuwa nikikufuatilia muda mrefu toka uanze uteja katika duka letu, umekuwa na tofauti kubwa na wanawake wengi wanaotoka Tanzania. Unajiheshimu pia ni mchangamfu, nimejikuta nikivutiwa na wewe. Mimi Naitwa Abdul Diabi ni mtoto wa mzee Diabi Mansul, tajiri wa hapa Dubai. Maduka makubwa hapa Dubai yenye bidhaa za bei nafuu ni yetu. Pia nilikuwa nina shida ya kufungua duka kubwa nchini Tanzania ambalo litakuwa likisambaza bidhaa zetu kwa bei nafuu.”



    “Nimekusikia japo jibu ulilotoa halikulingana na swali langu, hebu nipe makusudio ya swali lako lililoambatana na maelezo marefu.”



    “Maelezo yangu yote hayo nilitaka kwanza unifahamu kabla ya kueleza kusudio la swali langu kwako.”



    “Haya sema.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Nimetokea kukupenda na kutaka uwe mke wangu kama hujaolewa, lakini kama umeolewa sitakuwa na jinsi zaidi ya kumsifu mumeo kuwa na mke mzuri.”



    “Abdul mbona una Kiswahili kizuri kuliko Waarabu wengi niliokutana nao hapa Dubai?”



    “Ni kweli, mimi ni Mswahili nimezaliwa Tanzania na kusomea Tanzania, baba yangu mzee Diabi Mansul alikuwa na wanawake wanne, watatu walikuwa Dubai na mmoja Tanzania ambaye ni mama yangu.”



    “Kwa nini hamkufungua maduka Tanzania?”



    “Baada ya kifo cha mama yangu, baba alituchukua na kuja kuishi huku mpaka leo, kwa kweli sasa hivi Tanzania ni mgeni kabisa.”



    “Mmh! Pole sana kufiwa na mama.”



    “Asante.”



    “Hata mimi sina baba wala mama.”



    “Ooh! Pole sana walikufa kwenye ajali au kila mtu alikufa na wakati wake?”



    “Kwa ajali ya moto.”



    “Pole sana, sasa nani alikulea?”



    “Nimelelewa na wasamaria wema.”



    “Kwa hiyo nani kwa sasa ni msimamizi wako?”



    “Sina msimamizi, najiongoza mwenyewe kwa uwezo wa Mungu.”



    “Inasikitisha sana, je umeolewa?”



    “Mmh! Hata nashindwa nikujibu nini, naomba unipe muda nikirudi mara ya pili nitakupa jibu.”



    “Subira dhahabu lakini nenda ukijua Abdul ni mgeni wa moyo wako, nipo tayari tuishi sehemu yoyote duniani.”



    “Sawa nimekuelewa, nipe muda nitakupa jibu, kuwa na subira.”



    “Subira ninayo ndiyo maana nilikufuatilia muda mrefu na leo nimeweza kuufungua moyo wangu kwako. Nina imani jibu langu litakuwa zuri.”



    “Nipe muda, ni haraka sana kukujibu.”



    “Kwa kukubali kuzungumza na mimi kwa heshima na utulivu nimeamua nusu ya mzigo ulionunua hapa nitalipa mimi,” Abdul alimpa ofa Lakashina ambayo hakuitegemea.



    Baada ya makubaliano, Lakashina alirudi hotelini kwake. Alipofika mapokezi alishtuliwa na mhudumu.



    “Samahani dada.”



    “Bila samahani.”



    “Yule kaka aliyekulipia chumba alikusubiri sana lakini alipoona unachelewa aliamua kuondoka na kurudisha funguo,” kauli ile ilimshtua sana Lakashina.



    “Alirudisha funguo ina maana alikuwa chumbani kwangu?”



    “Si amesema ni mumeo.”



    “Sasa kama ni mume wangu kwa nini mumpe funguo bila ruhusa yangu? Meneja wa hoteli hii yuko wapi? Siwezi kufanyiwa vitu kama hivi,” Lakashina alikuja juu.



    “Lakini dada si ni wewe ndiye uliyesema ni mumeo.”



    “Sijamuona! Mpaka ningemuona ningejua kama mume wangu kweli.”



    “Basi dada tusamehe, lakini inaonesha ni mtu mwema tena mwenye pesa, pia aliniachia chupa hii ya manukato akasema ukimaliza kula na kuoga kabla ya kujipumzisha ujipulizie.”



    “Mmh! Sawa, hebu nipe.”



    Lakashina aliichukua ile chupa na kwenda chumbani kwake, alipofika chumbani alikuwa na mawazo mengi juu ya Lakashi mumewe kuwepo pale huku akishindwa kuonekana mbele yake zaidi ya kuonekana kwa wahudumu wa hoteli.



    Baada ya kula, alijipulizia manukato yale. Haikuchukua muda, usingizi mzito ukamchukua.



    Lakashina akiwa katikati ya usingizi aliota Lakashi yupo katika merikebu moja nzuri sana ambayo hakuwahi kuiona si katika njozi wala kwenye sinema. Ilikuwa merikebu ambayo katika kumbukumbu zake aliisoma kwenye kitabu cha Alfu lela ulela (siku elfu na moja) katika utawala wa ufalme wa Harun Rashid.



    Merikebu ilikuwa ya dhahabu iliyonakshiwa na fito za almasi na mapazia yake yalikuwa ya kitambaa cha hariri.



    Aliiiona merikebu ile ikisogea pwani na kutia nanga, wakateremka wanawake wazuri sana wenye mavazi meupe ya kupendeza ambao walitandika zuria jekundu lililokwenda kwenye gari zuri ambalo pia hakuwahi kuliona katika maisha yake.



    Alimuona Lakashi akiteremka na kwenda ndani ya lile gari ambalo liliondoka na kuingia mjini. Na mji wenyewe ulikuwa palepale Dubai, aliliona gari likitoka bandarini na kuja moja kwa moja katika hoteli aliyofikia kisha aliteremka peke yake na kuingia ndani ya hoteli. Alipofika mapokezi alimuuliza mhudumu.



    “Vipi yupo?”



    “Yupo.”



    “Ulimpa?”



    “Nilimpa, lakini alihoji wewe kuingia ndani mwake bila ruhusa yake.”



    “Ndiyo alisema hivyo?”



    “Ndiyo.”



    “Mmh! Sawa, pole sana,” Lakashi baada ya kusema vile alitoa pochi yake na kumpatia kiasi cha pesa huku akimwambia:



    “Pole kwa usumbufu niliokusababishia.”



    “Asante kaka mwema,” mhudumu alipokea na kushukuru.



    Lakashi aliachana naye na kwenda moja kwa moja chumbani kwake, japo mlango ulikuwa umefungwa aliingia ndani bila kuufungua na kukaa kwenye kiti pembeni ya kitanda akiwa ametulia kwa kukunja nne. Harufu kali na manukato ya Lakashi ilimuuliza pua Lakashina na kumfanya ashtuke usingizini.



    Alipoangalia kwenye kochi alimuona Lakashi akiwa amekaa kwenye mavazi yale yale aliyoyaota.



    “Asalamu aleykum,” Lakashina alimsalimia huku akipepesa macho na kukaa kitako.



    “Waleykum saalam.”



    “Karibu.”



    “Asante.”



    “Za siku?”



    “Nzuri.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Vipi umerudi rasmi?”



    “Bado.”



    “Japo nimekuona ndotoni wakati ukija mpaka kuingia ndani, siamini kukuona katika macho makavu kabla ya kurudi rasmi.”



    “Nimerudi mara moja kwa ajili yako kisha nitaondoka, nadhani huenda nisirudi tena.”



    “Kwa nini mume wangu?”



    “Lakashina umeolewa?” Lakashi alimuuliza Lakashina.



    “Na nani?”



    “Mbona unaniita mimi mumeo wakati humjui aliyekuoa?”



    “Sikukuelewa, nimeolewa na wewe.”



    “Kweli unakiri toka moyoni mimi ni mumeo?”



    “Ndiyo.”



    “Si kweli, kilichonileta hapa ni kimoja wala sitahitaji malumbano ila kutimiza dhamira yako iliyokusumbua muda mrefu kiasi cha kukunyima raha.”



    “Dhamira gani tena hiyo mume wangu?”



    “Lakashina huna fadhila, yote niliyokufanyia imekuwa bure.”



    “Lakashi nimefanya kosa gani?”



    “Mengi sana, imefikia hatua ya kunipatisha dhambi ili tu ujue mimi nipo lakini nilikuwa natwanga maji kwenye kinu. Leo nimekuja kukufanyia kile ulichokitaka, siwezi kuwa adui wa Mungu kila kukicha.”



    “Kweli niliamua kukukana kutokana na kuishi maisha ya vitisho kila kukicha.”



    “Ni vitisho gani zaidi ya kukupa muongozo mzuri wa maisha yako?”



    “Kwa hiyo unaamua nini?”



    Lakashina alimuuliza huku akiwa tayari kwa uamuzi wowote, na alipenda siku ile waachane kabisa, kwani alitamani kuishi maisha ya kidunia. Kabla hajaendelea adhana ya magharibi ilisikika, ikabidi Lakashi asogee pembeni kuswali magharibi, aliswali mpaka kumaliza Lakashina akiwa amekaa kitandani.



    Baada ya kumaliza kuswali alirudi kwenye kochi na kumuuliza Lakashina:



    “Mbona huswali?”



    “Sina udhu,” alijibu kwa mkato.



    “Una muda gani hujaswali?”



    “Hata sikumbuki.”



    “Mmh! Umekuwa mbuzi usiyekumbuka ulipotoka?”



    “Wewe fanya kile kilichokuleta, sihitaji vitu vingine visivyonihusu, kwanza dini yenyewe ngumu sina uhuru wa maisha.”



    “Mmh! Kweli eeh!”



    “Habari ndiyo hiyo, sema tu kila bwana anayenifuata ni Mwislam, bila hivyo ningerudia jina langu la Jeska.”



    “Asante, nipe pete yangu,” Lakashina alinyoosha mkono kuomba pete yake.



    Lakashina bila kusita aliivua pete ya ndoa na kumkabidhi Lakashi, aliipokea na kusema:



    “Asante, kuanzia leo upo huru kuolewa...









     “Asante, kuanzia leo upo huru kuolewa na mwanaume yeyote, ila utanitafuta na hutanipata tena.”



    “Maisha yangu namtegemea Mungu si kiumbe kinachomtegemea Mungu kama mimi.”



    “Asante.”



    Baada ya kusema vile Lakashi alishika kwenye paji la uso na ghafla alitoweka kwenye kiti. Lakashina aliamini kwa kauli ya Lakashi alikuwa na nafasi ya kumjulisha Abdul Diabi kuwa yupo tayari kuolewa. Alichukua simu yake na kupiga kwa Abdul, baada ya kuita upande wa pili ulipokea.



    “Haloo.”



    “Haloo nazungumza na Abdul.”



    “Hapana mimi ni mdogo wake.”



    “Naomba kuongea naye.”



    “Samahani Abdul amefariki ghafla sasa hivi hivi tupo katika harakati za kupeleka maiti yake hospitali kwa uchunguzi.”



    “Ooh! Nimekwisha,” Lakashina alipiga kelele ya mshtuko alianguka chini na kupoteza fahamu.



    ***



    Alipozinduka alijikuta amelala kwenye kitanda kilichoonesha sehemu ile ni hospitali. Taratibu alirudisha kumbukumbu alitokewa na kitu gani mara ya mwisho. Bado hakuamini alichokiwaza kweli kimetokea. Aliamini huenda ilikuwa ndoto na wala si kitu cha kweli.



    Akiwa katikati ya dimbwi la mawazo aliingia msichana mmoja aliyekuwa katika vazi la uuguzi, alimsogelea kwenye kitanda chake na kumsalimia kwa lugha ya Kiswahili ambayo Dubai ilikuwa ikitumika sana kutokana na watu wengi wenye asili ya Kiarabu kutokea visiwani Zanzibar kuwa pale.



    “Pole dada.”



    “Asante.”



    “Unaendeleaje?”



    “Namshukuru Mungu, hata sijui nililetwa katika hali gani?”



    “Mmh! Kwa kweli Mungu mkubwa, ulikuwa kwenye hali mbaya sana ila kuna kaka mmoja alifanya kazi ya ziada baada ya madaktari kukosa ufumbuzi.”



    “Ufumbuzi wa nini?”



    “Ulipoletwa hapa ulikuwa umeng’ata ulimi na macho kukutoka pima. Mganga mkuu alijitahidi kufanya anachokijua lakini hali haikubadilika. Lakini yule kaka ambaye amedai yeye ni msamaria mwema, aliwasaidia wafanyakazi wa hoteli uliyofikia kukuleta hapa.



    “Baada ya kukuleta aliwaruhusu wafanyakazi waondoke na yeye kusema atakaa hapa mpaka mwisho kuhakikisha hali yako inarudi kawaida. Wakati wakiendelea kukufanyia huduma yeye alikuwa nje ya chumba cha matibabu. Ilichukua zaidi ya saa mbili bila kupatikana ufumbuzi, wakati mganga mkuu anatoka ndani ya chumba, yule kaka alimuuliza kinachoendelea. Mganga aliyekuwa akivuja jasho alimueleza kuwa hali yako bado ni mbaya hakuna mabadiliko yoyote.



    Ajabu yule bwana aliyeonekana ni mtu wa ajabu kutokana na roho yake ya huruma, aliomba wampe nafasi na yeye ajaribu kutoa anacho kifahamu. Japo kwa sheria za kazi si rahisi kumuamini mtu asiye mfanyakazi wala kujua uwezo wake. Lakini kwa vile walikosa ufumbuzi walimruhusu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya kumruhusu nao walikuwa pembeni yake waone anataka kufanya nini, aliomba mafuta ya nazi ambayo alinunuliwa kwenye maduka ya nje ya hospitali. Baada ya kuletwa aliomba yapashwe moto. Baada ya kupashwa, aliyachukua na kujipaka kisha alianza kukuchua taratibu. Kuanzia kifuani kwenda shingoni na kichwani. Ajabu ulimi ulirudi ndani na macho yalifumba , madaktari walishangaa sana.



    Hakutaka kuendelea kuwepo pale kwa vile alikuwa na shughuli zake aliomba ruhusa, mganga mkuu alimruhusu baada ya vipimo vyote kuonesha unaendelea vizuri. Pia alikulipia fedha za matibabu na kuomba tusikupe dawa yoyote ukiamka urudi hotelini kwako ujiandae na safari.



    “Eti ni kweli Abdul amefariki?” Lakashina alijikuta akiulizwa swali lisilomuhusu muuguzi.



    “Mmh! Kweli nimekumbuka kabla ya kuondoka alinieleza jambo moja, kama ukiamka nikueleze.”



    “Jambo gani?”



    “Amesema kuwa kifo cha mumeo mtarajiwa Abdul akihusiani na mumeo wa zamani, ni amri ya Mungu.”



    “Amejuaje?”



    “Kwa kweli sikuwaza kumuuliza swali kama hilo, kwa vile sikuelewa anamaanisha nini.”



    “Huyo mtu yukoje?”



    “Mmh! Dada swali gumu lakini kama sikosei ana asili ya Kiarabu amevalia panjabi nyeupe na makubazi.”



    “Mmh! Anaitwa nani?”



    ”Japo hakunitajia jina, lakini kutokana na jinsi alivyoonesha moyo wa huruma na upendo ilibidi nimuulize jina lake.”



    “Alikujibu?”



    “Ndiyo.”



    “Anaitwa nani?”



    “Lakashi.”



    “Lakashiii?” Jina lile lilimshtua Lakashina.



    “Ndiyo anaitwa Lakashi, kwani vipi, una mfahamu?”



    “Kama ni yeye namfahamu.”



    “Lakini mbona yeye anaonesha hakufahamu.”



    “Mmh! Tuachane na hayo, kwa hiyo Abdul amefariki?”



    “Kutokana na maelezo yake, amefariki.”



    “Mungu wangu, haya sasa maisha gani nitakuwa mtu gani, kama Abdul amefariki lazima yeye anahusika tu.”



    “Dada sikuelewi, una maana gani kusema yule kaka kamuua Abdul?”



    Swali lile lilimshtua Lakashina na kukumbuka siri ile haikutakiwa watu waijue.



    “Basi dada tuachane na hayo, naweza kuondoka?”



    “Ngoja nikamwite daktari.”



    Muuguzi alitoka nje ya chumba na kumuacha Lakashina akishindwa kuelewa Lakashi anataka nini kwake ikiwa wamekwisha achana. Lakini msaada wake nao ulimchanganya akili kwa kujitolea kuyaokoa maisha yake baada ya ugonjwa wake kuwashinda wataalamu wa utabibu.



    Akiwa katikati ya mawazo mganga mkuu aliingia, baada ya kumfanyia vipimo vya mwisho alimruhusu kurudi hotelini kwake. Lakashina baada ya kutoka hospitali ili kupata uhakika alikwenda hadi katika duka alilokuwa akiuza Abdul. Alikuta limefungwa, alipouliza alipewa taarifa kuwa Abdul amefariki na atazikwa siku ile ile.



    Hakuwa na jinsi zaidi ya kuondoka siku ile ile kurudi Tanzania, alipofika Tanzania alikuwa kama mgonjwa kutokana na matukio ya mfululizo ya vifo vya wanaume waliomtaka kimapenzi. Kutokana na kauli ya Lakashi aliyomueleza ya kukubali kuhusika na kifo cha Sadat lakini alikataa ahusiki na kifo cha Abdul. Alijua kauli ile ilikuwa ya kujikosha tu lakini kifo cha Abdul yeye ndiye mhusika.



    Lakashina aliapa kuanzia kifo cha Abdul hatakuwa na uhusiano na mwanaume yeyote. Aliamua kuishi maisha ya kawaida si yale ya kujitunza kila wakati kuvaa nguo zinazouziba mwili wote. Aliyakumbuka maisha ya kihawara aliyokuwa akiishi na mzee Ezekiel, baba Edna enzi ya uhai wake.



    Alianza kunywa pombe kuvaa mavazi ya nusu uchi hata kwenda sehemu za starehe.Vile vile jina lake alibadili na kujiita la zamani la Jeska, hakutaka tena kuitwa Lakashina kila aliyemwita jina hilo alikosana naye. Jeska kama alivyopenda kuitwa vile, kwa hasira vitu vyote alivyokatazwa na Lakashi alivifanya kwa fujo, huku akipuuza kauli yake ya kuwa akifanya kinyume kwa aliyomkataza yatamkuta makubwa. Aliingiza nyama ya nguruwe na pombe nyumbani kwake na kula na rafiki zake.



    Aliogopa kuanzisha uhusiano na wanaume kuogopa kuwatoa kafara, aliamua kuelekeza mapenzi yake kwenye pombe akawa pombe na yeye, yeye na pombe. Muda mwingi baada ya kazi alikuwa akinywa pombe mpaka anapoteza uwezo wa kukumbuka. Watu wake wa karibu walimshangaa alivyobadilika, kutoka katika mavazi ya heshina na kuvaa ya nusu uchi huku akitumia kilevi muda mwingi.



    Wiki moja akiwa kwenye kumbi za starehe alipigiwa simu na mlinzi wake kuwa nyumba yake inaungua. Alitoka ndani ya ukumbi akiwa amelewa na kuendesha gari kwa kasi ili kuwahi nyumbani. Baada ya mwendo mfupi gari lilisimama ghafla, alipoangalia kwenye kioo kinachoonesha mita za gari ilimuonesha rejeta haina maji.



    Alishangaa na kujiuliza kutokewa na hali ile, kwani magari yake alikuwa akiyatunza vizuri sana. Aliteremka baada ya joto la ndani ya gari kuzidi, alisogea pembeni huku pombe zikianza kumtoka. Alipotaka kufungua boneti gari lilikuwa la moto sana kitu ambacho kilikuwa kipya maishani mwake, gari kukaukiwa maji na kuunguza kama moto.



    Akiwa bado anasikilizia maumivu ya mkono, sauti ya mtu ambaye hakumuona ilimueleza:



    “Dada sogea mbali gari linalipuka sasa hivi.”



    Alisogea mbali kidogo na gari haikuchukua muda gari lililipuka kama limepigwa na bomu. Alijikuta akizidi kuchanganyikiwa baada ya gari lake la thamani kuteketea huku akiliona. Akiwa bado anajifikiria afanye nini simu yake iliita tena:



    “Dada upo wapi, nyumba yote inateketea,” ilikuwa sauti ya mlinzi aliyekuwa akilia.



    “Mungu wangu mkosi gani huu! Umewapigia Faya?”



    “Dada ni maajabu, watu wa Faya wamefika lakini ajabu ya Mungu wameshangaa maji waliojaza kutoka kama mate na tenki kuishiwa.”



    “Mmh! Makubwa, huku na mimi gari lote limeteketea,” Jeska alisema kwa sauti ya kukata tamaa.



    “Mungu wangu mkosi gani huu.”



    “Kwa hiyo na magari yangu yote ?“



    “Mama hakuna kilichobaki huu ni moto wa ajabu, sijawahi kuuona katika maisha yangu.”



    “Na nyumba yangu?”



    “Mama utafikiri hapakuwepo na nyumba yoyote”



    “Mungu wangu nimekwisha Laka...nooo, Jeska miye.”



    Mara simu nyingine iliingia ilikuwa ya mmoja wa wafanyakazi wake wa dukani.



    “Dada upo wapi?”



    “Nani Sakina?”



    “Ndiyo dada, nimepigiwa simu kuwa duka lote limeteketea.”



    “Atiii?”



    “Yaani ninavyozungumza hivi nipo kwenye eneo la duka hakuna kilichobakia.”



    Jeska nguvu zote zilimwisha, alianguka chini na kupoteza fahamu.



    ****



    Alipozinduka alijikuta akiwa amelala juu ya kitanda cha hospitali, alijishangaa kujikuta akiwa na vazi la aibu la nusu uchi ambalo alitakiwa kulivaa kwenye kumbi za starehe tena akitoka ndani mwake na kuingia ndani ya gari siyo kutembea kwa miguu.



    Baada ya kupata fahamu alipepesa macho na kuwaona watu wawili wakizungumza huku wamempa mgongo. Mwanaume alionekana daktari kutokana na vazi lake la koti refu jeupe akiwa na muuguzi wa kike.



    “Unasema huyu ndiye dada aliyekuwa akimiliki duka kubwa la nguo?” Daktari aliuliza.



    “Ndiyo.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Si kweli?”



    “Kwa nini?”



    “Yule si anaitwa Lakashina, tena msichana aliyekuwa akijiheshimu kuna kipindi nilidhamiria kumuoa, lakini pete ya ndoa kidoleni kwake ndiyo iliyonifanya nisitishe zoezi langu. Lakini huyu mgonjwa si umesema anaitwa Jeska?”



    “Ndiyo, nasikia aliachana na mumewe na kuamua kurudia dini yake na jina lake la zamani ikiwa pamoja na kutembea uchi kama unavyomuona, kunywa pombe na kufanya kila jambo la kumchukiza Mungu.”



    “Labda alichanganyikiwa baada ya kuachwa!”



    “Walaa, talaka kaitaka mwenyewe kwa vile alipata bwana mwingine.”



    “Zubeda yote haya umeyajulia wapi?”



    “Bosi, kaka aliyemleta hapa inaonekana anamfahamu vizuri.”



    “Kivipi?”



    “Baada ya kumleta alisema amemkuta dada huyu amelala barabarani akiwa amepoteza fahamu baada kutokewa na balaa la kuunguliwa moto vitu vyake.”



    “Yeye alijuaje?”



    “ Bosi, huo muda wa kumhoji kama polisi sikuwa nao isipokuwa msamaria mwema aliyemuokota na kumleta hapa alidai anamfahamu.”



    “Alisema anaitwa nani?”



    “Jeska.”



    “Wewe huyu dada ulimfahamu kwa jina gani?”



    “Lakashina.”



    “Ulihoji kwa nini amwite Jeska badala ya Lakashina?”



    “Kutokana na maelezo niliyokupa mwanzo kuwa baada ya kuachana na mume wake aliamua kurudia jina na dini yake ya zamani pia kurudia tabia zake chafu.”



    “Mmh! Basi alikoelekea ni kubaya kuliko alikotoka, ona mavazi yake bila kuniambia, ningejua ni kahaba aliyeokotwa na wasamaria wema akijiuza kimwili.”



    Muuguzi alipogeuka alimuona Jeska aliyekuwa akitokwa na machozi ya uchungu kwa kuilaumu nafsi yake kumshauri vibaya.



    “Dokta naona kaamka.”



    “Ooh! Vizuri.”



    Daktari aligeuka na kusogea kitandani ambako Jeska alikuwa akiendelea kutokwa na machozi ya uchungu baada ya kupata ukweli wa kuunguliwa kwa mali zake zote nyumba, magari na duka.



    “Pole sana,” daktari alimsemesha kwa sauti ya upole.



    “Ni kweli vitu vyangu vimeungua?”



    “Bado hatuna uhakika,” daktari alijibu.



    “Hamna uhakika kivipi wakati nimesikia yote mliyokuwa mkizungumza?”



    “Aliyozunguza ni msamaria mwema anayekufahamu, sikuweza kukubali mara moja mtu aliyekuokota njiani ajue kila kitu kilichokupata kuwa umeunguliwa sijui gari, gari lilionekana kweli limeungua, lakini nyumba na duka lako amejuaje?”



    “Kwani aliyenileta alisema anaitwa nani?”









    “Mmh! La...la...shi...Jina lake kweli...sijuiii...”

    “Au Lakashi?”

    “Sawa sawa kabisa anaitwa Lakashi.”

    “Mungu wangu huyu kiumbe ananitaka nini?”

    “Unamfahamu?’

    “Ndiye aliyenisababishia yote haya.”



    “Mbona ndiye aliyekuokota na kukuleta hapa kisha kukulipia fedha za matibabu.”



    “Muongo mkubwa shetani mkubwa yule,” Jeska alisema kwa hasira.



    “Siamini usemayo, yule bwana ni mstaarabu kuliko wastaarabu, pamoja na kukufahamu kwa juu juu, huwezi amini jamaa kaondoka alfajiri baada ya hali yako kuwa nzuri, kama angekuwa mtu mbaya asingevumilia kuumwa na mbu pia kuacha usingizi wake,” muuguzi alisema.



    “Muuongo mkubwa, tena muuaji asiye na huruma,” Jeska alizidi kubwata kwa sauti ya juu.



    “Mbona hatukuelewi?”



    “Hamuwezi kunielewa, yule bwana ni mnafiki mkubwa, si tumeachana ananifuatia nini?”



    “Jeska uko sawa?” daktari alimuuliza.



    “Ni sawa wala sina tatizo lolote katika akili yangu, kama ni kweli alivyonipatia vimeungua aachane na mimi.”



    “Kumbe mnajuana?”



    “Alikuwa mume wangu tumeachana, lakini nashangaa bado ananifuata.”



    “Unataka kusema ndiye aliyefanya uharibifu wote huo?”



    “Ndiyo.”



    “Kwa nini usipeleke taarifa polisi?”



    “Haina haja kama kachoma vitu vyake ya nini kumpeleka polisi?”



    “Sasa utaishi vipi?”



    “Nitajua mwenyewe.”



    “Na kwa nini umebadili jina lako?”



    “Jibu mnalo, nashangaa mnaniuliza, huyo huyo mwana haramu aliyenitia umaskini, ndiye aliyenibadili jina na dini ili anifanye mtumwa wake.”



    “Mmh! Makubwa.”



    “Kutokana na tatizo lililokupata, vipimo hukupata tatizo kubwa zaidi ya mshtuko, kwa hiyo tutakupa ruhusa ya kutoka hospitali leo.”



    “Hakuna tatizo.”



    Jeska alisema huku akinyanyuka kitandani katika vazi la aibu, alikuwa amevalia gauni lililoacha wazi sehemu kubwa ya mwili wake. Mgongo wote ulikuwa nje na chini liliishia chini kidogo ya makalio. Vazi lile lilimfanya daktari asimuangalie mara mbili.



    “Una ndugu?” Alimuuliza.



    “Ninao, lakini simu nimepoteza.”



    “Mmh! Kweli, simu yako aliileta yule kaka aliyekuokota.”



    Muuguzi alikwenda ofisini na kurudi na simu ya Jeska pamoja na gauni refu. “Hili gauni la nani?”



    “Alisema uvae usitiri maungo yako.”



    Jeska hakubisha kulichukua gauni kutokana na vazi lake la aibu, baada ya kulivaa, alionekana mstaarabu, aliwapigia simu baba zake wadogo. Baada ya muda walifika hospitali kumchukua na kumpeleka kwao. Alipofika kwa baba zake muda wote alikuwa akilia akikumbuka maisha mazuri aliyokuwa akiishia na kubadilika ghafla kulikosababishwa na jini alilokuwa akiishi nalo.



    Jioni ya siku ile alitoroka na kwenda kuthibitisha mwenyewe kama kweli jumba lake la fahari limeungua moto. Alipofika alishuhudia hasara kubwa iliyosababishwa na moto wa ajabu. Roho ilimuuma hakuwa na jinsi zaidi ya kurudi nyumbani.



    Mwezi mmoja yalianza mazungumzo ya chini chini juu ya kuwepo pale bila msaada wowote. Kila kukicha alikuwa mtu wa mawazo juu ya maisha ya masimango. Akiwa amekaa barazani mkono shavuni, mama yake mdogo alimfuata na kumueleza:

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Jeska unaitwa na baba yako.”



    Jeska bila kusema kitu alinyanyuka na kuingia ndani, alimkuta baba yake akiwa amekaa kwenye kochi.



    “Kaa hapo,” Jeska bila kusema neno alikaa akiwa amejikunyata.



    “Mama tumekuita tuzungumze,” baba yake alimwambia.



    “Sawa baba,” alijbu kwa sauti ya chini bila kumuangalia usoni.



    “Unafikiri utaendelea na maisha haya mpaka lini?”



    “Hata sijui.”



    “Unasema vitu vyako vyote vimeungua?”



    “Baba swali gani nimesema au kweli vimeungua!”



    “Inawezekana nimekosea kusema, ila nia na madhumuni nilitaka kujua baada ya kupoteza vitu vyote una akiba gani?”



    “Baba ni maswali gani hayo ya kuniuliza, kila kitu kimeungua nitabakia na akiba gani?”



    “Yaani utajiri uliokuwa nao ukose hata akiba banki?”



    “Huwezi kuamini, fedha iliyokuwa benki nilinunulia mzigo wote niliotumwa na wateja ambao ungenilipa zaidi ya mara nne. Lakini kabla ya kuuza balaa limenitokea.”



    “Sasa sisi tutakusaidia nini, wewe ni mtu mzima na nyumba yetu kama unavyoiona inatutosha wenyewe. Huna hata bwana wa pembeni uende ukakae.”



    “Sikuwahi kuwanaye.”



    “Acha uongo, si ulisema mumeo alikasirika kutokana na kutaka kuolewa na bwana mwingine. Msaada wetu umekaribia mwisho mtafute bwana yako umeombe msamaha.”



    “Siwezi kuolewa na Jini.”



    “Leo hii ndiyo umemjua ni Jini, kiburi chake ndicho kilichokuponza, tuna nia ya kuendelea kuwa na wewe. Lakini toka uwe hapa maisha yamekuwa magumu kiasi cha kututishia hali yetu. Jana nimeota na nyumba yetu inaungua, ndoto ya jana imenitia wasiwasi huenda na nyumba yetu itaungua kwa hiyo tulikuwa tunaomba uondoke.”



    “Jamani niondoke niende wapi?”



    “Hiyo haituhusu utajua pakwenda, lakini hapa hutakiwi kukaa utatusababishia matatizo.”



    Kauli ile ilikuwa mkuki moyoni mkali mwa Jeska, aliona aliloelezwa na Lakashi la kutengwa na familia yake linatimia.



    “Lakini wazazi wangu hamuoni kunifukuza ni kunikumbusha uchungu wa vifo vya wazazi wangu na jinsi mlivyonifukuza na kuchukua mali za wazazi wangu?”



    “Sikiliza binti hatupo kukumbushana mambo yaliyopita ukitaka kujikumbusha mambo yaliyopita nenda makumbusho ya taifa.”



    “Sasa mnanifukuza nitakwenda wapi?”



    “Hiyo haituhusu, tulikuhifadhi kwa muda ili ujipange, lakini siku zinakatika bila kuona dalili zozote za kuondoka zaidi ya kila siku kutufanyia uchimvi wa kulialia. Ona sasa, hata hali zetu zimekuwa mbaya riziki imefunga kwa ajili yako, ndoto za kuunguliwa nyumba haziishi na mchomaji ninaye kuona ni wewe.”



    “Lakini baba hizo ni ndoto hazina ukweli wowote.”



    “Wewe mtoto mdogo hujui lolote, sisi tuliyewahi kuliona jua tunajua ndoto zina maana gani, hasa ndoto za kujirudia zina dalili mbaya.”



    “Hivi mnanifukuza niende wapi?”



    “Hiyo haituhusu, nenda kwa rafiki zako.”



    “Lakini kumbukeni pamoja na kunidhulumu mali zangu bado maisha yenu yalikuwa mabaya, hata mume wangu alipowalazimisha kulipa hamkuwa na kitu na kuniomba niwaombee msamaha. Nimewaombea na mkasamehewa ikiwa pamoja na kupewa maisha mazuri. Leo nimepata tatizo mnanigeuka?”



    “Jeska siku zote tenda wema uende zako usisubiri shukurani.”



    “Kwa hiyo umedhamiria kunifukuza?”



    “Kwa hali inayojitokeza lazima uondoke tu.”



    “Lakini kumbuka maisha haya ni kwa ajili yangu.”



    “Unatuchekesha, maisha haya na uliyokuwanayo nani alikuwa na maisha mazuri? Umeshindwa kumheshimu mumeo kwa upumbavu wako matokeo yake unatulaumu tusio husika.”



    “Siwalaumu bali nawakumbusha jinsi gani nilivyoonesha ubinaadamu kwenu japo hamkunitendea wema.”



    “Nataka nikueleze jambo moja ambalo sikupenda kukueleza mwanzo, njozi zangu za mara kwa mara za nyumba inaungua na mchomaji ni wewe zilinifanya niende kwa mtaalamu mmoja na kumuulizia njozi zile zina maana gani, baada ya kunitia wasiwasi.



    “Jibu la mganga ningekuwa na moyo mdogo ningekufukuza muda mrefu, lakini ubinaadamu ndiyo uliyokufanya uwepo mpaka leo.”



    “Kwa nini?” Jeska aliuliza akiwa anamtazama baba yake.



    “Mganga amesema ndoto ile ni ufunuo uliombele yangu wa juu ya kitu kinachotaka kunitokea.”



    “Utokewe na nini?”



    “Kuota moto ukiunguza nyumba na wewe ndiye mchomaji inamaanisha nyumba yangu muda wowote itaungua moto na wewe kuonekana ndiye mchomaji inaashiria kuwa chanzo ni wewe baada ya kutoheshimu masharti uliyopewa na mumeo.



    Hivyo basi kuendelea kuwepo hapa wakati tumeishajua tatizo ni nini, lazima nyumba yangu itaungua moto na sisi kuwa maskini wa kutupa.”



    “Lakini kwa nini muamini njozi, sasa huyo Lakashi kama anaendelea kunifuata basi animalize kabisa,” Jeska alisema huku akilia.



    “Jeska hata sisi hapa hatutumii vitu ulivyokuwa ukitumia, tuliacha pombe na nyama ya nguruwe baada ya mumeo kunionya, ili kuendelea kuwa rafiki yetu basi tuhakikishe vitu vyote asivyovipenda tusivitumie.”



    “Kwani hata mimi toka nije hapa mmeniona nakunywa au kula nyama ya nguruwe.”



    “Kiburi chako ndicho kilichomuudhi, kwa hiyo kwa usalama wa nyumba na mali zetu lazima uondoke si ombi bali amri.”



    “Baba kama atakuja zungumza naye basi, mimi nitakwenda wapi?” Jeska alizungumza kwa sauti ya kuomba kuhurumiwa.





     “Nilikusamehe toka nilipojua udhaifu wako, ila ndoa yetu iliisha siku uliponirudishia pete yangu.”





    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Nisamehe Lakashi.”

    “Nataka nikueleze kitu kimoja, siku zote kiburi si maungwana, nilikupenda na kuwa tayari kukusamehe kwa lolote. Lakini ulivuka mipaka, tulipoachana sikutaka kuchukua kila nilichokukupa. Uliyoyafanya ndiyo yaliyopoteza mali yako pombe na nyama ya nguruwe ndiyo iliyochoma.”



    “Najua Lakashi naomba unisamehe.”

    “Msaada wangu ni mmoja kukupa maisha mazuri, lakini ukifanya kosa lingine utageuka nguruwe milele.”

    “Nipo tayari kuyafanya yote utakayo yataka.”

    “Hakuna kitakacho badilika zaidi ya kuwa kama nilivyokueleza tukiwa pamoja.”

    “Nitashukuru Lakashi.”



    “Hakuna maisha mazuri kama mtu kujiheshimu na kuwaheshimu waliokuzunguka. Changua maisha yanayomfurahisha Mungu ndiyo uyafanye siku zote.”

    “Nimejifunza Lakashi, nisamehe.”

    “Basi rudi nyumbani kwako.”

    “Nyumbani kwangu wapi?”



    “Kwani ulikuwa unakaa wapi?”

    “Nyumba yangu si iliungua?”

    “Nani aliyekuambia imeungua?”

    “Niliona mwenyewe”

    “Nimekuambia rudi nyumbani kwako.”

    “Sawa.”



    “Haya rudi,” baada ya kusema vile aliitupa kamba chini iliyogeuka nyoka ambaye aliingia kwenye majani na kupotea. Jeska alitoka kwenye majani na kurudi nyumbani kwake kwa miguu.



    Njiani lilipita gari iliyompa lifti mpaka nje ya geti la nyumba yake, alishangaa kukuta nyumba yake ipo kama kawaida hakuamini na kujiuliza iliyoungua ilikuwa nyumba ipi. Alipoingia ndani alishangaa kukuta kila kitu kipo hata mlinzi wake alikuwepa kama kawaida.



    Aliyazungukia magari yake yalikuwepo kama kawaida hakuna lililoungua.

    “Dada,” mlinzi alimwita.

    “Abee.”

    “Za siku?”



    Swali lile lilimshtua na kujikuta akichukua muda kumjibu, alijiuliza ni mlinzi gani aliyempigia simu kuwa nyumba inaungua? Kabla mlinzi ajamshtukia alimjibu.

    “Nzuri tu.”

    “Naona safari hii umeondoka bila kutuaga?” mlinzi alimuuliza huku akimshangaa vazi alilokuwa amevaa.



    Kabla ya kufanya lolote alimuacha mlinzi bila kujibu kitu na kwenda ndani, hali ya ndani ilikuwa kama alivyoiacha ilikuwa katika hali ya usalama, ila hali ya hewa ilikuwa nzito kama kuna kitu kimeoza mle ndani. Alikwenda kuoga na kubadili nguo. Akiwa amekaa sebuleni sauti ilimjia akilini:

    “Naomba utoe uchafu wako wote uliouweka humo ndani mara moja.”



    Bila kujibu alinyanyuka na kwenda kumwita mfanyakazi wake kuondoa vitu vyote alivyokatazwa na Lakashi. Baada ya kuondoa chupa za pombe na vipande vya nyama na mifupa ya nguruwe haikuchukua muda hali ya hewa ilibadilika mle ndani na kuwa nyepesi tena yenye manukato aliyoyazoea.



    Hali ile ilimshangaza sana Jeska na kujiona kama mtu aliyezaliwa upya, akiwa bado haamini kilichotokea simu yake iliita alipopokea ilitoka kwa msichana wa dukani kwake:

    “Dada upo wapi?”

    “Nyumbani?”

    “Umerudi lini?”

    “Leo.”



    “Jamani dada mbona ukutuaga, mali zimekwisha wateja wanatusumbua sana.”

    “Jamani poleni, naomba jioni mje wote nyumbani.”

    “Huwezi kuamini tumefurahi kukuona.”



    Jeska alikata simu na kubaki akiwa katika dimbwi la mawazo na kujiuliza kilichomtokea kilikuwa ni ndoto au kiini macho. Alinyanyuka na kwenda kuangalia gauni alilopewa na Lakashi hospitali lilikuwa lilelile. Hakutaka kuamini mara moja, alikwenda moja kwa moja kwenye hospitali aliyolazwa baada ya kuokotwa na Lakashi.



    Majibu yalikuwa yale yale alipelekwa pale baada ya kuokotwa na msamaria mwema aliyesema kuwa amemkuta amelala pembeni ya gari lake lililokuwa limeungua moto, pia alieleza kuwa ameunguliwa na nyumba pamoja na duka. Kilichowashangaza ni muonekano mwingine wa nguo za heshima alizokuwa amevaa siku ile na kumsikia daktari kwa mbali akimuelezea muuguzi wake:

    “Huyu ndiye Lakashina ninaye mfahamu.”



    Kauli ile ilimuumiza sana moyo wake na kujua kabisa alikuwa amekosea njia, aliondoka na kurudi nyumbani. Alipofika alilia sana na kujutia yote aliyoyafanya, alitamani kumuomba radhi Lakashi na kuwa tayari kumsubiri kwa muda wowote hata miaka kumi.

    Baada ya kulia sana mpaka sauti ikamkauka, alipitiwa usiungizi. Hakuchukua muda Lakashi alitokea mbele yake.

    “Jeska unalia nini?” Lakashi alimuuliza kwa sauti ya upole.

    “Naomba unisamehe Lakashi,” Jeska alipiga magoti mbele yake.

    “Nyanyuka Jeska wa kupigiwa magoti ni Mungu peke yake,” Lakashi alimnyanyua Jeska na kumketisha kitandani.



    “Lakashi najua nimekukosea, Nipo chini ya miguu yako pamoja na yote niliyoyafanya sikuwahi kuisaliti ndoa yetu. Nakuahidi kuwa mke mwema na muaminifu pia nipo tayari kukusubiri hata miaka miamoja. Nimegundua wewe ndiye mume wa maisha yangu...Nakupenda Lakashi umekuwa msaada na kinga ya maisha yangu...nakuomba usiniache....nirudishie pete yangu. Kumbuka mimi ni mwanadamu niliye na upungufu mwingi, kukosa ni sehemu ya maisha ila nimejifunza kutokana na makosa.



    Umekuwa kiumbe wa ajabu pamoja na kukufanyia yote mabaya lakini bado umekuwa ukinijali na kunilinda. Nisipo yathamini hayo, mimi sifai tena kuishi chini ya jua kwa vile sina tofauti na viumbe vilivyomuudhi Muumba na kuviteketeza kwa gharika.

    Nakuahidi mbele ya Muumba tusiyemuona lakini yupo mbele yetu kuwa sitakuumiza tena, nitayashika yote uliyonifundisha ili niwe mke mwema katika maisha yangu yote.”

    “Jeska...Jeska...Jeska.”



    Jeska alishtuka usingizini baada ya kuitwa huku akitikiswa begani, alipofumbua macho alijishangaa kuona amezungukwa na familia yake. Alitulia kwa muda akiwaangalia waliomzunguka na kujiuliza alichokiona mbele yake ni kweli au aliota.

    Familia yake yote ilikuwa mbele yake, alijitahidi kunyanyua mdomo wake amwite mama yake.



    “Ma..a..ma,” aliita kwa sauti ya upole huku michirizi ya machozi ikiwa pembeni ya macho yake.

    “Abee mwanangu,” mama yake alimuitikia kwa upole.

    “Ni wewe mama au naota?”

    “Huoti mwanangu ni mimi mama yako.”

    “Baba yuko wapi?”



    “Alisafiri lakini atarudi leo.”

    “Mbona mmenizunguka?”

    “Toka ulipolala jana jioni mpaka usiku huu ndiyo unashtuka, kwani ulikuwa unaota nini mwanangu maana umetoa ahadi nzito ya ndotoni?”

    “Mama nampenda sana Lakashi najuta kumkosea.”



    “We Jeska, Lakashi ni nani?”

    “Mama mwanaume wa pekee aliyeonesha kunijali pamoja na kumfanyia makosa bado kanisamehe.”

    “We Jeska, utakuwa mwendawazimu huyo Lakashi anaishi wapi?”

    “Hata sijui mama.”



    “Hebu nyanyuka kwanza hapo kitandani.”

    Mama Jeska alimnyanyua mwanaye aliyekuwa akiendelea kulia.

    Baada ya kuoga, Jeska aligoma kula mpaka amuone Lakashi.

    “Jeska una nini mwanangu mbona sikuelewi, Lakashi ni nani?”

    “Ni mwanaume wa pekee aliyenipenda kwa dhati.”



    “Mbona familia yako hatumjui?”

    “Lakini mama mbona kama sielewi.”

    “Huelewi nini mwanangu?”

    “Inawezekana nilikuwa naota!”

    “Uliota nini mwanangu?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Jeska alimueleza mama yake jinsi alivyokutana na Lakashi, baada ya kumsikiliza mama yake alicheka na kusema:

    “Kumbe ndoto! Ona sisi wazazi wako na familia yote tupo hai.”

    “Mama, pamoja kuwa na ndoto maishani mwangu nitaolewa na mwanaume kama Lakashi.”

    “Kwa hiyo upo tayari kubadili dini?”



    “Nipo tayari, nakiri kumpenda Lakashi mpaka kufa.”

    Jeska aliamini katika maisha yake ile haikuwa ndoto bali maisha kamili na kuamini siku moja Lakashi atamtokea na kumuoa. Aliishi kwa kuzingatia yote aliyomuahidi Lakashi ndotoni.



    MWISHO.



0 comments:

Post a Comment

Blog