Search This Blog

Monday 20 June 2022

KIZUIZI - 5

 





    Simulizi : Kizuizi

    Sehemu Ya Tano (5)



      Emmy aliingia chumbani kwake, akajirusha kitandani. Akatazama katika kabati akakutana na suti na nguo mbalimbali za mume wake.

    Akashtuka kama ameona jinamizi. Akaliendea kabati akaamua kulifunga.

    Alipogeuka kurejea kitandani akautana na ukuta ukiwa na picha kubwa ya James siku ya harusi yao. Akatokwa na yowe la hofu.

    Akakiendea kitufe cha kuzima na kuwasha taa, akazimisha.

    Giza likatawala.

    Emmy akagaagaa kitandani, akamfikiria Jose B, akamlaani kimya kimya kwa kuuchezea mwili wake ilhali akijua fika kuwa anamuuza kwa James na wao ni kitu kimoja kabisa.

    Machozi yakamtoka.

    “Hivi inachukua dakika ngapi kuua?” alijiuliza bila kupata jibu.

    Aliamini fika kuwa Jose B si mwanadamu na stahili yake ni kuuwawa.

    “Nimemfungulia biashara, nimempangishia nyumba nzuri. Kumbe ananizomea tu.....ina maana hata msibani alipokuja alikuwa ananichora tu hayawani yule.”

    Kilio cha kwikwi kikaendelea kutawala.

    Emmy aliusikia moyo wake jinsi ulivyokuwa ukipashika kwa joto la uchungu. Machozi yakaendelea kuilowanisha shuka.

    “Ila Mungu atanilipia tu, kama nimeipigania ndoa yangu kwa njia zisizokuwa sahihi Mungu anisamehe, nimejaribu sana, nimejaribu kupigana mimi, nimeuacha mwili wangu uchezewe na baradhuli, nimetumia pesa nyingi kuiamarisha ndoa hii. Tazama sasa kumbe na mtoto sio ridhiki yangu huyu. Naenda kumzalia baba yangu mtoto. Aibu gani hii...” alilalamika sana huku akiendelea kulia.

    Baadaye akapitiwa na usingizi hadi alipokuja kuamshwa majira ya saa nane na nusu usiku.

    Usiku wa mauzauza, usiku ambao ulibadili kila kitu katika maisha ya yake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ***



    Jose B waukweli aligundua kuwa yu katika mikono salama baada ya mazungumzo ya muda mrefu kati yake na Mariam, alisimuliwa jinsi alivyoonekana katika macho yake tangu alipotekwa, akafikishwa mahali ambapo aliingizwa ndani kisha asubuhi akatolewa.

    Huko pote Mariam alikuwa akimfuatilia vyema akiwa na vijana wake pamoja na yule dereva machachali.

    Hatimaye akatupwa nje ya gari, wao wakalishuhudia tukio lile na sasa walikuwa naye wamemkomboa.

    “Kwa wema wako jijini Mwanza sidhani kama ningeweza kukuacha vile.” Mariam alimweleza Jose b ambaye alikuwa ameoga, na tayari alikuwa ametafutiwa nguo za kubadili.

    Wale vijana alikuwa analingana nao miili hivyo ilikuwa shughuli nyepesi. Jose B alikuwa msiri sana, alizoea kufanya biashara ya kuuza siri na kwa yule isiyomuhusu ya nini kumshirikisha? Kama analipia hapo sawa lakini kiundugu. Hapana.

    Jose B aliwadanganya kuwa Lameck alikuwa amemfananisha tu n’do maana alimwachia bila sharti lolote. Wote wakamwonea huruma.

    “Mariam nahitaji kesho niondoke zangu jijini humu.”

    “Kwanini wakati upo na mimi tayari.”

    “Naenda kumuona mama na kupumzika kidogo, akili yangu haipo sawa.”

    “Pumzika siku kadhaa hapa nitakulinda.” Mariam alisisitiza. Lakini Jose B akapinga na hatimaye akakubaliwa kuwa siku inayofuata ataondoka kwa usafiri wa basi.

    “Lakini kuna jambo nahitaji kufanya kabla ya kuondoka”, “Nahitaji kuonana na msichana mmoja kuna ujumbe iwe isiwe lazima nimpe” Jose alizungumza. Mchomo wa wivu ukapenya katika mbavu za Mariam kisha ukapanda hadi moyoni. Ni hapo ndipo alipokiri kuwa kuna kitu cha ziada alikuwa akikiona kwa Jose B.

    “Yuko wapi?” aliuliza, kwa sauti iliyokwaruza.

    Jose akaeleza, akaeleweka.

    “Lakini sasa hivi ni usiku sana.”

    “Hivyo hivyo, lazima nimuone.” Akakubaliwa.

    Kichwani mwake Jose B alimfikiria Emmy, alimpenda sana msichana yule kutokana na kumtimizia kila alichokuwa anahitaji.

    Sasa alihitaji kumlipa wema.

    Alihitaji kumweleza mambo kadhaa kuhusiana na mumewe.

    Jose B kwa mara ya kwanza akapata kihoro cha kugawa siri.

    Malipo ya Emmy yalikuwa kwa ajili ya siri ya kutembea na Lameck lakini hii ya siri ya James kuua jijini Mwanza aliamua amgawie Emmy bure.

    Kisha atoweke jijini Dar na kurejea Mwanza.

    Aliijua hatari ya kuendelea kuwa katika jiji lile. Kipigo cha mbwa mwizi kilichokaribia kuitoa roho yake kilimwogopesha sana.

    Usiku wa saa sita safari ikaanza, huku nyuma Maria akabaki kuumizwa na hisia zake.

    Wakaanzia nyumbani kwa Jose B. Huko akachukua vitu vyake vya msingi ikiwemo ile simu anayotumia kupokea na kuhamisha pesa kwa wateja, kadi ya benki na vinginevyo.

    Kisha ikafuatia safari ya kwenda kwa Emmy.

    Ilikuwa safari fupi sana kutokana na barabara kuwa wazi sana usiku huo mnene.

    Walipofika Jose aliazima simu kwa mmoja wa vijana wale, akarejesha kumbukumbu za namba za Emmy kisha akampigia.

    Simu ikaita kidogo na kupokelewa.

    “Nani?”

    “Sam hapa. ?Upo mwenyewe”

    “Unataka nini Sam?”

    “Nipo hapa nje nahitaji kuonana na wewe ni muhimu sana Emmy..muhimu.”

    “Nakuja”

    Simu ikakatwa.

    “Jose B akawapa maelekezo vijana waliomsindikiza. Wampokee Emmy kama akitoka wampeleke alipo yeye. Wakatelemka na kuliendea geti.

    Wakabisha kwa muda mrefu baadaye mlinzi ambaye huwa anakuja usiku na kuondoka asubuhi akafungua akiwa ametokea usingizini.

    “Emmy ana mgeni wake.” Akaelezwa yule mlinzi. Hakutaka kuelewa lolote kwa usiku ule. Akagoma kabisa.

    Emmy ambaye hakuwa na usiku mzuri aliyasikia makelele ya getini. Akashuka kitandani na kujongea hadi nje kwa tahadhari kubwa.

    “James n’do amekuja kuniua au? Ameamua kuja na Sam wake” alijiuliza.

    Akachungulia na kuona mlinzi akijibizana na watu mlangoni.

    Akawa anatetemeka. Hakujua kuna nini.

    Emmy akarejea nyuma hatua kadhaa kisha akaingia jikoni. Ni huko akakumbuka swali alilojiuliza kabla ya kulala.

    “Inachukua dakika ngapi kuua?”

    “Sasa naenda kupata jibu .” alijisemea huku akitetemeka.

    Mikono ikakutana na kisu kipya chenye makali ya ajabu.



    Jose B alikuwa mtulivu sana tofauti na siku nyingine alipokuwa anakutana na Emmy, alikuwa anaweka machachali mbele na kupenda kutawala maongezi.

    Tofauti na siku hizo zote, siku hii Jose B alikuwa katika utulivu wa hali ya juu sana. Emmy aliishihudia hali hii baada ya kukabiliana naye ana kwa ana.

    Kisu chake kikali kilikuwa katika pindo la nguo yake ya ndani.

    Wale vijana wawili walimwacha Jose B aweze kuzungumza na Emmy, wao wakarejea katika gari ambalo lilikuwa mita nyingi kutoka pale walipomwacha Jose.

    Emmy hakutaka kurudisha maamuzi yake nyuma, alikuwa amenuia kufanya kitu cha ajabu.

    Kisu kilikuwa kinampa ujasiri wa hali ya juu sana.

    Jose B alikuwa ameumuka usoni na alikuwa na michubuko katika paji la uso.

    “Mambo vipi Emmy. Za siku.” Jose alijaribu kuleta uchangamfu kiasi fulani.

    Emmy akaendelea kumsikiliza huku dhahiri akionekana kukereka na ujio huo wa usiku tena usiku wa manane.

    Je, mume wake angekuwepo? Alijiuliza.

    Lakini papo hapo akapata jibu kuwa James na Jose lao ni moja.

    “Sam..” aliita Emmy.

    “Naam.”

    “Unamfahamu vipi mume wangu.”

    “Nani yule James?..aah ndio namfahamu vipi kwani.” Aliuliza huku akitabasamu Jose B.

    “N’do nimekuuliza unamfahamu vipi?”

    “Tulia Emmy n’do nimekuja kukuletea habari zake huyo jamaa. Leo sina ubaya.” Alianza kuzungumza Jose kisha akasita,

    “Jamaa yako mtu mbaya sana ujue...yaani sijui hata nikuelezeje lakini tambua kuwa Jose ni muuaji....nakueleza haya nikiwa namaanisha kuwa kesho mimi narejea Mwanza, iwapo itavuja siri yoyote inayokuhusu wewe kwake na wewe uwe na makali ya kupingana naye. James ni muuaji na alimuua.....” akasita. Akamtazama Emmy, mwanadada huyu alikuwa anatetemeka sana.

    Jose B akamtazama, akamsogelea kama mpenzi wake wa siku nyingi. Akamkumbatia akiamini kuwa taarifa aliyompa ndiyo ambayo imemweka katika hali hiyo.

    Hakujua nini kinasafiri katika akili ya Emmy.

    Akamkumbatia, nguo nyepesi iliyouhifadhi mwili wa Emmy usiwe uchi ikaruhusu joto la kipekee kupenya katika mwili dhaifu wa Jose B, mzigo mdogo wa embe dodo ukamchoma kifuani pasi na maumivu bali raha i’so kifani na isiyokinai.

    Jose B akamkumbatia kwa nguvu zaidi. Hisia zake zikamsafirisha mbali akakumbuka mchezo aliokuwa anacheza na Emmy mafichoni. Ghafla bila kutarajia akautamani tena bila kujali mazingira.

    Emmy alikuwa anahema kwa nguvu, Jose akajua kuwa na yeye alikuwa katika uhitaji tena wa hali ya juu kuliko yeye. Giza likampa kiburi, akaupitisha mkono wake kwa kusitasita katikati ya miguu ya Emmy, mara akautoa akahamia katika tumbo la Emmy akaanza kupapasa.

    Emmy alikuwa ametulia bado akihema kwa fujo.

    Mara mkono ukazifikia zile embe dodo. Akaiminya moja. Mkono wa pili nao ukapata matamanio ya kuminya embe, ukapenya na kuingia kwa fujo katika embe lililosalia katika upweke. Sasa mikono yote miwili ikawa katika kumhenyesha Emmy.

    Laiti kama Jose angeyajua yanayopenya katika kichwa cha Emmy angefanya yake na kuondoka huenda angeiepuka adhabu mbele yake.

    Emmy alikuwa akilikumbuka swali lake la ‘inachukua dakika ngapi kuua?’ akiwa hajapata jibu, mnafiki anayejifanya kuwa rafiki anaanza kumpapasa, kisha anaingiza mikono katika kifua chake.

    Dharau ya hali ya juu. Aliwaza Emmy.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sasa akagundua kuwa, kuua huwa sio roho mbaya ya mtu bali huwa ni msukumo kutoka katika nafsi.

    Akausogeza mkono wake wa kuume, akampapasa Jose B.

    Jose akahema kwa fujo, alikuwa amezidiwa.

    Akampapasa tena tumboni, Jose hoi.

    “Tusogee huku mpenzi.” Jose akatoa wazo.

    Emmy hakujibu zaidi ya kukereka na jina hilo la mpenzi.

    Akasogea wakaufikia mchanga.

    Jose B akafanya kosa kubwa kupita yote katika karne.

    Akakubali kutangulia kulazwa chini. Emmy akawa juu yake.

    Emmy akiwa anaendelea kuzifuga hasira akaifungua zipu ya suruali ya Jose B wa ukweli. Jose akasahau maumivu yote na kipigo kutoka kwa Lameck.

    Akajisikia mtu mpya kabisa, na alikuwa katika pepo ya maajabu.

    Emmy akapanda juu akairudisha mikono yake nyuma.

    Akazikusanya nguvu zote, uchungu wa kufanywa mtumwa wa ngono na kijana huyu, ukamtawala.

    Akashuka kwa nguvu zote.

    Nguvu za maajabu.

    Mguno mmoja kisha kimya kikubwa kikatanda.

    Ardhi ikaanza kumeza damu. Emmy hakuridhishwa na kile kimya, ile damu iliyomrukia ikapandisha kichaa chake, akaendelea kuchoma kwa fujo hadi akaridhika

    Emmy akasimama wima.

    Yeyote aliyelishuhudia tukio hili na ajisogeze naye amalizwe mara moja.

    Hakuwa yule Emmy dhaifu tena.

    Uzuri ni kwamba hakuna aliyeweza kushuhudia, vijana walikuwa mbali sana!!



    Baada ya saa moja na nusu. Binti mkakamavu asiyeelewa huo ukakamavu aliutoa wapi alikuwa na mkakamavu wa ukweli kwa kupitia mafunzo ya kijeshi.

    Emmy na mjeshi Lameck.

    Lengo kuu likiwa kuukimbia mji.

    Emmy alikuwa amemueleza kila kitu juu ya ujio wa Jose B na hatua aliyoifikia baada ya kuhisi anadhalilishwa.

    Taarifa hiyo ilimshtua Lameck na kuamini kuwa yu pamoja na mtu sahihi kwa wakati ule.

    Lameck na Emmy walikuwa wanatoroka si kwa kitu kingine bali kuuwekea ukweli kizuizi usiweze kutoboka na kuwafikia walimwengu.

    Emmy akiwa ana mimba isiyokuwa yake na akiwa na uongo mkubwa wa kughushi bikra ili amlaghai mumewe. Lameck alibakia na siri ya kumuua mama yake Emmy na siri yake ambayo haikuwa yake pekee siri ya kupoteza maungo yake ya uzazi, nchini Sudan. Siri ambayo hakuhitaji mtu yeyote aitambue kiwaziwazi.

    Sasa alikuwa anapigania kiumbe katika tumbo la Emmy.

    Damu yake pekee katika ulimwengu.

    Lameck alimsihi Emmy azime simu yake huku yeye akiwasha yake ambayo aliweka namba isiyofahamika kwa watu wengine.

    Safari ikaanza rasmi. Emmy alikuwa na pesa na Lameck alikuwa na pesa vilevile.



    ****



    SAID NDULA. Kijana machachali katika umri wa miaka thelathini alikuwa akivinjari katika kiti cha ofisi ya baba yake mzee Ndula Baliwena. Aliitazama picha ya baba yake na kujisifia kuwa na baba kama yule.

    Baba aliyempigania hadi kufikia hadhi aliyonayo.

    Said alikuwa anamngojea baba yake akitoka msikitini kuswali waweze kubadilishana mambo mawili matatu.

    Lakini alikuwa na jingine kubwa la kumshirikisha.

    Aliona dakika azisogei, kimuhemuhe cha kumwonyesha baba yake kuwa na yeye anaweza mambo kilikuwa kimemtawala.

    Aliamini fika kwa taarifa ile baba yake lazima angempa sifa.

    Ulikuwa mtihani ambao baba yake aliusahau kabisa na kutambua kuwa huenda ulishindikana. Kwa kuwa hakuwepo wa kuuliza wamefikia wapi basi akauweka kapuni kama ilivyo kwa matukio mengine.

    Baadaye mzee Ndula akarejea ofisini.

    Akamkuta mwanaye wa kiume ambaye wamejikuta wakiendana sana.

    Said akasimama kikakamavu akampigia saluti baba yake, mzee ndula akatikisa kichwa kisha akachukua nafasi katika kiti cha kuzunguka.

    “Niambie dume la simba.”

    “Shwari..asalamaleykum shehe..”

    “Kha..asalamaleykum wakati hata msikiti hujui ulipo kichaa kweli wewe.” Mzee Ndulla alitania huku akichukua makablasha kadha wa kadha kutoka katika kabati kuukuu. Said akajichekesha kidogo, kisha akakaa vyema katika kiti.

    Akakukmbuka kuwa mzee wake huwa hapendi maongezi mengi akitia utani kidogo kinachofuata ni kwenda katika hoja.

    “Mzee....” alianza kuzungumza, Mzee Ndula akamkatisha.

    “Nani mzee wako...mi kijana bwana...” akatia utani mwingine.

    CID mpelelezi sajenti Said Ndula akatokwa na kicheko kikubwa.

    Wakarushiana maneno mawili matatu kisha Said akaingia katika hoja.

    “Mzee..unamkumbuka Devotha....”

    “Devotha yupi?” Ndula aliuliza huku akisita kuendelea kupekua makablasha.

    “Ile kesi namba S.6709/09/78 MAUAJI KWA KUTUMIA SUMU.” Alijibu Said.

    Mzee akafanya tathmini kidogo.

    “Nadhani naikumbuka si ya huyu mama bongebonge huyu. Mtoto wake yule alikuja kugalagala hapa kituoni, anaitwa nani sijui Emmy kitu kama hicho”

    “Huyo huyo. Mh mzee umemkumbuka hadi Emmy duh. Kuna jambo nitamshirikisha mama.” Said alimtania tena mzee wake.

    “Wee nakuweka jela miezi sita ukinigombanisha na mama yako” Mzee naye akatania, ilikuwa burudani ya kipekee.

    “Kimetokea nini?” mzee aliuliza kiutafiti. Sasa hakuwa na utani.

    “Kuna mambo yamejipa.”

    “Kivipi.”

    “Ile namba ya muuaji jana usiku nimeipata hewani.”

    “Acha masihala we dogo, una uhakika.”

    “Mi nataniana na wazee kama wewe tangu lini?” Said akamtupia dongo baba yake ambaye pia alikuwa mkubwa wake kikazi.

    Mzee akakuna kichwa chake baada ya kuwa ameivua kofia yake.

    “Na asubuhi nimeenda kwenye kampuni ya simu nimepewa maelezo yote.”

    “Kwamba.....” Mzee akawa na haraka.

    “Jamaa yupo hapa hapa Dar lakini kila mara minara inahama. Mara mnara wa Ubongo, Mbezi, na mara ya mwisho mnara ulioisoma namba hiyo ulikuwa wa Kibaha.” Said akasema kwa utulivu.

    “Bwege atakuwa anasafiri huyo.” Mzee Ndula akawaka kisha akatoa tusi zito. Hakuna aliyeshangaa kati yao. Hali hiyo ilikuwa ya kawaida sana katika sekta yao.

    “Hawezi kuniacha wallah labda aizime hiyo simu upesi.” Aliapa Said.

    “Na kama si yeye anayeitumia hiyo simu.” Mzee aliuliza.

    “Huyo huyo mwenye hiyo simu atatusaidia upelelezi. Nina hamu na kazi ujue.” Said alijibu.

    Mzee Ndula, akanyanyua mkonga wa simu na kubonyeza namba kadhaa, simu ikaita kidogo ikapokelewa.

    “Sajenti namwagiza kijana kwako mpe ushirikiano wa haraka sana.” Alizungumza kisha akakata simu.

    “Kazi ni kwako, cha msingi uwe makini si unajua tena we n’do kidume wa ukweli, ukifyatuliwa za kichwa nitapagawa. We ukiona mambo ni magumu achana na yo hiyo kesi sawa mwanangu.” Mzee Ndula akamsihi mwanaye, upendo wa dhati ukajichora katika paji la uso wake. Said akatabasamu.



    ***

     Wivu wa mapenzi ni kizuizi kingine katika maisha ya kawaida. Kizuizi hiki humfanya muhusika awe mtumwa katika maamuzi yake na anaweza kutenda lolote ilimradi tu aifurahishe nafsi yake.

    Kwa mwanamke mwenye kisasi kama Mariam ilikuwa ngumu kumtegemea anaweza kuwa na nafasia ya kuhifadhi upendo.

    Lakini moyo wa mtu ni mpana na ajuaye ni yeye na Mungu wake.

    Maria kwa kipindi kifupi alichofahamiana na Jose, aliamini katika hisia zake kuwa kuna jambo alitakiwa kujadili na kijana huyu.

    Jambo lenyewe lilikuwa mapenzi.

    Maria alitamani kujadili na Jose siku ile alipomsaidia baada ya kutupwa nje ya gari na bwana Lameck. Lakini Jose alikuwa na haraka na alihitaji sana kuonana na mwanamke mwingine.

    Wivu ukamchapa konde Maria, akatetereka na kuamini kuwa yule anayeenda kuonana naye ni mpenzi wake.

    Licha ya kwamba alidai kuwa usiku huo atakuwa naye na watazungumza mengi, hiyo haikutosha kumshawishi Maria.

    Baada tu ya watatu hawa kutoweka Maria alianza kuwafuatilia kwa ukaribu bila ya Jose kufahamu nini kinaendelea. Wale wenzake walijua nini kinaendelea.

    Baada ya kulifikia eneo la tukio. Maria aliegesha gari yake mbali zaidi na wenzake.

    Akachezesha akili upesi hakutaka kumngoja Jose amalize maongezi yake na yule mwanamke baada ya kuona amechukua kitambo kirefu.

    Katika kunyatia kwake anakutana na jambo ambalo aliliwaza.

    Wawili hawa walikuwa wanapapasana. Roho ikamuuma na kuamini kuwa alikuwa sawa kabisa kuweka hisia zake kuwa Jose ana mahusiano na huyo mwanamke.

    Kama hiyo haitoshi wakavutana na kujitupa katika michanga.

    Hapa sasa uvumilivu ukamshinda hakuwa tayari kuona nini kinachoenda kutokea. Akajiweka mbali zaidi. Akajiweka nyuma ya mti, akatoa sigara katika koti lake kubwa, akataka kuiwasha, akagundua kuwa aliacha kiberiti katika gari aliyokuja nayo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akajikongoja taratibu hadi akaifikia gari, akatwaa kiberiti.

    Ule mwendo wa kuifikia gari na kutwaa kiberiti lilikuwa kosa kubwa sana. Alimuachia Emmy upenyo wa kukitwaa kisu kisha akafanya tendo ambalo liliipa ardhi ladha tamu ya damu na pia kumweka Jose B wa ukweli katika kimya kikubwa.

    Sasa Maria alirejea akiwa amepandwa na maruhani ya kumshambulia huyo mwanamke.

    Akafika mbiombio akiwa na hasira, akapokelewa na maajabu makubwa.

    Nani aliyeizoea damu ya mwanadamu?

    Wapo lakini sio Maria.

    Akadondosha sigara na kutimua mbio kali.

    Kitimtim.......

    Maria akasahau kuwa ule ulikuwa ni usiku. Akajikuta anapiga mayowe.

    Wale wenzake ambao walikuwa katika gari nyingine, zote za kukodi walizisikia zile kelele, wakajiweka tayari na silaha mikononi.

    Akatokea Maria akiwa anapiga mayowe bado.

    Akawafanyia ishara ya kuwaita

    Wakatii.

    Akawasogeza hadi ulipokuwa mwili wa Jose. Wakastaajabu.

    Jose alikuwa amejeruhiwa vibaya na alikuwa ametulia tuli.

    “Mbebeni upesi...” aliamrisha Maria.

    Wakafanya alivyotaka, hadi katika gari, alikuwa anavuja damu bado.

    Damu kutoka sehemu za siri.

    “Yule malaya alitaka kumuua au amemuua?” aliuliza Maria.

    Hakuna aliyejibu.

    Safari ya kuelekea hospitali, usiku uleule.



    ***



    Baada ya Said kutoweka ofisini kwake, mzee Ndula alikumbwa na pepo la ajabu, pepo lililomshawishi kufanya jambo.

    Akainyanyua simu yake. Akampigia Said.

    “Njoo mara moja.” Akaamuru.

    Baada ya dakika tano akarejea.

    “Kumbe ulikuwa hujafika mbali sana.”

    “Nilikuwa nazungumza na katibu muhtasi wako.”

    “Unamuuliza kama huwa napokea wageni wa kike ili ukaseme kwa mamako.” Alitania mzee Ndula, Said akacheka.

    “Sikia nilikuwa nina wazo moja hivi kama litafaa.”

    “Wazo gani?”

    “Hivi kwanini usimfuatilie huyo jamaa kimya kimya, maana milolongo ya jeshi la polisi nadhani unaijua...watakuchelewesha hapo mpaka atokomee.”

    Said akatabasamu kisha akamjibu mzee wake, “Yaani kama vile ulikuwa katika kichwa changu. Nilikuwa nimejiuliza sana.”

    “Basi fanya hivyo, wewe fuatilia kimyakimya..halafu sikia....kama akiwa vizuri we zungumza naye myamalize.”

    Alinong’ona mzee Ndulla.

    Saidi akaelewa alichomaanisha.

    “Nadhani pikipiki itanifaa zaidi.” Alisema Said.

    Mzee akamwongoza hadi katika ofisi ambayo alitakiwa kuandika kuwa amechukua pikipiki. Baada ya nusu saa Said Ndula akiwa katika pikipiki kubwa aina ya Baja, alikuwa anapepea kwa kasi kubwa.

    Alikuwa anamsaka muuaji.

    Mawasiliano yake na kampuni ile ya simu yalikuwa ni ya mara kwa mara na alipewa ushirikiano wa hali ya juu sana.

    Simu yake ilijibiwa upesi sana.

    “Kilometa mbili kutoka hapo ulipo, mtandao wa Morogoro mjini unaisoma simu yake.....” yalikuwa majibu kutoka upande wa pili.

    Said akaipanda tena pikipiki yake na kuzidi kukata upepo.

    Hatimaye akalifikia basi ambalo lilikuwa limembeba aliyekuwa anaitumia simu ile.

    Said akaongeza mwendo, akaipita ile basi, akasimamisha pikipiki kwa mbele na kisha akapunga mkono wa kuisimamisha.

    Gari ikapunguza mwendo na hatimaye ikasimama.

    Said akajitambulisha kuwa yeye ni askari, akaonyesha kitambulisho chake. Kisha akaingia garini.

    Abiria walikuwa wametulia tuli wakiendelea na mambo yao.

    “Mwela yule..” Lameck alimnong’oneza Emmy aliyekuwa ametulia akijisomea gazeti.

    “Mwela ndio nani?”

    “Askari polisi.” Alijibu kwa sauti ya chini yule mwanajeshi.

    Emmy akashtuka, akalisahau gazeti lake, akabaki kushangaa. Ile kitendo cha kusikia juu ya askari kilimkumbusha kuwa alitoka kumtia kisu katika sehemu za siri. Jose B wa ukweli.

    “Vipi mbona unashtuka.” Lameck alimuuliza.

    “Wananitafuta mimi Lameck.” Alijibu huku akitetemeka.

    “Kivipi sasa, acha woga.”

    “Ni mimi kweli.” Alisisitiza Emmy.

    Macho ya yule askari yalikuwa makini kutazama huku na kule. Katika kusaili abiria mwenye wasiwasi hatimaye alipitisha kwa sekunde kadhaa macho katika uso wa Emmy. Akamwona akiwa katika hofu kuu.

    Alijaribu tena na tena kumtazama mtu mwingine mwenye hofu, hakuambulia.

    Akafanya tendo alilotegemea kulifanya.

    Akabofya kwa siri kubwa simu yake, macho yakawa yanatazama ni wapi mlio utatokea. Hakuna aliyemshtukia alipofanya vile, kasoro jicho la Lameck tu nd’o liling’amua jambo hili.

    Lakini hakujua nia yake na alikuwa amechelewa sana kufanya maamuzi.

    Mara simu yake ikaita.

    Ilikuwa katika koti lake.

    Upesi yule askari akawahi kumkabili.

    Lameck hakufanya ubishi wowote.

    Akatiwa pingu.

    Watu wakabaki kushangaa ni kipi kinatokea.

    “Upo chini ya ulinzi mkali, ukileta ubishi nakulipua.” Said akatishia. Lameck akatii.

    “Emmy fuatana nami.” Lameck akamwambia Emmy ambaye alikuwa anatokwa jasho kwa hofu.

    “Mnaweza kuendelea na safari jamani na mfike salama.” Said aliwaruhusu abiria wengine wakaondoka zao.

    Emmy, na Lameck wakashushwa eneo la Mikese, jirani na mji wa Morogoro.

    Kwa umbile la nje, Lameck alionekana kama bwege fulani, na hata utulivu aliouonyesha wakati wa kukamatwa ulikuwa mkubwa sana.

    Hakuna ambaye angeweza kumdhania kuwa alifuzu mafunzo ya jeshi na kisha kuchaguliwa kwenda kulinda amani nchini Sudan.

    “Rafiki, uliyemuua ni nani na kwa nini ulimuua.” Said alianza kukoroma.

    Lameck hakujibu kitu. Alibaki kumkodolea macho.

    “Rafiki nazungumza na wewe, mimi sitaki kukuchelewesha na wala sifikirii kukuacha na hizo pingu kwa muda mrefu mimi nataka kukuruhusu uondoke zako.”

    Lameck kimya.

    “Unamkumbuka Devotha?” swali hilo sasa likamshtua Emmy na Lameck.

    “Devotha?” aliuliza huku akitangaza wasiwasi wake.

    “Yule mama uliyemuua kwa kumpaka sumu, vipi dada ulikuwa unafahamu mumeo ni muuaji?” Said alifanya sanifu.

    “Halafu wewe ni kama...nani vile wewe sio Emmy?” askari aliuliza.

    Emmy akakumbwa na mshangao. “Ni mimi”

    “Kwa hiyo ulishirikiana na huyu jamaa kumuua mama yako mzazi. Halafu ukaja kutulilia kule kituoni.” Askari alizungumza kwa umakini zaidi.

    Lameck akafedheheka sana, siri ilikuwa nje kuwa ameua.

    Na huyu bwana hakuonekana kubahatisha anachokizungumza, Lameck akajiuliza ni kipi kimempa uhakika kiasi hicho hadi kuja kumuumbua mbele ya Emmy.

    Ni hapo ndipo alipoikumbuka simu. Simu aliyoitumia kuwasiliana na mama yake Emmy ndiyo ambayo alikuwa ameitumia katika siku za hivi karibuni.

    Akakumbwa na hasira akasonya.

    Said akacheka. Kisha akabonyeza namba kadhaa, akaomba msaada katika kituo kilichopo karibu naye.

    Lameck akamtazama Said usoni kwa macho yenye huruma.

    “Si umegoma kukiri sasa wewe na huyu mwenzako jela hiyoo inawaita.” Alizidi kupigilia msumari.

    “Mimi sijashirikiana na mtu jamani mimi sijamuua mama yangu..na sijui aliyeua..” Emmy alianza kulia akijitetea. Wakati huo walikuwa wameunganishwa kwa kutumia pingu moja na katu wasingeweza kukimbia. Maana mmoja akichoka basi mwingine hawezi kwenda.

    Kitendo cha yule askari kuomba msaada, kilimaan isha kuwa lazima Lameck na Emmy watarudishwa Dar es salaam na katika kipindi hicho siri zote zinaenda kuanikwa hadharani.

    Emmy angemchukia maisha mwake na jamii ingemlaani.

    Lameck akaamua kumwonyesha yule askari kuwa namba anayojaribu kucheza nayo ni namba nyingine.

    Kilikuwa kitendo cha sekunde zisizozidi mbili.

    Mjeshi alirudi nyuma kidogo kisha akiwa mzimamzima akakiachia kichwa chake kilichokomaa kwa kuvunja matofali jeshini.

    Kwa uzito usiopimika kwa wepesi kikatua katika kichwa cha yule askari ambaye alikuwa hajajiandaa kwa shambulizi lile.

    Alipotua chini hakupata nafasi ya kusema neno. Mguu mzito uliozoea mchamchaka na kichurachura ukanyanyuka na kutua katika kifua cha yule askari.

    Akapata nafasi ya kukohoa damu lakini hakusema neno lolote.

    Emmy alikuwa haelewi nini kinachoendelea.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Lameck akamsogelea yule askari akampekua na kuupata funguo.

    Akazifungua pingu.

    “Emmy ubaki salama.......” Lameck aliyasema hayo baada ya kuisikia gari ya polisi ikipiga king’ora kwa mbwembwe.

    Aliamini fika kuwa akiwa pamoja na Emmy lazima mambo yataharibika mbele ya safari, na alijua kuwa maneno ya askari yalikuwa yamemvuruga sana.

    Emmy alidhani Lameck anaondoka hivi hivi.



    ****



    Lameck hakutaka kuhangaika, akauvaa unyama mkubwa. Akaruka teke kubwa hewani kisha akazunguka mithili ya yule mcheza filamu za mapigano.. Jean Claude Vandamme, barabara likatua katika shingo ya Emmy.

    Ni hicho Lameck alikusudia, Emmy akaanguka na kupoteza fahamu.

    Mjeshi akatokomea vichakani.

    Akaacha ile mizoga pale chini.

    Lameck akaamua kujiweka mbali na ukweli ambao ungeweza kumwingiza matatani na kumtia aibu kubwa sana.



    Wakati Emmy akipokea pigo hili na kupoteza fahamu, Maalim Shabani alikuwa makini akiingojea simu kutoka kwa mwanadada huyu.

    Tayari alikuwa amemruhusu James kuendelea na mambo mengine huku akimzuga kuwa anaendelea na michakato ya kumsaidia.

    Masaa yakakatika bila kupokea simu aina yoyote ile. Alijaribu kumpigia Emmy lakini simu yake haikuwa inapatikana.

    Maalim akajiuliza kulikoni lakini hakulipata jawabu.

    Akaendelea kuvuta subira, hatimaye jioni ikaingia.

    Maalim akaingiwa na uoga, akahisi huenda Emmy atakuwa amemshirikisha James na sasa James ana hasira naye.

    Alijiuliza mengi, mwishowe akaamua kurejea nyumbani kwake akiwa hana jibu sahihi.



    ****



    James alifika maeneo ya nyumbani kwake alfajiri sana, akashangazwa na ukimya uliokuwa pale. Na cha ajabu zaidi ni geti kuwa wazi. Hili aliliona kuanzia mbali.

    James akapiga hatua ndogo ndogo huku akipiga mluzi.

    Hatua zake zikakoma ghafla. Kuna kitu alikuwa amekanyaga.

    Akateleza kidogo. Akasita, akapiga hatua moja mbele kisha akageuka kutazama nyuma.

    “Ina maana mvua ilinyesha?” alijiuliza, kisha akawasha simu yake. Akamulika eneo lile.

    Lahaulah!!

    Damu!! ilikuwa damu nzito.

    James akatokwa na mguno wa mshangao.

    Eneo lile lingekuwa linapitika magari angeweza kuwaza kuwa huenda ni paka amegongwa ama mbwa, au hata binadamu pengine. Lakini pale hapakuwa pakipitika kwa gari.

    James akastaajabu. Kisha akapuuzia na kukaza mwendo kulikaribia geti zaidi.

    Akalifikia geti, mlinzi alikuwa amelala na harufu ya pombe za kienyeji ilitawala eneo lile. James akamtazama kwa hasira kisha akasonya. Akapita bila kulifunga geti.

    Miguu ikaanza kuishiwa nguvu alipowaza kuwa baada ya sekunde kadhaa atakuwa chumbani na mkewe, hakuwa amejiandaa kuulizwa maswali ya ni wapi alikuwa na alikuwa anafanya nini, na ni kwa nini hakuaga.

    Liwalo na liwe.

    Akapitia mlango wa sebuleni, hatua moja baada ya nyingine akakifikia chumba chake.

    Mlango ulikuwa umerudishiwa. Akajaribu kuufungua bila kugonga.

    Haukufunguka.

    “Mh leo amejifungia ndani kabisa?” alijiuliza.

    Mara nyingine akajaribu kuugonga mlango kwa utaratibu.

    “Dear.......dear......Emmy, we Emmy amka unifungulie.” Alisema kwa kunong’oneza.

    Kimya kiliendelea.

    Jazba ikaanza kumpanda James, akaongeza ujazo katika kuugonga mlango.

    Bado Emmy hakufungua.

    James akatokomea na kuelekea jikoni, sasa hakuwa katika kunyata tena, akapapasa juu ya kabati la kuhifadhi vyombo. Akaukuta ufunguo wa ziada wa chumba chao.

    Akaufikia mlango na kuufungua.

    Akasukuma kwa nguvu. Akakutana na kigiza.

    “Ina maana wakati wote nabisha hodi hunisikii ama?” alifoka.

    Hakuna majibu kama awali.

    Akawasha taa.

    Akakutana na mashuka yaliyokuwa katika mpangilio wa shaghalabaghala, hapakuwa na mwanadamu pale ndani. James hakuamini akayaendea mashuka na kupapasa, hali ikawa ile ile.

    Akataharuki. Akakosa utulivu. Akatoka mbio mbio hadi katika chumba cha akina Grace na Gloria. Akabisha hodi akajibiwa, baada ya dakika kadhaa kikafunguliwa.

    “Wifi yako yuko wapi....wewe dada yako alienda wapi?” aliuliza bila kujibu salamu walizotoa.

    “Dada?” aliuliza.

    “Ndio kwani hujasikia nilichouliza au?” akafoka James

    “Mbona yupo chumbani kwake. Eti Gloria, si alilala jamani”



    Yupo chumbani mbona mi sijamuona??” alifoka.

    Grace na Gloria nao wakaenda kufanya ushahidi wa macho.

    Hakika Emmy hakuwepo. James akaona hawana msaada kwake, akapiga hatua kubwa kubwa, ikawa kama anakimbia na nusu anatembea.

    Akamfikia mlinzi.

    Bado alikuwa anakoroma.

    James akashindwa kujizuia akamnasa kofi yule mzee ambaye alikuwa anamzidi umri.

    Mzee akakurupuka, akataka kukimbia. James akamkamata.

    “Shkamoo bosi.” Yule babu kwa hofu alijikuta anatoa salamu.

    James akapiga kite cha ghadhabu.

    “Mke wangu ametoka usiku huu.”

    “Nani Emmy?” aliuliza swali la kijinga. James hakujibu. Yule mzee akajirekebisha, “Ahh alitoka lakini hakusema kama anaenda mbali, kuna vijana wawili walikuja hapa nikawakatalia katakata kuingia ndani, akatokea Emmy akafuatana nao..”

    “Vijana wawili? Saa ngapi.”

    “Alfajiri ilikuwa inakaribia”

    “Kwa hiyo alivyotoka hakurudi tena?”

    “Hajarudi tena. Aah labda alirudi lakini mh..” akakosa cha kusema.

    James akaikumbuka ile damu.

    Hofu ikatanda.

    Akahisi kuna jambo baya limemtokea mkewe. Akataka kumuuliza kitu mlinzi, lakini akahisi uelewa wake katika jambo hilo ni mdogo sana.

    Akaondoka pale bila kuaga. Akaingia ndani.

    Huko hakukaa sana. Akakumbuka jambo jingine.

    Mariam na Jose B.

    “Hawa viumbe wananifuatilia nyendo zangu na wananifanya wanavyotaka, sasa mbona hawasemi wanataka malipo yapi? Mwanzo wamemchukua mateka mdogo wa Emmy, sasa wameamua kumchukua Emmy kabisa.” Akatoa tusi.

    Kitanda kikawa kichungu alipoikumbuka damu yake katika tumbo la Emmy. Akili ikachachamaa, akatamani kuwashirikisha polisi lakini akatambua kuwa ingechukua miaka kupata ufumbuzi.

    Akaangaza huku na huko kama kuna ujumbe wowote Emmy ameuacha au hata jambo lolote ambalo Emmy alilifanya la mwisho kabla ya kutoka katika chumba kile.

    Kikaratasi kidogo kikamvutia akakitazama kwa dharau. Hakikuwa na ujumbe wenye uzito wowote. Zilikuwa tarakimu kadhaa. Zilirandana na namba za simu.

    Akakitwaa na kukitazama.

    Namba hizo amewahi kuziona mahali.

    Akaziingiza katika simu yake kisha akafanya jaribio la kupiga.

    Alhamdulilah. Jina likatokea.

    Maalim Shaban.

    James akajikuta katika mtetemo wa kushangaza, baada ya dakika kadhaa jasho likaanza kumtiririka. Mwandiko ulioandika namba zile ulikuwa wa mkewe.

    Emmy.

    Namba za Maalim Shaban? Kivipi?

    “Bwege naye kumbe walewale ameniuza huyu....yaani ameniweka gesti masaa yote yale kumbe ananiuza.......naua.” aliapa.

    Harakaharaka za Emmy alipokuwa anatoroka nd’o zilimfanya adondoshe kikaratasi kile ambacho alihifadhi namba zile siku aliyopigiwa na Maalim Shaban, hakutaka kufanya kosa kama alilofanya kwa kuziacha namba za Sam wa pili na hatimaye kufumaniwa na mumewe. Sasa alikuwa makini na kila namba yenye utata aliihifadhi pembeni.

    Umakini wake huo, amedondosha ile namba na sasa imeokotwa.

    James hakuweza kupoteza dakika nyingine pale ndani.

    Alitoweka, kisha akampigia simu Maalim.

    Maalim alishtushwa na mlio wa simu akiwa amepitiwa na usingizi nyumbani kwake.

    Alidhani atakuwa ni Emmy, haikuwa hivyo.

    Alikuwa James.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Sema kaka....” alianza.

    “Poa..vipi upo wapi..kuna wazo nimepata.” James alizungumza kwa sauti ya chini.

    “Nyumbani kwangu huku.”

    “Sipafahamu lakini.”

    Maalim akamuelekeza kwa umakini kabisa. Alikuwa ametokwa na macho ya tamaa, aliamini fika kuwa James ni bwege na ana pesa za kuchezea. Akaamini kuwa hilo wazo kama linamuhusisha lazima apate mgao fulani. Wazo la kuwa huenda Emmy atakuwa amemshirikisha mumewe juu ya Maalim alilitupilia mbali maana Emmy hakuwa mjinga wa kujisifia kwa mumewe kuwa ameshiriki mapenzi na Lameck ambaye ni baba yake mdogo.

    James akaelewa alivyoelekezwa.

    “Baada ya nusu saa nitakuwa hapo kaka.” Alisema James.

    Maalim akafarijika kusikia ameitwa kaka. Akaamini James alikuwa anamtegemea kwa sana.

    Laiti kama Maalim huyu angetambua kuwa James anakuja akiwa amekabwa na hasira.

    Angeukimbia mji mapema tu.



    ****



    Mida ambayo James alikuwa barabarani akiitafuta barabara ambayo itamfikisha nyumbani kwa Maalim. Hali ya Jose B wa ukweli ilikuwa tata bado. Alikuwa amepoteza damu nyingi sana na hakuwa amezinduka. Maria alipoona hali si shwari aliamua kumuita daktari pembeni waweze kuzungumza.

    “Nipe uhakika daktari, kuna kupona hapa?”

    “Mh...yupo katika hali mbaya lakini tunaamini atapona. Kuna mshtuko amepata, mshtuko mkubwa nd’o maana amechelewa kuzinduka. Kwani vipi.”

    “Nahitaji sana kumsikia. Nahitaji kujua chanzo cha kuchomwa kwake.”

    “Twende ofisini.”

    Wakaongozana hadi ofisini.

    “Ulikuwa na maana gani?”

    “Mimi na wewe tuzungumze.” Alijibu Maria. Sasa hakuwa na uso wa mapenzi tena wala ile huruma yake, alikuwa anataka kuikamilisha kazi yake.

    “Daktari, nahitaji jamaa aamshwe.” Maria alisema.

    “Kivipi?”

    “Dokta..wewe ni mtaalamu, si lazima niseme kwamba nahitaji apigwe maji ya uamsho.” Alikazia Maria, daktari hakutegemea kama msichana kama yule anaweza kuwa anayafahamu maji hayo.

    “Mh hapana aisee....unataka kuniuzia kesi.”

    Maria alimtazama daktari, akalithaminisha na koti lake akamwona ana njaa na alihitaji wazungumze biashara.

    “Nina laki moja. Nisaidie.”

    “Ipo wapi?”

    Maria akazama mkobani akatoka na pesa hiyo.

    Akamkabidhi daktari.

    “Ni mimi wewe na mgonjwa sitaki shahidi mwingine.” Daktari alitoa onyo. Maria akamuelewa.

    Baada ya nusu saa.

    Daktari alizidisha maji ya uamsho kwa mgonjwa aliyepoteza fahamu, maji haya yana ‘insurini’ ndani yake, mgonjwa aliyepoteza fahamu akijazwa chupa moja huweza kuamka, lakini ikishindikana kabisa kwa mgonjwa mahututi. Chupa mbili, na zikiwa tatu basi atakaa sawa kwa muda na akilala ni moja kwa moja.

    Watu wenye wagonjwa waliokata tamaa hufanya hivi ili waweze kuzungumza nao kwa mara ya mwisho.

    Maria aliijua mbinu siku aliyokuwa anahitaji kupata namba kadhaa za siri kutoka kwa Musa.

    Kijana aliyemuokoa kutoka katika domo la kifo.

    Jose B hatimaye akaamka.

    Ana kwa ana na Maria.

    Maria hakutaka kupoteza wakati.

    Akamshambulia kwa maswali kadhaa.

    Akapata majibu ya kustaajabisha, kwanza vifo vya Deo na Bibiana, pili mahusiano kati ya Emmy na Lameck.

    “Na wewe na huyo Emmy mlikuwaje tena.”

    Jose B akajieleza jinsi alivyomuuzia siri. Baadaye wakaingia katika malipo ya kuburudishana. Jose B alikuwa mchangamfu sana, aliamini kuwa amepona kabisa na hana tatizo la ziada. Hakujua kuwa alikuwa katika kuishi kwa nguvu za ‘insurini’ ambayo haidumu kwa muda mrefu.

    Simulizi ya Jose B ilikuwa ya kufurahisha sana. Maria alitamani kama kijana yule angeendelea kuishi ili aweze kushirikiana naye zaidi na zaidi.

    Lakini katu isingeweza kuwa hivyo.

    Hatimaye akalala tena.

    Hakulala na siri zake.

    Siri zikabaki duniani.

    Jose B akazikimbilia pepo.

    Na historia yake ikakomea hapo!!!



    ****



    Kikosi kilichopigiwa simu kwenda kutoa msaada, kiliipita mizoga iliyojilaza chini, mmoja wa kike na mwingine wa kiume.

    Waliangaza huku na huko kama watamuona muhusika.

    Hawakumuona. Wakajaribu kupiga simu, ikawa inaita bila kupokelewa.

    Hawakukumbuka kabisa juu ya vile viwiliwili kule barabarani.

    Mpita njia aliisikia simu inaita katika mifuko ya mwanadamu aliyelala chini katika hali ya utulivu, midomo yake ikiwa imegandiana damu.

    Alitamani kumpekua aweze kuichukua ile simu lakini akaingiwa na hofu mara ya kwanza.

    Mara ya pili tena uoga ukatanda. Aliangaza huku na huko hakuona mtu wa kumzuia.

    Hatimaye akaamua kuzama mifukoni, akachomoka na ile simu.

    Akaificha mfukoni bila kuizima.

    Ama kwa hakika kama mtu sio mwizi basi sio mwizi tu.

    Hakukumbuka kuizima simu.

    Askari walikuwa wamechezwa machale tayari, lazima kulikuwa kuna tatizo. Wakashuka kutoka katika magari yao.

    Wakaanza kufanya msako wa mtu na mtu.

    Simu ikaita katika mifuko ya raia mwema.

    Askari akang’amua hilo.

    Raia mwema akakosa maamuzi sahihi, akataka kuitoa simu ile.Lakini akawa amechelewa. Akawekwa chini ya ulinzi.

    Makofi mawili matatu akasema anachokijua.

    Akawapeleka katika ile mizoga.

    Ni hii waliipita wakati wanasogea eneo lile.

    Kama yule raia alitegemea kuwa ataachiwa kirahisi, haikuwa hivyo.

    Alitakiwa kusaidia upelelezi.

    Miili ile ikachukuliwa kwa uangalifu mkubwa.

    Walipofika hospitali.

    Ni Emmy aliyekuwa hai. Said Ndula alikuwa ameaga dunia tayari.

    Mapigo mawili muhimu na mazito kutoka kwa mjeshi yaliuondoa uhai wake.

    Emmy alirejewa na fahamu baada ya masaa kumi.



    Alipotulia kabisa alianza kuelezea kila anachojua kuhusiana na tukio lile.



    Alikumbuka kumtaja Lameck kama muuaji wa mama yake mzazi, pia muuaji wa yule askari.



    Kuzinduka kwa Emmy nd’o ikawa pona pona ya raia mwema.

    Simulizi ya Emmy nayo iliwasisimua wengi, hasahasa katika kipengele cha kwamba muuaji ni mwanajeshi. Tena wa kimataifa.

    “Kwanini mlikua mnatoroka?”

    “Alinishawishi baada ya kugundua kuwa mume wangu amegundua uhusiano kati yangu na yeye. Alinambia James ana mpango wa kuniua.”

    Askari aliyekuwa anasikiliza maelezo haya alikuna kichwa kwa tafakari. Aliamini kuwa palikuwa na mtihani mkubwa sana.

    Lameck ni mwanajeshi.

    Lakini ameua, amemuua askari na aliwahi kuua hapo kabla.

    Kizungumkuti.



    Mpelelezi akaachiwa kesi ile aendelee nayo.

    Upelelezi wake ukaanzia kwa Emmy kisha akaamua kumfikia mzazi wa marehemu.

    Ambaye ni mkuu wa kituo kikubwa cha polisi.

    Mzee Ndula.

    Akaipanga siku ya kumfikia na mbinu za kumwingia ili apate mawili matatu.



    ****



    JAMES alifika nyumbani kwa Maalim kwa kufuata maelekezo yote aliyopewa. Alimkuta Maalim nje ya nyumba akimngoja, alikuwa amevalia vazi lake jeupe la kanzu na viatu vya wazi.

    Baada ya salamu za mapokezi na maulizo ya hapa na pale ya kitanzania. Hatimaye alikaribishwa ndani.

    Mfumo wa nyumba ndogo ya kupanga aliyokuwa anaishi Maalim, ulimfurahisha sana James kwa jambo ambalo alikuwa amelipanga kichwani.

    “Samahani kwa kukusumbua usiku mnene namna hii.”

    “Usijali yakhe, ni alfajiri sasa panakucha. Hapa silali tena mpaka pakuche.” Maalim alimtoa hofu James.

    “Naweza kupata maji ya kunywa?” James aliuliza.

    Maalim akasimama na kukiendea chumba cha pili.

    James akautumia upenyo huo wa dakika chache kuitwaa simu ya Maalim aliyokuwa pale mezani. Akajaribu kutaka kuingiza namba za mkewe. Akakuta simu imefungwa kwa namba za siri.

    Akasonya na kuirudisha mezani.

    Hasira ikazidi kumwongoza.

    Akaikosa subira.

    Wakati anakunywa yale maji alimsoma Maalim na kumwona kama kijana muadilifu asiyekuwa na mashaka, lakini uso wake haukuwa na furaha kabisa.



    “Maalim, dili letu linaendaje?” James aliuliza kinafiki.

    “Dili? Dili linaenda poa sana. Ujue nimejaribu kuangali ile simu katika mtandao sijui nani ameiripoti hadi ikafungiwa....aisee wametuzidi ujanja. Kwa hiyo haujaona meseji?” alijibu bila kuwa na utulivu.

    James hakusema neno.

    “Lakini ujue nini? Mkeo.....sidhani kama hisia zako zipo sawa kwa kumwona mkeo muongo yaani mimi nahisi wana mawasiliano ya kawaida tu.” Maalim alizidi kumtia hasira James bila kujua.

    “Fala ananiona bwege sana.” Aliwaza James huku akimtafakari Maalim.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hivi unamkumbuka vizuri Emmy lakini? Maana ni mud asana tangu uonane naye pale ofisini.”

    “Aisee kitambo kirefu, yaani nikimuona sidhani kama nitamkumbuka. Ubaya zaidi hata namba yake sina wala yeye hana ya kwangu.” Alijibu huku akijichekesha Maalim.

    James akakunja ndita, akauma meno yake kwa nguvu sana kuidhibiti hasira.

    “Yaani nimechanganyikiwa hapa rafiki yangu. Sijui hata itakuwaje maana nampenda sana mke wangu nampenda sana. Na ana mtoto wangu tumboni.” Alilalamika James.

    Kwa akili ya harakaharaka akagundua ni kiasi gani tayari Maalim amedanganyika.

    Akaingiza mtego.

    “Hebu, simu yako ina kasalio kidogo nimcheki jamaa yangu hapa, aisee mimi naenda ka mganga ikibidi lakini huyu mtoto sitaki kumpoteza.” Aliongea kama aliyechanganyikiwa.

    Maalim akacheka ka sauti ya juu.

    Akatoa namba za siri katika simu yake na kumpatia James.

    James hakuingiza namba nyingine tofauti na za mkewe.

    “Emmy dili....” jina likasomeka vile.

    James akajikaza, kisha akamuagiza Maalim maji mengine ya kunywa.

    Maalim Shaban aliporejea na maji ya kunywa badala ya kuyapokea James aliyasukuma pembeni kisha akamrukia Maalim na kumkaba shati. Hasira ilikuwa imevuka mipaka tayari.

    Maalim hakutegemea ujio ule. Akakosa muhimili, akayumba kidogo aanguke, James akawahi kumuokoa.

    “Maalim...nahitaji kujua ulikuwa unawasiliana nini na Emmy, uliwasiliana nini na mke wangu. Na sasa yupo wapi? Nahitaji majibu ya maswali hayo. Kabla hatujaendelea na mengine”

    “Nani Mimi?” Maalim akauliza swali la kizembe, ambalo huulizwa na watu wengi hasahasa akiwa hajategemea kuulizwa swali.

    James akamnasa kofi moja.

    Maalim akili ikasogeleana. Akataka kujichomoa kutoka katika mikono ya James. Hakufanikiwa James alikuwa imara sana.

    Akapokea vibao vingine vitatu vya upesi upesi.

    Maalim akaamua kujitetea kiume.

    Na yeye akarusha ngumi ndogo, ikatua katika upande wa jicho la James.

    “Ayaaa.” Akapiga kelele.

    Kisha akaruka kwa kutumia goti, akatua katika tumbo la Maalim.

    Maalim akagumia kwa maumivu makali.

    Akajikunja hadi chini.

    James akatumia taaluma ya ugomvi wa kitoto.

    Akamkalia juu.

    “Utasema? Husemi?” alihoji huku akiwa anahema juu juu.

    Maalim alikuwa haamini kinachotokea.

    James hakutaka kuupooza ule ugomvi, akazungusha ngumi, akaituliza katika shavu la Maalim.

    Hapo sasa Maalim akanyanyua mikono juu akaropoka kila alichofanya na anachojua.

    “Emmy ana mahusiano na Lameck?” aliuliza James kwa hofu.

    Katika maelezo yote ya Maalim, jambo zito ambalo James hakulitegemea ni hilo. Emmy alikuwa na mahusiano na Lameck. Na chanzo cha Jose B kukutana naye kimwili ni kwa ajili ya kumfichia siri hiyo nzito.

    James alijikuta akiwa amemuachia huru Maalim.

    Akili ilisimama kufanya kazi.

    Lameck? Hapana hakuamini.

    Ghafla akavamia na hisia nyingine ambazo ni za kustaajabisha sana.

    “Inawezekana kuwa hata mimba ni ya jamaa, sio ya kwangu?” alijiuliza kwa sauti ya juu. Hakujali Maalim anasikia ama vipi.

    “Emmy yupo wapi kwa sasa?” aliuliza hatimaye.

    “Wallah hatujafanya naye biashara zaidi. Hadi sasa ninamsubiri, hakuweza kufika sijui alipo, tazama meseji katika simu yangu nd’o zitanitetea mimi.” Alijieleza kwa kutetemeka Maalim.

    James akamuamini baada ya kuzisoma meseji za makubaliano kati yao.

    James akatoweka bila kuaga.

    Maalim hakuamini kama amebaki hai kwa usaliti mkubwa alioufanya kwa James.

    Wazo la kuukimbia mji pakikucha lilimvamia.

    Akaamua kuondoka alfajiri sana.



     ****



    Wazee wawili walikuwa wanajadiliana jambo kwa kina. Umri wao uliendana sana na walionekana kushibana vilivyo.

    Mbele yao palikuwa na jagi la maji.

    Wote walikuwa wamevaa kanzu nyeupe na vibalaghashia huku mmoja akiwa na tasbihi akihesabu wakati mazungumzo yanaendelea.

    Mzee Ndula alikuwa haamini kama kitendo cha mtoto wake Said kujiingiza katika kufuatilia kesi iliyopita muda mrefu ndiyo ilikuwa tiketi yake ya kwenda akhera.

    “Mwanajeshi amemuua kijana wetu mzee Sadiki..hili si jambo la kunyamazia. Kesho tunamzika mi sitakubali lipite hivihivi.” Alizungumza kwa sauti ya chini, bwana Sadiki akatikisa kichwa kuashiria kukubaliana naye.

    Licha ya wazee hawa kulingana kiumri lakini kuna heshima kubwa kati yao.

    Mzee Ndula ndiye alikuwa mshenga wa Sadiki alipokuwa anataka kumchumbia mkewe wa sasa ambaye amezaa naye watoto wengi. Hivyo palikuwa na udugu kati yao zaidi ya urafiki.

    Uzuri wote walikuwa katika jeshi. Japo Sadiki alikuwa amestaafu tayari, lakini alitumikia jeshi kimya kimya.

    Bwana Sadiki aliahidi kushirikiana na Ndula bega kwa bega kuhakikisha huyo muuaji anapatikana na ikiwezekana kuadabishwa.

    “Nadhani unafahamu golgota ya nyumbani kwangu, labda asipatikane maana atajuta kuzaliwa, hakuna jasiri mbele ya pango lile.” Bwana Sadiki alijisifu, mzee Ndula naye akamuunga mkono.

    Jioni mzee Sadiki aliaga na kuondoka kwa minajiri ya kurejea tena baadaye.

    Sauti ngeni zilimpokea, alisikia mazungumzo ya tofauti katika nyumba yake. Akajihakikishia kuwa kuna mtu aidha amekuja kumtembelea ama ni mgeni kutoka kijijini.

    Bwana Sadiki akajikongoja hadi ndani.

    Akatabasamu baada ya kumtambua mgeni wake.

    “Dume la simba...lisilotetereka.” alitoa sifa kemkem.

    Mgeni akafanya tabasamu hafifu.

    Akasimama na kumwendea mzee Sadiki akamkumbatia.



    ****



    Lameck, baada ya kufanya dhahama ya aina yake kwa kumtengua Mpelelezi Said Ndula, na kumpoteza kifahamu mwanadada Emmy alitokomea kuelekea katika vijiji vilivyopo jirani.

    Alidumu katika vijiji akizunguka hapa na pale hadi kigiza kilipotanda.

    Akafanya safari ya kwenda barabarani kisha akarukia gari inayoelekea Morogoro mjini.

    Majira ya saa tatu usiku alikuwa katika nyumba za kulala wageni.

    Akalipia chumba.

    Chumba kilikuwa na luninga.

    Taarifa ya habari ya saa nne usiku ilimkuta akiwa anatokea bafuni kujisafisha mwili.

    Taarifa nzito ilikuwa juu ya mauaji katika kijiji cha Mikese.

    Mwanajeshi aliyeua na kujeruhi.

    Taarifa hii ilielezewa kwa urefu na ilikuwa na mashiko haswaa.

    Lameck alijikaza kijeshijeshi asijionyeshe kuwa ameshtuka sana.

    Lakini aliukosa usingizi.

    Aliamini kuwa baada ya muda sura yake itazagaa katika pande zote za nchi na huo utakua Mwanzo wa kuikosa amani.

    Lameck akaamua kufikiri kiume.

    Akamkumbuka Mwanajeshi mstaafu ambaye ndiye aliyemshawishi hadi kuingia jeshini. Akaamua kumchagua kuwa mshauri wake mkuu.

    Alimuamini sana tangu mwanzo wa kufahamiana kwao.

    Anakumbuka hata siku alipokuwa anampa kichapo Jose B alilitumia golgota la mzee Sadiki kumpa dawa yake kijana huyo ambaye alijikuta akisema kila kitu.

    Mzee Sadiki na golgota yake ni hatari. Alikiri Lameck.

    Usiku huo ukapita, siku iliyofuata kabla habari hazijatapakaa sana.

    Lameck akarejea jijini Dar, akaenda moja kwa moja nyumbani kwa mzee Sadiki.

    Mavazi aliyoyavaa hata wangeitangaza sura yake ilikuwa ngumu sana kumtambua.

    Alikuwa tofauti sana lakini mzee Sadiki alimtambua alipofika.

    Lameck akasimama akamkumbatia mzee Sadiki kisha akampigia saluti ya heshima.

    Lakini tatizo lilikuwa moja tu. Lameck hakuwa na furaha na mzee Sadiki hakuwa na raha.

    Wakati Lameck anawaza atajinasua vipi kutoka katika kashfa ya mauaji, mzee Sadiki alikuwa anawaza atalipa vipi heshima ya ushenga kwa kumsaidia mzee Ndula kumsaka muuaji wa mtoto wake.

    Kazi kwelikweli.

    “Mzee mimi si mkaaji sana....nahitaji tuzungumze kidogo tu...” Lameck alinong’ona.

    “Umenywea sana leo kani kuna nini?” aliuliza mzee Sadiki.

    Lameck hakujibu.

    Mzee Said akaongoza njia hadi katika ukumbi wa kuegesha magari.

    Palikuwa na viti kadhaa vya plastiki. Wakaketi pale.

    “Kinywaji gani dogo nikuletee.”

    “Hapana tuzungumze kwanza.” Alijibu Lameck.

    Mzee Sadiki akatulia katika kiti. Lameck akachukua nafasi ya kuzungumza.

    “Mzee wangu, mzee ninayekuheshimu sana, mzee uliyenifanya mimi niitwe mwanajeshi wa kimataifa..nipo mbele yako nina tatizo. Kijana wako uliyenituma kulipigania taifa nimelipigania sana, nimejitoa kwa uwezo wote kulipigania lakini bado leo nina tatizo nahitaji busara zako ili niwe na amani tena. Mzee nadhani unakumbuka kuwa nilienda Sudani na ulifanya sherehe ya kunipongeza, na niliporejea hukujua kwanini nimerejea japo vyombo vya habari vilipotosha umma. Mzee mimi si mwanaume tena....risasi ya mwarabu ilinifanya vibaya na kuondoka na heshima yangu yote. Sasa si mwanaume.

    Lakini hilo sio tatizo, kabla ya kwenda Sudani kuna mwanamke nilimuacha akiwa na mimba yangu, japo alikuwa mke wa mtu mtarajiwa......”, Lameck akasimulia kila kitu kuhusu yeye na Emmy, uhusiano wao na utata wa ile mimba.

    Akajieleza jinsi alivyopigania kuipata haki ya damu yake.

    “Lakini katika mapigano kuna kuua ama kuuliwa, mzee mimi niliua bila kutarajia. Hasira za risasi ya mwarabu zilinifanya niue.” Alisita Lameck kisha akaendelea kujieleza juu ya kifo cha mama yake Emmy na baadaye akasema jambo ambalo laiti kama mzee Sadiki asingekuwa amepitia jeshi basi mshtuko wake ungeonekana waziwazi.

    “Sijui alipata wapi taarifa za kutoroka kwangu, lakini sikuitaka aibu hii, nilimrukia kichwa kimoja na teke moja maridadi, sikutegemea kama atakufa.” Alimalizia.

    “Mzee nipo hapa kama nilivyosema nahitaji busara zako....na zangu zilizonijia kichwani ni kwamba namuhitaji Emmy, yule ndiye atakayenifunga mimi ama kuniweka huru. Namuhitaji kwa hali na mali.”

    Kimya kikatanda baada ya simulizi hiyo ya kustaajabisha, kuhuzunisha na kuchekesha katika baadhi ya vipengele.

    Mzee Sadiki alijitambua mwenyewe na hofu yake.

    Hakuamini kuwa yu katika kizuizi cha kutenda kazi.

    Amtendee yupi? Akimtendea Lameck kuna kizuizi cha mzee Ndula, akimtendea Ndula basi amemuweka katika kitanzi Lameck.....CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Patashika.



    *****



    HALI ya kiubaridi cha namna ya kipekee na harufu nzuri ya manukato ambayo aliyeyapuliza haonekani ilimfanya atabasamu.

    Jambo jingine lililompa faraja ni kusimama na wazungu daraja moja.

    Alifarijika sana na kujiona yu mtu kati ya watu.

    “Akina Rweyemamu nikiwaambia kwa maneno tupu hawataniamini..” alizungumza sauti ya chini ambayo bado ilikuwa imemezwa na lafudhi tamu ya kabila la wahaya. Kisha akachukua simu yake na kuanza kupiga picha na wakati mwingine kujipiga picha yeye mwenyewe.

    Alifanya hivyo hadi akaridhika.

    Akaitazama picha moja, ilimuonyesha vyema, jinsi alivyojawa na madevu. Na sura yake ilivyotangaza chuki na ubaya.

    Picha nyingine zilionyesha madhari ya uwanja wa ndege wa kimataifa wa mwalimu Nyerere jijini Dar es salaam ulivyo wa kipekee.



    Ilikuwa mara yake ya kwanza kusafiri kwa kutumia ndege na ilikuwa mara yake ya pili kutua katika jiji hilo.

    Baada ya kujiridhisha na kushangaa kwake.

    Aliandika namba kadhaa katika simu ya mkononi, kisha akapiga.

    Sasa hakuwa akitabasamu tena.

    “Nimewasili tayari. Nimevaa miwani nyeusi, suruali ya jeans na koti kubwa na kofia aina ya mzula.” Alitoa maelekezo kisha akakata simu.

    Baada ya dakika takribani tatu, aliguswa bega na mwanamke kisha akapitilizwa.

    Alielewa maana akamfuata yule mwanamke kwa mbali.

    Baada ya hatua kadhaa walikuwa katika gari moja.

    “Mussa Mujuni. Mume wangu kipenzi.” Sauti ya kike ilivunja ukimya. Maneno haya yakarejesha lile tabasamu alilokuwanalo uwanja wa ndege.

    Mwanaume hakujibu kitu.

    “Karibu jijini...karibu sana.” Mwanamke aliendelea.

    Akazidi kumfaidisha dereva wa taksi.

    Mwanaume hakusema neno hadi waliposhuka katika taksi.

    “Umesema kuwa yu tayari kwa kuchinjwa? Unaamini vipi?” hatimaye mwanaume alizungumza, sasa alikuwa ameondosha kofia yake na miwani yake.

    Cha kustaajabisha akaziondosha na zile ndevu.

    Hakika alikuwa kijana mtanashati.

    Kwa nini anajificha? Hilo likabaki kuwa swali.

    “Nimemtengeneza tayari hawezi kuchomoka yule, nimekuwahisha wewe kabla polisi hawajaingilia kati.” Alijibu bila wasiwasi.

    Mengi yalizungumzwa na mipango kufanyika. Kisha wakaingia kulala wakiwa wanaungoja utendaji tu.

    Baada ya starehe za kimwili, mwanaume alisinzia.

    Mwanamke akabaki macho, alikuwa na wasiwasi na huruma ilipiga hodi. Japo hakuikaribisha.

    Kitendo cha Jose B wa ukweli kumtamkia Mamu, siri kadhaa juu ya James na jinsi alivyowaua Bibiana na Deo ilimradi tu wasimuwekee kizuizi katika ndoa yake kilimuumiza sana na kuzidi kumwona James hana huruma hata kidogo.

    Tena hastahili kuonewa huruma.

    Mariam akaikumbuka siku aliyopata fahamu baada ya siku nane za kuishi dunia ya giza. Sura ya mwanaume ambaye si malaika ilikuwa mbele yake kumaanisha kuwa bado Mariam yu hai hajafa kama wabaya wake walivyotaka.

    Akamkumbuka Mussa, kijana mtanashati ambaye alimuokoa.

    Historia ya Mussa ilikuwa inaogopesha kiasi lakini cha muhimu ulikuwa uhai wake maana bila Mussa angekuwa marehemu tayari.

    Harakati za Mussa za kufanya ujambazi kisha kutokomea na kujificha porini ndizo zilimuwezesha kukutana na mwili wa Mariam ukiwa unapumua.

    Mariam akaokolewa na jambazi.

    Siku ambayo Mussa anamueleza juu ya shughuli yake na kwanini anafanya vile. Alimgusia juu ya umasikini uliokithiri pia ukosefu wa ajira kutokana na kukosa elimu.

    Mussa alilalamika kuwa hapendi kukaba wala kuua. Lakini bunduki ambayo alirithishwa na marehemu baba yake ambaye alikufa katika harakati za kusaka pesa kwa njia haramu ilimpa nguvu ya kufikiri mara mbilimbili. Hatimaye akauvaa ujambazi.

    Akawa anafanya uhalifu mjini na kujificha porini.

    Pori la Kakonko, na ni huku alipokutana na Mariam.

    “Mariam, mimi nikipata pesa ya kutosha huu ujambazi basi tena nakwambia. Unadhani napenda haya maisha ya kujifichaficha..” Mussa aliwahi kumwambia Mariam siku moja wakiwa katika chumba kimojawapo katika hoteli ya Katuma iliyopo katika mbuga za Katavi. Ni muda mrefu ulikuwa umepita tangu waanze kuishi pamoja japo Mariam hakushiriki sana vitendo vya uharifu.

    Mariam aliguswa na kauli hiyo. Ni siku hiyo alipomwambia Mussa kuhusu unyama wa Kindo (James).

    “Kwa hiyo jamaa anaweza kuwa na pesa hadi sasa?”

    “Lazima atakuwa nazo, yale madini yalikuwa ya thamani sana. Nimeona picha yake gazetini amefunga ndo ya kifahari”

    Mazungumzo haya hatimaye yakawaingiza katika harakati rasmi za kumsaka James.

    Sasa Mariam alikuwa amewasiliana na Mussa ambaye aliishia naye kinyumba na kujikuta wakizoea kuitana MAMU.

    Mussa alihitajika kwa ajili ya shughuli moja tu.

    Aidha kuua ama kumfilisi James.

    Sasa yu jijini na mipango tayari imesukwa ikasukika.

    Ni aidha James afe ama aachie mali zote.



    *****



    Bwana Sadiki alikosa jibu sahihi juu ya wapi pa kuegemea, je ni Lameck ama ni mzee Ndulla ambaye amefiwa na mwanaye, mkewe alishtukia jambo hilo lakini mzee

    Sadiki hakutaka kumshirikisha kwa kuhofia mambo ya wanawake wasivyojua kutunza siri.

    Mara amwambie mama Karim, mama Karim naye amshirikishe mama Abdul.

    Hakuna siri tena hapo.

    Mzee Sadiki, mjeshi wa zamani tena anayeheshimika sana hakutaka kuzikwa kwa dharau kwa kuficha maovu. Hivyo hakutaka kupaparuka.

    Alitakiwa kuwa makini sana.

    Usiku mnene akainuka kitandani, akaenda kukaa sebuleni. Akatoa pombe kali katika jokofu akaanza kuigida kwa utaratibu maalumu.

    Alipoitua mezani akachukua viganja vyake, akaisugua misuli ya kichwa chake.

    Kisha akaweka mezani mjadala, maneno yam zee Ndulla na maneno ya Lameck.

    Alipoyalinganisha akashambuliwa ghafla na jina ambalo halikuwa limetiliwa maanani kabisa.

    James.

    Katika maelezo ya mzee Ndula palikuwa na jina hili. Jina hili lilitajwa na Emmy ambaye alidai kuwa huyo ni mumewe ambaye alitaka kumuua yeye pamoja na huyo mwanajeshi ambaye ni Lameck. Hicho nd’o kilikuwa chanzo cha kuamua kutoroka.

    Hatimaye Sadiki akatabasamu.

    “Bwege huyu nd’o wa kunyutrolaizi mambo.....” alitokwa na sauti nzito.

    Akachukua bia yake katika mtindo wa tarumbeta akaipeleka kinywani.

    Alipoitua ilikuwa chupa tupu, uso umekujwa haswaa.

    Pombe ilikuwa imemuingia.

    Sadiki akafikiria kumuuzia kesi James, ili aonekane kuwa ndiye muuaji wa askari polisi na lolote lile baya ambalo litatokea liwe juu yake.

    Ili haya yatimie, Emmy hatakiwi kuwepo kutoa ushahidi.

    Kizuizi kingine.

    Emmy anapotezwa vipi katika ramani?

    Swali gumu.

    Kichwa kikaanza kumuuma tena japo si kwa maumivu makali kama mwanzo alipokuwa akifikiria juu ya Ndula na Lameck.

    Akajiondoa sebuleni na kukiendea chumba, akajitupa kitandani.

    Akautafuta usingizi huku kichwani akiwa na jina la Emmy.

    Palipambazuka mapema kutokana na kelele zilizopigwa na si yake.

    Alipoitazama alikuwa ni mzee Ndula.

    “Salama mkuu.” Alisalimia.

    “Salama, pole kwa kukutoa usingizini. Yule Emmy anapelekwa leo kwa ajili ya ukaguzi nyumbani kwake. Nilionelea kuwa akitoka huko tumchukue tukazungumze naye chemba moja.” Mzee Ndula alitetemesha katika simu.

    Mzee Sadiki hakupingana naye.

    Akakubali, kisha simu ikakatwa.

    Akatafuta namna ya kumshawishi mzee Sadiki waweze kumfanyia mipango Emmy ya kuwa huru ili mpango wao uende sawa.

    Akaendelea kuumiza kichwa.



    ****



    Baada ya kufanikisha kumuadabisha Maalim Shaban, na bado akiwa hajapata majibu ya wapi mkewe atakuwa amekimbilia.

    James akiwa amechanganyikiwa na uchovu ukiwa unaendesha akili yake aliamua kurejea nyumbani ili aweze kupumzika na kuangalia ni jinsi gani anaweza kuanza kumsaka Emmy.

    Kitoto katika tumbo la Emmy alikitilia mashaka, na sasa alimuhitaji Emmy kwa ajili ya mambo mawili, aidha kuitoa ile mimba na mahusiano yaendelee ama kutalikiana.

    James alifika nyumbani kwake, Grace na Gloria wakiwa bado wamelala.

    Naye akaingia chumbani kwake kulala.

    Usingizi ukampitia.

    Mara akajikuta kama yu ndotoni. Akawaona watu kadhaa wakiwa wanamchekea huku wakiwa na visu. Walikuwa wengi na vicheko vyao vilikuwa vya bandia. Walikuwa na hasira sana na yeye.

    James alijaribu kupiga kelele lakini haikutoka sauti.

    Akajikaza mara akayafumbua macho.

    Haikuwa ndoto tena.

    Chumbani kwake palikuwa na ugeni. Ugeni usiokuwa na heri.

    Bunduki mbili zilikitazama kichwa chake.

    Waliokuwa ndani walikuwa wamezificha nyuso zao.

    Hawakusema neno lolote.

    Kifo kilikuwa kinanukia. Na James hakujiandaa kukabiliana na tukio kama hili.

    Mara mmoja kati ya wageni hao akakifunua kitambaa chake.

    Uso kwa uso na James.

    “Kindo...” akaita yule mwanamke ambaye sasa alikuwa yu wazi. James akakodoa macho.

    Ana kwa ana na marehemu Maria.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Msichana waliyemuua ili wapate mali.

    Mali wakaipata lakini sasa inamtokea puani.

    Maria alikuwa ameshika kisu kikali. Hakuwa mzimu alikuwa mzima kabisa.

    James hakupata nafasi ya kujitetea. Mwanaume mwenye ndevu nyingi naye akajifunua.

    “Kadi ya benki, kadi ya magari na hati ya nyumba hii tafadhali.” Alizun gumza bila hata chembe ya utani, alikuwa na macho mepesi na mkono imara ulikuwa umeikamata bunduki kiustadi.

    James akiwa bado anatetemeka, ghafla alipigwa na kitako cha bunduki katika kiuno chake.

    Yowe la uchungu likamtoka.

    Alikuwa katika mtihani mkubwa sana hakutegemea kama itatokea siku akutane na maajabu kama haya, mwanamke ambaye anaamini kuwa alikufa sasa amemtokea chumbani mwake. Akiwa ameimarika kimapambano.

    James alifanya alivyoambiwa.

    Vilivyokuwepo akavitoa bila kusita.

    Wakati James akiwa katika kitimoto chumbani huku, Emmy alikuwa katika taksi na askari watatu waliovaa kiraia, jukumu kubwa walilopewa ni kufanya upelelezi katika chumba cha Emmy iwapo watakutana na takwimu zozote zitakazowawezesha kumtambua huyo mwanajeshi ambaye amemuua mpelelezi Said Ndula.

    Walilifikia geti lililokuwa wazi.

    Gari ikaegeshwa mbali kidogo.

    Askari wakiwa makini kabisa na mitutu yao walimtanguliza Emmy pale ndani katika nyumba ile iliyokuwa kimya sana.

    Emmy alikuwa amejitabiria tayari kuwa maisha yake lazima yaishie jela.

    Anaishia jela kwa sababu ya madhaifu yake kimwili yaliyomsababisha afanye mapenzi na baba yake mdogo.

    Sasa hakuna kesi ya kufanya mapenzi na baba mdogo bali kuua.

    Emmy katika hatia.



    Polisi ni tabaka ambalo linashangaza sana, kama ilivyo matabaka mengine kama wakutanapo vijana, ama wakutanapo wazee, ama wanawake. Akili zao huwa za kufanana.

    Nguo aliyokuwa amevaa Emmy ilikuwa nyepesi sana na ilikuwa imetepeta kutokana na kutoka kukalia maji huko selo alipokuwa.

    Alianza askari mmoja kumwonyesha mwenzake jinsi Emmy alivyokuwa anatikisika, mwenzake akajifanya hajavutiwa lakini kadri Emmy alivyozidi kutembea walijikuta wote wakimtazama kwa matamanio.

    “Nenda mbele, rudi nyuma...sogea huku...” zilikuwa amri zisizokuwa na msingi ilimradi tu waweze kumwona Emmy akitikisika. Mmoja akalifunga geti kabisa ili watu wapitao nje wasiweze kushuhudia lolote.

    Ni kawaida yao askari kumchezesha mtuhumiwa kiduku, kumrusha kichura chura...na hata hili halikushangaza.

    Mchezo wao huu wa kutoa amri za kiaskari huku wakiwa na bunduki mkononi ulinaswa na vijana wawili, walioongozana na Mariam na Mussa.

    Bunduki iliyowekwa kiwambo cha kuzuia sauti ikawekwa katika umakini wa hali ya juu sana.

    Vijana wawili ambao walikuwa wamewafunga kamba Grace na Gloria walikuwa makini kusubiri nini kitakachojiri. Kazi yao ilikuwa kulinda ulinzi wa nje na ni hili walikuwa wanafanya.

    Sasa wakabaini kizuizi kilichotaka kuingilia kati oparesheni yao.

    Jicho la mmoja likasafiri hadi katika tukio lililokuwa linaendelea nje.

    Msichana akichezeshwa sindimba na wanaume wawili.

    “Soja...njagu hao....” alinong’ona mmoja akimaanisha hao walikuwa polisi.

    “Tuwalegeze...” alijibu kwa sauti ya chini pia.

    Askari walikuwa kama watoto wakitazama ‘makalio’ ya Emmy yanavyotikisika.

    Emmy alikereka sana na kitumbo chake kilichoanza kuchomoza. Akachoka.

    Akagoma kuendelea.

    Wale askari wawili wakamsogelea.

    Kabla hawajamfikia walijikuta wakicheza mchezo wa kuruka sarakasi za maajabu.

    Ilikuwa kimya kimya.

    Mmoja akatokwa na yowe la uchungu, akarushwa mbali. Akapoteza fahamu.

    Mwingine ikawa bahati mbaya, wakati mlengaji alitaka kupiga magoti tu, yeye aliinama bila kujua kinachoendelea. Risasi mbili zikakifumua kifua chake.

    Akapoteza uhai huku akiwa na tabasamu usoni.

    “Fala unajua kulenga wewe......” walipongezana.

    Akina Mamu hawakujua kama kuna tukio kama hilo limetokea.

    Vijana walikuwa wamesawazisha tayari.

    Mizoga ya askari wale ikavutwa na kufichwa nyuma ya nyumba. Ilikuwa ngumu kugundua kama kuna tatizo limejitokeza ndani ya muda mfupi uliopita.

    “Wewe ni nani?” Emmy aliulizwa.

    “Naitwa Emmy.....”

    “Wewe ni nani hapa ndani...”

    “Mke wa James.”

    “James ni nani?”

    “Mwenye hii nyumba.”

    “Na hao polisi ni nani zako?” aliendelea kuulizwa maswali.

    Emmy akajaribu kuelezea kwa kifupi japo hakuweza kuliweka wazi sana tukio la yeye kukabiliwa na kesi ya mauaji.

    “Vipi tumshtue maza nini?” jambazi mmoja alimuuliza mwenzake.

    Wakakubaliana na mmoja akaenda kuifikisha taarifa.

    “Mlete?” aliamuru Mussa.

    Baada ya dakika kadhaa Emmy akafikishwa katika kile chumba ambacho kilifanania na jehanamu kwa wakati ule. Bunduki kila kona.

    Mariam alimtazama Emmy akamwonea huruma na kitumbo chake.

    Alitamani kusema neno lakini akasita.

    James alikabidhi hati za nyumba na kadi za magari yake huku roho ikimuuma.

    “Benki kuna sh’ngapi?”

    “Milioni thelathini.” Alijibu James huku akiwa anatetemeka.

    Mussa akafanya tabasamu kiasi, pesa hizo zilikuwa nyingi sana kwa upande wake.

    Aliona ule mpango wake wa kuachana na ujambazi unaweza kutimia baada ya kukipata kiasi kile.

    James alitoa namba za siri za kadi yake ya benki, hakudanganya baada ya kupewa tamko kuwa akithubutu kudanganya risasi itausambaza ubongo wake.

    Zoezi lilichukua muda mrefu kumalizika.

    Kisha ukafuata ule muda wa maamuzi ni ninji kifanyike kama kisasi kwa James, maana kumuacha hai mtu aliyetaka kuuondoa uhai wa mwenzake katika ujambazi lilikuwa kosa la jinai.

    Mariam akasihi James aachwe hai, Mussa akakataa katakata.

    Emmy alikuwa Amelia hadi koo limekauka na alingoja lolote ambalo litatokea na litokee.

    Wakiwa katika majibizano ya hapa na pale. James akafanya kosa ambalo laiti kama angepewa nafasi ya pili huenda asingethubutu kulifanya.

    Kosa la kumnyakua bunduki Mussa ili aweze kupambana.

    bahati mbaya ikawa kwake, hakujua kuwa kuna vijana walikuwa makini kutazama kila hatua.

    Risasi nne zilizolengwa kwa umakini mkubwa, kimya kimya zikakirarua kifua cha James.

    Hakupata nafasi ya kupiga kelele na hata risasi nazo hazikutoa kelele, bunduki ilikuwa katika kiwambo cha kuzuia sauti (Sound proof).

    Emmy akarukiwa na damu nyingi kutoka katika mwili wa James.

    Akapoteza fahamu.

    “Fala huyu nd’o ulitaka tumwache hai?” Mussa aliuliza huku akiitwaa tena bunduki yake.

    Mariam hakujibu kitu.

    “Twen’zetu” aliamuru Mussa, wakamfuata wenzake.

    Kiwiliwili cha kwanza kutoa pua yake nje kilikutana na dhahama ya aina yake.

    Ni kama kilikuwa kimepigwa shoti.

    Kikapeperushwa mita kadhaa mbali.

    Mussa akawahi kujirusha kando, alipotoka ikapita risasi na kuufyatua mlango.

    Mshambuliaji mwingine akawa macho, akawahi kurusha risasi ikamfikia katika bega mzee wa makamo lakini mkakamavu aliyekuwa anajiandaa kushambulia. Wakati anasikilizia maumivu ya bega, Mussa alijikunja vyema aweze kufyatua risasi.

    Mara akakoswa koswa na risasi nyingine lakini akawa mwepesi kufyatua.

    Yule aliyekuwa anaugulia akapokea adhabu nyingine.

    Risasi akapenya katika mbavu zake.

    Akatua chini kama mzigo.

    Kimya kikatanda ghafla si akina Mamu wala wale washambuliaji wengine waliokuwa na uhakika wa maisha yao.

    Mariam alikuwa amepagawa na alikuwa amelala chini tuli, mapigo ya moyo yakienda kasi.

    Aliyebaki na amani alikuwa mzee mmoja tu aliyekuwa amejifia tayari.

    Alikuwa nadhifu. Na jina lake aliitwa Ndula.

    Baba mzazi wa Said Ndulla.

    Aliyebaki katika mapambano alikuwa ni mwanajeshi mstaafu mzee Sadiki.

    Mzee Sadiki alikuwa anajutia kitendo chake cha kuacha silaha yake nyumbani jambo ambalo hakuwa na kawaida nalo hata kidogo.

    Alimlaumu mzee Ndula kwa papara zake maana ni yeye ambaye alimpitia pale nyumbani mbiombio waweze kufika eneo ambalo Emmy alipelekwa kwa ajili ya upekuzi.

    Kimya cha muda mrefu kilichotokea katika nyumba hiyo kiliwatia mashaka na hatimaye wakaamua kuingia ndani kwa njia ya panya. Ni hapo walipokutana na mizoga ya askari wawili.

    Upesi wakazitwaa bunduki zao zenye risasi chache na kujiandaa kwa ajili ya kushambulia. Hawakuwa na nafasi ya kufikiri mara mbilimbili kuwa ndani ya jingo lile kuna watu wabaya ambao muda wowote wanaweza kutoka.

    Hakika walitoka na mashambulizi yakaanza hatimaye risasi zikauondoa uhai wa mzee Ndula.

    Alibaki Mzee sadiki kuupigania uhai wake.

    Alitamani kuwasiliana na kituo chochote kwa ajili ya kutoa msaada lakini angewasiliana vipi.

    Kwa mara ya kwanza katika maisha yake ya kuruka viunzi vingi enzi za utumishi wake katika jeshi sasa anakutana na kifo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakika kile kilikuwa kifo, maadui walikuwa wengi na aliamini kuwa walikuwa na silaha nyingi na kali zaidi yake.

    Pale alipokuwa hapakuwa na njia ya kutokea kwa nyuma na mwendo wa kulifikia geti ilikuwa ni sawa na kuiweka rehani roho yake.

    Maumivu ya risasi ikipenya katika kichwa chake na kuuacha ubongo wake ukitapakaa kwa nje yalimvamia katika mfumo wa hisia, hisia mbaya.

    Mzee Sadiki hakuhitaji kufa kizembe vile. Lakini angefanya nini.

    Ghafla akaikumbuka imani yake ya kiislamu.

    Iwapo unakiona kifo ili uingie peponi unatakiwa ushahadie. Hii inakuwezesha kusamehewa dhambi zako zote na kufa ukiwa msafi kabisa.

    Ni nafasi ambazo watu wachache sana hupewa katika maisha. Mzee Sadiki akanyanyua mikono juu sasa akakubaliana na kifo.

    “Ash’hadu an’lailahah ilallah wa......”

    Akiwa katika kushahadia kabla hajamaliza mara alianguka chini kama mzigo.

    Kisha jambo la mwisho aliloweza kusikia ni risasi kutoka katika bunduki ambayo haijawekwa katika kiwambo cha kuzuia sauti.

    Baadaye kikatanda kimya kikubwa tena katika kiza kinene.



    ****



    MWANAJESHI vitani hutakiwa kuwa na akili ya ziada kumzidi mpinzani wake ili aweze kushinda vita.

    Mwanajeshi hutakiwa kufikiri mara mbili ya mpinzani wake.

    Na kamwe hatakiwi kuamini watu hovyo linapokuja suala la vita.

    Dhana hii huishi akili mwao na hatimaye hukaa katika damu yao milele.

    Lameck naye alikuwa muathirika wa dhana hii.

    Baada ya kuwa amemueleza Mzee Sadiki kuhusiana na ile kesi na aibu inayomkabili mbele yake. Hakutaka kujiaminisha kuwa mzee Sadiki atakuwa msiri.

    Na aliamini fika kuwa mashaka hayo yalitambuliwa hata na mzee Sadiki mwenyewe maana hata yeye alipita jeshi kwa muda mrefu tu.

    Lameck hakulemaa baada ya kuona mzee Sadiki anatoweka nyumbani huku akiwa katika hali ya mashaka.

    Aliweka mashaka yake upesi na hakutaka kungoja ngoja.

    Akaanza kumfuatilia.

    Akamuona akiingia katika gari aina ya Landlover.

    Upesi Lameck akajiweka katika pikipiki, akavaa kofia ngumu, sura yake haikuweza kuonekana.

    Hili jambo likampa kujiamini sana.

    Mwenye pikipiki akapewa sharti la kuifuatilia ile gari.

    Safari yao ikaishia jirani na nyumba ya James

    Lameck akamalizana na mwendesha pikipiki. Akabaki kuwashuhudia Mzee Sadiki na mzee mwenzake wakiwa makini kufuatilia jambo katika nyumba ya James.

    Naye akajikita katika kuifuatilia mienendo yao. Alijikausha kana kwamba hausiki katika kulifuatilia tukio lile ambalo alimini lilikuwa linamuhusu kwa sana.

    Baada ya muda wazee wale wakaruka ukuta kwa umakini na upesi wakaingia ndani ya ile nyumba.

    Hapa Lameck hakuendelea kujibanza, alinyata kwa umakini bila kuwaruhusu watu wa pembeni kuelewa nini kinaendelea.

    Akaupata upenyo akaweza kuchungulia ndani.

    Filamu ya mauzauza ikaendelea, akawaona wale wazee wawili wakikodoa macho katika miili ambayo ilikuwa imetapakaa damu na ni kama tayari ilifaa kuitwa maiti.

    Kila mmoja akatwaa bunduki kisha wakatulia tuli.

    Kuna jambo walikuwa wakilingoja.....

    Hakika lilikuwepo. Baada ya muda wa kusubiri hatimaye yalianza yale mapambano.

    Jicho la Lameck likamshuhudia yule bwana aliyemfyatua katika bega yule mzee mwingine, almanusura aitoe bunduki yake ndogo na kumshambulia, lakini alihofia kuvuruga mipango mapema na kumpa nafasi adui kutambua wapi alipo mpinzani wake.

    Akiwa bado anaduwaa mara risasi nyingine ikampata tena yule mzee, sasa akakosa muhimili akaanguka chini.



    Yakabakia mapambano ya mzee wake (Mzee Sadiki) na kundi la watu.

    Mzee sadiki alionekana kuzidiwa kwa kila kitu na alikuwa akikingoja kifo.

    Ni hapo Lameck alipouvaa ujasiri, akazunguka upande ule ambao mzee Sadiki alikuwepo, akaurukia ukuta kimya kimya kwa ustadi wa hali ya juu. Kisha akatua kwa mtindo wa sarakasi. Akamzoa mtama mzee Sadiki ambaye alikuwa katika sala ya mwisho.

    Baada ya hapo akajiingiza ukumbini.

    Mwanajeshi kijana. Akajikumbusha enzi za kupambana na makundi makubwa makubwa ya maadui.

    Mchezo ukakolea. Maadui walikuwa hawajajiandaa kwa shambulizi lile la hatari.

    Mmoja baada ya mwingine wakaangushwa chini.

    Kimya kikatanda.

    Lameck akafanya kosa la kuamini kuwa mapambano yamemalizika, akageuka na kwenda kumjulia hali mzee Sadiki pale chini.

    Risasi ikapenya katika bega lake, ikamrusha na kumbamiza ukutani.

    Kimya kikatanda.

    Mshindo ule wa ukutani na mayowe ya uchungu aliyopiga Lameck yakamshtua mzee Sadiki, akafumbua jicho lake moja akamuona Mshambuliaji mwenye ndevu nyingi akijipanga kufanya shambulizi jingine.

    Mzee akamuwahi, akabilingita na kujiweka sawa, kisha hakutaka kusita, akashambulia kwa fujo huku akipiga kelele.

    Risasi ikamrusha bwana Mussa maili nyingi mbali.

    Baada ya shambulizi hilo mzee Sadiki akaanguka tena.

    Akapoteza fahamu.

    Ukimya wa askari waliokuwa na dhamana ya kwenda kumpekua Emmy ili kesi iweze kuanza kuunguruma uliwashtua sana askari wengine waliokuwa na taarifa hiyo.

    Haikuwa kawaida kwa upekuzi kudumu kwa muda mrefu kiasi kile, simu zilipopigwa ziliita bila kupokelewa.

    Hatua zikachukuliwa, wakaagizwa watu wa kufuatilia ni kipi kinatokea.

    Kumbukumbu za namba ya dereva aliyewapeleka zikawarejea wakaamua kupiga simu ya dereva.

    Hii iliita kwa muda kisha ikapokelewa.

    Sauti yake ilikuwa inakwaruza sana, alikuwa amekurupuka kutoka usingizini.

    “Wapo wapi hao?”

    “Ahh wapo kwenye ile nyumba mimi m nipo ndani ya gari.”

    “Nenda uwatazame na uwaulize kwa nini hawapokei simu zangu.” Sauti iliamrisha.

    Dereva akaruka chini upesi na kuikimbilia ile nyumba.

    Akakutwa geti limefungwa, akajaribui kutikisa halikufunguka, akaamua kuchungulia.

    Alichokiona ukumbini ilikuwa habari tosha kabisa.

    Akapiga simu na kueleza anachokiona.

    Ilikuwa taarifa ya hatari sana.

    Mawasiliano yakafanyika.

    Baada ya saa moja sare mbalimbali za jeshi la polisi zilikuwa zimezagaa pale.



    ****



    Ukiondoa Grace na Gloria waliokutwa ndani wakiwa wamefungwa kamba ni Emmy, Mariam, mzee Sadiki na Lameck nd’o miili pekee iliyokutwa hai baada ya vita ile ndogo.

    Baada ya huduma kwa wote watatu na kujipatia unafuu hatimaye kesi ilianza kuunguruma.

    Emmy akamtambua Lameck kama muuaji wa mama yake mzazi, akamtambua pia kama muuaji wa askari mpelelezi. Hili halikupingika lilikuwa na ushahidi wa kutosha.

    Mzee Sadiki akamtambua Mariam kama mmoja wa majambazi waliomuua James pamoja na ma askari wengine, hili nalo lilikuwa wazi maana Mariam alipobanwa kidogo tu alijikuta akijitaja pia kama muuaji wa baba yake James na mdogo wake James pia.

    Lameck alitaka kumshutumu Emmy kuwa alimuua Jose B lakini akajikuta anaingiwa na roho wa huruma hasahasa alipolitazama tumbo la Emmy akakumbuka alikuwa amembebea damu yake halali. Hakutaka kuipoteza damu ile, ilikuwa heri yeye asiyekuwa na uwezo wa kuzaa akafie jela kuliko kitoto chake kile kupotea kirahisi.

    Lameck hakumuhukumu kwa lolote.

    Mariam naye alijaribu kumshutumu Emmy kuwa ni muuaji lakini akakosa ushahidi, maana kwa Emmy ilikuwa mara ya kwanza kuonana na mwanamke yule. Shutuma hizo zikawadhaifu sana. Zikatupiliwa mbali.

    Hatimaye kesi ikaunguruma.

    Baada ya hukumu ni Emmy peke yake aliyepata adhabu ya kulipa fidia kwa kutunza siri mbali mbali bila kulishirikisha jeshi la polisi.

    Lakini aliachiwa huru.

    Mtaa ukampokea Emmy, akiwa yeye kama yeye.

    Akalitazama tumbo lake, akamkumbuka Lameck na James.

    Akaamini mapenzi na pesa nd’o chanzo cha ukweli kugeuzwa kuwa uongo kwa muda mrefu. Kisha akakiri kuwa hakika hakuna siri ya watu wawili.

    Taarifa zilikuwa zimetapakaa mtaani pote juu ya baba na mwana kugeuzana mke na mume, hakika lilikuwa jambo la aibu sana.

    Emmy akapatwa na fikra za kuikimbia dunia. Lakini akakikumbuka kitoto chake.

    Akajikuta anakithamini kuliko maamuzi yake.

    Baada ya miezi kadhaa, akiwa anaishi na mama yake mdogo.

    Uchungu ulimshika, akakimbizwa hospitali.

    Huko akajifungua salama mtoto wa kike.

    Akamuita Devotha.

    Kukitoa kiumbe kile tumboni kukazifanya zile fikra za kuikimbia dunia zirejee kwa kasi.

    Emmy akafanya maamuzi bila kumshirikisha mtu yeyote.

    Akakiacha kitoto kichanga kwa mama yake mdogo.

    Akatoweka kwa siku mbili akitafutwa.

    Baada ya hapo zikapatikana taarifa kuwa amekutwa akining’inia katika mti.

    Emmy alikuwa amejinyonga.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alijinyonga kuikimbia aibu, aibu ambayo ilibaki uchi baada ya yale mavazi ya upendo na pesa kuzidiwa nguvu. Kama walivyotangulia wahusika wengine.

    Emmy naye akabaki katika historia, huku akikiruhusu kile kizuizi kilichohangaisha kuanzia kanisani jijini Mwanza kikiibuliwa na Jose B wa ukweli na kutambaa hadi jijini Dar es salaam kuwasulubu wahusika mbalimbali, kitokomee ama la kiwavae wahusika wapya.



    MWISHO



0 comments:

Post a Comment

Blog