Search This Blog

Sunday 19 June 2022

HATIA - 5

 





    Simulizi : Hatia

    Sehemu Ya Tano (5)



    Umati ukazidi kumfuata kwa macho mchungaji JK wakati akiwa ameweka kituo kidogo jirani na mahali ambapo mzee Keto alikuwa amesimama na waumini wengine.

    Mzee Keto aliyakumbuka masharti aliyopewa na mganga Manyaunyau na sasa alikuwa akishuhudia yale aliyoelezwa yakitokea mbele yake mchungaji JK alikuwa pembeni yake.

    “Akisogea tu angusha kitambaa chini…pale utakuwa umemaliza kila kitu..” maneno ya mganga yalikuwa yanajirudia rudia katika mfumo wa mwangwi kichwani mwa mzee Keto. Akajivika ujasiri huku akiwa anatetemeka akakichomoa kitambaa na kutaka kukidondosha chini. Ilikuwa ni kama mchungaji JK alikuwa akilisubiri tendo alilotaka kufanya mzee Keto na yeye aweze kugeuka, kile kitendo cha mzee Keto kudondosha kitambaa, kitambaa chekundu akakumbana na macho makali mithili ya Simba jike katika mawindo yalikuwa ni macho mawili ya mchungaji JK. Mzee Keto akaanza kutetemeka akataka kukimbia lakini mlango wa kutokea ulikuwa mbali sana, akafadhaika, sasa mchungaji JK alikuwa anapiga hatua katika namna ya majivuno, kanisa zima lilikuwa kimya, kiatu chake cha bei ghali kilikuwa kinasalimiana na ile ardhi yenye marumaru na kutoa mlio ambao haukuleta bughudha katika masikio ya waumini.

    Mzee Keto akazidi kutetemeka na sasa bila ridhaa yake alijikuta anakaa chini.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mchungaji akamfikia mzee Keto. Akaunyanyua mkono wake akauweka katika kichwa cha mzee Keto. Zamani mzee Keto hakuwahi kuwa na imani ya muumini kuguswa kichwani kisha anaangulka chini na kuanza kugaagaa, sasa leo ilikuwa zamu yake kuhakikishiwa kuwa hilo linawezekana. Mkono mmoja wenye nguvu wa JK ulianza kumhangaisha mzee Keto huku na kule, mzee Keto kwa kujitambua kuwa alikuwa na hatia akawa ametulia tuli bila kuleta fujo, waliokuwa wanamsukuma waliongezeka sasa akawa anasukumwa kwa fujo zaidi. Baada ya zoezi la kusukumwa huku sauti zinenazo kwa lugha ambazo hakuzitambua zikiendelea kubwabwaja maneno ambayo hakuelewa maana yake, mara mchungaji JK hakumshika kichwa tena, safari hii alimkamata hadi usoni, bado alikuwa akinena lugha zake kwa kufoka sana.

    Taratibu mzee Keto akanza kuandamwa na usingizi mzito, usingizi huu ulileta kero kubwa katika nuru ya mzee Keto, giza likawa kubwa, akatamani kufanya jaribio la mwisho la kujinasua kutoka katika mikono hiyo. Jaribio likashindikana akili ilitoa ushirikiano mdogo lakini viungo vikamsaliti, macho pekee ndio yalijitahidi hadi dakika ya mwisho, lakini baada ya viungo vingine kulala na yenyewe yakalala.

    Macho yalivyokuja kufunguka alijikuta katika chumba ambacho kilikuwa na hewa safi kabisa na mbele yake walikuwepo wanaume wanne,

    “Haleluya…bwana apewe sifaa!!!” Sauti moja ilisema halafu nyingine zikaanza kunong’ona bila mpangilio. Kila mmoja alikuwa kwenye kunena.

    Mbele ya mahali alipokuwa palikuwa na kitu mfano wa nyoka lakini alikuwa hatembei tena, huenda alikufa kwa maradhi aliyojua mwenyewe lakini hakuwa amepondwa kichwa chake. Hali ilivyomrejea vizuri akaelezwa kuwa yule nyoka alikuwa katika mwili wake. Yule nyoka alikuwa ni shetani.

    Mzee Keto almanusura aruke kutoka mahali alipokuwa, hakuamini kuwa alikuwa na kiumbe yule ndani yake. Lakini wale wanaume pale ndani ni kama walikuwa kwenye akili yake waliwahi wakamshikilia, mzee Keto akaelezwa kila kitu kuwa shetani alikuwa amemtuma kwa ajili ya kumuangamiza mtumishi wa Mungu. Lakini sasa huyo shetani alikuwa ameangamizwa. Hayupo tena!!!

    Mzee Keto hakuwa na la kujibu zaidi ya kuisikia HATIA ikimtia aibu mbele ya wanaume hawa, ile hatia ya kutaka kufanya mauaji alitegemea kinachofuata ni sheria kuuchukua mkondo lakini ilikuwa ajabu mchungaji JK alipomshika mkono akamnyanyua na kumkumbatia kisha akamwambia maneno haya.

    “Mungu baba amekusamehe na upo huru tangu sasa….mambo ya kidunia hayana mamlaka juu ya mwili na roho yako…okoka, tubu na umfuate yeye aliyekusamehe…” maneno yale yalipenya na kufanya ubaridi katika moyo wa mzee Keto, kisha yakazaa kitu kama upendo na kuanza kutambaa huku na kule katika mwili wake kwa kasi ya ajabu, laiti kama asingekuwa anamjua Mungu basi angekiri kuwa JK ni Mungu. Mzee Keto akamkumbatia kwa nguvu mchungaji JK.

    Tangu siku hiyo akawa mtumishi hai wa kanisa hilo. Akatoa ushuhuda na kuzidi kuwavuta waumini.

    Laiti kama angejua kuwa mchungaji JK na Manyaunyau yule mganga jambo lao ni moja, asingekubali kupelekwa na mkondo huu. Mzee Keto hakujua kuwa lile gari aliloliona likitoka kwa kasi kule kwa mganga Manyaunyau lilikuwa limempakiza mchungaji JK ndani yake. Manyaunyau alikuwa katika biashara moja na wachungaji feki wengi jijini Dar es salaam. Aliwapatia habari juu ya watu wanaoenda kuhitaji huduma zake kwa lengo la kuwakomoa watumishi hawa feki, mmoja wao alikuwa ni mzee Keto ambaye aliishia kuambulia aibu kubwa na baadaye kuwa mfuasi.

    Mfuasi wa shetani!!!!!

    Umaskini ukabisha hodi nyumbani kwa mzee Keto, kila wiki alilazimika kuuza kifaa cha ndani aweze kutoa sadaka kama shukrani kwa mchungaji JK na Mungu wake.

    Hakujua kuwa alikuwa anaibiwa!!!!! Alikuwa ni kipofu aliyedhani anajua njia!!



    *******



    Katika Hospitali ya mkoa ya Bugando jijini Mwanza, madaktari walikuwa bize katika kuokoa maisha ya mgonjwa aliyekuwa amefikishwa hospitali hapo na wananchi. Hali ya mgonjwa huyu ilionekana kuwa mbaya sana tofauti na hali ya mgonjwa mwingine. Alikuwa amepoteza damu na maji mengi mwilini. Dripu zilikuwa zinapishana katika mishipa yake kwa kasi, alikuwa anapumua kwa kutumia mashine. Kwa kuwa tatizo lilikuwa halijajulikana bado aliwekewa dripu za glucose ambazo hazikuonekana kumsaidia kitu, sasa walibadilisha na kumwekea ‘normal saline’ hii huwa haizidi chupa mbili kabla ya mgonjwa kurudiwa na fahamu lakini sasa ilikuwa chupa ya tatu ya normal saline huku mipira ikiendelea kutumika katika kumsaidia kupumua kiumbe huyu.

    Ni kama alikuwa amekata tamaa ya kuishi tena, uso wake na sehemu nyingine za mwili zilikuwa zimechubuka na kuvimba sana. Alionekana kama kibaka aliyenusurika kifo baada ya kupigwa sana na wananchi. Hakufahamika jina lake mara moja, lakini hivyo hivyo madaktari walilazimika kumshughulikia huku taarifa ikitolewa polisi juu ya tukio hilo.

    “Akizinduka yule mwenzake atatusaidia yeye hana majeraha kabisa!!” daktari mmoja aliwaambia wenzake. Wakakubaliana.

    Ndani ya masaa mawili punde tu baada ya ile dripu ya glucose kumalizika aliyetegemewa alizinduka, alikuwa na afya njema licha ya kupepesuka huku na kule kama anayetaka kuzimia tena. Hiyo ilikuwa hali ya kawaida sana kwa wagonjwa hivyo alisubiriwa hadi akakaa sawa. Alikuwa imara licha ya kuonekana amelegea. Aliendelea kushangaa shangaa kabla ya kumuuliza muuguzi wa kike aliyekuwa jirani yake juu ya ni wapi alikuwa. Alijibiwa yupo hospitali ya mkoa ya Bugando. Hakuuliza maswali mengi akabaki kama zezeta, kisha akafumba macho na kuvutia kasi ya matukio ya mwisho aliyoyapitia kabla ya kuwa katika hali hiyo.

    “Mimi ni nani??”

    “Nesi”

    “Na huyu??”

    “Simjui”

    “Unaitwa nani??”

    “Joy..”

    “Joy nani”

    “Naitwa Joyce….Joyce Keto” alijibu maswali yote kwa ufasaha, mwanadada Joyce kuthibitisha kwamba alikuwa anajitambua kweli kweli.

    Daftari la maelezo ya mgonjwa lililetwa ili maelezo juu ya Joyce na mwenzake yaweze kuandikwa kwa kumbukumbu iwapo litatokea lolote linalohitaji maelezo yakinifu. Baada ya maelezo kutimia daktari aliondoka akiongozana na nesi na baada ya muda alirejea nesi akiwa peke yake. Joyce akaanzisha mazungumzo ambayo yaliwapelekea kuzungumza juu ya ujio wake pale hospitali.

    “Yule uliyekuwanaye ni nani hivi maana ameumizwa huyo..” nesi alimwambia Joyce.

    “Hata simjui…” alijibu Joyce.

    “Kuna watatu wamekufa basi hapa polisi watatuuliza maswali weee!!” nesi aliendelea kupiga soga na Joyce ambaye hakuwa muongeaji sana bali msikilizaji.

    Neno ‘Polisi’ likamwingia katika akili yake akaanza kuiona hatari ikimnyemelea. Akavikumbuka vitisho vya John Mapulu, kisha akamkumbuka Michael. Aliamini kuwa Michael alikamatwa kwa kesi ya mauaji na polisi walikuwa wakimsaka yeye (Joyce) kwa ajili ya kusaidia upelelezi. Joyce aliwaogopa askari na usumbufu wao lakini aliiogopa zaidi milango ya gereza.

    Mawazo ya kutoroka yakaanza kumjia lakini hakumpa nafasi yule muuguzi kuelewa lolote linalosafiri katika kichwa chake. Muuguzi yule bila kujua kuwa Joyce yupo katika kumdadisi alitoa ushirikiano wa kutosha, ushirikiano uliomwezesha Joyce kukiacha kitanda chake na kutoroka usiku huo.



    *****

    Asubuhi Matha alikuwa wa kwanza kuikanyaga sebule ya John Mapulu maeneo ya Mecco Mwanza, John aliyekuwa amelala aliamshwa na vishindo vya Matha. Akajiweka sawa kisha akanyata na kumkuta sebuleni. Sasa Michael aliamshwa pia akakaa sawa halafu Bruno akakamilisha idadi.

    “Akuanzaye….” John alianzisha maongezi. Hakuna aliyejibu, hakujali kuhusu hilo.

    “Tunaenda kwa pamoja kumnyamazisha milele yule bwege”, “kuna watu yupo nao ni watu hatari kiasi fulani lazima kuwa makini…..kuna watu amewashikilia ni wa msingi sana kwangu siwezi kumwacha hivi hivi….”

    “Saa ngapi??” aliuliza kiujasiri Matha.

    “Nne usiku wa leo tunamaliza kazi…halafu pia hakuna mtu kwenda kule Nyasaka patakuwa katika hali mbaya” alitoa maelekezo John Mapulu kila mtu akawa anamsikiliza.

    Baada ya maelezo Matha alipewa jukumu la kumpa Michael somo la haraka haraka juu ya tukio walilokusudia kulifanya.

    Matha aliutumia huo mwanya kumshawishi tena Michael juu ya kutoroka kwao. Lakini kinyume na matarajio yake Michael aliweka ngumu, huku akimtaja John Mapulu kuwa alikuwa msaada wake mkubwa tangu akiwa rumande na amemuhifadhi kwa siku zote bila ubaya wowote.

    “Ndo umemlipa kwa kumjaza mimba mpenzi wake eti?.” Aliuliza kwa kejeli Matha, hasira zilikuwa zimemzidia kutokana na ubishi wa Michael. Michael aliwahi akamziba mdomo Matha na kumsihi asizungumze maneno kama hayo. Matha akatulia, Michael naye akaanza kuzungumza akamlaghai Matha lakini bado Matha hakuonyesha kukubaliana na Michael.

    “Lakini kwani huyo Adrian yeye ana jeshi kubwa kiasi gani??” Michael alimuuliza Matha katika lugha ya maelewano makubwa.

    “Adrian ndo nani?”

    “Si huyo ambaye John anamwita bwege??” Michael akajibu bila wasiwasi, ikawa zamu ya Matha kukaa kimya na kuduwaa bila kumruhusu Michael kugundua hali hiyo. Jina la Adrian likawa limemshtua Matha. Japokuwa majina huwa yanafanana lakini hili jina lilimpeleka moja kwa moja kwa Adrian Mhina mpenzi wake wa kwanza kabisa kabla ya John Mapulu. Japokuwa ni muda mrefu ulikuwa umepita lakini penzi hili halikuweza kusahaulika, na mara ya pili walivyokutana ukubwani ni kama walikuwa wamelianza upya penzi lao. Kukutana kwao ukawa muda muafaka wa wao kuliendeleza penzi lao. Matha kimyakimya akakiri kuwa alifanya makosa makubwa sana kumkimbia Adrian na kuingia katika uhusiano na John Mapulu. Hatia iliyokuwa inamfuata akaamua kuitua kwa kumrudia Adrian kwa usiku mmoja, usiku uliowazaa wawili hawa upya wakalitamani lile penzi walilolipoteza. Matha aliamini kuwa John hakumtendea haki mwanaume mwenzake lakini alibaki kimya hakusema neno, leo hii John anataka kumuondoa duniani Adrian, hapana!!! Alikataa Matha ndani ya moyo wake. huruma ikamwingia alivyoijenga picha ya sura ya upole ya Adrian Mhina ikiwa katika mikono iliyokomaa ya John Mapulu, mikono isiyokuwa na huruma katika kuzigeuza shingo za maadui, mikono iliyozoea damu. Mikono ya mauti!!!

    Lile wazo la kutoroka likayeyuka upesi mithili ya barafu ndani ya maji ya moto. Akaisahau ile mimba na mmiliki wake kwa muda akaweka mbele huruma, akajiona ni muhusika wa kumweka Adrian matatani. Hakuwa tayari kusikia Adrian amekutwa ufukweni akiwa amekufa kwa kupigwa risasi. Hakutaka kabisa kumsikia John Mapulu akijitamba kuwa amemuua adui wake kirahisi sana.

    Matha akaamua kumtetea Adrian, hakumwambia tena Michael kuhusu kutoroka na pia hakuwa na uwezo wa kumwambia Michael juu ya Adrian Mhina maana aliutambua wivu wa Michael. Matha akatulia tuli akitafakari nini cha kufanya.

    Walijikuta wameelekezeana migongo, Michael akiwaza juu ya kumkomboa Joyce Keto kutoka katika mikono ya mtu ambaye John alimwita bwege (Adrian Mhina) huku Matha alikuwa katika kizungumkuti cha kutafakari anamzunguka vipi John Mapulu na Michael Msombe ili aweze kumwokoa Adrian Mhina katika janga hili. Yalikuwa yamebaki masaa machache, wawili hawa walikuwa wamesahau juu ya MIMBA!!!!



    ******

    Wazo la Matha juu ya kutoroka sasa halikuwepo tena, alikuwa katika mtihani mwingine mkubwa mno ambao ulikuja ghafla bila yeye kuutegemea. Alikuwa katika nafasi ya kufanya maamuzi mazito, maamuzi ambayo aidha yanaweza kumweka huru ama kumuingiza katika matatizo mengine mapya. Matha alikitazama kitumbo chake ambacho ni yeye binafsi aliweza kukisikia kikiwa kinaanza kuwa kigumu kigumu katika dalili zote za kiumbe kuanza kukomaa. Matha alifikiria juu ya mambo mengi sana ambayo ameyapitia na hatimaye akafikia katika kuwafikiria John Mapulu na Adrian Mhina.

    Matha alizifikiria fadhila alizotendewa na Adrian Mhina enzi hizo za penzi lao la utotoni, akakumbuka jinsi alivyokuwa akimjali na kumsikiliza bila kuwaza juu ya kebehi mbalimbali kutoka kwa jamaa na marafiki. Adrian alikuwa mwema sana kwa Matha na hakika alimpenda kupindukia. Matha alilitambua hilo na sasa lilikuwa likimtesa nafsi yake alijihisi ana hatia ya waziwazi, hatia ya kumsaliti Adrian na kuwa katika mahusiano na John Mapulu licha ya mema yote aliyomtendea wakiwa katika mahusiano ya siri, na sasa baada ya kukutana ukubwani na kukumbushia uhusiano wao Matha akidhani kuwa ni njia mojawapo ya kuifuta ile hatia iliyokuwa inamfuata kwa nyuma kila alipoenda tangu amkimbie Adrian kumbe alikuwa anajiingiza katika hatia kubwa zaidi. Na hii ilikuwa ni roho ya Adrian, roho iliyokuwa katika kila dalili ya kutolewa na jitu baya, jitu lisilokuwa na huruma wala nafasi ya kujiuliza mara mbilimbili iwapo liue ama lisiue.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ******



    Msichana mrembo wa haja alikuwa peke yake chumbani akiyafikiria mambo kadha wa kadha yaliyomjengea tabasamu hafifu na aina fulani ya mshawasha katika mwili wake, alirusha miguu huku na huko na kukipa tabu kitanda kilichobeba godoro la futi sita kwa tano pamoja na yeye kujikaza ili kisimwangushe. Ni kama kuna kitu alikitegemea muda wowote ule ambacho kingempatia furaha na faraja ya pekee, ndio alikuwa na kila sababu ya kutabasamu hasahasa alipokuwa akivitazama vidole vya mikono yake. Vidole hivi vilitegemea kuongeza mzigo usiokera usiku huo. Mzigo wa pete. Pete ya uchumba!!!

    Huyu alikuwa ni Monica hakika furaha aliyokuwanayo aliijua yeye mwenyewe na nafsi yake. Ulikuwa ni usiku wa kipekee alioungojea kwa siku nyingi na sasa ulikuwa umefika!!!! Adrian alikuwa ameamua kumvisha pete ya uchumba zikIwa ni dalili za mwishomwisho za kumuoa.

    Feni ya juu aina ya ‘panga boi’ ilikuwa inazunguka kwa kasi sana ili kukipa kile chumba hali nzuri ya hewa. Monica hakuutambua msaada wa pangaboi ile hadi ilipoanza kupunguza kasi na kukoma kuzunguka. Monica akawalaani wafanyakazi wote wa shirika hili la umeme akiwemo mama yake mzazi ambaye alikuwa ni muhasibu wala hakuhusika na huu mchezo wa zima washa. Zile laana zikaanza kukosa maana baada ya macho ya Monica kushuhudia nyumba za jirani pakimeremeta vyema.

    “Mh!! Mbona tuko ‘line’ moja??” alijiuliza kwa sauti ya juu kidogo. Alipogundua kuwa hakuwa na haja sana na huo umeme, akajirudisha kwa kasi kitandani akapokelewa na godoro lililokidhi haja ya kuitwa godoro.

    Mawazo juu ya usiku huo wa aina yake yakarudi tena. Monica akiwa amefumba macho akaileta picha ya Adrian akiwa na rafiki zake watano aliowaalika katika tafrija hiyo fupi ya kuvishana pete halafu akawafikiria pia shoga zake aliowaalika, alijua kuwa wataumizwa sana na kitendo hicho cha kuvishwa pete na hilo hasa ndilo lilikuwa lengo lake ‘Kuwakomoa’ waliosema kuwa hataolewa na Adrian.

    “Watanunaje!!!!!!!” Monica akajikuta akisema kwa sauti ya juu kisha kikafuatia kicheko kikali sana kilichokoma ghafla baada ya kubaini kuwa hakuwa akicheka peke yake. Mbele yake kulikuwa na mfano wa kundi dogo la watu lisilokuwa na habari naye. Kundi hili ni kama lilikuwa likimngojea amalize kwanza kuwaza ndo liombe ruksa ya kuwa pale chumbani.

    Monica alitaka kujiaminisha kuwa wale ndo rafiki zake Adrian ambao aliwaalika kwa ajili ya kushiriki naye katika tafrija ya usiku huo. Lakini wageni hadi chumbani kwangu!!! Alijiuliza Monica, na mbona hawajachangamka kabisa.

    Hawawezi kuwa wageni hawa!!!! Aliendelea kuwaza na kuwazua.

    Jibu lilipokuwa gumu huku akiwa bado kaduwaa, jibu la uhakika lilitolewa. Mmoja kati ya wanaume waliokuwa hapo chumbani akachomoa kitu mfano wa mti uliochongwa vyema. Lakini mbele kilikuwa ni kijicho cha aina yake.

    Bunduki!!!.

    Monica akaanza kutetemeka, jicho likafunguka hadi hatua ya mwisho. Sura zote zilikuwa katika hali ya ukatili. Dalili ya urafiki haikuwepo kabisa.

    “Yupo wapi hawara yako??” sauti kali ya kiume ilimuuliza mwanamama huyu.

    “Si…si..siju..i” alijiumauma wakati akijibu swali hilo. Kiganja kilichotua kwa nguvu katika uso wake mweupe kiliacha alama za vidole vitano katika paji la uso wake na kisha kufuatiwa na kilio kikali.

    “Shhhh!!!!!!!” Kidole cha shahada katikati ya mdomo wa John mapulu kilimnyamazisha Monica akabaki kulia kwa kwikwi.

    “Yupo wapi Adrian…..” safari hii John aliuliza kwa utulivu. Monica naye akajaribu kuulazimisha utulivu, lakini bado alikuwa anatetemeka.

    “Sijui alipo…ila alisema kuwa atakuja” alijaribu kuzungumza japo kwa kutetemeka.

    “Hujui eeh!!” alizungumza kwa sanifu John. Kisha akawaamuru Michael na Bruno kumchukua Monica. Kama walivyoambiwa palepale wakamtwaa mzegamzega na kuanza kutoka naye nje.

    “Michael mwache Bruno amchunge huyo we njoo huku” aliamuru John, Michael akatii.

    Monica akabaki katika mikono ya Bruno. Michael na John wakaanza kuikagua vyema nyumba kama kuna uwezekano wa mabaki yoyote yanayoweza kuwasaidia kujua wapi Adrian yupo. Hawakupata chochote kile!!!



    Kishindo kilichosikika kwa nje kikawawekawawili hawa katika tahadhari kila mmoja akatoka akiwa ameiweka sawa silaha yake.

    Kitu kama furushi kilichomoza gizani, Michael akiwa ameitanguliza bunduki yake mbele alikimulika kwa tochi yenye mwangaza hafifu huku akikisogelea. John alikuwa anaelekea upande mwingine.

    “John!!” Michael aliita kwa sauti ya chini lakini iliyomfikia John. John hakuitika bali akarejea katika namna ya tahadhari kuu. Alipomfikia Michael alilitazama lile furushi, lilikuwa linapanda juu na kushuka chini. Halikuwa furushi bali alikuwa ni Monica mchumba wa Adrian akiwa amefungwa kamba vyema mikononi.

    “Bruno yuko wapi??” John aliuliza swali hilo, lakini aliamini kuwa hatapata jibu lolote kutoka kwa Michael kwani wote walikuwa wametokea ndani na walikuwa wamemwacha Bruno nje.

    Monica aliachwa hivyo hivyo akiwa amefungwa kamba. Michael na John wakaanza kumtafuta Bruno.

    “John!!!” Michael aliita, safari hii sauti ilikuwa ya juu mno. John akakurupuka kutoka alipokuwa akakimbilia sauti ilipotokea.

    Sasa kilikuwa ni kifurushi kingine lakini hiki cha sasa hakikuwa kikipanda na kushuka. Kilikuwa kimetulia tuli, huku kikiwa kina rangirangi nyekundu zisizokuwa rasmi.

    Kifurushi hiki kilifanana na jamaa yao na John , aliyeitwa Bruno.

    Walipokiita kwa jina hilo hakikuitika wala kutetemeka.

    Bruno alikuwa maiti!!!

    Kifua chake kilikuwa kimeruhusu risasi kupita katikati yake.

    Hofu ikatawala!!! John akapandwa na hasira. Akakitazama kifurushi kilichokwenda kwa jina la Monica. Akaiweka bunduki yake katika kiwambo cha kuzuia sauti.

    Akafyatua!!! Monica akaungana na Bruno katika safari hiyo!!!!!

    Michael na John wakatoweka. Huku wakiamini kuwa vita ndiyo imeanza.

    Kwa miungu yote aliyoiamini Michael alikuwa akiomba Joyce aendelee kuwa salama. John Mapulu yeye alikuwa akimlaani Adrian kwa kuianzisha vita hiyo.





    ****



    Adrian alikuwa kama anayekaribia kuchanganyikiwa, suala la Stallone kupoteza uhai akiwa katika kutekeleza alichomuagiza kulimtia katika hofu kuu. Aliamini alikuwa katika kuwindwa na muuaji, muuaji aliyeihalalisha roho ya Stallone kuingia peponi.

    Hata ule mpango wake wa kumvisha pete Monica aliuona kuwa ni batili sasa. Upesi upesi Adrian aliichukua simu yake na kuandika ujumbe mfupi wa kuhairisha shughuli hiyo kisha akautuma kwa wahusika wote.



    Baada ya zoezi hilo akaamua kuizima simu yake huku akiweka namba ambayo ni Monica na watu wengine wachache muhimu waliokuwa wanaitambua.

    Baada ya hapo aliingia katika mgahawa mmoja akaagiza kinywaji chenye kilevi. Alifanya hivyo kwa kurudia chupa hadi zikafike nne, alikuwa anakunywa kwa mfumo wa kupiga tarumbeta, hakutumia glasi iliyowekwa mbele yake. Mfululizo huu uliendelea hadi alipoanza kuona glasi iliyokuwa mezani ikizaa nyingine na kuwa mbili. Mara miujiza mingine na meza zikawa mbili na hata wahudumu wakaanza kuja wawili wawili kumuhudumia.

    Adrian akatabasamu!!!

    “We malaya..kuna vyumba hapo.” Aliuliza kwa sauti ya kilevi.

    “Vipo shilingi elfu kumi na tano!.” Alijibu yule mwanamke bila kujali alikuwa ametukan wa kabla ya kuulizwa. Hata kama angekataa kutoa huduma, angekuja mwingine angeitwa jina hilo hilo na angetoa huduma kama kawaida bila kinyongo.

    Akili ya Adrian bado ilikuwa na uwezo wa kufanya kazi. Akampatia yule msichana shilingi elfu ishirini kwa ajili ya chumba.

    Chumba kikalipiwa, chenchi haikurudishwa.

    Ningeitoa wapi kama ningekataa kuitwa malaya??? Alijiuliza yule muhudumu huku akiitia vyema katika pochi yake.

    Adrian alikuwa amejiweza kwa dozi ya pombe aliyojipatia kwani alipoingia tu alipitiwa na usingizi murua. Hakukumbuka hata kuvua viatu.

    Adrian alipoteza kumbukumbu majira ya saa tano asubuhi na sasa ilikuwa imetimu saa nne usiku, kumbukumbu zikarejea. Masaa kumi na mbili ya kuwa mbali na dunia.



    ****



    Suala la kumshirikisha kila jambo Michael Matha alianza kuliona kuwa ni la kipumbavu. Baada ya kuwa kimya kwa muda mrefu akifikia maamuzi yake ya kimya kimya si Michael wala John aliyepatwa na wasiwasi baada ya Matha kuwaeleza kuwa hataweza kuandama nao kwenda kumuadabisha Adrian.

    Michael alisikitika sana kwani alijua ni kipi kinamsumbua Matha. Michael alidhani Matha anasumbuliwa na utata wa mimba yake, lakini haikuwa hivyo wakati huu.

    Matha alikuwa katika mgongano wa nafsi yake akijifikiria jinsi ya kumwokoa Adrian katika kifo kisichomuhusu hata kidogo.

    Baada ya kuhakikisha kuwa John na timu yake wametoweka, harakaharaka Matha alimpigia simu Adrian. Simu iliita mara ya kwanza haikupokelewa, mara ya pili ikapokelewa.

    Sauti ya Adrian ilisikika ikiwa imetawalia na uoga. Matha aliligundua hilo lakini hakumuuliza.

    “Adrian mambo vipi mpenzi wangu?” Matha alizungumza kwa utulivu huku akiwa amezibana pumzi zake asiweze kusikika kama anahema kwa kasi.

    “Matha...hebu ngoja kidogo nitakupigia baadaye.” Alijibu Adrian kisha akakata simu. Matha alitaka kuongezea neno lakini tayari simu ilikuwa imekatwa.

    Haraka haraka Matha akabonyeza tena kitufe ili ampigie Adrian.

    Hakuwa anapatikana tena na tayari ilikuwa saa tatu usiku!!!!



    Matha alichanganyikiwa, alijiuliza ni kipi kinamsibu Adrian huko alipo. Wasiwasi wake ukawa kwamba Adrian anaweza akawa ameingia katika mikono hatari ya John Mapulu.



    Mwanaharakati huyu wa kike akaamua kucheza pata potea. Upesiupesi akavaa bukta ngumu na viatu vya michezo. Akabeba pochi yake ambayo kwa wanawake wa kawaida ungeweza kukuta wameweka vipodozi, kanga ya dharula, na simu zao. Lakini Matha hakuwa mwanamke wa kawaida sasa!!! Yeye alikuwa amehifadhi, visu viwili vyenye sumu kali katika ncha ya mbele. Bastola ndogo kabisa na unga unga mweupe usiokuwa kwa matumizi ya kawaida kwa watu wa kawaida.



    Kama mwanajeshi kamili aliyefuzu mafunzo kambini, Matha alilifunga geti akatoka nje. Giza lilikuwa nene lakini halikumtisha hata kidogo, ni yeye aliyelitisha giza hilo. Hatua kwa hatua, akakutana na dereva wa pikipiki. Akamsimamisha akapanda. Alivyokaa kwenye kiti, ile pensi yake ikapanda juu zaidi mapaja yakawa nje akafanana na wale machangudoa ambao huo ndio ulikuwa muda wao wa kutoka.

    “Wapi hiyo dada!!.”

    “Isamilo fasta.” Alijibu Matha.

    “Buku saba ipo hiyo.” Matha hakujibu kitu, pikipiki ikawashwa na kuanza kukata upepo kuitafuta Isamilo.

    “Niache hapahapa.” Matha walipoikaribia nyumba ya Adrian alimsihi mwendesha pikipiki. Naye akatii. Matha akatoa shilingi elfu kumi.

    “Nenda tu usijali.” Matha alimweleza yule mwenye pikipiki baada ya kumuona akihangaika kusaka chenchi. Dereva akashukuru akapanda pikipiki akatoweka kwa mwendo wa kawaida.



    Matha hakupiga hatua yoyote mbele badala yake alitulia tuli na kufanana na mti mkavu usio na matawi. Kuna jambo alikuwa analingojea. Tano...nne....tatu....mbili....puuu!! kilisikika kishindo kidogo, Matha akageuka na kutimua mbio kuelekea kishindo kilipotokea.

    Alijuakilichokuwa kinaendelea!!!CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alimkuta yule mwendesha pikipiki akiugombania uhai wake, alikuwa amejikita kumkabili israeli ili asiweze kuondoka na roho yake. Lakini Israeli alikuwa yupo katika kushinda na aliyejua hayo alikuwa ni Matha mtoto wa Mwakipesile. Dereva hakujua kama alitoa shukurani yake ya mwisho duniani. Matha alikuwa ameandaa ile noti ya shilingi elfu kumi kwa ajili ya kuondoa uhai wa dereva huyu. Matha alikuwa na shida na pikipiki. Hakuwa na njia zaidi ya kuua.

    Mwendesha pikipiki akaiaga dunia na kuiacha pikipiki yake ikiwa hai.

    Matha akatoa ‘glovus’ akavaa mikononi. Akainyanyua pikipiki akaufunga mkoba wake kwa nyuma akakaa juu yake. Akaipiga stata ikaitika, akapepea nayo.

    Akafunga breki katika baa moja ambayo hadi wakati huo ilikwa haijafungwa bado.

    “Samahani babu..aah!! shkamoo.” Matha alitoa salamu zake. Mzee aliyekuwa na mvi lakini akionekana kuupenda bado ujana alijibu kinyonge. Huenda hakupenda kusalimiwa.

    Matha alimnyenyekea yule mzee ambaye alikuwa ni mlinzi katika baa ile. Akamsihi amlindie pikipiki yake kwa ujira maalumu. Yule mzee akachangamka. Akakubali biashara, Matha akapaki pikipiki yake ya wizi. Akampatia shilingi elfu tano kama kianzio cha biashara. Kisha akatoweka kwa mwendo wa kawaida kama asiyekuwa na haraka, alipofika katika uchochoro akaanza kutimua mbio. Aliupita ule mwili wa mwendesha pikipiki kwa kuuruka kama vile gogo.

    Bunduki mkononi, Matha akawa ananyata sasa. Macho yake makali yaliweza kung’amua baadhi ya vitu gizani. Alisubiri kwa muda na sasa alichokingojea alikiona. Alishuhudia, viwiliwili viwili vikiwa katika hali tofauti. Kimoja kilikuwa cha kiume kikiwa wima na kingine cha kike kikiwa katika mateso makali, kilikuwa kimefungwa kamba.

    Baadaye kidogo kiwiliwili cha kiume kikaanza kunyata kuelekea gizani, Matha naye alianza kunyata kwa kutembelea vidole. Hakuweza kusikika. Alipoweza kukiona kiwiliwili kile tena sasa kilikuwa kimemkaba koo mwanaume. Huyu alikuwa ni Adrian na kiwiliwili kiliitwa Bruno. Mwanga hafifu ulimuwezesha kutambua hilo.

    Matha alishukuru kwa kumkuta Adrian akiwa hai, sakata la kukabwa na Bruno hata halikumshtua. Aliiweka bastola yake sawasawa, huku akihakikisha kuwa ipo katika kiwambo cha kuzuia sauti.

    Matha alitabasamu baada ya kumwona Adrian akiwa ametulia tuli kwahofu. Ni hivyo alitaka iwe, ili aweze kuipata shabaha yake vyema.

    Bastola ilinyanyuliwa, kisha ikakohoa kimyakimya, kama vile gunia Bruno akatua chini. Akiwa hana taarifa yoyote Adrian, katika taharuki kubwa alipitiwa kwa kasi kama vile mwewe anavyonyakua kifaranga, alikuwa amezibwa mdomo huku akilazimishwa kukimbia.

    Hakuamini kwa yule ni Matha!!!

    Haukuwa muda wa kuulizana maswali wala kutoa majibu. Adrian alilazimika kufuata amri.

    Matha alimsihi Adrian amsubiri mahali kwa dakika mbili. Adrian akaulia Matha akatoweka.

    Mzee alikuwa ameanza kusinzia Matha alipofika pale. Matha alimshtua naye akashtuka huku akizuga kuwa alikuwa hajalala.

    Matha alitaka kumtokomeza naye duniani lakini huruma ikamshika. Akamsamehe. Akamwongeza elfu tano nyingine,biashara ikaishia hapo!!!

    Pikipiki ikafunga breki miguuni mwa Adrian. Akatoa ukelele wa hofu.

    “Panda!!!.” Sauti ya kike iliamrisha. Ady akapanda.

    Kwa kasi kubwa mwanadada akaindoa ile pikipiki kutoka eneo lile.

    Walipoufikia mji, Matha akasimamisha ile pikipiki eneo ambalo halikuwa na watu wengi. Adrian akashuka, wakaanza kuelekea mahali alipopajua Matha na halmashauri ya kichwa chake.

    Wakaitelekeza pikipiki. Wakaenda nyumba ya kulala wageni. Kila aliyewatazama alijua kuwa Adrian alikuwa ameopoa changudoa mshamba anayekubali kuingizwa gesti hovyo.

    Haikuwa kama walivyodhani.!!!



    ****



    Jitihada za John na Michael kumsaka adui yao ambaye amemuua Bruno hazikuzaa matunda.

    “Adui katuzidi ujanja...hapafai hapa.” John alimtahadharisha Michael. Michael akakubali kwa kichwa. Wakatoweka eneo lile!!! Kwa tahadhari kubwa sana.

    Raundi ya kwanza John Mapulu na Michael Hoi!!!

    Mwili wa Bruno uliachwa palepale. Michael na John. Usiku ule ndio ulikuwa wa mwisho kuingia katika nyumba yao ya Mecco.

    Njia nzima walikuwa wakifikiria jambo moja tu. Kumchukua Matha na kutafuta hifadhi nyingine ya siri kwa muda wakati mapambano haya yakiendelea.

    Geti lilikuwa limefungwa kama ilivyo ada. Walifika na kutaka kugonga ili Matha awafungulie kwani simu yake haikuwa ikipokelewa kwa muda mrefu.

    Ilikuwa saa tisa kasorobo za usiku!!! Palikuwa kimya huku mbwa wakishindana kubweka pasipo sababu za msingi.

    Michael alijaribu kusukuma geti. Maajabu!!!! Likafunguka bila kikwazo chochote

    Tahadhari!! Kwa wote John na Michael.

    Hali ya hatari!!!

    John akachomoa bastola akaiweka makini kabisa kiwambo cha kuzuia sauti kikiwa katika utendaji kazi.

    Michael akalikanyaga geti. Likafunguka. Waaa!!!

    John akaingia upesi bunduki mbele, macho huku na kule.

    Hakuna kitu!!

    Michael naye akiwa katika hali ambayo hajapata kuwa nayo hapo kabla alihaha huku na kule huku John akiwa anamlinda na bunduki mkononi. Jitokeze ewe kiumbe hai na ubadilishwe kuwa maiti!!!

    Hakuna aliyejitokeza. Zama mpaka ndani, msako wa chumba kwa chumba. Hakuna kiumbe hai aliyejitokeza.

    Hofu kwa wote wawili.

    Hata Matha hakuwepo!!1

    Matha ametekwa!! Wote waliwaza hivyo. John akahisi kuchanganyikiwa. Kile alichokuwa anakipigania sasa kimetoweka pia.

    Adrian ameniwahi!! Alijisemea John. Michael akaguna.

    Hakika Matha hakuwepo eneo hilo. Wala vyumbani hakuwepo.

    Ameenda wapi? Wamempeleka wapi? Hayo yakawa maswali magumu kujibika. Mtihani!!!

    Hawakupata majibu. John akatoa maamuzi. Wakatoweka eneo lile. Tayari halikufaa tena kukalika. Walifunga kwa nje kufuri imara kabisa. Wakachukua vifaa walivyovihitaji kwa mapambano.

    Wakatoweka kwa uangalifu wa kufungiwa tela na maadui.

    Nyumba ya kulala wageni ndio ikawa makazi yao usiku huo.

    Michael akiwa katika mtihani mgumu sana. Joyce Keto, msichana aliyempenda kwa mara ya kwanza katika maisha yake sasa alikuwa amepotea kwa mara ya pili baada ya kuwa amepatikana tena. Mwingine ni Matha, msichana ambaye ni mali ya John Mapulu, msichana ambaye sasa amembebea mtoto katika tumbo lake ikiwa imebakia miezi kadhaa aweze kujifungua. Naye alikuwa ametoweka. Tena ghafla katika mazingira ya kutatanisha.

    Adrian!! Jina hilo lilivagaa kichwa chake na kumshtua moyo wake. Ni Adrian alikuwa anahusika na utekaji wa wawili hawa. Bahati mbaya iliyoje, Michael hakuwa amewahi kuonana na Adrian.

    Wakati Michael akiumizwa kichwa na mawazo haya, John ambaye alionekana kama amesinzia alikuwa hoi akishambuliwa na mzimu wa Adrian. Hakuwa na jingine la kufanya zaidi ya kuulaani mzimu huu. Mzimu unaomkosesha raha.

    Nikimpata nitamuua!!! Alinuia John.

    Hilo lilikuwa wazo lake la mwisho kabla ya kupitiwa na usingizi. Wakati anasinzia Michael alikuwa anakoroma.



    ******



    Hapakuwa na ushahidi wowote ulioweza kumtia Defao hatiani. Baada ya kusota rumande siku tano aliachiwa huru. Hakuwa na kesi yoyote ya kujibu. Maelezo yake yalikuwa yamenyooka na kwa kiasi kikubwa yalichangia yeye kuikwepa hatia.

    Siku tano rumande na tatu za kukaa hospitali zilitosha kumkongoroa haswa kijana huyu wa Singida aliyeponzwa na tamaa ya kupata mali nyingi na sasa alikuwa matatani.

    Ilikuwa ni bahati ya kipekee kwa Defao kuukwepa mtihani huu. Au labda tuseme ni Mungu aliegemea upande wake kwa kiasi kikubwa. Kwa hali halisi kesi kama hiyo isingeweza kumwacha lofa kama Defao arejee mtaani tena kuvuta hewa safi bure.

    HATIA ikamuangukia Joyce, ambaye alitoroka hospitali!!!



    Defao akafanya ishara ya msalaba na kisha kufanya majuto kidogo kwa kuilaani ardhi ya Mwanza kwa dhahama iliyompatia.

    Baada ya kukabidhiwa vifaa vyake vichache alivyokutwa navyo baada ya kutiwa hatiani Defao alitoweka. Alikuwa na noti kadhaa. Akataka kupanda daladala lakini akagundua kuwa mwili wake ulikuwa unatoa harufu sana. Akataka kupanda teksi napo akagundua pesa yake haikuwa ya kutosha sana.

    Alipofikiria juu ya pesa kutotosha, akakumbuka pesa zake nyingi alizoziacha chini ya kitanda katika hoteli aliyolala mara ya mwisho kabla ya kukumbwa na haya yaliyomkuta.

    Moyo ukashtuka na kusukuma damu upesi. Ilikuwa taarifa ya kushtua sana. Defao akajiwekea imani kuwa huenda ile pesa bado ipo mahali alipoiacha. Japo imani hiyo hakuipa nafasi kubwa sana.

    Defao akachukua maamuzi. Akaingia vyoo vya kulipia kwa ajili ya kujipatia huduma ya kuoga. Akalipia akaipata huduma hiyo. Akapaka mafuta mengi ili aweze kung’aa. Mafuta yalizidi usoni na kumfanya kwa namna moja awe kichekesho mbele ya watu.

    Hakujali!!!

    Sasa aliweza kupanda daladala. Akashukia mahali ilipokuwa hoteli aliyofikia mwanzo. Awali alikuwa anajiamini sana kurejea hotelini pale lakini mara akaanza kujihisi uoga na hofu baada ya kulitazama bango la hoteli ile.

    Hofu yake ililetwa na muonekano wake. Na mapokezi atakayoyapata katika hoteli hiyo, pia alijiuliza ni vipi asipozikuta zile pesa zake alizozificha pale. Siku yake inayofuata itakuwa vipi na maisha yake Mwanza yataendaje. Hana ndugu wala rafiki.

    Mungu saidia nikute walau nauli tu!! Ya kwenda Singida. Defao aliomba kwa Mungu wake.

    Kisha akaanza kutambaa gizani akiambaa pembezoni mwa barabara hadi akafikia sehemu ya mapokezi. Sura iliyokuwa pale mapokezi ilikuwa ngeni kabisa machoni mwake. Haikuwa sura aliyokutana nayo siku alipokuwa analipia chumba kimadaha. Huyu alikuwa mwingine!! Defao akashukuru kimoyomoyo kwani angekutana na sura anayoifahamu lazima angekumbana na maswali mengi ambayo yangembughuzi na kumwongezea hofu.

    “Kuna vyumba?.” Defao aliuliza kwa sauti iliyokuwa inatetemeka.

    “Mh!! Yah!! Vipo.” Yule dada alimjibu kwa mashaka kidogo huku akimtathmini hadhi yake ya kuwa hapo. Alikuwa akijiuliza iwapo kaka huyo mbele yake hajaziona nyumba nyingine za kulala wageni zenye hadhi sawa na yeye.

    “Vyumba vipi vipo wazi...” Swali hili kutoka kwa Defao likamdhihirishia yule dada kuwa mtu aliyeko mbele yake hakuwa mgeni wa eneo hilo. Imani ikarejea!!

    Badala ya kujibu kwa maneno, yule dada akampatia Defao orodha ya vyumba.

    Moja kwa moja akatazama chumba namba 18. Kilikuwa na mtu!! Na hakuwa wa kutoka siku hiyo.

    Shit!!! Alilaumu Defao. Akategemea yule mwanadada atamuuliza kitu. Hola!! Hakuulizwa.

    Nipe namba 25!! Hatimaye alitaja chumba alichokichagua. Akatoa pesa akalipia. Akaandikiwa chumba hicho kisha akapewa kijana maalum kwa ajili ya kumsindikiza.

    Hakuwa na mizigo!!

    “Ukitaka kuwasha taa unatumia kikadi hichi, ukitaka kutumia simu......”

    “Najua kila kitu toka njea!!!” Alitoa karipio kali Defao. Yule kijana akakoma kuzungumza kisha bila kuaga akatoweka.

    “Njoo ufunge mlango pumbavu wewe!!!” Defao akabwatuka baada ya kugundua kuwa mlango umeachwa wazi. Maneno hayo hayakumfikia yule kijana. Defao akasonya kisha akainuka na kwenda kuufunga mlango.

    Akarejea na kujirusha kitandani!! Akatua kama ambaye anaangukia mayai. Aliona aibu uchafu wa nguo zake kulalia mashuka meupe!!!

    Hasira zilikuwa zimemkaba kooni. Yule Defao aliyekuwa na mamilioni ya shilingi siku kadhaa nyuma. Leo hii hana hata senti tano mfukoni. Tumbo likaunguruma akatanabahi kuwa ni njaa. Hasira ikazidi.

    Yote haya kisa ni Pesa. Pesa ya bwelele. Pesa kutoka kwa John Mapulu na mpenzi wake. Matha Mwakipesile.

    “Hivi nimemuua John?.” Ghafla Defao alijiuliza!!!

    kujiuliza huko kukamfanya atetemeke na kutoamini ke imemteketeza John Mapulu!!



    *****



    *****CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    John Mapulu hakuwa amekufa kama Defao alivyoweza kufikiria. Lakini alikuwa kama mfu. Kila mpango wake ulikuwa batili. Alijaribu kumuwinda Adrian bila mafanikio yoyote yale. Michael alikuwa anaogopa kumsemesha jambo lolote kiumbe huyu kwani majibu aliyokuwa anayatoa yalikuwa yanasikitisha sana na wakati mwingine yalikuwa yanatia kero.

    John alikuwa katika majuto makubwa. Licha ya kuwa mbabe katika matukio makubwa makubwa. Mbele ya hili la kutekwa kwa Matha na Joyce alikuwa kiumbe dhaifu aliyeamini kuwa ameshindwa kumsaidia chochote Matha na pia aliamini kuwa amemfadhaisha Michael kwa kukaa kimya muda mrefu bila kumueleza juu ya uwepo wa Joyce Keto.

    Yaani Matha naye kweli ameshindwa kabisa kufanya lolote kujiokoa na huyu jamaa? John alijiuliza huku akiwa ameyafumba macho yake. Alimjengea picha Matha kama mwanamke aliye na chembe za mwanaume jasiri na makini ndani yake. Hakuwa mtu wa kukubali kushindwa kirahisi.

    Au jamaa walimpiga risasi? Alijiuliza tena. Katika hili hakutaka kuumiza kichwa chake kufikiria kuuona mwili wa Matha ukiwa umepasuka kifuani baada ya kushindiliwa risasi mfululizo alipojaribu kujitetea kwa kurusha mateke kadhaa aliyomfunza.

    Zilikuwa zimepita siku kadhaa na hakuwa amepata taarifa zozote zile juu ya kifo cha matha na Joyce au walau simu kutoka kwa mtekaji kumfahamisha alikuwa na shida gani hadi amewateka wawili hao.

    Timu anayoshirikiana nayo imejipanga!! Alikiri kwa sauti ya juu kiasi John. Michael Msombe akasikia lakini hakuchangia chochote.

    Tayari walikuwa wamehama nyumba za kulala wageni zaidi ya nne. Na sasa walikuwa Kisesa nje kidogo ya jiji la Mwanza.

    Michael akiwa msikilizaji na John mtendaji.

    Simu ya John ilipotoa mlio. Iliwafanya wawili hawa kushirikiana kuitazama simu ile kisha bila kutegemea wakatazamana.

    “Nani anapiga?.” Michael alimuuliza John. Hakujibiwa!!!

    John akaitazama simu iliyokuwa inaendelea kuita kisha akaipokea. Akaunguruma kwa sauti yake iliyojaa shari kama kawaida.

    “Mambo vipi mzee!! Umelala?.”

    “Aaah! Nipo tu!! Uchovu, vipi nambie.”

    “Aaah! Umenitupa mzee mzima vipi?.”

    John hakujibu!!

    “Vipi lakini dadangu mzima.”

    “Mzima tu kwani vipi?.” Alihoji John. Swali kutoka kwa mmoja wa waliokuwa kaka zake na Matha lilimtia mashaka.

    “Ah! Hamna nilimfananisha tu. Ndio maana nikataka nimjulie hali huenda nimemkumbuka tu!!.”

    “Wapi tena? Lini?.”

    “Huku Nyegezi, kwenye magari ya kwenda Arusha kitu kama hicho!!.”

    “Mh!! Arusha. Ujue nini, mimi nimesafiri kidogo. Sina taarifa zake halafu tulikuwa tumegombana kidogo si unamjua tena dadako. Ehee!! Ni gari gani hiyo.” John aliufuma uongo upesiupesi akaurusha kwa mzungumzaji upande wa pili.

    “Sijui ni basi gani lile sikutilia maanani, limeondoka kama saa mbili na nusu hivi.”

    John akatazama saa yake ilikuwa saa tatu na dakika tano.

    “Ahaa!! Huenda wamefanana tu!! Ngoja nipige simu nyumbani, nitakujulisha.”

    “Haya shemeji yangu, si unajua tena tunakulindia maana alikuwa na kidume yule kamganda kama nini. Sijui ni yeye ama vipi.”

    Akaendelea kuchombeza. John akawa anamsikiliza.

    “Basi poa Kelvin. Namba yako si ina huduma zile za kupokea pesa eeh!!.”

    Kelvin akakubaliana na John. Simu ikakatwa.

    John alikuwa anautambua usumbufu wa Kelvin akiwa hana pesa. Akamtumia kiasi cha pesa muda uleule kisha akajikita katika kuitumia ile taarifa aliyopewa na Kelvin.

    “Adrian anamtorosha Matha kuelekea Arusha.” John alimweleza Michael.

    “Vipi kuhusu Joyce?.” Michael aliuliza. John akakosa la kujibu.

    “Naondoka sasa hivi kuelekea huko wanapoenda. Itakubidi uhame hii hoteli.....eeh!! tutaondoka wote.” John alimweleza Michael huku akijiweka sawa. Michael naye akaendelea kuwa msikilizaji kama kawaida yake.

    Baada ya nusu saa walikuwa ndani ya teksi. Safari ya kwenda Nyegezi stendi.

    John alikuwa makini kabisa asiweze kukutana na Kelvin. Na hakumpa taarifa yoyote baada ya kumtumia ile pesa. Michael naye alikuwa akifuata yote yaliyotamkwa na John.

    Kwa kuwatumia watu wake walioko maeneo ya stendi ya Nyegezi ilimchukua nusu saa nyingine kupata jawabu kuwa hakuna abiria aliyesafiri siku hiyo akiwa na jina la Adrian lakini Matha alikuwepo.

    “Huyu amekata tiketi peke yake, hakuwa na mtu!!!.” Alipewa maelekezo hayo. Akashusha pumzi kwa fujo sana. Alianza kupoteza matumaini.

    John hakubarikiwa akili ya darasani lakini alikuwa na uwezo mkubwa wa kufikiri katika mambo mengine. Na alikuwa mwepesi wa maamuzi katika mambo magumu.

    Alipiga simu mara tatu. Kwa watu tofauti tofauti. Baada ya robo saa, akakabidhiwa gari aina ya Landcruiser na mmoja kati ya watu aliofahamiana nao.

    “Michael. We baki huku Mwanza. Nitahitaji sana msaada wako nikiwa huko niendako.” John alimnong’oneza Michael. Michael akaiona hofu iliyotanda katika uso wa John. Hakuleta ubishi wowote.

    Akapatiwa fungu la pesa!! John akazama garini.

    Akatoweka!!!

    Michael akaondoka akiwa ameinamisha kichwa chini. Miwani nyeusi ikiwa imehifadhi macho yake. Alikuwa amekata tamaa.

    Aliponyanyua kichwa chake kukabiliana na barabara ndefu ya kutoka stendi ndio hapo alipomuona!!!

    Mapigo ya moyo yakajitahidi kuongeza kasi. Akaivua miwani yake. Akatazama zaidi ni hapo alikuwa amemuona!!!

    Amuite ama asubiri!! Asubiri kitu gani sasa.

    Hakuwa peke yake.

    Macho hayakuwa yakimdanganya ni yeye!!!

    Ni yeye!!!



    ****



    Defao hakuweza kuupata usingizi kabisa. Hata hivyo hakuhitaji kupitiwa na usingizi.

    Wa nini sasa huo usingizi?

    Alikuwa akiwaza na kuwazua juu ya siku yake ya kesho na nyingine zilizosalia hapo Mwanza ataishi vipi? Alitamani sana kuingia katika kile chumba. Lakini bahati mbaya kilikuwa kina mteja. Usingizi huwa hauna hodi. Hatimaye ukamtwaa. Akalala!! Uso wake ukiwa na majonzi tele.

    Asubuhi ikafika!! Alitakiwa kulipia chumba upya tena!!

    Pesa haikuwepo tena!!!

    Hakuwa na budi kukiachia chumba. Defao akaingia kujichanganya mtaani. Kwa mavazi aliyokuwa amevaa alifanania na mlevi wa pombe za kienyeji asiyejielewa kabisa.

    Aanzie wapi? Hilo lilikuwa swali.

    Defao akaikumbuka simu yake. Aliyoinunua kwa bei ghali kipindi kile ana pesa. Akawaza kuiweka rehani aweze kupata senti kadhaa. Wazo hilo likapita katika kichwa chake.

    Ilikuwa saa nane mchana na njaa ilikuwa imemtafuna haswaa!!

    Kizuri chajiuza, kibaya chajitembeza.

    Haikuchukua muda akawa ameiuza kabisa maana hakuwa na mahali popote pa kuiweka rehani. Pesa aliyoipata si haba!! Ilimtosha kupata chakula kizuri na pia aliweza kulipia tena nyumba ya kulala wageni.

    Ileile ambayo aliamini kuna pesa zake. Sasa Defao alikuwa ameamua litakalokuwa na liwe.

    Usiku huu akiwa katika chumba kilekile alicholala usiku uliopita. Aliijiwa na wazo hilo la liwalo na liwe.

    Alijongea kutoka chumba chake. Hatua kwa hatua hadi chumba namba 18. Hofu ikamtwaa akahisi hatakuta chochote ndani ya chumba hicho ama anaweza kukumbana na ugumu kutoka kwa mteja aliyepanga katika chumba hicho.

    Eeh!! Mwenyezi Mungu saidia wasiwe wawili!! Defao alifanya sala fupi kwani alijua kabisa wakiwa mwanaume na mwanamke watakuwa na biashara zao nyingine ambazo kuwakatisha itakuwa ngumu sana na pia inaweza kumwekea matatizo kwani muhudumu wa mapokezi tayari alikwishamwekea mashaka tangu siku alipoingia mara ya kwanza tangu atoke rumande.

    Akapiga moyo konde!! Akaunganisha kiganja chake akagonda mlango!!

    Mara ya kwanza!! Kimya...akagonga tena. Kimya!!

    Mara ya tatu akasikia kitanda kikilalamika. Aah!! Wanafanya mambo yao hawa!! Aliwaza Defao huku akijilazimisha kujiweka katika hali ya kutokuwa na wasiwasi.

    “Nani?.” Sauti ya kike kutoka ndani iliuliza.

    Mh!! Kamtuma mwanamke ndo aje kufungua au?

    “Mimi....mimi.” alijiumauma.

    “Nani?.”

    “Muhudumu.” Alijikuta akijibu hatimaye.

    Mlango ukafunguliwa taratibu. Ndani palikuwa giza.

    “Nini?.” Aliuliza mwanadada kutoka ndani. Alikuwa katika mavazi yake ya kulalia, laini kabisa kuweza kumtamanisha yeyote atakayepata fursa ya kumwona akiwa katika mwanga. Defao hakumwona katika mwanga.

    “Samahani dada..kuna mteja anadai kuna kitu chake anaweza kuwa aidha alikisahau humu ndani. Siku kadhaa nyuma. Samahani sana kwa usumbufu wowote utakaojitokeza.” Defao akiigiza kama muhudumu wa hoteli hiyo alijieleza.

    “Aaah! Usumbufu huo sasa. Kwanini msije wakati wa usafi asubuhi.” Alilalamika huyu mteja.

    Defao hakujibu kitu!!

    “Subiri kidogo.” Alisema yule dada huku akiufunga mlango. Baada ya dakika tano akaufungua tena. Alikuwa amejifunga kanga.

    “Ingia...”

    Defao akapiga hatua akaingia katika chumba hicho.

    “Ila nisamehe sana...” Alisihi defao huku akielekea kilipo kitanda.

    “Samahani nataka kuinua hili godoro unaweza kutoa hii..” Defao alimweleza kiaibuaibu huku akiinyooshea kidole ile chupi ambayo kwa kila hali ilikuwa mali ya yule dada.

    Mara wakatazamana!!! Defao akaruka pembeni!! Akaziba midomo yake.

    Yule binti akatulia kama aliyepigwa shoti. Alikuwa amekumbvana na kiumbe cha ajabu katika maisha yake. Kiumbe ambacho alikiri kabisa akilini mwake kuwa kam we hakutaka kukutana na kitu kama hicho. Mara ya mwisho kukiona alijikuta anapoteza fahamu. Sasa alikuwa anayerembua macho yake.

    Taratibu Joyce Keto akalegea na kuanguka chini. Bila kupata msaada wowote kutoka kwa Defao kwa jina halisi Gervas.

    Defao alibaki katika mshtuko huo kwa sekunde kadhaa. Alikuwa haamini kama mbele yake amesimama Joyce Keto na kisha amelegea na kuanguka chini.

    Akili ikamkaa sawa akamsogelea na kuanza kumpepea, kisha akawasha kiyoyozi, hali ikawa ya ubaridi na bado hakuacha kumpepea.

    Joyce aliyeangukia mgongo, akarejewa na fahamu zake nusu saa baadaye. Alikuwa chumbani na mwanamme aliyembaka miezi kadhaa iliyopita na sasa alikuwa mjamzito. Defao!!

    “Gervas!!!.” Aliita Joyce.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Joyce!!.” Alijibu Defao. Kisha wakakumbatiana. Zile chuki na hasira ambazo Joyce alikuwa amezitunza kwa miaka mingi ziliyeyukia kifuani mwa Defao.

    “Umejuaje nipo humu Gervas.” Joyce alimuuliza Defao.

    Defao akapiga kimya kwa sekunde kadhaa akatazama darini kama mchunguzi fulani huku akiwa ameibana midomo yake na kuyauma meno yake.

    Kisha akajieleza. Maelezo yote yalimshangaza Joy, sasa wakafikia maelezo kuhusu pesa. Hapo sasa wote wakatazama lile godoro. Halafu wakalivamia na kuliinua.

    Huku na huko!! MAAJABU Pesa ilikuwepo!!

    Kama alivyoiacha Defao mara ya mwisho.



    Defao alipagawa kumkuta Joyce akiwa bado ana mimba aliyompatia katika njia ya kumbaka. Hali hiyo ikamfanya kuisahau kabisa ile pesa waliyoikuta pale ndani.

    Joyce naye akasahau kisasi cha kubakwa. Wawili hawa wakawa kitu kimoja. Defao akahamishia makazi katika chumba cha Joyce. Kile kitoto ndani ya tumbo la Joyce kikaleta pendo jipya.

    Japo mimba ilipatikana kwa kitendo cha ubakaji lakini mimba ilibakia kuwa mimba.



    Jiji la Mwanza halikuwa na usalama wowote kwa wawili hawa. Baada ya kuwa wamesimuliana kila mmoja nini kimemsibu sasa waliamua kwa sauti moja kutoweka katika jiji hilo. Jiji lililobadilisha historia ya kila mmoja.

    Mpango ukasukwa usiku huohuo. Na kesho yake wakaongozana kuelekea stendi kukata tiketi.

    Nyegezi!!! ni huku waliweza kuonwa na Michael bila wao kujua.

    Michael akawa amemuona Joyce. Pagumu hapa!! Mpambano mpya.





    Jiji la Mwanza halikuwa na usalama wowote kwa wawili hawa. Baada ya kuwa wamesimuliana kila mmoja nini kimemsibu sasa waliamua kwa sauti moja kutoweka katika jiji hilo. Jiji lililobadilisha historia ya kila mmoja.

    Mpango ukasukwa usiku huohuo. Na kesho yake wakaongozana kuelekea stendi kukata tiketi.

    Nyegezi!!! ni huku waliweza kuonwa na Michael bila wao kujua.

    Michael akawa amemuona Matha.



    ****



    John Mapulu aliiendesha gari kwa kasi sana kama inavyokuwa wakati wa matukio ya uhalifu hasahasa wa kuiba magari ama kuiba kwa kutumia silaha. Kichwani na moyoni mwake alikiri kuwa alikuwa amekufa na kuoza kwa penzi la Matha. Na alihisi kiasi fulani umuhimu wa Joyce Keto ukipungua kadri anavyozidi kumweka Matha kichwani.

    Tayari alikuwa amewapa taarifa washirika wenzake. Arusha mjini alikuwa ameweka watu wawili maalum kukagua kila gari linaloingia kutokea jijini Mwanza. Naye alikuwa katika mwendo kasi kuwahi jijini Arusha, jina la Adrian lilikuwa likimtia kero kila alipofikiria. Kumuua Stallone haukuwa mwisho wa mapambano!!!



    Wakati Michael anajaribu kumpigia ili kumtaarifu juu ya alichokiona tayari alikuwa eneo lisilokuwa na mtandao.

    Michael akakata tamaa nakuhisi bahati ile huenda isijirudie tena.

    Maamuzi binafsi!!! Michael akaamua.



    Kwa jinsi yule mwanaume alivyokuwa amejiweka jirani sana na Joyce huku akiwa amemshika mkono Michael alisoma kitu fulani wa oyce.

    Hofu!! Joyce alikuwa katika hofu kuu. Michael akaamini kuwa hakuwa katika mikono salama.

    Nguo alizokuwa amevaa yule mwanaume waliyekuwanaye nazo zilimtia mashaka.

    Mtekaji!!! Alijiwekea hisia hizo kicwani mwake.

    Akachukua tahadhari katika kukabiliana na suala hili. Akawa makini Joyce asiweze kumuona. Kwani akimuona lazima atafanya tafrani ambazo zinaweza kuzua mengine ambayo hakutaka yatokee.

    Wawili wale wakaifikia taksi moja wakapanda. Michael ambaye alikuwa ameanza kuiva kimbinu na ye akasubiri sekunde kadhaa akachukua teksi nyingine.

    “Ifuate taksi hiyo inayokata kona.” Michael alimwamuru dereva. Akatii amri.

    “Hakikisha hajui kama tunamfuatilia.”

    Safari ikaanza!! Michael alikuwa makini kabisa, zaidi ya dereva aliyekuwa anaongoza chombo. Hakutaka kuipoteza hata kidogo ile taksi.



    Mwendo wa dakika kama kumi ile teksi aliyokuwa amepanda Joyce na Defao ilisimama katika geti la hoteli. Defao alikuwa wa kwanza kushuka, kisha akamfungulia Joyce mlango naye akashuka.

    Bado Joyce hakuonekana kuwa na amani. Jambo hili lilizidi kumuweka Michael ambaye muda tu naye alikuwa ameshuka katika taksi aliyokuja nayo. Michael kwa tahadhari zaidi alizidi kufuatilia nyendo za wawili hawa na sasa walichukua funguo kutoka mapokezi wakaanza kupanda ngazi kuelekea juu.

    Kosa lililofanywa na muhudumu wa pale mapokezi, kuinama lilikuwa faida kwa Michael ambaye alipenya kama upepo na sasa alikuwa katika korido akiwafuatilia wawili hawa.

    Chumba walichoingia Michael akakikariri vyema. Hakutaka kupoteza muda. Akatazama huku na huko kisha akaitoa bastola yake mafichoni. Na kama alivyofundishwa akaweka kiwambo cha kuzuia sauti. Sasa akakiendea kile chumba.

    Bunduki mkononi!! Tayari kwa lolote.

    Akaufikia mlango akaugonga? Kimya?

    Kwa mbali akasikia sauti za kunong;onezana. Kisha hatua kwa hatua hatimaye zikasikika hatua zikikoma.

    Kitasa kikashushwa mlango ukafunguka!!

    Michael alikuwa anasubiri kitendo hicho!! Akausukuma ule mlango kwa kutumia goti lake. Aliyekuwa anauzuia akapinduka na kusalimiana na ardhi. Michael bunduki mkononi. Akamuelekezea Defao. Kimya kikatanda. Joyce hakuwepo!!

    Kabla Michael hajaulizia mlango wa bafuni ulifunguliwa. Joyce Keto ana kwa ana na Michael.

    “Mai....Mai..Michael..” aliita akionyesha kutoamini anachokiona.

    “Huyu bwege ni nani na anataka nini kwako?.” Michael alimuuliza kabla ya kuitikia.

    “Ni..Defao....Defao...”

    ”Ni nani?.” Michael alizidi kuwaka akiwa bado amemuelekezea bastola Defao. Defao alikuwa amenyanyua mikono juu.

    Joyce alijielezea kwa kifupi huku akimtoa Defao hatiani. Michael akayaamini maneno ya Joyce. Mara watatu hawa wakawa kitu kimoja. Japo Michael aliweka tahadhari kubwa sana katika kila dakika. Hakutaka kumwamini Defao kwa asilimia zote.

    Na mara kwa mara alimvuta Joyce pembeni na kuzungumza naye mawili matatu. Swali kubwa kichwani mwa Michael ambalo hakutaka kuliuliza ni juu ya tumbo la Joyce. Lilimtia katika hofu na wivu.

    Nani amempa mimba? Hilo lilikuwa swali.

    Lakini haukuwa wakati muafaka wa kuliuliza.

    Jioni watatu hawa walizunguka mjini kidogo kwenda kupata chakula.

    Michael akiwa ameambatana na Joyce huku Defao akiwa amebaki nyuma kidogo. Joyce na Michael hawakujua nini kinaendelea. Hadi walipojikuta kwa pamoja wanageuka nyuma kutazama umbali waliomuacha Defao.

    Joyce hakuweka mashaka yoyote lakini Michael kwa sekunde kadhaa tu huku akitumia ubongo wa John Mapulu alimg’amua kuwa Defao alikuwa mikononi mwa polisi.

    Akamsihi Joyce wakakaza mwendo!! Wakakifikia kiuchochoro na kujibanza huku wakishuhudia tukio la Defao akifungwa pingu.

    John Mapulu ana akili sana huyu jamaa!! Michael alikiri kimoyomoyo baada ya mafunzo aliyopewa na John kufanya kazi yake ipasavyo!!!

    Wakatoweka na hawakurejea tena katika hoteli ile. Michael aliendelea kuutumia ubongo wa John Mapulu.



    ****



    Steven Marashi, alikuwa mpelelezi pekee aliyeamua kufanya kazi ya kujitolea nje ya malipo ya kiofisi. Alikuwa akiupenda sana upelelezi na ilikuwa furaha kubwa kwake akikabidhiwa kesi afanyie upelelezi.

    Suala la Defao kukamatwa kwa tuhuma za mauaji kisha kuachia katika namna dhaifu kulimshangaza sana kijana huyu, japo kwa hakika Defao alionekana kuwa hana uwezo wa kufanya mauaji na hapakuwa na alama za vidole vyake katika bunduki zilizokutwa eneo la tukio. Bado Steve hakuridhika. Akaamua kufanya upelelezi wa kimya kimya. Alizifuatilia nyendo za Defao hadi siku aliyorejea pale hotelini na kuulizia chumba namba kumi na nane. Alikuwa ni Steve pia katika harakati za defao kutafuta mahali pa kuiuza simu yake kisha akarejea katika hoteli ile tena.

    “Ana nini huyu bwana...anauza simu kisha anarejea kupanga katika hoteli ya bei juu kiasi hicho? Lazima kuna kitu.” Marashi alijisemea huku akiufurahia upelelezi huu wa kimya kimya ambao aliamini kuwa una manufaa ama una siri nyuma yake.

    Defao aliingia peke yake katika hoteli ile. Lakini siku ya pili anatoka na mtu mle ndani.

    Marashi akawahi kwenda kuuliza mapokezi. Muhudumu akataka kuleta ugumu kutoa siri za wateja. Akaonyeshwa kitambulisho cha kazi ya muulizaji. Akalainika akamtaja huyo dada kuwa alikuwa chumba namba kumi nane.

    “Je ni mara ya ngapi huyu mgeni kupanga katika hoteli yenu.”

    “Mara ya kwanza...aah!! labda kama alihudumiwa na mwenzangu siku nyingine..lakini mimi ni mara ya kwanza.”

    “Siku ya kwanza aliulizia chumba namba kumi na nane unakumbuka?”

    “Ndio nakumbuka.”

    “Sasa inakuwaje unasema ni mara yake ya kwanza kupanga katika hoteli yenu?” akakoroma Marashi, muhudumu akakosa cha kujibu huku uso wake ukitawaliwa na hatia ya kutotunza kumbukumbu vizuri.

    “Na je? Mmoja kati yao amewahi kupata ugeni wowote?” alihoji kwa utulivu akiwa amemkazia macho muhudumu.

    “Hapana afande.”

    “Mpuuzi sana wewe na mbona wametoka wakiwa watatau wakati chumba walipanga wawili?” muhudumu kimyaa!!



    “Ok! Anaitwa nani?” Marashi aliuliza

    “Yupi huyu wa kike au mwanaume?”

    “Wote!!”

    Muhudumu akajikita katika uchambuzi wa majina kwa dakika chache.

    “Juliana na Said Ndulla” aliyataja majina kwa utulivu.

    Mshenzi anabadili majina!!! Alishtuka Marashi.

    “Naomba kutembelea vyumba vyao. Utakuwa shahidi hii ni dharula kwa usalama wa wote.” Muhudumu hakupinga akamwongoza Marashi hai chumba namba 25, huku hapakuwa na lolote. Lakini chumba namba 18, kilipatikana kile kilichopoteza muda wa Marashi kufuatilia. Bunduki!!

    Hatia ikamuangukia Defao kuwa ndiye mmiliki na wale wenzake ni majambazi pia. Sasa hakuchukulia kama mchezo tena akaingia kazini rasmi. Akachukua kitambaa akaikamata vyema ile bastola na kuihifadhi katika kikoba chake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Usiwaambie lolote lile...na wakirejea nipe tarifa. Ole wako uvujishe siri!!” alichimba mkwara. Akaacha namba ya simu akatoweka. Muhudumu akabaki akiwa amekodoa macho. Hakuwahi kuiona bunduki hapo kabla



    Alipotoka nje wawili wale waliokuwa wanaongozana hawakuwepo tena. Marashi akaingia ndani ya gari yake na kujaribu kufuata machale yake yalivyomtuma.

    Matunda yakaonekana baada ya kuingia mjini. Hapa ndip alimuona Defao akiwa peke yake. Mnyonge kabisa.

    Marashi hakutaka kuichezea bahati hii. Akamfikia Defao na kumweka chini ya uliznzi. Marashi aliamini kuwa lazima kuna hatia inamkabili bwana huyu.



    Safari hii Defao alijikuta akibanwa na kumtaja Minja. Upelelezi ukahamia Singida Minja akapatikana. Alikamatwa akiwa katika maziko ya sajenti Kindo ambaye alikuwa ameaga dunia kutokana na ugonjwa uliokuwa ukimsumbua muda mrefu!!

    Minja na Defao wakawa hatiani. Hatia ya kuua kwa kutumia bunduki ambayo ilikamatwa katika chumba alichokuwa anaishi Joyce na Defao.

    Sheria ikachukua mkondo wake!!



    ****



    John aliwasili Arusha akitanguliwa na basi moja tu la abiria. Mwendo alioondoka nao ulikuwa mkali sana na gari ile aina ya Pajero ilihimili mikikimikiki ya barabarani.

    John hakutaka kufanya pumziko lolote lile. Aliyatembelea mawindo yake aliyoyatega mapema baada ya kuambiwa juu ya msichana anayeitwa Matha aliyesafiri kutoka Mwanza kwenda Arusha.



    “Mmefanikiwa kumwona?.” Aliuliza kwa utulivu bila kujibu salamu alizopewa na washirika wake hao.

    “Tumemchukua na tumemuweka katika hifadhi.”

    “Alikuwa na nani katika safari hiyo.”

    “Tumemchapa makofi kadhaa anasisitiza kuwa alikuwa peke yake.”

    “Ahaa!! Ok!! Sawa.” John alikubali huku kichwani akiwa na lake jambo.

    Machale yalimcheza. Akayaheshimu. Hakutaka kuandamana na washirika wake kwenda kumtazama huyo wanayedai ni Matha. Maana hata muonekano waliomuelezea haukufanana na Matha anayemfahamu yeye. Japo hakuwaambia moja kwa moja alizuga kuna mahali anaenda kwanza kisha atarejea.

    Akatumia mchezo huo, kuendelea kutega pale.

    Masaa mawili yakapita, bado haukata tamaa alikuwa makini kabisa kufuatilia magari yanayowasili kutokea mikoani.

    Baada ya masaa manne machale yake anayoyaheshimu yalimpatia majibu. Sasa aliweza kumwona. John Mapulu aliweza kumuona Matha. Na pia alimuona Adrian. Akajisifu kimyakimya kwa kuyaheshimu machale yake kwani sasa yalikuwa yamemwezesha kupata alichokikimbilia Arusha. Kumpata Matha.

    “Wale wajinga wangenipoteza hivihivi.” Aliwaza John, huku akifuatilia nyendo za Adrian na Matha.

    “Huyu bwege anamtorosha malikia wangu. Namuua kwa mikono yangu.” Alizungumza kwa ghadhabu. Sasa aliweza kuwashuhudia Matha na Adrian wakiingia ndani ya Teksi.

    Kama kawaida akawafungia tela.

    Uvumilivu ulimshinda John, wivu ukachukua nafasi kubwa. Safari ya kuwafungia tela ikaanza kumchosha na ni kama vile alikuwa anachezea shilingi katika tundu la choo. Muda wowote ule inaweza kudondoka. John akamtazama dereva wa teksi ambayo alikuwa amekodi akamwona yupo makini kufuatilia gari aliyoelekezwa aifuate. Taratibu akazama katika mkoba ,mdogo aliokuwa nao.

    Alipoibuka alizua hofu na taharuki kwa dereva.

    “Utafuata nitakachokueleza sawa!!” aliamuru John. Dereva akawa amekodoa jicho. Gari ikiwa imepunguza kasi yake.

    “Simamisha!!.’ Amri zikaanza. Mdomo wa bunduki ukiwa makini kusubiri amri ya kutema risasi iwapo itatakiwa.

    Dereva akashika breki za ghafla. John kidogo apoteze muhimili wake na laiti kama yule dereva naye angekuwa masshuhuri katika mbinu za kinyang’anyi basi angeweza kumtia John mikononi mwake. Lakini yule dereva hakuwa na mbinu zozote. Gari ikasimama.

    “Bila kuleta ujanja wowote fungua mlango wa gari. Hatua kwa hatua bila kugeuka nyuma utoweke eneo hili kimya kimya.” Alitoa maelekezo Johnkisha akaendelea, “Ukithubutu kuleta ujanja na kuifanya gari hii ina thamani kuliko uhai wako.....” hakumalizia!!!

    Yule dereva akiwa katika taharuki ya hali ya juu alifuata maelekezo. Aliposhuka kiutaratibu. John akarukia katika siti ya dereva akaitia gari moto ikatoweka dereva akabaki peke yake barabarani!!!

    John aliondoka kwa mwendo kasi mkubwa. Alikuwa na hasira. Baada ya dakika chache akaziona namba za gari ambayo ilikuwa imembeba Matha na John. Barabara nzima ilikuwa kimya. Magari yalipita kwa uchache sana. Muda ulikuwa umeenda.

    Ugeni wa John katika jiji la Arusha ukamtia wasiwasi iwapo ataendelea kuwafuatilia akina Matha kwa muda mrefu. Aliamini watafika mahali watamuacha. Akaamua kuongeza mwendo. Gari ile ikawa kama inapepea.

    Ndani ya sekunde chache akawasha taa za kuomba kupishwa njia aweze kuwa mbele. Dereva wa ile teksi akasalimu amri akakata kushoto akimwacha John ampite kulia kwake.

    Likatokea tendo la ghafla. Badala ya ile gari kupita na kuendelea na safari zake. Ilipita kisha ikapinda kushoto na kuwa imeziba barabara. Dereva wa teksi akatoa yowe la hofu. Adrian aliyekuwa amelala hakujua nini kinaendelea.

    Breki kali zikafungwa. Kabla hajamaliza kuhamaki katika dirisha lake ikapenya silaha ya moto. Aliyeishika akavua miwani yake. Macho yake yalikuwa yanatisha.

    Dereva akapoteza fahamu!!!



    Huyu alikuwa ni John Mapulu. Akaanza kutoa makaripio na maonyo kwa yeyote atakayethubutu kutingishika ndani ya gari. Kimya!!

    Akatoa simu yake akawasha tochi akamulika mle ndani. Siti ya nyuma alikuwepo mwanaume peke yake akiwa hajulikani kama amesinzia ama amezimia. Matha hakuwepo!!

    Shit!! Akatukana John!!

    Akausogelea mlango wa nyuma akaufungua. Akatuliza kitako cha bunduki katika mguu wa Adrian. Akazinduka kutoka usingizini. Akawa anashangaa shangaa. Akamulikwa machoni. Akayafunika macho yake. Mara akashtuliwa na mkono mzito shingoni. Akatoa yowe la uoga na maumivu.

    “Matha...Matha...” aliita. Akapokea teke lililotua tena katika shingo yake. Akangukia katika siti ya dirishani. Taa zikawaka ndani ya gari. Alikuwa amegusa kitufe cha kuwashia.

    Ana kwa ana na John mapulu, baada ya miaka kadhaa kupita sasa alimuona tena John. Mwanaume aliyempokonya tonge mdomoni enzi hizo!!!

    “John!!.” Aliita. Akakutana na jicho lililojaa chuki.

    Akatetereka. Huyu hakuwa yule John mpole wa kipindi hicho. Huyu alikuwa mwingine kabisa.

    “Nakupa dakika moja ya kujieleza ni wapi ulikuwa unampeleka Matha, ni wapi umemuacha!!.” John aliunguruma.

    “Mi sijui..ni yeye mimi...sijui hata ni wapi ..” hakueleweka Adrian, na asingeweza kueleweka.

    “Bado dakika yako haijaisha. Ikimalizika sitakupa sekunde chache za kusali sala yako ya mwisho.” John alizidi kutetemesha.

    Adrian akabaki kama zezeta. Asijue nini kinaendelea. Akajiuliza Matha yuko wapi hakupata jawabu.

    Sekunde zikazidi kukatika na dakika ikawa inakaribia kuchukua hatamu. John alikuwa hatanii.

    Ni hapa ndipo MPAMBANO uliokuwa unasubiriwa ukaibuka!!!

    Bastola ya John iliyokuwa inasubiri amri ya kumuondoa Adrian duniani ilipigwa teke ikaruka juu sana. Haikufyatuka!! Adrian alikuwa amefumba macho. Huenda alikuwa anasali ile sala ya mwisho. Jasho likimtiririka

    John akatoa yowe la mshtuko. Alipogeuka akakumbana na na mguu imara wa ukasalimiana na fuvu la kichwa chake katika namna ambayo ni nzuri kutazama lakini usiwe mtendwa wewe.

    Akapoteza muhimili mikono miwili ikamzuia asiweze kuisalimia ardhi.

    Akageuka tena sasa bunduki isiyokuwa na masihara ilitazamana na uso wake.

    Mikono ya mwanamama illikuwa imepakata silaha hiyo ya moto. Mikono hii ilionekana kujua vyema matumizi ya hii kitu.



    Sekunde kadhaa zilizopita alikuwa amejirusha kutoka garini baada ya kuchezwa machale na mabadiliko ya mwendokasi wa gari iliyokuwa nyuma yao. Adrian aliyekuwa amelala hakujua lolote na hata dereva aliyekuwa ametaharuki hakushtukia tukio hili. Sasa alikuwa amerejea tena kufanya ukombozi.

    “Matha!!.” Aliita John. Lakini huyu hakuwa Matha aliyemtambua. Huyu alikuwa mwingine kabisa. Hakutabasamu hata kidogo.

    “Ukipiga hatua mbele nasambaratisha ubongo wako.” Matha naye akaunguruma. Adrian hoi akiitazama filamu hii ya kutisha.

    “Matha unasema?” alifoka John. Matha naye akafoka kwa namna ya kipekee, namna ya kuachia risasi iliyochimba pembeni kidogo ya mguu wa John.

    “Uwiiii.” John akapiga kelele. Hakutegemea kitendo hicho kutoka kwa Matha.

    Sasa akaingiwa na uoga wa kupoteza uhai. Akatii amri akatulia tuli akiwa ameinyanyua mikono yake juu. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake anatishwa na mwanamke tofauti na mama yake aliyemzaa.

    “John. Uonevu wako umezidi. Nakuheshimu sana lakini kwa kuipigania roho hii isiyokuwa na HATIA naapa heshima na iishe. Au lasivyo yawepo makubaliano ya amani. Adrian abaki huru bila kusumbuliwa. Hilo ni moja. Na pili...”

    “Huwezi kunipangia amri Matha...” Aliingilia kati mazungumzo Adrian.

    Risasi nyingine ikafyatuka. Ikatua palepale ilipotua ya kwanza.

    “Nadhani unafahamu kuwa huwa sikosei nikiamua kulenga.” Alisema Matha. John akaelewa mwanamama huyu ana maanisha nini. Alimaanisha kuwa anamkosa maksudi. Akiamua anamuua ndani ya sekunde moja.

    John akawa mtulivu!!.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “John, umeninyanyasa vya kutosha, umefikia wakati mimi kama mwanamke nahitaji kuwa na mtoto. Nahitaji kuwa na familia yangu. Lakini umekuwa nami kipindi hicho chote hujanieleza kama una tatizo la kuzaa na kamwe huwezi kuzaa. Haukunitendea haki hata kidogo. Sasa nimejitambua na hauwezi kunipelekesha tena.

    John akajisikia aibu, siri yake i wazi sasa.

    Adrian alikuwa anasikia maneno baadhi na mengine hakuyasikia kutokana na hofu!!.

    “Chaguo ni lako John, aidha uiache dunia ama uniache huru nikiwa na Adrian. Mwanaume ambaye alipangwa kwa ajili yangu hapa duniani.” Matha alitupa mada mezani.

    John akaipokea kwa uchungu!!

    Hakujibu kitu.

    “John!!!” Alishtua Matha. John akashtuka kwa mara ya kwanza akakiri kuwa alikuwa amewezwa.

    Huyu demu ni kiboko yao. Alijisemea huku akitafuta mbinu za kujinasua.

    “Niue.” Alijibu John kwa jeuri.

    Alitegemea Matha angeshtuka. Haikuwa hivyo!!

    “Nakuua kweli.” Alimalizia Matha. Akaiweka sawa bastola yake.

    Mkojo ukaanza kumpenya shujaa huyu, kamanda wa makamanda. John Mapulu.

    Macho ya Matha na ya John yalipotea ghafla kuelekea kelele zilipotokea. Alikuwa ni John aliyewahi kutumia mwanya huu wa kumshangaa yule dereva aliyekuwa amezimia sasa akiwa amerejewa na fahamu. Hatua moja kubwa kisha bastola ikapigwa teke na kupotelea mbali.

    Kisha akajitupa kumkabili Matha kwa hasira zote. Pigo lake likawa batili likatua katika mikono ya Matha. Akayumba kidogo kisha akajiweka sawa akarusha teke la kuzunguka, chinichini likamzoa Matha akatua kama mzigo. Akatoa yowe la uchungu. Adrian akachomoka mbio mbio kwenda kumkabili John. Akakutana na teke kali katika mbavu zake akaanguka chini na kuanza kuugulia.

    John alitaka kujirusha mzimamzima ammalize Matha lakini akaingiliwa na pepo la huruma. Akasogea taratibu kwenda kumjulia hali Matha. Msichana aliyempenda kupita wote duniani.

    Kosa kubwa!!

    Matha aliviringika ghafla. Miguu yake ikatazamana na John aliyekuwa anakaribia kuinama.

    Teke likakifumua kinywa cha John akaiachia bunduki aliyokuwa ameiokota tayari. Pigo lililofuata liliadhibu korodani za John. Yowe la sasa likawa kubwa kuliko yote aliyowahi kupiga.

    Maumivu yalipokolea akajikuta tena anatazama na mdomo wa bunduki.

    Matha tena alikuwa anamkabili.

    “Sekunde kumi za mwisho...sekunde za kutoa maamuzi.” Matha alizungumza huku akitweta.

    “Matha...nisikilize tafadhali.” John alijishusha na kusihi.

    Mara akapiga hatua kumkabili Matha. Kwa mara nyingine Matha akamwonyesha John ujuzi wake katika kulenga shabaha.

    Ni jambo hili John alikuwa analisubiri.

    Akaruka pembeni baada ya ile risasi kufyatuliwa. Ghafla akatua na kumkaba Adrian.

    “Bora tukose wote.” Alizungumza John huku akiikaba shingo ya Adrian. Matha alivyofanya jaribio la kufyatua risasi. Hola!!



    ******



    Michael alitokomea na Joyce kwa namna ya kujifichaficha huku wakichukua tahadhari kubwa sana. Giza liliwasaidia kutoonekana kirahisi. Hatimaye wakaifikia nyumba ya kulala wageni tofauti na ile ya kwanza iliyokuwa na gharama kubwa sana. Hii ilikuwa ya kawaida.

    Wakalipia wakapewa umiliki wa chumba.

    Michael alikuwa mkimya kama vile ni mgeni sana mbele ya Joyce, Joyce naye alikuwa ametawaliwa na hofu!! Hakuna aliyemsemesha mwenzake kwa kitambo kifupi.

    Kila mmoja alikuwa anawaza lake!! Michael hakutaka kumuamini Joyce kwa asilimia zote. Joyce naye alihisi visa vya John Mapulu tayari vimeingia katika damu ya Michael. Huenda naye ni muuaji.



    Michael alizidi kuutazama usiku ulivyokuwa unaenda, akaamua kuuvunja ukimya.

    “Joyce....”

    “Bee.”

    “Hapa Mwanza sio pa kukaa tena ujue. Unayo akiba yoyote ya pesa!!.”

    “Ipo pesa ya yule Defao. Lakini mi sitaki kuondoka.”

    “Kwanini unataka kuishi hapa Mwanza.”

    “Kivipi tunaondoka bila kujua hatma ya Defao.” Alizungumza kwa sauti ya kujiuliza peke yake. Michael akashusha pumzi zake, akamtazama Joyce na kumchukulia kama mwanamke kama wanawake wengine!! Huruma huwatawala.

    Michael alifikiria kwa sekunde kadhaa huku Joyce akisubiri jawabu.

    “Joy!! Natoka kidogo. Ngoja nifuatilie walimpeleka wapi wale wajinga.”

    Joyce akatoa tabasamu kwa kuisikia kauli ile ya matumaini.

    Michael akapiga hatua kadhaa akaufungua mlango akatoweka akimwacha Joyce ndani.



    Baada ya dakika tano akarejea tena. Alikuwa ana chupa ya maji ya kunywa. Akamrushia Joyce bila kusema lolote.

    “Dah! Ulijuaje kuwa nina kiu? Asante sana.” Alishukuru Joyce lakini Michael hakuongezea neno.



    Michael alitoka pale chumbani na kujiweka nje ya chumba kwa takribani dakika kumi. Aliporejea tena yale maji yalikuwa yamefanya kile yalichoagizwa. Joyce alikuwa amesinzia bila kupenda.

    Michael akampekua joyce akakutana na kibunda cha pesa, akazitwaa zote. Akatoweka.

    Safari yake ikaishia hospitali.

    Akanunua ugonjwa wowote ambao ungemfaa Joyce. Daktari akaandika huku akiwa ameifadhi pesa za rushwa katika koti lake jeupe.

    Michael alipofanikisha kupata kibali hicho cha kuthibitisha kuwa Joyce ni mgonjwa asiyejiweza. Alirejea hotelini.

    Alikuwa na bomba la sindano na dawa katika kichupa kidogo, akamdunga Joyce.

    Hapa sasa akawa na uhakika kuwa Joyce hataweza kuamka kwa masaa mengi.

    “Defao ndo mdudu gani hadi aendelee kukuweka Mwanza?? Ukizinduka utajikuta upo Dar.,” Michael alizungumza na mwili usiosikia wa Joyce. Kisha akajiegesha naye akasinzia.

    Asubuhi sana teksi ikawachukua Michael na mgonjwa wake hadi Nyegezi kituo cha mabasi.

    Wawili hawa wakaianza safari ya kuelekea jijini Dar es salaam.



    *****

    John alitambua uwepo wa risasi moja tu katika bastola aliyokuwa nayo na kosa alilofanya Matha ni kufyatua pembeni yake baada ya kumhadaa kwa kumsogelea.

    Kile kitendo cha kujaribu kufyatua halafu risasi haikutoka. Kikabariki mikono ya John kuizungusha shingo ya Adrian kuelekea upande usiowezekana hata kwa mazoezi.

    Safari yake ikamalizika kimya kimya bila kelele.

    Sasa Matha akawa kama aliyechanganyikiwa. Akamrukia John kwa miguu yake miwili. Akafanikiwa kumchabaga mateke kifuani. Kabla hajainuka akamuwahi tena palepale katika korodani kwa staili ya kikondoo akamfikia. Sasa ilikuwa zamu ya mikono kufanya kazi. Mikono yote miwili ilimnyonganyonga. John akajaribu kumpiga Matha kwa kutumia viwiko vya mkono Matha akiwa anapiga kelele kubwa hakumwachia John. Cha ajabu gari zilizopita hazikuthubutu kusimama. Wimbi la ujambazi lililokuwa limetanda lilimtisha kila mtu.

    Sasa John akatulia hakupiga tena viwiko. Matha naye hakuendelea kunyonga. Wote wakasalia tulivu!! Walikuwa chini.

    Tofauti kati yao ilikuwa moja tu!! Matha alikuwa bado anapumua na John alikuwa maiti. Matha alikuja kusimama usiku wa manane. Eneo lilikuwa vilevile. Kasoro gari moja tu ndio haikuwepo. Dereva yule aliyezinduka alitoweka.

    Matha alipohakikisha Adrian tayari ameuwawa na John naye ametangulia kwenye haki. Alijikaza akaingia katika njia za waenda kwa miguu akatoweka eneo lile.

    Asubuhi alikuwa jijini Arusha!! Nafsini akiugulia maumivu ya kumpoteza Adrian, hatia ya kumuua John na kubwa zaidi kumpoteza Michael. Baba wa mimba yake.

    Inauma!!!



    *****



    Joyce na Michael baada ya kugombana na hatimaye kupatana wakiwa jijini Dar es salaam, Michael akiwa amefanya upelelezi wa kimya kimya na kutambua kuwa hapakuwa na lolote baya lililokuwa linawakabiri walikuwa wamejifunga katika maneno watakayozungumza wakishakutana na wazaz\i ama uongozi wa shule wote wakawa na majibu ya kutekwa na mtu asiyejulikana. Hawakuthubutu kutoa majibu ambayo yangeweza kuwaweka hatiani. Mzee Keto, baba mzazi wa Joyce alidanganyika kuwa hiyo ni miujiza ya mchungaji JK. Hivyo akazidi kujikita katika dhehebu hilo. Joyce baada ya kumaliza kumlilia marehemu mama yake naye alijiunga katika dhehebu ambalo familia yao ambayo aliikuta ikiwa na umasikini wa hali ya juu yote ikiamini huko.

    Michael ambaye alikuwa ametajwa kama baba wa mimba ya Joyce naye aliamua kujiunga katika dhehebu hilo kwa ajili tu!! Ya kumfurahisha Joyce na si vinginevyo.

    Maisha yakaendelea!!



    BAADA YA MIEZI 18



    Ilikuwa siku ya ubatizo wa mtoto wa Joyce ambaye baba halisi alikuwa ni Defao ambaye sasa alikuwa anasota rumande kwa kesi ya mauaji na pia kukutwa na bunduki iliyokuwa inamkabili. Lakini siri hiyo walibaki nayo Joyce na Michael pekee. Sasa Michael Msombe alihesabika kama baba halali.

    Mzee Keto alikuwa na furaha sana kwani alikuwa hana mjukuu mwingine zaidi ya huyo mtoto aliyeitwa Jackson. Pia furaha yake ilichangiwa na uwepo wa mwanaye Joyce aliyekuwa amepotea na kudhaniwa kuwa amekufa.

    Sasa mwanae alikuwa hai na chuo kilikuwa kimewaruhusu kuendelea kimasomo mwaka ambao unafuata. Hilo lilikuwa jambo jema.



    Ubatizo ulimalizika. Na kama ilivyo kawaida hakuna ibada bila cha kunogeshea. Sasa ulifika ule wakati wa ushuhuda.

    Mchungaji JK alimwaga porojo zake nyingi huku akishangiliwa na hatimaye akaanza kuwaita watu wenye shuhuda mbalimbali wazitoe ili kuzidi kuongeza imani kwa washirika.

    Kanisa lilipiga vigelegele mbinja na makofi kwa mchungaji huyu machachari. Shuhuda kuu ikatanguliwa na shuhuda ndogondogo kama za kupona upele, kupata kazi, kupata mchumba na nyinginezo.

    Sasa ikafuata shuhuda kuu. Hii huwasisimua watu na ni moja kati ya vipengele ambavyo huwavuta wengi kuhudhuria ibada.

    “Atajitambulisha mwenyewe kwa jina, na atawaeleza Mungu amemtendea nini.”

    Mchungaji alisema kwa utulivu wakati mwanamama huyu akipanda katika madhabahu. Wanawake kwa ushuhuda!!!

    Vigelegele vikapigwa!!

    Alikuwa amevaa mavazi yanayovaliwa na watu kutoka Naijeria, mavazi yaliukaa vyema mwili wake mnene. Na kichwani alijitanda kitambaa kilichofanana na vazi lake lile.

    Aliongozana na msichana aliyebeba mtoto. Makofi yaliendelea kutawala. Alipokabidhiwa kipaza sauti makofi yakapona.

    Mwanamama yule akatoa salamu!! Wapendwa wakaijibu. Akakariri vifungu kadhaa vya biblia. Akapigiwa makofi.

    Sasa akaanza kujieleza jinsi Mungu alivyomtendea maajabu.

    Michael Msombe alikuwa amesinzia katika namna ya kujifanya ameinama akifuatilia ushuhuda huo. Isingekuwa usumbufu wa Jackson kumfinyafinya huenda hata angekuwa katika ndoto murua. Ndoto itakayomtoa nje ya kanisa kabisa na kumrejesha katika anasa za dunia.

    “Naitwa Hilder Mrosso, ni mkazi wa Arusha, neno la Mungu pekee limelita jijini Dar Es salaam. Nimeolewa na nimebarikiwa kupata mtoto mmoja mimi na mume wangu. Safari yangu hadi kufikia kuokoka haikuwa fupi. Imekumbwa na vikwazo vingi hadi hapa namshukuru Mungu kwani yeye ni mwema. Mtoto wangu anaitwa Michael. Ni huyu amenisababisha nifike mbele yenu leo.” Kusikia jina la mtoto Michael akainuka. Wakatazamana na Joyce wakatabasamu.

    Michael akainama tena!!

    Mwanamke akaendelea kutoa ujshuhuda.

    “Nikiwa na mimba ya huyu Michael, niliweza kuuona muujiza wa Mungu na huo ndio ulikuwa mwanzo wa kuamini katika yeye. Nilitekwa na majambazi ambao hadi leo sijui nia yao, walinitesa walinipiga sana huku wakimuua dereva na rafiki yangu. Hawakusema kwanini wananitesa. Mungu ambaye wala sikuwa namwamini alinipa nguvu. Nikajikuta napambana nao huku tumbo langu likiwa kubwa kabisa. Mwisho nikawa mshindi lakini nilijikuta peke yangu porini. Sikuwa mwenyeji wa eneo hilo lakini maajabu yake Mungu. Niliokolewa na mtu nisiyemfahamu. Akanipa huduma zote alizoweza. Mwisho wa siku nikapona kabisa. Nikaahidi nikimzaa mwanangu lazima nimlete mbele ya Mungu. Mungu huyu ni yule Mungu wa mwanaume aliyeniokoa na kumwokoa mwanangu...:” Akasita akaanza kulia, kanisa likamuunga mkono wanawake wakawa wanalia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Michael naye akashangaa maneno yale yanamchoma akanyanyua uso akatazama mbele akatikisa kichwa kwa huzuni.

    “Mwanaume ambaye ni mume wangu sasa ndiye amenifanya nimtambue Mungu. Ni muumini mzuri wa hili kanisa na ni yeye amenifanya niwe hivi. Baba Michael..” aliita yule mwanamama.

    Akasimama mwanaume mtanashati akahesabu hatua akamfikia mkewe. Kanisa likapiga kelele za shangwe. Familia hii ikakumbatiana. Mchungaji JK akafanya ishara za kuwabariki.

    Picha zikapigwa!!



    *****

    Ibada ilipomalizika, Joyce akamsihi Michael waende kupiga picha na wajina mwenzake. Michael alileta ubishi lakini tabia ya Joyce ya kuwa king’ang’anizi ikamfanya aende japo kwa shingo upande.



    “Ona kalivyokufanana ...” Joyce alimtania Michael wakati amekabeba kale katoto. Michael akatabasamu.

    “Mama yake yupo wapi?” joyce aliuliza.

    “Huyoo anakuja.” Alijibiwa. Akageuka kumtazama.

    Michael naye akageuka. Mara macho yao yakagongana. Wote wakashangaana. Joyce alikuwa amejikita katika kukabeba kale katoto. Hakupata nafasi ya kuuona uso wa Michael ulivyoshangaa.

    Walikuwa wamekutana ana kwa ana na Matha ambaye amejitambulisha kama Hilder katika ushuhuda.

    Matha akakwepesha macho. Kisha akaingiza mkono katika mkoba akatoa kijikaratasi. Alipomkaribia Michael akampatia kisirisiri. Hakuna aliyewaona.

    Michael akauelewa mchezo. Akakipokea akakihifadhi kisha akamchukua Joyce wakaondoka.

    Njia nzima Michael alikuwa tofauti kabisa. Laiti kama asingesingizia kuumwa basi hakuna ambaye angeweza kumwelewa.

    Alipoachana na Joyce na mtoto wake alijaribu kupiga zile namba lakini simu iliita haikupokelewa. Akahisi labda Matha bado yupo kanisani. Akairuhusu subira ivute heri.

    Usiku akampigia Matha kwa namba ileile. Sasa iliweza kupokelewa.

    Alikuwa ni Matha.

    “Michael siamini kama tumeonana tena.”

    “Yaani mimi ndio sijielewi kabisa.” Maongezi yakaendelea.

    Sasa Matha alimweleza Michael juu ya motto kuwa ile ilikuwa damu yake. Michael alipigwa na butwaa. Ilikuwa taarifa njema sana.

    “Nitakutafuta Michael tuzungumze kwa kirefu. Acha nilale kwa sasa. Yapo mengi sana ya kuzungumza mimi na wewe.” Alimaliza mazungumzo Matha. Simu ikakatwa licha ya Michael kutaka kuzungumza zaidi.

    Usiku ukawatwaa!! Kila mmoja na fikra zake.



    ****

    Matha ndiye aliyevurugwa sana na hali hii y kukutana na Michael tena. Alijikuta katika hali ngumu. Ni kweli alikuwa ameolewa lakini kitu kibaya alikuwa amemweleza mumewe kuwa baba wa huyo mtoto alikufa katika ajali. Sasa Michael ameonekana.

    Huruma ya Matha kwa mtoto wake na roho yake ambayo kidogo ilikuwa imeanza kutakasika vikaisumbua nafsi yake.

    Hakutaka kutangatanga tena. Hakutaka mtoto wake ateseke.

    Moyoni akakiri kuwa alimpenda mtoto wake kuliko huyo Michael Msombe ambaye ni baba yake.

    Asubuhi ilipofika akachukua maamuzi magumu!! Akabadilisha namba za simu kwa kumdanganya mumewe kwa maneno kadha wa kadha.



    Japo ilimuuma lakini alikuwa ameamua kujiweka mbali na Michael kwa usalama wa ndoa yake. Aliamini ipo siku atakuja kukutana na Michael na atadaiwa mtoto lakini hakutaka siku hiyo iwe mapema kiasi hicho.

    Ikabaki kazi ya Michael kuwa anapiga simu isiyopatikana kila siku. Matha na mumewe walikuwa wamerejea jijini Arusha tayari.



    *****



    Hali ilivyoendelea kuwa hivyo kila siku hatimaye Michael akazoea utumwa huu wa kulea damu isiyokuwa ya kwake. Kilichomuuma zaidi ni kuwa alipata nafasi ya kupiga picha na mwanae wa kumzaa. Hiyo picha ikabaki kumuumiza kila alipoitazama. Maskini Joyce hakujua lolote.

    “Ipo siku nitairejesha damu yangu. Kwa GHARAMA YOYOTE.” Aliapa Michael.





    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog