Search This Blog

Sunday 19 June 2022

MUUAJI ALIYEBAKIA - 3

 





    Simulizi : Muuaji Aliyebakia

    Sehemu Ya Tatu (3)



    Siku mbili baadaye walipokea vielelezo zaidi vilivyomuhusu James na mkewe na mwishoni uchunguzi ulibainisha kuwa watu waliouawa walikuwa ni wenyewe.

    Taarifa hizo zilitumwa kwa jeshi la polisi nchini Tanzania juu ya James na mkewe waliopatika wakiwa wameuawa. Jeshi la polisi lilitoa taarifa kwa kampuni ya JAJHO juu ya kupatikana kwa mwili wa James na mkewe na liliwahitaji wahusike na taratibu zote za mazishi.

    Jackson alitoa taarifa kwa wazazi wa mke wa James akiwaeleza juu ya kupatikana kwa maiti ya mwanao lakini hakufanya hivyo katika familia ya James ambayo alielewa ilijua juu ya kila kitu kilichoendelea. Kitendo cha ndugu zake hao kuondoka bila kuaga katika nyumba ya James aliamini kilitokana na kugundua kwao ugomvi uliokuwapo baina ya familia zao mbili za marehemu mzee Kibudo na Samola ambaye alikuwa baba yake. Aliondoka na wamiliki wenzie wa kampuni sambamba na ndugu kadhaa wa mkewe James kwa usafiri wa ndege wakielekea jijini Nairobi. Lengo lake alihitaji ahakikishe James na mkewe wanazikwa nchini Kenya, japo kulikuwa na maswali mengi juu ya vifo hivyo lakini aliamini hakuna mtu ambaye angeliweza kutegua kitendawili cha vifo hivyo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mara zote alionyesha huzuni juu ya tukio hilo lakini moyoni alikuwa na furaha kupindukia, alikuwa amefanikiwa kuwafukuza watu waliokuwapo nyumbani kwa James akiwamo mtoto wake. Alifanya hivyo akijifanya anaiuza nyumba hiyo kwani aliamini hakuna ndugu ambaye angethubutu kuifuatilia. Hilo lilijidhihirisha wazi kwani hata vyombo vya habari vilitangaza juu ya kupatikana mwili wa James na mkewe lakini hofu ya ndugu zake iliwafanya asijitokeze hata mmoja. Hatimaye walifika nchini Kenya na mara baada ya kuishuhudia miili ya James na mkewe walipewa kibali cha kuizika. Amos ambaye alikuwa miongoni mwa wamiliki ya kampuni yao alijifanya akitoa wazo la kuizika miili hiyo nchini humo. Alitoa mtazamo wake juu ya mazishi ya watu hao ambayo yalipaswa kufanyika katika kijiji cha James lakini hakuna ndugu yeyote aliyefika kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo.

    Hilo lilikuwa ni wazo lao toka awali na hawakutaka kurudi na miili hiyo nchini Tanzania wakihofia maswali mengi na zaidi uchunguzi ambao ungejitokeza. Waliwaeleza ndugu zake na mkewe James kuwa kampuni yao ilikuwa na matatizo ya kifedha wakati huo hivyo kupunguza gharama katika miili hiyo iliyokuwa ikizidi kuharibika waliomba waizike hapohapo nchini Kenya. Jambo hilo lilikubalika ingawaje kwa shingo upande na miili hiyo ilizikwa katika eneo walilopewa kibali cha kuzika. Jeshi la polisi lilidai kuwa liliendelea na uchunguzi juu ya watu waliokuwa wakihusika na mauaji hayo kwa namna moja au nyingine. Jackson na wenzie hawakuwa na hofu na walisisitiza kuwa walihitaji jeshi la polisi lifanye kazi yake kadri liwezavyo ili watuhumiwa wakamatwe. Walieleza hayo kwa vile walielewa hakuna mtu mabaye angeweza kutambua tukio zima la mauaji ya James na mkewe.

    Baada ya siku tano safari ya kurudi Tanzania kwa usafiri wa ndege iliandaliwa na siku iliyofuata walitakiwa kuwa safarini wakirudi. Jackson na wenzie waliona huo ulikuwa muda muafaka wa kumwachia kazi mr. Tyoso ambaye walishirikiana kufanikisha mauaji ya James na mkewe ili afuatilie zoezi la upelelezi huo. Walifanya hivyo katika hali ya kujihami lakini aslimia zote walizokuwa nazo waliamini hakuna mtu aliyeshuhudia mauaji hayo. Baada ya makubaliano hayo hatimaye siku iliyofuata walianza safari wakirudi Tanzania wakiamini hakuna jambo lolote ambalo lingeweza kujitokeza. Mr. Tyoso aliipokea kazi aliyopewa na wateja wake na kuwahakikishia kuwa siri hiyo isingeweza kuvuja.

    Kwa vile mtandao wake wa ujambazi ulikuwa mkubwa na alikuwa akishirikiana na askari kwa kiasi kikubwa aliamua kuongea na askari kadhaa ili wafuatilie kwa karibu kila kilichoendelea katika upelelezi huo. Kila siku nyakati za jioni alikuwa akiwapigia simu askari aliyokuwa amewaachia kazi hiyo na kuwauliza jambo lililokuwa likiendelea na hakupata taarifa yeyote iliyotoa hofu ya kuvuja kwa siri hiyo.Baada ya siku chache wakati upelelezi huo ukiendelea alisikia simu yake ikiita na aligundua mtu aliyepiga alikuwa ni askari aliyempa jukumu la kufuatilia kwa karibu upelelezi wa mauaji ulioendelea. Wakati huo ilikuwa yapata saa tano na nusu usiku “haloo mr. Tyoso kuna jambo limejitokeza mkubwa” alisikika askari huyo mara baada ya simu yake kupokelewa “jambo gani hilo?” aliuliza Tyoso kwa mshtuko

    “kuna mtu anadai ana filamu ya mauaji ya James na mkewe na ataileta kituo cha polisi kesho”. Baada ya kusikia hayo Tyoso alishtuka zaidi akiwa haamini juu ya jambo hilo aliloelezwa, alimwomba askari huyo afuatilie nyendo za mtu huyo haraka na zaidi alihitaji jina na namba yake ya simu.

    Alipatwa na mawazo ghafla na hakutaka kuwaeleza wateja wake juu ya jambo hilo lililokuwa linaendelea aliamini hakuna kitu ambacho kingeweza kufanikiwa. Aliwaza kuhakikisha filamu hiyo haifiki kituo cha polisi na zaidi mtu aliyekuwa na filamu hiyo alihitaji auawe kwa vile alikuwa na uwezo wa kuitoa siri hiyo muda wowote. Dakika kumi baadaye ujumbe mfupi wa maneno uliingia katika simu yake na mara baada ya kuusoma aligundua ulitoka kwa askari ambaye alikuwa amempigia simu. Alikuwa amemtumia namba ya simu na jina la mtu huyo aliyedai kuwa alikuwa na filamu ya mauaji aliyeitwa George Johnson.

    Bila kupoteza muda Tyoso alichukua simu yake na kumpigia mtu huyo akimweleza kuwa alikuwa askari wa upelelezi aliyehusika na uchunguzi wa mauaji ya James na mkewe. Alimweleza aliihitaji filamu hiyo ya mauaji usiku huo kwani ilikuwa ni muhimu sana kutokana na maagizo waliyopewa na mkuu wa upelelezi. Walielewana vizuri na baada ya Tyoso kuelekezwa eneo ambalo George alishi alianza kijiandaa kwa ajili ya kumfuata. Jambo kubwa alilolihitaji kwa mtu huyo ni uhai wake na kikubwa zaidi ni filamu aliyoelezwa ilikuwa na mauaji ya James na mkewe. Aliiandaa bunduki yake na kuweka risasi za kutosha akiamini jambo lilofuata lilikuwa ni mauaji, aliiweka katika koti lake kubwa alilovaa na kufanya mtu asiweze kugundua kirahisi kuwa alikuwa amebeba bunduki. Alivaa miwani yake iliyopoteza mwonekano wake wa sura na alipanda pikipiki yake na kuanza safari kuelekea eneo alilokuwa ameelekezwa.

    George alikuwa amepata taarifa zilizohusiana na kuokotwa kwa miili ya watu wawili waliokuwa wameuawa ambao aliamini taarifa zao alikuwa nazo kupitia filamu ya dakika ishirini na tano aliyofanikiwa kuipata katika mauaji hayo. Jambo lililomuogopesha ni ushauri ambao awali alipewa na mjomba yake kuwa asitoe siri kama hiyo akidai lazima angefanyiwa jambo baya. Baada ya kufikiria kwa siku kadhaa aliamua kufikia uamuzi wa kutoa siri hiyo, kufanikisha hilo siku moja majira ya saa nne usiku alipiga simu kituo cha polisi na kueleza juu ya filamu ya mauaji aliyokuwa nayo. Alielezwa aipeleke siku iliyofuta na masaa kadhaa baadaye aligiwa tena simu akielezwa filamu hiyo ingefuatwa usiku huo na mtu aliyekuwa askati wa upelelezi. Hakuwa na pingamizi juu ya jambo hilo alikuwa akimsubiri mpelelezi huyo aifuate filamu hiyo ya mauaji aliyoyashuhudia.

    Nusu saa baadaye mlango wa geti la nyumba yake aliyoishi peke yake uligongwa ilikuwa nyumba ambayo hata shughuli za uandaaji wa filamu alizifanyia humo mara baada kupiga picha sehemu tofauti. George alisimama na kuanza kutembea taratibu akielekea getini akiwa na imani kuwa mgeni aliyekuwa amegonga geti lake alikuwa askari mpelelezi. Mara baada ya kufungua geti mtu huyo aliingia akiwa na pikipiki yake na kuiegesha mbele ya nyumba hiyo ya George.

    “samahani kwa muonekano wangu, kazi hii inatuhitaji tuwe makini sana”aliongea mpelelezi huyo kama alivyo jitambulisha awali kwenye simu. “usijali karibu….” Ajibu George ambaye kwa kiasi alianza kuonyesha hofu na mgeni wake huyo. Mara baada ya kuingua ndani walianza kuongea mambo tofauti mbali na lile kubwa lililohusu filamu ya mauaji. Wakati huo mgeni wake alikuwa amevaa miwani ambayo haiku mwonyesha vizuri sura yake, baada ya dakika kadhaa mtu huyo alitoa miwani yake na sura yake ndiyo ilimuongeza hofu zaidi na kuanza kuingiwa na mawazo kuwa hakuwa askari. Alimfananisha na mtu mmoja ambaye alikuwapo kwenye tukio la mauaji ambayo aliyashuhudia kwa macho yake. Jambo hilo ndilo lilimfanya amuulize swali huku akiwa na uoga. “samahani askari kabla ya yote, naweza kukiona kitambulisho chako cha kazi?” aliuliza George ambaye hakujiamini.



    “Samahani askari kabla ya yote, naweza kukiona kitambulisho chako cha kazi?” aliuliza George ambaye hakujiamini.

    Mtu huyo alisimama na kuelekeza mkono wake kwenye koti lake kubwa alilokuwa amevaa alitoa bunduki na kuielekeza kwenye paji lake la uso wa George ambaye alichanganyikiwa ghafla. “hiki ndiyo kitambulisho changu, sasa mimi siyo askari sihitaji chochote toka kwako zaidi ya kila kitu kinachohusiana na mauaji uliyoyashuhudia” alisikika mtu huyo akiwa ametoa macho. Kwa uoga George alianza kutembea mpaka kwenye chumba alichokuwa akiandalia filamu hizo na alikuwa akifuatwa nyuma na mtu huyo. Mara baada ya kuingia kwenye chumba hicho aliitoa filamu iliyokuwa na mauaji aliyoyashuhudia na kuikabidhi ikiwa imeandikwa juu yake ‘MAUAJI’. “bado sehemu gani nyingine kuna picha za hii filamu” alisikika mtu huyo kwa ukali na kumfanya George ampe kamera yake aliyokuwa akipigia picha akidai picha hizo hazikufutwa kwenye hiyo kamera.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mara baada ya kuchukua vitu hivyo alimumiminia risasi tatu George tumbomi na kumfanya aangue huku damu nyingi ikimtoka. Mtu huyo aliye jitambulisha kama mpelelezi ambaye hakuwa mwingine bali ni mr. Tyoso aliichukua kamera na filamu hiyo na kuviweka katika boksi moja lililokuwa na filamu nyingine. Mawazo yake yalimtuma akiamini kuwa filamu hiyo ilikuwa imehifadiwa sehemu nyingi hivyo ingekuwa ni rahisi kupatikana tena. Alizipiga risasi kompyuta tatu zote zilizokuwapo katika chumba hicho akiamini zilitunza filamu hiyo. Wakati akifanya hayo yote George alikuwa akitupatupa mikono na miguu baada ya kupigwa risasi, tayari damu nyingi ilikuwa imemtoka.

    Mr. Tyoso aliondoka kwa kasi eneo hilo la nyumba ya George akiwa na boksi alilobebea filamu zote alizoziona katika kile chumba pamoja na kamera. Aliendesha pikipiki yake akiamini alikuwa amefanikisha ushindi wa siri hiyo iliyokuwa inataka kuvuja. Jambo ambalo bado lilikuwa linamuumiza kichwa ni kuhusiana na filamu hiyo alihisi ilikuwa haihusiani na mauaji waliyokuwa wameyafanya. Kumbukumbu zake zilimpa aslimia chache na filamu hiyo jambo alilokuwa akilisubiria kwa hamu lilikuwa ni kuiona filamu hiyo kama ni kweli ilikuwa ikihusiana na mauaji waliyokuwa wameyafanya na wateja wake.

    Saa nane kamili usiku aliwasili nyumbani kwake na kabla ya yote alianza kuiangalia filamu hiyo, baada ya dakika tatu tu za kuiangalia alisikika akiongea peke yake “Mungu wangu alituonaje mbwa huyu” . Alishangazwa na filamu hiyo ambayo aligundua ilionyesha kila kitu walichofanya siku ya mauaji. Haraka aliamua kuanza kuangalia filamu nyingine ambazo nazo alikuwa amezichukua, alishuhudia sherehe za harusi na nyingine ikiwamo misiba na filamu moja ilikuwa ikionyesha vyura wa aina tofauti. Baada ya muda mfupi wa kuziangalia kwa haraka pasipo kumalizia aliigeukia kamera ambayo aliweza kukutana na picha nyingine za mauaji alizokuwa amezishuhudia.

    Aliichukua filamu hiyo pamoja na kamera kisha akavichoma usiku huohuo, hakutaka kubakia na kumbukumbu za mauaji hayo ambayo na yeye alihusika akihofia usalama wake na wateja aliowafanyia kazi hizo. Filamu nyingine aliziacha kwani aliona zilikuwa hazina jambo lolote la hatari kwa usalama wao mara baada ya zoezi hilo alichukua simu na kumpigia Jackson. Ilikuwa yapata saa tisa usiku lakini aliona umuhimu wa mteja wake huyo kujua jambo ambalo lilitaka kuwatokea. Alipongezwa sana kwa kazi hiyo aliyokuwa ameifanya zaidi Jackson alishtushwa na taarifa hizo za kuwa kulikuwa na mtu aliyewafuatilia siku ya tukio la mauaji waliokuwa wameyafanya. Alimuahidi Tyoso kumtumia fedha siku iliyofuata kama pongezi juu ya zoezi hilo alilokuwa amelifanya.

    * * * *

    Mzee Rogart alikuwa miongoni mwa raia masikini walioishi nchini Guyana, alikuwa mkazi a jimbo la New Amsterdam aliyefanya shughuli kuu ya uwindaji pembezoni mwa mlima ambao kulitokea ajali ya ndege. Katika maisha yake mzee Rogart alikuwa na mke na watoto wawili ambao walikuwa wamemkimbia miaka kadhaa iliyokuwa imepita, walimwacha porini huko kutokana na ugumu wa maisha ambayo hawakuyaweza. Mzee Rogart alikuwa wa kwanza kufika katika eneo la ajali hiyo ya ndege na kushuhudia ajali hiyo, jambo alilolifanya siku hiyo ya tukio alimckukua mtoto mmoja aliyekuwa amejeruhiwa vibaya kutokana na ajali hiyo na alimpeleka mpaka nyumbani kwake akiwa na lengo haswa la kumtibu na hatimaye aanze kuishi naye.

    Aliamini hilo lingewezekana kutokana na vifo vya watu wengi vilivyokuwa vimetokea eneo la tukio na aliamini mtoto huyo naye angedhaniwa alifariki. Alikuwa akihitaji kuwa na mtoto kwa vile mkewe na watoto wake wawili waliokuwa wamemtoroka, walimpa imani iliyomkaa kichwani kuwa hawangerudi tena. Alianza kumtibu mtoto huyo kwa majani ya porini ambayo aliyatambua kama dawa kutokana na maisha ya miaka mingi aliyokuwa akiishi porini huko. Wakati akifanya hayo kila siku alikuwa akienda eneo ambalo ajali ya ndege hiyo ilitokea na kujumuika na askari waliotafuta miili ya watu waliokuwa wamefariki. Hatimaye zoezi lao lilikamilika pasipo kugundulika kuwa alimwiba mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo. Alikuwa akiishi umbali wa kilometa zaidi ya saba toka eneo ambalo ajali ilitokea, muda wote alikuwapo nyumbani kwake akisubiri kwa hamu mtoto aliyekuwa amemwokota arudiwe na fahamu.

    Alikuwa amevunjika mkono na mguu akiwa amepatiwa matibabu ya kufungwa vizuri na miti midogo midogo iliyoenda sambamba na maeneo aliyokuwa amevunjika. Mtoto huyo pia alikuwa na majeraha mengi sehemu tofauti za mwili wake, suala lililomuumiza kichwa mzee Rogart lilihusiana na kuchelewa kuzinduka kwa mtoto huyo aliyekuwa na shauku ya kumfahamu. Alipunguza kasi yake ya uwindaji na muda mwingi alikuwapo nyumbani kwake hapo akihakisha mtoto huyo anakuwa salama. Hakufanikiwa kupata vielelezo vyovyote vilivyohusiana na mtoto huyo zaidi ya picha akiwa na wazazi wake ambazo alizipata kwenye begi pembeni kidogo ya eneo ambalo alimchukua. Baada ya siku nne tangu kuchukuliwa kwa mtoto huyo toka eneo la ajali hatimaye alizinduka akiwa anashangaa eneo alilokuwapo na mtu aliyekuwa na ndevu na nywele nyingi zenye mvi. Kilichomshangaza zaidi ni eneo hilo la porini ambapo pia nyumba aliyokuwapo ilijegwa kwa miti na kuezekwa kwa majani. Hakuna jambo ambalo walielewana na mzee Rogart aliyezungumza lugha ya Hindu zaidi waliweza kutambuana majina.

    Rogart alifurahishwa na kuzinduka kwa mtoto huyo aliyebaini alikuwa raia wa Tanzania ambaye pia aliitwa Geofrey, aliendeleza matibabu yote aliyokuwa akiyafanya kwa mtoto huyo na hatimaye alipona baada ya miezi mitatu. Tayari alianza kuifahamu lugha ya Hindu aliyokuwa akiitumia, mara kadhaa Geofrey alionyesha nia ya kutaka kurudi Tanzania ila alipoelezwa nchi ambayo walikuwapo alikatishwa tamaa kabisa. Hiyo ilitokana na imani aliyokuwa nayo kuwa ingekuwa vigumu kwake kuondoka eneo hilo na kumfanya aanze kujifariji kuwa hayo yalikuwa makazi yake mapya. Suala la shule lilikuwa limepotea kabisa kichwani mwake, ingawaje hakuwahi kutembea na kukutana na watu wengi zaidi ya wawindaji wachache waliokuwa wakikutana mara kadhaa porini. Chakula chao kikubwa ilikuwa nyama na wakati huo alikuwa mwindaji mzuri akishirikiana na mzee Rogart ambaye alimpenda sana. Hakuthubutu kuisahau familia yake na alikuwa akizitizama picha za familia yake hiyo kila siku akiwa anaamini miujiza pekee ndiyo iliweza kumkutanisha tena na familia yake.

    Baada ya miaka mitano akiwa tayari na miaka kumi na tano alikuwa amepata mambo tofauti kutoka kwa mzee Rogart aliyekuwa na historia iliyojaa mikasa. Moja ya mambo aliyoyatambua toka kwa mzee huyo ambaye miaka ya nyuma alikuwa jambazi wa kutisha lilihusiana na mauajia aliyowahi kuyafanya dhidi ya mke wa rais wa nchi hiyo ya Guyana. Alimweleza miaka kumi na tano iliyokuwa imepita mzee Rogart akiwa jambazi wa kutisha nchini humo alipewa jukumu na chama cha upinzani cha nchi hiyo cha DPG ‘Democratic Part of Guyana’ la kumuuwa rais wa nchi hiyo aliyeitwa Zakheem Pirjah.

    Alikubaliana na kazi hiyo baada ya kupewa fedha za kutosha na siku ya tukio alisababisha ajali iliyomuua mke wa rais. Msako mkali ulifanywa wa kutafutwa kwake na rais huyo ambaye mpaka wakati huo alikuwapo madarakani akitumia ubabe. Alidai wakati huo alikuwa na umri wa miaka arobaini na tano, hivyo baada ya kuona mambo yalikuwa magumu aliamua kukimbilia porini hapo akiwa na familia yake. Aliacha mazoea aliyokuwa nayo ya kunyoa nywele na muda wote alikuwa na nywele ndefu zilizopoteza mwonekano wa sura yake.



    Aliacha mazoea aliyokuwa nayo ya kunyoa nywele na muda wote alikuwa na nywele ndefu zilizopoteza mwonekano wa sura yake.

    Aliishi na familia yake kwa muda mfupi porini hapo wakiwa hawajui mauaji hayo aliyoyafanya kwa mke wa rais zaidi ya vile walivyomtambua kuwa alikuwa jambazi. Baada ya kuona maisha ya porini yalikuwa magumu mkewe na watoto wake waliamua kuondoka na hawakuwahi kurudi tena porini hapo. Geofrey alishtushwa na historia hiyo ambayo mwishoe aliichukulia kama kitu cha kawaida kutokana na heshima aliyokuwa ameijenga kwa mzee Rogart akimchukulia kama mzazi wake. Muda wote wakiwa porini hapo katika shughuli za uwindaji walikuwa wakitembea na bunduki ambayo waliitumia siyo katika uwindaji tu bali ilitumika kama tahadhari ya usalama wa mzee Rogart aliyeamini rais wa nchi hiyo Zakheem alikuwa akimtafuta. Mara kadhaa pia walikuwa wakikumbana na wanyama wakali kama Simba hivyo waliitumia kujiokoa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Walikuwa wakipata risasi kwa kununua kwa wawindaji wengine ambao walikuwa hawaishi porini huko na hivyo ndivyo walivyoendeleza maisha yao. Siku moja Geofrey aliondoka peke yake akimwacha mzee Rogart aliyekuwa na homa nyumbani hapo. Alikuwa akifuatilia mitego waliyokuwa wameitega dhidi ya swala na wanyama wengine hususani nguruwe pori ambao haswa walikuwa nyama yao kubwa wakiwa porini hapo. Akiwa ametembea umbali wa kilometa kadhaa toka nyumbani kwao alishtushwa na askari waliokuwapo eneo hilo ambao mara baada ya kumwona walianza kumfuata.

    Alikuwa amevaa bukta pekee na kuacha eneo la juu kuwa wazi zaidi alikuwa hajavaa hata viatu, begani alikuwa na upinde sambamba na mishale mingi aliyoishika katika mfuko mdogo aliokuwa nao.

    Alitaka kukimbia lakini alijipa ujasili, mawazoni alihisi watu hao walitaka kuwakamata kutokana na uwindaji waliokuwa wakiufanya. Askari hao walianza kumshangaa kwa jinsi alivyokuwa amevaa lakini yeye kwake lilikuwa jambo la kawaida kwa miaka yote aliyokuwapo porini hapo. Mara baada ya kumfikia walimsalimia kwa lugha ya Hindu na hatimaye walitoa picha wakiashiria kuwa walitaka kumwuliza jambo. Mara baada ya kumwonesha picha hiyo ambayo aligundua ilikuwa ya mzee Rogart moyo wake ulishtuka ingawaje hakuonyesha hali yeyote ya mshtuko. Walimuuliza kama alimfahamu mtu huyo au yeyote aliyefanana naye lakini aliwajibu alikuwa hamfahamu na hakuwahi kukutana naye porini hapo.

    Picha hiyo ilionekana ilichukuliwa miaka mingi wakati mzee Rogart akiwa hana nywele nyingi kama alizokuwa nazo wakati huo. Baada ya majibu hayo polisi hao waliokuwa sita waliendelea na msako wao dhidi ya mtu huyo, Geofrey aliamua kuacha zoezi lake la kufuata mitego waliyokwa wameitega na kuanza kurudi nyumbani. Mara baada ya kufika katika nyumba waliokuwa wakiishi alishtusha na moto mkubwa uliokuwa ukiwaka ukiwa umeshia nyumba yao. Pembeni kulikuwa na madumu ya mafuta aina ya petroli ambayo yalionekana kuteketeza nyumba hiyo. Alizunguka maeneo yote ya sehemu hiyo waliokuwa wakiishi akiwa naimani huenda mzee Rogart alikuwa ameuawa lakini hakubahatika kuiona maiti yeyote.

    Hisia za kuwapo kwa kundi kubwa la polisi msituni hapo zilimwingia na kuamini kuwa mzee Rogart alikuwa amekamatwa. Aliongeza mishale mingine na wakati huu aliamua kuchukuwa dawa ambayo walikuwa wakiipaka katika ncha ya mishale ambayo ilikuwa ikiwafanya wanyama wapate usingizi pindi wakiwa mawindoni. Dawa hiyo ya majani ilikuwa katika kikopo kidogo na ilikuwa ikiwasaidia kuwapata wanyama hata kama walichubuliwa kidogo na mishale. Hakuwa tayari kuishi porini bila mtu aliyemheshimu kama mzazi wake na mazingira aliyoyaona eneo la tukio aliamini askari hao hawakuwa mbali na mzee Rogart. Aliondoka kwa kasi ya ajabu ambayo ilikuwa ya kawaida kwake kutokana na shughuli hiyo ya uwindaji waliyofanya. Aliachana na njia ambayo awali alikuwa ametokea na kuanza kufuata njia nyingine na baada ya kukimbia kwa muda mfupi alifanikiwa kuyaona makanyagio ya viatu vya kiaskari na hapo imani ya kukamatwa kwa mr. Rogart ilimkaa zaidi kichwani.

    Akili yake ilimtuma kufanikisha hata mauaji ili kuhakikisha anampata mzee huyo, alikimbia umbali wa zaidi ya kilometa thelathini pasipo mafanikio ya kuwaona askari ambao aliamini walikuwa wamemkamata mzee Rogart. Alianza kuingia hofu ya kushindwa kufanikisha lengo lake la kumuokoa mzee huyo wakati huo ikiwa jioni, alianza kutembea taratibu akiamini zoezi hilo lilielekea kushindikana. Hofu ya kuuawa kwa mzee Rogart ilizidi kumkaa kichwani na aliamini rais Zakheem Pirjah wa nchi hiyo asingeweza kumwacha hata kidogo. Tayari giza liliingia na hakukuwa na dalili zozote za kuweza kufanikisha kwake kumwokoa mzee huyo. Akiwa bado anaendelea kutembea porini humo huku akiwa amekata tamaa kwa kiasi kikubwa alishtushwa na chanzo cha moto kilichotoa moshi karibu na eneo alilokuwa akitembea wakati huo.

    Hisia zake zilimtuma akiamini kulikuwa na jambo lililokuwa likiendela eneo hilo wakati huo, japo hakuwashuhudia watu waliokuwapo kwenye chanzo hicho cha moto lakini aliamini kuwa ndiyo waliohusika na kukamatwa kwa mzee Rogart. Alianza kusogelea taratibu eneo ambalo moto huo ulikuwa ukiwaka huku akijificha kwenye miti alitaka kuwaona watu waliokuwapo eneo hilo. Hatimaye alitulia sehemu na kuweza kuwaona vizuri lakini pia akishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea eneo hilo. Walikuwa askari wanne waliokuwa wamezunguka chanzo cha moto kutokana na baridi iliyokuwapo muda huo, akili yake kwa haraka ilimpa jibu kuwa hao ndiyo walihusika na kukamatwa kwa mzee Rogart. Jambo lililomtatiza hakuweza kumwona mzee huyo eneo hilo, akaanza kuzungusha macho kila upande akiwa na lengo la kuhakikisha kama alikuwapo eneo hilo.

    Baada ya muda mfupi alimwona mzee Rogart kwa umbali akiwa amefungwa kwenye kwenye mti mkubwa uliokuwa pembeni na eneo ambalo askari hao walikuwa wakiota moto. Geofrey alianza kufikiri jambo la kufanya baada ya kuamini kuwa huo ulikuwa wakati muafaka wa kumuokoa mzee Rogart. Alichuchumaa taratibu baada ya kugundua jambo la kufanya na baada ya kufanya hivyo alianza kutoa matawi ya miti ambayo yalikuwa mengi chini ya miti iliyokuwa imezuguka eneo hilo. Mara baada ya kuyatoa alipata shimo lililomwezesha yeye kuingia kwa kiasi kikubwa akiwa ameweka mishale yake na upinde pembeni kidogo na eneo alilokuwapo. Alikuwa amebakiwa na mishale mitatu na dawa ambayo ilileta usingizi pindi walipokuwa wakifanikiwa kuwadhuru wanyama.

    Mara baada ya kujihakikishia usalama wake akiwa na mshale mmoja ambao tayari ulikuwa na dawa kwenye ncha yake alianza kupiga kelele kama za paka. Alizipiga kelele hizo kwa sekunde kadhaa na kuwafanya askari waliokuwapo kwenye chanzo cha moto washtuke na kuanza kutazama eneo ambalo kelele hizo zilitoka. Waliacha mazungumzo yao waliyokuwa wakiyazungumza na kuanza kuangalia eneo ambalo kelele hizo zilitoka. Baada ya muda mfupi mmoja wao aliwaondoa shaka akiwaambia kuwa hakuna jambo lolote, walikaa tena chini na kuendelea na mazungumzo yao. Dakika mbili baadaye walizisikia kelele hizo zikiwa zimeanza tena jambo lililomfanya mmoja wao achukue bunduki yake na kuanza kutembea kuelekea eneo ambalo alisikia kelele hizo. Ghafla hakusikia tena kelele hizo lakini aliendelea kutembea akielekea eneo ambalo alikuwa

    amesikia kelele hizo zikitoka.

    Alitembea mpaka eneo la ndani toka sehemu iliyokuwa na chanzo chao cha moto lakini hakuweza kuona kitu na alibaki amesimama huku akiwa anacheka akiwaeleza wenzake kuwa hapakuwa na kitu. Wakati huo Geofrey alikuwa amejifukia chini katika matawi ambayo askari huyo alikuwa pembeni yake akiwaeleza wenzie, walikuwa katika eneo lililokuwa na giza mbali na eneo lenye chanzo cha moto. Alianza kwa kujitoa kichwa taratibu na mara baada ya kutoka vizuri kwa kasi alimchoma yule askari na mshale katika mguu wake wa kulia, kabla ya kuuchomoa mshale huo kwa haraka na kurudi tena katika shimo alilokuwapo. Askari huyo alipiga kelele akitupa bunduki yake pembeni na kuanza kujiviringisha kwa maumivu aliyokuwa akiyapata.

    Wenzake walitoka mbio eneo walilokuwapo na kwenda kumshuhudia damu zikimtoka katika mguu wake wa kulia, hisia alizozipata askari huyo alidhani ni nyoka jambo lililowafanya askari wenzie wambebe mpaka kwenye chanzo cha moto. Walianza kumpa huduma ya kwanza kwa kumfunga kamba eneo la juu na sehemu aliyokuwa amepata jeraha hilo. Wakati huo kwa kasi akijiburuza kama nyoka, Geofrey alitoka na kuelekea eneo alilokuwa ameweka mishale yake na upinde akiwa amebakiwa na mishale miwili pamoja na dawa aliyitumia katika zoezi hilo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Geofrey alitoka na kuelekea eneo alilokuwa ameweka mishale yake na upinde akiwa amebakiwa na mishale miwili pamoja na dawa aliyitumia katika zoezi hilo.

    Alikimbia upande mwingine wa pembeni na kujilaza akiwa ameshaweka dawa ile iliyosababisha usingizi katika mshale mwingine na aliupachika kwenye upinde tayari kwa kuuachia.

    Alielewa kwa vyovyote vile watu hao wangerudi eneo lile kuangalia nyoka ambaye alikuwa amemdhuru askari mwenzao. Aliwasikia wakijadiliana jambo la kufanya huku wakiwa wamechanganyikiwa, hilo lilifuata baada ya kuona askari mwenzao akiwa amepatwa na usingizi wa ghafla. Walishauriana waendelee na safari ili wampeleke mwenzao hospitali, lakini umbali wa kilometa zaidi ya arobaini zilizokuwa zimebaki kuuacha msitu huo ndizo ziliwakatisha taama. Mmoja wao aliwaeleza wenzie kuwa rais Zakheem asingewaelewa hata kidogo endapo mzee Rogart angewakimbia, wakati huo mzee huyo aliangalia kila kilichoendelea.Baada ya makubaliano hayo waliona wabaki eneo hilo kutokana na hofu kubwa juu ya mzee Rogart waliyeamini hakuwa mtu wa kawaida kwa vile alitafutwa kwa miaka mingi pasipo kupatikana.

    Askari hao waliendelea kumpa huduma mwenzao aliyepatwa na usingizi wa ghafla wakiamini alikuwa ameg`atwa na nyoka. Baada ya muda mmoja wao alianza kutembea kuelekea eneo lililokuwa limetokea tukio hilo, mkono mmoja alibeba bunduki na mwingine alikuwa amebeba ukuni uliokuwa umeshika moto huku ukiendelea kuwaka. Mara baada ya kufika eneo hilo aliziona damu ambazo zilikuwa zimemtoka askari mwenzao na aliamini eneo hilo alikuwapo nyoka, aliendelea kuzungusha macho kila upande wa eneo hilo akijaribu kumtafuta nyoka huyo. Wakati huo kwa umbali mfupi katika eneo lililokuwa na giza Geofrey alimwona vizuri askari huyo aliyekuwa na ukuni wenye moto ulioangaza vizuri sehemu aliyokuwapo.

    Bila kuchelewa aliivuta kamba ya upinde wake iliyokuwa na mshale huku akiwa ameupima sawasawa akielekeza katika mguu mmoja wa askari huyo. Punde aliachia upinde huo ulioenda kutua sawasawa kwenye mguu wa kushoto wa askari huyo na ulizama kiasi cha kutaka kutoka upande wa pili wa mguu huo. Alitoka mbio na kuelekea upande mwingine uliokuwa karibu kabisa na eneo alilomwona mzee Rogart akiwa amefungwa. Askari huyo alipiga kelele na kutupa bunduki na ukuni uliokuwa na moto akiwa ameumia mguu wake na kuushuhudia mshale uliompata sawasawa. Kelele hizo ziliwashtua askari wenzie waliokimbia kuelekea eneo alilokuwapo na kumwona akiwa amedhuriwa na mshale huo. Askari mmoja alianza kumvuta kuelekea eneo ambalo lilikuwa na chanzo cha moto na mwingine alimua kuzima moto uliotaka kushika eneo hilo baada ya ukuni wenye moto kutupwa chini na mara baada ya kuzima alienda kuungana na mwenzake. Hisia za nyoka tena ziliwatoka kichwani mwao na walianza kuingiwa na hofu kubwa kuwa eneo hilo kulikuwa na adui, askari mmoja alianza kumpiga mzee Rogart akimshutumu alihusika na matukio hayo. Mara baada ya kumtoa mwenzao mshale na kupunguza kasi ya damu iliyokuwa ikimtoka wote wawili walishika bunduki zao wakiwa tayari kwa shari hiyo iliyoendelea. Muda mfupi mwenzao naye aliingia katika usingizi mzito, jambo hilo liliwachanganya na kuamini wenzao walikuwa wanakufa.

    Mzee Rogart alionekana kupata faraja kidogo moyoni akihisi huenda kuna mtu alikuwapo eneo hilo kumwokoa lakini bado alikuwa akihofia maadui zake kadhaa wa miaka mingi iliyokuwa imepita na kuwahusisha na tukio hilo lililokuwa likiendelea. Mawazo yake hata kidogo hayakumweka akilini kijana wake Geofrey aliyemchukulia kama mwanaye kuhisika na jambo hilo. Askari mwingine alimfuata kwa mara ya pili na kuanza kumpiga tena ngumi za tumbo akimtaka aseme mtu aliyehusika na tukio hilo. Wakati huo askari mwenzie alikuwa kwa mbali akizunguka eneo hilo akiwa na tahadhari kubwa ya usalama wake. Akiwa anaendelea kumpiga mzee huyo alishtushwa na mshale uliotua kwa kasi na kupenya sawasawa katika makalio yake na kumfanya aanze kupiga kelele kutokana na maumivu aliyoyapata.

    Bunduki aliyokuwa ameishika aliitupa chini na alianza kujivingisha kwa kelele za maumivu. Askari mwenzie aliyebakia kwa kasi alimfuata na kumvutia eneo walilokuwapo wenzake, aliingiwa na hofu ya ghafla na imani aliyoipata haraka ilimbainishia alikuwa katika hatari ya kupoteza maisha muda wowote.Akili yake ilikuwa haijatulia hata kidogo akiwa bado hajagundu jambo la kufanya askari huyo aliyejeruhiwa aliingiwa na usingizi kama wenzake. Jambo hilo lilimshtua askari huyo aliyekuwa amebakia akamua kutoka kwa kasi akikimbia kuondoka eneo hilo ambalo wenzake aliamini walikaribia kufariki. Aliongoza upande ambao walikuwa wakielekea na mzee Rogart na aliondoka bila hata kumsemesha jambo lolote akiwa na hofu kubwa.

    Mzee Rogart alikuwa bado katika mti aliokuwa amefungwa kando kidogo na chanzo cha moto huku hofu tele ikiwa imemjaa baada ya askari pekee aliyebakia kukimbia. Hofu yake ilitokana na mtu huyo aliyemwokoa alikuwa na lengo gani, zaidi aliamini hakuwa na mtu yeyote waliyefahamiana wakati huo ambaye angeweza kumsaidia. Kilichomtisha zaidi alikaa dakika kama kumi pasipo kuona dalili za mtu huyo akitokea, jambo hilo lilimtia hofu zaidi na alihisi na yeye mwisho wake ulifika. Akiwa na mawazo tele alishtushwa na mshale ulitoka kwa kasi ya ajabu upande wa mbele yake uliokuwa na giza na kutua juu kidogo na kichwa chake katika mti huo aliokuwa amefungwa. Hofu yake iliongezeka na hali ya ketetemeka ilifuata alipogeuza kichwa chake kuutazama mshale huo alishuhudia wote ukiwa umezama kwenye mti.

    Jambo hilo lilimfanya mzee huyo aanze kulia peke yake, baada ya kuanza zoezi hilo la uoga alishtushwa kumuona Geofrey akitoka katika eneo hilo la miti lililokuwa na giza huku akicheka juu ya hofu aliyoionyesha. Mzee Rogart hakuamini macho yake baada ya kugundua aliyekuwapo eneo hilo alikuwa ni Geofrey, aliacha kulia akiwa tayari ametokwa na machozi. Alimfungua haraka kabla ya kukumbatiana kwao, akili yake ilimrudia kichwani mzee Rogart na kuamini kuwa kila kitu alichokiona kilifanywa na mwanae huyo ambae alimtambua kwa uhodari wa kutumia upinde na mishale. Alikuwa hakosi pindi wakiwa katika shughuli zao za uwindaji, kila mshale siku zote ulikuwa lazima umpate mnyama. Walichukua bunduki zote nne za askari hao ikiwamo na ile ya askari aliyekimbia eneo hilo baada ya kuingiwa na hofu ya kuuawa walianza kukimbia kwa kasi kurudi eneo ambalo lilikuwa na makazi yao. Lengo lao kubwa lilikua ni kwenda kupanga na kujua jambo ambalo lingefuata wakati huo.

    Mzee Rogart ambaye alikuwa na umri wa miaka sitini alikuwa akijitahidi kukimbia kama vile alikuwa kijana mdogo ukimlinganisha na Geofrey. Tayari ilikuwa imegundulika kwamba waliishi porini na agizo la kukamatwa kwa mzee Rogart lilikuwa limetoka kwa rais wa nchi hiyo Zakheem Pirjah akiwa na machungu juu ya kifo cha mkewe miaka kadhaa iliyokuwa imepita. Rais huyo alionekana alihitaji kwa hamu Rogart akamatwe akiwa hai na lengo lake lilionekana kuwa alihitaji kumuua ili kulipiza kisasi katika kifo alichomsababishia mkewe. Majira ya saa kumi usiku wakikuwa wamefika eneo waliloishi huku wakiwa wamechoka sana na eneo hilo lilikuwa limeungua lote kiasi cha kukosekana kwa mabaki hata kidogo. Hiyo yote ilitokana na miti iliyotumika kuijengea nyumba hiyo na zaidi mafuta ya petroli ambayo askari waliyatumia kuichoma.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mzee Rogart alimweleza Geofrey kuwa alihitaji waelekee jimbo la Linden lililokuwa eneo la kusini mwa nchi hiyo ya Guyana. Mawazo yake yalikuwa ni kwenda kutafuta msitu mwingine katika jimbo hilo ili wakaendeleze maisha yao kama ilivyokuwa awali. Hakukuwa na pingamizi kutoka kwa Geofrey ambaye muda wote alimsikiliza mzee huyo aliyemchukulia kama mzazi na alikuwa tayari kufanikisha lolote ili apone. Kilichomuuma sana ni kuungua kwa kumbukumbu ya picha zake za familia alizokuwa akitembea nazo siku zote. Ila alifarijiwa na mzee huyo aliyempa imani kuwa siku moja lazima angerudi Tanzania kuwaona wazazi wake. Waliamua kulala eneo hilo ambalo lilikuwa na joto kutokana na moto uliounguza nyumba yao wakiwa wanapumzika baada ya kukimbia kwa muda mrefu. Siku iliyofuata waliamka majira ya saa tatu asubuhi na walikuwa na hofu wakihisi muda wowote askari waliotumwa na rais wangerudi tena eneo hilo.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog