Search This Blog

Saturday, 18 June 2022

HILA - 4





    Simulizi : Hila

    Sehemu Ya Nne (4)



    GARI za polisi aina ya Difenda zilitimua vumbi huku mojawapo ikipiga king’ora kwa sauti ya juu sana. Raia walibaki kushika vichwa kwa jinsi waendesha pikipiki walivyokuwa wakikoswakoswa na magari yale.

    Wengi wao wakahisi kuwa yawezekana kutakuwa na majambazi mahali. Lakini hilo hawakulitilia maanani sana kwa sababu ilikuwa kawaida ya jeshi la polisi kusuasua sana wanapopewa taarifa juu ya ujambazi kufanyika mahali. Iweje siku ile wawe wepesi kiasi kile.

    Gari zile tatu zilizojaa askari walio kwenye sare na wasiokuwa na sare zilizidi kuiacha wilaya ya Handeni mjini na kuifukuzia sehemu changamfu ya kwa Diboma nje kidogo ya wilaya ya Handeni, hapo napo zikapita kwa kasi kubwa, askari walikuwa wameshika bunduki zao imara kana kwamba kulikuwa na vita kuu ya silaha za moto mbele yao.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya mwendo wa takribani saa zima tayari kijiji cha Mafisa kilikuwa kinatetemeka, kilikuwa kimejaa maaskari tele huku kila mmoja akiwa ana silaha kali. Walionyesha umakini wa hali ya juu sana kana kwamba adui yao alikuwa anawakaribia huku akiwa na silaha pia.

    Moja kwa moja wakaongozwa naaskari ambaye hakuwa na sare rasmi wakaivamia nyumba ya John Masele waziri wa zamani wa mambo ya ndani na nje. Wakamtoa mzegamzega. Huku wakimtishia iwapo atafanya jitihada zozote za kupambana nao hawatasita kumimina risasi katika kifua chake.

    John Masele waziri wa zamani wa mambo ya ndani na nje akajikuta katika mojawapo ya fedheha kubwa kabisa mbele ya familia yake. Mke na watoto wakubwa kabisa. Aliburuzwa huku akisukwasukwa na kila mkono wa askari. Mkewe alivyojaribu kuwazuia maaskari alisukumwa na kuangukia mbali, mtoto wake wa kiume naye akataka kuingilia kati ule mzozoz akazolewa ngwala na kuanguka mbali.

    Ilikuwa kitimtimu!!

    “Nimefanya nini jamani…” alijaribu kuuliza, lakini badala ya kujibiwa alijikuta akipokea kitako cha bunduki katika mgongo wake akajikaza asilie kwa sauti ya juu ilhali akiwa kwenye maumivu makali.

    Sam amefanya nini huyu kijana!! John Masele alijiuliza wakati huo akiwa kwenye karandinga, pingu katika miguu na mikono yake. Aliutazama mwili wake ambao ulishaanza kuzeeka, akatambua kuwa hakuna mtu ambaye atamuonea huruma huko aendapo. Akamwomba Mungu amwepushie dhahama ile.

    Ilikuwa ya kushtukiza mno dhahama ile.

    WAKATI Masele akiwa katika dhahama ile, wilayani Handeni mambo yalikuwa makubwa zaidi. Mji ulikuwa umechafuka.

    Picha za Samwel Mbaule ambazo zilitumwa kwa njia ya Fax kutokea jijini Dar es salaam zilibandikwa kwa fujo zikiwa na neno ‘ANATAFUTWA DAU NONO LITATOLEWA KWA ATAKAYEFANIKISHA KUPATIKANA KWAKE’

    Tangazo lilibandikwa katika misitimu na kwenye nyumba za watu, wabandikaji walikuwa ni askari waliokuwa wamevaa kiraia na wengine wakiwa katika sare rasmi.

    Mji ulibaki katika sintofahamu wasipate kujua huyo Samwel Mbaule nd’o nani na ni kitu gani alikuwa amefanya.

    Wachache walimtambua kama mwandishi katika gazeti la HAKI.

    Hawakujua kiundani kama ni yeye kweli ama ni majina tu yalikuwa yamefanana.

    Askari walizagaa huku na kule, wakiwalazimisha akina mama waliovaa katika mfumo wa ninja kujifunua ili wakagulie. Waliothubutu kukaidi walivuliwa kwa nguvu huku wakipokea kipigo.

    Waume zao walipoingilia walitiwa pingu na kuishia kulala kituo cha polisi kwa kosa la kuizuai serikali kufanya kazi yake.

    Tanzania bwana!!



    Tangazo moja lilibandikwa katika kibanda cha internet ambacho Sam alienda kusoma barua pepe zake. Dada muhudumu wa pale akawa wa kwanza kuing’amua ile sura.

    Akatambua vyema kuwa mtu mwenye sura ile alikuwa pale kwa ajili ya huduma ya internet.

    Alimkumbuka kwa sababu alikerwa na kitendo cha Sam kumuuliza neno la kiingereza kisha akashindwa kuelewa anachoulizwa, ‘CD-rom’.

    Neno hilo lilimfanya yule dada amtazame Sam kama kijana anayejifanya mjuaji sana.

    Kero yake ikaenda mbali zaidi na kumwona Sam mwenye maringo sana. Hasahasa alipotoa shilingi elfu kumi na kumsumbua kutafuta chenchi.

    Ilikuwa lazima amkumbuke tu!

    He! Yule mringaji, mjivuni.. anatafutwa na polisi. Akaduwaa dada yule.

    Lakini hakujua ni wapi kijana yule alikuwa ameelekea, lile neno DAU NONO litatolewa likamtoa udenda. Alikuwa ameichoka ile kazi ya pale kibandani ambayo haikuwa na masilahi kabisa hivyo kwa kulipata donge lile nono kama lilivyoahidiwa na wabandika matangazo.

    Dau nono likamfanya aanze kumfikiria bosi wake ambaye ni mwanamke, akamwona kama katili sana kwa sababu tu huwa anamlaza sebuleni.

    “Sasa ni wakati wa kuanza maisha yangu, hapa kwa mfano wakinipa hata milioni mbili huyooo naenda zangu Dar. Natafuta chumba napanga, naanzisha biashara zangu, baada ya muda kidogo nawachukua wadogo zangu nakaa nao.” Yule dada alienda mbali zaidi na kuwa kama tahira anayeendesha gari kimawazo ilhali hilo gari hana.

    Dada yule mfupi kiumbo na machachari kimtazamo huku akiwa na sura isiyovutia sana alitambua kuwa iwe isiwe Sam atarejea tena katika kibanda kile kama alivyokuwa amemuahidi kuwa jioni ama usiku atarejea tena. Akaomba iwe hivi atakavyo.

    Yule dada kwa ustadi na wepesi wa hali ya juu bila kuonwa na mtu yeyote alilibandua lile tangazo lililokuwa limebandikwa katika ofisi yao.

    Kisha akapiga goti na kuomba Mungu wake yule Sam asiweze kukamatwa na watu wengine bali yeye ili hatimaye aweze kulipata lile donge nono na kubadili maisha yake.

    Akachukua namba ya simu iliyopachikwa pale akahifadhi katika simu yake ili akimuona tu Sam aweze kutoa taarifa.



    Tofauti na siku nyingine ambapo dada yule hufunga kile kibanda majira ya saa kumi na mbili, lakini hadi inafika majira ya saa moja usiku alikuwa hajafunga.

    Subira yavuta hili lakini ni pale tu itakapokuwa na dalili ya hiyo heri, muda ulizidi kusogea yule dada machachari hakumuona Sam. Majira ya saa mbili usiku huku roho ikimuuma aliamua kufunga ofisi.

    Alimuona Sam kama amemuonea vile kwa kutokuonekana kwake, akamuona mkatili na aliyemnyima ulaji. Ili kutii hasira zake akamtukana Sam kwa kikabila chao.

    “Duh! Nd’o unafunga Sista… nimechelewa eeh!” yule dada alishtushwa na sauti nyuma yake, alipogeuka alipigwa na butwaa alipokutanisha macho yake na Sam ambaye alikuwa anatabasamu.

    Yule dada alishindwa kuhimili mshtuko ule. Akaanza kuhangaika, mara ashike mkoba, mara achezee funguo mara ajichekeshe ilimradi kuhangaika tu kuutafuta ujasiri ambao ulikuwa umepotea.

    “Naweza kukufungulia kaka yangu… wala usijali mi ninachotaka ni hela tu na hapa nilifunga kwa sababu hapakuwa na wateja tu!” alijaribu kuongea lakini sauti yake ikiwa inatetemeka.

    Sam akamshukuru na pia kumpa pole sana kwa usumbufu ule.

    “Usijali kaka mteja ni mfalme…” alijibu huku akimalizia kufungua geti la ofisi yake mikono ikiwa inatetemeka haswa.

    Akaingia na kuwasha taa, kisha akawasha kompyuta na kumruhusu Sam aketi angojee mtandao ukae sawa. Sam akaketi!

    Yule dada tofauti na alivyokuwa makini mchana, lakini wakati huu alikosa umakini kabisa na alikuwa mtu wa kujilazimisha kucheka kila mara ambapo Sam alijaribu kumsemesha.

    Mwandishi wa habari ni mtaalamu wa taaluma nyingine zote. Kauli hii hakika ilifanya kazi, mawndishi wa habari ni mpelelezi, mwandishi wa habari ni mwanasaikolojia na mwandishi wa habari ni mtafiti.

    Sam licha ya kuendelea na mambo yake katika mtandao, bado alitumia sekunde chache kujiuliza ni kitu gani kinaendelea.

    “Samahani kaka una hela kubwa nikatafute chenchi kabisa maana naona kifurushi cha intaneti nacho kinakaribia kuisha nataka kwenda kununua…” yule dada alimweleza Sam.

    “Hapana hii hapa mia tano si nd’o bei ya nusu saa..” Sam alitoa noti na kumpatia yule dada.

    “Aah! Basi sawa naingia dukani mara moja kujua vocha niunge kifuruishi maana hicho kinakaribia kuisha hivyo”

    “Hamna shaka dada utanikuta!” Sam alijibu kisha akaendelea na mambo yake mengine.

    Yule dada alipotoka tu nje mara moja alipiga ile namba.

    “Nipo naye yule kijana mliyeweka mabango mnamtafuta, wahini jamani anakaa hapa kwa nusu saa… nusu saa tu…” alisihi yule dada.

    Upande wa pili mambo yakawaka moto, yule dada akaulizwa ni wapi ilipo ofisi yake. Akajieleza vyema.

    “Tunakuja sasa hivi!” sauti upande wa pili ilijibu.

    Yule dada akarejea kibandani. Akatulia tuli huku moyo ukipiga kwa nguvu mno. Akili yake yote ikabaki kuliwaza lile donge nono.



    ****



    UHOLANZI KASKAZINI, JIJINI AMSTERDAM



    KIUBARIDI kikali kilichoendelea kuvuma ukiwa ni msimu wake kiliwasukuma watu lukuki kujibanza katika migahawa ya kahawa iliyojazama katika jiji hilo maarufu kwa kuwa na migahawa mingi ya kahawa.

    Katika mgahawa mmoja uliokuwa kandokando ya barabara ielekeayo makumbusho ya Amsterdam, vijana watatu walikuwa wamejumuika wakipata kahawa baada ya kuwa wamemaliza kazi kwa siku hiyo.

    Walirushiana maneno ya utani hapa na pale huku furaha zao zikiongezwa zaidi na muziki uliokuwa ukilindima kwa mbali.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakati wakizidi kunogewa na kahawa ile nyeusi tii. Mara simu ya mmojawao iliita katika namna ambayo haikuwa ya kawaida katika masikio ya watatu wale.

    Upesi wakapeana ishara na kisha mzungu mwingine akatoa kifaa mfano wa kompyuta na kukifungua kisha akaunganisha na ile simu.

    Na hapo wakaweza kusoma kitu kilichoandikwa pale.

    Mzungu wa tatu akachukua simu na kupiga mahali kisha akasubiri kwa takribani dakika moja kabla simu haijapokelewa.

    “Yes sir, Five degree, thirty minutes south, thirty eight degree zero minutes East. Handen District, Tanga region Tanzania. (5º35’ S, 38º0’ E)” Kisha simu ikakatwa baada ya maelekezo yale mafupi.

    UPANDE wa pili ambaye alipokea simu alikuwa mzee mwenye ndevu nyingi. Alitabasamu baada ya simu hii kisha akachukua simu yake akabofya namba maalumu alizozifahamu na punde simu ikapokelewa jijini Dar es salaam Tanzania. Mpokeaji akiwa ni raisi wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania.

    “Ni upuuzi gani unaendelea Tanga…. Mnamruhusu vipi huyo mwanadamu kuanza kunipepeleza mimi. Sikiliza Saidi, hii ni hatari kwangu lakini ni hatari zaidi kwako. Mimi ni mtu mmoja tu lakini wewe ni mtu katikati ya watu. Utakufa vibaya, utakosa hifadhi popote pale kwa yote yanayoendelea kati yangu mimi na wewe Saidi…. Huyo kiumbe hafai na sijui ni kipi kiliwasukuma kumtoa rumande, huyo angeuwawa juu kwa juu…. Sijui unanielewa…” ilifoka sauti ile kwa kiingereza.

    Raisi akamtazama mkewe ambaye ni kama alikuwa akifuatilia mazungumzo yao, mke akajiondokea zake baada ya kuona anamnyima uhuru mume wake.

    “Lakini Ben, tulikubaliana kuwa tunamwacha huru ili tuweze kuupata ule mkanda. Utajuaje kama…..” kabla hajamalizia sauti ile ikaingilia kati.

    “Nahitaji kichwa chake Amsterdam nikiweke katika makumbusho yangu…. Na hapo mkataba wangu mimi na wewe utaendelea la sivyo sahau kama umewahi kukaa meza moja na Benson Van Bronchost!” na hilo likawa neno la mwisho na simu ikakatwa.

    Raisi akashusha pumzi zake kwa nguvu, akatazama katika karatasi ambalo aliandika mahali ambapo alielekezwa juu ya uwepo wa Sam. Na hii ni baada ya vijana wa uholanzi kupatiwa barua pepe ya Sam. Wakaihifadhi katika mtego maalumu ambapo kitendo cha kuifungua tu basi itawaonyesha wao mahali ambapo yupo kwa wakati huohuo.

    Naam! Mtego ukawa umenasa!!



    Benson akiwa na ghadhabu akachukua simu yake nyingine na kupiga tena kwa mtu mwingine.

    Moyoni mwake alijua kuwa licha ya kumchimba mkwara raisi wa Tanzania, hata yeye moyoni hakuwa na amani hata kidogo. Kwani kitendo cha kufahamika kwake na baadhi ya watu hakikuwa salama hata kidogo kwa mazingira yake ya ubia na serikali ya Tanzania.



    *****



    KIFO ni kitu kingine, hakuna hata mtu mmoja asiyeogopa kufa hasahasa akitambua kuwa anayo namna ya kujiepusha na kifo kile.

    Tina alikuwa mwanadamu tena mwanamke. Yale masaa yalikuwa yanazidi kukatika, masaa ambayo mzee Matata alimweleza kuwa yalikuwa yamesalia ili aweze kukatwa shingo yake ambayo itatenganishwa na kiwiliwili.

    Yakiwa yamebaki masaa mawili Mzee Matata aliingia katika chumba alichomuhifadhi Tina. Alikuwa na msumeno mkali na pia alikuwa na kitu kama runinga bapa. Akaichomeka katika umeme na hapo ikawa tayari kwa matumizi.

    Badala ya kuzungumza neno lolote aliiwasha runinga ile, na pale akaonekana dada mmoja akiwa uchi wa mnyama anatetemeka, wanatokea wanaume wawili wazungu wanamfunga kamba miguuni na kisha wanamkalisha katika kiti, mikono yake inafungwa nyuma ya kitu.

    Kisha wanaume wale wanatokeza wakiwa na misumeno miwili, wanaikamta shingo ya yule dada, wanaichuna kidogo anaanza kutokwa damu. Anapiga kelele lakini hawaonyeshi kujali.

    wanaishika ile damu na kumlazimisha yule dada ailambe. Anapobisha wanamzamishia kitu kama kisu kikali katika paja lake, damu inaruka mithili ya kuku aliyechinjwa.

    “Vipi tuimalizie hii filamu kwa vitendo ama leo utasema kila kitu…” Mzee Matata alimuhoji Tina huku akitabasamu.

    Tina macho yalikuwa yamemtoka huku jasho likimtiririka, meno yaligongana kinywani kwa fujo. Akili ilikuwa imemruka alipiga magoti na kumsihi mzee Matata asimuue lakini mzee yule hakuwa na huruma aliendelea kutabasamu kisha akaitazama saa.

    “Zimebaki dakika thelathini tu za maisha yako. Unajisikiaje kuungana na wafu wakati unao uwezo wa kuikataa ahera”

    “Nasema kila kitu… nasema…” Tina alijikuta akitokwa na lile neno ilhali hakujua ni kitu gani anaweza kusema kwa usahihi.

    Mzee Matata akamfanyia ishara kuwa aendelee kuzungumza. Tina akabaki kujiumauma, hakujua hata ni neno gani la kumshawishi mzee Matata.

    Na akiwa hajatokwa na neno lolote mara simu ya mzee Matata ikaita, akaitoa upesi na kutazama akakutana na namba zipigazo kutoka uholanzi.

    “Email imefunguliwa jijini Tanga wilaya ya Handeni, eneo hilohilo kuna kiumbe kinataka kujua juu ya Benson van Bronchost…. Hali ni mbaya. Nani ajuaye kuhusu Van Bronchost eeh! Nakuuliza wewe… nani ajuaye kuhusu Van??” sauti ilifoka na kusikika vyema kutoka na ile simu kuwa na sauti ya juu katika spika zake.

    Mzee Matata alikuwa anatetemeka na hakuwa na cha kujibu.

    “Upesi hakikisha jambo hili linazimishwa na huyo mtu anayelisaka hili jina akamatwe na yeyote ajuaye kuhusu Van Bronchost ikiwezekana auwawe mara moja. Nimemuagiza Saidi kuwa nahitaji kichwa cha huyo kiumbe… na wewe nakuagiza hivyo” Sauti iliamrisha kwa lugha ya kiingereza.

    Tina akatambua kuwa mzungumzaji alikuwa na cheo cha juu kuliko mzee Matata.

    Mzee matata akasahau kuwa alikuwa amekuja kwa ajili ya kummaliza Tina. Upesi akatoweka na kuingia chumbani, akapiga simu kwa IGP. Akamweleza kuwa wataalamu wake kutoka uholanzi wamenasa mahali ambapo muuaji wa Steven Marashi anapatikana.

    Na baada ya pale akazungumza na mkuu wa nchi moja kwa moja akamweleza kuwa kuna kiumbe kinaishi nchini na kinafahamu vyema juu ya Benson van Bronchost. Licha ya kuwa tayari raisi alikuwa amepigiwa simu alilazimika kumsikiliza mzee Matata kana kwamba nd;o anasikia kwa mara ya kwanza habari ile.

    Rais akavuta pumzi na kuzishusha kisha akatokwa na neno.

    “John Masele hakuna mwingine, nadhani kijijini hapamfai, anastahili kuishi jela. Noo sio jela anastahili kufa”

    “Fanya hima basi hili jambo limalizike upesi…” alishauri mzee Matata. Raisi akatii!

    “Tukutane Ikulu baada ya nusu saa tuweke mambo sawa…”

    “Nakuja sasa hivi…” mzee Matata akajibu kisha akakata simu.

    Mara ikaingia tena simu ya yule bwana kutoka uholanzi.

    “Maendeleo!”

    “Nimezungumza na raisi, kila kitu kitaenda sawa mkuu.”

    “Upesi tafadhali. Nahitaji kichwa chake nikiweke makumbusho” Akasisitiza.

    Wakati huo mzee Matata alikuwa nje akiwa anapanda garini.

    Kisha akatoweka huku nyuma akifanya kosa la karne!!

    Kosa ambalo kamwe hakuwahi kusamehewa!!

    Ikulu hapakuwa na maongezi mengi zaidi ya amri kutolewa juu ya John Masele kukamatwa mara moja huku muuaji wa Steven Marashi naye akisakwa kwa udi na uvumba. Na hapo polisi wakaingia kazini kwa fujo hadi kijijini Mafisa ambapo John Masele alikamatwa.

    Kisha oparesheni saka Samwel ikaendelea, amri ikitolewa kwa askari kuwa kiumbe yule akikamatwa na kujaribu kufanya ukaidi wowote basi na auwawe mara moja huku mwili wake ukipelekwa ikulu.

    Askari wakaingia kazini kwa fujo. Kutwa nzima hawakupata fununu zozote juu ya kuonekana kwa Sam. Na hii ni kwa sababu wakazi wa Handeni walikuwa wamenuna kwa namna ambavyo askari waliwadhalilisha wake zao. Hivyo badala ya kujishughulisha na hilo donge nono wao walijishughulisha na kuyachana matangazo yale ya msako.

    Lakini majira ya saa mbili usiku wanapokea simu ambayo inawapa matumaini na wanaingia msakoni tena.

    Wakati huu kwa nguvu zaidi kwani raisi aliwahimiza kuwa ambaye atamkamata basi kuna dau nono atapatiwa.

    Mzula ukawapanda!

    Kwa umakini wa hali ya juu wakakifikia kile kibanda walichoelekezwa. Wakakizunguka kila pande huku bunduki zilitazama mlango wa kutokea.

    Baada ya kuhakikisha kuwa wameweka uzio imara mkuu wa msafara akachukua kipaza sauti na kutoa onyo.

    “Samweli Mbaule, upo chini ya ulinzi wa polisi. Tunafahamu ya kuwa upo ndani ya kibanda hiki. Hivyo tunakuamuru utokea kinyumenyume, mikono yako kichwani. Hii ni kwa usalama wako na hili ni onyo la kwanza.” Sauti ikakoma kungojea kama Sam atatoka.

    Kimya! Hakuna mtu aliyetoka!

    “Tunaonya kwa mara ya pili Samweli Mbaule. Hatutasita kutumia nguvu ikiwa hautatoka kwa hiari yako. Hili ni onyo la pili na la mwisho.” Sauti ile kwenye kipaza sauti iliwavuta wakazi wengi wa Handeni katika eneo lile. Wengi walisimama kwa mbali wakiangalia ni kitu gani kinaendelea katika kibanda kile.

    Baada ya onyo lile la pili, askari yule kiongozi wa msafara alitoa neno la amri na hapo askari wakaanza kusogea mbele kwa tahadhari kubwa huku bunduki zikiwa mkononi mwao imara kabisa. Baadhi ya askari hasahasa wa Handeni hawakuwa wakijua lolotekuhusiana na Sam. Bali walifuata amri tu!

    Hatimaye wakakifikia kibanda na askari mmoja akajitupa ndani kiustadi kabisa akabiringita na bunduki yake kisha akatua kwa goti na hapo mdomo wa bunduki yake ukakutana ana kwa ana na dada mfupi akiwa anatetemeka huku sakafuni pakiwa pamelowanishwa kwa mkojo mwingi.

    Mkononi mwake alikuwa ameshikilia picha iliyokuwa imebeba tangazo lile la kutafutwa kwa Sam.

    Askari yule akawaita wenzake wakaanza kukipekua chumba kile, yule dada hakuwa amezungumza lolote midomo yake ilikuwa ikitetemeka mno.

    “Mwanamke… yupo wapi Samwel..” sauti kali ikamuuliza baada ya kukosekana kwa kiumbe yeyote mle ndani.

    Yule dada huku akiwa anatetemeka, magwanda ya askari na mitutu ya bunduki mbele yake ilikuwa kitisho kikubwa.

    Na hii ilikuja wakati mbaya haswa kwa sababu nd’o kwanza alikuwa ametoka kushangazwa na kuujiza wa Sam. Sasa yu katika mitutu ya bunduki.

    Akili yake ilikuwa aiamini kilichokuwa kimetokea ndani ya dakika chache zilizopita.

    Akabaki kuusimulia mkasa ambao alikuwa amekumbana nao dakika chache zilizopita baada ya kutoka kupiga simu. Huku akiwa anatetemeka akawasimulia kilichotokea akianzia pale ambapo alitoka kupiga simu.



    DAKIKA CHACHE BAADA YA KUTOKA KUPIGA SIMU



    “Vipi vocha umepata…” Sam akamtundika swali la ghafla bila kumtazama machoni.

    “Aaah! Eeh! Vocha aah! Nitanunua tu kesho….” Binti akabaki kujiumauma.

    “Oh! Sawa mimi nimemaliza dada nashukuru sana…” Sam alimweleza kiupole kabisa.

    “Ah! Nd’o unaenda, mbona bado dakika nyingi hivyo sasa, dakika sijui ishirini… malizia tu mi bado nipo…” alijibu yule dada lakini hakuwa anajiamini.

    “Hapana inabidi niondoke tu…” Sam alisisitiza huku akisimama.

    “He! Kwa nini sasa? CD nini sijui hiyo kwani haifanyi kazi tena” aliuliza huku akiingiwa na hasira za kukosa donge nono. Alitamani kama angekuwa mbabe aweze kumzuia Sam asitoke lakini alitambua kuwa hakuwa na jeuri ile.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa sababu jamaa zako watakuja hapa baada ya dakika thelathini ama wakiwahi sana ishirini…. Wakija wasalimie waambie nilikuwepo.” Sam alimweleza yule dada huku akitabasamu.

    “Jamaa gani? Jamani” aliuliza yule dada huku hatia ikimtawala. Mikono yake ikijifinyanga huku na kule.

    “Kuna jela dadangu acha tamaa za muda mfupi, ukienda jela watakuoa wanawake wenzako shenzi wewe!” Sam alimfokea kisha akamsukuma akaangukia kwenye meza ya kompyuta, Sam akatoka akamwacha dada tamaa akiwa amejiinamia huku akijiuliza Sam alijuaje juu ya ile njama.

    Hakujua kabisa kama Sam alimfuata kwa nyuma alipozuga anaenda dukani na kwa jinsi alivyokuwa na kitete akawa anaongea sauti ya juu. Sam akawa amesikia kila kitu kuhusu kusakwa kwake.

    Ama kwa hakika uandishi wa habari ni utaalamu wa taaluma nyingine zote. Mwandishi wa habari ni mpelelezi, mwandishi ni mwanamichezo, mwandishi ni mtafiti.

    Dili likageuka dirisha! Sam akatokomea.

    Na wakati anafikiria kutoweka pale kabla hawajafika aliowapigia simu, nd’o hapo alisikia yale matangazo ya vitisho.

    Alipotaka kutoka akakutana na midomo lukuki ya bunduki ikikitazama kibanda chake. Mkojo ukabisha hodi, alipogoma kufungua ukaamua kufungua wenyewe na kutoka.

    Dada akajikojolea huku akihangaika sakafuni, miguu haikuwa na nguvu. Akakiona kifo kikimnyemelea, lile donge nono alilolitamani akaliona likitaka kumtoa roho.

    Na hata askari alipobiringita na kuingia ndani ya kile chumba bado dada yule hakuwa na hali kabisa.



    Maelezo yake hayakuwatosheleza askari.

    Ni kweli waliendelea kumsaka Sam huku na kule. Lakini hawakumwacha yule dada kirahisi. Baada ya kumpiga makofi mawili matatu na kumtisha walimrusha ndani ya karandinga na kutoweka naye.

    Akaishia kutupwa mahabusu kwa usemi kwamba anaisaidia polisi upelelezi!!



    KWA UPANDE WA SAM



    Usiku uleule kwa kutumia usafiri wa pikipiki Sam akatokomea zake na alfajiri ikamkuta njiani kurudi Dar es salaam akiwa amejitoa muhanga wa aina yake. Alikuwa kwenye lori la lililobeba machungwa kutoka Tanga. Alikuwa amekaa na watu wasiojua nchi yao inatoka wapi na inakwenda wapi. Walikuwa ni watu waliokata tamaa ambao pesa kidogo aliyotoa Sam ili aweze kusafiri na lori lao kwao ilikuwa kubwa sana.

    Hili lilikuwa tabaka lisilokuwa tayari kupoteza muda kusikiliza ama kutazama taarifa ya habari.

    Naam! Hawakujua hata kana Sam anatafutwa!

    Hiyo ilikuwa bahati ya mtende kwake.



    *****



    ILIKUWA ni karata ya aina yake ambayo mama huyu aliamua kuicheza ikiwa hajui upande wa pili umezichanga vipi karata zake. Alifanya hivi bila wasiwasi hasahasa baada ya kugundua ule mchezo aliokuwa anashiriki uliitwa Kombolela.

    Mmoja akimuwahi mwenzake nd’o mwisho wa mchezo!

    Alikuwa amebeba kapu lililosheheni mchicha na mboga nyingine za majani.

    Alipita mitaa kadhaa kutafuta uzoefu na kisha akamlizia Magomeni mikumi, katika nyumba ambayo alikuwa akiishi waziri wa nishati na majini bwana Mathias Obhare.



    Siku hiyo alijaribu kufanya madaha ya hapa na pale ili geti liweze kufunguliwa lakini hakuna mtu aliyejitokeza kufungua.

    Majirani walidai kuwa katika nyumba ile ni mara chache sana wenyewe kuonekana na haijulikani rasmi iwapo waziri huwa anaishi pale ama ni mojawapo ya samani zake.

    Mama lao hakukata tamaa na siku iliyofuata kama kawaida alipitisha mboga huku akipita katika lile geti jeusi na kuita iwapo wenyewe wapo waweze kununua mboga.



    Na siku ya pili hali ikawa ileile. Mama lao ambaye alikuwa akiwasiliana na Yakubu Gama ambaye alikuwa Morogoro alianza kukata tamaa lakini Gama akamsihi kamwe asikate tamaa.

    Siku hii Mama lao alibahatika kuwakuta wenyeji wake.

    Akabisha hodi mlango ukafunguliwa akapenya ndani na beseni lake lililosheheni mboga mboga. Mapigo yake ya moyo yalikuwa juu sana alipoona geti likifungwa, tumbo lilimuunguruma kwa uoga lakini hakuacha kutabasamu.



    Mara akatokeza msichana mrefu mweusi, akamkaribisha mama lao na kumuuliza ni mboga gani alizokuwanazo katika kapu lake.

    Mama lao akazinadi mboga zote kwa ustadi huku akizipa sifa ambazo hazikuwepo hata kwa mbali.

    Baada ya maneno mengi ya mama lao yule binti akaingia ndani na kurejea na ungo ambao ulionekana kuwa unatumika mara kwa mara.

    “Niwekee zote!” yule binti akamweleza mama lao. Mama lao akashtushwa sana lakini hakuruhusu mshtuko ule waziwazi badala yake ili kumpoteza malikiti yule dada mrefu mweusi, mama lao akapiga magoti chini na kuanza kumshukuru yule binti.

    “Kawaida tu mama yangu, imekuwa bahati yako tu maana mara kwa mara huwa naenda kuhemea sokoni mwenyewe!”



    “Ubarikiwe sana mwanangu, ubarikiwe” mama lao akahitimisha kwa kunyanyua mikono juu na kumshukuru Mungu wake.

    Akamwaga mboga zote kwenye ule ungo. Yule dada akampatia shilingi elfu kumi, mama lao akataka kutoa chenchi yule binti akamruhusu aondoke nayo yote.



    Mama lao kwa mara nyingine tena akapiga magoti na kushukuru! Binti akamnyanyua mama lao akatii na kutoweka eneo lile.

    Alipofika nje ya geti tu akajisemea kwa sauti ya juu kiasi.

    Kombolela Obhare!



    Akimaanisha kuwa na Obhare naye alikuwa anelekea kupatikana. Kwani kujulikana kwa nyumba ile kuishi watu ni hatua kubwa.



    ***



    MWILI wa Yakubu Gama ulikuwa ukiimarika kadri siku zilivyokuwa zinasogea mbele, ripoti za mama lao zilikuwa zinazidi kumsisimua na kumfanya awe na kiu ya kukabiliana na wapinzani wake ambao alianza kuwajua mmoja baada ya mwingine japo kwa hisia.

    Sasa hakuwa akichechemea tena na aliweza kufanya mazoezi ya kukimbia na kuruka kamba. Mazoezi ambayo yalizidi kuichangamsha damu yake.

    Hatimaye yule daktari akakiri kuwa Gama ni mtu wa ajabu sana kwani alikuwa amepona upesi sana tofauti na alivyodhania awali.

    Gama akaruhusiwa rasmi kuendelea na shughuli zake.

    Kikosi kazi kikakamilika!

    Gama akatoweka mjini Morogoro akiwa amepewa kiasi cha kutosha cha pesa na bwana Robert ili aweze kuikamilisha kazi yake.

    Hatua ya kwanza kabisa alianzia pale mama lao alipokuwa ameishia.

    Mama lao alikuwa ameigundua nyumba ya waziri wa nishati na madini, Mathias Obhare. Nyumba ambayo hakuwa akiishi na familia yake lakini mara moja moja alikuwa akiingia na wageni na kisha kutoka bila kujulikana iwapo aliwaacha wageni mle ndani ama vipi.

    Gama akaanzia hapo na kutaka jibu la kuna nini ndani ya nyumba ile. Na kwanini mara kwa mara hakuna watu wanaoonekana kuishi pale.

    KOMBOLELA ikaendelea…..

    Mama lao akashauriwa na Gama apumzike kwani kazi aliyoifanmya ni kubwa na kipande kilichosalia ni kidogo sana ataweza kukimaliza peke yake upesi.

    Mama lao akakubali kuwa atapumzika!!



    *****



    MAJIRA ya saa nne usiku katika kijiwe cha kahawa maeneo ya Magomeni Mikumi wazee walikuwa wakibishana juu ya mambo ya siasa hasahasa juu ya uchaguzi mkuu wa raisi ambao ulikuwa umebakiza miezi kadhaa tu uweze kufanyika.

    Wazee waligawanyika makundi matatu, kundi moja likimuunga mkono Mathias Obhare, kundi la pili likikunga mkono chama cha upinzani na kundi la tatu likiwa haliungi mkono upande wowote.

    Kati ya wote waliozunguka kile kijiwe ni mzee mmoja tu ambaye hakuwa mwingi wa maneno, yeye alikuwa akibugia kashata na kushushia kwa kahawa, kanzu yake nyeupe iling’ara vyema gizani huku kibalaghashia chake kikihifadhi kichwa chake kiunadhifu. Miguuni alikuwa amevaa makubadhi ya gharama ya kawaida.

    “Eti ustadhi, wewe kwa akili ya kawaida tu unaweza kusema kuwa Obhare ana uwezo mzuri wa kutawala kuliko John Masele?” mzee mmoja akamuuliza yule bwana ambaye alikuwa mkimya.

    Yule bwana akakohoa kidogo kisha akatoa jibu ambalo liliumaliza ule mzozo.



    “Anayetakiwa kuzungumzwa kwa sasa si Masele tena kwa sababu hayupo kwenye kinyang’anyiro…. Jambo la msingi ni kumpokea huyo Obhare liwalo na liwe walishazoea watanzania sisi vichwa vya wendawazimu….”

    Kimya kikatanda, kila mmoja akatafakari kauli ile kwa uzito na majibizano yakaishia pale.

    Yule bwana akaendelea kubugia kashata na kahawa hadi kijiweni alipobaki yeye na muuzaji tu.

    Alipoitazama saa yake ilimwelekeza kuwa ilikuwa ni saa tano usiku.

    Wakati muafaka kabisa aliokuwa amepanga.

    “Dah! Haya magari hapa hivi shilingi ngapi wanalipia kupaki…” Yule bwana mwenye kibalaghashia akamuuliza muuza kahawa.

    “Dah! Halafu mlinzi alikuwa hapa muda si mrefu, yule mzee mbishi yule. Ungemuuliza sema sasa hiv atakuwa ameenda kujidunga ulabu, akirudi hapa ni kulala tu yaani…”

    “Duh! Yaani anafanya lindo huku amelewa mbona balaa…”

    “Tushamzoea yule na ana bahati kwa sababu Magomeni haina usiku, watu wanakesha hivyo vibaka hakuna.”

    Yule bwana akaifunua kanzu yake akatoa noti akamlipa yule muuza kahawa, akapewa chenchi yake na kutoweka kuelekea alipopajua yeye mwenyewe.

    Baada ya nusu saa akapita eneo lile lile kwa muuza kahawa akiwa amevaa bukta, na kofia kichwani, fulana nyeusi iliyoufanya mwili wake uonekane vyema kuwa ni wa mazoezi. Lakini akiwa gizani ilimfanya aonekane kama kivuli ama asionekane tofauti yake na giza.

    Naam! Mtu yuleyule lakini muonekano mwingine.

    Alikuwa ni Yakubu Gama.



    Hakusimama popote na alikuwa kama mwenyeji sana eneo lile. Akatembea usawa wa magari mengi yaliyoegeshwa eneo lile.

    Ukimya ulikuwa mkubwa sana hadi akaufikia ukuta ambao haukuwa mrefu sana.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kama afanyavyo paka, Gama akaruka na katika sekunde iliyofuata bunduki yake ilikuwa kiganjani akiwa amepiga goti, macho yake ya paka yakimsubiri yeyote ajikohoze na ayapokee mauti yake.

    Kimya! Hakuna aliyejitokeza.

    Na yeye hakujitikisa kwa sekunde takribani nne.

    Kisha akiwa amepiga goti vilevile alinyata kwa kuliruhusu goti jingine kupiga hatua na jingine kufuata.



    Akaufikia mlango wa kuingilia sebuleni, alipougusa na kujaribu kuufungua akasikia dalili ya kiumbe nyuma yake.

    Hakujiuliza mara mbilimbili, akafyatuka teke la punda kinyumenyume.

    Kiumbe nyuma yake kikabweka kwa maumivu.

    Wacha we! Mbwa mkubwa wa polisi alikuwa akitazamana na Gama huku hasira zikiwa zimemuwaka sana.



    Uzuri ni kwamba Gama hakuwa mgeni na mbwa wale! Alitambua kuwa mbwa wale sio wepesi kubweka na badala yake hurarua kimya kimya. Hii ilikuwa faida kwake kutoshtukiwa na watu kuwa yupo pale.

    Mara moja akafyatuka mzima mzima kisha akaunyoosha mguu wake barabara ukajikita katika shingo ya yule mbwa.

    Mbwa akalainika na kutua chini kwa kishindo kikubwa kishindo ambacho kilianza kuleta harufu ya vurumai. Kishindo kikamfikia mtu mwingine aliyekuwa macho katika nyumba ile.

    “Perry….. Perry…kuja kuja” sauti ya ikume ilisikika ikiita jina.

    Gama akatambua kuwa lile lilikuwa jina la mbwa.

    Kutokana na ukubwa wa yule mbwa Gama upesi upesi akajirusha na kujikunyata nyuma ya kule mbwa. Alifanya vile ili aweze kuipata shabaha yake vyema kama alivyokusudia wakati ule muitaji atakapofika.

    Naam yule muitaji akamkuta mbwa akiwa amelala chini kiubavuubavu..

    Kama alivyotaraji Gama kuwa yule bwana atafika kwa papara na kumwinamia yule mbwa ili ajue kulikoni.

    Hakika ilikuwa hivyo.



    Na katika ile sekunde aliyoinama naye Gama aliufyatua mguu wake ukajikita katika taya ya yule bwana, katika sekunde iliyofuata tayari alikuwa ameikaba shingo ya yule kiumbe.

    Ilifurahisha kutazama utaalamu wa Gama.

    “Nani wamo ndani?” aliuliza Gama.

    Jamaa akajipandikiza kiburi hakujibu!

    Gama akamjaza ngumi moja matata kiunoni, kisha akamziba mdomo.

    “Utanijibu sasa eeh!” akakoroma Gama.

    Lakini mara akausikia ubaridi ukipenya katika shingo yake. Akatambua kuwa ilikuwa ni bunduki.

    Gama akafyatua teke kinyumenyume upesi ili kumwadhibu mwenye ile silaha. Lakini mara akajikuta akipiga teke nguzo ya chuma.

    Na aliyeikamata ile bunduki akimtolea tabasamu la dhihaka.

    “Tulia hivyo hivyo kijana lasivyo nafyatua hicho kisogo chako!” sauti ya kike ikamuamrisha.

    Gama akafadhaika sana kukamatika kiulaini vile. Tena mbele ya mwanamke!!

    Akasalimu amri na mikono yake akanyoosha juu huku akili ikifanya kazi kubwa sana ya namna gani kuchomoka pale.

    Ghafla yule mwanamke ambaye hakuonekana kuwa na madhara zaidi ya kushika bunduki akafyatuka hewani kwa kushtukiza, na hapo Gama akapokea teke kali katika mbavu zake akalainika na kuangukia goti moja. Hakuamini kuwa yule alikuwa mwanamke.

    Dada yule akatulia kama sio yeye aliyeyemsulubu Gama.

    Hakufanania hakika!!

    “Naitwa Suzi… ni malikia wa nyumba hii samahani we ni nani mwenzangu.” Yule dada alimuuliza Gama kwa sauti nyororo huku amelegeza macho kana kwamba ni mpenzi wake. Gama alifura kwa hasira bila kujibu chochote.

    “Wewe ni nani katika ngome hii…. Elewa kwamba kunijibu ni lazima na kufa ni lazima vilevile, namaanisha utanipa jibu na utakufa vilevile.” Sauti ikasisitiza wakati huu ilikuwa ya kibabe. Gama akajaribu kuishughulisha akili yake lakini akajiona yu katika mtego mgumu sana. Aibu iliyoje kukamatika mbele ya mwanamke.

    “Wewe ni nani kijana shupavu mwenye mabaka kama chura…” yule msichana akahoji huku akipuliza hewani moshi wa sigara aliyokuwa akivuta. Na ghafla tena akatokwa na teke la haja, Gama akajaribu kupangua kwa mikono lakini akatupwa mbali akaangukia tumbo.

    Kimyakimya akakiri kuwa yule dada alikuwa amefuzu mafunzo fulani ambayo yaliondoka na hali yake ya usichana kiujasiri na kuvikwa uanaume wa shoka.

    “Nimesema kujibu ni lazima na kufa lazima ufe…”

    “Nyinyi ni nani wapumbavu nyinyi na mnajishughulisha na nini hapa…. Waoga wakubwa nyie m
 Waoga wakubwa nyie manalinda kwa mbwa na bado mnatumia risasi“ Gama akamkejeli yule dada ili kumtia hasira aje kwa pupa. Dada yule aliyejiita Suzi wala hakubabaika.

Kama kawaida yake akaiendekeza tabia yake ya uviziaji. Akaichukua sigara yake na kufanya kama anaisigina chini kwa sekunde moja na nukta iliyofuata akapaa mzimamzima, Gama akajaribu kukwepa lakini mapigo mawili ya nguvu yalikuwa yamemuingia usoni. Na alipokaa sawa na kutaka kurusha ngumi akakutana na ubaridi katika pua yake.
Bunduki!!!
“Sogea sentimita moja mbele, nyuma, pembeni ama popote pale na niisambaze pua yako vipande vipande dume la mbegu…” alikoroma yule msichana. Na hapo yule mwanamke mwembamba mrefu akaikoki vyema bunduki yake, hakuonekana kuwa kwenye mzaha hata kidogo.
Gama akaingiwa na uoga, akayafumba macho yake kuusubiria mlio wa risasi iwapo atausikia basi atakuwa yu hai bado na endapo hatausikia atakuwa amezimishwa!!
Badala ya kusikia mlio wa risasi, mara ghafla alishangaa anaangukiwa na yule msichana huku bunduki ikiruka mbali. Gama hakutaka kujiuliza kulikoni badala yake akatokwa na ngumi kali kupita zote alizowahi kuzipiga. Ilikuwa ni ngumi na kutoka katika kifo kuja tena kwenye uhai.
Akaipenyeza katika kitovu cha yule dada, Suzi akarushwa pembeni na kuanza kulia kama mtoto mdogo.
Gama licha ya kumfyatua yule dada pigo kali ambalo lilimaanisha kuwa hawezi kuamka ndani ya muda mfupi, bado hakujua ni kitu gani kilijiri hadi yule dada akaanguka ghafla na kupoteza uelekeo.
Gama akatulia na kuangaza huku na kule, mara akaisikia sauti iliyomshtua na kumweka katika mshangao wa muda mrefu kiasi.
“KOMBOLELA YAKUBU GAMA…”
Na hapo Gama akageuka akakutana ana kwa ana na mwanamke wa shoka akiwa anatabasamu.
Alikuwa ni mama lao!!
Gama hakuamini macho yake.

“Wakati wangu wa kupumzika bado sana. Naipenda sana kombolela, na ndo kama hivi nimebutua nimekuokoa…” Mama lao akamweleza Gama, na bila kupoteza muda wakamchukua yule dada ambaye alikuwa katika maumivu makali na kumtembezea kipigo cha haja!
Akaropoka kila kitu, Gama hakutaka kufanya makosa kama ambayo adui yake aliyafanya. Mara moja akaigeuza shingo yake na kuuondoa uhai wake.
Na hapo mama lao akaitambua ile sura kuwa ni ya yule dada ambaye alinunua mboga zote za majani siku ambayo mama lao kwa mara ya kwanza aliweza kuingia ndani ya kasri ile.
Gama alitambaa tena kiubavu ubavu bunduki yake mkononi akaufikia mlango, damu ilikuwa imechemka haswa. Maana alijiona ni mzuka uliofufuka ghafla.
Akaruka teke moja matata, mlango ukatikisika na kulegea. Aliporudi nyuma ili aruke teke jingine, mama lao alijirusha na kutumia makalio yake akaumalizia mlango.
Gama akajikuta anacheka mwenyewe!
Mama lao akajibu kwa tabasamu hafifu.
Ukimya ulikuwa mkubwa ndani ya nyumba ile, ni kama hapakuwa na mtu yeyote yule. Lakini mama lao alisisitiza kuwa mle ndani lazima kuna watu maana mboga alizonunua yule dada zilikuwa nyingi sana kiasi cha kuweza kutumiwa na walaji zaidi ya ishirini ama thelathini kwa kulizika kabisa.
Gama alikuwa amempigia saluti yule mama. Hivyo aliyaamini aliyokuwa akielezwa.
Msako ukaendelea kwa tahadhari kubwa sana, vyumba vya ile nyumba havikuonekana, ilionekana kama ghala tu.
Zaidi ya sebule ndogo ambayo chini palikuwa na magodoro. Hakuna kitu kingine cha ziada kilichoonekana.
Gama alianza kukata tamaa kuwa huenda wamecheza kombolela sehemu isiyokuwa sahihi na mtu aliyejificha hayupo eneo lile.
Mama lao naye akaingiwa unyonge juu ya kilichokuwa kinatokea pale.
“Inawezekana hakuna jipya humu!” Gama akazungumza na mama lao.

Lakini badala ya kupata jibu alishtushwa kuona mama lao akirusha na kutua kwenye kochi kubwa huku akitokwa na kelele ya uoga.
Bunduki ikakakamaa katika mkono wake tayari kwa pambano lolote.
Mara kabla hajafikiria kufyatua na yeye alivamiwa.
Akajikuta akikabiliana yule mbwa mkubwa ambaye awali alikuwa amezimia baada ya kupokea pigo tata kutoka kwa Gama.
Safari hii mbwa alikuwa na hasira zaidi.
Akawa juu ya mwili wa Gama huku akijiangaa kumng’ata, Gama naye akawa ameikamata shingo ya yule mbwa. Ikawa ni vita ya nguvu kwa nguvu.
Gama alimuhesabia sekunde yule mbwa kisha kwa ghafla akamrusha ukutani.
Ebwana ee!! Mbwa kwa uzito wake akaanguka na kubomoa ule ukuta wa ajabu.

Ebo! Haukuwa ukuta! Ilikuwa ni kipande cha mbao nyepesi kabisa kilichokuwa na rangi kama ya ukuta na baada ya kufunuka pale mara zikasikika sauti za watu zikinung’unika.
Bahati iliyoje kugundua hilo dakika za mwisho kabisa.
Sasa Gama alikuwa amesisimka zaidi, yule mbwa alivyojaribu kumvamia, mama lao alijikuta akipiga kelele kwa kudhania kuwa Gama ni mtu wa kawaida na atajeruhiwa na lile jibwa.
Gama badala ya kumtazama mbwa, ghafla akampa mgongo na kisha akaikunja ngumi yake katika nukta chache na kisha ghafla akageuka na kuituma ngumi ile katika mbavu za yule mbwa.
Mbwa akatokwa na kilio cha maumivu huku akijikunja pale chini.
Gama akammalizia kwa teke kali lililoondoka na uhai wake.
Mama lao akabaki nje wakati Gama akiingia katika kile chumba ambacho ,kilikuwa kimefichwa kama ukuta.
Hakika ya wanadamu waachie wanadamu!
Ni nani angeweza kugundua siri ile kirahisi!
Chumba katika pembe za ukuta??
Gama alimwachia mama lao bunduki, na kutaka kumpa maelekezo jinsi ya kutumia. Mama lao akatabasamu na kumpiga mgongoni Gama.
“Naitambua vyema SMG ni kama unataka kunifundisha kupika mtoto wa kiume wewe…”
Gama akaduwaa akazama mle ndani!
Tochi ikamuongoza hadi akazifikia nondo zilizokuwa zikiunda chumba kile.
“Nisamehe sitarudia naapa, nionee huruma mkuu nilikosea na sitadiriki tena, mnanionea jamani mimi sihusiki!” hizi ni sauti zilizosikika wake kwa waume zikilalamika.
Gama akamurika huku na kule hakuuona funguo!
Akawamurika watu waliokuwa wa,kilalamika.
Mungu wangu!! Akashtuka walikuwa ni watu wengi afya zao zikiwa zimedhoofu, wanaume kwa wanawake walikuwa wamechanganywa pamoja.
“Naomba utulivu wenu, msipige kelele. Nipo hapa kuwaokoa… naomba muwe kimya ili wote mtoke salama humu.
“Commando Gama wa Gama….” Mara akaisikia sauti ikimtambua. Akamulika tochi akamuona mwanaume amejiinamia chini, mara baada ya kumulikwa akaunyanyua uso wake ghafla.
LAHAULA!! Gama hakuamini macho yake!!
Alikuwa ni John Masele, waziri wa zamani wa mambo ya ndani na nje.

“Nilijua wapo vijana wanaoweza kupigania taifa lao. Wewe ni mmoja wapo.” Alijivuta kwa kutumia magoti, hakuwa anaweza kutembea na mikono yake ilikuwa dhaifu.
Gama hakutaka kupoteza muda akajipekua na kutoka na bunduki nyingine. Akawasihi wasipige kelele anafyatua lile kufuli.
Na pale akailenga shabaha lakini kabla hajafyatua akshtushwa na mlio wa risasi. Akasita na kukimbia hadi mlangoni huku bunduki yake ikiwa imara mkononi mwake.
Akamkuta mama lao akiwa anachokonoa meno yake kwa kijiti huku wasiwasi ukiwa mbali naye kabisa.
“Nini kimetokea..” aliuliza huku akiwa na wasiwasi.
“Hili jibwa lilijipindua kama linataka kusimama, na mimi nikajaribu kama risasi zipo…maana hukawii kunipa toi wewe.. wanaume mna maana basi..”
Gama akatikisa kichwa na kukiri kuwa yule mwanamke sio tu alikuwa na roho ya paka na kifua cha chuma kama alivyoagiza. Lakini huyu alikuwa zaidi ya alivyodhani.
Gama akatabasamu kisha akarejea na kufyatua lile kufuli! Geti dogo la chuma likafunguka.
“Gama.. mimi sitaweza kwenda popote pale, nitakuwa mzigo kwenu. Wamenipiga vibaya mno.. mno yaani, ninachokuomba kama hujaonana na yule mwandishi wa kuitwa Sam.. tafadhali kaonane naye ana mengi nimemwachia nenda akakupatie na uyafanyie kazi. Hii nchi imeoza, watawala wanatugeuza sisi watumwa wao. Pambane muupate uhuru wenu tena.” Alizungumza John Masele huku akitweta.

Gama hakuridhika na msimamo wa yule bwana lakini Masele alisisitiza vilevile.
Wale mateka wengine wapatao kumi wakatoka mmoja baada ya mwingine. Japokuwa palikuwa na giza lakini Gama alifanikiwa kukutana na sura moja ambayo haikuwa ngeni machoni pake.
Vijishimo vidogo katika mashavu yake vilimtambulisha upesi sana kwa Gama na hapa akaupigia mstari upelelezi wa jemedari mama lao. Licha ya binti yule kuwa amechakaa na kukondeana haswa lakini sura yake haikupotea.
Yule binti alikuwa ni Lilian, mpenzi wa mwisho kabisa wa Steven Marashi kabla hajapoteza uhai. Na ni huyu pekee aliyekuwa na jibu lililonyooka juu ya kifo cha Steven Marashi.
Gama akapata nguvu zaidi baada ya kumwona na hapo akaukumbuka mpangilio wa hisabati za shule ya msingi.
SWALI, KAZI, JIBU!!

Na hapo swali lilikuwa limetolewa, kazi imefanyika na lilibakia jibu tu kutoka kwa Lilian..
Mtihani ukawa mmoja tu namna ya kuwatoa watu wale nje ya geti lile salama bin salmin.
Wakati huo ilikuwa yapata saa nane usiku, Magomeni ilikuwa kimya kabisa kasoro sehemu moja tu. Lango la jiji huu ukumbi ilisikika mirindimo ya mziki wa pwani ikivuma.
Funguo ya geti ilisakwa bila mafanikio.
Gama alimwendea yule kijana ambaye alikuwa yu hai bado, yule ambaye alikuwa wa kwanza kukutana na pigo lake baada ya kuinama kumtazama mbwa aliyeanguka chini.
Gama alimmurika na kugundua bado yu hai. Akamuuliza maswali mawili matatu lakini yule kijana akaleta roho ngumu ya huko alipofundishwa kuwa na roho ngumu.
Gama aliendelea kuuliza kwa kulazimisha, yule bwana hakuwa tayari kusema. Wakati Gama akitafuta namna ya kumbana ili aweze kusema kumbe mama lao yeye alishawaza kabla yake. Akajisogeza mwanamke yule kama asiyekuwa na wazo lolote kichwani mwake huku akiyatikisa maungo yake kufuatisha mziki wa mwambao uliokuwa ukirindima. Mara ghafla kama amesetiwa akamfikia yule mwanaume pale chini. Akaupeleka mkono wake katika sehemu zake za siri akazikamata kisha akaanza kumnyanyua kuja juu.
Ebwana eeh! Jamaa akapiga yowe kubwa mno. Yowe lililomshtua hadi Gama mwenyewe. Halafu kwa kutumia ishara mama lao akamuuliza ni wapi zipo funguo.
Akalegeza kidogo mkono, jamaa akaelekeza mahali zilipo kiustadi kabisa. Gama akazichukua funguo na kuliendea geti na kufungua. Geti likaachia, wakati analifungua akamwona yule mlinzi mlevi akitembea huku anayumbayumba. Hakujua linaloendelea eneo lile.
Mama lao hakusubiri kila kitu kifanywe na mwanaume. Akaingia garini, akafungua milango na kuwaruhusu wale mateka wote kuzama garini. Wakaingia wote kwa kubanana na mlango ukafungwa.
Kabla ya kuondoka Gama alirejea tena kule chumbani na kumsihi tena John Masele waondoke wote lakini mzee alikataa, badala yake akamuita Gama na kumnong’oneza.
Gama akaelewa akatoweka!!



LICHA ya kuwa amepokea kipigo kikubwa sana ambacho kilikuwa ni sawa na kuua nyoka, bado John Masele alikataa kata kata kuwa hajawahi kukutana na mwandishi wa habari aitwaye Sam na wala hajui chochote kuhusiana na BvB.
Alipinga licha ya ukweli kuwa waliwahi kukutana na akazungumza naye na kumpatia nyaraka tata.
Masele alipinga kwa sababu alijua hata akisema bado mabaradhuli wale watamuua tu na kisha kumwahi Sam kabla hajatumia zile nyaraka kuwavumbua waovu. Ilikuwa heri afe lakini akiacha harakati zikiendelea nyuma yake.
Kitendo cha mzee Matata kuleta kiburi kilimkera sana raisi. Akaona kuwa ile ni dharau ya hali ya juu, alitambua kuwa anaweza kumpiga risasi na kumuua mara moja, lakini kwake yeye furaha isingekamilika. Badala yake akawasiliana na BvB na kumwomba huduma ya vijana wake kadhaa wanaojua nini maana ya kuua mwanadamu yeyote kwa mateso makali. Akamsihi tena kuwa hakuhitaji afe upesi, alihitaji afe kwa hatua. Ikiwezekana hata ndani ya siku kumi za mateso nd’o aruhusiwe kufa.
____

Raia wa kizungu wanne walipokelewa uwanja wa ndege wa kimataifa wea mwalimu Nyerere. Ugeni huu ulipokelewa na wafanyakazi kutoka ikulu, hivyo baada tu ya kuwasili walipelekwa hoteli ambayo ilikuwa imelipiwa kwa ajili yao.
Waliwasili majira ya saa nne asubuhi!
Muda uleule walipelekwa hotelini na hawakutoka tena hadi ilipotimu saa tisa usiku.
Kazi iliyowaleta kutoka huko walipotoka ni moja tu, kumbana John Masele ili aweze kusema iwapo aliwahi kukutana na Sam ama la!
Na ajieleze zaidi iwapo walikutana ni kitu gani alimpatia!
Hawa wazungu kutoka uholanzi waliaminika kwa kazi yao ya kuadabisha mateka wao. Walikuwa na roho mbaya sana zisizokuwa na huruma hata kidogo. Kuua kwao ilikuwa kama kichekesho tu, ni wazungu hawa ambao mzee Matata alikuwa na video zao na alimuwekea Tina ili kumtisha siku ile. Walikuwa wanatesa na kuua vibaya mno.
Wakiongozwa na dereva waliyekabidhiwa wakiwa kimya kabisa huku wakipuliza sigara kila mmoja. Hatimaye walifika magomeni.
Nyumba ambayo John Masele alikuwa amehifadhiwa.
Walifika na kubisha hodi lakini mfunguaji alichelewa. Wakabisha tena na hapo akafika na kuwafungulia geti haikuwa mara yao ya kwanza kufika katika ngome kadha wa kadha za namna ile.
Wakapita moja kwa moja hadi ndani, dereva akabaki nje na baada ya wao kuingia ndani na yeye akatoweka kwenda mahali alipopajua yeye kwa sababu tayari aliambiwa kuwa hawatatoka mapema. Na wanaweza wasitoke humo ndani kwa siku hiyohiyo. Hakujua hata walichokuwa wakikifuata mle ndani wanne wale.

Walipoingia ndani wakaenda moja kwa moja katika ule ukuta wakataka kupenya lakini wakashtushwa na utofauti wa maelezo waliyopewa awali juu ya mazingira ambayo yapo eneo lile.
Mzungu mmoja akatoa simu yake na kisha kutoka nje ili aweze kupiga.
Alipotoka nje akaenda kwa mlinzi ili aweze kuzungumza kwa lugha ya Kiswahili na wale mabwana wahusika wa ile ngome.
“Hey! Do you speak English?” mzungu akamuuliza mlinzi.
Yule mlinzi akajibu kuwa anaweza.
Yule bwana akabofya namba kadhaa na kutaka kumpatia yule mlinzi simu. Mlinzi akanyoosha mkono wake kuipokea ile simu. Lakini hakuchukua simu pekee.
Akaufyetua ule mkono wa mzungu na kuuvunja huku mkono wake mwingine ukiuziba mdomo wa yule bwana. Kisha akamvutia nyuma ya nyumba.
Akaitoa kofia yake na kuanza kumuhoji yule bwana kwa kiingereza.
“Who the https://jamii.app/JFUserGuide are you?” ilikuwa sauti ya Gama iliyo katika ghadhabu kuu.
Yule bwana hakujibu, Gama hakupoteza muda kuzungumza na bubu. Akatoa pigo kali la kareti katika mbavu za yule bwana, hata sauti hakuweza kutoa alibaki kugumia kwa maumivu.
“Who are you bastard!” akamuuliza tena huku akimwonyesha wazi kuwa anataka kutoa pigo jingine.
Mwanga hafifu wa taa ulimmulika mzungu yule ambaye alikuwa mwekundu huku sura ikiwa imemvimba.
“BvB” akatokwa na kauli ile. Kisha akatulia kimya!
Ni aidha alikuwa amepoteza fahamu ama kifo kabisa.
Upesi Gama akaondoka na kuelekea katika kile chumba ambacho walikuwa wamesalia wazungu watatu wakingoja maelekezo zaidi.
“Me, you zea” alizuga kuzungumza kiingereza kibovu Gama, hapa akiwa amevaa tena kofia yake na kufanana na mlinzi.
Mzungu mmoja akatoa kauli kuamriosha mmoja wao aende kutazama mwenzao anasema nini.
Naam! Ramani ya Gama ikaenda kama alivyokuwa anahitaji.
Akamwongoza hadi nje, na kumpeleka nyuma ya nyumba. Akafika na kumwonyesha mwili wa mwenzake.
Hakumpa muda wa kushtuka sana, akamvamia kwa kiwiko akaivunja pua yake.
Mzungu akataharuki na akataka kupiga kelele lakini alichelewa, Gama alifyatua kisu alichokuwanacho kikajikita katika shingo ya yule kaburu.
Kisu kilikuwa na sumu kali. Gama hakugeuka nyuma tena kutazama jinsi atakavyokata roho.
Sasa hakuvaa kofia bali aliingia tena moja kwa moja katika kile chumba.
“You bastard where are you from and who the hell is BvB” aliwauliza huku akiwa anawakabili machoni.
Wakamtazama kwa jicho la hofu wasijue ni kitu gani kinaendelea.
Mmoja akajaribu kumsogelea lakini hakufika mbali ukasikika mlio wa bunduki, alipogeuka alimshuhudia mwenzake akiangukia kichwa huku kisogo kikiwa kinavuja damu.
“Kombolela mzungu..” Sauti ikasikika kisha tena bunduki ikakohoa na kuvunja miguu ya yule bwana aliyebakia.
Na hapo John Masele akajitokeza huku akiwa anajivuta kwa magoti na tabasamu tele mdomoni mwake.
Mchezo walioupanga ukawa umekamilika!
Gama alikuwa amemshirikisha John Masele juu ya kombolela, na pale walikuwa wakilicheza.
“Utajibu maswali yote kwa hiari ama kwa lazima ikibidi?” Gama akamuanza yule mzungu pekee aliyebaki akiwa hai.
Yule mzungu hakujibu kitu Gama. Akatoka nje kisha baada ya dakika zipatazo kumi akarejea tena, mikono yake ikiwa imetapakaa damu na mkononi akiwa na vichwa viwili vya wazungu. Akavirusha mbele ya yule mzungu mbishi.
Hakika alipagawa!
“Do you love hell??” Gama akamuhoji. Na hapo hapo akanyanyua vidole vyake juu, kisha akavishusha katika kichwa kimojawapo katika pigo la ‘finga’ na hapo akachomoka na macho kutoka katika kile kichwa. Akayarusha mbele ya yule mzungu.
“I will chop your eyes while you are alive” akamkoromea huku akimsogelea. Kitete kikamkumbuka yule mzungu.
Mzungu akajibu kila alichoulizwa huku akiwasihi wasimuue kwa sababu yeye ni mjumbe tu.
Akamtaja BvB kuwa ndiye bosi wao na siku iliyokuwa inafuata alitarajiwa kuanza safari ya kuja nchini Tanzania kufuatilia maendeleo ya miradi yake na kubwa zaidi kuitazama ardhi kubwa yenye madini ambayo alipewa zawadi na raisi wa Tanzania kutokana na ukaribu wa kimisaada aliokuwa akimpatia.
Yule mzungu hakusubiri kuambiwa aseme nini maana ya BvB aliitafsiri mwenyewe na kisha akamtaja mzee Matata kama kijakazi wa BvB nchini Tanzania.
Gama alivyotaka kuujua muonekano wa BvB, mzungu yule aliapa kuwa hajawahi kumtia machoni bwana yule hata siku moja katika maisha yake.
“Imelaaniwa ardhi hii” John Masele alijisemea baada ya maelezo ya yule mzungu.
Gama akamkonyeza kwa jicho la kuume. Akatambua nini kinamaanishwa.
Na hapo akafyatua risasi, yule mzungu akabweka na kupoteza uhai. Gama akamchukua John Masele katika mgongo wake kisha akatoka naye nje kwa tahadhari kubwa.
Akampita yule mlinzi mlevi na kutokomea gizani zaidi!
_____

WAKATI Gama Yakubu akihangaika kupenya katika njia ambazo ni salama kwake pasipo kuonekana. Mama lao alikuwa akiichochea moto zaidi ile gari aina ya Noah ambayo aliichukua nyumbani kwa waziri usiku ule.
Wale mateka ambayo walikuwa wanaelekea kuwa huru walikuwa katika maombi mazito kila mmoja akimshukuru Mungu kwa namna yake ya kipekee. Lakini Lili alikuwa mtu wa kulia tu.
Mama lao akiwa ndani ya pensi aliendesha gari kuitafuta Kibaha kama ambavyo walikuwa wamekubaliana na Yakubu ambaye alibaki nyuma kwa ajili ya kuimalizia kombolera yake.
Mitaa ya Kimara na ubungo bado ilikuwa imechangamka changamka licha ya kuwa ulikuwa usiku mnene. Hapo alipita bila wasiwasi wowote.
Lakini shughuli ikawa pevu walipofika mlima wa kibamba kuelekea Kibaha.
Gari ya akina mama lao ilisimamishwa katika namna ya kipekee.
Mawe yalikuwa yamepangwa barabarani!
Watekaji! Mama lao alisema kwa sauti ya kuhamanika, na hapo kila mateka akazidisha maombi yake.

Mama lao alijua kwa namna yoyote ile hawezi kuvuka kikwazo kile na ilikuwa lazima asimame. Aliwaona watekaji wake wakiwa na mapanga na marungu.
Akapunguza mwendo na kusimama!!
Watekaji wakasogea hadi pale garini.
“Mwanamke… tunakupa dakika moja na sekunde mbili.. uwe chini na wote waliomo humu wawe chini na kisha mpotee mbele ya macho yetu… ubakishe funguo pekee humo ndani.” Amri ilitoka.
Mama lao akawageukia mateka wake akatazama namna wanavyomtazama kwa jicho la huruma na wengine wakiwa wamekata tamaa.
“Mnaijua kombolera…. Lili umewahi kucheza kombolera?” aliwauliza na kisha akamgeukia Lilian.
Lili akatikisa kichwa kumaanisha kuwa amewahi kucheza.
“Ili umuokoe mwenzako unatakiwa kufanyaje?”
“Mbona sikuelewi mama…..” alilalamika Lili.
“Sijakuuliza kama unanielewa jibu swali binti…”
“Unabutua….”
“Vizuri sana… unabutua…” mama lao akarudia jibu lile huku anacheka. Kisha akawaambia wasishuke garini anaenda kubutua.
Wakati mama lao anashuka kutoka garini alikuwa anajiona kama yu katika tukio ambalo aliwahi kuwa awali. Lakini tofauti ilikuwa moja tu tukio la awali lilitokea jijini Mwanza, ambapo katika utafutaji wake akiwa bado anatawaliwa na ujana aliangukia katika penzi la kijana mwenye pesa. Naam! Tangu akiwa mdogo alikuwa akitamani kuolewa na mtu mwenye pesa akidhani zile pesa hujileta zenyewe.
Baadaye kabisa penzi likiwa limekolea akajitambua kuwa amezama katika penzi la jambazi aliyekubuhu na hawezi kutoka tena.
Akakubaliana na hali, akafundishwa kushika bunduki na kuitumia, akafundishwa kuwa na roho mbaya inapobidi, akafundishwa kurusha mateke na kupiga ngumi!
Naam! Mama lao akawa mtu mwingine, na hatimaye akaanza kuandamana na mpenzi wake kwenda kuteka magari.
Wao walikuwa wakifanikiwa sana kutokana na mbinu walizokuwa wakizitumia, hii mbinu ya kuweka mawe barabarani mpenzi wake yule ambaye baadaye aliuwawa kwa risasi aliziita mbinu za kishamba. Na aliwahi kumweleza mama lao kwanini mbinu zile ni za kishamba na mama lao akazielewa.
Sasa mama lao naye ametekwa katika mbinu za kishamba hayupo pamoja na marehemu mpenzi wake sasa yu mwenyewe, kwanini asicheke, kwanini asitabasamu wakati anatambua kuwa washamba nd’o wanaojaribu kumteka.
Dhumuni kuu la mama lao kushuka chini peke yake ilikuwa ni kuhakikisha iwapo walimteka wana silaha ama vipi.
Macho yake makali yakapenya katika giza lile jepesi, kwa mbali akamuona mtu mwingine amesimama huku akivuta sigara, hakutazama mara mbili akawa katika marudio akatambua kuwa yule aliyesimama mbali ndiye ambaye huwa anakuwa na bunduki. Na mara zote ndiye huwa kiongozi wa msafara, mama lao akauchuna kama hajamuona lakini kichwani akikiri kuwa marehemu Swebe mpenzi wake alikuwa anajua mambo mengi sana.
Hapa akawa anaishi katika dunia mbili tofauti, kichwani alikuwa makini kuwatazama adui zake lakini kwa nje alionyesha ule uoga wa kike. Akawalaghai wale ‘washamba’ kuwa yeye ni mwanamke wa kawaida.
Wakawa wanamkemea huku wakicheka, walidhani ni mwanamke kweli.
Wakiwa bado wanamdharau mama yule aliyekuwa akiwaomba msamaha. Mara likatokea tukio ambalo huenda watasimulia kwa vizazi vyao vya majambazi ‘washamba’.
Kwa kushtukiza kabisa kama ilivyo katika filamu za mapigano kwa kutumia silaha. Mama lao akaangukia magoti kama anayeomba msamaha, upesi mkono wake mmoja ukaingia kiunoni, na sekunde iliyofuata akawa na bastola mkononi, akafyatua moja kwa moja kumwelekea yule aliye mbali akampata kifuani. Jamaa akarushwa mbali, mama lao hakutaka kujiuliza iwapo amekufa ama la.
Sekunde inayofuata bastola yake ikawa inawatazama wawili wale. Sas ikawa zamu yake kutabasamu na wale jamaa kuanza kubabaika.
“Wee! Thubutu kukimbia na uwe umekimbia milele mbwa nyie…” akawapia mkwara. Kisha akatoa amri upesi.
“Mnayatoa haya mawe kwanza ndani ya dakika moja na sekunde mbili kisha mnapotea machoni kwangu mara moja!! Upesi.”
Mara moja wawili wale wakaanza kuyaondoa mawe kama walivyoamrishwa, huku wakitetemeka. Ndani ya gari Lili ambaye muda wote alikuwa anachungulia kinachoendelea, akajikuta kwa mara ya kwanza akitabasamu.
Barabara ilivyokuwa safi. Mama lao akawatazama wawili wale ambao waliogopa kuondoka bila kuruhusiwa. Kisha akawarushia neno lililowashangaza.
“Kombolela majambazi!”
Akaruka garini na kuitia moto gari. Safari ikaendelea kwa amani kana kwamba hakuna kilichotokea!
Kila mmoja garini alibaki kujiuliza juu ya yule mwanamama.
Hawakupata majibu!!

****

ASUBUHI SANA eneo la magomeni lilijaa umati wa watu, kila mmoja alikuwa akiongea neno ajualo yeye juu ya kile alichokuwa akikiona.
Vichwa vinne vya wazungu vilikuwa nje ya geti la nyumba iliyosadikika kuwa ni ya mheshimiwa waziri wa nishati na madini.
Simu zilipigwa kituo cha polisi cha Usalama magomeni, na punde askari walifika na kujawa na mshangao juu ya jambo lile.
Simu za upepo zikafika makao makuu, na hatimaye mezani kwa Robert Masawe.
Alipigiwa simu na IGP kuelezwa kuhusiana na tukio lile la kutisha tena katika nyumba ya waziri.
Robert Masawe alitamani amweleze IGP juu ya uozo unaoendelea chinichini maana alimuona ni mtu anayetumikia kitu asichokijua. Lakini hakuwa radhi kujaribu kumweleza badala yake alichukua ile taarifa kama taarifa nyingine kisha aingie katika utendaji.
Wakati anakata simu alisimama akapiga saluti huku akiwa peke yake.
Kisha akajisemea “Umelaaniwa mkono wa GAMA….”
Kisha akafanya tabasamu hafifu la matumaini.

WAKATI tukio hili likiendelea, hali ya waziri wa nishati na madini, bwana Mathias Obhare ilikuwa mbaya sana, shinikizo la damu lilikuwa limepanda. Alikuwa amechanganyikiwa kabisa na hakujua ni nani aliyepenya na kuingia katika ngome ile na kufanya yale yote aliyoyafanya.
Taarifa ya maaskari ilitaja kukutwa pia miili ya waafrika wawili ikiwa haina uhai na mbwa aliyepigwa risasi pia akiwa hana uhai.

Si waziri peke yake aliyekuwa amepagawa bali raisi wa nchi alikuwa hajielewi kabisa. Alipiga simu uholanzi kutaka msaada lakini bahati mbaya simu ya Benson van Bronchost haikuwa ikipatikana.
Alisahau kabisa kuwa bwana yule alikuwa safarini kuja Tanzania.
Waandishi wa habari wakaanza kuandika mambo wanayohisi bila kuwa na uhakika nayo.
Wakaandika waziri ameua, wakaandika waziri anajihusisha na umafia na mengineyo mengi huku wengine wakienda mbali zaidi na kutaja kuwa ni vita ya kuelekea ikulu inaondoka na damu za watu.
Tamko la mkuu wa majeshi ya polisi likasubiriwa.
Na hilo lilikuja baada ya siku moja!
Akiwa ameagizwa na raisi kusema hivyo, IGP akazungumza nje kabisa ya utashi wake. Mmoja kati ya watu waliokuwa katika mkutano ule japokuwa kwa siri kubwa alikuwepo Sam ambaye alitoka katika maficho yake baada ya kusikia habari juu ya wazungu wanne na waafrika wawili kuuwawa katika nyumba ya waziri.
“Aliyekuwa waziri wa mambo ya ndani na nje ya nchi, bwana John Masele aliyekamatwa na silaha za moto, ametoroka mikononi mwa polisi wakati akihamishwa gereza la mahabusu. Serikali inamshuku kuhusika na mauaji yaliyotokea katika nyumba ya waziri Obhare. Msako mkali unaendelea dhidi yake.”
Taarifa ile ilipokewa kwa namna tofauti tofauti na waandishi wa habari. Wengi walinung’unika kuwa ilifanana na taarifa ya kupikwa lakini IGP hakujibu swali lolote lile.
Huo haukuwa mwisho wa utata!!
Sam akatabasamu huku akiitazama picha zilizokuwa mkononi mwake akazifananisha na vile vichwa vilivyopigwa picha na kuwekwa magazetini. Picha zilifanana kabisa na zile alizopewa kule kijijini na John Masele ambaye sasa anashutumiwa kuwa ni muuaji.
“Wajinga ndio waliwao… siku zenu zinahesabika!” Sam akasema kwa sauti ya chini huku akiondoka zake.


Ili kuupaka umma mafuta kwa mgongo wa chupa serikali ikamwongezea ulinzi waziri yule. Huku nyumba ambayo yalitokea mauaji yale nayo ikilindwa na wanajeshi ambao walikuwa wakipishana kila baada ya masaa manne.
Mathias Obhare naye akawa mtu wa kulindwa kila sekunde.
Nafsi yake haikuwa na amani hata kidogo, alitamani kuubadilisha ukweli uliokuwa unamkabili lakini haikuwezekana kufanya vile tena. Mambo yalikuwa yanaanza kuwakaa kooni yeye na raisi kutokana na hila zao.

Upande wa raisi, yeye alibaki katika fumbo kuu akiwafikiria wazungu wale walivyouwawa. Akiachilia mbali wale wazungungu, akamfikiria Suzi yule mwanadada mashuhuri ambaye aliaminika kuwa na roho saba.
Ni nani aliyeuondoa uhai wake kirahisi namna ile tena pasipo kutumia silaha? Hili jambo lilimvuruga raisi na ile hali ya Benson kutopatikana hewani basi alivurugika kupita maelezo.
Alitamani kumweleza mkewe juu ya wakati aliokuwa akipitia lakini akashindwa ni wapi angeanzia kwa sababu hata siku moja hakuwahi kumweleza juu ya hila zake serikalini na ubadhilifu aliokuwa akiufanya kwa kuwaruhusu wanyonyaji kula matunda ya nchi kuliko wazawa.
Hatia ikamsulubu, akajaribu kupambana na hali ile lakini hakuweza.
Akachukua simu yake na kumpigia mtu maalumu na kukatisha kikao cha bunge alichopanga kwenda kuhutubia.
Na baada ya pale akampigia simu IGP.
“Mkuu… una uhakika kuwa hakuna vijana wanatusaliti katika kambi ya usalama wa taifa…”
“Sijaelewa unamaanisha nini mkuu..” IGP alijibu.
“Haya mauaji we unayachukulia ya kawaida haya…. Wale wazungu na yule Suzi..” alijieleza Rais.
“Mkuu kwani unawafahamu hao watu..” IGP akahoji. Na wakati ule akatambua kuwa raisi alikuwa anatetemeka. Alama ya kuuliza ikajiunda katika kichwa chake.
Hao ni akinanani kwa raisi na wana mstakabali gani hadi awe katika hali ile.
“Mhh! Hapana siwafahamu lakini Obhare anaweza kuwa anawafahamu naamini…” alijikanganya raisi kisha upesi akakata simu.
IGP akaanza kuingiwa na mashaka.
Na hapo akajaribu kuwasiliana na mrakibu mkuu Robert Masawe na kumweleza iwapo amepata fununu zozote juu ya mauaji yale.
Robert akapiga fumbo.
“Inasadikika wameuwawa na watanzania wa kawaida ambao wamechoka kunyonywa….”
“Una maana gani na nani amesema.”
“Mkuu nimesema inasadikika, hivyo ni sisi kusadiki ama la!” akajibu mrakibu.
IGP akakata simu huku akizidi kuchanganyikiwa!!
Akabaki kujiuliza juu ya maneno ya Mrakibu msaidizi, kisha akahusisha na hali ya raisi.
Kuna kitu!!! Akapigia mstari.

****

NGUVU YA PENZI!!

USIKU wa mang’amung’amu ulimwandama Sam. Alijitazama kama kijana mzembe sana licha ya makwazo kadhaa aliyopitia.
Alizikumbuka ahadi tele ambazo alizipanga na Tina. Alikumbuka namna ambavyo kila mmoja aliapa kuwa yupo tayari kufa kwa ajili ya mwenzake.

Ajabu yeye Sam alikuwa nyumba ya kulala wageni ya bei ya chini kabisa maeneo ya Machimbo nje kidogo ya jiji la Dar es salaam. Alijiona yu mjinga kujificha ili asife wakati mtu ambaye walipanga naye ahadi kedekede alikuwa matatani. Na hakujua hata kama alikuwa yu hai ama amekufa tayari.
Wakati akiyafikiria hayo mara akamfikiria na mzee John Masele. Kuna maneno ambayo alimweleza na sasa akajiona kuwa ni msaliti muoga tena asiyejiamini.
Yale maneno yakajirudia kwa kasi kubwa kichwani mwake.
“Sam naona unatetemeka bila shaka kuna baridi sana huku kwetu..” John Masele alimuuliza Sam huku akiwa anatabasamu.
“Dah! Mzee huku ni tatizo kabisa hili baridi la Mafisa ni hatari sana, Iringa haioni ndani….” Sam alijibu.
“Sam unahisi ili baridi lipungue unahitaji nini…”
“Mzee hapa ni sweta zito kabisa nd’o linaweza kuleta nafuu” Sam akajibu, John Masele akacheka kidogo kisha akaendelea.
“Hivi umewahi hata siku moja kuzungumza na Sweta lako na kulishukuru kwa kukulinda kwa baridi?”
“Aaah! Mzee wangu lile sweta ni langu ya nini mimi kulishukuru sasa.. ule ni wajibu wake kunilinda mimi…” Sam akajibu huku akimshangaa John Masele.
“Safi sana Sam, ehe! Na vipi sweta lako likichakaa…”
“Naachana nalo nanunua jingine…”
“Ooh! Umejibu vizuri sana Sam. Ninachomaanisha hapa kijana wangu, wewe ni sweta kwa watanzania Sam, unatakiwa uwalinde watanzania pasipo kusubiri kupewa shukrani ama kupewa pesa kama wanavyotaka wengine. Au kupigiwa makofi kama ilivyo asili ya wapuuzi wengi, wewe sio mpuuzi Sam na usikubali kuwa mpuuzi ishi kama sweta. Kawasaidie watanzania, usisubiri watoe shukrani, na katika kuwasaidia huko utambue kuwa unaweza kuchakaa, unaweza kufa. Ukifa wewe utakuwa umetanua njia kwa masweta mengine mapya kuwalinda watanzania wasitetemeke kwa baridi, usiogope kufa Sam. Maana waliotupa uhuru wa bendera na wao walikufa sasa ni zamu yetu kuupata uhuru wetu…”
Haya yalikuwa maneno ya John Masele usiku ule alipozungumza na Sam. Sam akajikuta katika aibu, kwanza akamfikira mpenzi wake, pili akatii maneno ya John Masele.
Akakurupuka kutoka kitandani, akasimama wima na kujiuliza atalala na kujificha mpaka lini? Na ni nani ambaye atampigania ikiwa yeye hajaamua kujipigania.
.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/Sam akavinyoosha viungo vyake kisha akajisemea.“Mimi ni sweta na kesho naanza kazi rasmi.”Akarejea kitandani na kusinzia.Asubuhi akatazama kiasi cha pesa alichobaki nacho kilikuwa kinatosha kwa harakati alizokuwa amezipanga.Majira ya saa nne asubuhi Sam alikuwa katika ‘stationary’ moja isiyokuwa na watu wengi. Alikuwa ameketi mwenyewe kwenye kompyuta akitengeneza kitambulisho ambacho alipanga kwenda kukitumia mahali.Alitumia muda wa saa zima kukitengeneza kisha akakichapisha na kuondoka zake akiwa amelipia huduma ile.Sam akiwa amevalia suti yake nyeusi, miwani myeusi ya jua na kofia pana kichwani alichukua pikipiki ambayo ilimpeleka moja kwa moja maeneo ya Kurasini. Akashukia mbali kidogo na eneo alilopanga kwenda. Akapokelewa na mlinzi akajiandikisha jina lake na kuruhusiwa kuingia ndani.Kisha akatembea kwa miguu, akafanya dua fupi kisha akaingia katika ofisi za mkuu wa shule ya sekondari ya kimataifa iliyokuwa pale.Akasalimia huku akiwa amesimama kisha akatoa kitambulisho chake na kukionyesha mara moja kisha akajitambulisha kwa jina.“Inspekta Babu kutoka kituo cha kati, amri kutoka kwa IGP, Suzan anatakiwa kuwekwa mahali salama muda huu kwa usalama wake. Tafadhali namuhitaji sasa hivi, samahani kwa usumbufu ni amri kutoka kwa IGP…” Sam aliunguruma huku miwani yake ikiwa ipo bado machoni huku akiwa amekakamaa mithiri ya askari.Ama! Mwandishi wa habari ni muigizaji pia!Mkuu wa shule alitetemeshwa na ujio ule wa Sam ambaye mafunzo ya JKT aliyoyapitia yalikuwa yamemjengea uimara sana. Akafanana kabisa na askari.Pasipo kupoteza muda, mkuu yule wa shule alimuita mwanafunzi mmoja na kumuamuru amuite Suzan upesi.Punde msichana mrembo umri usiozidi miaka kumi na tano alikuwa mikononi mwa Sam. Sam alitembea kwa tahadhari kubwa huku akitazama kushoto na kulia kana kwamba kuna hatari yoyote anayojaribu kupambana nayo.Mkuu wa shule alibaki kuduwaa asijue ni kitu gani kibaya alitaka kufanyiwa mtoto yule hadi amri ikatoka kwa IGP upesi kiasi kile. Akabaki kutikisa kichwa asijue la kufanya!Sam akatokomea akiwa na yule binti mrembo!Siku iliyofuata taarifa zikatapakaa katika vyombo vya habari juu ya kutekwa kwa mtoto wa IGP.Mtekaji hakuwa akifahamika, zaidi ya kutumia jina feki, ‘Inspekta Babu’.Nchi ikaingia katika kizunguzungu kipya!!Na hapa ndipo mpasuko ulipoanzia!!Mpasuko wa aina yake!!!****Kwa kushtukiza kabisa kama ilivyo katika filamu za mapigano kwa kutumia silaha. Mama lao akaangukia magoti kama akanyeomba msamaha, upesi mkono wake mmoja ukaingia kiunoni, na sekunde iliyofuata akawa na bastola mkononi, akafyatua moja kwa moja kumwelekea yule aliye mbali akampata mguu.Sekunde inayofuata bastola yake ikawa inawatazama wawili wale.“Wee! Thubutu kukimbia na uwe umekimbia milele…” akawapiga mkwara. Kisha akatoa amri.“Mnayatoa haya mawe kwanza ndani ya dakika moja na sekunde mbili kisha mnapotea machoni kwangu mara moja!! Upesi.”Mara moja wawili wale wakaanza kuyaondoa mawe kama walivyoamrishwa, huku wakitetemeka.Barabara ilivyokuwa safi. Mama lao akawatazama wawili wale ambao waliogopa kuondoka bila kuruhusiwa. Kisha akawarushia neno lililowashangaza.“Kombolera majambazi!”Akaruka garini na kuitia moto gari. Safari ikaendelea kwa amani kana kwamba hakuna kilichotokea!Kila mmoja garini alibaki kujiuliza juu ya yule mwanamama.Hawakupata majibu!!****ASUBUHI SANA eneo la magomeni lilijaa umati wa watu, kila mmoja alikuwa akiongea neno ajualo yeye juu ya kile alichokuwa akikiona.Vichwa vinne vya wazungu vilikuwa nje ya geti la nyumba iliyosadikika kuwa ni ya mheshimiwa waziri wa nishati na madini.Simu zilipigwa kituo cha polisi cha Usalama magomeni, na punde askari walifika na kujawa na mshangao juu ya jambo lile.Simu za upepo zikafika makao makuu, na hatimaye mezani kwa Robert Masawe.Alipigiwa simu na IGP kuelezwa kuhusiana na tukio lile la kutisha tena katika nyumba ya waziri.Robert Masawe alitamani amweleze IGP juu ya uozo unaoendelea chinichini maana alimuona ni mtu anayetumikia kitu asichokijua. Lakini hakuwa radhi kujaribu kumweleza badala yake alichukua ile taarifa kama taarifa nyingine kisha aingie katika utendaji.Wakati anakata simu alisimama akapiga saluti huku akiwa peke yake.Kisha akajisemea “Umelaaniwa mkono wa GAMA….”Kisha akafanya tabasamu hafifu la matumaini.WAKATI tukio hili likiendelea, hali ya waziri wa nishati na madini, bwana Mathias Obhare ilikuwa mbaya sana, shinikizo la damu lilikuwa limepanda. Alikuwa amechanganyikiwa kabisa na hakujua ni nani aliyepenya na kuingia katika ngome ile na kufanya yale yote aliyoyafanya.Taarifa ya maaskari ilitaja kukutwa pia miili ya waafrika wawili ikiwa haina uhai na mbwa aliyepigwa risasi pia akiwa hana uhai.Si waziri peke yake aliyekuwa amepagawa bali raisi wa nchi alikuwa hajielewi kabisa. Alipiga simu uholanzi kutaka msaada lakini bahati mbaya simu ya Benson van Bronchost haikuwa ikipatikana.Alisahau kabisa kuwa bwana yule alikuwa safarini kuja Tanzania.Waandishi wa habari wakaanza kuandika mambo wanayohisi bila kuwa na uhakika nayo.Wakaandika waziri ameua, wakaandika waziri anajihusisha na umafia na mengineyo mengi huku wengine wakienda mbali zaidi na kutaja kuwa ni vita ya kuelekea ikulu inaondoka na damu za watu.Tamko la mkuu wa majeshi ya polisi likasubiriwa.Na hilo lilikuja baada ya siku moja!Akiwa ameagizwa na raisi kusema hivyo, IGP akazungumza nje kabisa ya utashi wake. Mmoja kati ya watu waliokuwa katika mkutano ule japokuwa kwa siri kubwa alikuwepo Sam ambaye alitoka katika maficho yake baada ya kusikia habari juu ya wazungu wanne na waafrika wawili kuuwawa katika nyumba ya waziri.“Aliyekuwa waziri wa mambo ya ndani na nje ya nchi, bwana John Masele aliyekamatwa na silaha za moto, ametoroka mikononi mwa polisi wakati akihamishwa gereza la mahabusu. Serikali inamshuku kuhusika na mauaji yaliyotokea katika nyumba ya waziri Obhare. Msako mkali unaendelea dhidi yake.”Taarifa ile ilipokewa kwa namna tofauti tofauti na waandishi wa habari. Wengi walinung’unika kuwa ilifanana na taarifa ya kupikwa lakini IGP hakujibu swali lolote lile.Huo haukuwa mwisho wa utata!!Sam akatabasamu huku akiitazama picha zilizokuwa mkononi mwake akazifananisha na vile vichwa vilivyopigwa picha na kuwekwa magazetini. Picha zilifanana kabisa na zile alizopewa kule kijijini na John Masele ambaye sasa anashutumiwa kuwa ni muuaji.“Wajinga ndio waliwao… siku zenu zinahesabika!” Sam akasema kwa sauti ya chini huku akiondoka zake.___Ili kuupaka umma mafuta kwa mgongo wa chupa serikali ikamwongezea ulinzi waziri yule. Huku nyumba ambayo yalitokea mauaji yale nayo ikilindwa na wanajeshi ambao walikuwa wakipishana kila baada ya masaa manne.Mathias Obhare naye akawa mtu wa kulindwa kila sekunde.Nafsi yake haikuwa na amani hata kidogo, alitamani kuubadilisha ukweli uliokuwa unamkabili lakini haikuwezekana kufanya vile tena. Mambo yalikuwa yanaanza kuwakaa kooni yeye na raisi kutokana na hila zao.Upande wa raisi, yeye alibaki katika fumbo kuu akiwafikiria wazungu wale walivyouwawa. Akiachilia mbali wale wazungungu, akamfikiria Suzi yule mwanadada mashuhuri ambaye aliaminika kuwa na roho saba.Ni nani aliyeuondoa uhai wake kirahisi namna ile tena pasipo kutumia silaha? Hili jambo lilimvuruga raisi na ile hali ya Benson kutopatikana hewani basi alivurugika kupita maelezo.Alitamani kumweleza mkewe juu ya wakati aliokuwa akipitia lakini akashindwa ni wapi angeanzia kwa sababu hata siku moja hakuwahi kumweleza juu ya hila zake serikalini na ubadhilifu aliokuwa akiufanya kwa kuwaruhusu wanyonyaji kula matunda ya nchi kuliko wazawa.Hatia ikamsulubu, akajaribu kupambana na hali ile lakini hakuweza.Akachukua simu yake na kumpigia mtu maalumu na kukatisha kikao cha bunge alichopanga kwenda kuhutubia.Na baada ya pale akampigia simu IGP.“Mkuu… una uhakika kuwa hakuna vijana wanatusaliti katika kambi ya usalama wa taifa…”“Sijaelewa unamaanisha nini mkuu..” IGP alijibu.“Haya mauaji we unayachukulia ya kawaida haya…. Wale wazungu na yule Suzi..” alijieleza Rais.“Mkuu kwani unawafahamu hao watu..” IGP akahoji. Na wakati ule akatambua kuwa raisi alikuwa anatetemeka. Alama ya kuuliza ikajiunda katika kichwa chake.Hao ni akinanani kwa raisi na wana mstakabali gani hadi awe katika hali ile.“Mhh! Hapana siwafahamu lakini Obhare anaweza kuwa anawafahamu naamini…” alijikanganya raisi kisha upesi akakata simu.IGP akaanza kuingiwa na mashaka.Na hapo akajaribu kuwasiliana na mrakibu mkuu Robert Masawe na kumweleza iwapo amepata fununu zozote juu ya mauaji yale.Robert akapiga fumbo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/“Inasadikika wameuwawa na watanzania wa kawaida ambao wamechoka kunyonywa….”“Una maana gani na nani amesema.”“Mkuu nimesema inasadikika, hivyo ni sisi kusadiki ama la!” akajibu mrakibu.IGP akakata simu huku akizidi kuchanganyikiwa!!Akabaki kujiuliza juu ya maneno ya Mrakibu msaidizi, kisha akahusisha na hali ya raisi.Kuna kitu!!! Akapigia mstari.****USIKU wa mang’amung’amu ulimwandama Sam. Alijitazama kama kijana mzembe sana licha ya makwazo kadhaa aliyopitia.Alizikumbuka ahadi tele ambazo alizipanga na Tina. Alikumbuka namna ambavyo kila mmoja aliapa kuwa yupo tayari kufa kwa amjili ya mwenzake.Ajabu yeye Sam alikuwa nyumba ya kulala wageni ya bei ya chini kabisa maeneo ya Machimbo nje kidogo ya jiji la Dar es salaam. Alijiona yu mjinga kujificha ili asife wakati mtu ambaye walipanga naye ahadi kedekede alikuwa matatani.Wakati akiyafikiria hayo mara akamfikiria na mzee John Masele. Kuna maneno ambayo alimweleza na sasa akajiona kuwa ni msaliti muoga tena asiyejiamini.Yale maneno yakajirudia kwa kasi kubwa kichwani mwake.“Sam naona unatetemeka bila shaka kuna baridi sana huku kwetu..” John Masele alimuuliza Sam huku akiwa anatabasamu.“Dah! Mzee huku ni tatizo kabisa hili baridi la Mafisa ni hatari sana, Iringa haioni ndani….” Sam alijibu.“Sam unahisi ili baridi lipungue unahitaji nini…”“Mzee hapa ni sweta zito kabisa nd’o linaweza kuleta nafuu” Sam akajibu, John Masele akacheka kidogo kisha akaendelea.“Hivi umewahi hata siku moja kuzungumza na Sweta lako na kulishukuru kwa kukulinda kwa baridi?”“Aaah! Mzee wangu lile sweta ni langu ya nini mimi kulishukuru sasa.. ule ni wajibu wake kunilinda mimi…” Sam akajibu huku akimshangaa John Masele.“Safi sana Sam, ehe! Na vipi sweta lako likichakaa…”“Naachana nalo nanunua jingine…”“ooh! Umejibu vizuri sana Sam. Ninachomaanisha hapa kijana wangu, wewe ni sweta kwa watanzania Sam, unatakiwa uwalinde watanzania pasipo kusubiri kupewa shukrani ama kupewa pesa kama wanavyotaka wengine. Au kupigiwa makofi kama ilivyo asili ya wapuuzi wengi, wewe sio mpuuzi Sam na usikubali kuwa mpuuzi ishi kama sweta. Kawasaidie watanzania, usisubiri watoe shukrani, na katika kuwasaidia huko utambue kuwa unaweza kuchakaa, unaweza kufa. Ukifa wewe utakuwa umetanua njia kwa masweta mengine mapya kuwalinda watanzania wasitetemeke kwa baridi, usiogope kufa Sam. Maana waliotupa uhuru wa bendera na wao walikufa sasa ni zamu yetu kuupata uhuru wetu…”Haya yalikuwa maneno ya John Masele usiku ule alipozungumza na Sam. Sam akajikuta katika aibu, kwanza akamfikira mpenzi wake, pili akatii maneno ya John Masele.Akakurupuka kutoka kitandani, akasimama wima na kujiulizaatalala na kujificha mpaka lini? Na ni nani ambaye atampigania ikiwa yeye hajaamua kujipigania.Sam akavinyoosha viungo vyake kisha akajisemea.“Mimi ni sweta na kesho naanza kazi rasmi.”Akarejea kitandani na kusinzia.Asubuhi akatazama kiasi cha pesa alichobaki nacho kilikuwa kinatosha kwa harakati alizokuwa amezipanga.Majira ya saa nne asubuhi Sam alikuwa katika ‘stationary’ moja isiyokuwa na watu wengi. Alikuwa ameketi mwenyewe kwenye kompyuta akitengeneza kitambulisho ambacho alipanga kwenda kukitumia mahali.Alitumia muda wa saa zima kukitengeneza kisha akakichapisha na kuondoka zake akiwa amelipia huduma ile.Sam akiwa amevalia suti yake nyeusi, miwani myeusi ya jua na kofia pana kichwani alichukua pikipiki ambayo ilimpeleka moja kwa moja maeneo ya Kurasini. Akashukia mbali kidogo na eneo alilopanga kwenda.Kisha akatembea kwa miguu, akafanya dua fupi kisha akaingia katika ofisi za mkuu wa shule ya sekondari ya kulipia.Akasalimia huku akiwa amesimama kisha akatoa kitambulisho chake na kukionyesha mara moja kisha akajitambulisha kwa jina.“Inspekta Babu kutoka kituo cha kati, amri kutoka kwa IGP, Suzan anatakiwa kuwekwa mahali salama muda huu kwa usalama wake. Tafadhali namuhitaji sasa hivi, samahani kwa usumbufu ni amri kutoka kwa IGP…” Sam aliunguruma huku miwani yake ikiwa ipo bado machoni huku akiwa amekakamaa mithiri ya askari.Ama! Mwandishi wa habari ni muigizaji pia!Mkuu wa shule alitetemeshwa na ujio ule wa Sam ambaye mafunzo ya JKT aliyoyapitia yalikuwa yamemjengea uimara sana.Pasipokupoteza muda, mkuu yule wa shule alimuita mwanafunzi mmoja na kumuamuru amuite Suzan.Punde msichana mrembo umri usiozidi miaka kumi na tano alikuwa mikononi mwa Sam. Sam alitembea kwa tahadhari kubwa huku akitazama kushoto na kulia kana kwamba kuna hatari yoyote anayojaribu kupambana nayo.Mkuu wa shule alibaki kuduwaa asijue ni kitu gani kibaya alitaka kufanyiwa mtoto yule.Sam akatokomea akiwa na yule binti mrembo!Siku iliyofuata taarifa zikatapakaa katika vyombo vya habari juu ya kutekwa kwa mtoto wa IGP.Mtekaji hakuwa akifahamika.Nchi ikaingia katika kizunguzungu kipya!!Na hapa ndipo mpasuko ulipoanzia!!****Daladala ilisimama maeneo ya Kibamba nje kidogo ya jiji la Dar es salaam. Sam akatelemka huku akiongozana na Sam pasi na kujua ni wapi alikuwa akipelekwa lakini hakuwa na mashaka yoyote kwa sababu ilikuwa kawaida kwa baba yake kuwaagiza mara kadhaa maaskari walio na vyeo vya chini yake kumchukua kutoka pale shuleni.Hata siku hii hakushangazwa na ujio wa Sam lakini alishangazwa na mahali ambapo walikuwa wanaelekea. Na ili kuinunua akili ya Suzan mtoto wa IGP wakati konda anakuja kudai nauli Sam akakitoa maksudi kitambulisho chake kilichosomeka kuwa yeye ni askari.Hilo likamwondolea hofu Suzan , Sam ambaye alikuwa amevaa miwani myeusi muda wote alikuwa ameikunja sura yake maksudi kabisa kama wafanyavyo askari watata.Ama hakika JKT ilikuwa imemsaidia sana na hakujutia ile miezi mitatu aliyoitumia kwenye mafunzo ya lazima baada ya kumaliza kidato cha sita.Baada ya kushuka Sam alimwamuru Suzan kusimama mahali amngojee huku akimsisitiza kuwa makini na mtu yeyote ambaye atajaribu kujiweka karibu naye.Akaondoka lakini kabla hajafika mbali akageuza tena kisha akamnong’oneza Suzan mtoto wa IGP.“Kuna maharamia wanataka kukulipua bomu… usipokee salamu ya mtu wala chochote kitu…”Maneno yale yakamtisha Suzan!! Akaingiwa na uoga kiasi huku akitii kila aliloambiwa.Na baada ya kama dakika kumi Sam alirejea na kumshikana mkono wakaongozana, wakazama bondeni na kisha kuibukia katika nyumba ya kulala wageni isiyokuwa na bango la kuitangaza.“Jifanye hauna hofu yoyote… we tabasamu tu!” Sam akamsihi Suzani. Binti bila kutambua kuwa anaendeshwa kama mtambo tuSuzan akatii!Wakaingia hadi katika chumba kimojawapo katika ile nyumba ambayo ilikuwa imekaa katika mfumo wa ‘uswazi’.Haikuwa na hadhi wala usalama!“Suzan… amani yetu watanzania inawekwa mashakani na watu wachache lakini jeshi letu lipo makini kupambana na watu hao na tupo tayari kwa lolote lile ikibidi hata kufa kwa ajili yenu.” Sam alizungumza huku akizunguka chumba kile kidogo huku na kule.Aliendelea kuzungumza bila kukoma, na baadaye akatoa pipi. Moja akamrushia Suzan wakati yeye alitupa moja kinywa na kuanza kumung’unya.Baada ya pipi ile kutupwa mdomoni mwa Suzani mtoto wa IGP. Mazungumzo hayakuendelea tena, kiza kikatanda wakati akisinzia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/**ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog