Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

DUNIA HAINA USAWA - 4

 






Simulizi : Dunia Haina Usawa

Sehemu Ya Nne (4)







Kila mtu aliyekuwa ndani ya chumba kile ikulu akapigwa na mshtuko, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona, rais wao alikuwa chini, alianguka baada ya kupata presha mara tu alipoona pesa zote alizokuwa nazo kwenye akaunti zilikuwa zimehamishwa kwenda katika hospitali moja nchini Marekani.

Wote wakamsogelea na kumbeba, vijana wanne kutoka humohumo ikulu wakafika, wakamnyanyua na kumpeleka katika chumba maalumu ambacho kilikuwa kikitumika kama hospitali ndogo humo ndani.

Presha yake ilipanda kutoka 120/80 mmHg mpaka kufika 230/130 mmHg. Kila mmoja alishtuka, walijua kabisa kwamba kama wasingefanya kazi ya ziada basi huo ingewezekana kuwa mwisho wa rais huyo.

Alitulia kitandani, hakutingishika kiasi kwamba ilikuwa ni rahisi kusema kwamba alikuwa amefariki dunia. Macho yake yaliziba, kwa jinsi alivyoonekana ilionyesha kama tayari system ya mwili wake haikuwa ikifanya kazi kabisa.

Mkewe alichanganyikiwa, akatoka chumbani na kwenda mpaka katika chumba kile cha matibabu, alipomwangalia mume wake kitandani pale, alibaki akilia kwani hali ilionyesha kwamba tayari mume wake huyo alikuwa marehemu.

“Imekuwaje jamani! Imekuwaje mume wangu kupatwa na tatizo hili?” aliuliza Bi Estelita huku akimwangalia mume wake kitandani pale.

“Mumeo alianguka na kuonekana presha kupanda kwa ghafla sana,” alisema daktari wa ikulu ambaye muda wote alikuwa humo kuhakikisha kila kitu kinakwenda salama.

“Ataamka tena?”

“Hatujui! Ndiyo tunaendelea kupambana! Vuta subira na umuombe Mungu! Natumaini kila kitu kitakuwa salama,” alisema daktari huyo ambaye alionekana kuwa bize kupita kawaida.

***

Hali ilikuwa imechafuka katika Benki ya Geneva nchini Uswisi, mkurugenzi wa benki hiyo aliitisha kikao cha haraka sana kwa ajili ya kujadili kitu kilichokuwa kikiendelea katika ‘system’ yao ambayo ilionyesha kulikuwa na muamala ilifanyika pasipo hata mwenye akaunti kuthibitisha muamala huo ufanyike.

Lilikuwa kosa kubwa, kiasi cha dola za Kimarekani milioni mia moja zilikuwa zimehamishwa kwenda katika akaunti nyingine nchini Marekani na mbaya zaidi hata kuzizuia walishindwa kwani pesa hizo zilipelekwa huku zikiwa na ulinzi mkubwa wa kiteknolojia.

Hawakujua mtu aliyefanya jambo hilo, vichwa vyao vilichanganyikiwa na wakati mwingine kuhisi kwamba kulikuwa na wafanyakazi ambao waliihujumu benki hiyo kitu ambacho kila mmoja alikana kufanya tukio hilo.

Lilikuwa tatizo kubwa, walitakiwa kupambana nalo kwa haraka sana hata kabla watu wengine hawakujua kilichokuwa kimetokea. Katika chumba kile kidogo kilichokuwa kikifanyika mkutano, mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Edward Peterson alivimba, kila kitu kilichokuwa kimetokea, kilimtia hasira.

“What the hell wrong?” (kuna tatizo gani?) aliwauliza viongozi wa benki hiyo akiwemo meneja mkuu, Bwana Linderfock.

Hakukuwa na mtu aliyejua kilichokuwa kikiendelea, walichokifanya ni kuwasiliana na watu wa IT hapohapo benki na kuanza kuzungumza nao. Wao wenyewe hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea, kulikuwa na mtu alikuwa ameingia kwenye database yao na kubana kila kitu, mafaili ya wateja wote yalifichwa kwa saa kadhaa na yalipokuja kuachiwa, tayari muamala ulikuwa umefanyika.

“Kweli hamuwezi kumgundua mtu aliyefanya hivyo?” aliuliza Bwana Peterson huku akiwaangalia.

“Tunahisi tutaweza kufanya hivyo! Cha kwanza tuzizuie pesa hizo kutoka kwenye akaunti ya hiyo hospitali,” alishauri jamaa mmoja.

Hilo ndilo lililofanyika, wakafanya mawasiliano na Bank of America na kuwaambia kilichokuwa kimetokea kwamba pesa zilizokuwa zimeingia katika akaunti yenye namba 08637621905 zilitakiwa kuzuiwa haraka iwezekanavyo kwani zilikuwa zimechukuliwa kiwizi kwenye benki kuu nchini Uswisi.

“Hakuna shida! Ila kwa jinsi zilivyo, nadhani hakuna mtu ambaye atakuwa na uwezo wa kuzitoa zaidi ya mhusuka tu, sisi tunazuia, ila hata mkisema tuzirudishe, tutashindwa kwa kuwa hata zilivyoingia tu, hatujui zimeingiaje,” alisema meneja wa Bank of America.

Hawakutaka kukubali, wakawasiliana nna watalaamu wa mambo ya IT na kuwaambia kilichokuwa kimetokea, kila mtu aliamini kwamba kazi hiyo ilikuwa ni rahisi sana kwani kama kulikuwa na virusi vilivyokuwa vimefanya figisu kisha kuhamisha pesa hizo basi vingewezwa kuangamizwa na kila kitu kurudishwa kama kilivyokuwa.

Vijana kumi na mbili kutoka nchini China wakafika nchin Uswisi kwa ajili ya kuifanya kazi hiyo. Walikuwa wataalamu waliobobea, waliokuwa akifanya kazi chini ya serikali, walipofika hapo, wakafanya kila linalowezekana kuweka mambo sawa lakini hakukuwa na kitu walichofanikiwa.

“Imekuwaje?” aliuliza Bwana Peterson.

“Bado tunapambana! Ila tunaweza kufanikiwa,” alisema kijana mmoja aliyeitwa Shu Yang ambaye alikuwa mtaalamu wa kucheza na system lakini kazi aliyokutana nayo hapo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.

****

Kuanguka kwa Rais Bokasa haikuwa siri tena, watu wengi wakafahamu kile kilichokuwa kimetokea huku sababu kubwa ya jambo hilo likiwa limefichwa kabisa. Watu walishangaa, hawakujua kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka rais huyo kuanguka na kuwa kwenye hali mbaya.

Si kila mtu aliyekuwa akihuzunika, asilimia kubwa ya Watanzania walikuwa wakifurahia, hawakuamini kilichotokea, wakapiga magoti na kumuomba Mungu kwamba kama ingewezekana rais huyo asifumbue macho yake, afe hapohapo kitandani kwani kwa maisha yaliyokuwa yakiendelea, kila mtu alikuwa akiyachukia.

Taarifa tofautitofauti zilikuwa zikiendelea kutolewa kutoka ikulu kwamba rais huyo alikuwa akiendelea vizuri. Taarifa hizo ziliwauma watu wengi kwani kusudio lao kubwa lilikuwa ni kumuona akifa kitandani pale kwani waliamini kwamba kama angekufa basi ingekuwa rahisi sana kwa maisha ya Watanzania wengi kubadilika.

Madaktari hawakutulia, kila daktari bingwa akaitwa kwa ajili ya kumtibu rais huyo, kila mmoja alikuwa akitaka kupewa sifa kwamba yeye ndiye aliyefanikisha mpaka rais huyo kupona ugonjwa huo.

Matibabu yaliendelea lakini hakuna aliyefanikiwa na hatimaye kusafirishwa kuelekea nchini India katika Hospitali ya Ganga kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.

Mpaka muda huo, hakukuwa na aliyekuwa na uhakika kwamba rais huyo angeweza kusimama tena, tangu alipoanguka na kupoteza fahamu hakuwa ameyafumbua macho yake japokuwa mapigo yake ya moyo yalikuwa yakiendelea kudunda kama kawaida.

Mitaani kulikuwa na stori nyingi juu ya tukio hilo. Kuna wengine walisema kwamba alipigwa na mkewe, wengine wakasema kwamba rais huyo alianguka akiwa bafuni, wengine walisema kwamba alitembea na mke wa mtu hivyo mwenye mume kuamua kumroga.

Hakukuwa na mtu aliyejua ukweli ila waliamini kwamba kila kitu kingewekwa wazi katika Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli kwani mtu huyo alionekana kama ofisa wa usalama wa taifa kwa jinsi alivyokuwa akipata taarifa nyingi tena kwa wakati.

Baada ya siku mbili tangu rais aanguke na kupoteza fahamu ndipo Godwin akaandika katika akaunti ile kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba yeye ndiye aliyesababisha rais huyo aanguke na kuumiza vibaya baada ya kuhamisha pesa zake alizowaibia wananchi kuwapelekea wagonjwa waliokuwa katika Hospitali ya St. Lucas nchini Marekani.

“Niliamua kuhamisha pesa zake zote katika akaunti yake iliyokuwa katika Benki ya Geneva, pesa zote hizo niliamua kuzipeleka katika Hospitali ya St. Lucas iliyokuwa nchini Marekani, sababu ya kufanya hivyo ni kwamba pesa si zake, ni pesa zangu, zako, zetu wote, tunalipa kodi, yeye ndiye ambaye aliamua kuzichukua kwa manufaa yake, sasa nimeamua kuziondoa kutoka kwake,” aliandika Godwin.

Hakukuwa na mtu aliyehuzunika, kila mmoja alifurahi kwani kwa kilichokuwa kimetokea, wote waliona kwamba rais huyo alistahili kufanyiwa kile alichofanyiwa.

Wananchi walikuwa wakiumia, kodi zilikuwa juu, ziliwaumiza kupita kawaida kiasi kwamba wengine hawakuona matunda ya kazi waliyokuwa wakiifanya ila kwa kuwa pesa zile walizokuwa wameibiwa kwa miaka mingi ziliondolewa kutoka kwa mbaya wao, walibaki wakimsifu Godwin kwa kile kilichotokea.

Viongozi wengine waliokuwa wameficha pesa zao huko wakashikwa na hofu na kuona kwamba kama wasingefanya kila liwezekanalo kuhamisha pesa hizo basi hata nao pesa zao zingechukuliwa na kupelekwa sehemu nyingine.

Walikuwa mawaziri watano, wakapigiana simu na kujadiliana ni kitu gani walitakiwa kufanya ili kuhakikisha pesa zao zinabaki salama katika mikono yao. Wakakubaliana kwamba ilikuwa ni lazima kuzihamisha pesa hizo kisiri kwenda kwenye benki nyingine nchini Tunisia ambapo zingewekwa kwa mtindo wa kuanzishwa taasisi ndogo ya Kiislamu ambayo iliweka kambi huko kwa ajili ya kusambaza misaada kwa watoto yatima na wanawake wagonjwa.

Wakati wakipanga mipango yao, hawakujua kama simu zao zilikuwa zikidukuliwa na Godwin ambaye alikuwa akifuatilia kila kitu, alipogundua kwamba viongozi hao walikuwa na mpango huo wa kuhamisha pesa zao na kupeleka katika moja ya benki nchini Tunisia, akaanza kucheza nazo kwa ajili ya kuzificha kama alivyomfanyia Rais Bokasa.

“Niwaambie tu kwamba viongozi watano waliokuwa wakiwasiliana jana kwamba watahamisha pesa zao kwenda kwenye moja ya benki nchini Tunisia, mpango wenu umekwamba kwani mpaka inafika asubuhi, hamtoweza kuziona pesa zenu,” aliandika Godwin katika akaunti yake kitu kilichowafanya watu wote kushangaa kwamba jamaa alikuwa akinasa vipi mawasiliano ya viongozi hao kiasi cha kuwatia hofu.

Alichokisema ndicho kilichofanyika, siku hiyohiyo akazizuia pesa za viongozi hao. Walipokuwa wakiingia, waliziona lakini walipotaka kufanya miamala, pesa hazikuwa zikionekana.

Haraka sana wakawasiliana na Mkurugenzi Peterson na kumwambia kilichokuwa kikiendelea. Hakuamini, alichanganyikiwa kwani Wachina aliokuwa amewaita kufanya kazi, walikuwa wakihakikisha Rais Bokasa anarudishiwa pesa zake, sasa kabla kazi hiyo haijafanyika na kukamilika, tayari kulikuwa na kesi nyingine, haikuwa kwa mtu mmoja, kwa wateja wao watano kiasi kwamba yeye mwenyewe hakujua afanye nini.

“Hebu subiri kwanza. Mnanichanganya,” alisema Bwana Peterson.

“Tunajua! Ila kwa nini pesa zetu hazitoki!”

“Kuna mtu amedukua akaunti zenu!”

“Inawezekanaje?”

“Naomba mnipigie baadaye. Sijui hali imekuwaje! Naomba mnipigie baadaye, tunashughulikia tatizo lenu,” alisema Bwana Peterson huku akionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida.

Simu ikakatawa, kila kitu kilikwenda ndivyo sivyo, kilichokuwa kikiwashangaza ni namna ambavyo mtu huyo alivyoweza kupata mawasiliano yao, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.

Walisikilizia simu kutoka nchini Uswisi, hawakupigiwa, dakika zilisonga, saa likakatika, saa mbili nazo zikaenda, mpaka saa tano, bado hawakupigiwa hali iliyowapa majibu kwamba watu hao walikuwa wakiendelea kuhangaika kuhakikisha kile kilichokuwa kimetokea kinapatiwa ufumbuzi haraka sana.

“Wakati tunasikilizia huko, waambie usalama wa taifa wamtafute huyo Godwin!” alisema Waziri wa Kilimo, Abraham Ojuku.

“Wanafanya kazi hiyo mkuu. Tatizo picha zake!”

“Hakuna picha zake?”

“Ndiyo! Kwenye mitandao zipo zile za utotoni!”

“Ukubwani hakuwahi kupiga picha?”

“Hapana!”

“Hebu waambie wafuatilie, aliposhuka na ndege alitoka wapi, alikuwa anafanya nini huko. Hakikisha wanafuatilia, na kama alikuwa akisoma chuo, alisoma chuo gani, tukipata yote hayo, tutafanikiwa kwani cha msingi tupate picha yake ya ukubwani, ya utotoni hatutofanikiwa kumpata kwani anaweza akawa na ndevu nyingi kama Osama,” alisema Waziri Ojuku huku akionekana kuchanganyikiwa.

“Tunafuatilia mkuu!”

***

Usalama wa Taifa hawakutaka kutulia, waliambiwa kwamba walitakiwa kufuatilia kuhusu Godwin na siku hiyohiyo kituo cha kwanza kabisa cha kuanza upelelezi wao kilikuwa ni uwanja wa ndege kulipokuwa na ofisi ya Shirika la Ndege la Orange.

Wakafika katika ofisi hizo na kitu pekee walichokuwa wakikihitaji ni taarifa juu ya msafiri ambaye alisafiri kwa ndege yao siku ya Jumamosi na hivyo kuwapa orodha ya majina ya watu waliosafiri kwa ndege hiyo.

Haraka sana wakaanza kupitia majina ya abiria hao, wala hawakuchukua muda mrefu wakaliona jina la Godwin Mapoto ambaye alikuwa amesafiri huku pembeni yake kukiwa na msichana mwingine aliyeitwa kwa jina la Manka.

Ilionyesha kabisa kwamba Godwin alitokea Dubai katika ndege iliyotokea nchini Japan ambapo huko hawakujua alikwenda kufanya nini kwani kutokana na Waafrika wengi kwenye katika nchini za Mashariki ya Kati, iliwafanya kutokundua kama alikwenda kibiashara au kusoma.

“Ni lazima tusafiri kwenda huko, inawezekana tukapata taarifa zaidi,” alisema Boniphace Ngumije, mmoja wa wanausalama walioambiwa wafuatilie kila kitu kuhusu Godwin na ikiwezekana waweze kupata picha zake.

Wakatoa taarifa kwa mkuu wao na kumwambia kwamba walikamilisha theluthi ya upelelezi wao na kugundua kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa ametokea nchini Japan lakini hawakujua dhumuni hasa la mtu huyo kuwa nchini humo.

“Nendeni mpaka huko, hakikisheni mnafanya kila linalowezekana kupata picha zake,” alisema mkuu wao.

Wakasafiri na kuelekea huko, njiani, walikuwa na mawazo tele, walikuwa wakimtafuta mtu ambaye waliamini kwamba alikuwa nchini Tanzania. Walikuwa wakijadiliana juu ya kitu gani kilitakiwa kufanyika mpaka kuhakikisha wanapata picha za mtu huyo na kurudi nazo nchini Tanzania.

Walichukua saa zaidi ya ishirini mpaka kufika Japan ambapo wakachukua chumba, wakalala na siku iliyofuata ilikuwa ni kufuatilia katika ofisi za Shirika la Ndege la Orange ili kupata kila kitu kilichokuwa kikiendelea.

Kama ilivyokuwa kule Tanzania, napo wakapewa jina la mtu huyo, namba ya tiketi yake lakini kuhusu kila kitu kilichokuwa kikiendelea, kupata picha yake ilikuwa ni lazima kuwasiliana na ubalozi wa Japan nchini Tanzania kuwaambia kuhusu mtu huyo.

“Taarifa hazionyeshi kitu chochote kile, huwa tunazihifadhi katika kompyuta zetu, cha ajabu taarifa za mtu huyo hazipo. Mna uhakika alikuwa Japan?” aliuliza balozi wa Japan nchini Tanzania ambaye alikuwa akitumiwa taarifa zote.

“Ndiyo! Au alizifuta?”

“Haiwezekani! Hakuna mtu anayeweza kuingia kwenye kompyuta zetu,” alisema balozi huyo pasipo kujua kwamba taarifa zote kuhusu Godwin, mwanaume huyo alizifuta.

Hawakutaka kukata tamaa, vijana waliokuwa Japan wakapewa taarifa kuanza kufuatilia katika vyuo nchini humo kuona kama kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo ambaye alimaliza chuo siku chache zilizopita.

Walizunguka kwenye kila chuo, jina walilokuwa wakiliangalia lilikuwa ni Godwin tu. Waliwapata vijana wengi lakini hawakuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa nguvu zote lakini baada ya kwenda katika Chuo Kikuu cha Waseda kilichokuwa Tokyo, wakaambiwa kwamba kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo, aliitwa Godwin Mapoto.

“Ndiye huyohuyo! Hebu tunaomba data zake zote,” alisema Boniphace huku akionyesha tabasamu, walikaa siku tatu nchini humo na hawakupata chochote kile, kitendo cha siku hiyo kupata mwanga, kiliwafurahisha.

“Alikuwa mwanafunzi wa mwisho mweusi kusoma katika chuo hiki. Alichukua PhD yake siku chache zilizopita. Alikuwa raia wa Tanzania. Data zake hizi hapa,” alisema mkuu wa chuo hicho huku akiwaonyeshea mwanaume huyo.

“Safi sana.”

“Ni mtu makini sana. Ana akili nyingi mno, inasadikiwa ndiye mtu mwenye akili kubwa na kucheza na kompyuta, mambo yote kuhusu programming, networking, huyo ndiye alikuwa balaa,” alisema mkuu wa chuo, hakuishia hapo akaanza kuwapa simulizi kuhusu Godwin ambayo iliwasumbua wataalamu wengi, hasa baada ya kuficha mafaili ya chuo.

Hawakuamini kama kungekuwa na Mtanzania ambaye angekuwa na akili kiasi hicho. Walibaki wakiangaliana na kukiri kwamba mtu waliyekuwa wakidili naye hakuwa mtu wa kawaida hata kidogo na ndiyo maana hata ile akaunti yake ilikuwa ni vigumu sana kufutwa na watu wengine.

“Sawa. Tunashukuru sana. Naomba kuuliza swali!” alisema Martin, kijana aliyeongozana na Boniphace.

“Uliza.”

“Mbona kwenye taarifa zake hakuna picha yake?” aliuliza Martin.

“Picha yake? Picha yake ilikuwepo hapa. Sijui imekwenda wapi lakini ilikuwepo hapa,” alisema mkuu wa chuo huku akishangaa, taarifa zote za wanafunzi zilikuwa zikiwekwa na picha ila cha kushangaza kwenye faili la Godwin hakukuwa na picha.

“Una uhakika picha zilikuwepo?”

“Ndiyo! Ni juzi tu zilikuwepo.”

“Tunaweza kuzipata?”

“Haina shida.”

Kuzipata picha za Godwin hakukuwa na tatizo lolote lile kwani kulikuwa na picha nyingi ambazo zilikuwa katika tovuti ya chuo watu walikuwa wamepiga. Mkuu huyo wa chuo alifungua tovuti hiyo na kuangalia picha zote, kitu cha ajabu kabisa ambacho kilimchanganya, kote huko zile picha zote ambazo mwanaume huyo alitokea, hazikuwepo kitu kilichowachanganya.

Boniphace na mwenzake hawakutaka kubaki Japan, walimwambia mkuu wao kwamba kule walipokuwa wamekwenda hawakufanikiwa kupata kile walichokuwa wakikihitaji ila kwa taarifa tu ambazo walizipata kutoka kwa mkuu wa chuo zilieleza kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa hatari sana katika kutumia kompyuta.

Hilo likawafanya kukata tamaa kupata picha zake, walichokifanya ni kuchukua picha zilezile alizokuwa mtoto mdogo na kuzisambaza katika vituo mbalimbali vya polisi ili kama wangemuona mtu aliyekuwa akifanana na mtoto huyo wamchukue na kumpeleka kituoni mara moja.

“Mmh! Hivi tunaweza kufanikiwa kweli? Sidhani ila haina jinsi, ni lazima tutii kile tulichoambiwa!” alisema mkuu wa Kituo cha Polisi cha Mkwajuni.

****

Godwin hakuwa na hofu hata kidogo, kwa kila kitu kilichokuwa kikiendelea kwake kulikuwa na amani tele. Alikuwa akiichanganya serikali, kila siku alikuwa akiwapa taarifa watu kuhusu madudu mengi yaliyokuwa yakitokea nchini Tanzania.

Watu walimshukuru ingawa kwa upande wa pili serikali ilikuwa ikichomwa na mbaya zaidi hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua mahali mwanaume huyo alipokuwa kwani kila walipojaribu kuidukua simu yake kujua alipokuwa, iliwaonyesha kwamba ilikuwa Urusi na wakati mwingine kuwaonyesha ilikuwa Dubai.

Walichanganyikiwa, walituma maofisa wa usalama wa taifa, waliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa katika mtaa mmoja wa kitajiri akila maisha hivyo kuwatuma watu wengi huko. Ni kama Godwin alijua kwani mara baada ya kutoka hotelini, akaondoka na kuanza maisha katika Mtaa wa Tandale kwa Mtogole, akapanga katika chumba kimoja chakavu, akanunua nguo za mtumba Tandale Sokoni na kila siku kazi yake ilikuwa ni kuendeleza harakati zake katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli.

“I want to know who killed my parents and sister,” (nataka kumjua aliyewaua wazazi wangu na dada yangu) aliandika Godwin kwenye akaunti yake kitu kilichozua maneno mengi na wengine kugundua kwamba inawezekana Godwin alikuwa akifanya hayo yote kwa kuwa kulikuwa na watu waliokuwa wameiteketeza familia yake.

Maoni yalikuwa mengi, wengi walikuwa wakiuliza kilichokuwa kikiendelea mpaka kuandika maneno hayo ambayo yaliwasisimua watu wengi. Kila swali alilokuwa akiulizwa, alilijibu pasipo tatizo lolote lile kitu kilichowafanya watu kugundua maovu makubwa yaliyokuwa yakifanywa na serikali iliyokuwa madarakani.

“Nilijua tu! Hii serikali magumashi sana. Inawezeje kuiangamiza familia nzima. Kwanza huyu jamaa ni mtoto wa familia ipi? Baba yake alikwishawahi kuwa kiongozi yeyote yule?” alihoji jamaa mmoja kwenye Mtandao wa Facebook huku akiwa ameipiga picha ile posti aliyoiandika Godwin.

Posti hiyo ikaibua mambo mengi, kila mtu mitaani alikuwa akizungumza lake. Kwa Godwin hakutaka kuzungumzia kitu chochote kwa undani ila alichokifanya ni kutafuta vifaa vyote vya kuchorea tatuu na kujichora tatuu kifuani iliyokuwa na maneno hayo aliyoandika kwenye akaunti yake.

“Hii ni vita ya kisasi na kamwe haitomuacha mtu salama,” aliandika Godwin na kuongezea maneno mengine mengi yaliyosomeka:

“Huu utakuwa mwezi wa viongozi wengi kujiua. Sitowaua mimi, ila ninatarajia viongozi wengi watakwenda kujiua. Kuna data nilikuwa nazikamilisha, zipo poa. Ninawahakikishieni kwamba viongozi wengi watajiua, si kwamba ninapenda kuwaua, hapana, watajiua wao wenyewe kwani kashfa zitakawatafuna, hakika hawatoona thamani ya kuishi.

“Kama mlikuwa hamjui, kuna msichana aliitwa Vanessa Fabian, msichana mrembo ambaye ndiye atasababisha viongozi hao kujiua. Unajua kwa nini? Nitakuandikia Jumatatu kila kitu kilichotokea kwa msichana huyu, wengi mtahuzunika ila mwisho wa siku mtatabasamu, itakuwa historia yenye kumgusa kila mtu. Unataka kuifahamu historia ya msichana huyo, nitawaandikia Jumatatu mahali haphapa,” ilisomeka posti hiyo ndefu.

Kila mtu akawa na hamu, wengi walitaka kumjua huyo Vanessa, alikuwa nani na alibeba historia gani yenye kuhuzunisha ambayo ingewafanya viongozi wengi wa serikali kujiua?

Maoni yakawa mengi mno na kila mmoja alionekana kuguswa kwa kile kilichokuwa kimeandikwa hivyo watu wengi kuwa na hamu ya kutaka kufahamu. Ni mambo gani yalitokea ambayo yangepelekea viongozi wengi kujiua? Kila mmoja alitaka kujua.

***

Godwin hakuwa mtu wa kutoka sana nje, alikuwa mtu wa kukaa ndani kila wakati. Japokuwa akaunti yake ilikuwa maarufu sana lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua kwamba yule mwanaume aliyepanga kwenye nyumba ile mbovumbovu ndiye yuleyule aliyekuwa akiinyima furaha Serikali ya Tanzania.

Kazi yake kubwa ilikuwa ni kudukua mawasiliano yote yaliyokuwa yakifanyika nchini Tanzania hasa kwa viongozi wa nchi hiyo. Alijua siri nyingi, mikataba ya siri iliyokuwa imesaniwa ambayo iliruhusu madini kuondoka, pesa za mitambo ya umeme, kila aina ya uchafu uliokuwa ukifanyika data zake alikuwa nazo.

Alitaka kuandika historia kuhusu msichana Vanessa, hakuwahi kukutana na msichana huyo ila historia yake alikutana nayo katika barua pepe ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Bwana Samson Mwinyimkuu.

Ilikuwa ni historia ya msichana Vanessa, msichana aliyekuwa mrembo mno ambaye aliamua kuiandika historia ya maisha yake na kumtumia waziri huyo ambaye aliiweka katika barua pepe yake na kuifanya siri nzito.

Godwin aliipata barua hiyo, ilikuwa ni ndefu mno lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kuiandika kwa ufasaha na kuiweka katika akaunti ile.

Watu walikuwa wakisubiri kwa hamu kubwa, kuanzia siku ya Jumamosi mpaka Jumatatu ilionekana kuwa kama mwezi mzima. Kila mmoja alitaka kujua kile kilichokuwa kimetokea kwa msichana huyo mrembo, hawakujua alikuwa Vanessa yupi kwani kwa kipindi hicho kulikuwa na wasichana wengi wenye jina hilo waliokuwa maarufu sana.

Mara baada ya Waziri Mwinyimkuu kuona posti hiyo, haraka sana akaingia katika barua pepe yake ili kuangalia kama ilikuwepo, aliiona ila hofu yake kubwa ilikuwa ni juu ya msichana huyo ambaye kwa kipindi hicho alikuwa marehemu, je, alimtumia Godwin barua hiyo hata kabla hajafa?

Wakati akiwaza hayo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, alikuwa na presha kubwa, alikuwa akiheshima na kila alipokuwa akipita watu walimpigia makofi, alikuwa mchapakazi ambaye kila siku viongozi wengi wa serikali waliambiwa waige utendaji kazi wake mkubwa.

Hakujua ni kitu gani kingetokea mara baada ya uovu wake aliomfanyia Vanessa kwa kushirikiana na viongozi wengine kuwekwa wazi. Alitetemeka, mapigo ya moyo wake yalidunda kupita kawaida.

Watanzania wengi waliona Jumatatu kuwa mbali lakini ni yeye tu ndiye aliyeiona siku hiyo kuwa karibu sana. Mishale ya saa yake ilikimbia kwa kasi ya ajabu, alijiona akiwa nje, kwenye umati mkubwa huku watu wakimwangalia, walimcheka na kumdhihaki na watu wengi kutamani kuona mwanaume huyo akifa kutokana na uovu aliokuwa ameufanya.

“Ngriiiii...ngriii...” alishtushwa na mlio wa simu, haraka sana akaichukua na kuipeleka sikioni, kwa jinsi alivyokuwa amechanganyikiwa, hata kuangalia jina la mpigaji hakuangalia.

“Mwinyimkuu! Upo wapi?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili.

“Ny..um..ban..i..” alijibu Mwinyimkuu huku akitetemeka.

“Umeona kilichopostiwa? Ile barua pepe uliifuta kweli au uliihifadhi kama jumba la makumbusho?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili, kama alivyochanganyikiwa waziri huyo hata na yeye alikuwa amechanganyikiwa.

“Sikuifuta!”

“Hukuifuta? Kwa nini? Isije kuwa huyu mtu anataka kuiandika ile historia ya yule binti!” alisema jamaa huyo.

“Sidhani! Hawezi! Atakuwa anatutisha tu!”

“Mh! Ya kweli hayo? Sasa amejuaje kuhusu Vanessa?” aliuliza.

“Sijajua kabisa. Ni bora kama yule msichana angekuwa hai tungemuuliza. Ibra, naomba unipigie baadaye,” alisema Mwinyimkuu na kukata simu.

Hakuishia kupokea simu ya Ibra tu bali alipokea simu za viongozi watatu ambao wote hao walimuuliza kuhusu kile kilichokuwa kimeandikwa, kila mmoja alikuwa na hofu kubwa na kuona kabisa kwamba uovu wote waliokuwa wamemfanyia msichana huyo sasa ulikuwa ukienda kujulikana na kila mtu.

“We are finished,” (tumekwisha) aliandika mwanaume mmoja ambaye naye alishirikiana na Mwinyimkuu katika kila kitu kuhusu msichana Vanessa.

Jumatatu asubuhi tayari watu walikuwa mbele ya kompyuta zao huku wengine wakiwa katika simu zao. Walitaka kushuhudia ni kitu gani kilikuwa njiani kuandikwa. Kazini, kila mfanyakazi alikuwa na simu yake, hakutaka kuiweka chini, walitaka kusoma kuhusu msichana huyo mwenye historia ya kusikitisha mno.

Saa 3:00 asubuhi Godwin akaposti sehemu ya kwanza kuhusu msichana huyo. Alianza kusimulia historia ya maisha yake, jinsi alivyokuwa kwenye maisha ya kimasikini mpaka pale alipoamua kumfuata Mwanyimkuu kwa ajili ya kumsaidia.

Mwanaume huyo alipofuatwa na msichana huyo, aliahidi kumsaidia kwa moyo mmoja lakini badala ya kufanya hivyo, akaanza kwa kumuomba penzi. Kilikuwa ni kitu ambacho Vanessa alimkatalia kwa nguvu zote kwani hakuwahi kufanya mapenzi na mwanaume yeyote, alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni msaada tu kwa kuwa aliamini mwanaume huyo alisaidia watu hivyo hata yeye angemsaidia.

“Bila penzi hakuna msaada.”

“Ila mama anaumwa sana. Naomba unisaidie, umasikini unatutesa, bila pesa, mama yangu atakufa, bila pesa, wadogo zangu watakufa kwa njaa, hatuna kitu, maisha yetu ni masikini, naomba utusaidie,” ilisema sehemu ya posti ile alipokuwa akizungumza msichana Vanessa.

“Bila penzi, mama yako atakufa, na bila penzi wadogo zako watakufa pia,” alisema mzee huyo.

Vanessa hakutaka kuona mama yake akifa, alipenda kuona akiendelea kuishi miaka yote na hivyo kumpa penzi mzee huyo. Alisikia maumivu makali kwa kuwa ilikuwa ni siku yake ya kwanza. Kiasi cha pesa alichokuwa akikihitaji hakukipata kutoka kwa mzee huyo zaidi ya kupewa asilimia ishirini ya kile alichokiomba.

Mzee Mwinyimkuu akatumia pesa na madaraka kumchezea msichana huyo, alimtumikisha kingono na alipoona kwamba ameridhika, akawaambia wengine matatizo ya msichana huyo na hivyo nao kumfanyia mchezo huo msichana huyo mdogo. Wanaume hao wengine watatu walikuwa ni Waziri Mamboleo, Kijuku na Mburu.

Msichana wa miaka kumi na sita akatumikishwa kingono na wanaume wanne, hawakuwa na huruma, waliendelea kumchezea pasipo kumsaidia na wakati alipokuwa akiwatisha kwamba ataenda polisi kushtaki, walimwambia kwamba wangemuua na hivyo kuogopa.

Ni maisha yaliyoogepesha na kusisimua mno. Mmoja kati ya wanaume hao alikuwa ameathirika ugonjwa wa Ukimwi, akamuambukiza Vanessa na kuwaambukiza wanaume hao wote.

Ilikuwa ni historia ndefu ambayo Godwin aliiandika kimafungumafungu, hakutaka kuishia hapo, alihakikisha anaweka kila kitu wazi, hawakujua majibu ya vipimo vya Ukimwi alivitoa wapi, aliweka karatasi za majibu ya damu zao baada ya kupima damu hospitalini.

“Mungu wangu! Kumbe wameathirika! Wamemuambukiza na mtoto yule jamani!” alisema jamaa mmoja.

Wanawake waliokuwa wakisoma historia ndefu ya msichana huyo hawakuvumilia, walikuwa wakilia kwa maumivu makali mioyoni mwake, walisisimka, hawakuamini kama kungekuwa na watu waliokuwa na hali ya kinyama kama viongozi hao.

“Hatuwezi kukubali! Tutaandamana kuwataka wajiuzulu,” alisema jamaa mmoja.

Vijana wenye msimamo, walioumizwa hawakutaka kubaki nyumbani kwao. Ilikuwa kashfa kubwa iliyolitetemesha taifa kwa ujumla, viongozi ambao kila siku walikuwa wakiheshimiwa kila walipopitwa kumbe walikuwa na maisha ya kinyama, kwa kutumia pesa na nguvu zao waliamua kumdhalilisha Vanessa kingono.

Msichana huyo alikufa miaka miwili iliyopita kwa ugonjwa huo ambao watu hawakujua aliupata wapi na mbaya zaidi, viongozi hao nao walikwenda kuhudhuria msiba huku wakijifanya kuwa na huzuni mno.

“Siwezi kuishi! Siwezi kuivumilia aibu hii,” alisema mwinyi mkuu, historia ndefu aliyokuwa ameambiwa na Vanessa ndiyo ambayo ilikuwa ikionekana katika akaunti ya Mabadiliko ya Kweli.

Hakujua mahali mtu huyo alipoipata kwani mara baada ya Vanessa kuiandika, akamtumia na alikuwa na uhakika kwamba hakutumiwa mtu mwingine kwa kuogopa kuuawa, sasa ilikuwaje mpaka mtu mwenye akaunti hiyo kuipata?

Aliumia, alijutia kila kitu alichokifanya maishani mwake. Hakujua Tanzania ingemuangaliaje, hakujua familia, ndugu, jamaa na marafiki wangemuangaliaje, uamuzi alioufanya ulikuwa ni mmoja tu, kujiua kwa kujipiga risasi.

“Mwinyimkuu amejiua!” alisema jamaa mmoja.

“Kweli?”

“Ndiyo! Hiyo ni breaking news wameiandika Global. Cheki braza,” alisema jamaa huyo huku akimuonyeshea simu mwenzake.

Huo ulikuwa ni kama mwanzo, ilikuwa ni fedhea, wahusika wote waliumia, hakukuwa na hata aliyebaki, ili kuogopa aibu kubwa mbele yao, wakaamua kujiua kwa vifo tofauti, yule alijipiga risasi, mwingine akajinyonga, mwingine akanywa sumu na mwingine akaamua kujichinja.

“Yapo mengi tu! Nilipowaambia nimekuja Tanzania kufanya kazi namaanisha nimekuja kufanya kazi. Nitaweka wazi mambo mengi sana! Nyie subirini, kuna vitu vingine havielezeki, nitawaelezea mpaka wachungaji ambao wanashirikiana na viongozi serikalini kuwaibia wananchi. Unajua wanawaibia vipi na wachungaji hao ni wakina nani? Nitawaandikia kesho mahali hapa. Lengo ni kuisafisha nchi, hilo tu,” aliandika Godwin, kwa kipindi hicho, kila kitu alichokuwa akikiandika kwenye akaunti ile alikuwa na uthibitisho nacho

Kwa kile kilichokuwa kimetokea, kila kona ikawa gumzo. Akaunti ile iliwasumbua watu wengi, katika nchi nyingine Afrika Mashariki kila mmoja alikuwa akizungumza lake, wengi walilaumu kwa kilichokuwa kimetokea, Tanzania ikaingia doa, kila kona ilizungumziwa vibaya lakini pamoja na hayo yote, watu wote walikuwa wakimsifu mtu aliyekuwa akiweka wazi madudu yote yaliyokuwa yakitokea nchini humo.



Vijana wa IT nchini Uswisi walikuwa wakihangaika kuzichukua pesa ambazo zilihamishwa kwenye akaunti moja nchini Marekani katika Benki ya American. Waliweza kuzizuia pesa hizo nyingi zisiweze kutoka lakini kitu cha ajabu kabisa hawakuwa wakiweza kuzichukua na kuzirudisha katika akaunti zilipotolewa.

Walitumia wataalamu wengi lakini kitu kilichokuwa kikiwatatiza kilikuwa ni virusi vilivyokuwa vimeingizwa katika data base yao ambavyo vilizuia pesa kurudishwa katika akaunti ile iliyokuwepo.

Mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Peterson hakulala kwa siku mbili mfululizo, kichwa chake kilichanganyikiwa na hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea. Vijana wa IT aliokuwa amewaita kwa ajili ya kufanya kazi hiyo walionyesha kila dalili za kushindwa kwani walichukua muda mrefu mno na hakukuwa na kitu chochote kile kilichofanyika.

Kwa siku tatu mfululizo watu walikuwa wakihangaika, wakaitwa wataalamu mbalimbali kutoka sehemu tofauti lakini hakukuwa na mtu aliyeweza kuzirudisha pesa hizo zilizokuwa zimetumwa katika akaunti ile ya Hospitali ya St. Lucas.

“Hebu tuwasiliane na mteja kwanza ili tumuombe radhi kwani tunaweza kuchukua muda mrefu kidogo,” alisema Bwana Peterson.

Ilikuwa ni lazima kuwasiliana na Rais Bokasa kumuomba radhi kwa kile kilichokuwa kikiendelea. Mawasiliano kwa njia ya simu yakafanyika na kilichowashtua zaidi ni kwamba mtu huyo alikuwa hoi hospitalini baada ya kuzimia alipopewa taarifa kwamba kiasi hicho kilikuwa kimechukuliwa katika akaunti yake.

Wakati wakiongea na mtu wa pili ndipo mkurugenzi huyo akaambiwa kila kitu kilichokuwa kimetokea. Aliambiwa kuhusu akaunti ya Mabadiliko ya Kweli, akaambiwa kwamba mtu aliyekuwa na akaunti hiyo ndiye ambaye alikuwa ameziiba pesa hizo na kuziweka katika akaunti hiyo, serikali ya Tanzania ilikuwa ikipambana kumtafuta lakini ubaya zaidi ni kwamba walikutana na mtu aliyekuwa akijua sana kutumia kompyuta.

“Kwa hiyo huyo mtu yupo huko?” aliuliza Bwana Peterson.

“Ndiyo! Ila hatufahamu yupo wapi!”

“Na akaunti hiyo anaitumia?”

“Ndiyo!”

“Hebu subiri!”

Alichokifanya Peterson ni kuwasiliana na rais wa nchi hiyo na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea. Kwanza akamuhadithia kuanzia mwanzo mpaka pale ambapo vijana waliitwa kwa ajili ya kurudisha pesa hizo, alipomaliza akamwambia kuhusu ile akaunti na mtu aliyefanya mambo hayo yote alikuwa nchini Tanzania.

“Haiwezekani!”

“Ndiyo hivyo!”

“Kwa hiyo ni Mwafrika?”

“Ndiyo mkuu!”

“Hebu subiri!”

Yaliyokuwa yakifanyika yalikuwa ni mawasiliano kwa njia ya simu. Ilikuwa ni lazima waunganishe nguvu zao kwa ajili ya kumpata mtu huyo ambaye alikuwa akiwasumbua muda wote. Rais hakutaka kukubali kwamba mtu aliyekuwa akiyafanya mambo hayo alikuwa Mwafrika.

Hakuamini kama Waafrika walikuwa na akili kubwa kama Wazungu, kwake, watu hao walionekana kama maboksi fulani ambayo yalikuwa yakifanya kile walichoambiwa wafanye lakini si wao kuwaongoza Wazungu.

Akawasiliana na Mkurugenzi wa usalama wa taifa nchini humo, The Federal Intelligence Service (FIS), Bwana Henrik Kom ambaye akamwambia kila kitu kuhusu mchakato mzima ulivyokuwa na kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima maofisa wawili wa FIS watumwe kuelekea nchini Tanzania kwa ajili ya kumtafuta mtu huyo ambaye aliisumbua Benki ya Geneva kwa kile alichokuwa amekifanya.

“Hilo si tatizo! Wamesema ni Mwafrika?”

“Ndiyo!”

“Mmh! Inawezekana vipi?”

“Ndiyo tunataka muendele mkajue ukweli huko,” alisema rais.

Hilo ndilo walilolifanya, ndani ya siku mbili, vijana wawili, wataalamu kwa masuala ya upelelezi wakatumwa kwenda nchini Tanzania huku wengine wakibaki hapo kwa ajili ya kuifuatilia akaunti hiyo ya Mabadiliko ya Kweli iliyokuwa katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram.

****

Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba yule kijana masikini aliyekuwa amehamia mtaani Tandale ndiye aliyekuwa akihusika katika kuuendesha mtandao huo. Hapo Tandale alipokuwa akiishi alikuwa mtu wa watu, alitaka kuyaficha maisha yake, kusiwe na mtu yeyote kumfahamu au hata kuhisi kwamba alikuwa yeye.

Alichokifanya ni kuanza kwenda katika vilabu vya pombe haramu na kuanza kushinda huko. Kazi yake ilikuwa ni kupiga stori, hakuwa mnywaji ila kila alipokuwa akirudi nyumbani kwake alijifanya kuwa mlevi mkubwa.

Watu walimshangaa, hawakuwahi kumuona mgeni ambaye alifahamiana na watu wengi kwa haraka kama ilivyokuwa Godwin, kila mtu aliyekuwa akiongea naye alijua kabisa kwamba alikuwa akizungumza na mlevi ambaye kila siku asubuhi, mchana mpaka jioni kazi yake ilikuwa ni kushinda klabuni tu.

Akajulikana zaidi kama mlevi, hawakujua kama mtu huyo ndiye aliyewanyima usingizi viongozi mbalimbali, kila siku usiku ilikuwa ni lazima kuangalia kwenye akaunti yake kuona ni jinsi gani watu walikuwa wakitaka aendelee kuwaumbua viongozi wa serikalini kwa maovu waliyokuwa wakiyafanya.

Alijua mambo mengi, watu waliokuwa wakimfuata inbox na kumtumia meseji walimwambia mambo mengi kuhusu viongozi wa serikali ilivyokuwa ikiwatumia wachungaji, maaskofu kwa ajili ya kuwaibia wananchi pesa.

Hakutaka kuliingilia suala hilo kwa pupa, kitendo cha kuwazungumzia wachungaji ilikuwa ni kama kuizungumzia dini fulani au kundi kubwa la watu fulani. Alitaka kufanya uchunguzi wake, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutafuta namba za wachungaji na maaskofu hao, wala hakupata tabu, akazipata na kisha kuzidukua ili aweze kunasa mazungumzo yao, na cha zaidi alichokifanya ni kudukua barua pepe zao.

***http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kwenye barua pepe hizo ndipo Godwin alipopata kila kitu alichokuwa akikihitaji, aliuona uovu mkubwa uliokuwa ukifanyika kwa wachungaji hao. Hakutaka kuvumilia, watu wengi walikuwa wakiangamia pasipo kujua kwamba watumishi hao wa Mungu walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuwachukulia pesa zao.

Alitaka kuweka kila kitu wazi, alitaka Tanzania na dunia nzima ifahamu kile kilichokuwa kikiendelea hivyo kuwaambia Watanzania kwamba alikuwa akitaka kuzitoa taarifa hizo, tena zikiambatana na ushahidi mkubwa mpaka watu ambao walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuhakikisha kwamba baadhi ya viongozi serikalini walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuwaibia wananchi.

“Nitaanza na Mchungaji Peter Kibatari,” alianza kuandika Godwin na baadaye kuweka picha ya mchungaji huyo na kuandika mambo mengi kuhusu huduma yake, jinsi alivyokuwa akitumika na viongozi wa serikali.

Kila mtu aliyekuwa na simu yake mkononi, alikuwa akisoma kila kitu kilichokuwa kimeandikwa. Kila mmoja alimfahamu mchungaji huyo, alikuwa ni mtu mwenye nguvu nchini Tanzania, alipokuwa akihubiri kitu chochote kile kila mtu alikuwa makini kumsikiliza.

Wakati mwingine, watu walikuwa wakitoka nyumbani kwao na kwenda kusikiliza mahubiri kanisani kwake. Alijua kucheza na akili za watu, alikuwa na usanii mkubwa ambao hakukuwa na mchungaji mwingine aliyekuwa nao.

Aliwachanganya watu, alipendwa, alikuwa mtu aliyezungumziwa, kitu cha kushangaza kabisa, kila kiongozi serikalini alikuwa akimzungumzia kwa mazuri, kila kitu kilichokuwa kikizungumziwa juu ya mchungaji huyo, kilizungumziwa kwa uzuri tu.

Watu hawakujua kilichokuwa kikiendelea, hawakujua siri iliyokuwa nyuma ya pazia. Televisheni ya Taifa ndiyo ilikuwa ikimtangaza kila siku kwamba alikuwa mchungaji mwenye nguvu ambaye alitakiwa kusikilizwa na kila mtu.

Maneno mengi ya kisiasa, kuingilia burudani na kuzungumzia kuhusu viongozi wengine wa siasa kuliwafanya hata Waislamu wengine nao kwenda kanisani kwake kusikiliza mahubiri, si kwamba walitaka kuingia katika dini nyingine bali walichokitaka ni kwenda kusikiliza siku hiyo mchungaji huyo alikuwa na umbeya gani.

Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba mchungaji huyo alikuwa akitumika. Serikali ilimtumia, watu zaidi ya elfu tano walikwenda kanisani kwake kila Jumapili, mapato ya sadaka yaliyokuwa yakipatikana yaligawanywa kwa viongozi mbalimbali ambao wao ndiyo waliokuwa wakihusika kumletea washirika wengi.

Viongozi hao wakawa wakinunua magari ya kifahari na kuyaingiza nchini kupitia kanisa la mchungaji huyo, biashara zote haramu kama madawa ya kulevya yalikuwa yakiingizwa nchini kupitia kivuli cha kanisa hilo, mizigo haikuwa ikikaguliwa, ilipita na kila mtu alipokuwa akiuliza, aliambiwa ni msaada kutoka nchini Marekani kwa ajili ya kanisa la Praise And Worship la Mchungaji Kibatari.

“Whaaaat?” (nini?) aliuliza jamaa mmoja, hakuwa akiamini alichokuwa akikiona, yeye mwenyewe alikuwa mshirika mzuri wa kanisa hilo.

“Kumbe Kibatari naye ni mtumishi wa serikali, na si mtumishi wa Mungu kama tunavyojua! Mungu wangu! Ni nini tena hii?” aliuliza mwanamke mmoja.

Kanisa la Praise And Worship likawa limechafuka, kila mshirika wa kanisa hilo akajitokeza na kuweka maoni yake hadharani. Mchungaji Kibatari ambaye alizoea kupigiwa promo kila siku akajitokeza na kuanza kujitetea lakini kujitetea kwake hakukuwa na nafasi hata kidogo kwa kuwa kila siku ushahidi ulikuwa ukiwekwa katika akaunti ile kwamba alikuwa akitumika.

“Kumbe hata Lucy si mke wake!” alisema jamaa mwingine, wote walijiuliza, kila siku mchungaji huyo alimtambulisha mwanamke aitwaye kwa jina la Lucy kama mkewe, kumbe hakuwa mkewe bali ni mwanamke aliyepewa kwa ajili ya kuwa naye kwa lengo la kuangalia mapato ya kanisa kila yalipokuwa yakiingia.

“Jamani! Kweli Lucy si mkewe?” aliuliza mtu mwingine.

Ili kuwaaminisha kwamba kila kitu kilikuwa ni ukweli, Godwin akaweka picha za mwanamke huyo akiingia katika nyumba nyingine nyakati za usiku kuonyesha kwamba alikuwa akienda kulala, kama kweli alikuwa mke wa Mchungaji Kibatari, kwa nini usiku alikuwa akieka kulala nyumba nyingine?

Kulikuwa na walinzi wanne wa nyumbani kwa Kibatari ambao walikufa katika vifo vya kutatanisha! Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba walinzi hao waliuawa kwa kuwa walitaka kutoa siri kwamba Lucy hakuwa mke wa Mchungaji Kibatari? Yaani kila kitu alichokuwa akikiandika Godwin, watu walishangaa mpaka wengine kufikia hatua ya kutotaka kwenda kanisani tena.

“Siwezi kwenda kanisani. Nilidhani nahubiriwa na mchungaji kumbe nahubiriwa na mhuni! Sirudi tena kanisani pale,” alisema mwanamke mmoja huku akionekana kukasirika hasa.

Siri hazikuwa hizo tu, Godwin aliendelea kuzitoa nyingi kuhusu mchungaji huyo, jinsi alivyokuwa akiwatumikia viongozi wa serikali na kuonekana kwamba alikuwa na nguvu kubwa, watu waliokuwa wakianguka mapepo kanisa, walitengenezwa kwa malipo makubwa.

Kwa kuwa kila alipokuwa akifanya mambo mengi makubwa alizungumziwa katika mitandao ya kijamii, hata alipogundulika kwamba alikuwa msanii pia aliandikwa sana katika mitandao hiyohiyo.

Jumapili ya kwanza tangu kashfa kubwa ilipoanza kuzungumziwa kwenye mitandao, hakutaka kwenda kanisani, alijifanya kuumia na hivyo kuomba udhuru kwamba alitaka kusafiri kuelekea nchini Israel kwa ajili ya kumuomba Mungu wake kwani kama kudhiakiwa, alidhiakiwa sana na ulikuwa muda wa Mungu wake wa Mbinguni kumsafisha.

Ilikuwa ni aibu, alipokuwa uwanja wa ndege kwa ajili ya kuondoka kuelekea nchini humo, watu walikuwa wakimwangalia, walimshangaa, hakuonekana kuwa kama mtumishi wa Mungu tena bali alionekana kuwa kama kituko cha mwaka, mtu ambaye alipambana usiku na mchana kuhakikisha anaingiza pesa kwa kutumia migongo ya viongozi wa serikali na kanisa ambalo kila siku alikuwa akiling’ang’ania.

“Nimechafuka sana,” alikuwa akizungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani, Godfrey Kamau ambaye naye alikuwa akimtumia mchungaji huyo kuingiza magari bandarini kwa kutumia kivuli cha kanisa lake.

“Pole sana. Nimeona jinsi yule mtu anavyokuchafua, huu ni wakati ambao hutakiwi kuteteleka,” alisema Kamau.

“Nitapambana na huyu mtu!”

“Utapambana naye? Utaanzia wapi? Hajulikani, halafu inaonekana ni mtu mwenye nguvu sana, kama utaweza kumuomba Mungu na kukuonyeshea mtu huyo, jua tutakuwa nyuma yako,” alisema Kamau wakati alipokuwa akizungumza na Mchungaji Kibatari kwenye simu pasipo kujua kama mazungumzo yao yalikuwa yakidukuliwa na Godwin na kuyarusha moja kwa moja katika akaunti yake kwenye Mtandao wa Instagram.

“Nitamjua tu!” alisema Kibatari na kukata simu.

Kila kitu ambacho walikizungumza kwenye simu, dakika arobaini zilikuwa nyingi sana kuyaona mazungumzo yao kwenye akaunti ile. Kila mmoja alishangaa, wakagundua kwamba simu zao zilikuwa zimedukuliwa na hivyo kuwasiliana na Kampuni ya Simu ya Alcatel na kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea.

Watu wa kampuni hiyo ya simu hawakujua kilichokuwa kikiendelea, hawakujua kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akidukua mawasiliano ya wateja wao. Wakawasiliana na wataalamu kutoka Afrika kusini ambayo nao wakaingia kwenye system kuona kama kulikuwa na mtu alikuwa na uwezo wa kudukua mawasiliano ya wateja wao, hawakubahatika kuona lolote lile.

“Ila Mchungaji Kibatari anasema kwamba mawasiliano yake na mheshimiwa waziri yalidukuliwa. Hebu ingia kwenye akaunti ya Mabadiliko ya Kweli,” alisema mkurugenzi wa kampuni hiyo.

Akaingia na kuangalia, posti alizokutana nazo huko zilihusu mawasiliano baina ya watu hao wawili. Walichanganyikiwa, hawakujua ni kwa namna gani mtu huyo alikuwa ameingia kwenye mitambo yao na kudukua mawasiliano hayo.

Wakati mitandao ya simu ikisumbuka kuziba udukuaji wa mawasiliano ya wateja wao, usalama wa taifa walikuwa mitaani wakimtafuta Godwin. Hawakumfahamu mtu huyo, walikuwa na kazi kubwa mno mbele yao. Kila walipokuwa, waliwaambia watu wawasaidie kumtafuta mtu aliyekuwa akitumia akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ambayo kwao ilionekana kama kuibua vuguvugu la vurugu nchini Tanzania.

“Hakikisheni kwamba mnafanya kila liwezekanalo huyo Godwin anapatikana. Sawa?” alisema mkurugenzi wa usalama wa taifa.

“Sawa.”

Wakati wao wakiendelea kumtafuta Godwin, mwanaume huyo aliendelea kujichimbia, hakutaka kugundulika kwamba yeye ndiye alikuwa mtumiaji wa akaunti hiyo.

Alikuwa mtu wa kushinda Tandale huku kila kitu alichokuwa akikifanya akikifanya chumbani kwake. Baada ya kukaa kwa wiki mbili ndipo alipoamua kuwa mpiga debe katika Kituo cha Daladala cha Makumbusho.

Hakukuwa na mtu aliyemfahamu, alikuwa mgeni kituoni hapo, alionekana kuwa kijana mwenye njaa kali, aliyechoka ambaye mwili wake huku mwili wake ukiwa dhaifu.

Alikuwa mchangamfu, aliyeongea sana, kila siku alipokuwa kituoni hapo alivalia kipensi kichafu, nywele timtim, chini alivaa kandambili zilizokuwa zimechoka huku wakati mwingine vipensi vya jinsi alivyokuwa akivivaa akivifunga kamba badala ya mkanda.

Ilikuwa ni vigumu kujua kwamba huyo ndiye alikuwa kijana aliyewanyima usingizi viongozi wa nchi na viongozi wa dini. Alitafutwa pasipo kujulikana alikuwa vipi. Akaanza kuzoeleka katika kituo hicho, hakuona kama kulikuwa na tatizo lake kujitambulisha kwamba alikuwa akiitwa Godwin, kwa jinsi alivyokuwa, ilikuwa vigumu sana hata kugundua kama mwanaume huyo alikuwa amesoma.

Hayo ndiyo yakawa maisha yake kila siku. Aliendelea kuwatesa viongozi, alionekana kuwa shujaa mkubwa, Watanzania wengi wakataka kumfahamu kwamba alikuwa nani, walitaka kumpongeza, hawakujua kama mtu huyo kila siku walipishana naye katika kituo hicho na hata wakati mwingine kumtukana kila alipowaletea utani wasichana.

Alipokuwa akiendelea kupiga debe katika kituo hicho ndipo alipokutana na msichana aliyeitwa Winfrida, msichana mrembo aliyekuwa akiwatetemesha wanaume wengi chuoni alipokuwa akisoma.

Hakujua lolote kuhusu msichana huyo, hakujua kama alikuwa akimpenda mpaka siku ambayo msichana huyo alimwambia ukweli. Kwanza akacheka sana, ilikuwaje msichana mrembo kama huyo ampende mwanaume kama yeye, mchafu, asiyekuwa na pesa, wakati mwingine akahisi kwamba inawezekana Winfrida alikuwa ofisa wa usalama wa taifa, akakubaliana naye kishingo upande na hivyo kuanza uhusiano wa kimapenzi, ila alikuwa na tahadhari kubwa mno kwani hakutakiwa kumwamini kila mtu.

***

Madaktari katika Hospitali ya Ganga nchini India walikuwa wakibadilishana ndani ya chumba alichokuwa amelazwa Rais Bokasa. Walikuwa wakihangaika kuhakikisha afya ya rais huyo inarudi na kuwa katika hali ya kawaida. Alikuwa kimya, tangu alipofikishwa hospitalini hapo hakuwa akizungumza kitu chochote kile, aliyafumba macho yake na kitu pekee ambacho kiliwaambia kwamba alikuwa hai ni mapigo ya moyo yaliyokuwa yakidunda kwa chini mno.

Mke wake, Bi Consolatha alikata tamaa, hakuona kama mume wake angeweza kufumbua macho yake tena kwani tangu alipokuwa ameanguka na kupoteza fahamu, mpaka siku hiyo alikuwa hivyohivyo, yaani kitandani pale alikuwa kama alivyokuwa ameingia.

Siku ziliendelea kukatika, madaktari walikuwa wakiifuatilia afya yake kwa ukaribu sana. Pale alipokuwa ameanguka, aliumia vibaya kichwani mwake, akatoka damu ambayo iliganda kwa kiasi kidogo katika ubongo wake na hivyo kuwa na hatari ya kupata ugonjwa mmoja kati ya magonjwa matatu.

“Inawezekana atapata kifafa, atapooza mwili wake au kusahau milele kila kitu kilichokuwa kimetokea maishani mwake,” alisema daktari huku akimwangalia Bi Consolatha pamoja na maofisa wa usalama waliokuwa wameongozana naye huko India.

“Jamani mume wangu!” alisema Bi Consolatha huku akilia.

“Tunajitahidi sana, tuna uhakika kwamba hatokufa lakini anaweza kupata tatizo moja kati ya hayo niliyowaambia,” alisema daktari.

“Daktari! Nini kinaendelea?” aliuliza Rais Bokasa mara baada ya kufumbua macho.

Kilichomfahamisha kwamba hapo palikuwa ni hospitali ni mavazi waliyokuwa wamevalia madaktari hao pamoja na kitanda alichokuwa amekilalia. Aliangalia kwa juu aliiona dripu ikiwa inaning’nia.

Hakujua kitu gani kilitokea mpaka kuwa mahali hapo lakini baada ya sekunde kadhaa, akaanza kukumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea. Aliikumbuka meseji aliyokuwa ametumiwa kwamba kiasi cha dola milioni mia moja kilichukuliwa kutoka kwenye akaunti yake iliyokuwa nchini Uswisi, moyo wake ulimuuma mno na hapohapo kitandani alipokuwa akaanza kulia.

Alirudiwa na fahamu lakini mwili wake ukawa na tatizo kubwa la kupooza. Alijaribu kuunyanyua mkono na mguu wake wa kulia lakini vilishindwa kuinuka, alihisi kama kulikuwa na mtu alikuwa amevikandamiza, alishangaa, alijaribu mara kwa mara lakini akashindwa kufanya hivyo.

“Nimepooza! Daktari nimepooza,” alisema Rais Bokasa huku akianza kulia kitandani pale alipokuwa.

Huo ndiyo ulikuwa ukweli wenyewe, kwenye matatizo aliyosema daktari, tatizo la kupooza lilikuwa mojawapo, alishindwa kufanya kitu chochote kile kwa upande wa kulia. Moyo wake ulimuuma, hali hiyo ilimaanisha kwamba kwa miaka yote mpaka kifo chake maisha yake yangekuwa juu ya kiti cha walemavu.

Alilia sana, hata alipomuona mke wake, hakuacha kulia, moyo wake uliumia sana, wakati mwingine alibaki akimuomba Mungu kitandani pale kwa kumtaka kubadilisha kila kitu kwamba maisha yake halisi yaliyokuwa yakiendelea basi yawe ndoto moja ya kusisimua ambapo baada ya muda fulani ashtuke kutoka usingizini.

“Mungu! Fanya kitu, nifanyie muujiza, wewe ni mponyaji, naomba uniponye Mungu wangu,” alisema Rais Bokasa pale kitandani. Kwa kipindi cha shida kama hicho ndicho kilikuwa kipindi cha kumkumbuka Mungu wake.

****

Godwin alihisi kwamba msichana aliyeanza kuzoeana naye alikuwa ni miongoni mwa maofisa wa Usalama wa Taifa. Hakutaka kuzungumza naye sana, kila alipokuwa akimfuata, msichana huyo alikuwa akimbugudhi kwa kumwambia maneno mengi ambayo hakutaka kujali kabisa.

Kila siku Winfrida alikuwa akifika hapo Makumbusho na kutaka kuzungumza naye, haikuwa kazi nyepesi kumzoea Godwin kwani alimuona kila mtu mbele yake akiwa adui mkubwa ambaye alikuwa akimtafuta kwa udi na uvumba.

Alihitaji muda mwingi kumzoea msichana huyo aliyekuwa akisomea mambo ya biashara katika chuo kimoja jijini Dar es Salaam. Marafiki zake waliokuwa katika kituo hicho cha Makumbusho walimuona kuwa mmoja wa watu waliokuwa na bahati kubwa, hawakuamini kama kungekuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa Winfrida kutokea kumpenda Godwin ambaye kwa kumwangalia tu, muonekano wake ulionyesha kwamba alikuwa mhuni asiyekuwa na mbele wala nyuma.

“Ninataka kuzungumza na wewe,” alisema Winfrida huku akimwangalia Godwin aliyekuwa kimya akimwangalia.

“Kuhusu nini?”

“Ninahitaji muda wa kukaa na wewe sehemu. Ninahitaji kuzungumza sana na wewe,” alisema msichana huyo huku akimwangalia Godwin aliyekuwa akionekana kushangaa sana.

“Sina muda.”

“Nakuomba.”

“Kweli sina muda. Unaweza kuniacha nikatafute pesa kwanza?” aliuliza Godwin huku akisimama.

Hakuwahi kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na msichana yeyote yule zaidi ya mwanamke mtu mzima Bi Rachel ambaye mpaka kipindi hicho hakujua mwanamke yule alikuwa akiendeleaje, kama alikuwa hai au alikufa pale hospitalini alipokuwa amemuacha.

Wakati Godwin akiondoka, moyo wa Winfrida ulikuwa ukimuuma sana, hakuamini kama mwanaume huyo alikuwa akiondoka pasipo kumsikiliza alichotaka kumwambia wakati huo, akaondoka mpaka kulipokuwa na magari ya kwenda Gongo la Mboto na kuanza kuita abiria.

Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake ya kila siku, Winfrida hakukoma, kila siku ilikuwa ni lazima kufika mahali hapo na kutaka kuzungumza na Godwin. Mwanaume huyo alikasirika, alimchoka Winfrida kwani kila alipokuwa akija, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutaka kutumia muda mrefu kuwa naye tu.

“Unanikera!” alisema Godwin, hakutaka kumficha msichana huyo.

“Najua! Nisamehe tu ila ninakupenda sana,” alisema Winfrida huku akimwangalia Godwin.

“Unanipenda mimi?”

“Ndiyo!”

“Hivi nilivyo?”

“Mapenzi hayachagui Godwin. Naomba unipende!” alisema Winfrida.

“Siwezi!”

“Nakuomba Godwin. Nakuomba unipende,” alisema msichana huyo, tayari machozi yakaanza kumtoka.

“Nimesema haiwezekani!”

Huo ulikuwa msimamo wake, hakutaka kuwa karibu na msichana huyo hata kidogo. Kila aliporudi nyumbani kwake, alijifungia ndani huku akiwa na rundo la magazeti na kuanza kuyasoma huku akisikiliza mawasiliano ya siri ya namba za simu alizokuwa amezidukua ambazo alikuwa akizirekodi kusikiliza kila kitu kilichokuwa kikiendelea wakati yeye alipokuwa kazini kwake.

“Vijana bado wanaendelea kumtafuta. Halafu nimepata taarifa kwamba vijana wa FIS (The Federal Intelligence Service) walikuwa wameingia nchini Tanzania tayari kwa kuanza kazi yao,” alisikika mkurugenzi wa Usalama wa taifa akimwambia waziri mkuu.

“Safi sana! Sasa hili jambo lisitoke, hutakiwi kumwambia mtu yeyote,” alisikika waziri mkuu.

“Haina shida mkuu!”

Godwin alijua kwamba watu hao walifika nchini Tanzania kumtafuta yeye, si kwa sababu alikuwa akitumia akaunti hiyo bali ni kwa sababu alizihamisha pesa hizo kwenda kwenye akaunti moja nchini Marekani.

Hakutaka kuchelewa, muda huohuo akaingia Instagram na kuwaambia wafuasi wake kwamba kulikuwa na wapelelezi kutoka nchini Uswisi ambao walifika Tanzania kwa ajili ya kumtafuta lakini kamwe wasingeweza kumpata hata kidogo.

Kila mtu alishangaa, mambo hayo yalitakiwa kufanyika kisiri lakini tayari mhusika aliyekuwa akitafutwa tayari alifahamu kila kitu. Watu wengine walishangaa lakini viongozi wengi wakajua kwamba mtu huyo alikuwa amedukua mawasiliano ya waziri mkuu na mkurugenzi wa usalama wa taifa, kumzuia Godwin kupata taarifa lilikuwa jambo gumu sana.

Hakutaka kuishia hapo, ilikuwa ni lazima aendelee kuwaumbua wachungaji wengine, hakuacha, aliwataja wachungaji wengine waliokuwa wakihusika katika kushirikiana na baadhi ya viongozi wakiwemo mawaziri kuwaibia Watanzania pesa zao huku wakati mwingine mtafaruku mkubwa ukitokea baina ya mchungaji na mchungaji mara baada ya kuona wakizidiana katika wingi wa washirika.

****

Kwa kilichokuwa kimetokea, jinsi Godwin alivyokuwa amewachoma wachungaji wengi, washirika wakaanza kupungua makanisani na wengine kuacha kabisa kuelekea huko. Ilikuwa ni sifa mbaya kwa kanisa kwa ujumla, kila mtu alishangaa kwamba ilikuwaje wachungaji waliokuwa wakiwaamini kila siku, kuwatolea mafungu ya kumi na zaka kufanya mambo ya kijinga kama hayo.

Ilikuwa ni vita kubwa, wachungaji wengine wakaamua kuondoka Tanzania na kukimbilia nchi nyingine kujificha, hakukuwa na mchungaji aliyetamani kubaki nchini Tanzania, kila mtu aliondoka kuyaokoa maisha yao kwani tayari kulikuwa na baadhi ya wananchi walikuwa wamepaniki mpaka kufikia hatua ya kutaka kuwamaliza wachungaji hao.

Wakati kila kitu kikionekana kwenda shaghalabaghala hapo ndipo mkurugenzi wa usalama wa taifa akaja na wazo moja kwamba watu wote waliokuwa na jina linaloitwa na Godwin walitakiwa kutekwa kinyemela na kupelekwa sehemu fulani ambapo huko walitakiwa kufanyiwa mahojiano.

Waliamini kwamba kwamba sababu Godwin alikuwa akijiamini kwamba asingeweza kukamatwa ilikuwa ni lazima kutumia jina lake kama kawaida kwa kuwa tu kulikuwa na watu wengi waliokuwa na jina hilo.

Msako huo ukaanza kufanyika kimyakimya. Vijana wengi waliokuwa na jina hilo kwenye mitandao ya kijamii wakaanza kutekwa na kushirikiwa ambapo huko walipolekwa kulikuwa na maswali mengi waliyokuwa wakihojiwa na wakati mwingine wakipigwa ili kusema wao walikuwa wakina nani na kwa nini walikuwa wakiisumbua serikali hiyo.

Rundo la vijana wenye jina hilo walikuwa wakitekwa. Hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua sababu ya vijana hao kupotea ghafla kwani kila kilichokuwa kikiendelea kilifanyika kimyakimya mno. Vyuoni, mitaani na sehemu zingine zote watu waliokuwa na jina la Godwin ilikuwa ni lazima kupotea mazingira ya kutatanisha.

“Kwa Dar es Salaam tuna Godwin mia saba mpaka sasa hivi,” alisema jamaa wa usalama wa taifa.

“Ni wote?”

“Hapana ndiyo tunaendelea kuwatafuta wengine.”

“Basi sawa.”

Godwin hakujua kilichokuwa kikiendelea. Siku moja akiwa katika kituo cha Daladala cha Makumbusho akiendelea na mambo yake akashangaa wanaume wawili waliokuwa na miwani ya jua wakija pale alipokuwa amekaa, hata kabla hajauliza swali lolote lile, mwanaume mmoja akamshika mkono na kumvuta pembeni.

“Jamani kuna nini?” aliuliza Godwin kwa sauti ya kisela tena huku akiwa na kipensi chake na sikioni akiwa na sigara.

“Twende huku!”

“Wapi masela! Mbona mnanishika kibabe washikaji?” aliuliza Godwin huku akiwashangaa watu hao, tayari alihisi kwamba walikuwa usalama wa taifa.

Wakati akiwa anauliza maswali zaidi, akashangaa kuona gari moja aina ya Noah ikija kule alipokuwa, mlango ukafunguliwa, akasukumiwa ndani ya gari na kuondoka mahali hapo huku kila mmoja akishangaa kwamba ilikuwaje mshikaji wao wa nguvu akamatwe kibabe namna ile.

***

Thomas First na Bruno Mendez wakaingia nchini Tanzania kama wapelelezi waliotumwa kutoka nchini Uswis na kwenda Tanzania kwa ajili ya kumtafuta mtu aliyekuwa amehamisha pesa kutoka katika akaunti ya Rais Bokasa na kwenda kwenye akaunti ya hospitali ya St. Lucas nchini Marekani.

Hakukuwa na mtu aliyejua chochote kuhusu watu hao, walionekana kuwa wa kawaida ambapo vibali vyao vyote vilionyesha kwamba waliingia nchini Tanzania kwa ajili ya kutembelea mbuga mbalimbali za wanyama.

Hapo uwanja wa ndege wakachukua teksi ambayo iliwapeleka moja kwa moja mpaka katika Hoteli ya Jumanji iliyokuwa Posta Mpya na kutulia hapo. Vichwa vyao vilikuwa vikifikiria kazi kubwa iliyokuwa mbele yao, hawakujua pa kuanzia lakini waliamini kwamba kama wangekutana na maofisa wa usalama wa taifa basi ingekuwa kazi nyepesi mno kujua ni kit gani walitakiwa kufanya.

Wakakaa katika vyumba tofauti ila kwa kuwa walikuwa na mengi ya kuzungumza, wakatumia chumba kimoja na kuanza kujadili ni kitu gani walitakiwa kufanya. Hawakujua Kiswahili ila kwa kuwa akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ilikuwa hewani na ilikuwa ikifanya kazi kama kawaida, wakataka kuitumia kumpata mtu wao.

Ilionyesha kwamba mtumiaji huyo alikuwa nchini Uingereza, walijua kwamba taarifa hizo hazikuwa sahihi hivyo walichokuwa wakikitaka ni kujua kwanza namba iliyokuwa ikitumika ilikuwa eneo gani kwa kipindi hicho.

“Kwenye hii akaunti ameweka namba yake ambayo inatumiwa na kila mtu anayetaka kumtumia taarifa, nadhani tukianza na hii tunaweza kufanikiwa,” alisema Bruno.

Katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli, Godwin aliweka namba ya simu ambayo ilitumika kwa watu waliokuwa mbali naye kumtumia taarifa za ukweli juu ya kitu kilichokuwa kikiendelea wakati wowote ule, kwa kupitia namba hiyo ya Kimarekani, alitumiwa picha na taarifa zingine ambazo hakuwa akizifahamu.

Alichokifanya Bruno ni kupiga picha na kisha kuituma katika namba hiyo, alipohakikisha kwamba picha imetumwa, akapiga simu mpaka Uswisi ambapo akaomba wawasiliane na watu wa mtandao wa WhatsApp na kuwaambia kuhusu namba ile na picha iliyokuwa imetumwa.

Hilo halikuwa tatizo, mawasiliano yakafanyika. Mara ya kwanza WhatsApp walipoambiwa walikataa kwani hawakutaka kabisa kutoa taarifa za mteja wao yeyote yule, waliwaambia hivyo kwa kuwa hata siku chache zilizopita kampuni ya Apple ilikutana na suala hilohilo la kutoa taarifa za mteja wao katika suala zima la kigaidi lakini wakakataa kufanya hivyo.

Waliwabembeleza mno, tena wakati mwingine kumtumia rais wao na kuwaambia ni kwa jinsi gani walikuwa wakimuhitaji mtu huyo ambaye alionekana kuwa hatari kupita kawaida kwa kufanya muhamala wa kifedha pasipo kibali cha mwenye akaunti.

Baada ya kuambiwa hivyo, WhatsApp wakakubaliana nao na kuwafanyia kile walichotaka kukipata. Wakapewa taarifa kwamba mtumiaji wa namba hiyo hakuwa nchini Marekani kama ilivyokuwa ikionyesha bali alikuwa barani Afrika, nchini Tanzania katika Jiji la Dar es Salaam.

“Dar es Salaam kubwa sana. Tutampataje sasa?” aliuliza Thomas.

“Subirini akifungua picha tutajua yupo wapi. Ila taarifa za mwisho zinaonyesha kwamba yupo ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

“Sawa. Tunasubiri!”

“Haina shida.”





Godwin alikuwa ndani ya gari na wanaume wale, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mahali hapo, aliwaangalia watu hao ndani ya gari lile, alijifanya kushangaa na wakati mwingine kuwauliza kilichokuwa kikiendelea mpaka yeye kukamatwa.

Hakukuwa na mtu aliyemjibu kitu chochote kile, kila mmoja alikuwa kimya huku akionekana kuwa bize na mambo yake. Godwin akaanza kujitetea kwamba yeye hakuwa mwizi, alikuwa mpiga debe na hata hakuwa akivuta bangi zaidi ya kuvuta sigara ambayo nyingine alikuwa nayo sikioni.

Gari liliendeshwa mpaka kufika Kibamba kwenye jumba moja kubwa. Likasimamishwa na kuingizwa ndani ya jumba hilo lililokuwa na eneo kubwa sana ambapo hapo akawakuta wanaume wengine wengi wakiwa humo.

Alishangaa, hakujua kilichokuwa kikiendelea. Kila mtu aliyemuona akiingia, alikuwa akimwangalia, watu hao waliokuwa humo waliendelea kujiuliza maswali juu ya sababu zilizowafanya kuwa mahali hapo.

“Tumefanya nini?” aliuliza jamaa mmoja.

“Sijui! Mimi nilikuwa nachoma mahindi! Washikaji wakaja na kunidaka,” alisema jamaa mmoja.

“Daah! Poapoa! Ngoja tusubiri! Tutajua ukweli. Naitwa nani?” alisema jamaa mmoja.

“Godwin!”

“Godwin?”

“Ndiyo!”

“Hata mimi naitwa Godwin!”

“Duuh! Kama bahati vile, jina hili huwa adimu sana,” alisema jamaa mmoja na mtu aliyekuwa pembeni akasikia na yeye kuwageukia wenzake.

“Kumbe na nyie mnaitwa Godwin! Hata mimi naitwa Godwin,” alisema mwanaume aliyekuwa akiwaangalia.

Mwanzo walihisi kama muujiza fulani lakini walipokuwa wakiwaulizana zaidi wakagundua kwamba kila mmoja aliyekuwa ndani ya jumba hilo alikuwa akiitwa Godwin.

Hapo ndipo wakapata jibu sababu ya kuwa ndani ya jumba hilo. Kulikuwa na mtu aliyekuwa akitafutwa ambaye waliamini kwamba kama wangewakamata watu waliokuwa na jina hilo basi ingekuwa rahisi kwao kusimamisha kile kilichokuwa kikiendelea mitandaoni.

Wakati watu hao wakiwa wamekamatwa na kupelekwa ndani ya jumba lile, huku nyuma maofisa wa usalama walikuwa wakiendelea kufuatilia kuona kama mtu aliyekuwa akitumia akaunti ile alikuwa akiendelea kufanya hivyo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Siku ya kwanza ikapita, ya pili, ya tatu mpaka siku ya nne ambapo hawakumuachia mtu yeyote yule, bado akaunti hiyo haikuwa imetumiwa kuonyesha kwamba mtu waliyekuwa wakimuhitaji alikuwa ndani ya jumba lile.

“Tunahisi mtumiaji wa akaunti hii yupo ndani ya jumba hili,” alisema ofisa mmoja wa usalama wa taifa.

“Sawa. Ila ni nani? Tuna watu zaidi ya mia saba, tutajua yupi ni yupi?” alihoji jamaa mwingine.

“Ni rahisi sana! Tuwe tunaruhusu watu watano halafu tuwe tunaangalia ni kitu gani kitaendelea,” alisema jamaa mwingine na kukubaliana kufanya hivyo.

Wakati hayo yakiendelea, kila mtu aliyekuwa ndani ya jumba lile alijua sababu iliyowapelekea kuwa humo. Godwin alikuwa na wasiwasi tele, aliamini kwamba kama asingekuwa makini basi watu hao wangeweza kugundua kwamba mtu aliyekuwa akitafutwa alikuwa yeye.

Alikuwa muulizaji mkubwa, kila wakati alikuwa mtu wa kuwauliza watu waliokuwa wakiwalinda kwamba nini ilikuwa sababu ya kufika mahali hapo lakini hakukuwa na mtu aliyemjibu chochote kile.

Humo, walikuwa wakiishi vizuri, waliletewa vyakula kila siku, walipewa huduma zote muhimu, nguo na kila kitu walichokuwa wakikihitaji isipokuwa simu tu. Pamoja na kufanyiwa yote hayo lakini bado hakukuwa na mtu aliyekuwa na furaha hata kidogo, kila mmoja alihitaji sana kuwa huru na si kufungiwa humo kama kuku.

Baada ya siku ya tano kuingia ndipo hapo wakaanza kutolewa. Idadi ambayo walikuwa wakitakiwa kutoka ilikuwa ni watu watano. Kabla ya kutoka walikuwa wakipigwa picha na kisha kupelekwa mpaka nyumbani kwao halafu kuwasikilizia kwa siku mbili kuona kama akaunti ile ingeandikwa kitu chochote kile.

“Kwa watano wa kwanza, hakuna mhusika. Hebu tuoneni watano wengine,” alisema mkurugenzi wa usalama wa taifa.

Ilikuwa kazi kubwa na ngumu lakini hawakuwa na jinsi, walichokuwa wakisema ni kwamba walitaka kuiokoa nchi yao kutokana na hali iliyokuwa ikiendelea ambayo walihisi kwamba kama wasingefanya juu chini basi nchi hiyo ingeweza kuchafuka.

Watu walitolewa zaidi, waliendelea kutolewa na baada ya mwezi mmoja na nusu ndipo Godwin ikafika zamu yake na kutolewa ndani ya jumba hilo. Mara baada ya kupigwa picha, yeye na wenzake wanne wakapakizwa ndani ya gari na kuanza kurudishwa nyumbani.

Hakukuwa na aliyejua kama walitakiwa kufuatilia kila walipokuwa wakiondoka, Godwin hakulijua hilo, moyo wake ulikuwa umevimba, alikuwa na dukuduku kubwa moyoni mwake kwamba atakapofika nyumbani ilikuwa ni lazima kuchukua simu yake na kuandika posti ndefu kwa kuwakashifu maofisa wa usalama wa taifa kwamba hawakuwa wakimtisha na kamwe wasingeweza kumgundua hata kama wangefanya nini.

“Nitawaonyesha! Subiri nifike nyumbani.”

Akapelekwa mpaka katika Kidtuo cha Daladala cha Makumbusho alichokuwa amechukuliwa kabla. Washikaji zake wote walikuwa wakimwangalia kwa mshangao, walitaka kufahamu kilichokuwa kimeendelea huko alipochukuliwa na watu wale.

“Walitupeleka sehemu fulani hivi, wapuuzi sana wale,” alisema Godwin.

“Kwa nini walikuchukua wewe tu hapa?”

“Sijajua! Au kwa sababu naonekana navuta bangi!”

“Hapana! Mikono yenyewe laini kama demu, kwa nini wakuhisi hivyo?” aliuliza jamaa mmoja huku akimwangalia Godwin kwa mtazamo ulioonyesha kutamani kusikia ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea huko.

“Sijajua! Niambieni, nimemisi nini kijiweni?” aliuliza Godwin huku akiwatoa watu hao kwenye ishu nzima ya kukamatwa.

“Demu wako alikuwa anakuja sana hapa!”

“Nani? Winfrida?”

“Ndiyo! Anasumbua kinoma, anasema kwenye simu hupatikani. Atakuja tu manake ndiyo mida yake hii,” alisema rafiki yake huyo.

Hakutaka kubaki mahali hapo, hakupenda kuonana na Winfrida na wakati moyo wake ulikuwa na dukuduku kubwa la kuandika kila kitu kilichokuwa kimetokea kule walipokuwa wamepelekwa.

Hakujua kwamba maofisa wale walikuwa wakifautilia kwenye akaunti ile ili kama wangeona posti yoyotesiku hiyo basi wajue kwamba miongoni mwa watu watano waliokuwa wamewaachia siku hiyo, mmojawapo ndiye alikuwa Godwin waliyekuwa wakimtafuta.

Hakuchukua muda mrefu akafika nyumbani, akaichukua simu yake, akaiwasha kisha kuingia Instagram ambapo huko akakutana na maoni mengi ya watu huku wengine wakiuliza maswali alikuwa wapi.

“Nimerudi!” alianza kuandika kwa kusindikizia na picha iliyoonyeshwa minyororo iliyofunga mikono ya watu ikiwa imekatika kumaanisha kwamba alikuwa huru.

Akaanza kuandika ujumbe mrefu hata kabla ya kuposti. Alielezea kila kitu kilichokuwa kimetokea huko, jinsi walivyokuwa wakiishi na hata uzembe waliokuwa nao usalama wa taifa. Alipomaliza, akaisoma posti ile na kujiandaa kuposti, akaifuata sehemu iliyoandikwa ‘share’ tayari kabisa kwa kuipost posti hiyo.

***

Hali ya Rais Bokasa iliendelea kuimarika kitandano alipokuwa, kila alipokumbuka sababu iliyomfanya kuwa kitandani hapo alibaki akilia, hakujua kama kiasi cha pesa kilichoondolewa katika akaunti yake kilirudishwa au la.

Alikuwa akilia, maishani mwake ilikuwa ni afadhali kukosa kitu chochote kile lakini si pesa alizokuwa ameibiwa. Aliiangalia familia yake, alikuwa akisikitika kwani alijua kwamba kama ingetokea siku ambayo angetoka madarakani, basi kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuzitumia pesa hizo na familia yake na ndiyo maana alikuwa ameziiba kwa kipindi kirefu.

Kupata ahueni kwa afya yake ilikuwa taarifa mbaya kwa Watanzania, hawakumpenda, walimchukia mno na katika kipindi chote alichokuwa nchini India, wengi walikuwa wakiombea afariki dunia kidogo ingeweza kuifanya Tanzania kuwa mpya, rushwa ipungue na hata pesa zipatikane kama kipindi cha nyuma.

Akapooza upande mmoja, akawa mtu wakusukumwa katika kibaskeli cha walemavu, hakuwa mzungumzaji sana kama zamani, alitia huruma, alisikitisha mno, yaani rais yule yule, mjanja, aliyekuwa akiwahujumu wananchi wake leo hii alikuwa kwenye kiti cha mataili.

Akaruhusiwa kurudi Tanzania, hakupokelewa kwa shangwe kama ilivyokuwa kwa marais wengine waliopita, alipokelewa kwa manenoo ya kejeli kwenye mitandao ya kijamii huku wengine wakiweka wazi hisia zao kwamba kama ingewezekana basi rais huyo afe hukohuko alipokuwa, ila wengine wakaibuka na kusema kwamba kwa kitendo cha kupooza mwili wake kilionyesha ni kwa jinsi gani Mungu alikuwa amewalipia.

“Bora! Manake alituonea sana, mnapoona Mungu yupo kimya msifikiri ni kiziwi hasikii au kipofu haoni,” aliandika jamaa mmoja pasipo kusema wazi kile kilichokuwa kimetokea, aliandika hivyo kama kuweka utata ili asichukuliwe hatua na sheria za mitandaoni.

Rais Bokasa hakuwa na amani hata kidogo, mawazo yalimtesa na muda mwingi alikuwa akizifikiria pesa zake, zilikuwa nyingi mno na aliamini ili kuzipata tena basi ingemchukua miaka na miaka.

Akaendelea kuwa rais wa Tanzania, kila siku akawa anawasiliana na vijana wake juu ya mahali walipofikia kumtafuta mwanaume aliyemfanya kukosa amani, mwanaume aliyemuibia pesa na kumsababishia matatizo aliyokuwa nayo.

“Yupo wapi?” aliuliza rais huyo.

“Bado hatujampata ila tumefanya jambo moja kubwa sana,” alisikika mkurugenzi wa usalama wa taifa.

“Jambo gani?”

“Tumewakamata wakina Godwin wote Dar es Salaam, na kweli tumefanikiwa kwani mpaka sasa hakuna kitu chochote kilichoandikwa katika ile akaunti,” alisema mkurugenzi huyo.

“Kwa hiyo huyo mwenyewe yupo humo?” aliuliza.

“Tunahisi. Sasa tunataka tuwaruhusu watano kwa siku kadhaa tuone kundi lipi likitoka posti itaandikwa ili tujue cha kuwafanya,” alisema mkurugenzi huyo.

“Wazo zuri! Hakikisheni mnafanya hivyo. Jamani huyo mtu akikamatwa, nitazungumza na majaji anyongwe tu,” alisema Rais Bokasa huku akionekana kuwa na hasira na mwanaume huyo.

Hilo ndilo lililofanyika, kwa kila kundi walilokuwa wakilitoa kazi yao kubwa ilikuwa ni kuangalia kwenye akaunti ile ili kama wataona kuna posti imeandikwa basi wajue kwamba ni kundi hilo ndilo lililohusika na hivyo kuwakamata tena.

Wakati wakiendelea kusikilizia, Godwin alikuwa amemaliza kuandika posti hiyo katika akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ya Instagram na kilichokuwa kikifuatilia ni kuposti posti hiyo.

Alikwishakwenda sehemu iliyoandikwa share lakini hata kabla ya kuposti, akaanza kuingiwa na hofu, akaanza kujiuliza maswali mengi kwamba kwa nini walikuwa wakiruhusiwa watanowatano kwa siku kadhaa, akahisi kitu, akajua kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, tena akahisi kabisa kwamba kama siku hiyo angeandika kwamba ni leoleo basi wangeweza kufuatiliwa, hivyo harakaharaka akabadilisha posti nzima na kuandika ‘Wakina Godwin wengi tulitekwa na watu wanaojidai usalama wa taifa, wiki iliyopita siku ya Jumatatu tukaruhusiwa, nimerudi uswahili pasipo kugundulika, sasa naanza tena kazi’ aliandika na kisha kuposti katika akaunti hiyo.

Kila mtu aliyeiona posti hiyo akafurahia, wengi wakamkaribisha kwa mbwembwe na kumshukuru Mungu kwa kumrudisha tena uraiani na hivyo kuendelea kupambana.

Godwin hakuishia kuandika posti hiyo tu bali alichokifanya ni kuifungua akaunti yake ya WhatsApp, akaona ametumiwa picha kwa namba ngeni, harakaharaka akaifungua na kuanza kuiangalia, ilikuwa picha iliyotoka katika namba ngeni ambayo hakujua kama ilikuwa ni namba ya wale wapelelezi, Thomas First na Bruno Mendez waliotoka nchini Uswisi ambao walitaka kujua alikuwa Tandale sehemu gani.

Usalama wa taifa waliokuwa wakifuatilia walipoiona posti hiyo, haraka sana wakawasiliana na wenzao na kuwaambia kwamba mtu waliyekuwa wamemshikiria na kumuachia alikuwa ameibuka tena na alikuwa katika kundi la watu walioondoka siku ya Jumatano wiki iliyopita.

Hawakutaka kuchelewa, haraka sana wakawasiliana na wenzao na kuwaambia kwamba ilikuwa ni lazima kuwatafuta watu wote waliowaruhusu siku ya Jumatano kwa ajili ya kuwarudisha tena na kubaki nao pasipo kugundua kwamba mtu aliyekuwa ameandika posti hiyo alitolewa siku hiyo kule walipokuwa wamehifadhiwa.

“Hakikisheni wote mnawapata. Si mnazo picha zao?” aliuliza mkurugenzi.

“Ndiyo!”

“Na wote mnajua wanapoishi au vijiwe vyao?”

“Ndiyo!”

“Basi watafuteni,” aliagiza na kisha kukata simu.

****

Moyo wa Winifrida uliendelea kuuma, aliumia kupita kawaida, kila siku alikuwa akienda katika Kituo cha Daladala cha Makumbusho kwa ajili ya kumuona mwanaume wa ndoto yake, mwanaume aliyeuteka moyo wake na kuuburuza vilivyo.

Siku moja alipofika hapo, akaambiwa kwamba Godwin hakuwa mahali hapo, alitekwa na watu wasiojulikana na kuondoka naye. Moyo wake ulichoma, alihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa kumuona mpenzi wake akiwa hai kwani wengi waliokuwa wakitekwa na gari aina ya Noah walikuwa wakiuawa na wakati mwingine kurudishwa wakiwa walemavu.

Akabaki akimuomba Mungu amlinde Godwin huko alipokuwa. Hakuacha kwenda Makumbusho, mara kwa mara alikuwa akienda huko kwa ajili ya kusikilizia kama mpenzi wake alikuwa amerudi au la.

Siku zilikatika mpaka siku ambayo alikwenda huko na kuambiwa kwamba mwanaume huyo alikuwa ameruhusiwa siku hiyo lakini kwa bahati mbaya alikuwa ameondoka na kurudi nyumbani kwake alipokuwa akiishi huko Tandale.

“Naomba mnielekeze,” alisema Winfrida.

“Haina shida!”

Akaanza kuelekezwa alipokuwa akiishi mwanaume huyo, hakutaka kupoteza muda hapo kituoni, akaondoka zake na kuelekea Tandale ambapo aliamini kwamba angemkuta mpenzi wake huko.

Hakuchukua muda mrefu akafika Tandale, akaanza kuulizia mpaka pale alipokutana na mtu aliyekuwa akimfahamu mwanaume huyo na kuanza kumpeleka huko alipokuwa akiishi.

Alipofika katika nyumba hiyo, moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama mwanaume aliyekuwa akimpenda alikuwa akiishi katika nyumba chakavu kama hiyo. Akaingia ndani, akakaribishwa na mwanamke aliyekaa ukumbini akikuna nazi.

“Karibu dada,” alimkaribisha mwanamke huyo.

Akamuulizia Godwin, akaambiwa kwamba alikuwa chumbani kwake, akaonyeshewa mlango na kwenda kugonga, sekunde ishirini nyingi, mlango ukafunguliwa na mwanaume huyo.

Moyo wa Winfrida ukamlipuka, hakuamini kama angeweza kumuona mpenzi wake, akamsogelea na kisha kumkumbatia kwa furaha ambayo ilimzidi na kuanza kumtoa machozi.

“Nimekukumbuka mpenzi,” alisema Winfrida huku akilia kwa furaha.

“Nimekukumbuka pia. Karibu,” alisema Godwin na kuingia naye ndani.

****

Walichokuwa wakikisubiri Thomas First na Bruno Mendez ni kuona picha ile ikipakuliwa na kuonekana mahali alipokuwa mpakuaji huyo. Baada ya kupiga siku kadhaa, wakaona picha ile ikiwa imepakuliwa ambapo moja kwa moja WhatsApp wakawapa eneo la mahali picha hiyo ilipopakuliwa.

“Tandale!” alisema Bruno.

“How can we get there?” (tutafikaje?)

“We have Google Map, let’s roll,” (tuna Google Map, twende) alisema Thomas na kuanza kuondoka kwenda huko.

Kutumia programu hiyo ya Google Map iliwarahisishia kupafahamu mahali walipokuwa wakielekea. Walichukua teksi na kuelekea huko ambapo hawakuchukua muda mrefu wakafika na kuendelea kuifuata simu yao ambayo ilionyesha mahali Godwin alipokuwa.

“We are hundred metre from red dot,” (tupo umbali wa mita mia moja kutoka kwenye kidoti chekundu) alisema Thomas huku wakiiangalia simu yao iliyoweza kuidukua simu ya Godwin, kidoti chekundu ndicho kilichokuwa kikionyesha mahali simu ya Godwin ilipokuwa.

Walitembea kwa mwendo wa haraka, kitendo cha kuwasiliana na WhatsApp na kuwaambia kwamba mwanaume huyo alikuwa Tandale na tena kuwapa ramani ya kumpata kwa kutumia simu yake iliwapa unafuu kupita kawaida.

Hawakuchukua muda mrefu wakafika nje ya nyumba moja na kusimama kwa nje, kidoti kilisema kwamba mtumiaji wa simu hiyo alikuwa ndani ya nyumba hiyo. Wakatoa bastola zao, hata watu waliokuwa hapo nje hawakutaka kuzungumza nao, wakaingia ndani, kitu walichokuwa wakikitaka ni kumkamata Godwin ambaye walihisi kwamba alikuwa ndani ya nyumba hiyo.

Wakatembea mpaka kulipokuwa na chumba ambacho kilionyesha kwamba ndani ya nyumba hiyo ndipo kulipokuwa na mtu huyo, walipotega sikio, wakasikia mwanaume na mwanamke wakizungumza ndani ya chumba hicho, hawakuwa na wasiwasi, hapohapo kwa teke moja tu, wakavunja mlango na kuingia ndani huku bastola zikiwa mikononi mwao.

“You are under arrest,” (upo chini ya ulinzi) alisema Thomas huku akiwa ameshika bastola yake, mwanaume huyo aliyeshika simu akaanza kutetemeka kwa hofu, akatamani kukimbia, akashindwa, alitamani hata kujificha chini ya kitanda, napo akashindwa, msichana aliyekuwa pembeni yake ambaye alikuwa mpenzi wake, akabaki akilia tu.

***

Mkurugenzi wa usalama wa Taifa Tanzania, Bwana Idrisa alikuwa na taarifa za kuwepo kwa maofisa wa Usalama wa Taifa wa nchini Uswisi nchini Tanzania lakini kitu cha ajabu kabisa mpaka kipindi hicho hakuwa amepewa taarifa juu ya mahali walipokuwa watu hao.

Akawasiliana na vijana wake kwa lengo la kutaka kujua mahali walipofikia maofisa hao, hilo halikuwa tatizo, wakamwambia mahali walipofikia na hivyo kuwatuma kwenda huko kwani alitaka kuzungumza nao hata kabla hawajaanza kazi ya kumtafuta Godwin.

Vijana wake wakaelekea huko lakini hawakuweza kuruhusiwa kwani watu hao walikataa kuonana nao na hivyo kuambiwa kurudi kesho. Hilo halikuwa tatizo, wakampa taarifa Idrisa ambaye akakubaliana nao na hivyo siku iliyofuata kurudi tena.

“Waliondoka,” alisema dada wa mapokezi.

“Kwenda wapi?”

“Walinionyeshea ramani, wakasema Tandale, ila sijajua Tandale sehemu gani,” alisema daa huyo, aliambiwa mahali walipokuwa wakielekea Thomas na mwenzake kwa kumuonyeshea ramani hata kabla ya kuchukua teksi.

Hawakutaka kubaki mahali hapo, wakahisi kwamba kulikuwa na kitu mahali huko hivyo nao kuanza kwenda Tandale. Hawakuchukua muda mrefu wakafika, hawakujua wanaume hao walipokuwa wameelekea, walitaka kuuliza lakini hawakujua wangeuliza kwa jinsi gani ili waweze kuwapata.

Wakati wakiangalia huku na kule, wakaliona kundi la vijana, wakaona hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yao ya kuwauliza kwani kwa jinsi walivyokuwa wengi, iliwezekana kuwauliza kuhusu Wazungu na wakapata kitu cha kuwaambia. Walipowakaribia, vijana hao nao walikuwa bize kuzunungumzia habari ambayo ikawafanya kusogea zaidi.

“Aisee! Wale Wazungu kama Arnold na Rambo. Kwanza wapo seriazi sana, halafu ile miwani, cheki zile bastola walizokuwa nazo, kitu cha Hollywood kabisa,” alisema jamaa mmoja, alikuwa akiwaambia wenzake.

“Kweli kabisa. Mhuni alivyotulia, anabaki analialia tu. Sasa sijui kwa nini wamekwenda kumkamata msela, au anauza madawa ya kulevya?” aliuliza mwingine.

Mpaka kufikia hapo maofisa wa usalama wa taifa wakaona kabisa kwamba hakukuwa na kazi kwao kuwatafuta wanaume hao, walichokifanya ni kuendelea kusikiliza kwani mwisho wa siku wangesema mahali walipokuwa.

“Sasa wanampeleka Marekani au?” aliuliza jamaa mmoja.

“Sijajua. Wameanza na hapo kituoni, sasa sijui nini kitaendelea. Ila ishu ilikuwa kama muvi la kibabe vile,” alisema jamaa mwingine.

Hawakutaka kuuliza, wakajua kwamba Wazungu hao walikuwa wameelekea katika Kituo cha Polisi cha Tandale na hivyo kuanza kwenda huko. Gari liliendeshwa kwa mwendo wa kasi, lilipita Tandale Sokoni kama lilikuwa kwenye mashindano ya magari kiasi kwamba kila mtu alikuwa akishangaa.

Ni ndani ya dakika mbili tu tayari walikuwa wamefika kituoni hapo, wakateremka na kuanza kwenda ndani ambapo wakawakuta Thomas na Bruno wakiwa kituoni hapo, wakawasalimia na kujitambulisha, hawakuishia hapo, wakataka kuonana na mkuu wa kituo na kuzungumza naye.

“Imekuwaje?” aliuliza jamaa mmoja, huyu aliitwa Issa.

“Hawa Wazungu wamemleta mtuhumiwa hapa,” alijibu mkuu wa kituo.

“Mtuhumiwa wa nini?”

“Si unajua ile ishu ya Godwin wa mtandaoni?”

“Ndiyo!”

“Ndiyo wamemleta. Wameniambia kwamba walikuwa wakifuatilia simu yake kwa kutumia GPS na hatimaye waliweza kubaini kwamba alikuwa Tandale na ndiyo maana wamekuja naye hapa,” alijibu mkuu wa kituo.

“Godwin?”

“Ndiyo! Wamefanikiwa kumpata!”

“Hebu tumuone!”

****

Kwa jinsi walivyoonekana, Thomas na Bruno walikuwa na hasira kali, walimwangalia mwanaume waliyekuwa wamemvamia chumbani kwake na kumchukua mzobemzobe na kutopka naye ndani huku wakimwacha mwanamke yule akilia ndani ya chumba kile.

Watu kutoka sehemu nyingine wakashangaa, hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea, hawakujua wale Wazungu walikuwa wakina nani na kwa nini walikuwa wakimkamata mwanaume huyo aliyejulikana Tandale kwa ukorofi na ulevi kupindukia.

Kwa jinsi Wazungu wale walivyoonekana, hawakuwa watu wa mchezomchezo hata kidogo, mikononi mwao walikuwa na bastola huku wakiwa wamevaa miwani hali iliyoonyesha hawakutaka kusogelewa hata kidogo.

Walimchukua mtu wao, wakamuingiza ndani ya teksi na kumwambia dereva kwamba walitakiwa kupelekwa kituo cha polisi.

“Braza! Waambie mimi sijafanya jambo lolote lile. Braza, waambie braza watakuwa wananionea tu,” alisema mwanaume huyo huku akilia, hakupigwa, ila kwa jinsi alivyokuwa ameshikwa wakati akipelekwa ndani ya gari, alishikwa kwa staili iliyomuumiza nyonga.

Dereva hakujibu kitu, alinyamaza tu mpaka walipofika kituoni ambapo wakamshusha kwa staili ileile iliyompa maumivu makali na kumpeleka kituoni ambapo walitoa maelezo yote kuhusu mwanaume huyo huku wakisema kwamba ilikuwa ni lazima kusafirishwa na kupelekwa nchini Uswisi haraka iwezekanavyo.

“Okey! Let’s loc him up,” (sawa! Acha tumfunge kwanza) alisema mkuu wa kituo.

Walichokifanya ni kuwasiliana na mkuu wao nchini Uswisi na kumwambia kwamba walifanikiwa kumpata Godwin aliyekuwa amejifungia uswahili Tandale kitu kilichomfurahisha kila mmoja na kuona kwamba kazi kubwa waliyokuwa nayo ilikuwa imefanikiwa kwa asilimia mia moja.

Mpaka Issa na wenzake wanafika kituoni hapo, tayari zilikuwa zimepita dakika ishirini, wakaambiwa kila kitu na kuhitaji kumuona Godwin na hivyo kuruhusiwa, walipomuona, hawakuamini kama kijana huyo angeweza kuisumbua serikali kiasi hicho, na hawakuamini kama kwa jinsi alivyokuwa alikuwa na uwezo hata wa kuwasha kompyuta.

“Yaani wewe ndiye umetusumbua sana mpaka rais wetu kupooza, hakika kiama chako kimefika,” alisema Issa huku akionekana kuwa na hasira mno.

“Braza sijafanya kitu. Braza...braza watasha wananionea, sijafanya kitu,” alisema mwanaume huyo huku akilia kama mtoto.

Hakukuwa na mtu aliyejali kitu chochote kile, walichokijua ni kwamba huyo ndiye mtu waliyekuwa wakimuhitaji, haraka sana mawasiliano yakafanyika, rais Bokasa akaambiwa kwamba Godwin alikuwa amepatikana.

Kwa jinsi alivyokuwa na hamu ya kumuona, hakutaka hata kubaki ikulu, akaagiza kwamba kijana huyo abakizwe hapohapo na yeye kwenda huko kituoni, alikuwa na hasira naye mno, alikuwa na uwezo wa kumnyonga hata siku hiyo ila kwa kuuwa Wazungu wale walikuwa na kazi naye, akaamua kumwangalia kwa hasira sana huku akiwa haamini kama kijana huyo ndiye aliyewasumbua namna hiyo.

“Ninahitaji pesa zangu! Ninahitaji pesa zangu, kwa jinsi ulivyozichukua kwenye akaunti yangu, zirudishe mulemule,” alisema rais mara baada ya kufika katika kituo hicho.

Thomas na Bruno hawakutaka kuzungumza jambo lolote lile, walichokuwa wakikihitaji ni kumchukua kijana huyo na kuondoka naye kuelekea nchinii Uswisi kwa ajili ya kufunguliwa kesi na kuzirudisha pesa zile katika akaunti aliyokuwa amezichukua.

Siku iliyofuata, kijana huyo akapandishwa ndani ya ndege. Siku hiyo ilikuwa ni hatari, kila kona stori zilikuwa zimetapakaa kwamba Godwin alikuwa amekamatwa, kwenye mitandao ya kijamii, stori zilikuwa ni Godwin ambapo taarifa hizo ziliendelea kusoma kwamba mtu huyo alikuwa njiani kuelekea nchini Uswisi.

Kila mmoja alisikitika, Godwin alikuwa shujaa wao, wengine walilalamika mpaka kulia, kwa jinsi mwanaume huyo alivyoonekana, alionekana kuwa shujaa mkubwa ambaye alitakiwa kupewa heshima kwani alikuwa na uchungu mpaka kuanza kuikosoa serikali pale ilipokuwa ikikosea.

“Kwa hiyo Mabadiliko ya Kweli ndiyo basi tena?” aliuliza jamaa mmoja.

“Ndiyo! Wazungu wamekuja kumkamata na kuondoka naye. Wale jamaa noma sana, sijui walimpataje!” alisema jamaa mmoja huku akionekana kushangaa.

Ndege ilichukua saa kumi na sita ndipo ikafika nchini Uswisi ambapo maofisa wa usalama wa taifa nchini humo, FIS walikuwa wakiwasubiria mahali hapo. Mtu huyo alipoteremshwa, akapakizwa ndani ya gari na kuanza kupelekwa sehemu kwa ajili ya mahojiano maalum.

“A man from Tanzania who stole more than $100m in Geneva Bank is under arrest,” (Mtu kutoka nchini Tanzania aliyeiibia Benki ya Geneva dola milioni mia moja amekamatwa) yalikuwa ni maneno makubwa yaliyosomeka katika televisheni wakati Kituo cha Redio cha CNN kilipokuwa kikiitangaza habari hiyo kwa mbwembwe nyingi.

****

“Guys...guys...come and look at this...” Jamani hebu njooni muone hii kitu) alisikika mwanaume mmoja aliyekalia mbele ya kompyuta yake, alikuwa akiwaita wenzake waliokuwa kwenye kompyuta nyingine.

“What is it?” (kuna nini?)

“Another $80m transferred from one account in Geneva Bank to American bank. Ooh my God! It is transferred in the same account,” (Pesa nyingine, dola milioni themanini kutoka kwenye akaunti moja ya Benki ya Geneva imehamishwa kwenda kwenye Benki ya Marekani. Ooh Mungu wangu! Imepelekwa kwenye akaunti ileile) alisema jamaa huyo wa kitengo cha IT katika Benki ya Geneva.

Kila mtu alichanganyikiwa, hawakuamini kilichokuwa kimetokea, haraka sana wakaangalia mmiliki wa akaunti hiyo, alikuwa mteja aliyeitwa Cosmas Buberwa, Mtanzania aliyekuwa na nyadhifa ya Uwaziri wa Nishati na Madini.

Wakampigia simu mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Peterson na kumwambia kilichotokea ambapo hata yeye mwenyewe alichanganyikiwa kwani kwa jinsi alivyokuwa ameambiwa, jinsi tukio lilivyokuwa, hata virusi vilivyokuwa vimecheza na data base ilionyesha kwamba alikuwa mtu yuleyule.

“How is it possible? He is under arrest already,” (inawezekanaje? Tayari amekwishakamatwa)

Alichokifanya ni kuwasiliana na mkurugenzi wa usalama wa taifa hapo Uswisi, Bwana Henrik Kom na kumwambia kilichokuwa kimetokea katika benki yao kwamba kulikuwa na pesa zingine zilizokuwa zimehamishwa kinyemela kwenda kwenye akaunti ileile nchini Marekani na inaonekana mhusika wa mwanzo ndiye yuleyule.

“It is impossibe, we have him here,” (haiwezekani! Tunaye hapa) alisema Bwana Kom huku akionekana kuchanganyikiwa.

***

Moyo wa Godwin ulikuwa kwenye maswali mengi, hakujua ni mtu gani alikuwa amemuelekeza msichana Winfrida nyumbani hapo. Hakutaka ukaribu naye kwani alihisi kwamba hakuwa mtu mzuri hata kidogo, alihisi kwamba angeweza kufanya jambo lolote lile baya kwa ajili ya kumkamatisha kwa polisi ambao kila siku walihangaika kila kona kumtafuta.

Alichokifanya, kitu cha kwanza ni kulog off akaunti zake za Mabadiliko ya Kweli kwenye Mtandao wa Instagram na Facebook kisha kuendelea na stori kwa kisingizio kwamba hata kama kungetokea kitu gani huko lingekuwa jambo gumu kwa msichana huyo kujua kwamba aliyekuwa akizungumza naye ndiye yule aliyekuwa mtu hatari katika kucheza na kompyuta.

Alibaki na msichana huyo chumbani kwake, walikuwa wakiangaliana tu na wakati mwingine walikuwa wakizungumza mambo mengi tangu siku ya kwanza kukutana na mpaka siku hiyo. Kila mtu alionekana kuwa na furaha lakini wakati mwingine Godwin alionekana kuwa na hofu kubwa.

Hakujua sababu, baada ya dakika kadhaa akamwambia Winfrida amsubiri kwa kuwa alitaka kwenda kumnunulia kinywaji, akamwambia kinywaji alichokuwa akikihitaji na mwanaume huyo kutoka kuelekea dukani huku akiwa na simu yake.

Akaondoka na kuelekea dukani. Wakati huo ilikuwa ni saa 1:15 usiku, alipofika katika kichochoro kimoja, macho yake yakatua kwa kijana aliyesimama mbele yake huku akiwa ameshika panga. Kijana huyo alikuwa akihitaji kitu kimoja, kuachiwa kila kitu alichokuwa nacho Godwin na kisha kuondoka zake.

Alibaki akitetemeka, matukio ya kihuni yaliyokuwa yakitokea Tandale yalimfanya kuogopa zaidi. Alitaka kukimbia lakini akashindwa kufanya hivyo kwani kijana yule alikuwa amemfikia na alichokifanya, hapohapo akampekua mifukoni, akamkuta na pesa kiasi cha shilingi elfu kumi na simu.

Wakati akiwa ametulia, mwanaume mwingine akatokea nyuma yake, naye alikuwa na panga, wakamuweka mtu kati, hakutakiwa kufanya lolote lile.

“Mtoto wa mama unatembea na elfu kumi tu! Nyie wengine ndiyo mnatufanya tuwaue, mwanaume mzima unatembeaje na elfu kumi?” alihoji kijana huyo huku akimchukulia simu yake.

“Nisamehe bro.”

“Siku nyingine nikikukuta na elfu kumi nakucharanga mapanga,” alisema kijana huyo, akachukua simu na kuondoka nayo.

Hiyo ikawa salama yake, hakutaka kujuta kupokonywa vitu bali alichokuwa akikihitaji ni maisha yake tu. Walipoondoka, hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo bali walichokifanya ni kuondoka zako.

Vijana hao ndiyo waliotafuta mtu wa kumuuzia simu hiyo, asubuhi sana tayari walikuwa wamempata mteja na kumuuzia simu hiyo, mteja wa hapohapo Tandale na ndiye ambaye huyohuyo alikamatwa kwa kuwa simu hiyo ilionyesha signo kwamba ilikuwa ikitumika mahali fulani, na bila kujua wakamkamata kijana aliyeuziwa simu hiyo kwa kudhani kwamba alikuwa Godwin waliyekuwa wakimtafuta.

****

Waziri wa Nishati na Madini, Bwana Buberwa alichanganyikiwa, hakuamini kilichokuwa kimetokea, alitumiwa ujumbe mfupi kwa njia ya simu akishukuriwa kwa kuchangia kiasi cha dola milioni themanini, zaidi ya bilioni mia moja sitini kutoka katika Hospitali ya St. Lucas iliyokuwa nchini Marekani.

Baada ya kuupokea ujumbe huo, akatulia katika sofa lake sebuleni, mkono wake akaupeleka kwenye sehemu ya moyo na kuanza kupumua juujuu, presha ilikuwa ikipanda, kiasi ambacho kilichukuliwa katika akaunti yake nchini Uswisi kilikuwa kikubwa mno na hakujua ni kwa jinsi gani angeweza kuishi bila pesa hizo.

“Mume wangu kuna nini?” aliuliza mkewe huku akimsogelea, alishangaa kumuona mumewe akiwa kimya, kijasho kikimtoka huku akiwa kwenye hali ambayo haikuwa kumkuta kabla.

Uzuri ni kwamba mkewe alikuwa daktari hivyo alivyoona hali hiyo akajua kwamba mumewe alikuwa na presha iliyopanda ghafla na hivyo kuanza kumpatia huduma.

Alijua kabisa kwamba kilichokuwa kimetokea kilisababishwa na simu ile, alitaka kujua ni kitu gani kilichokuwa kimetumwa katika simu ya mumewe, akaichukua na kuanza kuangalia kuona kulikuwa na kitu gani.

Akaiona meseji ile, akaanza kuisoma, yeye mwenye mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini alichokuwa akikiona, ilikuwaje kupoteza kiasi kikubwa cha pesa tena kwenda kwenye akaunti nyingine ambayo hawakuifahamu? Ni nani alikuwa amehamisha pesa hizo? Wakati akijiuliza maswali hayo ndipo kumbukumbu zikamjia kwamba hata Rais Bokasa naye aliwahi kufanyia hivyohivyo, pesa zake zilikuwa zimechukuliwa na mpaka siku hiyo hakuwa amezipata.

“Mume wangu...mume wangu...” aliita mwanamke huyo lakini alikuwa amechelewa, presha ya mume wake ilipanda kwa kasi kubwa mwilini mwake, moyo wake ukashindwa kuhimili mshtuko mkubwa aliokuwa ameupata, hapohapo kitandani alipokuwepo, akatulia tuli, pumzi ikakata na kufariki dunia huku mkewe akishuhudia.

***

Ulikuwa ni msiba mkubwa, hakukuwa na mtu aliyeamini kama waziri huyo alikuwa amekufa. Watu wengi walikuwa wakijiuliza sababu ya kifo chake lakini hakukuwa na mtu aliyejua kitu chochote kile.

Mkewe alilia, sababu kubwa ya mume wake kufariki ilikuwa siri, hakutaka kuzungumza kitu chochote kile kuhusu ujumbe mfupi wa maneno uliokuwa umetumwa katika simu ya mume wake, alitaka iwe siri lakini akashindwa kuitunza siri hiyo, siku hiyohiyo, tena huku akiwa analia ndipo akataja kilichokuwa kimetokea.

Kila mtu alishangaa, wengi wakajiuliza kuhusu pesa hizo. Buberwa alionekana kuwa mtu mwema, aliyependa maendeleo ya Watanzania, alijificha kwa mwamvuli wa utumishi wa Mungu, kila mtu alimwamini kwamba alikuwa mtu aliyependa sana dini na asingeweza kufanya jambo baya kama kuficha pesa katika akaunti moja huko nchini Uswisi.

Hata kabla ya watu hawajamaliza msiba tayari tetesi juu ya kilichomuua Bwana Buberwa kilianza kusikika kwamba alikufa alipopokea ujumbe wa simu uliooonyesha kwamba pesa zake, zaidi ya bilioni mia moja na sitini zilikuwa zimehamishwa kutoka katika akaunti yake huko Uswisi na kupelekwa katika akaunti nyingine nchini Marekani.

“Eeh!” alishangaa jamaa mmoja.

“Kuna nini?”

“Hujasikia kilichomuua mgonjwa?” aliuliza jamaa huyo, alishangaa mno.

“Kitu gani?”

“Kumbe alipata presha baada ya kuona pesa zake zilizokuwa Uswisi zimehamishwa na kupelekwa katika akaunti nyingine! Kama alivyofanyiwa Rais Bokasa!” alisema jamaa huyo.

Hakukuwa na siri tena, kila kitu kilichokuwa kimetokea kilijulikana huku watu wengine katika habari hiyohiyo wakiongeza chumvi kwamba pesa hizo alitaka kununua jumba la kifahari nchini Uswisi.

Wengi hawakuamini kama kweli waziri huyo angeweza kufanya jambo kama hilo. Alionekana kuwa mtu mwema kumbe upande wa pili alikuwa mtu aliyekuwa akipiga madili mengi na pesa kuzikimbizia katika akaunti yake hiyo.

Kwa kuwa pesa hizo zilipotolewa zilipelekwa katika akaunti ileile iliyopelekewa pesa za Rais Bokasa, watu wakajua kwamba mhusika alikuwa yuleyule wa Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli kwenye Mtandao wa Kijamii wa Instagram.

Hilo likaibua gumzo katika mitandao ya kijamii, kila mtu alikuwa akielezea lake, wengi walimpongeza Godwin bila kumfahamu kwamba alikuwa akifanya kazi kubwa ambayo hakukuwa na mtu mwingine ambaye angeweza kuifanya kama alivyokuwa akiifanya.

Rais Bokasa na usalama wa taifa walichanganyikiwa, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, ilikuwaje Waswisi waseme kwamba walimkamata Godwin na kuondoka naye kuelekea nchini Uswisi huku nyuma pesa hizo zikaibiwa katika mazingira yaleyale?

Rais hakutaka kukubaliana nao, akaanza kuamini kwamba mtu aliyekuwa amekamatwa hakuwa Godwin yule waliyekuwa wakimfahamu bali alikuwa mtu mwingine kabisa. Siku hiyohiyo kikao cha dharura kikafanyika akiwepo Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Idrisa, rais alichanganyikiwa kupita kawaida, mbele yake aliona giza kubwa, kitendo cha waziri huyo kuchukuliwa kiasi cha fedha katika akaunti yake ilimaanisha kwamba viongozi wote waliokuwa na akaunti katika Benki ya Geneva pesa zao zingechukuliwa na kupelekwa katika akaunti nyingine.

“Nimewaita hapa niseme kitu kimoja,” alisema rais huku akimwangalia kila mtu aliyekuwa mahali hapo.

“Ndiyo mkuu!”

“Huyu Godwin bado hajapatikana, na inawezekana kabisa wale Waswisi watakuwa wammpata Godwin mwingine,” alisema rais bokasa maneno ambayo kila mtu yalimfanya kushangaa mahali hapo.

Hakukuwa na mtu aliyehisi kwamba Wazungu wangeweza kukosea, walikuwa watu makini katika kazi zao, walikuwa wakimfuatilia Godwin kwa kipindi kirefu na hatimaye kumpata kule Tandale alipokuwa akiishia.

Mazingira ya kukamatwa kwake yalionyeshwa kwamba alikuwa mwenyewe kwani hata simu aliyokuwa akiitumia ilionyesha kwamba ni yeye, sasa ilikuwaje rais aseme kwamba yule aliyekuwa amekamatwa si Godwin na wakati Wazungu walithibisha hilo?

“Mkuu!” aliita Bwana Idrisa.

“Nimesema hivi kwa sababu moja. Au tufanye kwamba yule aliyekamatwa ndiye Godwin, sasa inakuwaje achukue tena pesa kutoka katika akaunti ya Bwana Buberwa?” aliuliza rais kitu kilichomfanya kila mtu kubaki kimya na kuanza kuangaliana kwani kwa kile alichokizungumza rais kilionekana kuwaingia akilini mwao.

“Sasa mkuu kama yule si Godwin! Godwin yupo wapi? Wamechukua simu, hivi kweli tutaweza kumpata? Tutampata kwa njia gani?” aliuliza waziri mkuu huku akimwangalia kila mtu aliyekuwa mahali hapo.

“Jenerali unasemaje hapo?” aliuliza Rais Bokasa.

“Ni habari ambayo inachanganya sana, sijui huyu mtu yupo wapi kwa kweli,” alisema Jenerali

Kikao cha dharura kilikuwa kizito, Godwin alivichangany vichwa vyao kiasi kwamba wakati mwingine walikuwa kimya wakijifikiria ni kitu gani walitakiwa kufanya lakini hawakuwa na majibu yoyote yale.

Muda ulizidi kwenda, wakati kikao kikiendelea, tayari taarifa ikaandikwa kwenye akaunti ile ya Mabadiliko ya Kweli kwamba kulikuwa na kikao kizito kilichokuwa kikiendelea ikulu.

“Guys! This man is back in business,” (Jamani! Huyu jamaa amerudi kazini) alisema waziri mkuu mara baada ya kuangalia kwenye akaunti yake Instagram.

Kila mtu akaingia kwa lengo la kuangalia kilichokuwa kikiendelea. Kila mmoja alishangaa, ilikuwaje mwanaume huyo ajue kwamba kulikuwa na kikao cha siri kilichokuwa kimeitishwa ikulu na wakati hakukuwa na mtu mwingine aliyejua hilo?

“Idrisa, simu yangu walirekebisha ili isidukuliwe, si ndiyo?” aliuliza Rais Bokasa.

“Ndiyo mkuu!”

“Sasa huyu mtu amejuaje?”

“Hata mimi sifahamu!” alijibu Idrisa huku akionekana kuchanganyikiwa.



“Halo! Nazungumza na bilionea Kizota hapo?” lilisikika swali kutoka kwenye simu ya bilionea mkubwa kuliko mabilionea wote nchini Tanzania, Gabriel Kizota.

“Ndiyo! Wewe nani?”

“Naitwa Godwin. Mmiliki wa Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli,” alijibu Godwin jibu lililomfanya bilionea huyo kunyong’onyea, hapohapo akatulia kochini.

“Please!” (tafadhali) alisema, alimjua mtu huyo kupitia mitandao, alikuwa mtu hatari sana.

“Nina taarifa zako nyingi sana, nitaziweka hadharani kama ukitaka. Najua kwamba kila siku ya Alhamisi unafanya mapenzi na mama yako, najua huwezi kubisha hilo. Nina meseji zenu mlizokuwa mkitumiana huku mkiitana bebi. Huwezi kubisha hilo. Nataka nikutane na wewe Mlimani City baadaye mchana, fanya hivyo, vinginevyo utaujua moto wangu mtandaoni,” alisema Godwin.

“Hakuna shida. Nitakuja mkuu!”

“Peke yako. Kuja na polisi kunamaanisha kwamba umevujisha meseji na picha zako,” alisema Godwin.

“Sawa. Mkuu!”

“Iwe saa kumi na mbili jioni. Mlimani City, utaingia katika jumba la sinema, tukutanie huko,” alisema Godwin na kisha kukata simu na kumuacha mzee huyo akiwa kwenye presha kubwa.

***

Godwin alishtuka baada ya kusikia taarifa za Wazungu waliokuwa wamekwenda Tandale na kumkamata kijana mmoja na kuondoka naye. Hakujua kilichokuwa kikiendelea lakini akahusisha tukio hilo na kuibiwa kwake simu usiku uliopita, akawa na hofu kwamba inawezekana Wazungu hao walikuwa wamemfuatilia, walifuatilia mawasiliano yake na kujua mahali alipokuwa.

Akaona kabisa kwamba vita alivyokuwa akipigana havikuwa na Watanzania wenzake tu bali kulikuwa na Wazungu waliokuwa wakimtafuta ambapo hakupata tabu kujua sababu, alijua kwamba kwa kuwa alihamisha pesa zile, basi inawezekana ikawa sababu ya watu hao kumtafuta kila kona.

Hakutaka kuona akikamatwa, kwa kuwa alikoswakoswa alichokifanya ni kuongeza umakini katika matumizi yake ya simu na siku hiyohiyo akaenda kununua simu aina ya iPhone 7, lengo lake kubwa ni kuzuia kutafutwa kwani aliamini simu hizo zilikuwa na ulinzi mkubwa.

Kwa kuwa aliifahamu IMEI namba ya simu yake, kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuifunga, akafuta namba zake katika mtandao na data base ya kampuni iliyotengeneza simu ile, hakutaka kuona mtu yeyote akijua kitu chochote kilichokuwa kikiendelea, baada ya kuhakikisha kwamba simu yake ilikuwa salama na kusingekuwa na mtu ambaye angeweza kufanya lolote, akaanza kuingiza taarifa zake katika simu mpya aliyonunua.

Bado alikuwa na kazi kubwa na viongozi wa Tanzania, aliwachukia, maisha waliyokuwa wakiishi Watanzania masikini yalimuumiza, alitaka kubadilisha kila kitu, alijua kwamba kulikuwa na viongozi wengi waliokuwa na akaunti katika Benki ya Geneva, hivyo alitaka kuzihamisha pesa hizo zote kutoka kwenye akaunti zao.

Hakutaka kuchelewa, akaanza kuingia kwenye data base ya benki ya Geneva na kuanza kuangalia akaunti za viongozi hao. Kuingia katika data base ya benki kubwa kama hiyo halikuwa jambo jepesi, kulikuwa na ugumu mno kwa kuwa kulikuwa na watu wengi, wenye ujuzi wa kompyuta waliokuwa wakilinda kila kitu katika benki hiyo lakini kitu cha ajabu kabisa, Godwin alikuwa akiingia bila hofu yoyote ile.

Alianza na akaunti ya Rais Bokasa, alichokifanya baada ya hiyo ni kuanza kufuatilia akaunti ya mtu mwingine, Waziri Buberwa na kufanya kile alichotaka kukifanya. Akaingia kwenye akaunti ya mwanaume huyo na kugundua kwamba alikuwa na dola za Kimarekani, dola milioni themanini ambazo zilikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni mia moja na sitini, alichokifanya ni kilekile, kuhamisha pesa hizo kwenda kwenye akaunti ya akaunti ya Hospitali ya St. Lucas ya nchini Marekani kisha kumtumia meseji Buberwa kwamba alishukuriwa kwa utu wake aliouonyesha wa kutuma pesa hizo kwenye akaunti ile.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alipomaliza ndipo akapata taarifa kwamba mzee huyo alishikwa na presha, alianguka na baada ya saa chache kufariki dunia. Hakutaka kujali, alichokuwa akikiangalia ni kuhamisha pesa za viongozi hao wote ili hapo baadaye azirudishe kwa Watanzania wenyewe.

Alipoona kwamba akaunti ya hospitali ile haikutakiwa kutolewa pesa yoyote ile, akatengeneza akaunti nyingine kwenye Benki ya Marekani na kuzihamishia pesa hizo katika akaunti yake.

Hilo likawachanganya Wamarekani, hawakuamini kile walichokiona, kwanza kitendo cha akaunti kuanzishwa ghafla na kuhamishiwa kiasi kikubwa cha pesa kikawafanya kuwa na walakini, wakachapisha taarifa ya akaunti hiyo na kuanza kuifuatilia, kwanza wajue ilifunguliwa na nani na kwenye tawi gani la benki hiyo.

“Which branch?” (tawi gani?)

“I don’t find his name. Oh my God! How does he manage to open this account?” (silioni jina lake hapa. Oh Mungu wangu! Amewezaje kufungua akaunti hii?) alijibu jamaa na kuuliza swali lililoonyesha kushangazwa na kile kilichokuwa kimetokea.

Waliiona akaunti hiyo ikiwa imefunguliwa, ilikuwa ikifanya kazi lakini kitu cha ajabu haikuonyesha ilifunguliwa katika tawi gani hapo Marekani. Hilo liliwashangaza, kiasi kikubwa cha pesa kilikuwa kimeingizwa na kilichowashtua zaidi, jina la akaunti hilo lilikuwa People of Tanzania.

Hawakujua ilikuwaje. Walijaribu kuifunga akaunti hiyo, walishindwa kufanya hivyo, wakawasiliana na watu mbalimbali wa kompyuta na kwenda kufanya kazi hiyo lakini cha ajabu kabisa walishindwa kwani mbali na kufunguliwa kwa akaunti hiyo, pia kulikuwa na virusi vilivyokuwa vimewekwa, kama wangeendelea kulazimisha kuifunga akaunti hiyo, virusi vingeingia kwenye data base na kuharibu mafaili.

Wakaangalia taarifa za pesa hizo, waligundua kwamba mara ya kwanza pesa hizo ziliingizwa kwenye akaunti moja ndani ya benki yao na kisha kutolewa na kurudishwa katika Benki ya Geneva, kilichotokea, pesa hizo zikachukuliwa tena huko na kupelekwa kwenye akaunti hiyo, mbali na pesa hizo, pia kulikuwa na dola milioni themanini ambazo nazo zilihamishiwa humo.

“Make a call to Geneva Bank,” (wapigie simu Benki ya Geneva) alisema mkurugenzi wa benki hiyo huku akionekana kuchanganyikiwa.

Mawasiliano yakafanyika na walichoambiwa ni kwamba wao wenyewe walishindwa kabisa kufanya jambo lolote lile kwani mtu aliyekuwa akiwachezea mchezo huo alikuwa mtu hatari sana ila bahati nzuri ni kwamba walikuwa wamemkamata.

“He is very dangerous man!” (ni mtu hatari sana) alisikika jamaa kwenye simu.

Wakati wao wakiendelea kuhangaika, Godwin alikuwa Tandale akiendelea kuwaambia watu kilichokuwa kikiendelea, jinsi alivyokuwa akizihamisha pesa za viongozi mbalimbali kwenye akaunti zao kule Uswisi kwamba hata kama viongozi wengine wangejaribu kwenda kuchukua pesa zao, wasingeweza kwa kuwa alikuwa amezifunga akaunti hizo.

“Nimefunga akaunti zao, hakuna atakayeweza kutoa au kuingiza pesa. Si wao tu, bali hata benki yenyewe haiwezi kufanya hivyo,” aliandika Godwin kwenye akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli.

Kila Mtanzania alifurahi, waliibiwa sana pesa zao na viongozi wao, kitendo cha Godwin kuibuka na kucheza mchezo huo kila mtu alimsifia kwani alikuwa akiwasaidia kwa kuzificha pesa za kodi zao ambazo zilikuwa zikiibwa kila siku na viongozi hao.

Baada ya kufuatilia mazungumzo kwa njia ya simu, akagundua kwamba hata Jenerali Ojuku Abraham alikuwa akihusika katika kuihujumu nchi kwa kujilimbikizia mali na pesa nyingi katika benki tofautitofauti nchini Tanzania. Alitaka kumkomesha, alitaka kumuondoa katika nafasi aliyokuwa nayo, aibuke hadharani na kusema kwamba hakuwa na imani na rais hivyo kuachia cheo hicho cha ukubwa wa majeshi Tanzania, kitu pekee alichokifikiria Godwin ni kuiteka familia ya jenerali huyo.

“Nani anaweza kuifanya kazi hii?” alijiuliza.

Jina la bilionea Kizota likamjia kichwani mwake, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kufuatilia mawasiliano yake kwa njia ya simu na meseji, alichokigundua kilimshangaza, hakuamini alichokuwa akikiona kwamba mwanaume huyo alikuwa akifanya mapenzi na mama yake hali iliyomfanya kupata utajiri mkubwa, mbali na kufanya uchafu huo pia alikuwa akiua watu kama njia ya kuwatoa kafara.

Ilimshangaza, utajiri mkubwa aliokuwa nao mwanaume huyo ulikuwa ni utajiri wa damu, hivyo alichokifanya ni kumpigia simu na kumwambia uchafu wote na kutaka kuonana naye.

Bilionea huyo alikuwa akitetemeka, muda wa kuonana na Godwin ulipofika, akaingia ndani ya gari lake huku akiwa na kofia kubwa na miwani, hakutaka kugundulika, walinzi walimshangaa, dereva wake hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mpaka bosi wake kukataa kwenda na mtu mwingine.

Hakuchukua muda mrefu akafika Mlimani City, akateremka na kuelekea kulipokuwa na mlango wa kuingilia kisha kwenda katika jumba la sinema alilokuwa ameambiwa. Alipofika, akachukua tiketi na kuingia ndani. Aliangalia huku na kule, hakumuona mtu yeyote yule, akakaa huku akiangalia macho yake huku na kule.

“Samahani mzee!” alisema kijana mmoja, alikuwa amemfuata mzee huyo. Akayainua macho yake na kumwangalia.

“Bila samahani!”

“Kuna mtu ameniambia nikuletee hii simu yako uliidondosha,” alisema kijana yule.

“Niliidondosha?”

“Kwa maelezo ya mtu huyo.”

“Sawa. Nashukuru!”

Alijua kilichokuwa kikiendelea, si kwamba aliidondosha bali iliwezekana Godwin alitaka kuzungumza naye. Wakati ameishika simu hiyo, ikaanza kuita, haraka sana kaipokea.

“Kuna maagizo tu ninataka kukupa,” alisikika Godwin kwenye simu.

“Niambie chochote kile nitafanya!” alisema mzee huyo huku akitetemeka.

“Ninahitaji uiteke familia ya Jenerali Ojuku.”

“Unasemaje?”

“Nadhani umenisikia. Una siku tatu za kufanya hivyo. Ukishindwa basi nitakwenda kutoa siri hiyo, tena haiishii hapo, bali nitasema mpaka mabasi yako yanavyoua watu na kuwatoa kafara,” alisema Godwin.

“Nitawezaje kuiteka familia ya Jenerali Ojuku?”

“Wewe ni bilionea. Utaweza tu. Kama ukishindwa basi picha zako na mama yako mkiwa kitandani zitakuwa mtandaoni. Kama hutaki kuziona picha hizo, basi fanya kazi yangu. Una siku tatu tu,” alisema Godwin na kukata simu.

“Halo..halo..halo..” aliita mzee huyo huku akikiangalia kioo cha simu hiyo.

Machozi yalikuwa yakibubujika mashavuni mwake, hakuamini alichokuwa ameambiwa, alitetemeka na muda wote alikuwa akilia kwa uchungu, kazi aliyokuwa amepewa ilikuwa ngumu, hakujua pa kuanzia, siku tatu alizokuwa amepewa zilionekana kuwa chache sana kuifanya kazi hiyo.

Kuiteka familia ya Jenerali Ojuku ilikuwa kazi kubwa, lakini kwa kuwa ilikuwa ni amri, hakuwa na jinsi, alitakiwa kuifanya kwa haraka sana vinginevyo angekwenda kudhalilika baada ya siku tatu pasipo kazi hiyo kufanyika.

“Why me? God why me?” (kwa nini mimi? Mungu kwa nini mimi?) aliuliza huku akiendelea kulia, japokuwa ndani ya ukumbi ule kulikuwa na kiyoyozi kilichokuwa kikipiga kiasi cha watu wengine kuingia na makoti kwa ajili ya baridi, lakini yeye ndiyo kwanza kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.

***

Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa nchini Uswisi, Henrik Koma alikuwa amechanganyikiwa mno, hakuamini kile alichokuwa akikiona.

Aliwatuma vijana wake mpaka nchini Tanzania kwa ajili ya kumkamata mtu aliyekuwa akihamisha pesa kutoka katika Benki ya Geneva na kisha kutamba katika mitandao ya kijamii, vijana hao wakaondoka mpaka huko, wakafuatilia mawasiliano kwa njia ya simu na kumkamata kijana huyo.

Waliondoka naye mpaka nchuni Uswisi, walijua kwamba walikuwa wamemaliza kila kitu lakini kitu cha ajabu kabisa, akaunti ile iliendelea kuandikwa na la kushangaza, kukawa na akaunti nyingine benki ambayo ilichukuliwa pesa.

Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, kijana yule ambaye alipelekwa kwenye chumba cha mahojiano aliyejitambulisha kwa jina la Ally Mneke aliwaambia polisi kwamba hakuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta na hakujua sababu iliyomfanya mpaka Thomas na Bruno kwenda kumkamata.

“Where did you find this phone?” (uliipata wapi simu hii?) aliuliza mwanaume mmoja aliyevalia suti nyeusi ambaye alikaa nyuma ya meza ya mahojiano.

“Someone came and gave me,” (kuna mtu alikuja na kunipa) alijibu Ally.

“Where did he get it?” (aliipata wapi?)

“He robbed someone,” (alimuibia mtu)

Kila alipokuwa akiulizwa, alijibu huku akionekana kuwa na uhakika na kile alichokuwa akikizungumza, hakujua kitu chochote kile, kila alichokuwa akiwaambia watu hao ndicho ambacho alikuwa na uhakika nacho.

Mtu aliyekwenda kumuuzia alikuwa mhuni wa mtaani, alipopelekewa, hakujua ni kwa namna gani mtu huyo aliipata ila alikuwa na uhakika kwamba aliiba sehemu fulani kwani bei yake ilikuwa tofauti na gharama yake.

Walikuwa na simu hiyo, walitaka kufuatilia kila kitu kilichokuwa kimetokea lakini jambo la ajabu kabisa, simu hiyo ilikuwa imefungwa. Walijitahidi kuifungua lakini wakashindwa, walichokifanya ni kuwasiliana na Kampuni ya Orange ambayo ndiyo iliyotengeneza simu ile kwa ajili ya kuwaambia waifungue lakini kitu kilichowastaajabisha ni kwamba namba ya simu hiyo haikuwa ikionekana katika data base yao.

“Unasemaje?” aliuliza Kom.

“Hatuna simu yenye IMEI hiyo. Iangalieni vizuri, ni Orange?” aliuliza mwanaume aliyesikika kutoka upande wa pili.

“Ni Orange!”

“Siyo Nokia au Samsung?”

“Hapana! Ni Orange!”

“Mbona hatuna simu yenye namba hiyo!”

Mpaka kufikia hapo Kom akawa na uhakika kwamba mwanaume huyo alikuwa amecheza mchezo mchafu wa kuifuta simu ile katika data base ya kampuni hiyo ya simu. Moyo wake ulimuuma mno, walionekana kuchezewa mchezo mchafu mno.

Aliwaangalia wenzake waliokuwa ndani ya chumba kile, aliwaona kama hawakuwa wakifanya kazi kwani kulikuwa na ugumu gani kumkamata mtu mmoja aliyekuwa akiwasumbua kwa kiasi kikubwa mno.

Malalamiko yalikuwa mengi, kwa jinsi pesa zilivyokuwa zikichukuliwa katika Benki ya Geneva ikawafanya watu wengi kuwa na mashaka na pesa zao huko hivyo wengi kutaka kujiondoa kwani kwa jinsi hali ilivyokuwa walihisi kwamba baada ya mtu huyo kuwaibia pesa watu hao, angehamia kwao.

Idadi ya wateja waliojiengua katika benki hiyo ikawa kubwa, mashirika mbalimbali yakajitoa, wafanyabiashara wengi wenye pesa nyingi nao wakajitoa, beki ikaingia hasara kubwa kwa kipindi kifupi sana hali iliyowafanya usalama wa taifa nchini humo, FIS kuwa na hasira zaidi ya kumtaka mtu huyo.

“Take him back,” (mrudisheni)

Hawakuwa na jinsi, Ally alitakiwa kurudishwa nchini Tanzania kwani hakuwa yule mtu waliyekuwa wakimuhitaji, walimkamata lakini cha ajabu bado pesa zilikuwa zikichukuliwa na mtu huyo hivyo kugundua kwamba huyo hakuwa mwenyewe.

****

Bilionea Kizota alichanganyikiwa lakini hakuwa na jinsi, kile alichoambiwa kilikuwa ni lazima kifanyike haraka sana. Mbele yake aliuona ugumu mkubwa lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima afanye kile alichoambiwa kwa kuwa tu kama asingefanikiwa kufanya hivyo ilikuwa ni lazima picha zake akiwa na mama yake faragha kuchapishwa katika mitandao ya kijamii.

Akawapigia simu vijana wake, alitaka kazi ya kuiteka familia ya Jenerali Ojuku ifanyike sana kwani alikuwa na siku tatu tu, kama isingefanyika basi ingeonekana kwamba amefeli kile alichotakiwa kufanya.

Vijana wawili wakaelekea nyumbani kwake, hao ndiyo walikuwa vijana aliowatumia kwa ajili ya kufanya matukio mbalimbali hasa kwa watu waliokuwa wakimsumbua. Akawaambia kile kilichotakiwa kufanywa, kila mmoja alishangaa, hawakujua sababu iliyomfanya bosi wao huyo kuchukua uamuzi huo kwani kuiteka familia ya Jenerali Ojuku lilikuwa jambo la hatari sana.

“Kuna nini mkuu! Mbona ni uamuzi mgumu sana huo?” aliuliza Sao, alikuwa mmoja wa vijana wake.

“Nina kazi nao. Kuna kitu kimetokea, ninahitaji kazi ifanyike haraka sana,” aliagiza Kizota.

“Basi haina shida mkuu!”

“Tuna siku tatu. Naomba jambo hili lifanyike kati ya leo, kesho, keshokutwa mwisho,” alisema Bwana Kizota.

“Haina shida mkuu!” alisema kijana wake mwingine, Abdallaman na kisha kuondoka mahali hapo.

****

Bi Matilda alikuwa ndani ya gari lake na watoto wake wawili wakielekea Mlimani City kwa ajili ya kunuunua baadhi ya bidhaa kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Alikuwa makini barabarani, redioni aliweka wimbo wa Injili wa Utanitambuaje ulioimbwa na mwimbaji Bonny Mwaitege. Hakuwa na habari kwamba nyuma yake kulikuwa na gari lililokuwa likimfuatilia, alikuwa bize kuangalia mbele na hata wakati mwingine alipokuwa akiliona gari hilo kwa kupitia kioo cha mbele, hakuwa na hofu hata kidogo.

Japokuwa alikuwa mke wa mtu mkubwa nchini Tanzania lakini hakukuwa na kitu ambacho hakuwa akikipenda kama kutembea akiwa na ulinzi, alizungumza sana na mumewe kwamba hakutaka mlinzi kwa kuwa alimwamini Mungu wake kwamba angemlinda katika kila kona alipokuwa akienda.

Mumewe, Jenerali Ojuku hakutaka kukubaliana naye, alimwambia kabisa kwamba hakutakiwa kujiamini kwamba watu wangeweza kufanya jambo lolote lile tena wakati wowote ule lakini mwanamke huyo alikataa katakata.

Hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kukubaliana naye tu. Miaka mingi ikapita, hakukuwa na jambo baya lolote lile lililotokea kitu kilichomfanya kuamini kwamba kweli hakukuwa na kitu kibaya chochote kile na kama angemuwekea ulinzi ingekuwa kama kumnyima uhuru wake.

Siku hiyo ambayo hakuwa akiitegemea alikuwa njiani kuelekea huko Mlimani City, hakuonekana kuwa na hofu mpaka alipoingia ndani ya eneo la jengo hilo kubwa. Bila kuwa na hofu, akateremka huku akiwa na watoto wake wawili mapacha wenye miaka kumi na mbili na kuanza kuelekea humo ndani.

Akafanya manunuzi yake yaliyochukua saa moja ndani ya jengo hilo kubwa na kutoka kuelekea sehemu alipopaki gari lake, alipofika, akafungua mlango wa nyuma, akaingiza vitu vyake kisha kufungua milango mingine kwa ajili ya kuondoka.

Wakati akiwa amewasha gari na kufunga kioo cha mlango wa mbele upande wake, akashtuka kumuona mwanaume mmoja mwenye sura yenye tabasamu pana akikigonga kioo chake kwa lengo la kukifungua.

Hakuona kama kulikuwa na tatizo, akashusha kioo chake tena huku akimrudishia tabasamu mwanaume huyo ambaye akamuuliza kuhusu kadi yake ya kuingilia ndani ya eneo hilo.

“Ulipewa kadi mama?” aliuliza mwanaume huyo.

“Ndiyo! Hii hapa.”

“Na lisiti ulipewa ndani baada ya kufanya manunuzi?” aliuliza.

“Ndiyo! Hizi hapa baba yangu!” alisema Bi Matilda huku akifungua mkoba wake na kutoa lisiti na kumuonyeshea kijana yule.

Wakati akizungumza naye pasipo kujua kama kijana huyo alikuwa mbaya wake, akatokea mwanaume mwingine, akamsogelea yule aliyekuwa akizungumza naye, akatoa bastola yake na kumuonyeshea mulemule garini huku akimtaka kutulia kabisa.

“Tunaomba utulie, ila fanya hivyo kama tu utatamani kuiona siku ya kesho,” alisema kijana huyo aliyefika mahali hapo, na yule mwingine naye akatoa bastola.

“Naomba msiniue...” alisema Bi Matilda huku akitetemeka.

“Hatuna mpango wa kukua, ila ukitaka, tutakuua tu kwani hiyo ndiyo kazi yetu kubwa. Kakae kiti kile kule,” alisema jamaa huyo, haraka sana mwanamke huyo akasogea katika kiti kile kingine na kutulia, kijama mmoja akaingia ndani, akashikilia usukani huku mwingine akipanda nyuma kukaa na watoto.

“Relax mama! Ukionyesha kutetemeka, nakuapia kwa Muungu wangu, nakuua,” alisema kijana aliyeshikilia usukani na kuanza kuliondoa gari hilo mahali hapo ambapo mbele kidogo dereva akatakiwa kutoa kadi, akatoa na kisha kuruhusiwa.

Watoto wake ambao walikuwa wakishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea nao walikuwa wakitetemeka, mbele yao waliviona vifo vyao, wanaume waliokuwa wameingia ndani ya gari lao walionekana kuwa watu hatari wasiokuwa na mchezo hata kidogo.

Wakati wakiwa njiani, wakawafunga vitambaa machoni na kisha kueendelea nasafari yao mpaka Tegeta, gari likasimama ndani ya eneo la jumba moja kubwa na kisha kuteremkshwa na kuanza kupelekwa ndani.

“Naomba msituue...naomba msituue,” alisema mwanamke huyo huku akiwa ameshikwa kwa nyuma na watoto wake.

“Wala msijali! Mtakuwa hai kabisa, ila mume wako asipofanya kile tunachokitaka, kesho atakuta maiti zenu ufukweni,” alisema Abdallahman huku wakiwaingiza ndani ya chumba kimoja ambacho kwa muonekano wake tu kilionekana kuwa chumba kilichojaa mateso makubwa.

“Jamani naomba msituue,” aliendelea kusema mwanamke huyo, wakatolewa vitambaa na kisha mlango kufungwa huku wakiwaacha watatu hao wakiwa wamekumbatiana, kwa jinsi hali ya chumba ilivyokuwa, ilionyesha kabisa kwamba kama wangetoka salama, basi ilikuwa ni bahati yao.

***

Bilionea Kizota akapigiwa simu na vijana wake na kuambiwa kwamba kile alichokitaka kilikuwa kimefanyika, familia ya Jenerali Ojuku ilikuwa imetekwa na kuhifadhiwa sehemu salama kabisa.

Hilo lilimfurahisha, hakutaka kuchelewa, hapohapo akampigia simu Godwin na kumwambia kwamba kazi kubwa aliyokuwa amempa ilikamilika kwa asilimia mia moja hivyo alikuwa na wajibu wa kunyamaza na kutokuzisambaza picha hizo.

Godwin akafurahi, kitu pekee alichomwambia ni kwamba alitakiwa kuishikilia familia hiyo zaidi na hakutakiwa kuiachia huru mpaka pale ambapo angemwambia kwamba alitakiwa kufanya hivyo.

“Hilo halina tatizo. Ila naomba usiziweke picha hizo kwenye mitandao ya kijamii,” alisema Bilionea Kizota huku akizungumza kwa njia ya simu na Godwin.

“Wala usijali! Nitumie picha za watu hao.”

Hilo nalo halikuwa tatizo hata kidogo, akawapigia simu vijana wake na kuwaambia waipige picha familia hiyo na kisha kumtumia Godwin ambaye akazichukua na kuzihifadhi katika kompyuta yake. Hakutaka kuchelewa, hapohapo akaiunganisha simu yake kwa kupitia simu ya kibandani ya mitaani ambayo moja kwa moja ilipiga mpaka katika namba ya Jenerali Ojuku kwa lengo la kuzungumza naye.

Mwanaume huyo alipopigiwa simu hiyo, akakiangalia kioo cha simu yake, alishangaa kuona akipigiwa na namba ngeni, tena simu ya mtaani iliyokuwa katika mabanda ambayo ilikuwa ikitumika kipindi cha nyuma. Haraka sana akapokea.

“Nadhani utakuwa umeshangazwa na simu hii. Kwa kifupi ni kwamba ninataka ujue kwamba nina familia yako, na muda wowote ule ninaiteketeza na maiti zao kuzitupa baharini,” alisema Godwin maneno ambayo yalimfanya Jenerali Ojuku kushtuka.

“Wewe nani?”

“Si lazima unijue. Ila jua familia yako ninayo. Nakutumia picha zao wakiwa chimbo wakisubiri vifo vyao,” alisema Godwin na kukata simu.

Ojuku akachanganyikiwa, hakuamini kile alichokisikia, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu mke wake, simu haikuwa ikipatikana, akampigia simu dada wa nyumbani ambaye alimwambia kwamba mama aliondoka kuelekea Mlimani City kufanya manunuzi ya chakula huku akiwa na watoto.

“Waliondoka muda gani?” aliuliza.

“Tangu saa tano asubuhi!” alijibu msichana huyo, Ojuku alipoangalia simu yake, ilikuwa saa kumi jioni.

Akachanganyikiwa zaidi, hakuamini alichokuwa ameambiwa, hapohapo akashtukia simu yake ikiwa imeingia ujumbe mfupi, akafungua, ujumbe huo ulikuwa ni kwenye akaunti yake ya WhatsApp ambapo alipoifungua, akakutana na picha za familia yake, mke wake na watoto wake wakiwa wamefungwa katika chumba kimoja kilichokuwa na mwanga hafifu huku wakilia na tena wakiwa wamekumbatiana.

“Nimekutumia picha zao kuona sura zao za mwisho,” aliandika Godwin kwenye mtandao uleule. Hapohapo Ojuku akampigia simu kwa lengo la kuongea naye, amwambie alikuwa akitaka nini lakini si kuiangamiza familia yake.

“Niambie unataka nini!” alisema Ojuku.

Ilikuwa vigumu kuamini kama mwanaume huyo alikuwa Jenerali nchini Tanzania, pale alipokuwa amesimama alikuwa akitoka jasho jingi, mwili wake ulikuwa ukitetemeka na alionekana kuogopa mno.

Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, ujasiri wote aliokuwa nao ukapotea, aliishiwa nguvu na kwa jinsi hali ilivyoonekana, kama angejifanya kiburi basi ilikuwa ni lazima familia yake iuawe kama zilivyouawa familia za watu wengine.

Hakutaka kuona hulo likitokea, alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile kuiokoa familia yake. Alimuomba sana Godwin aiache familia yake kwani ndiyo ilikuwa kila kitu maishani mwake lakini mwanaume huyo hakutaka kukubaliana naye hata kidogo, alisisitiza kwamba ilikuwa ni lazima aiangamize na kamwe asingeweza kujua mahali familia hiyo ilipokuwa.

“Nakuomba kaka yangu....nakuomba sana,” alisema Ojuku huku akitetemeka, alihisi presha ikianza kupanda.

“Nakupa saa mbili za kuifikiria familia yako, umuhimu wake kuwa pamoja nawe, baada ya hapo, nitaimaliza. Mtu yeyote akijua kama familia yako imetekwa, ni lazima niiue tena haraka sana,” alisema Godwin na kukata simu.

***

Bilionea Kizota akapigiwa simu na vijana wake na kuambiwa kwamba kile alichokitaka kilikuwa kimefanyika, familia ya Jenerali Ojuku ilikuwa imetekwa na kuhifadhiwa sehemu salama kabisa.

Hilo lilimfurahisha, hakutaka kuchelewa, hapohapo akampigia simu Godwin na kumwambia kwamba kazi kubwa aliyokuwa amempa ilikamilika kwa asilimia mia moja hivyo alikuwa na wajibu wa kunyamaza na kutokuzisambaza picha hizo.

Godwin akafurahi, kitu pekee alichomwambia ni kwamba alitakiwa kuishikilia familia hiyo zaidi na hakutakiwa kuiachia huru mpaka pale ambapo angemwambia kwamba alitakiwa kufanya hivyo.

“Hilo halina tatizo. Ila naomba usiziweke picha hizo kwenye mitandao ya kijamii,” alisema Bilionea Kizota huku akizungumza kwa njia ya simu na Godwin.

“Wala usijali! Nitumie picha za watu hao.”

Hilo nalo halikuwa tatizo hata kidogo, akawapigia simu vijana wake na kuwaambia waipige picha familia hiyo na kisha kumtumia Godwin ambaye akazichukua na kuzihifadhi katika kompyuta yake.

Hakutaka kuchelewa, hapohapo akaiunganisha simu yake kwa kupitia simu ya kibandani ya mitaani ambayo moja kwa moja ilipiga mpaka katika namba ya Jenerali Ojuku kwa lengo la kuzungumza naye.

Mwanaume huyo alipopigiwa simu hiyo, akakiangalia kioo cha simu yake, alishangaa kuona akipigiwa na namba ngeni, tena simu ya mtaani iliyokuwa katika mabanda ambayo ilikuwa ikitumika kipindi cha nyuma. Haraka sana akapokea.

“Nadhani utakuwa umeshangazwa na simu hii. Kwa kifupi ni kwamba ninataka ujue kwamba nina familia yako, na muda wowote ule ninaiteketeza na maiti zao kuzitupa baharini,” alisema Godwin maneno ambayo yalimfanya Jenerali Ojuku kushtuka.

“Wewe nani?”

“Si lazima unijue. Ila jua familia yako ninayo. Nakutumia picha zao wakiwa chimbo wakisubiri vifo vyao,” alisema Godwin na kukata simu.

Ojuku akachanganyikiwa, hakuamini kile alichokisikia, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu mke wake, simu haikuwa ikipatikana, akampigia simu dada wa nyumbani ambaye alimwambia kwamba mama aliondoka kuelekea Mlimani City kufanya manunuzi ya chakula huku akiwa na watoto.

“Waliondoka muda gani?” aliuliza.

“Tangu saa tano asubuhi!” alijibu msichana huyo, Ojuku alipoangalia simu yake, ilikuwa saa kumi jioni. Akachanganyikiwa zaidi, hakuamini alichokuwa ameambiwa, hapohapo akashtukia simu yake ikiwa imeingia ujumbe mfupi, akafungua, ujumbe huo ulikuwa ni kwenye akaunti yake ya WhatsApp ambapo alipoifungua, akakutana na picha za familia yake, mke wake na watoto wake wakiwa wamefungwa katika chumba kimoja kilichokuwa na mwanga hafifu huku wakilia na tena wakiwa wamekumbatiana.

“Nimekutumia picha zao kuona sura zao za mwisho,” aliandika Godwin kwenye mtandao uleule. Hapohapo Ojuku akampigia simu kwa lengo la kuongea naye, amwambie alikuwa akitaka nini lakini si kuiangamiza familia yake.

“Niambie unataka nini!” alisema Ojuku. Ilikuwa vigumu kuamini kama mwanaume huyo alikuwa Jenerali nchini Tanzania, pale alipokuwa amesimama alikuwa akitoka jasho jingi, mwili wake ulikuwa ukitetemeka na alionekana kuogopa mno.

Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, ujasiri wote aliokuwa nao ukapotea, aliishiwa nguvu na kwa jinsi hali ilivyoonekana, kama angejifanya kiburi basi ilikuwa ni lazima familia yake iuawe kama zilivyouawa familia za watu wengine.

Hakutaka kuona hulo likitokea, alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile kuiokoa familia yake. Alimuomba sana Godwin aiache familia yake kwani ndiyo ilikuwa kila kitu maishani mwake lakini mwanaume huyo hakutaka kukubaliana naye hata kidogo, alisisitiza kwamba ilikuwa ni lazima aiangamize na kamwe asingeweza kujua mahali familia hiyo ilipokuwa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Nakuomba kaka yangu....nakuomba sana,” alisema Ojuku huku akitetemeka, alihisi presha ikianza kupanda.

“Nakupa saa mbili za kuifikiria familia yako, umuhimu wake kuwa pamoja nawe, baada ya hapo, nitaimaliza. Mtu yeyote akijua kama familia yako imetekwa, ni lazima niiue tena haraka sana,” alisema Godwin na kukata simu.

Ojuku alikuwa akitetemeka, hakuamini kile alichokuwa ameambiwa, alipewa saa mbili za kuifikiria familia yake, aliifikiria kwa kina na baada ya muda huo akapigiwa simu na mwanaume huyo na kuambiwa kwamba kulikuwa na kazi alitakiwa kuifanya kwa nguvu zote vinginevyo angeishuhudia familia yake ikiteketezwa na miili yao kutiupwa baharini.

“Nipo tayari kufanya lolote lile. Nipo tayari kwa ajili ya familia yangu,” alisema Ojuku kiasi kwamba ilikuwa vigumu kuamini kama alikuwa Jenerali wa Jeshi la Wananchi.

Alichoambiwa ni kwamba kulikuwa na kazi kubwa alitakiwa kuifanya, kazi ya kuiteka familia ya Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Noel. Alitakiwa kujipanga vilivyo na kuifanya kazi hiyo haraka sana.

Ilikuwa kazi ngumu na kubwa kuifanya, hakujua kama angeweza kufanya hivyo kwani aliijua familia hiyo, ilikuwa ikilindwa na maofisa wengi wa usalama wa taifa. Alichoambiwa ni kwamba alitakiwa kuifanya kwa nguvu zote na hakutakiwa kutoa sababu zozote zile kwani kama angefanya hivyo ilikuwa ni lazima kuishuhudia familia yake ikiuawa na kutumiwa video.

“Nitafanya hivyo!”

“Una siku tatu tu!” alisema Godwin na kukata simu.

****

Moyo wa Godwin ukaridhika, hakuamini kama alifanikiwa kupanga mipango yake ambayo mpaka muda huo ilionekana ikienda kutimia. Kitu alichokifanya kwa haraka sana ni kuchukua simu yake na kisha kuandika posti katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli na kuwaeleza watu kwamba hatimaye Rais Bokasa alikuwa njiani kupinduliwa kitu ambacho kilimfanya kila mtu kuwa na furaha tele.

Hiyo ndiyo ilikuwa habari ya jiji, kila mtu aliyeisoma posti hiyo kwenye akaunti hiyo akaenda kuandika katika akaunti yake kwamba hatimaye rais huyo alikuwa njiani kupinduliwa kitu ambacho watu wengi kiliwafurahisha kwani tangu walipoanza kuifuatilia akaunti hiyo, hakukuwa na taarifa yoyote ya uongo ambayo iliwahi kuandikwa.

“Kama kweli huyu kiumbe atakwenda kupinduliwa, ni lazima nitachinja kuku,” alisema jamaa mmoja huku akionekanna kuwa na furaha tele.

“Hunishindi mimi. Nafikiri nitakunywa sana pombe, nilewe mpaka nivue nguo,” alisema jamaa mwingine huku akiwa ameshika simu yake akiisoma mara kwa posti ile iliyokuwa imeandikwa.

“Ila wewe si umeokoka!”

“Kuokoka ndiyo nini kwa jambo kama hili? Mama yangu alikufa hospitalini kwa sababu hakukuwa na dawa. Yaani nina hasira naye huyu,” alisema jamaa huyo.

Mara baada ya Rais Bokasa kupata ujumbe kuhusu posti ile iliyokuwa imeandikwa katika akaunti ile akachanganyikiwa, akapewa simu na kuiangalia kwa macho yake, hakuamini kile alichokuwa akikiona, alijua fika kwamba kila kitu kilichokuwa kikiendelea Godwin alikuwa akikifahamu, kwa sababu alikuwa na akaunti iliyokuwa na watu wengi, akahisi kabisa kwamba kulikuwa na watu alikuwa akiwapanga kwa ajili ya kumpindua.

Hakutaka kuona hilo likitokea, haraka sana akawasiliana na Jenerali Ojuku, Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel, Jaji mkuu, spika wa bunge na waziri mkuu. Alitaka kuzungumza nao juu ya kile kilichokuwa kimeandikwa, kama jeshi la Tanzania, Ojuku alitakiwa kuweka ulinzi wa nguvu kuhakikisha hakuna majeshi mengine yatakayoingia kwa ajili ya kumpindua.

“Haiwezekani! Ni lazima tusimame kuitetea nchi yetu na kunitetea Amiri Jeshi Mkuu! Ni lazima ulinzi uongezeke. Waziri mkuu zungumza na jeshi la polisi, waambie ulinzi usambazwe kila kona,” alisema Rais Bokasa huku akiwaangalia watu aliokuwa amewaita.

Akili yake ilimwambia kwamba kupinduliwa kwa jeshi ilikuwa ni lazima jeshi moja litoke nchi nyingine na kwenda kuvamia na kumtoa madarakani, hakuhisi kwamba jeshi lake hilohilo lingetumika kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Ojuku alikuwa kimya, kichwa chake kilikuwa kikiifikiria familia yake, alichanganyikiwa, ilikuwa ni lazima aiteke familia ya Noel na kuificha sehemu ili kuikoa familia yake isiweze kuuawa na mwanaume huyo ambaye alionekana kuwa mbaya wake.

Kikao cha dharura kilipomalizika, haraka sana Ojuku akarudi nyumbani ambapo aliendelea kupanga mipango yake. Aliipenda sana familia yake, hakutaka kuona ikiuawa hivyo ilikuwa ni lazima kufanya kile alichoambiwa akifanye, tena haraka sana.

Akawaita wanajeshi watatu, makomandoo na kuwapa kazi hiyo. Alipewa onyo kwamba kazi ilitakiwa kufanyika pasipo mtu yeyote kujua kama familia hiyo ilitekwa na kufichwa, hivyo alitakiwa kuwa makini kabisa.

“Ila nyumba yake ina ulinzi, tutaiteka vipi?” aliuliza komando mmoja.

“Hapa ndipo kwenye ugumu. Hebu subiri,” alisema Ojuku na kuondoka kuelekea chumbani.

Hakuwa sawa hata kidogo, kule chumbani akachukua simu na kumpigia Godwin, akamuuliza kwamba iliwezekanaje wafanye tukio la utekaji pasipo mtu yeyote kugundua kama familia hiyo ilikuwa imetekwa?

“Ni jambo rahisi sana. Nyumbani kwake kuna ulinzi wa Usalama wa Taifa. Msimamizi mkubwa wa ulinzi ni Andrew Carlos, unachotakiwa, iteke familia ya Andrew kwanza,” alisema Godwin, alikuwa akimpampango kabambe mwanaume huyo.

“Sawa. Halafu?”

“Baada ya hapo, niambie nimpigie simu aruhusu mchezo fulani uchezwe nyumbani hapo,” alisema Godwin.

“Mchezo gani?”

“Fanya hilo kwanza!”

“Sawa mkuu!” aliitikia Jenerali Ojuku kiheshima kwani alijua kwamba mtu huyo alikuwa na familia yake, hivyo ilikuwa ni lazima kumuheshimu.

***

Jenerali Ojuku akawapanga vijana wake kwamba ilikuwa ni lazima kuhakikisha familia ya Andrew inatekwa kwani yeye ndiye aliyekuwa kiongozi wa ulinzi na usalama katika nyumba ya Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel.

Hilo halikuwa tatizo. Kitu cha kwanza kabisa walichotaka kukifahamu ni mahali alipokuwa akiishi Andrew, wakawasiliana na ofisa mmoja wa Usalama wa Taifa ambaye hakuwa akijua chochote kile kilichokuwa kimepangwa, alipoulizwa mahali alipokuwa akiishi, akawaambia kwamba alikuwa akiishi Masaki hivyo walitakiwa kwenda huko.

Lengo kubwa la kwenda huko lilikuwa ni kuonana na mke wake, kuzungumza naye huku wakionekana kama kulikuwa na jambo limetokea, na wakati wakiwa katika hilo, Godwin alikuwa na kazi ya kuifunga simu ya Andrew, isiweze kutumika kwa kuingiza simu wala kutoa.

Kupapata nyumbani kwake hakukuwa na ugumu wowote ule, walifanikiwa na kuingia huku wakitaka kuonana na mwanaume huyo. Kwa jinsi walivyovaa, gwanda za kijeshi na hata kofia zilizoonyesha kwamba walikuwa makomando, hakukuwa na mtu aliyekuwa na hofu nao.

“Hayupo, aliondoka kwenda kazini!” alijibu mke wake.

“Basi sawa.”

“Kuna tatizo?”

“Lipo lakini tunakwenda, tutarudi tena baadaye,” alisema komando mmoja na kuondoka mahali hapo.

Mkewe, Selena akabaki na walakini, akahisi kwamba kulikuwa na tatizo lakini wanaume wale hawakutaka kumwambia ukweli. Akachukua simu yake kwa lengo la kumpigia lakini kitu cha ajabu kabisa simu haikuwa ikipatikana.

Hiyo haikuwa kawaida, mumewe hakuwa mtu wa kuzima simu, muda wote simu yake ilikuwa hewani, kwa nini azime simu hiyo? Hilo likazidi kumuingizia hofu moyoni mwake na kuwa na uhakika kwamba kweli kulikuwa na tatizo.

Wakati makomando walipotoka, wakawasiliana na Ojuku na kumwambia kwamba waliondoka nyumbani kwa Andrew. Ojuku akachukua simu na kumpigia Godwin na kumwambia kwamba kile alichokitaka tayari kilikuwa kimefanyika.

“Sawa. Subiri nitakwambia nini cha kufanya,” alisikika Godwin.

Hapohapo Godwin akaiunganisha simu ya Andrew ambayo alikuwa ameifunga na kisha kumpigia Selena kwa ajili ya kuzungumza naye. Kule alipokuwa, Selena alipoona simu ya mumewe ikiingia, haraka sana akainyanyua kwa lengo la kuzungumza naye, alitaka kujua kilichokuwa kikiendelea kwani moyo wake haukuwa na amani hata kidogo.

“Mume wangu! Nini kinaendelea?” aliuliza Selena huku simu ikiwa sikioni.

“Huzungumzi na mumeo. Unazungumza na Dk. Amani wa Hospitali ya Mwananyamala,” alijibu Godwin kwa kupitia namba ileile ya Andrew.

“Dokta! Mungu wangu! Naomba usinipe habari mbaya. Niambie mume wangu yupo wapi,” alisema Selena huku akianza kulia kwani kitendo cha kusikia kwamba mtu aliyekuwa akizungumza naye upande wa pili alikuwa daktari, akachanganyikiwa.

“Mumeo alipata ajali ya gari, ameletwa hapa Mwananyamala kwa matibabu. Nimechukua simu yake na kuona ameliandika jina lako kama mkewe na ndiyo maana nimekupigia” alijibu Godwin.

“Nakuja...nakuja kumuona mume wangu,” alisema Selena huku akionekana kuchanganyikiwa.

Hapohapo Godwin akakata simu na kumpigia Ojuku na kumwambia kwamba kila kitu kilikuwa tayari na muda wowote mwanamke huyo angeondoka nyumbani kwake hivyo watu wake walitakiwa kumsubiri njiani.

Hilo halikuwa tatizo, akawapigia simu vijana wake na kuwaambia kwamba mwanamke huyo alikuwa akiondoka nyumbani hivyo ilikuwa ni lazima wamteke.

Mpango huo ukaandaliwa, wakati Selena akiondoka nyumbani kwake huku akiwa na watoto wake mapacha waliokuwa na miaka mitano, akaingia ndani ya gari na kuanza kuliendesha kuelekea hospitalini huku akiwa amechanganyikiwa.

Kutoka Masaki mpaka Mwananyamala hakukuwa mbali sana, wakati gari lake likiwa limekata Mwananyamala Vijana, akashangaa kuliona gari jingine likimpita na ghafla kusimama mbele yake, akalisimamisha gari lake.

Wanaume wawili walioshika bunduki wakateremka, miili yao ilikuwa imejazia, walivalia kaoshi za kijeshi, watu walisimama pembeni wakiliangalia tukio hilo, wanaume hao wakapiga risasi nne hewani, kila mtu aliyekuwa mahali hapo akakimbia kuyaokoa maisha yake.

Wakafungua mlango, wakamteremsha mwanamke huyo na watoto wake, wakawaingiza ndani ya gari lao na kuondoka huku mahali hapo kukiwa hakuna mtu hata mmoja, na hata wale waliokuwa baa walikimbia na kuziacha chupa za pombe mezani, kila mmoja alitaka kuyaokoa maisha yake.

Haraka sana wakampigia simu Ojuku na kumwambia kwamba watu aliokuwa akiwataka walikuwa mikononi mwao na walikuwa wakielekea sehemu kwenda kuwahifadhi, Ojuku alipoambiwa hilo, haraka sana akampigia simu Godwin na kumwambia kwamba kile alichokuwa akikitaka tayari kilifanyika na hivyo aliihitaji familia yake.

“Wala usijali! Familia yako ipo salama sehemu. Hatujamaliza kazi. Itunze hiyo familia mpaka nitakapokwambia uiachie. Umenielewa?” alisema Godwin na kuuliza.

“Ndiyo! Lakini....”

“Kwenye hili hakuna lakini. Fanya nilichokwambia. Au unataka baadaye uende ukazione maiti za familia yako ufukweni?” aliuliza Godwin kwa mikwara mizito.

“Hapana! Hapana mkuu!”

“Basi sawa. Ngoja niwasiliane na Andrew,” alisema Godwin na kukata simu.

***

Andrew ndiye aliyekuwa akihakikisha ulinzi unakuwa wa kutosha nyumbani kwa Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Noel Joseph. Kila siku kazi yake ilikuwa ni kuwapanga maofisa ambao walitakiwa kuwa nyumbani hapo kwa zamu huku akihakikisha kwamba kila kitu kinakuwa salama kabisa.

Yeye ndiye aliyeamua nani alitakiwa kukaa na nani alitakiwa kupumzika. Hiyo ndiyo ilikuwa kazi yake ya kila siku, aliifanya kwa nguvu kubwa, kitendo cha kuiacha familia hiyo ikipata tatizo basi ingekuwa hatari sana kwake, hivyo ilikuwa ni lazima kuona akiwahimiza maofisa wa Usalama wa Taifa wailinde nyumba hiyo kuliko kitu chochote kile.

Siku ambayo tukio la utekaji wa familia yake ulikuwa ukifanyika alikuwa nyumbani huko. Moyo wake ulikuwa na hamu na kukaa na familia yake, alihitaji kupata mapumziko na tayari aliandika barua ya likizo ya mwezi mmoja na wakati huo alikuwa akifikiria ni kwa jinsi gani angekwenda Visiwani Zanzibar kula raha na familia yake.

Aliikumbuka sana, alikuwa karibu nayo kupita kiasi, aliipenda na wakati mwingine alikuwa radhi kupoteza kila kitu lakini si familia hiyo. Wakati akiwa hapo ndipo akakumbuka kumpigia simu mke wake, Selena japo azungumze naye na kumjulia hali.

Cha ajabu, simu yake haikuwa ikitoka, alishangaa mno, alijaribu kupiga zaidi na zaidi lakini simu hiyo haikuwa ikitoka kabisa. Akawaambia wenzake wajaribu kumpigia na kumtumia meseji matokeo yalikuwa yaleyale, hakukuwa na simu iliyoingia wala kutoka jambo ambalo likamfanya kuhisi kulikuwa na tatizo.

“Hii mitandao ya simu inazingua sana,” alisema Andrew huku akionekana kukasirika.

Akawasiliana na huduma kwa wateja kwa kupitia simu ya rafiki yake na kuambiwa kwamba ombi lake lingepatiwa ufafanuzi haraka sana. Akatakiwa kusubiri, alisubiri na kusubiri, dakika ziliendelea kwenda mbele na baada ya saa moja, akaona simu yake ikianza kuita, haraka sana akaipokea, akafurahi kwamba hatimaye kulikuwa na uwezekano wa simu yake kufanya kazi kama mwanzo.

“Halo!”

“Halo Andrew Carlos,” alisikika Godwin, Andrew akashtuka.

“Nazungumza na nani?” aliuliza.

“Kunijua si suluhisho. Sikiliza. Nina familia yako. Nimeiteka kwa ajili ya kazi moja tu. Kuimaliza kwa kuitumbukiza katika pipa la tindikali,” alisikika Godwin akiongea kwa msisitizo kabisa uliomfanya Andrew kutetemeka mno.

“Unasemaje?”

“Nadhani umenisikia. Nakupa mtihani mdogo sana, ukiweza, utaiona familia yako tena, ila ukishindwa, utaiona ahera,” alisema Godwin maneno yaliyomfanya Andrew kuogopa.

“Familia yangu imefanya nini mpaka uiteke? Hivi unanijua mimi? Hivi unajua adhabu nitakayokupa mwanaizaya wewe?” alisema Godwin huku akionekana kupaniki.

“Kwa kuwa unapaniki na kutoa vitisho, baadaye saa kumi na moja jioni nitakupigia simu kukwambia maiti za familia yako zipo wapi,” alisema Godwin na kukata simu.

Andrew akachanganyikiwa, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu mke wake, simu haikuwa ikipatikana, alichanganyikiwa, haraka sana akaondoka nyumbani kwa bosi wake na kuelekea nyumbani kwake. Machozi yalikuwa yakimtoka, hakuamini kilichokuwa kimetokea. Hakuchukua muda mrefu kufika Masaki, akaingia ndani, akaita na kuita lakini hakukuwa na mtu aliyeitikia zaidi ya mfanyakazi wake.

“Wifi yako yupo wapi?” aliuliza Andrew huku akionekana kuchanganyikiwa.

“Eeh! Kaka! Mbona wifi aliondoka kwenda hospitalini!” alisema mfanyakazi huyo.

“Aliondoka kwenda hospitalini? Nani anaumwa? Watoto?”

“Hapana! Aliambiwa wewe umepata ajali ndiyo amekwenda huko,” alijibu mfanyakazi huyo.

“Mimi nimepata ajali? Muda gani?” aliuliza Andrew lakini hata kabla hajajibiwa maswali yake, akatoka ndani na kurudi kwenye gari kuelekea katika Hospitali ya Mwananyamala.

Aliendesha gari kwa kuchanganyikiwa, hakuchukua muda mrefu akafika hospitalini huko ambapo moja kwa moja akaanza kuzunguka huku na kule kumtafuta mkewe kwa kuamini kwamba alifika mahali hapo kwa ajili ya kumuona baada ya kupewa taarifa kwamba alikwenda huko kwa kuwa aliambiwa kwamba alipata ajali mbaya ya gari.

Alikaa huko kwa dakika arobaini na tano akimtafuta, alishindwa kumuona, alikuwa akilia, moyo wake uliumia, alikuwa tayari kupoteza kila kitu katika maisha yake lakini si kuipoteza familia yake. Wakati akiwa anaifikiria ndipo akakumbuka kwamba alipigiwa simu na mwanaume mmoja na kumwambia kwamba alikuwa njiani kuimaliza familia yake, haraka sana akachukua simu yake na kumpigia.

“Halo! Halo! Naomba usiiue familia yangu, nitakupa kiasi chochote cha pesa unachokitaka,” alisema Andrew huku akionekana kuchanganyikiwa.

“Unatania sana, sasa nitataka nikuonyeshee mfano ili iwe adabu kwa watu wengine,” alisema Godwin kwa mikwara ili kumtia presha.

“Naomba usiiue familia yangu! Nakuomba sana.”

“Sawa. Una bahati kwa kuwa umeomba msamaha! Nahitaji ufanye mambo mawili tu, ukishindwa, naimaliza familia yako,” alisema Godwin.

“Niambie kitu chochote kile, nitafanya.”

“Sawa. Kwanza hatakiwi mtu yeyote kufahamu kama familia yako imetekwa, hata polisi hawatakiwi kufahamu hilo,” alisema Godwin.

“Sawa. Nitaficha siri.”

“Cha pili nataka ukaiteke familia ya mkurugenzi wake, Noel,” alisema Godwin.

“Unasemaje?”

“Najua umenielewa. Ninakupa siku tatu kufanya mambo hayo mawili.”

“Siwezi kuiteka, sijui nitaiteka vipi!”

“Basi kama hujui, subiri niwaue watoto wako kwanza ndiyo utajua jinsi ya kuiteka,” alisema Godwin na kukata simu.

“Halo..halo...halo...” aliita Andrew.

Akachanganyikiwa, akajua kabisa kwamba mwanaume huyo angeweza kuimaliza familia yake, akampigia simu, ilipopokelewa, akamuomba sana, akamwambia kwamba angefanya kama alivyotakiwa kufanya pasipo pingamizi lolote lile.

“Una bahati! Ndiyo pipa lililetwa hapa kwa ajili ya kutumbukizwa. Kama upo tayari. Kafanye kazi kisha nipe taarifa,” alisema Godwin na kukata simu.

Andrew akabaki akishusha pumzi ndefu huku akijifikiria ni kwa namna gani angeweza kuifanya kazi hiyo aliyopewa ndani ya siku tatu tu.

***

Mipango ya Godwin ilikuwa ikienda kama ilivyotakiwa kwenda, hakuona ugumu wa kazi hiyo mbele yake, alihisi kwamba angefanikiwa kwa kuwa kazi kubwa ilikuwa ni kwa watu ambao aliwapa kazi hiyo lakini si yeye.

Hakutaka kumteka mtu yeyote yule, alitaka kuwatumia wenyewe kwa wenyewe kufanikisha mambo yake kitu kilichoonekana kuwa rahisi kupita kawaida.

Hakutaka kuiweka mipango hiyo katika mitandao ya kijamii, kitu pekee ambacho aliwaambia watu ni kwamba ndani ya miezi miwili ilikuwa ni lazima Rais Bokasa apinduliwe kama tu hatoweza kuachia madaraka kwa hiari.

Watu wakawa na hamu ya kuona rais huyo akijiuzulu, lilionekana kuwa jambo gumu kwa kuwa hata Jenerali Ojuku alionekana kuwa upande wake kwa asilimia mia moja kwani hata kwenye mikutano aliyokuwa akiweka rais huyo, yeye alikuwa pembeni na kumuahidi rais huyo kwamba angepambana na wabaya wake kwa asilimia mia moja.

Si huyo tu bali hata Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel alionekana kuwa upande wake, aliwatuma vijana wake kuwatafuta wabaya wa rais huyo, wengine walikuwa wakitumia akaunti feki katika mitandao ya kijamii kuhakikisha rais hachafuliwi, kama Godwin alisema ndani ya miezi miwili rais Bokasa alitakiwa kujiuzulu vinginevyo angepinduliwa, ni kwa jeshi gani lingetumia kumpindua?

Wengi waliiamini akaunti ya Mabadiliko ya Kweli iliyokuwa kwenye Mtandao wa Kijamii wa Instagram, hakukuwa na habari ya uongo iliyokuwa ikiandikwa, kila kitu ambacho kilisemwa, kilitokea, sasa ilikuwaje jambo hilo litokee na wakati kila mtu aliyetakiwa kufanya hivyo alikuwa upande wa rais huyo? Hakukuwa na mtu aliyekuwa na majibu.

“Yaani kauli ya Mabadiliko ya Kweli inanishangaza sana,” alisema jamaa mmoja, alikuwa miongoni mwa wafuasi milioni thelathini na tano waliokuwa wakiifuatilia akaunti hiyo.

“Kila mtu anashangaa, si wewe tu, hata mimi mwenyewe nashangaa, hivi huyu jamaa ni mtu wa aina gani aisee, au ofisa wa Usalama wa Taifa?” alisema jamaa mwingine na kuuliza swali.

“Inawezekana! Ila kama ni ofisa wa Usalama wa Taifa, mbona mkurugenzi wake yupo upande wa dikteta? Itawezekana kweli?”

“Hatujui! Ngoja tusubiri!”

Hilo ndilo lililobaki, hawakujua mtu yule aliyekuwa akiiendesha akaunti ile angefanya jambo gani kumuondoa rais huyo madarakani. Kila mtu mtaani alizungumza lake, hakukuwa na mtu aliyependa kumuona rais huyo akiendelea kuwa madarakani kwani hakuwa mtu mzuri, aliifinya katiba, alivunja baadhi ya vipengele na mbaya zaidi alibadilisha kifungu muhimu kilichomtaka rais akae madarakani miaka mitano na yeye kuweka kwamba alitakiwa kutawala mpaka kifo chake.

Kwa kuwa alikuwa na mkakati wa kumuondoa madaakan rais huyo, alichokifanya ni kuwasiliana na mwenyekiti wa Chama cha Upinzani cha Tanzania National Party, Bwana Elius Kambili na kumwambia kwamba alikuwa katika mpango mkubwa wa kumuondoa Rais Bokasa madarakani hivyo alitakiwa kujipanga na watu wake kwa ajili ya kuichukua Tanzania.

“Sisi tuichukue Tanzania?” aliuliza Kambili, hakuamini alichokisikia.

“Ndiyo! Mpo tayari?” aliuliza.

“Ndiyo! Ila itawezekana vipi? Kwanza nazungumza na nani?” aliuliza, hakuonekana kujiamini hata kidogo. Walihangaika kwa miaka ishirini kuichukua Tanzania lakini wakashindwa mpaka pale katiba ilipobadilishwa na kumfanya rais huyo atawale mpaka kifo chake.

“Mabadiliko ya Kweli!”

“Aiseee! Hivi matukio yote unayapata wapi? Nimesoma ulivyoandika kwamba ndani ya miezi miwili unataka Rais Bokasa ajiuzulu au atapinduliwa, itawezekana vipi?” aliuliza Kambili.

“Niachie mimi. Cha msingi fanya kile nilichokwambia. Anza kupanga nani atakuwa makamu wa rais kama wewe utakuwa rais, nani atakuwa waziri mkuu na vyeo vingine,” alisema Godwin.

“Basi hakuna shida. Ngoja nifanye hivyo!”

“Ila kumbuka kitu kimoja. Iwe siri kubwa, ishu ya kumtoa madarakani huyu dikteta niachie mimi,” alisema Godwin.

“Sawa bosi.”

Godwin akakata simu, hakutaka kujulikana mahali alipokuwa, kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilikuwa siri kubwa. Hakutaka kumwamini mtu yeyote yule na ndiyo maana hata kuwasiliana na Kambili alitumia simu yake na si kuonana ana kwa ana.

Alipomaliza, akampigia simu Andrew na kumuuliza kama alikuwa amekamilisha ule mpango aliokuwa amempa wa kuiteka familia ya Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Noel.

“Umefikia wapi?” aliuliza Godwin.”

“Mkuu! Bado! Ndiyo nataka kujipanga!”

“Unakumbuka kwamba una siku mbili tu?”

“Nakumbuka mkuu! Naomba usiiue familia yangu,” alisema Andrew.

“Ikimalizika siku ya tatu, hautoiona tena familia yako,” alisema Godwin na kukata simu.





Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa nchini Uswisi, Bwana Henrik Kom alikuwa kwenye kikao kizito baadhi ya viongozi wa nchi hiyo akiwemo waziri mkuu, Bwana Stevenson Paul pamoja na mkurugenzi wa Benki ya Geneva, Bwana Anrik Morov aliyekuwa na asili ya Urusi.

Walikutana katika kikao hicho cha dharura kwa ajili ya kujadili matatizo yaliyokuwa yakiikumba Benki ya Geneva kwa pesa zake kutoka katika akaunti za wateja wao kuibwa na kuhamishwa katika benki nyingine nchini Marekani kabla ya kupelekwa katika akaunti nyingine.

Kwao, jambo lile lilionekana kuwa geni kabisa. Benki ilikuwa na ulinzi mkubwa, data base ililindwa saa ishirini na nne na watalaamu wa kompyuta lakini kitu kilichoshangaza kabisa, kulikuwa na mtu ambaye alifanikiwa kuingia katika akaunti hizo na kuhamisha pesa pasipo wao wenyewe kufahamu.

Walichanganyikiwa, waliona kuwa na uhitaji wa kupambana na mtu huyo kwani kama alikuwa na uwezo wa kuhamisha benki kutoka katika akaunti ya watu wawili, basi angekuwa na uwezo wa kuhamisha pesa kutokana hata kwa viongozi wengine na kuendelea kuichafua akaunti hiyo na kupoteza wateja zaidi kwa kuonekana hawakuwa na ulinzi wowowte ule.

Hawakutaka kuona aibu hiyo ikiwakuta, ilikuwa ni lazima kupambana na ndiyo maana aliweka kikao hicho cha dharura kwa ajili ya kuangalia ni kwa jinsi gani wangeweza kupambana na mtu huyo ambaye alikuwa nchini Tanzania.

“Ulisema ulituma vijana lakini walishindwa kumkamata?” aliuliza Bwana Stevenson.

“Ndiyo!” alijibu Kom na kuanza kumuhadithia namna vijana wake walivyosafiri kwenda nchini Tanzania, walivyodukua namba yake kwa kutumia picha waliyoituma katika Mtandao wa Kijamii wa WhatsApp lakini mwisho wa siku walimpata kijana mmoja aliyeitwa Ally ambaye alidai kwamba simu ile alikuwa ameuziwa na kibaka.

“Ulijuaje kama si yeye huyo mliyemkamata?” aliendelea kuuliza.

“Ni kwa sababu wakati tukiwa naye mikononi mwetu, akaunti ya pili ikaibiwa pesa.”

“Ooh! Sawa. Kwa hiyo mnataka kuniambia kwamba mmeshindwa kupambana naye?”

“Si kwamba tumeshindwa.”

“Bali?”

“Tutapambana naye na ndiyo maana nimeita kikao hiki kwa ajili ya kujadiliana kwani mtu ambaye tunadili naye ni mtaalamu wa masuala ya kompyuta. Mtu aliweza kufungua akaunti katika Benki ya America na hakukuwa na mtu aliyejua. Huyo mtu si mchezo,” alisema Bwana Kom.

Kikao kilikuwa kizito mno, hawakujua ni kwa namna gani wangeweza kumpata mtu huyo aliyeonekana kuwa hatari sana. Maofisa wa Usalama wa Taifa nchini humo, FIS walikuwa wakihangaika kila siku kumtafuta katika mitambo yao lakini hawakufanikiwa.

Waliambiwa kwamba mtu huyo ndiye alikuwa mmilikiwa akaunti ya Mabadiliko ya Kweli iliyokuwa Instagram, waliitumia akaunti hiyo kumtafuta na kujua mahali alipokuwa lakini hawakufanikiwa hata kidogo.

Walikwishawasiliana na Instagram wenyewe na kuwaambia juu ya uhitaji wa mtu huyo, waliwaambia kuwapa taarifa mahali alipokuwa lakini wao wenyewe walikataa kutoa ushirikiano wowote ule kwani kwa kuingilia kitu kama hicho ilikuwa ni sawa na kuvunja sheria ya kimtandao ya mtu kuingilia mambo ya mtu binafsi, tena kwa akaunti kama hiyo ambayo ilikuwa ikiongoza kuwa na wafuasi wengi barani Afrika, ilikuwa ikiwaingizia pesa nyingi tu.

“Wamekataa kushirikiana nasi?” aliuliza Bwana Stevenson.

“Ndiyo! Instagram wamekuwa wagumu sana, kama Apple kipindi kile walipotakiwa kutoa taarifa za ugaidi kwa mtumiaji wao wa iPhone, wamekataa kabisa,” alisema Kom.

“Cha msingi fanyeni kitu kimoja. Tumeni tena watu kwenda huko!”

“Unamaanisha maofisa wa FIS?”

“Ndiyo. Mnasema kwamba huyo mtu mlimpta jijini Dar es Salaam?”

“Ndiyo!”

“NA eneo linajulikana?””Ndiyo!”

“Basi mtumieni msichana wa kwenda huko. Awe mmoja, msichana mweusi, mrembo ambaye atakwenda huko kwa ajili ya kufanya kazi moja tu, kumtafuta na kumpata,” alishauri Stevenson.

“Kivipi?”

“Waafrika wanapenda sana ngono kuliko kazi!”

“Najua!”

“Mtumieni msichana mrembo tu. Akienda huko afanye kazi ya kumtafuta mwanaume huyo, akimpata, aanze kujilainisha kwake, itakuwa kazi nyepesi sana. Hata asipompata, yule mtu ambaye atakuwa akimuhofia ndiye aanze kujenga naye ukaribu na kumwambia kuhusu siri zake, hata kama si yeye, inawezekana kuna mtu hapo atakuwa anamfahamu,” alisema Stevenson.

“Sawa.”

“Tuna Mtanzania yeyote FIS?”

“Ndiyo! Lakini yupo nchini Somalia akiendelea kudadisi kuhusu Al Shaabab!”

“Mtoeni huko, mwambieni aende Tanzania.”

“Sawa bosi!”

“Anaitwa nani?”

“Halima!”

“Basi mtumeni aende huko mpaka katika mtaa ambao simu hiyo ilipopatikana, nina uhakika tutampata tu,” alisema Stevenson.

“Haina shida.”

Hakukuwa na la kuchelewa, haraka sana simu ikapigwa mpaka nchini Somalia na msichana huyo mrembo, Halima kupewa taarifa kwamba ilikuwa ni lazima asafiri mpaka nchini Tanzania, kwenye Jiji la Dar es Salaam katika Mtaa wa Tandale ambapo ndipo simu hiyo ilipopatikana kwa ajili ya kumtafuta mwanaume huyo.

Hilo halikuwa tatizo kwa Halima, kwa kuwa alikuwa msichana mrembo aliyekubuhu katika kuwatafuta watu wengi barani Afrika, akaondoka kuelekea nchini Tanzania huku kichwani mwake kukiwa na jambo moja tu, kumpata mwanaume huyo ambaye hakuijua hata sura yake, na hakujua alikuwa na muonekano gani, ila alichokuwa akikitaka ni kumpata na kumkamata kwa ajili ya kuirudishia sifa Uswisi.

***

Rais Bokasa hakuwa sawa, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria Godwin ambaye alikuwa tishio katika maisha yake. Moyo wake ulimuuma, hakuwa radhi kuona akiachia madaraka, aliupenda urais aliokuwa nao, kwake, alikuwa tayari kupoteza kila kitu lakinis si urais.

Hakujua mwanaume huyo alikuwa wapi, aliwatuma maofisa wa Usalama wa Taifa kwa ajili ya kumtafuta mwanaume huyo lakini hawakuweza kumpata, alichanganyikiwa, mawasiliano yake ya simu yalidukuliwa, hilo lilimchanganya na wakati mwingine alihisi kwamba hata watu wa mitandao ya simu walikuwa wakihusika lakini baada ya kupewa taarifa kwamba hata Usalama wa Taifa wa Uswisi walishindwa kumpata mwanaume huyo, akaona kulikuwa na kazi kubwa sana mbele yake.

Watu mitandaoni walizidi kulijadili suala lake, hakukuwa na mtu aliyemuonea huruma, wengi walikuwa wakijadili kwenye mitandao hali iliyokuwa ikiendelea nchini Tanzania, kila mmoja alikuwa akimuunga mkono mmiliki wa Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli kwamba alikuwa mtu sahihi ambaye alitakiwa kuwakomboa Watanzania kutoka katika hali ngumu ya maisha waliyokuwa nayo.

Wakati yeye akihangaika kuhakikisha kwamba anaibakiza nafasi yake, upande wa pili Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania National, Bwana Elius Kambili aliendelea kuwaambia wenzake kwamba huo ndiyo ulikuwa muda wa kupambana, walikuwa na miezi miwili kuwaweka watu sawa kabla ya kuingia madarakani.

“Mkuu! Unaamini vipi uvumi wa mitandaoni?” aliuliza katibu wa chama hicho, Bwana Golden Kumba.

“Nimepigiwa simu na huyo jamaa,” alisema Bwana Kambili.

“Amekupigia simu? Hebu tuone namba yake.”

“Hii hapa!”

Kumba hakuwa akiamini, aliona kila alichokuwa akiambiwa kilikuwa ni uongo, akaipiga namba ile kwa lengo la kuhakikisha kama kweli ilikuwa ni ya huyo mwanaume lakini namba haikuwa ikipatikana. Kila mtu akaonekana kutokumuamini, ni kweli walikuwa wakipitia kila posti iliyokuwa imewekwa, hawakujua mwanaume huyo angefanya njia gani kumuondoa madarakani Rais Bokasa kwa kuwa alikuwa na kila kitu, alikuwa na jeshi, Usalama wa Taifa, je, angetumia kitu gani na wakati vyote hivyo vilikuwa vikimuunga mkono?

“Sidhani kama ni kweli! Huyu mtu anataka kucheza na akili zetu,” alisema Kumba maneno yaliyoungwa mkono na kila mmoja.

Kambili hakurudishwa nyuma, aliamini kwamba mwanaume huyo aliyempigia simu alikuwa na uwezo wa kubadilisha kitu chochote kile, aliwaambia wazi kwamba imani yake kubwa ilikuwa kwa mwanaume huyo hivyo kila mmoja alitakiwa kuamini kwamba kweli ndani ya miezi miwili rais huyo angachia madaraka.

Alichokifanya ni kuandaa mikutano ya kisiasa, aliwaeleza wananchi hisia zake, aliwaambia ukweli kwamba ndani ya miezi hiyo rais aliyekuwa madarakani alitakiwa kujiuzulu au nchi kupinduliwa. Watu wengi, hasa wanachama wamuunga mkono japokuwa viongozi wenzake ndani ya chama hakukuwa na mtu yeyote aliyekubaliana naye.

“Hivi nyie mtu anafanya mikutano ya kunichafua mnaangalia tu!” alisema Rais Bokasa huku akiwa na hasira.

Alikuwa akiongea na IGP, Gabriel Ng’osha, hakutaka kumuona Kambili akisimama jukwaani hasa katika kipindi cha hatari kama hicho, haraka sana akaagiza mwanaume huyo akamatwe, kazi ikafanyika, huku Kambili akiwa jukwaani, akavamiwa na polisi na kukamatwa.

Hali hiyo ndiyo iliyoibua zogo kila kona nchini Tanzania, ilikuwaje mtu akamatwe kwenye mkutano wa siasa kwa kuelezea kile kitu kilichokuwa kikiendelea katika mitandao ya kijamii na kila mtu alikuwa akijua ukweli?

Akapelekwa kituoni, maagizo kutoka juu yakaagiza Kambili ahojiwe na kusema mahali alipokuwa Godwin kwani kama alipigiwa simu na kuambiwa hivyo, alikuwa na uhakika kwamba alikuwa akimfahamu mwanaume huyo na alijua mahali alipokuwa.

“Alinipigia simu tu! Sijui yupo wapi,” alisema Kambili.

“Utakuwa unajua! Sasa subiri, leo utatuambia ukweli tu,” alisema polisi mmoja aliyekuwa na mwili mkakamavu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Wakamchukua na kumuingiza katika chumba kimoja kilichoandikwa Sobibor mlangoni, kilikuwa chumba cha mateso ambacho waliingizwa watu waliokuwa jeuri kuzungumza kitu chochote kile. Humo kulikuwa na ng’e, nyoka, nyigu, maji machafu, mbu wengi na mateso ya kila aina.

Akatupwa, maji machafu yakamchafua, alibaki akilalamika kama mtoto, akaanza kuumwa, akaanza kutambaliwa na nyoka ambao walitolewa meno, hao walitumika kama kumtisha. Muda wote alikuwa akipiga kelele, alitakiwa kukaa humo mpaka pale ambapo angekuwa tayari kuzungumza ukweli juu ya mahali alipokuwa Godwin.

Muda wote IGP Ng’osha alikuwa akipiga simu kuulizia kilichokuwa kikiendelea. Pamoja na mateso hayo yote lakini Kambili alisema vilevile kwamba hakuwa akimfahamu Godwin na hakujua alikuwa mahali gani.

“Hivi kweli nyie mnatesa au mnambembeleza?” aliuliza IGP huku akionekana kukasirika kwani nyuma yake alikuwa rais, kama Kambili asingesema ukweli ilimaanisha naye kibarua chake kingekuwa matatani kwa kuonekana hafanyi kazi.

“Mkuu! Tunafanya kazi! Bado hasemi.”

“Mwacheni huko kwa siku tatu mfululizo.”

Hayo yalikuwa maagizo, IGP alivimba kwa hasira, muda wote alikuwa mtu aliyekuwa akitamani kufanya jambo fulani ili apokee sifa kutoka kwa Rais Bokasa. Polisi wake waliendelea kumsikilizia Kambili ili awaambie ukweli juu ya mahali alipokuwa Godwin lakini jibu lake lilikuwa lilelile kwamba hakuwa akifahamu mahali alipokuwa mwanaume huyo.

“Ngoja nije mimi mwenyewe. Nadhani nyie mnamshikashika tu,” alisema IGP, akatoka nyumbani kwake, akaingia stoo na kuchukua jenereta, akalipakiza ndani ya gari, akachukua nyaya mbili na kuondoka nazo, alikuwa amepania kukumbushia enzi zake jinsi alivyokuwa akiwatesa wahalifu wakubwa ambao hawakutaka kusema kilichokuwa kikihitaji mpaka kufikia hatua ya kusema.

Hakuchukua muda mrefu akafika kituoni hapo, akaagiza polisi wawili washushe jenereta na zile nyaya na kuzipeleka katika chumba kingine na kuwaambia wamchukue Kambili na kumpeleka katika hicho chumba kilichowekwa jenereta.

“Nasikia umekataa kuwaambia vijana wangu ukweli!” alisema Ng’osha huku akimwangalia Kambili aliyekuwa hoi.

“S..ij..u..i..ch..oc..ho..t..e,” alisema Kambili huku akimwangalia Ng’osha aliyekuwa akivua shati lake.

“Basi sawa! Tuingie kazini,” alisema Ng’osha na kuwaagiza vijana wake wawashe jenereta.

Kilichofuata kilikuwa ni mateso makali, Ng’osha hakuonekana kukubali, alitaka kuhakikisha mwanaume huyo anasema mahali Godwin alipokuwa na hivyo wao kumfuata.

Alimpiga kwa shoti ya umeme huku akiwa mtupu kabisa lakini bado mwanaume huyo aliendelea kusema kwamba hakujua mahali alipokuwa mwanaume huyo. Alishangaa, aliwahi kukutana na wanaume waliokuwa na viburi lakini kwa Kambili alionekana kuwa ni zaidi ya watu hao wote.

Alipitia mateso makali sana lakini bado msimamo wake ulikuwa uleule. Baada ya dakika ishirini za mateso mfululizo, Kambili akashindwa kuzungumza, hakuweza hata kuufumbua mdomo wake, yote hayo yaliyokuwa yametokea yalikuwa ni kwa ajili ya Godwin, kitendo cha kupokea simu ya mwanaume huyo lilionekana kuwa tatizo.

Wakati akiendelea kumtesa Kambili ndani ya chumba kile, akaanza kusikia simu yake ikianza kuita kwa kutetemeka, haraka sana akaichukua kutoka mfukoni kwani alijua kwamba alikuwa rais ambaye alitaka kujua kilichokuwa kikiendelea. Hakukuwa na namba, aliona neno lililosomeka unknown likiwa na maana kwamba mtu aliyekuwa akipiga simu hakuwa akijulikana. Akaipeleka sikioni.

“Kila kitu kinachotokea kina gharama, je utakuwa tayari kulipia gharama?” lilikuwa swali la kwanza alilokutana nalo.

“Wewe nani?”

“Godwin!”

“Godwin?”

“Jiandae kulipia gharama. Baada ya dakika tano ingia kwenye akaunti ya Mabadiliko ya Kweli! Kuna mengi utayaona, siri zako nyingi zitakuwa huko kwa kuwa ulihisi hakuna anayejua. Hizo ni gharama, kama Biblia kwenye Kitabu cha Malaki kinasema Bwana angezipaka nyuso zao mavi, basi nakwambia kwamba nami nitakupaka mavi, kila mtu atakayekuangalia atauona uchafu wako,” alisema Godwin huku Ng’osha akiwa makini kusikiliza.

“Hahah! Unatakiwa uingie kwenye vikundi vya vichekesho, uwe unaigiza na sisi tuwe tunacheka. Unadhani naogopa!” alisema Ng’osha huku simu ikiwa sikioni.

“Sawa. Unawakumbuka wale majambazi waliokwenda kuvamia Benki ya Wananchi? Unakumbuka wale watu waliouawa katika Msitu wa Pande akiwemo mtoto wa Bilionea Ngolisho? Unakumbuka kuhusu wale wanaume waliokamatwa na madawa ya kulevya yenye gharama ya bilioni moja? Unakumbuka ule wizi wa mafuta yanayotokea bandarini? Unamkumbuka msichana Yunus na dada yake jinsi walivyouawa kinyama na mpaka leo muuaji hajulikani? Ng’osha, ninakwenda kukupaka mavi, kila mtu atakayekuangalia, atauona uchafu wako. Tukutane mtandaoni kwa picha za sauti yako na watu hao,” alisema Godwin na hapohapo kukata simu.

“Halo...halo..Godwin halo...Godwin usifanye hivyo...Godwin haloooo....” aliita IGP Ng’osha huku akitetemeka, kijasho kikaanza kumtoka, mapigo ya moyo yakapanda, mdomo ukaanza kuchezacheza kama mtu aliyekuwa akisikia baridi kali.

“I am finished,” (nimekwisha) alisema IGP Ng’osha huku akikaa chini na kunyoosha miguu.

***

Ndege ya Shirika la Kenyan Airlines ilikuwa ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. Bila kupoteza muda, Halima na abiria wengine wakaanza kuteremka na moja kwa moja kuelekea katika jengo la uwanjani hapo na kwenda sehemu ya kusubiriwa mizigo ambayo ilikuwa ikipita katika sehemu ya kuchunguziwa.

Baada ya dakika kadhaa, akachukua begi lake na kuondoka mahali hapo. Alikuwa mzuri mno, kila mwanaume aliyekuwa akipishana naye ilikuwa ni lazima kugeuka na kumwangalia. Alivalia suruali, miwani na blauzi iliyomfanya kutoka chicha.

Alitembea kwa mwendo wa mikogo kama mwanamke aliyekuwa akiringa sana, alipofika nje ya jengo lile, akaifuata teksi moja na kusimama karibu yake, dereva mmoja akamuona, akamfuata na kumtaka kuingia.

Hakuzungumza kitu, alichokuwa akikihitaji ni kupelekwa katika Hoteli ya Tasmania iliyokuwa Posta Mpya ambapo baada ya kupewa chumba na kupumzika, asubuhi iliyofuata akaanza kuelekea Tandale Sokoni kwa ajili ya kununua nguo za mitumba ambazo aliamini zingemfanya kuwa na muonekano wa mwanamke wa Dar es Salaam, hasa uswahili ili asiweze kushtukiwa.

Alinunua nguo nyingi na siku hiyohiyo akaelekea mpaka Tandale sehemu iitwayo Fogo iliyokuwa Tandale kwa Tumbo ambapo kwa kumtumia dalali wa chapchap akapata chumba alichotakiwa kulipia shilingi elfu thelathini kwa miezi kumi kitu ambacho hakikuwa tatizo lolote lile.

“Ni chumba kizuri sana. Nimekipenda,” alisema Halima huku akikiangalia chumba hicho.

“Umeolewa?” aliuliza mwenye nyumba.

“Hapana! Nipo singo.”

“Basi humu kuna wanaume wengi tu. Unaweza kuchagua yeyote,” alisema baba mwenye nyumba kiutani huku akiachia tabasamuu pana.

“Nashukuru. Nadhani nitampata mmoja,” alisema Halima huku naye akirudisha tabasamu pana. Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba msichana huyo alikuwa mpelelezi aliyefika kwa kazi maalumu.

***

Ilikuwa ni Andrew afanye kile alichokuwa ameambiwa vinginevyo asingeweza kuiona familia yake tena. Alipewa siku tatu na tangu alipoambiwa kwamba ana siku hizo za kufanya kazi hiyo vinginevyo familia yake ingeuawa, akaona mshale wa dakika ukienda kasi kupita kawaida.

Kichwa chake kilikuwa kikiifikiria familia yake tu, alikuwa mjanja, aliyeweza kupambana na watu wengi kisiri au hata kuwatuma Usalama wa Taifa kumtafuta mtu yeyote yule aliyekuwa amejificha lakini kwa kuipata familia yake aliona jambo gumu mno kutokana na siku chache alizokuwa amepewa.

Akarudi mpaka nyumbani kwa bosi wake, Noel. Hakuonekana kuwa sawa, alipokuwa akiwaona vijana wake wakiendelea kulinda mahali pale alijua kabisa kwamba walitakiwa kufanya jambo fulani kuhusu familia ya bosi wake huyo vinginevyo asingeweza kuiona familia yake katika maisha yake yote.

Hiyo ilikuwa kazi kubwa ambayo asingeweza kuifanya peke yake, ilikuwa ni lazima kushirikiana na wenzake mpaka kufanikisha suala hilo. Hakujua ni nani alitakiwa kushirikiana naye katika suala hilo ambalo lilihitaji usiri mkubwa mno.

“Selemani Kijogoo anaweza kweli?” alijiuliza.

“Sidhani!” akajijibu.

Kila mtu aliyekuwa akijaribu kumchekecha kichwani mwake hakuona kama alikuwa na moyo wa kutunza siri kwa kile alichotaka kukifanya. Jambo moja kubwa ambalo lilimjia kichwani mwake haraka ni kumshirikisha mtu aliyekuwa amemwambia afanye lile alilotakiwa kulifanya. Hapohapo akampigia simu Godwin.

“Naomba unisaidie kitu kimoja,” alisema Andrew mara baada ya simu kupokelewa na Godwin.

“Nikusaidie nini?”

“Simuamini mtu yeyote mahali hapa, ninatamani niifanye kazi hii peke yangu! Niifanye vipi? Naomba unisaidie, sitaki kuiona familia yangu ikiangamia, naomba unisaidie ili niweze kuifanya peke yangu,” alisema Andrew huku machozi yakimtoka, moyoni mwake alikuwa akisikia maumivu makali mno kwani aliamini kwa kushindwa vile ilimaanisha kwamba asingeweza kuiona familia yake tena.

“Sawa. Subiri! Baada ya dakika kumi, mwanamke huyo ataomba kuondoka kuelekea Magomeni Usalama kwenda kumuona rafiki yake, hakikisha haondoki na mtu kwenda huko. Akiondoka, wewe mfuatilie, huko ndipo utakapomteka yeye na mtoto wake,” alisema Godwin.

“Sawa!” aliitikia Andrew kwa heshima zote.

****

Godwin alikuwa akifahamu mambo mengi, kwa kutumia ujuzi wake wa kudukua namba za watu mbalimbali aliweza kujua siri nyingi mno. Alijua mawaziri waliokuwa wakitembea nje ya ndoa, alijua mtu aliyetakiwa kuuawa siku fulani, kila kitu kilichokuwa kikiendelea aliweza kunasa mawasiliano kwa haraka sana kuliko hata mitandao ya simu ambayo ilikuwa na kazi hiyo.

Katika kufuatilia mawasiliano ya mke wa Noel, akagundua kwamba kulikuwa na mwanamke mwingine aliyekuwa akiwasiliana naye sana, huyo aliitwa Amina na alikuwa akiishi Magomeni Usalama karibu kabisa na Tanesco.

Alifuatilia mawasiliano hayo zaidi na kugundua kwamba kulikuwa na mchezo hatari uliokuwa ukichezwa na mwanamke huyo. Japokuwa alikuwa na mume, familia lakini bado alikuwa akitembea na kijana aliyeitwa Masalu aliyekuwa akiishi Magomeni Usalama.

Ilikuwa siri kubwa, huyo alikuwa mwanaume wake aliyeunganishiwa na Amina ambaye alitokea kumuelewa sana. Yakaanza mazoea ya kuonana na kijana huyo katika chumba cha Amina huko Magomeni na mwisho wa siku kuzama katika penzi zito lililoanza kuiyumbisha ndoa yake ila kwa kuwa Noel alimpenda sana mkewe, hakuwa na la kufanya.

Godwin alinasa mazungumzo yao, alisikia kila kitu kilichokuwa kikiendelea, akafuma meseji za siri, picha walizokuwa wakitumiana kwa siri ambazo hazikuwa zikistahili hata kuchapishwa magazetini. Baada ya kugundua hilo, hapo ndipo alipoanza kuona kwamba kulikuwa na kazi nyepesi ya kumnasa mwanamke huyo, tena kwa urahisi sana.

Akachukua simu yake na kumpigia, akajitambulisha kama mwanaume aliyekuwa akiitwa Lukonge na alikuwa na taarifa zake nyingi kuhusu uhusiano wa siri uliokuwa ukiendelea baina yake na Masalu kitu kilichoonekana kumchanganya sana.

“Unasemaje?” aliuliza mwanamke huyo, kwa jinsi alivyoambiwa kila kitu kilichotokea, picha zake, akachanganyikiwa mno.

“Picha zako zote zipo. Ni picha chafu sana. Hivi mwanamke kama wewe mwenye familia yako, umewezaje kupiga picha kama zile. Hivi huyo mtoto wako, Vanessa atajifunza nini? Mwanamke mchafu sana wewe. Sasa kwa taarifa yako nazipeleka Facebook na WhatAapp. Tena kwa yule jamaa wa Mabadiliko ya Kweli,” alisema Godwin kwa kujiamini kabisa, tena wakati akizungumza na mwanamke huyo kwenye simu, mguu aliweka mezani, alikuwa na uhakika na kazi yake.

“Kaka yangu naomba usifanye hivyo, nakuomba usifanye hivyo nipo tayari kukupa kitu chochote kile,” alisema mwanamke huyo, tena kwa kuonyeshewa mfano, akatumiwa picha yake moja aliyokuwa mtupu kabisa ambayo alipiga chumbani kwa Masalu.

“Huna uwezo wa kunipa ninachohitaji!”

“Nina uwezo huo. Naomba nikupe chochote unachokihitaji!”

Mwanamke huyo alijiweka tayari kwa kila kitu, hakutaka kujali kuhusu heshima yake, alibanwa, alikuwa maji ya shingo. Aliongea kwa kutetemeka huku akisema kwamba alikuwa radhi kutoa kitu chochote kile, hata kama angeombwa penzi, kwa wakati huo alikuwa tayari lakini ilimradi tu picha zile zisiwekwe katika mitandao ya kijamii.

“Njoo Magomeni Usalama huku karibu na jengo la Tanesco, tena ukiwa wewe na mtoto wako tu. Nakupa dakika ishirini, ukichelewa naziweka haraka sana. Pia njoo na milioni tano, hizo ni kwa ajili ya kununua picha hizo, huwezi kuzipata bure,” alisema Godwin.

“Nashukuru baba! Nashukuru sana!” alisema huku akitamani hata kupiga magoti.

Hakutaka kuchelewa, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuchukua kadi yake ya benki kwa lengo la kuondoka kuelekea huko. Kwa kuwa kwenye simu yake alikuwa na milioni mbili, aliamini kwamba angeweza kutoa milioni tatu katika mashine ya ATM na kuwa na milioni tano na kwenda kumpa kijana huyo.

Aliifahamu mitandao ya kijamii, ilikuwa na nguvu sana, picha yako inapowekwa, ndani ya dakika kumi ilisambaa dunia nzima, kila mtu aliiona. Hakutaka kuona akipata aibu, alitaka kuona akiwa salama kabisa mpaka siku atakapoingia kaburini.

“Natoka!” aliwaambia walinzi ambao ni maofisa wa Usalama wa Taifa.

“Abdul! Twende naye!” alisema kijana mmoja.

“Hapana! Sitaki kwenda na mtu. Ninakwenda kwenye mambo ya kifamilia,” alisema huku akionekana kuwaka si kidogo.

Kila mmoja akatulia, haikuwa mara ya kwanza kwa mwanamke huyo kutaka kwenda sehemu peke yake kwani hata alipokuwa akienda kuonana na Masalu alikuwa akienda peke yake. Walinzi wote wakatulia, wakabaki wakimwangalia mwanamke huyo akiingia ndani ya gari na kuondoka zake.

Andrew alishangaa, hakujua mwanaume yule aliongea nini na mwanamke huyo. Hiyo ilikuwa nafasi yake na ilikuwa ni lazima afanye kile alichotakiwa kufanya. Alipoona mwanamke huyo ameeondoka, naye akaaga na kuanza kumfuatilia huku akiwa ndani ya gari lake.

“Umemuona?” aliulizwa na Godwin mara baada ya kupigiwa simu.

“Ndiyo! Nifanye nini?”

“Umteke. Nimekusaidia sana, bado unahitaji msaada wangu?”

“Naomba unisaidie! Nimechanganyikiwa, kichwa changu hakipo sawa. Naomba unisaidie, nakuomba sana mkuu,” alisema Andrew, kwa jinsi alivyokuwa akiongea ilikuwa vigumu kuamini kama mwanaume huyo alikuwa ofisa wa Usalama wa Taifa aliyekuwa mbabe.

Aliendelea kulifuatilia, gari lilipofika pembezoni mwa mahali kulipokuwa na nyumba za kota Magomeni Usalama nyuma ya jengo la Tanesco, akaambiwa na Godwin asimame na atulie kwani angefika mahali hapo muda si mrefu.

“Nimemsimamisha. Mfuate, ziba uso wako, mchukue na kuondoka naye, nenda kamfiche sehemu fulani salama kwani utakaa naye huko kwa siku kadhaa,” alisema Godwin.

“Sawa.”

Wakati mke wa Noel akiwa ndani ya gari, akashtukia mlango wa gari lake ukifunguliwa na mwanaume aliyekuwa kifua wazi huku akiwa ameziba uso wake kininja kwa kutumia kaoshi aliyokuwa ameivaa. Akamwambia mwanamke huyo akae nyumba ya gari na mtoto wake ili yeye aendeshe kuelekea sehemu.

“Naomba usiziweke picha zangu mitandaoni kaka! Nakuomba sana,” alisema huku akionekana kutetemeka, Andrew akaitikia kwa kutingisha kichwa,juu chini, chini juu.

Akaliwasha gari na kuondoka mahali hapo huku akimuweka mwanamke huyo katika walakini, ishu ilikuwa ni picha, kilikuwa kitendo cha kupewa na yeye kukabidhi pesa, ila kwa nini alikuwa akiondoka naye? Kila alichokiuliza, akakosa jibu.

***

Bi Sandra, mke wa Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel alikuwa akishangaa, hakujua kilichokuwa kikiendelea mpaka mwanaume huyo kuingia ndani ya gari na kuanza kuondoka naye. Alitamani kuuliza lakini kwa jinsi mwanaume huyo alivyokuwa amevaa, hakuthubutu hata kuufumbua mdomo wake na kumuuliza mahali walipokuwa wakielekea.

Gari liliendeshwa mpaka Kinondoni B na kuingizwa katika jumba moja kubwa na kuingizwa humo. Lilionekana kutokukaliwa na mtu kwani hata geti lenyewe alilifungua mwanaume huyo na kuliingiza ndani. Haraka sana akamfuata na kumfungulia mlango kisha kumwambia aelekee ndani pamoja naye.

“Jamani kaka yangu kuna nini? Mbona umenileta hapa na wakati uliniambia nije na pesa yako?” aliuliza Bi Sandra lakini Andrew hakujibu kitu.

Akawachukua wote wawili, yaani yeye na mtoto wake na kuwaingiza ndani. Alibadilika, hakutaka kuleta urafiki, alikuwa akiyafanya hayo kwa ajili ya familia yake ambayo wakati huo hakujua ilikuwa mahali gani. Akawapeleka ndani ya chumba kimoja kilichokuwa na mwanga hafifu na kuwahifadhi humo, akafunga mlango na kuondoka mahali hapo pasipo kuongea jambo lolote lile.

Bi Sandra alikuwa akilia na mwanaye, hawakujua kama mwanaume yule alikuwa Andrew, kijana waliyekuwa wakimpenda kutokana na utendaji wake mzuri wa kazi. Alitamani kumpigia simu mume wake na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea lakini alishindwa kwani mwanaume yule alipowaacha chumbani, aliichukua simu yake na kuondoka nayo.

Andrew hakutaka kubaki mahali hapo, akaingia ndani ya gari na kuondoka mahali hapo. Moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama ingetokea siku angekuwa mtekaji kama alivyokuwa. Alikuwa tayari kufanya lolote kwa wakati huo kwa familia yake, hakutaka kuona ikiuawa na wakati alitakiwa kufanya jambo ambalo alikuwa na uwezo nalo.

“Nimefanya kama ulivyoniambia! Familia yangu ipo wapi?” aliuliza Andrew alipompigia simu Godwin.

“Utaipata tu. Kuwa mpole,” alijibu Godwin huku akitoa tabasamu pana.

Upande wa pili alichokifanya Godwin kilikuwa ni kumpigai simu Noel na kuanza kuzungumza naye. Alimuanzia mbali lakini mwisho wa siku akamwambia kwamba kulikuwa na ktu alichotaka kumwambia hivyo amsikilize kwa makini kabisa.

“Kwanza wewe nani?” aliuliza Noel huku akionekana kuwa na hamu ya kusikia jibu kutoka kwa mwanaume huyo.

“Huna haja ya kunifahamu mimi ni nani! Ila ninataka ufanye jambo moja tu. Kusimama hadharani na kumshauri rais kwamba anatakiwa kuachia madaraka haraka iwezekanavyo,” alisema Godwin maneno yaliyomfanya Noel kushangaa, kwanza akacheka kwani kile alichoambiwa kilikuwa ni kitu kisichowezekana hata kidogo.

“Hahaha! Unanichekesha sana rafiki yangu!” alisema Noel huku akicheka kwa dharau.

“Sawa. Mpigie simu mke wako uzungumze naye,” alisema Godwin na kisha kukata simu.

Hilo likamchanganya Noel, hakutaka kuchelewa, kama alivyoambiwa ndivyo alivyofanya, akapiga namba za mke wake, simu haikuwa ikipatikana, hakujua kulikuwa na kitu gani na kitendo hicho kilianza kumpa shaka kwamba inawezekana jamaa huyo alikuwa amefanya jambo fulani kwa mkewe.

Akapiga simu nyumbani, akapokea mfanyakazi wa ndani ambaye alimwambia kwamba Bi Sandra hakuwepo, aliondoka kwenda mahali fulani, hakuaga, aliondoka ghafla sana.

“Hujui alipoondoka?”

“Ndiyo!”

“Hebu subiri!”

Akakata simu, alichanganyikiwa kwa kuhisi kwamba kweli kulikuwa na tatizo lililokuwa limetokea. Haraka sana akampigia Andrew ili kujua mahali alipokuwa mke wake. Alipompigia, mwanaume huyo alimwambia kwamba mke wake aliondoka, alipoondoka, hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua kwani alisema kwamba angerudi kama siku nyingine.

“Kwa nini hukuwaambia vijana kwenda naye?” aliuliza Noel.

“Alikataa katakata! Tukaona haina shida kiongozi, tukafanya kama alivyotaka. Kwani kuna tatizo lolote mkuu?” alisema Andrew na kuuliza kana kwamba hakujua kilichokuwa kimetokea.

Noel hakujibu swali hilo, akakata simu na kuondoka ofisini kwake kuelekea nyumbani. Alichanganyikiwa, alihisi kaibisa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, ilikuwaje apigiwe simu na mwanaume huyo na kuambiwa kuhusu mke wake na wakati aliondoka nyumbani na hakukuwa na mtu aliyejua?

Wakati akiwa njiani, akasikia simu yake ikilia mlio ulioashiria kwamba kulikuwa na ujumbe umeingia, haraka sana akaichukua simu yake na kuangalia ujumbe huo, ulikuwa uliosomeka ‘mkeo ametwekwa. Usijisumbue sana kumtafuta. Fanya nilichokwambia, vinginevyo nitawaua wote wawili, yeye na mtoto wako. Kingine cha msingi, hatakiwi mtu yeyote afahamu kama wametekwa, kitendo cha kufahamu tu kinamanisha kwamba utazikuta maiti zao baharini hapo kesho’.

“Wewe ni nani?” aliuliza baada ya kupiga simu.

“Mshikaji wako! Unatakiwa kufanya kila kitu nilichokwambia kwenye meseji na mara ya kwanza nilipokupigia simu. Una siku tatu tu za kufanya hivyo,” alisema Godwin na kisha kukata simu.

Ulikuwa ni mtihani ambao hakufikiria kama ingetokea siku moja angekuja kukutana nao. Akasimamisha gari pembeni na kuegemea usukani. Alikuwa na mwazo mengi kichwani mwake, ni kweli aliipenda familia yake lakini kuzungumza hadharani kwamba Rais Bokasa alitakiwa kujiuzulu lilikuwa jambo gumu mno.

Alimfikiria rais huyo, alikuwa mtu muhimu kwake, alikuwa akishirikiana naye kwenye kila kitu, hakuona kama kulikuwa na sababu ya kufanya mambo hayo yote, alipambana kila siku na alimuhakikishia kwamba kila kitu kilichokuwa kimeharibika kingewekwa sawa lakini kitu cha ajabu hata kabla hajaweka sawa mambo yake, tayari alitakiwa kumkana.

Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya. Kwa siku tatu alizokuwa amepewa zilikuwa chache sana hivyo alichokifanya ni kuelekea nyumbani kwake, alipofika tu, hakumuuliza mtu yeyote juu ya mke wake, alikumbuka kwamba aliambiwa hakutakiwa mtu yeyote afahamu kilichokuwa kimetokea.

Akaingia chumbani kwake na kulia sana, alishindwa kujua ni kitu gani alitakiwa kufanya lakini baada ya kulia sana, akaamua kusimama, kichwani mwake ulikuja uamuzi mmoja tu, kufanya kile alichoambiwa na mwanaume yule, kumtaka Rais Bokasa aachie madaraka haraka sana kwani nchi haikuwa ikielekea mahali pazuri.

“Nitazungumza kwa ajili ya familia yangu!”

Huo ndiyo uamuzi aliokuwa ameuchukua, hakutaka kuchelewa, huku akilia, akachukua simu yake na kumpigia rais kwa lengo la kuzungumza naye na kumwambia kwamba kuna kitu alikuwa njiani kwenda kukifanya hivyo asishangazwe na uamuzi huo, alikuwa akifanya hivyo kwa ajili ya familia yake tu.

“Kitu gani?” aliuliza Rais Bokasa, katika siku zote alizokuwa akimfahamu Andrew, hakukuwa na siku aliyosikia au kumuona akilia kama siku hiyo.

“Ni uamuzi mgumu sana, utakuumiza lakini nakuomba unielewe kwamba ninafanya haya kwa ajili ya familia yangu. Ninaipenda, ni kila kitu kwangu, siwezi kuiona ikiangamia na wakati nina uwezo wa kufanya jambo lolote lile kuiokoa,” alisema Andrew.

“Kuna nini tena?” alisikia rais akiuliza.

“Naomba unisamehe!”

“Nikusamehe kwa lipi? Niambie! Unataka kujiuzulu?”

“Hapana!”

“Kumbe?”

“Naomba unisamehe mheshimiwa rais, ninafanya hivi kwa ajili ya familia yangu,” alisema Andrew na kukata simu.

Hakuacha kulia, alikuwa akijifikiria ni kwa namna gani angelifanya jambo hilo. Alijua ni kwa jinsi gani watu wangeshtuka, alijua kwamba kila kona angezungumziwa yeye kwa kile alichokuwa akitaka kukifanya lakini hakutaka kujali, ilibidi kufanya vile kwa ajili ya familia yake tu.

Rais Bokasa alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, alimpigia simu Andrew kwa lengo la kuzungumza naye na kugundua tatizo alilokuwa nalo lakini mwanaume huyo hakutaka kupokea simu tena.

Alichokifanya ni kufunga safari na kumfuata nyumbani kwake, Masaki. Alitaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea mpaka kutaka kufanya uamuzi huo ambao aliamini kwamba ungekuwa ni wa kumuumiza kupita kawaida.

Alipofika nyumbani kwake, hakumkuta mwanaume huyo, aliambiwa kwamba alitoka kwenda kuzungumza na waandishi wa habari kwani alikuwa na jambo zito alilotaka kulizungumza.

“Amekwenda kukutana na waandishi wa habari?” aliuliza Rais Bokasa.

“Ndiyo mkuu! Ana press na waandishi!”

“Wapi?”

“Habari Maelezo!”

Hakutaka kuchelewa, ilikuwa ni lazima kwenda huko haraka sana. Wakati akiwa njiani, akafungua redio ya Taifa kwa lengo la kusikia kilichokuwa kikiendelea huko. Mtangazaji alitangaza kwamba kulikuwa na mkutano uliotarajiwa kuanza muda mfupi ujao kwani Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Noel alikuwa na mambo ya kutaka kuzungumza na waandishi wa habari Tanzania nzima.

“Wahini kabla hajaanza kuzungumza,” alisem Rais Bokasa huku akionekana kuchanganyikiwa, aliamini kwamba kwa lolote ambalo mwanaume huyo angelizungumza kwa waandishi hao lilikuwa jambo la kumuumiza tu kitu ambacho hakutaka kabisa kuona kikitokea.



IGP Ng’osha alichanganyikiwa, hakuamini kama mpigaji simu ambaye alijitambulisha kwa jina la Godwin alijua maovu yake yote ambayo kwake yalikuwa siri kubwa. Alibaki akitetemeka, ubabe wote aliokuwa nao ukatoweka na kuwa mdogo kama kidonge cha pritoni.

Aliogopa, alikuwa kiongozi wa jeshi la polisi Tanzania lakini alikuwa mbabe, aliyefanya mambo mengi ya chini, tena wakati mwingine kufanya mauaji kwa kuwa hara serikali yenyewe ilikuwa ya hovyo, iliyoongozwa na rais wa hovyo.

Akahisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake. Alimfahamu mtu huyo, alikuwa hatari, aliyaweka mambo mengi hadharani, watu walimsifia kwa kuwa kila alichokuwa akikiandika kilikuwa ni ukweli mtupu.

Pale alipokuwa amesimama, akahisi miguu ikikosa nguvu na kukaa kwenye kiti kiasi kwamba hata polisi wenzake wakabaki wakimshangaa.

“Mkuu!” aliita polisi mmoja kwa unyenyekevu mkubwa.

“Mfungueni huyo, hakikisheni mnaita waandishi wa habari na kuwaambia kwamba hakuwa na kosa,” alisema Ng’osha.

“Lakini mkuu...”

“Nimesema mfungueniiiiiii...” alisema kwa sauti kubwa iliyoonyesha kwamba hakuwa na utani juu ya lile alilokuwa akilitamka.

Kambili akatolewa katika chumba alichokuwa amefungwa, hakuelewa ni kitu gani kiliendelea kwani mateso aliyokuwa ameyapata siku hiyo hakuwahi kuyapata hapo kabla.

Waandish wa habari wachace wakaitwa na kupewa taarifa kwamba Kambili aliachiwa huru na kupelekwa nyumbani kwake. Alipofika, akatulia, mwili wake ulikuwa umevimba sana na kila wakati mkewe alipokuwa akimwangalia, alikuwa akilia tu kama mtoto.

Wakati akiwa hapo, akapokea simu kutoka kwa Godwin ambaye alimwambia kuwa kila kitu kilichokuwa kimetokea alikipanga yeye hivyo alitakiwa kufanya kila liwezekanalo, kuwaweka sawa wanachama wake kwani baada ya siku kadhaa, rais atatoka madarakani na yeye ndiye atakayekuwa rais.

“Mimi niwe rais?” aliuliza Kambili huku akiwa haamini.

“Ndiyo! Wewe ni mpambanaji sana, utakuwa rais wa nchi hii. Kesho mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel anakwenda kumkataa rais, huo ni mwanzo, akitoka huyo watakuja wengine na wengine, waambie wanachama wako huu ndiyo muda wa kugangamara, watakaoshindwa, achana nao. Nitahakikisha mpaka unaingia ikulu,” alisema Godwin kwenye simu.

“Unanichanganya! Yanawezekana vipi haya?”

“Fanya kwa nafasi yako. Ya nafasi yangu, niachie mimi,” alisema Godwin na kukata simu. Kambili akabaki akiwa hafahamu ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.

***

Haikuwa lengo la Noel kuwaita waandishi na kuwaambia kwamba hakuwa akiridhishwa na rais na hakutaka kumuunga mkono bali nyuma kulikuwa na kitu ambacho kingeweza kuiondoa familia yake duniani.

Alikuwa akiipenda, kwake, Sandra na mtoto wake walikuwa kila kitu, alikuwa radhi kupoteza kitu chochote kile maishani mwake ikiwemo kazi lakini si kuiona familia hiyo iliyokuwa ikimpa furaha wakati wa huzuni, upendo wakati wa kukata tamaa ikiondoka mikononi mwake.

Waandishi wa habari walikuwa wamekusanyika kwa wingi Habari maelezo, walitaka kusikia kile kilichomfanya mkurugenzi wa Usalama wa Taifa kuwaita mahali hapo na kutaka kuzungumza nao jambo muhimu.

Hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua kilichokuwa kikiendelea, kila mmoja alikuwa na hamu ya kutaka kusikia kile ambacho Noel alikuwa tayari kukizungumza mbele ya waandishi wa habari.

Watu waliokuwa majumbani, walifuatilia moja kwa moja mkutano huyo katika televisheni na redio zao huku wale waliokuwa katika nchi mbalimbali wakifuatilia kila kitu katika televisheni zilizokuwa katika Youtube ikiwemo televisheni ya Global TV.

Baada ya waandishi wa habari wote kuwa tayari, Noel akaingia ukumbuni hapo na moja kwa moja kuelekea katika meza pekee iliyokuwa humo ambayo ilikuwa na viti kisha kutulia.

Siku hiyo alionekana kuwa tofauti, watu walimfahamu kama mtu aliyependa sana kutabasamu kila anapokuwa mbele ya waandishi wa habari lakini siku hiyo alionekana kuwa tofauti, uso wake ulionyesha picha mbaya kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea.

“Habari zenu,” alianza kwa kusalimia.

“Salama tu kiongozi,” wakaitikia waandishi wengine.

Moyo wake ulikuwa na dukuduku kubwa, aliwaangalia waandishi wale, kichwa chake kikaanza kufikiria kile ambacho magazeti na vyombo vya habari vingeandika juu yake. Alijua kwamba kungekuwa na watu ambao wangemlaumu hasa viongozi lakini aliamini kwamba asilimia tisini ya Watanzania wangemuunga mkono kwa sababu hakukuwa na wananchi wengi wakimpenda Rais Bokasa.

“Nimewaita kwa jambo moja tu. Najua wengi mnaona jinsi ninavyopambana, jinsi ninavyorekebisha mambo kutoka huku kwenda kule. Nimekuwa nikiwatumikia wananchi kwa nguvu zote, niliapa kufanya hivyo, na ninamshukuru Mungu kwa kuwa alinipa nguvu,” alisema, akanyamaza, akawaangalia waandishi na kuendelea:

“Ninawashukuru waandishi wa habari, mmekuwa pamoja nasi, tulipokosea, mlitusema, tulipopatia, mkatupongeza. Nimekaa na kuangalia hali ya nchi, kiukweli, nimeamua kuweka uamuzi mmoja. Sikulazimishwa, nimekaa na kuamua hivyo kwa manufaa ya Watanzania.,” alisema, kisha akanyamaza tena, akainamisha kichwa chake, baada ya sekunde kadhaa, akakiinua, machozi yakaanza kumlenga.

“Simuungi rais mkono!” alisema sentensi ambayo ilizua minong’ono mahali hapo, kila mtu aliyesikia hakuamini kama kweli sentensi hiyo ilitoka kwa mwanaume huyo ambaye kila siku alikuwa bega kwa bega kuhakikisha unyonyaji na unyanyasaji wa Rais Bokasa ukiendelea kwa wananchi, inakuwaje leo, tena kwa kujiamini atamke sentensi hiyo.

“Najua mmeshtuka. Nimeiangalia Tanzania, kule tunapoelekea, si pazuri, na hata hapa tulipo si pazuri kabisa. Nikiendelea kuweka msimamo wangu wa kumuunga mkono, nitakuwa nawaumiza Watanzania wengine. Nimenawa mikono yangu, simuungi mkono rais wetu. Sina imani naye hata kidogo,” alisema Noel, akanyamaza na kuwaambia kwamba alikuwa akikaribisha maswali mawili tu.

“Samahani mkuu! Umesema humuungi mkono rais, je, ni kweli suala la kukosa imani naye limeanza hili au kuna kitu nyuma ya pazia?” aliuliza mwandishi wa Gazeti la Uwazi.

“Hakuna kitu! Huwa sifanyi jambo kwa sababu ya mtu fulani. Huu ni muda wangu wa kutulia na familia yangu, naomba muelewe kwamba sijalazimishwa na mtu kuamua hivi,” alijibu Noel. Mwandishi wa Global TV naye akanyoosha mkono kuuliza swali.

“Nakumbuka kwenye Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli, yule msumbuaji aliandika kwamba anampa rais miezi miwili kujiuzulu vinginevyo atapinduliwa, je, huu ni mmoja wa mkakati?” aliuliza mwandishi huyo, Amani Madebe.

“Huwa siingii kwenye mitandao ya kijamii, sijui chochote kinachoandikwa huko, sifuatilii, kama liliandikwa hilo, sijui chochote kile, ninachoomba ni kwamba ieleweke kuwa nimefanya hivi kwa ajili ya familia yangu, ninahitaji kukaa nayo, ila pia kwa jinsi Watanzania wanavyoishi, nadhani damu zao zitadaiwa mikononi mwangu,” alijibu Noel, hakutaka kuendelea, akasimama na kuondoka zake.

Wakati Noel akiwa amemaliza, Rais Bokasa alikuwa akikaribia Habari Maelezo, ndani ya gari alipokuwa akisikiliza mahojiano hayo yaliyokuwa yakiendelea, moyo wake ulimuuma, kijasho chembamba kikaanza kumtoka huku akiwa haamini kilichokuwa kikitoka mdomoni mwa Noel.

Alimwamini kijana huyo, alipambana naye hasa baada ya kufanya mauaji ya mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Kimwinyi aliyeuawa nchini Nigeria, aliamini kwamba huyo ndiye angeenda naye mpaka mwisho lakini mwisho wa kila kitu kilikuwa ni kuwaita waandishi wa habari na kuwaambia kwamba hakuwa na imani naye.

“Hivi kweli Noel anaweza kufanya uamuzi wa kijinga kama huu?” alijiuliza bila majibu.

Msafara huo ukafika mahali hapo, rais akashindwa kuteremka, alichokifanya ni kumwambia mlinzi wake kwamba msafara ugeuke na kuelekea ikulu kwani aibu aliyokuwa nayo ilikuwa kubwa mno na kuhisi kama alipakwa kinyesi usoni.

Haraka sana msafara ukageuka na kuondoka huku waandishi wa habari waliokuwa nje wakipiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.

Hiyo ndiyo ilikuwa stori ya siku, gumzo la nchi nyingi kwamba hatimaye mkurugenzi wa Usalama wa Taifa hakuwa na imani na rais wake. Wengi walishangaa lakini kwenye mitandao ya kijamii alipokea sifa kwamba alikuwa mzalendo wa kweli na viongozi wengi walitakiwa kumuunga mkono kwa kile alichokuwa amekifanya.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Yaani huyu jamaa nilikuwa simpenda, ila kwa hili alilolifanya, hakika yeye ni shujaa,” aliandika jamaa mmoja kwenye akaunti yake Facebook.

“Hata mimi! Huyu jamaa nilikuwa simpendi mno. Duuh! Leo imekuwaje mpaka kabadilika hivi?” alihoji jamaa mwingine kwenye posti hiyo.

Hakukuwa na mtu aliyejua sababu ya Noel kufanya hivyo, hawakujua kama familia yake ilitekwa na alifanya hivyo kama njia mojawapo ya kutaka wasiuawe. Siku hiyohiyo baada ya Noel kumaliza kuzungumza, Godwin akaandika katika akaunti ya Mabadiliko ya Kweli maneno yaliyosema: ‘Asipojiuluzu, atapinduliwa. Sijawahi kusema uongo’, posti ambayo ilizua mijadala mingi kwamba je, ni yeye aliyekuwa nyuma ya hilo? Hakukuwa na mtu aliyejua.

***





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog