Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

FURAHA HATIMAYE - 2

 






Simulizi : Furaha Hatimaye

Sehemu Ya Pili (2)







Chumba cha mahabusu kilikuwa na giza nene, harufu ya mkojo kila mahali watu zaidi ya hamsini walikuwa wamelala kwenye chumba kidogo chenye uwezo wa kuchukua watu ishirini. Dk Othman alikuwa katikati,kimya kabisa mwenye majuto moyoni mwake, fikra zake zilimfikisha kwenye aibu ambayo angeipata baada ya watu kusoma habari zake kwenye magazeti, bila shaka kila mtu angemwona ni mpumbavu, mtu asiye na busara ambaye kwa sababu ya mwanamke tu aliamua kuua wakati alikuwa na uwezo wa kumpata mwanamke mwingine yeyote, pengine mzuri kuliko Halima.

Mawazo yake yakampeleka kwa mama yake mzazi, roho ikamuuma sana, alijua ni kiasi gani mama yake alimpenda, hakuwa na uwezo wa kuyapima maumivu ambayo angeyapata akiwa mtoto tegemeo kwa familia yake! Othman alishindwa kujihurumia, hakuwa na uwezo wa kuyabeba maumivu yaliyokuwemo moyoni mwake, akajichukia, akajiona hafai kuishi! Hakuwa na ujasiri wa kushuhudia mama yake akilia, hakuwa na ujasiri wa kuonana uso kwa uso na watu ambao wangekuja kituoni kumwona. Alipomfikiria Balozi Lutta ndio wasiwasi ulizidi kumkumba zaidi, alielewa ni kitu gani kingempata mwisho wa siku; kitanzi! Akaigusa shingo yake na kuona haikustahili kabisa kutiwa kitanzi na mtu mwingine, kwa unyonge huku akilia akanyanyuka na kuivua suruali yake huku mahabusu wengine wakiwa wamelala, akapanda juu akikanyaga kwenye nondo, mpaka akafanikiwa kuzifikia mbao za juu akaifunga suruali yake kwenye moja ya mbao kisha kufunga upande wa pili shingoni mwake, AKARUKA NA KUNING’INIA!

*****

Halima alikuwa amekaa pembeni mwa kitanda cha Gerald, akiendelea kulia kwa uchungu, hakumfikiria tena Dk. Othman wala kumwonea huruma. Aliamini duniani hakuwepo binadamu mwenye roho mbaya kama yeye, jambo ambalo hakulitegemea kabisa kwani ni Dk. Othman huyo huyo ndiye aliokoa maisha yake baada ya kupata ajali! Hilo alilifahamu lakini hakutaka kabisa kulikumbuka, kitendo cha kumchoma Gerald sindano ya PPF kwenye mshipa ili afe kilikuwa kimemuumiza sana moyoni na kila alipomwangalia Gerald kitandani akizidi kuhangaika, akihema kwa kutumia mashine ya hewa na mwili wake ukizidi kuvimba, maumivu yaliongezeka.



Bado alimpenda na alitamani sana apone ili hatimaye waweze kuoana kama walivyopanga wakiwa shuleni, alikuwa tayari kuyasamehe yote yaliyojitokeza kati yao mpaka Gerald akapotea na yeye kuamini alikuwa ametelekezwa! Mara kwa mara alifumba macho na kumwomba Mungu atende muujiza ili Gerald aweze kuzinduka katika usingizi wa kifo aliokuwa amelala lakini bado aliendelea kuwa kimya kitandani, hakuwa na uhakika kama angepona.



Saa 3:00 asubuhi Profesa Kayuga aliingia wodini akiwa ameongozana na madaktari wenzake, wakamwomba Halima atoke nje ili wampime mgonjwa. Hakwenda mbali, alitoka na kuketi nje kando ya mlango akiendelea kuyafikiria mambo yote yaliyokuwa yakimtokea, kitu ambacho hakukifiria kabisa ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wala hakuwaza kwamba alikuwa mwanafunzi na wenzake walikuwa wakiendelea na masomo ya mwaka wa pili, alimfikiria Gerald, alikuwa tayari hata kurudia mwaka lakini awe naye.



"Binti!" Aliitwa nusu saa baadaye mlango ulipofunguliwa, alichokifanya ni kunyanyuka na kukimbia hadi ndani bila kumsikiliza mtu aliyemwita, wasiwasi wake ulikuwa ni kwamba pengine Gerald alikuwa ameaga dunia.



"Vipi daktari?" Alimuuliza Profesa Kayuga.

"Hali ya mgonjwa inazidi kuwa mbaya, kinachohitajika hapa si kingine ni figo tu, akipata figo sasa hivi hali yake itakuwa nzuri, kinachomsumbua si dawa iliyochomwa kwenye mshipa tena, hiyo imekwishayeyuka na moyo wake unafanya kazi vizuri!"

"Mnahitaji figo ngapi daktari?"

"Moja tu!"

"Niko tayari kutoa, sasa hivi nipelekeni chumba cha upasuaji!"

"Kweli?"

"Kundi lako la damu ni?"

"O!"

"Sawa, jiandae, kuna mtu ungependa kumuuliza? Labda wazazi wako?"

"Nina miaka zaidi ya kumi na nane, hivyo ninaweza kuamua mambo yangu mwenyewe kwa uhuru, siwezi kumwacha Gerald afe wakati mimi ninazo figo mbili, nipeleke chumba cha upasuaji haraka daktari!"

"Sista, hebu mpeleke huyu binti akapimwe hivi vipimo nilivyoviandika hapa kwenye cheti!" Profesa Kayuga alimwambia muuguzi mmoja akimkabidhi faili la Gerald.

"Twende!" Muuguzi alimwambia Halima wakaanza kutembea kuelekea mlangoni, kabla hawajatoka mlango ukafunguliwa, mzee mrefu mwembamba aliyevaa suti iliyoonekana kuwa ya thamani kubwa aliingia akiongozana na mwanamke mfupi mnene, Halima alipomwangalia tu usoni bila hata kujiuliza alimtambua kwa jinsi alvyofanana na Gerald kwa sura, alikuwa Balozi Lutta na mkewe, alithibitisha jambo hilo alipomsikia profesa Kayuga akimwita.



"Karibu sana Balozi!"

"Ahsante, vipi hali ya mwanangu?"

"Sio mbaya sana, ila ni vizuri mmekuja!"

"Tatizo nini?"

"Moja ni lile nililokueleza kwenye simu, pili ni figo, figo zake zote zinaelekea kufa, muda si mrefu kama hatujachukua hatua za kupata figo nyingine jambo ambalo sote hatulitaki linaweza kutokea!"

"Yuko wapi huyo daktari kwanza?"

"Lutta hilo limeshashughulikiwa, tutalirejea baadaye, kwa hivi sasa tutafute figo kwanza, kuna huyu binti amejitolea kutoa figo yake moja!"



Balozi Lutta hakuweza hata kuyasikia maneno hayo, akili yake yote ilikuwa kitandani kwa mtoto wake, mikono yake yote miwili ilikuwa ikimpapasa Gerald usoni, akishangazwa na namna alivyokuwa amevimbiana kuanzia usoni hadi miguuni, hakuweza kuyazuia machozi lakini ilikuwa tofauti sana na mwanamke aliyeongozana naye, yeye hakuonyesha kuumizwa sana na tukio hilo.



"Daktari umesema kuna binti amejitolea kutoa figo?"

"Ndio!"

"Yuko wapi?""Huyu hapa ndio alikuwa anakwenda maabara!"

"Mh! Binti ahsante sana, wewe ni nani?"

"Naitwa Halima!"

"Wewe ndiye ulikuwa unanisumbua kunipigia simu wakati ule ukimuulizia Gerald?" Mwanamke aliyeongozana na Balozi Lutta aliongea akimwangalia Halima kuanzia kichwani hadi miguuni kisha akasonya kwa nguvu, watu wote chumbani kuanzia madaktari hadi wauguzi wakamshangaa.

"Mke wangu, acha tabia hiyo!"

"Ya nini figo yake, unamfahamu huyu binti? Visichana vya siku hivi vichangudoa hivi, kije kimpe mwanetu figo yenye virusi halafu afe? Kwenda zako, kenge wee!" Mama alitukana bila hata aibu, watu walioko wodini wakaweka mikono midomoni katika hali ya kutokuamini kwamba maneno hayo yalikuwa yametoka mdomoni mwa mke wa balozi.



Huzuni ya hali ya juu ilimshika Halima, akaanza kutembea kwa unyonge kuelekea mlangoni huku machozi yakimtoka! Haikuwa rahisi kabisa kuamini kuwa jambo hilo lilikuwa limemtokea, nia yake ilikuwa ni kuokoa maisha ya Gerald lakini mwanamke aliyeonekana ndiye mama yake wa kufikia kutokana na maelezo ambayo Gerald alimpa siku za nyuma alikuwa amemfukuza kama Mbwa, akafungua mlango na kutoka nje akiwa amegubikwa na aibu pamoja na simanzi, alihisi miguu yake inapoteza nguvu, hata hivyo akajitahidi kutembea taratibu na kuizunguka wodi hadi dirishani kwenye chumba alichokuwa amelazwa Gerald.



"Sasa umemfukuza wewe utatoa figo?"

"Ndio, kwani tatizo nini? Kama wewe ulimpa wakati ule kwanini mimi nishindwe, hata kama Gerald si mwanangu wa kuzaa, siwezi kumwacha afe, sipo tayari kuona anapewa figo na watu wasioeleweka!"

"Basi jiandae uende maabara ukapime!"

"Twendeni!"

"Je, ukikutwa figo yako ni tofauti tutafanyaje?"

"Haiwezekani!"

"Kundi lako na damu ni lipi mama Balozi?"

"O!"

"Inawezekana ikafanana!" Profesa Kayuga aliongea na kushauri mwanamke huyo apelekwe chumba cha maabara haraka iwezekanavyo, hiyo ilimuumiza sana moyo Halima aliyesikia maongezi yote hayo kutoka nyuma ya wodi, akilia machozi alianza kukimbia mbio kutoka nje ya hospitali ambako alipanda daladala lililompeleka mpaka Mwenge, huko akaunganisha kwa daladala jingine hadi Chuo Kikuu, njia nzima alikuwa akilia na alipofika chumbani hakumkuta msichana waliyechangia naye chumba, akaingia na kuchukua begi lake dogo, akachukua nguo kadhaa na kuweka ndani yake kisha kuchukua karatasi na kalamu, akaandika maneno machache na kuweka juu ya meza.



Nimechoka kuishi, bora nife, niagie kwa wazazi wangu

Ni mimi

Halima,

Marehemu mtarajiwa.



Hakutaka tena kupoteza muda, akatoka nje na kuanza kukimbia hadi nje ya mabweni ambako alichukua teksi na kumwamuru dereva aondoke kwa kasi.



****



“Mnapima nini na nini?”

“Figo zako kama zitashabihiana na za mgonjwa!”

“Kingine?”

“Damu!”

“Damu?”

“Ndio!”

“Kuangalia nini?”

“Kama iko sawa na ya mgonjwa, pia kama imeathirika au la!”

“Mh!”

“Mbona unaguna mama?”

“Mnapima na damu kubwa?”

“Unamaanisha nini damu kubwa?”

“Virusi vya Ukimwi!”

“Hiyo ni lazima!”

“Mh! Kama ni hivyo basi tena, mimi siko tayari kupimwa kipimo hicho!” Mama Lutta aliongea akitoka nje ya chumba cha maabara na kuwaacha wafanyakazi hawaamini walichokishuhudia.

*****

“Wapi dada!” Dereva teksi aliuliza akiondoa gari nje ya hosteli za Mabibo huku macho yake yakimwangalia Halima usoni, kuna kitu alijifunza kabla hajajibiwa.

“We twende tu!”

“Mpaka wapi sasa? Nataka kufahamu ili nikuambie bei!”

“Nyoosha moja kwa moja hadi Ilala Shauri Moyo karibu na ofisi za TRA, utaniacha hapo!”

“Shilingi elfu mbili!”

“Twende, usijali sana kuhusu bei, we niwahishe tu!”

Gari liliondolewa kwa kasi ya ajabu na kuingia barabara ya Mandela iliyokuwa mita kama mia hivi kutoka kwenye lango la kuingilia hosteli, dereva akanyoosha moja kwa moja hadi Ubungo kwenye makutano ya barabara za Mandela na Morogoro, yeye akakata kulia kuingia barabara ya Morogoro na kunyoosha hadi Magomeni. Muda wote akiendesha gari alimwangalia mteja wake kupitia kioo kilichokuwa juu ya kichwa chake na kumuona akibubujikwa na machozi.

“Vipi dada umefiwa?” Dereva aliuliza lakini Halima hakujibu kitu, aliendelea kulia kwikwi ikiwa imemkaba.

Kichwa chake kilikuwa kimevurugika sana, mambo yaliyomtokea yalikuwa ya kuumiza mno. Kitendo cha kufukuzwa wodini kama mbwa wakati alikuwa amejitolea kutoa Figo yake moja kwa Gerald, kilimsabaishia maumivu sawasawa kabisa na mtu kuchomwa mkuki moyoni. Hakufikiria tena juu ya elimu yake ya Chuo kikuu, wala wazazi wake, alichotaka yeye wakati huo ni kufa ili aondoke duniani kwenda kupumzika, kwake kufa ilikuwa ni sawa na kutangulia ahera ambako angemsubiri Gerald waishi maisha ya raha bila kuingiliwa na mtu yeyote, fikra hizi zilimfanya azidi kulia kwa uchungu hasa alipopiga picha kwa akili yake na kumuona Gerald akihangaika kitandani.

“Samahani dada nimekuuliza kama umefiwa!”

“Hapana!”

“Sasa mbona unalia hivyo? Jikaze, usije ukaumia kichwa!”

“Ahsante sana!” Halima aliitikia.

Dakika tatu baadae teksi iliegeshwa mbele ya jengo la ghorofa, Halima alipokisoma kibao kilichokuwa mbele yake aliona maandishi “Tanzania Revenue Authority, Ilala Region, akamkumbuka binamu yake aitwaye Mwangaza, aliyefanya kazi katika ofisi hiyo, moyo wake ukamuuma zaidi hasa alipofikiria kwamba hata yeye alikuwa anamwacha duniani baada ya kufa, alishindwa kuelewa angezipokea habari za kifo chake. Akiliangalia jengo hilo, Halima akafungua mlango wa gari na kushuka.

“Chukua fedha yako kaka, nashukuru sana kwa kunifikisha salama, nasikitika hatutaonana tena!”

“Kwanini unasema hivyo? Binadamu hukutana, kwani wewe sio mwanafunzi wa chuo?”

“Nilikuwa mwanafunzi!”

“Umemaliza?”

“Hapana, nimeamua kukatisha masomo!”

“Kwanini?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Halima hakuweza kujibu tena swali hilo, machozi mengi yakambubujika, hakutaka tena kubaki sehemu hiyo, akavuka barabara na kuanza kukimbia akimwacha dereva amesimama eneo hilo. Hatua kama hamsini hivi mbele yake, alikutana na reli akakata kushoto na kuanza kufuata reli hiyo kuelekea chini ambako hapakuwa na watu kabisa, akaketi juu ya reli na kuanza kulia.

“Nataka nigongwe na treni, nyama zangu tu ndio zipatikane zikiwa katika vipande vipande! Sitaki kuishi tena, najua nitawaumiza sana wazazi na ndugu zangu, wengi wataniona mjinga nisiye na akili, lakini hawatakuwa wamebahatika kuyafahamu maumivu yaliyonipata!” Halima alijisemea moyoni mwake akizidi kulia, ghafla picha ya Dk. Othman ikamwingia kichwani mwake, BADO ALIMCHUKIA KWA KITENDO ALICHOKIFANYA.

Alilala kifudidudi akiwa amekatika reli na kusubiri treni lije.

**********

Katika hali ambayo si madaktari wala Balozi Lutta aliitegemea, Gerald alifumbua macho yake na kuangalia huku na kule chumbani, akamuona baba yake, hakukomea hapo akaendelea kuzungusha tena zaidi kama vile aliyekuwa akimtafuta mtu mwingine zaidi, mwisho akarejea tena kwa baba yake.

“Shika….moo ba….ba!” Akaongea kwa tabu.

“Marahaba hujambo?”

“Naumwa, hali yangu ni mbaya, nafikiri figo zangu zimekufa tena, nahitaji mtu wa kunisaidia!”

“Ndio maana tuko hapa mwanangu, mama yako amekwenda maabara kupima damu kuona kama figo zake na za kwako zinaweza kuwa sawa, subiri kidogo mwanangu, utapona tu!”

“Umekwishaonana na msichana mmoja anaitwa Halima?”

“Ndio!” Balozi Lutta aliitikia.

“Ni mchumba wangu, kama ikitokea nikapona ni lazima nimuoe, amenisaidia sana mimi nina uhakika hata yeye anaweza kunipa fig…Aaah! Mamaaaa, na wewe umekuja? Ahsante sana kwa kukubali kunipa figo yako!”

“Nani? Atoe figo? Mimi? Haiwezekani, siwezi kupimwa kipimo cha Ukimwi hapa Tanzania, kama wanataka nitoe figo basi nitoe bila kupimwa Ukimwi!” Aliongea mama wa kambo wa Gerald na kuwafanya watu wote ndani ya chumba ikiwa ni pamoja na balozi Lutta washike midomo yao kwa mshangao, hakuna aliyetegemea hata kidogo kwamba mwanamke huyo angetoa maneno kama hayo mbele ya mgonjwa wakati alishakubali yeye mwenyewe kwenda maabara kupima, watu wote wakamkumbuka Halima.

“Sasa kama ulijua hauko tayari kutoa figo ni kwanini ulimfukuza Halima aliyekuwa tayari kutoa figo? Au unataka mwanangu afe?” Balozi Lutta aliuliza akilengwalengwa na machozi.

Gerald aliposikia maneno hayo tu, alikakamaa na kurejea katika hali ya kupoteza fahamu, hewa ya oksijeni ikawekwa puani na mdomoni kwake, kilichowashangaza madaktari ni presha yake, ilishuka kwa kasi ya ajabu.





Halima akiwa amechanganyikiwa baada ya kufukuzwa wodini na mama wa kambo wa Gerald, ameamua kufa hivyo amekwenda mpaka Ilala na kulala relini akisubiri treni ije kumgonga afe. Je, nini kitatokea? Wodini nako hali ya Gerald in mbaya, alizinduka kwa muda mfupi lakini baadaye fahamu zake zikapotea tena baada ya kuambiwa Halima amefukuzwa, presha yake inazidi kushuka kwa kasi ya ajabu. Je, nini kitaendelea wodini? Fuatilia…



Halima alizidi kulala juu ya reli, akielewa kabisa jambo alilokuwa akilifanya halikuwa sahihi lakini alikuwa amedhamiria kulifanya. Kwake kufa ilikuwa ni jambo bora kuliko kuendelea kuishi na maumivu aliyokuwa nayo moyoni mwake, aliwafikiria wazazi wake, rafiki zake roho ikamuuma lakini hakuwa na jinsi ilikuwa ni lazima afe kifo alichokuwa amekichagua.



Kwa karibu dakika arobaini na tano nzima alikuwa juu ya reli, akisubiri kwa hamu kubwa treni lifike ile aondoke duniani, hakuogopa wala kutetemeka ingawa kila alipolifikiria kitendo cha mwili wake kugawanywa na matairi ya chuma ya treni, mwili wake ulikufa ganzi. Dakika tano baadaye, akasikia honi ya treni likija kwa kasi, akajua tayari mwisho wake umefika, akafumba macho na kuukakamaza mwili wake tayari kwa vyuma kumchanachana.



“Mungu nisamehe,najua kwa jambo hili lazima nitakwenda motoni, lakini sina jinsi!” Aliwaza akisikia muungurumo wa treni ukizidi kumkaribia.



*****

Pilika pilika ilianza tena wodini, juhudi za kupandisha mapigo ya moyo wa Gerald zilikuwa zikifanyika. Madaktari walikuwa hawajakata tama,walitaka kufanya kila kilichowezekana kuokoa maisha ya kijana huyo. Balozi Lutta alibubujikwa na machozi alipoona mtoto wake akihangaika kitandani, lawama zote zilikuwa kwa mke wake, alihisi kwa vyovyote mwanamke huyo alikuwa amedhamiria kumuua Gerald kwa sababu alikuwa mtoto wake wa kambo. Kwa hali aliyokuwa nayo madaktari hawakutaka balozi Lutta aendelee kuwepo wodini, ikaamriwa atolewe nje ambako aliendelea kulia, alimpenda Gerald na hakutaka kabisa afe.



Dakika thelathini baadaye, mlango wa chumba ukafunguliwa, Profesa Kayuga akatokeza akikimbia kuelekea ofisini kwa wauguzi, jasho jingi likimtoka, balozi Lutta akajua tayari mwanae alishakata roho! Wakati anarudi alimtangizia na kusimama katikati ya njia.

“Vipi Kayuga?”

“Hali ya mtoto si nzuri sana lakini bado tunajitahidi!”

“Jitahidi ndugu yangu, okoa maisha ya mtoto wangu ambaye pia ni mwanao!”

“Sawa niache basi nikaendelee na kazi!” Profesa Kayuga aliongea, balozi Lutta akampisha njiani na kuanza kukimbia tena kuelekea chumba alicholazwa Gerald.

Balozi Lutta na mke wake walibaki wameketi kwenye benchi nje ya wodi, hawakuongea chochote, kila mtu akiwa na mawazo yake kichwani, wakati balozi alifikiria kuokoa maisha ya mwanae, mke wake alifikiria namna ambavyo Gerald angekufa na kuuacha urithi wa balozi Lutta mikononi mwa watoto wake, kuendelea kwake kuishi kungempa haki ya mtoto wa kwanza, ndio maana alifikia uamuzi wa kumfukuza Halima wodini ili asitoe figo yake.

Haukuputa muda mrefu sana kabla mlango haujafunguliwa tena, safari hii akajitokeza muuguzi na kumwita balozi Lutta, akanyanyuka na kumfuata mlango alipokuwa amesimama, kichwani mwake alielewa jambo moja tu, alikuwa anakwenda kupewa taarifa za msiba, machozi yaliyokuwa yameanza kukauka yakamtoka tena na kulowanisha mashavu yake, siku hiyo hakujali tena kama alikuwa kiongozi mwenye mamlaka makubwa katika nchi.

“Vipi binti?” Balozi alimuuliza muuguzi huyo.

“Kidogo afadhali, presha imedhibitiwa, sasa hivi iko tisini chini ya hamsini!”

“Pyuuuuu! Bwana apewe sifa!” Balozi Lutta akashusha pumzi kisha kumshukuru Mungu.

“Sasa nimekuita sababu ya kitu kimoja, tatizo la Gerald ni figo, uchafu hautoki mwilini ndio maana hali yake inazidi kuharibika, profesa ameniomba nikuulize kama unaweza kupata mtu mwingine wa kutoa figo!”

“Mtu mwingine? Haraka kiasi gani?”

“Haraka iwezekanavyo!”

“Sina uhakika, nahitaji kumtafuta yule binti, kwani anaishi wapi?”

“Kwa taarifa nilizonazo ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu, anaishi Mabibo hostel!”

“Hali ya Gerald inaweza kuniruhusu niende kumtafuta?”

“Subiri nimwite profesa uongee naye, atakuwa kwenye nafasi nzuri ya kujibu swali hilo!”

Muuguzi akaondoka kwenda ndani, sekunde chache baadaye profesa Kayuga akajitokeza na kumkuta balozi Lutta amesimama akionekana mwenye wasiwasi mwingi, akampa maelezo yote kama yalivyokuwa yametolewa na muuguzi, mwisho akasisitiza hapakuwa na muda zaidi ya masaa ishirini na nne kabla damu ya Gerald haijabadilika na kuwa na uchafu uitwao Urea, ambao ungemuua hata kama wangefanya kitu gani.

“Wacha nikajaribu kumtafuta huko Chuo Kikuu!”

“Sawa, jitahidi!”

Profesa Kayuga aliondoka mbio hadi sehemu ya maegesho ya magari, hakukumbuka hata kumuaga mke wake. Dereva alikuwa akimsubiri, akaingia na kumwamuru waondoke haraka iwezekanavyo kuelekea Hostel za Mabibo. Kutoka hospitali ya Muhimbili hadi hosteli za Mabibo kupitia barabara ya Ali Hassan Mwinyi, Sam Nujoma, Mandela na hatimaye Mabibo ilikuwa ni safari ya muda wa nusu saa lakini kwa amri ya balozi Lutta akiwa tayari kwa lolote, zilitumika dakika ishirini tu gari likawa limeegeshwa mbele ya lango la kuingilia Mabibo.

“Vipi wazee?” Mlinzi aliwauliza kabla hajafungua lango.

“Nimekuja kumfuatilia binti yangu!”

“Anaitwa nani?”

“Halima!”

“Mbona alitoka!”

“Kwenda?”

“Sifahamu lakini alipanda teksi ya Awadhi!”

“Yuko wapi huyo Awadhi?”

“Subiri!” Mlinzi akasema na kusonga mbele ambako alianza kuita jina la Awadhi kwa kama dakika mbili.

“Yeeees, abiria?”

“Hapana, kuna mzee ana shida na wewe hapa!”

“Yuko wapi?”

“Hapa kwenye gari!”



Balozi Lutta alishtukia mlinzi akisimama dirishani kwake akiwa na kijana shombe wa kiarabu, ambaye alimwamkia na baadaye kuuliza kama angemsaidia jambo lolote maana hakuonekana mtu anayehitaji usafiri.

“Kijana, uliondoka hapa na Halima?”

“Ndio!”

“Mimi ni mzazi wake, namtafuta!”

“Kuna nini lakini? Maana yeye mwenyewe njia nzima alikuwa analia, nikamuuliza kama alikuwa amefiwa lakini hakujibu chochote, nilihisi kuna matatizo makubwa!”

“Ulimpeleka wapi?”

“Nilimshusha Ilala karibu na ofisi za TRA!”

“Akaelekea wapi?”

“Nilimshuhudia akitembea kusonga mbele na baadaye akashuka chini akiifuata reli, sikuelewa kabisa ni kwanini alikuwa akielekea huko!”

“Unaweza kutupeleka?”

“Kazi yangu?”

“Tutakulipa, mimi nitapanda gari lako halafu dereva wangu atatufuata nyuma!”

“Poa!” Aliitikia Awadhi, balozi Lutta akashuka na kutembea hadi mahali ilipoegeshwa gari lake, akapanda na safari kuelekea Ilala ikaanza, hapakuwa na foleni ndefu sana bararabarani katika muda huo wa siku, hivyo ndani ya dakika ishirini nyingine magari yote mawili yalikuwa yameegeshwa mbele ya jengo la TRA, wote wakashuka na Awadhi akaanza kuwaongoza kuelekea mahali ambako Halima alionekana akielekea.

“Alishuka akifuata reli hii hii!” Awadhi alisema maneno hayo wakizidi kusonga mbele hatua kama thelathini mbele, wakashangaa kuona kundi mzunguko wa watu, wengi wakiwa wameshika mikono yao vichwani.

*****

Hali ya Gerald inaendelea kuwa mbaya sana, jopo la madaktari sita wakiongozwa na Profesa Kayuga wanakutana na kupeana mawazo juu ya nini cha kufanya ili kuweza kuokoa maisha ya Gerald.

“Hali ya mgonjwa ni mbaya sana kwa kweli lakini lazima tuhakikishe hali yake inarejea kama kawaida, halafu isitoshe huyu ni mtoto tegemezi wa balozi wetu, lazima tuokoe maisha yake!” Alisema Profesa Kayuga.

“Ni kweli kabisa Profesa, tutajitahidi kufanya hivyo!”

“Muuguzi naomba umpime presha yake tafadhali!” Baada ya Profesa Kayuga kusema hayo, haraka Muuguzi akachukua mashine ya kupima presha kisha akampima.

“Mh!” Muuguzi aliguna.

“Vipi tena?” Dk. Kazimoto aliuliza.

“Presha yake ni mbaya sana, imezidi kushuka!”

“Profesa Kayuga, hapa akili ya ziada inahitajika!”

“Mimi nilikuwa na wazo!” Alikuwa ni Dk. Susuma, akishauri.

“Wazo gani hilo Dk?”

“Hali ya Gerald inazidi kuwa mbaya na hakika kama hatuchukua hatua za makusudi tunaweza tukampoteza, sasa nilikuwa naona bora tutoe matangazo katika vyombo mbalimbali vya habari kuomba mtu yeyote ambaye anaweza kujitolea kumsaidia figo!”

Lilikuwa ni wazo zuri sana, wote wakakubaliana na kuanza kuchukua hatua hiyo mara moja. Waligawana majukumu, wengine walituma matangazo katika magazeti na wengine walipeleka matangazo kwenye vituo vya Redio na Televisheni.

Jioni ya siku hiyo, vituo vya Redio na Televisheni, walianza kurusha matangazo hayo huku wakiahidi kutoa zawadi nono kwa atayejitolea kuokoa maisha ya Gerald. Magazeti karibu yote ya siku iliyofuta yalitoa tangazo wakiomba msamaria yeyote kujitolea figo.

Ikiwa ni siku ya pili tangu kuanza kutoa matangazo katika vyombo vya habari, hakuna hata mmoja aliyekuwa tayari kutoa figo yake kwa ajili ya Gerald. Maisha ya Gerald yalitegemea figo, kama angetokea mtu yeyote na kukubali kutoa figo yake kwa ajili ya Gerald, hali yake ingekuwa nzuri na angerejewa katika hali nzuri.

“Tutafanya nini Profesa, hali ya Gerald inazidi kuwa mbaya na mpaka sasa hakuna mafanikio yeyote wala dalili za mtu kukubali kutoa figo!” Aliuliza Dk. Susuma.

Wakiwa wanajadiliana juu ya hali ya Gerald, mara ghafla mlango wa ofisi ukafunguliwa, akaingia Muuguzi akiwa anahema kwa kasi, inaonekana alikuwa na taarifa mbaya sana alizowaletea madaktari.

“Vipi, kuna nini tena?” Profesa Kayuga aliuliza.

“Gerald!”

“Gerald amekuwaje, amekufa?” Daktari mwingine aliuliza.

“Hapana, anatupa mikono na miguu, anaonekana kama anataka kukata roho!”

Hawakumpa nafasi ya kuendelea kuzungumza zaidi, haraka madaktari wote wakakimbia mpaka wodini. Hali waliyoikuta iliwatisha sana, Gerald alikuwa akitupa mikono huku na huko ghafla akatulia kabisa na kunyooka. Madaktari wote wakashika mikono kichwani.



******

Grace rafiki yake Halima anachanganyikiwa, kila anapokumbuka ujumbe alioachwa na rafiki yake alipata picha mbaya juu ya maisha ya Halima. Akaupa ubongo wake kazi ya kuchambua vizuri mambo, ndipo akapata wazo moja kichwani.

“Ni lazima niwasiliane na shangazi yake Halima haraka iwezekanavyo!” Aliwaza lilikuwa wazo la busara sana, hakuchelewa, akachukua simu yake na kumpiga.

“Natuami wewe ni shangazi yake na Halima, mimi ni rafiki yake naitwa Gracen kuna matatizo kidogo yametokea hivi ninavyongea na wewe Halima ana siku ya pili sijamwona hapa Chuoni na mazingira aliyoondokea yananichanganya sana.

“Unasemaje?” Shangazi yake Halima akauliza.

“Halima ameondoka chuoni siku ya pili sasa!”

“Siku ya pili? Amekwenda wapi?” Shangazi akauliza tena.

Ilikuwa ni kazi ya Grace kumweleza kila kitu juu ya matatizo ya Halima na ni kwanini alichukua uamuzi wa ajabu kiasi hicho. Alimweleza ujumbe aliomwandikia kabla ya kuondoka.

Shangazi yake Halima akaamua kupiga simu Kilosa kwa baba yake Halima, mzee Mohamed na kumweleza kila kitu kilichotokea na juu ya Halima.

“Kesho asubuhi nitakuja huko kwa ajili ya kazi moja tu kumsaka mwanangu ni lazima apatikane!” Alisema baba yake Halima kwa sauti ya majonzi. Siku ya pili yake aliwasili jijini Dar es Salaam na mipango ya kumsaka Halima ikaanza mara moja bila kuchelewa.



Kitu cha kwanza walichoshauriana ni kutoa taarifa polisi kwanza kabla ya kuanza uchunguzi, moyoni kwa mzee Mohamed kulijaa mawazo juu ya mtoto wake Halima, alimpenda kupindukia na alikuwa tayari kufanya kitu chochote ili kumlinda.



“Mungu wangu nimempoteza mwanangu, Halima wewe ni tegemeo langu, umekwenda wapi mama? Ni kitu gani umekosa kutoka kwangu?” Baba yake Halima alisema kwa uchungu.

“Usiseme hivyo bado tuna nafasi ya kumtafuta mtoto, usikate tamaa kaka naamini tutampata!” Shangazi yake Halima alisema.

“Tumeshangahangaika sana, lakini haonekani tutampaje, bora ningeona maiti yake ningejua moja kuwa mwanangu amefariki lakini sio hivi!”

“Usijali kaka, halafu kuna jambo moja nimekumbuka, naamini huenda tukapata mwanga kidogo tukizingatia hilo!”

“Jambo gani hilo?”

“Nafikiri twende Chuoni tukazungumze na rafiki yake ambaye alinipigia simu, naamini atakuwa na jambo la kutuambia ambalo litatusaidia katika uchunguzi wetu!”

“Hata mimi naunga mkono jamno hilo!” Mama Ashrafu ambaye ni jirani yao aliyewasindikiza, alisema. Hawakuchukua muda mrefu kufikiria jambo hilo, haraka safari ya kwenda Chuoni ikaanza.

******

Haikuwa shida sana kumpata rafiki yake Halima, Shangazi yake alimpigia simu na kuzungumza naye wakakubalina kukutana.

“Kwani nyie mko wapi?”

“Tupo hapa Pentagon!”

“Nakuja sasa hivi!”

Dakika tano baadaye tayari Grace alifika kituoni, aliwasalimia wote wakaongoza mpaka kwenye mgahawa kisha wakaketi na kuanza mazungumzo.

"Alisema anaenda wapi?"

"Hakuniaga ila aliniandikia ujumbe kwenye karatasi, ujumbe unaosikitisha sana!"

"Ujumbe gani? Uko wapi huo ujumbe?" Akasema baba yake Halima.

Hakuchelewa haraka akatoa kikaratasi kidogo kilichokuwa na ujumbe alioandika Halima kisha akawapa.

“Mungu wangu! Halima mwanangu umeamua kujiua kwa sababu ya mwanaume?” Alisema kwa mshangao shangazi yake Halima.

Machozi yalitiririka machoni mwa Shangazi yake Halima baada ya kusoma ujumbe huo. Ilikuwa ni kazi ya ziada kwa Grace kueleza kila kitu kilichoendelea kati ya Halima, Dk.Othman na Gerald.

“Binti kwani Halima waliachana na Dk.Othman?” Mzee Mohamed aliuliza kwa mshangao wa ajabu.

“Ndio!”

“Sababu gani ilipelekea wakaachana?”

“Kurejea kwa Gerald!”

“Gerald?”

“Ndio!”

“Ina maana Gerald yuko hai?” Akauliza tena.

“Kabisa!” Grace akajibu kwa kujiamini.

“Yuko wapi kwa sasa?’

“Hivi ninavyoongea Gerald yuko hospitali ya Taifa ya Muhimbili, amelazwa na hali yake ni mbaya!”

Maelezo aliyoyatoa yaliyotosha kuanza safari mpya ya kuanza uchunguzi wao, ilikuwa lazima waende Muhimbili kwenye wodi aliyolazwa Gerald wakiamini wangepata mwanga katika upelelezi wao.

"Lakini kwani alivyoondoka hapa mara ya mwisho aliondoka na nani na usafiri gani?"

"Alikwenda na teksi ya kaka Awadhi!"

Kabla ya kwenda Muhimbili ilikuwa lazima wamtafute Awadhi dereva aliyeondoka na Halima mara ya mwisho. Walimtafuta kwa muda mrefu bila mafanikio lakini wakiwa katika harakati za kuondoka kwenda hospitali, Grace akaona gari lililofanana kabisa na la Awadhi likija, lakini baada ya kufika na kuegesha akagundua kuwa hakuwa yeye. Wakaamua kuondoka kwenda hospitalini.

******

Foleni barabarani ndiyo iliyowaangusha, safari yao ambayo ingeweza kutumia dakika kumi ilikuwa ndefu kutokana na foleni hiyo. Walitumia barabara ya Sam Nunjoma, walipofika Bamaga kwenye makutano ya barabara ya Shekilango na Ali Hassan Mwinyi, walinyoosha kuendelea kuifuata barababara ya Ali Hassani, walipofika kwenye daraja la Salenda, walikata kushoto na kufuata barabara ya kuelekea hospitali ya Muhimbili.

Dakika thelathini baadaye walishafika hospitalini, waliegesha gari sehemu nzuri kisha haraka wakashuka.

“Ni lazima tumpate Balozi Lutta huyu anaweza akawa na maelezo mazuri juu ya wapi mwanangu Halima alipo” Alisema mzee Mohamed kwa hasira.

Wakaenda moja kwa moja mpaka mapokezi, wakauliza wodi aliyolazwa Gerald, haikuwa kazi ngumu kupata maelekezo ya wapi alikolazwa Gerald.

Wote kwa pamoja wakiongozwa na mzee Mohamed, walikwenda moja kwa moja mpaka wodini na kuingia.

Wakiwa mlangoni walipishana na machela iliyofunikwa shuka ikisukumwa na wauguzi hawakuhangaika nayo shida yao kubwa ilikuwa ni kujua wapi alipokuwa Gerald kwa wakati huo.

Haraka wakaingia katika wodi aliyolazwa Gerald, hali waliyoikuta iliwafanya wote washikwe na mshangao! Gerald hakuwepo kitandani.

****

Umri wa Balozi Lutta ulikuwa si chini ya miaka hamsini na tano lakini siku hiyo alikimbia kama kijana mwenye umri wa miaka ishirini na tano akiwa nyuma ya dereva teksi Awadhi, hakuna mtu aliyemhitaji siku hiyo kama Halima! Alikuwa mtu muhimu sana katika kuokoa maisha ya mtoto wake, alimwona mkewe aliyemfukuza kabla hajatoa figo kama muuaji aliyekuwa amedhamiria kuondoa uhai wa Gerald kwa sababu zake binafsi, asingeweza kumfukuza Halima akidai yeye angeweza kutoa figo halafu baadaye akakataa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Hatua kama ishirini hivi tayari walikuwa wamefika kwenye kundi la watu waliotengeneza duara wakiwa wamezunguka reli, wengine wakiwa wameweka mikono yao kichwani huku baadhi ya akinamama wakilia. Walishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea eneo hilo, wakasogea karibu na kumwita mmoja wa akina mama aliyekuwa akilia.

“Mama vipi? Kimetokea nini hapa?” Awadhi aliuliza.

“Kuna binti mmoja alikuwa amelala kwenye reli…!” Hakuweza kumalizia sentensi yake akaangua kilio.

“Akawaje?’“Masikini binti wa watu mzuri kama nini! Sijui wamemfanyia kitu gani mpaka achukue uamuzi mbaya kiasi hiki!”

Majibu yake ya mzunguko badala ya kuwa suluhisho yalizidi kuwakera, wakajikuta wao wenyewe wakifikia uamuzi wa kupenya katikati ya watu kwenda kujiona kilichokuwa kimetokea hasa baada ya kuambiwa kuwa kuna msichana alikuwa amepatwa na matatizo. Macho yao hayakuamini walipokuta msichana amelala chini katikati ya watu hao, pembeni mwa reli, kwa kumwangalia tu mara moja Awadhi alimtambua.

“Ni yeye!” Akamwambia Balozi Lutta.

“Kweli?”

“Ndio!”

“Mzima?”

“Sijui, namwona ametulia tu!”

Wote wakatembea haraka haraka kwenda mahali ambako Halima alikuwa amelala kifudifudi ardhini, Awadhi na balozi Lutta wakamshika na kumzungusha, walitaka kuhakikisha kama alikuwa hai au amekufa.

***

Profesa Kayuga na madaktari wengine walishindwa nini cha kufanya, Gerald alikuwa alinyooka kitandani kama mtu aliyepoteza kabisa uhai, roho zikawauma, juhudi zao zote zilionekana kutozaa matunda hata kidogo. Profesa Kayuga akachomoa mfukoni kipimo cha mapigo ya moyo kiitwacho Stethoscope na kukichomeka masikiono kisha kuanza kuusikiliza moyo wa Gerald kwa umakini.

“Anahitaji kushtuliwa sana moyo wake, tumuhamishe chumba cha upasuaji haraka, moyo wake unaanza kupungua nguvu, kule kuna mashine nzuri zaidi ya kushtulia moyo, masista hebu naomba mkimbizeni haraka chumba cha upasuaji, mtatukuta sisi tumekwishafika!” Profesa Kayuga aliongea na kuanza kuondoka wodini akiongozana na madaktari wenzake.

Wauguzi hawakuwa na jambo jingine la kufanya zaidi ya kumwandaa Gerald kisha kuleta machela na kumpakia juu yake, hata wao alishakuwa sehemu ya maisha yao, wote walimpenda na walitaka apone na kurejea katika hali yake ya kawaida, walipokamilisha wakaanza kumsukuma kwenda chumba cha upasuaji, nje wakapisha na mzee wa Kiarabu pamoja na wanawake kadhaa alioongozana nao, wakiingia katika chumba walichotoka, hawakuwajali sana, walichotaka ni kumuwahisha Gerald chumba cha upasuaji kama alivyoagiza profesa Kayuga.

“Aliyeondoka nafikiri ni Gerald!” Grace aliongea.

“Wewe umejuaje?”

“Ndio maana nimewaleta kwenye chumba hiki, nilikuja hapa jana kumtafuta Dk.Othman nikitaka kufahamu wapi alikokuwa Halima, wauguzi wakaniambia kila kitu kilichotokea, kwamba Dk. Othman yupo mahabusu kwa sababu alitaka kumuua Gerald, nikauliza mahali Gerald alikolazwa nikaonyeshwa chumba hiki, nina uhakika kabisa aliyepitishwa kwenye machela ni yeye, twendeni!” Alisema Grace akionyesha msisitizo, hawakutaka kumbishia, wakaanza kumfuata.

Walitembea kwa haraka wakiifuata machela, hawakuweza kuiwahi kabla haijaingizwa chumba cha upasuaji, lakini baadaye wauguzi wawili wakisukuma machela walijitokeza na mzee Mohamed akamfuata mmoja wapo na kumuuliza kama aliyeingizwa chumba cha upasuaji ni Gerald.

“Ni kweli, ni ndugu yenu?” Muuguzi aliwajibu na kuwauliza.

“Hapana, lakini tunamtafuta msichana mmoja aliyekuwa naye!”

“Nani? Halima?”

“Ndio!”

“Mh!”

“Mbona unaguna binti?” Mzee Mohamed aliuliza kwa mshangao..

“Basi tu, alikuwa hapa lakini akapotea katika mazingira ya kutatanisha, hivi sasa Balozi Lutta amekwenda kumtafuta sijui kama amempata!”

“Amekwenda kumtafutia wapi?”

“Nasikia Chuo Kikuu anakosoma!”

“Tumetoka huko sasa hivi hatujamwona Halima, huyu msichana ndiye wanasoma naye na kuishi chumba kimoja!”

“Basi hii ni Kasheshe!” Aliongea muuguzi na kuanza kusukuma machela pamoja na mwenzake kuelekea wodini akimwacha mzee Mohamed katika mawazo mengi, shangazi na mama yake Halima tayari walikuwa wameshaanza kulia machozi wakiamini mtoto wao alikuwa amejiua na kuiacha dunia.



****

“Halima! Halima! Halima!” Balozi Lutta aliita akimtingisha.

“Bee!” Halima aliitika na kufumbua macho yake.

“What are you doing here?” (Unafanya nini hapa?)

“I came here to die!” (Nilikuja hapa kufa!)

“Why?” (Kwanini?)

“Life is treating me bad!” ( Maisha hayanitendei wema!)

“What do you mean?” (Unamaanisha nini?)

“I cant live without your son, I love Gerald so much!” (Siwezi kuishi bila mwanao, nampenda sana Gerald!)

“He love you too and he wants you to save his life, he is dying right now!” (Anakupenda pia na anataka uokoe maisha yake, sasa hivi anakufa!)

“But your wife chased me!” (Lakini mkeo alinifukuza!)

“I am so sorry for that, forgive me seven times seventy, that is what the Bible says!” (Nisamehe kwa kosa hilo, nisamehe saba mara sabini, hivyo ndivyo neno la Mungu linasema!)

“I have forgiven already, that why I want to die!” (Nimekwishasamehe tayari, ndio maana nataka kufa!)

“No! Don’t say that, lets go and save Gerald’s life if you really love him!” (hapana! Usiseme hivyo, twende tukaokoe maisha ya Gerald kama kweli unampenda!) Balozi Lutta aliongea akijaribu kumnyanyua Halima kutoka ardhini kwa kusaidiwa na Awadhi, akasimama wima na kumshika mkono kijana mmoja aliyekuwa pembeni..

“Ahsante sana!” akamshukuru.

“Nani huyu?” Awadhi akauliza.

“Ndiye alinivuta kutoka kwenye reli treni lilipotaka kunigonga, nilikuwa nimeamua kufa kabisa, bila yeye hivi sasa ningekuwa vipande vipande na roho yangu ingekuwa imerudi kwa Mola!”Akaongea Halima kwa uchungu huku akibubujikwa na machozi.

Alichokifanya Balozi Lutta ni kuchomoa noti ya shilingi elfu mbili mfukoni mwake na kumkabidhi kijana huyo, kisha wote wakaanza kutembea kwenda mahali walipoyaacha magari yao, Halima akapanda kwenye gari la Balozi Lutta.

“Sasa mzee, mimi nitoe basi, si umempata mtu wako?”

Balozi Lutta hakuwa na ubishi, msaada aliokuwa ameupata ulikuwa ni mkubwa sana, akachomoa noti ya shilingi elfu kumi na kumkabidhi Awadhi, kilichofanyika baada ya hapo ni kasi ya ajabu ambayo kwa umri wake hakupaswa kabisa kuitumia mpaka akafika hospitali ya Muhimbili na kuegesha gari lake nje ya wodi aliyolazwa Gerald, akashuka haraka na kuzunguka upande wa pili ambako alimkuta Halima amekwishashuka wote wakaanza kukimbia kuelekea wodini, hawakukuta kitu! Wakaingia ofisini kwa wauguzi na kuelezwa kwamba Gerald alikuwa chumba cha upasuaji.

“Ahsanteni!” Balozi Lutta akajibu, hakuhitaji maelezo mengine zaidi ya hayo, alichokifanya ni kutimua mbio hadi chumba cha upasuaji akiwa na Halima.

“HALIMA!” Ilikuwa sauti ya mzee Mohamed akinyanyuka kwenye kiti na kumfuata mwanae.

“Bee baba!”

“Ulikuwa wapi?”

“Baba tutaongea baadaye, shikamoo!”

“Nataka kufahamu!”

“Mzee mwenzangu, mimi ni Balozi Lutta!”

“Nakufahamu!”

“Mtoto wangu anaumwa sana, anahitaji figo ili kuokoa maisha yake, binti yako amekubali kutoa figo yake moja!”

“Weeee! Nini? Figo? Nakuambia Balozi hapo ni fullstop, mwachie mwanangu!” Mzee Mohamed alifoka.

*******

Furaha yake yote ya kutoa Figo kuokoa maisha ya Gerald ilianza kuingia dosari, taarifa alizopewa na muuguzi kuwa hali ya Gerald ilikuwa ikiendelea kuwa mbaya zilimsikitisha sana Halima. Alikuwa ndio kwanza amerejewa na fahamu zake na kujikuta yuko wodini na alikuwa na mshono mkubwa tumboni mwake, lakini Halima hakuujali hata maumivu aliyokuwa nayo alijaribu kuyapuuza na kujikuta akitaka kunyanyuka ili aende kitandani kwa Gerald kushuhudia mwenyewe hali yake, hakuweza kufanya hivyo, kwani kabla hajanyanyuka muuguzi alifika kitandani na kumzuia.

“Halima!”

“Bee!”

“Nini tena?”

“Nataka kumuona Gerald, nataka kumuombea, sitaki afe!”

“Sio sasa hivi, huwezi kuinuka kitandani kwa wakati huu, tafadhali endelea kulala chali, usiwe na wasiwasi, hali yake inaendelea kudhibitiwa, muombe tu Mungu hapo hapo kitandani!”

Halima alitulia kitandani akibubujikwa na machozi, hakutaka kabisa kukubaliana na mambo aliyokuwa ameambiwa. Alikuwa amepoteza uhusiano na wazazi na hata uhai wake kuokoa maisha ya Gerald, kwani pia kulikuwa na uwezekano wa kufia chumba cha upasuaji wakati akitoa figo, kwa fikra hizo alijikuta hayuko tayari kumpoteza Gerald, hata hivyo aliendelea kutulia kitandani akishuhudia madaktari na wauguzi wakiendelea na mahangaiko yao.

Nusu saa baadae, alishuhudia wauguzi na madaktari wakitulia na wote wakashusha pumzi, tabasamu zikajaa usoni mwao huku baadhi yao wakijifuta na vitambaa vya jasho, mwanga wa matumaini ukaonekana kurejea. Nusu yao wakageuka kumwangalia Halima kitandani na Profesa Kayuga akatembea kuelekea kwenye kitanda chake.

“ Binti hongera sana!”

“Kwanini daktari?”

“Mapigo ya moyo ya mchumba wako yamerejea katika hali ya kawaida, umeokoa maisha yake, huu ndio upendo wa kweli, ulikuwa na kila sababu ya kukataa kuchumbiwa na Dk. Othman, nakubali unampenda Gerald, naomba tu Mungu hata yeye pia awe anakupenda hivyo hivyo!”

“Tunapendana sana daktari, ni dunia tu ilitutenganisha, tulishapanga kuoana tangu tukiwa shule ya msingi, bahati mbaya mwenzangu akapotea ndipo mimi nikaanza kujihusisha na Dk. Othman, laiti angekuwepo Gerald nisingediriki kujihusisha na Dk.Othman kabisa!”

“Haya ugua pole, tutakuja kukuona tena baadae, usijaribu kunyanyuka kitandani mpaka utakaporuhusiwa kufanya hivyo!”

“Nawashukuru sana madaktari kwa wema wenu, mmejitahidi sana kuokoa maisha ya Gerald”

“Wewe ndio inapasa ushukuriwe, ni watu wachache sana duniani wanaoweza kutoa figo zao kuwapa watu wengine, si unaona mama wa kambo wa Gerald alikataa! Tena kumpa mwanaume? Wakati sisi tunajulikana ni vigeugeu!”Dk. Kapaya akatia neno.

“Wanaume wote mnaweza kuwa vigeugeu lakini si Gerald, namwamini mno ndio maana nikakubali kuachana na Dk.Othman, kutoa figo yangu kumpa yeye!” Halima aliongea uso wake ukionyesha kuwa na tabasamu pamoja na maumivu yote aliyokuwa nayo.

“Basi ugua pole binti!”

Madaktari wakaondoka na kuwaacha wauguzi wakimfunika Gerald na mashuka kisha kurekebisha vizuri mashine yake ya Oksijeni nao wakamuaga Halima na kuondoka zao. Dakika kama tano tu hivi mlango ukafunguliwa, macho ya Halima yakaelekea mlangoni kuona ni nani alikuwa akiingia, Balozi Lutta akasimama mbele ya mlango uso wake ukiwa umejawa na tabasamu lililogongana na la Halima, nyuma yake alikuwepo mke wake, sura ikiwa imekunjwa na mashavu yamevimba kuonyesha bado alikuwa na chuki.

Badala ya kwenda kwenye kitandani cha Gerald, balozi Lutta alinyoosha moja kwa moja hadi kwenye kitanda cha Halima, akainama na kumpiga busu usoni kisha kumtaka hali yake.

“Ahsante sana binti, profesa Kayuga amenieleza kila kitu kuhusu hali ya kijana wangu, hakika bila wewe Gerald angekufa!”

“Usijali baba, ni wajibu wangu, nampenda mno Gerald!”

“Nalijua jambo hilo, nasikitika hatukulifahamu mapema!”

Wakati yote hayo yakiendelea, mama wa kambo wa Gerald alikuwa kimya kabisa tena akimwangalia Halima kwa jicho la chuki, alishindwa kuelewa ni kwanini hali hiyo ilijitokeza wakati jambo alilolifanya kwa mtoto wao lilikuwa jema mno. Mwisho aliamua kumpuuza mwanamke huyo, maongezi yakawa kati yake na balozi Lutta ambaye tayari alikuwa pembeni mwa kitanda cha Gerald akimwangalia na kumgusagusa, akiwa katika hali ya kutoamini kilichokuwa kimetokea alirejea tena kitandani kwa Halima kuendelea kutoa shukrani.

Walibaki pamoja mpaka saa tatu usiku ndipo balozi Lutta na mke wake wakaondoka, mpaka wakati huo hapakuwa na neno lililokuwa limetoka mdomoni mwa mama wa kambo wa Gerald.

Hali iliendelea kuwa nzuri kwa Halima kiasi kwamba siku mbili tu baadae akaruhusiwa kuwa ananyanyuka kitandani kufanya mazoezi ambayo hata hivyo hayakwenda mbali zaidi ya kilipokuwa kitanda cha Gerald ambaye mpaka wakati huo alikuwa hajarejewa na fahamu zake, alilala kitandani akiwa hajitambui, madaktari walidai sumu iliyokuwa ndani ya damu yake ilikuwa imeharibu sehemu ya ubongo, hii ilifanya baadhi ya madaktari washindwe kutoa jibu la uhakika kama Gerald angeweza kuongea tena maishani mwake au la.

Kila siku Balozi Lutta alishinda nao hospitalini mpaka jioni ndipo akaondoka kurejea nyumbani, huo ndio ulikuwa utaratibu wake wa kila siku akitarajia mwanae angezinduka kutoka usingizini lakini haikuwa hivyo, siku ya tano katikati ya usiku, Halima alizinduka usingizini baada ya kusikia mtu akijitingisha kwenye kitanda cha Gerald, alipoangalia vizuri alimuona Garald akijigeuza.

“Mmh!” Akaguna kwani halikuwa jambo la kawaida kutokea, mara zote ni wauguzi walioifanya kazi hiyo.

Alishuka kitandani haraka na kuanza kutembea kwenda kwenye kitanda cha Gerald, alipofika alishangaa kumkuta amefumbua macho akiangalia huku na kule katika hali ya mshangao, alionekana kutotambua ni wapi alipokuwa na alipomwangalia Halima usoni ghafla akatabasamu.

“Halima hujaenda darasani?” Gerald akauliza.

“Gerald!”

“Naam!”

“Unafahamu hapa tuko wapi?”

“Chuo Kikuu!” Akajibu Gerald na kumfanya Halima azidi kushangaa, kwani hawakuwahi kusoma darasa moja Chuo Kikuu bali walikutana kwenye ngazi yeye akishuka kwenda kwenye gari ili aende ukumbini kuvishwa pete ya uchumba.

“Hapana!” Halima akakataa, uso wake ulikuwa ukilengwalengwa na machozi, si ya huzuni bali ni furaha, hakuamini kabisa kwamba hatimaye alikuwa akiongea na Gerald.

“Tuko wapi?”

“Hospitali ya Muhimbili!”

“Muhimbili? Tunafanya nini?”

“Ni habari ndefu sana mpenzi wangu, nafurahi tu kuona utapona, tutaongea mambo mengine baadae, wacha kwanza nikawaite wauguzi!” Halima aliongea na kutoka akikimbia, wala hakujali kwamba tumboni alikuwa na nyuzi zilizotakiwa kutolewa siku iliyofuata, aliporejea dakika mbili tu baadae aliongozana na wauguzi wawili.

“Kweli, mpigie simu Profesa!”

“Sawa!”

Muunguzi mmoja akakimbia tena hadi ofisini ambako katika hali ya kutokuamini alimpigia simu Profesa Kayuga na kumweleza kila kitu juu ya yaliyotokea wodini, dakika kumi tu baadae daktari alifika wodini naye akapigwa na butwaa alipowakuta Gerald na Halima wakiongea tena kwa furaha kubwa.

“This is a miracle!” (Huu ni muujiza) Profesa Kayuga aliongea.





Halima anakubali kutoa figo yake ili kuokoa maisha ya mwanaume aliyempenda, Gerald aliyekuwa akiugua ugonjwa wa figo kuharibika na alikuwa katika hatari ya kufa. Kitendo hiki kinatafsiriwa na wazazi wake kama usaliti hivyo kujikuta akitengwa na familia yake, hakujali sana kwa sababu alifanikiwa kuokoa maisha ya Gerald ambaye angeishi naye siku zote za maisha yake.



Vijana hao wawili ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, baada ya kupona waliruhusiwa kutoka hospitali na kurejea nyumbani kwa balozi Lutta, baba yake na Gerald ambako walishindwa kupumzika kwa sababu ya visa wa mama wa kambo na kuamua kurejea chuoni ambako rafiki mkubwa wa Halima, Grace aliwapokea.



Baada ya hapo maisha yaliendelea kama kawaida, kitabu kipapamba moto, Halima na Grace wakiwa mwaka wa pili na Gerald mwaka wa kwanza. Kila walipokwenda walikuwa watatu, urafiki wao ulizidi kukomaa na kuwa kama ndugu, jambo hili lilimfurahisha sana Halima bila kufahamu kilichokuwa kikiendelea moyoni mwa rafiki yake.



Hakutilia mashaka hata alipowaona wako karibu, wakati mwingine Grace na Gerald walitoka usiku hata kwenda kwenye kumbi za starehe, aliamini walikuwa ni mtu na shemeji yake! Lakini kama jinsi maisha ya chuo yalivyo, maneno husafiri kama upepo, ghafla akaanza kusikia kuwa Grace na Gerald walikuwa na uhusiano wa siri, hakuamini, alichukulia mambo yote aliyoyasikia kama majungu yenye lengo la kuvuruga uhusiano wao mzuri.



Baadaye akamuona rafiki yake akiwa na dalili za ujauzito na watu wakaanza kudai mimba hiyo ilikuwa ya Gerald! Safari hii Halima hakutaka kuyapuuza maneno hayo, akaenda hatua moja mbele na kuamua kufanya uchunguzi. Siku moja kabla ya hawajaondoka chuoni kwenda likizo ambayo yeye na Gerald walikuwa wamepanga kusafiri kwenda Italia kwa Balozi Lutta, Gerald na Grace walitoka kwenda disko, Halima akaamua kuwafuatilia akiwa amevaa nguo za kuficha sura yake.



Ndani ya ukumbi wa Billicanas kulikokuwa na giza sababu ya taa, aliwatafuta na kufanikiwa kuwapata kwenye moja ya kona za ukumbi huo, akaketi kando yao na kuanza kushuhudia mambo ambayo hakuwahi kutegemea yangetendwa na mtu kama Gerald; walikuwa wakipigana mabusu na kunyonyana ndimi, Halima alisikia mwili wote ukifa ganzi, baadaye macho yakaingiwa na giza, hakuelewa kilichofuata. Je, nini kiliendelea? Fuatilia…



Baadhi ya watu kwenye kona ambayo Gerald na Grace walijificha ndani ya ukumbi huo wakifanya mambo yao ya siri, walijilaza juu ya makochi, hii ilifanya isiwe rahisi kwa mtu yeyote kuhisi kwamba msichana aliyekuwa amelala kwenye kochi pembeni tu mwa Gerald na Grace akiwa na kofia kubwa kichwani alikuwa ni Halima tena akiwa amepoteza fahamu, alizimia baada ya kusikia maneno yaliyokuwa yakisemwa na vitendo vilivyokuwa vikifanywa na watu ambao siku zote aliwaamini.



“Achana naye, anafikiri figo ndio kila kitu! Watu tunataka burudani yeye analala tu!” Yalikuwa ni maneno ya kikatili kutoka mdomoni mwa Gerald, isingekuwa rahisi hata kidogo awe amesahau kwamba huyo anayemwona hafai ndiye aliyeokoa maisha yake, Halima hakuweza kuyavumilia maneno hayo, fahamu zikampotea.



Alizinduka kama dakika ishirini hivi baadaye na kuketi kitako, akatupa macho kushoto kwake na kuwaona Gerald na Grace wakiendelea na mambo yao, roho ikazidi kumuuma! Hakuwa na uwezo wa kuyazuia machozi, hata kama angebembelezwa na nani, alichokuwa akikishuhudia kwa macho yake kilikuwa ni zaidi ya mtu kufiwa na mtu aliyempenda, maumivu hayo hayakuwa na mzani wa kuyapima.



Maneno mengi ya kejeli yalizidi kusemwa, Grace akizidi kumbeza Halima kuanzia namna alivyovaa akidai alikuwa mchafu, asiyejua kuchagua nguo na alikuwa akimuabisha Gerald mbele za watu! Mvulana kama yeye hakufaa kabisa kuwa na mwanamke wa aina hiyo, ambaye mchana kutwa alivaa mabaibui kuficha maungo yake.



“Mwanamke vimini bwana, kila siku kujifunika mabaibui, usafiri anao, hipsi anazo lakini kila siku kazifunika, hakyanani mimi ningekuwa na mguu kama ule? Mh! Sijui, Chuo kikuu wangenitambua!” aliongea Grace akimkumbatia Gerald, ni kweli kabisa, Halima alikuwa mtu wa kuficha maungo yake, aliishi kama alivyolelewa akiwa mtoto wa Kiislamu pamoja na kwamba alishakosana na wazazi wake.



“Achana naye bwana, nakwenda naye Italia safari hii tu, nikirudi nammwaga, nataka kutunza mtoto wangu! Mabaibu yake yataniabisha sana lakini sina jinsi” Gerald aliongea akicheka bila kuelewa ni kiasi gani alikuwa akimuumiza Halima.

Machozi yalizidi kumbubujika Halima, moyo wake ulikuwa ukimuuma mno, ilikuwa ni bora kuchomwa na mkuki wa moto moyoni kuliko maumivu aliyokuwa akiyapata! Alishindwa kabisa kukubaliana na alichokuwa akikiona, akahisi macho yake yalikuwa yakimdanganya au alikuwa ndotoni kwani isingewezekana hata kidogo mwanaume aliyempenda kwa moyo wake wote, akakubali hata kutoa uhai wake ili amwokoe na kifo ndiye aliyekuwa akimfanyia ukatili wa aina hiyo.



“Ningejua nisingekuja, Mungu kwanini umeniruhusu nije ukumbini kushuhudia jambo la aina hii?” Halima alijikuta akitamka maneno hayo kwa uchungu kisha kusimama wima akiendelea kububujikwa na machozi yaliyolowanisha kabisa fulana yake.



Upande mmoja wa moyo wake ulimwambia awavamie na kuanza kupigana lakini upande mwingine ukamwambia “kamwe usilipize ubaya kwa ubaya, mwachie Mungu ndiye atahukumu!” Yalikuwa ni maneno ya mama yake aliyoambiwa mara kwa mara akiwa mtoto mdogo, pale alipopigwa na mtoto mwenzake. Kumbukumbu zikamrejesha nyumbani kwa wazazi wake, akamwona mama yake kifikra akimlilia, machozi yakazidi kumbubujika. Alijisikia mkosaji mbele ya Mungu na wazazi wake, pengine alichokuwa akifanyiwa ni adhabu kwa sababu ya kutowatii wazazi wake.

“Lakini halikuwa kosa kuokoa maisha ya Gerald, kwanini niadhibiwe?” Alijiuliza akiwashuhudia Gerald na Grace wakilaliana, Grace chini na Gerald juu, hakuna mtu aliyewaona kwa sababu ya giza.



Kwa hilo aliloliona, Halima hakuweza kuvumilia zaidi, aliusikia moyo wake ukikamuliwa kama ambavyo nguo hufanywa kabla ya kuanikwa! Taratibu akageuka na kuanza kutembea kwenda nje huku akilia. Moyoni mwake hakuona tena sababu ya kuishi, alinusurika kwa kifo cha treni, hakuamini kama angenusurika tena na kifo kilichokuwa mbele yake usiku huo, kwake ilikuwa ni bora kufa kuliko kupambana na aibu iliyokuwa mbele yake, lawama za wazazi wake baada ya kugundua alikuwa ametelekezwa pamoja na kutoa figo yake.



“Lazima nife!” Alitamka maneno hayo akipande kwenye teksi bila kuelewa sauti ilikuwa ikitoka.

“Kwanini unasema hivyo sista?”

“Nipeleke Chuo Kikuu, shilingi ngapi?”

“Elfu moja!”

“Twende kwa kasi”



Safari ikaanza kupitia barabara za Ali Hassan Mwinyi hadi Mwenge ambako walikata kushoto kuingia Sam Nujoma, dereva akiendesha kwa kasi ya kilometa mia moja kwa saa kwa sababu hapakuwa na magari barabarani, dakika tano baadaye walikuwa wakiegesha mbele ya bweni la Halima, akamlipa dereva na kushuka akikimbia hadi chumbani ambako alifanya jambo moja tu, kuchukua kisu jikoni na kuanza kukinoa kwenye kisu kingine mpaka kikawa na makali ya kutosha.



“Sifi peke yangu, naondoka nao, nawasubiri wakija tu, nitawapokea vizuri na kuwachekea kama vile hakijatokea kitu chochote, wataniona mjinga, baadaye lazima sababu ya kulewa, Grace atalala usingizi hapo ndipo nitakapokizamisha kisu mara kadhaa kifuani na tumboni mwake, nitamfunika na mto ili asipige kelele, nikimaliza nitamfuta Gerald chumbani kwake na kujifanya nataka kulala pamoja naye, akisinzia tu namfanyia hivyo hivyo, baada ya hapo nitarudi hapa chumbani na kujining’iniza kwa khanga na huo ndio utakuwa mwisho wangu!”

****

Mpaka saa tisa na nusu ya usiku siku hiyo Halima alikuwa bado yuko macho kitandani mwake akiendelea kuyatafakari mambo yote yaliyojitokeza maishani mwake, uamuzi wake wa kutoa figo kwa mtu aliyempenda, hakuujutia hata kidogo, ulimfurahisha kwa sababu tayari Gerald alikuwa hai! Hakuacha kuufikiria uhusiano mbaya uliokuwepo na wazazi wake kwa wakati huo, watu waliompenda na yeye kuwapenda ambao siku zote hawakupitisha hata siku moja bila kufahamu hali yake, tayari walishabadilika na kuwa maadui sababu ya kushindwa kuheshimu maamuzi yake maishani.



“Ipo siku wataelewa kuwa nawapenda na kuwaheshimu, kilichonikosanisha nao ni maamuzi yangu!” Aliwaza Halima.



Kila mawazo yake yalipompeleka kwenye fikra za wanaume na tabia zao, alikata kona kurudi nyuma, hata kidogo hakutaka kutokomea upande huo ambako alijaribu kupiga picha siku ambayo Gerald angekuja kumuumiza na kuondoka na mwanamke mwingine, mambo ambayo mara nyingi aliyasoma kwenye vitabu vya hadithi, hakuwa na mzani wa kutosha kuyapima maumivu ambayo angeyapata. Alishasikia mara nyingi juu ya maumivu yaliyosababishwa na wanaume maishani mwa wanawake kuliko kinyume chake, hakuwa tayari kwa hilo ndio maana hakutaka kusonga sana akiamini kwa wema aliomtendea Gerald asingeweza kumfanyia jambo la aina hiyo, hakufanana kabisa na tabia hiyo.



“Sio Gerald, hawezi kufanya hivyo, bila mimi angekuwa marehemu…mh! Lakini mbona mimi nilimfanyia Dk.Othman…?” Alijiuliza Halima alipofikiria ajali iliyompata maishani mwake na Dk.Othman kumfanyia upasuaji wa ubongo na kuokoa maisha yake wakati huo Gerald akiwa amepotea lakini hakuyafikiria yote hayo, akaamua kumuacha tena siku ya kuvalishwa pete kwa sababu ya Gerald, alipofika hapo Halima alishindwa kutabiri chochote lakini akabaki kung’ang’ania jambo moja tu kwamba Gerald hawezi kufanya hivyo.



Saa kumi na nusu ndipo alipatwa na usingizi, akili yake haikupumzika hata kidogo, ndoto zilimiminika kama mtu aliyekuwa akiangalia sinema! Katika moja ya ndoto alizoota alimwona Gerald akiwa na msichana mwingine mrembo kupita kiasi ndani ya kanisa wakifunga ndoa mbele ya Padri, alipomwangalia msichana huyo usoni hakumtambua na akaanza kulia mbele za watu waliohudhuria! Ghafla akagutuliwa usingizini na kufumbua macho yake, Gerald alikuwa amesimama kando yake akiwa amevaa tisheti nyeupe kifuani ikiwa na maandishi “Forever I will love you”, jasho jingi lilikuwa likimtoka Halima huku akihema kwa nguvu na alipozungusha macho yake chumbani alimwona Grace akiwa ameketi kitandani kwake, nguo alizovaa zilimtisha, hazikufaa kabisa kuvaliwa mbele ya mpenzi wa rafiki yake, juu alivaa sidiria na chini alivaa chupi ya rangi nyeupe akiwa ameacha mapaja yake makubwa nje.



“Vipi?” Gerald aliuliza.

“Ndoto!”

“Ndoto gani?”

“Nimeota nadumbukia kwenye shimo refu!” Halima alidanganya, hakutaka kueleza wazi kilichotokea ndotoni mwake.

“Pole shosti, mwenzio joto linanisumbua kama nini”

“Ndio uvae hivyo?”

“Sasa? Kwani tatizo nini, Gerald? Kwani tungekuwa ufukweni ingekuaje?”

“Ufukweni ni ufukweni shosti!” Alijibu Halima akitabasamu.

“Halima usiwe na wasiwasi kiasi hicho, niamini mpenzi wangu! Mambo uliyonifanyia ni makubwa mno, bila wewe nisingekuwa hai, hata kama Grace angebaki kama alivyozaliwa wala siwezi kuingia majaribuni…nimefika hapa muda mrefu sana nikakuta umelala, sikutaka kukusumbua, amka basi ujiandae twende kwa Mkuu wa Taaluma, tunahitaji kushughulikia mambo yote ili tuanze kuingia darasani” Gerald aliongea akitabasamu, ilikuwa tofauti kidogo kwa Grace, uso wake ulikunjika ghafla kuonyesha ni kiasi gani kauli ya Gerald ilikuwa imemuumiza.



“Shosti mbona umechenji ghafla?”

“Vidonda vya tumbo!”

“Pole!”

Halima aliingia bafuni, akaoga, kupiga mswaki na kutoka hadi chumbani ambako aliendelea kujipodoa, alipomaliza wote watatu waliondoka pamoja hadi nje ya lango la mabweni ya Mabibo, njiani walikopita kila mtu aliwasimamisha na kuwasalimia kisha kumpa pole Gerald. Tayari suala lao lilishakuwa maarufu Chuoni, watu wengi walimwona Halima kama msichana tofauti aliyekuwa tayari kutoa uhai wake kwa sababu mtu mwingine aliyempenda.

“Samahani dada!”

“Ndio!”

‘Naitwa Issa Mnally au International Photographer, natokea gazeti la Mchapakazi, nimekuja hapa chuoni kufanya mahojiano na wewe juu ya ujasiri ulioufanya kukoa maisha ya umpendaye, nimepishana na ninyi pale lakini sikuwatambua, mtu niliyemuuliza ndiye akanionyesha, sijui unaweza kuongea?”

“Unataka nikueleze nini kaka?”

“Nini kilikusukuma mpaka ukafikia uamuzi wa kutoa figo yako wakati wazazi wako walishakataa?”

“Upendo!”

“Hicho tu?”

“Kabisa!”

“Hebu nieleze suala zima lilikuwaje?”

“Tunataka kuondoka kaka!”

“Kwenda wapi?”

“Mlimani!” Alijibu Halima akimaanisha Chuo Kikuu sehemu ya Mlimani yalikokuwa madarasa ya wanafunzi.

“Nitawapa lifti kwenye gari yangu!”

“Eti Gerald, niongee?”

“Endelea!”



Halima akamsimulia mwandishi huyo kila kitu kilichotokea maishani mwao, namna alivyowapenda wazazi wake na alivyokuwa akiwaheshimu. Baada ya maongezi hayo, mwandishi aliwabeba hadi Chuo Kikuu Mlimani ambako aliwashusha wakaenda moja kwa moja hadi kwa Mkuu wa Taaluma, hapakuwa na tatizo lolote, Chuo kilikubali kuwapokea lakini wakatakiwa kuongeza juhudi katika masomo yao vinginevyo mitihani ingewashikilia au kulazimika kufukuzwa Chuo. Siku iliyofuata gazeti la Mchapakazi lilitoka na chini ya kichwa cha habari Nawapenda na kuwaheshimu wazazi wangu-Asema msichana aliyetoa figo, ikiambatana na picha yao wakiwa wamekumbatiana, umaarufu wao ukazidi kuongezeka, wanafunzi wote Chuo Kikuu walitaka kumwona Halima.



Siku iliyofuata walianza masomo kama kawaida, Gerald akiwa mwaka wa kwanza na Halima akiendelea na mwaka wake wa pili, yeye na Grace wakiwa darasa moja! Utatu wao uliimarika zaidi, walikwenda kula chakula bwaloni pamoja na waliondoka kurejea mabwenini pamoja. Hayo ndiyo yakawa maisha yao, afya ya Gerald na Halima ziliendelea vizuri, wala haikuwa rahisi kufahamu kwamba watu hao walikuwa na figo moja miilini mwao. Mwishoni mwa wiki ilikuwa ni lazima watoke kwenda mahali kupumzika, mara nyingi walikwenda kwenye ukumbi wa disko wa Bilicanas ambako wanafunzi wengi walipendelea kwenda.



Maisha yalikuwa ya raha hasa baada ya Halima na Gerald kuchukua kasi ya masomo vizuri, wakaanza kwenda na wenzao. Jambo moja tu lilimsumbua Halima kichwani mwake, wazazi! Hata mara moja hakuwahi kupata simu wala barua kutoka kwa baba na mama yake, si wao tu bali hata shangazi na wajomba zake, alielewa kilichokuwa kimetokea bila hata kuelezwa; alikuwa ametengwa na ukoo. Roho ilimuuma lakini hakuwa na jinsi, upendo aliokuwa nao kwa Gerald ulikuwa mkubwa mno wala hakujutia uamuzi aliochukua wa kutoa figo yake moja, uliowakera wazazi wake kupita kiasi.



Mwezi mmoja baadaye, Balozi Lutta na mkewe waliondoka kurejea Italia, wakiwa wamemwachia Gerald gari aina ya Peugeot 405 ili liwe likimsaidia kusafiri kutoka bwenini kwenda darasani, akawa miongoni mwa wanafunzi wachache wenye magari chuoni hapo na kujiongezea umaarufu, uliozidishwa na uzuri wa sura yake pia msichana aliyekuwa karibu naye.



Wazazi wa Grace walikuwa ni wafanyabiashara wenye uwezo mkoani Arusha, hakuishiwa fedha hata mara moja, wakati mwingine Gerald alipokosa fedha ni Grace aliyemuazima au kumsaidia. Halima hakuwa na kitu chochote cha kuchangia, mpenzi wake alifanya kila kitu akifahamu hakuwa na uhusiano na ndugu yeyote. Ushirikiano huu uliongeza mshikamano kati yao, kitu pekee alichoweza kufanya Halima katika uhusiano huo kilikuwa ni kumsaidia Grace katika mitihani darasani, hakuwa na akili hata kidogo, ili afaulu ilikuwa ni lazima Halima ambebe mgongoni mwake na kumfanyia mitihani yake, kifupi asingeweza kuwa chuoni bila yeye, katika kipindi chote ambacho hakuwepo chuoni wastani wake wa maksi ulishuka kupita kiasi.



Kwa jinsi walivyokuwa wakiishi vizuri, pamoja na tabia mbaya ya Grace kumvalia Gerald nguo zisizostahili haikutokea hata mara moja Halima akaingiwa na wasiwasi, alimwamini mpenzi wake kupita kitu kingine chochote mpaka kufikia hatua wakati mwingine ya kuwaacha wao wawili watoke peke yao usiku na kurudi saa kumi na nusu Alfajiri Grace akiwa amelewa kupita kiasi, haikumshtua wala kumtia hofu, alimwamini sana Gerald, jambo kama hilo lilitokea mara nyingi sana katika maisha yao ya Chuo.



Baadhi ya watu hasa wasichana walimfuata Halima na kumtahadharisha juu ya tabia ya rafiki yake anapokuwa ametoka na Gerald, aligombana nao na kuwaita wachonganishi waliotaka kuvuruga uhusiano wa watu watatu walioelewana na tangu siku hiyo hakuongea na watu wote waliomletea habari hizo, alimsimulia Gerald kila kitu.

“Waongo hao, wambea wakubwa!”

“Kwanini wanaingilia maisha ya watu?” Grace aliuliza.

“Hata mimi nawashangaa, badala wasome wanabaki kuchunguza nani amefanya nini, kinawahusu nini?”

“Bwana achaneni nao, twendeni zetu Njenje!”

“Jamani mimi siendi, najikisia nimechoka sana…Grace nenda na Gerald!”

“Hata mimi nimechoka sana, kesho nina mtihani!”

“Jamaaaaani, Grace twende basi, yaani akikataa Halima na wewe hutaki?”

“Ok! Poa!”

Waliondoka na kurejea kesho yake asubuhi, siku hiyo hata Gerald akinukia pombe! Jambo lililofanya taa nyekundu ziwake kichwani mwa Halima lakini hakutaka kuuliza zaidi ya kumuasa mpenzi wake asijiingize katika ulevi.

“Gerald! Usinywe pombe tena, kumbuka una figo moja tu, unaizidishia kazi ya kuchuja mkojo…sitaki kukupoteza, nakupenda mno…Grace, tafadhali usimpe Gerald pombe siku nyingine!”

“Shosti, kwani yeye mtoto mdogo?”

“Usiniulize swali hilo Grace, huyu ni mpenzi wangu!”

“Samahani shosti, sikujua kama utakasirika!”

Mwishoni mwa mwaka wakati Gerald anaingia mwaka wa pili, Halima na Grace wakiingia mwaka wa tatu, Grace alianza kuugua mara kwa mara, asubuhi akawa na tabia ya kutapika kabla ya kwenda darasani na Matiti yake yakavimba. Habari zikaanza kusambaa chuoni kwamba alikuwa mjamzito na mimba ilikuwa ya Gerald, hakuyaamini maneno hayo, kama ilivyokuwa kawaida yake alimsimulia mpenzi wake ambaye alikataa kata kata na kudai yalikuwa ni majungu ya watu waliotaka kuwachonganisha. Safari hii Halima hakutaka kuyapuuza maneno hayo, alichofanya ni kuzama katika uchunguzi. Kabla hawajaondoka chuoni kwenda likizo, Gerald aliwataka wote watoke pamoja kwenda kwenye ukumbi Bilicanas kucheza muziki kwa mara ya mwisho.

“Leo siendi najisikia vibaya!”

“Grace twende!”

“Poa, tena leo ni Alhamisi, Ladies free!” Aliongea Grace akinyanyuka kitandani na kuanza kuvaa, ilikuwa yapata saa nne na nusu ya usiku, wote walikuwa na furaha sababu walikuwa wamefaulu mitihani yao ya mwisho wa mwaka na Gerald pamoja na Halima walikuwa na safari ya kwenda Roma, Italia.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Gerald akamchukua Grace na kuondoka kuelekea ukumbini, watu walikuwa wengi mno tena idadi kubwa wakiwa ni wasichana. Hali hii pamoja na taa zenye kuleta giza zilizowaka ukumbini ziliwafanya Gerald na Grace wasigundue kwamba Halima alikuwa ndani ya ukumbi huo akiwa amevaa kofia kubwa kuficha uso wake. Aliondoka kuwafuata dakika kumi tu baada ya wao kuondoka, akapanda teksi hadi katikati ya jiji, akaingia ukumbini na kuwatafuta mpaka akawapata, sababu ya giza lililokuwepo alifanikiwa kuketi kando yao, Grace alikuwa amekaa miguuni kwa Gerald, mara nyingi akishusha mdomo wake na kuunganisha na wa Gerald.

“Huyu mjinga atalala sana, mpaka nijifungue ndio atakuja kujua ukweli wa jambo hili, wajinga ndio waliwao!” Grace alijitapa.

“Achana naye, anafikiri figo ndio kila kitu! Watu tunataka burudani, yeye analala tu”

Maneno hayo yaligota kwenye masikio ya Halima moja kwa moja, akahisi mwili ukiishiwa nguvu, macho yakaona giza.

****

“This is a miracle!” (Huu ni muujiza!) profesa Kayuga alijikuta akisema maneno hayo bila kutegemea baada ya kumwona Gerald kitandani akiwa amefumbua macho yake akiangalia huku na kule kama mtu aliyekuwa bado akiendelea kujiuliza maswali juu ya wapi alikokuwa.



Ni kweli muujiza ulikuwa umetendeka, hakuna mtu hata mmoja kati yao pamoja na juhudi zote walizozifanya aliyetegemea hatimaye Gerald angeweza kuwa katika hali hiyo. Madaktari na wauguzi wakakumbatiana pamoja na Halima wakifurahia ushindi waliokuwa wameupata, wa kuokoa roho ya mwanadamu. Halima alikuwa akibubujikwa na machozi ya furaha, yote yaliyokuwa yakitoka chumbani yalikuwa ni kama ndoto tu kwake, hakuamini hata kidogo kuwa hatimaye Gerald alikuwa anakwenda kupona ili waitimize ahadi yao, waliyojiwekea tangu wakiwa watoto wadogo; kufunga ndoa.



Ghafla alijikuta akimkumbuka Dk.Othman, hakuelewa ni wapi alikokuwa wakati huo, upande mmoja wa akili yake ukamwambia pamoja na yote yaliyojitokeza mpaka akafikia uamuzi wa kutaka kumuua Gerald, daktari huyo hakuwa mtu mbaya kwani ni yeye aliyeokoa maisha yake alipogongwa na lori nje ya ofisi ya Wizara ya Mambo ya nchi za nje alikokwenda kutafuta namba ya simu ya Balozi Lutta, hakuelewa kabisa ni nini kilitokea mahabusu ambako Dk. Othman ili kuepusha aibu alikuwa ameamua kujinyonga siku tu aliyotupwa mahabusu, hakuwa tayari kupambana na aibu ya kufanya mauaji.



“Dr what happened to me?” (Daktari nini kimenipata?) Gerald akauliza.

“You have to thank God Gerald, not only God but this beautiful young lady too!” (Inabidi umshukuru Mungu Gerald na si Mungu peke yake bali huyu msichana mrembo pia!)

“I will do that, but tell me what happened?” (Nitafanya hiv yo lakini niambie nini kimetokea?)

“Your Kidneys!” (Figo zako!)

“What happened to my Kidneys again because I had a transplant operation in Italy,?” (nini tena kimetokea kwenye figo zangu sababu nilishafanya operesheni ya kubadilisha figo huko Italia!) aliendelea kuuliza Gerald huku akibubujikwa na machozi, hakuelewa kabisa ni kitu gani kilikuwa kimetokea.



Kufikia hapo daktari hakuwa na sababu ya kuendelea kuficha, isitoshe ilikuwa ni haki yake Gerald kuufahamu ukweli juu ya kilichomtokea, profesa Kayuga akaanza kueleza kila kitu huku watu wengine wakiwa kimya kabisa, Halima muda wote alikuwa akiendelea kulia kwa furaha.



“Kwa hiyo Halima amenipa figo yake?”

“Kabisa, bila huyu msichana hakukuwa na namna yoyote ya kuokoa maisha yako!”

“Halima!” Gerald akaita.

“Bee!”

“Sogea karibu yangu!”

Halima huku akijifuta machozi alikisogelea kitanda na kuinamisha kichwa chake ili asikilize jambo ambalo Gerald alitaka kusema, badala ya kusema chochote Gerald alimubusu usoni, naye akashindwa kuvumilia machozi yakamtoka kwa wingi huku mwili wake wote ukitetemeka katika hali ya kutokuamini kama yote aliyoelezwa yalimpata yeye. Kumbukumbu ya karibu aliyokuwa nayo ni alipokutana na Halima kwenye ngazi za bweni akionekana mwenye haraka, wala hakuelewa habari za kutaka kuuawa na Dk. Othman ili yeye ndiye amuoe Halima.

“I will always love you Halima, thanks a lot for bringing me back to life!” (Nitakupenda siku zote Halima, ahsante sana kwa kunirudisha duniani!)

“I love you Gerald, with all my heart, you don’t have to thank me, it is my responsibility baby, Iam happy you are back, I know soon we are going to get Married as we promised!” (Nakupenda Gerald kwa moyo wangu wote, huhitaji kunishukuru ni wajibu wangu, ninafurahi kwamba umerudi, najua muda si mrefu sasa tutaoana kama tulivyaohidiana!)

Gerald akatabasamu na baadaye kutamka sentensi moja tu ndefu “YES, THAT IS WHY I HAVE COME BACK, TO MARRY YOU, THEREAFTER I WILL BE READY TO DIE” watu wote ndani ya chumba wakashangilia, wauguzi wala hawakujali walikuwa hospitali, walijikuta wakipiga vigelegele! Mabadiliko ya afya ya Gerald yaliwashangaza wote, alivyoonekana ilikuwa ni kama alirejewa na fahamu zake siku kadhaa kabla.

“Thank you Gerald! That is why I too droped Dr, Othman for you” (Ahsante Gerald, hiyo ndiyo sababu nilimwacha Dk. Othman kwa ajili yako!)



Haikuwa siri tena, uhusiano wao sasa ulikuwa wazi kwa kila mtu, madaktari walielewa ni kwa sababu gani Halima alijitolea figo yake, pia ni kwanini Dk. Othman alifikia uamuzi wa kumuua Gerald! Muda mfupi tu baadaye mlango ukafunguliwa, Balozi Lutta akaingia akikimbia, mmoja wa wauguzi alishachomoka kwenda kumpigia simu, akaenda moja kwa moja hadi kitandani kabla ya kumsalimia mtu yeyote.

“Baba!”

“Ndio mwanangu, kweli Mungu ana nguvu, umepona?”

“Ndio baba! Pole sana kwa kuniuguza, Mungu ametenda muujiza, namshukuru sana huyu binti, sikuwahi kukutambulisha kwake kabla kwa sababu wakati wa kufanya hivyo ulikuwa bado, anaitwa Halima, ni mke wangu mtarajiwa!”

“Namfahamu, tumehangaika naye sana, amekwishakuambia kwamba alitaka kujiua kwa kugongwa na treni baada ya kufukuzwa alipotaka kukupa figo?”

“Bado!’

“Basi ndio hivyo, Gerald usije ukamuumiza moyo huyu binti, anakupenda tena kwa dhati, huwezi kupata mwanamke mwingine kama huyu aliye tayari kukosana na wazazi wake kwa ajili yako, amejitoa, amejitoa sana huyu msichana!”

“Baba nakuelewa, sitafanya hivyo, mimi pia nampenda mno!”



Baada ya kuwasalimia madaktari na wauguzi wakiongozwa na profesa Kayuga, balozi Lutta alishindwa kuvumilia akawaomba apige magoti kumshukuru Mungu kwa muujiza aliotenda, hakuwepo mtu wa kumkatalia, cha kushangaza watu wote waliokuwemo ndani ya chumba wakapiga magoti kukizunguka kitanda na kuanza kusali wakimshukuru Mungu, hakuna aliyeamini kuwa yaliyotendeka ni kwa uwezo wa akili za mwanadamu.



“Ameni!” Dakika tano baadaye wote waliitika na kusimama.

Ilikuwa ni furaha ya ajabu kwa kila mmoja wetu, Halima alishinda kitanda kwa Gerald kila siku akimuuguza, alishasahau kabisa kwamba yeye mwenyewe alikuwa mgonjwa.



****

Kilichofuata baada ya hapo ni maendeleo mema ya afya zao wote, wiki moja baadaye haikuwa rahisi kufahamu walikuwa wagonjwa na kwamba Gerald alikuwa na hali mbaya zaidi, alianza kunenepa na kunawiri, sura yake ikaanza kurejea katika hali ya kawaida yenye mvuto, uzuri wake ukaanza kuonekana wazi.



Habari zao hazikuwa siri tena nchini Tanzania, redio, televisheni na magazeti yote yaliandika juu ya ujasiri wa Halima kutoa maisha yake kwa ajili ya mtu aliyempenda, wazazi wake waliposoma magazeti roho zilizidi kuwauma, walihisi kusalitiwa na mtoto wao wa kuzaa lakini hawakuwa na jinsi! Chuo Kikuu walikuwa gumzo, wanafunzi mamia kwa mamia walimiminika kwenda hospitali ya Muhimbili kuwaona ili kuamini kama kilichoandikwa kilikuwa ni kweli.



Mwanzoni mwa wiki ya pili, waliruhusiwa kutoka hospitali, badala ya kwenda chuo moja kwa moja walikwenda kwenye nyumba nyingine ya balozi Lutta maeneo ya Mikocheni, kwani nyumba ya mwanzo alikwishakuiuza, walimkuta mama wa kambo ambaye wala hakuonyesha furaha ya aina yoyote ya kurejea kwa Gerald, muda wote alikuwa amewanunia Gerald na Halima.

“Mama kwanini uko hivyo?” Gerald alimuuliza siku iliyofuata.

“Sipendi kujibu swali hilo!”

“Hukutaka nipone?”

“Nasema sitaki kujibu na sitaki kumwona huyu msichana hapa nyumbani!”

“Kwanini?”

“Gerald usiniulize maswali mengi!”



Akaamua kuwa kimya, baadaye akamshirikisha baba yake ambaye hakumficha chochote juu ya yaliyotokea. Gerald akachukia, hakutaka tena kukaa nyumbani kwao akamwomba baba yake ruhusa awaruhusu kurejea chuoni ambako wangeendelea kupona taratibu huku wakiangalia mambo ya masomo, Balozi Lutta hakuwa na pingamizi kwa suala hilo, akawaruhusu siku iliyofuata warejee chuoni.



“I cant believe this!” (Siwezi kuamini!) msichana aliyeishi chumba kimoja na Halima alisema baada ya kufungua mlango wa chumba na macho yake kukutana nao wakiwa wamesimama, nyuso zao zimejaa tabasamu.

“Why?” (Kwanini?) Gerald akauliza.

“You were seriously sick Gerald!” (Ulikuwa unaumwa mno Gerald!)

“I am ok now!” (Sasa nimepona!)

“Come in, how are you Halima?”(Ingieni ndani, unaendeleaje Halima?) Aliuliza Grace akimpokea Gerald mfuko na kuuingiza ndani, alipouweka chini akarejea tena na kumkumbatia kwa muda mrefu isivyo kawaida

“Mh!” Halima akaguna baada ya kuona mtindo wa kukumbatia uliotumika, hasa kitendo cha kumwekea Gerald mdomo sikioni na kuanza kumhemea kwa karibu, Grace hakuonekana kujali kabisa kwamba Halima alikuwa hapo.

“Mbona umeguna?”

“Aaah! Aaaah! Basi tu”

“Karibuni mkae jamani niliwakumbuka sana, samahani nilishindwa kufika wodini siku za hivi karibuni nilikuwa bize sana na mitihani!”

“Usijali!”

Walikaa pamoja kwa karibu saa mbili, Grace akatayarisha chakula, baada ya kula ndipo wakamsindikiza Gerald kwenda chumbani kwake na kurudi chumbani kwao ambako waliendelea kuongea mambo mbalimbali, maongezi ya Grace hayakumfurahisha Halima hata kidogo kwani asilimia sabini na tano yalikuwa ni ya kusifia uzuri wa Gerald.





Halima akiamini mpenzi wake Gerald alikuwa na mapenzi ya dhati, anaamua kukosana na wazazi wake lakini aokoe maisha ya kijana huyo aliyekuwa katika hali ya kufa kwa ugonjwa wa figo zake zote kuharibika. Halima anakubali kuingia chumba cha upasuaji, kinyume kabisa cha mapenzi ya wazazi wake na kutoa figo yake moja kumpa Gerald ambaye baadaye anakikwepa kifo na wanarejea chuo kikuu ambako rafiki mkubwa wa Halima, Grace anawapokea.

Watu hawa watatu wanatokea kuwa marafiki wa karibu kupita kiasi, Halima anamwamini Grace kuliko anavyojiamini yeye mwenyewe kiasi cha kumruhusu aende mahali popote na Gerald hata disko nyakati za usiku kwani yeye hapendelei sana kutoka usiku.

Baadaye Grace anaonyesha dalili za ujauzito na maneno yanasambaa chuoni kwamba mimba hiyo ni ya Gerald! Halima anakataa kata kata, anamwamini mno mchumba wake, hawezi kumfanyia jambo hilo, lazima atakuwa anakumbuka kuwa bila yeye Halima, angekuwa marehemu. Maneno yalipozidi, siku moja Halima anaamua kuwafuatilia watu hao ndani ya ukumbi wa Billicanas, alichojionea huko na maneno aliyoyasikia yanamfanya azimie ndani ya ukumbi huo, aliporejewa na fahamu alirejea bwenini ambako aliendelea kulia akiwa katika hali ya kutoamini, mwisho akaamua kitu kimoja kwamba, GERALD NA GRACE HAWAKUSTAHILI KUISHI. Amenoa kisu akiwasubiri ili wakija awaue na baadaye yeye mwenyewe ajiue. Je, nini kitafuata? Endelea…



Chumba kilikuwa na giza nene, taa zote zikiwa zimezimwa. Halima alikuwa amelala chali kitandani mwake akibubujikwana machozi yaliyoshuka taratibu kupitia pembeni mwa macho yake na kuyakatiza masikio kisha kudondoka kila upande wa kichwa chake kwenye godoro lililoendelea kulowa taratibu. Moyo ulikuwa ukimuuma mno, alijisikia kusalitiwa, kuadhibiwa kwa kosa ambalo hakulifanya. Mara kadhaa alijikuta akitamka “Gerald! Kweli amenitenda hivi? Nimekomkosea nini?” maneno hayo yalimfanya azidi kulia kwa uchungu, hakuna kitu alichotaka kufanya wakati huo zaidi ya kuua na yeye kufa, duniani hapakuwa mahali pake pa kuishi tena, alitamani kwenda ahera na alikuwa tayari kwa adhabu ambayo angeifanya.



“Hivi hata Mungu nitakampokutana naye na kumuuliza, kwa maumivu haya ninayoyapata yeye angefanya nini? Sijui kama atakuwa na jibu la kunipa…Gerald na Grace wanastahili kufa!” Aliwaza Halima.



Hakuwa tayari kutoa msamaha hasa alipokumbuka mambo aliyoyafanya nyuma kwa ajili ya Gerald, uhusiano na wazazi wake ulikuwa umeharibika, aligombana na Dk.Othman, kijana aliyeokoa maisha yake na baadaye kuamua kumuoa lakini yeye Halima akaamua kumuacha tena siku ya kuvishana pete ya uchumba kwa sababu ya Gerald ambaye sasa alikuwa amemuumiza. Hasira zikampanda, akatamani wakati huo huo mlango ufunguliwe ili atimize alichokuwa amekipanga, akakichukua kisu kilichokua pembeni yake mkono wa kulia na kuanza kukigusa ncha zake, kilikuwa na makali ya kutosha kutimiza azma yake.



“Masikini Othman, alinipenda lakini mimi nikamuumiza, tena kwangu alikuwa akiumia kwa mara ya pili baada ya kuwa ameachwa na mwanamke mwingine siku za nyuma, kwa kweli sikutenda jambo jema kama maumivu aliyoyapata ndio haya, nafikiri Mungu ananionyesha jinsi alivyoumia ili nijue kabisa kwamba duniani usiwatendee watu mambo usiyopenda kutendewa!” alizidi kuwaza Halima akilia.

Alitamani kukutana na Dk. Othman wakati huo huo amwombe msamaha kwa yote aliyomtendea baada ya kuwa amefahamu ni maumivu makali kiasi gani aliyapata, ukiachana na aibu ya kukataliwa sikuya kuvishana pete ya uchumba na mwisho kabisa akijaribu kuokoa uchumba wake na mwanamke aliyempenda aliamua kuua, jambo lililompeleka mahabusu.



Mpaka wakati huo hakuelewa hata kidogo ni wapi alikokuwa na kitu gani kilimpata baada ya kukamatwa na polisi, Gerald aliushikilia ubongo wake sawasawa kiasi cha Halima kutotaka kusikia habari za Dk. Othman kabisa lakini usiku wa siku hiyo, alitaka kufahamu, alitaka kuongea naye ili amweleze mambo aliyotendewa. Ni katika kufikiria jambo hilo ndipo jina la Dk. Ringo, rafiki mkubwa wa Othman likamwijia kichwani mwake, akaivuta simu ya mkononi iliyokuwa mezani pembeni mwa kitanda na kuanza kutafuta namba yake mpaka akaipata na kubonyeza namba 0742-382855, haukupita muda mrefu sana ikaanza kuita, Halima akafuta machozi yake na kunyanyuka, akaketi vizuri kitandani, hakuwa na uhakika kama bado daktari huyo alitumia namba ile.



“Hallow!” Ilikuwa sauti ya Dk.Ringo ikiuliza kwa sauti ya chini yenye kukwaruza, ikionyesha mtu huyo alikuwa amezinduliwa usingizini kwani saa ya mkononi ya Halima ilisomeka saa tisa na dakika arobaini na tano.

“Dk. Ringo?”

“Ndio, sauti yako ni kama naifahamu lakini sijui ni nani?”

“Ni mimi Halima!”

“Halima gani?”

“Niliyekuwa mchumba wa rafiki yako Dk. Othman!”

“Aaah! Shemeji, habari ya siku? Mbona simu usiku huu? Hujambo?” Dk. Ringo aliuliza maswali mfululizo.

“ Sijambo kidogo, nina matatizo na nilitaka sana kufahamu ni wapi aliko Othman kwa sasa!”

“Masikini, unaulizia habari za Othman? Zinasikitisha sana!”

“Kwanini?”

“Baada ya kukamatwa akiwa mahabusu, hakuona sababu ya kuendelea kuishi na kwa kutumia suruali yake akaamua kuyakatisha mai…!” Dk. Ringo hakumalizia sentensi yake, Halima akakata simu, mlango ulikuwa umefunguliwa, taa zikawashwa na Gerald na Grace wakaingia wakiwa wamelewa taabani, kisu alichokuwa nacho akakiweka kwa haraka chini ya mto na kunyanyuka kitandani uso wake ukiwa umejawa na tabasamu la plastiki.

“Hi!Honey!”(Hujambo asali wa moyo wangu!) Gerald alitamka maneno hayo akimsogelea Halima na kumkumbatia, mkuki wa maumivu ukapenya moyoni mwa Halima, machozi yakambubujika.

“ I am fine baby, mafua tu ndio yananisumbua, vipi Billicanas leo?”

“Ilikuwa full kujirusha, sijui kwanini hukuja?”

“Mafua tu ndio yananisumbua, nilitaka sana kwenda, vipi Grace mbona amefikia kitandani?”

“Kinywaji, si unamjua huyu ni mtu wa pombe, hata muziki hajacheza, ilikuwa ni mvinyo mtindo mmoja, yaani mpaka akanikera, sitaki tena kuwa natoka naye bila wewe kuwepo!”

“Usijali, huyu ni rafiki yangu wa siku nyingi, unaweza tu kuendelea kutoka naye, namwamini mno!” Aliongea Halima akijitoa mikononi mwa Gerald na kuanza kutembea kukifuata kitanda cha Grace aliyekuwa amejitupa kitandani.

“Grace! Grace! Grace! My best friend, wake up, tell me what happened at the Bills today!”(Grace! Grace!Grace! Rafiki yangu mpendwa, amka, nieleze nini kimetokea Billicanas leo!) Aliongea Halima akikumbuka sinema ya The Best Friend of Mine, ambayo ndani yake wasichana wawili walikuwa wakizungukana kwa mwanaume mmoja, mambo yaliyotokea katika sinema hiyo ndiyo yalikuwa yakimtokea Halima usiku huo.



Grace hakuitika, aliendelea kukoroma, hicho ndicho alichokihitaji Halima ili isiwe kazi ngumu kuutoa uhai wake akiwa usingizini. Akarejea kwa Gerald na kukumbatia akimsihi aende chumbani kwake kupumzika ili kesho yake aweze kuwa na nguvu za kufuatilia taratibu za usafiri wa safari yao kwenda Italia, Gerald hakubisha akamwomba Halima amsingikize hadi chumbani kwake naye akakubali, wote wawili wakaanza kutembea wakishuka ngazi hadi chini kisha kuelekea kwenye bweni la Gerald lililokuwa kiasi cha mita mia moja kutoka bweni lake.

Gerald alifungua mlango na kuingia ndani akifutiwa na Halima nyuma yake, akajitupa kitandani akimruhusu Halima arudi chumbani kwake lakini kabla ya kuondoka msichana huyo akiwa na maumivu makali moyoni mwake alijipa moyo na kumsogelea Gerald kitandani akapiga magoti chini na kumbusu usoni.

“Gerald!” Akamwita.

“Yes baby!” Gerald akaitika katika hali ya usingizi usingizi.

“Ungefanya nini kama leo hii ungegundua kuwa mimi nimetembea na Tom?” Aliuliza Halima akimaanisha rafiki mkubwa wa Gerald.

“Kwanini unaniuliza swali hilo?”

“Basi tu nilitaka kufahamu!”

“Hakyanani nitakuua siku hiyo hiyo, wala sitaogopa kwenda jela, mimi mwanaume hata nikinyongwa sawa tu!”

“Aisee, basi usiku mwema, lala salama mpenzi wangu, muda si mrefu mimi na wewe tutakuwa kwenye usingizi mzuri!”

“Ahsante mpenzi wangu, nakutakia usingizi mwema, rudisha tu huo mlango!” Gerald aliongea akiusikia baadaye mlango wake ukibamizwa, Halima akawa ameondoka.

Alipita kwenye ngazi peke yake, akijaribu kutafakari juu ya jibu alilopewa na Gerald, akathibitisha kabisa kwamba adhabu aliyokuwa ameamua kuwapa watu hao wawili ilikuwa ni sahihi kabisa! Gerald na Grace walistahili kufa, kama yeye angemuua kwa kutembea na Tom basi pia Gerald alistahili kufa kwa kufanya kosa hilo na Grace. Hasira ikazidi kupanda maradufu.

Alipofika chumbani kwake, badoGrace alikuwa akikoroma, Halima akaketi kitandani kwake joto la hasira likiendelea kuongezeka, hakuwa binadamu wa kawaida, shetani alishachukua kila idara mwilini mwake, kuanzia akili mpaka kucha. Alichofikiria wakati huo Halima ni kumwaga damu. Akiwa katika fikra hizo, ghafla mawazo juu ya wazazi wake yakaingia, akamwona mama yake na baadaye baba na shangazi zake, moyoni akajisikia mkosaji mkubwa lakini pamoja na hayo alitaka alitaka kuwaeleza wazazi wake namna alivyojuta kabla hajakatisha maisha yake, isingekuwa vyema afe bila kuwaomba msamaha. Alipofikia hapo Halima, akajivuta na kuisogelea meza iliyokuwa pembeni mwa kitanda chake akachukua kalamu na karatasi na kuanza kuandika juu yake huku mashavu yake yakiendelea kulowa na machozi;



Wapendwa baba na mama,

Nawaandikia barua hii ikielekea kuwa alfajiri ya leo tarehe 25. Moyoni mwangu nina masikitiko makubwa mno, yaliyonipata ni makubwa, nashindwa hata kuyaeleza. Mtu aliyenikosanisha nanyi wazazi wangu, amenitenda! Gerald niliyempa figo yangu ili niokoe maisha yake kinyume na matakwa yenu, amenifanyia kitu ambacho kwa hakika kinanifanya nisione maana ya kuendelea kuwa hai; AMEMPA MIMBA RAFIKI YANGU GRACE na nimewafumania ndani ya ukumbi wa Billicanas wakinisema maneno mabaya ya kunibeza na kunitukana, roho inaniuma sana. Hivyo basi nimefikia uamuzi wa kuyakatisha maisha yangu, labda hili litakuwa jibu la matatizo yanayonikabili lakini kabla sijafanya hivyo, barua hii ni ya kuomba msamaha kwenu, baba na mama naomba mnisamehe kwa yote niliyowatendea, najua niliwaumiza sana lakini yaliyopita si ndwele, mkinisamehe ninyi nitabakiza dhambi moja tu mbele ya Mungu;KUUA NA KUJIUA. Ambayo kwa hakika niko tayari kukutana nayo.

Nitashukuru sana kama mtanisamehe.

Gerald na Grace nimeondoka nao, hawa tutajadiliana huko huko ahera baada ya kukutana, niagieni ndugu zangu wote, nawatangulieni mbele ya haki.

Ni mimi mwanenu Halima.

Nimeiandika saa kumi usiku, dakika chache zijazo nitakuwa marehemu.

*****

Kulikuwa na ukimya wa ajabu nje ya chumba chao, hakuna mwanafunzi aliyepita koridoni, wengi walishaondoka baada ya shule kufungwa, waliokuwepo walikuwa usingizini wengi wakikoroma bila kuelewa kilichotaka kutokea ambacho kingeushtua ulimwengu wote wa wasomi wa Chuo Kikuu, Halima amewaua Grace na Gerald? Lingekuwa swali la kila mtu siku iliyofuata, hakuna ambaye angeamini kwani hakuwa na sura ya kiuaji. Alipiga picha kwa akili yake na kuona damu imetapakaa chumbani, maiti ya Grace ikiwa imelala sakafuni, vivyo hivyo ingekuwa kwenye chumba cha Gerald na yeye mwenyewe angekuwa amening’inia kwenye ubao wa kuning’inizia chandarua, akiwa marehemu.

“Habari hii itatangazwa mpaka BBC!” Aliwaza akibubujikwa na machozi kwa wingi yaliyolowanisha mashavu yake, hakuwa na muda zaidi wa kuishi duniani, dakika zake zilikuwa zinahesabika.

Ghafla mawazo yake yakamrejesha tena Morogoro, akawaona wazazi wake, yakampeleka Mikocheni, akamwona shangazi yake. Akaelewa ni namna gani watu hao wangelia na kuumia mioyo yao, bila shaka wangejilaumu sana kwa uamuzi mbaya wa kumtenga mtoto wao sababu tu aliamua kuokoa maisha ya mtu aliyempenda ambaye hata hivyo baadaye alikuja kumsaliti na kumsababishia maumivu yaliyopelekea kufanya mauaji na baadaye yeye mwenyewe kukatisha uhai wake.

“Masikini mama, najua ataumia, pengine uamuzi wa kunitenga aliufuata tu kwa sababu baba alikuwa ameamua, sina jinsi, kwa yaliyonipata ni bora tu nife!” Aliwaza Halima na kukichomoa kisu chake chenye makali kotekote na ncha iliyochongoka na kuanza kutembea huku akitetemeka kukielekea kitanda alicholala Grace akikoroma sababu ya pombe nyingi alizokunywa.

Aliposimama mbele ya kitanda cha Grace kengele ya saa ya ukutani ililia, tayari ilikuwa imegonga saa kumi na moja na nusu ya alfajiri, muda ambao katika hali ya kawaida alitakiwa kuamka na kujisomea lakini siku hiyo ilikuwa tofauti, alitakiwa kuua! Mara moja picha ya ndani ya ukumbi ikamwijia tena kichwani mwake kama sinema, akamwona Grace akiwa amekaa miguuni mwa Gerald wakinyonyana ndimi na walipoachiana maneno ya matusi mazito yakafuata, kumkashfu yeye! .



Alipofikia hapo kimawazo, Halima hakuona sababu ya kumfanya amwache Grace hai, adhabu pekee aliyostahili ni kifo. Kama alidiriki kumchukua mchumba wa rafiki yake bila huruma huku akiielewa vizuri historia kwamba ni Halima aliyeokoa maisha ya mwanaume aliyekuwa akimchukua, ni wazi hakuwa rafiki mwema, hivyo basi alistahili kilichokuwa mbele yake yaani kifo.

“Ee Mungu wa Mbinguni, najua kabisa jambo ninalotaka kulifanya ni baya, sitakiwi kukatisha uhai wa binadamu mwenzangu, maana wewe mwenyewe ulituambia “USIUE” lakini kwa mambo ambayo mtu huyu amenifanyia, Ee Mungu wangu, nipo tayari kuchomwa moto siku ya kiama lakini nimwondoe ulimwenguni, ameniumiza Mungu hata wewe unajua… kama utaona nafaa kusamehewa basi unaweza kufanya hivyo lakini mimi nimeamua kumuua Grace na baadaye nimuue Gerald!” Alitamka maneno hayo Halima mikono yake yote miwili ikiwa juu ikisubiri kushuka tumboni mwa Grace kwa kasi ili damu iruke, akichomoe tena na kukizamisha mara ya pili na ya tatu kisha kumalizia kwenye moyo, baada ya hapo amfunike puani na mdomoni na mto wa kulalia ili afe taratibu bila mtu yeyote kusikia sauti yake.

“Moja…mbili…ta…!” Alihesabu akizidi kububujikwa na machozi huku dudu likiwa limekaba kooni, ilikuwa ni hasira ya ajabu.



****

“Mhhhhh!Mhhhh! Aaaaiii! Mama yangu weeee!” Ilikuwa ni sauti ya mwanamke akigugumia kitandani.

“Mama Halima! Mama Halima!” Sauti ya mzee yenye kukwaruza ilifuatia huku akimtingisha mwanamke aliyelala pembeni mwake ambaye alikurupuka kitandani na kuketi kitako.

“Vipi?”

“Ndoto!”

“Ndoto gani?”

“Nimeota ndoto mbaya sana!”

“Ndoto gani?”

“Bila shaka mwanangu atakuwa katika matatizo makubwa sana!”

“Nani?”

“Halima!”

“Umeotaje?”

“Nimemwona akifikishwa mahakamani kwa mauaji, Hakimu akamhukumu kunyongwa kwa sababu alikuwa amewaua watu kwa kutumia kisu, alikuwa akilia mno na kutuomba msamaha sisi wazazi wake na kutulaumu kwamba ndio tulichangia kumfanya awe muuaji baada ya kumtenga!”



Hakuna jibu lililotoka kwa mzee aliyelala pembeni mwa mwanamke huyo, badala ya kusema chochote alivuta shuka yake na kujifunika kama vile amepuuza kilichokuwa kikisemwa, ilikuwa ndoto ya ajabu mno kwa mwanamke huyo, jasho jingi lilikuwa likimtoka na kwa kweli ilikuwa ni zaidi ya ndoto, isipokuwa ni kama alikuwa akionyeshwa jambo, hakutaka kupuuza, mara moja akashuka kitandani na kusujudu akiwa ameelekeza kichwa chake Kibra na kuanza kumwomba Mwenyezi Mungu amrehemu mtoto wake na kumwepushia mabaya yote ambayo yangempata, alipomaliza kuswali aliketi pembeni mwa kitanda na kuendelea kutafakari ndoto yake huku mumewe akiendelea kukoroma.



Alikuwa hajamwona mwanae Halima kwa muda mrefu sana lakini moyoni mwake hakuondoka, bado alimpenda! Alikuwa mwanae hata kama alikuwa amefanya kosa gani, mara kadhaa alijaribu kumshauri mume wake wamsamehe na kumpa nafasi nyingine na kwamba kumtenga kusingesaidia chochote lakini mzee Mohamed hakukubali, hakutaka hata kusikia habari za Halima kabisa.



Barua nyingi za Halima kuomba msamaha zilipokuja mzee hakutaka hata kuziona lakini mama alipozisoma alilia siku nzima, maneno ya Halima yalimchoma mno moyoni mwake hasa aliposema “ Nakupenda mama, hata nikifa leo nitakufa nikiwa nakupenda!” Pamoja na mtoto wake kuwa mbali na yeye kutotaka kumwonyesha mumewe kwamba hakumuunga mkono katika adhabu aliyotoa, bado Halima hakuondoka akilini mwake, siku zote aliishi moyoni mwake na alimwota mara nyingi mno, aliamini siku moja yote yaliyojitokeza yangekuja kupita na wangeishi tena kama familia iliyojaa upendo.

“Baba Halima! Baba Halima!” akaita.

“Naam!”

“Hivi kwanini tusimsamehe mtoto?”

“Tafadhali, naomba uniache nilale!”

“Sio hivyo mume wangu, yule ni mwanetu, mkono ukikosea huwezi kuukata!”

“Nasema niache nilale, kama wewe Halima ni mwanao sana basi ondoka umfuate, hapa ndani hatii mguu na nikifa jeneza langu asiliguse, baba yake keshakuwa mzee Lutta, huko huko na yatamkuta makubwa mtoto yule, kanipuuza sana!” Alifoka mzee Mohamed na kujifunika kwa blanketi kichwani.



Hizo ndizo zilikuwa kauli zake, siku zote alikuwa mzee mgumu sana kutoa msamaha kwa watu waliomkosea. Iitwayo hisia ya sita, ilikuwa imewasiliana na mke wake, ikamjulisha kilichotaka kutokea bwenini kwa mtoto wao lakini mzee Mohamed hakuwa na uwezo huo, angejua angemsikiliza mke wake.



***

“Ta…” Kabla Halima hajakamilisha neno “Tatu” ili kisu kishuke tumboni mwa Grace na kumuua kabisa, ghafla aliliona tumbo lililovimba, mimba! Mikono yake ikafa ganzi hapo hapo, kulikuwa na kiumbe kingine tumboni mwa mwanamke huyo mbaya ambacho hakikuwa na hatia kabisa, asingeweza kumuua mtoto huyo, ni kweli mama yake alikuwa amemtendea jambo baya lakini si yeye, hakustahili adhabu ya kifo kwa makosa ya mama yake.

“Mbona sisi leo hii tunakufa kwa makosa yaliyofanywa na babu na bibi yetu wa mwanzo? Mimi nakufa leo, kwani nilikula tunda lililokatazwa?” Aliwaza Halima kichwani mwake, alielewa vizuri fungu hilo ingawa alikuwa Mwislam.

Alijaribu kwa nguvu zake zote kujenga utetezi ili akamilishe zoezi la kumuua Grace lakini bado upande mmoja wa moyo wake ulimwambia hapana, mikono ikiwa bado iko juu huku machozi yakimtoka, ghafla alishtukia mlango unafunguliwa, sura ya Gerald ikaonekana.

“Halimaaaaaa! What are you doing? Don’t kill!” (Halimaaaaa! Unafanya nini? Usiue!) Alisema kwa sauti ya juu.

“Leave me alone, leave me alone Gerald, enough is enough! I want to die, but before I die you and Grace should be dead, leave this room!” (Niache! Niache Gerald, imetosha! Nataka kufa lakini kabla sijafa wewe na Grace lazima muwe mmekufa, ondoka chumbani!)

“Why?” (Kwanini?)

“You know why!” (Unajua kwanini!)http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Please don’t do that, let me explain, give me the chance to tell the truth!” (Tafadhali usifanye hivyo, acha nikueleze, nipe nafasi ya kukueleza ukweli!) Aliongea Gerald akitambaa sakafuni akiwa amepiga magoti na kukusanya mikono yake pamoja kama mtu aliyekuwa akisujudu.

“Don’t worship me, I am not God, please standup and leave or else I will stab you with this knife in your neck, I hate you Gerald, I don’t love you anymore! How can you forget that I have only one Kidney in my body and you are carrying the second? And I did that just to save your life?” (Usinisujudie kwa sababu mimi sio Mungu, simama na uondoke vinginevyo nitakuchoma na kisu shingoni, nakuchukua Gerald, sikupendi tena! Unawezaje kusahau kwamba nina figo moja mwilini, nyingine unaibeba wewe? Na nilifanya hivyo kuokoa maisha yako?)

“What have I done?” (Nimefanya nini?)

“You love this prostitute, you have made her pregnant! Gerald, why do this to me? Cant you think? Why hurt me? Have I did anything wrong?” (Unampenda huyu Malaya, umemjaza mimba! Gerald, kwanini unanifanyia hivi? Huwezi kufikiria? Kwanini unaniumiza? Nimekukosea kitu chochote?) Alizidi kuongea Halima, Gerald akiwa amemkumbatia mapajani na kuweka kichwa chake mbele ya tumbo lake la chini, kichwani mwake Halima alifikia uamuzi wa kukizamisha kisu mgongoni kwake.

*****

Grace alikuwa bado akikoroma, hakuwa na habari kabisa na kilichotaka kumtokea. Pombe ilikuwa imemzidi, kiasi kikubwa sana kilikuwa kichwani mwake, lilipokuja suala la pombe alikunywa bila kujali alikuwa mjamzito na alipojitupa kitandani hakujigeuza mpaka asubuhi. Huo ndio ulikuwa utaratibu wake wa mwishoni mwa wiki. Halima aliendelea kulia mkononi akiwa ameshikilia kisu, Gerald akiwa amepiga magoti chini naye akibubujikwa na machozi huku mikono yake yote miwili ikiwa Halima imemzunguka mapajani.



“Niachie, niachie Gerald, sitaki kukuona, nataka kuwaua wewe na Grace baada ya hapo mimi mwenyewe nife! Umenitenda, umenifanyia jambo baya wakati mimi nimeshakufanyia mazuri, ni mimi niliyeokoa maisha yako Gerald, hivi nilitoa figo yangu ili uje kunifanyia haya?” Aliuliza Halima akizidi kulia.



“Sio hivyo, ni shetani tu! Grace alinishawishi kunywa pombe baadaye akafanikiwa kunishawishi kufanya naye tendo la ndoa, nimekutana naye mara moja tu mpenzi wangu ndipo akapata ujauzito, nisamehe, naomba unisamehe niko chini ya miguu yako Halima, nimekukosea bila kupanga, nakupenda na ninakumbuka vizuri sana wema ulionitendea, bila wewe hakika nisingekuwa hai!”

“Gerald, nimekosana na wazazi wangu kwa ajili yako, kwanini lakini? Kwanini umenifanyia hivi?”

“Nisamehe mpenzi, binadamu tumeumbiwa makosa!”

“Hapana, unasingizia Gerald, uliamua kunitendea hivi,kumbuka nilikuwa nakusihi kila siku uwe mwangalifu na ukanihakikishia kwamba usingeanguka kwenye mitego ya Grace, unaona sasa?”

Alipomaliza kusema maneno hayo Halima, akili yake ikamrudisha ndani ya ukumbi wa Billicanas ambako aliona kila kitu kama sinema na kuyasikia maneno ambayo Grace na Gerald walikuwa wakiongea, hasira ikampanda upya, Gerald amwite mshamba? Hapana, hakustahili kutendewa ukatili huo, akanyanyua mikono yake yote miwili juu kwa lengo la kumchoma Gerald mgongoni na huo ndio uwe mwisho wake lakini kabla hajakishusha Gerald akanyanyuka ghafla, mabega yake yakafika kwapani kwa Halima, akashindwa kukishusha kisu.

“Niachie!” Halima akaongea kwa sauti ya juu lakini Gerald hakufanya hivyo, akafanikiwa kumnyang’anya kisu kilichokuwa mikononi mwake na Halima akaanguka chini akilia.

“Nisamehe, naahidi sitarudia tena kosa hilo!”

“Tayari ana mimba yako!”

“Hata kama, ni yeye ndiye alinidanganya, ikibidi kuitoa tutaitoa!”

“Hapana! Usiue Gerald kiumbe kisicho na hatia, endelea naye tu kwa sababu unampenda, maneno uliyoyaongea ndani ya ukumbi wa Billicanas nimeyasikia na yameniumiza kweli, sitakusamehe Gerald, leo umenifanya nimkumbuke Dk. Othman, mwanaume aliyenipenda kwa moyo wake wote lakini nikamwacha kwa sababu yako, kumbe ulikuwa unakuja kunitenda haya?” Halima alimaliza na kuanza kukimbia kwenda nje, Gerald akimfuata nyuma.



Walishuka ngazi kwa kasi mpaka nje ya bweni ambako Halima aliendelea kukimbia kuelekea langoni, ulikuwa bado ni usiku hakuna mwanafunzi aliyeonekana kupita mahali popote.Halima hakwenda mbali sana, Gerald akawa amekwishamfikia na kumkamata kwa mikono yake miwili.

“Lets talk!” (Tuongee!)

“About what?” (Juu ya nini?)

“My apology!” (Msamaha wangu!)

“It is finished between you and I, let me face the world alone! Go ahead with the woman you love, the one who knows what dressing is all about” (Imekwisha kati yangu mimi na wewe, wacha nipambane na dunia peke yangu, endelea na mwanamke umpendaye, anayejua kuvaa kuliko mimi!)



Gerald hakukubali alizidi kumkumbatia Halima, ukweli wote aliuelewa, kwa kiasi kikubwa sana alikuwa amemuumiza Halima. Hakutakiwa kumfanyia kitendo cha aina hiyo, moyo wake ulikuwa umejaa majuto makubwa, aibu ilikuwa imemfunika. Aliendelea kumbembeleza ili akubali waende chumbani kwake kuongea vizuri, Halima hakukubali mpaka asubuhi akiwa amekaa kwenye jiwe, muda wote akilia na kuwakumbuka wazazi wake. Saa moja kasorobo, walimwona Grace akishuka ngazi na kuanza kutembea hadi mahali walipokuwa.

“Nyanyuka twende, sitaki kuongea na huyu mtu!” Gerald aliongea akijaribu kumnyanyua Halima kutoka alipokaa, safari hii alikubali, wote wawili wakaanza kutembea kuelekea chumbani kwa Gerald, Grace akiwafuata nyuma akionekana kutofahamu jambo lolote lililotokea. Kabla ya kulifikia bweni, Gerald alimgeukia uso wake ukiwa umefura.

“Najua una mimba yangu, lakini samahani sana kwani kuanzia leo sitaki uhusiano wa aina yoyote, uliniingiza katika mapenzi bila mimi kutaka, ukanisahaulisha mwanamke nimependaye, akili yangu imerejea katika hali ya kawaida!Sitaki tena kukuona Grace, tutasaidiana kulea mimba na mtoto!”

“Gerald! Umechanganyikiwa?”

“Grace, wewe ni rafiki yangu, nilikuamini kupita kiasi, hata mara moja sikuwahi kufikiri ungeweza kutembea na Gerald, ilikuwa nikuue usiku, mshukuru sana Mungu bado unapumua mpaka dakika hii, sio siri historia ingekuwa tofauti mno hivi sasa, utumbo wako ungekuwa umesambaratika kabisa, nakusihi uondoke na tangu sasa sitaki kukuona!”

Grace alibaki amesimama hapo wakati Halima na Gerald wakipandisha ngazi kuelekea ghorofa ya kwanza kilikokuwa chumba cha Gerald akiishi peke yake. Siku nzima waliongea kuhusu uhusiano wao, Gerald akiendelea kuomba msamaha, hatimaye Halima akakubali kumsamehe na kumwomba asirudie tena siku nyingine lakini asidiriki kuitoa mimba.

“Msiitoe, acha kabisa!”

“Sawa!”

“Nakupa nafasi nyingine Gerald, nakupenda, naamini Mungu alinipa wewe uwe mume wangu na si mtu mwingine yeyote, usiniumize tena, nakuomba!”

“Nimekuelewa, nimekwishajifunza kiasi cha kutosha!”



Hawakutaka tena kubaki Dar es Salaam, kila kitu kiliwakumbusha ugomvi wao hivyo siku iliyofuata baada ya taratibu zote za usafiri kukamilika wakaondoka uwanja wa ndege wa Dar es Salaam wakipitia Nairobi, Cairo, Paris na baadaye Italia. Machozi yote ya Halima yalikuwa yamefutika kabisa, akathibitisha usemi kwamba hakuna kitu ambacho mwanamke alihitaji zaidi ya kubembelezwa na kuombwa msamaha. Walipokelewa katika uwanja wa ndege wa Roma na balozi Lutta, mkewe pamoja na watoto wengine wawili wa balozi na kwenda moja kwa moja nyumbani kwake mtaa wa Guscon yalikokuwa makazi ya balozi.



“Karibu Italia, hapa ndio nyumbani kwetu!”

“Ahsante sana darling!” Alijibu Halima, tayari alishasahau machungu yote aliyokuwa nayo.

“Vijana karibuni, nafurahi sana kuwaona, habari za Tanzania?” Balozi Lutta aliuliza.

“Ni nzuri tu baba!”

“Halima!”

“Bee!”

“Nakupenda sana mwanangu, kwa sababu umekuja mambo yote lazima tuyaongee huku!”

“Mambo gani baba?”

“Nisiwe na haraka, ili mradi mmekwishafika!”

Wote wakacheka, Gerald alielewa ni kitu gani baba yake alimaanisha, hakuna kitu alichokihimiza kila siku alipoongea na mwanae kwenye simu kama kuona watu hao wawili wakifunga ndoa na kuishi pamoja kama walivyoahidiana miaka mingi kabla ukizingatia bila Halima Gerald asingekuwa hai na alishatengwa na wazazi wake, familia pekee aliyoitegemea katika maisha yake ilikuwa ni ya Balozi Lutta.



******



Likizo yao nchini Italia ilikuwa nzuri mno, Halima alitembezwa sehemu mbalimbali za nchi hiyo na kujionea maajabu, alikwenda mpaka Milano, Verona na Vatican. Kote huko walitembea na Balozi Lutta ambaye kazi yake ilikuwa ni kuwashawishi wafunge ndoa kabla ya kurudi Tanzania, baada ya muda mrefu wa kazi hiyo hatimaye akafanikiwa, harusi ndogo ya watu hamsini, marafiki wa balozi ilifanyika nyumbani kwake. Waliporejea Tanzania, Halima hakuwa Halima tena bali Blandina, alishabadili dini yake na mapenzi kati yao yalikuwa yamekolea kupita kiasi. Hakuna aliyemkumbuka wala kumwongelea Grace tena.



Masomo yao yaliendelea vizuri, baadaye wakasikia kwamba Grace alijifungua mtoto wa kike nyumbani kwao Moshi na kumwacha na mama yake yeye akarudi Chuoni kuendelea na masomo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa mpaka wakamaliza chuo na kuingia mitaani, Halima bado akiwa hana mawasiliano kabisa na wazazi wake, alielewa ni kiasi gani familia yake ilimchukia na isingekuwa tayari kumpokea hata kama angerudi hivyo akaamua kuendelea na maisha yake tegemeo kubwa maishani likiwa ni mume na familia ya mzee Lutta, hakuwahi kupata simu wala barua kutoka kwa ndugu zake.



Halima ambaye hivi sasa ni Blandina baada ya kubadili dini na kuolewa na Gerald amekubali kusamehe yaliyojitokeza na kuendelea na maisha hivi sasa wakiwa mtu na mke wake, hakuna anayetaka tena kuongelea habari za Grace ambaye wamesikia alishajifungua mtoto na kumwacha kwa wazazi wake huko Moshi kisha kurudi chuoni kuendelea na masomo mpaka wote walipomaliza chuo na kuingia mtaani. Je, nini kitaendelea? Fuatilia.



Wote walikuwa na digrii vichwani mwao tena na heshima juu na wakiwa miongoni mwa wanafunzi waliofanya vizuri kuliko wengine wengi chuoni hapo, hasa Blandina ambaye Chuo Kikuu kilimtaka abaki hapa kufundisha lakini akakata kabisa.

“Eti, nifundishe darling?” Blandina alimuuliza mume wake baada ya kupewa nafasi hiyo na uongozi wa Chuo Kikuu.

“Hapana, kazi ya kufundisha ni ngumu mno, itakunyima muda wa kukaa na mimi, kweli wewe unataka muda wote uwe unasahihisha mitihani ndani ya nyumba yetu?”

“Kwa kweli hata mimi kufudisha sitaki!”

“Inakupasa upumzike kwanza, kama mwaka mmoja hivi tufaidi ndoa yetu!”

“Tutakula nini?”

“Mimi nitatafuta kazi, wewe utakuwa mama wa nyumbani kwa muda mfupi au?”

“Gerald, lakini kumbuka wanawake na maendeleo!”

“Sawa, naona na wewe unaanza kuleta mambo ya akina Getrude Mongela na jinsia ndani ya nyumba yetu!”

“Sio hivyo mume wangu, basi nitafanya unavyotaka, nakupenda mno Gerald, sitaki kukuumiza wala kukusikitisha!”

“Ahsante mke wangu!”

Balozi Lutta na familia yake walikuwa bado wako Ubalozini Italia, hivyo baada ya kutoka chuoni Blandina na mumewe waliingia moja kwa moja ndani ya nyumba yam zee Lutta na kuanza maisha ya kujitegemea. Haukupita muda mrefu sana, Gerald akapata kazi katika shirika binafsi lililojihusisha na mambo ya sheria na uchumi. Ilikuwa ni kazi ya mkataba wa miezi sita kabla hajaajiriwa moja kwa moja na aliipata mwezi Desemba mwishoni.

****

ukumbi mdogo wa Serengeti ndani ya hoteli kubwa ya Sheraton ulikuwa umejaa wafanyakazi zaidi ya thelathinin wa kampuni ya Legal & Economy Consultancy wote wakiwa na furaha, ilikuwa ni tafrija ya kuukaribisha mwaka mpya wa 1996. Mkurugenzi wa kampuni bwana John Adebayor, Raia wa Nigeria pamoja na viongozi wengine wa kampuni walikuwa wamsimama meza ya mbele, wafanyakazi wakipita mmoja baada ya mwingine na kugonganisha glasi. Gerald alikuwa kwenye mstari akiwa amevaa suti nyeusi, mke wake Blandika alivaa gauni la rangi ya dhahabu lenye kumeremeta, lilimbana vizuri kuonyesha umbile lake lilivyo, kiuno kilikuwa chembamba kama alikuwa anataka kukatika, lakini chini ya kiuno tu kulikuwa na mfumuko wa nyama kila upande na sehemu ya nyuma uliomfanya afanane kabisa na umbile la Kibuyu.

Blandina ndiye alikuwa wa kwanza kugonganisha glasi na bosi, kisha Gerald akafuatia. Macho ya bosi wakati anagonganisha glasi na Gerald wala hayakuangalia kilichokuwa kikiendelea, alikuwa akimwangalia Blandina kwa jicho ambalo kila aliyemwona alielewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea kichwani mwake.

“Gerald!” Bosi aliita.

“Yes boss!”(Ndio bosi!)

“Who is this? Your girl friend? Your sister? Or?”(Huyu ni nani? Mpenzi wako, dada yako? Au?)

“My wife!” (Mke wangu!)

“Are you married?” (Umeoa?)

“Yes, didn’t I tell you that?” (Ndio, sikukuambia hilo?)

“You never told me, anyway your wife is so, so, so cute! Oh, my God, I have never seen such a beautiful woman since I came here five years ago, you are blessed to have her!”( Hukuwahi kuniambia, tuyaache hayo mke wako ni mzuri,mzuri, mzuri mno! Oh Mungu wangu, sijawahi kumwona mwanamke mzuri kiasi hiki tangu niingie katika nchi hii miaka mitano iliyopita, umebarikiwa sana kuwa na mwanamke huyu!)

“Thank you, thank you my boss!” (Ahsante, ahsante mkubwa wangu!) Gerald alishukuru akimsogelea mke wake na kumtaka amsogelee bosi kumsalimia, Blandina kwa sababu ya aibu alionekana kusita au kutopenda kitu hicho lakini Gerald akakunja uso kuonyesha hasira.

“Yaani wewe nakuambia uende kumsalimia bosi wangu unakataa, Blandina utaniudhi!”

Blandina hakutata kubisha tena, akamsogelea bwana Adebayor na kumpa mkono, wakati wamegusana, kidole cha shahada kilimtekenya Blandina kwenye kiganja chake kikionyesha ishara kwamba bosi alikuwa katika mapenzi mazito kwa Blandina. Moyo wake ukapiga, akageuka kumwangalia mume wake ambaye hakujua lolote zaidi ya kuendelea kukenua na kufurahia jambo lililokuwa likitokea.

“Your so beautiful!” (Wewe ni mzuri sana!)

“Thank you!” (Ahsante!)

“Gerald!”

“Yes boss!” (Ndio bosi!)

“I need to talk to you, before we leave here today! Is it possible?” (Nahitaji kuongea na wewe kabla hatujaondoka hapa leo! Je, inawezekana?) Bosi aliuliza.

“Yes Lord!” (Ndio bwana!)

John Adebayor alikuwa mwanaume mwenye misuli mingi, mrefu mwenye sura ya kutisha, kama ungesema alikuwa mweusi kama jembo jipya lazima mwalimu wako angekupa vema darasani na si ajabu akakuandikia neno “Excellent”. Sio siri mwanaume huyu kutoka jimbo la Kanu huko Nigeria, aliyesomea nchini Uingereza na Marekani mpaka kupata digrii ya tatu katika mambo ya uchumi na baadaye kuja Afrika kuanzisha kampuni ya ushauri, alikuwa na sura mbaya! Alifanana sana na watu wa mwanzo duniani, wengi walitania na kusema Mungu alimleta duniani ili kuwaonyesha watu miundo ya watu wa kale ilikuwaje.

Hakuwa na mke, wala hakuwahi kuoa, siku zote alichukua wasichana na kuwaacha shida yake ilipokwisha lakini alilifanya jambo hili kwa siri kubwa bila kugundulika kiasi kwamba hata wafanyakazi wake hawakuwahi kufahamu ni mwanamke gani alihusiana naye kimapenzi. Wapo waliohisi hakuwa mwanaume rijali jambo ambalo halikuwa na ukweli wowote, kilichotokea kilikuwa ni uamuzi binafsi wa Adebayor, aliwachukia wanawake kwa sababu mwanzoni katika maisha yake kabla hajapata mafanikio, wanawake walimkataa sababu ya sura yake mbaya.



“Sijui bosi anataka kuongea na mimi kitu gani?” Gerald alimwambia Blandina.

“Sijui”

“Natamani tu awe anataka kuniambia ananiajiri moja kwa moja!”

“Utafurahi eeh?”

“Sana, wanalipa vizuri mno hapa!”

“Itakuwa vizuri, lakini ana sura ya kutisha?”

“Wewe sura yake inakuhusu nini Blandina? Cha muhimu ni kufikia malengo yetu!”

“Basi uje uende ukamsikilize!”

Masaa mawili baadaye tafrija ilikuwa ikifikia mwisho, wafanyakazi wengine walishaanza kutoka nje na kuingia kwenye magari yao tayari kwa kwenda nyumbani. Blandina na Gerald walikuwa bado wameketi ndani wakimsubiri bwana Adebayor ambaye muda mfupi tu baadaye alionekana akitembea kuelekea mahali walipokuwa wameketi.

“Gerald!”

“Yes Lord!”

“Can we talk?” (Tunaweza kuongea?)

“No problem!” (Hakuna tatizo!)

“Follow me!” (nifuate!)

Gerald akamuaga mke wake kwa busu na kuanza kutembea kuelekea nje akimfuata Adebayor, aliwashuhudia wakitokomea gizani kulikokuwa na bustani kando ya bwawa la kuogelea ambako walikaa kwa karibu nusu saa nzima bila kurejea mpaka Blandina akaanza kuingiwa na wasiwasi kwani alikuwa amebaki peke yake ukumbini, akanyanyuka na kutembea akiusogelea mlango.

“Wanaume wenye sura mbaya kiasi hiki, wakati mwingine wanakuwa mabasha, asije akanichukulia mume wangu bure na hivi ana hamu ya kuajiriwa?” aliwaza Blandina akitabasamu, moyoni mwake alijua jambo hilo haliwezi kutokea.

Kabla hajatoka mlangoni, alikutana na mume wake akitembea kwa kasi kuingia ndani, kwa kumwangali tu usoni mtu ilikuwa ni lazima ujifunze kitu. Uso wake ulijaa wasiwasi mkubwa, macho yake yalionekana kutaka kulengwa lengwa na machozi, Blandina alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea, akalazimika kudadisi.

“Vipi?”

“Hakuna kitu mke wangu, bosi wangu tu ametualika nyumbani kwake usiku huu huu kwa ajili ya kuukaribisha mwaka sisi watatu!”

“Mh! Gerald, are you sure?” (Mh! Gerald, una uhakika?)

“Kwanini nisiwe nao, hana matatizo, ni mvinyo kidogo tu halafu tunaondoka!”

“Lakini kumbuka tayari ni saa saba ya usiku?”

“Sawa una wasiwasi gani? Wakati atatupeleka hadi nyumbani, usiniangushe mpenzi, lazima tumfurahishe bosi wangu ameahidi kuniajiri!”

“Gerald! Gerald, nahisi matatizo hapa!”

“Hakuna, naomba uniamini mimi!”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Ok! Kwa sababu niko na wewe nitakwenda lakini ningekuwa peke yangu, hakika nisingediriki kufanya hivi!”

Mara moja wakatoka ukumbini na kutembea hadi kwenye maegesho, huko walilikuta gari la bwana Adebayor aina ya LandCruiser likiwa limeegeshwa, akashuka na kumfungulia Blandina mlango wa mbele, alisita kupanda kwani katika hali ya kawaida mume wake ndiye alitakiwa akalie kiti hicho.

“Panda tu darling!”

“Gerald! What is happening?” (Gerald! Nini kinatokea?)

“Nothing!” (Hakuna kitu!)

Gerald akapanda kiti cha nyuma na safari kuondoka hoteli ikaanza. Bwana Adebayor aliishi Masaki nyuma ya shule ya Kimataifa ya Tanganyika, alikuwa na jumba kubwa la kifahari lenye bustani kubwa mbele yake. Gari liliposimama mbele ya jumba hilo lango la mbele likafunguliwa na mlinzi, wakaingia na kuegesha gari sehemu maalum ya maegesho kisha kushuka na kuingia ndani. Pamoja na Gerald kuwa mtoto wa Balozi, hakuwahi kuingia kwenye nyumba nzuri kiasi hicho maishani mwake, hawakukaa sebuleni bali walinyoosha hadi kwenye chumba kingine kilichokuwa pembeni kabisa, walipoingia ndani walishangaa kukutana na baa ndogo na alikuwepo mtumishi akiwasubiri.

“Karibuni sana, jisikieni mko nyumbani!”

“Ahsante!’ Gerald aliitikia.

“Utakunywa nini Blandina?”

“Soda!”

“Mvinyo kidogo?”

“Hapana, situmii pombe kabisa!”

“Jaribu kidogo leo mke wangu, kunywa kidogo umfurahishe bosi wangu!” Gerald alimnong’oneza Blandina sikioni.

“Gerald, nini kinaendelea hapa?” Aliuliza Blandina kwa wasiwasi.

“Hakuna kitu!”

Muda mfupi tu baadaye, vinywaji vikawekwa mezani, blandina akapewa soda aina ya fanta kwenye glasi na bwana Adebayor na Gerald wakaendelea kunywa mvinyo, mara kadhaa Blandina alijaribu kumkumbusha Gerald juu ya tabia hiyo ambayo madaktari walishamzuia lakini hakusikia, aliendelea kunywa. Kitu kama nusu saa hivi baadaye, Blandina alianza kusikia macho yamekuwa mazito, usingizi na baadaye kutojitambua kabisa.

Alizinduka asubuhi ya siku iliyofuata akiwa amelala uchi wa mnyama kitandani,akaangalia huku na kule kama alikuwa ndani ya chumba chake na kukuta haikuwa hivyo na Gerald hakuwepo, sekunde chache tu baadaye alimwona bwana Adebayor akitokea bafuni naye akiwa uchi wa mnyama uso wake ukiwa umejawa na tabasamu.

“Your so sweet baby!” (Wewe ni mtamu sana mpenzi!) bwana Adebayor alisema akijitupa kitandani.

*****

Bwana Adebayor alilala pembeni mwa Blandina ambaye uso wake ulikuwa bado ukionyesha wasiwasi mwingi, alikuwa bado hajapata jibu la ilikuwaje mpaka akawa ndani ya chumba hicho. Baada tu ya kulala kitandani, bwana Adebayor alianza kumpapasa mwilini akihema kwa nguvu. Blandina akaruka kitandani na kusimama wima akiwa kama alivyozaliwa mwili wote ukitetemeka, hisia zilimtuma kwamba mume wake alikuwa amemuuza ili afanye mapenzi na bosi wake, jambo hilo alilifikiria tangu mwanzo lakini hakutaka kulichukua kama ukweli, isingewezekana mume wake wa ndoa amfanyie ukatili kama huo.

“What is this? What are you trying to do?” (Nini hiki? Unataka kufanya nini?)

“Not trying, I wanted to go for a fourth round!” (Sio kujaribu, nilitaka kwenda tena raundi ya nne!)

“What?” (Nini?)

“Yes! You are so beautiful Blandina, have never been to bed with such a gorgeous girl!” (Ndio! Wewe ni mzuri sana katika maisha yangu sijawahi kulala na mwanamke mrembo kama wewe!)

Blandina hakutaka kujiuliza tena mara ya pili, picha kamili ikamwijia kichwani mwake, alileweshwa kwa madawa ya usingizi ndani ya soda aliyokunywa kisha kuletwa nyumbani kwa bwana Adebayor kufanya naye ngono! Roho ikamuuma sana, kwa mara nyingine tena Gerald alikuwa amemuumiza kupita kiasi hakuwa na uhakika kama angemsamehe, kwa muda mrefu alikuwa amemvumilia na alijitolea sana kuokoa maisha yake, hivyo hakustahili hata kidogo kutendewa ubaya.

“No!” (Hapana!) alijikuta akitamka maneno hayo na kugeuka kuanza kukimbia kuelekea mlango aliotokea bwana Adebayor ambao bila hata kuuliza alielewa ni bafu, akafunga mlango nyuma yake na kuanza kujichunguza. Machozi yalimtoka aliposhuhudia majeraha aliyokuwa nayo sehemu za siri, ni kweli alikuwa ameingiliwa na mwanaume huyo.

Hakuwa na la kufanya isipokuwa kutoka hadi chumbani ambako alimkuta bwana Adebayor ameketi kitandani uso wake ukiwa umejawa na tabasamu, akaendelea kumwita ili aende kitandani wafanye ngono lakini Blandina hakuwa tena na muda, alichokifanya huku akilia ni kuchukua nguo zake na kuanza kuvaa kisha kuondoka bila kuaga hadi nje ya ngome ambako alitembea mpaka kwenye kituo cha daladala, akapanda lililompeleka mpaka maeneo ya Mikocheni kwa Nyerere akashuka na kuanza kutembea hadi nyumbani kwake.

“Gerald? Kweli amenifanyia hivi? Kwanini mwanaume huyu hana shukrani lakini? Mwisho wangu na yeye umefika, hakyanani lazima anieleze, hakuna tena mapenzi kati yetu, yaani anafikia hatua ya kuniuza?” aliwaza akizidi kutembea.

Nyumbani lango kubwa lilikuwa wazi, akaingia ndani na kukuta gari ya Gerald halipo, haikuwa kawaida yake kuondoka asubuhi kiasi hicho. Akausogelea mlango na kujaribu kuufungua, pia ulikuwa umefungwa, mara kadhaa akaita jina la Gerald lakini hakuitikiwa akaelewa moja kwa moja hakuwepo ndani ya nyumba. Alichofanya ni kwenda mahali ambako wote wawili huficha ufunguo, akaukuta na kuuchukua hadi mlangoni akafungua mlango na kuingia ndani, Gerald hakuwepo.

Alihitaji sana kuwasiliana naye, kichwani mwake alikuwa na hatua nyingi alizotaka kuchukua, ikiwemo kwenda kuripoti suala hilo polisi lakini kabla hajafanya lolote kwanza alitaka aongee na mume wake ili ajue ni kwanini alimtendea ukatili huo. Akaisogelea simu na kubonyeza namba ya Gerald ya simu ya mkononi, hakupatikana! Wasiwasi ukazidi kumwingia, hata hivyo alipojaribu kupiga simu ya mezani alifanikiwa kumpata sekretari wake.

“Nani anaongea?” Sekretari aliuliza.

“Ni mimi mke wake!”

“Blandina?”

“Ndio!”

“Hongereni sana!”

“Kwanini?”

“Huna habari?”

“Ndio!”

“Mumeo si kapandishwa cheo, hivi sasa kawa Mkurugenzi Msaidizi!”

“Mh!” Blandina aliguna na hapo hapo akaelewa ni kwanini aliuzwa.

“Mbona unaguna badala ya kufurahi?”

Hakujibu, mara moja akakata simu na kuendelea kulia kwa uchungu. Hakumtafuta tena Gerald, aliamua kujifungia ndani na kuendelea kulia, fikra juu ya wazazi wake zilianza kumwingia kichwani baada ya mwanaume aliyekuwa anamtegemea maishani kuanza kumsaliti. Kwa mara ya kwanza alifikiria kurejea kwa wazazi wake na kuomba msamaha lakini aliogopa, alimfahamu vizuri baba yake, angeweza hata kumpiga risasi na baadaye kujiua yeye mwenyewe. Katika wakati aliokuwa nao, Blandina alihitaji msaada, si kutoka kwa mtu mwingine yeyote isipokuwa mume wake, huyo ndiye ndugu pekee aliyekuwa naye.

Saa kumi na mbili na nusu jioni alisikia honi ya gari langoni, alielewa moja kwa moja huyo alikuwa ni Gerald anarejea, moyo wake ukapiga kwa nguvu! Hasira ikampanda, alishindwa kabisa kuelewa ni kitu gani kingetokea baada ya Gerald kusimama mbele yake, alielewa wazi ni lazima angemwomba msamaha kwa yote yaliyotokea.

Haukupita muda mrefu sana mlango wa chumba ukafunguliwa, Gerald akaingia uso wake ukiwa umejaa tabasamu na kusimama mbele ya kitanda, mikono kiunoni na kumwangalia Blandina ambaye bado macho yake yalimwaga machozi kuonyesha uchungu aliokuwa nao.

“Mambo?” Gerald alisalimia lakini Blandina hakujibu kitu, aliendelea kulia tu.

“Najua umekasirika, lakini nina habari nzuri kwako, nimepandishwa cheo!”

“Gerald!”

“Naam!”

“Yaani unamuuza mkeo kwa mwanaume mwingine afanye naye ngono sababu unataka kupanda cheo?”

“Nisamehe mke wangu, sikuwa na jinsi!”

“Funga domo lako, usiniita mkeo tena, niite changudoa!”

“Sio hivyo, najua kwa kazi niliyopata maisha yetu yatakuwa safi!”

“Hunipendi Gerald!”

“Sio hivyo, nakupenda mno, tamaa tu ya maisha ndiyo inasumbua, yote haya nimeyafanya kwa ajili yetu sisi sote wawili, naomba unielewe!” Akiongea maneno hayo Gerald tayari alishamfikia Blandina miguuni na kuanza kulamba vidole vyake, akionyesha kujutia jambo lililotokea.

“Gerald unafanya hivi kwa sababu unajua sina mahali pa kwenda? Umenigombanisha na wazazi wangu ndio unaninyanyasa? Sasa kwa taarifa yako naondoka!”

“Hapana baby! Usifanye hivyo, nakupenda na sitarudia tena kosa nililofanya!”

Blandina akainamisha kichwa chake chini na kuendelea kulia huku Gerald akimbembeleza, mpaka saa nne usiku alikuwa bado akiifanya kazi hiyo, akitubu makosa yake! Bila kutegemea Blandina alijikuta akitamka maneno ambayo hakuyapanga kabisa kwamba amemsamehe mume wake lakini akamtaka asirudie tena kosa alilolifanya na siku nyingine asimkutanishe kabisa na bosi wake Adebayor.

“Ahsante mke wangu!”

Baada ya hapo maisha yaliendelea, Blandina akijaribu kwa uwezo wake wote kuifuta kichwani mwake historia ya jambo lililojitokeza lakini hakufanikiwa. Picha ya Adebdayor iliendelea kumsumbua kichwani mwake, zaidi ya hayo yote, jambo jingine pia lilimpa shida! Hesabu zake za mwezi zilionyesha siku alipolala nyumbani kwa Adebayor alikuwa kwenye siku za hatari.

Hofu ya mimba ilikuwa imemtanda, alikuwa na wasiwasi mkubwa wa kuwa na mimba ya Adebayor jambo ambalo hakupenda kabisa litokee, maishani mwake hakuwa msichana aliyefikiria kutoa mimba mara baada ya kuipata, hakutaka kuua kiumbe kisicho na hatia.

Pamoja na Gerald kujaribu kadri ya uwezo wake kumbembeleza kwa kumpeleka sehemu mbalimbali za starehe, kumnunulia zawadi nyingi, bado alibaki mwenye huzuni akisubiri kwa hamu sana hedhi yake, mwisho wa mwezi ulipofika, hakuiona! Blandina akamwaga machozi, lakini akaendelea kujipa matumaini kwamba, huenda ilikuwa bado iko njiani lakini ikawa hivyo kwa mwezi wa pili na wa tatu, akawa na uhakika kabisa alikuwa mjamzito.

“Gerald!”Alimwita mume wake siku moja walipoingia tu kitandani.

“Ndio mke wangu!”

“Nina mimba!”

“Mimba? Ya nani?”

“Ndio! Ya kwako, kwani nani mwingine?”

Gerald hakuonyesha furaha hata kidogo na uso wake ukakunjika, akanyanyuka kitandani na kuketi kitako akihema kwa nguvu kuonyesha hasira. Blandina akaelewa tayari lililokuwa likisubiriwa limefika, akashindwa kuelewa ni kwa sababu gani Mungu alikuwa akimpitisha katika mambo mazito kiasi hicho.

“Labda ya Adebayor!” Gerald aliongea maneno yaliyogeuka mkuki wa moto moyoni mwa Blandina.





Gerald akiwa na tamaa ya kupandishwa cheo kazini kwake, anaamua kumtoa mke wake kufanya mapenzi na bosi wake bwana Adebayor bila kujali atamuumiza kiasi gani Blandina! Kweli anapandishwa cheo lakini kwa Blandina ni mateso, wala hafurahii kilichotokea kwani tayari ana mimba ambayo kwa uhakika anafahamu ni ya Adebayor kwani alipokutana naye kimwili bila ridhaa kwani alileweshwa, ilikuwa ni wakati wa siku mbaya! Anampa Gerald taarifa hizi na anaruka kimanga na kusema mimba hiyo si yake labda ya Adebayor, moyo wa Blandina unauma.

Je, nini kinafuata?



Blandina akaelewa mara moja tayari maumivu yalikuwa yamerejea tena. Gerald alikuwa njiani kuikana mimba hiyo, roho ilimuuma mno ukizingatia ni yeye mwenyewe aliyempeleka kwa Adebayor, wakamlewesha madawa ya kulevya na kujikuta amefanya ngono bila ridhaa yake. Sasa alikuwa na mimba ambayo wala hakuelewa baba wa mtoto wangekuwa nani kati ya wanaume wawili aliokutana nao kimwili katika mwezi mmoja, kilichokuwa kikisikika kutoka ndani ya moyo wake ni kwamba mimba hiyo ilikuwa ni Mnigeria Adabayor kwani siku aliyokutana naye ilikuwa ni katika zile siku ambazo wazungu huziita “Danger Days” yaani siku za hatari ambazo hata yeye mwenyewe hakudiriki kufanya ngono na mume wake kwa kuogopa mimba ambayo hawakuipanga.



Gerald alikuwa pembeni mwake akiendelea kufoka na kudai mimba hiyo haikuwa ya kwake na asingependa kabisa kuhusishwa nayo, Blandina akazidi kumwaga machozi ya uchungu! Bila kupelekwa kwa Adebayor asingefanya naye tendo hilo, isitoshe alishakataa kabisa na mumewe aliyeamua kumuuza ili apande cheo kazini kwake lakini sasa alikuwa akimsaliti.



“I want to have an abortion immediately!” (Nataka uitoe mimba hiyo haraka sana!) Gerald alifoka.

“Gerald! But you wanted this yourself!” (Gerald! Lakini ulitaka jambo hili wewe mwenyewe!)

“How?” (Kivipi?)

“Why did you sell me to your boss?” (Kwanini uliniuza kwa bosi wako?)

“I wanted a promotion not a baby!” (Nilitaka kupandishwa cheo sio mtoto!)

“Now listen, Gerald you have done anything good to me! I left doctor Othman for you, I betrayed my parents to donate one of my kidney to save your life, but later you slept with my friend Grace! As if that wasn’t enough, you sold me to your boss Adebayor, where I got this pregnancy and today you are denying it! I will never abort this pregnancy, I will never kill, whatever happens to me is okay!” (Sasa sikiliza, Gerald hujawahi kunifanyia kitu chochote kizuri, nilimwacha Dk. Othman aliyekuwa tayari kunioa kwa ajili yako, nikawasaliti wazazi wangu ili tu nikupe figo yangu moja kuokoa maisha yako lakini bado ukafanya mapenzi na rafiki yangu Grace! Kama vile hiyo haitoshi ukaniuza kwa bosi wako nifanye naye ngono ambako nilipata mimba hii, leo unaikana! Sitaitoa, sitaua, chochote kitakachonipata acha kitokee!) aliongea Blandina akibubujikwa na machozi.

Picha nzima ya maisha yake tangu kuzaliwa mpaka siku hiyo ilianza kupita mbele ya uso wake kama sinema, akakumbuka Kilosa alikozaliwa na kukulia, akawakumbuka wazazi wake waliompenda na kuwa tayari kufanya lolote kwa ajili yake lakini akakubali kukosana nao kwa sababu ya mwanaume aliyempenda ambaye usiku huo alikuwa amemuumiza kwa mara nyingine. Hakuona mahali popote maishani mwake alikowahi kupata furaha zaidi ya wakati akiishi na wazazi wake, maisha yalikuwa yamejaa huzuni na machozi, kwa mara nyingine akafikiria kufa kama alivyokuwa amefikiria kuwaua Grace na Gerald chumbani siku za nyuma kisha yeye mwenyewe kujitoa uhai.



“Bora nisage chupa, ninywe nife niachane na hii dunia iliyojaa mateso!” Akawaza kisha kunyanyuka kitandani na kuanza kutembea kuelekea jikoni ambako aliwasha taa na kuchukua chupa ya cocacola iliyokuwa juu ya kabati, akaipiga chini mpaka ikavunjika kisha kuchukua vipande vyake na kuanza kusaga.

Alikuwa na uhakika kabisa Gerald alikuwa amesikia sauti ya chupa ikivunjika lakini hakutaka kumfuatilia ili kufahamu nini kilikuwa kinaendelea! Hapakuwa na mapenzi tena kati yao, bila shaka Gerald alikuwa amefika alikokuwa akielekea, baada ya kumtumia Blandina kama ngazi hivyo hata kama angekufa yeye isingemuumiza moyo, hivyo ndivyo alivyowaza muda wote akisaga vipande vya chupa mpaka vikalainika kabisa kisha kuviweka ndani ya glasi, akaweka maji na kukoroga.



“Mungu nisamehe…!” Alitamka maneno hayo akinyanyua glasi, alipoifikisha tu mdomoni na kugusa mdomo wake wa chini, picha ikamwijia kichwani mwake akaikumbuka sababu iliyomfanya asimuue Grace chumbani; mtoto! Alikuwa na kichanga tumboni mwake, ambacho hakikuwa na hatia yoyote wala hakikukufahamu ni kitu gani kilikuwa kikiendelea duniani.



Mawazo hayo yalimfanya Blandina ashushe glasi chini na kutembea hadi kwenye sinki la maji akilia kwa uchungu, akamwaga vipande vya chupa kwenye sinki na kuisafisha glasi kisha akaamua kurejea tena hadi chumbani ambako alimkuta Gerald amejilaza kitandani, kama alivyosema mwanzo aliendelea kumsisitizia kuhusu kuitoa mimba na Blandina alikataa kata kata.



“Shauri yako, mimi usiniambie kitu chochote juu ya mimba wala mtoto atakayezaliwa, siwezi kuwa na mtoto ambaye sina uhakika kama ni wangu!” Gerald alitamka maneno hayo, kifupi alikuwa amesahau kabisa wema wote aliotendewa na mwanamke aliyekuwa akimlaumu na kumuumiza moyo usiku huo na kwamba ni yeye ndiye aliyesababisha mimba hiyo itokee, katika tamaa yake ya kutafuta cheo.



“Sawa tu Gerald, endelea kuninyanyasa, mimi namwachia Mungu, I have done my best, so I leave the rest for God!” Aliongea Blandina kwa sauti ya kutia huruma akimaanisha alikuwa amejitahidi kadri ya uwezo wake na sasa alikuwa anaacha kila kitu mikononi mwa Mungu.



***

Hawakuongea tena kitu chochote cha maana kuanzia siku hiyo, kama kuna kitu kilisemwa basi ilikuwa ni kuuliza swali na mwingine kujibu. Kila siku iliyokuja na kupita Gerald alikuwa amevimba kwa hasira na kumfanya maisha ya Blandina ndani ya nyumba yaendelee kuwa magumu. Alitamani awe na mahali pa kwenda lakini hapakuwepo, asingeweza kwenda kwa shangazi yake tena akiwa mjamzito, aliifahamu vizuri familia yake na misimamo waliyokuwa nayo.



Aliahidi kuvumilia mpaka mwisho akiamini lazima siku moja Gerald angeamka akiwa ameingiwa na huruma kidogo baada ya kuelewa mkewe hakuwa na kosa lolote. Haikuwa hivyo, Gerald aliendelea na tabia yake mbaya na kwa sababu alikuwa amepandishwa cheo, sasa alikuwa na safari nyingi ndani na nje ya nchi, hakujali kumuaga mke wake alipotakiwa kusafiri. Moyo wa Blandina ulizidi kuuma lakini bado aliendelea kuvumilia.



Mpaka miezi sita baadaye, uhusiano wao ndani ya ndoa ulikuwa bado mbaya kupita kiasi, alichofanya Gerald ni kuacha fedha ya matumizi juu ya meza kila siku au ilipotoka akawa anasafiri alimtuma dereva wa kampuni kumpelekea Blandina fedha nyumbani. Hiyo ndiyo ilikuwa dalili kwamba mume alikuwa amekwenda safari, wakati mwingine hakurudi nyumbani kabisa hata kwa wiki nzima ingawa mimba ilikuwa imemdhoofisha sana mke wake.



Uchungu ulipompata Blandina, Gerald hakuwepo nyumbani na wala hakuelewa wapi alikokuwa. Ni majirani waliomchukua na kumkimbiza hadi hospitali ya TMJ huko Mikocheni ambako yeye na mume wake walilipiwa gharama za matibabu na kampuni. Alipokelewa vizuri na wauguzi, akashughulikiwa kama ilivyopaswa na baadaye kupelekewa chumba cha kujifungulia.



“Umesema mume wako ni nani?”

“Gerald!”

“Gerald Lutta?”

“Yule Mkurugenzi msaidizi?”

“Ndio!”

“Yuko wapi?”

“Safarini!” Ingawa hakuwa na uhakika wa mahali alikokuwa Blandina alijikuta akitamka neno hilo.

Kwa saa karibu sita alilala kwenye chumba cha kujifungulia akisubiri uchungu wake ukamilike, alipofika alitegemewa kujifungua baada ya saa kama mawili lakini iliwashangaza Wakunga saa sita zilipotimia, njia ilikuwa wazi lakini mtoto alikuwa hatoki! Ilibidi daktari aitwe kuja kumpima.

“Kichwa kiko hapa karibu, chupa imekwishapasuka, nashindwa kuelewa ni kwanini mtoto hatoki? Nahisi huyu mama ana CPD!”

“Unamaanisha nini daktari?”

“Namaanisha Cephalo Pelvic Dispropotion!”

“Unamaanisha nini daktari?” Mmoja wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Afya Muhimbili aliyekuwa chumbani hapo aliuliza.

“Nyonga na kichwa cha mtoto haziwiani, inawezakana kabisa kichwa cha mtoto huyu ni kikubwa sana!”

“Tufanye nini sasa?”

“Hakuna kitu kingine zaidi ya kumpeleka chumba cha upasuaji, anahitaji kufanya Caesarian Section haraka iwezekanavyo kama tunataka kuokoa maisha yake na mtoto!” Dk. Aliongea akimshuhudia Blandina akihangaika na maumivu makali kitandani.

Ilikubalika apelekwe chumba cha upasuaji, hivyo maandalizi yakaanza kufanyika na saa moja na nusu ya asubuhi alipakiwa kwenye machela akapelekwa chumba cha upasuaji ambako madaktari walikuwa wakimsubiri, hali yake ilikuwa mbaya, mwili haukuwa na nguvu, sababu ya kujaribu kusukuma mtoto kwa muda mrefu.

*****

Ilikuwa inauma mno, kwake maisha yalikuwa kama ndio yanafikia mwisho! Blandina alihisi kusalitiwa, kunyanyaswa na kuonewa katika dunia ambayo Mungu alimweka ndani yake ili afaidi maisha. Alijilaumu yeye mwenyewe kwa yote yaliyotokea, wakati kama huo aligundua umuhimu wa wazazi wake, akaelewa kumbe hakutakiwa kukosana nao na mwisho kupoteza baraka alizostahili, machozi yalimbubujika kupitia pembeni mwa macho yake akiingizwa chumba cha upasuaji, mwili wake haikuwa na nguvu kabisa, hakuwa hata na uwezo mdogo tu wa kusukuma mtoto aliyekuwemo ndani yake, mtoto wa aidha Adebayor au Gerald.



“Msogezeni huku!” Blandika alisikia sauti hiyo ikisema pembeni mwake lakini hakumwangalia aliyetamka maneno hayo ni nani, alichohisi ni kwamba mtu huyo alikuwa daktari na wauguzi wakafanya kama walivyoagizwa mpaka Blandina akapandishwa juu ya kitanda cha upasuaji, daktari akaanza kumpima kwa kutumia vidole vyake vilivyovishwa mipira kuona kama mlango wa uzazi ulikuwa umefunguka au la!

“Vipi?” Daktari mwingine aliuliza.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Mlango uko wazi sentmita kumi na nimekigusa kichwa ingawa hakijashuka sana na kinaonekana kuwa kikubwa kuliko kawaida!” Dk. Masawe bingwa wa upasuaji wa akinamama aliongea.

“Sasa?”

“Au tujaribu vacuum extraction?” Dk. Simbakalia, bingwa mwingine wa masuala ya wanawake aliyekuwepo chumba cha upasuaji aliongea.

“Vaccum haiwezekani, kama kichwa hakijashuka itakuwa si rahisi cap kukikamata kichwa, mimi nafikiri hapa hakuna jingine tunaloweza kufanya isipokuwa upasuaji!”

“Sawa, basi tuingie kazini!” Dk. Masawe aliongea.

Blandina alianza kuandaliwa, kwanza tumbo lake lilisafishwa kwa dawa ya kuua wadudu iitwayo Iodine, kazi hiyo ilipokamilika akafunikwa vizuri na nguo za kijani zitumikazo chumba cha upasuaji, safi zisizo na vimelea vya wadudu! Kichwa peke yake na sehemu ya mbele ya tumbo ndio iliachwa wazi, taa kubwa iliyokuwa juu ikashushwa na kumulika sehemu iliyotakiwa kupasuliwa. Kitu kama kikombe chenye bomba kikaletwa na kuufunika mdomo na pua ya Blandina.

“Vuta pumzi kwa nguvu!” Muuguzi akamwambia Blandina ambaye aliendelea kuvuta hivyo mara kadhaa.

“Umeolewa?”

“Ndio!”

“Na nani?”

“Gerald!”

“Unampenda?”

“Sa…na lak…ini kani….umi…za!” Aliongea kwa taabu tayari fahamu zilishaanza kupotea, mwisho hakuweza kujibu swali kabisa, muuguzi akaachana naye tayari kwa kuanza kazi.

Madaktari walishajiandaa vizuri kwa kufanya kitu kiitwacho Scrubbing, yaani kuisugua mikono yao vizuri kabla ya kuvaa mipira na nguo salama, walikuwa wakisubiri Blandina apoteze fahamu tu waanze kazi. Hilo lilipotokea hawakuwa na jambo jingine la kufanya isipokuwa kukamata mikasi yao na kuanza kulipasua tumbo lake wakipita kwenye kuta za mbele mpaka wakaufikia mfuko wa uzazi na kuupasua pia, wakaingia hadi ndani ambako walikuta mtoto akiwa mzima.

“Mh!” Dk. Simbakalia aliyekuwa akifanya upasuaji huo kwa kusaidiwa na Dk. Masawe aliguna kwa sauti ya juu, wenzake wote wakashtuka.

“Vipi?”

“Ndio sababu, huyu mtoto asingepita, uliposema ni CPD nilitilia mashaka sasa nimeamini, jamani huyu mtoto ni Malformed, ameharibika, nafikiri mama yake alikunywa madawa fulani akiwa mjamzito, masikini hebu mwoneni macho yake makubwa kuliko kawaida, kichwa chake masikini, kikubwa mno na kina mabonde! Haaa! Hana masikio wala pua, atakuwa mtoto gani jamani huyu? Mama yake atamkubali kweli? Inabidi awe na moyo sana” Dk. Simbakalia aliongea kwa huzuni, yeye mwenyewe alikuwa mwanamke alielewa uchungu wa kuzaa mtoto mwenye ulemavu, kwa mara ya kwanza katika maisha yake ya kazi alihisi machozi yakitaka kumtoka.

Operesheni hiyo iliyochukua muda wa saa mbili, ilimalizika kwa mafanikio makubwa, pamoja na mtoto kuwa na hali ya udhaifu lakini alikuwa mzima na alilia vizuri kama ilivyo kwa watoto wa kawaida, akakimbizwa haraka kwenda chumba cha hewa ya oksijeni ambako aliendelea kutunzwa na kulishwa! Wakati mama yake akiwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi.

Saa kumi na mbili baadaye Blandina alizinduka kutoka katika usingizi mzito aliolala, ambao ulisababishwa na dawa aliyopewa katika chumba cha upasuaji. Kitu cha kwanza alichoulizia ni mtoto wake, wauguzi wakamwangalia kwa macho ya mshangao, walishamwona mtoto, walielewa ni kiasi gani angeumia baada ya kumwona! Kwa muda walibaki kimya wakitafakari nini cha kumwambia.

“Jamani mwanangu yuko wapi? Mbona hamnijibu? Kafa? Au baba yake kamuua?”

“Hapana dada, yupo!”

“Wapi?”

“Chumba cha watoto mahututi!”

“Mh! Kwani ana matatizo gani?”

“Sio matatizo makubwa!”

“Nipekelekeni nikamwone mwanangu, mwanangu peke yangu, asiye na baba!”

“Huwezi kutoka kitandani sasa hivi, hali yako sio nzuri!”

“Hapana, nipelekeni!”

“Haiwezekani dada, bado tumbo lako halijapona vizuri, au umesahau kwamba umefanyiwa upasuaji?”

“Nakumbuka!”

“Sasa?”

“Mpaka lini nitamwona?”

“Vumilia kidogo!”

“Baba yake kashakuja?”

“Hapana!”

“Jamani mpigieni simu angalau aje, nahisi atakuwa tayari kumkubali!”

“Namba yake?”

“0750111222!”

“Wacha nitumie simu yangu!” Muuguzi mmoja aliongea, wote walikuwa tayari kumsaidia, walimwonea huruma na hata alipowaangalia machoni aliligundua jambo hilo ingawa hakuelewa ni kwa sababu gani.

Simu ikapigwa, kwa maongezi aliyoyasikia Blandina kupitia kwa muuguzi, alielewa wazi Gerald alikuwa amekataa kwenda hospitali kumwona mtoto! Muuguzi alimbembeleza kwa muda lakini mwisho simu ilikatika, kila mmoja akaelewa ilikuwa imekatwa, Gerald hakumuhitaji mtoto huyo.

“Mh!” Aliguna muuguzi aliyekuwa akiongea kwenye simu.

“Vipi dada kasemaje?”

“Amebanwa kidogo ofisini atakuja baadaye, amesema nikupe pole na anakupenda!”

“Dada mbona unanifanya mimi mtoto mdogo?” Blandina aliongea, alishaelewa kilichokuwa kikiendelea, muuguzi alikuwa akijaribu kumfariji ili asichanganyikiwe zaidi.

Kwa wiki nzima alibaki kitandani bila kumwona mtoto wake, hamu ikazidi kuongezeka, kitu pekee alichoambiwa ni kwamba mtoto alikuwa mzima na hali yake ilikuwa ikiendelea vizuri, hakuna aliyediriki kumweleza wazi juu ya maumbile mpaka siku ya saba muuguzi alipoingia chumbani kwake akiwa amebeba mtoto mkononi, kitu cha kwanza alichokiona ni kichwa kikubwa, kwa sababu kulikuwa na akinamama zaidi ya wanne ndani ya chumba hicho, hakuwaza kabisa kuwa mtoto huyo alikuwa akipelekwa kwake.





Blandina amejifungua mtoto mwenye maumbile yasiyo ya kawaida, aliumia akiwa tumboni mwa mama yake! Kihistoria mimba ya mtoto huyo ilipatikana baada ya mumewe (Gerald) kumtoa bila hiari yake (Blandina) afanye mapenzi na bosi wake ili aweze kupanda cheo na baadaye mimba hiyo kupatikana uhusiano ndani ya nyumba ukaharibika kabisa ingawa kweli Gerald alipanda cheo ofisini na kuwa Mkurugenzi Msaidizi.

Hamtaki tena mkewe, anahangaika na mimba na hatimaye amejifungua mtoto mwenye maumbile yaliyoharibika. Je, nini kitafuata? Endelea…



Maumbile ya mtoto huyo yalimshangaza Blandina, katika maisha yake hakuwahi hata mara moja kumwona mtoto mwenye sura mbaya kiasi hicho! Aliamini hakuwa wake, pengine alikuwa akipelekwa kwa mmoja wa akina mama waliokuwa ndani ya chumba hicho. Cha kushangaza muuguzi aliwapita wengine wote na kunyoosha moja kwa moja hadi kwenye kitanda chake na kumlaza mtoto huyo kitandani, Blandina akiwa ameshika mikono yake kichwani kwa mshangao na machozi yakimlengalenga, ilikuwa ni kama ndoto ya kutisha, katu huo usingeweza kuwa ukweli, ulimi wake ulikuwa umenasa chini yam domo, hakuweza kusema chochote. Alihisi adhabu zinazidi kumwandama.

“Pole dada, usiumie sana kwani Mungu aliyeruhusu jambo hili litokee, anaielewa sababu!”

“Ahsante!”

“Nakusishi umependa mtoto wako, huyu ni mwanao wala usidiriki kumfanyia kitu chochote kibaya, umeokoka?”

“Hapana, mimi ni Mwislamu!”

“Mbona unaitwa Blandina?”

“Nilibadili dini ili niolewe, sijawahi kujisikia Mkristo hata siku moja, jina langu naitwa Halima!”

“Pole Halima, simama imara!”

“Ahsante! Nitamthibitishia Mungu kwamba ninaweza na hakufanya makosa kunipitisha katika mtihani huu, haya ni mapito tu dada na nitashinda!” aliongea Blandina akainama na kumbeba mtoto wake mkononi, hata hivyo hakuweza kabisa kufanya machozi yasibubujike, aliendelea kulia kwa uchungu akikumbuka njia yote aliyopita maishani mpaka kufika mahali alipokuwa, hakuwa na kumbukumbu ya aina yoyote ya kufurahia maisha, kwake ilikuwa ni hili, baadaye lile! Machozi na vilio havikukatika.

Muuguzi hakuongea kitu zaidi akaaga na kuondoka, alipofunga mlango nyuma yake, akina mama wengine wote waliokuwemo wodini walinyanyuka kwenye vitanda vyao kwenda kitandani kwa Blandina na kuanza kumpa pole! Hao ndio walimzidishia uchungu na kumfanya azidi kububujikwa na machozi, hisia za uchawi zikaanza kumwingia, kwamba pengine wazazi wake walimfanyia kitu cha kishirikina ili ateseke baada ya kuwaasi, hilo likazama kichwani mwake.

“Usijali shoga, hata sisi hatujui watoto tutakaoletewa wakoje, asiwepo mtu wa kukushawishi kumuua mtoto wako!’ Mmoja wa wanawake hao alisema akimtolea mfano wa mwanamke aliyezaa mtoto Albino na kuamua kumuua, aliposhika mimba akazaa tena mtoto wa aina hiyo hiyo.

“Siwezi kufanya hivyo, nampenda sana mwanangu!”

“Baba yake yuko wapi?”

“Amesafiri!”

“Ana habari juu ya jambo hili?”

“Ndio!”

“Hatujamwona akija hapa lakini?”

“Kwa sababu yuko safarini!”

“Mnaelewana ndani ya nyumba?”

“Tunapenda mno!” Blandina alidanganya, hakutaka kila kitu maishani mwake kifahamike kwa watu ambao wala hakuwa na uhusiano nao.

Kwa mara ya kwanza akamnyonyesha mtoto wake, pamoja na maumbile aliyokuwa nayo alikuwa mtoto mwenye nguvu kwani alinyonya bila matatizo yoyote mpaka akashiba kabisa. Nusu saa baadaye, muuguzi alirejea na kumchukua kumrejesha kwenye chumba cha watoto waliozaliwa na matatizo, Blandina alitaka kumkatalia lakini baada ya kueleweshwa aliruhusu mtoto achukuliwe.



****



Hayo ndiyo yakawa maisha ya Blandina wodini, mtoto aliletwa kwake mara nane katika masaa ishirini na nne kunyonya, hiyo ikiwa ni kila baada ya saa tatu! Upendo kwa mtoto wake ukaanza kuongezeka, hakujali kabisa Gerald angemchukuliaje, hata kama angemkataa kama alivyotamka mwanzo yeye angeendelea kumpenda, kumtetea na kumlinda siku zote za maisha yake. Suala la nani alikuwa baba wa mtoto huyo halikumuumiza moyo, ilimradi alikuwa kiumbe hai. Kichwani mwake wazo la kumtafuta Adebayor wala halikumwingia, mtu aliyefanya naye ngono siku moja, tena kwa kuuzwa na mume wake mwenyewe, hakustahili kuwa baba wa mtoto wake. Blandina alikuwa tayari kumlea mwanae na baadaye kuja kumwambia, baba yako alikufa katika ajali ya gari kuliko kumpeleka kwa Adebayor.

Wiki ya kwanza ikakatika, hatimaye ya pili na ya tatu mpaka mwezi mmoja ukatimia bila Gerald kuonekana wodini wala kujaribu kuwasiliana naye. Alikuwa na uhakika kabisa taarifa alishazipata, kwani marafiki zake walipokuja wodini aliwatuma kumfikishia ujumbe. Roho ilimuuma lakini hakuwa na jambo la kufanya, ilibidi awe mvumilivu, kilichomfurahisha zaidi mtoto wake alikuwa akiendelea vizuri, hakuwa na matatizo yoyote zaidi ya maumbile mabaya jambo ambalo halikumsumbua tena, mapenzi mazito sana yalishaanza moyoni mwake.

“Genesis njoo unyonye mwanangu, mimi ndiye baba na ndiye mama yako, sitakudhuru, sitakuumiza na nitakuwa nawe hadi mwisho, nakupenda na ninamshukuru Mungu kwa kuniamini na kunikabidhi mtoto kama wewe, nitamthibitishia kwamba ninaweza!” Alisema maneno hayo akimnyanyua mwanae, hilo ndilo jina alilompa mara tu baada ya kumwona.

Muuguzi alimshangaa lakini wote walishamzoea, Blandina alikuwa kama hana akina sawasawa lilipokuja suala la mtoto wake, alionyesha mapenzi ya ajabu ambayo akinamama wengi hawakuyategemea. Baadhi walifikiri angemfunika usiku na mto wa kulalia angalau afe ili apange kupata mtoto mwingine lakini haikuwa hivyo, hili liliwafanya wauguzi wampende Blandina kuliko kawaida. Wakati anamnyonyesha ghafla mlango wa chumba ulifunguliwa, alijua lazima huyo alikuwa mgeni wake kwani chumbani alishabaki peke yake, akaingia kijana mweusi mrefu, mkononi akiwa na bahasha nyeupe.

“Shikamoo!” Alimwamkia Blandina na baadaye muuguzi aliyekuwa amesimama pembeni

“Marahaba hujambo?”

“Sijambo, bila shaka wewe ni Blandina au Halima?”

“Ndio!”

“Nimetumwa nikuletee hii barua!”

“Na nani?”

“Gerald!”

“Ahsante!” Blandina aliipokea kwa mkono wa kulia akiwa amempakata mtoto wake huku mwili wote ukitetemeka, alihisi kilichokuwa ndani ya bahasha hiyo ni kitu cha kumuumiza zaidi, akatamani kuiweka mdomoni na kuitafuna lakini upande mwingine wa ndani wa moyo wake ukamwambia aisome.

Muuguzi alipoondoka na mtoto, Blandina akajikakamua na kuifungua bahasha hiyo, kulikuwa na karatasi nyeupe iliyoandikwa kwa wino mwekundu, kabla ya kuisoma aliutambua mwandiko, ni kweli ulikuwa ni wa Gerald! Moyo ukaanza kumwenda mbio akizidi kuikunjua karatasi hiyo mpaka akaiona anwani, jina la Gerald liliandikwa upande wa kulia wa karatasi hiyo.



Halima,http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Nimelazimika kukuita Halima leo kwa sababu tangu unapoisoma barua hii wewe si Mkristo tena, uliingia katika dhehebu hili kunitafuta mimi ambaye hivi sasa nimeamua kukuacha! Kifupi nimesikia habari ya mtoto uliyejifungua, anatisha! Mtoto mwenye sura mbaya kiasi hicho unataka kumpeleka wapi? Kwanini usimuue?

Binafsi nimeamua kuangalia ustaarabu mwingine wa maisha, wewe baki na hicho kinyago chako! Nakushukuru sana kwa yote uliyonitendea, najua ulinipa figo yako na bila wewe ningekuwa marehemu, kwa hilo niko tayari kukulipa shilingi milioni kumi na tano ili tuachane kwa amani.

Kwa haya niliyoyasema, naomba uelewe kwamba hutakiwi kufika nyumbani kwangu wakati wowote ukitoka hospitali, tafuta maisha sehemu nyingine! Kama ni fedha zako niambie nikuwekee katika akaunti gani.

Ni mimi,

Gerald.



Ilikuwa ni shida kuvumilia barua ya namna hiyo, uchungu alioupata Blandina ulikuwa mkubwa mno, alihisi moyo wake ukitaka kupasuka! Filamu aliyozoea kuiona kila siku juu ya wema aliomtendea mwanaume hiyo ilianza kucheza tena ubongoni mwake, akauona mpaka uhusiano na wazazi wake, machozi yakambubujika. Alishazoea kulia lakini siku hiyo alilia kwa aina tofauti, mwisho fahamu zikampotea na kuendelea hivyo kwa muda mpaka alipozinduliwa na muuguzi aliyekuwa akiwaga chakula, tayari ilishagonga saa nane ya mchana.

“Karibu chakula Blandina!”

“Ahsante sista, leo sitakula!”

“Kwanini?”

“Basi tu najisikia nimeshiba!”

“Jaribu hata kidogo, leo tumepika ndizi!”

“Sawa, lakini sijisiki kula!”

“Mbona unabubujikwa na machozi?”

“Mafua!”

“Haya ahsante!”

Muuguzi akaondoka na kumwacha Blandina peke yake akiendelea kuisoma barua hiyo mara kadhaa bila kuamini alichokuwa akikiona kwa macho yake, hatimaye nusu saa baadaye akaamua kuikunja na kuiweka chini ya mto akiwa ameahidi moyoni mwake angeitunza barua hiyo ili aje kumpa mtoto wake akikua na kuwa mtu mzima ili aelewe mama yake alipita katika mazingira magumu kiasi gani. Saa nzima baadaye alishtuliwa akiwa katikati ya mawazo na mlango ulipofunguliwa, muuguzi akaingia akiwa na mtoto.



“Balozi Blandina! It is nyonyesha time!” muuguzi aliongea kwa utani. Walimwita Balozi kwa sababu ya kukaa wodini muda mrefu.

Akanyanyuka na kumpokea mtoto wake, alipomwangalia machozi yalimtoka tena, alielewa kazi ngumu kiasi gani ilikuwa mbele yake katika malezi ya mtoto huyo lakini akauahidi moyo wake kwamba angefanya kila kilichowezekana katika kuhakikisha Genesis anakua, hata kama kungekuwa na matatizo makubwa kiasi gani katika safari hiyo.

Akamnyonyesha kwa mapenzi yote na mwisho akamlaza kitandani, hakuwa tayari kumrejesha tena kwa muuguzi, alitaka akae naye mpaka siku iliyofuata. Hilo halikuwa jambo la kuamua mtu mmoja ingawa hali ya Genesis haikuwa mbaya sana, ilibidi daktari wa watoto atafutwe na alipokubali ndipo ombi la Blandina likakubaliwa, Genesis akaachwa chumbani kwake.

Siku iliyofuata saa nne na nusu asubuhi daktari aliingia chumbani akiongozana na kundi la wauguzi na madaktari wengine, wakaingia moja kwa moja hadi kitandani kwa Blandina, walimkuta amelala mtoto akiwa pembeni mwake, uso ukiwa umejawa na huzuni. Hata hivyo alimudu kunyanyuka na kuketi kitako.

“Blandina, habari za asubuhi?” Dk. Simbakalia alisema.

“Nzuri shikamoo daktari!”

“Marahaba hujambo? Nimekuletea habari njema!”

“Habari gani tena?”

“Leo unakwenda nyumbani!”

Tofauti kabisa na alivyotegemea daktari kwamba Blandina angefurahia taarifa hiyo, alimwona anainamisha kichwa chini kama mtu mwenye mawazo, kichwani mwake hakuna alichokifikiria zaidi ya kumbukumbu ya barua ya Gerald kwamba akitoka hospitali asiende nyumbani kwake. Alishazoea kukaa wodini na kupaona kama nyumbani kwake, alitamani kubaki hapo hapo mpaka mtoto wake akue lakini lilikuwa ni jambo lisilowezekana.

“Mbona umebadilika?” Daktari aliuliza.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Hapana niko vizuri!” Hakutaka kuonyesha matatizo yake.

“Haya, kwa sababu mtoto wako ana nafuu sasa, nakushauri uende nyumbani na utarudi baada ya mwezi mmoja, tutakupatia dawa za kutosha kutumia katika kipindi hicho!”

“Ahsante daktari, nashukuru kwa kila kitu, bila wewe ningekufa na pengine mwanangu pia asingekuwepo, nitakukumbuka kwa wema wote ulionitendea, sina cha kukulipa!” Blandina aliongea kwa sauti ya chini, hakutaka kabisa kulia wala kuonyesha udhaifu wa aina yoyote.

Mchana wa siku hiyo hiyo baada ya kupewa kila kitu, alikusanya mizigo yake na kutoka wodini hadi nje ambako alisimama na kutafakari wapi pa kwenda! Kulikuwa na sehemu tatu angeweza kuelekea, kwa wazazi wake Kilosa, kwa shangazi yake Mikocheni na nyumbani kwake ambako Gerald alimwambia asiende. Baada ya kutafakari kwa muda hatimaye alifikia uamuzi wa kwenda nyumbani kwake, kwa msaada wa fedha kidogo alizochangiwa na wauguzi alikodisha teksi iliyompeleka moja kwa moja hadi mbele ya lango la kuingilia nyumbani kwake, mwili wote ukitetemeka utafikiri alikuwa akiingia kituo cha polisi.

Akasukuma lango na kuingia ndani na kutembea hadi mlangoni, kabla hajafungua alishangaa kuona mlango unafunguliwa na mtoto mdogo akitambaa akatokeza, alipomwangalia mtoto huyo alifanana kabisa na Gerald, moyo wake ukapiga kwa nguvu, hakuhitaji jibu juu ya hilo, alikuwa mtoto wa mume wake! Akamkwepa na kuingia ndani, Gerald na Grace walikuwa wamelala kwenye kochi wakiwa wamekumbatiana.

“Na wewe? Ulisahau nini chako hapa?” ilikuwa ni sauti ya Gerald.

Blandina akaikumbuka figo yake.

****

“Gerald!”

“Yes!”

“Why are you doing this to me? Cant you have mercy? Cant you look back and see the goodness I did?” (Kwanini unanifanyia hivi? Huwezi kunihurumia? Huwezi kuangalia nyuma na kuona wema niliokutendea?)

“I don’t care, that is just history!” (Sijali, hiyo ni historia tu!)

“History?” (Historia?)

“Yes! Mrs Adebayor!” (Ndio! Bibi Adebayor!) badala ya Gerald kujibu, Grace akafungua mdogo wake na kutamka maneno ya kuumiza, tayari alishasimulia kila kitu! Blandina alihisi kupasuka kwa hasira, akamlaza mtoto kwenye kochi huku akitetemeka na kuanza kumfuata Grace tayari kwa kupambana, maneno aliyoambiwa yalikuwa yamemchoma moyoni kama mkuki wa moto.

“Shut up! You prostitute!” (Funga domo lako Malaya wewe!) alifoka Grace akisogea kwenye kochi walilolalia lakini kabla hajafanya lolote lile, Gerald alishanyanyuka akamkamata na kumsukuma hadi sakafuni. Akaenda kwenye kochi na kumnyanyua mtoto kisha kuanza kutembea naye kwenda nje kama vile anakwenda kumtupa, Blandina hakuweza kuvumilia wala hakutaka tena kupambana Grace, mtoto wake Genesis alikuwa kitu cha kwanza maishani, akaanza kukimbia akimfuata Gerald.

“Nipe mwanangu!”

“Chukua na uondoke!”

“Gerald, unamwogopa Mungu?”

“Ahaa! Usiniletee mambo ya dini hapa, utajua wewe mwenyewe na Mungu wako, niondolee huyu mtoto kwenye nyumba yangu mpeleke kwa Adebayor!”

“Sawa lakini nataka kukuambia kitu kimoja kwamba, sijali sana nani ni baba wa mtoto huyu, unaweza kuwa wewe au Adebayor maana sina uhakika lakini kumbuka kitu kimoja kwamba mimi sikuwahi kumfahamu Adebayor kabla, ni wewe ndiye ulikwenda kuniuza kwake! Leo hii unanitenda mambo haya, Gerald unatakiwa kukumbuka tulikotoka, hivi sasa mimi sina ndugu duniani zaidi yako, umenikosanisha na wazazi wangu sababu tu niliamua kukupa figo yangu na mwisho nikabadili dini na kuwa Mkristo kwa sababu yako jambo ambalo lilinitenganisha kabisa na wazazi wangu, nihurumie, tafadhali nihurumie, niache nikae hapa ndani hata kama na Grace atakuwepo!”

“Hahaaa!Haaaah! Yaani mimi nioe wanawake wawili? Mimi sio Mwislam…!”

Kabla hajamalizia sentensi yake, mlango ulifunguliwa na Grace akatokeza na kuanza kumvuta Gerald kuingia ndani! Haikuwa rahisi kuamini kwamba watu hao waliwahi kuwa marafiki wakubwa lakini sasa walikuwa wakigombana. Mlango ukabamizwa na baadaye kufungwa, ulipofunguliwa sekunde chache baadaye, mfuko wenye nguo za Blandina pamoja na masanduku ya nguo zake nyingine yalikuwa yakitupiwa nje.

Blandina hakuweza kuvumilia kilichokuwa kikitokea, machozi yakamtoka, kwa uchungu akapiga magoti chini akiwa na mtoto wake na kuanza kusali akimwomba Mungu amsaidie kupita katika wakati mgumu uliokuwa mbele yake, dunia nzima ilikuwa imemgeuka na hakujua kosa lake lilikuwa ni nini. Hata mara moja hakutaka kumlaumu Mungu kwa yote yaliyokuwa yakitokea, aliamini ni mapito mbele ya safari kulikuwa na mapumziko.

“…nisaidie Eee Mungu, niweze kusimama imara, pamoja na mateso yote ninayoyapata kitu kimoja tu naahidi siwezi kufanya; kumuua mwanangu Genesis, nampenda mno, niko tayari kwa jambo lolote lakini awe hai kwani hana hatia..” alisema Blandina katika sala yake.

Hakutoka mahali hapo kwa sababu hakuwa na mahali pa kwenda, akaendelea kuketi peke yake akilia mwisho alipochoka akajilaza pembeni mwa mizigo yake! Haikuwa rahisi kuamini mwanamke huyo alikuwa na digrii kichwani mwake. Saa mbili ya usiku ilipogonga, mlango ulifunguliwa, Grace na Gerald wakatoka wakiwa na mtoto wao, wamependeza na kunukia manukato. Wala hawakujali kulikuwa na mtu kwenye veranda, walikwenda moja kwa moja hadi kwenye gari, wakapanda na kuondoka zao, kicheko kikimfikia Blandina aliyekuwa amekaa akimnyonyesha mtoto wake.

“Tunaacha lango wazi, ukiamua kuondoka utaondoka!” ilikuwa ni sauti ya Gerald akirudishia lango baada ya kutoa gari, kilichofuata ni muungurumo wa gari likitokomea! Blandina alielewa kabisa walikuwa wakienda wapi maana hiyo ilikuwa ni kawaida ya familia yao, kwenda kula chakula cha usiku kwenye mgahawa wa Alcove katikati ya jiji la Dar es Salaam mtaa wa Samora.

Blandina alibaki hapo akitafakari nini cha kufanya, ilipotimu saa nne ya usiku alihisi njaa kali. Hakuona tena sababu ya kuendelea kubaki eneo hilo, akanyanyuka taratibu akiwa na mfuko wenye nguo za mtoto peke yake na kutembea hadi langoni ambako alitoka na kuanza kutembea hadi stendi ya teksi.

“Wapi dada?”

“Mikocheni!””Mikocheni gani?”

“Kwa Nyerere!”

“Shilingi mia tano!”

“Sawa twende! Nitakwenda kulipa huko huko”

Hatimaye baada ya kuwa amewaza sana, Blandina aliikosa sababu ya kuendelea na mateso aliyokuwa nayo wakati ndugu zake walikuwepo tena wakiwa na uwezo mkubwa kifedha. Sasa alikuwa ameamua kwenda kwa shangazi yake usiku huo huo, kuomba msamaha kwake halikuwa tatizo tena! Ilikuwa ni lazima arejeshe uhusiano mzuri na familia yake lakini kwa mtoto aliyekuwa naye hakuwa na uhakika kama angesamehewa, hata hivyo alikkuwa tayari kujaribu.

“Mtoto anaumwa?” Dereva aliuliza.

“Ndio!”

“Pole sana!”

“Ahsante!”

“Unakwenda kwa nani?”

“Kwa shangazi yangu!”

“Na huku umetokea wapi?”

“Nyumbani kwangu!”

“Baba wa mtoto yuko wapi?”

“Amesafiri!” hakuwa na jinsi zaidi ya kudanganya.

“Mtoto wako anaumwa sana lakini atapona, usiwe na wasiwasi, Mungu anaweza!”

“Najua, umeokoka?”

“Ndio!”

“Wewe?”

“Hapana!”

“Inabidi ufanye hivyo!”

“Nitalifikiria jambo hilo!”

“Simama hapo!” Alimwambia dereva walipofika mbele ya nyumba ya shangazi yake, ilikuwa kubwa ya kifahari.

Iliposimama Blandina alishuka na mtoto wake pamoja na mfuko wa plastiki aliokuwa nao na kusogelea lango, akabonyeza kengele na mlango ukafunguliwa, mlinzi wa Kimasai akachungulia. Alikuwa ni yule yule aliyemzoea.

“Mama yeyoo, jambo?”

“Sijambo, shangazi yupo?”

“Iko, lakini …!”

“Lakini nini Yero?”

“Iliambia mimi wewe ikija hapana ingia ndani!”

“Unasema?” Ingawa alikuwa amesikia, Blandina hakuyaamini masikio yake.

“Ilisema wewe hapana ingia hapa, kisa haribu mambo, wewe siku hizi eti Kristu!”

“Mh! Yumo lakini?”

“Iko!”

“Niitie!”

“Subiri hapo nje!” Masai aliongea na kufunga lango, kisha nyayo zake akitembea kuelekea ndani zilisikika.

Haukupita muda mrefu sana nyayo za watu wawili wakitembea kuelekea langoni zikafuatia, Blandina alikuwa akitetemeka mwili wote, hakutaka kabisa kuyachukua maneno aliyoambiwa na Masai kama ukweli, lakini hakuelewa shangazi yake angemwambia kitu gani. Lango likafunguliwa, shangazi yake amesimama mbele uso ukiwa umekunjwa.

“Umenilea matatizo au mjukuu?”

“Shangazi naomba tuingie ndani tuongee”

“Haiwezekani, mpaka uyamalize kwanza na kaka ndipo naweza kukuruhusu! Kaka Abdallah ataniua”

“Shangaziiii, naomba!”

“HAIWEZEKANI, MASAI FUNGA LANGO TULALE!”

****

Kilichokuwa kikimtokea Blandina kilikuwa ni kama hadithi ya kutunga, mambo aliyozoea kuyasoma katika vitabu vya akina Katalambula, Elvis Msiba na Ben Mtobwa sasa yalikuwa yamtokea mwenyewe! Kuna wakati alifikiri labda alikuwa akiota ndoto mbaya na kwamba baada ya muda si mrefu angezinduka na kujikuta yupo pamoja na mume wake Gerald lakini haikuwa hivyo! Aliendelea kusumbuka, Dunia ilikuwa ikimuadhibu kwa kosa ambalo hakika hakulitenda.

“Paaa!” Mlango ulibamizwa na Mmasai

“Shangazi!” Aliita lakini tayari alishaondoka, akahisi kuishiwa nguvu miguuni na kuporomoka hadi chini akiwa na mtoto wake mkononi ambaye kubamizwa kwa mlango kulimshtua na kujikuta akilia kwa sauti ya juu. Muda huo huo manyunyu ya mvua yakaanza kudondoka, hayo ndio yaliyoyaficha machozi yake.

Dereva alikuwa bado yupo ndani ya gari akiangalia kila kitu kwa uangalifu, kilichotokea hata yeye kilimshtua! Pamoja na kwamba hakuambiwa wala kupewa maelezo, alielewa mara moja kulikuwa na tatizo, hakuweza kuvumilia akafungua mlango wa gari na kutoka kisha kuanza kutembea mpaka mahali alipokuwa amekaa Blandina akiendelea kufikiria juu ya maisha yake.

Huku akilia na kunyeshewa na mvua, akili yake ilikuwa imemrudisha hadi utotoni mwake, akakumbuka alivyoishi maisha mazuri na wazazi wake, akidekezwa na kupewa kila kitu alichohitaji ikiwa ni pamoja na kupelekwa jatika shule nzuri walizosoma watoto wa matajiri, kamwe hakutegemea ipo siku angekuja kuishi maisha kama aliyokuwa nayo usiku huo ukizingatia baba yake alikuwa na utajiri mkubwa! Akarejea shuleni kimawazo na kumuona Gerald, akakumbuka walivyopendana na namna alivyompa ahadi nzuri za maisha huku akimhakikishia kwamba alimpenda kupita kiasi, haikuwa rahisi hata kidogo kwa mtu mwenye akili za kawaida kutarajia kwamba siku moja Gerald angekuja kumtenda mambo hayo, aligutushwa katika mawazo na dereva alipomgusa begani.

“Dada!”

“Bee, naomba unihurumie kaka yangu yule aliyefunga mlango na kuondoka ndiye shangazi yangu, nilitegemea anipe fedha nikulipe, sina hata senti tano!” Aliongea kwa sauti ya huruma.

“Usijali, wala sijakufuata kukudai, nimekuhurumia sana, kwani jambo gani limetokea?” Dereva aliuliza lakini Blandina hakuweza kujibu, aliendelea kulia bila kusimama, dude likiwa limemkaba shingoni.

“Bila kuwa na huyu mtoto, ningejiua! Sioni sababu yoyote ya kuendelea kuishi kaka yangu!”

“Kwanini unasema hivyo?”

“ Dunia imenigeuka! Nenda tu kaka, niache hapa na mwanangu kama umekubali kunisamehe deni lako!”

“Hapana, siwezi kukuacha! Tafadhali nyanyuka tuondoke, usimwache mtoto anyeshewe na mvua kiasi hiki, twende nyumbani kwangu ingawa nina chumba kimoja, mke na watoto wanne lakini nitabanana na wewe hapo hapo!”

“Nisikusumbue sana kaka yangu, wewe nenda tu!”

“Haiwezekani!” Aliongea dereva huku akimsaidia Blandina kumbeba mtoto, aliponyanyuka wote wakatembea hadi kwenye gari, Blandina akakaa mbele na kukabishiwa mtoto ndipo dereva akazunguka upande wa pili, akawasha gari na safari ya kuelekea nyumbani kwake ikaanza, muda wote Blandina alikuwa akilia huku akijitahidi kumbembeleza mtoto wake ambaye pia alikuwa akilia kwa sauti ya juu.

Walinyoosha kutokea Mikocheni kwa Nyerere hadi Sayansi ambako walivuka na kuingia barabara ya Kijitonyama na kusonga hadi Tandale kwa Mtogole, dereva akaiacha barabara ya lami ielekeayo Magomeni na kuingia kulia, katikati kwenye vijumba vidogovidogo dereva aliegesha gari mbele ya jengo lililoandikwa Chama cha Mapinduzi, mtu aliyefanana kabisa na mlinzi kwa mavazi yake akawasogelea.

“John vipi?”

“Safi tu!”

“Mbona leo mapema, hukeshi?”

“Nimemleta huyu sista angu katokea kijijini!”

“Ifakara?”

“Ndio”

“Dada karibu!’

Blandina hakujibu muda wote alikuwa akiendelea kulia, kichwa chake kikiwa kimetawaliwa na Gerald na unyama aliomtendea. Sekunde chache mlango ulifunguliwa, dereva akamsaidia kubeba mtoto na pia baadhi ya mizigo aliyokuwa nayo, wakaanza kutembea kukatiza katikati ya nyumba ndogondogo. Dakika kumi na tano baadae walikuwa bado wakitembea bila kufika, wakiwa wamepita kwenye vichochoro vingi ambavyo kama Blandina angetakiwa kurudi mpaka lilipokuwa gari, hakika asingeweza.

“Pole sana, tumefika!” Alisema dereva wakiwa wamesimama mbele ya kijumba kidogo kisicho na madirisha, Blandina akilingana nacho kwa urefu, dereva akaanza kugonga dirishani.

“Mama Mwamvua, Nifungulie mlango!” Alisema mara kadhaa bila kuitikiwa baadae sauti nyembamba ikasikika na mlango ukafunguliwa, mwanamke mnene aliyevaa hereni nyingi masikioni pamoja na kipini kilichong’ara puani akajitokeza.

“Hee! vipi tena na kitoto saa hizi? Hatutaarifiani?” Mwanamke huyo aliongea.

“Imetokea dharura!”

“Dharura gani? Nyumba ndogo yako imefukuzwa kwenye nyumba?”

“Mama Mwamvua, tafadhali hebu tuingie ndani tuongee vizuri, tusiwape watu faida!” Dereva aliongea na mke wake akaingia ndani akifuatiwa na Blandina, dereva akawa wa mwisho.

Ndani ya nyumba, dereva alijaribu kumuelewesha mke wake kidogo alichokifahamu juu ya Blandina na mwanae, mwisho akamuomba ajieleze yeye mwenyewe na akafanya hivyo, akimalizia kwa kuomba msaada wa mahali pa kuishi akitafakari aelekee wapi. Mama Mwamvua alikuwa kimya bila kusema chochote.

“Sasa kwanini hakwenda Ustawi wa Jamii? Hapa tutaishi naye vipi chumba chenyewe kimoja? Atalala wapi na mwanae mgonjwa?”

“Tutalala naye tu, naomba unielewe!”

“Sawa lakini…” Mama Mwamvua alionekana kutoridhishwa kabisa na uamuzi wa mumewe, Blandina akaelewa safari ilikuwa bado ikiendelea, msaada alikuwa hajaufikia.

Walikuwa na miaka saba katika maisha ya mke na mume bila kufunga ndoa, kikwazo kikiwa ni dini, mwanaume alikuwa Mkristo na mwanamke Mwislamu, ndoa yao ilipingwa sana lakini wakaamua kuishi hivyohivyo sababu walipendana na Mungu akawajalia watoto wanne wakiwa pamoja, walipofikia hapo suala la kufunga ndoa likafutika vichwani mwao.

Usiku mzima mtoto alilia sababu ya joto kali na njaa, Blandina hakuwa na maziwa ya kutosha kumnyonyesha! Mke wa John alilalamikia sana usingizi wake huku Blandina akimuomba msamaha kwa yote yaliyojitokeza.

“Kwa kweli kama hali ni hii itabidi mahali pengine pa kuishi, siwezi kama huyu baba anakuonea huruma basi akupangishie chumba!” Aliongea mama Mwamvua.

Saa kumi na mbili alfajiri John alimuaga Blandina kuwa anakwenda kazini na angerejea mchana kumletea maziwa ya kopo ili yamsaidie, akiyasema maneno hayo alionekana kununa kupita kiasi, ilikuwa ni chuki ya waziwazi.

“Ahsante!” Alijitahidi Blandina kuitikia, bila kumuangalia mwanamke huyo usoni.



Baada ya kutoka hospitali na kunyimwa hifadhi na shangazi yake, Blandina na mwanae mgonjwa Genesis wanapewa hifadhi nyumbani kwa dereva teksi ambaye mke wake hana moyo wa huruma, anashindwa kuvumilia na kumfanyia Blandina visa. Kwa hali ilivyo anajua hapo alipo hajafika, ameamua kutafuta kazi lakini vyeti vyake aliviacha nyumbani kwa Gerald alikofukuzwa. Anaondoka na dereva taksi had nyumbani kwa Gerald na kuvichukua vyeti kisha kutembea hadi kituo cha mabasi cha Sayansi ambako anasimama kusubiri basi, ghafla bila kutegemea gari dogo linasisimama, alipotupa macho ndani alimuona Ringo, rafiki mkubwa wa marehemu Othman, kijana aliyetaka kumuoa lakini akakataa sababu ya Gerald, anamtaka apande ndani ya gari lake, badala ya kufanya hivyo Blandina anaanza kukimbia akivuka barabara, kumbe hakuangalia pande zote, gari la mchanga likawa limefika! Dereva akajitahidi kadri ya uwezo wake wote kukanyaga breki lakini alikuwa amechelewa, vyeti vya Blandina vikaonekana vikipepea hewani. Je, nini kinafuata? Endelea.

Dereva wa lori la mchanga alikanyaga breki kwa nguvu zake zote, likajivuta likikwangua lami na kuegesha kando ya barabara, bila kuchelewa akijua wazi alikuwa ameua, aliruka na kuanza kukimbia mbio kwenda upande wa pili na kutokomea maeneo ya Kijitonyama. Watu wote waliokuwa eneo hilo hawakuamini kilichotokea, kama ni bahati basi Blandina alikuwa nayo, lori lilipofunga breki mbele yake alianguka na kulala kifudifudi akiwa amemkumbatia mtoto wake, gari likapita juu na kumuacha akiwa hajaguswa wala kukwanguliwa na kitu chochote, si yeye tu hata mtoto wake Genesis.

Tayari watu walishafika mahali alipolala Blandina, miongoni mwao akiwepo Dk. Ringo, wakimnyanyua kutokea chini, waligundua hakuwa na fahamu, mtoto wake pekee ndiye alikuwa akilia. Wakambeba na kumpakia kwenye gari ya Ringo, mwanamke mmoja akiwa amejitolea kumbeba mtoto wake, usoni akionyesha mshangao wa wazi kwa sura ya Genesis. Ringo alikata kushoto na kuingia barabara ya Mikocheni hadi kwa Nyerere, akakata kulia kuingia barabara ya zamani ya Bagamoyo, mbele ya hospitali ya TMJ akakata kulia kuingia ndani.

“Vipi?” Muuguzi wa mapokezi alimuuliza Ringo.

“Kuna huyu dada yeye na mtoto wake wamenusurika kugongwa na gari, nimeona nimkimbize hapa kwa matibabu!”

“Ameumia?”

“Hapana, gari limepita juu yake, nafikiri amepatwa mshtuko, si unaifahamu Neurogenic shock?” Dk. Ringo alimuuliza muuguzi.

“Ndio, inatokana na mshtuko!”

“Basi ndio tatizo lake!”

“Mleteni huku chumbani kwa daktari!”

Mtoto wa Blandina alikuwa ametulia kimya kabisa kama vile hakikutokea kitu chochote, hakuumia sehemu yoyote ya mwili wake. Yeye na mama yake wakapelekwa hadi kwenye chumba cha daktari ambapo Dk. Ringo alilielezea tukio zima kwa daktari aliyemkuta, ambaye baada ya kumchunguza Blandina alimtambua.

“Huyu si ni mke wa Gerald?”

“Sifahamu, kwa kipindi kirefu sana sijamuona!”

“Alikuwa akitibiwa hapa, mume wake ni mfanyakazi wa kampuni moja ambayo wafanyakazi wake huhudumiwa na hospitali yetu!”

“Basi naomba umsaidie!”

Daktari akamchunguza pia mtoto na kugundua hakuwa na tatizo lolote zaidi ya yale ya siku zote, Blandina akaondolewa hapo na kupelekwa chumba cha mapumziko ambako alitundikiwa maji yaliyopita kwenye mshipa kuingia mwilini mwake, huku kitanda chake kikiwa kimenyanyuliwa miguuni ili damu nyingi iende kwenye ubongo, haukupita muda mrefu sana, fahamu zake zikarejea, akafumbua macho na kumkuta mwanae amelazwa pembeni mwake, kwenye kiti akiwa ameketi Dk Ringo.

“Ringo!”

“Ndio mimi!”

“Hapa niko wapi?”

“Hospitali!”

Akakumbuka kila kitu kilichotokea na machozi yakaanza kumbubujika, moyoni mwake aliumia sana kila alipofikiria mambo aliyomtendea Dk. Othman, rafiki mkubwa wa Ringo, ilikuwa ni aibu kubwa kukutana tena na mtu aliyetumia uwezo wake kuhakikisha Othman na Blandina wakati huo akiitwa Halima wanaoana lakini Blandina alikataa katakata na kuamua kuolewa na mtu ambaye baadae alikuja kumharibia maisha yake.

“Najua wewe ndiye umenileta hapa hospitali!” Blandina aliongea uso wake ukiwa umeinamishwa chini.

“Ndio, ni kwanini ulikimbia?”

“Aibu, sikutaka kabisa kuonana na wewe, najisikia kushtakiwa ndani ya nafsi yangu kwa kusababisha kifo cha rafiki yako mpendwa Othman!”

“Usijali, hayo yalishapita, hebu niambie kwanza, unajisikiaje hivi sasa?”

“Najisikia vizuri!”

“Ulikuwa unatoka wapi?’

“Kuchukua vyeti vyangu”

“Kwa nani?”

“Kwa aliyekuwa mume wangu!”

“Kwa aliyekuwa mume wako, unamaanisha nini?”

“Gerald amenifukuza baada ya kuzaa mtoto huyu mwenye ulemavu!”

“Gerald? Uliyempa figo?”

“Ndio!”

“Ambaye bila wewe angekuwa marehemu?”

“Kweli!”

“Aliyekufanya usiolewe na Othman?”

“Ni yeye huyo huyo, huwezi kuamini!” Blandina aliongea akibubujikwa na machozi huku akimwangalia mtoto wake, moyoni alikuwa na mapenzi mazito mno kwa mtoto huyo, pamoja na ulemavua aliokuwepo nao yeye ndiye alikuwa ulimwengu kwake.

Ringo alishindwa kujizuia, alishakutana na matukio mengi ya kusikitisha lakini lililokuwa mbele yake muda huo, pengine lilikuwa la kusikitisha zaidi kwani alijikuta akibubujikwa na machozi. Halima hakuwa yule aliyemfahamu kwa miaka mingi, uzuri wake wote ulikuwa umepotea na mwili umeporomoka, pamoja na kuwa na umri mdogo alifanana na mama mtu mzima, nguo zake zikiwa zimepauka! Moyoni Ringo aliumia, akaapa katika maisha yake hata siku moja asingemfanyia mwanamke kitendo cha kinyama kiasi kile.

“Hivi sasa unaishi wapi?”

“Sna pa kuishi, wazazi wangu hawataki kuniona kwa sababu nilibadilisha dini na kuitwa Blandina! Baada ya Gerald kunifukuza nilikwenda kuishi kwa dereva mmoja wa teksi aliyeamua kunipa msaada baada ya kuona sina mahali pa kwenda, lakini mke wake ni mkatili sana hataki kuniona ndani ya nyumba yake, sitegemei tena kurudi kule!”

“Pole sana, unataka nikusaidie nini?”

“Usinipe pesa lakini unipangishie chumba na unisaidie kupata kazi…..ahaaaa, masikini vyeti vyangu, uliponiokota hukuona vyeti Ringo?”

“Ninavyo kwenye gari!”

“Ahsante sana, nisaidie tu kupata kazi!”

“Ulisomea sheria?”

“Ndio!”

“Nitakusaidia kupata chumba, leo tukitoka hapa tutakwenda nyumbani kwangu upumzike kwanza!”

“Umeoa Ringo?”

“Bado!”

“Mpaka leo?”

“Nilikwenda Marekani kusoma, nimerejea miezi sita tu iliyopita!”

“Itabidi utafute mchumba uoe!”

“Ndio natafuta!”

Saa nzima baadae Dk.Ringo aliondoka hospitali ya TMJ kwenda Muhimbili, kituo chake cha kazi kutoa taarifa juu ya tatizo lililomkuta na kuomba mapumziko ya siku mbili, aliporejea TMJ alilipia gharama zote na wakaondoka na Blandina pamoja na mwanae hadi Mbezi Tankimbovu ambako aliishi ndani ya nyumba kubwa yenye vyumba vinne peke yake, bila mfanyakazi wa ndani. Blandina alipewa chumba cha pembeni kabisa kilichokuwa na kila kitu ndani, akajisikia yuko nyumbani, furaha ikaanza kurejea kidogo baada ya kuona ameingia katika mikono sahihi.

Kwa wiki mbili aliishi ndani ya nyumba hiyo, ndani ya muda huo alishalazwa hospitali ya Muhimbili mara mbili, mtoto wake akiwa ameishiwa damu! Lilikuwa tatizo jipya ambalo huko nyuma halikuwahi kumpa tabu, madaktari walikuwa wakijitahidi kadri ya uwezo wao wote kujaribu kutafuta sababu ya kwanini hasa Genesis alikuwa akiishiwa damu kirahisi kiasi hiki. Wakati hilo likiendelea, jioni moja, Dk. Ringo akarejea nyumbani akiwa na habari njema.

“Halima…..aaah….Blandina!”

“Bee!”

“Unalifahamu shirika la WLO!”

“Hapana! Ni nini?”

“Women Law Organization! Ni shirika lisilokuwa la Kiserikali, linalojishughulisha na misaada kwa wanawake kisheria”

“Ndio, kuna nini?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Nimekupatia kazi, unatakiwa kuanza Jumatatu!”

“Mwanangu?”

“Itabidi nikutafutie mfanyakazi, kazi hiyo usiache! Watakulipa mshahara mzuri sana, vyeti vyako wamevipenda na wanashindwa kuelewa kwanini hukufanya kazi mahali popote mpaka leo!”

“Ahsante Ringo, ahsante kwa kila kitu, najua nilikusikitisha sana kwa yaliyotokea nyuma lakini naomba tu unisamehe na uendelee kunisaidia, Mungu atakulipa!”

“Hakuna shida, kabla ya Jumatatu nitakuwa nimekwishaleta mfanyakazi wa kubaki na mtoto wakati wewe ukienda kazini!”

“Ahsante mara Milioni moja!” Aliongea Blandina wakiangaliana na Ringo, wote wakatabasamu, uzuri wa Blandina ukachomoza kutoka kwenye mwili dhaifu aliokuwa nao, Ringo akaushuhudia, mziki laini ulioimbwa na Whitney Houston uitwao I will always love you ulikuwa ukiimbwa kwenye redio iliyokuwa sebuleni, wote wakausikia.

****





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog