Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

FURAHA HATIMAYE - 3

 






Simulizi : Furaha Hatimaye

Sehemu Ya Tatu (3)





Masaa kumi na sita ambayo Blandina na mwanae Geniss waliishi ndani ya nyumba ya John na mkewe Mama Mwamvua yalikuwa ni kama miaka kumi na sita! Kulikuwa na kila dalili za kutotakiwa ndani ya nyumba hiyo, nyimbo za taarabu zilizojaa mafumbo na zenye kumuumiza moyo Blandina zikimuita mpenda dezo zilipigwa kutwa nzima, roho ilimuuma sana lakini hakuwa na la kufanya kwa sababu hakuwa na kimbilio jingine wakati huo, alichokifanya ni kuendelea kulia na kumuomba Mungu amuondolee mateso aliyokuwa nayo, roho ilimuuma zaidi alipomfikiria Gerald na ubaya aliomtendea pamoja na kwamba yeye alimtendea mambo mengi mema pamoja na kumpa Figo yake moja ili asife.

Kutwa nzima hakutoka nje, lakini habari zake zilisambaa mitaa yote ya jirani, watu wakaanza kufurika kuja kumuona mtoto wake waliyemuita wa ajabu! Blandina hakulipenda kabisa jambo hilo lakini alipowazuia watu kuingia ndani, mama Mwamvua aliingia kati akidai yeye ndiye mwenye nyumba alikuwa na uwezo wa kuruhusu mtu yeyote aingie ndani ya nyumba yake, Blandina akanywea na kukubali mtoto wake mpendwa ageuzwe maonyesho.

“Lakini kwanini unanifanyia hivi mama Mwamvua? Wewe hujawahi kupata shida maishani mwako ukasaidiwa na watu wengine?”

“Maswali gani tena hayo, kama nilipata shida wewe zinakuhusu nini? Tena fanya mpango uondoke bwana, nyumba yangu msiigeuze kliniki, kama John anakutaka basi akupangishie hata ukiwa mke mdogo sawa tu, lakini hizi kelele ndani ya nyumba yangu na hiki kidudumtu chako sitaki!” Alifoka mwanamke huyo bila kuelewa ni kwa kiasi gani alikuwa akimuumiza Blandina.

Alikuwa na elimu ya kutosha kichwani mwake ambayo kama angeamua kutafuta kazi hakuna mwajiri ambaye angemkataa, lakini hilo halikumwijia Blandina kichwani mwake, kipaumbele kwa watu huo kilikuwa ni mwanae, asingeweza kumuacha peke yake na kwenda kazini! Genesis alikuwa ni jaribu kwake, kipimo cha utu wake, kama alivyokwisha kataa kumdhuru, asingemwacha mikononi mwa mtu mwingine akiamini kabisa lazima Gerald angekuja nyuma kumteka na kumuua jambo ambalo hakuwa tayari kulifanya, alishaapa kumlinda Genesis kwa nguvu zake zote mpaka akue mtu mzima au Mungu amchukue mwenyewe kwa amri yake.

Saa tano na nusu ya usiku, John alirejea kutoka kazini na kumkuta mtoto bado analia kama alivyomwacha alfajiri, alishangaa sana na alipouliza ni kwa sababu gani, Blandina hakuchelewa kumjibu kwamba ni sababu ya njaa kwani maziwa yake yalikuwa hayamtoshi.

“Nimekuletea kopo moja la Lakitojeni!”

“Ahsante kaka!” Aliitikia Blandina akitamani kumrukia John na kumkumbatia, kwake alikuwa mkombozi wa kweli alishangaa ni kwanini yeye na mke wake walitofautiana kiasi hicho katika mioyo yao.

Baada ya kukabidhiwa kopo alichofanya ni kulifungua na kuchota vijiko kadhaa na kuchanganya na maji ya uvuguvugu kwa kufuata maelekezo yaliyoandikwa juu ya kopo la maziwa hayo. Kwa kuwa hakuwa na mpira wa kunyonyeshea mtoto, kikombe kidogo cha plastiki kilitumika kumnyweshea Genesis maziwa hayo, alipomaliza kunywa akalala usingizi na hakulia tena mpaka alfajiri.

“Nimegundua tatizo ni chakula, mwanangu anasumbuliwa na njaa, nahitaji fedha John na ninajua huwezi kunipa maziwa kila siku, nahitaji kutafuta kazi!” Alimwambia John kabla hajaondoka.

“Kazi?”

“Ndio!”

“Kazi ni ngumu sana kupata kama hujasoma!”

“Nimesoma John!”

“Mh! Mpaka la ngapi?”

“Chuo kikuu, nina digrii ya ……!”

“Digrii kabisa?”

“Ndio kaka!”

“Unadanganya Blandina!”

“Kwa nini nifanye hivyo? Nilimaliza Chuo kikuu mwaka …… tena pamoja na mume wangu lakini hakuniruhusu kutafuta kazi baadae nikawa mjamzito wa mimba ya mtoto wangu Genesis!”

“Kama ni hivyo kazi utapata, lakini kwa unavyoonekana hakyanani sio rahisi mtu kuamini una digrii kichwani!”

“Huo ndio ukweli!”

“Vyeti?”

“Viko nyumbani kwa mume wangu, itabidi nivifuate!”

“Basi sawa, wacha mimi niende kazini!”

“Kama itawezekana naomba tuondoke wote, ukaniache tu pale Sayansi mimi nitatembea kwa miguu hadi nyumbani kwake, shida yangu ni vyeti tu!”

“Atakupatia?”

“Sifahamu lakini ni haki yangu!”

“Ok, jiandae!”

Hakuwa na maandalizi yoyote, alichokifanya ni kumnyanyua mtoto wake kutoka kitandani na kumfunga mgongoni kwa khanga kisha kubeba mfuko mdogo wa Rambo uliokuwa pembeni mwa jamvi alilolalia sebuleni, humo ndimo kulikuwa na matambala ya kumbadilisha mtoto wake, akaanza kumfuata John hadi ofisi ya CCM lilikoegeshwa gari lake, wakati wanapanda tu, adhana ilipigwa.

Safari hadi eneo la Sayansi Kijitonyama iliwachukua dakika kumi tu kwa sababu ya kutokuwepo kwa magari barabarani wakati huo, badala ya kumshusha barabarani John aliamua kumpeleka moja kwa moja hadi nyumbani ambako alimshusha giza likiwa limetanda kila mahali.

“Bado wamelala?” John aliuliza.

“Ndio, nitawasubiri!”

Akaondoka zake na kumuacha ameketi kando ya lango la kuingilia, aliendelea kubaki hapo mpaka saa kumi na mbili na nusu asubuhi ndipo akaanza kugonga, muda mfupi baadae akasikia mlango wa nyumba ukifunguliwa na hatua za mtu akitembea kuelekea langoni, lilipofunguliwa, Gerald alisimama mbele ya Blandina akiwa amejifunga taulo tu kiunoni.

“Nini kimekurudisha hapa?” Aliuliza Gerald kwa ukali, iliyokuja kichwani mwa Blandina ni picha ya Gerald akipelekwa chumba cha upasuaji, mtu wa kutoa figo akihitajika haraka, Blandina hakuweza kuyazuia machozi yaliyokuwa mlangoni, akalia.

“Nakuuliza umefuata nini?”

“Vyeti vyangu!”

“Subiri hapa nje!” Alisema Gerald akifunga lango nyuma yake na kuanza kutembea kwenda ndani, aliporejea walikuwa na fremu mbili ambazo ndani yake kulikuwa na vyeti, kimoja cha kumaliza kidato cha sita na kingine cha Chuo Kikuu, akavitupa chini na kuondoka zake.

“Ahsante Gerald!” Blandina aliongea akijaribu kujifanya hajaumia, lakini ukweli wa mambo ni kwamba maumivu aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake yalikuwa makali mno, kichwani mwake ikaingia taswira ya Gerald siku alipokuja Chuo Kikuu kwa mara ya kwanza akiwa amekonda kupita kiasi, walipokutana kwenye ngazi yeye Blandina akimuwahi Dk. Othman aliyekuwa akimsubiri kwenye gari ili waende kuvishana pete ya uchumba, roho ikamuuma sana lakini hakutaka kujilaumu kwa yote yaliyotokea ingawa kwa upande mwingine aliamini labda mwanaume aliyetakiwa kuwa mume wake ni Dk. Othman.

“Maskini Othman, alinipenda kupita kiasi mpaka kufikia uamuzi wa kutaka kumuua Gerald, laiti angekuwepo leo hii ningekwenda nyumbani kwake kumuomba msamaha, pengine angekubali kunipokea, nilimuumiza sana!”

Kulipopambazuka na watu kuanza kupita mbele ya lango la nyumba ambayo sasa ilikuwa Grace na Gerald, Blandina alianza kusikia aibu, watu wengi sana walimfahamu mitaa hiyo, akaamua kuondoka hadi barabara ya Ali Hassan Mwinyi akiwa na vyeti vyake mkononi, alisimama kwa karibu dakika kumi na tano bila hata gari moja kusimama kumchukua, makonda wote walipochungulia na kumuona mtoto wake walimuamuru dereva aondoe gari.

Muda mfupi tu baadae, alishtukia gari likisimama ghafla mbele yake, vioo visivyoruhusu mtu kuona ndani vikafunguliwa, mwanaume mmoja mnene alikuwa amekaa nyuma ya usukani usoni mwake akiwa amevaa miwani ya rangi nyeusi. Mwanzoni Blandina hakumtambua, mpaka sauti ya mwanaume huyo ilipotoka.

“Halima! Nini kimekupata?” Aliita mwanaume huyo kwa jina ambalo Blandina alishaanza kulisahau.

“Ringo?”

“Ndio! Panda kwenye gari uende ukinisimulia yaliyokupata”

Badala ya kupanda, Blandina alianza kukimbia akivuka barabara kwenda upande wa pili, kumbe hakuangalia kushoto na kulia, ghafla lori la mchanga lilikuwa mbele yake, dereva akijitahidi kukanyaga breki kadri awezavyo, alishachelewa kilichosikika ni tairi zikijivuta kwenye lami, vyeti vya Blandina vilionekana vikipepea hewani. Watu waliokuwa jirani na eneo hilo mikono yao ilikuwa kichwani kila mtu akitoa maneno aliyoona yanafaa kuelezea tukio lililokuwa mbele yake.





Baada ya kuteseka kwa muda mrefu hatimaye Blandina ameingia mikononi mwa Dk. Ringo, rafiki wa marehemu Dk. Othman, kijana aliyetaka kumuoa Blandina lakini akamkataa kwa sababu ya Gerald, jambo lililomfanya ajikute mahabusu baada ya kujaribu kumuua Gerald, ni huko Mahabusu ndiko alikojitundika. Ringo amemsaidia Blandina, kwanza amemkaribisha nyumbani kwake ambako anaishi naye kisha kuamua kumtafutia kazi ambayo ameipata. Ni hivi punde tu amemaliza kumpa taarifa juu ya kazi hiyo, Blandina amepata furaha isiyo na kifani, anamwangalia Dk. Ringo kugundua kitu kingine; uzuri wa sura yake, ni jambo ambalo hakuwahi kuliwaza hata mara moja, wanaangaliana na kugonganisha macho, Ringo anatabasamu, naye akauona uzuri wa Blandina. Yote hayo yakitokea mzito mtamu wa Whitney Houston, uitwao I will always love you, ulikuwa ukipigwa kwenye redio sebuleni. Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO…



Ghafla kitu cha ajabu kilikuwa kimechipuka moyoni mwa Blandina, hata mara moja katika maisha yake hakuwahi kukitegemea! Alianza kama utani kwa kusema “Ona macho yake” “Tazama midomo yake” “Tena ana dimposi kama mwanamke” “Ringo ni mzuri, ona mwili wake ulivyojengeka utafikiri mwinua vitu vizito?” kauli hizo ziliendelea kumiminika kichwani mwake akimwangalia Dk. Ringo kwa jicho la pembeni, hakutaka azigundue hisia zilizokuwemo moyoni mwake kwani hakufahamu yeye angemchukuliaje baada ya hapo.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Akiwaza hayo yote walikuwa wameketi mezani wakila chakula cha usiku, wakiongea mambo mbalimbali kuhusu maisha yao, Dk. Ringo akijaribu kumweleza Blandina umuhimu wa kuichukua kazi iliyokuwa imepatikana, akimhakikishia ingebadilisha maisha yake kabisa na kumfanya asahau matatizo yote aliyokuwa amepata kabla ya kukutana naye, alimtaka afute historia ya nyuma na hata akiikumbuka kamwe asiikumbuke kwa machungu bali aichukulie kama changamoto na awe tayari kuwasamehe wote waliomkosea, asiingie katika siku za usoni na mambo ya siku za kale. Kazi ya Ringo ilikuwa ni kumpa Blandina ushauri nasaha akiamini kabisa kwamba, moyoni alikuwa na vidonda vingi vilivyohitaji kupona.



“Blandina!”

“Bee!”

“Mbona unaniangalia jicho la aina hiyo?”

“Mh!Mh! hakuna kitu!”

“Hapana, hivi unafahamu nimesoma saikolojia na nina uwezo wa kuyaona yaliyoko moyoni kupitia machoni mwako?”

“Wewe unafikiri nini?”

“Umeanza kunipenda kwa upendo tofauti!”

“Upendo gani Ringo?”

“Umeanza kunipenda kimapenzi, macho yako yananionyesha hivyo!”

“Ni kweli, tena imenitokea ghafla, sikupanga, wema wako umekuwa wa ajabu mno kwangu, sijui kama utanikubalia kwa jinsi nilivyochakaa nikiwa na huyu mtoto mlemavu, ni kinyume kabisa cha utamaduni wa Mwafrika mwanamke kueleza hisia zake kwa mwanaume ingawa yeye pia ni mwanadamu, kama utaniruhusu naona niseme, nakupenda Ringo!”

“Nikuulize swali?”

“Uliza tu?”

“Naomba usijisikie vibaya lakini!”

“Unataka kunikatalia Ringo?”

“Nataka tu kujua kitu fulani!”

“Naomba usiniumize lakini!”

“Umeamua kunipenda kwa sababu nimekusaidia kupata kazi?”

“Hapana, imenitokea tu! Unanichukia Ringo?”

“Hapana, nakupenda pia Blandina, wala haijaanza leo tu, ni tangu siku nyingi sana lakini nilishindwa kufanya chochote kwa sababu ya rafiki yangu Othman!”

“Kweli?”

“Ni kweli kabisa lakini…!” Ringo alisema lakini kabla hajamaliza, tayari Blandina alishafika na kumkumbatia, wakaanza kupapasana miili yao taratibu, kama mchezo bila kutegemea ghafla pua zao zikagusana, pumzi ya uvuguvugu ikaanza kuwapuliza kwenye ngozi zao! Kilichofuata baada ya hapo ni midomo kusogeleana, ikagusana na kufunguka, kama vile nyoka afanyavyo, ndimi zao zikachomoza! Kabla hawajasonga mbele, huku wakihema kwa fujo wakiwa wamemsahau hata mtoto wao aliyelala kwenye kochi, Ringo akashtuka.

“No!” (Hapana!)

Moyo wa Blandina ukapiga kwa nguvu na kumfanya awe kama mtu aliyezinduka kwenye usingizi, fahamu zake zikawa zimerejea. Hakuelewa ni kwanini Ringo alikataa wakati walishakwenda kilometa nyingi wakizidi kuisogelea mbingu, Blandina akamwachia na kushika mikono kiunoni.

“Why?” (Kwanini?)

“It is not right!” (Sio sawa!)

“Why? Don’t you love me?” (Kwanini? Hunipendi?)

“I do! But…” (Nakupenda lakini…!)

“But whaaat, Ringo?” (Lakini nini, Ringo?)

“I have a reason!” (Nina sababu!)

“How big is that reason? Is it because I am worn out or because I used to be your friend’s girlfriend, Othman is not in the world Ringo?” (Hiyo sababu ni kubwa kiasi gani? Je, ni kwa sababu nimechakaa? Au kwa sababu nimewahi kuwa mpenzi wa rafiki yako, lakini Othman hayupo duniani tena Ringo?)

“One day you will understand why I am saying no and you will thank me for the decision I am making here today, I love Blandina but we cant have sex, I will do whatever I am supposed to do to help but not sleeping with you!” (Siku moja utakuja kuelewa kwanini nasema hapana na utanishukuru kwa uamuzi ninaofanya hapa leo, nakupenda sana Blandina bila kujali unavyoonekana lakini hatuwezi kufanya ngono, nitafanya chochote ninachotakiwa kufanya kukusaidia lakini si kuingiliana kimwili!) aliongea Ringo akimwangalia Blandina kwa macho ya huruma, ghafla akamshuhudia akipiga magoti mbele yake.

“Nisamehe Ringo, shetani tu ameniingia, sikutakiwa kabisa kufanya mambo haya lakini ni kweli nakupenda, naheshimu maamuzi yako!” Blandina alisema akiwa sakafuni.

“Simama! Simama Blandina, usinisujudie, wewe ni binadamu kama mimi nilivyo, una hisia kama mimi nilivyo, huna sababu hata kidogo ya kuomba msamaha! Sijakasirika!” Baada ya kusema maneno hayo Ringo akamsaidia Blandina kunyanyuka, hawakukaa tena sebuleni kila mmoja akaondoka kwenda chumbani kwake ambako Blandina aliendelea kulia akijisikia aibu kupita kiasi.

Siku iliyofuata ilikuwa Ijumaa, Blandina hakutoka chumbani mapema kama ilivyo kawaida yake, alikuwa amejawa na aibu kiasi cha kushindwa kukutana uso kwa uso na Ringo ambaye akilifahamu jambo hilo alilazimika kumfuata chumbani kwake kumsalimia kama vile hakikutokea kitu chochote, akambeba mtoto Genesis na kumpiga mabusu usoni, kwa kitendo hicho Blandina alijisikia nafuu kidogo. Ringo akaondoka kwenda kazini kwake Muhimbili, mchana alipiga simu mara mbili kuuliza namna mtoto alivyoendelea, Blandina akaendelea kuomba msamaha.

“Yaache hayo, tusirudi tena Misri, twende Kanaan, iko siku utakuja kuelewa kwanini ilikuwa hivyo jana, kuna kitu kizuri mno kinakusubiri mbele ya safari, siwezi kukuambia hivi sasa!”

“Ahsante!”Jumamosi Dk. Ringo hakwenda kazini, vivyo hivyo Jumapili, kazi aliyoifanya kwa siku hizo mbili ni kutafuta mfanyakazi mpaka akampata sehemu za Kiwangwa huko Bagamoyo ambako rafiki yake mpendwa Bonye aliishi akiendesha kilimo cha Mananasi na Mihogo. Alipomleta nyumbani msichana huyo, Fatma mwenye umri wa miaka kumi na nane, Blandina akaelewa kweli amepata kazi. Alionekana kuwa msichana mpole na mtaratibu, karibu usiku mzima wa siku hiyo ulitumika kumfundisha namna ya kumwangalia mtoto, haikuwa kazi ngumu kwake kuelewa, alishafanya kazi ya kulea mtoto sehemu nyingine kabla.



****

Jengo la WLO lilikuwa Kijitonyama nyuma ya jengo la Sayansi na Teknolojia, kutoka nyumbani kwa Dk. Ringo Mbezi hadi kwenye jengo hilo hapakuwa na umbali mkubwa, dakika ishirini zilitosha kwao mpaka kuegesha gari mbele ya jengo, ikiwa ni saa moja na nusu ya asubuhi. Ilibidi wasubiri saa mbili itimie muda ambao walikuwa wametakiwa kuonana na Mkurugenzi wa shirika hilo, Bi. Majorica Lukonge, Mjerumani aliyeolewa na Mtanzania. Mama huyo alifika saa mbili kasoro dakika kumi na tano na kuwakaribisha ofisini kwake ambako Dk. Ringo alimtambulisha Blandina.

“Una vyeti vizuri sana nashangaa ni kwanini hujafanya kazi mahali popote, vile vyeti ni vyako?”

“Kabisa mama!”

“Sasa mbona uko hivyo?”

“Basi mama maisha, kuna mahali niliharibu lakini hakuna shida sana nimekubali kuanza upya, nitafurahi kama utaniajiri na kwa hakika nitakufanyia kazi yako kwa uaminifu mkubwa!”

“Hakuna shida, nitakuuliza tu maswali machache kuthibitisha kama kweli unaelewa sheria!”

“Sawa!”

“Hakuna shida nikikuuliza mbele ya Dk. Ringo?”

“Hakuna shida!”

Maswali yakaanza kuporomoka yote yakajibiwa kwa ufasaha kama vile kabla ya kwenda mahali hapo asubuhi hiyo, Blandina alikuwa amekesha akisoma! Bi. Majorica alishangaa na kujikuta akitamka bila kipingamizi chochote kuwa “You are our legal officer from today, your salary will be seven hundred dollars a month, is it ok?” Akimaanisha wewe ni Afisa wetu wa sheria kuanzia leo, mshahara wako utakuwa dola mia saba kwa mwezi, ni sawa?.

“Thank you madam!” (Ahsante mama!) alijibu Blandina akinyanyuka kitini na kupiga magoti akimshukuru Mungu, mikono yake yote miwili ikiwa hewani.

“Let me prepare the contract!” (Acha nitayarishe mkataba!) aliongea Bi. Majorica na kunyanyuka kitini kwenda kwa katibu Mhutasi wake kutoa maelekezo, mlango ulipofungwa tu, Blandina akamgeukia Dk. Ringo.

“Nimwambie kama nina mtoto mgonjwa?”

“Blandina! Unataka useme kila kitu, wewe chukua kwanza kazi mengine yatajulikana baadaye!”

“Sawa!”

Aliporejea Bi. Majorica, akiwa na katarasi mkononi kitu kama dakika kumi baadaye, Blandina alitakiwa kutiwa saini na akafanya hivyo. Kilichofuata baada ya hapo ni kuonyeshwa mahali ofisi yake ilipokuwa, hata Dk. Ringo hakuwa na ofisi nzuri namna hiyo Muhimbili, ilikuwa na samani za thamani kubwa, meza ya kung’ara, kiti cha kuzunguka, kiyoyozi, jokofu dogo lenye vinywaji, kabati kubwa pembeni iliyojaa vitabu vya sheria, akavisoma baadhi kwa juu; Commercial law, Criminal Procedure Act, Matrimonial law, kumbukumbu zake zikamrejesha Chuo Kikuu, akamwona Gerald na kutamani angekuwa na kamera ya kumwonyesha mambo yaliyokuwa yakitokea ndani ya jumba hilo, ulimwengu mpya ulikuwa umefunguka, mateso yake yalikuwa yamefika mwisho.

“Hii ndio itakuwa ofisi yako, yule msichana pale anaitwa Grace, atakuwa katibu muhutasi wako!”

“Katibu Muhutasi? Sio gharama kubwa sana?”

“Usijali, huo ndio utaratibu wetu!”

Kila kitu kilikuwa kikitokea kama ndoto, Blandina hakuwa tayari kuamini kwamba kweli maisha yake kufumba na kufumbua yalikuwa yamebadilika, tayari alikuwa bosi! Akawa na uhakika tangu siku hiyo asingehangaika tena iwe chakula cha mtoto wake wala mahali pa kulala. Alimshukuru Dk. Ringo kwa kila kitu, aliletwa kwake na Mungu kama Malaika mlinzi kumwokoa na matatizo aliyokuwa nayo. Wakaondoka kurejea nyumbani njiani walipita kwenye maduka ya Mwenge ambako Dk. Ringo alimnunulia Blandina nguo na viatu vipya pamoja na mkoba kwa ajili ya kubebea vitu vyake, alitaka apendeze siku iliyofuata akienda kazini.

*****

Ulikuwa ni mwanzo wa maisha mapya, Blandina akawa kama vile kazaliwa kwa mara ya pili. Bado hakutaka kwamba yeye ndiye alikuwa Mwanasheria wa shirika lililojihusisha na msaada wa kisheria kwa Wanawake WLO mshahara wake ukiwa dola mia saba kwa mwezi! Halikuwa jambo rahisi kwake kuamini.

Blandina ambaye kwake hata shilingi tano ilikuwa ni sawa na milioni tano ndiye anapokea kiasi hicho cha fedha? Hata yeye mwenyewe hakutaka kukubali, mpaka mwisho wa mwezi ulipofika na kusimama dirishani, noti saba za dola mia zikapenya dirishani, akatia saini na kuondoka zake, mbele kidogo machozi yakaanza kumtoka, hayakuwa ya huzuni bali furaha kubwa aliyokuwa nayo moyoni mwake.

Zaidi ya mshahara huo mkubwa, Blandina alipewa gari la ofisini aina ya Landcruser mkonge lililompeleka kazini na kumrudisha nyumbani, maisha yake yalibadilika kabisa. Alivaa vizuri na kusuka rasta ndogondogo za Kimasai zilizomfanya azidi kupendeza, ngozi yake ilirejea kwenye rangi yake ya awali, midomo yake ya duara ikawa laini kama ilivyokuwa mwanzo! Blandina akapendeza, mwili wake ukachongeka tena katika umbo la namba nane, alipovaa suti nyeusi za kazi zilimfanya avutie kupita kiasi, hakumkumbuka tena Gerald, vidonda moyoni mwake vilishapona.

Kizuri na kilichomfurahisha zaidi ni mwanae Genesis, hakuugua hata mara moja! Kila siku alimuacha na mfanyakazi wa ndani, Fatma ambaye upendo wake kwa Genesis ulionekana wazi kabisa, alimpenda mtoto huyo kupita kiasi wala hakujali maumbile yake, kwake mtoto alikuwa mtoto! Kwa hili, bila kujiuliza mara mbili, Blandina alijikuta katika mapenzi mazito na binti huyu; akawa kama mtoto wake, akimfanyia jambo jema ambalo kila binadamu alitakiwa kumfanyia mwenzake.

Kila siku asubuhi Blandina alifuatwa nyumbani na kupelekwa kazini, saa kumi na nusu jioni ndio aliondoka tena kurejea nyumbani. Ilikuwa ni kawaida yake kupita kwenye Super Market kubwa iliyoko eneo la Mbezi kufanya manunuzi ya matumizi ya nyumbani, kwa mshahara aliokuwa nao hakuhitaji kumtegemea Dk. Ringo tena, msaada aliokwishampa ulikuwa mkubwa mno. Hakuwa na sehemu nyingine yoyote ya kupita baada ya kufanya manunuzi yake, alichokifikiria kichwani ni Genesis, hiyo ndio ilikuwa ratiba yake ya kila siku.

“Griii! Griii!” Simu yake ililia alipoingia tu ndani ya gari mbele ya jengo la Super Market ya Patco, akaichukua na kuangalia kwenye kioo, ilikuwa namba ya Dk. Ringo.

“Haloo!”

“Blandina?”

“Ndio! Uko wapi?”

“ Nyumbani!”

“Saa hizi?””Nimewahi kidogo!”

“Kuna nini?”

“Njoo nyumbani haraka!”

“Niambie tu!”

“Naomba uwahi!”

“Kuna tatizo gani?”

“Naomba uje Blandina, tuache kupoteza muda kwenye simu!”

Hisia yake namba sita tayari ilishamuonyesha kilichotokea, lazima Genesis alikuwa mgonjwa tena taabani! Alichokifanya Blandina kuingiza gea ya kurudi kinyumenyume, gari ikaanza kuserereka kwa kasi, hakujua kulikuwa na gari jingine likipita, kilichomshtua ni mlio akajua tayari amegonga gari la mtu, moyo wake ukapiga paa!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Hata hivyo aliweza kulizima gari na kushuka chini, mwanamke aliyevimba na kufura kwa hasira akamfuata akitupa mikono yake hewani na kutoa matusi machafu ya nguoni. Blandina alipovua miwani aliyokuwa amevaa usoni Macho yalitua juu ya uso wa mwanamke huyo, akamfahamu! Alikuwa Grace, mwanamke aliyemuondoa nyumbani kwa Gerald, moyo wa Blandina ukaruka mapigo kadhaa, Grace akasimama akiwa ameduwaa mbele yake mwili wake ukitetemeka kwa hasira, macho yake yalionyesha kabisa mshangao aliokuwa nao.

“Samahani sana Grace, ni bahati mbaya!”

“Yaani uliponunua gari ndo unaanza kugonga watu ovyo ovyo! Vitu vya kupatia ukubwani bwana, nitakutwanga sasa hivi!”

“Usifanye hivyo ni bahati mbaya, sikupanga!”

Tayari Grace alishamsogelea zaidi, wakati huo akimhemea usoni, kulikuwa na kila dalili kwamba watu hao wangekamatana na kuangushana chini. Hapo Blandina alitamani dereva wake angekuwepo, kwa siku mbili alikuwa mgonjwa jambo lililomfanya alazimike kuendesha gari yeye mwenyewe. Kabla Grace hajamkaba, alishikwa na mtu na kuanza kuvutwa nyuma, Blandina alipomuangalia mtu huyo usoni pia alimtambua; alikuwa Gerald kwenye mkono mmoja akiwa ameshikilia chupa ya chai iliyoonekana kabisa aliinunua ndani ya duka muda mfupi kabla.

“Blandina!” Gerald aliita akionyesha mshangao.

“Bee!”

“Ni wewe?”

“Ni mimi, bahati mbaya nimegonga gari ya mke wako, au sijui ni yako!”

“Usijali! Ni bahati mbaya, ulikuwa wapi siku zote hizi? Umependeza sana, mambo yamekunyokea!”

“Gerald sitaki maneno mengi, hii hapa ni kadi yangu pelekeni gari lenu gereji yoyote, nitakuja kulipa!”

“UTAKUJA KULIPHAA!” Grace aliyarudia maneno yaliyosemwa na Blandina akiwa amebana pua yake kwa mkono wa kushoto kuonyesha dharau.

“Sitaki kugombana na wewe Grace, naomba niwahi nyumbani mwanangu anaumwa!” Aliongea Blandina na kumtaka Gerald aliondoe gari lao, akafanya hivyo bila ubishi wowote huku macho yake yakimuangalia Blandina akiondoka, hata Grace mwenyewe alikielewa kilichoendelea moyoni mwa mume wake.

Kwa kasi ya ajabu, Blandina aliendesha gari lake kuelekea nyumbani lakini kabla hajafika alikutana na gari la Dk. Ringo, pembeni akiwa amekaa msichana wa kazi akiwa amembeba Genesis begani, gauni lake likiwa limelowa damu nyingi kwa nyuma iliyooneka kutoka puani kwa Genesis kwa mabonge! Blandina alihisi mwili wake unaishiwa nguvu, machozi yakaanza kumlengalenga, hakuna kitu hakupenda duniani kama kumuona Genesis akiumwa, kwa muda mrefu sana alikuwa amepumzishwa, lakini alihisi sasa zamu imewadia. Alichokifanya ni kuegesha gari lake pembeni na kuruka bila hata kutoa ufunguo, akaingia ndani ya gari la Dk. Ringo na safari kuelekea hospitali ya Lugalo ikaanza. Walipokelewa mapokezi na kuonyeshwa chumba cha daktari bingwa wa magonjwa ya watoto, Dk. Mwinula.

“Ameanzaje huyu mtoto?”

“Mimi nilipigiwa simu na huyu msichana wa kazi, akaniambia mtoto anavuja damu puani, kwa sababu sikuwa mbali sana nikawahi nyumbani na kumkuta amelowanisha godoro kwa damu, mabonge yalikuwa juu ya kitanda!”

“Mtoto wa nani?”

“Wa dada yangu!”

“Yuko wapi?”

“Huyu hapa!” Dk. Ringo alijibu akimsota Blandina ambaye muda wote alikuwa akibubujikwa na machozi, moyoni akijua wakati ulikuwa umefika tena, wa kuhamia hospitali.

“Bila shaka wewe ni Dk. Ringo?” Dk. Mwinula aliuliza baada ya kuwa amechukua maelezo ya kutosha kutoka kwa Blandina.

“Kweli kabisa!”

“Kwa aina hii ya uvujaji wa damu na maelezo niliyoyapata nashawishika kusema huyu mtoto ana Haemophilia, huu sio uvujaji wa kawaid wa damu!”

“Ugonjwa gani huo daktari mwanangu anaumwa?”

“Nahisi kuna tatizo kwenye viwanda vyake vya kutengeneza chembechembe za damu, kuna aina fulani inanitwa Platelets au chembe sahani, hizi uhusika hasa na ugandaji wa damu, nina wasiwasi kwamba mtoto wako hazalishi vya kutosha au kama zinazalishwa basi zina matatizo!”

“Unamaanisha Chembemundu au Sikoseli?” Blandina akauliza tena..

“Hapana, hili ni tatizo tofauti, Dk. Ringo atakueleza vizuri baadae wacha niwasiliane na watu wa chumba cha kuhifadhia damu ili tuone kama tutapata damu ya kutosha tumuongezee haraka iwezekanavyo!” Aliongea Dk. Mwinula na mara moja akapiga simu chumba cha damu, chupa tano za damu zikapatikana, Genesis akakimbizwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi ambako alilazwa na kutundikiwa damu muda mfupi baadae ikiwa ni pamoja na kushomwa sindano za kusaidia damu kuganda.

Juhudi zote zilizofanyika hazikuzaa matunda, hali ya Genesis iliendelea kuwa mbaya kwa siku tatu baadae, damu ikivuja na kuacha! Yote iliyoingizwa kupitia kwenye mishipa ilionekana kutoka nje kupitia upande wa pili, mwili wake wote ukabadilika na kuwa mweupe kama karatasi. Pamoja na Dk. Mwinula kuwafariji na kuwatia moyo Dk. Ringo na Blandina ghafla kukawa na kila dalili kwamba Genesis hatimaye angeaga dunia.

“What can we do? I have money saved in my account, I can use it for my daughter!” (Tufanye nini? Nina fedha kwenye akaunti yangu, naweza kuitumia kwa ajili ya mwanangu!”) Aliongea Blandina akimuuliza Dk. Ringo.

“Don’t worry, she will be fine!” (Usiwe na wasiwasi, atapona!) Dk. Ringo alimfariji.

“Hapo ndipo madaktari huwa mnakosea, kumwambia mtu anayeuguza nenda kalete uji wakati mgonjwa anakata roho! Ringo, nimekwishaona kabisa kwamba mwanangu anakufa halafu wewe unaniambia atapona?” Blandina aliuliza akizidi kulia, alipomuangalia mtoto wake alimuona akikakamaa.





Baada ya mateso ya muda mrefu akiwa na mtoto wake mlemavu, Blandina anapata kazi ya Uanasheria kwenye shirika la kutetea haki za wanawake liitwalo WLO. Mshahara kwa kazi hii ni mkubwa kuliko alivyofikiria, maisha yake yanabadilika ghafla kwani amepewa mpaka gari la kumwendesha kwenda na kurudi nyumbani kwa Ringo ambako bado anaishi.

Cha kushangaza mtoto wake ametulia kabisa, Genesis haugui tena kama ilivyokuwa zamani! Huu ni muujiza kwa Blandina ambaye sehemu kubwa ya maisha yake tangu mtoto huyo azaliwe na ulemavu, yalihamia hospitali, akihama moja kwenda nyingine.

Akiamini mtoto wake anaelekea kupona, Blandina anapokea simu kutoka kwa Ringo ikimtaka afike nyumbani haraka, Genesis ni mgonjwa! Wakati simu hiyo inaingia alikuwa mbele ya duka kuu la Patco, Mbezi na anaanza kurudisha gari kinyumenyume, bila kufahamu atagonga gari jingine nyuma.



Inatoka kuwa mwenye gari hilo ni Grace, msichana aliyeingilia ndoa yake na Gerald na kumwondoa Blandina ndani ya nyumba, kabla hawajakamatana Gerald alitokea na kumshika Grace, huku akimshangaa Blandina kwa jinsi alivyobadilika na kuwa mzuri na mwenye mvuto.

Blandina hakutaka kuongea chochote, alichofanya ni kuwaachia kadi yake ili wapeleke gari mahali popote kwa matengenezo, yeye angekwenda kulipa baada ya hapo akaondoka moja kwa moja kuelekea nyumbani. Anakutana na Ringo njiani, hali ya mtoto ni mbaya, anavuja damu puani mfululizo.



Wanamkimbiza haraka hadi hospitali ya Lugalo ambako anapokelewa na daktari bingwa wa watoto, Dk. Mwinula ambaye baada ya kumwangalia tu mtoto anahisi ana tatizo hatari la kuganda kwa damu mwilini, Haemophilia. Muda mfupi tu baadaye wakiwa chumba cha wagonjwa mahututi, mtoto anakakamaa.

Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO…



“Masikini mtoto wangu!” Blandina alilia alipomwona Genesis akikakamaa kitandani, dalili zilionyesha alikuwa akikata roho.

“Hebu mpelekeni nje huyu mama tupate nafasi kufikiria nini cha kufanya!” Dk. Mwinula aliongea ndipo Dk. Ringo akambembeleza Blandina mpaka akakubali kutoka nje ambako hata hivyo aliendelea kulia kwa uchungu mwingi.



Mpaka hapo hakuwa tena na matumaini ya Genesis kuendelea kuishi, ilimuuma sana kwani kwa muda mrefu sana alikuwa amehangaika kuokoa maisha yake lakini mwisho alitakiwa kufa, hakuwa na jinsi tena ya kumbakiza mwanae duniani! Uwezo wake wote ulikuwa umekomea hapo mengine yote aliyaacha mikononi mwa Mungu na alielewa ni kiasi gani Gerald angefurahishwa na taarifa za kifo cha Genesis, kwake ungekuwa ushindi kwani alitamani jambo hilo litokee tangu mtoto alipozaliwa.



Dk. Ringo alijaribu kutumia uwezo wote aliokuwa nao kumtuliza lakini haikuwezekana, Blandina aliendelea kububujikwa na machozi akilia kwa uchungu huku akieleza wazi kilichokuwemo moyoni mwake, kwamba bila Genesis maisha yake hayakuwa na maana yoyote tena. Kwa mwanamke kawaida mpenda starehe aliyoyasema yalionekana ni kichekesho kwani kifo cha Genesis kingekuwa ni kuepuka shida zote alizosababisha mtoto huyo mlemavu. Kwa Blandina ilikuwa tofauti, suala la ulemavu wa mtoto wake halikuwa na uzito, alichotaka ni Genesis kuendelea kuwa hai, upendo aliokuwa nao kwa mtoto huyo ulizidi alivyojipenda yeye mwenyewe.



Hali ya hewa ilikuwa ya baridi jioni hiyo, tofauti na siku nyingine nyingi katika mwezi huo wa Oktoba, manyunyu yalikuwa yakidondoka na kuwalowanisha Blandina na Dk. Ringo lakini hawakutoka sehemu waliyokuwa wamekaa, waliendelea kuwashuhudia wauguzi wakikimbia kutoka kwenye chumba cha wagonjwa mahututi alicholazwa Genesis na kuingia ofisini, waliporejea walikuwa na vifaa na dawa mikononi mwao, alichoweza kukiona Dk. Ringo kwa macho yake kilikuwa ni mashine ya hewa ya Oksijeni, iliyoingizwa mara ya mwisho na muuguzi akikimbia, hiyo ilionyesha hali ya mgonjwa ilikuwa bado ni mbaya.



Baada ya hapo ulifuatia ukimya wa kama nusu saa, Blandina akiendelea kumlilia mtoto wake, muda wote akisali kimoyo moyo kumwomba Mungu atende muujiza na Wanaume kwa wanawake walioonekana kuwa ni madaktari waliendelea kuingia ndani ya chumba hicho wakitembea kwa mwendo wa kasi, kichwani mwake Dk. Ringo alifahamu kilichokuwa kikiendelea, upande mmoja wa akili yake ulimweleza kwamba Genesis tayari alishaaga dunia, alishindwa kabisa kuelewa angemtuliza vipi Blandina baada ya hapo, hakuwa na jibu.



“Dk. Ringo!” Dk. Mwinula aliita nusu saa baadaye baada ya kufungua mlango, macho yake yalionyesha wasiwasi mwingi, uso haukuwa na tabasamu hata kidogo.

“Naam daktari!”

“Nakuomba mara moja!”



Akiwa amejawa na hofu tofauti na siku nyingine zote za kufanya kazi kama daktari, Dk. Ringo alinyanyuka na kutembea kuelekea mlangoni, Blandina naye hakuweza kuvumilia na kubaki sehemu aliyokuwa amekaa, alitaka kufahamu kila kitu kilichoendelea ndani ya chumba cha wagonjwa mahututi. Dk. Ringo aliposimama mbele ya Dk.Mwinula, Blandina alikuwa nyuma yake akitetemeka mwili mzima, masikio yake yote mawili yakiwa wazi kusikia ambacho kingeongewa.

“Ndio daktari!”

“This is a very complicated case, but we haven’t given up, we still are trying to control the profuse bleeding under support of an oxygen machine! But…” (Huyu mgonjwa tatizo lake ni kubwa, lakini hatujakata tamaa, bado tunajaribu kudhibiti damu inayovuja vibaya huku tukiwa tumemwekea mashine ya oksijeni! Lakini…) aliongea Dk. Mwinula.

“Yes, I am listening, go ahead Doctor! Have you confirmed your diagnosis that this is Haemophilia?” (Ndio, nakusikiliza, endelea! Umekwishathibitisha kuwa tatizo ni Hemofilia?)

“Not yet, anyway that is what we are thinking about, though we need to do a lot of lab investigations, family history is also very important, Blandina is there any history of profuse bleeding in your family?” (Bado, lakini hicho ndicho tunachokifikiria, ingawa tunahitaji kufanya uchunguzi zaidi, historia ya familia pia itasaidia, Blandina kuna watu katika familia yako walishawahi kupatwa na tatizo la kuvuja damu sana?) Dk.Mwinula alimuuliza Blandina.

“Why are you asking that question doctor?” (Kwanini unauliza swali hilo daktari?)

“Haemophilia is one of the hereditary diseases! It tends to run in families” (Hemofilia ni moja ya magonjwa ya kurithi! Una tabia ya kuandama watu wa familia moja)

“Yes, I was told that my grandmother cut herself with knife and bled to death many years ago!” (Ndio, niliwahi kuwambiwa kuwa bibi yangu alijikata na kisu akavuja damu mpaka kufa miaka mingi iliyopita!)

“Oh!My God, then you might be right!” (Oh! Mungu wangu, kama hivyo ndivyo basi mnaweza kuwa sahihi!) Dk. Ringo alimwambia Dk. Mwinula.

“We need to do investigations as quickly as possible!” (Tunahitaji kufanya uchunguzi haraka iwezekanavyo!)

“What will happen if you find out that Genesis is having Haemophilia?” (Kitatokea nini kama mkigundua kwamba Genesis ana Hemofilia?) Blandina aliuliza, muda wote waliongea kiingereza utafikiri hawakuwa Watanzania.

“The only thing we can do at the moment is to put her under oxygen while we continue with blood transfusion, injectable coagulants and take a bone marrow specimen for laboratory investigation, unfortunately we don’t have the equipments here, so the sample will have to be taken to South Africa and have the results!” (Kitu pekee tunachoweza kufanya kwa sasa ni kuendelea kumpa hewa ya Oksjeni wakati huo tukiendelea kumwongezea damu na kumchoma sindano za kugandisha damu na tutachukua sehemu ndani ya mfupa wake kwa ajili ya kwenda kupima, bahati mbaya hatuna maabara ya kufanya kazi hiyo, hivyo tutapeleka Afrika Kusini na tutapata majibu ndani ya muda wa siku tatu!)

“Mungu wangu, mtoto wangu atakuwepo kweli mpaka majibu yarudi?”

“Mungu atasaidia!”

“Mkishathibitisha?”

“Kwamba?”

“Yaani majibu yakirudi na kuonyesha ana tatizo hilo?”

“Atatakiwa kufanyiwa upasuaji unaoitwa bone marrow transplant!”

“Ni nini hiyo daktari?”

“Kubadilisha uboho wa mifupa yake!”

“Mh! Sio gharama kubwa?”

“Ni kubwa, bahati mbaya tena upasuaji huu hauwezi kufanyika hapa!”

“Mpaka wapi?”

“Johannesburg, Afrika Kusini!”

“Mungu wangu, itagharimu shilingi ngapi?”

“Sio chini ya dola elfu kumi na tano, mara ya mwisho kuna mtoto nilimtuma huko alitumia karibu kiasi hicho cha fedha!”

“Akapona?”

“Anaendelea vizuri!”

Blandina akamwangalia Dk.Ringo usoni, baada ya hapo akili yake ikaenda moja kwa moja kwenye akaunti yake benki ya Dar es Salaam Community Bank, akakiona kiasi kilichokuwepo na kugundua hakikuzidi hata shilingi milioni moja! Pale pale akakata tamaa, kimbilio pekee alilokuwa nalo ni ofisi kwake, ilikuwa ni lazima aende kuongea na Mkurugenzi wake kuona kama angeweza kukopeshwa kiasi cha fedha ili kimsaidia katika matibabu ya mwanae, alipofikiria muda mfupi aliofanya kazi na mkopo aliokuwa akihitaji zaidi ya shilingi milioni kumi na nne, akakata tamaa kabisa na kujikuta akilifuta wazo la kuomba mkopo ofisini.

“I am going to get this money, for Genesis I will do anything to save her life!” (Nitazipata fedha hizi, kwa mwanangu Genesis niko tayari kufanya lolote!) Blandina alijisemea moyoni akibubujikwa na machozi, hakujua zilikuwa wapi lakini aliamini zipo.



Baada ya hapo akaomba aruhusiwe kuingia ndani kumwona mwanae, daktari hakuwa na kizuizi akawataka wasubiri kwa dakika chache apate kuangalia kitu gani kilikuwa kikiendelea chumbani kwa wakati huo, alipofungua mlango baadaye zilikuwa zimepita kama dakika tano, akawaruhusu waingie. Blandina alipomwona mwanae alishindwa kusimama kidete, picha ilikuwa inatisha, mashuka yalikuwa yamelowa damu, matundu yote ya pua yakiwa yamefunikwa na pamba ambazo hata hivyo zote zilikuwa zimebadilika na kuwa nyekundu!



Genesis alionekana katika hatua za mwisho kabisa za uhai wake kama jambo la maana lisingefanyika, Blandina alielewa jukumu alilokuwa nalo, kuokoa maisha ya mtoto wake. Akapiga magoti kando mwa kitanda na kuanza kusali akimwomba Mungu amsaidie kukusanya kiasi cha fedha kilichohitajika, aliponyanyuka macho yake yalikuwa makavu tofauti na alipofumba.



“Sitalia tena, kulia hakunisaidii lazima niwe zaidi ya mwanamke, nitafute fedha zinazohitajika kuokoa maisha ya mtoto wangu!” alisema Blandina akimwambia Dk. Ringo kwa sauti ya chini.

“Tutazipata wapi?”

“Unaweza kuniangalizia mtoto mimi nikazunguke mitaani!”

“Hakuna shida, lakini itanibidi niwataarifu ofisini juu ya jambo hili ili nipate angalau ruhusa ya siku tatu!”

“Sawa, nenda basi ofisini halafu ukirejea ndipo mimi nitaondoka!”

Wote wawili wakatoka nje ya chumba cha wagonjwa mahututi na kuwaacha madaktari wakiendelea kumshughulikia Genesis, Dk. Ringo hakukaa, akaondoka hadi kwenye gari lake ambako aliwasha na safari kuelekea hospitali ya Muhimbili ikaanza. Muda mfupi tu baada ya Dk. Ringo kuondoka, Blandina alishuhudia mlango wa chumba ukifunguliwa, machela ikatolewa ikiwa inasukumwa, alipowaangalia wauguzi usoni mwao, akagundua kitu! Hakuhitaji tena kumuuliza mtu juu ya nini kilikuwa kimetokea, ahadi yake ya kutokulia ikafutika, MACHOZI YAKAMTOKA.

“Baada ya mateso ya muda mrefu, hatimaye Mungu ameninyang’anya mwanangu!” Aliongea machozi yakilowanisha mashavu yake.

“Blandina!” Muuguzi mmoja alimwita.

“Bee!”

“Unatakiwa uwe na moyo wa uvumilivu…!”

****

“Blandina!” Muuguzi aliyekuwa akisukuma machela alisema.

“Bee!” akaitikia.

“Unatakiwa uwe na moyo wa uvumilivu, mtoto wako bado hajafa, tunampeleka chumba cha upasuaji ili madaktari wachukue kipimo kwenye mfupa wake ili upelekwe Afrika Kusini kwa ajili ya uchunguzi kuthibitisha kile ambacho wanafikiri ni tatizo la mwanao, safari ya kumuuguza Genesis ni ndefu, inabidi uvute subira sana mwanagu!” Aliendelea kuongea mama huyo mwenye umri sawa kabisa na mama yake Blandina.



“Fuuuuuh!” Blandina akashusha pumzi kwa nguvu zake zote, huku furaha ikimrejea moyoni, kitendo cha kugundua Genesis alikuwa bado akipumua kilikuwa ni faraja mno kwake.

Alitembea harakaharaka mpaka akaifikia machela na kuinamisha kichwa chake, akambusu mwanae usoni na kumtakia Afya njema, alimtia huruma kila mtu aliyemwona. Hakukomea hapo Blandina aliifuata machela mpaka nje ya chumba cha upasuaji, akaketi kwenye benchi peke yake mpaka dakika ishirini baadaye Dk. Ringo alipoungana naye.

“Vipi?”

“Ameingizwa humo ndani!”

“Kuna nini?”

“Wanachukua kipimo!”

“Blandina usiwe na wasiwasi, mimi najua Genesis atapona!”

“Ahsante sana kwa faraja zako kaka Ringo, lakini ataponaje bila kuwa na fedha?”

“Mungu atasaidia, fedha zitapatikana!”

“Amina!”

Walibaki nje ya chumba cha upasuaji kwa saa nzima, ndipo Genesis akatolewa na kurejeshwa wodini ambako aliendelea kuongezewa damu na kupumua kwa kutumia mashine, wakisubiri majibu yarejee kutoka Afrika Kusini. Yalipokuja siku tatu baadaye, hakuna kilichokuwa kimekosewa, ni kweli Genesis alikuwa na ugonjwa wa Haemophilia, uboho katika mifupa yake haukuwa na uwezo wa kutengeneza chembechembe sahani zenye uwezo wa kukausha damu kila ilipokuwa ikivuja. Blandina alibubujikwa na machozi hasa alipofikiria gharama ya matibabu.



Taratibu za safari zilianza kufanyika, Blandina na Genesis hawakuwa na hati za kusafiria ilibidi mara moja suala hilo lianze kushughulikiwa na Dk.Ringo. Wakati Ringo akifanya kazi hiyo, Blandina alilazimika kumwacha mtoto wake chumba cha wagonjwa mahututi na kwenda hadi ofisini kwake ambako alipata nafasi ya kuongea na Mkurugenzi wake, alimweleza shida zote alizokuwa nazo na kuomba ofisi imkopeshe kiasi cha shilingi milioni kumi na tano ambazo angezirejesha taratibu baada ya mtoto wake kupona. Alipotamka kiasi hicho cha fedha, Mkurugenzi alionyesha mshtuko wa ajabu usoni kwake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Kiasi gani?”

“Milioni kumi na tano!”

“Mh! Blandina, yaani umefanya kazi miezi mitatu tukukopeshe milioni kumi na tano?”

“Nina shida Mkurugenzi, mwanangu anaumwa sana, nisaidie niokoe maisha ya kiumbe hiki, nitafanya kazi hapa mpaka deni hilo liishe, sitahama!”

“Sawa lakini ni nyingi sana, nikijitahidi mno naweza kukukopesha milioni tatu!”

“Mungu wangu! nitazitoa wapi nyingine masikini mimi?”

“Wazazi wako wako wapi?”

“Walishafariki!” Ilibidi Blandina adanganye kwani angemtaja mzazi wake kwa jinsi alivyokuwa tajiri, mabasi yakipita kila siku barabarani yaliyoandikwa jina lake kati ya Dar es Salaam, Morogoro na Kilosa, Mkurugenzi asingeamini kuwa aliyekuwa akiongea naye ndiye mtoto mkubwa wa familia hiyo.

“Pole sana, ndugu wengine?”

“Sina ndugu!”

“Mh! Inawezekanaje Blandina?”

“Wazazi wangu walikuwa wakimbizi, naomba unisaidie Mkurugenzi mambo mengine tutayaongea nikirejea kutoka Afrika Kusini, naahidi fedha hizo nitazilipa!” akasema Blandina akinyanyuka kitini na kupiga magoti mbele ya Mkurugenzi wake huku machozi yakimbubujika.

“Sawa lakini ni nyingi, kifupi siwezi kukupa zaidi ya milioni tatu na nusu, hiyo ni kwa maagizo ya bodi, zaidi ya hapo lazima bodi ikae na huwa inakaa baada ya mwezi mmoja!”

“Fuuuuuuh!” Blandina akashusha pumzi tena na akili yake ikamrudisha tena wodini, akamwona Genesis akiwa amejazwa pamba puani kuzuia damu isiendelee kutoka, hakutaka kukata tamaa kabisa, ilikuwa ni lazima mtoto wake apone, kama tiba ilikuwepo Afrika Kusini kumpeleka lilikuwa jambo la lazima.



“Ahsante Mkurugenzi, umenisaidia kiasi cha kutosha, mchango wako nitaukumbuka siku zote za maisha yangu, wacha niende mtaani kuhangaika!” Aliongea Blandina akinyanyuka.



“Gari liko wapi?”

Alipoulizwa swali hilo Blandina alikaa kimya, alikuwa amesahau mahali gari lilipokuwa, sekunde chache baadaye alikumbuka mahali alipokutana na Dk. Ringo akiwa na Genesis kwenye gari wakielekea hospitali, hapo ndipo alipoliacha gari na kuingia kwenye gari la Ringo! Hakulikumbuka tena, hata funguo zake hakuelewa mahali zilikokuwa.

“Liko nyumbani!”

“Kwanini huendeshi?”

“Siwezi, dereva wangu alikuwa anaumwa!”

“Tukupe gari jingine, unakwenda wapi?”

“Mikocheni!”

“Acha basi dereva wangu akupeleke, ukitoka huko upite hapa tukupe hiyo fedha!”

“Ahsante Mkurugenzi!”

Wakaagana, Blandina akatoka nje ya jengo ambako alisimama kwa muda akitafakari juu ya wapi pa kwenda baada ya hapo, alipomfikiria vizuri shangazi yake wa Mikocheni alikotaka kwenda alielewa wazi asingesaidiwa chochote kwa jinsi familia yake ilivyokuwa na msimamo inapomtenga mtu.

Gari lilipokuwa tayari alimwambia dereva ampeleke Wizara ya Afya akajaribu bahati yake, kwenye jengo la Wizara hiyo mtaa wa Samora karibu na Chuo cha Usimamizi wa Fedha, aliomba kuonana na Mganga Mkuu wa Wizara, Dk. Gabriel Mapunda, alipokutana naye baada ya kusubiri karibu saa nzima alielezea shida yake.

“Mh! Sijui kama tutakusaidia, unaiona ile orodha pale?” Aliongea daktari huyo akisonta ukutani, kulikuwa na makaratasi yenye orodha ndefu ya majina ya watu.

“Ndio!”

“Hao wote wanasubiri kwenda nje kutibiwa, tunasubiri fungu litoke waanze kwenda kwa zamu, nikikuchukua wewe inabidi nikuingize hapo chini, nafikiri itakuchukua kama miezi sita ijayo kupata nafasi!”

“Miezi sita? Wakati mgonjwa wangu anakufa? Mbona unaongea mambo ya ajabu daktari?” Blandina alifoka bila kuogopa.

“Huo ndio ukweli binti!”

Akanyanyuka na kufunga mlango kwa nguvu kisha kutoka nje, wala hakumuaga Katibu Mhutasi wake na kwenda moja kwa moja hadi nje kwenye gari. Kulikuwa na sehemu moja tu ambayo angeweza kwenda kujaribu tena, hakupenda kabisa kwenda sehemu hiyo lakini hakuwa na jinsi, alikuwa tayari kufanya lolote hata kama ni jambo la aibu kiasi gani lakini aokoe maisha ya mtoto wake, ilikuwa ni nyumbani kwa Gerald, ambaye kwa vyovyote alikuwa na kila sababu ya kumsaidia akiamini pengine alikuwa baba wa Genesis.

Akamwelekeza dereva mpaka nyumbani kwa Gerald na wakaongozana na kuegesha mbele ya nyumba, akakumbuka kila kitu kuhusu nyumba hiyo! Lakini hayo hayakuwa na umuhimu tena, akamwacha dereva kwenye gari na kuanza kutembea kuelekea langoni, uzuri ilikuwa ni siku ya Jumapili, lazima wangekuwepo nyumbani. Akaanza kugonga, hakuchukua hata dakika tano , mlango ukafunguliwa, alikuwa ni Grace.

“Vipi umekuja kulipa fedha za matengenezo ya gari?” Grace alimuuliza kabla hata ya salamu.

“Hapana, namhitaji Gerald!”

“Wa nini, lete fedha za watu nikachukue gari langu!”

“Nitalilipia baadaye, hivi sasa nina matatizo makubwa!”

“Matatizo yako ndiyo uyalete kwa mume wangu?”

Kabla hawajaendelea sana, Gerald alifika na kumkuta Halima langoni, Grace akaondoka na kuwaacha wawili wakiongea, Blandina akamwelezea Gerald kila kitu na kumwomba amsaidie hata kama hakuwa baba wa Genesis ili aweze kuokoa maisha ya mtoto.

“Mimi sio baba wa mtoto wako, mtafute Adebayor!”

“Gerald kuwa na huruma kidogo, nikopeshe basi nitakurudishia!”

“Mimi? Nikukope…!” Kabla hajamaliza sentensi yake, Landrover 110 ya Polisi iliegesha kando yao, hawakujua kama Grace alikuwa amewasiliana na polisi, kwa muda polisi walikuwa wakimtafuta baada ya Grace kutoa taarifa polisi kwamba mtu aliyemgonga alikimbia lakini akamtaja kwa jina.

“Yuko wapi huyo mwanamke mwenye kiburi, anagonga magari ya watu halafu anaondoka?” Aliongea askari mmoja akionyesha hasira, ilivyoonekana Grace alikuwa amewajaza maneno mengi ya uongo juu yake, kabla hajasema chochote akapigwa kibao usoni.

“Huyu hapo!” Grace akaongea baada ya kutokeza, Blandina akapigwa pingu mkononi na kupandishwa kwenye gari huku machozi yakimbubujika hasa alipomfikiria mtoto wake wodini na juhudi za kuokoa maisha alizokuwa akizifanya.

“Jamani nina mwanangu anaumwa!”

“Weeee! Wacha usanii, twende utajieleza mbele ya safari!”





Ukiumuuliza Blandina kuhusu maisha, hakuna anachoweza kukueleza zaidi ya huzuni! Kwani hicho ndicho anachokifahamu na yote hiyo imetokana na mapenzi. Mwanamke huyu alizaliwaa akiitwa Halima, kwenye familia ya mfanyabiashara maarufu mkoani Morogoro. Akiwa shule ya msingi alikutana na mvulana aitwaye Gerald, penzi likazaliwa kati yao na wakaendelea nalo mpaka wakiwa sekondari.



Baada ya kumaliza elimu ya sekondari, Gerald akapotelea nje ya nchi alipomfuata baba yake aliyekuwa balozi, hii ilifanya Halima akiwa Chuo Kikuu aanze uhusiano na mvulana mwingine aitwaye Dk. Othman, baadaye Gerald alierejea akiwa na hali mbaya tena siku hiyo ndiyo Dk.Othman alikuwa akienda kumvisha Halima pete ya uchumba. Kumwona Gerald, Halima alibadilisha mawazo, akagoma kuvishwa pete ya uchumba na kurejea kwa mvulana wake wa zamani.



Hii ilikuwa ni aibu kubwa kwa Dk. Othman, ambaye alifikia uamuzi wa kufanya mipango ya kumuua Gerald ili ambakize Halima mikononi mwake, kitendo ambacho hakikufanikiwa na kujikuta akitupwa mahabusu ambako aliamua kujinyonga.

Baadaye Gerald anaugua na Halima anatoa figo yake moja kuokoa maisha yake, wazazi wake waliokataa hilo lisifanyike wanachukizwa na kitendo hicho. Kama vile hiyo haitoshi, Halima aliamua kubadilisha dini baadaye na kuolewa na Gerald, jina lake likawa Blandina.



Bila huruma yoyote akiwa amesahau wema wote wa Blandina, Gerald anaamua kumlewesha mke wake kwa dawa za kulevya na kumuuza kwa bosi Adebayor ili apandishwe cheo. Hilo linatokea, anapandishwa cheo lakini mke wake anapata mimba ambayo anajifungua mtoto mwenye maumbile ya ajabu, ndipo Gerald akaamua kumfukuza Blandina pamoja na mwanae akidai mtoto huyo alikuwa ni wa Adebayor, uamuzi huu unafikiwa baada ya Blandina kukataa kumuua mtoto huyo, Genesis.



Hapo ndipo taabu na shida zinaanzia, Blandina anahangaika na mtoto wake huku na kule duniani, hospitali hadi hospitali, pamoja na elimu yake ya chuo kikuu akiwa amesoma sheria anaonekana ni sawa na mtu ambaye hajasoma! Mwisho anakutana na Dk. Ringo, rafiki mkubwa wa Dk. Othman, huyo anamtafutia kazi na maisha yake yanarejea katika mstari kwa muda mfupi kabla Genesis hajaanza kuumwa tena, safari hii ugonjwa wa kuvuja damu unaohitaji mamilioni ya fedha kwenda kutibiwa nchini Afrika Kusini. Blandina hana fedha hizo, anaomba ofisini kwao ambako wanakubali kumpatia milioni tatu na nusu kati ya kumi na tano zinazohitajika, alipotoka hapo hakuwa na mahali pengine pa kwenda isipokuwa kwa Gerald, siku chache kabla alikuwa amegonga gari la Grace, mke wa Gerald na kuahidi kulitengeneza. Alipoonekana tu nyumbani kwao, simu ilipigwa polisi, wafika na kumtia pingu. Je, nini kinaendelea?



“Jamani nina mwanangu anaumwa!” Blandina alilia akisukumwa kwenda mbele, Grace na mume wake walikuwa wakicheka.

“Weeee, wacha usanii, twende utajieleza mbele ya safari!”

Kama utani, Blandina akapakiwa ndani ya gari la polisi Landrover 110 na kukalishwa chini, bado aliendelea kulia akimwomba Gerald amtoe mikononi mwa askari hata kama alikuwa amewakosea kitu gani sababu alikuwa katika wakati mgumu sana maishani mwake, aliyasema hayo gari la polisi likigeuzwa.

“Si ulijifanya una nyodo, eti una dola? Ukatuachia kikadi chako tukupigie, tumepiga sasa, pokea!” Grace aliongea kwa kejeli nyingi.

“Grace naomba unihurumie, kuwa na moyo wa kumfikiria mwanamke mwenzako, nina matatizo mwanangu anaumwa, nikitoka hospitali nitalipa!”

“Toka hapa, yule naye ni mtoto? Tuulize sisi wenye watoto!”

Gari likaondoka kwa kasi hadi kituo cha polisi cha Kijitonyama, ambako Blandina aliingizwa ndani na kukalishwa chini, alichojifunza ni kwamba kulikuwa na ushawishi mkubwa sana wa Grace na mume wake, fedha ilikuwa imetembezwa kiasi cha kutosha! Kwani hakuna askari hata mmoja aliyekubali kusikiliza maelezo yake juu ya mtoto kuwa mgonjwa, akaanza kupekuliwa, simu yake ikachukuliwa na kuzimwa ili kusiwe na mawasiliano kati yake na mtu yeyote.

“Njoo tuchukue maelezo yako!”

“Siwezi kuongea bila Mwanasheria wangu kuwepo!”

“Paaa!” Ulikuwa ni mlio wa kibao shavuni mwake.

“Kwanini unanipiga? Ina maana wewe hujui kama nina haki ya kuwa na Mwanasheria?

“Unajifanya mjanja sio? Nyanyuka!” askari huyo aliongea na kuanza kumsukuma Blandina kuelekea nyuma kulikokuwa na lango kubwa la nondo, likafunguliwa na akasukumwa kuingizwa ndani ambako alipokelewa na wanawake wengine.

“Kwani vipi anti?” mwanamke alimuuliza.

“Eti kesi ya trafiki tu, wananiweka mahabusu wakati nauguliwa na mtoto wangu hospitali, nimetaka kuwa na mwanasheria hawataki kunisikiliza, badala yake wananipiga!”

“Pole sana, hapa ndivyo mambo yalivyo, njoo ukae hapa!” Mwanamke huyo alimwita Blandina, akamsogelea na kuketi chini kulipolowa na kitu ambacho hakuelewa kilikuwa ni jasho, maji au mkojo.

Mara moja kumbukumbu zake zikamrejesha hospitali, akamwona Genesis akihangaika kitandani, moyoni akafahamu mtoto wake angekufa bila yeye kuwepo. Aliumia mno na kujikuta akiahidi kutomsamehe Gerald, mambo aliyokuwa amefanyiwa sasa yalikuwa yamemfika puani, ulikuwa ni unyama uliokithiri, kumweka ndani wakati mtoto anaumwa? Blandina alijikuta akiuahidi moyo wake kwamba angelipa kisasi wakati fulani maishani mwake kama Genesis angekufa.



Alikaa ndani mpaka usiku wa manane bila kupata usingizi wala kufumba macho, hakuwa na namna yoyote ya kuwasiliana na ulimwengu wa nje na alielewa wazi mpaka wakati huo Dk.Ringo alikuwa akimtafuta sana, alitamani sana kuwasiliana naye ili angalau ajue mtoto wake alikuwa akiendeleaje lakini jambo hilo lilikuwa haliwezekani.

“Anti mimi nitatoka leo, nielekeze tu mahali ndugu zako waliko nitawapelekea taarifa!” alisema mwanamke aliyeketi jirani yake, alfajiri jogoo alipowika.

“Unaitwa nani anti?”

“Mimi? Naitwa Monica”

“Mimi naitwa Blandina, kama ukitoka naomba uende hospitali ya Lugalo, muulizie pale Daktari aitwaye Mwinula au Ringo, ukiwakosa wote hao nenda chumba cha wagonjwa mahututi, mwanangu amelazwa pale anaitwa Genesis! Ukiwapata waambie mahali uliponiacha, nitakushukuru sana!”

“Sawa anti, mimi kesi yangu ndogo tu, asubuhi hii lazima nitawekewa dhamana!”

“Kesi gani?”

“Aa! Mwanamke mmoja aliniletea huu bombani, nikampa mambo, kavimba uso ndio kanileta hapa!”

“Pole!”

Asubuhi ya siku hiyo kweli kama alivyosema mwanamke huyo, alitolewa kwa dhamana, saa nzima tu na nusu baada ya kuondoka kwake, Blandina alishtukia akiitwa na kutoka mahabusu, Dk. Ringo alikuwa kaunta akimsubiri, alishamwekea dhamana lakini hakuruhusiwa kuondoka mpaka atoe maelezo yake, Blandina hakuwa na ubishi tena kwa sababu alitaka kumwona mtoto wake hospitalini, baada ya maelezo akatoka nje na kupokelewa na dk. Ringo.

“Pole!”

“Ahsante! Mwanangu anaendeleaje jamani?”

“Vile vile tu!”

“Kweli?”

“Ndio!”

“Niambie ukweli Ringo!”

“Sina sababu ya kukudanganya!”

“Hati za kusafiria?”

“Unatakiwa kutia saini kwenye fomu ndipo nikazichukue, fedha?”

“Sijapata, nikwenda kwa Gerald kuomba msaada ndipo akaniitia polisi!”

“Sababu?”

“Bahati mbaya siku uliponipigia simu niligonga gari yao!”

“Pole sana!”

“Usijali, lazima nipitie kwenye mambo hayo ili niifahamu dunia vyema!”

Dakika arobaini na tano baadaye tayari walishafika hospitali ya Lugalo, Blandina akaruka kabla gari halijasimama vizuri na kuanza kukimbia kuelekea wodini ambako alimkuta mtotowake bado akihangaika kitandani, damu zikimtoka puani! Akainamisha kichwa na kumbusu, daktari aliyekuwa jirani alimsogelea.

“Blandina!”

“Bee daktari!”

“Vipi? Umepata fedha?”

“Bado!”

“Mungu wangu, jitahidi!”

“Nina milioni nne na nusu tu daktari, tena tatu na nusu lazima nizifuate ofisini kwetu!”

“Lakini leo ni sikukuu!”

“Sikukuu gani?”

“Uhuru, umesahau kwamba leo ni 9 Desemba?”

“Nitakumbukaje na matatizo yote niliyonayo daktari?” akasema Blandina, hapo hapo wazo likamwijia kichwani mwake, kwa wazo hilo aliamini fedha zingepatikana, akamwita Dk. Ringo pembeni.

“Vipi?”

“Sikiliza Ringo, ni lazima niokoe maisha ya mtoto wangu, siwezi kukubali Genesis afe, ni bora nife mimi! Naondoka, nikirudi hapa lazima fedha ziwe zimepatikana, Tanzania ina fedha nyingi mno, haiwezekani mwanangu akafa, angekuwa mtoto wa Waziri angekufa kwa kukosa fedha?”

“Sio rahisi!”

“Basi kaa na mwanangu, utanisikia baadaye kwenye bomba, leo lazima unisikilize kwenye taarifa ya habari!”

“Ukifanya nini? Ukichangisha?”

“Hapana, wewe subiri tu!”

“Ok, lakini usifanye jambo baya!”

“Naomba ufunguo!”

“Utaweza kuendesha?”

“Ndio!”

Nusu saa baadaye alikuwa akiegesha gari lake nje ya uwanja wa Taifa ambako maadhimisho ya uhuru wa Tanganyika yalikuwa yakiendelea, akashuka na kuingia uwanjani, Rais alikuwa akimalizia hotuba yake, Blandina hakutaka kukaa mahali walikoketi wananchi wa kawaida, akafunikiwa kupenya wavu na kwenda mbele kisha kuanza kujisogeza taratibu mpaka sehemu waliyokuwa wameketi waandishi wa habari, hakuna aliyemshtukia. Muda wote akibubujikwa na machozi, hasa alipomkumbuka mwanae wodini.

Sherehe zilipokwisha Rais, Rais alishuka ngazi taratibu kuelekea kwenye gari lake, waandishi wakaanza kulisogelea, Blandina akiwa miongoni mwao, gari lilipokuwa kama mita tano kutoka walipokuwa alikimbia na kujitupa chini ya gari la Rais na kupotelea ndani! Tayari waandishi wa habari walikuwa wakipiga picha, maaskari wakazama chini na kuanza kumvuta huku wakimpiga.

“Niueni lakini mwanangu lazima apelekwe Afrika Kusini kutibiwa!”

*****

Lilikuwa ni jambo la ajabu mno, Maafisa Usalama na walinzi wa Rais walishindwa kabisa kuelewa mwanamke huyo alikuwa amepitia wapi mpaka kufanikiwa kuingia chini ya benzi ya Rais. Kwa nguvu zao zote wakaanza kumvuta miguu ili atoke huku wengine wakimpiga lakini mwanamke huyo hakuachia chuma alichokishika chini ya gari huku akilia na kudai alikuwa tayari kufa lakini mtoto wake aishi. Tayari Rais akawa amekwishafika karibu kabisa na gari na kuanza kushangaa ni nini kilikuwa kikiendelea, mabosi wa usalama walijaribu kuziba ili asione lakini tayari kwa purukashani zilizokuwepo huku waandishi wakipiga picha kwa ajili ya magazeti, redio na televisheni, haikuwa rahisi kumficha kiongozi wa nchi.



Kwa nguvu nyingi sana, walifanikiwa kumng’oa Blandina chini ya gari, virugu kadhaa vikatua kichwani mwake na kumpasua na kufanya damu ianze kumvuja ikilowanisha nguo zake, lilikuwa ni tukio la kusikitisha lililomfanya Rais anyooshe mkono wake juu na kumwita Mkurugenzi wa usalama wa Taifa Bw.Abrahaman Maalim aje karibu yake.

“Acheni kumpiga, mpelekeni hospitali mara moja kisha mumlete Ikulu, nataka kuongea naye! Unasikia?”

“ Sawa Mheshimiwa Rais!”

“Vijana wako wanatumia nguvu nyingi sana hata mahali panapohitaji kutumia nguvu kidogo!”

Mlango ukafunguliwa, Rais akaingia ndani ya gari na kuanza kuondoka kuelekea Ikulu kwenye msafara wake uliolindwa kila upande, dakika arobaini na tano tu baadaye, Blandina akiwa amefungwa bendeji kichwani aliingia Ikulu ya Tanzania, akiongozwa na Mkurugenzi wa Usalama, Mkuu wa Jeshi la Polisi na Mkuu wa jeshi la wananchi, wote walionekana kama wanamlinda. Ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Blandina kuingia Ikulu, mwili wote ulikuwa ukitetemeka, alikuwa kimya kabisa bila kuongea chochote, kichwani akimfikiria mtoto wake kitandani hospitali ya Lugalo, hakuwa na uhakika kama mpaka wakati huo alikuwa bado akipumua.

Wote wakaingia ndani ya chumba cha Mkutano na kuketi vitini, wakiwa kimya kabisa, hata wakuu wa majeshi hawakuongea chochote, ilivyoonekana hata wao pia walimwogopa sana Rais. Dakika kama tano hivi tangu waingie, mlango wa pembeni ulifunguliwa, Rais akaingia akiongozana na katibu wake bwana George Msomi, usoni akiwa amejawa na tabasamu tofauti kabisa na alivyotegemea Blandina.



“Pole dada yangu!” ndivyo alivyoanza kusema Rais baada ya kuketi, badala ya kuitikia Blandina alinyanyuka kitini, akapiga magoti mbele ya Rais na kuanza kulia kwa uchungu.

“ Nyanyuka tu, usinisujudu mimi sio Mungu, una tatizo gani dada?”

“Mwanangu anakufa!”

“Kwanini?”

“Ana ugonjwa wa Haemophilia, damu inamvuja puani bila kukoma, anatakiwa kupatiwa matibabu nchini Afrika Kusini ambayo gharama yake ni milioni 15, lakini sina hata senti moja, nimejaribu kutafuta msaada Wizara ya Afya nikaambiwa nisubiri mpaka baadaye wakati mtoto wangu anakufa, utanisamehe Mheshimiwa Rais kwa yote niliyoyafanya, najua unaweza kuamua nipelekwe jela, naomba usifanye hivyo, nihurumie, nihurumie, nihurumie mimi na mwanangu Genesis!”

“Umeolewa?”

“Niliwahi kuolewa lakini mume akaniacha baada ya kuzaa mtoto mwenye ulemavu!” akajibu Blandina na baadaye kuendelea zaidi akisimulia namna alivyokutana na Gerald, akamtaja pia baba yake na Rais akaonekana kumfahamu, alivyompa Figo yake, Rais akalikumbuka tukio hilo lililotokea kabla yeye hajaingia madarakani.



Katika hali ya kushangaza kabisa, watu wote ndani ya chumba walishuhudia Rais akichomoa kitambaa cheupe kutoka mfukoni mwake na kuanza kujifuta usoni, hawakuelewa ilikuwa ni jasho au kitu gani, walipomwangalia vizuri wakagundua macho yake yalikuwa mekundu, historia ya Blandina ilikuwa imemchoma kama Mkuki moyoni.



Alichofanya mbele ya Blandina, Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Mkuu wa Jeshi la polisi na Mkuu wa Jeshi la wananchi ni kumuagiza katibu wake, haraka sana ampigie simu Waziri wa Afya ili afike Ikulu mara moja kwa mazungumzo, maagizo ya Rais yakatekelezwa haraka, dakika kumi tu baadaye Waziri wa Afya aliingia na kuketi baada ya salamu za heshima.

“Mheshimiwa Waziri wa Afya!”

“Mheshimiwa Rais!”

“Unaweza kunisaidiaje mtoto wa huyu dada apelekwe Afrika Kusini kwa matibabu, alishakuja ofisini kwako lakini hakushughulikiwa vizuri, nafikiri ni sababu ya hili tatizo tunalopambana nalo; Rushwa! Mtoto wake amelazwa katika hospitali ya Lugalo, anaugua ugonjwa uitwao Haemophilia, madaktari wanasema lazima apelekwe Afrika Kusini haraka iwezekanavyo, nimekutana naye Uwanja wa Taifa, kwa kweli historia yake imenisikitisha sana, hii inanipa changamoto kwamba ni lazima tuhakikishe tunashughulikia uboreshaji wa huduma zetu za afya, hii ni aibu, hivi hatuna wataalam wakutibu tatizo hili hapa nchini?”

“Wapo Mheshimiwa Rais, hata mimi mwenyewe ni mtaalam wa magonjwa hayo, tatizo ni vifaa, hii ni sawa kabisa na ugonjwa wa moyo, leo hii ni arobaini tangu tupate uhuru wetu lakini magonjwa ya moyo yanasumbua nchi, kila mgonjwa lazima tumpeleke nje ya nchi wakati tuna wataalam wa kutosha hapa nyumbani!”

“Hii ni aibu! Nitalishughulikia suala hili, haraka iwezekanavyo kwani tumekwishatumia fedha nyingi sana kupeleka watu wetu kufanyiwa upasuaji wa moyo!”

“Itakuwa vizuri Mheshimiwa Rais, maisha ya watu wengi sana yatakuwa yameokolewa!”

“Kwa hili la huyu dada unanisaidiaje?”

“Acha niondoke naye hadi hospitali ya Lugalo Mheshimiwa Rais, tutajitahidi kadri ya uwezo wetu kuokoa maisha ya mtoto wake!”

“Haya mkutano wetu umekwisha!” Rais aliongea na kunyanyuka.



****

Blandina alipoingia hospitali ya Lugalo, kichwani akiwa amefungwa bendeji zilizolowana damu na uso wake umevimba sababu ya kipigo, akiongozana na ujumbe kutoka Wizara ya afya, si Ringo tu aliyeonyesha mshtuko bali hospitali nzima! Hakuna aliyetegemea mchana wa siku hiyo wangetembelewa na Waziri wa Afya tena bila taarifa, madaktari walianza kukimbia huku na kule wakikusanyana na kwenda wodini alikolazwa Genesis, akiwa bado katika hali mbaya.



Mkutano ulifanyika wakiwa wamekizunguka kitanda cha mgonjwa, Dk. Ringo na Blandina wakiwa nje ya wodi ambako Blandina alimsimulia kila kitu kilichotokea, Ringo akafunika mdomo wake kwa kiganja, kuonyesha wazi mshtuko alioupata. Hakutegemea kabisa, Blandina angekuwa na ujasiri kiasi hicho; kuingia chini ya gari la Rais, lilikuwa ni jambo la hatari mno ambalo kwa hakika lingeweza kusababisha apoteze maisha yake, alichojua Blandina ni juu ya jinsi alivyokuwa tayari kufa lakini mtoto wake aokoke.

Ghafla mlango ukafunguliwa, Waziri wa Afya akatoka akiongozana na ujumbe wake, safari hii alikuwepo daktari aliyekuwa akimtibu Genesis, Dk. Mwinula, huyo ndiye aliyesimama mbele yao na kuwaeleza kila kitu juu ya mpango uliokuwa umeandaliwa kwenda Afrika Kusini kwa matibabu haraka iwezekanavyo.



“Lini daktari?”

“Tunamuandaa mtoto ili awe katika hali nzuri ya kustahimili safari angani, nina uhakika tutaweza kuifanya kazi hiyo kwa leo na kesho asubuhi tutaanza safari yetu!”

“Atakuwa bado yuko hai?”

“Usitie shaka Blandina, timu ya madaktari wote wa Lugalo watajitahidi kuhakikisha mtoto wako haishiwi damu wala kupungukiwa hewa ya oksijeni mwilini mwake! Sawa?” Waziri wa Afya aliongea.

“Sawa daktari!”

Siku hiyo Blandina alishinda akimwomba Mungu anusuru maisha ya mtoto wake, saa zilikwenda taratibu kuliko siku nyingi zote, akitamani asubuhi ifike. Waliongea mengi na Dk. Ringo wakiwa nje ya wodi kwenye kiti, wakakubaliana Blandina aondoke na mgonjwa hadi Afrika Kusini, Dk.Ringo alijitahidi kadri ya uwezo wake kumwondoa wasiwasi, ukizingatia sasa alikuwa chini ya ungalizi wa Ikulu ya Tanzania, alipongeza sana kwa ujasiri aliouonyesha ingawa ulimgharimu majeraha kichwani na kuvimba uso.



“Kila kitu kizuri kina gharama zake, lazima tuwe tayari kupoteza uhai wetu kwa ajili ya watu wengine, ndivyo walivyofanya mashujaa wa kale, unamkumbuka Yesu Kristo nafikiri, Mahatma Ghandi na Martin Luther King pia, watu hawa walitoa uhai wao kwa ajili ya wenzao ndio maana mpaka leo wanakumbukwa!”



***

Saa kumi na mbili na nusu siku iliyofuata gari la wagonjwa la hospitali ya Lugalo liliwasili uwanja wa ndege wa Dar es Salaam, mgonjwa akashushwa akiwa kwenye kitanda, wauguzi watatu na madaktari wawili walikuwa wakiongozana naye katika safari hiyo kuhakikisha hakuna kitu kingeharibika njiani, damu zingeendelea kudondoka vizuri kuingia kwenye mishipa ya Genesis na pia angepumua bila taabu wakiwa juu angani mpaka wawasili Johannesburg.



Ukaguzi ulipokamilika mgonjwa akapandishwa kwenye ndege na kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi, ambako madaktari na wauguzi waliendelea kumshughulikia kama vile alikuwa bado yuko hospitali ya Lugalo! Walitulia tu ndege ilipokuwa inataka kuacha ardhi, lakini wakiwa angani waliendelea na kazi mpaka wanatua kwenye uwanja wa ndege wa Johannesburg ambako gari la wagonjwa kutoka hospitali kubwa ya Nelson Mandela General Hospital lilikuwa likimsubiri mgonjwa ndani yake kukiwa na wauguzi pamoja na madaktari.



Kilikuwa kitendo cha nusu saa tu kukamilisha kila kitu na kutoka nje ya uwanja, gari likaondoka kwa kasi likipiga ving’ora na kupishwa barabarani hadi hospitali ambako pia madaktari wa idara ya damu iliyoitwa Haematology walikuwa wamewekwa tayari kwa kazi iliyokuwa mbele yao.



Genesis alipopokelewa aliwekwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi huduma za vipimo vikaanza mara moja, siku moja baadaye kila kitu kilishakamilika na ugonjwa wake kuthibitishwa, ili kuokoa maisha yake ilikuwa ni lazima kubadilisha kabisa uboho wa kwenye mifupa yake mikubwa ili kuifanya iwe na uwezo wa kutengeneza chembechembe imara za damu ambazo zingefanya damu iwe inaganda kwa urahisi. Blandina alifurahi mno, kusikia mtoto wake hatimaye angeweza kupona.



“We are facing only one problem!” (Tuna tatizo moja tu!) Daktari aliongea, Blandina akimsikiliza.

“What is the problem? Blood?” (Tatizo gani? Damu?) Blandina akajikuta ameuliza.

“Not blood, but people who will be ready to donate their bone marrows for us to plant in your child’s bones!” (Sio damu, isipokuwa watu ambao watakuwa tayari kutoa uboho wa mifupa yao ili tupandikize kwenye mifupa ya mtoto wako!) daktari mmoja mzungu aliongea, maneno yake yakamrudisha Blandina nyuma kabisa, matumaini yake yakaanza kufutika.

“Cant I be?” (Mimi siwezi kuwa?)

“No!” (Hapana!)

“My God!” (Mungu wangu!) Akatamka Blandina na kuketi chini.

*****

“Huwezi kumtolea mtoto wako Uboho!”

“Kwanini daktari? Si ni mwanangu?”

“Hata kama ni mwanao, mnatofautiana!”

“Nini?”

“Damu zenu ni tofauti, vipimo vilivyochukuliwa vinaonyesha kundi lako la damu ni AB na mwanao ni O, hii inaonyesha vitu vingi sana ndani yenu vitakuwa vinatofautiana, hivyo isingekuwa vyema tuchukue uboho kwako kumwekea Genesis!”

“Sasa tutafanyaje daktari?”

“Bado tunajitahidi kadri ya uwezo wetu kupata mtoaji mwingine, hatujakata tamaa, tumewasiliana na watu wa SABC, ili waje wakufanyie mahojiano ili angalau uonekane kwenye televisheni wewe na mwanao, inawezekana kabisa tukapata mtu wa kutoa, itakuwa vizuri sana akiwa mtoto mdogo wa umri kama wa kwake!”

“Daktari, nimeanza kupoteza matumaini, nani atakayekubali kumtoa mtoto wake atoe uboho kumsaidia mwanangu?”

“Omba Mungu!”

Siku hiyo hiyo mchana watangazaji wa shirika la utangazaji la Afrika Kusini walfika hospitali ya Nelson Mandela na kumhoji Blandina na kupigwa picha mwanae akiwa kitandani kwenye wodi ya wagonjwa mahututi. Saa moja na nusu ya usiku, kila kitu kilionyeshwa kwenye taarifa ya habari, walioshuhudia wengi walilia machozi kwa kumwonea huruma mtoto hasa kwa maumbile aliyokuwa nayo na kwamba alihitaji uboho ili apate kuishi, Blandina aliwaomba watu wa Afrika Kusini wamsaidie.

“Mom! I want to give my bone marrow to that kid!” (Mama! Nataka kutoa uboho wangu kwa huyu mtoto!) Ilikuwa ni sauti ya mtoto mwenye umri wa miaka tisa ndani ya nyumba ya bwana na bibi Kennedy Dandla katika eneo la matajiri la Strawberry Yard, pembeni kidogo mwa jiji la Johannesburg.

“No! You are to small for that!” (Hapana! Ni mdogo mno kufanya hivyo!)

“No dady! I feel pity for that little unprivileged kid, I have to do it”(Hapana baba! Namwonea huruma sana mtoto huyo, ambaye hajabahatika, lazima nifanye!)

“Shut up Mike, go to bed now!” (Funga mdomo wako Mike, nenda kalale sasa hivi!) Mama wa mtoto huyo alifoka na kuondoka kuelekea chumbani.

Mpaka saa saba za usiku Mike alikuwa macho huku akilia mfululizo, sauti yake ikawafikia wazazi chumbani na kulazimika kuhamia chumbani kwa Mike ili kujaribu kumbembeleza alale lakini hakukubali, kila alipojaribu kufumba macho yake alimwona mtoto mgonjwa aliyevimba kichwa akiwa kitandani, huzuni ikazidi kumshika. Mwisho, wazazi wake walimtaka alale mpaka asubuhi ili waende pamoja hospitali kufuatilia kama jambo hilo liliwezekana, kilichowashangaza ni kauli hiyo, ilimfanya Mike asinzie na kuanza kukoroma ndani ya dakika ishirini ndipo wakaondoka kwenda chumbani kwao ikiwa tayari ni saa tisa na nusu za usiku.



Saa kumi na mbili asubuhi, Mike alikuwa mlangoni kwa wazazi wake akigonga, wote wakaamka na kujiandaa kwa safari ya kwenda hospitali. Saa moja na nusu walikuwa tayari, wakaondoka hadi hospitali ya Nelson Mandela ambako walijitambulisha mapokezi na kueleza nia yao, wakatakiwa kumwona daktari wa Genesis, Dk.Henric Gupta ambaye kwanza alipomwona Mike na kuelezwa historia yake, hakuamini kama mtoto mdogo wa umri huo angefikia maamuzi makubwa kiasi hicho.

“Haina tatizo sana, Mike bado anakua hivyo hata tukiondoa sehemu ya uboho kwenye mifupa yake bado haitamsumbua, mwingine tena utaota!”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Hawezi kuwa na matatizo?”

“Daktari kasema siwezi!” Mike alidakia kabla ya daktari.

“Hawezi, cha muhimu ni kumpima tuone kama damu yake ya mtoto mgonjwa inafanana!”

Wazazi wake wakaangaliana, kisha kumwangalia Mike, uso wake ulikuwa bado umejawa na tabasamu wala hakuonyesha uwoga. Hii iliwafanya wasiwe na jambo jingine, wakaacha kila kitu mikononi mwa Mungu wakiamini ndiye alikuwa amemtuma mtoto wao kuchukua uamuzi huo na kukubali Mike apelekwe chumba cha Maabara kwa uchunguzi, majibu yalipotoka zilikuwa ni taarifa njema mno kwa Blandina aliyekuwa amekata tamaa, kila kitu kilikuwa sawa.



“Thank you! “ (Ahsante!) Blandina alisema alipokutana na familia hiyo wodini ambako Genesis alikuwa amelazwa, hakuamini kama mtoto mdogo namna hiyo alikuwa ameamua kujitolea maisha yake, Blandina akaelewa maombi yake yalikuwa yakipata majibu kutoka kwa Mungu.

Mike akalazwa wodi hiyo hiyo aliyolazwa Genesis na maandalizi yakaanza, siku mbili baadaye hali ya Genesis ikiwa imekaa sawa kidogo, wote wawili waliingizwa chumba cha upasuaji ambako timu ya madaktari bingwa saba, mmoja akiwa amesafiri kutoka Marekani kwa ajili ya upasuaji huo walishirikiana kutoa uboho kwenye mifupa ya Mike na kupandikiza kwenye mifupa mikubwa ya Genesis, ilikuwa ni operesheni ya saa kumi na sita mpaka kukamilika.

Muda wote huo Blandina alikuwa nje ya chumba cha upasuaji akisali na kumwomba Mungu atende muujiza ili mwanae mpendwa atoke chumba cha upasuaji akiwa salama, alisali kwa imani kubwa huku machozi yakimtoka na moyoni aliamini Genesis angetoka salama, angepona na baadaye kuja kuwa mtu muhimu katika taifa lake la Tanzania pamoja na shida zote alizopata, hiyo ndiyo sauti aliyoisikia kutoka moyoni mwake.

Saa kumi na tatu baadaye, ikiwa ni usiku wa manane, watoto wote wawili walitolewa chumba cha upasuaji na kupelekwa wodi ya wagonjwa mahututi, hali ya Genesis ilikuwa bado mbaya na Mike pia alikuwa katika hali ya kupoteza fahamu! Wazazi ambao walishakuwa marafiki tayari walizifuata machela zilizokuwa zikisukumwa hadi kwenye jengo hilo lililoandikwa kwa nje ICU, hawakuruhusiwa kuingia ndani, wakaonyeshwa chumba kilichokuwa jirani ambako waliketi pamoja wakiongea hili na lile mpaka asubuhi waliporuhusiwa kuingia ndani na kukuta bado watoto hawajarejewa na fahamu.



“Itakuwa hivi mpaka lini?” Baba wa Mike alimuuliza daktari.

“Haitachukua muda mrefu sana kwa Mike, ila kwa Genesis itachukua muda mrefu zaidi kwani alikuwa dhaifu hata kabla ya upasuaji huu! Ila usiwe na wasiwasi, watoto wenu wote watapona!”

“Ahsante daktari, sina cha kukulipa, maneno yako hakika yamenitia nguvu! Kweli mwanangu atapona?”

“Atapona, usiwe na shaka mama, tumefanya upasuaji huu kwa umakini wa hali ya juu na takapozinduka na kukaa kwa muda wa kama wiki tatu hadi mwezi, kila kitu kitakuwa sawa, damu itakuwa haivuji tena! Kidogo tutakuwa tumemsaidia kupunguza mataitzo katika maisha yake!”

“Nashukuru daktari!”

Blandina hakuondoka wodini hata wazazi wa Mike walipomshawishi kufanya hivyo, alitaka kwanza ashuhudie mtoto wake akizunduka. Cha kushangaza, tofauti na alivyosema daktari, saa arobaini na nane baadaye, Genesis ndiye alikuwa wa kwanza kuzinduka na baadaye Mike akafuatia saa sabini na mbili baadaye, Blandina hakuificha furaha yake aliruka juu na kushangilia kisha kupiga magoti katikati ya wodi akisali na kumshukuru Mungu kwa muujiza alioutenda, alimwombea sana Mike akimsihi Mungu amfungulie baraka katika maisha yake.

Ingawa bado Genesis alitokwa na damu puani huku chupa za damu ziliendelea kutundikwa na kuingia kwenye mishipa yake, hali yake iliendelea vizuri, kwa mara ya kwanza Blandina alishuhudia tabasamu la mwanae baada ya muda mrefu kupita! Furaha yake ikaongezeka yote yaliyotokea yalikuwa ni muujiza kama ule wa kuponywa kwa kipofu Batromayo katika Biblia!

Mtoto Mike alifurahi zaidi, kwake huo ulikuwa ushindi, habari zake ziliandikwa na magazeti yote ya Afrika Kusini akiitwa shujaa aliyejitolea maisha yake kuokoa uhai wa mtoto mwenzake! Televisheni za BBC na CNN, zilitangaza habari zake dunia nzima ikamfahamu, mpaka kufikia kuingizwa katika orodha ya watu maarufu nchini Afrika Kusini, maelfu ya watu walimiminika hospitali kumwona yeye pamoja na Genesis.

Wiki mbili baadaye Mike aliruhusiwa kutoka hospitali, hali yake ilikuwa nzuri ingawa bado hakuruhusiwa kwenda shuleni mpaka miezi miwili baadaye ili mifupa yake ipate kupona vizuri, wazazi walilazimika kumtafutia mwalimu wa kumfundisha nyumbani. Haukupita muda mrefu sana, pia Genesis akaruhusiwa akiwa na nafuu kabisa hakutoka damu puani tena, wakakaribishwa kuishi na familia ya bwana na bibi Dandla kabla ya kurejea nyumbani Tanzania wiki moja baadaye, ulikuwa ni ushindi mkubwa mno kwake Blandina lakini pia kwa Rais aliyejitolea kugharamia matibabu ya mtoto huyo, walipokelewa uwanja wa ndege na waziri wa Afya na baadaye kwenda nyumbani kwa Dk.Ringo ambako walikuta mlango umefungwa.

Majirani walioelewa kilichoendelea walimfuata Blandina na kumpa pole kwa matatizo yaliyomkuta, wote walikuwa wamesoma au kusikia kupitia vyombo vya habari kila kitu juu ya Genesis. Ni hao ndio walimwambia, Ringo aliwaachia ufunguo na kusafiri kwenda Ifakara kikazi, alipokabidhiwa ufunguo, Blandina alifungua na kuingia ndani pamoja na mizigo yake, macho yake yakatua kwenye meza na kuona kipande cha karatasi, ilikuwa bahasha ambayo juu iliandikwa Blandina. Akaifungua na kuanza kuisoma, haukupita muda mrefu sana machozi yakaanza kumtoka akiwa na mtoto wake mgongoni.





Maisha ya Blandina yamejaa majonzi, mateso, maumivu makali moyoni, kwake kupitisha siku bila kutokwa na machozi ni neema kubwa, hii ni kutokana na kuhangaika kwa muda mrefu na mtoto wake aliyezaliwa na ulemavu na sasa amegundulika kuwa na ugonjwa mwingine uitwao Hemophilia, unaosababisha damu kuvuja bila kuganda. Matibabu ni mpaka Afrika Kusini ambako daktari watabadilisha ‘Bone Marrow’ (Uboho) kwenye mifupa yake ili iweze kutengeneza chembechembe za damu zilizokomaa, tiba hiyo itamfanya Genesis apone.

Blandina anafanikiwa kupata msaada kutoka serikalini ambako anampeleka mwanae Afrika Kusini, Nelson Mandela General Hospital. Baada ya uchunguzi wa ikathibitika kuwa Genesis anasumbuliwa na Hemophilia, tatizo kubwa ni namna ya kumpata mtu atakayeweza kutoa uboho wake ili awekewe, hapo ndipo angepona.

Kutokana na upendo wa Blandina kwa mwanae, anaamua kujitolea Uboho wake, lakini daktari wanamkatilia kwa sababu damu zao haziendani, Mike mtoto mwenye umri wa miaka tisa anafanikiwa kuokoa maisha ya Genesis kwa kujitolea Uboho wake, wanaporejea nyumbani Tanzania katika nyumba wanayoishi na Dk Ringo. Anakutana na barua iliyomfahamisha kuwa Dk. Ringo ameacha kazi Muhimbili na alihamia Ifakara.

Haraka akatoka kwenda ofisini kwake huko anakutana na msichana mwingine mgeni ambaye anamtambulisha kuwa anaitwa Joseline. Katikati ya mazungumzo simu ya ofisini ikaita, alipopokea akaagizwa na mama Majorica aende ofisini kwake kwa ajili ya mazungumzo. Nini kitafuata? SONGA NAYO…



Ndani ya ofisi ya Mama Majorica, Blandina aliketi nyuma ya meza ya bosi wake na kumsikiliza kwa makini sana, alijua kwa vyovyote kuna jambo jipya juu ya mgawanyiko wa kazi katika kitengo cha Wanasheria. Hii ni kutokana na msichana mgeni ambaye alimkuta ofisini kwake muda mfupi na kujitambulisha jina la Joseline!

"Sasa mwanangu nimekuita!"

"Ndio mama!"

Blandina alijibu kwa heshima, akiwa makini sana kumsikiliza, uso wa mama Majorica ulisomeka wazi kuwa kuna kitu fulani kizito, ni baada ya mama Majorica kuvuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu, akamtizama Blandina kwa huruma.

"Samahani sana, Blandina!"

"Bila samahani!"

"Kuna jambo muhimu sana natakiwa kukueleza asubuhi hii, najua litakukwaza lakini ni vema ukalipokea na kulichukulia jambo la kawaida, nadhani si wewe wa kwanza kukumbana na tatizo hilo!" Kwa jinsi mama Majorica alivyozungumza, Blandina alizidi kuchanganyikiwa, hakuelewa wazi kulikuwa na tatizo.

"Blandina, mpaka sasa ofisi imeamua kuajiri Mwanasheria mwingine na kukuachisha kaz..." Kabla mama Majorica hanamalizia, alimuona Blandina alibubujikwa na machozi ya uchungu.

"Mama, naomba unisaidie, sina mahala pa kukimbilia sina pesa ingawa mwanangu sasa hivi ana nafuu!"

"Blandina, siwezi kukusaidia, Bodi imekasirishwa sana na jambo ulilolifanya la kutelekeza gari la ofisi!" Mama Majorica alisisitiza na kumuomba Blandina akubaliane na hali iliyomkuta.

"Mama, maisha yangu yapo mikononi mwako, naomba unionee huruma mwanao pamoja na mjukuu wako Genesis, bila kazi maisha yetu yapo hatarini!"

"Siwezi kuajiri wafanyakazi wawili, naomba ukubaliane na hali halisi, kuhusu deni lako la milioni tatu na nusu nimekusamehe!"

Kila sentensi moja ya mama Majorica ilipotoka, ilimuumiza sana Blandina, msamaha wa milioni tatu na nusu haukutosha kumpa faraja. Alikuwa tayari kukatwa robo tatu ya mshahara wake mfululizo kwa miezi yote katika ajira yake, lakini sio kufukuzwa kazi, hakujua angeweza kuishi vipi na mwanae Genesis ambaye toka kuzaliwa kwake hadi kufikia hapo aliteseka sana.



Pamoja na Blandina kumuomba Mama Majorica amsaidie kumrudisha kazini, bado msimamo wa mama Majorica. Kwa uchungu sana Blandina, alimuomba Mkurugenzi wake amsikilize na kumpa nafasi ya mwisho kazini, huku akifuta machozi alisimulia.



"Mama maisha yangu yanasikitisha sana, nimepata tabu kuanzia usichana wangu hadi sasa, nilitokea kumpenda kijana mmoja aliyefamika kwa jina la Gerald, mwanzo wa uhusiano wetu tulikuwa na mapenzi ya dhati, aliniahidi ningeishi naye siku zote za maisha yetu.

“Baadaye Gerald alipata matatizo ya figo ikabidi nimtolee figo yangu moja na kubaki na moja, hali hiyo ilinifanya nitengwe na wazazi wangu wakinilaumu kwa ujinga wangu wa kujitolea figo Gerald, nilikubali lawama zote na kuendelea na uhusiano wa kimapenzi na Gerald.

“Baadaye mpenzi wangu alinisaliti kwa kutembea na rafiki yangu, akaniomba msamaha nikamsamehe, alipomaliza chuo tukafunga ndoa. Maisha ya ndoa yalikuwa mazuri sana, akawa anafanya kazi katika mazingira magumu sana, siku moja tukiwa katika sherehe ya kampuni bosi wake alinitamani, Gerald alitumia mbinu na kunichukua hadi kwa bosi wake na kuninywesha kilevi, nikapitiwa na usingizi niliposhtuka niliona bosi wake akiwa kando huku baadhi ya sehemu nikihisi maumivu makali sana.

“Miezi mitatu baadaye nilihisi dalili za ujauzito, nilipoenda kupima niligundulika kuwepo na ujauzito, nilipomfahamisha mume wangu alinikana na kudai mimba si yake ni ya bosi wake!

“Alinishauri niitoe lakini sikutaka kuua kiumbe kisicho na hatia, hatimaye nikajifungua mwanangu Genesis mwenye ulemavu. Ni hapo sasa Gerald alinitenga na kunifukuza nyumbani kwake, nilihangaika sana na mwanangu nikiomba msaada wa kumtibu, Mungu akanikutanisha na msamaharia mwema Dk. Ringo aliyejitolea kunisaidia…"



Blandina alisimulia mkasa mzima uliopata huku machozi yakiendelea kuchuruzika mashavuni, macho yake yalikuwa yamevimba kutokana na kulia muda mrefu, wakati huo mama Majorica alitulia akimsikiliza kwa makini.

"Pole sana Blandina, mmh! Sidhani kuwa nina msaada mwingine kutoka kampuni yangu!"

"Tafadhali mama Majorica, naomba unipe kazi nyingine katika kampuni yako, sina fedha!"

"Sehemu zote zina wafanyakzi, tukihitaji mfanyakazi tutakutaarifu!" Mama Majorica akamjibu kwa nia ya kumuondoa Blandina ili kuendelea na kazi zingine zilizokuwa zikimsubiri.

"Mama nitakosa hata kazi ya usekretari!"

"Hakuna mwanangu, nitakusiadia laki moja ya kukusogeza siku mbili tatu, ukitafuta kazi mahala pengine!" Blandina alizidi kuumia moyoni, alimlaumu mwanaume aliyemuingiza katika maisha ya mateso, asingeweza kumsahau Gerald siku zote za maisha yake, ni mwaume aliyemfananisha na muuaji.



Alijikuta akilaumu kukutana na Gerald, alizidi kuulaumu moyo wake kumpenda mtu asiye na mapenzi, ubongo wake ulihama na kwenda nyumbani alipomuacha mwanae na Mwajabu, pamoja na nafuu ya mwanae alijua angeteseka kwa kukosa huduma muhimu kama mtoto.



Mama Majorica alivuta droo yake na kumkadhi Blandina shilingi laki moja, hakuweza kuzikataa alipokea akilia sana, akimuomba Mungu amuondolee mateso yaliyokuwa yakimzonga maisha mwake, furaha kwake ilikuwa siku moja tena kwa bahati lakini kulia kwake alishazoea na matatizo alijua ni sehemu kubwa ya maisha yake.

"Mungu nisaidie, nitaishi vipi kila kitu kwangu ni bahati mbaya, nisaidie niwe na maisha mazuri, sina raha katika dunia hii, moyo wangu unaendelea kuteseka na sijui lini mateso yangu yataisha, nakuomba Mungu unipunguzia matatizo!" Alisema akitoka ofisini kwa mama Majorica.



Wafanyakazi wote walimuonea Blandina huruma kiasi alivyokuwa akilia kwa uchungu baada ya kuambiwa hakuna kazi.



Nusu saa baadaye Blandina alifika nyumbani kwake, hali ya mwanae ilikuwa ikiendelea vizuri sana hilo alimshukuru Mungu na kumuomba aendelee kumsaidia mwanaye afya njema. Siku nzima, Blandina aliendelea kulia sana, hakujua maisha yake yangekuwaje bila kazi.



Ilipofika saa kumi na mbili jioni, Blandina alichukua simu yake na kumpigia Dk. Ringo ili kujua anaendeleaje Ifakara mkoani Morogoro. Simu iliita muda mrefu sana na baadaye ilipokelewa.

“Halow! Dk.Ringo?” Alisema punde simu ilipopokelewa.

“Mmhh! Dk Ringo hayupo, amesafiri kikazi wiki mbili, mimi naishi naye nyumba moja!”

“Ohhh! Samahani sana!”

“Bila samahani, ongea tu shida yako!”

“Shida yangu ni kuongea na Dk. Ringo, nadhani matatizo yangu yatapungua, amesafiri kwenda wapi?”

“Malinyi Ulanga kufanya utafiti wa Malaria! Kwani wewe ni nani wake?”

“Dada yake, nina shida kubwa sana!”

Blandina alimwelezea matatizo yake ya kufukuzwa kazi na kudai anataka kwenda Ifakara kumuona.

“Ok, utakuja kesho?”

“Ndio!”

“Panda basi la Ifakara, ukifika unifahamishe nitakuja kukupokea!”



Alielekezwa, jinsi atakavyoondoka hadi kufika Ifakara, kesho yake asubuhi Blandina aliondoka na basi la asubuhi sana, saa kumi jioni aliwasili Ifakara. Akapokewa na Dk. Albert Mkambila, urefu wa Dk. Mkambila, ulikuwa sawa na mrefu wa mtu aliyemfahamu, sauti na hata tembea yake pia ilimtia hofu na kujaribu kuvuta kumbukumbu kuwa mwanaume huyo alimpata wapi bila mafanikio.

“Karibu sana Ifakara!”

“Ahsante!”



Saa moja baadaye waliwasili nyumbani kwa Dk. Ringo, alikaribishwa kwa heshima kama dada wa Dk. Ringo.



Katika mazungumzo, Blandina alibaki akijiuliza maswali mengi juu ya mwanaume aliyesimama mbele yake, sauti haikuwa ngeni masikioni mwake na alipoangalia mkono wa kuume wa mwanaume huyo aliona kovu ambalo pia alishawai kuliona kwa mtu mwingine ambaye hakuweza kumkumbuka.



Siku mbili baadaye, walipokuwa mezani wanakula chakula cha usiku, Blandina aliamua kumuangalia sana Dk. Mkambila, maswali mengi aliyokuwa amejiuliza, sasa aliona ni vema kumuuliza. Sura ya Dk. Albert Mkambila ni ngeni lakini urefu, sauti na hata kicheko alikifananisha na mwanaume aliyewahi kumuona.

“Samahani, Dk. Mkambila, sura ni ngeni lakini sauti na mwendo wako vinafanana na mtu niliyewahi kumfahamu siku nyingi kabla!”

“Mimi!!” Dk. Mkambila aliuliza kwa mshangao.

“Ndio!”

Dk. Mkambila hakuwa na jibu.



*****

“Samahani Dk. Mkambila, sura ni ngeni lakinin sauti na mwendo wako vinafanana na mtu niliyewahi kumfahamu siku nyingi kabla!”

“Mimi?”

“Ndio!”

“Hapana, labda unanifananisha, duniani wawili wawili! Unanifananisha na nani?”

Blandina hakujibu haraka, kwa muda mrefu alikuwa amejiuliza swali hilo bila kupata jibu, akainamisha kichwa chake chini na kuzikusanya kumbukumbu zake sawasawa mpaka akafanikiwa na kunyanyua kichwa chake tena, akamkuta Dk. Albert Mkambila ameketi akiendelea kusikiliza huku uso wake ukiwa umejawa na tabasamu.

“Una undugu na familia ya akina Othman?”

“Othman gani?”

“Hivi sasa ni marehemu, alikuwa daktari huko Dar es Salaam!”

“Hapana sina uhusiano nao, sura zetu zinafanana?”

“Hapana, yaani sauti yako ni kama ya Othman, kwa muda mrefu sana kijana huyo alikuwa mpenzi wangu na alitaka kunioa lakini bahati mbaya mimi ndiye nikamvunja moyo kwa kumwacha na kuchukuliwa na mwanaume mwingine ambaye baadaye alinisababishia yote yanayonipata leo!”

“Aah! Pole sana, sasa kwanini ulimwacha?”

“Ujinga tu! Nilikuwa bado sijawa na akili timamu, nasikitika sana alikufa!”

Blandina akatumia dakika nyingine ishirini kuelezea historia ya maisha yake tangu alipoachana na Othman, namna kijana huyo alivyokufa akiwa mahabusu baada ya kujaribu kutaka kumuua Gerald! Dk.Mkambila alikuwa kimya muda wote akisikiliza habari hiyo ya kusikitisha, ghafla machozi yalianza kumlenga lenga, Blandina akashuhudia na kumsogelea karibu.

“Mbona unalia?”

“Nimesikitika sana, kwa hiyo sasa hivi Othman angekuwa hai kwa mambo yote yaliyokutokea, ungekubali kuwa naye?”

“Nilimpenda sana Othman, kwa moyo wangu wote, shetani tu alinidanganya, akitokea sasa hivi ingawa najua hawezi na akakubali kunichukua mimi na mtoto wangu, jinsi alivyo nitakubali kuwa naye, si kuwa naye tu bali kuishi naye milele na milele, nimejifunza mambo mengi mno hapa duniani!”

“Pole sana, kula basi!” Dk. Mkambila aliongea akijifuta machozi kwa kitambaa.

“Ahsante kwa kujali!”

Wakala tena pamoja mpaka wakashiba, baada ya hapo ndipo Blandina akamlisha Genesis, Mkambila akiwa ameondoka kwenda chumbani kwake kuoga na baadaye kujipumzisha! Asubuhi ya siku iliyofuata walionana wakati wakifungua kinywa, Dk. Mkambila akaondoka kuelekea kazini, macho ya Blandina yakimsindikiza, kwa jinsi alivyotembea akiwa ametega mgongo haikuwa rahisi hata kidogo kwa mtu kumtofautisha na Othman.

Saa nane mchana alirejea, wakaendelea kuwa wote. Hayo ndiyo yakawa maisha yao mpaka Dk.Ringo aliporejea kutoka Malinyi, alifurahi mno kumwona Blandina na mwanae tena, akamtia moyo na kumwambia yote yaliyotokea yalikuwa ni sehemu ya maisha, bado zilikuwepo nafasi nyingi mbele na za yeye kufanikiwa lakini ilikuwa ni lazima ajiepushe na suala la kuumizwa na historia yake kama kweli alikuwa na nia thabiti ya kufanikiwa.

“Inabidi ubadilishe akili yako, fikra zako ziwe tofauti, inavyoonekana akiba yako kichwani ni matatizo, hakuna unachokifahamu kuhusu raha ya dunia wala mafanikio, wewe ni vilio tu! Usiache kabisa historia yako ikaharibu maisha yako ya kesho, unasikia?”

“Nasikia kaka!”

“Ni kweli kabisa Blandina, anayoyasema Ringo ni sahihi, watu wengi duniani wanateswa sana na historia zao, kwa mambo uliyonisimulia ni rahisi sana wewe kuendelea kuhukumiwa na yaliyopita! Hii ni dunia mpya, ya jana ni ya jana na ya leo ni ya leo! Kamwe usiingie kesho na mizigo ya jana, tatizo lako ni kwamba unatembea na mizigo ya historia kichwani, ni sawa na mfungwa aliyeachiwa huru kutoka gereza lakini bado anatembea mtaani na magwanda ya jela! Huyu atakuwa huru kweli? Hapana, akifikia mjini watu watamkamata na kumrejesha gerezani wakidai ametoroka kumbe yuko huru, hapo ninaamanisha ni laizma uvue magwanda ya jela kuonyesha kwamba kweli uko huru, ni lazima uachane na mizigo ya zamani, machozi ya nyuma kama umedhamiria kubadilisha maisha yako, ukiliweza hili, nakuhakikishia Blandina utakuwa mtu mwenye furaha kuliko mwingine yeyote!” Dk. Mkambila aliongea akimwangalia Blandina kwa macho ya huruma.



“Nitajitahidi kaka Albert ingawa ni kazi ngumu sana!”

“Itawezekana!”

Wote wawili walimpenda na si yeye tu bali pia Genesis, walimpa kila kitu alichohiitaji na kumchukulia kama dada yao tumbo moja, maisha yalikuwa ya furaha, Dk. Ringo akisafiri mara kwa mara kwenda vijijini kufanya utafiti na kumwacha Blandina na Dk. Mkambila, Genesis hakusumbua kwa jambo lolote kubwa, ilipotokea anaumwa alitibiwa katika hospitali ya St. Francis, gharama zikilipwa na madaktari hao wawili, safari za Ringo zilimchukua wiki mbili na kurudi tena Ifakara, kila aliporejea tatizo likawa namna ya kulala, yeye na Mkambila ilibidi wachangie chumba kimoja.



Jambo hili ilimfanya Mkambila aamue kutafuta nyumba nyingine, hapakuwa na kipingamizi ili mradi alihakikisha kwamba mara kwa mara angekuwa anakwenda kuwatembelea! Nyumba aliyopata ilikuwa mjini Ifakara, hii ilimfanya ashindwe kutimiza ahadi yake ya kuwatembelea Ringo na Blandina kama walivyokubaliana, wakawa wanaonana mara chache mno, hii ilimfanya Blandina kuishi peke yake pale ambapo Ringo alisafiri kwenda kijijini lakini hakuogopa chochote, alishazoea na tayari alikuwa na majirani ambao siku zote walihisi alikuwa mke wa Ringo.

Siku zilizidi kukatika, hatimaye mwaka mmoja na nusu ukapita, Genesis akatimiza miaka mitatu, katika umri huo alishaanza kuonyesha hakuwa mtoto wa kawaida! Aliweza kuhesabu moja mpaka ishirini na kuongea vitu ambavyo hata mama yake hakuvifahamu, aliwashangaza wengi, hata Dk. Ringo na Mkambila.

“Anko!” Genesis alimwita Dk.Ringo wakiwa wamekaa sebuleni.

“Naam!”

“Ubongo umegawanyika katika sehemu mbili? Yaani Left and right hemispheres? Au?”

“Wewe mtoto, nani amekufundisha mambo hayo katika umri huu?”

“Nilisikia redioni, tena wakasema moyo una vyumba vine, vya juu vinaitwa Atrium na vya chini vinaitwa Ventricles!”

“Mh!” Dk. Ringo aliguna, hakuamini alichokisikia ikabidi amwite Blandina aliyekuwa jikoni akipika na kumuuliza kama alikuwa amemfundisha Genesis kitu chochote juu ya aliyoyaongea.

“Hapana, sijamfundisha kitu, mimi mwenyewe namshangaa sana, wiki iliyopita alinifuata na kuniambia habari za chembechembe nyekundu na nyeupe za damu, nilipomuulizia vizuri akaniambia eti alisikia redioni, nikafikiri labda wewe ndiye ulimfundisha!”

“Basi huyu mtoto ana kitu, katika hali kama hii sio jambo la kawaida hata kidogo mtoto kuongea mambo makubwa kiasi hiki, kumbukumbu yake sio ya kawaida!” Dk. Ringo aliongeza huku akimwangalia Genesis kwa jicho la mshangao.

Hii ilikuwa ni furaha kubwa kwa Blandina, hakutegemea hata siku moja mtoto wake ambaye alitakiwa kufa mapema angekuwa na uwezo mkubwa kiasi hicho. Alipopelekwa shule ya awali, aliwashangaza walimu wake pia, ikabidi wawasiliane na mratibu wa Elimu wa kata, ambaye aliwasiliana na Afisa Elimu wa Wilaya, akafika kujionea mwenyewe maajabu ya mtoto Genesis. Ndani ya muda mfupi tu, taarifa zikawa zimekwishafika mkoani.

*****

Si viongozi wa wilaya na mkoa tu walioshangazwa na uwezo wa mtoto huyo, sura na maumbile yake yalikuwa mabaya kupita kiasi, alikuwa na kichwa kikubwa, bila pua wala masikio lakini Mungu hakumtupa Genesis, uwezo wake wa akili ulitisha! Alitunza kumbukumbu zaidi ya kompyuta, akimwona mtu mara moja hawezi kumsahau, akiandikiwa namba yoyote na kuambiwa hii ni namba fulani basi hiyo isingebanduka tena. Jambo hili lilifanya wageni wengi wamiminike kijijini Ifakara kumshuhudia mtoto huyu hasa baada ya vyombo vya habari kuandika na kutoa picha yake gazetini na kumweka kwenye mtandao wa Internet.

“Hii sio kawaida!” Dk. Eliud Mbwilo, bingwa wa saikolojia kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam alisema baada ya kuongea na Genesis, wakati huo akiwa na umri wa miaka mitatu tu.

“Ni kweli, ana high IQ!” Dk. Tungaraza, pia bingwa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliongea.

“Ni nini hiyo?” Mwenyekiti wa mtaa aliyekuwepo akauliza.

“Kirefu chake ni Intelligent Quotient!”

“Hujanisaidia umezidi kunichanganya daktari!”

“Ni kipimo cha akili ya mtu!”

“Aisee, kwa hiyo huyu mtoto chake kiko juu?”

“Sana, sijawahi kuona mtoto mwenye akili nyingi kama huyu, Taifa litanufaika sana na huyu mtoto kama tu ikitokea akaendelezwa, tutawasiliana na serikali mara tu tukirejea Jijini Dar es Salaam, hata mimi sikuwa na akili nyingi kiasi hiki!”

“Kweli? Mbona mimi naona kawaida tu, wewe si una PhD au udaktari wako ni kama wa anko Ringo?” Genesis aliuliza kama mtu mzima na kuzidi kuwashangaza.

“Ndio nina PhD, umejuaje habari za PhD Genesis?’

“Zamani sana nilimsikia anko Ringo na Anko Albert wakiongea!”

“Zamani sana lini na wewe una miaka mitatu duniani?” Dk. Tungaraza aliongea akitabasamu, kila kitu kilichotokea kiliwashangaza.

Blandina alikuwa haamini kama mwanae ndiye alikuwa na akili hizo, mara nyingi alipiga magoti chini na kumshukuru Mungu kwa kumpa ujasiri wa kupambana kuokoa maisha ya mtoto wake. Aliporudisha kumbukumbu zake nyuma, alimwona Gerald akimsisitizia wamuue mtoto aliyemzaa kwa sababu alikuwa mgonjwa, moyoni akasikitika na kujiona shujaa kwa kukataa alichokuwa akishawishiwa kufanya, akaamini yote yaliyotokea yalikuwa ni kwa uwezo wa Mungu peke yake kwani kwa mapenzi aliyokuwa nayo kwa Gerald ilikuwa ni rahisi sana kukubali kumuua mtoto huyo.

“Ahsante Mungu!” ndilo neno pekee alilosema, akiamini furaha yake hatimaye ingetokana na Genesis.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

***

Wiki moja tu baadaye ujumbe mwingine tena mzito wa serikali ukiwa umeongozana na wawakilishi wa Balozi za Japan, Marekani, Uingereza na Canada uliwasili Ifakara kumwona mtoto waliyesoma na kusikia habari zake, wao pia hawakuamini kama kulikuwa na binadamu mwenye akili nyingi kiasi hicho! Walichofanya ni kumshawishi Blandina akubali mtoto wake achukuliwe kwenda kusomeshwa nje ya nchi, cha kushangaza na kilichomshtua ni namna Mabalozi hao walivyomgombania mtoto kila mmoja akitaka aende kusomeshwa nchini kwake. Mwisho kabisa Blandina alikataa akihofia usalama wa mtoto wake, akachagua mtoto asomee Tanzania.

Serikali ilimpa Blandina ofa ya nyumba maeneo ya Masaki, kila kitu angepewa kuanzia matibabu ya mtoto, gari kusafiria na matumizi ya kila siku lakini ampeleke mtoto kusoma shule ya Tanganyika International school. Hakutaka kukubali mpaka Ringo aliporejea kutoka Malinyi, wakajadiliana na kukubaliana na uamuzi uliokuwa umefikiwa na serikali kwani kwa uwezo aliokuwa nao Blandina tena bila kazi ya kufanya kujiingizia kipato asingeweza kumwendeleza mtoto wake hata kama angekuwa na akili nyingi kiasi gani.

“Itabidi uende, mimi nitawasiliana na wewe mara kwa mara na nikija Dar es Salaam nitakutembelea, tumekwishakuwa ndugu tena wa damu!”

“Ahsante sana, tumetoka mbali sana!” alijibu Blandina akionyesha furaha kuanzia kwenye nywele mpaka kuchani, macho yake hayakulengwalengwa na machozi tena, hatimaye Genesis alikuwa amemletea furaha.

“Mom!” (mama!) Genesis alimwita mama yake.

“Yes my darling!” (Ndio mpendwa wangu!)

“You are so happy today!” (Una furaha sana leo!)

“For sure, you have made me happy at last my daughter!” (Kwa hakika ninayo furaha, hatimaye umenifanya niwe nayo binti yangu!)

“How?” (Kivipi?)

“You cant understand!” (Huwezi kuelewa!)

“I can!” (Naweza!)

“Ok! We will be leaving this place tomorrow for Dar es Salaam where will start new life!” (Sawa! Kesho tutaondoka hapa kwenda Dar es Salaam ambako tutaanza maisha mapya!)

“With uncle Ringo?” (Na anko Ringo tunaondoka naye?)

“No!” (Hapana!)

“Why?” (kwanini?)

“He will be staying here, you need to go to the best school in Tanzania, that is why we are leaving!” (Atabaki hapa, wewe unahitaji kwenda kwenye shule bora nchini Tanzania, hiyo ndiyo sababu pekee tunaondoka!)

“To me any school is the best!” (Kwangu shule yoyote ni nzuri!)

Blandina alitumia karibu saa mbili akijaribu kumwelewesha mtoto wake juu ya sababu ya kuondoka, alimpenda sana Dk. Ringo, kwake alikuwa ni zaidi ya Anko, alimchukulia kama baba yake mzazi. Baadaye alikubali na siku iliyofuata wakaondoka kurejea Dar es Salaam, ilikuwa ni huzuni sana kwa Dk.Ringo wakati akiwaaga stendi ya basi, machozi yaliwatoka. Ilikuwa ni kama vile wasingeonana tena, alishamzoea Genesis na siku zote alimwona ni mtoto wake, wakati wengine walimchukulia kama mtoto asiye wa kawaida, yeye hakuiona tofauti yake na watoto wengine.

***

Mabalozi waliporejea jijini Dar es Salaam wote walipiga simu kwenye nchi walizotokea, wote wakielezea juu ya mtoto waliyemwona. Marais wao hawakuamini kama mtoto mwenye akili za aina hiyo angeweza kupatikana Afrika, Marekani ikawa inamhitaji haraka iwezekanavyo kwa ajili ya kupambana na nchi za China na Japan katika ulimwengu wa teknolojia ili yenyewe ibaki juu. Wakati Marekani ikiwaza hivyo, ndivyo Japan na China walivyokuwa wakipanga.



Bila Blandina wala serikali wa Tanzania kuelewa, vikao vilikuwa vikiendelea katika nchi hizo tajiri ili mtoto huyo mwenye hazina ya ajabu kichwani mwake apatikane kwa gharama yoyote ambayo ingehitajika. Nchini Marekani kikao kilikuwa kikiendelea ndani ya Ikulu ya nchi hiyo.

“We need that kid!” (Tunamhitaji mtoto huyo!) Mkurugenzi wa ubunifu ndani ya kampuni ya kompyuta ya Microsoft alisema.

“Tanzania will not say yes, they need her too!” (Tanzania haitakubali, hata wao wanamhitaji!)

“We will capture the kid!” (Tutamteka mtoto!)

“How?” (Kivipi?)

“The information I have, that kid has joined Tanganyika International School, which is run by American people!” (Kwa taarifa nilizonazo, mtoto huyo amejiunga na shule ya Kimataifa ya Tanganyika ambayo inaendeshwa na Wamarekani!)

“So?” (Kwa hiyo tutafanyaje?) Waziri wa Mawasiliano wa Marekani aliuliza.

“A Tanganyika International school kindergarten trip to America should be planned and Genesis should be among the children, while they are here, we will capture the kid for you, Tanzania will never see her again because we will change her Identity!” (Safari ya watoto wa Tanganyika International School kuja hapa Marekani kujifunza lazima iandaliwe, wakiwa hapa tutamteka mtoto, Tanzania haitamwona tena kwani tutabadilisha utambulisho wake!)

“That is a good idea, can you start implementing it now!” ( Hilo ni wazo zuri, tunaweza tukaanza utekelezaji wake sasa?)

“Sure?” (Hakika?)

***

Miezi mitatu baadaye bibi Mary Gibson, mkuu wa shule ya kimataifa ya Tanganyika alikuwa ofisini kwake, saa ya ukutani ilisomeka saa mbili na nusu asubuhi. Simu ya mezani ikalia, alipoipokea sauti ya kike iliongea, mtu akijitambulisha kama mfanyakazi wa ubalozi wa Marekani na kumpa taarifa kwamba serikali yake ilikuwa imetoa ofa kwa shule hiyo kusafirisha wanafunzi wa shule ya awali ishirini na tano, kwenda nchini mwao kwa matembezi ya kujifunza, gharama zote zingegharimiwa na serikali ya nchi hiyo lakini sharti liwe moja, Genesis awe miongoni mwao.

“No problem, we are so happy to be given that offer!” (Hakuna shida, tunafuraha mno kupewa ofa hiyo!)



Shida, mateso, dhiki na taabu zote zilikuwa za kawaida katika maisha yake, siku zote alilia kutokana na kuandamwa na matatizo yasiyoisha! Huyu ni Balandina! Baada ya kurejea Afrika Kusini alipokuwa kwa ajili ya matibabu ya mwanaye Genesis.

Alipokwenda katika Kampuni aliyokuwa akifanyia kazi, akakutana na habari mpya, tayari kulikuwa na mfanyakazi mwingine aliyeajiriwa! Balandina anazidi kuchanganyikiwa, hakuwa na la kufanya zaidi ya kurudi nyumbani. Baada ya kuwasiliana na Dk. Albert Mkambila, akaenda Ifakara ambapo aliishi hapo mpaka Dk. Ringo aliporudi.

Akiwa na miaka mitatu tu, Genesis akaonyesha uwezo wa ajabu sana wa utambuzi, akatambelewa na Balozi za nchi mbalimbali ambapo baadaye Serikali ikaamua kumchukua na kumsomesha katika Shule ya Kimataifa ya Tanganyika. Pasipo walimu, serikali wala Blandina kujua, vikao vya siri viliendelea nchini Marekani, ambapo baadaye walipanga kumteka mtoto huyo mwenye akili za ajabu. Hawakuwa na njia nyingine ya kufanya zaidi ya kuandaa safari ya wanafunzi wa shule hiyo nchini Marekali ili waweze kukamilisha mipango ya kumteka Genesis.

Baada ya kumpigia simu Mkuu wa Shule hiyo bibi Mary Gibson, hakukataa! Huo ulikuwa mwanzo mzuri wa kumteka Genesis, mtoto mwenye akili za ajabu ambazo walipanga kuzitumia ili kuifanya nchi yao iendelee kuwa bora zaidi katika mambo ya Teknolojia. Nini kitafuata? SONGA NAYO…



Furaha aliyokuwa nayo Mkuu wa Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (Tanganyika International School), haikuwa ya kawaida! Kupewa ofa ya kwenda kutembelea nchi kubwa kama Marekani bila malipo yoyote ilikuwa bahati kubwa sana kwake.

“Huwezi kuamini mwalimu!”

“Juu ya nini?”

“Ubalozi wa Marekani!”

“Ubalozi wa Marekani, umefanya nini sasa? Mbona unaoneka una furaha sana mama Gibson?”

“Imeipatia ofa ya pekee shule yetu, inahitaji wanafunzi ishirini kwa ajili ya kutembelea vivutio mbalimbali vya nchi yao, kwa ajili ya wanafunzi wetu kujifunza!”

“Bila malipo yoyote, siamini kabisa Mkuu!”

“Amini mwalimu, tena ni dakika mbili tu zilizopita wamenipigia simu!”

“Hongera sana Mkuu!”

“Nashukuru, ila hii ni changamoto kwetu sote!” Yalikuwa mazungumzo kati ya Mkuu wa Shule na Mwalimu wa Nidhamu shuleni hapo Nancy Ngatengwa.

Ilikuwa furaha kubwa sana kwa shule yao, nusu saa baadaye kikao cha walimu wote kikafanyika, kisha Mkuu wa Shule akatoa taarifa hiyo kwenye kikao.

“Hii ni bahati ya pekee kwa shule yetu!” Mmoja wa walimu alisema.

“Hakika!” Mwingine akadakia.

Hapakuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya kuiwasilisha maombi hayo kwa Wizara ya Elimu, ambayo haikuwa na kipingamizi.

“Hakuna tatizo juu ya hilo, lakini lazima tuwasilishe suala lenu Ofisi ya Rais kwanza!”

“Hakuna tatizo Mheshimiwa, tuna imani tutakubaliwa!”

“Bila shaka, kikubwa ni kuwashirikisha tu, sisi kama wizara tuna uwezo wa kupanga na kuamua mambo yanayohusu wizara yetu kwa uhuru, ila ni utaratibu ambao tumejiwekea!”

“Nafurahi sana kusikia hivyo Mheshimiwa!”

“Ahsante sana mama Gibson!”

“Kazi njema, ila tutegemee majibu lini?”

“Nitakupigia simu!”

“Ahsante sana!”

“Nawe pia!”

Furaha ikazidi kutawala katika moyo wa mama Gibson, hakuwahi kufikiria siku moja wanafunzi wa shule yake wangekwenda kutembelea Marekani, kwake ilikuwa ni zaidi ya kutalii, ilikuwa safari kujifunza na kupanua uwezo wa wanafunzi wake.

Siku tatu tu, baadaye mama Gibson akiwa ofisini kwake alipigiwa simu kutoka Wizara ya Elimu, simu ambayo ilimfanya azidi kuifurahia siku hiyo. Hakika siku yake ilikamilishwa na simu hiyo.

“Mama hongera sana, ombi lako limekubaliwa!”

“Nashukuru sana, nimefurahi sana!”

“Tutawatumia kiibali baadaye, lakini mnaweza kuendelea na taratibu nyingine!”

“Nashukuru sana Mheshimiwa!” Ilikuwa ni simu kutoka ofisi ya Waziri wa Elimu.

Hawakuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya kuanza kufanya mipango. Jambo la kwanza alilofanya ni kumpigia simu Mwalimu wa Nidhamu shuleni hapo Nancy Ngatengwa kwa ajili ya kupanga mipango ya safari hiyo.

“Mwalimu, kila kitu kipo tayari, serikali haina tatizo juu ya safari yetu, kibali kitakuja baada ya muda mfupi, sasa tuanze kupanga mipango safari!” Mama Gibson alisema akionyesha furaha yake wazi wazi.

“Hakuna shida mwalimu, ila ni lazima tujue wanafunzi wataokwenda kwanza!”

“Ndio maana nikauita mwalimu, zoezi hili nataka ulisimamie wewe! Kuanzia kuratibu mpaka kwenda nao, wewe utakuwa kiongozi wa msafara!”

“Hakuna shida mwalimu, wacha nikaanze kupanga!’

“Sawa ila hutakiwi kumsahau Genesis!”

“Nimekuelewa Mkuu!”

Mwalimu Ngatengwa alikuwa hodari sana shuleni, saa tatu tu, baadaye tayari alikuwqa na idadi ya majina kamili ya wanafunzi aliokuwa amepanga kwenda nao nchini Marekani. Alipomaliza kuteua wanafunzi hao, akawaandikia barua wazazi wao na kuwaeleza juu ya safari hiyo, kila mwanafunzi aliyeteuliwa kwenda alipewa, hata Genesis pia alipewa.

Alipoteremshwa na gari la shule nje ya geti la nyumba yao iliyopo Masaki, alisukuma geti haraka na kuingia ndani huku akiita jina la mama! Mama! Mama! Mama…

“Kuna nini Genesis?”

“Habari nzuri mama!”

“Habari gani Genesis mwanangu?”

“Chukua hii barua ya mwalimu uone!” Akamrushia kisha akakimbia chumbani kwake kwa ajili ya kubadilisha nguo zake za shule. Genesis alikuwa na furaha sana, alitamani sana kufika katika nchi aliyokuwa akiisikia katika vyombo vya habari pekee. Aliamini akiwa huko, angejifunza mambo mengi sana wanayofundhishwa shuleni kwao na mengine mapya.

Aliporudi sebuleni akashangaa kumkuta mama yake akiwa amejiinamia kwa uchugu.

“Nini kmetokea mama?”

“Huwezi kwenda Marekani mwanangu, ni mbali sana huko, hali yako sio nzuri sana kiafya!”

“Haiwezekani mama, lazima niende!” Genesis akasema huku akilia machozi.

“Huwezi kwenda mwanangu, mimi ndiye ninayefahamu matatizo yako!” Yalikuwa mabishano makali sana, ambayo hayakumalizika vizuri. Genesis aligoma kula kutokana na mama yake kumzuia kwenda Marekani.

Blandina alipata kazi ya ziada kumbembeleza mwanaye mpaka akatulia na kula. Siku iliyofuata, Blandina alikuwa ofisini kwa Mkuu wa Shule.

“Mwalimu, mwanangu ana matatizo ya kiafya, hawezi kwenda Marekani, ni mbali sana kwake! Hawezi kuwa mbali na mimi kiasi hicho!”

Hapana mzazi, atakuwa chini ya uangalizi wa mwalimu, atakuwa salama, hakuna jambo baya litakalompata! Tupo makini sana, naomba umruhusu tafadhali!”

“Haiwezekani!” Ilikuwa kazi ngumu sana kumshawishi Blandina, ili akubaliane na safari hiyo ya mwanae kwenda Marekani. Mama Gibson alifahamu vyema umuhimu wa Genesis katika safari hiyo. Kama Genesis singekwenda, basi safasi ya huko isingekuwepo tena! Ilikuwa lazima amshawishi sana Blandina ili akubaliane na safari hiyo.

Mama Gibson hakuelewa mipango ya Marekani ilikuwa mbele ya mtoto Genesis, kwake ilikuwa safari ya kujifunza vitu vipya. Ilikuwa lazima atumie akili yake yake ili aweze kumshawishi Blandina akubaline na hilo. Hatimaye mama Genesis alikubali.

“Nashukuru sana mama Genesis kwa uelewa wako, amini kuwa mwanao atakuwa salama, baada ya wiki mbili tu atakuwa amesharudi nchini!” Mkuu wa Shule akamwambia kwa sauti ya kusihi.

“Hakuna shida mwalimu!” Mama Genesis alijibu.

Moyo wake haukuwa na amani kabisa, alikubali kwa sababu alishinikizwa lakini moyoni mwake, bado alitawaliwa na mawazo tele. Kwa Genesis ilikuwa tofauti, alimshukuru sana mama yake kumkubalia.

*********

Ilikuwa ni siku ya jumatatu tulivu sana, anga la jiji la Dar es Salaam, lilifunikwa na wingu zito, ingawa hapakuwa na dalili ya mvua, lakini kulikuwa na baridi kali asubuhi hiyo. Wazazi, walimu na watoto waliokuwa tayari kwa safari ya kwenda Marekani walikuwa katika Uwanja wa Ndege ya Kimataifa wa Mwalimu Nyerere.

Kila mzazi alikuwa akimuaga mwanae aende salama kwa ajili ya kujifunza mambo mapya nchini Marekani. Wengi waliishia kuwabusu watoto wao mashavuni na kuwapungia lakini kwa Blandina ilikuwa tofauti sana. Hakuweza kuelewa ni kwa nini moyo wake ulikuwa mzito kiasi hicho! Hakuamini kama mwanaye angeweza kuondoka na kurudi salama nyumbani.

“Mama tupige magoti tuombe kwa ajili ya safari!” Genesis alimwambia mama yake huku akitabasamu. Blandina hakubisha, akapiga magoti chini pamoja na mwanaye kisha wakaanza kuomba pamoja. Kila mtu aliwashangaa kutokana na namna waliyokuwa wakisali, walisali pamoja huku Blandina akilia machozi. Baadaye akamwachia mwanaye akaenda kujiunga na wenzake.

Muda wa ndege kuruka uliwadia, wanafunzi wote ishirini pamoja na mwalimu Ngatengwa waliondoka haraka kuelekea shehemu maalum ya ukaguzi. Blandina alionekana kuwa na wasiwasi sana moyoni mwake, alikuwa akimfuata mwanaye na kumwita kisha anambusu halafu anamwachia. Alirudia kufanya hivyo zaidi ya mara sita.

Sasa walifika katika chumba maalum cha ukaguzi, wanafunzi wote kumi na tisa waliingia, isipokuwa Genesis pekee, aliyekuwa akiagana na mama yake. Blandina hakuwa na amani na safari aliyokuwa akienda mwanaye. Daima alilia, hata hivyo hakuwa na kitu cha kufanya zaidi ya kumuacha Genesis aingie katika chuimba hicho akaungane na wenzake kwa ajili ya safari.

Dakika kumi na nato baadaye, ndege iliyokuwa na wanafunzi wa Tanganyika International School, iliruka! Mapigo ya mama Genesis yakaongeza kasi, akainua mkono wake juu na kupipungia ndege mpaka ilipopotelea, hakutaka kujua kama mwanaye alikuwa akiona mkono wake au vinginevyo! Ilikuwa ni kama safari ya mwisho ya mwanae.

Ghafla mwili wa Blandina ukaingiwa na ubaridi mkali, akahisi kizunguzungu, akaamua kukaa chini ambapo alianza kulia bila kukoma.



Ingawa alishawishiwa sana na walimu juu ya safari ya mwanaye kwenda Marekani, moyo wake haukuwa tayari kabisa na safari hiyo. Hakuwa na namna ya kukataa baada ya kuhakikishiwa usalama wa kutosha wa mwanaye. Blandina alimpenda sana Genesis, ni yeye ndiye aliyeufahamu uchungu wa mwanaye vizuri.

Mateso na manyanyaso yote aliyoyapata aliyafahamu yeye mwenye mwenyewe, hata hivyo hakuwa na wasiwasi kwa kuwa alitambua wazi kuwa baada ya mateso yote aliyopata katika maisha yake, hatimaye Genesis angerejesha furaha upya! Alimpenda sana Genesis, hakutaka kaumini kama alikuwa ameshapona kabisa kiasi cha kuwa mbali na yeye kwa muda mrefu.

Siku ya safari ikafika, akiwa uwanjani alisali pamoja na mwanaye na kumtakia safari njema! Muda wote aliokuwa uwanjani alikuwa akimbusu mwanaye na kulia machozi, hakuwa na uhakika sana na safari ya mwanaye, moyo wake uli,mwambia kitu tofauti sana, alihisi matatizo makubwa sana mbeleni. Wakati matukio yote yakigfanyika uwanjani, mwalimu Daniel Mponda alikuwa akipiga picha.

Muda wa kuingia katika chumba maalum cha ukaguzi ukafika, hakuwa na jambo la kufanya zaidi ya kumruhusu mwanaye aingie tayari kwa safari. Alipoingia aliendelea kubaki amesimama huku akiipungia ndege mpaka ilipoishilia mawinguni. Lakini ghafla akahisi mwili wake ukishika ganzi, taratibu akahisi kizunguzungu, akaketi chini kisha akaendelea kulia kwa uchungu. Nini kitafuata? SONGA NAYO…



Kila mmoja alishangazwa sana na kitendo cha Blandina kubadilika ghafla kisha baadaye kuanza kulia. Tayari watu walishamzunguka na kutaka kufahamu kilichokuwa kikiendelea. Watu walimuonea huruma sana, machozi yalizidi kutiririka machoni mwake, akili yake haikutaka kuamini kuwa mwanaye angekuwa salama, kila nukta moja ilipoondoka alihisi matatizo kwa mwanaye.

“Amefanyaje?” Mmoja wa watu waliokuwepo mahali pale aliuliza.

“Sijui ana nini, labda tumuulize!” Mwingine alidakia.

Kweli ndivyo walivyofanya, wakasogea mpaka mahali alipokuwa amekaa kisha wakaanza kumhoji maswali.

“Unajisikiaje dada yangu?”

“Sina tatizo!”

“Sasa mbona unalia?”

“Sijazoea kukaa mbali na mwanangu, isitoshe nahisi kuna tatizo linaweza kutokea!”

“Tatizo gani tena mwenzetu? Mbona hata watoto wetu nao wameenda huko? Kuna usalama wa kutosha dada yangu, wamekwenda kwa ajili ya kujifunza!”

“Nashukuru kwa kunipa moyo, lakini mwanangu ana matatizo, hawezi kukaa peke yake mbali na mimi!”

“Usijali dada, atakuwa salama tu!”

Kwa kiasi fulani alifarijika sana na maneno aliyokuwa akiambiwa na watu waliokuwa wamemzunguka. Hakuwa na jambo lingine la kufanya zaidi ya kwenda kupanda gari na kwenda nyumbani. Kichwa chake bado hakikukaa sawa, hisia mbaya juu ya maisha ya mwanaye bado zilizidi kutawala ubongoni mwake.

Saa tisa kamili za jioni akiwa amepumzika sebuleni kwake akasikia simu yake ikiita. Moyo wake ukazidisha kasi, alishaanza kuhisi kitu kibaya mbele yake. Akasogea taratibu mpaka mahali simu ilipokuwa, kisha akanyanyua mkonga wa simu na kuweka masikioni mwake.

“Hallow!”

“Habari yako mama Genesis?”

“Salama, nazungumza na nani mwenzangu?”

“Mkuu wa Shule ya Tanganyika, mama Gibson!”

“Oh! Mama Gibson una habari zozote mpya?”

“Hapana, ila nilioata taarifa kuwa hukuwa na hali nzuri uwanjani, unaendeleaje sasa?”

“Sijambo!”

Ondoa shaka Blandina, Genesis atakuwa salama!”

“Ok!” Simu ya Mkuu wa Shule, ilimchanganya sana Blandina, hata hivyo hakutaka kuumiza sana kichwa chake, akaamua kuendelea na shughuli zake kama kawaida.

*********

Saa kumi na mbili za jioni kwa saa za Marekani, ndege ilitua katika Uwanja wa JF Kennedy, wanafunzi na walimu wote walikuwa na furaha sana. Watu waliokuwa uwanjani walikuwa wakiwaangalia huku wakitabasamu, walikuwa watoto wadogo waliovaa vizuri na kupendeza sana.

Hawakupata shida, kila kitu kilikuwa kimeandaliwa, watu maalum wa kuwatembeza ziara nzima tayari walikuwa wanawasubiri uwanjani. Mwalimu Nancy Ngatengwa aliona bango kubwa lilionyesha jina la shule yake, lilikuwa limeandikwa; ‘TANGANYIKA INTERNATIONAL SCHOOL KARIBUNI MAREKANI’ Hakuwa na muda wa kupoteza zaidi, akasogea mpaka alipokuwa yule mtu aliyeshika bango.

“Habari yako!”

“Salama karibu!”

“Ahsante sana, naitwa Mwalimu Nancy Ngatengwa kutoka Tanzania!”

“Mimi ni John William kutoka Ubalozi wa Tanzania, karibuni sana Marekani!”

“Tunashukuru sana bwana John!”

Wakaondoka moja kwa moja mpaka kwenye gari waliloandaliwa. Wakapanda na safari ya kwenda Hostel ikaanza. Kila mwanafunzi alionyesha kuwa na furaha sana.

Kati ya wanafunzi walioonekana kuwa na mwaswali mengi zaidi ni Genesis, kila wakati alikuwa akiuliza maswali kwa mwalimu wake. Hata John alishangazwa sana na jinsi mtoto mdogo kama Genesis kuwa na uwezo mkubwa wa kuuliza maswali magumu kama mtu mzima.

“Mwalimu, mji mkuu wa Marekani unaitwaje?”

“Washington DC!”

“Ah! Pazuri sana, naamini nitajifunza mambo mengi sana!”

“Ni kweli kabisa Genesis!”

Udadisi wake uliwashangza wengi sana, kila alichokiona mbele yake ilikuwa lazima aulize. John William mwenyeji wao nchini Marekani, naye alikiri kuwa mtoto huyo alikuwa na akili za kipekee.

Safari yao iliishia katika Hostel moja maalum kwa ajili yao, walipanga kukaa nchini Marekani kwa siku kumi na nne! Usiku wanafunzi wote walilala.

*********

Wanafunzi walitembea vivutio mbalimbali nchini Marekani, kila siku waliondoka asubuhi na kurudi usiku. Walitembezwa katika vituo mbalimbali vya Redio na Televisheni, Stesheni ya Treni ya umeme na sehemu mbalimbali. Waliishi kwa furaha sana nchini Marekani.

Siku ya kumi na mbili nchini Marekani, ikiwa zimebaki siku mbili tu kabla ya safari ya kwenda Tanzania haijaanza, mama Genesis alimpigia simu Mwalimu Nancy Ngatengwa akitaka kujua maendeleo ya mwanaye nchini humo. Hakuwa na amani hata kidogo katika moyo wake, alihisi huenda akapatwa na matatizo.

“Habari za huko mwalimu?”

“Salama tu, watoto wanafurahia sana mazingira ya huku!”

“Genesis anaendeleaje?”

“Ni mzima sana, nina imani akija huko, atakuwa na vitu vingi sana vipya akilini mwake!”

“Ni kweli kabisa mwalimu, naweza kuzungumza na Genesis?”

“Bila shaka!”

Si mwalimu Ngatengwa, Mkuu wa Shule mama Gibson wala Wizara ya Elimu ya Tanzania waliokuwa wakifahamu mpango wa Marekani. Nia ya kuandaa ziara ile ilikuwa moja tu, kumpata Genesis! Tayari mipango ilishapangwa kuhakikisha Genesis anabaki nchini Marekani. Hawakutaka akili ya kipekee ya mtoto kama Genesis ibaki katika nchi masikini kama Tanzania. Ilikuwa lazima Genesis abaki Marekani.

Mwalimu Ngategwa hakuwa na kipingamizi, haraka akamkabidhi simu Genesis na kumtaka azungumze na mama yake.

“Shikamoo mama!” Genesis alimsalimia mama yake.

“Marhaba mwanangu, unaendeleaje sasa?”

“Sijambo kabisa, yaani nimejifunza mambo mengi sana!”

“Genesis mwanangu, unajua nakupenda sana, sipo tayari kukupoteza niambie kama una matatizo yoyote!”

“Nakupenda pia mama, sina tatizo lolote!”

“Nashukuru sana kusikia hivyo mwanangu, naomba unibusu!”

“Sawa mama, acha nikubusu ufurahi mama yangu, najua unanipenda sana hata mimi nakupenda pia! Siwezi kusahau siku uliponiambia mimi nimeresha furaha katika maisha yako!” Genesis alisema maneno hayo kisha akambusu mama yake.

“Ahsante sana mwanangu, nimefurahi kupata busu lako, leo mna ratiba gani?”

“Tunakwenda Miami Beach!”

“Safari njema mwanangu!”

“Ahsante mama!”

Genesis akawa na furaha sana moyoni mwake, kusikia sauti ya mama yake kulimfanya ajisikie vizuri sana. Alimpenda sana mama yake, alikuwa kila kitu katika maisha yake. Wanafunzi wote wakapanda gari kisha safari ya kwenda Miami Beach ikaanza.

Watoto walikula na kunywa kwa furaha sana, walicheza ufukweni. Mpaka inafika saa mbili za usiku, bado walikuwa ufukweni wanacheza. Wakati watoto wakiendelea kucheza, ghafla wakatokea wanaume watatu wakamchukua Genesis na kukimbia naye mpaka kwenye gari kisha wakatoweka.

Watoto wote wakakimbia ufukweni. Mwalimu Ngatengwa hakuwa hakuwa anajua kilichikuwa kikiendelea. Akashangaa wanafunzi wanamfuata wakikimbia!

“Kuna nini?” Mwalimu Ngatengwa akauliza.

“Genesis!”

“Amefanyaje?”

“Amekamatwa na watu kule ufukweni, kisha wakakimbia naye!”

“Nini?” Mwalimu Ngatengwa hakuwa tayari kuamini kilichotokea, John mwenyeji wake na kiongozi wa msafara, alijua kila kitu, ni yeye ndiye alimshawishi wabaki hotelini wakati watoto wakicheza ufukweni. Alifahamu vizuri ilikuwa kazi ya Marekani!

*********

Blandina aliamka akiwa mchovu sana siku hiyo, kila kitu alichotaka kufanya alijikuta anashindwa. Akili yake ikafanya kazi haraka zaidi ya kawaida, alihisi lazima kulikuwa na tatizo lililokuwa mbele yake.

“Hapana kuna kitu kibaya mbele yangu, lazima niwasiliane na Mwalimu Ngatengwa sasa hivi!” Aliwaza. Alikuwa na kila sababu ya kuwasiliana na mwalimu, kila nukta moja ilipoondoka mapigo yake ya moyo yalizidi kuongeza kasi.

Haraka akampigia mwalimu, alipomuuliza habari za Genesis mwalimu akaanza kulia.

“Kuna nini mwalimu?” Blandina aliuliza, lakini mwalimu hakujibu zaidi ya kuendelea kulia. Haraka akampigia simu Mkuu wa Shule ili amwulize kama alikuwa na taarifa zozote juu ya mwanaye lakini naye aliishia kulia.

“Kuna nini? Lazima kuna matatizo, ngoja nimpigie Dk. Ringo nimfahamishe juu ya hili!” Aliwaza.

Akiwa anajiandaa kumpigia simu Dk. Ringo, akashangazwa sana na habari habari aliyoiona kwenye Kituo cha Televisheni cha CNN zilimshtua sana. Juu ya kioo cha TV kulisomeka maneno ‘Breaking news’ yakimaanisha kwa kiswahili habari za kushtukiza. Chini kabisa ulipita mstari wa maneno yenye rangi nyekundu yaliyosomeka; Tanzanian Child Captured at the Beach! Yakimaanisha Mtoto wa Kitanzania ametekwa Beach!

Mapigo ya moyo yakaongezeka, akasogea karibu na TV yake ili aweze kusikiliza vizuri. Aliposikia jina la mtoto wake na shule anayosoma, akatetemeka kwa hofu.

Macho yake yalifunikwa na machozi.



Mapenzi ndio chanzo cha matatizo katika maisha ya Blandina! Hakuna kitu kilichosababisha mateso katika maisha yake kama mapenzi, kuna wakati fulani alianza kujichukia alivyo mrembo, aliamini kama asingekuwa mrembo asingepatwa na matatizo yote katika maisha yake.

Baada ya kujifungua mwanaye Genesis, mpenzi wake Gerald alimkataa na kumfukuza, huo ukawa mwanzo wa maisha yake kuwa mabaya yasiyotamanika! Ni Gerald ndiye aliyemnywesha pombe Blandina na kumruhusu bosi wake amwingilie akiwa ulevini!

Pamoja na mateso yote, mwanaye alikuwa na matatizo ambapo alimpeleka nchini Afrika Kusini kutibiwa na kurudi Tanzania, huko hali ikawa mbaya zaidi baada ya kukuta ofisini kwao kumeshaajiriwa mtu mwingine! Hakuwa na jinsi zaidi ya kuwasiliana na Dk. Ringo ambaye hata hivyo hakuwepo, simu yake ilipokelewa na mtu mwingine aliytejitambulisha kwa jina la Dk. Albert Mkambila, huyo alimwagizia Ifakara na kumpokea. Baada ya siku kadhaa Dk. Ringo alijerea kutoka vijijini alipokuwa akifanya utafiti wa Malaria.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Siku zikaenda, Genesis akazidi kukua, uwezo wake wa akili uliwashangaza wengi, ambapo wageni mbalimbali walifika Ifakara kumwangalia, alikuwa na uwezo wa aina yake! Akisikiliza kitu kwenye redio hakiwezi kutoka tena akilini mwake. Ni hapo sasa Serikali ya Tanzania ilipoamua kumsomesha katika Shule ya Kimataifa ya Tanganyika.

Akiwa shuleni hapo, akachaguliwa kuwa mmoja wa wanafunzi watakaokwenda kutembelea vivutio vya nchi ya Marekani. Ni safari iliyokuwa na mashaka sana kwa mama yake, hakutaka kuamini kama safari ile ilikuwa na mafanikio kwa mwanaye zaidi ya matatizo. Hata hivyo baadaye alikubali kwa shingo upande.

Ikiwa ni saa chache baada kuzungumza na mwanaye kwenye simu, akaona kitu cha ajabu sana kwenye TV yake, ni juu ya mtoto wa Kitanzania kutekwa ufukweni. Zilikuwa habari za kuumiza sana kwake, hakuwa tayari kuamini kama ni kweli alichokiona kilikuwa yakini. Macho yake yakafunikwa na machozi! Nini kitatokea? SONGA NAYO…



Kutokana na mateso aliyopata katika maisha yake, hakuwahi kufikiria siku moja angepata furaha! Pamoja na fikra hizo, lakini Mungu ambaye hakuna linalomshinda chini ya jua, alimpa furaha tena katika maisha yake. Genesis alikuwa furaha tosha katika maisha ya Blandina.

Kitendo cha kupewa nyumba kubwa ya kifahari tena eneo wanaloishi watu wenye hadhi ya juu Masaki, ilikuwa ni mwanzo wa furaha katika maisha yake. Alitamani sana furaha hiyo iendelee kutawala katika maisha yake yote yaliyosalia hapa duniani. Mwanaye Genesis ndiye angekuwa mkombozi wa maisha yake, alimpenda na kumthamini siku zote. Uwezo wake wa akili shuleni ulimfurahisha sana, alimini siku moja lazima mwanaye angeshika nafasi ya juu nchini. Hiyo ilikuwa ndoto lakini ni kama aliona kila kitu kilichokuwa kikitokea katika maisha yake yajayo na mwanaye.

Hata lilipokuja suala la kusafiri na wenzake kwenda nchini Marekani, hakukubaliana na hilo hata kidogo, baada ya mabishano ya muda mrefu sana tena baada ya kushawishiwa na baadhi ya viongozi wa juu wa serikali ndipo akaamua kumruhusu mwanaye aende Marekani.

Wakati akiagana naye uwanjani, ilikuwa ni kama anamuaga kwa mara ya mwisho! Alihisi tukio baya litaka kutokea katika maisha yake. Habari aliyoiona kwenye Kituo cha Televisheni cha CNN zilimtisha!

“…Haiwezekani, jamani Genesis mwanangu, hapana…” Blandina alipaza sauti kisha akaanguka chini na kupoteza fahamu!

*********

Kila neno moja lilipoingia masikioni mwa Mwalimu Nancy Ngatengwa, machozi nayo yalikaribia, aliifahamu vizuri Marekani, sasa alianza kukumbuka maneno ya mama yake Genesis. Kila mmoja alikuwa akimpinga alipokuwa akikataa mwanaye asiende Marekani lakini sasa aliona umuhimu wa kuyafuata maneno ya mama Genesis.

Pamoja na hayo, alikuwa ameshachelewa sana, hakuwa na kitu cha kufanya. Wanafunzi walikuwa waoga wanatetemeka kwa hofu, wakiwa wamemzunguka mwalimu wao na John William waliokuwa wamekaa chini ya mwavuli wa makuti! Mvinyo waliokuwa wanakunywa sasa ulikuwa haunyweki tena!

“Ilikuwaje?” Hatimaye Mwalimu Ngatengwa akauliza.

“Walikuja watu wanne, warefu wanene, wakatuletea ice cream, lakini baadaye wakamkamata Genesis kisha wakakimbia naye!” Mmoja wao akajibu.

“Wameelekea wapi?”

“Kule!” Mwingine akasema huku akisonza kidole, mahali walipoondoka na Genesis.

“John, ni nini kimetokea?”

“Mwalimu si tulikuwa wote hapa muda wote!”

“Sawa, sasa tutafanyaje?”

“Hakuna kitu cha kufanya zaidi ya kwenda kutoa taarifa Polisi!”

“Unadhani watatusaidia kumpata?”

“Inawezekana, si ndio kazi yao?”

“Sawa basi, twende mara haraka!”

“Hakuna tatizo!”

Mwalimu Ngatengwa alichanganyikiwa sana, hawakuwa na kitu cha kufanya zaidi ya kuondoka na kwenda katika Kituo cha Polisi kutoa taarifa za kutekwa kwa Genesis. Wakiwa njiani, kabla hawajafika kituoni, simu yake ikaita haraka akapokea, ingawa alikuwa amechanganyikiwa kwa mawazo tele kichwani mwake.

“Bila shaka nazungumza na Mwalimu Ngatengwa!” Alikuwa ni Blandina amempigia simu mwalimu Ngatengwa.

“Ndio mimi!” Alijibu huku akihema kwa kasi.

“Kuna nini kimetokea huko?”

“Hakuna kitu, kwani nazungumza na nani?”

“Blandina… mama yake Genesis!”

Alipogundua alikuwa akizungmza na mama yake Genesis akachanganyikiwa zaidi. Hakujua sababu ya mama Genesis kumpigia simu, lakini alihisi taarifa hizo zilishamfikia, hata hivyo hakutaka kuamini sana jambo hilo. Kwa alivyofahamu, haikuwa rahisi ndani ya dakika thelathini na tatu tu, taarifa hizo kufika Tanzania.

“Umesema wewe ni nani?”

“Mama Genesis!”

“Ohoo! Kumbe wewe? Hakuna tatizo!” Akajikaza kujibu, ingawa ukweli ni kwamba Genesis alikuwa ameshatekwa!

Baada ya kubanwa maswali mengi alishindwa kujibu ipasavyo, akajikuta akiangua kilio kwenye simu, hakuweza kuficha huzuni na wasiwasi alionao ingawa pia hakuweza kumweleza ukweli wa kilichotokea.

“Mwalimu kuna nini, mbona sikuelewi?”

Mwalimu hakujibu kitu, baadaye akaamua kukata simu. Safari yao ya kuelekea kituoni ikaendelea. Walipofika, waliegesha gari lao nje ya kituo kisha Mwalimu Ngatengwa na John kwa pamoja wakaongoza kuelekea mapokezi. Kila askari aliyewaona, alijua wazi kuwa kulikuwa na tatizo kubwa lililojitokeza. Kwa John ilikuwa sawa na sinema, alifahamu kila kitu kilichokuwa kikiendelea.

*********

Blandina alipoteza fahamu kwa muda wa saa mbili na ushee, muda wote alikuwa ameanguka juu ya sofa kubwa lililokuwa sebuleni, bila msaada wowote! Hakujua kilichokuwa kikiendelea. Alipozinduka akaanza kuangaza macho yake huku na huko, mpaka alipokumbuka kilichotokea!

Hapo sasa akaanza kulia upya! Mwanaye alikuwa kila kitu katika maisha yake, kichwa chake kikavurugika! Haraka akavuta kumbukumbu juu ya jambo alilokuwa akitaka kufanya, akakumbuka kila kitu, alikuwa anataka kumpigia simu Dk. Ringo. Muda huo huo bila kuchelewa akasogea mpaka mezani, kisha akazungusha namba na kumpigia Dk. Ringo, baada ya muda mfupi, simu ilipokelewa. Kilio ndio ilikuwa salamu yake!

“Unalia nini Blandina?”

“Inanipasa kufanya hivi!”

“Kwanini?”

“Si unakumbuka juu ya taarifa za Genesis kwenda Marekani?”

“Ndio, tena kesho kutwa anarudi sio?”

“Ndio, lakini kuna taarifa mbaya nimeona kwenye TV!”

“Taarifa gani hizo Blandina?”

“Genesis ametekwa ufukweni!”

“Nini?”

“Ni vigumu kuamini lakini ndivyo halisi ilivyo, naomba uje Dar es Salaam haraka ili unisaidie, hapa nilipo sina la kufanya!”

“Leo hii nitakuwa Dar es Salaam usiku!” Baada ya hayo, wakakata simu, kila mmoja alipatwa na majonzi sana katika moyo wake. Blandina alizidi kulia, hakuwa tayari kumpoteza mwanaye wa pekee aliyempenda kuliko kitu chochote duniani! Kumpata ilikuwa ndoto ambayo alitamani sana siku moja itimie.

Alitamani sana kukutana na mwanaye kwa mara nyingine. Kuanzia hapo muda wote alikuwa akilia, alimsubiri kwa hamu kubwa sana Dk. Ringo akiamini ndiye msaada pekee uliokuwa umebaki.

*********

Marekani haikuandaa safari ya wanafunzi wa Shule ya Kimataifa ya Tanganyika kwa nia ya kujifunza, walikuwa na nia moja tu, Genesis! Sifa za uwezo wake kiakili, ziliwafanya wafikirie kumchukua kisha kumpotezea kumbukumbu zote kwa sindano maalum, ili abaki Marekani kama raia wao! Genesis alikuwa na akili kuliko kawaida!

Baada ya watu waliomteka Genesis kuondoka ufukweni, walikwenda moja kwa moja mpaka katika msitu mkubwa uliokuwa nje kidogo ya jiji la Washington, ilikuwa ni amri ya wakuu wao wa kazi. Waliamriwa baada ya kufika katikati ya msitu huo, ambapo kulikuwa na sehemu maalum kwa ajili ya kumficha, wangemchoma sindano yenye dawa ya kupoteza fahamu na kumbukumbuku, kitaalamu iliitwa Memory Fraser II.

Baada ya kuchomwa sindano hiyo, Genesis asingekumbuka kitu chochote kilichopata kutokea katika maisha yake, angekuwa mpya asiyejua chochote, lakini Marekani ilipanga kumfundisha kila kitu upya ili awe hazina yao. Safari ya kwenda msituni iliwachukua takribani saa nne kwa gari ndogo. Genesis alilia sana lakini hakuna aliyemsikia.

“Mnanipeleka wapi?”

“Tulia wewe, huruhusiwi kuuliza maswali!” Genesis alijibiwa kama mtu mzima, kumbe alikuwa mtoto mdogo mwenye umri wa miaka mitatu na nusu tu!

“Mnataka kunifanya nini?”

“Shut up!”

Genesis hakuwa na kitu cha kufanya zaidi ya kulia muda wote, baada ya mwendo mrefu, usiku wa saa tano magari yao mawili yalisimama katikati ya msitu katika eneo lililoandaliwa kwa kazi ya kumchoma Genesis sindano ya kumpotezea kumbukumbu zote za maisha yake.

****

Furaha iliyokuwa katika maisha yake ilishatoweka, pamoja na kutoweka huko, tayari alishaanza kuona mwanzo wa furaha nyingine ambayo ililetwa na Genesis, lakini ikayeyuka ghafla baada ya kutekwa na majangili ufukweni! Blandina alilia sana, hakuweza kufanya kitu chochote tena, alishinda akilia kila siku!

Blandina hakutaka kuamini mara moja kuwa mwanaye alitekwa, alitamani sana kuishi na mwanaye, alikuwa ndio furaha pekee iliyobakia katika maisha yake, moyo wake ulimuuma sana, hakuwa na njia yoyote ambayo angeweza kuitumia ili ampate Genesis. Kichwa chake kikawa kizito sana, mtu pekee ambaye aliamini angeweza kuwa msaada katika hilo ni Dk. Ringo! Aliendelea kumsubiri kwa hamu kubwa. Kila aliposikia kengele ya getini ikilia, akili yake ilimtuma moja kwa moja kuwa alikuwa ni Dk. Ringo, ila alipotoka haraka kufungua mlango, alikuwa ni mgeni mwingine.

Lilikuwa jambo lililomuudhi sana, ni kama alikuwa akicheza sinema! Mpaka inafika saa mbili unusu za usiku, Dk. Ringo alikuwa hajafika nyumbani kwake. Hata hivyo Dk. Ringo hakutoa taarifa yoyote kuhusu kukwama kufika Dar es Salaam, Blandina akachanganyikiwa zaidi!

“Nahisi nimeumbwa ili niteseke, msaada wangu wa pekee uliobakia ni Dk. Ringo lakini mpaka sasa hivi hajafika, kuna nini?” Aliwaza Blandina, baadaye akapata wazo jipya, ilikuwa lazima ampigie simu ili kujua kilichompata. Alipompigia simu alichanganyikiwa zaidi, simu ya Dk. Ringo haikupatikana.

Hapo ukaja msululu mrefu wa maswali ambayo hakuweza kuyapatia majibu yake haraka. Machozi yakazidi kumtoka machoni mwake, aliamini aliumbwa ili aumie, moyo wake ukazidi kwenda kasi, aliamini mwanaye alikuwa amepatwa matatizo makubwa sana.

Baada ya kumsubiri Dk. Ringo kwa muda mrefu bila mafanikio, mwishoni aliamua kuingia chumbani kwake kulala! Alijitahidi kuvuta usingizi kwa kila hali lakini hakuweza kuupata. Akaamua kuwasha TV yake ili aendelee kupata habari za matukio mbalimbali. Baadaye kidogo akasikia mlango wa chumba chake ukigongwa, hakuwa na wasiwasi sana, aliamini alikuwa ni Diana msichana wake wa kazi.

Haraka akateremka kitandani kisha akaenda mlangoni na kuufungua, hakuwa amekosea, alikuwa ni Diana, lakini swali lililopata nafsi katika ubongo wake ni kwamba alikuwa anataka nini usiku mwingi kiasi kile? Tayari ilishafika saa nne na ushee za usiku.

“Vipi Diana, kuna usalama kweli?”

“Usalama upo mama, usijali!”

“Nimeshtuka kukuona usiku huu, sio kawaida yako!”

“Ni kweli mama ila kuna mgeni wako mlangoni, baada ya kusikia kengele nilizungumza naye kwa simu ya mlangoni, nikaona nikutaarifu kwanza!”

“Anaitwa nani?”

“Dk. Ringo!”

“Unasema nani?”

“Dk. Ringo, mbona umeshtuka?”

Blandina alishtuka sana, hakutaka kuamini haraka kuwa Dk. Ringo alikuwa ameshafika nyumbani kwake. Hakutaka kuuliza maswali zaidi, alichokifanya ni kutoka moja kwa moja mpaka getini ambapo alifungua geti na kumruhusu Dk. Ringo kuingia ndani.

“Karibu Dk. Nilijua usingekuja!”

“Ahsante sana, ilikuwa lazima nije, ila kuna mambo yaliingiliana kidogo!”

“Pole sana Dk.”

“Ahsante sana!”

Muda huo huo taksi aliyokuja nayo Dk. Ringo ikaondoka, Blandina na Dk. Ringo wakaongozana hadi ndani, moja kwa moja wakaishia sebuleni.

“Enhee, ilikuwaje?” Dk. Ringo akaanza kumuuliza Blandina haraka haraka.

“Ni habari ndefu kidogo Dk. lakini kwanini simu yako ilikuwa haipatikani?”

“Iliisha chaji, halafu usafiri ulikuwa wa shida sana, gari limeharibika mara tatu, Kisawasawa, Kilombero na Mikumi yaani ilikuwa safari ya mkosi sana, sikutegemea kama ningefika salama, lakini namshukuru Mungu kwa uangalizi wake!”

“Amen!”

“Enheee!” Dk. Ringo alikuwa na hamu sana ya kutaka kujua chanzo cha tatizo.

“Nimeona kwenye TV habari hizo, kimsingi mtoto ametekwa!”

“Na nani sasa?”

“Wanadai majangili!”

“Ili wampeleke wapi?”

“Hakuna anayefahamu, lakini si unakumbuka jinsi Genesis alivyokuwa akipiganiwa na Japan, China na Marekani? Huwezi kuona kuwa kuna kitu kimefanyika hapo?”

“Sidhani kama kuna kitu cha aina hiyo, lakini si umesema kuwa askari wa huko wanafuatilia?”

“Ndio, lakini nahisi wanajaribu kuidanganya dunia!”

“Sasa tulale, halafu asubuhi nitakuambia mahali pa kuanza kufuatilia!”

“Sawa Dk.” Blandina akamwelekeza Dk. Ringo chumba chake kwa ajili ya kulala. Naye akaenda chumbani kwake kulala.

*********

Uwezo wa kiakili wa Genesis uliwavutia wengi, nchi kama Marekani, Japan na China walikuwa wakifuatilia kwa makini nyendo za mtoto huyo mwenye kipaji kila kukicha! Siku zote walitamani mtoto huyo awe wa nchi yao. Kila nchi kupitia vitengo maalum vilivyoteuliwa vilikuwa makini kufuatilia maisha ya Genesis, kila nchi ilipanga mikakati ya kumteka!

Japan iliwaza mbali zaidi, pamoja na kupanga mikakati madhubuti, lakini walitambua wazi uwezo wa Marekani katika kupanga mitego ya mateka! Kwa kutambua umuhimu wa hilo, haraka wakamtuma mmoja wa wapelelezi wao kwenda kufanya uchunguzi juu ya kutekwa kwa Genesis nchini Marekani!

George Elias ndiye aliyeteuliwa kufanya kazi hiyo, alifika Marekani kisha akafanya upelelezi na kuweza kujua kundi zima lililoandaliwa kumfutilia Genesis. George alikutana na Jacob ambaye alikuwa mmoja wa majangili wa Marekani na kumpa kila kitu kilichopagwa!

“Ila naomba usije ukanisaliti ndugu, maana kifo kitakuwa halali yako!” Jacob alimwambia George.

“Usiwe na shaka ndugu yangu!”

“Malipo yangu yapo vipi?”

“Mazuri sana, nchi yetu inamhitaji sana Genesis, tutakupa kiasi chochote cha pesa utakachohitaji!”

“Hakuna tatizo, nitawasaidia ila kama nilivyokuambia mwanzo kuwa ukinisaliti, uhai wako utakuwa halali yangu!”

“Nakuahidi ndugu yangu!”

“Timiza ahadi yako!”

“Usijali ila nataka kujua kazi itafanyika vipi? Mpaka sasa hivi mmefikia wapi?”

“Tumepanga shule yao ije itembelee vivutio vya huku nchini kwetu, sharti tulilowapa ni kwamba Genesis lazima awepo, hapo ndipo tutakapomteka!”

“Sawa basi, naomba tuwasiliane kila hatua!”

“Hakuna tatizo!” Ndivyo ilivyokuwa, Jacob na George wakawa wanawasiliana kwa kila hatua.

Siku Genesis alipotekwa ufukweni, Jacob alimfahamisha George ambaye alikuja na ndege yao akiwa na majangili wenzake. Haikuwa kazi ngumu sana, kwa kutumia mawasiliano ya kifaa maalum alichokuwa amevaa Jacob kiunoni mwake aliweza kuwapa ramani yote mpaka msituni walipokuwa wamepanga kwenda kumchoma Genesis sindano ya kupoteza kumbukumbu!

*********

Katikati ya Msitu wa Marakon uliokuwa pembeni mwa mji wa Hawaii kulikuwa na nyumba kubwa kwa ajili ya shughuli za kijasusi kwa manufaa ya nchi ya Marekani. Walipofika walimshusha Genesis na kumwingiza katika chumba maalum kwa ajili ya kumchoma sindano ya kumpotezea kumbukumbu!

Kabla hawajafanya kitu chochote, ikiwa ni dakika ishirini tu baada ya kufika katika nyumba hiyo, wakasikia mlio wa risasi nje.

“He, kuna nini tena?” Mmoja wao akauliza.

“Lazima kuna tatizo, hebu nendeni nje mkaangalie!” Kiongozi wao akawaamrisha.

“Ila lazima muwe makini sana!” Akawatahadharisha.

“Sawa mkuu!” Hawakutaka kupoteza muda, haraka wakatoka nje, ghafla wakashangaa kuzungukwa na watu waliojifunika sura zao, wakiwa na bunduki kila mmoja mikononi mwao.

“Haya shusheni silaha chini!” Mmoja wao akasema.

“Hatushushi!” mmoja wa majangili wa Marekani wakajibu.

“Unasemaje?” Alipomuuliza, akampiga risasi moja iliyompata mguuni.

“Nasema shusheni bunduki zenu chini!” Hakuna aliyeshusha, walionekana wamejiandaa kupambana nao!

Kukataa kwao kulimaanisha ubishi na kuonyesha jeuri, muda huo huo wakainua bunduki zao juu kisha majangili waliomteka Genesis, wakamiminiwa risasi zilizosababisha vifo vyao papo hapo! Majangili wote watano waliotoka nje walikufa!

“Ingieni ndani mkawamalizie na hao wengine!” Kiongozi wao akawaambia.

Hawakupoteza muda, wakaingia haraka mpaka ndani, kabla hawajafika katika chumba alichokuwa amefungiwa Genesis, wakasikia vishindo vya mtu akija uelekeo wa mahali walipokuwepo!





Wanafunzi wa Tanganyika International School walikuwa ufukweni mwa Bahari wakicheza na kwa furaha. Kila mmoja alikuwa akifurahia mazingira mapya mjini Hawaii Marekani. Ufukwe wa Miami ulikuwa umechangamka sana siku siku, wakati wanafunzi wakiwa wanaendelea kucheza, mwalimu wao aliyeitwa Ngatengwa, alikuwa ameketi chini ya mwavuli wa makuti akipata mvinyo na mwenyeji wake John William.

Wakiwa wanaendelea kucheza, wakatokea wanaume wawili na kuwafuata, wakawagawia ice crem kila mmoja, ghafla wakamvuta Genesis na kukimbia naye mpaka kwenye gari. Bila kupoteza muda wakaondoka kwa kasi ya ajabu ufukweni.

Walikuwa majangili! Baada ya kuingia garini safari ya kwenda katika Msitu wa Marakon ikaanza! Huko wakajiandaa kumchoma Genesis sindano ya kumpotezea kumbukumbu, kabla hawajafanikiwa kufanya hivyo, wakasikia mlio wa risasi nje, majangili wengine watano wakatoka nje, nao wakakutana na kifo! Ni akina nani hao waliowavamia? SONGA NAYO…



Pori lilikuwa tulivu sana, hapakuwa na sauti yoyote iliyosikika zaidi ya ndege na wanyama wa porini. Katikati ya msitu huo kulipokuwa na nyumba kubwa ya majangili, kulikuwa na mvurugano kati ya majangili wa Marekani waliomteka Genesis na wavamizi wengine ambao mpaka wakati huo, Wamarekani hawakuweza kuwafahamu ni akina nani!

Siri ilikuwa moyoni mwa Jacob pekee ambaye alikuwa akiwapata taarifa majangili wa Japan kila hatua iliyokuwa ikiendelea porini, wakiwa wapo katika hatua za mwanzo za kumchoma sindano Genesis, tayari walishafika na kuwapuputisha majangili watano, ambao walikufa papo hapo! Baada ya kuwaua majangili hao watano, walitakiw akuingia ndani haraka na kumalizia kazi waliyoifuata, haikuwa nyingine zaidi ya kumpata Genesis! Genesis ndiye ambaye alihitajiwa na Japana na sio kitu kingine chochote!

Uwezo wa akili wa Genesis ulikuwa na thamani kubwa sana kwao! Wakiwa wanataka kuingia katika moja ya vumba vilivyopo katika nyumba hiyo, wakasikia kitu kama kishindo, ilibidi wasogee pembeni kwa tahadhari wakisubiri kitakachotokea!

“Lazima tuwe makini jamani, kuna mtu nadhani anakuja!”

“Sawa sawa, tumekusoma mkuu!” Wote wakaitika.

Kiasi cha sekunde ishirini na tatu, wakasikia vishindo vikiongeza sauti, baada ya muda kidogo, wakaona majangili watatu waliofunika macho yao wakipita, haraka wawili kati yao wakafuata kwa nyuma, wakiwa wanakaribiria kufika katika mlango mkubwa wa nje, wakageuka nyuma, lilikuwa kosa kubwa sana, haraka majangili wa Kijapan wakawamiminia risasi na wote wakaanguka chini kama mizoga.

“Tuachane nao, hebu tuwahi ndani kwenye mtoto kwanza!”

“Hakuna tabu twendeni!” Wakaingia kwa hatua za taratibu mpaka walipofika ndani. Wakaingia katika mlango mwingine mkubwa, kwa mbali wakaanza kusikia sauti ya mtoto akilia.

“Hii sauti inatokea wapi?”

“Nadhani ni chumba cha pili!”

“Sasa gawanyikeni, waingie wawili kwanza halafu mkifika anzeni kazi, ikiwashinda mtoe ishara tuje tuongeze nguvu, wacha sisi tuimarishe ulinzi hapa, hakuna chura yoyote atakayepita hapa!” Mmoja wao akasema.

“Sawa!” Muda huo huo wakaingia katika chumba walisikia sauti ya kelele ya mtoto, ilikuwa lazima wawe makini sana.

Walipoingia tu, ndani wakawazunguka majangili wawili waliokuwa ndani, huku mmoja akiwa ameshika bomba la sindano tayari kwa kumchoma Genesis.

“Acha unachotaka kufanya sasa hivi!”

“Nyie kama nani mnaoweza kutuamrisha?”

“Nimekuambia acha hicho unachotaka kufanya!”

“Siachi!”

“Nimesema acha haraka, tena tupa sindano chini kabla sijakubadilisha jina sasa hivi!”

“Hamuwezi kutufanya kitu chochote nyie!”

“Unasemaje?”

“Hamuwezi…” Hawakutaka kupoteza muda zaidi, waliona kuchelewa kwao kungeweza kuwasababishia matatizo zaidi mbeleni, hilo lilikuwa jambo ambalo hawakulitarajia kabisa, kwao ilikuwa lazima waondoke na Genesis na kuwauwa majangili wote, isipokuwa Jakob!

Kwa kuwa Jakob alikuwa akielewa kila kitu kilichokuwa kikiendelea, muda mfupi kabla majangili wa Japan hawajaiteka nyumba hiyo, alijificha stoo! Baada ya kuridhika kuwa kati yao hapakuwa na Jacob, kazi yao ilikuwa moja tu, kuwamiminia majangili wote risasi ambao walianguka chini kama mizoga!

“Sasa nini kinaendelea?”

“Nini tena zaidi ya kumchukua huyu mtoto?”

“Mchukue huyo mtoto tuondoke!” Mmoja wao akasema. Ndivyo ilivyokuwa, haraka wakamchuku na kuingia naye haraka kwenye gari, kabla hawajaondoka, Jacob akawasilina nao kwa simu ya upepo, wakamsubiri!

“Najua mmeshafanikiwa, ila naomba sana msije mkanisaliti!”

“Hakuna tatizo!” Wakamjibu, gari likawashwa kisha safari ya kwenda Hawaii ikaanza, akili ya mkuu wa msafara ilifanya kazi kuliko kawaida, kumuacha Jacob hai kulimaanisha matatizo mbeleni.

Alichokifanya ni kuiweka bunduki yake kisha akamwita Jacob kwa sauti kubwa. Jacob aliposikia akatoka nje haraka, alipokaribia gari akapigwa risasi zisizo na idadi katikati ya kichwa chake! Akaanguka chini kama mzigo wa kuni.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Kwanini umefanya hivyo mkuu?”

“Hili suala ni zito sana, tungemuacha huyu, lazima angetuchoma siku moja!”

“Unamaanisha nini?”

“Lazima atabanwa na wakubwa zake, kwanini wenzake wote wafe, halafu yeye abakie mzima?”

“Ni kweli!” Wakaondoka moja kwa moja mpaka Hawaii, hapo ndege yao ilikuwa tayari kwa safari, wakaingi na safari ya kwenda jijini Tokyo, Japan usiku huo huo ikaanza.

*********





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog