Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

MY CLASSMATE - 4

 






Simulizi : My Classmate

Sehemu Ya Nne (4)







Daniel alienda Dar es salaam kwa lengo Moja mtu, kupata lishe bora ili kurejesha siha yake.Arudi katika mapambano haya mazito !



Kutokana na matunzo na vyakula akivyokula, baada ya wiki moja hali ya Daniel ilirudi kama zamani.



Baada ya kupona Daniel kabisa alisimuliwa na IJP madhara waliyoyafanya wauaji kipindi chote alichokuwa kuzimu.Walishaua watoto wa vigogo wengine watano.Toka katika mikoa tofauti .Walishaua wapelelezi kumi na moja na raia wema ishirini.Wote waliwauwa kwa mtindo uleule.Kwa kutumia sumu kali aina ya proxine !



"Nchi sasa ipo katika hali ya hatari sana.Tegemeo pekee ni wewe Daniel. Najua ulishapiga hatua flani katika upelelezi wako.Nchi inakutegemea sana.Raisi anakutegemea sana.Watanzania wanakutegemea sana. Hebu nenda kaumalizie upelelezi wako."IJP John Rondo alikuwa anaongea kwa sauti ndogo na yenye hisia.



"Usijari mkuu.Nakuahidi ndani ya siku tatu nitakuwa nishawaonesha hawa mahayawani mimi ni nani ?Hii ni ahadi mkuu"

"Nakuamini na kukutegemea sana Daniel"



Daniel sasa aliingia kazini kwa kasi mpya.Alibeba dhima ya Taifa.Nyuma yake kulikuwa na Watanzania zaidi ya milioni hamsini wakimtegemea yeye.Wakimtumaini yeye pekee.

*************



Daniel alienda Arusha.Pamoja na mauaji kusambaa Tanzania nzima.Lakini Daniel alienda Arusha.Aliamini ndio kitovu cha mauaji haya ya kikatili !.



Mida ya saa kumi jioni ilimkuta yupo jijini Arusha .Kitu cha kwanza alienda moja kwa moja kituo cha Polisi Arusha. Kuongea na Abdul.Hadi hapo hakuwa anajua kama Mzee aliyemuokoa msituni ndiye Baba yake Abdul.



"Habari za siku Abdul"

"Safi.Vipi ulifanikiwa kaka Abdul"

"Tunaelekea katika ushindi sasa"

"Daah nashukuru sana kaka daniel"

"Hivi ulishawahi kumuona mumewe Raiya?"

"Hapana"

"Unajua chochote kuhusu yeye"

"Mmmmmm yah nimekumbuka, Mayasa alisema ni mtoto wa baba yake mdogo"

"Safi sana.Ndani ya siku tatu tutajua mbivu na mbichi.Umenipa pa kwenda kumalizia sakata hili"

"Mimi nakuombea kila la heri"

Waliagana.



Daniel alitoka katika chumba kile cha siri akiwa na pakuanzia.Aliamua kwenda Zanzibar. Nyumbani kwa wazazi wa Salehe angeyajua mengi.Alijipongeza kwa kitendo chake cha kuja kuongea na Abdul kwanza.



Ndege ya alhamisi asubuhi ilimchukua Daniel.Kumpeleka Zanzibar.

Ndege ilimfikisha hadi kiwanja cha ndege cha Zanzibar. Sasa alijiona anaukaribia ukweli wa sakata hili.



Alianza kuulizia nyumba ya kina Salehe.Daniel alishangazwa sana na umaarufu wa Salehe. Cha ajabu yeye hakuwahi kumsikia kabisa kabla ya sakata hili.



"Unaelekea wapi ?"

"Nyumbani kwa Mzee Makame"

"Makame yupi ?"

"Yule ndugu na makamu wa Raisi"

"Ahaa Makame Abdullah,ni elfu tano nauli"

'Haina shida"



Dakika ishirini baadae Daniel aliteremshwa barazani mwa Nyumba ya mzee Makame.Roho ilikuwa inamdunda.Nywele zilikuwa zinamsisimka.Hakujua kwanini ?

Alipapasa bastola yake ilikuwa sehemu sahihi.Alipiga hatua kuelekea kwenye nyumba ile iliyomtia shaka sana Daniel .

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alipiga hodi mara tatu.Alisikia mlio wa miguu mtu akija kufungua mlango.Mlango ulifunguliwa na kijana mmoja aliyekuwa na asili ya kiarabu.Walitazamana na Daniel !



Macho ya yule kijana yalikuwa ya kawaida kwa mtu wa kawaida.Lakini kwa Daniel hayakuwa macho ya kawaida.Macho ya kijana yule yalikuwa na woga na wasiwasi ndani yake .



"Anaogopa nini ?" Daniel alijiuliza mwenyewe.



"Habari kijana ?"

"Nzuri"

"Samahani namhitaji Mzee makame"

"Una miadi nae ?"

"Hapana"

"Nimwambie mgeni anaitwa nani ?"

"Njemba "Daniel alidanganya.

"Sawa"



Kijana hakuruhusu Daniel aingie ndani.Alimuacha palepale mlangoni.Kwa utamaduni wa watu wa Zanzibar haikuwa kawaida.



"Kuna kitu" Daniel alijisemea tena.



Baada ya dakika tatu mlango ulifunguliwa tena na kijana yuleyule.



"Karibu ndani"

"Ahsante"



Walifika sebuleni.Daniel alichagua sofa moja.Akakaa.



"Naenda kumwita mzee"

"Sawa"



Yule kijana alipotoka.Daniel alizungusha macho yake mle sebuleni kwa harakaharaka.Hakuona la ajabu.

Akatulia sofani.



Alitokea Mzee mwenye umri kati ya miaka sitini na sitini na tano.Daniel akajua huyo ndiye mzee Makame.

Walisalimiana kwa kupeana mikono.Mzee makame alikaa kwenye sofa likilotazamana na Daniel.



"Eeh nakusikiliza kijana"

"Naona mnakaribia kufanikiwa"Daniel alisema akiwa anamtazama Mzee Makame.

"Sijakuelewa kijana"

"Nazungumzia mpango wenu wa Angamizo"

"Mzee alistuka kidogo.

" hahaha nilijua tu, wewe ni Daniel Mwaseba.Umekifata kifo chako !"

"Sijakuelewa Mzee"

"Utanielewa baada ya dakika tano"



Kumbe Mzee makame Alimuona Daniel tangu anashuka kwenye teksi.Alikuwa anamtambua Daniel .Alichokifanya ni kukimbilia chumbani wakati yule kijana akimchelewesha Daniel kwa makusudi pale mlangoni.



Alipaka sumu hatari ya Proxine mkononi Halafu alivyoingia walisalimiana na Daniel kwa mikono.Alikuwa anategemea Daniel atakufa muda wowote ! Daniel atavuka ngozi !



"Nisalimie kuzimu Daniel" Mzee Makame alisema kwa kebehi.

Daniel alikaa kimya!



Mzee Makame alikuwa anaongea huku anatoa dawa ya kutoa madhara ya Proxine mfukoni kwake.Ili ajipake kujinusuru yeye.



Daniel alisimama......!



*************

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Daniel alisimama..!



Daniel Mwaseba alikuwa ana akili kuliko Mzee Makame alivyokuwa anafikiria.

Daniel alisimama, akaanza kumfuata Mzee Makame pale aliposimama.

Mzee Makame alikuwa anajishughulisha kutoa ile dawa mfukoni kwa haraka.Alibabaika sana.

Hakufanikiwa!



Daniel alimkaribia zaidi, alipiga karate kali katika mkono aliokuwa anatolea dawa.Mzee Makame na uzee wake karate ilimuingia hasa mkononi.

Mzee Makame alibaki na mshangao usoni huku akiugulia maumivu.Alikuwa anashangaa kwanini Daniel yuko imara.Pamoja na kumpaka sumu ile Kali ya Proxine !.



Yeye alianza kuisikia ile sumu kwa mbali.Ilikuwa inaanza kumdhuru taratibu.Wakati Daniel Alikuwa ngangari !



Yule kijana aliyemfungulia mlango Daniel alikuja ukumbini. Alishangaa kumkuta Mzee Makame yupo katika hali mbaya kidigo.Huku Daniel akiwa imara.Alitia mkono mfukoni kutaka kutoa akichotaka kutoa.

Hakuwahi!

Naye alipigwa kareti moja ya kiume ya shingo.Hakuweza kustahamili uzito wa karate ile kwa sehemu aliyopigwa.

Alienda kuzimu taratibu !



Mzee Makame alianza kuvuka ngozi sasa.Kwa mara nyingine Daniel alijipongeza kwa hatua yake ya kwenda kumhoji Abdul kwanza Arusha.Na kuja Zanzibar kufatilia sakata lile.



Daniel sasa alivua ngozi laini aliyovaa mkononi.Ilikuwa ngozi ya plastiki inayofanana na ngozi ya kiganja chake.Alikuwa amevaa kama 'gloves'

Akavua mikono yote miwili.Akajisachi mfukoni akatoa ngozi zingine mpya.Akazivaa .

Akaanza kuipekua nyumba ile ya Mzee Makame.



Alipekua nyumba mzima hakupata kitu.Alikata tamaa.

Mwishoni aliamua kupanda juu ya dari .

Akayakuta maboksi kumi makubwa.Ya rangi ya bluu.

Daniel akatabasamu !



Akiwa kule kule darini alijaribu kulifungua boksi moja.

Alikuta vichupa vidogovidogo vingi. Vimeandikwa Proxine !.



"Hawa jamaa wana nia gani lakini ?"

Alijiuliza mwenyewe.Hakukuwa na wa kumjibu.

Akayashusha yale maboksi yote kumi.

Akawa anafikiri ayafanye nini ?



Alikumbuka.

Alipiga simu kwa IJP Rondo.

Ndani ya dakika kumi gari ya Polisi waliokuwa doria waliwasiri.Waliyabeba maboksi yote ya sumu.Pamoja na miili ya marehemu.

Wakati Polisi wanaenda kituoni.Daniel alipanda boti kuelekea Dar es salaam.Bado aliendelea na kazi.



Ndani ya masaa matatu Alikuwa feri.

Alishuka kama abiria wengine.Hakuna aliyekuwa anajua kama Daniel ametoka kufanya jambo kubwa sana Kisiwani Zanzibar muda mfupi uliopita.Vichupa vile visingekamatwa vingesababisha watanzamia wengi sana wauwawe.Daniel alijiona shujaa.Na kweli alikuwa shujaa !



Safari yake ilimpeleka moja kwa moja kwenye nyumba ya Salehe,Mikocheni. Alipokaribia aliona jinsi walivyoimarisha ulinzi.Kulikuwa na walinzi wanne getini .



Aliamua kuingia nyumba ile mchana uleule.

Hakuwa na muda wa kupoteza.

Alidhamiria kulimaliza suala lile ndani ya siku tatu tu.

Alienda pale getini kulikuwa na walinzi watatu.



"Tukusaidie nini Bosi ?"

"Namuulizia kaka Salehe"

"Hayupo"

"Kaenda wapi ?"

"Kaenda Zanzibar,kuna matatizo"

"Ameenda kwa usafiri gani ?"

"Ndege"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sawa"



Walinzi wale walionesha hawakuwa wanajua ubaya wa Bosi wao.Wao walikuwa wameletwa tu na kampuni moja ya ulinzi kulinda usalama wa nyumba ile.Walikuwa na nidhamu ya kazi nzuri.



Daniel alimpigia simu IJP Rondo.Atume askari wa kutosha uwanja wa ndege wa Zanzibar.Kuhakikisha Salehe anakamatwa hapohapo uwanjani.



Muda huo Salehe alikuwa ndani ya ndege ndogo ya Coastal.Alikuwa amechanganyikiwa sana.Hakuamini alipoambiwa kuwa baba yake mzazi amefariki.Baba yake Alikuwa anajua mbinu za kijasusi.Ingawa siyo kwa kiwango kikubwa sana.Lakini hakuwa mtu wa kufa kama kondoo.Alishangaa sana .

Na aliuwawa vipi wakati Proxine zilikuwa ndani.Kwanini hakuzitumia alipoona hatari inamkaribia?



Mbaya zaidi kikichomuumiza kichwa Salehe ni maboksi kumi ya Proxine yaliyopo darini.

Kati ya maboksi kumi na tano yaliyoingia nchini kumi waliyahifadhi kwa Mzee Makame.

Alikuwa anajiuliza ni nani aliyeikaribia ngome yake kiasi kile.Hakumfikiria kabisa Daniel Mwaseba. Alijua Daniel kashajifia zamani huko Bagamoyo porini.



Ndege aliyopanda Salehe ilikuwa inatua uwanja wa ndege wa Zanzibar .

Askari wakiwa makini.

Salehe akiwa hana hili wala lile.Hakujua kama kuna kundi la askari lilikuwa linamsubiri kumlaki nje ya uwanja.



Wakati huohuo Daniel alikuwa ndani ya boti anarudi Zanzibar tena.Alikuwa anataka kumhoji mwenyewe Salehe atakapokamatwa ili aujue kiundani mpango wao wa Angamizo..!



Wakati Ilipokuwa inatua ndege Salehe alihisi kitu.Alihisi kuna hali ya hatari uwanjani.Ni machale tu yalimcheza.Akawa tayari kwa lolote.

Tayari kuua!

Tayari kufa !



Kaspersky na Zwangendaba walikuwa ndani ya Noah ndogo nyeusi iliyopaki pale uwanja wa ndege.Walikuwa wanamsubiri Bosi wao Salehe wampeleke nyumbani kwake.Wao walitangulia kufika. Wakiwa na laptop yenye siri nzito !



Hawakuzielewa elewa kabisa sura walizoziona uwanja wa ndege.Waliona sura nyingi za kiaskari wakiwa kama wanamsubiri mtu.Hawakuwa askari wa kawaida wa uwanja wa ndege.

Ingawa walivaa nguo za kiraia ila haikuwapa shida kwa kina Kerspesky.



Umakini wao uliongezeka huku wakifikira njia ya kumtoa Salehe kwenye mtego ule mujarabu..!



Wakati ndege inatua kaspersky alimpigia simu Salehe.



"Hallo Kerspersky, ndio natua hapa"

"Kuwa makini Bosi.Hali si shwari nje huku"

"Usijari, nishastuka, nitawaachia manyoya tu !"

"Nakuamini"

Simu ilikatwa.



Ndege ilitua salama katika uwanja wa ndege wa Zanzibar.

Huku Salehe akisubiriwa kwa hamu kupokelewa na askari Polisi makini zaidi ya thelathini wenye silaha za kila aina, ashuke wamtie mbaroni.!





Ndege ilitua salama katika uwanja wa ndege wa Zanzibar. Askari wote walikuwa makini na watu wote waliokuwa wanashuka ndani ya ndege ile. Ilikuwa ni ndege ndogo ya watu 6 ya kampuni ya Auric.



Alishuka abiria wa kwanza alikuwa mama wa makamo akiwa kabeba mtoto mdogo mgongoni.

Alishuka abiria wa pili, alikuwa kijana wa makamo wa kizungu, aliyekuwa kabeba begi kubwa mgongoni.

Alishuka abiria watatu, alikuwa kijana wa miaka 18 wa kike, mwenye asili ya kiasia.

Abiria wa nne alikuwa ni mama wa makamo mjamzito.

Abiria watano nae alishuka, alikuwa ni mzee wa kiarabu mwenye ndevu nyingi. Abiria wa mwisho katika ndege ile ndogo alishuka, yeye alikuwa kijana wa kichina.



Kila abiria alipokuwa anashuka askari thelathini walikuwa makini kuangalia picha ya Salehe iliyokuwa mkononi kwa kila mmoja.

Lakini taswira ya mtu waliyekuwa na picha yake hakushuka ! Salehe alipotea mithili ya upepo !



Askari waliduwaa na picha zao mikononi. Askari watano waliingia ndani ya ndege kuona kama Salehe alijificha mle ndani. Walitafuta kila kona ndani ya ndege ile.

Salehe hawakumuona !



Wakati huo Salehe alikuwa mbali na uwanja wa ndege. Alikuwa ndani ya Noah nyeusi akikaribia nyumbani kwa baba yake, Mzee makame. Nani angejua kama yule mama mjamzito waliyemuona akishuka alikuwa Salehe ?

Alitumia dakika tatu kujibadiri pale pale kwenye siti kwa usiri mkubwa. Alivaa sura ya bandia, alivaa mwili wa bandia, begi lake liligeuka mimba ya bandia. Dar es salaam alipanda ndege Salehe, Zanzibar alishuka kwenye ndege mama mjamzito !



Ndani ya gari alijibadirisha. Sasa alikuwa na taswira halisi ya Salehe .

Walifika nyumbani kwa baba yake Salehe baada ya muda mfupi. Walishuka ndani ya gari na kutembea kwa mwendo wa tahadhari. Walijua chochote kinaweza kutokea ndani ya nyumba ile.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Walikuta nyumba tupu.Tupu kabisa. Hakuna mtu. Hakuna dalili ya uhai. Waliingia ndani. Salehe alipanda darini. Alichoka kabisa !

Hakukuwa na boksi za sumu Proxine hata moja. Ilikuwa hasara kubwa sana. Kulikuwa na boksi kumi za Proxine. Na kila boksi moja ilikuwa vinakaa vyupa elfu moja vya sumu ile hatari. Kuibiwa kwa boksi kumi, ilimaanisha vyupa elfu kumi vya sumu ya Proxine viliibiwa. Hasara ilioje ?



"Sumu zote zimechukuliwa. Sasa wametangaza vita. Hivi ni vita vikuu vya tatu vya Dunia. Nitauwa kila kiumbe anayepumua katika nchi hii. Nitaua nitaua nitaua ! Baada ya kufanya mauaji ya kutisha, na kutosheke, ndipo tutafanya Kitu kitakachowaacha watanzania watakaobaki midomo wazi. " Salehe alisema kwa jazba kule darini, machozi yalikuwa yanamtoka.



Salehe, Zwangendaba na Kerspersky walitoka ndani ya nyumba ile vichwa chini. Na kutokomea kusikojulikana. Sasa walidhamiria kuuwa, na walienda kuuwa !



Daniel alikuwa anashuka kutoka katika boti bandarini Zanzibar. Alishapewa taarifa za Polisi kuachwa kwenye mataa katika uwanja wa ndege wa Zanzibar. Hakuwalaumu Polisi, alizijua mbinu za watu wale.



Alipofika Zanzibar, moja kwa moja alielekea nyumbani kwa Mzee Makame. Kwa tahadhari kubwa sana aliingia ndani ya nyumba ya Mzee Makame. Alikuwa amechelewa, wakina Salehe walikuwa wameshaondoka.



Daniel alipanda darini na kutoa kidudu kidogo mfano wa kigoroli.

Kilikuwa kinasa sauti ! Alichokiweka kabla hajaondoka kwenda Dar es Salaam. Alikitega makusudi nia ni kusikia mstuko atakaoupata Salehe baada ya kugundua mabox ya Proxine yametoweka.

Alishuka chini na kuweka kile kigoroli kwenye simu yake. Hakusikia tu mshtuko. Alisikia pia maneno ya jazba na hasira kutoka kwa Salehe.



"Sumu zote zimechukuliwa. Sasa wametangaza vita. Hivi ni vita vikuu vya tatu vya Dunia. Nitauwa kila kiumbe anayepumua katika nchi hii. Nitaua nitaua nitaua ! Baada ya kufanya mauaji ya kutisha, na kutosheke, ndipo tutafanya Kitu kitakachowaacha watanzania watakaobaki midomo wazi. "

Daniel alitabasamu.



Daniel alitoka nyumbani kwa Mzee Makame akiwa hana uelekeo maalumu. Hakujua Salehe atakuwa ameelekea wapi ? Alikuwa anatembea tu mitaani. Labda atakutana na chochote kitakachomsaidia katika kutatua mkasa huu mzito !

Hakukutana na chochote.



Aliamua kutafuta hoteli iliyotulia na kupumzisha mwili na akili .



*************



Ndani ya hoteli ya Green view iliyopo mtaa wa Uzunguni jijini Mbeya, kulikuwa na kikao cha Siri. Kikao kilichokutanisha watu watano muhimu sana katika mpango huu.

Mpango Angamizo !



Walikuwa ni walewale wanajeshi wanne na Salehe Makame. Walikuwa wanajadiri maendeleo ya mpango wao kabla ya kuuhitimisha. Zilikuwa zimebaki siku mbili kuhitimisha mpango huo. Mpango wenye nia ya mbaya kwa Serikali ya Tanzania. Mpango wenye Kuleta hofu na kuteteresha hali ya usalama kwa wananchi na viongozi wa nchi ya Tanzania. Mpango uliopangwa kwa kuanza kufanya mauaji ya kikatili kwa watoto wa vigogo, ili kupunguza umakini kwa Polisi.Nia ya kuuwa watoto wa vigogo ni kuwapoteza lengo Polisi. Walitaka Polisi nchi nzima wawe bize kutafuta muuaji wa watoto wa vigogo vyuoni. Ili wao wautumie kwa urahisi mpaka wa Tunduma, kutoka Tanzania kwenda Zambia kutorosha.....!



Mpango wa Angamizo ulikuwa hivi. Mkoani Iringa, Katika kijiji cha Makete kulikuwa na ghala kubwa sana la silaha. Lilikuwa ni ghala la silaha kubwa kuliko yote katika nchi ya Tanzania.

Mpango wa watu hawa ulikuwa ni kuiba na kutorosha nje ya nchi silaha zote katika ghala lile. Walikuwa wameongea biashara na kikundi kimoja cha kigaidi cha huko Somalia. Walipanga kupita kwa siri katika mpaka wa Tunduma kwa kutumia rushwa Ili kupita Tunduma kuelekea Zambia. Halafu kutokea Zambia silaha hizo zisafirishwe tena kwa njia ya ndege kwenda Somalia. Hawakutaka kuzipandisha ndege silaha hizo kutokea Tanzania. Hali ya ulinzi Tanzania ilikuwa nzuri zaidi ya Zambia.



Ulikuwa ni mpango uliopangwa na vigogo watatu wakubwa wa Serikali. Huku ukiratibiwa na watendaji wakuu watano. Waliokutana leo ndani ya Green view hotel.



"Salehe tuna jumla ya kontena kumi na tano tupu. Lazima tuzijaze silaha na tuzipitishe mpakani leo usiku. Najua sahivi macho ya vyombo vya ulinzi vyote vipo Arusha, Mwanza na Zanzibar. Sisi usiku wa leo tutaenda kuiba silaha hizo katika ghala kuu la Serikali Makete, kesho usiku lazima tuzisafirishe. Lazima tuwe makini sana katika hatua hii.Tena ili kulichanganya zaidi jeshi la Polisi inabidi leo mtu auwawe Dar es salaam. Tena awe mtoto wa kigogo, maana akifa mtu wa kawaida Serikali inadharau." Meja Ndondi Ndanga aliyekuwa mwenyekiti wa kikao kile alitoa maelekezo.

"Sawa nimekuelewa.Naamini Mpango wetu utafanikiwa. Lakini wewe umeshauri tuuwe mtu mmoja Dar es salaam. Lakini ili tuwachanganye vizuri inabidi watu watatu wafe leo !. Dar es salaam, Mara na Kigoma. Hapo tutawaweza. Kwa kuwa ghala kuu lipo Iringa mauaji yakitokea Mara, Dar es salaam na Kigoma, askari wengi watapelekwa sehemu hizo. Kwa hiyo itatupa uraisi kuziiba silaha hizo ".

Salehe nae alitoa wazo lake.

"Sawa Salehe.Wazo zuri sana" Meja Ndondi Ndanga alikubaliana na mpango wa Salehe.

"Na mimi nitaanzisha vita vya tatu vya Dunia hapahapa Mbeya ! " Salehe alisema kwa ghadhabu

Kikao kilifungwa.



Salehe alienda uwanja wa ndege wa Songwe uliopo nje kidogo ya mji wa Mbeya, kutafuta tiketi tatu za kwenda mikoa tofauti. Alibahatika kupata tiketi mbili za kwenda Kigoma na Mara. Ndege ya kwenda Dar es salaam Ilikuwa imejaa.



Alifikiria yule mtu wa Dar es salaam. Aliongea na mtu wake wa Zanzibar. Ndege ilipatikana. Salehe akakata tiketi ya kutoka Mbeya hadi Zanzibar, ili atakayeenda Dar es salaam ataenda kwanza Zanzibar, halafu atatafuta ndege ya kwenda Dar es salaam .



Daniel alikuwa amelala vya kutosha pale hotelini. Aliamka, alioga na kuagiza chakula palepale hotelini. Baada ya kula alipiga simu kwa rafiki yake Mhudumu uwanja wa ndege wa Zanzibar, akajibiwa kuna ndege ya saa kumi inayoenda Dar es salaam. Akamuomba amkatie tiketi moja. Daniel aliamua kurejea Dar es salaam tena !http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Ndege ya saa kumi jioni kwenda Dar es salaam ilijikuta imepandwa na maadui wawili. Daniel Mwaseba na Kerspersky . Hakuna aliyekuwa kamuona mwenzie.



Daniel ndiye alikuwa wa kwanza kuingia kwenye ndege. Alikwenda uwanja wa ndege mapema zaidi. Alikosa cha kufanya kule hotelini. Aliona bora awahi kwenda uwanjani. Saa nane kamili ilimkuta ndani ya uwanja wa ndege wa Zanzibar. Akisubiri muda wa kuondoka ndege ufike.

Arudi Dar es salaam.



Kerspersky yeye alifika baadae pale uwanjani. Alifika Zanzibar saa tisa na nusu akitokea Mbeya. Baada ya kumaliza utaratibu wa pale uwanjani, Kerspersky aliingia ndani ya ndege.



Daniel alikuwa amekaa katika siti ya nyuma kabisa ya ndege ile. Akiwa amezongwa na mawazo tele. Hakutegemea kama kazi ya kuwafichua wauaji wale ingekuwa ngumu kiasi kile. Sasa aliona siku tatu ni chache sana. Kutokana na kuelemewa na mawazo mengi aliamua kuyapunguza kwa kusoma riwaya. Alifungua kibegi chake kidogo na kutoa kitabu cha kipelelezi, Hila , riwaya iliyotungwa na Gwiji wa riwaya Tanzania, George Iron Mosenya. Alikifunua taratibu na kuanza kukisoma. Mambo ya Mama Lao katika riwaya ile yalimsahaulisha kidogo Daniel adha za Dunia. Alielea katika dunia nyingine kabisa.



Wakati Daniel anasoma kitabu ndipo Kerspersky aliingia ndani ya ndege ile. Alikaa siti za mbele kabisa. Kerspersky hakuwa makini kuwachunguza watu waliokuwepo katika ndege ile. Alitulia shwari katika siti yake. Akiiwazia kwa kina kazi iliyopo mbele yake.



Kerspersky alipanga kwenda katika chuo cha usimamizi wa fedha IFM kutekeleza adhma yake. Chuo alichokuwa anasoma mtoto wa waziri wa kilimo na chakula, Mheshimiwa Nyongo Daudi. Alidhamiria kwenda kumuua Janeth Nyongo. Mtoto wa waziri wa kilimo na chakula.



Saa kumi kamili ndege ile iliiacha ardhi ya kisiwa cha Zanzibar, kuelekea Dar es salaam.



Baada ya muda mchache ndege iliwasiri katika uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere, Jijini la Dar es salaam. Abiria mmojammoja walianza kushuka kwenye ndege ile. Daniel alikuwa abiria wa mwisho kushuka katika ndege ile. Akitanguliwa Kerspersky na abiria wengine.



Daniel alikuwa makini sana. Alikuwa anaifata kila hatua akiyopiga Kerspersky . Jamaa hakujua kabisa kama anafuatwa.



Alichukua teksi pale nje ya uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, na kuelekea Posta, maeneo kilipo chuo cha IFM. Daniel nae alifata kwa kutumia teksi. Ulikuwa mfuatano wa kimya kimya.

Kerspersky hakuwa makini kabisa. Hakuwa ana wasiwasi kabisa. Alifika posta, akashuka. Akawa anaelekea IFM kwa miguu, Daniel akiwa nyuma yake !





Kerspersky alifika chuoni IFM. Kerspersky akapita katika geti la chuo bila wasiwasi wowote. Hakuwa na hofu yoyote, na wala hakuna aliyemtilia shaka.



Alianza kuwauliza wanafunzi. Mwanafunzi wa kwanza hakuwa anajua Janeth anakaa chumba gani, mwanafunzi wa pili bila kujua dhamira ya jamaa yule alimuelekeza Kerspersky hosteli aliyekuwa anakaa mtoto wa waziri wa kilimo na chakula, Janeth. Taratibu Kerspersky akawa anaelekea huko alikoelekezwa.



Kerspesky alikuwa anaelekea hosteli huku akigeuka nyuma mara kwa mara. Lakini hakumwona mtu wa kumtilia shaka.

Alipanda ngazi za kuelekea hosteli kwa mwendo wa haraka sana.

Sasa damu ilikuwa inamchemka mwilini mwake, alikuwa amedhamiria kuuwa !



Akafika chumba namba 33. Chumba alichoelekezwa kuwa ndicho anachokaa Janeth. Aligonga hodi kwa kutumia mpini wa kisu chake kirefu, lakini mlango haukufunguliwa.

Akarudia kugonga tena. Sasa taratibu mlango ulikuwa unafunguliwa .

Alikutana na bastola !

Alikuwa Daniel Mwaseba!



Kumbe Kerspersky alivyokuwa anamuuliza mwanafunzi wa kwanza na kumfata wa pili. Daniel alimfata yule wa mwanafunzi wa kwanza. Baada ya kumuuliza alimwambia yule jamaa alikuwa anamuulizia Janeth, Daniel alipiga hatua moja mbele. Kwa haraka akaenda kumuuliza mwanafunzi mwengine. Alielekezwa chumba cha alichokuwa anakaa Janeth. Alitangulia yeye chumba namba 33. Kwa bahati nzuri kilikuwa kimefungwa. Alifungua kwa kutumia funguo wake malaya. Alitulia kitandani akimsubiri mgeni wake.



Kerspersky alipigwa na butwaa. Hakutegemea kumkuta Daniel pale. Pia hakutegemea kukaribishwa kwa mtindo ule.



"Karibu sana"

Kerspersky hakujibu.

Daniel alitabasamu.

"Najua hukutegemea kukaribishwa na mimi.Ila imekukuta bahati mbaya "

Jamaa kimya.

"Natakaa uongee ukimya haukusaidii ! " Daniel alisema kwa ukali.

Hakujibu.



Daniel alikasirika. Alimpiga kwa kutumia kiwiko cha mkono kwenye mdomo. Kerspersky alianza kutokwa na damu.



"Utaongea huongei?"

Jamaa aligeuka bubu.

Alimchukua na kwenda

kumhifadhi kituo cha Polisi pale Posta.



Daniel alitoka nje ya kituo kile akiwa hajui anaelekea wapi ? Alikuwa na mawazo mengi sana. Hajui aelekee wapi ? Hajui afanye nini? Baada ya masaa mawili kuzunguka mtaani alirudi tena kituo cha Polisi Posta.



"Naomba unitolee yule Mhalifu"

Kerspersky akaitwa.

Akakaa mbele ya Daniel.

"Utaongea sasa hivi" Daniel akasema kwa upole.

Kerspersky akawa anamwangalia tu.

"Usinilazimishe kufanya ninachotaka kukufanya"

"Nifanye chochote sikwambii chochote "

Daniel akaisikia sauti ya Kerspersky kwa mara ya kwanza.



Daniel alinyanyuka. Akaenda pale kwenye kabati la pale kaunta . Akafungua droo moja ya kabati. Akachukua mkanda mdogo, ulikuwa kama saa ya mkononi ndogo.

Akamvesha ule mkanda mkononi kwa Kerspersky.

Ulimkaa vizuri sana.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Akamfunga mkono mwengine kwa pingu akiunganisha na kile kiti cha chuma alichokalia Kerspersky .

Baada ya muda mfupi ule mkanda ukaanza kumbana Kerspersky. Ulianza kumbana taratibu, baadae kasi ya kubana ule mkono iliongezeka. Ukazidi kubana ule mkanda !

Kerspersky alianza kusikia maumivu yakizidi. Maumivu yakazidi sasa. Ule mkanda ukaanza kupita kwenye nyama za mkono wa Kerspersky.

Machozi yalianza kumdondoka







ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog