Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

MACHUNGU YA USALITI - 4

 






Simulizi : Machungu Ya Usaliti

Sehemu Ya Nne (4)





Alimpenda sana Evelyne na aliamini hakukuwa na msichana mwingine ambaye angeweza kuiziba nafasi hiyo katika moyo wake, wakati ambao alikuwa akiendelea kuyawaza hayo nyuma ya pazia hakujua kuwa kumbe alikuwa amepigwa picha za utupu na Monalisa ambazo zilitumwa kwa Evelyne na picha hizo ndizo ambazo zilimfanya abadilike kiasi cha kuondoka kabisa eneo la chuo.

Walipokuwa wamepanda kwenye panton Richard alitamani liongeze mwendo ili aweze kufika haraka nyumbani alipokuwa akiishi Evelyne, alitamani kumuona mpenzi wake na kuzungumza naye kwa wakati huo. Alipokuwa ameketi alipaona kuwa kama kuna misumari iliyomchoma hivyo hakutaka kuendelea kuketi sehemu hiyo, alisimama na kuanza kuzunguka huku na kule kama mtu aliyeanza kuchanganyikiwa, kitendo hicho kiliwafanya baadhi ya watu waliyokuwemo kwenye panton hiyo waanze kumshangaa Richard.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kichwani alikuwa akimuwaza Evelyne tu, hakutaka kuzungumza lolote na Happy, kimoyomoyo alikuwa akiomba wawahi kufika haraka ili aweze kuzungumza na mpenzi wake huyo.

Baada ya kupita dakika kadhaa waliweza kuvuka salama kisha wakaianza safari ya kuelekea nyumbani alipokuwa akiishi Evelyne pamoja na Happy, palikuwa na umbali kidogo hivyo waliamua kutumia usafiri wa bajaji ambao uliweza kuwafikisha kwa haraka sana.

Baada ya bajaji hiyo kuwafikisha walishuka kisha Richard akamlipa dereva wa bajaji kiasi cha pesa alichokuwa anawadai, alipomalizana na dereva huyo walitembea kidogo mpaka kufika katika chumba ambacho alikuwa anaishi Evelyne pamoja na Happy.

Walipoingia ndani ya chumba hicho walimkuta Evelyne akiwa amejilaza kitandani huku akiwa analia, alionekana kutochukua muda mrefu tangu alipoweza kuingia katika chumba hicho. Alipohisi kuna watu wameingia ndani aliamka na kuwatazama.

Hakutaka kuamini macho yake baada ya kumuona Richard akiwa ndani ya chumba hicho, hasira zilizidi kumpanda, alihisi kumuona adui mkubwa wa maisha yake ambaye alimchukia sana.

Alichokuwa anakihitaji Richard kwa wakati huo ni kupewa nafasi ya kuzungumza na Evelyne ili aweze kujua ni nini kilichokuwa kimetokea mpaka akaamua kuondoka chuoni lakini nafasi hiyo ilikuwa ngumu mno kupatikana. Evelyne hakuwa tayari kuzungumza naye lolote.

“Happy naomba umtoe huyu ibilisi nje, sitaki kumuona katika macho yangu,” alisema Evelyne huku akiendelea kulia.

“Kuna nini kimetokea Eve mbona sikuelewi?” aliuliza Happy huku akizidi kuchanganywa na maneno ya rafiki yake, hakuelewa ni nini kilichokuwa kimetokea mpaka kikamfanya Evelyne abadilike kiasi kile.

“Nimesema sitaki kumuona Richard katika macho yangu, naomba utoke Richard, sikutaki kukuona,” alisema Evelyne kisha akaanza kumfukuza Richard.

“Lakini Richard si mpenzi wako?” aliuliza Happy.

“Alikuwa mpenzi wangu lakini sio sasa naomba umtoe,” alijibu Evelyne kwa sauti ya kilio iliyo sanjari na maumivu pamoja na hasira.

Richard hakutaka kuamini kile alichokuwa akikisikia kutoka kwa mpenzi wake huyo, aliamini hakukuwa na tatizo lolote lile hivyo bado alizidi kuomba kupewa nafasi ya kuzungumza naye.

“Mpenzi wangu naomba unipe nafasi ya kuzungumza na wewe, niambie nini kimetokea mbona unanichukia bila sababu?” aliuliza Richard huku akimtazama Evelyne ambaye alikuwa akilia kwa wakati huo, hakutaka kuendelea kuyashuhudia machozi ya mpenzi wake yakiendelea kumbubujika mfululizo, alichoamua kukifanya akakitoa kitambaa mfukoni mwake kisha akahitaji kumfuta machozi lakini kabla hajamsogelea kwa lengo la kumfuta machozi alishtukia akipigwa kofi zito na Evelyne.

“Naomba utoke Richard sitaki kuzungumza lolote na wewe,” alisema Evelyne kisha akamfukuza Richard, wakati huo alikuwa akilia.

Richard alishindwa kabisa kuamua nini la kufanya kwa sababu kila alilokuwa anahitaji litokee kwa muda huo lilishindikana, alimbembeleza sana mpenzi wake huyo ili aweze kumuambia ni nini ambacho kilikuwa kimetokea lakini hakuwa tayari kuzungumza lolote.

Hakutaka kuondoka kirahisi wakati alipokuwa akifukuzwa lakini mwisho ilibidi Happy amuombe aondoke eneo hilo kwani ilikuwa ni kawaida ya Evelyne kutozungumza lolote kipindi ambapo alikuwa katika hasira. Alimuahidi kipindi ambapo hasira za Evelyne zitakapokuwa zimeisha ndipo angeweza kupata muda wa kuzungumza naye.

***

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

SURA YA TANO



Tukio zima la kuondoka Evelyne darasani pamoja na Happy akifuatiwa na Richard kila mtu aliliona, siku hiyo wanachuo hawakuwa na stori nyingine zaidi ya kuwajadili wawili hao. Kila mtu alizungumza lake huku wale marafiki wa wakaribu wa wahusika hao wakijaribu kuwatetea.

“Yule jamaa anafeli asipoangalia yani demu anamchanganya kiasi kile,” alisema mwanachuo mmoja mvulana alipokuwa kwenye kundi la wavulana wenzake.

“Unajua hata Lecture hajapenda kabisa walivyoondoka ameona kama wamemdharau,” alisema mwanachuo mwingine ambaye alionekana kumuunga mkono mwenzake.

Kila mtu alisikika akisema lake lakini kwa upande ambao alikuwa amekaa Monalisa, Penina, Mary pamoja na Adela mazungumzo yao yalikuwa tofauti kidogo.

“Na bado huu ndiyo mwanzo tu,” alisema Monalisa.

“Yani mpaka nakuonea wivu?” alisema Mary.

“Richard lazima atabaki mikononi mwangu, mimi ndiyo Mona mwingine fotokopi,’ alisema Monalisa huku akijishebedua.

“Nakuaminia shosti huwezi kuniangusha,” alisema Penina kisha wakagongeana huku wakicheka kwa sauti kubwa.

Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kati ya Evelyne na Richard, Monalisa alifahamu yeye kuwa ndiye chanzo hivyo hakuonekana kujali lolote. Muda wa furaha ndiyo ulikuwa umetawala katika maisha yake, aliamini kwa asilimia zote kuwa ule ndiyo ulikuwa mwanzo wa kushiriki mapenzi na Richard tena kwa uhuru baada ya kufanikiwa kumpa maumivu Evelyne.

Kwa upande wa Adela hakuonekana kupendezewa na kitendo kile alichokuwa amekifanya Monalisa japo alikuwa ni rafiki yake waliyeshibana chuoni pale lakini alimuona kuwa kama binadamu katili, mwenye roho mbaya mithili ya mnyama.

Kila alipokuwa akimtazama alishindwa kummaliza, wakati ambao Monalisa, Penina na Mary walipokuwa wakifurahia tukio hilo yeye alibaki akimuhurumia Evelyne.

Licha ya kuwa kipindi cha nyuma aliwahi kumpenda Richard na kuhitaji kuwa naye kimapenzi lakini baada ya kugundua kuwa Evelyne ndiye msichana pekee ambaye alikuwa akijihusisha kimapenzi na Richard aliamua kubadili mawazo yake, hakutaka kuliingilia penzi hilo ambalo wasichana wengi chuoni pale walitamani kuliingilia.

Aliamini kwa vyovyote ni lazima Evelyne alikuwa katika maumivu makali sana baada ya kutumiwa picha za utupu zilizokuwa zikimuonyesha mpenzi wake akiwa pamoja na Monalisa kitandani.

Hakutaka kuendelea kuushuhudia ukatili huo wa kimapenzi aliyokuwa akiufanya Monalisa, alipanga kufanya lolote lile ilimradi aweze kulirudisha penzi la wawili hao ambalo tayari lilikuwa limeshapotea.

****

Richard alirudi chuoni na aliamua kumtafuta Monalisa, alihitaji kuzungumza naye, alihisi alifahamu kila kitu kilichokuwa kikiendelea lakini kabla ya mazungumzo yao kuanza Monalisa alimrudishia simu yake.

“Nini umefanya Monalisa?” aliuliza Richard kwa sauti ya ukali baada ya kuipokea simu yake ambayo ilikuwa imezimwa, aliiwasha.

“Nimefanya nini kuhusu nini?” aliuliza Monalisa kisha akaanza kucheka kwa sauti ya kinafki.

“Umemuambia nini Evelyne mbona amenichukia ghafla?” aliuliza Richard.

“Kuna kitu gani ambacho hukifahamu kinachoendelea kati yetu.”

“Mona kama kuwa katika mahusiano mimi na wewe tulizungumza na siku ile ndiyo ilikuwa mwisho kwa nini lakini unataka kuniharibia mapenzi yangu, kwa nini unataka kunigombanisha na mpenzi wangu.”

“Nikugombanishe mara ngapi?”

“Unasemaje?”

“Richard nimeamua kuuweka ukweli wazi kuwa mimi na wewe ni wapenzi na tena kama ulikuwa hujui nilikupiga picha za utupu wakati ulipokuwa umelala na nimemtumia,” alijibu Monalisa huku akionekana kujiamini, hakuishia kuzungumza kwa maneno bali alichoamua kukifanya ni kuiwasha simu yake na kuanza kumuonyesha picha hizo.

Richard hakutaka kuamini kile alichokuwa akikiona kwa wakati huo, alihisi kuchanganyikiwa.

“Richard wewe ni mwanaume gani usiyeelewa kuwa nakupenda, kila siku nateseka kwa ajili yako, naishi kwa wasiwasi kwa sababu yako na nimeamua kufanya yote haya kwa sababu yako nakupenda mno na kama tatizo ni huyo kinyago wako Evelyne nimeshamkomesha,” alijibu Monalisa maneno ambayo aliyatamka kwa hisia, muda huo machozi yalikuwa yakimdondoka.

Richard alizidi kuchanganyikiwa baada ya kusikia kuwa picha hizo ziliweza kutumwa kwa mpenzi wake. Hilo lilizidi kumuweka katika wakati wa mawazo sana, kama kumsaliti ni kweli alikuwa tayari ameshamsaliti mpenzi wake japo hakupenda lakini kibaya kilichozidi kumuumiza ni kitendo cha kupigwa picha za utupu bila kujijua, hilo lilizidi kumuumiza mno moyo wake.

“Lakini kwa nini umefanya haya Mona?”

”Kwa sababu nakupenda Richard hivi ulitaka nifanye nini ili ujue kuwa nakupenda, nakupenda nakupenda Richard mno,”alijibu Monalisa huku akijaribu kumkumbatia Richard lakini hakuweza kufanikiwa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Richard hakutaka kuendelea kubaki eneo hilo, aliamua kupanda kwenye gari lake kisha akaondoka zake. Alipokuwa barabarani kichwa chake kilitawaliwa na mawazo sana, alikuwa akimfikiria mpenzi wake lakini kikubwa zaidi alichokuwa akikiwaza ni juu ya picha za utupu ambazo alipigwa bila kujijua na kibaya zaidi aliweza kutumiwa mpenzi wake.

Moyo wa Richard bado uliendelea kumuuma, alijilaumu sana kwa kitendo alichokuwa amekifanya cha kumsaliti mpenzi wake ambaye kwa wakati huo alikuwa akifahamu kila kitu kilichokuwa kimetokea. Hakutaka kuamini hata mara moja kila alipokuwa akiyakumbuka maneno ya Monalisa na jinsi ambavyo alikuwa akijitamba, kuna muda alianza kumchukia lakini huo haukuwa ndiyo mwisho wa suluhisho wa kile kilichokuwa kimetokea.







Alipokuwa barabarani simu yake ilianza kuingia jumbe nyingi sana, alipozifungua na kuzisoma zilikuwa ni za mpenzi wake Evelyne ambazo zilimtaarifu kuwa alikuwa akimpigia simu kipindi ambapo alikuwa hapatikani. Hilo lilizidi kumuumiza mno.

Alipofika nyumbani siku hiyo hakuonekana kuwa sawa kama ilivyokuwa siku nyingine, ilibidi wazazi wake wamuulize baada ya kumuona mtoto wao akiwa katika hali hiyo, wakati huo walikuwa mezani wakila chakula cha usiku.

“Nini kinachokusumbua mwanangu?” aliuliza Mama yake aliyekuwa akijulikana kwa jina la bibi Magreth.

“Hakuna kitu Mama nipo sawa,” alijibu Richard.

“Sema kinachokusumbua sisi wazazi wako bado tupo hai usitufiche, kama tatizo ni pesa sema tunauwezo wa kukusaidia,” alisema Baba yake aliyekuwa akijulikana kwa jina la Mzee Gombanila.

“Baba na Mama sina tatizo lolote linalonisumbua,” alisema Richard.

Richard hakutaka kuwaeleza ukweli wazazi wake wa kile kilichokuwa kimetokea kati yake na mpenzi wake ambaye tayari walikuwa wakimfahamu.

“Umegombana na Evelyne?” aliuliza Mama yake.

“Hapana,” alijibu Richard.

“Sasa nini tatizo?” aliuliza tena Mama yake.

“Hakuna kitu Mama,” alijibu Richard.

“Unaonekana kuna kitu unajaribu kukificha lakini moyo wako unakataa, tuambie sisi wazazi wako tunaweza tukakusaidia,”alisema Baba yake.

“Hapana Baba sidhani kama kuna msaada ninauhitaji kutoka kwenu kwa sasa ila kama ikitokea nitakuwa nikiuhitaji nitafanya hivyo,” alisema Richard.

Baada ya kuona maswali ya wazazi wake yamezidi kuwa mengi pale mezani aliamua kuacha kuendelea kula kisha akaenda chumbani kwake, alipofika humo alijifungia. Moyo wake bado uliendelea kumuuma mno, hakutaka kuamini kama ule ndiyo ulikuwa mwisho wa mapenzi yake na Evelyne.

“Evelyne siamini kama huu ndiyo mwisho wa mapenzi yetu sitaki kuamini hata mara moja kama naenda kukupoteza katika maisha yangu, sitakubali tukio kama hili linitokee, nitahakikisha unabaki kuwa wangu peke yangu,” alijisemea Richard, wakati huo alikuwa akiitazama picha ya Evelyne.

****

Evelyne alikuwa ni mtu wa kulia muda wote, Happy alipata kazi ya kumbembeleza rafiki yake bila mafanikio. Mpaka kufikia muda huo hakufahamu ni nini kilichokuwa kimetokea. Baada ya kuona Evelyne anazidi kulia bila kuwepo mafanikio yoyote ya kunyamaza aliamua kuichukua simu yake na ndipo hapo alipoweza kuziona picha za utupu za Monalisa pamoja na Richard.

Picha hizo zilimshtua sana, hakutaka kuamini kile alichokuwa akikiona katika picha hizo, kuna muda alianza kuhisi labda pengine alimfananisha mwanaume aliyekuwa akimuona katika picha hiyo na Richard lakini ukweli ulibaki kuwa mwanaume huyo hakuwa mwingine isipokuwa ni Richard.

“Mungu wangu ni nini hiki?” alijikuta akiuliza swali ambalo hakutegemea kama angeliuliza, hakukuwa na mtu wa kumjibu zaidi ya sauti ya kilio cha kwikwi kutoka kwa Evelyne ndiyo ilikuwa imetawala ndani ya chumba hicho.

Mapenzi yaligeuka kuwa maumivu makali mno katika moyo wa Evelyne, alijutia mambo mengi sana ambayo aliwahi kuyafanya na Richard, licha ya kuwa alitokea katika maisha ya kimasikini lakini shina la mapenzi halikuacha kuchipua kati yake na Richard mwanaume aliyeanzisha mahusiano naye tangu mwaka wa kwanza wa degree yake chuoni.

Katika mapenzi yao walifanya starehe nyingi sana, walienda sehemu mbalimbali lakini kubwa ni kiapo ambacho waliwahi kuwekeana katika mapenzi yao kuwa hawatoweza kusalitiana wala kupeana maumivu ya aina yoyote ile ya kimapenzi.

Muda ambao Evelyne alikuwa akilia ulikuwa ndiyo muda ambao moyo wake tayari umeshapokea maumivu ya kimapenzi, hakutaka kuamini kama Richard yule ambaye aliwahi kula kiapo mbele yake kuwa hatoweza kumsaliti wala kumpa maumivu yoyote ya kimapenzi ndiye ambaye alikuwa amemsababishia maumivu katika moyo wake, hilo lilizidi kumuumiza.

“Siamini kama kweli Richard ameweza kunifanyia hivi, yani mapenzi yangu yote niliyompa bado amenisaliti ama kweli wanaume wabaya sana,” alisema Evelyne kwa sauti iliyoandamana na kilio.

“Kumbe kweli anatembea na Monalisa?” aliuliza Happy.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Mwanzoni sikutaka kuamini niliposikia kuwa wanamahusiano, nilimuamini sana lakini katika hili siwezi tena kumuamini, ameuvunja uaminifu wangu kwake, namchukia sana,” alisema Evelyne.

Huo ulikuwa ni ukweli wenye kuuma mno tena mara zote alipomkumbuka mpenzi wake hakutaka kuamini, machozi yalikuwa yakimtoka.

****

Richard alizidi kuchanganyikiwa, kila alilokuwa akiliwaza kulifanya kama ishara ya kumuomba mpenzi wake msamaha aliona kama anakosea. Alizidi kuwa katika wakati mgumu sana kipindi ambacho alikuwa akimuona Evelyne darasani, kuna muda alitamani kuzungumza naye kisha amuombe msamaha lakini Evelyne hakuwa tayari, alimchukia mno Richard tena chuki za waziwazi.

Hakuwa na njia nyingine ya kufanya zaidi ya kumfuata Happy na kuamua kuzungumza naye, alihitaji kumuomba msamaha Evelyne lakini aliamini ilikuwa ni vigumu sana kwa yeye kuweza kueleweka, alijua kuwa alifanya makosa sana kwa kumsaliti mpenzi wake lakini bado hakutaka kuamini kuwa huo ndiyo mwisho wa mapenzi yake kwa Evelyne.

“Najua nimemkosea sana Evelyne lakini tafadhali mwambie asinichukie moyo wangu bado unampenda,” alisema Richard huku akimtazama Happy kwa macho ya huruma.

“Richard hivi kwa nini umeamua kumsaliti Evelyne?” aliuliza Happy.

“Sijui ata niseme nini? Nashindwa kujielezea Happy, nashindwa nimejikuta tu namsaliti,” alijibu Richard.

“Richard embu acha kunifanya mimi mtoto mdogo wakati picha zako za uchafu na huyo mchepuko wako nimeziona yani sikutegemea kama ungeweza kumfanyia ukatili huu rafiki yangu, Richard wewe ni mbaya sana unatembea na Monalisa?” aliuliza Happy.

“Hapana usiseme hivyo narudia tena moyo wangu bado unampenda Evelyne na ninahitaji anisamehe, najua ananichukia sana lakini tafadhali jaribu kuzungumza naye pengine anaweza akabadili mawazo yake,” alisema Richard.

“Unadhani ni kazi rahisi kama unavyodhani?” aliuliza Happy.

“Najua ni ngumu lakini naomba unisaidie,” alijibu Richard kisha akampatia Happy kiasi cha shilingi laki mbili za kitanzania.

Baada ya mazungumzo hayo kumalizika Happy alimuahidi Richard kumsaidia katika hilo japo ilikuwa ni kazi ngumu ya kuzungumza na Evelyne lakini alijipa imani kufanikiwa kumshawishi mpaka akubali kumsamehe.

Aliporudi nyumbani siku hiyo Happy aliamua kuzungumza na Evelyne juu ya Richard. Evelyne baada ya kulisikia jina la Richard likitajwa mbele yake alibadilika, alimchukia sana mwanaume huyo.

“Rafiki yangu najua ni jinsi gani unavyomchukia Richard lakini kuna muda inabidi ukumbuke ni wapi mlipotoka, rudisha moyo wako nyuma,” alisema Happy.

“Unamaanisha nini?”aliuliza Evelyne.

“Richard bado anakupenda sana na anaomba umsamehe sana, anajutia kosa alilolifanya.”

“Kwa hiyo?”

“Kwa nini usimsamehe halafu maisha yakaendelea?”

“Siwezi kufanya hivyo hata mara moja halafu kuanzia leo naomba iwe ndiyo mwanzo na mwisho kusikia ukitamka jina la Richrd mbele yangu.”

“Msamehe tu.”

“Siwezi Happy, mwambie siwezi kumsamehe,” alisema Evelyne.

Alichokuwa akihitaji kukiona Happy ni Evelyne kukubali kumsamehe Richard lakini kila alipokuwa akijaribu kuzungumza naye ilishindikana, hakuwa tayari kumsamehe mpenzi wake.





Richard alikosa raha kabisa, alishindwa kula vizuri, alishindwa kulala pia muda wote aliutumia katika kumfikiria mpenzi wake. Licha ya utajiri wa familia yao, muonekano wake, urijali pamoja na wingi wa wasichana waliyokuwa wakimsumbua lakini alihisi kupoteza kitu cha thamani katika maisha yake.

Kitendo cha kumkosea Evelyne kiasi cha kushindwa kabisa kumsamehe alihisi kuipoteza nuru katika maisha yake. Alimjua vizuri Evelyne, alikuwa ni msichana wake ambaye aliyemuonyesha uvumilivu sana, alimuonyesha mapenzi ya dhati na mapenzi hayo ndiyo alikuwa ameyakumbuka.

***

Baada ya Monalisa kufanikiwa kulisambaratisha penzi kati ya Richard na Evelyne, hakutaka kuona wawili hao wakirudiana tena, alipanga kumdhibiti Richard, alihitaji kuona anakuwa mali yake hata hivyo hakukuwa na ugumu katika hilo, alipokumbuka kuwa bado zile picha pamoja na video alizozirekodi za utupu alikuwa nazo aliamua kuzitumia kama udhaifu wa kumnyanyasa kimapenzi Richard.

Licha ya kuwa kila siku Richard alijitahidi kumbembeleza Evelyne amsamehe kwa kosa alilokuwa amelifanya la usaliti lakini bado aliendelea kuwa na mahusiano ya kimapenzi na Monalisa, aliamua kufanya hivyo hii ni kutokana na vitisho alivyokuwa akivipata kutoka kwa msichana huyo ambaye alimwambia kuwa kama wasingeweza kuendelea kuwa na mahusiano ya kimapenzi basi picha hizo angekuzisambaza katika mitandao ya kijamii.

Richard alihofia utajiri wa baba yake pamoja na heshima aliyokuwa nayo, Baba yake Mzee Gombanila alifahamika kama mfanyabiashara mwenye utajiri mkubwa sana hapa Tanzania hivyo hakuwa tayari kuona picha hizo zinamchafua yeye pamoja na Baba yake.

***

Happy alijitahidi kadri ya uwezo wake katika kumshawishi rafiki yake akubali kumsamehe Richard lakini jambo hilo lilikuwa ni gumu mno kutokea, kila mbinu aliyokuwa akiitumia iligonga mwamba.

Ilibidi afanye mawasiliano na Richard kisha wakapanga sehemu ya kukutana kwa ajili ya mazungumzo yao, walipanga kukutana Mlimani City, Samaki Samaki na sehemu hiyo ndipo walipopanga kufanya mazungumzo yao.

“Rich, Evelyne anakuchukia sana hataki kulisikia jina lako hata mara moja,” alisema Happy.

“Nalijua hilo lakini amesemaje?”

“Amekataa kabisa kukusamehe.”

“Umekumbuka kumueleza kuwa ninampenda?”

“Ndiyo ila kwa kifupi hataki kusikia habari zako,” alisema Happy kisha Richard akaonekana kuwa mwenye mawazo.

“Rich naweza kukuuliza kitu?”

“Ndiyo niulize.”

“Kwani bado unaendelea kuwa na mahusiano na Monalisa?” aliuliza Happy swali ambalo lilimchukua muda Richard kuweza kulijibu.

“Hapana sipo naye,” alijibu Richard baada ya kumaliza kutafakari.

Richard hakuona sababu ya kumueleza ukweli Happy, aliamua kumficha lakini moyo wake bado ulizidi kuumia, alimpenda sana Evelyne, hakuwa tayari kumpoteza katika maisha yake.

***

Wakati wa mawazo bado uliendelea kumtawala, alipokuwa nyumbani kwao usiku aliuona kuwa mrefu, kichwa chake kiliendelea kimfikiria mpenzi wake ambaye mpaka kufikia muda huo alikataa kumsamehe.

Aliwaza kumnunulia zawadi kama gari, kumpangishia nyumba kama ishara ya kumuomba msamaha lakini alipokumbuka uzito wa kosa alilokuwa amelifanya aliona zawadi hizo zisingeweza kufidia maumivu ambayo alikuwa amempa mpenzi wake.

Wakati akiendelea kuwaza hayo aliamua kuichukua simu yake kisha akaamua kumtumia ujumbe Evelyne, ujumbe huo uliweza kujibiwa kwa haraka sana.

“Mambo mpenzi.”

“Sorry nachat na nani?”

“Ina maana namba yangu umeifuta?”

“Hujajibu swali, nimekuuliza nachat na nani?”

“Mimi Richard.”

“Nikusaidie nini?”

“Evelyne mpenzi wangu mbona hivyo?”

“Umesahau nini tena kwangu.”

“Sijasahau kitu ila naomba unisamehe mpenzi.”

“Nimeshakusamehe tangu siku ya kwanza uliyonipa maumivu ila kurudiana na wewe siwezi.”

“Kwa nini?”

“Endelea na Monalisa nadhani yeye ndiye anayeweza kuliziba pengo langu kwako.”

Kila ujumbe aliyokuwa akitumiwa na Evelyne alipousoma ulizidi kumuumiza sana, alitamani mpenzi wake asahau mambo yote yaliyotokea kisha amsamehe lakini tukio hilo lilikuwa gumu mno kutokea.

Siku zilizidi kukatika huku moyo wa Evelyne ukiendelea kuhifadhi chuki kwa Richard, hakutaka kumsamehe kirahisi kama Richard alivyokuwa akihitaji.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Maisha ya chuo yaliendelea huku maelewano kati yake na Richard yakiwa bado sio mazuri, wafikia kipindi wakawa hawazungumzi lolote zaidi ya salamu ambayo muda mwingine haikuweza kujibiwa. Hilo lilizidi kumuumiza sana Richard, kila siku alikuwa ni mtu wa kulilia penzi la Evelyne bila mafanikio yoyote.

Moyo wake uliendelea kumpenda Evelyne lakini kwa upande mwingine penzi la Monalisa lilizidi kuwa kikwazo, alitamani kuwa mbali na msichana huyo lakini alionekana kuwa na nguvu kubwa ya kuendelea kuwa naye.

Kichwa chake kilizidi kutafakari mambo mengi sana juu ya msichana huyo ambaye alikuwa ndiye sumu ya penzi lake, alizikumbuka picha ambazo alikuwazo na ndizo zilizokuwa zikimfanya akose maamuzi ya kumpenda msichana mmoja.

Alichowaza kukifanya ni kumpigia simu Monalisa kisha akamwambia kuwa siku hiyo alihitaji kuonana naye kwani alikuwa ana mazungumzo naye ya umuhimu sana, alimwambia muda ambao alihitaji kuonana naye kisha wakapanga kukutana katika hoteli ya kifahari ya Golden Tulip.

muda wa kukutana ulipofika waliweza kukutana na kuyaanza mazungumzo yao.

“Sitaki niendelee kukudanganya.”

“Kwa nini?”

“Umeulazimisha moyo wangu ukupende lakini hisia zangu hazipo kwako.”

“Una maanisha nini Richard?”

“Hisia zangu zipo kwa msichana mwingine, moyo wangu unampenda msichana mmoja tu na si mwingine bali ni Evelyne.”

“Richard umeshachelewa.”

“Kivipi?”

“Nina ujauzito wako Richard hivyo usijidanganye kuwa unaweza ukaniacha kirahisi.”

“Unasemaje?”

“Nina ujauzito wako.”

Yalikuwa ni mazungumzo mafupi yaliyofanyika ndani ya chumba cha kifahari cha hoteli hiyo, Richard hakutaka kuamini aliposikia kuwa Monalisa alikuwa amebeba ujauzito wake, ilikuwa ni taarifa ya ghafla! ambayo ilimshtua sana, moyo wake haukumpenda hata kidogo msichana huyo na kwa wakati huo alikuwa tayari ameshaubeba ujauzito wake, hilo lilizidi kumchanganya.

“Umebebaje ujauzito lakini?” aliuliza Richard kwa ghadhabu.

“Kwani ukiingia unaingiaje inamaana umesahau jinsi ulivyokuwa umelala na mimi?” alijibu Monalisa.

Richard alishikwa na kigugumizi mara baada ya kusikia maneno hayo kutoka kwa msichana huyo, hakutaka kumuamini alihisi labda alikuwa akimdanganya ili asiweze kumuacha lakini kitu cha kushangaza Monalisa alipoona Richard hamuamini aliamua kutoa cheti cha majibu ya dakatri ambayo yalikuwa yakimuonyesha kweli kuwa ni mjamzito.

****

Mapenzi yaligeuka kuwa mwiba wa maumivu kwa upande wa Evelyne, licha ya moyo wake kumpenda Richard lakini mwanaume huyo tayari alikuwa ameshamsaliti, hilo liliendelea kuwa tukio lililozidi kumuumiza sana, alikosa raha ya maisha, alishindwa kusoma, ulimwengu wa mapenzi alichukia.

Maumivu ya kimapenzi hayakuishia kwa kusalitiwa tu bali alizidi kuumia mara baada ya kusikia kuwa Monalisa alikuwa amebeba ujauzito wa Richard na ujauzito huo ndiyo ulizidi kumfanya azidi kumchukia mwanaume huyo.

“Sidhani kama nitakuja kupenda tena katika maisha yangu,” alisema Evelyne huku akijiapiza.

“Usiusemee moyo huwezi kujua nini kitakachotokea baadae,” alisema Happy.

“Sijui Happy kama nitapenda tena moyo wangu unakidonda na sijui kama kitapona na hata kama kikipona bado kitaniachia jeraha la maisha,” alisema Evelyne huku machozi yakianza kumdondoka.

Kipindi ambacho moyo wa Evelyne uliweza kupata maumivu ya kimapenzi, alijikuta akiwa ni mpenzi wa kuperuzi mtandao wa kijamii wa Instagram, aliuamini mtandao huo na ndiyo ambao uliweza kumsahaulisha maumivu yote ya kimapenzi ambayo moyo wake ulikuwa umeyapata.

Ndani ya mtandao huo wa Instagram katika kipindi asichokitarajia alikutana na mvulana aliyejulikana kwa jina la Fredick na kama utani alijikuta akianzisha urafiki na mwanaume huyo na baadae urafiki huo uliweza kuibua penzi kati yao.

Aliendelea na masomo yake ya chuo huku penzi hilo jipya likionekana kumbadilisha kwa kiasi fulani, hakuonekana kuwa mtu wa kuumizwa tena na mapenzi, moyo wake tayari ulikuwa umepata tumaini lingine, alimpenda sana Fedrick kwake mwanaume huyo alimuona kuwa sawa na malaika ambaye alikuja kipindi asichokitarajia.

****

Richard hakuwa tayari kuona Monalisa anaendelea kuubeba ujauzito, alichoamua kukifanya ni kumshauri autoe ujauzio huo lakini hilo lilikuwa ni jambo gumu mno kuweza kufanyika, Monalisa hakuwa tayari kufanya kitendo hicho.

Alizidi kuchanganyikiwa baada ya kusikia kuwa Evelyne alikuwa ameshampata mwanaume mwingine, hakutaka kuamini ilibidi atafute nafasi ya kuzungumza na msichana huyo ambaye moyo wake ulikuwa bado unampenda sana.

“Naomba uniache na maisha yangu,” alisema Evelyne.

“Siwezi kufanya hivyo hata mara moja nakupenda Evelyne,” alisema Richard.

“Upendo wako hauna faida tena kwangu.”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Kwa nini unasema hivyo kwa nini unauumiza moyo wangu?”

“Siamini kama kweli ninauumiza moyo wako ila jaribu kuchunguza sababu ya maumivu yako.”

“Evelyne nataka urudi kuwa wangu.”

“Kwasasa haitawezekana kwa sababu moyo wangu anaumiliki mwanaume mwingine.”

“Yupi.”

“Fredrick.”

“Hapana Evelyne, Hapana.”

“Huo ndiyo ukweli.”

“Nakupenda Evelyne.”

“Nilikupenda Richard,” alisema Evelyne kisha akaondoka eneo hilo.









ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog