Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

UTANIKUMBUKA TU! - 2

 






Simulizi : Utanikumbuka Tu!
Sehemu Ya Pili (2)






Edga alitaharuki sana aliposikia Kayumba kamtaja Catherine kwa huzuni huku akitiririsha machozi,hakutaka kujua papo hapo sababu hasa iliyopelekea hali hiyo, zaidi alimshika mkono wakarejea maskani. Baada ya chakula, sasa Edga alitaka kujua ukweli alionao Kayumba kipi kinacho msibu. Alishusha pumzi kisha akasema "Kayumba, nakumbuka niliwahi kukuuliza sababu gani ambayo inakufanya mara kadhaa uso wako usionyeshe tabasamu. Lakini hukutaka suala hilo tulizungumzie badala yake ukadai tuzungumzie masuala ya kazi,lakini pia leo wakati tunatoka kazini, kuna gari fulani hivi ulikuwa ukulikodolea macho, na baada nikakusikia ukitaja jina Catherine. Hivi huyu Catherine ndio nani kwako, na kwanini umelitaja jina ilihali ukiwa na majonzi? Tafadhali sana Kayumba usinifiche we niambie tu ukweli ", aliongea Edga kwa sauti ya chini huku akimtazama Kayumba katika mwanga hafifu uliopenya mahali walipolala kutokea umeme uliokuwa ukimulika kwenye moja ya nyumba. Kayumba alishusha pumzi ndefu kwanza, alijisonya mara mbili mfululizo huku moyo wake ukihisi uchungu, hali ya kuwa kinywa chake nacho kikihisi uzito kunena kile kilicho mkuta ingawaje baadaye alianza kumsimulia hali jinsi ilivyokuwa. Alisema "Edga, kuna wakati najikuta naogopa kulala. Sababu kila nikifumba macho yangu namuona Catherine. Ubongo wangu umevurugika, kiasi kwamba siwezi kukaa masaa matatu pasipo kumkumbuka Catherine. Catherine ni mwanamke ambaye nilianza naye mahusiano angali wadogo sana, kijiji kizima kilatambua uwepo wa penzi langu na yeye mpaka tunafika umri wa utu uzima. Nilimpenda sana Catherine wangu kiasi kwamba wanawake wengine nikawaona hawafai", Kayumba kabla hajaendelea kusimulia akayafuta machozi yake yaliyokuwa yakimtiririka,kwisha kufanya hivyo alisema "Ilikuwa hivi...." akaanza kukumbuka.

*********

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Kayumba mpenzi wangu, pole sana kwa matokeo lakini siku zote kuferi shule sio kuferi maisha", ilisikika sauti ya Catherine akimwambia Kayumba,pindi wawili hao walipokutana na kuanza kuzungumza mstakabali wa penzi lao mara baada kuona dhahiri shahili Elimu u karibu kuwaweka mbali baada Catherine kuchaguliwa kuwa moja ya wanafunzi waliofauru kuendelea na Elimu ya sekondari. Catherine aliongea maneno hayo huku akiwa amemkumbatia Kayumba

"Ni kweli kabisa Catherine, ila hilo lisikupe shida. Akili yangu kwa sasa inawaza kutafuta pesa ili nihakikishe unafikia malengo yako. Nakupenda sana Catherine wangu", alijibu Kayumba. Catherine aliangua kicheko, kisha akaongeza kusema "Na mimi nakuombea mpenzi wangu, na sitosita kuendelea kukwambia kuwa nakupenda sana zaidi ya sana. Nitasoma kwa bidii, ili nipate kazi nzuri itakayo nipa kipato kizuri ambacho kitatufanya tujenge familia bora"

"Ahahahah hahahaha", Kayumba alicheka. Alipohitimisha kicheko chake akasema "Catherine, unajua wanaume wengi wa sasa wanaamini kwamba mchumba hasomeshwi, dhana hiyo imejengeka baada wale wasaliti kuwa fanya wapenzi wao kuumizwa. Kwa maana sasa, mimi Kayumba nataka nionyeshe dhana hiyo ni potofu. Nitapigana mpaka dakika ya mwisho kuhakikisha unatimiza malengo yako "

" Amini mpenzi wala sitokusaliti japo nitakuwa mbali na wewe ", isisitiza Catherine mbele ya macho ya Kayumba. Wawili hao walifurahia sana, na sasa walisubiri siku ile ambayo Catherine ataondoka kwenda kuanza masomo ya kidato cha kwanza iweze kuwadia. Mazungumzo mengine kadha wa kadha yalifuatia, lakini hayakuchukuwa muda mrefu sana Catherine akamuaga Kayumba huku akidai kuwa anakwenda kuandaa chakula cha usiku.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Usiku mwema mpenzi wangu Kayumba..", kwa sauti ya chini Catherine alimuaga Kayumba wakati huo akiwa kando yake hatua kadhaa mbele. Kayumba alimtazama akatikisa kichwa ilihali tabasamu likiupamba vema uso wake, kisha akajibu "Usiku mwema pia".. Yote hayo Kayumba aliyakumbuka na sasa alikuwa akimueleza rafiki yake Edga. Hakuisha hapo, kwa sauti iliyoambatana na kilio Kayumba alisema "Basi tulisubiri ile siku ya yeye kwenda kuanza masomo iweze kuwadia, wakati huo siku hiyo ikisubiriwa mimi niliendelea kutafuta pesa kwa kulima vibarua. Siku hiyo ilifika, kuanzia hapo mimi na Catherine tukawa tunaonana kwa nadra hasa hasa pindi nimpelekeapo fedha za kutatulia shida mbali mbali. Ilinilazimu kusafiri mpaka mjini kumpelekea fedha, msaada pekee nilikuwa mimi sababu hakuwa na mama wala baba. Wazazi wake walifariki miaka mingi sana iliyopita aliishi na bibi yake ambaye naye hali yake ilikuwa duni. Hivyo Catherine mpaka anahitimu kidato cha nne, anaingia cha tano. Ghalama zote zilikuwa juu yangu mimi lakini kati kati ya msimu upatikanaji wa fedha ukawa mgumu kijijini kwetu. Nikawaza nitafanya nini, na hapo ndipo nilipoamua kuvaa moyo wa kijasiri, kijijini kwetu kuna mzee mmoja ni tajari, anang'ombe, mbuzi na mifungo mingineyo achilia mbali maduka mjini. Mzee huyo alikuwa na kawaida moja, kila baada ya siku mbili anasafiri kuelekea mjini,na saa za kurudi alipenda kurudi jioni sana kwenye giza totoro. Akili ya haraka ikanijia, nilipoona nachelewa kupata fedha ikanibidi nipange njama ya kumpora begi alilopenda kutembea nalo. Niliamini fika begi hilo litakuwa na fedha za kutosha,sikuona hatari kwa maisha yangu yote sababu ya penzi la Catherine. Kwani wakati nawaza hayo, Catherine tayari alikuwa amerudi nyumbani shauri kwa muda. Kweli nilifanya hivyo, na nilibahatika kuondoka na begi lake. Lakini kumbe wakati nakimbia baadhi ya watu waliniona, pasipo mimi kujua. Nguvu ya pesa aliyokuwa nayo yule mzee ilimfanya kunifungulia mashtaka na wala hakutaka mzunguko mrefu moja kwa moja nikafikishwa mahakamani". Alisema Kayumba kwa kirefu, na punde si punde akakumbuka tukio hilo. Ilikuwa ni siku ya vilio sana mahakamani, mzee Masasa baba yake Kayumba alilia kiume hali ya kuwa Bi mitomingi mama Kayumba na Catherine hawakuweza kuzuia sauti zao. Waliangua vilio, ni pale baada Kayumba kusomewa shatka lake linalo mkabili. Miaka saba ndiyo ilikuwa hukukumu yake, ajabu wakati ndugu jamaa na marafiki wakiwa katika hali ya majonzi, Kayumba yeye alionekana kutabasamu. Aliposhuka kizimbani, Catherine kwa sauti ya kilio alisema "Pole sana mpenzi wangu, najua umefanya haya kwa kujali ndoto zangu. Sina baba sina mama. Na wewe ndio ulikuwa nguzo yangu tegemezi achilia mbali bibi yangu. Leo hii unaondoka?.."Catherine alilia.

" Catherine. Hupaswi kulia, najua bado tupo pamoja ndani ya moyo wako. Na hivyo basi pesa nilizokupa ni Nyingi sana, zitakusaidia kwa kiasi kikubwa. Ila tu, ombi langu naomba upendo wangu usiutupe.. ", alijibu Kayumba wakati huo akivutwa na moja ya askari. Pumzi ndefu alishusha Kayumba baada kumsimulia Edga namna alivyomjali na kumthamini Catherine. Hakika ni kumbukumbu ambayo iliuumiza moyo wake. Alikaa kimya kidogo, punde alivunja ukimya huo akasema na kusema." Baada changu kumalizika nilitamani sana nimuone Catherine. Nikapata habari kwamba yupo Dar es salaam, tayari amepata kazi na maisha yake anayeendesha vizuri. Nilifurahi sana, sikuwa na ndoto ya kukanyanga ndani ya jiji hili, lakini ilinilazimu kuja kumuona mpenzi wangu nikiamini kuwa atafurahi sana kuniona. Ila sasa kilicho tokea Edga, huwezi amini Catherine amenikataa,amenikana akidai kuwa penzi langu kwake limepata na wakati kwa kigezo kikubwa kuwa yeye ni msomi, hawezi kuwa na mimi mtu nisiye na Elimu. Edga! Catherine wa kunifanyia mimi haya? Inamaana amesahau fadhila zangu zote? .. ", alisikitika sana Kayumba,achilia mbali Edga ambaye alionyesha upole wa hali ya juu. Kisa cha Kayumba kilimuacha mdomo wazi, maumivu aliyoyahisi hayakuwa na mfano. Lakini baadaye, Edga alimgusa Kayumba kisha akamwambia

" Pole sana Kayumba rafiki yangu, siku zote mtu hujifunza kutokana na makosa. Hakika ni kosa kubwa sana ulilolifanya braza, mchumba hasomeshwi. Labda nikujuze kitu kimoja, wanafunzi vyuoni wanakawaida ya kuwa na wapenzi wengi. Dhana hii nafikiri itakuwa imemkumba na Catherine wako na ndio maana akaona heri atoke na msomi kuliko wewe usiye na Elimu. Na kama sivyo basi hakupenda kutoka moyoni na utambue kuwa yale hayakua mapenzi, ilihali ulimuonyesha kujali lakini yeye hakuliona hilo, hivyo basi huna budi kumuacha aende!! Kwa maana kila jambo hutokea kama kipimo cha maisha. Ngoja nikwambie jambo muhimu katika maisha yako. Ni vizuri sana unaufahamu mto,maji ya mto hukabiliana na vikwazo mbali mbali lakini havizuii maji kutiririka. Mto unapokutana na miamba hata mara moja hauwezi bali hutengeneza njia yake juu ya mwamba huo. Mto unanguvu kiasi kwamba binadamu hujenga madaraja juu yake ili waweze kuvuka na pale unapojaa huweza hata kuyabomoa. Amini jitihada huwa hazizidi kudra, hebu kuwa wewe kama mto. Nina imani ipo siku atakukupumbuka tupige kazi ", Alisema Edga. Maneno ambayo yalimfanya Kayumba kuyatafakari mara mbili mbili. Punde akaachia tabasamu hafifu.





Aliachia tabasamu pana Kayumba, dhahiri shahili maneno ya Edga yalimfariji vilivyo. Na wakati akiwa kwenye hali hiyo ya tabasamu, Edga aliongeza kusema. "Kazi ndio kila kitu, wewe ni zaidi ya ndugu sasa Kayumba kwahiyo sipo tayari kuona moyo wako unasononeka. Vile vile kama ulikuwa hujui, mwenzio nafikiria kukutafutia kazi nyingine. Kazi ya kubeba mizigo naona ni adhabu kwako".

"Ahahahah, ni kweli kabisa ila usipate tabu bwana. Hakuna kazi rahisi hapa chini ya jua", alijibu Kayumba akitanguliza kicheko.

"Hivi kuendesha mkokoteni unaweza?..", aliuliza Edga.

"Ndio naweza", Kayumba alijibu kishujaa.

"Basi naomba kesho twende sehemu, kuna mchongo nataka nikuunganishe nao. Natumai utafurahi sana", aliongeza kusema Edga.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Naam! Kweli wewe mtoto wa mjini, maana unamipango zaidi ya raisi wa Marekani bwana Barack Obama", alisifia Kayumba wakati huo macho yake yakiitazma mahali pakulaza mbavu zake. Muda huo ilikuwa yapata saa saba usiku, hivyo basi hawakuwa na lazida walilala kwa dhumuni la kesho panapo MAJALIWA yake Mungu kukuche waende kusaka tonge. Usiku huo ulikuwa mzuri sana kwa kijana Kayumba, aliyatuliza vilivyo mawazo yake kwa kuwaza mstakabali wa kuisaka shilingi, zoezi hilo halikuchukuwa muda mrefu sana mwishowe usingizi ulimpitia. Kesho yake alfajiri na mapema alikurupuka kutoka usingizini baada Edga kumuamsha. "Ahahahah hahahahah", Edga aliangua kicheko. Alipokatisha kicheko chake akasema "Yani huwezi amini Kayumba, ukiamshwa kutoka usingizini unaonekana mbaya. Uso mkavu kama gurudumu la trekta", alitani. Kayumba aliachia tabasamu huku akiyafikinya macho yake, alipohakikusha kuwa sasa yanaona vizuri alimuuliza muda Edga. "Hivi itakuwa saa ngapi muda huu?.."

"Sina saa ila nafikiri saa kumi na moja na dakika zake, kumekucha. Sasa twende huko nilikokwambia". Edga na Kayumba walianza safari. Walifika sehemu hiyo husika, ilionekana mikokoteni mingi sana. Wawili hao bado walivuta hatua zao, kuuacha mkokoteni moja baada ya mwingine huku macho yao yakiiangalia. "Karibuni..", alisikika mtu mmoja akiongea. Mtu huyo alikuwa amesimama kando huku mkononi akiwa ameshika daftari ndogo. Mtu huyo alikuwa akikodisha mikokoteni na kuuza pia.

"Tunaangalia upi unatufaa", alijibu Edga.

"Mnanunua au mnakodi?..", aliuliza bwana huyo.

"Hapana tunakodi..", Kayumba alijibu, punde si punde macho yake yaligota kwenye mkokoteni ambao alivutiwa nao.

"Huu unatufaa sana", alisema Kayumba. Ndipo muhusika alimsogelea na kisha kukamilisha taratibu stahiki.

"Hiki ni kitendo kikubwa mno cha mkokoteni hapa mjini, kwa maana hiyo basi uaminifu ndio nguzo pekee ya kufikia malengo yako. Na ndio maana jambo la kwanza tunalo zingatia ni kufahamu kituo chako maalumu unachofanyia kazi, na mengine kadha wa kadha tuliyoorodhesha hapa kwenye daftari letu tu. Kazi njema ".

" Shaka ondoa ndugu yangu ", alisema Edga wakati huo akihesabu fedha na kisha akamkabidhi mtu huyo. Zoezi hilo lilipokamalika, waliondoka mbali na eneo hilo. Walienda nje kidogo ya jiji, huko palikuwa na minazi mingi mno. Vijana mbali mbali walioonekana kuwa na mikokoteni wengine baiskeli walikuwa shap kulangua madafu,fujo za hapa na pale zilisikika huku Lugha mbali mbali za maudhui nazo zikitamba achilia mbali utani kadha wa kadha kuhusu soka na siasa.

"Penye wengi kuna mengi bwana", alisikika mzee moja akisema maneno huku macho yake yakitazama namna vijana waliyokuwa wakichakarika,wakati huo huo Edga aliingiza mkono mfukoni akachomoa kiasi kadhaa cha fedha akamgeukia Kayumba kisha akasema "Kayumba, kama nilivyokwisha kukueleza hapo awali rafiki yangu. Sisi ni wasaka tonge, kwa maana hiyo basi lazima tupange mipango madhuti jinsi ya kusaka pesa. Asikwambie mtu braza heshima pesa, shkamoo kelele. Nina imani kabisa tutafanikiwa.. Hii fedha tuliyoweka, nimeona bora tununue madafu ukayauze mtaani wakati huo mimi naendelea na kazi yangu ya kubeba mizigo ".

" Wazo nzuri sana rafiki yangu, ila nisingependa uendelee kuifanya ile kazi. Kaka utavunjika mgongo angalia kijana ujue!?.. ", alisema Kayumba akimuasa Edga.

" Ahahahaha hahahaha ", Edga aliangua kicheko. Alipokihitimisha akasema." Mwanzo mgumu, acha nipambane najua Mungu u karibu nami. Na sasa tusogee ili tuchukue mzigo ukaanze kazi. Ammmh! Siku ya leo nitatembea na wewe ukariri maeneo ili kesho na hata siku nyingine usipate shida".

"Sawa". Edga akiwa sambamba na Kayumba walijongea kununua mzigo wa madafu. Zoezi hilo halikuchukuwa muda mrefu, na sasa wakaanza safari ya kurejea jijini huku wakikokota mikokoteni wenye madafu. Siku hiyo walizulula karibu Wiliya yote ya Ilala na viunga vyake, mnao saa kumi na mbili mzigo wote ulikuwa umekwisha. Hakika walifurahi sana, maswahiba hao walishangilia kwa kuruka ruka huku wakitembea miondoko ya kunyata ikiwa ishara ya masihara. Watembea kwa miguu waliwashangaa sana, achilia mbali abiria waliokuwemo ndani ya daladala na wale waliokuwemo ndani ya magari yao binafsi. Wote macho yao yalisonga kwa vijana hao wasaka tonge, Kayumba na mwenzake Edga ambao wote kwa pamoja walishindwa kuzizuia hisia zao za furaha mara tu walipomaliza mzigo.

"Hii kazi inakufaa sana rafiki yangu Kayumba, hesabu zetu zimegonga pale pale. Nilikwambia mzigo huu ukiisha tutakuwa na faida kubwa, tazama sasa mtu wangu. Ahahahah hahahahah",alisema Edga huku akiwa na furaha isiyo kifani. Fedha walizopata siku hiyo si haba kwa maisha yao ya kulala nje, walirizika nayo jambo ambalo liliwapelekea kuanza kupanga mikakati ya kununua mkokoteni wa kwao ili kuepukana na adha ya kukodi.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Hilo wazo nzuri sana", Edga alimuunga mkono Kayumba ambaye alitoka wazo la kununua mkokoteni wao.

"Kwa sababu endapo kama tutafanya hivyo itatuwea rahisi kupanga chumba chetu na maisha yakaendelea..", aliongeza wazo Kayumba. Hakika ni mawazo chanya ambayo yalimfanya Edga kuachia tabasamu na kisha akasema "Unasikia Kayumba? Kauli yetu nikisema wasaka, wewe unaitikia tongeeee, tunarudia mara mbili baada ya hapo sasa tunatishiana kwa kurushiana ngumi. Yani nikipiga juu wewe unainama, ngumi inapita halafu unajibu mashambulizi vile vile na mimi naikwepa"

"Ahahahah.. Hahahahah", Kayumba alicheka. Na hayo yote Edga aliyafanya kwa jitihada ili Kayumba apate kumsahau Catherine, binti aliyemuachia kovu la mapenzi kwa kumtakataa kuwa hana elimu alidiriki kusahau kuwa elimu hiyo anayojivunia alisomeshwa na nguvu Kayumba. Mpango huo kwa asilimia kadhaa ulikwenda vema, Kayumba wakati wote alionyesha kufurahia maisha.

Siku iliyofuata alikwenda peke yake. Alinunua mzigo na kisha kwenda kuuza, ajabu siku hiyo alimaliza mapema. Saa tisa alasiri alirejea maskani hali ya kuwa jioni saa kumi na mbili Edga naye alirudi. Alishangaa sana kumkuta Kayumba, kwa sauti ya juu akacheka sana kisha akasema "Wasaka.."

"Tongee..", aliitikia Kayumba, maneno ambayo wawili hao waliyarudia mara mbili mbili na punde si punde wakaanza kurushiana ngumi na kuzikwepa. Baada ya hapo waligongeana tano kisha wakaketi na kuanza kupeana pole ya mihangaiko ya kutwa nzima.

"Kazi inakwenda vizuri sana braza.. Lakini pia habari njema ni kamba kichwa changu kwa sasa hakimfikirii tena Catherine.."

"Kayumba? Unasema kweli?..", Edga alitaharuki baada kuyasikia maneno hayo aliyoyasema Kayumba. Alimtazama kwa mshangao, wala asiyaamini masikio yake.

"Hahahah, hebu rudia tena unasema Catherine?..", alihoji Edga kwa tabasamu bashasha. Kayumba aliongeza kusema "Ukweli ni kwamba kichwa changu kwa sasa hakimfikirii tena Catherine"

"Oyoooooh! Vizuri sana", alishangilia Edga, kisha akasema "Amini kwamba na wewe una moyo na sio jiwe,kwahiyo ipo siku atajua thamani yako kwake. Na ndio utajua kuwa wewe ni mstahili juu yake. Kayumba kutesa kwa zamu, nakuhakikishia ipo siku atakumbuka kuwa wewe uikuwa mtu sahihi kwake,wakati huo wewe huna tena hisia juu yake. Sababu yule aliyebadilisha mikate mitano ikashibisha maelfu ya watu,na ndio yule aliebadilisha maji kuwa divai. Basi huyo huyo anaweza kuubadilisha moyo wake kukuhitaji wewe. Na hapo ndipo Catherine atakapojua utofauti kati ya mimba na ujauzito.", alisema Edga, maneno ambayo yalimfanya Kayumba kuachia tabasamu.



Hayo ndiyo yakawa maisha ya Kayumba na Edga, maisha ya furaha wakati wote. Wasaka tonge hao walipambana kufa na kupona kuisika shilingi, hakuna hata mmoja aliyeonyesha uvivu kumtegea mwenzie. Na kadri siku zilivyozidi kwenda, ndivyo mtaji wa kununua madafu ulipoongezeka. Awali Kayumba alikuwa akinunua madufu themanini, sasa hatimaye idadi iliongezeka.

"Mambo sio mabaya rafiki yangu", aliongea Kayumba akimwambia Edga, muda huo ilikuwa yapata saa moja usiku wakiwa wameketi ndani ya mgahawa wakila chakula.

"Naam! Nafikiri juma lijalo tununue mkokoteni wetu sasa", alijibu Edga.

"Hata mimi nilikuwa nafikiria suala hilo hilo"

"Kweli?..", alihoji Edga. Kayumba akajibu "Ndio..", kisha wote kwa pamoja wakaangua kicheko. Walipohitimisha vicheko vyao, Edga akasema "Unajua rafiki yangu siku zote jasho la mtu haliliwi, na endapo kama utathubutu kulila basi ujue utapata madhara. Kayumba wahenga wanasema kazi mbaya ikiwa yako, mimi naomba tupambane ukweli njia ya utajiri naiona siku za usoni"

"Hahahahahahah..", aliangua kicheko Kayumba, maneno ya Edga yalionekana kumvunja mbavu.

"Usicheke bwana huo ndio ukweli, na nilicho gundua wewe unanyota ya fedha. Hivyo basi nyota yako hiyo hiyo ndiyo itakayo tupatia utajiri", aliongeza kusema Edga.

"Huwenda ikawa kweli, maana kama lisemwalo halipo basi linakuja. Mimi nakubaliana na maneno yako Edga", alijibu Kayumba wakati huo wakitoka ndani ya mgahawa huo na kisha kuanza safari ya kuelekea maskani kwao. "Unajua mpaka sasa sijajua ni kwanini wale jamaa zako wameamua kuchagua maisha yale, maisha ambayo kifo kipo mkononi", aliongeza kusema Kayumba.

"Rafiki yangu Kayumba kuishi ni kuchagua, wale jamaa wameamua kuchagua yale maisha kama ambavyo sisi tumechagua...",Edga alijibu kisha kimya kidogo kilitawala. Lakini baadae kidogo kimya hicho kilitoweka, Edga akaongeza kusema "Utakuwa unajiuliza ni kwanini na mimi niliamua kuungana nao"

"Ndio kwa sababu tabia yako haiendani na tabia zao", Kayumba alikubali,na ndipo Edga aliposhusha pumzi ndefu, tayari walikuwa wamefika maskani waliketi balazani kabla hawajalala Edga akaongeza kusema "Ni simulizi ndefu sana Kayumba, tuombe Mungu hapo kesho tumalize shughuli zetu mapema ili tukifika nyumbani niweze kukusimulia. Ila kwa sasa naomba tupumzishe akili na nguvu kwa niaba ya kesho".

"Sawa usiku mwema kwako braza", aliongea Kayumba huku akijikunyata barazani tayari kwa safari ya kuutafuta usingizi. Kesho yake asubuhi palipokucha, anga karibia lote la jiji lilikuwa limetanda wingu nzito la mvu. Hali hiyo iliweza kutandabaisha kuwa wakati wote wote mvua itanyesha, Kayumba na Edga walikurupuka kutoka usingizini ghafla wakaingiwa na hofu kuhusu hali hiyo ya hewa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Naona hali ya hewa si rafiki", aliongea Edga.

"Ni kweli kabisa ila haiwezi kututisha, twende zetu tukausake utajiri", alijibu Kayumba. Na sasa safari ikaanza, kila mmoja alielekea kwenye kiwanja chake. Upande wa Kayumba, biashara ilikuwa ngumu siku hiyo. Hali hewa ilimpelekea madafu kutonunulika. Ilimvunja moyo ila hawakuwa tayari kukata tamaa, mikono nyuma kichwa chini jasho ndembe ndembe likiulowesha mwili wake aliuvuta mkokoteni wake mpaka mahali ambapo palikuwa na maduka mengi huku watu kadhaa wa kadha wakionekana kuingia na kutoka ilihali manyunyu ya mvua nayo yakionekana kuanza kushuka kulimwagilia vilivyo jiji. Pumzi ndefu alishusha Kayumba, akamtazama huku na kule kisha macho yake akayarudisha kwenye mkokoteni wake akaona ni heri apumzishe mwili wake kwa kuegemea pembezoni mwa mkoteni na punde si punde usingizi ukianza kumnyemelea. Lakini kabla hajasinzia, alisikia mayowe "Mwizi..mwizi.. Jamani mwizii", ilikuwa ni sauti iliyopenya vema kwenye masikio ya masaka tonge Kayumba, mara ghafla akayafumbua macho yake. Alistuka kumuua binti mrembo,akipiga mayowe akilalama kupolwa mkoba wake. Macho ya Kayumba yakatazama mbele zaidi, yakamuona kijana wa makamo akitimua mbio huku mkononi akiwa ameshika mkoba wakati huo watu wakiishia kumsindikiza kwa macho na hata wasimsaidie binti yule. Moyo wa huruma ulimuingia Kayumba, alikurupuka kutoka kwenye mkokoteni wake akamkimiza yule kibaka. Juhudi zake zilizaa matunda, Kayumba alifanikiwa kumpokonya yule kibaka mkoba alipola. Kwa tabasamu bashasha Kayumba alimkabidhi binti yule mkoba wake, binti ambaye alionekana kuwa mzuri mithili ya maraika. Alivaa hijabu nyeusi, ngozi yake ilidhilisha kuwa ni mtu kutoka ng'ambo. Binti wa kiarabu.

"Ahsante sana", aliongea mrembo yule.

"Usijali, siku nyingine kuwa makini dada yangu. Dunia imebadirika sana", alijibu Kayumba na kisha akaondoka zake kuelekea kwenye mkokoteni wake huku nyuma yule binti akimsindikiza kwa macho na mwishowe aliachia tabasamu pana ikiwa Kayumba tayari ameshaondoka zake na mkokoteni wake.

Jioni aliporejea maskani alimueleza Edga hali harisi biashara ilivyokuwa, Edga akasema "Siku zote siku huwa hazifanani Kayumba, hata sisi leo magari yalikuwa machache sana kwahiyo mizigo haikuwa mingi. Nadhani mikoani mvua itakuwa imenyesha nyingi, labda magari mengi yamekwama"

"Naam! Maana barabara zetu bwana nayo changamoto kubwa hapa nchini", Kayumba aliunga mkono. Na sasa waliekea mgahawani kupata chakula cha jioni, wakiwa njiani Kayumba alimsimulia Edga namna alivyo msaidia mwanadada pindi alipo polwa mkoba wake. Edga alifurahi sana kisha akasema "Ni jambo la heri ulilolifanya, sababu huwezi jua atakaye kusaidia hapo baadaye".

"Ni kweli kabisa lakini Edga unakumbuka jana uliniahidi nini?..", alihoji Kayumba. Edga akaguna halafu akasema "Ndio nakumbuka bila shaka ni lile suala la mimi kujiunga na kundi la Boko"

"Eeh, ulisema leo ndio utaniambia"

"Sawa Kayumba hofu ondoa, tukirudia maskani nitakupa mkasa mzima". Edga na Kayumba walifika mgahawani, walikula chakula walichonunua na hatimaye walirejea maskani huku Kayumba akiwa na shauku ya kutaka kujua ni sababu ipi iliyomfanya Edga kutumbukia kwenye kundi lile la maharamia, kundi la uharifu ambalo linaongozwa na Boko pande la baba mwanaume mwenye miraba minne. Pumzi ndefu alishusha Edga,ni simulizi ambayo inatonesha kidonda chake, lakini kwa kuwa rafiki yake wa karibu alihitaji kujua hakuwa na budi kumueleza namna ilivyo kuwa. Hivyo alipokwisha kushusha pumzi alisema. "Haya maisha yanasafari ndefu sana Kayumba. Katika tumbo la wazazi wangu, tumezaliwa wawili mimi na mdogo wangu wa kike anaitwa Sinsia. Wazazi wetu walifariki kwa ajari ya gari wakati huo mimi nina miaka kumi na mitano huku mdogo wangu akiwa na miaka kumi. Tiliishi maisha ya tabu sana pasipo kuwa na wazazi, tulinyanyaswa kadri ndugu walivyo weza. Huwezi amini Kayumba mashamba walitunyang'anya, nyumba wakauza tukakosa makazi. Na huo ndio ukawa mwanzo wa kuikosa Elimu,kwa sababu maisha yetu yalikuwa ya kutangatanga pasipo na muelekeo maalumu. Lakini miezi kadhaa mbele, kijijini kwetu alikuja aliyekuwa rafiki yake marehemu baba. Mzee yule alijiweza nikimanisha kwamba maisha yake yalikuwa si haba na siku hiyo alikuja kuhani msiba baada kutohudhuria mazishi. Bahati nzuri wakati anaingia kijijini, nilionana naye akastuka kuniona nipo katika mazingira yale ", alishusha pumzi ndefu Edga kabla hajaendelea kusema kile kilicho msibu mpaka kujiunga na kundi la Boko,machozi hayakuwa mbali na mboni za macho yake. Yalimtiririka huku Kayumba akimtazama kwa macho ya huzuni kunako giza totoro. Alikaa kimya kidogo, punde akaendelea kusimulia...

"Edga, ni wewe mtoto wa mzee Nyoni au macho yangu yanadanganya?..", Aliuliza kwa taharuki mzee huyo aliyekuwa na ukaribu na marehemu baba Edga. Mzee huyo aliitwa Ezlom.

"Ndio ni mimi", Edga alijibu wakati huo uso wake ukionyesha kubeba huzuni kubwa ndani yake.

"Sinsia naye yuko wapi?..", aliongeza kuhoji mzee Ezlom.

"Anaishi kwa mjomba, ila...",kabla Edga hajaendelea kuongea machozi yalimtoka, na ndipo mzee Ezlom alipozivuta hatua kumkaribia. Alipomfikia akasema "Edga, hebu kaza moyo. Niambie kipi kinaendelea kwa sasa tangu kifo cha wazazi wenu". Edga aliongea ukweli wote wa maisha anayoishi na mdogo wake tangu wazazi wao wafariki,hakika roho ilimuuma sana mzee Ezlom jambo ambalo lilimpelekea kuchukuwa jukumu la kwenda kuishi nao jijini Mwanza ambako ndipo yalipokuwa makazi yake huku akiwaahidi kuwasomesha nguvu zote. Mzee Ezlom aliishi mke na watoto wawili ambao wote ni wa kike, mzee huyo aliipenda sana familia yake na wote waliishi kwa furaha ila ujio wa Edga na Sinsia ghafla ulibadirisha mwenendo wa maisha. Ile furaha iliyokuwa ikitamaraki katika nyumba ya mzee Ezlom ilipotea, Edga na mdogo wake walinyanyaswa na mama mwenye nyumba, mkewe Ezlom. Sinsia alifanyishwa kazi ngumu zilizozidi umri alio nao, na pindi Edga ipokwenda kumsaidia aliambulia kipigo na matusi ya kejeri. Yote hayo watoto hao walikuwa wakifanyiwa baada mzee Ezlom kusafiri nje ya nchi.

"Kayumba hiyo hali iliweza kuniumiza sana, nilimpenda sana mdogo wangu na bado nampenda. Yale yote aliyokuwa akifanyiwa mimi roho ilikuwa inaniuma lakini nilimpa moyo nikiamini yale ni mapito na ipo siku yatakwisha..",alisema Edga kwa uchungu huku akipandisha kamasi jepesi,punde aliendelea kukumbuka.

Jioni moja, familia ya mzee Ezlom ilitoka kuelekea kwenye matembezi, nyumbani wakiwacha Edga na Sinsia wakilinda nyumba huku.

" Kaka Edga, maisha haya tutaishi mpaka lini?..", aliuliza Sinsia kwa sauti ya chini iliyojaa huzuni ndani yake.

"Naona bora nirudi kijijini kwa mjomba kuliko kuendelea kunyanyasika hivi", aliongeza kusema Sinsia, na safari hiyo machozi yalionekana kutiririka kunako mashavu yake. Edga alishusha pumzi ndefu, alijaribu kuyazuia machozi ila alishindwa naye hivyo hivyo yalimtoka wakati huo huo akasema "Ukweli sipendi kusikia habari ya kurudi kijiji kwa mjomba, maisha ya kule heri ya hapa hapa. Cha muhimu mdogo wangu, vumilia baba akirudi tutamueleza kila kitu na tutaishi kwa amani"

"Amani gani kaka?..", Sinsia aling'aka kisha akasema "Siku yoyote naondoka ndani ya nyumba hii, mimi najua baba yangu amefariki na huyo unayemsubiri ni baba yako wewe". Kwisha kusema Sinsia akaingia chumbani.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Na hiyo ndiyo ilikuwa siku yangu ya mwisho kuonana na kuongea na mdogo wangu,anaitwa Sinsia. Alitoroka nyumbani hatukujua ni wapi kaelekea,siku hiyo sikuwa na furaha ,kwani sikujua huko alipo u hali gani lakini baadaye mtu mmoja aliiambia kwamba ameuona Sinsia akiwa ndani ya basi liendalo Dar es salaam. Hofu ilizidi kutanda, sikuwa tayari kukaa mbali na mdogo wangu,ndani ya moyo wangu nikala kiapo lazima nimfuate Dar. Lakini niliwaza nitapat aje nauli?.. ", Edga alisimulia huku Kayumba akiwa kimya akimsikiliza rafiki yake. Edga akiendelea kukumbuka.

Anaonekana Edga akiwa chumbani amelala, ghafla mlango wa chumba chake unagongwa. Hima anakurupuka, sauti inasikika ikisema" We mwanaharamu unalala mpaka sahizi!? Hii nyumba ya baba yako?.. ", maneno hayo alikuwa akiyatamka mkewe mzee Ezlom, aliyaongea kwa sauti ya juu.

" Samahani mama, uchovu ndio umepelekea kuchelewa kuamka ", alijibu Edga kwa sauti ya upole. Mwanamke huyo alimtazama kwa hasira kisha akaongeza kusema" Natoka na mabinti zangu, naomba maua yale yote uyamwagilie, madirisha yafute vumbi nikirudi nikute kila kitu kipo safi "

" Sawa mama ", alikubali Edga kisha akarejea kitandani alijitupa mithili ya mzigo huku mawazo yake yote yakifikifia kuondoka. Mlinzi wa nyumba hiyo alipofunga geti, Edga tayari alikuwa nje akiishuhudia gari ndogo iliyobeba familia ya mzee Ezlom ikiishia. Haraka sana Edga alirudi ndani, moja kwa moja alijitupa kwenye sofa sebuleni,ghafla macho yake yakatazama mahali kilipo chumba cha mzee Ezlom, Edga akagundua kuwa chumba kipo wazi.

"Khaa, inamaana huyu mama kasahau kufunga chumba?..", alijuliza Edga na kisha akanyanyuka, kazipiga hatua za pole pole kukisogelea chumba hicho. Alipokikaribia alizama ndani zaidi, akafungua droo pole pole huku akiwa na wingi wa hofu. Punde alistuka, alichokiona ndani ya droo hakuweza kukuamini palikuwa na pesa nyingi. Lakini wakati akiwa kwenye hali hiyo ya taharuki, mara ghafla....





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog