Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

UTANIKUMBUKA TU! - 1

 










IMEANDIKWA NA : ALEXIS WAMILAZO



*********************************************************************************



Simulizi : Utanikumbuka Tu!
Sehemu Ya Kwanza (1)


 "Ahahahaaaaa! Nacheka kwa madaha kwani furaha niliyo nayo moyoni siwezi kuelezea. Baada ya kiza cha muda mrefu, hatimaye napata kuona mwanga. Ama kweli Mungu mkubwa. Kayumba sasa nipo huru huku macho yangu yakitamani kumuona mpenzi wangu Catherine mwanamke nimpendae kwa dhati kutoka kati kati ya kiini cha moyo wangu. Kwa hakika jinsi nimpendavyo nipo tayari hata kufa kwa ajili yake, na ndio maana nilikubali kufungwa jela ili nifanikishe hitaji la moyo wake.. Catherine sasa mwanaume wa ndoto yako nipo huru, najua miaka saba ni mingi sana ukiwa hujanitia machoni, lakini leo hii narejea uraiani na bila shaka niliyokusisitiza uyafanye utakuwa umeyatekeleza ingawa waswahili husema kwamba mchumba hasomeshwi. A hahahahaaaa! Hapana sitaki kuamini maneno yao,bila shaka Kayumba nitakuwa mwanaume wa kwanza aliyethubutu kufanya jambo hilo. Naamini nitakuwa mfano wa kuigwa. Ahahahah hahahah". Maneno hayo Kayumba alikuwa akijisemea ndani ya nafsi yake wakati huo uso wake ukionyesha wingi wa tabasamu. Furaha isiyo kifani ilitamaraki kwa kijana Kayumba hasa baada kumaliza kifungo chake cha miaka saba aliyohukumiwa baada kukutwa na hatia ya kuiba mali ya mwananchi. Kayumba aliona dunia imebadirika sana, vitu vingi vimeongezeka na vingine vimeboreshwa. Lakini vyote hivyo havikumfanya kustaajabu sana bali akili yake sasa aliielekezea kwa Catherine mpenzi wake. Alijawa na shauku ya kutaka kumuona. Hatimaye alifika kijijini kwao. Sherehe na ndelemo vililindima, ndugu jamaa pamoja na marafiki walifurahia ujio wa ndugu yao. Mzee Masasa akaamuru mwanawe achinjiwe Jogoo mkubwa kuliko wote ndani ya wale aliowafuga,yote hayo ikiwa furaha isiyo kifani juu ya kijana wake aliyerejea uraiani. Jioni ya siku hiyo waliifanya kuwa sikukuu. Na siku iliyofuata, Kayumba alizunguka kijijini huku na kule. Alishangaa sana kuona kijiji chao kikiwa na mabadiriko, maendeleo mbali mbali yalimfanya Kayumba kuzidi kupigwa na bumbuwazi jambo ambalo lilimpelekea kujawa na tabasamu wakati wote. Moja kwa moja alifika nyumbani kwa rafiki yake wa karibu sana, rafiki ambaye walikuwa wakisaidiana kila jambo kabla hajafungwa jela. Aliitwa Fikiri. Fikiri hakuyaamini macho yake baada kumuona Kayumba. Kwa taharuki ya aina yake alisema "Kayumba? Niwewe ama ndoto?"

" Fikiri, hapana wala sio ndoto. Kayumba nipo huru ". Alijibu Kayumba huku uso wake ukionyesha tabasamu bashasha.

" Ebwanaeeh! Mungu mkubwa kaka "Aliongeza kusema Fikiri wakati huo akimlaki kiume na kisha akamsogezea kigoda. Kayumba aliketi kisha akaanza kumuuliza juu ya maisha yalivyokuwa wakati yeye yupo jela. Fikiri aliongea yote, maneno ambayo yalimfurahisha Kayumba lakini marafiki hao hawakuishia hapo, zaidi Kayumba aliuliza maendeleo ya Catherine.

"Catherine?.." Fikiri alishtuka.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Ndio Mbona kama umeshtuka? Kuna nini rafiki yangu?.." Aliuliza kwa taharuki ya hali ya juu. Fikiri kabla hajasema jambo lililompekea kustuka, alishusha pumzi ndefu kwanza kisha akasema "Ndugu yangu Kayumba, ni kweli Catherine ulimpenda sana na yeye alikupenda vilivyo. Ila sasa baada wewe kuhukumiwa jela, Catherine alibadirika sana. Cathe aliyekuwa akikuaga kwa kilio na machozi siku ile ya hukumu, sio Cathe huyu wa sasa". Alijibu Fikiri.

"Bado Fikiri sikuelewi. Hivi unamaana gani kusema maneno hayo?.." Kayumba aliongeza kuhoji kwa mshangao huku macho yake yakimtazama Fikiri. Na kabla Fikiri hajaongeza neno lolote, Kayumba akaongeza kusema "Na je, unaweza kunisindikiza nyumbani kwao? Nikamuone.."

"Nyumbani? Catherine kwa sasa yupo Dar es salaam, baada ya masomo yake alipata ajira huko huko, kwahiyo kwa sasa hapa kijijini akija anakuja kusalimia tu.." Alijibu Fikiri. Kayumba alistushwa na jibu hilo, mara mapigo yake ya moyo yakamuenda mbio, huku hamu ya kumuona Catherine ikizidi kutamaraki katika fikra zake hali ambayo ilimfanya kupoa kidogo. Hali hiyo ilimuogopesha sana Fikiri na hapo ndipo aliposema "Kayumba, hupaswi kuumiza kichwa juu ya jambo hili. Kwanza mshukuru Mungu kwa sasa upo huru, na jambo la pili endapo kama unataka kumuona Catherine wako basi nipo tayari kukupatia maelekezo mahali pakumpata Jijini Dar es salaam. Mtaka cha uvunguni sharti ainame"

" Fikiri, nipo tayari kuinama ilimladi nikipate cha uvunguni. Sioni tabu kutoka hapa kuelekea Dar es salaam kumfuata Catherine.. Naomba unipe muongozo namna ya kumfikia, sipo tayari kumpoteza Catherine wangu ". Alisema Kayumba kwa hisia kali juu ya Catherine. Fikiri akainuka kwenye kigoda akaingia ndani, muda mchache baadae akatoka na karatasi iliyokuwa na maelezo ambayo yalielekeza wapi anapopatikana Catherine, akamkabidhi karatasi hiyo kisha akamwambia." Hii hapa ramani kaka, bila shaka huwezi kupotea hata iweje. Ramani hii alinipa siku moja alipokuja kutusabahi hapa kijijini, na leo hii ramani hii nakukabidhi wewe mshakaji wangu sababu nafahamu umuhimu wako kwa Catherine japo Catherine wa zamaani sio wa sasa "

"Nakushukuru sana Fikiri, wewe siku zote umekuwa bora sana. Na ndio maana hata nilipo kuwa jela nilikuwa nasali na kuomba ili siku moja niwe pamoja nawe uraiani. Fikiri kuna watu wanakwambia kwenda jela ni ujanja, bila shaka hao watu hawajawahi kuingia huko. Ujanja wakati kila kitu unapagiwa?.. "

" Ahahahah Hahaha "Fikiri aliangua kicheko mara baada kuyasikia maneno hayo ya Kayumba. Alipokwisha kukatisha kicheko chake akahoji" Mungu mkubwa ndugu yangu. Enhee nambie safari lini?..".

" Wiki ijayo, siku za hapa katikati nitakuwa katika harakati za kutafuta nauli na pia fedha ya kumnunulia Catherine japo vizawadi". Alijibu Kayumba kwa tabasamu bashasha.

"Sawa nakuombea ili ufanikiwe" Alikata kauli Fikiri, maongezi yao yakawa yamekomea hapo ambapo Kayumba alinyanyuka kutoka kwenye kigoda chake akaonda nyumbani hapo kwa rafiki yake aitwae Fikiri.

Ni dhahili shahili Kayumba alipania kumfuata Catherine jijini Dar es salaam,alitamani sana kukutana naye huku fikra zake zikiamini kuwa Catherine hatakama inasemekana kabadirika kamwe hawezi kumbadilikia na yeye. Fikra hizo zilimfanya Kayumba kucheka ndani ya moyo wake na kisha kujisemea " Itakuwa msimamo anaoonyesha Catherine wangu, ndio unao muhukumu kuwa kabadirika. Vijana wengi hupenda mwanamke anayrjirahisisha pindi aelezeapo hisia juu yao. Wakidiliki kabisa kusahau kuwa siku zote mwanamke imara huwa hajilengeshi. Bila shaka hii kitu ndio inayomfanya Catherine wangu kuhukumiwa kwa makosa hayo, nadhani hukumu yangu imemfanya aikumbuke ahadi yake aliyoniahidi siku ile ya hukumu yangu. Nami nasema Catherine baki na msimamo huo huo kwani tayari mwanaume wa ndoto zako nipo uraiani. Ahahahah hahaha " Alihitimisha kwa kicheko Kayumba mara alipokwisha kujesmea maneno hayo. Kamwe hakutaka kuamini kama Catherine kabadirika,na hivyo alingojea kwa shauku sana siku ya ile aliyopanga kumfuata Catherine iweze kutumia. Hatimaye siku ilikaribia. Aliwaeleza wazazi mzee Masasa na Bi Mitomingi juu ya safari ya kuelekea Dar es salaam kutafuta maisha na wala hakutaka kuwaambia ukweli kuwa anaenda Dar kumtafuta Catherine.

"Ni jambo jema sana mwanangu, ingawa mapema sana tangu utoke jela. Wazee wako tulihitaji uendelee kukaa nasi maana miaka saba si haba kijana wangu" Alisikika akisema hivyo mzee Masasa baba yake Kayumba. Muda huo ilikuwa yapata saa mbili usiku, usiku wa mbalamwezi wakiwa wameketi kando ya moto kwani msimu huo ulikuwa wa baridi kali,mahindi nayo waliyegeuza kwenye mafiga, zogo nalo likiufanya moto kukolezwa vilivyo.

"Lakini kwa kuwa umeamua kwenda kutafuta maisha, basi Mungu akutangulie kwa kila jambo mwanangu" Alidakia Bi Mitomingi mama Kayumba ambaye yeye muda huo alijitenga kando kidogo ya moto ingawa alionekana kujikunyata ndani ya blanketi. Kayumba alifurahishwa na namna wazazi wake walivyolipokea suala hilo,usiku huo huo alienda kumuaga Fikiri kisha kesho yake alfajiri safari ikaanza. Safari ya kuelekea Dar es salaam kumfuata Catherine mwanamke mpenzi wake ambaye alijitolea kumsomesha kwa udi na uvumba akihakikisha kuwa ndoto yake isiyeyuke.

Dar es salaam alifika mapema sana, hivyo kupita ramani aliyopewa iliweza kumuongoza mpaka mahali ilipo nyumba anayoishi Catherine. Ni nyumba nzuri sana, nyumba iliyopo Mikocheni B. Nyumba ambayo ilipendeza sana kwa kuitazama. Kayumba baada kugundua tayari kafika, alijitazama kwanza akaachia tabasamu wakati huo akiushika vema mfuko uliokuwa na zawadi aliyomeletea Catherine. Akazipiga hatua za pole pole kulisogelea geti, punde alibisha hodi geti likafunguliwa.

"Habari yako kaka" Kayumba alimsabahi mlinzi aliyefungua geti.

"Salama sema shida yako" Alijibu mlinzi huyo kwa sauti ya jazba. Kayumba akatabasam kidogo kisha akasema "Samahini naitwa Kayumba, bila shaka hapa ni nyumbani kwa Catherine.." Aliongeza kusema Kayumba.

"Catherine?.. Ndio nani huyo?.." Mlinzi alishtuka kulisikia jina hilo.

"Ndio, inamaana humfahamu?.."

"Ndio simfahamu, umepotea nyumba. Huyo Caselini wako mimi simjui unanipotezea muda bwana" Alijibu mlinzi na punde akataka kufunga geti lakini Kayumba alizuia huku akisisitiza kuwa nyumba hiyo ndio anayoishi Catherine,kitendo ambacho kilizua tafarani hapo getini. Lakini wakati tafarani hiyo ikiendelea mara Ilisikika sauti ikisema kwa jazba "We mzee Masumbuko! Vipi mbona sielewi kunanini hapo getini?.." Sauti hiyo ilisababisha tafarani hiyo kutulia wakati huo mlinzi akageuka kumuitika bosi wake. Hapo Kayumba anapata kumuona Catherine, tabasamu bashasha liloonekana usoni mwake na wala asiyaamini macho yake ilihali muda huo mzee Masumbuko akasema "Kuna mshamba hapa ananisumbua"

"Hebu mruhusu". Catherine aliamuru, amri ambayo mzee Masumbuko aliweza kuitii akamruhusu Kayumba aingie. Hakika Kayumba alifurahia sana, furaha aliyokuwa nayo moyoni mwake haikuwa na kipimo. Alizipiga hatua kumsogelea Catherine hali ya kuwa Catherine akionekana kusimama na wala asistushwe na ujio wake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Oooh! Malikia wa moyo wangu, Catherine mpenzi kipenzi changu nimerudi, Kayumba nipo huru sasa" Alisema Kayumba alipomkaribia Catherine.

"Mbona kama hufuraishwi na ujio wangu? Maana sioni ukionyesha hata tabasamu? Unataka kuniambia miaka saba yote hujanikumbuka?.." Aliongeza kusema Kayumba huku akimtazama Catherine uso kwa tabasamu bashasha ilihali Catherine akionyesha uso wa hasira. Mwisho akakohoa kidogo kisha akasema." Kayumba, naomba useme shida iliyokutoa kijijini ikakuleta nyumbani kwangu. Nina kazi nyingi za kufanya ndani sitaki unipotezee muda wangu". Kayumba alistushwa na maneno hayo ya Catherine. Akashusha pumzi kisha akasema "Hebu acha utani Catherine, basi twende ndani nikakusaidie kazi"

"Umsaidie nani? Nafasi pekee ambayo anaweza kunisaidia ni mpenzi wangu na sio wewe" Alijibu Catherine kwa sauti ya juu.

"Inamaana kwamba mimi sio mpenzi wako? Catherine umenisaliti?.." KWA sauti ya chini iliyojaa huzuni ndani yake aliuliza Kayumba. Hapo Catherine akacheka kwa dharau kisha akajibu "Ndivyo ilivyo Kayumba, asante kwa kunisomesha lakini kwa sasa nafasi yako imezibwa na mtu mwingine. Ulitegemea miaka yote saba niishi bila mwanaume? Ungelikuwa wewe ungeweza?"

"Sio rahisi hivyo Catherine", alisema Kayumba kwa msisitizo.

"Hupaswi kupingana na ukweli, kwa maana hiyo basi nakuomba utoke nyumbani kwangu haraka sana iwezekanavvyo...." alifoka Catherine huku mdomo ukimtetemeka kwa hasira ilihali maneno hayo yalimchanganya Kayumba, hakuamini kile alichokisikia akajihisi kukosa nguvu wakati huo huo machozi yakimtiririka machoni mwake. Kwa huzuni akasema" Kwanini Catherine umeamua kunifanyia unyama huu? Yote niliyokifanyia kama pendo langu kwako leo hii malipo yake ni haya? Umesahau kuwa wewe ndio sababu ya mimi kufungwa jela?.. Kwanini Catherine kwanini lakini? Kumbuka Catherine uliniahidi nini siku ile nahukumiwa jela, kumbuka Catherine kumbuka ", alisema Kayumba kwa uchungu huku machozi yakizidi kutiririka.





"Kayumba, kwa sasa sihitaji ngojera zako. Nimeshakwambia kuwa tayari nina mtu wangu. Na hivi karibuni tunaraji kufunga ndoa. Hebu jitazame, hivyo ulivyo unaweza kunimiliki mimi? Mimi ni msomi lakini pia mimi ni mwanamke mzuri nahitaji matunzo ya ghalama, wewe huwezi kunihudumia ", aliongea Catherine huku akimzunguka Kayumba ambaye kwa muda huo alikuwa amesimama, uso wake ukionyesha huzuni. Machozi mithiri ya jasho yalimtiririka. Hakuamini maneno ayasemayo Catherine. Kwa sauti ya huzuni na kilio, Kayumba aliongeza kusema.

" Catherine, inamaana umesahau msaada wangu juu yako? Kumbuka nilidiriki kujinyima ili wewe upate kile anacho kitaka Catherine. Kijijini waliniita kila aina jina la kuchukiza, na yote sababu ya kukuhudumia wewe ingali familia yangu siijali. Umesahau kuwa pasipo mimi kukulipia ada na kukusaidia mambo mengine zaidi leo usingekuwa na maisha haya? Elimu yako ndio kitu pekee unachojivunia mpaka kufikia hatua ya kuvunja ahadi yetu si ndio?", alipiga magoti, akayafuta machozi yake kisha akaendelea kusema." Nipo chini ya miguu yako, tafadhali rudisha moyo wako nyuma Catherine. Usidanganywe na hawa mabishoo wa mjini. Nakupenda sana Catherine wangu ".

"Nimeshakwambia sipo tayari kwa hilo, tena naomba uondoke ndani ya nyumba yangu haraka sana iwezekanavvyo" alisema Catherine kwa hasira. Maneno ambayo yalimfanya Kayumba kuzidi kutiririsha machozi. Moyo ulimuuma. Na wakati Kayumba yupo kwenye hali hiyo punde alikuja mpenzi wake. Ni mwanaume aliyeonekana shupavu kulingana na muonekano wa mwili wake ulivyo. Kwenye sikio lake la kushoto alivaa hereni. Kayumba alistuka alipomuona mwanaume huyo, alinyanyuka kutoka chini huku akimtazama kwa jicho la hasira. Akataharuki wakati huo huo mwanaume huyo alimkumbatia Catherine kwa mahaba mbele ya macho yake. Roho ilimuuma sana Kayumba, ni kama mwanaume huyo alizidi kumtonesha kidonda. Baada ya kitendo hicho, sauti ilisikika ikisema "Huyu ndio umemuona anafaa kukusaidia kazi?.."

"Hapana mpenzi wangu, huyu kaka alikuwa mpenzi wangu zamani sana enzi za utotoni kijijini" Alijibu Catherine, akimjibu mpenzi wake juu ya kile alichouliza. Aliitwa Johnson.

"Oooh! Eeh kwahiyo?" aliuliza Johnson.

"Amenifuata ili turudiane, ni jambo ambalo haliwezekani katika maisha yangu. Johnson hivi unionavyo mimi wa kuishi na huyo huyo mwanaume? Asiye na mbele wala nyuma?."

"Hapana kamwe haiwezekani, labda kama atapenda tumpe kazi ya kusafisha mazingira hapa nyumbani ili ajikimu na maisha. Ahahahah huwenda kaupenda mji"

"Hana maisha marefu hapa uraiani tangu atoke jela, kumpa kazi huyu mtu ni kukaribisha hasara humu ndani. Huyu mtu ni mwizi Johnson hafai kabisa",alidakia Catherine, maneno hayo aliyaongea kwa nyodo, Kayumba alishangazwa sana na maneno hayo,alibaki kuduwaa huku mikono akiwa ameiweka kichwani. Alishusha pumzi ndefu kisha akasema "Braza. Najua humpendi kwa dhati Catherine ila upo kwa niaba ya kumchezea tu. Hujui ni wapi mimi yeye tumetoka lakini hakuna shida, nimekubali kushindwa. Catherine naondoka ila nina imani ipo siku ipo siku utanikumbuka tu". Alipokwisha kusema hayo Kayumba alizipiga hatua kuelekea getini tayari kwa safari ya kuondoka ndani ya nyumba ya Catherine. Aliumia sana ndani ya moyo wake, katu hakuamini kama Catherine angeliweza kuthubutu kuvunja nadhiri yao.

"Hahaha hahahahah!.." kicheko cha mlinzi kilisikika, na punde akasema "Pole sana kijana, karibu Dar es salaam sasa. Nafikiri ulishindwa kusoma alama za nyakati kaka. Tangu lini mchumba akasomeshwa? Ni heri pesa zako ungelima mpunga, kuliko kumsomesha mchumba. Kwa kiswali chepesi tunasema, umejilipua.."

"Sitaki kusikia upuuzi wako mjinga mkubwa wewe", alidakia Kayumba akimjibu mlinzi.

"Kwenda zako huko, ukweli nimeshakwambia", mlinzi alifoka. Kayumba aliondoka mahali hapo akiwa ameinamisha uso wake chini mikono nyuma ilihali muda huo Catherine na Johnson walicheza kwa kukimbizana, mahaba moto moto yalionekana huku kila mmoja akiwa na hamu na mwenzie. Na kabla wawili hao hawajaingia ndani, Catherine alizipiga hatua kumfuata mlinzi. Alipomfikia alisema "Mzee Masumbuko, siku nyingine usimruhusu huyu mbwa kuingia ndani ya nyumba hii. Mimi na yeye mkataba ulishamalizika sawa sawa?.."

"Sawa bosi!", aliitikia. Baada ya hayo Catherine alirudi kumkumbatia Johnson kisha wakaingia ndani.

Jua tayari lilikuwa limezama, kwenye giza totoro anaonekana Kayumba akitembea huku hana hili wala lile. Mfukoni hakuwa na hata senti, sababu pesa aliyokuwa amebaki nayo kama akiba alimnunulia Catherine zawadi ya nguo ambayo nayo haikupokelewa. Kayumba alijikuta akijutia, neno laiti ningelijua halikuwa chachu mdomoni mwake, kila mara alilitamka. Kitendo alichomfanyia Catherine aliona ni cha kinyama sana ambavyo hakutarajia kama Catherine angeliweza kumfanyia. Pumzi ndefu alishusha Kayumba, mikono aliweka kiunoni, macho yake nayo yalitazama kila pande la jiji. Aliona magari yakipishana, watembea kwa miguu nao wakirejea kurudi majumbani baada ya mihangaiko ya kutwa nzima. Alitikisa kichwa, akisikitika kisha akajisemea.

"Naam! Dunia sasa imekuwa kigeugeu upande wangu. Catherine ameniachia kovu la milele moyoni mwangu. Laah! Amenifanya niwachukie wanawake ingawa najua pasipo hawa viumbe kamwe Dunia haitakuwa imekamirika. Lakini, mimi katika hili nitajitahidi kujizuia kupenda, nitaishia kutamani na sio kumuamini mwanamke kwa asilimia zote. Hatimaye usiku umeingia, Kayumba sielewi ni wapi nitaegesha ubavu wangu, ghafla nimekuwa kama kichaa. Eeh Mungu wangu nisaidie mimi ",alijisemea maneno hayo Kayumba huku akiwa amesimama kando ya barabara. Alikuwa mfano wa tiara, hakuwa na muelekeo. Ghafla mbele yake akaonekana kijana wa makamo akivuka barabara, Kayumba akavaa moyo wa ujasiri akamvagaa kijana huyo.

" Bro.. Bro.. Braza", aliita Kayumba. Kijana huyo aliyekuwa akivuka barabara aligeuka kutazama kule inapotokea sauti wakati huo huo Kayumba tayari alikuwa amemkaribia, alimsalimu. "Habari yako kaka"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Njema tu za kwako", kijana huyo alimjibu Kayumba huku akimtazama kwa wasi wasi.

"Kwangu pia njema. Ammmh! Kaka jina langu naitwa Kayumba. Naomba msaada wako tafadhali sina pakulala usiku huu, vile vile mimi mgeni hapa mjini, ndio leo nimefika. Sijui wapi pakuanzia wala pakuishia, nisaidie kaka nakuomba nipo chini ya miguu yako"

"Nikusaidieje? Na unawezaje kufunga safari ya kuja mjini pasipo kuwa na muelekeo? Halafu wewe hunijui wala mimi sikujui, haya itakuaje kama nikikupokea halafu ukanifia mikononi mwangu? Nitaanzia wapi kujieleza? Na je, unaniaminije mpaka ukathubutu kuvaa moyo wa ujasiri ukahitaji msaada wangu! Braza hapa mjini, mji huu unamambo mengi sana baadhi mchana watu ila usiku sio watu..", aliong'aka kijana huyo. Lakini mbali na kuongea maneno hayo kwa sauti ya ukali ila Kayumba aliendelea kumng'ang'ania amsaidie, wala hakujali,punde machozi yalimtoka wakati huo akishuka chini kumpiga magoti huku akiendelea kuomba msaada kwa mtu huyo asiyemfahamu, ni jambo ambalo limpelekea mtu huyo kuingiwa na huruma juu ya kile alichokionyesha Kayumba, hivyo alimshika mabega akamuinua kisha akasema.

"Sawa nitakusaudia kwa usiku huu, lakini kwanza yakupasa ukaze moyo na vile vile uwe jasiri na mtu mwenye siri "



"Jina langu naitwa Edga, sijui mwenzangu wewe unaitwa nani", aliongea jamaa huyo aliyekuwa akiombwa msaada na Kayumba. Kayumba alijitambulisha kisha akaambatana na Edga mpaka maskani anapoishi. Kijana Edga hakuwa na nyumba, alilali nje pembezoni mwa frem za maduka.. Hakuwa peke yake bali walionekana vijana wengine. Hiyo hali ilimshtua sana Kayumba, na hapo ndipo alipokumbuka maneno yale aliyoambiwa na Edga, lakini wakati akiwa katika hali ya kustaajabu, Edga alimgeukia kisha akasema "Kayumba, awali unaniomba msaada nilikwambia kwamba yataka moyo. Mjini hapa mimi sina nyumba wala chumba,kwahiyo nilishindwa kukukatalia kwa sababu siwezi jua roho niliyonayo mimi kama na wenzangu wanayo. Haya sasa ndio maisha ninayo ishi, hawa wote unao waona ndio washkaji zangu shaka ondoa "

" Edga, mimi ni mwanaume. Nakabiriana na kila hali, kwahiyo kuhusu suala hili wewe ondoa hofu kabisa ", alijibu Kayumba huku akiachia tabasamu bashasha usoni mwake, wakati huo huo baadhi ya vijana kadhaa waliokuwa wamelala waliamka. Mmoja wao alisema."Muda wote mmsimama kulikoni?.."

"Ni mimi Edga, jamani tumepata mgeni. Anaitwa Kayumba. Huyu jamaa nimekutana naye njiani alikuwa hana dira, hajui anzie wapi wala aishie wapi..."

"Kwahiyo?..", Edga kabla hajamaliza kuongea alichotaka kusema, aliulizwa.

"Nimeamua kumsaidia ili awe moja ya familia yetu, wasaka tonge", alijibu Edga. Punde si punde mtu mwingine aliamka, kwa sauti kali akasema "Huu utaratibu wa wapi? Unawezaje kumsaidia mtu kihorera? Hapa mjini mbona Edga unakuwa kama wakuja? Unajifanya unaroho nzuri sana sindio! Usitufanye sisi wajinga, akili ya kuambiwa changanya na yako, hakuna mtu mwenye akili timamu anayeweza kutoka kwao akaja mjini pasipo dira ", alifoka mtu huyo, aliitwa Boko. Kijana ambaye ni pande la mtu.

" Afadhali kiongozi utusaidie suala hili ", mtu mwingine aliunga mkono kile alichokiongea Boko. Roho Ilimuuma sana Kayumba, alijua fika yeye ndio chanzo chote cha mzozo huo,lakini hali ya ugeni wa jiji la Dar es salaam ilimlazimu kukaa kimya huku akimuomba Mungu Edga asije akapindua mawazo yake. Baada ya zogo la hapa na pale, hatimaye Boko, kiongozi wa vijana hao wasaka tonge alitoa amri, kwa sauti kali akasema "Kayumba, huyo mtu wako mstiri kwa leo tu ila kesho ajue pakwenda aidha ikiwezekana uondoke naye"

"Sawa kaka hakuna shida", alijibu Edga kwa sauti ya chini kabisa kisha akamshika mkono akasonga naye mahali anapolaza mbavu zake. Alipofika alimkabidhi Kayumba box la kulalia, kisha yeye akaegemea ukuta akiwa amekaa tayari kwa safari ya kuutafuta usingizi.

Ni suala ambalo upande wa Kayumba lilikuwa ngumu sana kuweza kupata lepe la usingizi, mawazo yake yote yalikuwa yakimfikiria Catherine. Alikumbuka maisha ya nyuma kabisa aliyokuwa akiishi naye, mpaka kufikia hatua ya kuthubu kumkana huku akidiriki kumtukana. Hakika roho ilimuuma sana, hasa akifikiria namna alivyokuwa akijitoa kwake kwa hali na mali kuhakikisha binti huyo anafikisha walau asilimia kadhaa ya ndoto zake. Baada kuwaza kwa muda mrefu, mwishowe alipitiwa na usingizi. Alilalia ila hata alipokuwa usingizini bado aliota ndoto kadhaa zilizomuhusu Catherine, moja ya ndoto aliyoota ni kumuona Catherine akichukuwa uamuzi wa kujiuwa baada kuteswa na mapenzi.

"Catherine.. Catherine", Kayumba akiwa kwenye dimbwi la njozi alilitaja jina la Catherine, na punde si punde alizinduka kutoka kwenye dimbwi hilo, akajikuta kuwa ilikuwa ndoto. Hakika alisikitika roho ilimuuma sana, machozi nayo hayakuwa mbali, yalimtiririka huku akililia moyoni. Lakini pindi alipokuwa katika hali hiyo, ghafla macho yake yalitazama kulia kwake,hatua kadhaa mbele alipata kuona kundi la vijana wakihesabu baadhi ya mali walizopora usiku wa siku hiyo. Alistuka Kayumba,na hapo ndipo alipojua kuwa amelala na watu ambao sio watu wema. Moyo wa woga ulimuingia, ikapelekea kumsahau Catherine kwa dakika kadhaa huku kijasho chembamba kikimtririka.

"Hapa ni pasu kwa pasu wala hakuna zuruma", Kayumba alisikia sauti ya Boko ikitoa amri ilihari zoezi hilo la kugawana mali likiendelea, mali hizo ilikuwa ni simu na fedha kadhaa. Mara baada zoezi hilo kukamilika, Boko aliongeza kusema "Sasa ndugu zangu kuna jambo ambalo nataka kuwaeleza. Dhahiri shahili, tayari ndungu yetu ameshaanza kuleta uhuru wa manyani kwenye kikundi chetu. Kwa maana hiyo basi tunacho takiwa ni kumchukulia uamuzi mgumu kabla mipango yote haijakwenda kombo"

"Uamuzi gani huo!?..", aliuliza moja ya watu waliokuwa wakimsikiliza Boko kile anacho kisema.

"Mimi nafikiria tumfukuze mahali hapa", alijibu Boko wakati huo macho yake yakitazama kulia na kushoto, moyo wake ukiwa na wasi wasi kwani tukio walilotoka kufanya muda mchache uliopita katu lisingeliweza kuuruhusu moyo wake kuwa na amani. Kimya kidogo kilitawala mara baada Boko kuongea maneno hayo, lakini punde si punde kimya hicho kilitoweka mtu mwingine naye akatoa wazo lake, alisema "Kumfukuza huyu mtu sio suruhisho, kwa sababu ni kama tutakuwa tumempa nafasi ya kutuchafua huko alipo hata ikiwezekana kutochongea kwa jeshi la polisi. Kwahiyo cha kufanya ni kumuuwa tu", Kayumba alistuka kusikia maneno hayo ambayo Boko na watu wake walikuwa wakiyaongea. Ilikuwa ni njama ambayo walikuwa wakiipanga wakiamini kuwa hakuna anayewasikia.

"Safi sana", Boko aliunga mkono wazo hilo la kumuuwa Edga.

"Au mnaonaje?..", aliuliza Boko.

"Hakuna tabu"

"Hakuna shaka"

"Ndivyo kabisa", walisikika kwa sauti tofauti tofauti vijana hao wakiunga mkono suala la kumuua Edga.



Kesho yake alfajiri, Edga alimuamsha Kayumba kwa dhumuni la kumuga akitaka kuelekea kwenye mihangaiko yake ya kila siku.

"Kayumba Kayumba", aliita Edga. Kayumba alikurupuka kutoka usingizini.

"Abwanaee! Kumekucha sasa. Mimi naingia mtaani kusaka tonge", alisema Edga wakati huo akiwa amesimama. Kayumba alinyanyuka akajinyooshea kisha akajibu "Sawa braza. Lakini bado nahitaji msaada wako kaka!.."

"Msaada gani sasa? Inamaana hujaona kama tayari umeniponza?Kayumba umeshavuruga kambi ninacho kuomba fuata ustarabu wako", alifoka Edga.

"Tazama kila mmoja ameshaondoka kuelekea katika mihangaiko yake, mimi tu ndio nimebaki. Kosa langu kukutaarufu kuwa natoka? Na jana situlikubaliana kuwa leo utajua ustarabu wako? Haya nini tena unataka kutoka kwangu!..", aliongeza kusema Edga. Maneno hayo aliyaongea huku akimtazama Kayumba kwa macho ya hasira kiasi kwamba ilimpelekea Kayumba kuwa mnyonge maradufu. Na alipokwisha kumwambia maneno hayo, alizipiga hatua kuondoka zake huku Kayumba akiishia kumtazama tu,moyo wake nao ukimshawishi amwambie Edga juu ya kile alichokisikia usiku wa jana. Ndipo kwa sauti ya upole Kayumba alipasa sauti kumuita Edga, kijana Edga hakugeuka mpaka pale alipoitwa zaidi ya mara mbili "Unasemaje?..", aliuliza Edga mara baada kumgeukia Kayumba. Kwa masikitiko, Kayumba akasema "Ahsante sana kwa msaada wako kijana mwenzangu, lakini nitakuwa mchoyo wa fadhila endapo kama nitashindwa kukueleza kile kinachoendelea nyuma ya pazia",alisema Kayumba, maneno ambayo yalimstua sana Edga hima alimsogelea Kayumba kisha akamuuliza "Unamaana gani kusema maneno hayo?.."

"Edga, kifo kipo mkononi mwako. Jamaa zako wamepanga wakuuwe,mipango yao waliipanga usiku walipotoka kazini wakati huo ulikuwa umelala. Tafadhali usipuuze", alijibu Kayumba, kisha akayafuta machozi yake. Roho ilimuuma sana, aliamini kuwa huwenda Edga akawa msaada wake katika jiji hilo la Dar es salaam,jji ambalo limejaza kila aina ya maisha. Lakini pia mbali na suala hilo, maumivu ya kile alichokumbana nacho kutoka kwa Catherine bado yaliutesa sana moyo wake hali iliyopelekea kutokwa na machozi. Na wakati Kayumba akiwa katika hali hiyo ya majonzi, upande wa Edga alionekana kuduwazwa na maneno ya Kayumba. Alishusha pumzi ndefu, akainua uso wake kutazama juu. Akakumbuka.

**********

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Edga, kuna dili lipo mbele yetu. Unatakiwa ukachukue nyaraka kwenye nyumba ya Mr Omon. Hili ni dili kubwa sana, na sisi tumekuteua wewe ili ulikamilishe..", alisikika akisema Boko kiongozi wa kundi,maneno hayo alikuwa akimwambia Edga.

"Hii nyumba ngumu sana, kuingia na kutoka pia. Hivyo basi umakini unahitajika ili dili hili liweze kulikamilisha. Kila sehemu kuna ilinzi, tena ulizi madhubuti", aliongeza kusema.

"Lakini nitawezaje wakati mimi bado mgeni katika mambo haya? Ni heri tungeshirikiana hata wawili braza", alijibu Edga kwa sauti ya woga. Boko alikasirika kusikia maneno hayo, alimtazama kwa hasira kisha akasema "Usinipangie kazi, unataka kusema miezi hii mitatu uliyojiunga nasi bado hujazoea? Hiki ni kipimo cha maisha, na kuishi ni kuchagua siku zote ukitaka kuruka sharti uagane na nyonga".

"Hapana bro, kwa hilo sipo tayari", alikacha Edga, akikataa agizo la kiongozi wake, kitendo ambacho kilimkera sana Boko. Na tangu siku hiyo maelewano baina yake na yao yakawa ya kususua huku kwa mara kadhaa wakimtenga kwenye ufanyaji wao wa kazi.

Alishusha pumzi Edga baada kuyakumbuka hayo, alitikisa kichwa ishara ya kukubali jambo fulani wakati huo huo akaikumbuka na ile ndoto ambayo aliota akizikwa mzima mzima huku muhusika mkuu katika ndoto hiyo akiwa Boko ambaye alishirikiana na watu ambao hakuwafahamu. Mapigo ya moyo wake yalimuenda mbio, kijasho chembamba kilimtoka. Na hapo ndipo alipoamini kuwa kweli kifo u mkononi mwake wakati wowote, na hivyo hana budi kumfukuza Kayumba. Aliona ni heri aungane naye wakajenge maskani nyingine wakiwa pamoja, alihisi Kayumba ni zaidi ya ndugu na hivyo alimkimbilia ili amuombe msamaha huwenda akawa mkosefu juu yake.

"Braza..braza..braza", Edga alipasa sauti kumuita Kayumba huku akimkibilia, lakini Kayumba hakugeuka na wala sauti hiyo hakuweza kuisikia,mawazo yake yote alikuwa akimuwaza Catherine mwanamke wa ndoto yake aliyempenda kwa dhati ambapo alidiriki kumsomesha akiamini kuwa hiyo ndio zawadi pekee anayostahiri. Ila wakati Kayumba akiwa kwenye dimbwi hilo la mawazo, punde alizinduka baada kuguswa bega. Alisimama kisha akageuka nyuma ghafla ilimuona Edga.

"Samahani sana Braza Kayumba,naomba usiondoke ", Aliongea Edga huku akitaharuki kumuona Kayumba uso wake ukiwa umechoshwa na machozi, aliamini kuwa huwenda kitendo cha kumtaka aondoke maskani kwao ndicho kimempelekea amwage machozi na hata asijue kuwa Kayumba anasiri nzito ndani ya moyo wake. Hivyo pumzi alishusha Kayumba mara baada kuyasikia maneno hayo ya Edga,kisha akasema "Edga..Edga..moyo wangu unaumia macho yangu yanavuja machozi juu ya yale maumivu ninayo yahisi. Kayumba najiuliza nimemkosea nini Mungu. Lakini Kuna wakati najiona mimi ni fungua kukosa, sina budi kukubaliana na kila hali. Ahsante sana kwa msaada wako braza sasa acha nikafie mbele ya safari",alisema kwa uchungu Kayumba huku machozi yakimbubujika mikono nyuma uso akiwa ameinamisha chini aliondoka zake!



Kayumba akiwa katika hali ya huzuni na majonzi aliondoka huku akimuacha Edga amesimama akimsindikiza kwa macho,lakini moyo Edga hakuwa tayari kumuacha Kayumba aondoke, alijua fika kijana huyo hana mahali pakuishi mjini na hivyo kwa mara nyingine tena alikimbilia na kisha kusema naye akimuomba waungane kuwa kitu kimoja ili waendeshe maisha mbali na kundi lile lililo chini ya Boko.

"Kayumba braza, ukweli sipo tayari kukuruhusu uondoke. Wewe ni kama ndugu sasa, kwa maana hiyo nataka tuwe kitu kimoja. Mjini maeneo ni mengi sana, vile vile kazi ni nyingi pia", aliongea Edga mara baada kumfikia Kayumba.

"Tufanye hivyo Kayumba, kwa kile ulicho nieleza kamwe sipo tayari kurudi kambini. Wale ni watu wabaya", aliongeza kusema Edga,ikwa wakati huo Kayumba akimtazama tu pasipo kuongea neno lolote. Baadaye Kayumba alishusha pumzi kidogo kisha akajibu "Mimi sijasoma, itawezekana vipi kupata kazi?.."

"Kayumba..", aliita Edga kisha akasema "Kila mtu na riziki aliyoandikiwa, sio kila aliyefanikiwa amesoma lahasha. Unaweza usiwe na elimu yoyote lakini ukapata mafanikio makubwa kuliko yule mwenye elimu. Wangapi hawana elimu ila wanawaajiri wanye elimu zao? Utakuta mtu kasoma mpaka macho yamepovuka ila pesa hana! Na vile vile utakuta mtu elimu ziro lakini utajiri alio nao moto wa kuotea mbali. Amini nakwambia braza, kusoma sio kupata kazi. Kwa maana hiyo basi, mimi na wewe ni wasaka tonge, tupambane tutumie nguvu zetu kusaka tonge...",alisema maneno hayo Adga akimuasa Kayumba ilihali muda huo Kayumba alionekana kuinamisha uso wake chini kana kwamba kuna jambo alikuwa akilitafakari. Punde aliinua uso kisha akajibu " Sawa kaka nimekubali ", hakika lilikuwa ni jibu ambalo lilimpelekea Edga kuonyesha tabasamu, alimpokea Kayumba begi kisha akasema "Hakuna kukata tamaa, kwani wao wana nini na sisi tuna nini mpaka tushindwe". Edga alipokwisha kusema hivyo alishikana mkono na Kayumba wakagongeana mabega kisha wakaondoka. Sasa walau furaha inamrejea kijana Kayumba, jambo la kupata rafiki ndani ya jiji la Dar es salaam inampelekea kuwa na amani kidogo ndani ya moyo wake tofauti na hapo awali alivyokuwa akifikiria namna ya kuishi baada Catherine kumkana. Ni saula ambalo lilimfanya kumshukuru Mungu, na sasa aliweka mikakati ya kusaka pesa ili apate nauli ya kumrudisha kijijini kwao akaendelee na maisha ingawaje ilimuwea ngumu kumsahau Catherine gaidi wa moyo wake. Kila leo Kayumba alikumbuka Catherine, ni maumivu makali sana ambayo alihisi huku akitamani siku yoyote amsahau ili moyoni awe na amani.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Hii maskani ni nzuri sana, vile vile kuna utulivu wa kutosha. Hapa panatufaa sana kwa kuanza maisha mapya ingawa jambo la kuzingatia ni kuwahi kuamka ili tusiwe kero kwa mwenye duka", alisikika akisema Edga,maneno hayo alikuwa akimuasa Kayumba baada kufurahishwa maskani mpya walionzisha kwenye moja ya duka Kinondoni.

"Ni kweli Edga, na sitochoka kukushukuru kwa wema wako",alisema Kayumba kwa sauti ya chini huku mkono ukiwa shavuni.

"Ahahahaha.. Hahahahah", Edga aliangua kicheko kisha akasema "Hilo ni jambo la kawaida Kayumba, vile vile hata mimi nastahiri kukushukuru kwa sababu mpaka sasa nadhani nisingekuwa duniani. Kifo kilikuwa karibu yangu,na laiti usingeniambia basi ningezidi kuwaamini wale watu, kitendo ambacho kingenipelekea kifo. Aah! Kayumba. Tuachane na hayo, kitu ambacho mimi sijafurahishwa nacho kutoka kwako "

" Kitu gani Edga?.. ", alihoji Kayumba wakati huo akitoa mkono shavuni. Edga akajibu." Muonekano wako, tangu siku ya kwanza tuonane uso wako hujawahi kuonyesha tabasamu kwa muda mrefu. Kwa maana hiyo unaonyesha moyo wako unasiri kubwa mno, vipi unaweza kunieleza kinacho kusibu?.."

"Aah, Edga. Ni kweli upo sahihi, ni story ndefu sana lakini kwa sasa hebu tuzungumze kuhusu maisha. Hasa hasa kazi ya kufanya"

"Vizuri, acha hilo suala tuliweke kiporo kwanza. Siku tukiwa na nafasi basi utanijuza.."

"Shaka ondoa", aliunga mkono Kayumba. Ndipo Edga alipoanza kuzungumza uwezekano wa kupata kazi. Aliwaza hili na lile, mwishowe alishusha pumzi ndefu akamtazama Kayumba kisha akamuuliza "Hivi kubeba zege unaweza?.."

"Bila shaka, mimi ni mwanaume Edga inanibidi nipambane ili mkono uende kinywani", alijibu Kayumba. Maneno hayo yalimfurahisha sana Edga ambapo alimpigia piga Kayumba kunako bega huku akisema "Hayo ndio maono ya mwanaume,mwanaume hasifiwi kula bali anasifiwa kazi. Basi kesho twende sehemu moja hivi, najua pale hauwezi kukosa kazi",

"Ni kazi ngumu ila nina imani utaiweza", aliongeza kusema Edga kisha wote kwa pamoja wakafurahi wakagongeana tano, na mara moja safari ya kusaka lepe la usingizi ilianza ambapo wawili hao walilalia mabox huku pasipo na shuka.

Usiku ulikuwa wa tabu sana kwa kijana Kayumba hasa pale anapoyatuliza mawazo yake, sura ya Catherine ilimjia mara kadhaa pindi alipoyafumba macho yake. Jambo hilo lilimpa shida ingawaje alitamani sana siku moja aweze kumsahau, akiamini kuwa endapo ikMitokea siku hiyo atafurahia maisha daima. Lakini baadae alipitiwa na usingizi, aliamka alfajiri mapema baada Edga kumuamsha.

"Kumekucha kaka", aliongea Edga huku akiliweka pema box lake la kulalia.

"Mmh, ni siku nyingine sasa", alijibu Kayumba wakati huo akizinyoosha mbavu zake kwa kujipinda kulia na kushoto mbele na nyuma. Zoezi hilo lilipo kamirika, naye alilihifadhi mahali pema box lake kisha akasema "Nipo sawa, tuondoke zetu"

"Ahahahah...hahahaha..", aliangua kicheko Edga, maneno ya Kayumba yalimfanya afurahi. Alipoakatisha kicheko chake akasema "Nakukubali sana braza", Edga alipokwisha kusema hivyo safari ya kwenda kusaka tonge ikaanza. Wawili hao walitembea kutoka Kinondoni mpaka Kawe, huko walipata kibarua cha kubeba zege kwenye moja ya mradi wa kujenga gholofa uliokuwa ukifanyika. Vijana wengi walionekana wakichakarika, wapo waliokuwa wakichanganya zege na wengine wakibeba vile vile wengineo wakijenga. Ni kazi ambayo ilionekana kuwa ngumu sana, kiasi kwamba ilimfanya Kayumba kushusha pumzi huku akijishauri mara mbili mbili uwezekano wa kuweza kuifanya kazi hiyo.

"Nitapambana hakuna namna", aliapa Kayumba ndani ya nafsi yake wakati huo huo ilisikika sauti ikisema "Edy naona kwa sasa umeokoka, au mambo yamekua magumu?.."

"Ahahahaha.. Acha zako bwana", alijibu Edga akianza kwa kuanguka kicheko.

"Hujui tu, ila kitambo nilikuwa najua kazi yako na wenzako, ila ukweli ni kwamba yale sio maisha. Kifo kilikuwa karibu yako, jasho la mtu haliliwi Braza", aliongeza kusema mtu huyo, akimwambia Edga. Dhahiri shahili alifahamu fika Edga na ndio maana alikuwa akimueleza masuala hayo ambayo yalimpelekea Edga kuishia kucheka. Punde si punde sauti nyingine ilisikika ikitoa amri. Ilisema "Huu muda wa kazi, maongezi baadaye"

"Sawa kiongozi", mtu huyo aliyekuwa akisema na Edga alitii amri kisha akaendelea kuchakarika kama ilivyo kwa Kayumba na Edga ambao nao walianza kazi kwa kasi na nguvu ya hali ya juu.

Jioni ilipowadia kila mmoja alipata ujira wake, shilingi Elfu tatu. Na sasa walirejea maskani ingawaje kila mmoja alikuwa hoi bin'taabani hasa hasa Kayumba. Alilalama maumivu kila sehemu ya mwili wake, ilichoka sana siku hiyo jambo ambalo lilimpelekea kutokurudi kazini siku iliyofuata na wala Edga hakuweza kumuwekea kinyongo kwani alitambua fika kijana mwenzake hana uzoefu wa kazi hizo. Siku iliyofuata Kayumba alijihisi kuwa shwari, nguvu na uchovu walau ulipungua na hivyo aliona ni vema akiendelea kusaka tonge huku kichwani akiwa na malengo ya kurudi nyumbani kwao baada kuona alichofuata mjini kimekwenda kombo.

"Mwili wangu sasa upo safi kabisa. Ukweli ile kazi ni ngumu sana asikwambie mtu", alisikika akisema Kayumba,wasaa huo ilikuwa yapata saa nne usiku.

"Hahahaha..", Edga alicheka kisha akasema "Kabisa, yani hapa mwili wangu umechoka mithiri ya samaki aliyechina. Ila nimepata wazo"

"Wazo gani?.", alihoji Kayumba wakati huo akionekana kuwa makini kumsikiliza swahiba wake. Edga akajibu "Ngoja kwanza nikanunua chakula kwa mama Zamoyoni halafu nije nikukwambie". Edga alinyanyuka kisha akazipiga hatua kuelekea mgahawani kunua chakula, alinunua na maji kisha akarejea maskani. Wawili hao waliketi na kuanza kula, huku zogo mbali mbali nalo likitawala.

"Enhee nipe maneno sasa", aliongea Kayumba.

"Wazo langu ni kwamba tubadirishe upepo, nikiwa na maana kwamba ile kazi ya kubeba zege tuachane nayo. Tutafute kazi nyingine, hata ya kuosha magari nayo pia sio mbaya aidha kazi ya ukuli"

"Kweli hilo wazo nzuri sana, unaaakili mno ", aliunga mkono Kayumba. Kicheko kilizuka baina yao kisha wakagongeana tano, na sasa walilala wote wakiwa na dhamila moja tu.

Kesho yake palipokucha, Edga alimuamsha Kayumba wakaanza safari ya kusaka kazi. Mabibo sokoni walifika, ujanja ujanja wa kijana Edga ulipelekea kukubaliwa kuungana na wabeba mizigo wa ndani ya soko hilo. Na ndipo walipoanza kufanya kazi,istoshe siku hiyo ilikuwa siku njema upande wao, sokoni yalifurika maroli kibao yaliyo sheheni mizigo ambayo ilitakiwa kushushwa. Kayumba alichakarika kwa nguvu zote, mwili wake ulioonyesha kuwa wa mazoezi aliutumia ipasavyo mpaka pale alipojihisi kuchoka ilihali jua tayari lilikuwa likitoweka kwa maana hiyo jioni iliwadia. Walipokea ujira wao wasaka tonge hao kisha safari ya kurejea maskani ikaanza. Lakini wakati wapo njiani, mara ghafla Kayumba alipigwa na butwaa baada kumuona mrembo akizipiga hatua kuelekea kwenye moja ya duka huku nyuma akiwa ameacha gari lake hatua kadhaa. Kayumba alimkodolea macho mrembo yule huku macho yake yakitia shaka kuwa huwenda amemfananisha na sasa alingojea ageuke ili amtazame. Punde si punde mrembo yule alirejea, na hapo ndipo Kayumba alipogundua kuwa macho yake yapo sahihi. Kwenye kiza totoro alipata kumuona Catherine akilisogelea gari wakati huo huo kabla hajalikaribia gari hilo, ndani alitoka mwanaume ambapo walikumbatiana huku kwa macho yake Kayumba akishuhudia. Roho ilimuuma sana, machozi hayakuwa mbali kumtoka ilihali muda huo huo Edga alipasa sauti kumuita.

"Kayumba.. Kayumba..hebu tuondoke bwana", aliita Edga huku akisogea mahali aliposimama Kayumba.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Kayumba..", alipomkaribia alimuita kwa mara nyingine tena, na hapo ndipo Kayumba alipoyaondoa macho yake yaliyokuwa yakiisindikiza gari la Catherine, na sasa alimgeukia rafiki yake huku akiyafuta machozi. Edga alitaharuki kumuona Kayumba akilia machozi, lakini wakati akiwa kwenye hali hiyo ya taharuki,kwa sauti ya majonzi Kayumba alisema "Hivi nimemkosea nini mimi Catherine?..Kosa langu ni mimi?.."

"Catherine?..", alizidi kutaharuki Edga juu ya maneno hayo aliyoongea Kayumba.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog