Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

PENZI CHUNGU - 5

 





    Simulizi : Penzi Chungu

    Sehemu Ya Tano (5)





    Mwandishi wa habari Veronica Baro ndiye mtu aliyenifanya niamini kuwa Suto ni muuaji ! Aliandika kila siku ubaya kuhusu Suto Sutani, tena kwenye kurasa ya mbele, alimpa Suto sifa zote mbaya unazozijua wewe, Suto jeuri, Suto kiburi, Suto muuaji, nami nikaamini bila kufanya uchunguzi wowote, mbaya zaidi nikaanza kumchukia Suto Sutani, mpenzi wangu.

    Nilimwacha Suto akiteseka gerezani, nilimwacha mwanamke niliyempenda zaidi duniani akinyanyasika gerezani, namini nikaingia katika mikono ya mibaya, mikono ya baradhuli, mikono ya shetani!

    MANKA.

    Nilimsahau kabisa Suto Sutani na kuangukia katika mikono michafu ya Manka. Sikujua, sikujua, sikujua, kumbe Manka hakuwa mwanamke, Manka alikuwa ni nyoka, nyoka mwenye sumu kali sana ! Ninaposema Manka alikuwa shetani namaanisha!.

    Wazazi wangu, wakishirikiana na huyo mshenzi aliyetoka hapa, eti mwandishi wa habari mahiri nchini Tanzania, Veronica Baro...... Walinitoa peponi na kunipeleka motoni! Wakati penzi langu na Suto Sutani lilikuwa tamu sana, penzi tamu sawa na zile hadithi nzuri za wale wanawake wa peponi. Penzi langu na Manka lilikuwa chungu sana, chungu mithili ya mwarobaini!

    Naweza sema penzi langu na Manka lilikuwa ndio penzi baya zaidi kuwahi kutokea hapa duniani.

    Nilifaidi penzi la Manka siku tatu tu za awali, baada ya hapo yalikuwa mateso, yalikuwa manyanyaso" Bruno aliacha kuongea na kumwangalia Daniel usoni. Aliridhika na umakini na utulivu aliokuwa nao Daniel Mwaseba. Utulivu ambao aliusoma sana vitabuni, lakini leo alikutana nao.



    "Hivi Daniel unaweza ukaamini ndani ya wiki moja nilimfumania Manka na wanaume watatu tofauti?http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Manka alikuwa kahaba, tena kahaba wa kimataifa!

    Daniel! Sitaki kuikumbuka juzi, sitaki kuikumbuka, sitaki kabisa....aaah juzi Manka ndio alinionesha yeye ni mnyama kiasi gani...aibu kusema lakini Manka alinifanyia kitu kibaya sana, unastahili kufa Manka. Tena kifo kibaya sana, Manka siyo binadamu kabisa, nakwambia Manka ni mbwa Daniel "

    Sauti ya Bruno ilipanda juu, mpaka meza za jirani walikuwa wanakisikia anachosema huku wakigeuka kumuangalia mzungumzaji.

    "Juzi alikufanyaje Manka?" Daniel Mwaseba aliuliza kwa sauti ya upole.



    Bruno alilia kwa sauti kubwa. Watu wote walishangazwa pale baa. Wengine wakidhani labda pombe imemzidia. Daniel akajua kuna jambo kubwa sana ambalo Bruno alifanyiwa. Nae akazidi kupata kimuhemuhe cha kukitaka kukijua hiko kitu.

    "Usilie kaka, ni nini tatizo? Punguza jazba"

    Sasa Bruno aliyaacha machozi yambubujike, hakujishughulisha kabisa kuyafuta, Bruno hakuyahofia macho na masikio ya walevi, waliomakinika kwa kumtazama. Kwa sauti ya kwikwi Bruno alisema kitu kilichomshangaza sana Daniel.



    "Manka alikuwa ni shetani!

    Babaaa...baba naye alikiwa ni ibilisi, ndiyo baba yangu mzazi alikuwa ni ibilisi. Sioni aibu na wala siogopi kusema kuwa baba yangu ni miongoni mwa baba wabaya kabisa duniani!" Bruno aliacha kuongea, aliangalia juu kwa muda. Alikutana na taa nzuri za rangi ya bluu, ziking'inia juu ya mgahawa ule.



    "Walifanyaje hao Bruno" Daniel aliuliza akiwa na kihoro kikubwa cha kutaka kujua.

    Bruno alitulia kama dakika tano, akilia huku akiiangalia ile taa ya bluu, baadae Bruno alinena kwa utulivu sana.



    "Nakumbuka juzi nilitoka Chuo saa kumi na mbili jioni. Niliamua Kupitia kwa mpenzi wangu Manka kabla sijaenda nyumbani. Nilifika nyumbani kwa Manka, lakini nilikaribishwa kwa namna tofauti na niliyoizoea , nilikaribishwa na sauti za malalamiko ya Manka nilipofika tu mlangoni. Manka alikuwa analalamika, Manka alikuwa analiaaaa"

    Bruno alianza kulia tena. Daniel alinyanyuka na kwenda kusimama pembeni na alipokaa Bruno. Alimpigapiga mgongoni, na kumshika bega. Alimnyanyua na kutoka nae nje ya ule mgahawa. Kule nje waliingia katika gari aliyokuja nayo Bruno. Daniel alikaa kwenye usukani. Wakati Bruno alikaa katika kiti cha pembeni ya dereva. Kabla hajaulizwa Bruno aliendelea kisimulia.

    "Nilizunguka nyuma ya dirisha. Ilikuwa ni bahati mbaya kwao hawakukumbuka kushusha panzia...niliwaona....niliwaona Daniel..." Bruno alikuwa anaongea huku anapigapiga mapaja yake kwa mikono yake yote miwili.



    "Baba alikuwa juu, mpenzi wangu Manka alikuwa chini. Walikuwa wanafanya mapenzi Daniel !

    Baba alikuwa anafanya mapenzi na mkwewe, ilikuwa ni picha mbaya sana kuwahi kuitazama katika maisha yangu, Manka wangu na baba yangu mzazi walikuwa wananisaliti ! Ulinipata uchungu mkali sana Daniel, hakuna uchungu duniani kama uchungu wa penzi, Penzi Chungu sana usiombe Daniel. Machozi yalinitoka siku ile, nililia pale dirishani kama mtoto mdogo. Manka alikuwa analia mle chumbani, mimi nilikuwa nalia pale nje, sote tulikuwa tunalizwa na baba !

    Nilijua nitazimia, lakini sikuzimia. Nilishikwa na hasira sana siku ile. Nilitoka kwa kasi pale na kuelekea nyumbani. Nilikoswakoswa kugongwa na magari njiani mara kadhaa. Sikuwa na umakini kabisa. Mapenzi huuwa Daniel, nakwambia mapenzi yanauwa Daniel, unaelewa ninachokwambia? Ushawahi kupenda wewe? Ushawahi kuumizwa na mapenzi wewe? Fikiria unasalitiwa na baba yako mzazi! Fikiria Daniel !

    Siku ile nilijua baba ni nguruwe, lakini sikujua kabisa kama mama yangu alikuwa mbango...aaaah kumbe baba yangu ni Nguruwe na alimuoa mwanamke ambaye naye ni Mbango. Siyo kama nawatukana wazazi wangu, hapana!

    Siyo kama siwapendi wazazi wangu....hapana! Nawapenda sana wazazi wangu, lakini wacha niwe tu mkweli wazazi wangu ni watu wa ajabu sana. Wazazi wangu ni zaidi ya wanyama Daniel...



    Nilipofika mlangoni nyumbani, nilisikia kelele za malalamiko, kelele sawa na nilizozisikia nyumbani kwa kina Manka. Sauti, sauti, sautiiii za malalamiko..." Bruno alianza kulia tena. Kwa bahati mbaya Daniel hakuwa mbelezaji mzuri. Alikuwa anamwangalia tu jinsi Bruno akivyolia.

    Baada ya kulia na kutosheka, Bruno aliendelea kusimulia.

    "Kulwa, Kulwa, kulwa ....ndio neno kuu niliokuwa nalisikia mle ndani. Sauti iliyokuwa inatokea puani kwa mama yangu mzazi. Sauti ilikuwa inamaanisha Mama alikuwa anafanya mapenzi na mwanaume akiyeitwa Kulwa. Nilitamani tena kuzimia lakini nashangaa sikuzimia.

    Niliondoka kwa hasira kubwa sana, na kuelekea kwa rafiki yangu Magomeni, rafiki yangu wa siku nyingi sana, alikuwa anaitwa Dotto. Nilisoma nae kidato cha tano na cha sita katika Sekondari ya Benjamini Mkapa. Nilijua huko labda nitapata tulizo.

    Niliyoyakuta !



    Nilimkuta Dotto amekaa sebuleni, na mwanadada mmoja. Nilipofika tu yule mwanadada aliaga na kuondoka. Baada ya kuondoka yule dada, Dotto aliniuliza kama yule namfahamu, nilimjibu hapana, jibu alilonipa liliniacha hoi sana. Nilitamani nimkimbilie yule dada ili anijibu maswali yangu kadhaa niliyokuwa nayo juu yake, lakini sikuwa na jinsi, Dotto angenielewaje?..umemjuana nae vipi yule dada Dotto?". Nilithubutu kumuuliza.

    " Tuna kazi ya kufanya na Veronica Baro. Kazi ambayo ina maslahi makubwa sana"

    "Huwezi kunambia Dotto rafiki yangu hiyo kazi?"

    "Kuna kazi ndogo sana ya kumuua kidudu mtu, si unajua kazi zetu kaka?"

    "Anaitwa nani huyo kidudu mtu Dotto?"

    "Anaitwa Suto Sutani !"



    Nilibaki mdomo wazi Daniel.



    Dotto alinieleza kila kitu kuhusu mbinu zao chafu, mbinu chafu zilizosababisha Suto Sutani aende jela bila hatia yoyote. Mama yangu mzazi alitumia pesa zake vibaya, Veronica Baro alitumia kalamu yake vibaya, Kulwa, Dotto na Dungu walitumia nguvu zao vibaya. Manka Edward alitumia uzuri wake vibaya. Walitumia vibaya ili kuhakikisha Suto Sutani anafungwa maisha, au Suto Sutani anauwawa!.



    Dotto alinisimulia bila kujua kama mimi nilikuwa mhusika mkubwa sana katika mambo yale aliyokuwa ananisimulia. Hapo ndipo nilipoweka kisasi kwa mama yangu mzazi, kisasi kwa baba yangu mzazi, kisasi kwa Kulwa, Dungu na Veronica Baro. Mwandishi niliyetaka kumuua masaa machache yaliyopita.



    *****



    Huko Mwenge hoteli kwa Suto Sutani, Suto alipumzika vya kutosha, usiku ulovyoingia Suto Sutani alitoka nje kupata mlo wa usiku. Alipotoka nje alipata wazo, alitafuta duka na kununua kanga zingine. Alizivaa kanga palepale dukani. Ile laki mbili ilikuwa inamlinda bado. Alirejea kule hotelini na kuingia Mgahawani, alikaa katika Mgahawa mkubwa wa hoteli ya Ocafona inn, huku akimsubiri Mhudumu amwagizie chakula. Aliangaza watu waliokuwemo katika hoteli ile, alimwona!. Alimwona yule askari polisi aliyemuingiza kwenye gari kwa nguvu siku ile ya kwanza Suto kuingia selo. Yule askari aliyemwangalia kwa jicho la hasira wakati Suto Sutani akiingizwa katika gari la polisi.



    Bila kujua kama kaikaribia hatari, askari yule akiwa na mwanamke mmoja pale mezani wakinywa sharubati na vibanzi. Nia ya Suto Sutani ilikuwa ni moja tu, kumfundisha yule askari madhara ya msukumo ule aliomsukuma Suto kwa nguvu kumuingiza ndani ya gari la Polisi. Suto alimuona Mhudumu wa mgahawa ule na kumuita kwa ishara ya mkono. Mhudumu alienda na Suto Sutani alimuagiza mchemsho na maji makubwa. Aliletewa na kuanza kula taratibu. Huku akimwangalia yule askari mara kwa mara. Mara, yule askari alinyanyuka, alikuwa anaelekea maliwatoni. Suto Sutani nae alinyanyuka, alibeba begi lake lenye visu, na kuelekea maliwatoni nae, kulekule alikoelekea yule askari....



    Askari alienda kwa mwendo wa kasi maliwatoni, mwendo ukioashiria alibanwa sana na haja ndogo. Alifanya kosa kubwa sana askari yule, aliingia ndani ya choo bila kufunga mlango. Askari alifungua zipu ya suruali yake, hakumaliza alichotaka kufanya, askari alipatwa na mstuko mkubwa sana, mle maliwato walikuwa watu wawili sasa. Alipata ugeni, ugeni wa Suto mtoto wa Sutani. Askari akiwa kashika zipu ya suruali yake macho yalimtoka!

    Hakuamini.

    Hakutegemea.

    Suto alitabasamu kidogo, kisha alimuuliza yule askari.

    "Unanikumbuka?"

    Askari hakujibu.

    "Naitwa Suto Sutani!"

    Kutajiwa jina hilo, mkojo wa yule askari ulitoka kwa kasi, alijikojolea jamaa.

    Suto Sutani hakujali ule mkojo, na wala hakujisumbua kuuangalia mkojo ule. Yeye alikuwa makini akiungalia uso wa askari yule. Uso uliotaharuki sana.



    "Hivi hujui kumpandisha Mtuhumiwa ndani ya gari kistaarabu? Kwanza unajua maana ya Mtuhumiwa? Au wewe Mtuhumiwa unamchukulia kama mhalifu kamili. Nilikuwa Mtuhumiwa, ukanifanyia vile, ulinisukuma vibaya sana, unakumbuka Askari? Hivi nikikukosea nini mimi?



    Swali hilo liliamsha kitu, kwa mara ya pili Askari ulimtoka tena. Sijui kama huu mkojo wa sasa kama ulikuwa umebakia toka ule wa mwanzo au ulikuwa mpya. Lakini Askari alijikojolea tena mbele ya Suto Sutani.

    " Kumbe mwoga sana askari, hahaha, acha uwoga askari, sikuuwi, kosa lako halistahili kifo. Nitakupa adhabu ndogo tu Askari, hapana siyo adhabu, hizi ni salamu zangu kwenda kwa Inspekta Jasmine Wahabu. Naomba mkono wako..."

    Huku akitetemeka askari alinyoosha mkono wake na kumpa Suto Sutani. Sijui alikitoa muda gani, sijui alikata muda gani, lakini kidole gumba cha mkono wa kulia cha yule askari kilikuwa kinarukaruka katika sakafu chafu za choo, damu zilikuwa zinambubujika Askari mkononi !.



    "Hizo ni salamu zangu kwa Inspekta Jasmine"



    Suto alisema na kutokomea gizani, akimwacha askari akipiga kele kule maliwatoni..





    Wateja wa Ocafona inn walijaa kule chooni. Wakimwangalia yule askari akibubujikwa damu mkononi. Huku akipiga makelele na kulitaja jina la Suto Sutani.

    Ilikuwa hekaheka!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Meneja wa hoteli ya Ocafona inn, alipiga simu kituo cha Polisi kuwajulisha taarifa ile mbaya. Baada ya muda mfupi Polisi waliwasiri pale hotelini, na kuchukua maelezo juu ya taarifa ile. Wote walibaki mdomo wazi, kusikia athari ile ililetwa na Suto Sutani. Askari yule alikimbizwa hospitali, Mwananyamala huku msako mkubwa sana ulianza pale Mwenge na vitongoji vyake. Wakazi wa Mwenge nao waliipata hekaheka ya msako wa Suto Sutani. Lakini Suto Sutani hakuonekana, ilikuwa ni kama hakuwahi kufika Mwenge.



    Yule askari aliyejeruhiwa alipelekea hospitali, askari alitibiwa kidonda chake. Kidonda kilifungwa na alipumzishwa kwa muda. Muda wote yule askari alikuwa analia huku akimtaja Suto Sutani.



    Taarifa za kukatwa kidole yule askari zilimfikia Inspekta Jasmine akiwa nyumbani kwake. Na aliambiwa kwamba kidole hiko kilikuwa ni salamu zake. Inspekta Jasmine aliipokea taarifa hiyo siyo kwa mstuko mkubwa sana, kwa kuwa alikuwa na sehemu ya kuyahamishia matatizo yale, moja kwa moja alimpigia simu Daniel Mwaseba, na kumwambia salamu zile mbaya zilizotoka kwa Suto Sutani. Kama alidhani atasikia mstuko toka kwa Daniel, alifeli. Daniel hakustuka kabisa. Walipanga kukutana usiku uleule kuweka sawa mipango yao.



    Wakati akiwaachia vumbi askari wa Mwenge baada ya kumkata kidole yule askari kama salamu zake kwa Inspekta Jasmine, Suto Sutani sasa alikuwa Tegeta.



    Suto Sutani alikuwa Tegeta amekaa kwenye kibanda kimoja cha mshona viatu. Suto Sutani ilimshangaza sana kumuona fundi yule akifanya kazi usiku. Ilikuwa ni nadra sana kwa fundi viatu kushona viatu usiku jijini Dar es salaam. Eneo lile kulikuwa na mwanga hafifu ukioangazia sehemu ile. Alitulia kwenye benchi kama anasubiri huduma pale, au anamsubiri mtu pale. Suto Sutani alikaa kimya huku akishuhudia vijana wakicheza mchezo wa draft.

    Suto alitulia kimya akiangalia vijana wale wakicheza draft kimajigambo makubwa huku wakitupiana maneno ya kejeri.

    Suto aliitathmini sehemu ile na kuona ni sehemu sahihi ya kuupitisha usiku ule. Nyumba ya kulala wageni alikuwa anaziogopa kwa siku ile. Alikuwa anajua walivyo Polisi wa Tanzania. Usiku wa tukio hufanya msako mkubwa sana. Lakini baada ya siku mbili tatu wanaacha. Hilo ndilo lililomfanya Suto Sutani apange kulala pale katika kibanda cha mshona viatu. Huku akichangamshwa na wale vijana wacheza draft.



    "Mimi huniwezi Dula"

    "Si utaona, nakufunga hili"

    "Unajidanganya Dula"

    "Hayaaaaaa nimeingia Suto hiyo, mveshe" Kibondo alisema baada ya kete yake moja kuingia king, alitumia neno Suto badala ya king.

    Kauli ambayo ilimnyanyua Suto pale. Aliona pale siyo mahali sahihi tena. Alinyanyuka na kuondoka bila kuaga. Baada ya dakika kama kumi na tano Suto kunyanyuka pale kwa fundi viatu, waliingia Polisi kwa gari yao kwa kasi kubwa sana. Ilikuwa mshikemshike!

    Polisi walifika palepale kwa fundi viatu...



    Hii sasa shughuli, je SUTO atatoka salama Tegeta?





    "Habari zenu wazee"

    "Salama kaka" Wale jamaa waliitikia huku wakiacha kucheza draft.

    "Aisee kuna msichana mmoja tunamtafuta amejifunika kanga za bluu, chini na juu. Mrefu wastani hivi na ana begi mkononi"



    Wale vijana walibaki vinywa wazi. Sifa zote walizotajiwa zilikiwa ni sifa za dada aliyekuja pale kwa kuwasalimia vizuri lakini kuondoka bila kuaga.

    "Alikaa hapo!" Dula alisema huku akilionesha kwa kidole lile benchi alilokaa Suto Sutani.

    "Una hakika alikuwa hapa, Polisi mmoja alisema huku akiwa na uwoga kidogo"

    "Alikaa hapo na kaelekea kule muda mfupi uliopita"



    Yule Polisi aliongea kwenye radio call kwamba Suto Sutani alikuwa Tegeta. Wale vijana walistuka sana baada ya kusikia Dada waliyekaa nae pale ni Suto Sutani, muuaji hatari sana nchini Tanzania.

    Gari kumi za Polisi kutoka kituo kikuu cha Polisi zilikuwa njiani kuelekea Tegeta. Askari walikuwa wamevaa kivita, zana za kivita, na gari zikiwa kasi hasa kumuwahi Suto Sutani !



    Askari walijipanga sana. Ilikuwa mithili wanaenda kumkamata jambazi mkubwa sana mwenye silaha za kutisha. Kumbe walikuwa wanaenda kukamata kumbe dhaifu kabisa, mwenye silaha dhaifu sana, visu.



    Watu njiani walishangaa sana kasi ya gari zile kumi, zenye wastani wa askari kumi kila moja. Kwa hiyo zaidi ya askari mia moja walikuwa wanaenda Tegeta, Kuhakikisha Suto Sutani anakamatwa.



    Taarifa za kuonekana kwa Suto Sutani Tegeta ziliwafikia pia Daniel na Inspekta Jasmine, nao walijipanga vizuri na kuelekea huko. Ilikuwa iwe isiwe, Suto Sutani lazima akamatwe!



    Zile gari kumi za askari ziliwasiri Tegeta kwa fujo. Askari wote walishuka kabla ya zile gari hazijasimama. Kila mmoja akiwa na bunduki mkononi. Waligawa vizuri, na kila askari akiwa analijua vizuri jukumu lililomleta Tegeta.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    "Kumpiga risasi Suto Sutani kisha kumkamata, na kumuuwa siyo mbaya pia" Ilikuwa ni kauli toka kwa Mkuu wa Operesheni ile. Kamanda wa kanda maalum ya Dar es salaam, Elvis Lema.



    Askari waliingia kazini, huku maneno ya kamanda wao yakiwa kichwani mwao. Askari walitafuta sana, kwenye hoteli , kwenye mabaa, kwenye nyumba za kulala wageni lakini ilikuwa kazi bure. Hawakufanikiwa kumuona Suto Sutani.

    Kwa mara nyingine tena Suto Sutani aliyeyuka!



    Polisi sasa waliuhamishia msako wao mtaani, watembeaji usiku walikoma sana siku hiyo. Ilikuwa ni lazima uhojiwe, na ukijibu kisichoeleweka lazima upigwe kidogo na ikiwezekana uwekwe ndani. Ulikuwa usiku mbaya sana kwa walevi.



    Inspekta Jasmine na Daniel Mwaseba nao walikuwa wanaenda kwa kasi kubwa sana Tegeta. Kwa lengo moja tu, kumkamata huyo Suto Sutani. Mwanamke aliyekuwa anatafutwa mithili ya gaidi kwa sasa.

    Baada ya muda mchache nao walijiunga na wenzao pale Tegeta, walienda kuongeza nguvu, na nguvu iliongezeka hasa. Lakini nguvu hiyo haikusaidia kabisa katika kumkata Suto Sutani.



    Wakati Polisi wakiigeuza Tegeta nje ndani, kumsaka Suto Sutani. Suto Sutani mwenyewe alikuwa katika kituo cha kujazia mafuta kama mlinzi Tegeta ileile.



    Suto Sutani alivyotoka pale kwa mshona viatu, alitembea huku akiwaza wapi itakuwa sehemu salama kwake. Hakutaka kabisa kulala katika nyumba za kulala wageni, alijua huko atakamatwa haraka sana. Suto Sutani aliongoza barabara akienda asikokujua, mara akaiona sheli pembeni mwa barabara, hapo ndipo alipata fikra mpya, fikra ya kuupitisha usiku ule pale sheli, alihisi ni sehemu salama zaidi.

    Alichunguza kwa makini mazingira ya sheli ile. Aligundua kuna mlinzi mmoja tu wa kike. Mlinzi aliyekuwa anasinzia gizani pembeni kabisa mwa sheli ile. Kwa mwendo wa kunyata alimsogelea mlinzi yule wa kike. Pigo moja tu la Suto Sutani aliyebadirika lilimfanya mlinzi yule azimie. Alimburuza hadi kichakani, alimbadirisha nguo, alimvesha nguo zake yake yeye, na Suto Sutani akavaa nguo za kilinzi. Alirudi tena kule sheli na kukaa kiti kile kile cha mlinzi, Suto nae alisinzia.



    Inspekta Jasmine na Daniel walizunguka sana mtaani, mafuta ya gari yao yalipungua, wakaiona sheli. Wakawa wanaelekea kujaza mafuta sheli ileile aliyolinda Suto Sutani.





    Suto Sutani alikuwa bado amesinzia pale sheli. Hakusikia kabisa muungurumo wa gari walilopanda inspekta Jasmine na Daniel Mwaseba. Mhudumu wa sheli ile alienda kuwahudumia kina Daniel Mwaseba.

    "Hivi hii sheli haina mlinzi, mnajua kama kuna hali ya hatari sana Tegeta?" Daniel Mwaseba alimuuliza yule Mhudumu huku akimwangalia usoni.

    "Mlinzi yupo, weee Anithaa!" Mhudumu aliita kwa sauti kubwa.

    Suto Sutani akiwa usingizini aliisikia kwa mbali sauti ikiita jina la Anitha, lakini hakuamka kwa sababu yeye si Anitha. Alisahau kabisa kama yeye kwa sasa alijivika mavazi ya Anitha, kazi ya Anitha na alikaa katika kiti cha Anitha. Atake asitake alikuwa Anita.

    "Anithaaaa!" Yule Mhudumu wa sheli aliita tena.

    "Basi achana nae" Inspekta Jasmine alishauri.

    Baada ya kutiliwa mafuta waliyoyahitaji, Inspekta Jasmine na Daniel Mwaseba waliondoka kuendelea na msako wao wa kumsaka Suto Sutani !

    Suto Sutani aliendelea kulala pale kwenye kiti, bila kujua kwa kiasi gani alikaribiwa na hatari. Daniel Mwaseba hakuwa mtu wa mchezo kabisa. Kuwa karibu nae namna ile tena akiwa amelala ilikuwa ni hatari kubwa sana.

    Saa kumi usiku Suto Sutani aliamka usingizini, akiwa hajui kabisa kwa namna gani Polisi walivyozagaa pale Tegeta kumsaka yeye. Wakati akiwasumbua Polisi zaidi ya mia na kuwakeshesha usiku kucha, yeye alikuwa amelala tu kwenye kiti.

    Alifumbua macho taratibu na kuangazaangaza, akili yake ikakaa sawa na kugundua sehemu aliyokuwa. Akiwa na nguo zake za ulinzi alinyanyuka na kutokomea mtaani. Mtaa ambao ulikuwa umejaa maaskari wa kutosha wakimsaka yeye.

    "Wewe hebu simama!" Ilikuwa sauti ya askari ikiyomuamuru Suto Sutani asimame. Huku akiwa anatetemeka Suto Sutani alisimama.

    "Kwanini unatembea usiku wewe?" Askari watatu walisimama mbele ya Suto Sutani, na mmoja kumuuliza.

    Suto alitetemeka kwa sekunde thelathini, kisha alibadirika ghafla, akawa imara na kujiamini.

    "Anitha, mlinzi wa sheli, natoka kwenye lindo sahivi" alijibu kwa sauti imara, na ya kujiamini sana.

    "Dada usitembee usiku, kuna msako wa Mhalifu hapa, bora urudi sheli huko unakofanyia kazi ukae mpaka asubuhi"

    "Sawa Afande"

    Suto Sutani aliachana na wale askari. Kwa mara ya pili Suto alinusurika katika mdomo wa mamba. Sasa alitembea kwa tahadhari kubwa zaidi. Akitafuta namna ya kutoka nje ya Tegeta. Ilikuwa alfajiri ambayo haikuwa na mbalamwezi, Suto aliambaaambaa gizani akiifata njia inayoelekea Bagamoyo. Alikuwa anapita pembeni kabisa ya barabara, akitembea kwa magoti, au wakati mwengine akitumia tumbo lake kutambaa kama mwanajeshi. Ilikuwa alfajiri chungu sana kwa Suto Sutani. Mara nyingi ilimpasa kulala vichakani ili kuruhusu vikundi vya askari Polisi vipite, ili nae aendelee na safari yake. Sehemu chache alizoziona salama, alitembea na zingine alikimbia kabisa. Alijipongeza sana kwa kuvaa ile suruali ya bluu ya kilinzi, ilimpa afueni sana katika safari yake ngumu usiku ule, angekuwa na zile kanga ingempa shida sana.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kina Kulwa hawakuwa na habari kabisa juu ya msako wa Suto Sutani uliokuwa unaendelea huko Tegeta. Sasa hawakuwa wanapata uelekeo wa msako toka kwa Veronica Baro. Veronica Baro na Inspekta Jasmine hawakuwa marafiki tena. Kina Kulwa sasa walikuwa na kazi ngumu zaidi. Kupeleleza mahali alipo Suto Sutani na kumfatilia.



    Kwasasa kina Dungu walikuwa Tabata, huku masikio yao yakiwa wazi ili kuweza kupata habari kwamba Suto Sutani alikuwa wapi?.

    Lakini hawakupata!

    Kwa mtindo uleule, wa kutambaa, kukwawa, kutembea na kukimbia, Suto Sutani alikuwa anakaribia kuimaliza Tegeta na kuwaacha Polisi kwenye mataa!

    Wakati anaimaliza Tegeta, alisikia sauti ya ajabu na ya kutisha sana. Wakati huo alikuwa anatambaa katika nyasi chache chachechache pembezoni mwa barabara.

    "We hebu simama!" Suto alistuka sana, akiwa bado kalala nyasini aliangalia upande sauti ile ya kutisha ilipotokea.

    Alikuwa Askari Polisi !

    Suto aliishiwa nguvu pale chini.

    "Nimekwambia simama, huelewi, nitakifumua kichwa chako sasa hivi!" Yule askari aliongea huku akimuonesha Suto Sutani bunduki aina ya 22-Caliber iliyojazwa risasi za 22 LR.

    Suto hakuwa na jinsi, alisimama taratibu huku akituliza akili, mtetemo ulimuisha na umakini ulimrejea tena. Sasa wakawa wanatazamana na yule askari.

    Askari alipomwangalia Suto usoni alimtambua.

    "Ndiye!" Askari alijikuta karopoka.

    Sasa yule askari aliingiwa na woga kuona anatazamana na Suto Sutani aliyebadirika.

    "Nakusikiliza" Suto alisema kwa kujiamini.

    Askari alipoteza kabisa ujasiri, ilikuwa sawa anatazamana na chui, alisahau kabisa oda aliyopewa na kamanda wa Polisi wa mkoa wa Dar es salaam. Suto Sutani aliona hiyo ndio nafasi ya dhahabu, anapaswa kuitumia ili kujiokoa.

    "Upo chini ya ulinzi, nyoosha mikono yako juu" Askari alithubutu kutamka maneno hayo.

    "Halafu nikishanyoosha mikono juu?" Suto aliuliza kwa kujiamini alishaugundua udhaifu wa yule askari.

    Hakuiogopa kabisa ile bunduki iliyoshikwa kwa mkono ukiotetemeka.

    "Hata akinifyatua, kufa na kuishi kwangu ni sawa" Suto Sutani alijisemea mwenyewe kimoyomoyo. Jibu hilo lilizidi kumbabaisha yule askari.

    Ghafla, kitendo bila ya kuchelewa Suto Sutani alirusha teke lililoenda kuipangusa ile bunduki aliyoishika yule askari. Ile bunduki ilirushwa na kupotelea nyasini.

    "Usinilazimishe nikuue!"

    Suto aliongea huku akiipigia mahesabu ile bunduki iliyodondoka pale chini. Alikuwa anaongea huku akipapasa kwa siri pale chini kwa kutumia mguu wake. Mguu ukagusa kitu kigumu!

    Akajua kile ndio kitu alichopaswa kuchukua kwa wakati ule na kuumaliza mchezo! Kwa kasi Suto Sutani aliinama na akivyoinuka alikuwa na bunduki mkononi!

    Suto hakuwahi kushika bunduki tangu azaliwe, kwa hiyo alikuwa hajui hata namna ya kuitumia. Lakini kwa bahati mbaya kabisa alipaswa kuitumia sasa bila mafunzo yoyote.

    "Fumba macho, sali sala yako ya mwisho!" Suto aliamrisha.

    Yule askari alifumba macho huku akiomba muujiza wowote utokee. Alikuwa anasali huku akiwa haelewi risasi ya 22 LR itazama sehemu gani katika mwili wake.

    Hali ikawa kimya huku yule askari akiwa amefumba macho vilevile.









    *****



    Pamoja na maeneo ya Tegeta kuzungukwa na maaskari wengi sana, lakini madereva pikipiki maarufu kama bodaboda waliendelea na kazi zao, ilikuwa saa kumi ya usiku lakini bado madereva hao walikuwa katika pilikapilika.



    Suto Sutani alikuwa barabarani sasa, na bunduki yake mkononi, kwake bunduki ile ilikuwa kama fimbo tu, kwakuwa hakuwa anaweza kabisa kabisa kuitumia. Alimuacha yule askari muoga kule palepale, akiwa amepiga magoti huku amefumba macho. Suto hakutaka kumuua askari yule, alimuacha pale na kusogea barabarani, kuangalia uwezekano wa kumtoa eneo lile lilikuwa hatari sana kwake.

    Pikipiki, iliyokuwa inakuja ilirudisha umakini wa Suto Sutani. Aliipungua mkono nayo ilisimama. Dereva wa pikipiki ile hakumwangalia abiria wake wa kike, macho yalitua kwenye ile bunduki, aliogopa sana !

    Alitaka kutimka na pikipiki yake, lakini alipoangalia mavazi ya mwanamke yule, alisimama kabisa, Aligundua kuwa alikuwa mlinzi. Kuamini huko ndio lilikuwa kosa pekee alilolifanya mwendesha pikipiki alfajiri ile. Aliposimama tu macho yake yalitua alielekezwa bunduki!. Alitaka kuondoka lakini alikuwa ameshachelewa.



    "Nataka unifikishe Bagamoyo, katika njia ambazo hatukutana na mtu hata mmoja....

    Lakini usiogope sana, tukikutana na mtu naweza kukusamehe, ila tukikutana na Polisi, jua nawe unakufa hapo hapo!"





    Dereva wa pikipiki alikuwa anatetemeka, hakutarajia kabisa kukutana na mkwara kama ule asubuhi ile. Suto Sutani hakusubiri dereva yule aitikie, alipanda katika siti ya nyuma ya pikipiki ile. Na dereva nae akiwa na woga kiasi aling'oa pikipiki ile. Safari ya kuelekea Bagamoyo kwa njia za vichochoroni ilianza. Yule dereva alikuwa anazijua njia za vichochoroni kweli. Hadi wanaiacha Tegeta walipishana na watu wawili tu. Alivyoiacha Tegeta Suto Sutani alimshukuru mwenyezi Mungu, kwa mara nyingine tena alifanikiwa kuwatoroka Polisi.

    Polisi walitafuta sana pale Tegeta. Lakini hawakuambulia kitu.



    MISUKOSUKO BAHARINI.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Saa kumi na moja alfajiri radio call za askari polisi zilikuwa kazini. Askari walikuwa wanataarifiana juu ya kuokotwa kwa mlinzi mmoja mtaroni, na kutambulika kama alikuwa mlinzi wa sheli. Hakuna aliyemuelekeza mwenzie, askari wote walijua kwamba hiyo ilikuwa ni kazi ya mikono ya Suto Sutani.



    Daniel Mwaseba nae alikuwa ana maelezo mazuri zaidi kichwani mwake. Alijua kwamba Suto Sutani alimpiga mlinzi kisha akavaa nguo za kilinzi na kutokomea nazo, au kajificha mahala.



    Nusu saa baadae yule askari alifikisha taarifa ya kuporwa bunduki na Suto Sutani.

    Sasa katika picha za askari polisi vichwani mwao zikaongezeka. Popote alipo Suto Sutani basi amevaa nguo bluu za kilinzi na bunduki. Bunduki kuwa mikononi mwa Suto Sutani, iliongoza hofu kubwa sana kwa askari Polisi. Polisi waliona balaa zaidi liko njiani. Kama Suto Sutani kwa kutumia kisu aliua kiasi kile, sasa alikuwa na bunduki.



    "Natamani kukuuwa, lakini nakuonea huruma, niahidi hutomwambia mtu yeyote kama uliwahi kuonana na mimi"

    "Siwezi kumwambia mtu, naapa"

    "Safari njema"



    Dereva pikipiki aliondoka huku akiwa haamini kama alitoka salama katika mikono ya Suto Sutani. Alishukuru njia mzima.



    Pamoja na kumuachia dereva pikipiki na kumuonya. Lakini Suto Sutani hakuamini kabisa kama dereva pikipiki yule atamfichia siri yake. Kichwani mwake alijua kuwa Bagamoyo haikuwa sehemu salama. Aliamua kuitelekeza ile bunduki na kuelekea pwani, kutafuta chombo cha kumtoa nje ya Bagamoyo, Suto Sutani sasa alikuwa hamwamini mtu yeyote.





    Boti alilopanda Suto Sutani lilikuwa linaelekea katika kisiwa cha Mafia. Baada ya kulipa nauli ndipo aligundua kuwa alipongukiwa kiasi kikubwa cha pesa. Suto alikuwa anahitaji pesa zingine ili ziweze kumvusha katika harakati hizi hatari. Atazipata wapi?

    Hata mwenyewe hakuwa anajua.

    Boti lilitembea kwa kasi kubwa sana, wakiwa katikati ya bahari ghafla ulianza kuvuma upepo. Upepo uliozaa mawimbi makubwa sana mle baharini. Suto alikuwa amelala, sauti ya nahodha ndio iliyomuamsha.



    "Abiria kuna hali ya hatari , bahari imechafuka sana, na kwa bahati mbaya hatuna 'life jackets' humu, tunaomba mtulie hivyo hivyo tunajitahidi kuweka hali sawa"



    "Kuweka hali sawa? Wao ni Mungu mpaka waweke hali sawa , hapa ni kutafuta namna ya kujiokoa" Suto Sutani alijisemea kimoyomoyo.



    Ingawa Suto alikuwa anawaza kutafuta namna ya kujiokoa. Bila shaka alisahau, walikuwa katikati ya bahari ya Hindi, bahari yenye kina kirefu, atajiokea vipi. Suto aliangalia macho yake mbele, aliona maji tu mpaka upeo wa macho yake ulipokomea. Aligeuka nyuma pia aliona maji mpaka upeo wa macho yake ulipokomea. Aliangalia kulia na kushoto, hali ilikuwa hiyohiyo , walizungukwa na maji mengi sana, huku wakifatwa na upepo mkali sana. E bwana eeee! Alipogeuka mbele, aliona wimbi kubwa sana likiwa linaifata boti yao!



    Lile wimbi kubwa na lenye nguvu liliipiga ile boti kwa nguvu kubwa sana!

    Boti liliyumba myumbo mkuu. Watu wasiojishikia imara walitupwa baharini!

    Boti lilikuwa na watu 12, baada ya wimbi lile na bahari kutulia kidogo, boti lilibakiwa na watu wanne tu. Watu nane walizamishwa majini kwa nguvu ya wimbi lile.



    Kwa bahati mzuri nahodha wa chombo kile alipona kutokana na dhoruba ile. Alisimama imara kujaribu kuokoa roho yake na za abiria wake waliobakia. Hali ilikuwa ya hatari sana!



    Mawimbi sasa yaliwapa nafasi ya kutafakari. Yalikuwa yanakuja mawimbi ya wastani.



    Ndani ya boti abiria wote walitulia kimya. Kila mmoja akimuomba Mungu wake .



    Boti sasa lilibakiwa na Watu wanne pekee. Wanaume watatu na mwanamke mmoja imara aitwaye Suto Sutani.

    Suto alikuwa anasalia kimoyomoyo ili anusurike katika dhoruba ile ili akaikamilishe orodha yake ya kifo!



    Dua ya Suto Sutani ilipoisha na dhoruba kubwa sana lilikuwa inaifata ile boti. Dua ya Suto Sutani ilikuwa kama ndio ilioliita lile wimbi kubwa zaidi. Kubwa kuliko wimbi la mara ya kwanza. Wimbi kubwa mithili ya nyumba. Wimbi lile kubwa sana liliifikia boti ya kina Suto Sutani. Ililikinyanyua kile chombo juujuu, kikarudishwa chini kwa kasi kubwa sana. Hakikuwa chombo tena, yalikuwa mabaki ya chombo. Boti lilipasuka vipande vingi sana!. Boti lilipanda juu ya wimbi likiwa na watu wanne, vipande vilishuka chini vikiwa hamna mtu hata mmoja. Hapohapo ilianza kunyesha mvua, mvua kubwa sana baharini!

    Hali ilizidi kutisha!



    *****



    Huko katika kisiwa cha Mafia, katika gati lilipo katika kijiji cha Kilindoni kulikuwa na rundo la askari. Walikuwa wanaisubiri boti aliyopanda Suto Sutani. Yule dereva pikipiki hakuwa na kifua, aliitoa siri ya kumpakia Suto Sutani kwa askari Polisi. Kwa bahati mbaya zaidi aliitoa hiyo siri baada ya kuchunguza uelekeo wa Suto Sutani. Alimwona mpaka Suto Sutani alivyopanda katika ile boti iliyokuwa inaelekea Kisiwani Mafia.



    Daniel Mwaseba na Inspekta Jasmine waliingia katika boti ya Polisi kumsaka Suto Sutani. Na Polisi wa Kilindoni Mafia, walitaarifiwa juu ya ujio wa Suto Sutani, nao walijipanga vizuri. Huku boti tatu za Polisi zikiingia kazini kumkaribisha Suto Sutani zikitokea Kulinda. Ilikuwa ni lazima Suto akamatwe, atake...asitake!



    Kwa bahati mbaya mtego wa Polisi uliharibiwa na mchafuko wa habari. Ule msukosuko iliokuwa inaipata boti ya kina Suto Sutani, ulikuwa umetokea kwanza katika zile boti tatu zilizotokea Kilindoni, Mafia. Na pia ziliifikia boti iloyotoka jijini Dar es salaam, boti aliyopanda Daniel Mwaseba na Inspekta Jasmine..



    Shughuli pevu kwa Suto, Mbele kuna askari nyuma kuna wakina Daniel Mwaseba..kimbembe!



    Kwa bahati mbaya Suto Sutani hakuwa anajua kuogelea kabisa. Hakuwahi hata kujaribu kuogelea hata siku moja enzi za uhuru wake. Leo hii aliujua umuhimu wa kuogelea. Suto Sutani alikuwa anasubiri rehma za Mungu tu!

    Wimbi lile kubwa la pili lilimwacha Suto Sutani hewani, alirudi chini kwa kasi kubwa sana! Hakujua kuogelea lakini ilimpasa kufanya chochote ili kukiepuka kifo!

    Rejeo lile la Suto Sutani lilimpeleka chini ya maji moja kwa moja, alikunywa mafunda matatu safi ya maji. Baada ya kunywa mafunda matatu ya maji ya chumvi akili ilimkaa sawa. Alichapachapa miguu na mikono ndani ya maji. Chapachapa ile ilimsaidia, alijikuta anaibuka juu. Kichwa kufika tu juu kilikumbana na mvua kubwa sana. Alikuwa anamuona izrael kwa mbali. Alijitahidi kuangaza huko na huku kwa mbali alikiona kipande cha ile boti. Suto Sutani alijua kipande kile ndio kitu pekee kinachoweza kumuokoa. Ila tatizo sasa kilikuwa mbali kidogo na yeye. Alichapa tena miguu, akashangaa alikuwa anarudi tena majini. Maji yalimlaki tena, akanywa nusu funda, alichapa mikono kwa fujo, alirejea tena juu, kichwa kinaelea huku kinalowa.

    Ilikuwa Balaa !





    Akili ya Suto Sutani ilikuwa imejisogeza mpaka pale kwenye kile kipande cha boti, lakini mwili wa Suto ulibaki palepale. Na kwa bahati mbaya zaidi alikuwa anazidiwa nguvu na maji, machozi yalianza kumtiririka, nani wa kuyaona machozi yale, machozi yalikuwa yanapitiwa na mvua ile kisha kupotelea baharini. Sasa Suto Sutani alikuwa anazama chini taratibu.....





    Suto alizama chini kweli, akawa haonekani kabisa. Akiwa ndani ya maji alikuwa akiwaza, mawazo ya mwishomwisho.



    "Siko tayari kufa namna hii"



    Kwa nguvu zake za mwisho zilizobakia suto alichapa kwa nguvu mikono na miguu yake, taratibu alirudi tena duniani. Alipofika juu bahati ilikuwa yake. Kile kipande cha boti kilikuwa karibu yake. Bila shaka kililetwa na mawimbi madogo madogo. Aliking'ang'ania kipande kile kwa nguvu zake zote!



    Mawimbi yale makubwa mawili kabla hayajalifikia boti alilopanda Suto Sutani, kwanza yalitokea katika ufukwe wa bahari ya Kilindoni. Ufukwe uliokuwa umejaa Polisi wengi sana wakati huo. Wakimsubiri Suto Sutani. Wimbi la kwanza tu lilitosha kuizamisha boti moja ya Polisi, kati ya boti zile tatu zilizokuwa katika operesheni ya kumsaka Suto Sutani. Wimbi la pili ndio lilimaliza kila kitu. Boti mbili zilozobakiwa zilipasuliwa vibaya sana na kuzamishwa majini. Habari kuhusu askari wale, zaidi ya thelathini iliishia hapohapo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mawimbi yale mawili yalimalizia hasira zake pia katika boti ndogo waliyopanda Daniel Mwaseba na Inspekta wa kike, Inspekta Jasmine. Nao hadithi ilikuwa vilevile. Walistahamili wimbi la kwanza, lakini wimbo la pili liliipasua vibaya sana boti yao. Nao walibaki majini wakitapata. Bahati ilikuwa yao, wote walikuwa wataalam wa kuogelea. Wote walikuwa wanaelea majini wakiwa hawana uelekeo maalum.

    Bahati mbaya ikawavaa wale askari wawili. Mvua ilikuwa ni kikwazo kikubwa sana kwao. Walipata shida sana!



    Patashika baharini, nani atatoka salama?





    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog