Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

FURAHA HATIMAYE - 1






IMEANDIKWA NA : ERIC SHIGONGO



*********************************************************************************



Simulizi : Furaha Hatimaye

Sehemu Ya Kwanza (1)



“Umeolewa?”

“Ndio!”

“Mume wako yuko wapi?”

“Dar es Salaam!”

“Sijawahi kumwona hata mara moja akija hapa hospitali!”

“Ana kazi nyingi sana ofisini kwake, hata hivyo huwa anajitahidi kufika anapopata nafasi!” Maneno hayo yalitoka mdomoni mwa mwanamke mwenye nywele chafu kichwani mwake, ambazo kwa kuziangalia zilionekana siku za nyuma ziliwahi kuwekwa dawa lakini baadaye zikaachwa bila matunzo! Alivaa fulana yenye rangi ambayo haikuwa rahisi kuijua kati ya kahawia na nyeupe sababu ya uchafu, pamoja na hali hiyo bado kwa kumwangalia vizuri mwanamke huyo zaidi ya namna alivyovaa, haikuwa rahisi kushindwa kuugundua uzuri wa sura yake, alikuwa na macho makubwa ya kuita, urefu wa wastani, kiuno chembamba na matiti yaliyosimama wima kama vile hakuwahi kuwa na mtoto, chini ya kiuno upande wa pembeni kulivimba vitu kama mito ya kulalia chini ya sketi chafu aliyovaa, ambayo ufupi wake uliacha miguu yake kuanzia magotini kushuka chini ionekane wazi, alikuwa na mguu adimu, mguu ambao wengi waliuita mguu wa bia.

“Unaniambia kweli?”

“Ndio daktari!”

“Mbona sijawahi kumwona, anaitwa nani?”

“Gerald!”

“Mh!”Daktari aliguna, alikuwa amehisi kudanganywa, macho na midomo ya mwanamke huyo vilitofautiana kabisa.

Alikuwa ndani jengo la wodi ya watoto katika Hospitali ya Mtakatifu Francis huko Ifakara, mkoani Morogoro. Kitanda namba 9 chumba cha pili. Hali ya hewa nje ya jengo mchana wa siku hiyo ilikuwa ni ya joto tofauti na siku nyingine zote katika kipindi hicho cha Masika. Hakuwa peke yake ndani ya wodi, kitandani alilala mtoto mdogo, mwenye maumbile ya ajabu, kichwa chake kilikuwa kimejaa mabonde na nundu nyingi, viungo vyote mwilini mwake vilikuwa vimevimba! Alikuwa mtoto mwenye umri wa miaka kumi lakini alionekana kama mtoto wa miaka mitatu kwa jinsi alivyokuwa mdogo kwa umbile.

Alikuwa Genesis, mtoto wa kike wa Blandina, alimwita jina hilo akiwa na maana ya neno ‘Mwanzo’ kama ilivyo kwenye kitabu Kitakatifu kitumiwacho na Wakristo; Biblia, akiamini ulikuwa ni mwanzo wa maisha ya raha aliyoyafikiria na kuyatamani siku zote, kuja kwa Genesis katika maisha yake ulikuwa mwanzo wa furaha! Haikuwa hivyo, hakupanga mipango yake akimshirikisha Mungu, kama ni kosa basi hilo ndilo alilofanya kwani kuja kwa Genesis badala ya kuwa mwanzo wa furaha, kulibadilika na kuwa mwanzo wa matatizo na balaa katika maisha yake kiasi cha kumfanya apoteze hata Imani ya Kikristo aliyokuwa nayo, akamchukia Mungu akisema “Kama kweli Mungu alikuwepo na aliwapenda watu ni kwanini alimpa adhabu aliyokuwa akiipata akiamini hakuwa na kosa alilotenda kustahili mateso hayo!”

Pembeni kwa kitanda alicholalia Genesis, kulikuwa na kabati, juu ya kabati hilo kulikuwa na redio ndogo aina ya National Panasonic, ikirusha matangazo ya Radio One, mtangazaji siku hiyo alikuwa Misanya Dismas Bingi, akili na mawazo yote ya Blandina yalikuwa yameelekea kwa mtoto wake, alitamani siku moja Genesis apone ili arejee tena jijini Dar es Salaam kuungana na familia yake, kwa muda mrefu alikuwa ameishi peke yake, akihama hospitali moja kwenda nyingine ndani na nje ya Tanzania akitafuta uzima wa mtoto wake.

“Leo katika ukumbi wa Mango Garden, Twanga Pepeta watakuwa pale chini ya mwanamuziki Mahiri nchini Tanzania Ali Choki mtoto wa Kibaha, jukwaa litakuwa linashambuliwa ipasavyo, usikose kiingilio ni shilingi elfu mbili…! Ukitoka hapo unaweza kwenda Bilicanas au Police Officers Mess ambako wazee wa zamani watakuwa wakiserebuka na mzee Ndala Kasheba pamoja na King Kiki katika ile miondoko ya Bakurutu…!” Alimaliza Misanya bila kuelewa ni kitu gani alikuwa akikisababisha moyoni mwa Blandina.

Machozi yalimlengalenga, kumbukumbu za Dar es Salaam zilimiminika kichwani mwake, akamwona mume wake Gerald na kuamini alikuwa bado akiendelea na starehe wakati yeye akiteseka na mtoto hospitalini! Ilimuuma.

Alitamani dunia ingebadilika na kurejea ilikokuwa kabla ya kuzaliwa kwa Genesis ambaye alibadilisha kila kitu katika maisha ya Blandina na kumfanya awe mtu wa machozi usiku na mchana, akili yake ilimrudisha nyuma miaka kumi na mbili na kumfanya azikumbuke nyakati ambazo yeye na Gerald walikuwa wapenzi wakitoka karibu kila mwisho wa wiki kwenda sehemu za starehe pamoja, Gerald akimwita majina yote mazuri kama Sweet, Honey , Darling, Baby na mengineyo mengi. Hali hiyo haikuwepo tena, alikuwa peke yake katika dunia akihangaika kuokoa maisha ya mtoto wake, haikuwa rahisi kuhisi aliwahi kuwa Miss Dar es Salaam kwa jinsi alivyokuwa mchafu, uzuri wa sura na urembo haikuwa na maana tena kwake, kitu cha muhimu kilikuwa mtoto wake Genesis.

“Mom!” (mama!) Genesis aliita katikati ya maumivu mkononi akiwa ameshikilia picha ndogo ya mtoto.

“Yes my darling!”(Ndio mpenzi wangu!)

“Is this my photo when I was small?”(Hii ni picha yangu nilipokuwa mdogo?) Mtoto aliuliza kwa sauti ya huzuni.

“Yes my sweet!”(Ndio mpenzi wangu!)

“No! This is somebody else!”(Hapana! Huyu ni mtu mwingine!)

“Why?”(Kwanini?)

“How comes I am this ugly and shapeless if at birth I was this cute?”(Inawezekanaje nikawa na sura mbaya kiasi hiki kama wakati wa kuzaliwa nilikuwa mzuri namna hii?)

Lilikuwa swali gumu sana kwa Blandina, badala ya kulijibu alijikuta akiangua kilio mbele ya mtoto wake na kumfanya yeye pia ashindwe kuvumilia, wote wawili wakaanza kulia! Picha ndani ya chumba hicho ilikuwa ni ya kuhuzunisha mno na daktari aliyekuwa pembeni akiandika mambo fulani kwenye faili aliyemfariji na kumtuliza Blandina, alielewa mwanamke huyo alikuwa akipita wakati mgumu kiasi gani. Halikuwa jambo rahisi kwa mwanamke wa kawaida kustahimili shida alizokuwa akizipitia, kwa muda wa miezi tisa alikuwa amelazwa katika hospitali hiyo akimuuguza mtoto wake, kabla ya hapo alishalazwa hospitali nyingi tu jijini Dar es Salaam bila nafuu yoyote kwa mtoto wake.

Kifupi katika miaka minane tangu mtoto wake aanze kuugua, labda ni miezi miwili au mitatu tu ndio alikuwa amekaa nyumbani kwake! Siku nyingine zote alikuwa hospitali akihangaika na mtoto wake, hakuwa tayari kukata tamaa mpaka mwisho uonekane na alitaka mwisho wa maisha ya Genesis utokane na Mungu mwenyewe, kwani mara kadhaa alishashauriwa mpaka na watu wa karibu kabisa maishani mwake amuue mtoto wake ili azae mwingine kwani huyo hakuwa na faida yoyote katika maisha yake zaidi ya kuwa mzigo, kauli kama hii ilitoka pia kwa mume wake ambaye hakuwa tayari kabisa kukubaliana na ukweli kuwa yeye na mke wake walikuwa wamepata mtoto mwenye matatizo na hivyo walitakiwa kushikamana.

“Blandina!” Daktari alimwita.

“Ndio daktari!”

“Nimefanya kazi miaka ishirini lakini sijawahi kukutana na mama mwenye moyo kama wako, Mungu akubariki sana!”

“Ahsante daktari!”

“Unampenda sana mtoto wako sio?”

“Sana!”

“Usikate tamaa, iko siku utapumzika…!”

“Ahsante daktari, endelee kuniombea!”

“Genesis!” Daktari alimwita mtoto.

“ Yes!”(ndio!)

“Do you know that your mom loves you?”(Unajua ya kwamba mama yako anakupenda?)

“Yes I do! I love her too, I haven’t seen my father for a long time, but she is always here with me, she is a good mother!”(Ndio najua! Nampenda pia, sijamwona baba yangu kwa muda mrefu sana, lakini yeye yuko hapa pamoja nami siku zote, ni mama mzuri!) Mtoto aliongea akilengwa lengwa na machozi.

Blandina aliona aibu, alichokuwa akijaribu kukificha kilikuwa kimewekwa wazi na mtoto, siku zote hakupenda kumuaibisha Gerald, alikuwa mume wake. Pamoja na upungufu wote aliokuwa nao, bado alitaka kumlindia heshima yake.

“Blandina”

“Ndio daktari!”

“Ulinidanganya?”

“Nini daktari?”

“Kwamba mumeo huwa anakuja hapa kukuona!”

“Samahani daktari, ni habari ndefu!”

“Ningependa kuifahamu!”

“Nitakusimulia kesho!”





Blandina ndiye mwanamke aliyeko ndani ya wodi, mchafu kupita kiasi, asiyejijali tena ambaye aliwahi kuwa Miss Dar es Saalam na kwa uzuri wake bila shaka alipendwa na wanaume wengi lakini akamchagua mmoja tu, Gerald. Hivi sasa yuko ndani ya hospitali ya Mtakatifu Francis huko Ifakara, akimuuguza mtoto wake mdogo Genesis mwenye umri wa miaka kumi lakini kwa kumwangalia unaweza ukafikiri ana miaka mitatu, afya yake ni mbaya sababu ya ugonjwa unaomsumbua tangu akiwa na miaka miwili.

Blandina ndiye anayeteseka na mtoto huyu wodini bila mume wake, ambaye siku zote alimwambia anampenda na angekuwa naye katika shida na raha! Amehama Dar es Salaam kwenda kutafuta uzima wa mtoto wake Ifakara, hayupo tayari kumwacha Genesis afe, ndio maana hajijali wala kuangalia na uzuri aliowahi kuwa nao, cha muhimu kwake hivi sasa ni mwanae.

Daktari amevutiwa na Blandina na kumwambia wazi kuwa katika maisha yake ya kutibu wagonjwa hospitali hakuwahi kumwona mwanamke mwenye moyo kama wake, aliye tayari kuacha kila kitu sababu ya mtoto ambaye ni wazi asingekuwa na faida maishani mwake hata kama angepona, daktari huyu anataka kuelewa ni nini hasa kilitokea maishani mwa Blandina na kwanini mume wake alikuwa hafiki hospitali kumwona mtoto na mama yake.

Sasa tuendelee na sehemu ya pili ya hadithi hii yenye mafundisho makubwa kwa akinamama wote…



SONGA NAYO..



Muda wote akiongea Blandina alikuwa akilengwalengwa na machozi, kila siku alipogusia habari za Gerald alikosa uvumilivu na kujikuta akilia! Haikuwa rahisi kuamini hata mara moja kuwa mwanaume mwenye sura nzuri kama yeye angeweza kuwa katili kiasi hicho, hasa alipofikiria walikotoka pamoja, mambo ambayo Blandina alikuwa ameyaacha kwa sababu yake ikiwa ni pamoja na kutengwa kufutwa kabisa katika ukoo wa baba yake mzee Mohamed Abdallah, mfanyabiashara tajiri mjini Morogoro.

Blandina alikuwa peke yake duniani, hakuwa na ndugu wala mtu wa kumweleza matatizo yake isipokuwa Gerald, ambaye tayari alikuwa amemkimbia, roho ilimuuma sana na ilimuuma zaidi alipofikiria namna ambavyo yeye mwenyewe alijitoa na kuokoa maisha ya Gerald akiwa katika wakati wa kufa, alikuwa na uhakika bila yeye Gerald asingekuwa hai!

“Kwa wema niliomtendea hakustahili hata kidogo kunilipa ubaya kama huu! Mungu anajua!”Alijikuta akitamka maneno hayo.

“Nani Blandina?” Dk. Albert Mkambila alimuuliza.

“Daktari acha tu, nitakusimulia kesho, huwa sipendi sana kuyaongelea mambo hayo lakini sina jinsi itabidi nikushirikishe labda unaweza kunipanua mawazo!”

“Wazungu wana msemo usemao, to be healthy you have to share your problems with others!” Aliongea daktari akimaanisha ili mtu awe na afya ni lazima ashirikiane na wengine katika matatizo yake!

“Ndio nakuelewa, lakini huwa nashindwa kuwashirikisha watu wote maana wengi hawatanisaidia chochote zaidi ya kunicheka na kuniona mpumbavu!”

“Basi niamini mimi!”

“Nitanya hivyo!”

“Nitakuja kesho baada ya raundi ya mchana, kama saa nane hivi na nusu!”

“Hakuna shida daktari, nimeahidi kukusimulia kuhusu maisha yangu na nitafanya hivyo!”

Kutwa nzima akimuuguza na kumbembeleza mtoto wake kitandani, Blandina pia alikusanya kumbukumbu zake vizuri kichwani tayari kwa kumweleza daktari mambo yote yaliyotokea maishani mwake! Mambo yaliyomtokea maishani mwake yalikuwa mengi mno kiasi cha mengine kuanza kupotea kwenye kumbukumbu zake, ilibidi aweke kila kitu sawa kwa ajili ya siku iliyofuata, alikuwa ameamua kumweleza daktari kila kitu ili atue mzigo mzito aliokuwa ameubeba kifuani kwake kwa muda mrefu.

Siku iliyofuata kama alivyoahidi, Dk Mkambila alifika wodini na kumkuta Blandina akimlisha mtoto wake cha mchana, hakuna kazi nyingine aliyokuwa nayo zaidi ya kumjali Genesis! Alimkaribisha kitini ili kwanza akamilishe kazi hiyo.

“Nakusubiri, masaa yamekwenda taratibu mno mpaka kufika saa nane na nusu, kila saa ilionekana ni mwaka mzima kwa jinsi ambavyo nina hamu ya kusikia historia yako!”

“Usiwe na wasiwasi ili mradi nimekwishaamua kukusimulia!”

“Ahsante!”

“Habari za kazi lakini?”

“Sio mbaya, nimemaliza kuona wagonjwa wangu sasa hivi ndio nikaja hapa!”

“Nashukuru sana!”

Dakika saba hivi baadaye Blandina alimaliza kumlisha mwanae na kumlaza kitandani kisha kumfunika na shuka ndipo akamgeukia Dk.Mkambila tayari kwa kumsimulia historia ya maisha yake.

“Unataka kusikia historia yangu?”

“Ndio!”

“Niahidi kitu kimoja!”

“Kitu gani?”

“Hutamweleza mtu mwingine kuwa mimi ni nani na wazazi wangu ni akina nani!”

“Sitafanya hivyo, mimi ni daktari niliyekula kiapo cha kuficha siri!”

“Haya! Unao muda lakini?”

“Ninao!”

“Historia yangu ni ndefu sana!”

“Wewe nieleze tu!”

Blandina akainamisha uso wake chini na kunyamaza kwa kama dakika tano, aliponyanyuka alikuwa akitokwa na machozi, kazi ya Dk. Mkambila ikawa ni kumbembeleza kwanza mpaka alipotulia ndipo akaanza kuongea.

“Sikuzaliwa Blandina kama watu wote wanavyoniita, nilizaliwa nikiitwa Halima Mohamed Abdallah, mwaka 1969 huko Kilosa mkoani Morogoro!”



Saa 4:00, Agosti 10,1969, hospitali ya Kilosa.



Wodi ya wazazi ya hospitali ya wilaya ya Kilosa iliyojengwa kilimani kidogo kama kilometa moja kutoka mjini ilikuwa kimya kabisa, sauti za akinamama wakilia kwa uchungu kutoka chumba cha pili zilimfikia bwana Mohamed Abdallah akiwa chumba cha kusubiria, alikuwa na hamu kubwa ya kufahamu mke wake angejifungua mtoto gani! Kwa muda wa karibu miaka nane ya ndoa yeye na mke wake walikuwa wameishi bila kupata mtoto, siku hiyo ilikuwa ni ya furaha sana kwake kwani pamoja na mafanikio makubwa kifedha aliyokuwa ameyapata hayakuwa na maana kama hakuwa na mtoto! Nyumba yao ilihitaji mtoto ili angalau kuongeza vuguvugu na mapenzi kati yao. Hakutaka hata kurudi nyumbani kwake mpaka mke wake ajifungue.

Mohamed alikuwa kijana wa Kiarabu kutoka familia ya Abdallah Rahman, mfanyabiashara maarufu mjini Morogoro na muumini mzuri wa dini ya Kiislam. Kama taratibu na desturi za Waarabu wengi zilivyokuwa, Mohamed alitegemewa kumwoa msichana kutoka kwenye ukoo wao tena Mwarabu mwenzake, cha kushangaza alikwenda kinyume na matarajio ya wengi na kuamua kumwoa msichana wa Kikaguru waliyesoma naye shule moja, Rehema Ramadhan.

Alipigwa na kila mtu kwenye ukoo wake, wengi wakidai alikuwa analeta haramu kwenye familia yao jambo ambalo yeye hakukubaliana nalo kabisa akidai binadamu wote ni sawa na alihitaji kumwoa mwanamke aliyempenda! Baada ya tishio la kumtenga kushindikana hatimaye aliruhusiwa kumwoa Rehema, ndoa ikafungwa kwa taratibu zote za Kiislam na maisha yakaanza tena ya raha mustarehe.

Akiwa katikati ya mawazo juu ya mtoto ambaye angezaliwa, mara mlango wa chumba cha akina mama kujifungulia ulifunguliwa, mkunga aliyemfahamu kwa jina la mama Muhombolage akatokeza na kumsalimia, wote walifahamiana kwa sababu waliishi katika mji mmoja.

“Hongera shemeji!”Aliongea mkunga huyo.

“Vipi?”

“Tayari!”

“Salama lakini?”

“Salama tu!”

“Mtoto gani?”

“Wa kike!”

“Namshukuru Mwenyezi Mungu! Naweza kumwona mke na mtoto wangu?”

“Hakuna shida! Njoo tu nimekwishawapeleka wodini”

Akiwa na furaha ya ajabu, Mohamed alimfuata mkunga nyuma hadi wodini ambako alimkuta mke wake amelala kitandani, pembeni akiwepo mtoto mchanga akainama na kuwapiga busu wote wawili! Macho yake yalibaki kwa mtoto, uzuri wake ulionekana hapo hapo kitandani pamoja na kuwa mtoto mchanga.

“Hongera mke wangu na pole!”

“Ahsante sana!”

“Umezaa mtoto mzuri!”

“Tumshukuru Mungu!”

“Kwa uzuri wake huyu mtoto kwa kweli inabidi tu tumwite Halima!”

“Ni vyema!”

Masaa arobaini na nane baadaye kwa sababu Bi Rehema hakuwa na matatizo yoyote waliruhusiwa kutoka hospitali na kurejea nyumbani ambako furaha iliendelea kuwatawala, Mohamed hakusafiri tena aliamua kubaki nyumbani mpaka siku arobaini zikatimia mtoto akatolewa nje na jina la Halima likapitishwa moja kwa moja, mtoto huyo akawa Halima Mohamed Abdallah, mtoto wa kwanza na kipenzi cha wazazi wake, kila mtu aliyemwona alikiri mtoto huyo angekuwa tishio kwa uzuri aliokuwa nao alichukua sura na rangi kutoka kwa wazazi wake wote wawili.

Mwaka wa kwanza ukapita salama na uzuri wa Halima ukizidi kuchomoza, hata wazazi wake uliwatisha! Hakuwa mtoto wa kawaida kuanzia macho, mashavu, midomo, shingo, kifupi uzuri wa mtoto uliizidi familia yao uzito! Halima akaendelea kukua hatimaye akatimiza miaka miwili na nusu na kujiunga na shule ya mwanzo iliyoendeshwa na Kanisa Katoliki mjini Kilosa, tofauti na watu wengine mzee Mohamed hakujali sana shule hiyo iliendeshwa na nani, alichotaka yeye ni elimu kwa mtoto wake, alikuwa tayari kutumia kila kitu alichokuwa nacho mahali popote ili mradi Halima apate elimu hiyo ikiwa ni sambamba na elimu ya dini ya Kiislam.

Miaka mitatu baadaye, alikuwa tayari kwa darasa la kwanza, mzazi wake hakuona shule yoyote ya kumsomesha wilayani Kilosa na kuamua kumtafutia shule jijini Dar es Salaam na kufafanikiwa kupata shule ya Tanganyika International School iliyoko maeneo ya Masaki ambako Halima alianza darasa la kwanza katika darasa ambalo yeye peke yake ndiye alikuwa Mwafrika, wengi wa watoto wakiwa ni wale wa Mabalozi, viongozi mbalimbali wa nje pamoja na wafanyabiashara wenye asili ya Kiasia, ilikuwa ni shule ya gharama kubwa lakini Mohamed alikuwa tayari kutumia kiasi chochote cha fedha kwa ajili ya elimu ya mtoto wao.

Ilikuwa ni shule ya bweni, wakati wa likizo tu ndipo alirudi Kilosa kupumzika na wazazi wake ilipofunguliwa alirejea tena shuleni kuendelea na masomo, katika darasa lake aliendelea kuwa Mwafrika peke yake mpaka wakiwa darasa la saba ndipo mtoto mwingine aitwaye Gerald alipoungana nao, huyu alikuwa mtoto wa Balozi wa Tanzania nchini Marekani Salva Lutta.

Ni kipindi hicho utawala wa Mwalimu Nyerere uliamua kupunguza matumizi ya Balozi zake nje ya nchi na kuwaagiza Mabalozi wote warudishe watoto wao nyumbani kwa ajili ya masomo, Gerald alikuwa miongoni mwa watoto hao, akajiunga na shule ya Tanganyika International School. Darasa la Halima likawa na watu weusi wawili, tofauti kati yao na watoto wengine iliwafanya bila kupenda wawe karibu na ukaribu wao ukaendelea kukua kadri siku zilivyozidi kwenda, wakiwa kidato cha pili kitu ambacho hawakukitegemea kilianza kujitokeza; MAPENZI.



Blandina ni mwanamke mrembo lakini aliyechakaa sababu ya kukosa matunzo, amelazwa katika hospitali ya Mtakatifu Francis huko Ifakara akimuuguza mtoto wake mdogo wa kike Genesis aliyeugua tangu akiwa na miaka miwili, kuanzia kipindi hicho Blandina ni mtu wa kuzunguka kutoka hospitali moja kwenda nyingine akitafuta uzima wa mtoto wake ambaye hivi sasa ana umri wa miaka kumi lakini anaonekana kama mtoto wa miaka mitatu!

Hata siku moja mume wake Gerald hajawahi kufika hospitali ya Ifakara kumwona mtoto wao, jambo hili linamfanya daktari aliyekuwa akimtibu Genesis; Dk. Mkambila atake kufahamu ni kwanini hali ilikuwa hivyo, hakusita kumuuliza Blandina ukweli ambaye kwanza alidanganya na kusema mume wake hufika hospitali lakini baadaye siri ilikuja kuwekwa wazi na mtoto Genesis aliyeueleza.

Kwa mara nyingine daktari akamtaka Blandina amweleza ukweli lakini badala ya kusimulia alianza kulia kwa uchungu jambo lililomwonyesha daktari kuwa kulikuwa na tatizo kubwa na baadaye alipotulia Blandina aliahidi kumweleza daktari ukweli juu ya maisha yake siku iliyofuata.

Daktari amefika wodini na Blandina ameanza kumsimulia historia ya maisha yake, inaanzia tangu tarehe 10 agosti, 1969 alipozaliwa katika hospitali ya wilaya ya Kilosa akiitwa Halima Mohamed Abdallah, mtoto wa mfanyabiashara maarufu mkoani Morogoro kutoka ukoo wa Abdallah Rahman.



Akiwa na umri wa miaka mitano na nusu, Halima alipelekwa katika shule ya kimataifa iliyoitwa Tanganyika International school jijini Dar es Salaam kuanza darasa la kwanza, wazazi wake walikuwa tayari kutumia chochote walichokuwa nacho lakini mtoto wao apate elimu bora si bora elimu. Ndani ya darasa lake ni yeye peke yake mwenye rangi mchanganyiko yaani mweusi na Mwaraabu, wengine ni wahindi na wazungu! Anasoma hivyo mpaka darasa la saba, mtoto mwingine aitwaye Gerald Salva Lutta anahamia kutoka nchini Marekani ambako baba yake ni Balozi wa Tanzania katika nchi hiyo.

Tofauti yao na wanafunzi wengine, inawafanya Gerald na Halima wawe karibu kupita kiasi, ukaribu huo ulizaa kitu kingine ambacho wote wawili hawakukitegemea; mapenzi.

Je, nini kitaendelea? Fuatilia…http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Gerald alikuwa mtoto wa kwanza katika familia yao ya watoto watatu lakini kipenzi cha baba yake! Mama yake mzazi alifariki dunia kwa ajali ya gari jijini Dar es Salaam Gerald akiwa na umri wa miaka miwili tu, hakubahatika kumwona wala hakumkumbuka kwa sura. Familia yao ikawa ni ya watu watatu, Gerald, baba yake pamoja na mtumishi wao wa ndani, msichana aliyeitwa Grace. Mzee Lutta alichanganyikiwa sana baada ya kufiwa na mke wake na aliahidi kutooa tena kwa sababu asingempata mwanamke mwenye sifa za Cecilia, mama yake Gerald.



Kwa miaka mitano mzee Lutta aliishi bila mke na haikutokea hata siku moja akaingia na mwanamke ndani ya nyumba yake, wala hotelini au kuonekana akiwa na mwanamke mahali popote! Siku zote aliogopa kashfa alizoamini zingeweza kumharibia maisha yake ya baadaye Kisiasa.



Ghafla mwanzoni mwa mwaka wa sita wa kuishi mpweke, Gerald akiwa na umri wa miaka minane, watu walishangaa kumwona Grace, mfanyakazi wake wa ndani akiwa mjamzito na mzee Lutta ndiye akimpeleka kliniki na hospitali kupimwa, hawakuhitaji kuelekea kitu chochote, walielewa kilichotokea! Alikuwa amemhalalisha msichana huyo kuwa mke wake, tukio hilo lilimfedhehesha sana mzee Lutta, akakosa raha hasa pale maadui zake walipoanza kulipeleka suala hilo kwenye vyombo vya habari, kwa kumwonea huruma, Rais aliamua kumwondoa nchini, akampeleka kuwa balozi nchini Marekani ambako Grace alijifungua mtoto mwingine wa kiume, Patric.



Mapenzi ambayo Grace alikuwa nayo kwa Gerald tangu akiwa mtoto, yalianza kupungua baada ya kuzaliwa kwa Patric! Akawa hampendi tena Gerald, chuki za mama wa kambo zikaanza, mzee Lutta aliligundua jambo hilo na kulikemea lakini haikusaidia, Grace hakumheshimu mzee huyo na siku zote alisisitiza Gerald aondolewe nyumbani akasome shule ya za bweni kwa sababu alikuwa na kiburi na haelewani na mama yake.



Serikali ya Tanzania ilipoamua kuwarejesha watoto wa Mabalozi nyumbani ili kupunguza gharama, Mzee Lutta aliitumia nafasi hiyo kumwondoa Gerald Marekani na kumrejesha Tanzania aendelee na shule, hivyo ndivyo ilivyotokea, akajiunga na shule ya Tanganyika International school ambako siku ya kwanza tu aliyoripoti alimgundua Halima kabla ya kumgundua mtu mwingine yeyote, alivutiwa na vitu vingi kwa msichana huyo.



“She is cute!”( Ni mzuri sana!) Alisema mwenyewe Halima alipopita mbele yake, kama mtoto aliyekulia Marekani, katika umri huo mdogo Gerald alikuwa na uwezo wa kumtofautisha mwanamke mzuri na mbaya wa sura.

Gerald alikuwa kijana mrefu mwembamba, mpole na mwenye macho ya kufanya mtu yeyote amwonea huruma! Alikuwa na kipaji cha ajabu kuelewa masomo darasani, katika umri huo alifahamu mambo mengi ya dunia kuanzia akina Martin Luther King mpaka Nelson Mandela, Che Guevara mpaka Julius Kambarage Nyerere na Kwame Nkurumah! Alielezea kila kitu juu ya watu hao kinagaubaga, zaidi ya hayo alikuwa na uwezo wa kuongelea mwili wa Mwanadamu na namna ulivyotenda kazi, kuanzia ubongo, moyo, figo, ngozi, mifupa na macho bila kukose mahali popote, uwezo wake uliwaacha Maprofesa nchini Tanzania midomo wazi. Zaidi ya hayo alikuwa mcheza mzuri wa mpira wa Kikapu.



Sifa zote hizi zilimfanya Gerald awe mwanafunzi maarufu kuliko mwingine yeyote katika shule ya Tanganyika International school, shule ilijivunia kuwa na mwanafunzi kama huyo. Aliwavutia wasichana wengi kimapenzi, mamia ya barua pepe zilimiminika kuingia kwenye anuani yake kila alipofungua wasichana wakitaka awe mpenzi wao, Gerald hakuwa tayari kwa hilo, siku zote alivutiwa na msichana mmoja tu katika shule hiyo, naye ni Halima Mohamed Abdallah.



Walikuwa karibu mno, Halima alifanya kila kitu na Gerald, pengine hiyo ilisababishwa na kauli aliyoambiwa na wazazi wake kuwa shuleni ahusiane na kujenga urafiki na watu wenye akili kuliko yeye, hao wangemsaidia kufanya vizuri katika masomo yake! Uhusiano wao ulikuwa, siku zote wakijichukulia ni marafiki wa kawaida mpaka walipokuwa kidato cha pili katika shule hiyo hiyo ndipo Gerald akaanza kuhisi kitu zaidi ya uhusiano wa kawaida, akaanza kuuona uzuri wa Halima katika mwanga tofauti! Akaanza kumtamani akitaka awe mpenzi wake.



“Kuna kitu nimekificha kwa muda mrefu, leo ningependa nikuambie!”

“Kitu gani hicho kaka Gerald?”

“Ningependa hizo herufi nne katikati ya sentensi yako uziondoe!”

“Zipi? Kuna gani na kaka”

“Gani haina matatizo, tatizo liko kwenye hiyo kaka ningependa iondoke!”

“Badala yake tutumie neno lipi?”

“Mpenzi!”

“Unamaanisha nini?”

“Nakupenda Halima! Ningependa mimi na wewe tuwe wapenzi! Ikiwezekena siku moja uwe mke wangu”

“Mh!” Halima aliguna.

“Kwanini unaguna?”

“Ni jambo gumu, ni jambo lisilowezekana, mimi na wewe tuna tofauti kubwa mno!”

“Tofauti gani? Au kwa sababu wewe unamchanganyiko wa Mwarabu na mimi mweusi?”

“Sio hivyo!”

“Ila?”

“Dini zetu, wazazi wangu ni watu wenye msimamo mkali mno kidini, haiwezekani kabisa mimi na wewe tukaoana, isitoshe ni mapema mno kuanza kujadili jambo kubwa kama hili Gerald, mimi bado mdogo, nahitaji kukua! Hivi unaweza kuamini Gerald kwamba tangu nizaliwe sijawahi kukutana na mwanaume kimwili?”

“Aaa wapi! Hizo fiksi za kibongo tu, haiwezekani katika umri ulionao uwe haujafanya!”

“Hakyanani, amini usiamini sijawahi!”

“Lakini nakupenda Halima, tofauti yetu ya dini mimi sioni kama ni kizuizi, angalia hapa shuleni wasichana wanavyotaka kuwa na mimi lakini siku zote sitaki, nimekuchagua wewe! Naomba usiniangushe, tafadhali kubali, usiniumize moyo Halima, nakupenda tena kwa moyo wangu wote!”

“Nitafikiria hilo kwa sababu tuko pamoja, lakini kipaumbele kwangu kwa hivi sasa ni elimu, mambo kama hayo nitaanza kuyawaza nikiwa Chuo Kikuu!”

Ni kweli kabisa, Halima alikuwa bado ni bikira! Malezi ya Kiislamu aliyoyapata kutoka kwa wazazi wake yalimwongoza kuwa msichana mwaminifu, hofu ya Mungu, magonjwa ya zinaa na maoni ya watu juu ya tabia yake ilimfanya awe msichana mtulivu akiitunza bikra yake kwa ajili ya mwanaume ambaye angemwoa! Hata yeye mwenyewe moyoni mwake, alihisi mapenzi aliyokuwa nayo kwa Gerald hayakuwa ya kawaida lakini hakuwa tayari kumvulia nguo na kufanya naye tendo la ndoa, maneno ya maonyo ya mama yake yalisikika akilini mwake.



Gerald hakukasirishwa na jibu alilopewa, akiamini mambo mazuri hayahitaji haraka! Aliendelea kuwa na Halima kila siku, siku za mwisho wa wiki wakipata nafasi ya kwenda kupumzika ufukweni na kuongea mambo mengi kuhusu maisha, waliporejea shuleni walikumbatiana wakapigana mabusu na kuagana, hiyo ilikuwa desturi yao kila mwisho wa wiki! Walitengana wakati wa likizo peke yake, Halima aliporudi nyumbani kwao Mogorogo na Gerald kwenda NewYork na kurejea mwezi mmoja baadaye akiwa na zawadi kedekede kwa ajili ya Halima, vivyo hivyo Halima naye alirejea na zawadi nyingi kutoka nyumbani kwa wazazi wake.



“Mama yangu amejifungua mtoto mwingine wa kiume, jina lake Fayaz, ni mtoto mzuri sana!”

“Ulifurahi eeh?”

“Sana lakini nilikukumbuka mno!”

Walipeana zawadi na maisha yakaendelea hivyo hivyo mpaka wakiwa kidato cha sita, ndipo mapenzi kati yao yakazidi kupamba moto, Halima hakuweza kujizuia tena, tayari alishazama katika bahari nzito ya mapenzi! Akajikuta amekubaliana na kila kitu na kumpa Gerald heshima aliyokuwa amemtunzia mume wake, bikira. Haikuwa rahisi kwa Gerald kuamini alichokishuhudia, maneno ambayo siku zote aliyachukulia kama uongo sasa yalionekana ni ukweli, akamkumbatia Halima na kumbusu kwa furaha.

“Nimeamini!”

“Wewe si ulifikiri nakundandanya?”

“Haikuwa rahisi kuamini, sasa nakuambia kitu kimoja, kama utakubali kuolewa na mimi, basi nitafanya hivyo Halima, nimekuharibia lengo lako, hivyo sina budi kukupa furaha unayoihitaji!”

“Dini?”

“Sio tatizo, naweza kubadili dini nikawa Mwislam, Mungu wetu ni mmoja!”

“Kama ukifanya hivyo, wakati wowote nitakuwa tayari!”

“Tukiingia tu mwaka wa kwanza Chuo Kikuu ni lazima tufunge ndoa, unaonaje?”

“Nitafurahi!”

“Na jina langu la Kiislamu litakuwa Malcom!”

“Hakuna kinachoweza kunifurahisha hapa duniani kama mimi na wewe kuoana Gerald, nakupenda mno, tumetoka mbali tangu tukiwa watoto mpaka leo hii tuko kidato cha sita!” Aliongea Halima wakiwa wamekumbatiana, alimpenda na kumwamini Gerald kuliko kitu kingine chochote, kwa alipokuwa amefikia lolote ambalo angeambiwa na Gerald alikuwa tayari kulitenda ili mradi asimpoteze, maisha yake bila Gerald yalikuwa sawa na bure.





Halima ni binti wa mfanyabiashara tajiri mkoani Morogoro, mzee Mohamed Abdallah! Ndiye mtoto wa kwanza akifuatiwa na kaka yake mdogo Fayaz katika familia yao, anapendwa kupita kiasi na wazazi wake na wako tayari kutumia kila walichonacho kumpatia elimu bora mtoto wao ndio maana wamempeleka katika shule ya gharama kubwa jijini Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla, Tanganyika International School.



Ni katika shule hiyo ndiko anakutana na mtoto mwingine aitwaye Gerald, huyu ni mtoto wa Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Salva Lutta. Gerald amerudishwa nchini na wazazi wake baada ya agizo la Serikali kuwarudisha watoto wa Mabalozi kusomea nyumbani ili kupunguza mzigo kwa serikali.



Wanasoma katika darasa moja na ukaribu wao darasani ndio umewafanya wajikute katika hali ambayo hawakuitegemea; mapenzi! Mwanzoni Halima alikataa lakini kadri siku zilivyozidi kwenda wakiwa kidato cha sita alijikuta akikubaliana na ombi la Gerald kuwa mpenzi wake, mapenzi yakazidi kukomaa mpaka Halima akakubali kupoteza Bikra yake ambayo siku zote alimtunzia mume ambaye angemuoa, kwa sababu ya Gerald.



Baada ya Gerald kukuta kweli Halima hajaguswa, alifurahi mno na kuahidi kumuoa kama tu Halima angekuwa tayari kufanya hivyo wakiwa mwaka wa kwanza Chuo Kikuu, alikuwa tayari hata kubadilisha dini na kuwa Mwislam kwa sababu ya mwanamke aliyempenda. Je, nini kitaendelea katika maisha ya watu hao wawili? SASA FUATILIA…



Hatimaye furaha ya Gerald ilitimia, kuwa mpenzi wa Halima kwake ulikuwa ni ushindi mkubwa mno, alimpenda kwa kila kitu na hakusita kuonyesha mapeniz yake waziwazi kiasi kwamba kila mwanafunzi katika shule ya sekondari ya Tanganyika iliyoendeshwa na Wamisionari, aliufahamu uhusiano wa watu hao wawili, walisoma pamoja, walitembea pamoja, walipumzika pamoja na walisaidiana katika masomo yao kufikia hatua ya kuwa wanashindania namba, Gerald akishika namba moja basi nyuma yake alikuwepo Halima na ilipotokea Halima akashika namba moja basi nyuma yake alikuwepo Gerald. Hata walimu waliufurahia uhusiano wao.



Vichwani mwao sasa waliwaza kitu kingine ambacho huko nyuma hawakuwa nacho, ndoa! Gerald aliona siku zilikuwa zikienda polepole mno kabla hawajaingia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alitaka waanze mwaka wa kwanza na mara moja wafunge ndoa! Tayari alishamtaarifu baba yake ambaye kwa wakati huo hakuwa tena Marekani bali Italia akiendelea na kazi yake ya Diplomasia, hakuwa na kizuizi chochote kwa uamuzi wa mtoto wake kama yeye alipenda kufanya hivyo.



Kwa Halima mambo yalikuwa tofauti kidogo, hata mara moja asingediriki kufungua mdomo wake na kumwambia mzee Mohamed kuwa eti alikuwa amepata mchumba, familia yake ilikuwa ni ya Kiislam kwelikweli iliyofuata maadili yote ya dini hiyo! Alibaki kimya akisubiri wakati muafaka wa kuzungumza neno hilo mbele ya wazazi wake ufike.



Walipofanya mitihani yao ya kidato cha sita na kuondoka shuleni, Halima hakwenda moja kwa moja nyumbani Morogoro, alibaki kwenye nyumba ya akina Gerald huko Masaki kwa muda wa wiki nzima wakiponda maisha pamoja, karibu kila siku usiku walitoka kwenda katika kumbi mbalimbali za starehe kucheza muziki, kunywa pombe, kuvuta sigara mambo ambayo Halima hakuwahi hata siku moja kuyafanya maishani mwake, kila kitu alikuwa amefundishwa na Gerald.



Ilikuwa ni dunia tofauti kabisa na aliyowahi kuishi msichana huyo, akilelewa Kiislamu muda wote ushungi na baibui, sasa alivaa sketi fupi na vitopu vilivyoacha kitovu chake nje, umbile lake lilimvutia kila mwanaume aliyemtazama! Na wote walikiri kweli Halima alikuwa msichana mwenye mvuto wa ajabu. Baada ya starehe zao walirejea nyumbani na kulala pamoja, wakishirikiana hata katika tendo la ndoa kama mtu na mke wake ingawa wakati ulikuwa bado.



Mwanzoni mwa wiki ya tatu waliagana, Gerald akaondoka kurejea Marekani kwa wazazi wake na Halima akarejea nyumbani kwao Morogoro, mama yake alipomwangalia tu aligundua tofauti kubwa katika tabia ya mtoto wake, kwanza mavazi aliyofika nayo nyumbani hayakuwa yale ambayo familia yake iliyasisitiza, siku zote alikuja akiwa amevaa Hijabu kuficha nywele zake pamoja na sketi ndefu lakini siku alipowasili baada ya kumaliza kidato cha sita, alivaa sketi fupi ya dengirisi, juu akiwa amevaa kifulana kidogo kilichoacha kitovu chake wazi, miwani ya jua usoni.

“Halima! Ndo umetuvaliaje hivyo mwanangu? Utamwona vipi baba yako? Mtoto unataka kuharibika weye?”

“Hapana mama, tunakwenda na wakati!”

“Halima mtoto wa Kiislamu wewe, hutakiwi kuvaa hivyo, wakati gani huo unaokwenda nao? Hebu chukua hiki kitenge ufunge ukamsalimie baba yako yupo ndani!”

“Mama bwana, mpaka kitenge, enewei basi!” Halima aliongea akikipokea kitenge na kujifunga kiunoni kisha kuingia ndani ambako alimsalimia baba yake, hata hivyo bado mzee Mohamed aligomba ni kwanini hakuwa na Hijabu au ushungi kichwani jambo ambalo ni kinyume kabisa cha Dini ya Kiislamu.

“Usiache kichwa wazi mwanangu, watu hawatatuelewa, ni kinyume cha Dini hicho, wasikia weye?”

“Nasikia baba!”

“Haya karibu, shule imekwenda sawasawa?”

“Ndio baba!”

“Chuo Kikuu waenda weye?”

“Nitakwenda baba!”

“Basi vizuri, nenda huko nyuma kamsaidie mama yako kazi, au umechoka?”

“Kidogo sio sana!”

Maisha ya Kilosa mkoani Morogoro yalionekana kutomfaa tena Halima, kwa namna alivyokuwa hakulingana kabisa hata na wasichana wengine katika mji huo mdogo unaokaliwa na wakaguru pamoja na Waluguru wengi. Alijikuta hana rafiki hata mmoja, muda wote alifungiwa ndani kwa mila na desturi za Kiarabu, alijisikia kama mfungwa! Jambo hili lilizidisha kumbukumbu zake kwa Gerald, roho ilimuuma sana, alitamani kumwona tena na aendelee kuishi naye, maisha aliyomuonjesha yalikuwa matamu mno, alitaka kuendelea nayo akiwa na Gerald.

Mapenzi yao sasa yalirejea kwenye simu, alitumia fedha nyingi za baba yake kuongea na Gerald kutokea Kilosa! Ankara ya simu ambayo siku zote haikuzidi shilingi elfu ishirini sasa ilianza kugota shilingi laki moja mpaka laki moja na nusu kwa mwezi, mzee Mohamed akaanza kuwa mkali akitaka kujua ni wapi ambako Halima alipiga simu. Msichana huyo hakuwa tayari kuuweka ukweli wazi, alichokifanya mzee Mohamed ni kwenda kampuni ya simu na kuomba atolewe machapisho ya simu zote zilizopigwa kutoka kwenye namba yake, namba moja tu ilijirudia, namba ya Gerald, akarudi nyumbani na kumuuliza kama aliifahamu namba hiyo.

“Ndio!”

“Ni ya nani?”

“Rafiki yangu!”

“Mvulana au msichana?”

“Mvulana!”

“Rafiki yako kivipi?”

“Tulikuwa tunasoma naye shule na hapo baadaye tuna mpango wa …!”

“Mpango gani mwanangu?”

“Kuoana kama Inshallah!”

“Anaitwa nani?”

“Gerald!”

“Gerald?”

“Ndio baba!”

“Mkristo?”

“Ndio!”

“Unanieleza habari za kuolewa na Mkristo?”

“Kwani sio mtu baba?”

“Halima! Unaongea kitu gani?”

“Ndio hivyo mzazi wangu, nampenda siwezi kuishi bila yeye!”

“Anaweza kubadili dini?”

“Ndio, alikwishakubali jambo hilo!”

“Ahaa! Sawa, lakini kwa hivi sasa nakuomba sana uachana kwanza na hayo mambo usome!Sitaki kuona unajihusisha na mambo ya mapenzi!”

“Sawa baba!”

“Ina maana tayari mmekwishaanza mambo hayo?”

“Bado! Ni urafiki wa kawaida tu!”

“Mama Halima, hebu nikuone kidogo pembeni!” Mzee Mohamed alisema akinyanyuka mahali alipoketi na kuanza kutembea kuelekea nje, mke wake akimfuata kwa nyuma.

“Vipi?”

“Nina wasiwasi sana na huyu binti yako!”

“Hunishindi mimi!”

“Hebu kamchunguze, isije kuwa keshapoteza hata hiyo zawadi uliyonitunzia mimi mpaka siku ya ndoa yetu!”

“Kwa ninavyoona, sidhani kama anayo!”

“Kwani hukumchunguza aliporudi?”

“Sikufanya hivyo!”

“Naomba ufanye na unipe majibu ili kama ameanza mambo hayo nijue jinsi ya kushughulika naye, asije akaniingiza kwenye aibu bure!”

“Sawa mume wangu!” Mama yake Halima alijibu na kurejea ndani ambako alimnyanyua Halima kitini na kumwongoza hadi chumbani ambako amri moja tu ilitolewa.

“Vua nguo zako!”

“Ili nifanye nini mama?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Umesahau siku zote nikikuleta chumbani na kukutana uvue nguo huwa nataka kufanya nini?”

Halima alianza kutetemeka, alielewa wazi kitendo cha kukutwa hana bikra kingemsababishia matatizo makubwa sana na baba yake, tangu ajiunge na shule ya Tanganyika International School, ilikuwa ni lazima akaguliwe sehemu zake za siri kila aliporejea nyumbani likizo! Siku za nyuma wala hakushtuka lakini siku hiyo mwili wake wote ulikuwa ukitingishika kwa hofu, alielewa kabisa hakuwa nacho kitu ambacho mama yake alikuwa akitafuta.

“Mama ninayo!”Alisema.

“Wacha nijionee mwenyewe!”

*****

“Nasema vua nguo zako!”

“Nifanye nini mama?”

“Umesahau siku zote nikikuleta chumbani na kukutana uvue nguo huwa nataka kufanya nini?” Mama yake Halima aliuliza.

“Nafahamu mama!”

“Sasa mbona unauliza maswali mengi? Hebu vua bwana!”

“Mama ninayo!”

“Nini?”

“Bikra!”

“Wacha nijionee mwenyewe, vua nguo, ukiendelea kunileta ubishi nitamtaarifu baba yako kwamba hutaki, wewe mwenyewe unamfahamu, shughuli yake itakuwa nzito!”



Halima alikuwa akitetemeka mwili mzima, kuanzia kichwani mpaka miguuni, alitamani ardhi ipasuke na adumbukie ndani yake, alielewa aibu iliyokuwa mbele yake ni kubwa kiasi gani! Si aibu tu pia adhabu ambayo angeipata kwa kupoteza bikra, akiwa bado anasita kuvua nguo zake, mama yake alianza kuvuta gauni alilokuwa amelivaa na kulishusha chini.

“Mama!”

“Bee!”

“Hivi hujui kama nilishavunja ungo na sasa hivi niko kwenye … si uache kwanza mpaka nimalize”

“Sasa mbona husemi? Lione macho, unanisumbua tu!”

“Leo siku ya ngapi?”

“Ya pili, nilianza jana!”

“Huwa unatumika siku ngapi?”

“Nne!”

“Leo juma ngapi?”

“Jumatatu!”

“Ijumaa uchunguzi uko pale pale sawa?”

“Hakuna shida!”Alijibu Halima ingawa hakuwa na uhakika kabisa nini kingefanyika ili siri yake isigundulike, mpaka jioni ya siku hiyo alikuwa mwenye mawazo mengi hata usiku hakuweza kula akitafakari! Katikati ya usiku akiwa kitandani alimkumbuka bibi Mwanahawa, kungwi aliyeendesha shughuli za kuwafunda wanawake, alihisi angeweza kumsaidia kama angemweleza shida zake! Wazo hilo kichwani mwake lilionekana zuri na kama angeshindwa kumpa jibu basi ingebidi awe tayari kwa lolote, alitamani asubuhi ifike mara moja.

Usiku mzima hakupata usingizi, aliwaza mambo mengi juu ya jambo ambalo lingekwend kutokea, alimfikiria sana Gerald na heshima aliyompa ambayo sasa ilikuwa ikimwingiza kwenye matatizo na wazazi wake! Alitamani angalau angeelewa taabu aliyokuwa akiipata kwa sababu yake ili azidishe mapenzi, saa kumi na mbili asubuhi alikuwe kwenye simu akiongea na Gerald na kumsimulia kila kitu.

“Nakupenda Halima, nisamehe kwa kukusababishia usumbufu, mimi na wewe mpaka mwisho wa uhai wetu, naomba tu uwe mvumilivu!”

“Nakupenda pia Gerald, naomba tu usije kuniumiza moyo!”

“Siwezi kufanya hivyo, naapa mbele ya Mwenyezi Mungu, kama kweli nitakuja kukusaliti basi nianguke chini sasa hivi nife!”

“Usiapie Gerald, nakuamini! Ok, kwaheri, acha tumpunguzie mzee Mohamed bili ya simu analalamika mno siku hizi!”

“Ok! Baadaye!”

Kulipokucha asubuhi baada tu ya kifungua kinywa, Halima aliaga kuwa anakwenda kwa rafiki yake Mwasi Kaswiza, ambaye walisoma naye shule ya awali ya Kilosa na baadaye kuwa marafiki wakubwa tangu wakiwa watoto, wazazi wake hawakuwa na kizuizi chochote kwani hawakuelewa nini lilikuwa lengo lake, wakamruhusu lakini badala ya kwenda alikokuwa amepanga, Halima alikata kona kuelekea eneo lililoitwa Mtendeni kwa bibi Mwanahawa, alihakikisha hakuna mtu aliyemwona wakati anaingia ndani ya nyumba ya bibi huyo.

“Karibu mjukuu!”

“Ahsante, shikamoo bibi!”

“Marahaba hujambo?”

“Sijambo!””Vipi tena asubuhi hii?”

“Bibi mimi nina tatizo!”

“Tatizo gani mjukuu wangu?”

“Nimepoteza bikra yangu, wazazi wangu wanataka kunichunguza na mimi sitaki wagundue hili!”

“Halo!Halo! Nani kakuelekeza hapa?”

“Nakufahamu muda mrefu bibi!”

“Wewe mtoto wa nani?”

“Wa mzee Salehe wa Kimamba!”Halima alidanganya, hakutaka kabisa bibi huyo atambue alikuwa mtoto wa mzee Mohamed Abdallah.

“Umetoka Kimamba wewe?”

“Niko hapa kwa shangazi yangu!”

“Unazo fedha?”

“Shilingi ngapi bibi?”

“Elfu mbili, maana lazima ninunue vitu fulani vya kuchanganya katika hiyo dawa!”

“Ninayo!”

“Nipe basi, uondoke urudi jioni!”

Halima akamkabidhi bibi huyo noti ya shilingi elfu tano aliyokuwa nayo, akaondoka zake, ili kupoteza ushahidi baada ya kutoka hapo aliamua kwenda Manzese kwa rafiki yake Mwasi na kuongea naye kama saa nzima hivi ndipo akamwomba amsindikize hadi nyumbani kwao ili kuwafanya wazazi waelewe ni kweli alikuwa amekwenda kwao! Hakumtaka aondoke mpaka jioni alipomsindikiza hadi barabarani, wakaagana na yeye badala ya kurudi nyumbani akakimbia hadi nyumbani kwa bibi Mwanahawa.

“Umekuja?”

“Ndio bibi!”

“Chukua hii, utakuwa unaitumia kujisafisha bondeni mara tatu kwa siku, fanya hivyo siku kwa muda wa siku nne ndipo umruhusu mama yako akuchunguze, sawa?”

“Sawa bibi, hakuna matatizo yoyote!”

“Hakuna, utavimba kidogo tu lakini usiwe na wasiwasi!”

“Sawa bibi kwaheri!”

“Chenji yako?”

“Baki nayo tu!” aliongea akitoka.

Halima aliondoka nyumbani kwa bibi Mwanahawa na kurejea nyumbani bila kugundulika, usiku wa siku hiyo hiyo alifanya kama alivyoelekezwa, akaendelea asubuhi siku iliyofuata, mchana na usiku! Kwa siku nne alifanya kitendo hicho, akimwambia mama yake alikuwa bado hajatoka katika hedhi kumbe lengo lake likiwa ni kutimiza muda wa matumizi ya dawa aliyopewa na bibi Mwanahawa.

“Vipi leo? Baba yako anataka jibu”

“Nimeshatoka, unaweza tu kunichunguza!”

“Twende basi ndani, tumwondoe wasiwasi baba yako!”

“Mama kwanini huniamini?”

“Sio kwamba sikuamini, nataka kujiridhisha!”

“Twende basi mama!” Aliongea Halima akitabasamu, hakuwa na wasiwasi tena moyoni mwake, chumba alivua nguo zake na kulala chali kitandani, mama yake akamsogelea tayari kwa kuanza uchunguzi.

“Mh!”Mama yake aliguna.

“Vipi mama mbona unaguna?”

“Wee mtoto, umekuwaje tena?”

Halima akawa kimya, mapigo yake ya moyo yakabadilika ghafla, alihisi ujanja wake umegundulika.



Halima ni mtoto wa kwanza katika familia ya kitajiri ya Mzee Mohamed Abdallah, mkazi wa Mjini Kilosa mkoani Morogoro! Anapendwa sana na wazazi wake ambao wapo tayari kutumia chochote kuhakikisha mtoto wao anapata elimu bora, katika kulifanya hili ndio maana waliamua kumtoa Kilosa na kumpeleka jijini Dar es salaam kwenye shule ya kimataifa ya Tanganyika ambako watoto wa matajiri peke yao husoma.



Wazazi walifanya jambo hili kwa nia njema kabisa bila kuelewa walikuwa wakimtia mtoto wao katika hatari ya mmomonyoko wa maadili, kwani katika shule hiyo ndipo alikutana na kijana Gerald, mtoto wa balozi wa Tanzania nchini Marekani na baadaye Italia. Ni huyu Gerald ndiye alimlewesha Halima kwa mapenzi, jambo ambalo hakuwahi kulitegemea katika umri huo, akamfundisha na tabia ambazo hakuwa nazo kabisa kama kuvuta sigara, kunywa pombe na kuvaa mavazi yaliyo kinyume na maadili ya Uislamu, akasahau kabisa hata tabia ya kuswali swala tano aliyolelewa nayo tangu utotoni.



Walipomaliza kidato cha sita, Gerald aliondoka Tanzania kurejea Marekani ambako familia yao ilikuwa bado ikiishi, akiwa ameahidi kurejea Tanzania kuendelea na masomo ya Chuo Kikuu pamoja na Halima ambaye alirejea nyumbani kwao Kilosa kusubiri matokeo.



Akiwa Kilosa wazazi wake wanagundua mabadililo ya tabia ya mtoto wao, mtu wa kwanza kuliona hilo alikuwa mzee Mohamed na kumwamuru mke wake amchunguze Halima kuona kama bado alikuwa na bikra yake! Ukweli wa mambo ambao wazazi wake hawakuuelewa ni kwamba, Halima hakuwa bikra tena, alishamzawadia kitu hicho cha thamani mpenzi wake Gerald.



Mama yake alipomwingiza kwenye chumba na kumwamuru avue ili ampime, Halima alidanganya kwamba alikuwa katika siku zake hivyo kumshawishi mama yake waahirishe zoezi hilo mpaka siku nne baadaye, siku iliyofuata asubuhi baada ya kukubaliwa, Halima alidamka mapema na kwenda hadi eneo liitwalo Mtendeni nyumbani kwa kungwi bibi Mwanahawa na kumsimulia tatizo lake kamili akimwomba msaada.



Kwa gharama ya shilingi elfu mbili ingawa yeye alitoa elfu tano, bibi Mwanahawa alimpa Halima majimaji Fulani na kumtaka ayatumie kuosha sehemu zake za siri kwa muda wa siku nne, bikra yake ingerudi! Na wazazi wake wasingegundua kuwa alishaipoteza.



Kama alivyoelekezwa na bibi Mwanahawa, Halima aliyejawa na hofu moyoni mwake akielewa kabisa kitendo cha kugundulika hakuwa na bikra kingempa matatizo makubwa, anayatumia maji hayo kwa siku nne mfululizo, siku ya tano anamruhusu mama yake ampime lakini alipopandishwa kitandani na kuvulishwa nguo zote mama yake anagundua kitu kisicho cha kawaida katika sehemu hizo.

Je, nini kinaendelea? Fuatilia…



Halima alikuwa akitetemeka mwili mzima huku macho yake yote mawili yakimwangalia mama yake usoni, alikuwa amepigwa butwaa na kuonekana kutoamini kilichokuwa mbele yake! Halima akaamini tayari ujanja wake ulikuwa umegundulika, bila kutegemea akahisi mkojo unataka kumpenya, fikra ya kipigo kilichokuwa kinafuata kutoka kwa baba yake zilizidi kumtia hofu, ilikuwa ni lazima atoroke kwenda mahali kokote lakini si kukutana na mzee Mohamed mwenye hasira. Alihisi joto la mwili wake likipanda ingawa hakuwa na homa.



“Wee mtoto, umekuwaje tena?”Mama yake aliuliza kwa mara ya pili baada ya kuona Halima amekaa kimya.

“Kwani vipi mama?”Aliamua kuyajaribu maji ili kujua kipi hasa kilimshtua mama yake kiasi hicho.

“Kwanini umevimba hivi?”

“Ahaa! Kumbe hilo? Nilitumia kemikali fulani kujisafisha sehemu zangu za siri ni daktari bingwa alinishauri kuwa kila ninapokuwa kwenye hedhi nitumie dawa iitwayo Savlon kujisafisha, bahati mbaya niliitumia bila kuchanganya ndio maana ikaniunguza!” aliongea Halima kwa kujiamini, kwa hali aliyokuwa nayo hakuna binadamu angeweza kukubali kwa urahisi kwamba.

“Pole!”mama yake aliongea kwa masikitiko, Halima akashusha pumzi na kuhisi ushindi.

“Sasa Tufanyeje?”

“Kuhusu nini mama?”

“Kukupima!”

“Endelea tu!”

“Maumivu?”

“Yapo! Sasa nitafanyaje na wewe huniamini ninapokuambia bikra bado ninayo?”

Mama yake Halima alitulia kwa muda akimwangalia mtoto wake, moyoni akasikia huruma na kwa jinsi mwanae alivyokuwa akiongea kwa kujiamini alijikuta akibadilisha mawazo na kuchukua yale ambayo Halima alikuwa ameyasema kama yalivyo bila hata kumchunguza.



“Lakini hii ni siri, baba yako hatakiwi kufahamu!”

“Mama, kuna binti anaweza kuongea na baba yake juu ya jambo kama hili kweli?”

“Basi yamekwisha, tulia ndani mpaka upone kabisa, mimi nitamwambia baba yako kwamba uko vizuri lakini endelea kuwa mwangalifu mwanangu, dunia imebadilika sana hivi sasa, mwanaume asije akakudanganya akakuharibia maisha yako ya baadaye!Unakumbuka niliwahi kukuambia nini juu ya ubikra wako?”

“Ndio nakumbuka!”

“Nini?”

“Kwamba ni heshima ninayotakiwa kumtunzia mwanaume atayenioa!”

“Ahsante kwa sababu unakumbuka, nyanyuka basi uvae!” aliongea mama akifungua mlango tayari kutoka chumbani, nyuma Halima alinyanyuka na kuanza kushangilia, shukrani zote zikimwendea bibi Mwanahawa kwa msaada aliompa vinginevyo angeweza kuaibika na amani ingepotea ndani ya nyumba! Hakutoka tena mpaka usiku wakati wa chakula na baada ya hapo alirejea tena kitandani na kulala mpaka asubuhi.



Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, hakuwa na mahali pa kwenda wilayani Kilosa, kila siku alishinda ndani akisoma vitabu vya hadithi na kuangalia televisheni, alitoka chumbani tu pale alipotaka kwenda dukani kununua sigara alizozivutia chooni kila siku! Hakukumbuka kwenda kuswali swala tano kama alivyofanya siku zote za maisha yake, jambo hilo ndilo liliibua ugomvi mkubwa na wazazi wake lakini Halima hakubadilika, alikuwa mtu mwingine tofauti na waliyemzoea, umbali na wazazi wake ulikuwa umeingiza kichwani mwake mafundisho tofauti na yaliyotegemewa na baba na mama yake.



Kila siku ilikuwa ni lazima aongee na Gerald kwa simu, wakati mwingine alipigiwa na pia yeye alipiga simu Marekani ingawa gharama ilikuwa kubwa! Hakujali, alimpenda Gerald kupita kitu kingine chochote, alikuwa tayari kufanya lolote kumfurahisha. Katika simu walipanga mambo mengi kama ilivyokuwa kabla ya kutengana, lakini kubwa kuliko yote lilikuwa ni ndoa yao baada ya kuingia chuo kikuu, hiyo ndiyo ahadi ambayo wote waliitarajia na umbali uliokuwepo katikati yao ulizidi kuyaimairisha mapenzi kuliko mwanzo, kila mmoja alitamani kumwona mwenzake tena.

“Unafikiri unaweza kurudi lini?”

“Aaa..mh! Baada tu ya matokeo na kupangiwa chuo!”

“Matokeo yatatoka mwezi wa sita!”

“Kupangiwa chuo?”

“Mwezi wa saba na kuingia chuoni ni mwezi wa tisa!”

“Basi mwezi wa tisa nitakuwa hapo!”

“Au wazazi wako wanataka kukusomesha Marekani?”

“Hapana! Baba amesema hana fedha za kutosha kwa hivi sasa isitoshe amehamishwa Italia, baadaye itabidi familia imfuate huko!”

“Kwa hiyo utarudi?”

“Siwezi kukudangaya mpenzi! Hata ahadi yetu ya kuoana iko pale pale”

“Sijui siku nitakayokuona itakuwaje?”

“Hata mimi nashindwa kuelewa, Halima…!”

“Yes!”

“Acha basi tukomee hapo kwa sasa, nitakupigia tena baadaye, sijisikii vizuri sana leo, nina maumivu makali ya kiuno na miguu yangu inavimba sijui ni kwa sababu gani hata mwili wangu hauna nguvu!”

“Utapona mpenzi!”

“Ok, bye! Nitakupigia baadaye jioni ya huko kwenu!”

“Nitafurahi kusikia sauti yako tena!”

Simu ilikatika, Halima akajitupa kitandani na kuendelea kuwaza juu ya Gerald, alishindwa kuelewa maisha yake bila mvulana huyo yangekuwaje, hakika yangekuwa nusu! Hivyo ndivyo alivyoamini. Hakuwa hata na jibu la nini kingetokea kama mzee Mohamed asingempenda Gerald na kuamuru aolewe na binamu zake wa Kiarabu kama utamaduni wao ulivyokuwa, bila shaka huo ndio ungekuwa mwanzo wa kukosana na wazazi wake.



Hakutoka chumbani hata mara moja akisubiri simu ya Gerald iingie lakini haikuwa hivyo, simu ilipolia na yeye kunyanyua mkono wa simu walikuwa ni watu wengine, aidha shangazi, wajomba, binamu au rafiki zake! Ingawa siku zote alifurahi sana simu za watu hao, siku hiyo ilikuwa tofauti, alichotaka yeye ni kusikia sauti ya Gerald tu basi!



Haikuingia simu yoyote kutoka Marekani mpaka asubuhi ya siku iliyofuata, halikuwa jambo la kawaida hata kidogo kwa Gerald kuahidi uongo, hali hiyo ilimchanganya Halima ikabidi yeye mwenyewe aamue kupiga lakini hata simu yake haikupokelewa zaidi ya kujibiwa na mashine! Kichwani mwake aliamini kwa sababu ya tofauti ya masaa kati ya Marekani na Tanzania, Gerald na watu wa familia yake walikuwa usingizini ndio maana hakupiga na simu yake haikupokelewa, mawazo hayo yakampa faraja kidogo.



“Akiamka atanipigia!” Aliwaza Halima na hata kuacha ujumbe wa maneno kwenye simu ya nyumbani kwao na Gerald.

Kutwa nzima alishinda bila kupigiwa simu, usiku pia na hali ikaendelea hivyo kwa wiki nzima! Halima akazidi kuchanganyikiwa na alipopiga simu yeye mwenyewe haikupokelewa zaidi ya kujibiwa na mashine, roho ikazidi kumuuma, moyoni akaanza kuhisi kulikuwa na tatizo kubwa lililojitokeza baada ya kuongea na Gerald kwa mara ya mwisho. Hata hivyo baada ya kuwaza sana aliamua kutumia barua pepe kuuliza sababu za ukimya huo lakini nazo hazikujibiwa.

Mwezi mmoja ukapita Halima akiwa mwenye mawazo mengi, hatimaye wa pili mwisho matokeo ya kidato cha sita yakatoka! Yeye Halima akiwa amepata daraja la kwanza ya pointi 6 na Gerald akiwa amepata daraja la kwanza kwa pointi 7. Ulikuwa ushindi mkubwa mno kwa wote wawili, kwa asilimia mia moja walikuwa na uhakika wa kujiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam kama walivyokuwa wamepanga.



Ilikuwa ni furaha kubwa mno kwa Halima, ambayo alitaka kuichangia na Gerald lakini hakuwa na namna ya kumfikia, alishatumia njia zote kuwasiliana naye bila mafanikio! Jambo hilo lilimkosesha raha na kumfanya akonde na kushindwa kufurahia matokeo yake zaidi, hakuwa na uhakika kama Gerald alikuwa amemwacha au la! Na kama ilikuwa hivyo kwanini hakumwambia moja kwa moja, mara ya mwisho walipoongea alihidi kumpigia simu jioni lakini hakufanya hivyo.

“Wanaume huwezi kuwaamini sana, yawezekana ndio kaniacha hivyo pamoja na kumpa heshima ya bikra yangu! Huu ni unyama, namwomba Mungu huko aliko Gerald awe anafahamu naumia kiasi gani ili abadili msimamo wake na kurejea kwangu, nampenda Gerald tena kwa moyo wangu wote!” aliwaza Halima akilia chumbani kwake.



Mawasiliano kati ya Gerald na Halima yanakatika ghafla, mara ya mwisho walipoongea alihidi angempiga simu jioni lakini hakufanya hivyo na ukimya ulidumu kwa muda mrefu jambo lililomchanganya sana Halima, alimpenda sana Gerald na hakutaka kumpoteza, matokeo ya kidato cha sita yalipotoka wote wawili walikuwa wamefaulu na uhakika wa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ulikuwa mkubwa.



Halima alitaka kushirikiana na Gerald katika furaha hiyo lakini hakuwa na namna ya kumfikia, alipopiga simu siku zote alijibiwa na mashine ya kutoa majibu kwamba wenye simu hawakuwepo hivyo aache ujumbe na aliacha ujumbe kwamba apigiwe simu lakini hata siku moja haikutokea, moyoni mwake akanaza kuhisi tayari alikuwa ameachwa, roho ilimuuma sana kuona alishampa Gerald zawadi ya bikra yake akiamini ndiye angekuwa mume wake.



Je, nini kitaendelea?Fuatilia…



Halima alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea. Halikuwa jambo la kawaida hata kidogo kwa Gerald kukaa kimya kiasi hicho. Hata hivyo aliendelea kuvumilia akivuta subira kwamba siku moja angepokea simu au barua pepe kutoka kwa mwanaume aliyempenda kuliko wote duniani lakini haikuwa hivyo, siku zikazidi kupita hatimaye matokeo ya chuo Kikuu yakatoka, yeye na Gerald walikuwa wamechaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya Mlimani, Gerald kusomea Uchumi na Halima kusomea Sheria.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Hii ilikuwa ni furaha nyingine ambayo Halima alitaka kuisherehekea na Gerald lakini hapakuwa na uwezekano, hayakuwepo mawasiliano kati yao. Bado aliendelea kupiga simu na majibu yaliendelea kuwa yale yale, ni mashine iliyoongea kutoka Marekani kumtaarifu kwamba wenye simu hawakuwepo hivyo aache ujumbe na barua pepe alizoandika zote zilirudi bila kupokelewa! Halima alizidi kuchanganyikiwa, mwili wake ulipoteza uzito mwingi, kifupi mapenzi yalimwathiri kupita kiasi.



Jambo hili liliwatia shaka kubwa wazazi wake kwani tofauti na walivyotegemea kwamba mtoto wao angefurahia ushindi aliopata, walishangaa kumwona akizidi kuhuzunika, muda mwingi akiutumia kulia na kujifungia ndani. Kwao furaha ya Halima ilikuwa kitu cha kwanza, walimpenda mno mtoto wao na waliamini pamoja na kuharibika kwa tabia yake bado walikuwa na uwezo wa kumrejesha alipokuwa. Bado alikuwa mtoto wao wasingeweza kumkana au kumpa mtu mwingine, kila kitu walichokuwa nacho kilikuwa chake, kwa ushindi alioupata katika masomo yake alistahili furaha, ilibidi mzee Mohamed amwite kwa mazungumzo mbele ya mama yake.



“Niambie tu mwanangu, kitu gani kinakusumbua? Umefaulu vizuri, sasa nini? Kwanini unazidi kukonda tu? Kwa matokeo uliyopata ulitakiwa kufurahi sana Halima, unakwenda Chuo Kikuu, watoto wengi hawakupata nafasi kama uliyopata wewe!” Aliongea mzee Mohamed akimwangalia Halima.



Halima hakuongea kitu, machozi yalianza kumbubujika mbele ya wazazi wake. Kwake kitu cha muhimu wakati huo hakikuwa Chuo Kikuu, bali Gerald! Huyo ndiye alikuwa furaha yake, maisha bila yeye hata kama angekuwa na digrii nyingi kiasi gani au utajiri mkubwa bado yasingekuwa na maana yoyote, alimhitaji Gerald kwa gharama yoyote. Mzee Mohamed alipomwona analia, alivutiwa zaidi na kujikuta akitaka kufahamu nini kilikuwa kikimsumbua mtoto wake, akamsogelea na kumwekea mkono begani.



“Niambie! Niambie mwanangu, kama kuna kitu chochote mimi na mama yako tumekuudhi, tueleze tu wala usiogope!”

“Ha…ku..na!”Alijibu Halima kitu kizito kikiwa kimemkaba kooni.

“Sasa kwanini unalia?”

“Nime..umi..zwa!”

“Na nani?”

“Gerald!”

“Kafanya nini?”

“Niliongea naye mara ya mwisho akaahidi kunipigia simu, hajapiga tena! Ninapojaribu kumpigia mimi najibiwa na mashine, nikiandika barua pepe zinarudi, nashindwa kuelewa ni kitu gani kimemtokea!”

“Mwanangu, vijana wa siku hizi ndivyo walivyo, pengine keshakutana na msichana mwingine na kujikuta akisahau huku Tanzania, inabidi ukubaliane na ukweli kisha usonge mbele na kitu cha muhimu zaidi katika maisha yako, elimu!”

“Sawa baba lakini…!”

“Lakini nini Halima?”

“Nahitaji kufahamu kama Gerald ameniacha, pengine kuna matatizo!”

“Ni kweli lakini sasa hivi cha muhimu kwako ni Elimu, inapaswa ujiandae kwenda Chuoni na kama Gerald amepangwa na Mungu kuwa na wewe basi atakukuta huko huko Chuo, si umesema na yeye amefaulu?”

“Ndio!”

“Basi vumilia tu!”

Wazazi wake wote wawili walimshauri na kumtia moyo lakini bado maneno yao hayakumwingia sawasawa moyoni, yaliingilia huku na kutokea huku! Kwa alivyofahamu yeye mwenyewe Halima hapakuwa na jambo jingine la kumpa faraja isipokuwa kukutana na Gerald. Alizidi kuingiwa na simanzi kadri siku zilivyozidi kusonga lakini mawazo yake yote sasa alikuwa ameyawekeza chuoni.



Tamaa ya kuondoka Kilosa kwenda Dar es Salaam kujiandaa na Chuo Kikuu ilimwingia, aliamini huko angeweza hatimaye kupata ukweli juu ya Gerald kuliko kuendelea kukaa Kilosa, wazazi wake hawakuwa na ubishi, mzee Mohamed akampa fedha za kutosha na kumruhusu kwenda Dar es salaam ambako alifikia eneo la Mikocheni kwa shangazi yake. Wao pia walishangazwa na hali aliyokuwa nayo, alionekana kama mtu aliyechanganyikiwa, wakapiga simu Kilosa na kusimuliwa kila kitu juu ya binti yao.



Siku iliyofuata badala ya kwenda Chuo Kikuu, Halima aliondoka Mikocheni na kwenda hadi Masaki kwenye nyumba ya akina Gerald, akitumaini labda angeweza kumkuta au kukutana na mtu ambaye angemweleza nini kilikuwa kikiendelea katika maisha yake! Hakumkuta mtu, si hivyo tu hata nyumba yenyewe haikuwepo, eneo lote lilikuwa limezungushiwa mabati kuonyesha kulikuwa na ujenzi uliokuwa ukiendelea.



“Shikamoo babu!” Alimwamkia mzee wa Kimakonde aliyemkuta eneo hilo, aliyeonekana kuwa mlinzi.

“Marahaba hujambo mjukuu?”

“Babu naomba kuuliza?”

“Ndio!”

“Wenye nyumba iliyokuwa hapa unawafahamu?”

“Nani? Bwana Patel?”

“Hapana Balozi Lutta!”

“Nyumba hii haikuwa ya Lutta, alikuwa mpangaji tu, aliirudisha kwa mwenyewe naye akaamua kuibomoa ili ajenge ghorofa!”

“Mh!”

“Mbona unaguna?”

“Nawatafuta hao akina Lutta!”

“Sina taarifa zao kabisa!”

“Labda huyo bwana Patel!”

“Amesafiri muda mrefu na familia yake kwenda London!”

“Mungu wangu!”

“Kwanini unawatafuta?”

Alipotaka kumsimulia kisa kizima, moyo wake ukasita, hakuona sababu ya kuanika siri iliyokuwa ndani ya moyo wake! Kwa unyonge Halima akamshukuru mzee huyo na kutembea taratibu hadi kituo cha basi ambako alipanda daladala na kurejea Mwenge ambako alipanda gari jingine lililompelekea hadi chuo Kikuu, njia nzima alikuwa akibubujikwa na machozi, hakuelewa alichokuwa akikifanya.



Akili yake yote ilikuwa imetawaliwa na Gerald, kichwani mwake alitamani akifika chuo Kikuu akutane na Gerald, amkimbilie na kumkumbatia kisha kumpiga mabusu akimwomba msamaha kwa yote yaliyotokea, alitamani sana iwe hivyo lakini haikuwa, Gerald hakuwepo chuoni, rafiki zake wengi aliosoma nao ndio aliokutana nao, wote wakimshangaa kwa jinsi alivyokuwa amekonda. Alijiandikisha kama kawaida, akapewa kila kitu kilichohitajika mpaka bweni alilotakiwa kuishi ndipo akarejea tena Mikocheni ambako alijifungia ndani na kuendelea kulia, hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, alinyanyuka tu na kujitokeza wakati wa kula ingawa hata chakula alichokula kilikuwa kidogo mno.



Wiki moja kabla hajaripoti Chuoni ndipo wazo jipya likamwijia, mpaka wakati huo bado alikuwa hajapata mawasiliano yoyote, alijikuta akiifikiria Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, ambayo ilisimamia balozi zote za Tanzania nje ya nchi. Aliamini hapo angeweza kupata taarifa zote za Balozi Lutta na familia yake, kwa vyovyote vile kwa kutembelea ubalozi huo angepata mwanga wa namna fulani.



“Lazima niende!” Aliwaza katikati ya usiku na asubuhi ya siku iliyofuata badala ya kwenda chuoni kukamilisha mambo yake alidandia lifti ya mume wa shangazi yake hadi katikati ya jiji la Dar es Salaam karibu na Mnara wa Askari ambako alishushwa na kutembea kwa miguu hadi Wizara ya Mambo ya nchi za Nje iliyopo ufukweni mwa Bahari ya Hindi. Kwenye idara ya Mapokezi aliulizia ofisi iliyohusika na Balozi za Tanzania nje ya Nchi.



“Unakwenda kumwona nani?”

“Mtu yeyote!”

“Mtu yeyote?”

“Ndio!”

“Anayehusika na nini?”

“Balozi za Tanzania nchini Marekani na Italia!”

“Pandisha ghorofa ya kwanza chumba namba 112, utamwona bwana Maulid yeye ndiye anashughulika na balozi za Ulaya na Marekani!” Aliongea dada mmoja aliyemkuta Mapokezi wakati akimkabidhi kitambulisho cha wageni wa Wizara, Halima akakibandika kwenye blauzi yake na kuanza kutembea kuingia ndani ya jengo kisha kupanda hadi ghorofa aliyoelekezwa, kwenye chumba namba 112 aligonga na kuingia ndani, kijana mrefu mwembamba aliyevalia suti nzuri alikuwa ameketi nyuma ya meza kubwa.

“Shikamoo!”

“Marahaba! Nikusaidie binti?”

“Nina shida!”

“Najua una shida ndio maana uko hapa, shida gani?”

“Natafuta namba ya Balozi Lutta!”

“Lutta?”

“Ndio!”

“Ya hapa au Italia?”

“Italia!”

“Hilo tu?”

“Ndio!”

“Subiri!”

Halima akashusha pumzi kwa nguvu na mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda kwa kasi kubwa! Kwa macho ya akili yake alianza kumwona Gerald, kwani kuipata namba ya Balozi Lutta peke yake ulikuwa ushindi mkubwa mno, mwili wake wote ukitetemeka huku akiomba kimoyomoyo mtu aliyekuwa mbele yake asije kumwambia namba ilikuwa haionekani.



“Una kalamu?” Aliuliza kijana huyo ambaye bila hata kuelezwa Halima alijua ndiye mwenye jina la Maulid.

“Ndio!”

“Andika basi!”Alisema na baadaye kumtajia namba ya nyumbani kwa balozi Lutta, alipomaliza alisimama huku machozi yakimtoka, yalikuwa machozi ya furaha kwani hatimaye aliamini alikuwa amempata Gerald tena! Akashukuru kisha kutoka akikimbia, watu aliopishana nao kwenye ngazi wakati anashuka walimshangaa na kushindwa kuelewa ni nini kilikuwa kimemtokea.



Aliendelea kukimbia hadi nje lakini wakati akijaribu kuvuka barabara ya Kivukoni kuelekea kwenye kibanda cha simu kilichokuwa jirani alisikia mlio wa tairi la gari zikijivuta chini, kwa sababu ya furaha aliyokuwa nayo alikuwa amevuka bila kuangalia pande zote mbili za barabara, lori kubwa aina ya Scania lililobeba wafungwa likielekea Mahakama Kuu lilikuwa mbele yake, pamoja na dereva kufunga breki hakuweza kulifanya gari lishindwe kumfikia Halima, kilichosikika baada ya hapo ni mlio mmoja tu;PAAAAAA! Msichana akaonekana akirushwa hewani na kuanguka upande wa pili wa barabara, damu nyingi zilikuwa zikimtoka puani, masikioni na mdomoni! Watu wote waliokuwa jirani na eneo hilo mikono yao ilikuwa kichwani, wengine wakiwa wamefumba macho ili wasishuhudie kilichokuwa kikitokea.



Msichana wa Kiislamu Halima na mvulana wa Kikristo Gerald, wanakutana shule ya kimataifa ya Tanganyika jijini Dar es Salaam. Bila kutegemea wanajikuta wamekuwa wapenzi mpaka walipomaliza kidato cha sita, Gerald akaondoka Tanzania kuungana na familia yake huko Marekani, baba yake mzee Lutta alikuwa Balozi wa Tanzania nchini humo kabla ya kuhamishiwa Italia. Mawasiliano kati yao yanaendelea vizuri, lakini baadae yanakatika ghafla, Halima anashindwa kuelewa ni kwa nini! Anampenda Gerald kuliko kitu kingine chochote pamoja na kuwepo kwa tofauti ya dini kati yao.

Hivi sasa katika juhudi za kumtafuta Gerald kwa simu na barua pepe bila mafanikio, kila anapopiga simu anajibiwa na mashine! Amechanganyikiwa, kabla ya kujiunga na Chuo moja kwa moja anaamua kwenda Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kutafuta namba ya Mzee Lutta, anaipata na kuondoka kwenye jengo hilo akiwa na furaha kupita kiasi lakini wakati anavuka barabara kwenda upande wa pili kulikokuwa na kibanda cha kupigia simu, lori kubwa lililobeba mahabusu kuwapeleka mahakamani linamgonga! Damu zinamtoka puani, masikioni na mdomoni.

Je, nini kitatokea? Endelea.



Halima alilala kwenye lami katikati ya barabara, akiwa hajitambui. Gari lililomgonga wala halikusimama, lilikwenda moja kwa moja mahakamani na kushusha mahabusu, damu nyingi ilikuwa bado ikiendelea kumtoka masikioni, puani na mdomoni. Watu waliokuwa jirani na eneo hilo walianza kukimbia kuelekea mahali alipolala, ilikuwa ni ajali mbaya kuliko zilizotokea kwenye barabara ya Kivukoni katika siku za karibuni. Baadhi ya akina mama ambao hujishughulisha na kazi ya kuuza chakula kando kando ya barabara, walikuwa wakilia kwa kumuonea huruma Halima, uzuri wake wote wa mchanganyiko wa Mwafrika na Mwarabu ulikuwa umeharibiwa, kichwa chake sehemu ya juu kilikuwa kimebonyea kuashiria mfupa ulikuwa umevunjika na pengine ubongo. Kwa hali hiyo, hakuna mtu hata mmoja aliyetegemea Halima ambaye mpaka wakati huo hakuna mtu aliyemtambua, angepona.



“Keshakufa huyu!” Mmoja wa wanaume alitamka maneno hayo baada ya kumgusa Halima kifuani.

“Maskini msichana wa watu sijui alikuwa akitokea wapi!”

“Nimemwona akitokea hapo Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje!”

“Sasa?” Mwanaume mwingine aliuliza.

“Tumpelekeni hospitali!”

“Sawa simamisha gari!”



Wote wakakubaliana na mmoja wao akasimama pembeni mwa barabara ambako magari yalikuwa yakizunguka na kuanza kupunga mkono hewani, haukupita hata muda mrefu gari aina ya Datsun likasimama, lilikuwa likiendeshwa na mwanamke wa kizungu! Akashuka na kwenda mahali alipolala Halima, alisikitika sana alipomuona katika hali hiyo, nae akainama na kumgusa kifuani, tofauti na aliyemgusa mwanzo, yeye aligundua kwamba moyo wa Halima ulikuwa ukipiga kwa mbali, akakimbia kwenye gari lake haraka na kuchukua mipira na kuvaa mikononi akaja nayo na kuwagawia wanaume wanne, wote wakavaa na kumbeba hadi kwenye gari ambako walimpakia na kuondoka kwa kasi kubwa. Bila kufuata sana sheria za Usalama barabarani walifanikiwa kuwasili Hospitali ya Muhimbili dakika kumi na tano baadae, Halima akashusha na kuingizwa katika chumba cha daktari.



“Kawaje huyu?” Daktari aliuliza.

“Kagongwa na gari!”

“Poleni sana, kuna ndugu yake hapa?” Daktari aliuliza akimpima Halima mapigo ya moyo, alikunja sana uso wake wakati akifanya kazi hiyo, jambo lililoashiria alichokigundua hakikuwa kitu kizuri.

“Hakuna ndugu yake daktari, sisi tumemsaidia tu, kwani vipi?”

“Anahitaji kufanyiwa upasuaji sasa hivi, nina uhakika ingawa bado sijampiga picha ya kichwa chake, lazima atakuwa ameumia kwenye ubongo, na kama atahitaji kufanyiwa upasuaji lazima zinahitajika chupa za damu!”

“Samahani daktari, kwa kweli hapa hakuna ndugu yake!”

“Mko tayari kumsaidia damu?”Wanaume zaidi ya wanne waliokuwemo ndani ya chumba cha daktari walibaki kimya bila kuongea chochote, mama wa kizungu ndiye akakubali kujitolea damu yake, daktari alielewa ni kwa nini wanaume walibaki kimya na wala hawakutaka kuwachimba zaidi. Watanzania wengi tangu tatizo la gonjwa la Ukimwi liingie wamekuwa waoga sana kutoa damu kwa kuhofia kupimwa na kujulikana wameathirika! Wakati daktari anawapigia simu watu wa kupiga picha kichwa, kundi la maaskari magereza liliingia na kujitambulisha ndio waliosababisha ajali hiyo lakini walishindwa kusimama kwa sababu walikuwa wamebeba wafungwa wenye makosa ya mauaji, kusimama kwao pengine kungeweza kusababisha wafungwa kutoroka, wawili kati yao pia walikubali kutoa damu zao, daktari akawatuma pamoja na yule mama wa kizungu kwenye maabara.

Muda huo huo Halima akiwa bado hajitambui na akihema kwa taabu alichukuliwa na kupelekwa chumba cha wagonjwa mahututi ambako mara moja aliwekwa kwenye mashine ya hewa ya oksijeni na nyingine ya kusaidia moyo wake kupiga, dripu zilichomekwa kwenye mishipa ili kusaidia mapigo yake yaliyokuwa yakishuka kwa kasi yapande tena. Yote hayo yalipokamilika, picha ya kichwa cha Halima ilipigwa kwa kutumia mashine iitwayo CT Scanner, majibu yalipotoka yalionyesha kama alivyokuwa amesema daktari, fuvu lilikuwa limevunjika na damu nyingi ilikuwa ikiendelea kuvuja chini ya fuvu na kuugandamiza ubongo. Dk. Othman aliyekuwa akimshughulikia Halima alikuwepo kuangalia majibu.



“ Nilisema, dalili zote za contusion zilikuwepo, ni lazima tufanye upasuaji haraka sana ili kuokoa maisha ya huyu binti, mpigie simu Dk Kantarama na Lema, wafike chumba cha upasuaji sasa hivi, inawezekana wako wodini, wakati haya yanafanyika, mbebeni haraka sana huyu mgonjwa mlete thieta, mimi natangulia, mnasikia?”

“Sawa daktari!”

Dk Othman alifungua mlango na kutoka nje ambako aliwapa taarifa baadhi ya watu waliompeleka Halima hospitali juu ya matokeo ya kipimo cha CT Scanner, wote wakasikitika. Badala ya kutembea kwenda chumba cha upasuaji ingawa palikuwa karibu tu, Dk Othman ilibidi akimbie, alipofika aliingia ndani na kuwataarifu watu wa dawa za usingizi pamoja na wauguzi wa chumba cha upasuaji kwamba kulikuwa na upasuaji wa haraka sana hivyo wajiandae, dakika tano baadae, Dk Kantarama na Lema waliingia, hawa ndio walikuwa mabingwa wa upasuaji katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

“Mgonjwa yuko wapi?” Aliuliza Dk Lema baada ya salam.

“Analetwa sasa hivi kutoka chumba cha wagonjwa mahututi”

“Nini tatizo?”

“Amepata ajali mbaya sana na damu nyingi inavuja chini ya fuvu, tunahitaji kumfanyia upasuaji haraka kuondoa damu iliyoganda na kugandamiza ubongo!”

“Mmefanya CT Scan?”

“Ndio!”

“Ubongo umeharibika?” Dk Kantarama aliuliza.

“Bahati nzuri ubongo wake haukuharibika, nafikiri amepoteza fahamu kwa sababu tu ya ubongo kutikisika pamoja na damu iliyoganda kugandamiza sehemu ya ubongo, ndio maana nataka tumfanyie upasuaji haraka iwezekanavyo, kuchelewa kwetu kutasababisha maisha ya binti huyu kupotea!” Dk Othman aliongea wakati machela inaingizwa chumba cha upasuaji, Halima akiwa amelala juu yake, mpaka wakati huo hakuna mtu aliyemfahamu.

“BP yake?”

“Ilikuwa inashuka, nikamwanzishia Normal saline na sindano ya Hydrocortisone, masista presha yake iko ngapi sasa hivi?”

“Tisini chini ya sabini!”

“Imepanda kidogo, vipi tunaweza kumfanyia?” Dk Othman aliwauliza madaktari wenzake.

“Tumuulize Dk Ngido!” Dk Lema aliongea akimwangalia mwanaume mfupi aliyekuwa amesimama jirani akisikiliza maongezi yao kwa makini, alikuwa bingwa wa dawa za usingizi au kwa kiingereza aliitwa Anaesthesiologist, Hospitali ya Muhimbili ilimwamini kuliko mtu mwingine yeyote kila lilipokuja suala la nusu kaputi!

Dk Ngido alimsogelea Halima akiwa kwenye machela na kumwangalia ndani ya kope, kisha kumpima mapigo ya moyo, akatingisha kichwa chake, hali ya mgonjwa ilimtisha, hata hivyo aliwashauri madaktari waendelee kufanya kila kilichowezekana kupandisha presha ya mgonjwa wakati upasuaji ukiendelea ndani ya chumba cha upasuaji. Walipokubaliana juu ya hilo, suala kubwa likabaki kuwa ni damu, ambayo dakika kumi baadae ilipatikana chupa tatu toka benki ya damu baada ya watu wote waliojitolea kutoa damu kumsaidia Halima, damu yao kuonekana haikuwa sawa na ya mgonjwa. Kwa damu hiyo iliyopatikana, huku upande mwingine kukiwa na maji ya Normal Saline yakiingia kwenye mishipa, operesheni ilifanyika kwa saa nne mpaka kumalizika, Halima akatolewa chumba cha upasuaji akiwa hajitambui na kuendelea kubaki katika hali hiyo kwa wiki nzima ndipo akafumbua macho yake kuangalia, hakuelewa mahali alipokuwa na kumbukumbu zake hazikuwa sawa, hata kilichotokea hakukifahamu.

“We ni nani?” Dk Othman aliyekuwepo pembeni aliuliza.

Halima hakujibu kitu, alibaki kimya na baadae kufumba macho yake.



****



“Yaani huyu mtoto tangu ameondoka hapa Kilosa hata simu?” Mama yake Halima aliuliza.

“Hata mie nashangaa, sio jambo la kawaida, jana nilimpigia simu shangazi yake akaniambia, aliondoka nyumbani asubuhi wiki moja iliyopita akiwa ameaga kwenda Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na kwamba baada ya kutoka huko angekwenda Chuoni kuanza masomo”

“Hata wao hajawasiliana nao tena?”

“Bado!”

“Mh!””Kwa nini unaguna?””Sio kawaida ya Halima kukaa kimya kiasi hicho, labda kwa sababu aliondoka hapa amechanganyikiwa na suala la Gerald, isije kuwa kadanganya anakwenda Wizara ya Nchi za Nje kumbe ndio katoroka kumfuata mwanaume, ninavyomwona huyu mtoto si jambo la ajabu kufanya hivyo!”

“Basi itabidi labda mimi niende kesho Dar es Salaam nikajaribu kufuatilia!”

“Itakuwa vyema!”

Siku hiyo wazazi wa Halima walilala na wasiwasi mwingi, saa tisa na nusu za usiku, Mzee Mohamed aliondoka kwa gari lake aina ya Land Cruiser na kusafiri hadi Dar es Salaam akipitia Morogoro. Kitu cha kwanza alichokifanya baada ya kuingia jijini ni kwenda moja kwa moja hadi kwa dada yake Mikocheni ambako Halima alifikia, wakaondoka hadi Chuo Kikuu kwenye ofisi za Utawala, jibu walilopewa liliwafanya waishiwe nguvu na kuketi kitini.

“Halima alikuja hapa kuripoti, akaonyeshwa chumba akaondoka akiahidi kurudi siku inayofuata lakini hakufanya hivyo, tunashindwa kuelewa yuko wapi!”

“Mungu wangu weee, mtoto huyu atakuwa wapi?” Mzee Mohamed aliuliza akiwa ameshika mikono kichwani.





Baada ya kupoteza kabisa mawasiliano na mpenzi wake Gerald ambaye ni mtoto wa balozi wa Tanzania nchini Marekani na baadaye Italia, Halima mtoto wa mzee Mohamed, mfanyabiashara maarufu mkoani Morogoro anahisi kuchanganyikiwa! Anaamini hawezi kuishi bila Gerald kwani kijana huyo amekwisha muingia sana moyoni mwake, ndiye aliyemruhusu aivunje bikira yake akiamini angemuoa. Ukimya wa Gerald umemfanya Halima ahisi ameachwa kwenye mataa kwani alipoongea naye mara ya mwisho, aliahidi angempigia jioni lakini hakufanya hivyo.

Furaha yote aliyokuwa nayo Halima iliyeyuka, hata matokeo ya mtihani wa kidato cha sita yalipotoka na kuonyesha alikuwa amechaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Gerald vivyo hivyo, hakufurahi hata kidogo, kitu cha muhimu kwake alikuwa Gerald.

Pamoja na maumivu yote aliyokuwa nayo moyoni, Halima aliweza kusafiri mpaka Dar es Salaam kwenda kujiunga na chuo Kikuu baada ya kushauriwa sana na wazazi wake. Jijini alifikia nyumbani kwa shangazi yake Mikocheni na kuanza kufuatilia mambo ya Chuo wakati huo huo akimfuatilia Gerald, hakupata wala fununu za mahali alipokuwa.

Mwisho alifikia uamuzi wa kwenda kwenye ofisi za Wizara ya mambo ya nchi za nje, huko alifanikiwa kupata namba ya baba yake na Gerald. Akiwa na furaha isiyo na kifani, aliondoka mbio Wizarani akielekea kwenye kibanda cha kupigia simu kilichokuwa ng’ambo tu ya barabara ili apige simu Italia, hakukukumbuka kuangalia pande zote za barabara kwani wakati anavuka lori la Magereza lililobeba wafungwa lilimgonga akaanguka chini na damu zikaanza kumtoka, puani, mdomoni na masikioni.

Alibebwa haraka na kukimbizwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambako baada ya vipimo iligundulika damu ilikuwa imevuja chini ya fuvu la kichwa na ubongo ulikuwa umevurugika hivyo kuvuruga kabisa kumbukumbu zake, alikimbizwa chumba cha upasuaji haraka ambako kichwa chake kilifunguliwa, damu iliyoganda ikaondolewa. Baada ya operesheni hiyo alirejeshwa wodini ambako aliendelea na matibabu, wiki moja baadaye alifumbua macho. Daktari alikuwa pembeni mwa kitanda chake.

Je, nini kinaendelea? Fuatilia.



Dk. Othman alimwangalia Halima bila kuyaamini macho yake, kwa maelezo ya namna ajali ilivyotokea ni muujiza ulikuwa umetendeka. Watu wengi waliopatwa na ajali za aina hiyo hawakupona, cha kushangaza ubongo wa Halima wala haukuguswa zaidi ya mshipa mmoja kupasuka na kuvuja damu chini ya fuvu lake, kwa siku kadhaa alikuwa amejaribu kutafakari msichana huyu alikuwa nani bila kupata majibu. Aliamini hakuwa mkazi wa Dar es Salaam, kwa uzuri aliokuwa nao lazima angekuwa anamfahamu na angekuwa amekwisha shiriki mashindano ya urembo.

“Unaitwa nani?” Aliendelea kumuuliza mara kadhaa lakini Halima hakujibu kitu chochote.

“Au hamkupima vizuri daktari, ubongo wake umeharibika?” Muuguzi aliyekuwa pembeni aliuliza.

“Hapana, ubongo wake uko safi kabisa ila ulitingishika na kujikuta amefuta kumbukumbu zote, ndio maana hawezi kukumbuka hata jina lake, si hivyo tu hakumbuki hata kilichotokea mpaka akawa hapa, hali hii inaitwa Tempolary Amnesia!”

“Kwa hiyo unaamini atapona na kurejea katika hali yake ya kawaida?”

“Ndio! Ingawa siwezi kufahamu kumbukumbu zake zitarejea lini”

“Inaweza kuchukua hata mwezi?”

“Hata miezi mitatu!”

“Mh!” Muuguzi aliguna bila kusema kitu kingine zaidi.

Siku zilizidi kukatika mpaka wiki ya pili ikaingia bila kujitokeza mtu hata mmoja aliyedai kupotelewa na ndugu yake na hakuna aliyekwishakumfahamu Halima kati ya madaktari na wauguzi waliomhudumia. Ingawa bila jina walishatoa taarifa polisi, bado hakuna mtu aliyejitokeza. Hatimaye wakaamua kutangaza kwenye televisheni baada ya Halima kuwa na uwezo wa kuketi mwenyewe kitandani na sura yake kuonekana vizuri uvimbe ulipopungua.



************

Mzee Mohamed na dada yake waliondoka Chuo Kikuu wamechanganyikiwa kabisa, vichwani mwao walikuwa na maswali mengi yasiyo na majibu. Walishindwa kuelewa ni wapi alikoelekea Halima baada ya kutoka Chuo Kikuu kuripoti.

“Hakurudi kabisa nyumbani?”

“Ni kweli hakurudi, kwa sababu tangu amekuja tabia yake niliiona imebadilika sana nikafahamu kulikuwa na kitu kilichomsumbua, nilipomuuliza hakutaka kusema, hivyo nilipoona yupo kimya nikajua anaendelea na masomo wala sikujihangaisha naye sana, kumbe hata Chuoni hayupo, unafikiri atakuwa amekwenda wapi kaka?”

“Nahisi jambo moja ingawa sina uhakika nalo sana!”

“jambo gani?”

“Atakuwa ameamua kumfuata mpenzi wake!”

“Yupi?”

“Alituambia ana kijana mmoja mtoto wa balozi wa Tanzania nchini Italia, walikuwa wamekorofishana kidogo, kijana huyo akawa hampigii simu kabisa! Mwanetu alionyesha kuchanganyikiwa kiasi cha kutosha, hata Chuoni alikuwa hataki kuja ila mimi na wifi yako tukamshawishi sana ndio akakubali, hatukujua alikuwa na mpango wa kutoroka, kwa kweli Halima ameniudhi sana! Sina la kufanya kwa sababu ni yeye mwenyewe ameamua, mimi narudi zangu Kilosa, mwache aende huko Italia, asiyefunzwa na mamaye hufunzwa na......”

“Ulimwengu” Shangazi yake Halima alijibu.

“Wewe unaonaje?” Mzee Mohamed aliuliza.

“Mimi naona ni sawa tu, hawa watoto wetu wa siku hizi hawawezekani, yaani yeye anaona mwanaume ni bora kuliko elimu!”

Mzee Mohamed alimrejesha dada yake Mikocheni na saa hiyo hiyo akawasha gari kuelekea Morogoro na baadaye Kilosa, njiani alifikiria mengi kuhusu mwanae roho ikawa inamuuma sana, alimpenda Halima, ndiye alikuwa mtoto pekee mkubwa katika familia yake na alipenda sana asome.

Nyumbani alifika akiwa na huzuni nyingi, mke wake ndiye alikuwa wa kwanza kumgundua na kuanza kudadisi.

“Baba Halima mbona uko hivyo? Kuna nini?”

“Nitakwambia acha nipumzike kwanza!”

“Unajua kabisa siwezi kuvumilia muda mrefu, tafadhali niambie, Halima ana matatizo? Yuko hai? Nieleze sio kawaida yako wewe kuwa katika hali hiyo!”

Mzee Mohamed bado hakutaka kusema chochote, aliendelea kuinamisha kichwa chake huku machozi yakimlengalenga. Kuona hivyo mama yake Halima alishindwa kuvumia akaondoka hadi chumbani ambako alijifungua na kupiga simu Dar es Salaam kwa wifi yake akitaka kuujua ukweli.

“Halima katoroka!”

“Katoroka?”

“Kwani baba yake hajakueleza wifi?”

“Kagoma kabisa!”

“Anaogopa kuamsha presha yako!”

“Basi wewe nieleze!”

“Tumekwenda Chuoni tukakuta hayupo, mpokeaji wa wanafunzi ametueleza alifika hapa mara moja na kuripoti kisha akaondoka akiahidi kurejea, hakutokea tena!’http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Sasa atakuwa wapi mtoto huyu?”

“Baba yake amesema inawezekana ametoroka kwenda Italia kwa mpenzi wake!”

“Mlipata nafasi ya kufuatilia Ubalozini kuona kama alichukua viza?”

“Hatukufanya hivyo wifi!”

“Hapo mlifanya kosa, mnaweza mkasema ametoroka kumbe ana matatizo makubwa!”

“Ni kweli wifi!”

“Mlikwenda kwenye vituo vya polisi!”

“Hapana wifi!”

“Wifi kwanini mnafanya mambo kama watoto wadogo?”

“Kaka alikuwa amekasirika sana, nisingeweza kumwambia chochote akanisikiliza!”

“Tunakuja huko sasa hivi!” Aliongea mama Halima na kukata simu.

Alichofanya ni kurejea sebuleni ambako alimueleza mzee Mohamed kila kitu kilichotokea Dar es Salaam kama alivyosikia kutoka kwa wifi yake kwenye simu.

“Sasa ulikuwa unanificha nini?”

“Sikutaka kukuumiza mapema!”

“Sasa sikiliza, mimi na wewe tunarudi Dar es Salaam sasa hivi kuendelea kumtafuta mwanangu!”

“Utampataje kaishaondoka nchini?”

“Nani kakuambia hivyo baba Halima?”

“Sasa wewe unafikiri atakuwa amekwenda wapi? Si ajabu wewe unafahamu, nyie akina mama huwa mnaelewa mipango ya watoto wenu wa kike tena usinitibue, ondoka mbele yangu”

“Baba Halima acha ukali mume wangu, nakusihi ukubali tusafiri pamoja kurudi tena Dar es Salaam, kama amekwenda Italia basi tukatafute hiyo namba ya Balozi katika ofisi za Wizara ya nchi za nje, tukiipata tupige na kuomba kuongea naye, kama yuko huko kweli basi atarudi.

“Sawa, twende, nimechoka lakini sababu ya mwanagu nitakwenda”

Tayari ilikuwa saa tatu na nusu ya usiku, mzee Mohamed na mkewe waliiaga familia yao na kuondoka kurejea Dar es Salaam, usiku huo huo majira ya saa tisa waliwasiri katikatika ya jiji la Dar es Salaam. Hawakuta kumsumbua mtu yeyote wakati huo wa usiku, walichofanya ni kulala kwenye gari kwenye kituo cha mabasi cha Ubungo, siku iliyofuata asubuhi walikuwa watu wa kwanza kufika kwenye jengo la Wizara ya mambo ya nchi za nje.

“Tunaomba kumuona mtu anayehusika na Ubalozi wa Italia!”

“Shida yenu?”

“Tunaomba namba ya balozi Lutta!” Mzee Mohamed aliongea kwa sauti ya unyonge, mke wake akiwa pembeni, macho mekundu sababu ya kulia! Alimpenda mno Halima, alikuwa mtoto pekee wa kike waliyekuwa naye na tegemeo la familia nzima. Utajiri wote aliokuwa nao baba yake ulikuwa ni wa kwake ndio maana walimpeleka katika shule nzuri ili aweze apate uwezo wa kuendeleza mali za baba yake, kitendo cha kutoroka kama alivyokuwa akielewa kilikuwa kimemuuza sana.



“Nina namba ya ofisini tu!”

“Tusaidie hata hiyo hiyo!”

“Ya nini?”

“Ni ndugu yetu, nataka kuwasiliana naye kabla sijasafiri kwenda huko!” Ilibidi mzee Mohamed adanganye, haikuwa tabia yake lakini siku hiyo hakuwa na jinsi alitaka kufahamu mahali alipokuwa mtoto wake mpendwa Halima.

“Ok!”Aliongea mwanamke waliyemkuta, hakuwa na maneno mengi alichukua kitabu kidogo mezani kwake kilichoandikwa juu maneno “Balozi zetu nje” akanakili namba ya ubalozi wa Tanzania nchini Italia na kumpatia mzee Mohamed kwenye karatasi kidogo, wakamshukuru na kuondoka zao.



Nje waliingia ndani ya gari lakini kabla ya kuondoka walijadiliana na kuona ilikuwa inafaa waende kwenye jengo la EX-Telecoms, mtaa wa Samora katikati ya jiji kuliko kuwa na mahali ambako huduma za kupiga simu nje zilitolewa, wakakubaliana na kuondoka kwa kasi hadi mbele ya jengo hilo ambako gari liliegeshwa, siku hiyo mzee Mohamed wala hakufuata sana sheria za usalama wa barabarani, wote wawili wakashuka na kuanza kutembea hadi kwenye chumba cha kupigia simu.



“Tusaidie Italia binti!” Mzee Mohamed alimwambia msichana aliyemkuta nyuma ya meza kubwa yenye vichwa vingi vya simu juu yake.

“Shilingi mia moja dakika!”

“Sawa tu!”

“Namba?”

“Hii hapa!”

Binti huyo alianza kubonyeza kwenye namba alizopewa, haukupita hata muda mrefu akamkabidhi mkono wa simu mzee Mohamed, mke wake akiwa ameketi pembeni akiangalia kila kitu kilichoendelea! Masikio yake yalikuwa yamefunguliwa vizuri, jambo pekee alilotaka kusikia ni kwamba, Halima alikuwa Italia na angekubali kurejea nchini mara moja kuendelea na masomo.



“Huyu mtoto anataka kuniua na presha!” Aliwaza mama yake Halima akimsikiliza kwa makini mume wake akiongea kwenye simu, hakutaka apitwe na neno hata moja.

“Hapa ni Tanzania…hapo ni Italia?.. naomba kuongea na Balozi Lutta… hayupo?...yuko Verona?...oh! Mungu wangu!...nilikuwa na shida naye…kijana wake aitwaye Gerald je?...ni mgonjwa?...Figo?... kwa hiyo hujamwona binti mmoja wa mchanganyiko wa Mwarabu na Mwafrika?...kweli?...ok! kama mnaishi nyumba moja basi ahsante!...hapana sina ujumbe…!” Alimaliza mzee Mohamed na kukata simu, mke wake alishakiacha kiti, muda wote wakati akiongea alikuwa amemkumbatia na sikio lake moja likiwa karibu kabisa na sikio ambalo mzee Mohamed alilitumia kuongea na simu, machozi zaidi yalimbubujika.Baada ya maongezi hayo mzee Mohamed alilipa shilingi mia mbili na kumshika mkono mke wake, wakatoka hadi nje na kuingia kwenye gari.



“Vipi?”

“Nimeongea na kijana mmoja, anasema anaishi nyumba moja na Balozi Lutta, ndio nyumba waliyopangishiwa na serikali, kifupi kaniambia balozi Lutta hayupo ofisini yuko katika mji mmoja unaoitwa Verona huko Italia, mtoto wake Gerald ambaye Halima huwa anamwongelea sana ni mgonjwa, figo yake moja imekufa na balozi Lutta amempeleka kwenye hospitali moja kubwa katika mji huo ili kwenda kutafuta figo nyingine ya kumwekea!”Aliongea mzee Mohamed, mke wake akilia.



“Sasa tutafanyaje?”

“Twende Mikocheni kwa dada tukaongee vizuri!”

“Vyema, lakini mimi nahisi hapa kuna mpango unaendelea, si ajabu ni uongo, huyo Gerald kama anaishi nyumba moja na huyo kijana uliyeongea naye amepanga mpango wa kutudanganya, inawezekana akawa amemwambia mtu yeyote akipiga simu kutoka Tanzania kumuulizia msichana wa aina fulani mwambie hayupo na hata akitaka kuongea na baba mwambie pia hayupo, tunatakiwa kutumia akili!”Mama yake Halima aliongea mzee Mohamed akisikiliza kwa makini, mtu yeyote mwenye akili timamu angeweza kuwaza kama mama huyo, maneno yake yalimwingia mzee Mohamed moja kwa moja kichwani mwake na kuanza kuzunguka ubongoni, mpaka wanafika nyumbani kwa shangazi yake na Halima tayari alishaanza kukubaliana na mawazo hayo.



“Karibuni! Mmerejea tena?”

“Haiwezekani kukaa Kilosa wakati mtoto hajapatikana!”

“Kweli kabisa, ingieni ndani!Wifi jikaze, nina uhakika mtoto yuko hai, ni haya mambo ya vijana wetu ya kushindwa kufanya uchaguzi mwema maishani mwao, njooni tujadiliane nini cha kufanya”



Kilichoendelea sebuleni ndani ya nyumba kilikuwa ni kumpa habari shangazi yake Halima juu ya kilichoendelea baada ya mzee Mohamed kuondoka, walimweleza kila kitu mpaka namba ya simu walivyoichukua Wizara na maongezi yaliyofanyika kati ya Mzee Mohamed na kijana mmoja wa Ubalozini nchini Italia, alipomaliza kuongea mzee Mohamed alimwangalia dada yake.

“Kaka, hapa kuna mchezo, usikubali, jambo la kufanya hapa ni moja tu, nenda Italia moja kwa moja ukajionee mwenyewe kama mtoto hayupo, mimi nahisi wamemficha labda huyo Gerald anataka kumuoa! Inawezekana wapi mtoto wa Balozi awe anaumwa figo tena anataka kubadilishiwa tusisome hata kwenye Magazeti? Huo ni uongo, kaka nenda, Italia sio mbali ni safari ya siku moja au mbili umefika!”

“Mimi nimemwambia, haiwezekani hapa kuna mchezo!” Mama yake Halima aliongea.

Wote walikuwa gizani, hakuwepo mtu wa kuwaeleza juu ya kilichotokea! Baada ya kushawishiwa sana hatimaye Mzee Mohamed alikubali ushauri aliopewa, siku hiyo hiyo wakaenda ubalozini kutafuta viza, wakiwa hapo walijaribu hata kuulizia kama kuna mtu mwenye jina la Halima Mohamed aliyechukua viza na kuondoka lakini hawakupata jina hilo, wakahisi labda aliondoka kwa kupitia Nairobi Kenya. Saa tisa alasiri siku hiyo hiyo walifanikiwa kupata viza, hapakuwa na kitu kingine tena kilichohitajika isipokuwa tiketi, wakirudi kutoka ubalozini walipitia ofisi ya shirika la Ndege la Uholanzi ambako mzee Mohamed alikata tiketi ya kuondoka siku hiyo hiyo saa tano na nusu usiku.

Waliporejea nyumbani jambo pekee lililofanyika ni maandalizi ya safari, muda wote walikuwa ni wenye huzuni, hakuna mtu hata mmoja aliyefikiria kusikiliza redio wala kuangalia televisheni! Ulikuwa ni msiba, mioyoni mwao walihisi mtoto wao alikuwa katika hatari au hakuwa duniani kabisa.



Saa tatu na nusu usiku tayari walikuwa uwanja wa ndege wa Dar es Salaam wakisubiri muda wa kuingia, mama na shangazi yake Halima walimsindikiza mzee Mohamed, mbele ya mahali walipokaa kulikuwa na televisheni kubwa iliyokuwa ikionyesha mambo mbalimbali hakuna mtu hata mmoja aliyeijali wala kuitupia macho, hakikuwa kitu muhimu kwao na ilipogonga saa nne kamili mzee Mohamed aliwakumbatia wote na kuwaaga, akaingia ndani ya uwanja.

Mama na shangazi yake Halima hawakuondoka mara moja, walibaki hapo kwa muda wakimwangalia mzee Mohamed kupitia kwenye vioo akishughulikia tiketi yake mwisho akawapungia na kutokomea ndani, wakabaki kwa dakika nyingine kumi na tano wakiwa kimya, ndege zilisikika zikiruka na kuiacha ardhi ya Tanzania.

“Wifi twende!” Shangazi yake Halima alimwambia mama Halima akigeuka kuangalia kwenye luninga.

“Subiri kidogo wifi!”

“Kha!” shangazi yake alishtuka.

“Vipi wifi?”

“Yule sio Halima?”

“Wapi?”

“Kwenye luninga?”

Picha ya msichana akiwa amefungwa bendeji kichwani ilionekana, wote wawili wakanyanyuka na kusogea karibu kabisa na luninga ili kuhakikisha walichokiona, haikuwa rahisi kuamini. Macho yao yalikuwa hayawadanganyi,Halima alikuwa kwenye luninga, mwanaume mrefu mnene aliyevaa koti jeupe akiwa amesimama pembeni yake akiongea.

“…kwa hiyo yeyote aliyepotelewa na ndugu yake anaweza kufika wodi ya MOI, hapa Muhimbili aulizie Dk. Othman…”

Macho yao yalionekana kutoamini walichokuwa wakikiona, ikabidi waisogelee luninga hiyo mpaka karibu kabisa, kiasi cha mita moja na kuiangalia vizuri picha iliyokuwa ikionekana mbele yao, wakagundua macho yao yalikuwa yakitafsiri ukweli, alikuwa ni Halima kichwa chake kikiwa kimefungwa bendeji kila upande huku macho yake yakiwa yamevimba na yenye rangi nyekundu kwa ndani sababu ya kuvilia damu. Shangazi yake Halima aliruka juu na kushangilia akimshuhudia mama yake akibubujikwa na machozi.



“Ni yeye!” Mama yake Halima aliongea akimsogelea wifi yake na kumkumbatia.

“Kweli kabisa!”

“Kumbe alipata ajali!”

“Hakika!”

“Sasa tufanyeje kuhusu baba yake?”

“Twende pale dirishani!” Shangazi aliongea akimwonyesha mama Halima dirisha lililoandikwa INTERLINE.

“Tukafanye nini?”

“Tukawaombe wapige simu ndani sehemu ya kusubiria ndege ili baba Halima aahirishe safari!”

“Atakuwa hajaondoka kweli?”

“Sijui wacha tujaribu!”

Wote wawili wakatembea kwa haraka hadi dirishani, ndani ya ofisi hiyo walimkuta mwanaume mrefu mweusi ambaye baada ya kujitambulisha kwake aliwaeleza yeye aliitwa Thabit, wakamweleza historia fupi ya tatizo lao na kuomba awasaidie ili mzee Mohamed asiondoke.



“Tutawahi kweli?”

“Tafadhali tusaidie!”

“Nina wasiwasi milango isijekuwa tayari imekwishafunga!”

“Tafadhali jaribu!”



Akiwaangalia kwa macho ya huruma, mwanaume huyo alinyanyua simu na kuanza kubonyeza namba kadhaa, sekunde chache baadaye alianza kuongea na mtu upande wa pili, akamsimulia kila kitu juu ya msaada ambao watu waliokuwa mbele yake waliuhitaji.



“…ndio…naomba utusaidie…basi tunasubiri…!” Alisema maneno hayo mama Halima na wifi yake wakiwa kimya, vichwa vyao vikicheza kufuatia namna alivyokuwa akiongea.



“Vipi kasemaje?” Mama Halima aliuliza baada ya Thabit kukata simu.

“Tayari wamekwishaingia kwenye ndege, lakini anajaribu kuwasiliana na watu waliomo ndani ili waone kama wanaweza kusaidia…mnaweza kuketi pale kwenye kiti mkasubiri, wamesema watanipigia simu!”

“Ahsante!” walijibu kwa pamoja na kuanza kutembea mpaka mbele ya ofisi hiyo kulikokuwa na benchi, wakaketi kimya kila mtu akitafakari maneno yake kichwani. Ubongo wa mama halima ulitawaliwa na picha aliyoiona kwenye luninga, alitaka mume wake apatikane ili waondoke pamoja kwenda Muhimbili, alitamani sana hata kama Halima angekuwa zezeta lakini awe hai, kuliko kufa. Akiwa ameketi aliendelea kuswali na kumwomba Mwenyezi Mungu atende muujiza kama aliokwishatenda tayari.



Macho yao yote yalikuwa yameelekezwa kwenye dirisha na INTERLINE ambako dakika tano baadaye walimwona Thabit akiongea na simu huku uso wake ukiwa umejawa na tabasamu na macho yake yakiwaangalia wao, mama Halima akashusha pumzi na kuamini mambo yalikuwa yamekwenda vizuri! Alipokata simu Thabit, aliwaonyesha ishara ya kuwaita, wote wawili wakatembea haraka hadi dirishani.



“Vipi?”

“Mna bahati, milango ilikuwa bado hajaifungwa!”

“Ahsante Mungu!” alitamka maneno hayo Mama Halima.

“Sasa?” Shangazi akauliza.

“ Nendeni mkamsubiri kwenye mlango wa kutokea, anakuja sasa hivi!”

Wakashukuru na kuondoka hadi kwenye lango waliloelekezwa lililopo upande wa Mashariki mwa Uwanja, dakika kumi tu baadaye, mzee Mohamed alionekana akisukuma mzigo wake kutoka ndani ya uwanja hadi nje ambako walimpokea na kuanza kumbusu kwa furaha!

“Imekuwaje tena?”

“Baada ya wewe kuondoka tu, tulitupa macho kwenye luninga na kumwona Halima, hajatoroka kwenda Italia!”

“Yuko wapi?”

“Yuko hospitali ya Muhimbili, alilazwa kumbe alipatwa na ajali!”

“Mnasema kweli?”

“Kabisa, twende tu tukamwone!”

Mzee Mohamed akiwa amejawa na furaha moyoni mwake, bila kuamini kilichokuwa kikitendeka, alitupa macho kwenye saa yake na kugundua ilikuwa tayari ni saa nne na dakika thelathini na tano, wote watatu wakaondoka mbio hadi mahali gari lilipoegeshwa. Mzee Mohamed ambaye wakati huo angekuwa kwenye ndege, akisubiri kupaa, alikaa nyuma ya usukani, akaomba ufunguo kutoka kwa dada yake ambaye alimkabidhi, akawasha na kuliondoa gari kwa kasi kubwa. Upungufu wa magari barabarani wakati huo wa usiku uliwafanya wawasili Muhimbili dakika ishirini tu baadaye na kuegesha.



“Tuanzie wapi?”

“Mapokezi!”

“Hiyo itakuwa ni njia ndefu, kwani mlisikia kalazwa wodi gani?”

“MOI!”

“Sio hapa tuzungukeni upande wa pili!” Mzee Mohamed alisema na wote wakaingia kwenye gari, akawasha na kuondoka kuelekea nyuma ya hospitali ambako kitengo cha Mifupa kilikuwepo, akaegesha kwa mara nyingine na wote wakashuka na kuanza kukimbia hadi mapokezi.



“Habari za leo mama?”

“Nzuri tu, niwasaidie?”

“Ndio! Binti yetu amelazwa hapa leo ni wiki ya pili, hatukuwa na habari ila tumeona kwenye luninga wakati wa taarifa ya habari!”

“Yupo huyo?”

“Anaitwa Halima!”

“Hebu subirini niangalie kwenye daftari, alilazwa lini?”

“Wiki iliyopita!”

“Mnakumbuka tarehe?”

“Hapana!”

Bibi huyo alianza kuchambua majina ya wagonjwa wote waliolazwa katika kitengo hicho kwa mwezi mzima, hakufanikiwa kuona jina la Halima, akawageukia na kuwauliza kama kulikuwa na jina jingine lolote tofauti na hilo ambalo mgonjwa alilitumia.

“Hakuna!”

“Sasa mbona simwoni? Anaumwa nini?”

“Alipata ajali ya kugongwa na gari!”

“Huyu anayetangazwa kwenye luninga?”

“Ndio!”

“Yupo chumba namba 106 lakini nasikitika hamwezi kumwona sasa hivi!”

“Kwanini?” Mama Halima aliuliza.

“Huu ni muda wa wagonjwa kupumzika, haturuhusiwi kuingiza mgeni mpaka saa kumi na mbili asubuhi, hivyo nawashauri rudini nyumbani mje asubuhi!”

Walimbembeleza bibi huyo kwa muda lakini hakukubali, mzee Mohamed akadiriki hata kupenyeza noti ya shilingi elfu kumi lakini bado bibi huyo hakukubali! Walichofanya ni kutoka nje ya jengo la hospitali na kuingia kwenye gari ambako walilaza viti na kupumzika hadi saa kumi na mbili asubuhi, bila kunawa uso wala kupiga mswaki wakiwa wamechoka taabani wakasogea kwenda mapokezi ambako waliruhusiwa kuingia na kwenda moja kwa moja hadi chumba namba 106.

Halima alikuwa amelala kitandani, macho yake yakiwa yamefunguliwa, mama yake akapiga magoti chini na kuanza kumbusu usoni kwa furaha! Baba yake pamoja na Shangazi wakasujudu na kuanza kuswali wakimshukuru Mungu, waliponyanyuka wote watatu wakakizunguka kitanda na kuanza kumwita Halima lakini hakuwaitika, ingawa alikuwa akiwaangalia kabisa kwa macho yote mawili alionekana kutowatambua.

“Halima! Halima mwanangu, unanitambua mimi?” mzee Mohamed aliongea lakini Halima hakujibu chochote, alizidi kumshangaa.

Waliendelea kumwita bila kuitikiwa mpaka saa moja na nusu Dk. Othman alipoingia akifuatana na wauguzi wawili, wote walishangaa kukuta watu wamezunguka kitanda cha mgonjwa wao.

“Karibuni, ninyi ni akina nani?”

“Wazazi wa huyu binti!”

“Mlikuwa wapi siku zote?”

“Hatukuwa na habari kama amepatwa na tatizo hili, ni jana tu tuliona kwenye luninga!”

“Wala hamkugundua kwamba amepotea?”

“Sisi tunaishi Kilosa, huyu ni shangazi yake anaishi hapa jijini, alikuja hapa kujiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam, nafikiri alipata ajali akiwa katika hatua za mwisho za kujiandaa maana chuo kikuu alikuwa ameshakamilisha kila kitu! Lakini ni kitu gani kilichotokea daktari?”

“Alipata bahati mbaya ya kugongwa na lori la polisi lililobeba mahabusu nje ya jengo la Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, akaletwa hapa kwetu, tulipopima ubongo wake tuligundua haujaharibika ila umetingishika kiasi kwamba kumbukumbu zote zimefutika! Hapa alipo haelewi kitu chochote, kila kitu kitakuja taratibu!”

“Atapona? Iko siku atakuwa kama zamani? Ataweza kuendelea na Chuo Kikuu?” Mama yake aliuliza.

“Kupona amekwishapona, hawezi kufa tena, kitakachochelewa ni kumbukumbu zake!”

“Unafikiri zinaweza kurejea lini ili aendelee na shule?”

“Siwezi kuliongelea suala hili kwa uhakika, wengine huwa wanawahi na wengine wanachelewa, kuna watu huwa wanafikia mpaka mwaka mmoja!”

“Mungu wangu!!” Mama yake Halima alitamka maneno hayo kwa huzuni.

Haikuwa rahisi kuamini kuwa Halima msichana aliyekuwa na sura ya kuvutia ndiye alikuwa katika hali mbaya kiasi hicho, kichwa chake kikiwa kimevimba na kufungwa bandeji kufuatia upasuaji aliofanyiwa ili kuondoa damu iliyoganda chini ya fuvu lake, wazazi wake hawakuamini kilichokuwa kikionekana mbele yao! Pamoja na hali ya mtoto wao kuwa mbaya, akiwa hana kumbukumbu za kila kitu kilichotokea, walifurahi hatimaye kumpata akiwa hai, hasa baada ya daktari kuwahakikishia ya kwamba Halima angepona ingawa kumbukumbu zake zingechelewa kidogo kurejea.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Ilivyoonekana ni kama ndoto yake ya kusoma na kufikia kiwango cha juu kielimu ilikuwa imefikia mwisho, hapakuwa na mtu mwenye uhakika kama kweli angerejea kwenye hali yake ya kawaida kati ya watu watatu baba, mama na shangazi yake waliosimama chumbani wakiendelea kumshukuru Mungu! Waliendelea kumwita lakini hakuitika, alipowaangalia alionyesha wazi kuwa hakuwafahamu, kichwa chake hakikuwa na kumbukumbu yoyote.



“Halima! Halima mwanangu, mimi mama yako!” Mama yake alisema lakini hakujibiwa.

“Sasa hivi mnasumbuka bure kumwita, hakuna anachokielewa, itachukua muda mrefu kama nilivyokwishasema kwa Halima kumtambua mtu, mwacheni apumzike, nyie mshukuruni Mungu kwamba mmepata mtoto wenu akiwa hai, ilikuwa ni ajali mbaya mno hata mimi mwenyewe nashangaa imekuwaje ubongo wake haujaharibika! Kweli Mungu yupo, leo ndio nimeamini!” Dk. Othman aliongea akiwaomba mzee Mohamed, mkewe na shangazi watoke nje ili aendelee kumhudumia mgongjwa, hawakuwa wabishi walifanya kama walivyoagizwa.



Mlangoni wakati wakitoka nje walipishana na wauguzi wakisukuma kitoroli kidogo kuingia chumbani kwa Halima ambako Dk. Othman alikuwa akisubiri, nje ya wodi walisimama kwa karibu dakika tano bila kuongea chochote kila mmoja wao akitafakari juu ya kilichotokea.



“Utafanya nini sasa kuhusu hiyo tiketi?” Shangazi yake Halima, Bi. Mwajuma aliuliza.

“Hiyo ndio basi tena!”

“Kwanini? Si hukusafiri?”

“Ningekuwa sijapewa hati ya kuingilia kwenye ndege ningeweza kurudishiwa fedha zangu, ukishapewa kitu kiitwacho Boarding Pass, si rahisi kurudishiwa fedha maana huwa inachukuliwa kama umesafiri!”

“Kwa hiyo ndiyo basi tena?”

“Haijalishi sana ili mradi nimempata mwanangu mpendwa, fedha tutatafuta baadaye!”

“Kweli kabisa!”Mama yake Halima aliongea.

Huo ndio ukawa mwanzo wao kuishi hospitali kumuuguza mtoto wao, wakibadilishana mmoja baada ya mwingine, wiki ya kwanza ikakatika, ikaja ya pili, hatimaye ya tatu mpaka mwezi ukaisha Halima bado alikuwa hospitali kumbukumbu zake hazijarejea ingawa alishakuwa na nywele tayari zilishaota na kuanza kufunika sehemu ya kichwa chake iliyopasuliwa! Hawakuelewa nini kingetokea mpaka kumbukumbu zake zirudi, walimsumbua sana Dk.Othman kwa swali hilo naye aliendelea kuwahakikishia kuwa siku moja Halima angerejea katika hali yake ya kawaida ingawa kama ilivyokuwa kama kule mwanzo hakuwaahidi ni lini.



“Nategemea kuwaruhusu mrudi nyumbani kesho, Halima ataendelea kutumia dawa huko huko na mtakuwa mnamleta hapa kwa uchunguzi kila wiki ili tuone maendeleo yake, hospitalini si pazuri sana kumweka mgonjwa ambaye amefikia hali kama ya kwake, mwisho anaweza kupata magonjwa mengine ambayo hakuja nayo hapa! Sawa ndugu zangu?” aliuliza Dk. Othman wakati alipopita chumbani kwa Halima kumpima.

“Hakuna shida!” Mzee Mohamed na mkewe waliokuwepo wodini siku hiyo waliitikia.

Kama alivyosema daktari, kweli siku iliyofuata Halima aliruhusiwa kutoka hospitali, kwa kumwangalia alikuwa amepona kabisa, tatizo pekee alilokuwa nalo ni kumbukumbu! Mtu yeyote aliyemwona kama hakuwa na taarifa juu ya tatizo alilokuwa nalo, haikuwa rahisi hata kidogo kutambua kuwa alipatwa na ajali na kufanyiwa upasuaji wa kichwa au hakuwa na kumbukumbu juu ya kilichotokea na hata jina lake mwenyewe, wazazi wake walikuwa akina nani na kwamba alipatwa ajali hiyo akitoka wapi, kufanya nini! Hata jina la Gerald mvulana aliyesababisha apatwe na ajali hiyo akitokea Wizara ya Mambo ya nchi za nje kutafuta namba ya simu ya Italia ambako baba yake alifanya kazi kama balozi wa Tanzania nchini humo, pia halikuwemo kichwani mwake.



Mchana wa saa saba na nusu shangazi yake Halima aliwasili hospitali akiwa na gari lake, kwanza wakasomba mizigo na kupakia, baadaye Halima akasaidiwa kusimama na kutembea mwenyewe hadi kwenye gari, mlango ukafunguliwa akapanda akiwa kimya kabisa, gari likaondoka hadi Mikocheni ambako maisha ya kuuguza yaliendelea, dawa pekee alizopewa wakati huo ilikuwa ni vitamini B12 na vitamini C ili kusaidia ubongo wake kurejea katika hali ya kawaida.



Akiwa kwa shangazi yake wanafunzi aliosoma nao shule ya Kimataifa ya Tanganyika walikuja mara kwa mara kumwona kama walivyofanya alipokuwa hospitali, wengi wao walikuwa Chuo Kikuu lakini hata wao wao alipowaona pia hakuwatambua! Hali ikaendelea hivyo kwa muda wa wiki tatu zaidi, taarifa zikiwa tayari zimeshatolewa Chuo Kikuu kuwa hali ya Halima bado haikuwa nzuri na uongozi wa Chuo uliendelea kutoa muda zaidi ili mara tu kumbukumbu zake zikirejea arejee chuoni kuendelea na masomo yake, lakini asiwe amezidisha mwezi mmoja na nusu, zaidi ya hapo ingebidi arudie mwaka.



Mwezi ukaisha, hatimaye wiki moja zaidi! Zikiwa zimebaki siku chache tu kabla mwezi mmoja na nusu haujakatika, katikati ya Usiku mzee Mohamed akiwa amelala kwenye chumba cha wageni na mama Halima pamoja na shangazi yake wakiwa kwenye chumba ambacho Halima alilala, walishtushwa na kelele za mtu akilia, mwanzoni walifikiri labda ni ndoto lakini walipotulia waligundua Halima alikuwa akilia kwa sauti ya juu.



“Nakufaa!Nakufaa! Nisaidieni, gari linanigonga!” Alizidi kupiga kelele, wakanyanyuka na kumshikilia, mwili wake wote ulikuwa ukivuja jasho, dakika mbili baadaye mzee Mohamed aliingia.



“Vipi?”

“Ameamka na kuanza kupiga kelele, anadai gari linamgonga!”

“Fahamu zake zimerejea, Mungu ni wa ajabu, hivi ndivyo Daktari alivyosema itatokea… Halima, ”

“Bee baba!”

“Vipi?”

“Gari baba, linataka kunigonga!”

“Liko wapi?”

Akatulia huku akihema kwa nguvu , hakuwa na jibu, haikuwa ndoto bali kumbukumbu zilikuwa zimerudi, akaangalia huku na huku chumbani na kugundua alikuwa amelala chumba alichotumia akiwa kwa shangazi yake! Akawaangalia pia watu waliokuwa chumbani na kuwatambua, akamwamkia mama na baadaye shangazi yake. Kisha kuendelea kuwasimulia kila kitu kilichotokea, alikuwa akitoka wapi kufanya nini, hakuamini alipoambiwa baadaye kwamba alikuwa amelala kitandani kwa karibu miezi mitatu bila kumbukumbu! Alishangaa zaidi alipoambiwa kweli ajali ilitokea na alishafanyiwa mpaka upasuaji wa kichwa kuondoa damu iliyoganda.



“Siamini!”

“Huo ndio ukweli!” baba yake alijibu.

“Baba Halima hebu mpigie simu daktari Othman umtaarifu juu ya habari hizi njema, atafurahi mno kusikia Halima amerejewa na fahamu zake, anampenda mno mtoto wangu!”



Mzee Mohamed aliondoka chumbani kwenda kwenye chumba alicholala ambako alichukua simu yake na kuanza kubonyeza akitafuta jina la Dk. Othman, alipolipata alibonyeza kitufe cha kupigia, sekunde chache tu baadaye, sauti ya daktari Othman ilisikika.



“Daktari!”

“Naam!”

“Halima amerejewa na fahamu zake sasa hivi!”

“Kweli?”

“Ndio!”

“Mko wapi?”

“Mikocheni karibu na kwa Nyerere!”

“Nakuja!”

“Ukifika kwenye sheli ya BP, nipigie simu nije nikuchukue!”

“Sasa hivi nafika hapo, naishi hapa Kijitonyama si mbali sana na Mikocheni!”



Simu ikakatika, Mzee Mohamed akarejea chumbani na kuwapa taarifa juu ya ujio wa Dk.Othman, dakika kumi na tano baadaye simu ikalia, mzee Mohamed akaondoka hadi kituo cha mafuta cha BP ambako alimkuta Dk.Othman akimsubiri kwenye gari, wote wakapanda na kuelekea nyumbani kwa shangazi yake Halima, gari likaegeshwa na wote wakashuka na kuingia ndani ya nyumba mzee Mohamed akiwa ndani.



“Mungu ni wa ajabu!” Dk.Othman aliongea baada ya kumwona Halima.

“Sana!”

“Halima hujambo?”

“Sijambo Daktari!”

“Unanifahamu mimi?”

“Ndio mara ya kwanza kukuona!”

“Huwezi kunikumbuka, naitwa Othman, daktari katika hospitali ya Muhimbili ni mimi niliyekupokea mara ya kwanza ulipoletwa, nikahangaika na wewe mpaka dakika hii! Hali yakoilikuwa mbaya lakini nilijitahidi kadri ya uwezo wangu, sikutaka ufe, msichana mzuri kama wewe hukutakiwa kufa wakati ukiwa kijana namna hii!”

“Ahsante daktari kwa wema wako, kwa maelezo niliyopewa ninafahamu bila wewe nisingekuwa hai! Wewe ni daktari kijana lakini unafanya mambo makubwa, nimefurahishwa na kazi yako, sijui nikulipe nini!”

“Hakuna cha kunilipa, mimi kama daktari kazi yangu ni kuokoa maisha ya watu, basi! Kazi hiyo nimeifanya kwako kama nilivyoifanya kwa watu wengine!” Dk. Othman aliongea kwa upole, wazazi na shangazi yake Halima wakimwangalia kwa makini, sauti yake ya upole na mvuto ilikuwa na uwezo wa kumfanya mtu yeyote aache shughuli zake na kumsikiliza.

Halima alipomwangalia usoni aliugundua uzuri wake, lakini ghafla picha ya mtu mwingine; GERALD, ikamwijia kichwani mwake, machozi yakaanza kumbubujika.



Halima amenusurika kifo cha ajali mbaya ya gari, aligongwa na gari la polisi lililobeba wafungwa akitokea Wizara ya Mambo ya nchi za nje kufuatilia namba ya simu ya Balozi Luta, baba yake Gerald. Huyu ni mpenzi wake waliyesoma pamoja katika shule ya Kimataifa ya Tanganyika na kukubaliana kufunga ndoa mara tu wakiingia chuo Kikuu lakini kijana huyo baada ya kurejea Marekani alipotea katika mawasiliano, jambo lililoashiria kuwa amemtema Halima.

Halima aliumia sana kwa sababu alimpenda Gerald kuliko kawaida mpaka kufikia uamuzi wa kumpa heshima ya bikra yake, kitendo cha kupotea kilifanya alihisi kuchanganyikiwa! Ajali aliyopata ilitokea kabla ya kujiunga na chuo kikuu, iliharibu kumbukumbu kichwani mwake ingawa haikuharibu ubongo wake.

Anaruhusiwa kutoka hospitali akiwa hana kumbukumbu lakini baadaye akiwa nyumbani katikati ya usiku kumbukumbu zake zinarejea, anapiga kelele pale tukio la ajali lilipoanza kujirudia kichwani mwake kama sinema! Wazazi wake wanafika chumbani kwake na kumfika anatoka jasho, wanafikia uamuzi wa kumpigia simu daktari wake, Othman ambaye anafika muda mfupi baadaye na kuwaeleza kuwa tayari kumbukumbu zimerejea!

Wote wanamshukuru daktari kwa kazi yake, hata Halima mwenyewe, anashindwa amlipe nini daktari na alipomwangalia usoni akagundua kuwa daktari huyo alikuwa na sura nzuri na ya kuvutia lakini akiwaza juu ya jambo hilo ghafla sura ya Gerald inaingia kichwani mwake, anaanza kulia.

Je, nini kitaendelea? Fuatilia…



Katika umri wa miaka ishirini na saba tu, tayari Dk. Othman alikuwa daktari bingwa wa Upasuaji kwa kitaalam watu wenye cheo kama chake waliitwa Surgeon, iliaminika alikuwa ndiye daktari bingwa wa upasuaji mdogo kuliko mwingine yeyote katika Afrika Mashariki. Kwa umbile alikuwa mrefu, mwenye kifua kipana na mwili uliojengeka vizuri sababu ya mazoezi. Uso wake ulikuwa wa duara, vishimo kwenye mashavu na mwanya mdomoni mwake, rangi ya ngozi ya mwili wake ilikuwa ni maji ya kunde.

Kifupi Dk. Othman alivutia na ukiongezea uzuri huu wa sura yake kwenye sifa alizokuwa nazo kielimu, hakika haikuwa rahisi kwa mwanamke kumkwepa kijana huyo, hata kama hakumpenda kimapenzi lakini lazima angesema alikuwa na sifa zote. Cha kushangaza Dk. Othman alikuwa miongoni mwa wanaume mabachela katika jiji la Dar es salaam, ni kweli wasichana wengi walimfuata na kujipitisha mbele yake lakini hakuwepo hata mmoja aliyeonekana kumvutia, rafiki zake walipompa ushauri juu ya kuoa jibu lake lilikuwa moja tu; Mke mzuri hutoka kwa Mungu mwenyewe.

Akiwa kwenye chumba alicholala Halima nyumbani kwa shangazi yake Mikocheni, aliendelea kumshangaa msichana akilia huku akiliita jina la Gerald, daktari hakumfahamu mwenye jina hilo alikuwa nani lakini alifahamu ni moja ya kumbukumbu za Halima zilizokuwa zimerejea, ilibidi wazazi pamoja na daktari mwenyewe waingilie kati kumtuliza Halima ili asiusumbue ubongo wake ambao ulikuwa bado haujapona vizuri.

“Gerald! Wee Gerald wangu wee, kwanini ulinifanya hivi? Nilikukosea nini mimi? Ajali hii niliyoipata ni kwa sababu yako, bila wewe kuniacha nisingekwenda Wizara ya Mambo ya nchi za nje ambako hatimaye niligongwa gari, sikukukosea kitu chochote Gerald, kwanini ulinitenda hivi?” Aliuliza Halima akibubujikwa na machozi, Dk. Othman alikuwa ameketi pembeni mwa kitanda na kumwekea Halima mkono wake wa kulia begani na kuendelea kumpapasa taratibu huku akimbembeleza.

“Usijali, usijali Halima, kwani kuna nini wazazi? Nini kilitokea kati ya Halima na huyo Gerald?”

“Ni habari ndefu, sijui kama tunaweza kukueleza sasa hivi!”

“Sio vibaya nikifahamu, kwa sababu ya Halima najisikia sehemu ya familia yenu, tangu nianze kazi ya kutibu wagonjwa nafikiri huyu ni mgonjwa pekee ambaye amepona kwa miujiza ya Mungu!”

“Mama Halima msimulie daktari!”

Bila kuficha kitu mama yake Halima aliweka kila kitu wazi juu ya uhusiano wa Halima na Gerald na namna ulivyomwathiri mtoto wao baada ya kijana huyo kupotea moja kwa moja nchini Marekani, wakati akisimulia, Halima alizidi kulia na Dk. Othman aliendelea kumbembeleza bila kuchoka, mwisho mama alipomaliza daktari alimgeukia Halima na kuanza kumpa maneno ya kumtia moyo.

“Unahitaji kusahau yote yaliyopita Halima, dunia ndivyo ilivyo, wakati mwingine watu huwa tunaumizwa na watu tuliowapenda lakini inabidi tuukubali ukweli, usiruhusu kabisa Gerald akachukua furaha yako wakati labda huko aliko tayari ana mtu mwingine! Siku tukipata nafasi nitakusimulia ni kwanini mpaka leo hii mimi sijaoa, yaliyonipata ni makubwa lakini naendelea na maisha yangu kama kawaida, Mungu atakufariji, inabidi ukipona urudi shule kuendelea na masomo, nafahamu Mungu atakupa mtu mwingine!”

“Sitaki mtu tofauti na Gerald!”

“Sawa, lakini…!”

“Lakini nini daktari?”

“Unahitaji kuyaacha mambo yachukue mkondo wake, huwezi kulazimisha kitu kitokee kama Mungu hakukipanga Halima! Unamwamini Mungu?”

“Sana!”

“Basi tulia, mwache Mungu afanye kazi yake, naelewa ni kiasi gani unampenda Gerald lakini huna jinsi!”

“Ahsante daktari, nitajitahidi ingawa itakuwa ni kazi ngumu kumsahau Gerald!”

Kumbukumbu za Halima zilisharejea kabisa, kwa mtu yeyote ambaye hakuwahi kumwona akiwa na hali aliyokuwa nayo kabla ya siku hiyo, hakika asingeweza kukubali kuwa msichana huyo alipatwa na ajali mbaya iliyosababisha kumbukumbu zake zote kupotea, ambacho kingemtambulisha kuwa alipata ajali ni majeraha ambayo bado yalikuwa hayajapona vizuri mwilini mwake lakini upande wa kumbukumbu na ufahamu asingeweza kuelewa jambo lolote.

Ilikuwa ni furaha kubwa mno katika familia ya mzee Mohamed, hakuna aliyepata usingizi mpaka asubuhi, walikuwa wakiongea mambo mengi kuhusu maisha na matatizo waliyopitia katika kumuuguza mtoto wao, Dk. Othman pia hakuondoka mpaka saa moja na dakika kumi alipoaga na kusindikizwa na Halima mpaka kwenye gari akapanda, kuwasha na kuondoka akimwacha Halima amesimama sehemu hiyo hiyo akimwangalia.

Siku mbili baadaye tafrija kubwa ya kumshukuru Mungu ilifanyika nyumbani kwa shangazi yake, Dk. Othman na wauguzi wote walioshiriki katika kumtibu Halima pia walikuwepo, watu wakala, kunywa na kusaza! Muda wote wa tafrija hiyo Dk. Othman alikaa na Halima, wazazi na watu waliokuwepo walianza kuhisi kitu, jambo lilikuwa limetokea katika akili za vijana hao wawili, mzee Mohamed wala hakuchukizwa na hali hiyo, alielewa ni kiasi gani binti yake alihitaji mtu wa kumfariji ili aweze kumsahau mwanaume aliyemvuruga akili na baadaye kumtoroka, isitoshe Dk. Othman alionekana kuwa mtu mzuri, tena Mwislam kama alivyokuwa Halima, zaidi ya hapo ndiye aliyeokoa maisha yake! Hivyo lolote ambalo lingetokea kati yao familia ingeliona kama baraka.

Tafrija ilianza saa mbili za usiku na kumalizika saa sita na nusu, ndipo Dk. Othman akaaga na kama ilvyotokea siku ya kwanza alisindikizwa tena na Halima hadi kwenye gari lake ambako waliendelea kuongea kwa karibu nusu saa nzima wakiwa mbalimbali bila kusogeleana wala kugusana! Kabla ya kuondoka Dk. Othman alimsisitizia sana Halima juu ya kumsahau Gerald na kurejea chuo Kikuu haraka iwezekanavyo kuendelea na masomo kwa sababu tayari akili yake ilikuwa katika hali ya kawaida.

“Yes, he is a good man, gentleman and handsome on top of that, he saved my life, I would be dead without him, I don’t know what is going to happen though I can feel something developing within my heart. I cant allow this to happen, Gerald will come back one day, he will, I know he will one day because he always said he loved me!” (Ndio, ni mtu mzuri, muungwana na mzuri, zaidi ya hayo ameokoa maisha yangu, pengine ningekuwa marehemu bila yeye, sijui kitakachotokea ingawa nahisi kitu fulani kinaendelea kukua moyoni mwangu, siwezi kuruhusu jambo hili litokee, Gerald atarudi siku moja, atarudi, najua atarudi kwa sababu mara zote alisema ananipenda!) Halima aliongea maneno hayo peke yake akishuhudia gari la Dk. Othman likipotelea gizani.

Kila kitu kilikuwa kikitokea ghafla mno maishani mwake, alikuwa na siku mbili tu tangu arejewe na fahamu zake na kuelezwa juu ya ajali mbaya iliyompata lakini mambo yalikuwa yakienda haraka kuliko alivyotegemea na hakutaka kufanya kitu kwa sababu tu alikuwa ameumizwa na Gerald, alihitaji muda kutulia, kujipanga upya kabla hajafikiria kuwa na uhusiano mwingine kimapenzi, moyo wake bado ulimpenda sana Gerald na aliamini lazima angerudi siku moja.

“Halima!” Mama yake ndiye alimshtua.

“Bee mama!”

“Mbona umesimama gizani peke yako?”

“Ninapunga upepo na ninataka kwenda kupumzika sasa!” Hakutaka kuyaeleza mawazo yaliyokuwa kichwani mwake.

“Mlikuwa mnaongea nini na Dk. Othman?”

“Alikuwa ananishauri juu ya kurudi shule!”

“Umeamua nini?”

“Nitarudi mama, elimu ni kitu cha muhimu sana kwangu! Ingawa moyo wangu bado una maumivu nitajitahidi kumsahau Gerald, Dk. Othman ameahidi kuwa karibu na mimi ili niweze kupona moyo wangu na kumsahau kabisa mtu aliyeniumiza”

“Anamaanisha uhusiano kimapenzi?”

“Hapana, hajagusia kabisa jambo hilo, hata mimi mwenyewe sifikirii, utakuwa ni urafiki wa kawaida tu nitakapokuwa shuleni!”

“Amekueleza pia mambo aliyosema atakuambia siku moja?”

“Ndio!”

“Ni nini?”

“Aliwahi kuwa na mchumba, Mtanzania ambaye walikuwa wakisoma naye nchini Uingereza, siku ya harusi msichana huyo alimkataa Dk. Othman mbele ya Mwanasheria wakati wakifunga ndoa na kuondoka na mwanaume mwingine wa Kinigeria, aliumia sana na tangu siku hiyo anasema aliwachukia wanawake kuliko kitu kingine chochote, hajamwona mwanamke wa kumpenda wala kumwamini tena maishani ndio maana hajaoa!”

“Aisee! Alipatwa na tatizo kubwa sana?”

“Sana! Lakini anasema hivi sasa amekwishasahau ingawa ilikuwa ni kazi ngumu, amesema kwa uzoefu aliona atanisaidia pia mimi kusahau!”

“Itakuwa vizuri..nenda basi ukapumzike mwanangu!”

“Sawa mama!”

Halima aliingia ndani akawaaga wageni wote walioalikwa, shangazi pamoja na baba yake akaondoka kwenda chumbani kulala, kupata usingizi haikuwa rahisi kama alivyotegemea, taswira mbili ziliendelea kumsumbua kichwani mwake; ya Gerald na Dk. Othman, kwa jinsi mambo yalivyokuwa yakienda alielewa safari ya Dk. Othman iliishia wapi, alichokuwa akifanya ni kucheza mchezo wa kuonyesha kama hataki wakati ukweli wa mambo ni kuwa tayari alishampenda Halima, dalili zote zilionekana machoni, wakati huo huo bado Halima alikuwa na mapenzi mazito kwa Gerald, ndani ya moyo wake aliamini kuna tatizo lililomkuta na siku moja angerejea na kumtafuta, hivyo kujiingiza katika mikono ya Dk. Othman ingeuweka uhusiano wake katika wakati mgumu kama angerejea.

Saa tisa na nusu usiku ndipo alipata usingizi na kuzinduka saa tatu asubuhi, mama yake alipofika kumjulia hali, hakutaka tena kuendelea kulala, alichofanya ni kunyanyuka kitandani, kupiga mswaki kisha kuoga. Kifupi alisharejea katika hali yake ya kawaida kabisa, wala hakusikia maumivu mahali popote mwilini mwake, saa nne kamili baada ya kifungua kinywa alianza kuongea na baba yake na kumwambia juu ya nia yake ya kurudi Chuoni, akamwomba aende kufuatilia ili kama ingewezekana siku iliyofuata aripoti Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuendelea na masomo yake ingawa wenzake wangekuwa wamekwishafika mbele sana kimasomo.

“Nitafanya hivyo leo!” baba yake alisema.

Halima alitaka kwenda Chuoni kuhakikisha kama kweli Gerald alikuwa hajajiunga na chuo, hakutaka kumruhusu Dk. Othman azidi kuingia moyoni mwake mpaka pale atakapokuwa na uhakika kuwa kweli Gerald asingerejea tena.



Aliyeokoa maisha yake ni daktari kijana aitwaye Othman, huyu ni bingwa wa upasuaji, ndiye aliyemfanyia Halima operesheni ya ubongo na kuondoa bonge la damu lililoganda. Baada ya kupona Halima anashindwa kuelewa ampe nini Daktari huyo mwenye sura ya kuvutia kama shukrani yake kwa wema aliomtendea.



Kama ilivyo kwa Halima aliyeumizwa na Gerald, Dk. Othman pia amewahi kuumizwa na mchumba wake nchini Uingereza ambaye alimkataa siku ya ndoa na kuondoka na mwanaume mwingine. Historia za watu hawa ni za kufanana na zinaonekana kuwaunganisha, kitu cha ajabu kinaanza kutokea kati yao, Halima anaanza kumwangalia Dk. Othman kwa jicho tofauti, anahisi kumpenda lakini anapomkumbuka Gerald anashindwa kuzikubali hisia hizo, bado anaamini ndani ya moyo kuwa ipo siku Gerald atarejea na kuendelea na mpango wao wa ndoa.



Kwa ushauri wa Dk. Othman, Halima amekubali kurejea Chuo Kikuu kuendelea na masomo, daktari huyo akiwa ameahidi kumsahaulisha Halima juu ya mtu aliyemuumiza ingawa hakutaja uhusiano wa kimapenzi kati yao.

Je, nini kitaendelea? Penzi litazaliwa kati yao? Gerald yuko wapi? Atarejea? Endelea…



Ni Dk. Othman aliyekuja nyumbani kwa shangazi yake Halima huko Mikocheni na gari lake aina ya LandCruiser VX kumchukua pamoja na mizigo yake kwenda Mabibo kwenye mabweni ya wanafunzi wa Chuo Kikuu baada ya taratibu zote kuwa zimekamilika, si baba, mama wala shangazi aliyekuwa na wasiwasi na Dk. Othman, kifupi wote walishamkubali kabla yeye mwenyewe hajatamka lolote juu ya binti yao, hawakuwa na kipingamizi tena kama ilivyokuwa kwa Gerald.



Alikuwa amechelewa sana lakini Chuo kilikubali kumpokea kama tu angejitahidi kusoma mpaka awapate wenzake na kuwa tayari kwa mitihani iliyokuwa ikija miezi mitatu mbele yake! Uongozi wa Chuo ulilazimika kukubali baada ya kuyaona matokeo ya Halima na walipoiangalia sababu ya yeye kushindwa kujiunga na Chuo.



“Unahitaji kusoma kwa nguvu sana!”

“Nitajitahidi Othman, nakuahidi ili mradi tu umeahidi kunisahaulisha Gerald, bila hivyo shule nisingekwenda! Nakupenda Othman” Hivyo ndivyo alivyomwita, tayari alishamzoea hata neno daktari hakulitamka tena.

Dk. Othman alitabasamu vishimo vikaonekana kwenye mashavu yake, uzuri wa sura yake ndio ukaongezeka maradufu, mwisho akamalizia kwa kusema neno “Nakupenda pia Halima”

“Ahsante!”

“Nitakufanya mwanamke mwenye furaha kuliko mwanamke mwingine yeyote duniani!”

“Mimi pia nitakusahaulisha kabisa mwanamke aliyekuumiza moyo Othman, alifanya ktiendo cha kikatili, hakutakiwa kukufanyia hivyo!”

“Ahsante!”

Waliongea hayo wakiwa wamesimama nje ya mabweni ya Mabibo, yaliyojengwa na Shirika la Hifadhi ya Taifa la NSSF, kulikuwa na idadi kubwa sana ya wanafunzi wakipita maeneo hayo na kuwaangalia, walionekana kumfahamu Othman lakini si Halima, baadhi yao walimwamkia, walikuwa ni wagonjwa aliowahi kuwatibu.

“Wewe ni maarufu sana Othman?”

“Sio sana, ukisema mimi maarufu Rais wa nchi utamwitaje? Hao ni wagonjwa tu ambao nimewahi kuwasaidia”

Dk. Othman alimsaidia Halima kubeba mizigo yake na kupandisha ghorofa ya pili ya bweni A chumba namba 28, hicho ndicho chumba alichotakiwa kuishi akiwa Chuo Kikuu, msichana mmoja aliwapokea.

“Huyu anaitwa Grace, ndiye nitakuwa naishi naye katika chumba, Grace huyu ni rafiki yangu anaitwa Othman!”

“Namfahamu!”

“Mh!” Halima aliguna.

“Tuliwahi kukutana eeh?”

“Ndio hospitali ya Muhimbili, ulimfanyia mama yangu operesheni ya utumbo uliojisokota!”

“Ahaa! Wagonjwa ni wengi inakuwa vigumu kuwakumbuka wote!”

“Nimekuambia wewe ni maarufu ukakataa!” Halima alisema.

“Watu wachache sana wananifahamu, Grace akiwa mmoja wao, haitoshi kuniita maarufu!”

“Halima umesema ni rafiki au mchumba wako?”

“Ni rafiki tu!” Alijibu Halima kichwani mwake akiwa na moja kichwani.

“Kuna ubaya akiwa mchumba wangu?” Dk. Othman aliuliza.

“Hakuna ubaya wowote, mnapendeza kuwa mtu na mke wake!”

Ingawa ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Dk.Othman kukutana na Grace, kwa Halima haikuwa mara ya kwanza kwani jana yake alipokwenda Chuoni kufuatilia bweni alikutana naye, waliongea mengi sana, Grace alionekana ni mcheshi na mchangamfu ndio maana maongezi yao yaliendelea kwa muda mrefu.



Saa moja na nusu usiku ndio Dk. Othman aliaga na Halima kumsindikiza hadi kwenye gari ambako walikumbatiana na kuagana kwa upendo kama mtu na rafiki yake, Othman akaondoka zake na kumwacha Halima amesimama sehemu ile ile akizisoma taa nyekundu za LandCruiser, alishindwa kuelewa ni kwanini mambo ndani ya moyo wake yalikuwa yakienda kasi kiasi hicho. Alihisi kuzidi kumpenda Dk. Othman, ingawa hakupenda kabisa hali hiyo iendelee na alijaribu kwa nguvu zake zote kuzuia, bado kadri saa zilivyozidi kupita ndivyo Othman alivyozama moyoni mwake kiasi cha kutomfikiria kabisa Gerald kila alipokuwa naye, mawazo juu ya Gerald yalirejea tu Dk. Othman alipoondoka, gari lilipopotelea gizani alitembea taratibu hadi chumbani kwake.



“Haiwezekani Halima!” Grace aliongea.

“Haiwezekani nini shosti?”

“Mh! Mwanaume mzuri kiasi hicho awe rafiki yako tu! Impossible, yaani mwanaume ukimwangalia tu unasikia damu inakwenda mbio! Sema ukweli shosti, kijana anaishambulia Baghdad, au?”

“Hakyanani tena, ni rafiki yangu tu!”

“Kwanini?”

“Amenisaidia sana, bila yeye ningekufa, ndiye aliyenifanyia operesheni niliyokusimulia jana, ni daktari mzuri, tunavyokwenda naye inaonekana kuna kitu kitatokea lakini bado, hivi sasa kila mtu anamtegea mwenzake!”

“Wewe unampenda?”

“Nahisi kitu cha aina hiyo lakini kuna mtu mwingine nampenda pia!”

“Yuko wapi?”

“Italia!”

“Shoga asiyekuwepo machoni na moyoni hayupo, wewe chukua hicho kitu, ukicheza hapa chuoni hakuna mchezo watu watadaka halafu utaanza kulaumu, shauri yako!” Grace aliongea akitabasamu, hata yeye mwenyewe alionekana kufyekwa kimapenzi na Dk. Othman.



“Acha tuone kitakachotokea!”

Grace akawa ndio rafiki mkubwa wa Halima, darasani na nje ya darasa! Gerald hakuwepo chuo Kikuu, hata miezi sita baadaye walipofanya mitihani ya muhula wa kwanza na Halima kufaulu vizuri, Gerald alikuwa bado hajaripoti Chuo Kikuu na ukaribu kati ya Dk.Othman na Halima ulikuwa umeongezeka maradufu, kila mwisho wa wiki ilikuwa ni lazima watoke pamoja kwenda kula chakula cha usiku kwenye hoteli kama Sea Cliff, Alcove, Sheraton na kwingineko kwingi mwisho walimalizia kwenda disko kupumzisha akili zao, huko walicheza kila aina ya muziki ikiwa ni pamoja na bluzi wakiwa wamekumbatiana na Halima alimfanyia Dk. Othman kila aina ya mbwembwe na madoido ili angalau asisimke na kujikuta akimtamkia neno “ Nataka uwe mpenzi wangu” lakini haikuwa hivyo bado Dk.Othman aliendelea kumchukulia kama dada yake.

“Mpaka lini Othman?” Halima alimuuliza jumapili moja wakiwa nje ya ukumbi wa Billicanas saa tisa za usiku, haukuwa ukweli, karibu kila siku alimfikiria kijana huyo na alishindwa kuelewa kama siku moja angetokea ingekuwaje wakati tayari alishaanza kumruhusu Dk. Othman amwingie na wazazi wake walimkubali kwa kila kitu.

“Mpaka lini vipi sista?”

“Mimi tayari nimekwishamsahau Gerald!”

“Ahsante sana, hilo ndilo lilikuwa lengo langu, nafurahi!”

“Sasa kinafuata nini?”

“Mh! Uhusiano wetu lazima udumu!”

“Katika nyaja zipi?”

“Nakupenda Othman, unajua, kwanini unanitesa kiasi hiki?”

“Hata mimi pia!”

Ghafla bila kutegemea walijikuta wakisogeleana, wakakumbatiana, midomo yao ikasogeleana hatimaye kugusana, wa Dk. Othman ukaufunika wa Halima, kilichoendelea katikati ya midomo yao hakuna akijuae, ila waling’ang’aniana kwa karibu dakika tano, walipoachiana, Halima alikuwa akibubujikwa na machozi.

“Kwanini unalia?”

“Ni siku nyingi mno tangu nijisikie hivi, Gerald alinizoeza, baadaye akaniumiza na kunitoroka! Wewe pia utafanya hivyo Othman?”

“Haiwezekani, siwezi kufanya ukatili wa aina hiyo, naelewa inauma kiasi gani kwa sababu ilishanitokea, isitoshe nakupenda sana Halima, nataka kukuoa haraka iwezekanavyo! Sasa ni kwanini nikuumize?”

“Ahsante Othman, haya ndiyo maneno niliyokuwa nayasubiri kutoka kwako kwa muda mrefu!”

“Hutaniacha Halima?”

“Ndio!”

“Hata akitokea Gerald leo?”

Halima akakaa kimya, machozi yakazidi kumbubujika, picha ya Gerald ikamwingia kichwani mwake.

*****

Ghafla hali ilikuwa imebadilika kabisa, furaha yote ambayo Halima na Dk.Othman walikuwa nayo ndani ya ukumbi wa disko wa Billicanas ilikuwa imeyeyuka! Halima alikuwa akibubujikwa na machozi akiwa mikononi mwa Dk. Othman, swali aliloulizwa lilikuwa gumu kwake kulijibu. Siku zote fikra juu ya Gerald zilimuumiza mno, alimpenda sana kijana huyo na mpaka wakati huo alikuwa bado hajaamini kama kweli alikuwa amepotea moja kwa moja.



Sehemu fulani katika moyo wake ilimwambia iko siku Gerald angerejea na kumwomba msamaha kwa yote yaliyojitokeza, lakini tayari alishaanza kulewa kwa penzi la Dk. Othman aliyemrejeshea furaha iliyokuwa imepotea. Mawazo juu ya Gerald yalimiminika kichwani mwake mithili ya sinema, katika muda mfupi tu alijikuta amerejea mpaka shule ya Kimataifa ya Tanganyika walikosoma pamoja.



“Pole sana Halima, bila shaka nimekuumiza kwa swali langu, naelewa ni kiasi gani bado unampenda Gerald! Lakini ukweli ndio huo, alishakuacha, nina uhakika sasa hivi ana mwanamke mwingine kama hivyo ndivyo, kwanini uendelee kuumia wakati mimi nipo na ninakupenda?”

“Naelewa Othman, ni kweli unanipenda lakini inaniwia vigumu sana kumtoa Gerald kichwani mwangu, nitaendelea kujitahidi, nakuahidi wala usijisikie vibaya, nataka uelewe kuwa ninakupenda sana Othman!”

“Lakini swali langu ni kwamba, je akirudi Gerald leo bado utaendelea kuwa na mimi?”

“SITAKUACHA OTHMAN, NAKUPENDA NA NINAENDELEA KUKUPENDA KADRI SIKU ZINAVYOZIDI KWENDA, HATA HIVYO TULIPE PENZI LETU NAFASI YA KUKUA, TUCHUNGUZANE ILI KUEPUKA MAUMIVU YA NAMNA HII TENA SIKU ZA USONI!”

“Sina haraka sana Halima, mvumilivu hula mbivu!”

Baada ya maongezi hayo Dk. Othman aliiangalia saa yake, ilisomeka saa 10:00 ya usiku, mbele yao kulikuwa na masaa mawili tu kabla hakujapambazuka! Siku hiyo walikuwa wamechelewa sana kurudi nyumbani, bahati nzuri siku iliyofuata haikuwa ya kazi wala masomo, wangepata muda wa kulala muda mrefu zaidi. Dk. Othman alimshika Halima mkono na kumwongoza hadi kwenye gari, akamfungulia mlango akaingia na kuketi, ndipo akafunga na kuzunguka upande wa dereva ambako alifungua mlango, kuingia, kuwasha gari na kuondoka kwa kasi hadi nyumbani kwake Upanga.



Hivyo ndivyo ilivyotokea kila siku walipokwenda disko, Halima hakurudi chuoni bali alikwenda nyumbani kwa Dk. Othman kulala mpaka asubuhi ya siku iliyofuata, wakati mwingine alishinda hapo hadi jioni ndipo akarejea chuoni! Hawakuongea tena juu ya Gerald, wala hawakulala usingizi, jua lilichomoza wakiwa bado hawajafumba kope zao! Kilichotokea chumbani mwao walikijua wenyewe. Sababu ya uchovu hawakuweza kutoka kitandani mpaka saa nane na nusu mchana walipoamshwa na mfanyakazi wa ndani kwa ajili ya chakula.



“Sina apetaiti!” Halima alikaataa kunyanyuka.

“Jitahidi bwana!” Dk. Othman aliongea akimpigapiga mgongoni.

“Hapana niache nilale kidogo, wewe nenda tu kale!”

“Acha basi nikaoge kwanza!” Aliendelea Dk. Othman na baadaye kunyanyuka kitandani na kukimbia bafuni ambako alijimwagia maji mwili mzima kuondoa usingizi, akaoga vizuri, dakika kumi baadaye alirejea chumbani na kumgusa Halima kwa mikono yake ya baridi, akaruka na kuketi kitako kitandani.



“Bwanaaa! Uchokozi huo!”

“Nenda kaoge tukale!”

Halima hakukataa tena, akanyanyuka na kutembea hadi bafuni ambako alijimwagia maji kuondoa usingizi kisha kuoga na kurejea chumbani akavua nguo ya kulalia na kuvaa nguo nyingine safi kisha wote wawili wakaondoka taratibu wakiwa wameshikana mikono kwenda chumba cha chakula ambako meza ilikuwa tayari ikiwasubiri wao, Halima ndiye aliyepakua.



“Karibu!”

“Ahsante!”

Kifupi walikuwa ni kama mtu na mke wake tayari ingawa bado ilikuwa haijahalalishwa, walifurahi kuwa pamoja, ilipotokea hawajaonana wiki nzima kwao ilikuwa ni sawa na mwaka mzima! Maisha yao yalikuwa hivyo kila wiki labda pale Dk. Othman alipokuwa safarini au Halima kuwa amebanwa na mitihani. Ukaribu huu hatimaye ulifanya iwe inapita siku nzima bila Halima kumfikiria Gerald, jambo ambalo siku za nyuma lilikuwa haliwezekani kabisa, baadaye ikawa siku mbili, tatu hatimaye wiki bila wazo la Gerald kumwingia kichwani, lakini ilipotokea siku mawazo ya Gerald yameingia kila mtu chuoni aligundua Halima hakuwa sawa sawa.



Pamoja na kutokuwepo moyoni bado alipenda kufahamu nini kilimtokea Gerald huko alipokuwa, mara kadhaa alishajaribu kupiga simu Ubalozi wa Italia kuongea na Balozi Lutta, lakini alipojitambulisha tu kuwa yeye ni Halima, simu ilikatwa au aligombezwa na kuonywa asipige simu siku nyingine! Hii ilimkatisha tamaa lakini bado alitamani kumwona Gerald siku moja na alishindwa kuelewa ni kwanini wazazi wake hawakutaka awasiliane na mtoto wao.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Wakati wanasherehekea mwaka mmoja wa uhusiano wao, ndio Halima alikuwa akiingia mwaka wa pili, mwaka ambao yeye na Gerald walipanga kuoana! Aliamua kuongea na Dk. Othman juu ya jambo hilo na namna lilivyokuwa likimuumiza moyoni mwake, alitaka kumshirikisha katika kila jambo lililomsumbua.



“Unataka kuolewa?” Dk. Othman aliuliza.

“ Sio nataka, natamani na ndivyo tulipanga na Gerald!”

“Uko tayari nikuoe?”

“Kwanini isiwe hivyo? Nitafurahi mno, hapo ndio nitaamini kwamba kweli unanipenda Othman!”

“Lakini nakupenda Halima bila hata ya ndoa!”

“Naelewa lakini utanihakikishia zaidi nikivaa pete yako kidoleni!”

“Kweli?”

“Hakika!”

“Basi yamekwisha!”



Wiki moja tu baadaye, walikuwa ndani ya LandCruiser VX wakielekea wilaya ya Kondoa mkoani Singida, nyumbani kwao na Dk. Othman ambako shughuli moja tu ilikuwa inakwenda kufanyika; Halima kutambulishwa kwa wazazi na ndugu zake, Dk. Othman alikuwa ameamua kufanya kweli, siku zote alitaka kumfanya Halima ajisikie mwanamke mwenye furaha kuliko mwingine yeyote chini ya jua.



Kama walivyokuwa wamefikiria, hakuna mtu hata mmoja aliyempinga Halima, uzuri wake uliwatatanisha kuanzia Wazazi mpaka watoto, alikubalika isivyo kawaida! Suala moja tu likawa linaulizwa, ndoa lini? Na Dk. Othman aliwapa uhakika kwamba isingechukua muda mrefu kuanzia siku hiyo, Halima alifurahi mno, mpaka wanarejea Dar es Salaam mawazo ya Gerald hayakuwemo tena kichwani mwake, aliamini alishamsahau kabisa, akili yake yote ilikuwa imeishia kwa Dk.Othman.



Dar es Salaam maisha yaliendelea kama kawaida, Dk. Othman akiwa kazi kwake na Halima akiwa Chuoni akiendelea na masomo yake, Chuo kilikuwa hakijakamata kasi yake sawasawa, wanafunzi wa mwaka wa kwanza ndio wengi walikuwa wakiwasili kuanza chuo, hatimaye alikuwa ameingia mwaka wa pili tena akiwa amefaulu vizuri na zaidi ya yote ndoa na mwanaume aliyempenda ilikuwa kilometa chache tu kutoka alikokuwa amesimama.



Ajali aliyoipata akitokea Wizara ya Mambo ya Ndani ilikuwa imebadilika na kuwa Baraka badala ya mkosi, alimshukuru hata dereva aliyemgonga kwani bila yeye kufanya hivyo asingekutana na Dk. Othman na hivyo asingeolewa naye! Wiki moja baadaye asubuhi akijiandaa kwenda darasani kusoma na wenzake, simu yake ya mkononi ililia, akainyanyua na kuanza kusikiliza.

“Hallow!”

“Halima!” Ilikuwa ni sauti ya Dk. Othman.

“Ndio sweetie!”

“Sitaki kufanya kitu bila kukutaarifu!”

“Kuna nini tena? Unataka kuniacha?”

“Hapana! Jioni kutakuwa na sherehe ndogo kwenye hoteli ya Sea Cliff!”

“Ya nini?”

“Nataka nikuvalishe pete ili nikupunguzie msululu wa wanafunzi wanaokuandama hapo chuoni! Najua wapo, au?”

“Hao tena? Wacha, unanivisha pete leo?”

“Kabisa!”

“Saa ngapi?”

“Nitakuja kukuchukua saa kumi na mbili, unatoka darasani saa ngapi?”

“Kipindi changu cha mwisho kinakwisha saa kumi!”

“Basi nitakuja muda huo!”

“Nimwambie na Grace ajiandae?”

“Hakuna tatizo, hata wazazi ukiweza!”

“Ah! Wako Kilosa, sisi wenyewe tunatosha!”

Siku hiyo darasani vitu havikusomeka, kichwani mwake Halima kulijaa mawazo ya juu ya pete ambayo angevaa, bado alikuwa haamini, ilikuwa ni kama ndoto ya mchana! Hakika Dk. Othman alikuwa anakwenda kuthibitisha pendo lake, saa kumi kamili jioni alitoka kwenye kipindi, akamwita Grace pembeni na kumtaarifu juu ya shughuli iliyokuwepo mbele yao jioni ya siku hiyo.

“Mimi tena? Kwa minuso ndio mwenyewe, twende shosti nikusindikize ukang’arishe kidole! Lazima wapambe tuwepo!” Grace alisema baada ya kutaarifiwa.

Waliporejea mabwenini walikuwa na kazi ya kujiandaa kwa ajili ya sherehe, ilipogonga saa kumi na mbili kamili walikuwa tayari, Halima akachungulia nje kupitia dirishani na kumwona Dk. Othman ameegesha gari lake.

“Shosti twende, shemeji yako kaja!”

“Poa!”

Wakabeba mikoba na kuanza kukimbia wakishuka ngazi kwenda chini, mlangoni kabla hawajatoka, Halima alisikia sauti nyuma yake, haikuwa sauti ngeni sana, kumbukumbu zilimwonyesha alishaisikia kabla, ilikuwa sauti ya kiume.

“Halima!” Kijana huyo aliendelea kuita, ikabidi Halima ageuke.

“Haaaa! GERALD!” Akasema kwa mshangao, ghafla mwili wake ukalegea na kuporomoka chini kama mzigo, fahamu zilikuwa zimempotea.

******

“Geraaaaald?” Halima alipiga kelele, hakuwa tayari kuamini kilichokuwa kikionekana

“Halima?” ndilo neno pekee ambalo Gerald alisema akishusha mizigo yak echini.

“Yes baby, where have you been all these days?” (Ndio mpenzi, umekuwa wapi siku zote hizi?) Halima aliuliza swali macho yake yakilengwalengwa na machozi.

“It is a long story baby, I will tell you later once we have time!” (Ni habari ndefu mpenzi, nitakueleza mara tutakapokuwa na wakati!)



Halima alikuwa akibubujikwa na machozi, kilichokuwa kikitokea mbele yake haikuwa rahisi kuamini ni halisi, zaidi sana kilionekana kuwa ni ndoto. Hakutaka kabisa kukubali kuwa mtu aliyekuwa mbele yake ni Gerald, mvulana aliyempenda kwa moyo wake wote halafu akapotea na kumuumiza moyo wake, mvulana aliyemtafuta kwa nguvu na gharama zote bila mafanikio, mvulana aliyesababisha akapata ajali ambayo ilikuwa kidogo tu ichukue maisha yake au kumfanya awe mlemavu siku zote za maisha kama Dk. Othman asingejitahidi kuokoa maisha yake, wakasogeleana na kukumbatiana huku wote wawili wakilia, bila kuelewa ni kwa furaha au huzuni.

“ I love you Halima, I still want to marry you!” (Nakupenda Halima bado nataka kukuoa!)

“Me?” (Mimi?) Halima aliuliza kwa mshangao, akili yake ikampeleka haraka sana nje ya jengo ambako Dk.Othman alikuwa akimsubiri kwa ajili ya kwenda ukumbini kumvisha pete ya uchumba.

“Yeah! You, have you forgotten the promise?” (Ndio! Wewe, umesahau ahadi tuliyoweka?) Gerald aliongea na baadaye kuuliza swali.



Halima akazidi kububujikwa na machozi, jambo lililokuwa likimtokea ilikuwa ni sawa kabisa na mkuki moyoni hasa alipomfikiria Dk. Othman nje ya jengo alikuwa akimsubiri waende kwenye tafrija ya kuvishana pete ya uchumba, mtu ambaye baada ya Gerald kupotea tayari alishamwingia moyoni na pia kuteka akili yake, Halima aligundua ni mtihani mzito Kiasi gani alikuwa akikabiliana nao.



“Oh My God, please make this be a dream! “(Oh Mungu wangu tafadhali ifanye hii kuwa ndoto) Halima aliongea kwa sauti.

“Why are you saying those words Halima? You don’t love me any more?” (Kwanini Halima? Hunipendi tena?) Gerald aliuliza huku akizidi kububujikwa na machozi.



Uzuri wa Gerald ulikuwa bado uko palepale ingawa kulikuwa na mabadiliko makubwa mwilini mwake, kwanza alikuwa amepoteza uzito mkubwa mwilini mwake na rangi ya ngozi yake ilikuwa imebadilika na kuwa kahawia huku miguu yake ikionekana kuvimba, hivyo ndivyo ilivyokuwa pia kwa mashavu yake. Alikuwa na kila dalili ya ugonjwa uliomsumbua mwilini! Halima alitamani kuuliza lakini alishindwa, macho yake kila mara yalikuwa kwenye saa akiangalia muda na kumfikiria Dk. Othman aliyekuwa nje akimsubiri kwa hamu.



Siku hiyo kwa Dk. Othman ilikuwa muhimu kuliko nyingine zote ambazo aliwahi kuishi duniani, kwa sababu ndio siku ambayo angepata uhakika kwamba hatimaye angemuoa Halima baada ya kuumizwa na msichana mwingine miaka michache kabla na kuapa kutopenda tena maishani mwake. Alipolifikiria hilo, Halima aliukosa uwezekano wa yeye kuwa na Gerald tena.



“It is too late!” (Umechelewa!)

“Too late for what? I love you Halima and you Know this! Something bad happened to me, that’s why I disappeared” (Nimechelewa? Nakupenda Halima na unajua hilo! Kitu kibaya kilitokea ndio maana nikapotea)

“You kept so quite Gerald, for so long baby what do you expect? Yes, I love you too Gerald, you know this, you are the only man I gave my virginity to, just because I knew you were gonna my husband!” (Ulinyamaza kwa muda mrefu mno Gerald, ndio, nakupenda na unalijua hilo, wewe ndiye mwanaume pekee niliyekupa heshima ya bikira yangu nikijua ungekuwa mume wangu!)

“Then? I am still going to be your husband” (Kwa hiyo! Bado nitakuwa mume wako!)

“No! It cant happen, let me go someone is waiting for me outside this building!” (Hapana! Haiwezi kutokea tena, acha niende kuna mtu ananisubiri nje ya jengo hili!) Halima aliongea akijifuta machozi, bado alitaka yaliyokuwa yakitokea yabadilike kuwa ndoto, moyoni mwake alihisi penzi zito kwa Gerald lilikuwemo ingawa Dk. Othman tayari alishazamisha mizizi kwenye akili yake. Hakutaka kabisa kufikiria suala la kumwambia Dk. Othman kuwa asingeolewa tena kwa sababu Gerald alikuwa amerejea, alipolikumbuka swali ambalo Dk. Othman alilomuuliza siku nyingi kabla kama angeendelea kuwa naye hata kama Gerald angerejea na kumhakikishia asingemwacha, Halima alielewa wazi uwezekano wa kuwa pamoja na Gerald ilikuwa simulizi.

“Who is this someone?” (Mtu gani huyo?)

“I will introduce him to you one day!” (Nitakutambulisha siku moja!)

“So it is him, right?” (Kwa hiyo ni mwanaume, sawa?)

“Yeah, my fie…!” (Ndio mchu…) aliongea Halima lakini akashindwa kuimalizia sentensi yake, kwikwi ya kulia ikamkaba.

“No! No! No! Halima, you are my baby no matter what happened in between, I love you, I can’t let you get married to someone else! Cant let you go” (Hapana!Hapana! Hapana Halima, wewe ni mpenzi wangu hata kama kilitokea nini katikati , nakupenda, siwezi kukuacha uolewe na mtu mwingine, siwezi kukuacha uende!)

“It is too late, please understand Gerald, you have to face the truth! My fiancée is waiting for me outside!” (Umechelewa, tafadhali elewa Gerald, lazima ukubaliane na ukweli! Mchumba wangu ananisubiri nje!)

Mwili wa Gerald ulianza kutetemeka na kubadilika rangi, uso wake ukapauka na ghafla akaanguka chini miguuni mwa Halima! Alipoinama kumwangalia, hakuwa na fahamu tena. Jasho jingi lilikuwa likimtoka mwilini mwake, bila kujali alianza kumfanyia kile ambacho wazungu hukiita ‘Kiss of life” ili kuokoa maisha yake, midomo yake laini ikafunika midomo ya Gerald na kuanza kumpulizia pumzi kifuani kupitia mdomoni huku akiwa ameziba pua yake kwa mkono wa kushoto, alipomaliza kufanya hivyo aliupigapiga moyo ili kuushtua, alijilaumu kwa kumpatia Gerald habari hizo katika mtindo ambao haukufaa.

“Nilipaswa kusubiri!” Aliwaza.



Tayari Wanachuo walishafika eneo hilo kwa lengo la kutoa msaada, wakamshika Halima na kumnyanyua juu ili wapate nafasi ya kumbeba Gerald kwenda nje kwenye hewa ambako wangetafuta usafiri wampeleke hospitali. Kwa yaliyojitokeza, kichwani mwake Halima hakuwa tena na kumbukumbu juu ya Dk. Othman, lakini walipofika nje na kumlaza Gerald kwenye nyasi ili apunge upepo, aliliona gari la Dk. Othman na kukimbia hadi mahali hapo.

“Vipi mbona umechelewa?’

“Tafadhali njoo, njoo Othman utusaidie, kuna tatizo, mwanafunzi mwenzetu ameanguka kwenye ngazi na kupoteza fahamu!” alisema akiwa amejikausha ipasavyo ili Othman asigundue kama mtu aliyepata matatizo alikuwa na uhusiano naye.

“Nani tena? Halima kumbuka kuna watu wanatusubiri ukumbini na wameshapiga simu hapa mara nyingi tafadhali twende zetu, waambie wenzako wampeleke hospitali sisi twende ukumbini!”

“Hapana! Hapana Othman, hatuwezi kufanya hivyo huo ni ukatili na kinyume cha taaluma yako!”

“Ok twende basi haraka!” Dk Othman hakuwa na ubishi mbele ya Halima, alimpenda mno Kiasi cha kuwa tayari kufanya lolote Wakati wowote, mara moja akashuka garini na kuongozana na Halima hadi mahali alipolazwa Gerald.

“Mh!” Aliguna baada ya kumwona Gerald, kwa mwanga kidogo uliokuwepo aliweza kuona vitu visivyo vya kawaida mwilini mwake.

“Vipi?” Halima alidadisi.

“Huyu ni mgonjwa wa muda mrefu?” Badala ya kujibu Dk. Othman akauliza.

“Sijui, ndio kwanza ameingia chuoni leo hii na ni mwaka wa kwanza!” Halima alijibu,

“Ni nduguyo?” Dk. Othman akazidi kuuliza.

“Hapana, nimekutana nae kwenye ngazi wakati nikija chini!”

“Mbona unalia sasa? Yaani ni kama ndugu yako vile?”

“Namwonea huruma tu!” Halima alizidi kuficha.

“Jamani, huyu mwenzenu ni mgonjwa tafadhali tusaidiane kumbeba ili tumkimbize hospitali haraka!” Alisema Dk. Othman akiinama na kuanza kumnyanyua Gerald akisaidiwa na wanafunzi wengine, wakampeleka mpaka kwenye gari.



Aliendesha gari kwa kasi kuelekea hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kichwani mwake akiwafikiria watu waliokuwa ukumbini, pete ya uchumba iliyokuwa ndani ya koti lake! Hakuelewa kabisa kilichoendelea kichwani mwa Halima, wakiwa maeneo ya Magomeni aliwapigia simu rafiki zake waliokuwa ukumbini na kuwaeleza wazi juu ya kilichotokea, hivyo angechelewa wote wakakubali kumsubiri.

Eneo la fire alikata kona kuingia barabara ya Umoja wa Mataifa hadi hospitali ya Muhimbili ambako walimshusha Gerald akiwa bado hana fahamu na kumkimbiza hadi wodi ya wagonjwa mahututi (ICU) ambako kwa agizo la Dk. Othman ambaye wafanyakazi wa wodi hiyo walimfahamu, mashine ya oxygen iliwekwa puani kwake bila kupoteza Wakati.

“Jina lake?” Dk. Othman aliuliza akiandika kwenye cheti!

“Anaitwa Gerald!” Halima aliitikia.

Dk. Othman akasita kidogo kuandika jina hilo kwenye cheti, badala yake akanyanyua uso kumwangalia Halima usoni huku macho yake yakionyesha aina fulani ya wasiwasi. Badala ya kugonganisha macho Halima aliinamisha uso wake chini akijutia kosa alilokuwa amelifanya, hata hivyo sekunde chache baadaye Dk. Othman aliendelea kuandika kwenye cheti.

“Jina lake baba yake?”

“Hilo silifahamu labda mpaka yeye mwenyewe angekuwa na fahamu zake!”

“Umemfahamu kwa muda gani?”

“Leo tu! Tena kwenye ngazi”

“Mh! Ukamfahamu hapo hapo kuwa anaitwa Gerald?’

Halima hakuwa na jibu, Dk. Othman akatabasamu, jambo hilo lililozidishia Halima wasiwasi zaidi moyoni mwake.

“Kwa ninavyomwangalia huyu mgonjwa anaonekana kuwa na tatizo katika figo, wapigieni watu wa maabara haraka ili waje wachukue vipimo vyake, pia wasilianeni na Dk. Ngofilo ili amchunguze vizuri zaidi, yeye ni mtaalam wa magonjwa ya figo. Ahsanteni sana!” Alimaliza Dk. Othman na kuwakabidhi wauguzi cheti alichoandika maelezo ya mgonjwa na kuwasisitizia kuendelea kumpima mapigo ya moyo, kumwekea dripu na pia dawa za kutia moyo nguvu baada ya hayo alimgeukia Halima.

“Twende darling!”

“Tumwache mgonjwa?” Halima akauliza kwa mshangao.

“Hakuna wasawasi yupo katika mikono sahihi hata tukikaa hapa sisi haisaidii chochote, nimekwishamwanzishia dawa nzuti tu wala usiwe na shaka mpenzi!” Dk. Othman aliongea akimpigapiga Halima mgongoni.

Alichokifanya Halima ni kutingisha kichwa chake na kukubali kwa shingo upande huku akibubujikwa na machozi, jambo lililozidi kumtia Dk. Othman wasiwasi zaidi.

“Kwani vipi, Halima mbona umebadilika ghafla kiasi hiki?” Hatimaye aliamua kumuuliza.

“Hapana! Namwonea tu huruma huyu mgonjwa!”

“Wewe huwaonea wagonjwa wote huruma kiasi hiki au huyu tu?’

“ Yeyote!”

“Basi ulitakiwa kuwa daktari si mwanasheria, bwana twende kumbuka kuna watu wanatusubiri ukumbini!”

Wakaanza kutembea kuelekea nje ya wodi lakini kabla hawajatoka Halima akageuka nyuma kumwangalia mgonjwa kitandani machozi yakazidi kumtoka! Hali hii ilizidi kumtia Dk. Othman wasiwasi, hasa kila alipokumbuka jina la Gerald lililotoka mdomoni mwa Halima.

“Hivi hii engagement party itafanyika kweli?” Dk. Othman aliuliza walipoingia kwenye gari.

“Kwanini unauliza swali hilo Othman!”

“Umebadilika ghafla mno, ndani ya saa nzima nimemwona Halima tofauti na yule niliyekuwa nikimfahamu siku zote!”

“Usijali!”

“Au lile jina Gerald lina uhusiano na Gerald uliyewahi kunieleza habari zake?”

Halima hakuwa na jibu, akachukua kitambaa chake na kuanza kujifuta usoni, hapakuwa na maneno ya kumwambia DK. Othman, asingeweza kumkana au kudai hampendi Gerald tena Wakati ndani ya moyo wake alikuwa na mapenzi mazito kwake.



Hakujua ni kitu gani kingetokea siku hiyo ukumbini kwani kuna sehemu fulani moyoni mwake ilimwambia asikubali kuvaa pete ya Dk. Othman Wakati Gerald alishapatikana, lakini hakuwa na Gerald huko wodini angenusurika kifo kwa ugonjwa uliomwangusha! Dakika ishirini baadaye walishafika hoteli ya Holiday Inn ambako tafrija ya kuvishana pete ilikuwa ikifanyika wakaegesha gari lao na kuingia ukumbini, watu wote wakanyanyuka vitini na kushangilia kwa furaha lakini Halima hakuwa yule ambaye siku zote walimfahamu. Alikuwa ni kama mtu aliyepigwa na baridi.

“Halima kwanini unaonyesha tabia mbaya leo? Tena mbele ya rafiki zangu?” Dk.Othman alimuuliza Halima akimnong’oneza taratibu.

“Nashindwa Othman, siwezi kuigiza, nimechanganyikiwa vibaya mno akilini mwangu!”

“Kwanini?”

“Yule ndiye Gerald!”

******

Ilikuwa heka heka chumbani, madaktari wote wakihangaika kufanya kila kilichowezekana kuokoa maisha ya Gerald aliyekuwa akitupa kichwa chake huku na kule kama mtu anakata roho huku mapovu yakimtoka mdomoni na mwili wake ukibadilika rangi kuwa wa bluu. Madaktari wawili walikuwa wakimwekea mashine ya oksijeni puani huku mwingine akimpigapiga kifuani kuushtua moyo wake ulioonekana wazi kutaka kusimama, hawakuelewa ni kitu gani hasa kilitokea baada ya wao kuondoka chumbani hapo kufuata mashine ya kusafishia figo ambayo mpaka wakati huo walikuwa hawajaitumia baada ya kukuta hali ya mgonjwa imebadilika ghafla.



“Nesi!” Daktari mmoja aliita.

“Bee!”

“Nini kimetokea baada ya sisi kuondoka?”

“Labda tumuulize Dk.Othman ndiye alikuwepo hapa ndani, alikuja ofisini kwetu kuchukua dawa ya PPF pamoja na bomba la sindano kwa kweli sisi hatufahamu ni kitu gani kimetokea!”

Dk. Othman alisimama pembeni ya kitanda akitetemeka mwili mzima, bomba la sindano lilikuwa mfukoni mwake, aliomba dua asiwepo mtu wa kumtilia mashaka na kuamua kumpekua. Halima hakuwepo tena chumbani wakati huo alishatolewa nje ambako aliendelea kulia kwa uchungu, sauti yake ilifika mpaka ndani, madai yake kwamba Dk. Othman alikuwa amemuua Gerald yalifikika masikioni mwa madaktari, wote wakageuka kumwangalia lakini hakuna aliyemuuliza chochote, alikuwa daktari mwenzao aliyekula kiapo cha kuokoa maisha ya wagonjwa na si kuwaua, wote walimchukulia Halima kama mtu aliyechanganyikiwa.



“Dk unazisikia lawama hizo?” Mmoja wa madaktari waliokuwepo chumbani aliyejulikana kwa jina la Dk. Mashauri alimuuliza Othman.

“Nazisikia!”

“Huyo si ndiye mchumba wako?”

“Ndio!”

“Sasa inakuwaje tena anaibuka na tuhuma nzito zenye uwezo wa kukupeleka jela? Kwani huyu mgonjwa ni nani yake?” Dk. Mashauri alizidi kudadisi huku shughuli za kuokoa maisha ya Gerald zikiendelea.

“Kwa kweli sijui!” Othman hakuwa na jibu, mambo yote yaliyokuwa yakitokea mbele yake siku hiyo yalimwogopesha, kwa mara ya kwanza katika maisha yake alianza kuiona milango ya jela ikifunguliwa ili aingie! Akaumia na kujikuta akijilaumu kwa kitendo alichokifanya, machozi yakaanza kumtoka.

Hakuweza tena kukaa chumbani, akatoka hadi nje ambako Halima alikuwa akigalagala chini na kulia kwa uchungu huku akimtupia Othman lawama zote kama ingetokea Gerald akafa. Tayari watu walishaanza kumzunguka wakitaka kufahamu kitu gani kilikuwa kimetokea.



“Sista, tafadhali naomba umwingize huyu mtu ndani, mwondoe mahali hapa, anapigia wagonjwa wengine kelele!” Dk. Othman alimwambia muuguzi aliyekuwa nje na Halima.

“SITAKI! NASEMA SITAKI, ACHANA NA MIMI MUUAJI MKUBWA WEE!” Halima alifoka.

“Halima!” Dk. Othman alimwita akijaribu kumshika mkono, Halima akaukwepesha mkono wake kisha kusimama wima na kuanza kutembea kuelekea ndani.

Kila kitu kilishabadilika kabisa, hawakuwa tena mtu na mchumba wake, wala hawakuwakumbuka watu waliowaacha ukumbini wakiwasubiri ili wavishane pete! Hiyo tayari ilikuwa ni historia, hapakuwa na dalili tena kwamba watu hao wangekuwa pamoja maishani mwao, Dk. Othman alikuwa akibubujikwa na machozi kama mtoto mdogo. Kwa haraka alitembea hadi ofisini kwa wauguzi ambako alimkuta Halima na kupiga magoti mbele yake akimwomba msamaha.

“Unaniomba msamaha?”

“Ndio!”

“Kwa hiyo unakubali kwamba umemuua?”

Dk. Othman hakuweza kujibu swali, aliendelea tu kububujikwa na machozi yaliyolowanisha mashavu na koti alilovaa, Halima wala hakumwonea huruma, mapenzi yake yalisharejea kwa Gerald, mbele ya muuguzi aliyemheshimu Dk. Othman alimsukuma na kumwangusha sakafuni akanyanyuka tena na kuanza kukimbia kwenda kwenye chumba alicholazwa Gerald, akasukuma mlango na kuingia ndani bila kubisha hodi. Macho yake yakaenda moja kwa moja hadi kitandani ambako alimshuhudia Gerald akiwa ametulia kabisa huku shuka jeupe likiwa juu ya mwili wake.

“Dada samahani, naomba kwanza usubiri nje, tupe nafasi ya kufanya kazi tutakueleza kila kitu kilichotokea baadaye!”

“Niambieni tu kama amekufa!”

“Subiri kwanza nje, tafadhali tunaomba!” Dk. Mashauri aliongea akiwa amefungua mlango na Halima akatembea taratibu hadi nje na kurejea tena ofisini ambako alifika na kumvamia Dk. Othman kisha kuanza kumshambulia kwa ngumi na mateke.

“Umemuua Gerald wangu!”

“Nisamehe!”

“Lazima nikushtaki, huu ndio mwisho wa taaluma yako ya udaktari, nafikiri hujui baba yake Gerald ni nani katika nchi hii hakika unakwenda kufia jela, hakyanan… nakuambia Othman, kama ulizoea kuua watu wengine kwa mtindo huu, basi hapa umekwama! Yaani umemuua Gerald kweliiiiiii?” Halima aliongea kwa uchungu akiwa ameshika mikono yake yote miwili kichwani.

“Nisamehe, nihurumie Halima naomba tafadhali usinipeleke jela kwani adhabu ya kukupoteza wewe tu inanitosha kabisa!”

Halima hakujibu kitu, akaketi kwenye kiti pembeni na kuanza kuwaza, picha ya siku waliyokutana na Gerald kwa mara ya kwanza aliikumbuka, namna walivyopendana, namna walivyoishi na mara ya mwisho walipoagana wakiwa wameahidiana ndoa wakiwa Chuo Kikuu! Kila kitu kilimiminika kichwani mwake kama sinema, roho ikamuuma sana.

Chuki ya ajabu iliingia moyoni mwake, hakuwahi hata mara moja kufikiri angekuja kumchukia Dk. Othman kiasi hicho, ndiye mtu aliyeokoa maisha yake kutoka katika kifo alipogongwa na gari na kuumia ubongo wake. Ni kweli bila yeye asingekuwa hai, lakini hiyo ilikuwa haitoshi kabisa kumruhusu amuue Gerald halafu aendelee kuishi huru, Halima aliapa kuhakikisha maisha ya Dk. Othman yanaishia jela.

“Halima, naomba ukumbuke tulikotoka, hebu pata hata dakika moja ya kufikiria mambo niliyoyafanya maishani mwako ingawa ulikuwa wajibu wangu, sistahili kwenda kufia jela, Watanzania bado wanahitaji msaada wangu, huyu ni shetani tu ameniingia tena kwa sababu yako, nakupenda mno Halima, sikuwa tayari kukupoteza lakini hivi sasa niko tayari kukuacha uende zako na mtu mwingine!”

“Niende na nani wakati tayari umekwishamuua Gerald? Usiniudhi, tena nyamaza kabisa!”

Mlango ukafunguliwa, muuguzi akaingia akikimbia na kwenda moja kwa moja kwenye kabati iliyokuwa juu ukutani, ambalo juu yake liliandikwa “Anti-coagulant” na kuifungua, akachukua kichupa kidogo na kutoka tena akikimbia.

“Vipi?”Muuguzi aliyekuwa ofisini alimuuliza mwenzake.

“Dk. Mashauri kanituma Dicumarol” Alijibu muuguzi huyo na kutoa mbio, kichwani mwa Halima alielewa dawa hiyo ilikuwa ni ya kutunzia maiti.





Dk. Othman akiwa hataki kumpoteza Halima, ameamua kumuua Gerald kwa kumchoma sindano ya dawa iitwayo PPF kwenye mshipa, jambo ambalo ni kinyume kabisa na linapofanyika mgonjwa hupoteza maisha! Hivi sasa Gerald anahangaika kitandani, madaktari wanafanya kila kinachowezekana kuokoa maisha yake ingawa kuna dalili zote kuwa kijana huyo atakufa, tayari Halima anaamini Gerald amekwishakufa na anazidi kumtuhumu Othman kwa kifo hicho.

Je, nini kinaendelea? Fuatilia…



Halima aliendelea kulia baada ya muuguzi kuondoka mbio na dawa ya Dicumarol, kichwani mwake alifahamu jambo moja tu; Gerald alikuwa ameaga dunia si kwa ugonjwa wa figo tena bali Dk. Othman alikuwa amemuua kwa makusudi kuzuia kuungana kwao tena, roho ilimuuma mno, akamsogelea Dk. Othman machozi yakizidi kumbubujika.

“Toka! Toka nje muuaji wewe, sikujua una roho mbaya kiasi hiki, si ni bora hata mimi ungeniua kuliko kuniacha hai halafu ukaja kumuua mtu nimpendaye!” Alifoka Halima akimpiga Dk. Othman wala hakujali mahali alipokuwa ni wapi ni wodini, tayari muuguzi alishafika kuwatenganisha.

“Una uhakika gani kwamba amemuua?” Muuguzi aliuliza.

“Naelewa, najua ninachokisema!”

“Unaongea maneno ya hatari sana dada, unaweza kumtia Daktari wetu matatani, kama ni kifo mgonjwa wako atakuwa amekufa sababu ya matatizo yake ya figo!”

“Sio kweli!”

“Unakataa kwanini?”

“Muulize mwenyewe daktari wenu, kwanini alinitoroka ukumbini na kuja hapa kisha hali ya mgonjwa kuwa mbaya?”

“Dk.Othman naomba ukae nje kidogo, anapokuona hapa hasira zinampanda, tafadhali naomba tu unisikilize, najua umechanganyikiwa kiasi kikubwa lakini jitahidi!”

Kwa unyonge Dk. Othman alinyanyuka kutoka kwenye kiti alichokuwa amekaa na kuanza kutembea kwenda nje ya wodi ambako aliketi juu ya jiwe na kuanza kulia, moyoni mwake alijilaumu mno kwa kitendo alichokifanya! Hakika alikuwa amekwenda kinyume na taaluma yake na kusababisha kifo cha mgonjwa, yeye mwenyewe ndani ya nafsi yake alishindwa kabisa kujipa msamaha ingawa maisha ya jela au hukumu ya kunyongwa ilimtisha kupita kiasi. Ghafla alijikuta akiwafikiria wazazi wake masikini waliomsomesha kwa kila kitu walichopata wakiwa wafanyakazi wa serikali, baba Mwalimu na mama Muuguzi mpaka wakajikuta katika ufukara sababu yake.

“Sasa nakwenda jela bila kuwasaidia wazazi wangu kitu chochote, mama yangu ataumia sana! Lakini kwanini sikuacha tu kuchukua uamuzi wa kumuua Gerald? Kuna wanawake wangapi duniani ambao wangependa kuolewa na mimi?” Dk. Othman akajuta moyoni mwake, huku mashavu yake yakizidi kulowa kwa machozi, alitamani kila kilichotokea kibadilike na kuwa ndoto, aamke na kujikuta amelala ndani ya nyumba yake kwenye kitanda chake alichokipenda cha sita kwa sita na Halima akiwa pembeni amemkumbatia lakini ukweli uliendelea kuwa ukweli.

Alishindwa kabisa kufahamu wazazi wake wangezichukuliaje habari hizo, rafiki zake aliosoma nao Chuo Kikuu cha Muhimbili na hata Uingereza wangesema nini baada ya kusikia aliamua kuua mgonjwa wake kwa sababu ya mapenzi! Fikra zake zikamfanya pia amfikirie baba wa Gerald ambaye Halima alikwishamweleza habari zake kwamba alikuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, kwa wadhifa wake lazima angependa kuona haki inatendeka, hiyo ingemaanisha yeye kunyongwa! Alipofikia hapo alilia zaidi na kuona ndoto zake zilikuwa zimefikia mwisho, asingeweza tena kuwa Daktari bingwa wa upasuaji nchini Tanzania, ndoto yake ya kuingia katika Siasa na baadaye kuwa Waziri wa Afya isingetimia tena, kamba shingoni ingekomesha uhai wake.

“Ni Halima peke yake anaweza kunisadia katika suala hili, nitambembeleza mpaka akubali kunifichia siri, kwa wengine wote hakuna hata mtu mmoja mwenye uhakika kuwa nimemchoma Gerald sindano ya PPF kwenye mshipa!” Aliwaza Dk. Othman na kunyanyuka kwenye jiwe tayari kwa kuingia ndani kwenda kumbembeleza Halima ili ayanusuru maisha yake. Akitembea kwa unyonge, ghafla alishtukia akiitwa kwa nyuma, aliitambua sauti ilikuwa ni ya Dk. Ringo, baada ya kuwa wamesubiri ukumbini kwa muda mrefu na kupiga simu zao wote wawili bila kupokelewa hatimaye waliamua kufuatilia nyumbani na baadaye hospitali.

“Vipi?” Ringo aliuliza alipomfikia Othman.

“Matatizo!”

“Matatizo gani tena?”

“Yule mgonjwa niliyemleta hospitali kabla sijaja ukumbini amefariki!”

“Aisee, pole!” Dk. Ringo aliongea, kabla Dk. Othman hajajibu chochote, Halima alichomoka kutoka ofisini baada ya kuwaona Ringo na wenzake.

“Mwambieni awaeleze vizuri, muuaji mkubwa huyu, yeye ndiye amemuua mchumba wangu wa zamani!” Aliongea Halima huku akilia, alishasahau kila kitu kilichotokea kati yake na Dk. Othman, alichofikia wakati huo hakikuwa kingine ila mwanaume huyo kufikishwa mbele ya sheria bila hata kukumbuka kuwa ni yeye ndiye aliokoa maisha yake.

“Nisamehe, nisamehe Halima!”

“Umeua kweli?” Dk. Ringo alimuuliza Dk. Othman.

****

“This Cynosis is a sign that, there is impairment in the oxygen supply to the tissue!” (Hii hali ya bluu inayojitokeza kwenye ngozi yake ni dalili kabisa kwamba kuna matatizo katika usambazaji wa hewa safi ya oksijeni kwenda kwenye mwili!)

“Sure! Can this be related to the kidney failure?” (Hakika! Hii inaweza kuwa na uhusiano na figo kushindwa kufanya kazi?)

“I don’t think so!” (Sidhani!)

“So what can we do?” (Sasa tufanye nini?)

“As we continue doing dialysis we should also do an urgent cardiography, for the sign I see are significant to an obrustruction somewhere in the heart!” (Wakati tunaendelea kusafisha figo zake, tupige picha moyo wake,kwa sababu dalili ninazoziona hapa zinaashiria kuna sehemu Fulani ndani ya moyo wake imeziba!) Aliongea Profesa Kayuga, bingwa wa magonjwa na upasuaji wa moyo katika hospitali ya Muhimbili, alikuwa mwalimu wa Dk. Othman akisoma Chuo Kikuu cha Muhimbili miaka mingi kabla, aliaminiwa na kila mtu lilipokuja suala la matatizo ya moyo.

Wakati simu ikipigwa ili watu wa idara ya X-ray wafike haraka katika chumba cha wagonjwa mahututi, Gerald alizidi kuhangaika kitandani akitupa shingo yake huku na kule, ngozi ya mwili wake ikiendelea kubadilika na kuwa bluu! Hali yake ilitisha, hata Madaktari walionekana wazi wakikuna vichwa, walishakutana na wagonjwa wengi wenye matatizo ya figo lakini hata siku moja hawakuwahi kukutana na mgonjwa wa aina hiyo.

“Tena nimemsikia yule dada pale nje anasema huyu kijana ni mtoto wa Balozi Lutta!”

“Lutta ambaye yuko Italia?” Profesa Kayuga aliuliza.

“Ndio!”

“Nilisoma naye Tabora Boys yule, tulikuwa pamoja na akina Mungai, Kapuya, Makweta na ni rafiki yangu wa siku nyingi, inabidi tufanye kila kinachowezekana kuokoa maisha ya huyu mtoto!” Profesa Kayuga aliongea akiusikiliza moyo wa Gerald kwa kutumia kipimo kiitwacho Stethoscope, macho yake yalionyesha kushtuka.

“Vipi daktari?”

“Mapigo yake yanabadilika, tena yanaanza kushuka na kuna pigo jingine la ziada, si la kawaida, hawa watu wa X-ray wako wapi?” Aliuliza lakini kabla hajajibiwa chochote mlango ukafunguliwa, ya kwanza kuingia ilikuwa ni mashine kubwa ya X-ray ikisukumwa kisha wakifuatia vijana wawili.

“Fanyeni haraka!” Profesa Kayuga aliongea, Gerald akabebwa juu juu kwa ushirikiano wa watu wote waliokuwemo ndani na kulazwa juu ya mashine hiyo, picha ikapigwa na majibu yake kutoka saa hiyo hiyo na kukabidhiwa kwa Profesa Kayuga ambaye wala hakutaka kuyaangalia akamkabidhi daktari mwingine aliyekuwa pembeni yake.

“Dk. Lema hebu tueleze kuna nini kwenye moyo wa huyu kijana?” Alimuuliza wakati anamkabidhi, daktari huyo ndiye alikuwa bingwa wa mambo ya X-ray wa hospitali ya Muhimbili, akaipokea X-ray hiyo na kuiweka nyuma ya taa iliyokuwa kwenye mashine hiyo.

“Uko sahihi!”

“Kwanini?”

“Kuna kitu kimeganda kwenye mshipa wake wa Pulmonary hivyo damu inashindwa kwenda kwenye mapafu kuchukua hewa safi ya oksijeni!”

“Kwa hiyo tunahitaji dawa ya kusambaza hicho kitu kilichoganda?”

“Kabisa tena haraka!”

“Sista hebu tuletee Dicumarol haraka iwezekanavyo!”Profesa Kayuga aliongea akiandika kwenye faili la Gerald na muuguzi akaondoka mbio kuelekea ofisini, dakika mbili tu baadaye alisharejea, dawa hiyo ikachomwa kwenye mshipa wa Gerald, haukupita muda mrefu rangi ya ngozi yake ikaanza kurejea katika hali ya kawaida na hata kuhema kwake kukabadilika, Gerald akawa hatupi tena shingo, akatulia kabisa kitandani, dakika kumi baadaye profesa Kayuga alipompima aligundua mapigo yake yalikuwa yamekaa sawa!

“Siamini!” Profesa alisema.

“Kwanini?”

“Nilishakata tamaa kabisa!”

“Hata mimi!”

“Kwa hiyo atapona daktari?” Muuguzi akauliza.

“Tatizo tumekwishaliondoa, kilichobaki hivi sasa ni figo tu, inavyoonekana figo zake zote hazifanyi kazi, anahitaji figo haraka iwezekanavyo na kama kweli ni mtoto wa Balozi Lutta wacha mimi nimpigie simu sasa hivi!” Profesa Kayuga aliongea na kuanza kutembea kwenda ofisini kwake, alipoufungua tu mlango alishuhudia kundi kubwa la watu, Dk. Ringo akiwa mmoja wao.

“Shikamoo profesa!”

“Marahaba hamjambo?”

“Hatuwezi kuwa hatujambo, tunataka kufahamu hali ya mgonjwa kwanza!”

“Afadhali kidogo! Kulikuwa na kitu kimeziba kwenye moyo wake, hatujaelewa ni kitu gani mpaka sasa hivi, ila kuna wasiwasi kidogo”

Dk. Othman aliruka juu na kushangilia kwa sauti kubwa, hakutegemea kama Gerald angepona, hofu ya kwenda jela ikaanza kupotea. Uso wa Halima pia ulionekana ukikunjuka, Ringo akawavuta wote wawili kuwapeleka pembeni ili waongelee jambo lililojitokeza, Halima akaanza kusimulia kila kitu na ni kwanini alihisi Othman ndiye angekuwa amemuua Gerald kama angekufa, kabla Dk.Othman hajaanza kuongea chochote, maaskari wenye bunduki wakafika eneo hilo.

“Nani ni Othman kati yenu?”

“Yule pale!” Mmoja kati ya watu walioongozana na Ringo kutoka ukumbini alisema, maaskari wakanyoosha mpaka sehemu waliyokaa Halima, Othman na Ringo na kuuliza swali hilo hilo.

“Ni mimi!” Othman akaitikia.

“Uko chini ya ulinzi!”

*****

Mwili wa Dk.Othman ulikuwa ukitingishika kwa hofu, furaha yote aliyoipata baada ya kuelezwa kuwa Gerald alikuwa akiendelea vizuri iliyeyuka baada ya kuwaona maaskari wamesimama mbele yake tena wakiwa na pingu mikononi. Dk. Othman alihisi mkojo ukimpenya, ghafla ndoto zake zote za kuwa daktari bingwa zaidi ya alivyokuwa zikaonekana kuanza kufifia, alijiona mpumbavu na mjinga asiyestahili kuhuurumiwa. Alishindwa kuelewa ni shetani gani alikuwa amemwingia mpaka kujikuta akitenda dhambi kubwa kiasi hicho na kusahau kabisa taaluma yake, kwa muda mrefu alikuwa amefanya kazi kwa uaminifu na kuaminiwa na kila mtu ingawa alikuwa kijana mdogo lakini sasa ghafla tu heshima yote aliyokuwa nayo ilikuwa inapotea.

“Simama juu!” Askari mmoja aliamuru, Dk. Othman akasimama akiwaangalia rafiki zake waliokuwepo kwa macho ya huzuni, aibu na huruma, hata siku moja katika maisha yake hakuwahi kuwaza angejikuta katika hali hiyo.

“Afande kafanya nini huyu ndugu yetu?” Dk. Ringo aliuliza akimgusa askari begani. Alichokipata badala ya jibu ni kibao kilichosababisha matone kadhaa ya mate yaruke kutoka mdomoni mwake.

“Haaa!” Wenzake wakaguna.

“Unaingilia kazi ya Polisi?”

“Naingiliaje kazi ya polisi kwa kuuliza ina maana sina haki ya kufahamu?”

Kabla hajajibiwa chochote tayari Dk. Othman alikuwa akisukumwa kwenda mbele, huku machozi yakimbubujika na kulowanisha mashavu yake. Alilia kama mtoto mdogo, moyoni mwake alijaa majuto yasiyo na kipimo, alishindwa kabisa kuelewa ni shetani wa aina gani alikuwa amemwingia moyoni mwake na kujikuta akitenda dhambi kubwa kiasi hicho.

Dk. Ringo na wenzake walimwacha Halima ameketi nje ya wodi akilia na kuanza kumfuatilia Othman aliyekuwa akisukumwa kwa nguvu na maaskari kupelekwa nje ya hospitali, kila mmoja wao alikuwa na maswali yasiyo na majibu kichwani mwake. Walishindwa kabisa kuelewa ni jambo gani baya ambalo Othman alikuwa ametenda mpaka kufikia hatua ya kupigwa pingu tena siku ya tafrija ya kumchumbia Halima siku chache kabla hajafunga ndoa. Kifupi kila kitu kilikuwa kimebadilika, hakuna mtu hata mmoja kati yao aliyekuwa na furaha, wote walikuwa na hamu ya kufahamu ni jambo gani limefanyika.

Kwenye kituo cha polisi kilichokuwepo mita mia tano nje ya hospitali ya Muhimbili Dk. Othman alifunguliwa pingu zake mikononi, akaamriwa kufungua mkanda na kuvua viatu kisha kupelekwa kwenye chumba maalum kuanza kutoa maelezo.



Muda mfupi baadaye aliwasili Profesa Kayuga akiongozana na wauguzi kadhaa pamoja na Halima ambaye bado alikuwa akiendelea kulia, nje ya kituo waliwakuta Dk. Ringo na wenzake wakiwa wamejawa na huzuni, usoni kwa Profesa Kayuga alionyesha hasira kali, tabia ambayo mara nyingi hakuionyesha, pamoja na hali hiyo bado Dk. Ringo aliweza kumsogelea na kumsimamisha.

“Profesa!”

“Naam”

“Napenda kufahamu nini kimetokea hasa!”

“Rafiki yako mtu mbaya sana, ni mimi ndiye nimewapigia simu polisi baada ya kugundua alichokifanya kwa mgonjwa!”

“Amefanya nini?”

“Amemchoma mgonjwa PPF kwenye mshipa, kwa lengo la kumuua? Hii haikubaliki ni kinyume cha taaluma yetu, kwa kweli lazima suala hili nilisimamie ipasavyo, kazi ya daktari si kuua ni kuponya!”

“Umejuaje profesa?”

“Acha kuniuliza maswali mengi, ruhusu sheria ichukue mkondo wake, baada ya upelelezi polisi watakuambia kila kitu kilichotokea ila ni ukweli kwamba rafiki yako alimchoma mgonjwa PPF kwenye mshipa ikaenda kukwama kwenye moyo, imebidi tumchome sindano ya kuyeyusha bonge lililokuwa kwenye mshipa vinginevyo angekufa, kibaya zaidi huyu mtoto wa rafiki yangu, Balozi Lutta, yuko Italia nimeongea naye kwa simu na atawasili hapa kesho, kifupi huyu rafiki yako mwisho wa taaluma yake umefika!” Alimaliza Profesa Kayuga na kuanza kutembea kuingia kituoni.

Akiwa hayaamini masikio na macho yake kwa jinsi alivyomfahamu Dk.Othman, Ringo alimkimbilia Halima na kumgusa begani, akitaka kufahamu kama habari zilizotolewa ni kweli, huku akibubujikwa na machozi msichana huyo alitingisha kichwa kukubaliana na kitu kilichosemwa.

“Mungu wangu! Why?” Aliuliza Ringo.

“Ndiye mchumba wangu wa zamani, aliyepotea, nimemwona leo wakati tukijiandaa kuja kwenye sherehe ya kuvishana pete, aliponiona tu alianguka chini na kupoteza fahamu hasa baada ya kumwambia nilikuwa nakwenda kuvalishwa pete ya uchumba, mimi na Othman tukambeba kumleta hospitali na kumwacha ndipo tukaja ukumbini kumbe mwenzangu akanitoroka kuja wodini kumchoma sindano ya kumuua, nimeumia sana shemeji, kumbe Othman anaweza hata kuniua mimi!” Alimaliza Halima na kuanza kuingia ndani ya kituo.

Ringo alihisi kuchanganyikiwa, alishindwa kuelewa ni nini hasa kilikuwa kimempata Othman, rafiki yake wa siku nyingi tangu wakisoma pamoja nchini Uingereza. Alichofahamu kuhusu rafiki yake ni kwamba alikuwa mpole, mvumilivu, asiyetaka kuonyesha hisia zake, hakupenda ugomvi siku zote alikuwa msuluhishi. Alishindwa kuyakubali maneno aliyoyasikia akahisi kulikuwa na njama za kumkomoa.

“Jamani, ni habari ya kusikitisha, Othman kamchoma mgonjwa sindano ya sumu!”

“Saa ngapi wakati tulikuwa naye ukumbini?”

“Kwa maelezo ya Halima, kumbe alipoondoka alikuwa anakuja wodini kumuua mvulana mmoja mwanafunzi wa chuo kikuu ambaye aliwahi kuwa mpenzi wa Halima enzi zile wakisoma sekondari lakini akapotea ghafla, wameonana leo muda mfupi kabla hawajaja ukumbini, ndio maana walipokuwa nasi hawakuwa na furaha hata kidogo kumbe kulikuwa na jambo, hivyo Othman alirejea wodini kumchoma sindano ya sumu huyo kijana!”

“Umesema walikutana muda mfupi kabla ya kuja ukumbini?”

“Ndio!”

“Sasa imekuwaje tena yupo wodini?”

“Alipoteza fahamu baada ya kuambiwa na Halima ukweli kuwa anakwenda kuvishwa pete ya uchumba!”

“Mungu wangu, sasa itakuwaje?”

“Nashindwa kuelewa! Profesa Kayuga kaniambia kitu kingine cha kusikitisha zaidi”

“Kipi?”

“Eti kijana mwenyewe ni mtoto wa Balozi Lutta!”

“Aliyekuwa Marekani sasa hivi yuko Italia?”

“Ndio!”

“Aisee hii ishu, lazima tujipange!”

Hawakuweza kuondoka, walibaki kituoni hapo mpaka saa tisa za usiku, Profesa Kayuga alipotoka kituoni akiongozana na wauguzi pamoja na Halima ambaye bado aliendelea kulia. Dk. Ringo alipotaka kumsimamisha Profesa Kayuga ili kumuuliza kilichoendelea ndani, hakuwa tayari kusimama, aliwaongoza watu wote aliokuwa nao hadi kwenye gari na kuondoka zake. Ringo na wenzake wakaingia ndani ya kituo, ambako walishuhudia Othman akiwa amevulishwa shati na kusukumwa akipitishwa nyuma ya kaunta, mlango wenye nondo nene ukafunguliwa akasukumwa tena kuingizwa ndani, kwa kufuli kubwa mlango ukafungwa.

“Habari yako Afande?” Dk. Ringo alimsalimia askari wa kike aliyekuwa mapokezi.

“Nzuri tu kaka habari yako!”

“Samahani naomba kuuliza!”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Uliza tu kaka yangu!”

“Nini kinaendelea kuhusu huyu bwana? Tunaweza kumdhamini?”

“Kaka inawezekanaje kumdhamini wakati mgonjwa hata hali yake bado haijatengamaa?Kesi hii haina dhamana, nende tu nyumbani mkapumzike kesho asubuhi mrudi mtaelezwa nini kinafuata! Nani yenu?”

“Mfanyakazi mwenzetu!”

“Poleni sana!”

Ilikuwa vigumu kukiacha kituo lakini hapakuwa na jinsi, watu wote waliokuwa wamealikwa kwenye tafrja ya Halima kuvishwa pete ya uchumba na Dk.Othman ambaye sasa alikuwa amegeuka muuaji waliingia katika magari na kuondoka kwa huzuni kubwa.



****





ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog