Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

ZEE LA NYWILA - 2

 






Simulizi : Zee La Nywila
Sehemu Ya Pili (2)




Baada ya kukabidhiwa chumba chake, alikaa kochini, kidogo akainuka, akapiga ukaguzi wa dakika chache chooni, akapita bafuni kisha akamalizia machinjioni, ni eneo analoliheshimu zaidi ya nyumba ya ibada, nazungumzia kitandani.

Nyuso yake ilionesha kuridhishwa na muonekano ndani humu. Huku akili yake ikianza kuichora ramani fupi ya namna afanye kazi ikamilike.

Alitoa koti lake la suti akatundika pembeni, akalegeza tai yake kidogo ili apate nafasi ya kufungua vishikizo viwili vya shati aliyokuwa amevaa. Akajitupa kitandani!



Zilikuwa ni dakika nane za hesabu Kali! Alizitathmini taarifa chache alizopewa, akavuta muonekano wa msichana kama alivyo katika picha zilizotumwa. Alijumlisha, aligawanya, alizidisha akawake mkato kidogo. Akarudisha kumbukumbu katika kurasa nyingi za vitabu vya saikolojia ya wanawake alivyosoma, vikamjia tena kichwani. Taratibu alizipekua, mambo yakaja. Tabasamu mahbibu likamtoka, kuashiria jibu limepatikana.



Haraka alifungua begi lake, akatoa kidadavuzi mpakato (laptop) chake, hakutaka kuona hata sekunde ikipotea; aliingia katika mtandao, akachapa ujumbe kwa Patrick..

"Boss, tayari nimefika,natarajia kazi hii kuimaliza leo leo usiku. Fanya juu chini, nipate ndege ya kesho asubuhi sana." Alimaliza na kuituma.



Mipangilio ya maangamizi ilianza rasmi.

Alitoa suruali nyeupe, yenye kitambaa kigumu ila chepesi. Juu atavaa nini? Aliandaa shati jepesi la bluu bahari, lisilo na mikono. Akatoa simu yake, Yeye mwenyewe anaiita simu ya kazi. Usijali, utafahamu kwanini ameibatiza hivyo.

Akaingia bafuni!.



Baada ya muda, tayari Abuu alishapendeza, alipendeza zaidi ya neno lenyewe pendeza. Suruali nyeupe iliyomkaa vyema, shati lisilo na mikono likimuonesha matuta komavu aliyonayo mwilini. Alijipulizia marashi na unyunyu,akavaa miwani onyeshi - yenye vioo vyeupe.

Utamjua? Nakuuliza, utamjua?

Aakh! Sitaki kuongezea na uzuri wake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Kwa mwendo wa madaha, wenye asili ya kiume, alishuka hadi chini ya hoteli ile, kulikowepo na mahali mahsusi, iliyotengwa kwa ajili ya watu kupata vyakula na vinywaji. Alikuwa na uhakika wa asilimia zote, kama si mia moja kuwa; Magreth, shabaha yake ya usiku wa leo lazima atakuja mahali hapa.



Hakuagiza chakula, hakuagiza kinywaji, alifungua simu yake ama simu ya kazi akaanza kuiperuzi huku macho yake yakiwa hayaachi kuangaza huku na kule, kumnasa swala wake amrushie mshale, haujalishi ni wa kisasa ama utakuwa wa kale, ilimradi chini akimdondosha akamle.



Shaabash! Mtoto akaingia bwana.

Mtoto ana umbo la kuvutia, sura ndiyo kidogo ya kuvumilia, ila huo urefu jamani ni wa kulilia, kigauni fulani hivi kifupi amevalia, huko nyuma sasa! Mamamamama! Usiombe ukamuangalia.



Abuu mate ya tamaa yalimkaba, kupita kooni hayapiti kurudi mdomoni haya'afiki. Alibaki kati, shimali hakaribii kuumeni hakulilii.



ALIONGOZA moja kwa moja, mpaka meza ya tatu nyuma, kutoka katika ile aliyokaa Abuu. Alikuwa hana habari na mtu, zaidi ya kushughulishwa na sikanu (smartphone) yake aliyokuwa nayo mfukoni.



Kimbembe kilikuwa kwa ZEE LA NYWILA, Zee la mipango, zee ambalo halitongozi likakataliwa. Alikuwa yuko katika tafakari za kuanza, huku moyo ukiahidi zawadi ya kumaliza. Akafanya maamuzi.

Alinyanyuka, akaweka shati lake sawa;

Mguu funika mguu funua, hadi katika meza aliyoketi Magreth.



"Hellow!" Abuu alianza na salamu, iliyosindikizwa na uzito wa tabasamu.



"Hellow!" Magreth naye alijibu, uso wake ukitoa taswira ya shaka kwa mbali.



"May I sit with you?,"

(Naweza kukaa Pamoja nawe?)

Abuu aliingizia ombi lake, alihitaji aianze kazi yake kwa wakati, akajivika ustaarabu wa hadhi ya dhahabu, kumbe mshenzi na msaliti wa adabu.



"Yeah! You can,"

(Ndiyo, unaweza)

Magreth alimkubalia, moyoni msitu mkubwa wa maswali ukianza kuota, ukishinikizwa na mvua kubwa ya ugeni wa sura iliyo mbeleni mwake.



Abuu alikaa, akashusha pumzi nyepesi nyepesi za taratibu, alihitaji atulize moyo wake pupa isimkumbe. Zikapita sekunde kadhaa, wote wakitazamana. Hii Abuu aliifanya kwa makusudi, kumfanya Magreth ajenge tafsiri ya Mwanzo kwa muonekano wake.



Na kweli, alimuweza vilivyo katika hilo.

Huyu ni nani? Kwanini kaja kukaa na Mimi? Ananijua? Lakini anavutia sana.

Vyote hivi vilikuwa katika tafakari za binti huyu wa Kinyarwanda, Magreth. Taratibu alianza kupendezwa na Abuu.

Laiti angefahamu Simba mmaliza kijiji ndiye aliye mwake machoni , hata kumuangalia asingetamani.



"Am Michael,"

(Mimi ni Michael).

Abuu alijitambulisha kwa jina la uongo.



"Magreth!", Msichana wa watu naye akatoa jinale, akihisi anayeongea naye hawafahamiani, kumbe anamjua kuanzia akilicho mpaka akitoacho, aamkapo mpaka alalapo, akizungumziacho hadi akinyamaziacho. Anamfahamu kila kitu.



" Ooh Magreth! Nice to meet you Magreth,"

(Oooh Magreth! Imekuwa vyema kukutana na wewe).

Abuu alizungumza kwa sauti ya utaratibu, akampa mkono wa furaha.

Magreth naye akatoa mkono wake, wakashikana.

Kwa mara ya kwanza, toka aifahamu sayari hii, Magreth hakuwahi kupata hisia kali kama Baada ya kushika mikono ya Abuu. Alijikuta anashindwa kumuachia, walizidi kuangaliana, macho ya Abuu kwa Magreth, ya Magreth kwa Abuu.



"What can we serve you?,"

(Tuwahudumie nini?).http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Walishtushwa na sauti ya mhudumu, ndipo wakaachiana, aibu ya kike ikamuingia Magreth, akashindwa kuzungumza na kutizama chini, ufundi alioutumia Abuu kuukamata mkono wake, ulimuacha katika dimbwi zito la huba, akiwa hawezi kuogelea, taratibu alianza kutamani mvulana huyu aliye mbele yake aingie waogelee wote.



Abuu alishaelewa hilo, alitabasamu kiume, ni tabasamu fulani gumu, huwa nalo wanaume Wachache mno, wengine huzaliwa nalo ingawa Abuu alijifunza.

Magreth akabahatika kuliona tabasamu hilo, moyo ukaanza kumlipuka, ni hali isiyo ya kawaida kabisa ilianza kumfika, Jeshi "mapenzi" la Abuu lilianza kumteka, tena kwa hiyari bila ya risasi wala mieleka.



"I just need water, You Magreth?"

(Ninahitaji maji tu, Wewe Magreth?)

Abuu aliagizia maji tu, ndivyo alivyofundishwa;

Akikutana na Msichana kwa mara ya kwanza, katika mazingira kama haya- ni kuagizia maji tu.

Unataka ufahamu kwanini?

Acha nikueleze kidogo,

Saikolojia ya wanawake inaonesha; miongoni mwa viumbe wanaofikiria jambo sana, hata liwe dogo namna gani, ni wanawake.



Laiti Abuu angeagiza soda, sijui chakula au juice. Kuna tafsiri fulani angeiweka Magreth kichwani kwake. Ila, kitendo cha kuagiza maji, kilimfanya Magreth azidi kutamani kumfahamu Abuu, Abuu alishajenga upekee moyoni mwake, ndani ya muda mchache tu.



"Juice! Mango juice!"

(Sharubati! Sharubati ya embe!)

Magreth akaagizia Sharubati (juice) ya embe, mhudumu akaondoka.



"You are a Rwandan, If am not mistaken?"

(Wewe ni Mnyarwanda, kama sijakosea?)

Abuu aliendeleza maongezi. Hakutaka kuruhusu kimya kichukue nafasi, alihitaji amzoee Magreth na Magreth amzoee yeye ndani ya muda mfupi. Na hivyo ndivyo itasaidia kazi yake kukamilika.



"Sure! How did you know?"

(Kweli, umejuaje?)

Magreth alikubali kwa mshangao, ikamhiyari aulize.



"It's known, Rwandans are the most beautiful girls in our continent"

(Inajulikana, Wanyarwanda ni wasichana wazuri kuliko katika bara letu).

Abuu alimpiga sifa, huku akujiua anampaka mafuta kwa mgongo wa chupa.



"Hahahah! You are so charming. Where are you from?"

(Hahahah! Wewe ni mchangamfu kweli. Unatokea wapi?)

Magreth akafurahi, alihisi kumfahamu Abuu ndani ya miaka, ingawa zilizowakutanisha ni dakika. Alimuuliza wapi anatokea.



"Am from Tanzania!"

(Mimi natokea Tanzania). Abuu alijibu, uso wake ukiwa bado katika muonekano wenye bashasha.



"Wooow! Are you from Tanzania?"

(Wooow! Unatokea Tanzania?). Magreth aliuliza kwa kustaajibika.



"Yes!"

(Ndiyo), Abuu alijibu.



Magreth aliwaka kwa mshtuko wenye furaha, aliona kabisa aliye mbele yake ni mtu wa karibu kwake.

Maongezi yaliendelea, yakawachukua wote wawili, yakawapeleka ulimwengu wa mbali. Ulimwengu usio na udhalili, isipokuwa upendo ulio jamili.



Wakaizungumzia Tanzania, ikafuata Mzizima, wakauchambua mji mzima, haikutosha! Wakaenda Rwanda, wakapeana story za huko, Wakaipitia Kigali kwa uchache Walifurahi kwa Pamoja, wakazoeana, tena si tu kuzoeana.

Wakatambuana kiundani; Magreth akasema hana mchumba, Abuu naye akaweka yake Kasumba...

"Hata Mimi sina mtu!"



Baada ya muda, huku maongezi yakiwa yanasonga, Abuu akaitoa ile simu yake.

Akaishika shika kwa dakika kadhaa, kisha akaiweka chini.

Kidogo! Akajifanya ameshikwa na haja, akaelekea msalani kujikidhi, simu ikiwa ameiacha palepale mezani.



Zikapita dakika mbili akarudi, alirudi kwa kasi kuonesha ana uharaka wa kitu fulani, alienda Mpaka pale alipokuwa amekaa na Magreth…



"Oh! Sorry Magreth! For the whole time, being here talking with you, I forgot that; I have some body's work that have to be accomplished. See you tomorrow Magreth! Am in room number 45, you're welcomed,"

(Oh! Samahani Magreth! Kwa muda wote, niliokuwepo hapa nazungumza nawe, Nimesahau kuwa; Nina kazi ya mtu inatakiwa ikamilishwe. Tutaonana kesho Magreth! Nipo chumba nambari 45, Unakaribishwa)

Abuu alimuaga, akamalizia utani wa kumkaribisha chumbani kwake, wote wakaangusha kicheko kwa Pamoja.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Mr. Password! Kama anavyopenda kujiita, akaenda zake- kashaweka kila kitu sawa, imebaki kazi tu hapo.



Unaikumbuka ile simu?

Enhee! Simu ya kazi ile. Abuu aliiacha palepale juu ya meza, kwa makusudi!.

Magreth akaiona, akawaza vipi atampelekea?. Alikosa jibu.

Aliamua kusubiri kwa dakika chache, muda ulizidi kusonga. Maneno yakamrejea kichwa ni..



"..Nina kazi ya mtu inatakiwa ikamilishwe. Tutaonana kesho Magreth! Nipo chumba nambari 45, Unakaribishwa!"



Chumba namba 45! Hapo alipigia mstari, taratibu aliinuka na kuamua kumpelekea.

Kama angepigia mstari huo maneno; "KUNA KAZI YA MTU INATAKIWA IKAMILISHWE".

Wallahi! Asingeelekea.



Aligonga mlango, Ukafunguliwa.

Abuu akatoka na kipensi, kifua wazi. Acha mtoto mwili umsisimke!

Kwa haya, akainama chini na kumpatia Abuu simu yake.

Abuu akaishika simu Pamoja na mkono wake , alimkamata kimahaba, mtoto akakamatika. Wakajikuta wote wanatazamana; Wakachekeana.

Magreth alishadata, Kwa Abuu amenata.

Waah! Kifuani mtoto akajivuta. Nini kingine?

Kitanda walikifuata.



VITA ya tatu ya dunia ilizuka ndani ya chumba namba 45, Vita isiyotoa sauti ya mishale wala mlio wa bunduki, zaidi ya manung'uniko na pumzi zenye umithili ya watokao nduki. Hii vita, haikuwa na majeruhi bali ilijaa mikiki.

Wote walikataa kuonekana kwenye penzi mamluki, Abuu alipeleka Magharabi na Mashariki, Magreth naye akahakikisha hakamatiki.



Vita ilidumu kwa takribani nusu saa, hatimaye wote wakapitiwa na usingizi.

……

Ni saa 2:15 asubuhi,

Ndani ya chumba namba 45, ambamo ndani yake usiku uliopita kulifanyiwa ubadhilifu wa kimapenzi.

Magreth alishtuka kutoka usingizini, akakaa kitako kwa sekunde kadhaa, kutafakari yaliyojiri jana yake, akasikitika, akamalizia na tabasamu la kujidharau.

Hapo hapo akamkumbuka Abuu, mwanaume aliyemteka moyo wake ndani ya masaa machache, hadi akamkabidhi undani wake. Kipindi hiko hakuwepo kitandani wala chumbani. Hakuingia shaka, akahisi huenda akawa yuko msalani.



Dakika zilizidi kuyoyoma, akaamua kumfuata huko huko chooni. Hakujiuliza Mara mbili! Kwanini sasa ajiulize? Wakati kama kufunuliana, vyote jana walioneshana.

Laa haula! Hakumkuta.



Mmnh! au itakuwa amekwenda kuchukua kifungua kinywa?

Magreth alijiuliza bila ya kupata ithbati. Akaketi chini kwa mara nyingine. Utanashati aliokuwa nao Abuu usiku uliopita, alitegemea atakuwa amekwenda kumletea chai chumbani kabisa.

Waapi! Alikuwa amejidanganya masikini msichana wa watu. Lisaa lilikatika, Hakutokea Abuu wala kivuli chake.



Hofu ikaanza kumtanda, akaamua kutoka chumbani, akaelekea mpaka mahali pa kufanya maagizo ya vyakula; Abuu hakuwepo.



Mbona nimeanza kuingiwa wasiwasi hivi? Hapana! Hapana! Shaka ondoka ndani yangu. Atakuwa ametoka nje kidogo. Labda kuna "surprise" anataka kunifanyia.

Magreth alijipiga moyo konde, akijiziua woga usimtande.



Aliamua kurejea tena chumbani, safari hii alirudi chumbani mwake, sio chumbani kwa Abuu, ama Michael kama amtambuavyo. Akajitupa kitandani, kwa uchovu mkubwa aliuopata kutoka na "kashikashi" ya Abuu - Akajikuta analala.



"Khee! Yawezekana akawa amerudi na asinione. Ukizingatia chumba changu hakijui"

Magreth alijisemea maneno haya, akikurupuka kutoka usingizini huku saa yake ya mkononi ikionesha tayari imeshatimu tano kasoro sita asubuhi.



Hata kuoga aliona atachelewa, alienda katika kioo, haraka haraka akaosha uso kwa sabuni, akabadilisha gauni alilovaa, "body-spray" iko wapi?; akajipulizia. Huyooo! Kiguu na sakafu kumuwahi Abuu.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Akafika mpaka nje ya chumba kile.

Kwa madaha, huku akiweka nguo zake sawa. Akitegemea mapokezi yenye umithili wa yale ya jana. Ila, hakuna aliyemfungulia.

Aligonga tena!, hakuna aliyefungua.



Bado hakukata tamaa msichana wa watu,alihisi Abuu bado hajarudi. Ikabidi aufungue…

Kila akijaribu kuufungua , haukufunguka.

Akasukuma tena, hakuna kilichobadilika - mlango ulibaki vile vile.

Akainua macho juu, alihisi labda amekosea chumba. 'NO. 45', yalisomoka maneno juu ya chumba kile.

"Ndiyo hiki hiki! Sasa mbona kimefungwa?"

Alijiridhisha na kujiuliza, akakosa jibu.



Alizidi kuhangaika binti wa watu, akaelekea mpaka mapokezi, hapo alimkuta msichana mfupi, mweupe, Mwenye taswira ya upole na ukarimu katika sura yake…



"Welcome madam! What can I help you?"

(Karibu! Naweza kukusaidia nini?)

Msichana yule alimuuliza Magreth, huku akimtolea tabasamu jepesi.

Ilihali anayetolewa tabasamu hilo, kijasho chembamba kilianza kutiririka katika mfupa mkuu wa pua. Akakifuta kwa mkono, hakukumbuka leso muda huo. Kisha naye akatabasamu kwa kujilazimisha na kumjibu.



"Thanks! I want to ask about room no. 45,"

(Shukrani! Nataka kuulizia kuhusu chumba namba 45).Magreth aliuliza kiuchovu.



"Oooh! Do you wanna book it?"

(Oooh! Unataka ukichukue?), yule mhudumu aliuliza kwa shauku, akizidi kuulazimisha uchangamfu wa kibishara. Angali moyo wa Magreth ukiomeshwa kuingiwa na baridi nzito.



"No! I know it is already taken,"

(Hapana! Najua kimeshachukuliwa,") Magreth alijibu, akionesha uhakika mzito kwa azungumzayo.



"Sorry madam! This room was unbooked since 10:00 am,"

(Samahani madam! Hiki chumba kilikuwa wazi tangu saa nne asubuhi).

Yule mhudumu alijibu, akimtolea kitabu cha wageni ili kumthibitisha.



Magreth wala hakutaka kukitizama,alianza kuhisi kizunguzungu akashindwa kusimama, aliona walimwengu wote wanamsakama, kwa maneno ya kejeli na kuudhi wanamsema,

Moyo ulimkaza akashindwa hata kuhema.

Maskini! Magreth wa watu alihisi jahazi kwake ndo lishazama, asiweze kupapatika na kuita hata mama!.



****

Nchini Tanzania, ndani ya hoteli kubwa katikati ya mji...



Ni Abuu, Patrick na Harrison. Wapo katika maongezi ya upongezaji, meza yao ikiwa imezungukwa na vinywaji vingi na kila aina.



"Daah! Nashkuru sana Abuu. Sikutegemea kazi ifanyike kwa haraka na ubora wa namna hii," Harrison alitoa shukrani huku macho yake yakiendelea kutazama picha alizowasili nazo Abuu.



"Hahahah! Mimi nimekwambia Harry. Huyu ndiye ZEE LA NYWILA!," Patrick aliongea kwa furaha na kicheko kikubwa.

Abuu hakuwa na pupa, aliwatazama kwa zamu, akamalizia kwa mbali kicheko adhimu.



"Sasa Mr. Password!," Harrison aliita.



"Naam!," Abuu akaitika.



"Pesa yako tayari nimeshakuingizia katika akaunti, ila! Kuna kazi nyingine mezani. Je uko tayari?".

Harrison aliuliza, huku akitoa simu yake ili atafute kitu fulani.



" Bila shaka!" Abuu alikubali kiume, anajiamini! Na hii ndiyo sifa ya mwanaume. Hakuna kuyumba katika maamuzi wala kuchelewesha.



"Kuna wasichana wawili, ni mapacha na watoto wa sheikh mkuu mkoani Mbeya. Wanaitwa Nuru na Ney. Picha zao zinahitajika ndani ya wiki moja. Zote wawili kwa Pamoja!.

Utapata sh. milioni 100. Utaweza?," Harrison alitoa maelezo, akahitimisha kwa swali.



"Kazi rahisi hiyo!" Abuu alijibu, akashushia funda moja la kinywaji kilichomo katika glass iliyo mkonini mwake.



Mazungumzo mengine yaliendelea, mipango yote ya safari wakaiweka. Wakaburudika, wakafurahi na kumkabidhi shume za kutosha na kongole Abuu.

Baadae waliondoka, wakamuacha Abuu pale pale hotelini.



Haraka Abuu aliingia zake chumbani, akatoa kidadavuzi-mpakato chake, kwa kasi ya hali ya juu, alichakata ujumbe kwenda mtu aliyemhifadhi kama 'G.C.I'.

Haikueleweka ina maana gani, alimsevu hivyo hivyo tu ; G.C.I!

Ujumbe ulisoma hivi….



"Boss, nimeshakamilisha kazi ya kwanza waliyonituma, Wamenipa kazi nyingine nitakayoanza wiki ijayo!"

_____



Kabla hajamaliza kuandika ujumbe, alianza kusikia michakato ya nyayo ikiikaribia mlango wa chumba chake, akatuliza masikio yake, akayapa uelekeo wote upande ulioko mlango, ni kweli. Mlango ulianza kugongwa.

'ngo! ngo! ngo!'



Haraka, aliifunika 'laptop' yake, akajiweka sawa na kuinuka aende akaufungue…

"Nani tena huyu?" Alijiuliza kichwani,asijue jibu la swali alilojipachika bongoni.

"Nani mwenzangu?" Abuu aliuliza, mkono wake wa kulia ukiwa umekamatia kitasa, wa kushoto-funguo.

"Patrick!"Iliitikia sauti kutoka mlangoni.

Abuu akafungua, baada ya kujiridhisha kwa mrandamo wa sauti pamoja na jina la aliyejitambulisha.



Alishaikariri sauti ya Patrick, ni sauti iliyojaa chembechembe za ulegevu, ulegevu unaotokana na vilevi vikali anywavyo kila kukicha. Hakusita kuufungua, alijawa na hakika ya juu kabisa kuwa ni Patrick, jambo lililokuwa kinyume chake. Hakuwa Patrick.



Mlangoni kulisimama sura za wanaume wawili asizozijua, ila msichana waliongozana naye anamfahamu,anamjua ipasavyo!.

Si mwingine, alikuwa ni Magreth.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Magreth? Magreth amefikaje huku? Ndani ya muda mfupi namna hii?

Yote haya alijiuliza Abuu, kwa sura yenye taharuki iliyojaa aibu.



" Woow! Happy to see you again Mr. Password!"

(Woow! Nina furaha kukuona tena Mr.Password)



"Khee! Mr.Password? Amejuaje naitwa jina hili?"

Abuu alijisaili, kabla swali halijatoka katika akili, Paap! Patrick aliingia ndani, bila ya shaka wala wasiwasi wa idadi ya watu aliowakuta, kuonesha anafahamu kipi kinaendelea.

Dakika moja! Harrison naye alifika.



"Parick! Harrison! Tunafanyiana nini tena hivi?".Abuu alihoji, moyo wake ukizidisha kasi ya mapigo, hakuelewa na hakutaka kuamini kwa alichokuwa anakiona machoni mwake.



" Kamata huyu msaliti! Apate dozi ya kutosha. Halafu mtamfanya mtakavyo, ninachohitaji auwawe."

Hayo ndiyo maneno ya mwisho kusikia Abuu, kabla hajapata kipigo kizito kichwani, mpaka akapoteza fahamu papohapo.

Hakuelewa kipi kilifuatia na kujiri baada ya pale.



…………..

Vuta na sukuma za kitu kizito, kulikoambata na upepo mkali wenye baridi lichomalo, kulimfanya afunue macho yake, yaliyogoma kufunguka kwa uchovu na maumivu makali anayoyahisi katika mwili.

Alikuwa ni Abuu, akiwa mtupu kama alivyozaliwa,hajiwezi kwa lolote! Alielea juu kwa juu, karibu na ufukwe wa bahari.

Upepo na mawimbi yalimpelekea uelekeo autakao na asioutaka, wenye hatari usio na hatari. Ilimradi tu, ulikuwa ni wa bahari.

Hakufaa kwa lolote lile yani, ujanja wote, kelele nyingi na mbwembwe! Leo havikuwa na nafasi kuja kumsaidia, Abuu alionesha kudhibitika haswa.

Hali aliyozinduka nayo,haikuwa nzuri hata thumuni, akajikuta anapoteza fahamu tena palepale juu ya maji.



Kuja kushtuka kwa mara nyingine, alijikuta yuko ndani ya chumba.

Taratibu, moshi na harufu kali za madawa ya kienyeji,yalivamia mifereji ya pua zake, kadiri muda ulivyoyoma, yakausokota utulivu wa ubongo wake…

"Koh! Koh! Koh!" Alishindwa kujizuia, akaanza kukohoa kwa ukali.



"Pole! Pole kijana." Aliisikia sauti ikimpoza pembeni yake.

Hakumtambua ni nani, kila alipojaribu kumgeukia amtazame, shingo na kiwiliwili vyote viligoma kushirikiana kufanya hivyo.

Alihisi maumivu makali sana, zaidi ya sana.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Tulia hivyo hivyo! Utaumia sana ukilazimisha kujisogeza". Yule mtu wa pembeni yake akaendelea kumtuliza.



Hakuwa na namna nyingine Abuu, akatulia vilevile kama alivyoelekezwa, akapokea matibabu bila ya kujua amtibiaye, afanye nini sasa?.

Alikuwa ni mwenye kutambua kabisa kuwa alipata kipigo kizito, na waliosababisha yeye kufanywa hivyo anawafahamu pia.

Ila, chanzo kikuu cha wao kufikia kumtendea unyama hakukifahamu.

Alibaki njia panda.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog