Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

NIKUITE NANI? - 2

 






Simulizi : Nikuite Nani? 
Sehemu Ya Pili (2)






Mazoea ya Jamila na Abdul yalitengenezwa kwa asilimia kubwa na mama yake Jamila. Ama mlezi kama Jamila mwenyewe anavyomtambua. Yeye hakuwa na nia hiyo. Ila ilimbidi kufanya hivyo aweze kuficha kilichoshamiri moyoni mwake. Kisasi, dhidi ya wanaume. Fuadi wake hukuruhusu chembe ya upendo kwa mtu yeyote mwenye jinsia ya kiume. Aliwachukia haswa, sababu ikiwa kifo cha mama yake mzazi aliyewahi kubakwa hapo nyuma, hata naye pia. Alibakwa!



Akikumbuka tukio hilo hujawa na machungu, kiasi kwamba hutamani aingie mtaani ararue watu wa aina hiyo hadi pale nafsi yake itaporidhika.

“Nilishajiapiza. Katika ukamilishaji wa kazi hii sipaswi kuzoeana na mwanaume yeyote. Sasa huyu kinyaragosi aliyeanza kuniingia ndani anaweza niharibia,” alijisemeza Jamila. Akiwa kasimama moja ya kuta chumbani kwake akiisaili picha iliyobandikwa kwenye ukuta huo. Picha ya Abdul.

“Nikizembea atanisumbua. Dawa yake, ni kufanya kile nilichowafanyia wenziye,” aliendelea kujisemeza. Huku akihama hatua moja na kusogea sehemu nyingine. Ambapo napo kulikuwa na picha. Picha ya mzee Namahala.

“Wewe ndiye nikutakaye kwa udi na uvumba. Umesababisha niishi maisha ya utangaji na mwishowe ukanifanyia kitendo kibaya. Najuta kupokea msaada wako, ningelijua…”

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kauli ya usimhukumu mtu pasipo kujua ukweli hapa ndipo ilijidhihirisha. Jamila alikuwa na lake moyoni. Tena fukuto kubwa ambalo halikutuliza akili. Muda wote alikuwa na mshawasha wa utulizaji, na njia pekee ambayo aliiona ni kulipiza kisasi. Je, ni sawa ukosewapo lazima ulipize kisasi? Vilevile kuna ulazima wowote wa kumsaidia mtu akuchukiaye na asiyehitaji chembe ya msaada toka kwa mtu yeyote?



Tusubiri majibu toka kwa Jamila.

__________



Hatua ya kwanza katika harakati niliyoianza niliuweka pembeni utukufu ulioniiva kwa kiasi, na kujivika matendo yasiyostahili ili niweze kuendana vyema na yule nitakaye kumsaidia. Nikaanza ratiba ya kutembelea maeneo mengi yahusishwayo na biashara ya uuzaji mwili.



Nikaanza kutembelea sehemu za baa, ambazo kwa asilimia kubwa wengi wao wajihusishao na biashara hiyo hutumia. Nilipita baa moja baada ya nyingine, sikuishia hapo, nikatembelea na maeneo ya wazi. Ambayo hutumika haswa usiku.

“Kwa urembo alionao, itakuwa anafanyia shughuli yake kwenye mabaa,” nilijisemeza, wakati huo nikichanja mbuga kurejea nyumbani baada ya kamilisho la hatua ya kwanza. La kufahamu maeneo yatumiwayo kwa hiyo shughuli.



Hatua ya pili niliianza kiza kilivyoingia. Saa moja usiku. Nikajikoki vyema, kwa mavazi mazito na yenye kutengeneza maficho yampayo mtu ugumu wa utambuzi. Nikarudi sehemu zilezile nilizopita mchana. Kweli! Nikawakuta wadada wengi wakiwa katika makusanyo yaliyowapa fursa ya kujadiliana huku wakisindikiza na fundo la vinywaji tofauti tofauti vilivyomo kwenye bilauri.



Nilipita baa moja baada ya nyingine. Lakini angaza yangu haikuwa yenye manufaa. Nilikuwa naangaza angaza juu juu tu, hali iliyonipelekea nijione mpuuzi baadaye. Kwamba nawezaje kumpata yule nimtakaye kwa kile nifanyacho? Nilijipuuza, kisha nikajitafakari na kupanga shambulizi lingine nililoamini litanisaidia.

“Yanipasa kutoka na dada mmoja. Kufanya hivyo, kutanipatia dondoo za shughuli zao zitazonirahisishia kumdhibiti Jamila. Maana kwa namna alivyo mrembo vile hafananii kufanya hii kazi,” nilijisemeza. Wakati huo nikiingia kwenye baa moja maeneo ya Mwanjelwa. Ifahamikayo City pub.



Wakati huo mfukoni mwangu nilikuwa na kiasi cha shilingi elfu kumi na tano. Niliyoitoa katika akiba yangu niitunzayo nyumbani. Niliangaza huku na kule, baadaye nikapiga hatua hadi kwenye kona moja ambako kulikuwa na meza iliyo tupu. Nikavuta kiti na kuketi. Punde, nikafuatwa na dada mmoja mhudumu kunisaili huduma nitakayo.

“Nipatie grand malta,” nilimjibu yule dada baada ya kuniuliza.



Akaondoka!



Hakukawia, sekunde sabini na tano baadaye alirejea akiwa na sahani iliyo na kinywaji nilichohitaji. Akiwa anadengua kwa kuutingisha mwili wake huku na kule na kuwafanya aliowageuzia mgongo watumbue macho kumshangaa.



Japo sikufahamu washangaacho, ila nikahisi kitu gani washangaacho. Makalio, ikanibidi nami nijawe na hamu ya subira pale atapogeuka baada ya kunihudumia nimwangalie vyema nihakikishe kitu nihisicho kinachowachukulia muda washangaao.

“Unahitaji huduma nyingine?” aliniuliza. Baada ya kutua kile kinywaji.

“Nitakuita nikihitaji.”

“Sawa. Nikutakie wakati mwema.”

“Ahsante!”



Akaondoka!



Alivyogeuka na kunipatia mgongo, nikaruhusu uathirika wa kupotezewa muda. Niliyatumbua macho yangu pima, kwenye kigingi kilichompa uzito katika utembeaji. Makalio. Alikuwa na makalio makubwa sana, tofauti na uhalisia wa mwili alionao.

“Mmmh!...haya ya mchina ama?” nilijisemeza, baada ya kumbukizi ya kauli za vijana nilipokatiza kijiwe kimoja mtaani. Kwamba siku hizi wanawake wengi wenye makalio makubwa si ya asili, bali ya kutengenezwa na vifaa maalumu.

“Ina maana hakuridhishwa na uumbaji wa muumba wetu? Au katumia ule msemo jisaidie nami nitakusaidia?” niliendelea kujisemeza, wakati huo taratibu nishaanza konga koo yangu kwa fundo la kile kinywaji.



Nilipiga fundo tatu za haraka haraka na kukitua. Kisha nikapiga jicho huku na kule kusaili mazingira yalivyopambika. Kwa watu waliokuwa wanaburudika kwa mdundo uliosikika toka kwenye spika ndogo ndogo zilizotegwa kila kona. Wengi wao waliokuwa wanafanya shughuli hiyo walikuwa wadada. Walioonekana wazi wanapelekeshwa na akili ya ziada iliyochipua baada ya kupiga vinywaji ambavyo walikuwa wamekamatia mkononi.

“Hawa ndiyo walewale,” nilijisemeza. Macho yangu yakiwa pima kaunta kusaili nyonga zinyongwavyo. Hakika zilinisisimua, kiasi kwamba mwenye jinsia alisimama kidete kuonyesha umbo lake halisi surualini.



Nikapandwa na mzuka. Mshawasha wa kutosha. Hali iliyonificha neno ustahimilivu. Kidume nikajipamba, kwa kulainisha koo, kupitia ukohoaji mdogo nilioufanya. Kisha nikayaondoa macho yangu kule kaunta. Nikayaangaza kwenye uwazi ulio na meza zilizokaliwa na watu mbalimbali wakijinafasi. Nikamuona mmoja wa wahudumu. Nikampungia mkono uliomwashiria kumuhitaji. Kwa bahati, aliifahamu hiyo ishara. Akapiga chapuo akanifuata nilipo.

“Samahani,” nilisema, punde alivyonifikia.

“Bila samahani kaka yangu. Niko kwa ajili ya kukuhudumia,” alisema yule muhudumu. Ambaye umri wake kwa mtazamo wangu haukuzidi miaka thelathini. Mhudumu wa kike, aliyebarikiwa ngozi yenye rangi asili ya kiafrika. Kwa umbo, hakutofautiana sana na yule aliyenihudumia awali. Wamelandana, tofauti imejitokeza kwenye rangi. Yule wa awali hakuridhishwa na uumbaji wa muumba wetu hata kwenye rangi. Alijichubua.

“Naomba uniitie m—dada mmoja kati ya wale warembo pale kaunta.”

“Unahitaji huduma nyingine tofauti na hiyo?”

“Ukinikamilishia hiyo nitafurahi.”

“Sawa,” alisema yule muhudumu taratibu akipiga hatua kuelekea nilikomuelekeza.



Dakika chache baadaye mmoja miongoni mwa wale wadada waliokuwa wanasakata rumba pale kaunta alizuru kwenye meza niliyopo. Sikusita kufurahi. Kutokana na imani niliyoanza kuijenga moyoni mwangu, kwamba mtu huyo ana uwezekano mkubwa wa kuniambia habari za Jamila. Kwa sababu wengi wao hufahamiana.

“Naweza kukuongezea kinywaji?” nilimuuliza.

“Litakuwa jambo jema,” alinijibu. Wakati huo akiwa katupa jicho katika wajihi wangu. Nadhani alikuwa ananitathmini nifananavyo.

Punde nikatii takwa lake. Nilimuita muhudumu na kumuamuru amletee kinywaji. Sehemu kubwa ya maungo ya mwili wake kukata kiuno yakiwa wazi. Alivaa sketi fupi.



Taratibu nikayaanza maongezi pindi tunamsubiri muhudumu. Nilianza kwa kutaka ufahamu wake, naye pasi na hiyana akanieleza japo sina hakika kama ulikuwa halisi. Ila sikutilia maanani sababu halikuwa lengo langu. Isitoshe hata yule aliye mbele yangu hakuwa na lengo la mada hiyo.

“Dada u—mrembo sana. Natamani tuufukuze usiku wa leo tukiwa pamoja,” nilimchombeza, jicho likiwa kwake, nikamshuhudia akilegeza macho yake, na kutingisha tingisha matiti, lengo anisisimue vilivyo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Hamna shida. Sema utalipa bei gani usasambuke na goma lote hili kwa muda wote utakao?”



Swali hilo likanipa ukimya wa tafakuri. Kuhusu kiasi cha pesa nilichonacho mfukoni kisha kile nilichoacha nyumbani. Nilivyokitathmini, na kuona kinamfaa, nikamjibu.

“Nakupa elfu thelathini.”

“Acha utani. Yaani zigo lote hili nilale nawe kwa kiasi hicho? Ongeza hela bhana! Hebu angalia,…angalia…” alisema yule dada. Akiwa kainuka na kujigeuza geuza nishuhudie umbo lake kwa ufasaha.

“Unahitaji niongeze kiasi gani?”

“Elfu ishirini.”

“Napandisha elfu kumi hapo juu, ishirini sitomudu kuilipa.”

“Mmmmmh!...sawa. Hamna shida.”



Muhudumu alivyorejea aliparamia kile kinywaji na kugugumia kwa pupa. Haikumchukua dakika mbili, alivyokitua, chupa ilisalia na kimiminika robo.

“Oooh! Hapa sasa niko vyema. Naweza kata uno kwa namna yoyote na kuruhusu kuingiliwa kwa mtindo wowote na Abdallah kichwa wazi wa kimo chochote pasipo kuhisi maumivu,” alisema yule dada akiwa kashaamka na kutingisha makalio yake. Yalikuwa tepe tepe kwa ulegevu. Hakuvaa nguo yoyote ya kumstiri amfanyaye awe na kiburi kwa vidume.



Uwepo wa kukaa eneo lile ulikatishwa mara baada ya kulipa bili niliyopatiwa kulingana na huduma niliyofanya. Tukajikokota taratibu, kwa sababu yule dada tayari alikwisha lewa, hivyo hakuwa na nguvu ya kutosha ya kumwezesha kutembea. Tulivyofika umbali fulani niliita bajaji, tukapanda kisha nikamwamuru dereva atufikishe maeneo ya nyumbani.



Mwendo wa dakika nane tu, ukatufikisha nyumbani. Nililipa, tukateremka na hatimaye nikamwongoza kuelekea chumbani kwangu. Tukapokelewa na kiza kizito chenye kuleta uogofyaji. Ila hali hiyo ilifukuzwa nilipowasha taa na kuruhusu nuru iangaze vyema mule chumbani.

“Hiki kitanda kitahimili mikiki mikiki? Maana siwezi kulala kwa goli moja, goli tatu ndizo hunipa mwanga kidogo. Tena ukiweza kunifikisha hivyo? Utakuwa mwanaume wangu utakayelisasambua goma langu pasipo malipo,” alisema. Akiwa anatomasa tomasa godoro kupima uimara wake.



Zoezi lile alilisitisha ghafla, alipoiona picha fulani usawa niwekao mito.

“Hee! Unamfahamu huyu?” aliniuliza akiwa mwingi wa mshtuko, picha kaikamatia mkononi akiisaili.

“Ndiyo, namfahamu. Kulikoni?”



Kikapita kimya, takribani sekunde arobaini na tano, macho yake pima kwangu, uonaji ulionitambulisha ananitathmini.

“Pumbavuuu. Hata kama nafanya hii kazi. Ila siwezi kutembea na mwanaume aliyetembea na huyu dada,” alisema yule dada, akafuatia kuitupa ile picha akafungua mlango na kuondoka.



Ikanibidi nami nikaze miguu kumfuata. Kutokana hakuwa na ukawaida, pombe aliyokunywa ilimpelekesha na kumfanya mzito katika utendaji hakufika mbali nilimfikia. Nikamkamata na kumgeuza.

“Utanikimbiaje wakati ushakula cha kwangu?” nilimuuliza, nikijivika hasira ya uongo kumwaminisha nina hasira kali.

“Hapana, hapana, siwezi kufanya na wewe kitu chochote. Kama unataka gharama zako, tuongozane nikapate wanaume wawili watatu wanifanyie kazi nikurejeshee,” alisema akiwa anayumba yumba.

“Acha ujinga. Huwezi ondoka pasi na maelewano. Turudi tukaelewane vyema ndani,” nilisema, huku nikijitahidi kumvuta vuta lakini ilishindikana, kwani alijishikiza sehemu fulani iliyonipatia ugumu wa kumfanya aachie.

“Usinilazimishe. Nishakuambia siwezi kutembea na mwanaume aliyetembea na yule dada. Nitawezaje kujipeleka sehemu ambayo najua matokeo yake ni kifo? Yule dada ni malkia wa hii biashara hapa mjini, si anaitwa Selina? Hakuna asiyemfahamu. Wanaume, kwa wanawake wa kutosha wameteketea kwa sababu yake. Hivyo niache siwezi…” alisema, ila sikumpatia nafasi ya kumalizia kauli yake nikamkatisha.

“Anawauwaje?”





Hakujibu lile swali. Nikashangaa kumuona akinisukuma kwa nguvu na kukimbia kwa kujiokoteza. Kabla sijamfukuzia kwa mara nyingine, ikanibidi nigeuke nyuma yangu kuangalia kulikoni, maana kwa namna alivyonisukuma kuna kitu fulani alikiona nyuma yangu cha kuogofya kikamsukuma kufanya hivyo. La haula! Sikuamini nilichokiona. Shangazi alikuwa nyuma yangu, na kwa mbali nilimuona mtu fulani akitokomea uchochoroni, nilivyojaribu kumtupia macho yenye lengo la kumfahamu sikumtambua, ila muonekano wake, haikutofautiana sana na muonekano wa Jamila.

“Shangazi!” nilimuita.

“Turudi nyumbani.”



Sikusita, nilitii amri yake. Taratibu, tulipiga hatua kuelekea nyumbani. Lakini nilijikuta nina sintofahamu kubwa kumfikiria yule dada, na shangazi pia, usiku ule anatoka wapi. Nilivyoyachunguza mavazi aliyovaa, yalinipa utata zaidi wa kunihimiza nimfuatilie kiundani.

__________



Asubuhi. Punde baada ya kupambazuka nilipata stafutahi, baada ya hapo nikajifungia chumbani kwangu kufanyia kazi yale yaliyonitatanisha na kuumiza akili yangu. Kuhusu yule dada niliyomchukua jana baa, shangazi na Jamila pia, ambaye yule dada alimuita kwa jina la Selina. Ndiye mtu ambaye alimuona kwenye ile picha. Niliyoiacha pale kitandani, nikiwa na azma nifahamu kama kweli anajihusisha na hiyo biashara.

“Jamila ni nani?” nilijiuliza, nikiwa nimekamatia ile picha. Nikimtathmini vilivyo.

“Haendani kabisa na ayafanyayo. Mwanamke mzuri, anayestahili kuwa ndani ya ndoa, lakini…” nilijisemeza, ila sikumalizia kauli yangu, baada ya kushindwa kupata neno sahihi la kulitamka.

“Na kama anafanya mauaji si angelikamatwa? Ama hayo mauaji anayatekeleza kwa namna ipi?” niliendelea kujisemeza, ila hali hiyo ilikatishwa mlango wa chumba changu ulivyogongwa.

“Dully njoo nje nina maongezi nawe,” ilisikika sauti toka nje mara baada ile ya kugongwa kumalizika.



Sababu niliitambua ni sauti ya nani nikatii takwa lake. Nilijiinua nilipoketi, kisha nikapiga hatua hadi nje. Nikamkuta shangazi kaketi kigodani usawa wa kiambaza.

“Shangazi. Ile jana ulikuwa unatokea wapi?” nilimtupia swali hata kabla ya salamu.

“Mihangaiko mwanangu.”

“Mihangaiko? Mihangaiko gani ya usiku?”

“Mwanangu. Nilikuwa natafuta amani ya moyo wangu?”

“Kivipi?”

“Mimi na Jamila, ni washirika…” alisema shangazi, ila hakumalizia kauli yake, nikamkatisha.

“Shangazi, nawe unafanya biashara ya kuuza mwili?” nilimuuliza nikiwa nimehamaki vya kutosha.

“Ndiyo kazi iliyonisaidia kukutunza vyema.”

“Mmmmh!”

“Usijisikie vibaya. Kuna stori ndefu katika hili. Ndiyo maana siku zote nakuambia usimhukumu mtu pasipo kufahamu chanzo cha hali aliyonayo.”

“Kwa hiyo unataka kuniambia nawe unauwa?”

“Sahihi. Tunafanya hayo si kwa matakwa yetu. Bali ni hali ya maisha kwa yale tuliyopitia.”

“Sasa, ule ushauri wako una maana gani kwangu wakati nawe ni walewale?”

“Ukiuona haukufai, usiutumie, ukikufaa endelea kuutumia,” alisema shangazi. Sauti ikiwa imetapakaa unyonge, ulionisukuma kujenga huruma moyoni mwangu.



Hali hiyo ikanisukuma kupata kumbukizi tangu mwanzo nilivyokutana naye. Hapo ikanipa picha juu ya kauli alizoniambia sasa. Ikanipa nafasi nyingine pia ya kuchanganua. Kwanini anajihusisha na matendo hayo ambayo ni ovu kwenye jamii yetu. Nikaenda mbali zaidi, kwa kukumbuka ushauri anipatiao na maana halisi ya yote afanyayo kwangu, sikupata jibu.



Kumbukizi hiyo ilikatishwa na ujio wa gari ya jeshi la polisi, aina ya Toyota Land cruiser ikiwa na askari watatu ndani. Gari ilivyoegeshwa wakateremka chap na kuongoza pale tulipo. Nilivyotupa jicho kwa shangazi nikamshuhudia kakumbwa na hali ya katisho la tamaa. Hakuwa na hili wala lile. Wale askari walivyotufikia walitusabahi na kujitambulisha, walikuwa askari wa kitengo cha upelelezi, kwa uthibitisho walitoa vitambulisho vyao na kutunyooshea tuhakikishe.



Utambulisho ulivyohitimishwa wakaeleza dhamira ya ujio wao. Kumweka chini ya ulinzi shangazi na kuondoka nao kwenda kituo cha polisi. Shangazi hakupinga, alinyoosha mikono, akavikwa bangili (pingu) na kuondoka naye taratibu kuelekea gari ilipo.

“Abdul, fanya uliyoyadhamiria. Hili lisikurudishe nyuma, litapita tu. Shangazi yako nimefanya kosa kubwa sana, ambalo naamini adhabu nayopaswa kupatiwa ni kunyongwa. Sina kikubwa cha kukuachia zaidi ya shajara niliyoiacha kitandani kwangu. Naamini yaliyomo yatakusaidia,” alisema shangazi, chozi likimtiririka kama mtoto mdogo.

“Umefanya kosa gani?”

“Usiku wa jana nimetimiza nilichopanga. Siku zote nilikuwa nakung’ang’aniza umfuatilie Jamila ili uniachie nafasi ya kufanya mambo yangu kwa uhuru. Namshukuru Mungu hilo nimefanikiwa. Kilio changu kimetimia, majibu ya mihangaiko niliyokuambia ndiyo haya. Sasa nina amani ya moyo. Ila nakuomba, hakikisha ile ahadi yako inakuwa timilifu. Mkomboe Jamila na wanawake wengine wenye tabia kama zake.”

“Shangazi, mbona sikuelewi?”

“Nime… Nimemuua, yule…yule…” alisema shangazi pindi wale askari wakijitahidi kumpakiza ndani ya gari.



Baadaye gari ikawashwa na kuondoka.

Hapo ndipo nikaja amini ule msemo, usimwamini mtu. Kwani ubaya na wema wa mtu hautambuliki kwa muonekano.

__________



Siku iliyofuata jiji lilienea taarifa iliyoleta uogofyaji ndani mioyo ya wengi. Taarifa ya mauaji. Kifo cha mfanyabiashara maarufu na mashuhuri jijini. Raibu Mwakipe. Taarifa hii niliisikia redioni, nikiwa naperuzi shajara aliyoniachia shangazi. Nathubutu kusema, katika shajara ile aliandika maneno yaliyojaa hekima yaliyonishangaza na kunifikirisha sababu iliyomsukuma ajihusishe na ile tabia.

Ile taarifa ikanisitisha kwa muda kuendelea kusoma yaliyoandikwa. Niliweka tuo na kutega sikio vyema kusikiliza sauti ya mtangazaji.

“Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya, kathibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusadiki kuwa mtuhumiwa kakamatwa na hivi sasa yupo chini ya jeshi la polisi. Kamanda huyo kaenda mbali kwa kusema, mtuhumiwa wa tukio hilo ni mwanamama, akadiriwaye umri wa miaka arobaini na saba…” ilisikika sauti redioni. Lakini haikufika mwisho, mawimbi yakaanza haribu ile habari.

Moja kwa moja taarifa hiyo nikaihusisha na tukio lililompata shangazi. Hakika niliamini inamhusu, imani hiyo ikaja ongezeka nilivyorudisha jicho kwenye kurasa za shajara na kukuta kifungu kidogo cha maneno yaliyoandikwa kwa wino mwekundu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Raibu Mwakipe, umeyafanya maisha yangu kuwa ya kutanga tanga punde ulivyonigeuza mtumwa wa ngono, mwishowe ukadiriki kupora mali za wazazi wangu na hatimaye kuwauwa. Nakuahidi, nawe siku moja utawafuata wazazi wangu walipo nikiwa kama msababishaji wa kifo chako.”



Maneno haya niliyarudia zaidi ya mara tatu kuyasoma. Na kunifanya nikumbuke kauli za shangazi. Mwisho wa kumbukizi nilitokwa na sikitiko liliniamrisha nimsaidie atoke sehemu aliyopelekwa awe uraiani. Ila Nitawezaje? Ulikuwa mtihani kwangu. Nikijumlisha na ule wa Jamila ndiyo kuzidi.



Jioni ya siku hii nikazuru kituo cha polisi alikopelekwa shangazi. Huku nikiwa na picha ya tukio alilofanya ambalo nilisikia na kutazama habari zake kwenye kijiwe fulani. Dhahiri, alifanya kitendo cha kikatili. Kitendo ambacho hakivumiliki kwa mtu yeyote, ila kwangu alikuwa mlezi na ni mzazi, sikuwa na budi kumsamehe.



Yule tajiri alimuua kifo cha kikatili sana. Kwani alimbana korodani, na uume alimuwekea kitu fulani kilichosukuma utoke mapele tele, kuvimba, na hatimaye kupasuka.

“Shangazi, kwanini umemfanya vile yule mwanaume?” lilikuwa swali langu la kwanza punde nilivyopata nafasi ya kuzungumza naye.

“Abdul! Maumivu yanauma. Sikuwa na lingine la kufanya zaidi ya lile nililofanya. Yule mtu alinifanyia vitendo vya kinyama sana…” alisema shangazi na kuweka tuo. Kabla hajaendelea nikamkatiza.

“Kitendo gani?”

“Katika maisha yangu nafahamu ladha ya mwanaume mmoja tu, ambaye ni yule. Mwakipe ndiye mwanaume wangu wa kwanza na wa mwisho kuutumia fahari yangu. Mwakipe nilimruhusu anitumie atakavyo, kiasi kwamba nikaamini kile nipatacho kwake ndiyo mapenzi ya dhati. Nikamwamini, na kusahau msemo hupaswi kumwamini mtu. Uaminifu wangu kwake ukanifanya niwe zezeta, kwa kutosikia kitu chochote kimhusucho. Najutia hali hiyo…” alisema shangazi na kuweka tuo. Takribani sekunde kumi na nne, kisha akaendelea.

“…uaminifu wangu uliniponza Abdul. Uaminifu wangu akautumia kunisaliti, kwa kuruhusu rafikiziye waniingilie. Sikuamini kile kitendo, hadi leo hivi, sikiamini. Mwakipe alinifanyia ukatili wa hali ya juu, ambao msamaha wake ni kurudisha ukatili. Kwani juu ya alichofanya, hakuona kinatosha, alienda kuwalaghai wazazi wangu wakampatia kiasi kingi cha pesa, ambacho alikirejesha kwa kukatiza uhai wao.”

“Ina maana, alienda kuwakopa walivyomhitaji awarejeshee aliwauwa?”

“Ndiyo. Tena kifo cha kikatili sana. Kifo cha moto. Alichoma moto usiku wa manane nyumba waishio. Tena akisaidizana na wale rafikiziye walioniingilia. Mmoja miongoni mwao, ni mzee…” alisema, ila hakumalizia nikamkatisha.

“Mzee Namahala?” nilimuuliza, nikiwa na hamaniko tele.

“Yule ni mnyama, ambaye hapaswi kuendelea kuwepo duniani. Mzee Namahala kaua ndoto ya Jamila. Kamgeuza Jamila kuwa mtumwa wa ngono asiyehitaji kusikia maneno mawili tu hapa ulimwenguni, Mapenzi na upendo. Jamila anafanya yale si kwa mapendo, bali kwa kiwango cha kisasi kilichopo moyoni mwake. Hivi, nini utafanya, endapo utabaini unayeishi naye kahusika na kifo cha mtu umpendaye?” aliniuliza shangazi. Mboni zikiwa zimeshindwa kustahimili maumivu ajisikiayo moyoni na kuruhusu machozi.



Nilishindwa kumjibu lile swali kwa wakati ule. Nikaishia kumtumbulia macho kana kwamba simfahamu ama ndiyo mara ya kwanza kuonana.

“Natamani kuiona dunia ikibadilika. Ila si dunia, bali waliomo ndani ya dunia. Kama kweli utaweza, jitahidi kuhakikisha ndoto yako inatimia. Nenda kaizuie mioyo yenye visasi, ijae ubaridi wenye kusahaulisha maovu. Fanya hili liwezekane. Mtumie Jamila kuwa wa mfano kwa watu wenye tabia kama zake. Kwani ukiweza hapo, wengine watashawishika kumfuata uelekeo ataokuwa nao. Mengi yapo kwenye ile shajara, kayasome kisha yatumie.”



Maelezo hayo ya mwisho yakahitimisha maongezi yetu. Shangazi akarudishwa mahabusu, nami nikasalia na ambukizwo la huruma lililonishinikiza kuruhusu machozi mbonini. Nilishindwa kutoa sauti tu, ila moyo uliniuma sana baada ya kuzungukwa na ufahamu ulionibainisha duniani kuna mengi, na yote hupaswi kuyaamulia pasipo kuyaelewa. Kuwa na ufahamu nayo!

__________







Niliondoka ndani ya jengo la polisi kiunyonge sana. Hatua zangu zikiwa fupi fupi, huku nikifikiria maisha yangu yatakuaje pasipo shangazi. Nilipolifikia lango la kuingilia nikasita kwa muda, kwani kuna sauti fulani niliisikia, ijapokuwa halmashauri ya kichwa changu ilikinzana kwa sekunde chache kunitaarifu kuwa kitendo hicho ni njozi, na upande mwingine, uliniaminisha ninaitwa. Baadaye ikanibidi nigeuke nyuma kuthibitisha. Kweli! Nilikuwa naitwa, na mmoja miongoni mwa askari walionipatia ruksa ya kufanya maongezi na shangazi. Sikuwa na budi, nikaweka tuo la utembeaji kumsubiri.

“Pole sana kijana,” alisema yule askari alivyonifikia, huku akinivuta pembeni ili tuache nafasi pale langoni.



Tukipiga hatua hadi nje ya jengo. Kisha tukaenda kuketi kwenye benchi fulani lililopo karibu na jengo la kituo. Muda wote macho yake yakiwa pima kwangu kunisaili. Nililigundua hilo, baada ya kupiga jicho la kujiiba iba nililokuwa nalitoa kila baada ya sekunde kadhaa.

“Kijana! Natamani nitoe huruma yangu niitue mwilini mwako, iweze kukutakasa na kutoa mwanga mpya wa maisha unayopaswa kuishi,” alisema yule askari. Niliyemtambua kwa jina la Mzee Seleman baadaye.

“Kwanini?” nilimuuliza baada ya kutafakari kauli yake na kushindwa kuipatia maana.

“Kuipata amani ya kweli, ni lazima tuwe na huruma na matatizo ya wenzetu. Huruma itayotushinikiza kuwa na mioyo ya usaidizi wa tatizo husika. Natamani kumsaidia shangazi yako…”

“Hapana!” nilisema kauli hiyo kwa uharaka hata kabla hajahitimisha kile alichokuwa anazungumza.

“Shangazi yangu haitaji msaada wa kutoka mule ndani. Naamini kafanya vile kulingana na azimio alilonalo. Shangazi yangu anahitaji amani ya kweli japo kahusika na uhalifu. Kule aliko anaenda kutengeneza ulimwengu mpya utaoshangaza wengi,” nilisema. Baada ya kukumbuka andiko moja nililolisoma kwenye shajara yake. Mahabusu na magereza yanazalisha chuki. Ni vyema wale waliomo mule ndani wakasafishwa kuondolewa zao hilo.



Kauli hii ikanipa imani, kwamba kule aliko bado hajapotea. Anaenda kumalizia maisha yake huko kwa kuondoa zao teule lijengwalo ndani ya mioyo ya wengi pasi na matakwa.



Maongezi yetu yalichukua zaidi ya dakika kumi, ndipo tukatamatisha huku nikichukua kadi ya mawasiliano ya yule askari ikiwa na miadi nitapopatwa na tatizo limhusulo na ambalo liko ndani ya uwezo wake kwa utatuzi nimtafute. Baada ya kuondoka mahali pale kituo changu kikawa nyumbani. Tena chumbani kwangu. Nikajipumzisha kwa muda kitandani, takribani dakika tano, baadaye nikaenda chumbani kwa shangazi, nikachukua shajara aliyoniambia nikarejea tena chumbani kwangu.



Siku hii ilipita kwa mafikirio. Kuwakumbuka Jamila, shangazi na yule dada niliyemuopoa baa ule usiku. Walinichukulia muda wangu mwingi sana, kiasi kwamba nilikosa hisia na chakula. Nikalala njaa.



Asubuhi kulivyopambazuka nikaanza panga mambo yangu. Nini nianze kufanya na kipi kifuate. Mipango ilivyokaa sawa utekelezaji ukafuatia. Utekelezaji huo ulianza saa tano asubuhi, punde nilivyopata stafutahi na kuifanya akili na mwili kwa ujumla kukaramka.

“Yanipasa kuanza na yule dada,” nilijisemeza. Taratibu nikiuacha faja wa nyumba yetu.



Azma yangu ya kwanza, ni kumtafuta yule dada niliyemchukua baa siku chache zilizopita. Nikafanya hivyo. Nilipiga hatua hadi City pub, nikapata eneo nikaketi. La pembezoni kidogo, lenye lengo la kuwashuhudia watu waingiao. Wahudumu walivyonifuata kunisaili huduma nitakayo, niliwaongopea kuwa kuna mtu namsubiri, ndiye atayekuja kutoa oda ya huduma tutakayo. Wakawa wanaondoka na kuniacha nijinafasi kufanya nilichodhamiria.



Wakati wote macho yangu hayakuacha kuangaza huku na kule, kumwangalia yule dada, na muhudumu niliyemuagiza ile siku akaniitie. Lakini jitihada hizo zote, hamna nilichoking’amua hadi muda niliodhamiria kuondoka baada ya kuona napoteza muda. Ondoko langu likawa la taratibu. Likichangamana na tahayari ndani, huku nikiendeleza kuangaza pande zote.



Nilivyolifikia lango la kuingilia ikawa bahati kwangu. Hamadi! Bin vuu, nikakumbana na muhudumu aliyenisaidia kumuita yule m—dada. Tukashangaana!

“Samahani,” nilisema. Baada ya kumgonga kidogo sehemu ndogo ya bega, hadi ikampelekea kuyumba.

“Ahsante,” alijibu na kutaka kunikwepa ili aendelee na safari, nikamzuia.

“Nina shida nawe mara moja,” nilisema, huku nikimkingia mkono kumzuia asiendelee kuondoka.

“Fanya haraka, maana nina shughuli tele zinanisubiri.”



Tukasogea pembezoni kidogo mwa lile lango. Tukaweka tuo hapo na kuyaanza mazungumzo taratibu macho yangu yakiwa pima usoni kwake, lengo kupima, kama kile aongeacho kinalandana na muonekano alionao. Ijapokuwa dhana hii mara nyingi siitilii mkazo katika kuamini.

“Namtafuta yule dada uliyenisaidia kumuita ule usiku.”

“Hee! We kaka? Nini kimekunogea kutoka kwake? Unataka kumuoa? Utamuweza? Ama nawe ni mmoja miongoni mwa machokoraa mnaofichwa na unadhifu wa muonekano?” alinitupia maswali mfululizo. Maswali ambayo yalinishinikiza kuanza kujenga haya akilini mwangu. Kwa sababu kuna watu fulani walikuwa pembeni yetu na baadhi ya wateja waingiao na kutoka.



Ghafla nikapatwa na kumbukizi fupi, iliyonisukuma kujenga taswira ya shajara aliyoniachia shangazi, na kwenda mbali hadi kwenye moja ya kurasa iliyokuwa na andiko lililobebwa kwenye aya mbili, zenye mistari takribani tisa.

“Wanadamu wengi dunia ya leo tumekuwa na mioyo iliyosheheni unafiki. Hebu waangalie viongozi wa dini na wote waliotawaliwa udini. Kila kukicha huomba na huimiza watu watende matendo mema, lakini ndiyo hao hao huongoza kuwasema vibaya wale wote wenye imani zao wanaothubutu kutumia sehemu ya maisha yao kuwanusuru wale wenye mazingira hatarishi. Hufanya haya, pale wasipofahamu dhamira ya mtu. Na hata wakiambiwa hupinga, kwa kuamini wao wako sahihi nyakati zote.

“Watu kama hawa mwanangu, wasikupe shida. Wapuuze, haijalishi wana nafasi gani kwako. Wapuuze, ili siku wakikutana nawe, wakupigie magoti yenye ombi la msamaha, na kukupa hongera kwa kufanikisha ulichothubutu kufanya. Pia itawapa fundisho, kwamba uwepo wao duniani, na taaluma walizobarikiwa, lengo kuu ni kuleta mabadiliko chanya kwa watu wenye aina ile unayotaka kuwabadilisha, na wote wenye matendo ovu. Mwisho, watu wajihusishao na matendo ovu, hawapaswi kukimbiwa. Bali wanatakiwa wafuatwe, ili wawezeshwe wapate kujinusuru katika lindi waliloko.”



Kumbukizi hii, ikanifanya nimuunganishe yule muhudumu katika kundi la watu waliotajwa. Kwamba ananidhihaki kwa kujiaminisha yeye ni msafi. Hakika, nilishindwa nimjibu vipi, nikaishia kumuomba radhi na hatimaye kumpa ruksa ya kuendelea na safari. Nami nikaianza taratibu pasipo kufahamu uelekeo maalumu wa kwenda. Nilizunguka huku, nilizunguka kule, mwishowe nikajikuta nimeweka kituo ndani ya baa maarufu pia jijini Mbeya. Carnival.



Hapa nikafanya huduma. Ya maji tu, ambayo niliyanywa taratibu huku nikiangaza mazingira yalivyo. Kwani ilikuwa mara yangu ya kwanza kuingia ndani ya baa hiyo. Nikajionea mengi. Yaliyonifurahisha na kunisikitisha, ila sikuyatilia maanani, nilichokiwaza muda wote ni namna nitakavyompata yule dada anipatie dondoo anazozifahamu zimuhusuzo Jamila.



Uwepo wangu ndani ya baa hii ulihitimishwa punde nilivyofanya malipo ya huduma niliyopatiwa. Nikaondoka, nikiwa na kiapo nafsini mwangu kwamba nitarejea usiku kwa lengo la uchunguzi zaidi baada ya kufahamu nimtakaye anaweza akawa amepumzika ili afanye shughuli vyema usiku.

__________



Saa 4:49 usiku. Nikawa ndani ya baa ya Carnival baada ya kuondoka City pub na kushindwa kumpata yule nimtakaye. Huku nako nilijaribu kudodosa baadhi ya watu hasa wenzake wafanyao shughuli lakini sikupata jibu lililo jema lenye kukonga moyo wangu na kunipa mwanga wa dhamirio nililothubutu kulitekeleza.



Hadi naondoka mahali hapa, nilipata dondoo mbili tu. Moja imhusuyo yule dada, nyingine Jamila. Ambaye na hapo nilitambulishwa kwa jina la Selina. Tena nilipeleka mshangao wa hali ya juu kwa watu niliowauliza. Mshangao uliopeleka uogofyaji kwao, wakiamini mimi ni mtu mbaya. Hapa nikapata picha kamili. Kwamba Jamila, si mtu mwema kabisa. Ambaye hapaswi kuwa na rafiki. Kutokana na matendo aliyoyatengeneza mbele ya jamii aishiyo.

“Hivi wanafahamu kuwa alibakwa ndiyo maana yuko hivyo?” nilijiuliza, nikilivuka lango la kuingilia taratibu kuianza safari ya kwenda nyumbani. Kichwani nikiwa na picha ya kitu cha kufanya siku inayofuata.



Punde nilivyowasili nyumbani nikaelekea moja kwa moja hadi chumbani kwangu. Kitu cha kwanza kufanya, nilichukua shajara nilikoihifadhi nikaendelea na muendelezo wa kusoma maandiko mbalimbali ambayo yalinipa nguvu katika utendaji wa yale niliyodhamiria. Niliijenga hiyo hali kuwa kawaida. Wakati wa kuamka, na kulala pia. Nilipitia maandiko kadhaa ndipo nafanya jambo lingine. Kama kulala, nalala. Ama kufanya usafi wa mazingira niishio basi nafanya.



Usiku huu nikavutiwa na andiko lililoniarifu kuhusu watu wasaidiwawo. Shangazi alinena ya kwamba “usithubutu kumuamini umsaidiaye hata kama yuko katika mazingira hatarishi kiasi gani. Kwani kubadilika, haimchukui muda. Fanya mambo kwa hadhari kubwa, ili usije ukageuzwa kuwa mbaya zaidi ya yule apaswaye.”



Maneno haya yakaniongezea mwanga pia. Namna gani napaswa kufanya. Lilivyomalizika hitimisho la usomaji nikaanza maandalizi kwa ajili ya kulala. Ila kabla sijahitimisha, nikakatishwa na sauti ya mlango ukigongwa. Nikasita kwa muda kutafakari, tafakuri iliyonishawishi kuweka ukinzani nifungue mlango ama lah. Ila baadaye nilikata shauri, nilipiga hatua hadi mlangoni, nikafungua mlango. Sikuamini macho yangu, nilimkuta yule dada niliyemchukua siku ile baa.



Moyo ukalipuka shangwe. Kwa kuamini naenda kupata dondoo kamili zimuhusuzo Jamila. Kwa pupa, nikamruhusu anieleze dhamira ya ujio wake.

“Siku zote nimekuwa nikikosa amani niishiko kwa ajili yako. Ile siku ulinionyesha ukarimu mwingi wa kuhitaji huduma yangu lakini nikashindwa kuwa muelewa. Leo nimekuja kufanya malipo. Hivyo kama utakuwa ridhaa, naomba uniruhusu kuingia ndani tufanye yetu kila mmoja afarijike kwa kile alichokitumia,” alisema yule dada.



Sababu nilikuwa na shida naye sikutilia maanani suala la hofu na vitu vingine viletavyo hatari. Nikamruhusu. Akaingia ndani nikafuatia kufunga mlango.



Kabla hatujafanya kitu chochote kihusicho maambatano ya mwili baina yetu, nikamuomba anieleze ukweli anaoufahamu kuhusu Jamila. Naye pasi na hiyana, akaridhia, akanieleza habari moja baada ya nyingine kwa namna anavyomfahamu.



Habari alizonihadithia hazikutofautiana sana na zile ambazo alinihadithia mama Jamila. Alivyohitimisha za Jamila, akapachikia zinazomhusu zilizopelekea naye aingie ulimwengu huo.

“Ile siku uliniambia huwezi kuishi na mwanaume aliyetembea na Jamila (Selina) imekuaje leo umerudi?” nilimtupia swali, baada ya kumaliza kunihadithia.

“Nilikutana na shangazi yako usiku uleule ukiachana na pale. Akanihadithia mambo mengi yakuhusuyo. Mambo yaliyonishawishi kukuona mwanaume unayepaswa kutunukiwa donge nono lisilohesabika. Kwani wengi tuliopo kule tunatamani kujiondoa, ila ushindwa hujitokeza…” hakumalizia kauli yake nikamkatisha.

“Ina maana nawe unahitaji…” nami sikumalizia kauli yangu akadakia.

“Nahitaji kubadilika. Niwe mtu mwenye stara nitayekuwa mfano kwa wengine. Nibadilishe, ili nami nikubadilishie maisha yako siku moja.”

“Kwa namna ipi?” nilimuuliza. Lakini hakujibu lile swali. Zaidi ya kunitumbulia macho pima yaliyojaa ulegevu wa kumvuta mwanaume rijali.



Hatimaye kikapita kimya zaidi ya dakika tatu. Kila mmoja akimsaili mwenziye, usaili wa waziwazi uliotoa picha kuna kitu fulani chaweza kuja mbeleni.

__________







Wingu zito lilitanda. Upepo wa wastani ukibarizi huku na kule na kusababisha ongezeko la baridi kwa kiasi fulani. Wakati huo nilikuwa barabarani kuelekea nyumbani kwa kina Jamila. Mkono wa kuume nimekamatia vyema bahasha moja iliyo na karatasi ndani niliyoandika ujumbe mfupi umuhusuo.

“Yanipasa kuuacha ujumbe huu pindi hayupo, ili nisije zalisha varangati buree!” nilijisemeza. Huku nikizidi kuchanja mbuga.



Mwendo wa dakika arobaini ukaniwezesha kuwasili nyumbani kwao. Mazingira niliyokutana nayo yakanipa mashaka na ulizo kubwa nililoshindwa kujijibu.

“Ina maana Jamila kadhamiria kufanya kweli? Kasahau wema wao uliowasukuma waishi pamoja kwa muda wote?” nilijiuliza, nikiwa umbali wa mita kumi toka jengo lilipo.

Mazingira niliyokutana nayo yalinitambulisha kutowepo na mtu aishiye ndani ya jengo hilo. Kwani mazingira yazungukayo jengo yalikuwa machafu mno tofauti na vile nilivyokuwa nayafahamu siku zote kipindi cha nyuma.

“Hivi wenye nyumba hii wapo kweli?” nilimuuliza m—dada mmoja aliyekuwa anapita mbele yangu toka nyumba jirani.

“Yupo mtoto wao pekee. Tena hapatikaniki mara nyingi,” alijibu yule dada. Jibu lililonifahamisha mama Jamila hayupo tena ndani ya nyumba hiyo na ukaaji wa Jamila ni wa kufikirika.



Ila sikujalisha sana. Nilichoamua ni kupiga hatua hadi lango la kuingilia nikaipenyeza ile bahasha kwa chini, kati ya ulipoishia mlango na sakafu, kisha nikajiondokea.

“Kwa yale maneno niliyoyaandika nina hakika alichonacho atabadilisha. Apate nafasi ya kujifikiria ndipo awe na ufahamu wa kitu gani cha kufanya,” nilijiaminisha. Na kuupa moyo kazi ya kufanya subira kutarajia jibu la ujumbe wangu. Japo sikukosa shaka la kutojibiwa.

__________

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Jumanne. Ikiwa tulivu pasi na vuguvugu. Saa 4 asubuhi, nilikuwa ndani ya chumba changu nimejilaza kitandani punde nilivyotoka kumsindikiza Eddy. Yule dada tuliyefahamina naye baa. Ambaye kwa sasa alishageuka zaidi ya rafiki kwangu. Muda mwingi alikuwa nyumbani, akinisaidia shughuli mbalimbali, huku akinihadithia matamanio yake na namna alivyoianza shughuli ya kujiuza.



“Abdul! Maisha, yanachangia kwa kiasi kikubwa wengi wetu kufanya shughuli tusizozipenda na ambazo hazikuwa katika matarajio yetu. Natamani ningelikuwa nimekufahamu kwa muda mrefu, naamini sasa ningelikuwa kwenye historia ya kuhesabiwa kuwa nilikuwepo,” nilikumbuka kauli ya Eddy, ikachangia niwe na mafikirio mengine ya kuendelea kumkumbuka.



Kumbukumbu yangu ilihitimishwa nilivyosikia sauti ya mlango ukigongwa. Nikainuka pale kitandani na kuanza kupiga hatua kuelekea mlango ulipo nikafungue. Ila ajabu iliyoje nilipofika katikati baina ya kitanda na mlango, nilishuhudia mlango ukisukumwa kwa nguvu na kufunguka. Kwani sikufunga, niliuegemeza na kistuli.

“Hey! Kulikoni? Mbona mnaingia nyumba za watu pasipo idhini?” niliuliza. Baada ya kuwaona vijana wawili wakiwa wamesimama pale mlangoni.



Walikuwa vijana ambao waliumbwa kwa maumbo membamba, wakitawaliwa na rangi nyeusi pamoja na nywele za kipilipili kichwani. Uvaaji wao wa nguo haukuwa wa kistara. Nilishuhudia suruali wamezivalia makalioni, juu wakiwa tupu, mashati yao waliyafunga mkononi lengo nishuhudie vifua vyao vilivyojaza. Pamoja na zana walizokuwa wamechomeka kwenye mkanda kiunoni, zilizonitambulisha ujio wao si wa wema. Maana walikuwa na visu, bomba la sindano pasi na sahau ubao mdogo uliopigiliwa misumari.

“Wewe ndiye unajifanya kufundisha tabia njema?” aliniuliza mmoja wao, taratibu akinisogelea nilipo, nami kuona hivyo ikanibidi nisogee kinyume nyume niweze kupata nafasi ya kujitetea.

“Tusipoteze muda. Si unakumbuka maelezo ya tajiri?” aliuliza mwenziye.

“Yah! Nakumbuka. Tumpatie huduma itayompa fundisho la kutofuatilia maisha ya watu.”

Kwa maelezo hayo mafupi waliyokuwa wanajiongelesha yakanifungulia kitu fulani akilini mwangu. Nikajipa kazi ya kujifikirisha mara mbili kwa wakati mmoja. Yaani nilifikiria tukio lililoko mbele yangu, na huyo wamuitaye tajiri yao ambayo namfuatilia. Moja kwa moja nikamhisi Jamila. Kwa sababu sikuwa na mtu mwingine nimfuatiliaye zaidi yake.

“Ina maana, Jamila kaamua kunilipa hivi baada ya kumpelekea ule ujumbe?” nilijisemeza, akili ikiwa mbali kumchambua Jamila na namna ya kujihadhari mbele ya vijana walioko mbele yangu. Ambao kwa mazingira waliyonayo yakaniongezea utambuzi, kuwa ni watumiaji wa madawa ya kulevya.



Hali hiyo ilikatishwa punde ngozi yangu ilivyoruhusu hisio la vidole vikitembea tembea. Nikashtuka, nilivyotaka kujiweka sawa kwa makabiliano, ikibidi kuwakimbia, niliishia kukamatwa kama mtoto mdogo huku wakinitupia makonde sehemu mbalimbali za maungo ya mwili wangu. Nikajaribu kujifurukuta, kwa kujitingisha tingisha huku na kule lakini sikuambulia mafanikio ya uokozi, zaidi ya kuruhusu sehemu zisizopaswa kupigwa wapige.



Walivyoona nawapatia wakati mgumu ulioashiria matokeo mazuri upande wangu hawakusita kutumia zile zana walizokuja nazo. Kuna muda nilikuwa nazisikia namna zipenyavyo hasa hasa sindano. Walikuwa wanaitumbukiza mwilini kama vile daktari achomavyo mfu.



Kwa namna ambavyo walinibananisha hata sauti ya kuomba msaada kwa majirani sikuweza itoa. Kwani walinisundikia matambala mengi mdomoni yaliyochangia kwa kiasi kikubwa nipokee kipigo. Yalinisababishia upungufu wa nguvu na nishindwe kujihimili.

“Kwanini tajiri ajatoa amri tumuondoe kabisa duniani?”

“Eeh! Angeturuhusu tu.”



Walijadiliana, wakati huo nikichuruzika damu baadhi ya sehemu. Hakika, walinitupia makonde watakavyo. Nami nikashindwa namna ya kujirudishia kwa sababu mmoja wao aliibana mikono yangu na kuniwekea kitu fulani cha ncha kali ambacho endapo nitatingisha tingisha mikono kitanichoma. Dhahiri! Nilikosa ujanja na mbinu za kujitetea. Na kunifanya niwe gunia.



Naam! Wema wangu uliniponza.



Walivyojihakikishia kipigo walichonipatia ni onyo kwangu la kutoweza kujihusisha na shughuli waliyonihadhari nayo wakaondoka. Na kuniacha nikiugulia maumivu, hususani yale ya sindano, ambayo niliamini walikuwa wanatumia kwenye shughuli zao za kujidunga. Sanjari na makonde waliyonitupia sehemu zisizo taka kuguswa guswa kwa nguvu.



Hakika, kitendo hicho kilinipa umivu ambalo kamwe silisahau. Sikuamini, kwamba kile kilichonitokea ni matokeo ya himizo nililojiwekea la kuhakikisha yule aliyefanikisha nuru kichwani mwangu naye anakaa sawa. Namtoa kule, ambako jamii inawapigia kelele siku zote, kwamba wafanyacho hakiendani na maadili.



Muda mchache baada ya kuondoka, takribani dakika nne, Eddy naye akaja. Ujio wake ulikuwa wenye bashasha, ila ulipotea ghafla kutokana na hali aliyonikutana nayo. Chozi halikusita kumdondoka. Kwani alianza kuwa mwingi wa huruma kwangu hivyo hakupenda kuniona nikiwa matatizoni.

“Abdul, nini kimekupata mpendwa?” aliniuliza. Huku akionekana mwenye kuchanganyikiwa kwa kushindwa aanze kufanya kipi.

“Hii ndiyo dunia ya leo,” nilimjibu. Kwa kunukuu kauli ya shangazi.

“Unamaanisha nini?”

“Eddy! Dunia ya leo, malipo ya mema ni ubaya.”

“Bado sijakuelewa. Kwanza hii hali uliyonayo imekupata vipi?”

“Haya ni malipo. Niliyolipwa na yule ambaye…” sikumalizia akanikatisha.

“Jamila kakufanyia haya?”

“Sina hakika. Maana walionifanyia hivi ni vijana wa kiume.”

“Huisi kawatuma?”

“Shangazi alinifundisha nisiishi kwa kisio na hisio.”

“Hapana Abdul. Maumivu yako ni sawa na maumivu yangu. Usiniruhusu niwe na kulilia kwani utanifanya kuwa mdhoofu. Hitajio langu kwako ni nuru itayosisimua ndani ya mwili wangu. Nategemea fariji toka kwako ndiyo maana nimethubutu kuambatana nawe pamoja…” alisema Eddy na kuweka tuo. Takribani sekunde nne, kisha akaendelea.

“…tekeleza hayo nikubadilishe. Nawe uitwe majina mengi ambayo yatakufanya uitwapo uwe na kumbukizi yangu nyuma yako.”

“Unamaanisha nini?” nilimuuliza, huku nikijivuta na kuketi naye kwa ukaribu.

“Tamanio langu, na hitajio kubwa nililonalo. Nahitaji nisimame kama mshirika namba mbili wa mafanikio yako.”

“Hey! Unataka nikuoe? Wewe, kahaba?” nilijikuta namuuliza kwa kuropoka, kiasi kwamba alianza kujisikia aibu hata hamu ya uwepo wake pale kwangu alianza uona mchungu. Nililifahamu hilo kupitia machozi aliyokuwa anadondosha. Yalizidi yale ya mwanzo.



Nilimfanya ajisikie vibaya. Nami nilivyokuja kufikiria kauli niliyoizungumza, nikajuta na kujilaumu kwanini nimeitamka. Ila vilevile ilinipa ufikirio, wa kufikiria alichozungumza Eddy.

“Inawezekana vipi kahaba akaolewa na kuwekwa ndani? Nyumba si haitotulia kwa migogoro kila uchao? Jamii pia itanionaje, mtu mwenye heshima zangu najipeleka kwenye shimo la wakosa heshima,” ilikuwa sehemu ya fikirio langu. Ambalo lilikatishwa na sauti ya Eddy.

“Abdul, kwa heri. Nakutakia uugue salama, na maisha mema pia,” alisema Eddy. Sauti ikitamalaki unyonge wa kutosha. Huku akijitahidi kubana sauti nyingine ya kilio isimtoke.

Akaondoka!

__________



Alhamisi. Yapata saa 4:47 asubuhi. Nilifunga safari hadi nyumbani kwa kina Jamila. Wakati huo mwili wangu ukiwa na maumivu kiasi yatokanayo na kile kipigo. Yaliyopelekea tembea yangu kubadilika na utendaji wa kazi kupungua. Ila sikujalisha. Kwani niliamini hiyo ni kama changamoto nyingine zizuiazo mipango kukwama. Kwamba yule mtu, ambaye moja kwa moja nilijiaminisha kuwa ni Jamila, kawaagiza wale watu ili niache mipango yangu inayomhusu.



Nami nilikuwa na uwezo huo. Ila kilichonifunga ni kiapo nilichojiwekea na kuthamini ule muda ambaye mwenzangu aliutumia kwangu. Hivyo sikuhitaji kuingiza chuki dhidi yake sababu tu, katuma watu waje wanipige. Ushujaa wangu nilijihakikishia upo kwake. Kwa kumtoa kule aliko na kumfanya mwenye kutamanika kwenye jamii yetu.



Purkushani, ndicho kitu pekee kilichonipokea. Nilivyoingia kwenye uga wa nyumba waishio. Niliwakuta watu wakikimbizana huku sehemu kubwa ya miili yao ikiwa tupu. Nilivyowasaili, nikawabaini, kuwa mmoja wao ni Jamila. Akiwa kavaa khanga pekee aliyoifungia juu ya mwanzo wa matiti. Ndani akiwa tupu, na kumfanya pindi akimbiapo aruhusu sehemu kubwa imbebayo kama mtoto wa kike ionekane kutokana na upepo uliokuwa unapeperusha khanga aliyoivaa.



Jamila wake hakuacha kubarizi mazingira yaliyomzunguka. Japo mapaja yalijitahidi kumbana mbana asionekane. Sambamba na askari wafupi wafupi waliotoka kufanyiwa usafi siku chache zilizopita.



Tukio hili likanisahaulisha maumivu na kunifanya nianze kunonoka na umbile la Jamila. Nikawa nameza funda la mate tu, huku nikijisemeza, raha ya huyu mtoto ni kumla kavukavu. Kile nilichokiona kilinifanya nisisimke kwa muda. Tena mwenyewe hakutilia maanani kabisa kama anayaonesha yasiyofaa kuonyeshwa hadharani. Kama kula kwa macho, basi hapa nilikula mpaka nikakinai. Tena nilivyopoteza ustaarabu, macho yangu yaliganda kwa Jamila pekee, yule aliyekuwa anafukuzana naye sikuwa na mpango naye. Ambaye ni mzee Namahala. Naye akawa kavaa pensi na kakamatia shati mkononi, tumbo, na maungo mengine ya juu ya kiuno yakiwa wazi.

“Mmmh!...hawa walikuwa wanafanya…” nilijisemeza, lakini nilishindwa imalizia kauli yangu baada ya kusikia sauti ya ukali toka kwa Jamila kumwendea mzee Namahala ambaye alikuwa anatokomea kwenye vipenyo vya majengo.

“Usirudi. Nenda kayaendeshe maisha yako hukohuko uendako. Na ni lazima, hiki nilichokuanzia nikumalizie. Utanitambua mimi ni nani, mwanahizaya mkubwa wee! Mzee lizima kazi kuharibu watoto wa watu, ama kwa sababu hauna ndiyo maana unadiriki kufanya haya?” ilisikika sauti ya Jamila.



Kauli hii ikaniaminisha kile nilichohisi kipo sahihi. Kwamba walikuwa wanapeana raha zilizofichwa ndani ya miili yetu. Ila! Inawezekanaje baba na mtoto? Hapa kuna walakini.



Baadaye ikanibidi nitoe macho pima kwa Jamila. Wakati huo ndipo nikamuona akijaribu kumsitiri Jamila wake kwa kushikilia ile khanga isipeperuke peperuke. Akawa anatembea kwa kujitingisha tingisha hali iliyosababisha makalio yapoteze ustahimilivu kwangu. Tena sio kwangu tu, hata vidume walioketi mbali wakishuhudia lile tukio walishindwa. Nililithibitisha hilo kupitia miluzi waliyokuwa wanaipiga.



Alivyoingia ndani nami nikaingia. Nikamkuta kaketi sofani sebuleni uso ukiwa umejaa mikunjo ishara ya kukasirika pamoja na jasho tele likimtiririka.

“Pole sana,” nilisema. Huku nikijitupia kuketi sofani, macho yangu yakitua mwilini mwake.

“Nawe umefuata nini?” aliniuliza kwa ukali.

Sikujibu muda huohuo, nilitulia kwa muda takribani sekunde saba kisha nikafungua mdomo wangu kuzungumza.

“Jamila, haya ni maisha. Ukiyatengenezea uhasama, kamwe hautofika sehemu nzuri. Hebu jitathmini, namna ulivyokuwa mrembo, mrembo mwenye kuchanganya akili ya mwanaume yeyote rijali. Jaribu kuwa na huruma, kisha upoe na kunipa nafasi ya kunisikiliza. Yamkini nilichonacho akilini mwangu ni chema, chenye uwezo wa kukusaidia maisha yako ya baadaye,” nilisema kwa utulivu. Macho yangu nikiwa sijayabandua mwilini mwake.

“Abdul. Nawachukieni sana watu wenye jinsia yenu. Hivyo siwezi kukusikiliza, kwa sababu kile utachoniambia hakitonishawishi,” alisema, kidogo akiwa amepunguza munkari.

Nikasita kwa muda, kwa mara nyingine, nikaweka koo safi kwa kujikohoza kisha nikaomba maji ya kunywa ili nililainishe vyema. Maneno nitayoyatamka yatamkike vyema pasipo kizuizi.



Hakusita, aliinuka, akapiga hatua hadi kabatini, akachukua bilauri baadaye akaelekea lilipo jokofu. Akafungua, na kumimina maji yaliyomo kwenye chupa ya lita moja ya kampuni ya maji ya Kilimanjaro. Alivyojihakikishia ujazo aliouweka utanikidhi, alirejea na kunikabidhi. Huku akipiga jicho la wizi kunisaili. Akaenda kuketi alipoketi awali.



Nami sikukawiza. Niliyagugumia yale maji kwa uharaka na kuyamaliza ndani ya sekunde thelethini nikaitua bilauri na kuweka sakafuni.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Nnnnh!...nnnh!...nhnhnhnh!” nilijikohoza kusindikiza masalia ya maji yaende vyema kooni.



Nikajiweka sawa pale nilipoketi baada ya kuhisi kiungo kimoja wapo kuchoka kwa mkao nilioketi. Nilipojihakikishia hisio limemalizika nikaufukuza ukimya.

“Jamila, thamani yako ni kubwa sana. Ndiyo maana leo hii naamua kuwa muwazi kwako. Siwezi kuficha hisia zangu kwa kile ulichofanya kwangu kwani kimenisaidia. Hivyo nami sipaswi kufanya jambo lenye msaada kwako litalokusaidia…” nilisema na kuweka tuo. Nikavuta hisia, na kujawa kumbukizi siku ile nilivyomtembelea shangazi kituo cha polisi. Nikaenda mbali zaidi kwa kukumbuka maongezi baina yangu na yule askari. Hasa hasa nilikumbuka kauli yake ihusuyo huruma. Nikainukuu.

“Jamila, mwenzio nina huruma ya kweli, ndiyo maana nimethubutu kuyavaa matendo yako. Matendo yako yamenifanya nifikie hatua hii. Yameniweka wazi, japo hujadiriki kunitamkia…” sikumalizia kauli yangu, akanikatisha.

“Matendo yapi?” aliuliza.

“Jamila, umeugeuza mwili wako kuwa kitega uchumi. Nikiwa na maana, unajiuza,” nilisema, kana kwamba sifahamu sehemu ndogo ya historia yake.

“Kwa hiyo unatakaje?” aliuliza kwa ukali. “…unataka nawe nikupe? Sema, ni pesa yako tu nakupatia, ila inabidi uwe radhi kwa matokeo utayokutana nayo mwisho wa mchezo,” aliendelea kusema. Huku akiinuka pale alipoketi na kupiga hatua kunifuata nilipo. Taratibu, akiifungua khanga aliyovaa, lengo nishuhudie sehemu maridhawa impayo kiburi kwa wanaume.



Ila sikuruhusu hilo litokee. Chap! Nami nikanyanyuka kumfuata nikiwa na azma nimzuie asiitoe ile khanga. Kwa sababu nilishafahamu kuwa hajavaa kitu chochote ndani. Fahamu hiyo iliniaminisha kwa muono ule wa awali pindi anafukuzana na mzee Namahala. Lakini sikufanikiwa. Nilikwishachelewa. Kwani, hatua mbili tu, toka pale nilipoketi tayari alikwishaifunua na kuruhusu mboni zangu zisaili umbile.









Wakati huo kauli za shangazi zikizunguka kwenye ufahamu wa ubongo wangu. Nikazipambanua moja baada ya nyingine, ile yenye nguvu ihusiyo mazingira niliyopo ikagota. “Wengi wetu, tunavyodiriki kutoa msaada kwa mtu, hutengeneza imani fulani, ambayo hujaza tamanio, msaada utavyokuwa na manufaa kwa yule nimsaidiaye siku za mbeleni nami nitahitaji anisaidie. Hali inayojenga utumwa muda mwingine, ambao kimsingi, hauna umuhimu endapo imani hii haitokuwepo,” Nilikumbuka .



Kumbukizi hiyo ikanifanya nivae ujasiri wa kumkabili mtoto wa kike aliyebarikiwa mvuto umjazao mate mwanaume yeyote amuonaye. Kiasi kwamba akidiriki kuona sehemu ndogo ya nyama zizuiwazo na mavazi yatambulikayo nguo za ndani hatoacha kufanya ushawishi. Wa kumshawishi japo aongeze furaha kwa kupitia fahari yake.



Sikujalisha hali iliyoko, hususani binafsi. Ambayo urijali wangu ulionekana dhahiri shahiri kupitia mwenye mamlaka aliyekuwa anajitutumua kila sekunde iongezekayo.

“Siwezi nikathubutu kuvunja kiapo changu,” nilijisemeza, nikiwa nishamfikia na kutanua mikono yangu lengo niikamate ya kwake niikutanishe tumboni. Kwani kufanya hivyo ningelikuwa nishakamilisha dhamirio langu. Ila sikufanikiwa.



Aliniwahi. Pindi naitanua mikono yangu, ya kwake aliirejesha maeneo ya tumboni na kumfanya nimtengenezee nafasi ya kufanya kitu chochote mbele ya kifua changu. Akanisukumiza. Nikandondoka chini, naye akafuata juu yangu. Akanikalia, huku akiniachia uwanja wake niutazame kwa ukaribu. Ile khanga aliidondosha.



Nikawa na wakati mgumu. Ulionishinikiza nichakarishe akili yangu nichukue uamuzi gani utaoniweka katika mazingira mazuri. Ilifikia hatua, hata ule ujasiri niliojivika kuanza kupotea, taratibu, na akili kuruhusu nichukue uamuzi wa kusafiri ulimwengu wa huba, ili nisije onekana mshamba, kama wadaivyo vijana wa mjini. Upande wa pili wa fikirio nao hukusita kujitokeza. Uliopingana vikali na ule wa mwanzo. Huu ulinihimiza nisifanye kile kilichochukua nafasi kubwa ya kunishawishi. Wakati huo uteute laini wa fahari ya Jamila ukitiririka taratibu na kulowanisha shati nililovaa.

“Endapo utafanikiwa kupata nafasi kwa uchache ya kumshawishi Jamila akueleze sehemu ndogo ya historia ya maisha aliyopitia, itakufaa katika kukamilisha azma uliyojiwekea,” nilikumbuka. Kauli ya shangazi aliyoniambia siku kadhaa zilizopita.

“Hii ndiyo nafasi pekee ya kupata ufahamu wake,” nilijisemeza, huku nikitupa macho pima kusaili sura yake.

Hakika! Jamila ni msichana mrembo.

__________



Pale chini tulikaa zaidi ya dakika sita. Alivyoona sijihangaishi dhidi yake akainuka, nami nikafanya vivyo hivyo. Akaiokota khanga alikoitupia na kuivaa.

“Unaweza ondoka,” alisema Jamila, uso ukiwa na kingi kisirani kilichonihadhari.



Sikupinga. Nilipiga hatua kadhaa hadi mlangoni nikasimama, kisha nikatupa macho nitokeapo nikamuona Jamila hana habari juu yangu. Ina maana alikuwa na dhamirio tosha kwa kile alichokifanya.

“Nishakuambia toka, usinichefue, na usitake nikuharibie maisha yako sasa hivi,” aliendelea kusema. Kauli iliyonihimiza nami niwe na neno kwake.

“Jamila, muda mwingi nikuonapo najawa na furaha, tena furaha isiyo hata na chembe ya huzuni ndani ya moyo wangu. Nakupenda sana, sina budi kukutamkia hivyo japo sina hakika kama ujumbe huu utauelewa vyema. Jaribu kuwa na fikirio pana la ukumbusho, litalokukumbusha kuwa haya ni maisha, na kumchukia mwenzako, sawa na kukataa sadio la madhila yako ya baadaye.

“Jamila, kila nikukumbukapo naishia kutabasamu huku kwa mbali nikilengwa lengwa na machozi. Je, unahitaji kufahamu kipi kinachonipelekea niwe katika hali hiyo? Naamini, laiti ungelikuwa karibu nami kifikra, ungelinijibu. Na jibu lako lingekuwa ndiyo. Ila kwa sasa huwezi kufanya hivyo, kwa sababu uko mbali nami kifikra, sijajua jibu lako litakuwa la namna gani.

“Jamila, machozi yanitokayo, ni machozi ya furaha yenye majuto ndani yake, kwa sababu mwenzangu umeruhusu chuki dhidi yangu pasipo kisa cha msingi. Wewe ni hitajio kubwa kwa jamii, fikra zangu zinaniamisha hivyo, baada ya kutambua uwezo wako wa ufundishaji ulionao. Tena ni mfundishaji mzuri unayepaswa kutoa mafundisho rika zote. Yakufaa ubadilike, na kuondoa roho ya kisasi iliyokutawala. Kwani sihitaji mwisho wangu utawaliwe na malalamiko, na majuto tele kwa sababu yako. Nahitaji mwisho wangu uwe mwisho wa amani, utaonisukuma kuweka kumbukumbu ya kushukuriwa muda wote na vizazi vitavyopata kuwepo wakati huo, ama mwenzangu unahitaji uwe mtu wa aina gani?” nilizungumza kwa ukarimu wa hali ya juu, muda wote Jamila akinitumbulia macho yake na kuonyesha wajihi wa tafakuri kuhusu kile niongeacho.



Nikatulia kwa muda, nikiweka tegemeo la kujibiwa swali langu lakini haikuwa hivyo. Matokeo yake, nilimuona Jamila akitoka mbio kuelekea chumbani kwake huku chozi jembamba likimtiririka. Nikafuata nyuma yake.



Nilipiga hatua hadi chumbani kwake. Nikamkuta kaketi kitandani huku kiwango cha chozi kikiendelea kuongezeka kila alivyoinua kingo ya mdomo wake. Sikujalisha, mazingira aliyonayo. Nikaketi jirani naye na kuanza kumbembeleza baada ya kuhisi maneno yangu yamemgusa vilivyo na kumpatia kumbukizi fulani aliyoshindwa kuivumilia.

“Abdul, naomba uniache, huna uwezo wa kunisaidia matatizo niliyonayo,” alisema Jamila. Kwa sauti iliyojaa kwikwi za kilio.

“Hapana. Ni wajibu wangu kama rafiki, na raia wa taifa moja kukupatia msaada. Niambie kipi kinakusababishia udondoshe chozi ilhali kauli zangu hazikujijenga kwa minajili hiyo?”

“Abdul. Naomba unielewe. Hamna chochote utachofanya, ambacho kwangu kitaonekana ni msaada. Maisha yangu yaliharibika angali nipo mdogo, punde mama alivyobakwa nami nikabakwa pia, na walewale vidume waliomuingilia mama yangu. Hivyo sina budi kujenga chuki kupitia tukio hili, vilevile sina budi kujenga amani ya wangu fuadi kupitia tukio hili pia.

“Baadaye, nikapata sehemu ambayo niliiamini inaweza kuwa yenye fariji upande wangu. Sehemu iliyoniaminisha itanisaidia kuwachukulia hatua wale waliotufanyia ukatili, ila haikuwa hivyo. Ile sehemu ilinibadilisha kuwa mtumwa wa ngono, ukizingatia nilikuwa na unofu wote umtoao mate mwanaume rijali ijapokuwa nilikuwa mdogo kiumri…”

“Sehemu ipi hiyo ilikugeuza mtumwa wa ngono? Mahakamani?” nilimuuliza, hata kabla hajatamatisha kauli yake.

“Heri ingelikuwa mahakamani, wapo ambao wangelinionea huruma.”

“Sasa ilikuaje?”

“Mzee Namahala ndiye aliyenifanyia hivyo. Hakujali umri wangu, akadiriki kunirubuni, mwishowe akaanza jinafasi na mwili wangu. Iliniuma, ila nilikosa sehemu ya kwenda kutoa umivu hili, matokeo yake nikabaki nalo moyoni, siku hadi siku, nililopata utimamu, ikanibidi nithubutu kulipa kisasi dhidi yake, ukizingatia, urubuni alinitumilia ni ule wa lipa nikulipe.”

“Una maanishaje?”

“Pindi anaanza, alinihadaa, nikitaka mambo yaende kwa wepesi, nikubali kufanya aliyonifanyia. Hakika sikupingana naye, ijapokuwa nilikuwa mdogo, lakini sikuwa na jinsi. Isitoshe, kilichonisukuma zaidi sikuwa na uhakika wa maisha, niliamini kwake ni sehemu sahihi kwa imani ya kauli yake ya kwanza mara aliponiona.”

“Alikuambiaje?”

“Njoo uishi nyumbani. Ewe ni mtoto mdogo hupaswi kutanga tanga. Aliniambia hivyo punde nilivyomhadithia kwa uchache yaliyonisibu.”

“Pole sana.”

“Hapana. Huu si wakati wa pole, wakati huo ulishapita, sasa ni wakati wa kumfunda yule mzee kwa sababu alishindwa kutimiza alichoniahidi.”

“Vipi kuhusu wanaume wengine? Uwafanyiao…” nilisema, ila kabla sijahitimisha akadakia.

“Nawapa fundisho, la kutambua umuhimu wa hisia za mapenzi za mwenza wao.”

“Vipi kuhusu wanawake?”

“Wapo wanaume wafanyao kazi kama yangu. Nina hakika, wanatoa fundisho lifananalo na lile nifundishalo.”

“Mmmmh!...makubwa.”

“Heri yawe makubwa. Kwa sababu yatatoa onyo kwa wahusika, wasahaulifu na wale watamaniao.”



Kwa kiasi fulani majibu ya Jamila yaliniongezea ufahamu ndani ya ubongo wangu. Kwamba yote yatendekayo ulimwenguni, hayatendwi kwa nia ovu. Bali mengine, hutendwa kwa nia ya kutoa somo kwa watu washuhudiao. Tena masomo yaletayo mafikirio. Kwa mfano, wizi; mtu aibapo hujenga picha kwa watu wasikiao ama waonao, mtu akiibiwa humpunguzia kasi ya maendeleo aliyothubutu kuyafikia.



Kikapita kimya. Kila mmoja wetu akioneka mwenye tafakuri tele, sijajua kwa mwenzangu alikuwa anafikiria nini? Ila kwa upande wangu nilikuwa nawaza namna ya kumsaidia, awe mtu huru atayeondoka kwenye lindi aliloko ijapokuwa kwa mtazamo wa pili liliniamisha ni sahihi kwa sababu hutoa funzo kwa wasiojihusisha. Na wahusikao pia.



Niliufukuza ukimya huo dakika mbili baadaye, nilipoinua kingo za mdomo wangu na kuruhusu sauti kunitoka, iliyoambatana na kikohozi kwa kiasi kidogo.

“Jamila, hebu jitathmini. Angalia maisha tuliyokuwa tunaishi baina yetu awali hata kama ulikuwa unatumia ulaghai. Juu ya mafundisho yako hukuisha vituko na utani mwingi kwangu. Ila leo hii vyote havipo, badala yake uhasimu umechukua nafasi. Ukosefu wa hivyo vitu, umenifanya nigeuke mwenye majuto makubwa, majuto yanichukuliayo muda mwingi kukukumbuka, kujilaumu na kulia pia inapobidi. Kwa sababu mwenzangu umekataa njia nyoofu kutokana na kuruhusu kisasi kikutawale.

“Kila nifikiriapo kisa kilichopelekea tuwe mbali na kupunguza mawasiliano baina yetu huwa naishiwa nguvu, maana sijajua kama ni sisi wenyewe, ama kuna msukumo mwingine nyuma yetu. Maana tulikuwa tunaenda vizuri sana, hadi kupelekea kuufukua uhusiano uitwao undugu,” nilisema. Jamila akiwa tuli, ananisikiliza. Macho yake kayatupa pima sakafuni, kama aonaye haya kwa kile nimwambiacho.

“Jamila! Unahitaji uwe mtu wa aina gani?...” nilimuuliza na kutulia kwa muda, kumpa nafasi ajibu swali langu. Lakini mwenzangu hukufanya hivyo. Aliendeleza ukimya wake hali iliyonipa nafasi ya kuzidi kumwaga kauli kwake.

“Natamani sana unipatie jibu la swali langu. Japo nafahamu itachukua muda kujibiwa, ila nakuomba, ujitahidi. Kwani hapa nilipo nimejawa na hamu, hamu ya uhitaji wa kufahamu mambo mbalimbali yakuhusuyo, ambayo naamini yana ishara fulani kwenye jamii tuishiyo. Pia,…” nilisema, ila sikumalizia kauli yangu, nikakatishwa na muungurumo wa gari iliyoegeshwa kwa fujo.



Tukio hilo likatuchukulia muda wetu. Kila mmoja akaonekana mwenye tafakuri kuwazia nini kiendeleacho nje. Kabla hatujapata muafaka, tukashtushwa na muungurumo mwingine kwa mara ya pili. Huu wa sasa ulikuwa wa kuvunjwa kwa mlango. Ulipigwa teke, tena teke kali ambalo lilipelekea uharibifu sehemu moja ya bawaba. Iliachia! Kisha sauti nzito zilizojaa ngurumo zikaanza kusikika.

“Humu ndipo anaishi?”

“Ndiyo afande, hata nami makazi yangu yalikuwa humu. Ila siwezi tena kutokana na matendo yake huyu mtoto. Ni mkatili sana, kiasi kwamba juu ya udume wangu wote sina budi kuwa na hofu naye.” Ilisikika sauti ya mzee Namahala, na kutubainishia mzee huyo kaongozana na askari wa jeshi la polisi, wakiwa na lengo la kumkamata Jamila.



Baadaye nikajawa na hisia, pindi wakiendelea kukagua chumba kimoja baada ya kingine kwamba lengo la ujio wao ni kumkamata Jamila juu ya kile nilichokuta kikiendelea. Lakini sauti ya askari yule yule aliyeuliza mwanzo ikaniondoa mwanzo baada ya kumtupia mzee Namahala swali lingine.

“Ilikuaje kuaje hadi akamuua mama yake?” aliuliza. Swali lililonishinikiza kutahamaki na kumtumbulia macho pima Jamila, huku nikivuta taswira ya mke wa mzee Namahala.

“Hee! Kamuua? Kwanini?” nami nilijiuliza kimoyomoyo, wajihi wangu ukijaa unyonge, uliomsukuma Jamila awaze jambo kunihusu.



Kweli! Hazikupita dakika mbili, taratibu nikamuona akinisogelea nilipo. Alivyonifikia, mkono mmoja akakamata shingo yangu kama anataka kunisihi jambo, lakini haikuwa hivyo, kwani, sekunde kadhaa baadaye, nikahisi kitu chenye ncha kali kikipasuka ngozi yangu kuzama ndani. Usawa wa moyo.



Nilivyokuja kushtuka kutokana na maumivu niliyoyapata, na ili nianze kujitetea asiendelee kunifanyia kile alichokianza, nilikwishachelewa; alinisukumiza ukutani, msukumo nilioshindwa kuuhimili nikaangukia ukutani huku kikitangulia kichwa sakafuni. Nikatoa mshindo mkubwa uliowashtua wale askari wakimbilie mule chumbani wakati huo Jamila akijitahidi kufungua dirisha arukie nje.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Dakika moja baadaye, nikashuhudia, kwa uono wa mbali wale askari wakizingira chumbani nilipo. Baadhi yao wakiwa wamekamatia vyema bunduki, aina ya Sub—machine gun (SMG) mikononi mwao.

“Kamata huyo, na wengine fukuzieni yule aliyeruka pale dirishani,” alisema mkuu wao, aongozaye lile kundi lililokuja.



Askari walioamriwa hawakusita, chap! Walitii amri kwa kijigawa. Baadhi yao walinisogelea nilipo wakanifunga bangili za serikali, wengine waliruka pale dirishani kumkimbiza Jamila alikoelekea.





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog