Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

PENZI LA MZOA TAKATAKA - 1

 






IMEANDIKWA NA : ALEXIS WAMILAZO



*********************************************************************************



Simulizi : Penzi La Mzoa Takataka 
Sehemu Ya Kwanza (1)


 Ilikuwa alfajiri saa kumi na moja kengere ya gereza la Segelea ililia kuashiria kuwa tayari kumekucha na ni wasaa wa wafungwa kuamka na kisha kuhesabu namba kabla ya kwenda kulitumikia Taifa kwa nguvu, hivyo wafungwa wote waliokuwemo vyumbami walikurupuka kutoka usingizini haraka sana wakajongea mstarini. Zoezi hilo la kuhesabu namba lilifanyika kwa haraka haraka wakati huo bwana jela akionekana kutembea huku na kule. Lakini wakati wafungwa hao wakien kujihesabu, upende wa pili alionekana mfungwa mmoja aitwae Nyogoso, kijana huyo alikuwa bado yupo amelala na hata asiwe na habari kama wasaa wa kuhesabu namba umewadia.

1...2...3..4..sauti za wafungwa wakihesabu namba zilisonga sikika kwa kupokezana mmoja baada ya mwingine,ghafla muda mchache baadae Askari magereza walistuka baada mfungwa mwenye jezi namba 15 ambayo ndio jezi anayovaa mfungwa Nyogoso. Haraka sana kipyenga cha kuashilia hatari kilipulizwa, kilisikika eneo lote la magereza. Punde si punde Askari karibia wote walijikusanya kumsikiliza mkuu wao anasema nini. Mkuu huyo aitwae Afande Mudy alisema "Mfungwa namba kumi na tano haonekani, nadhani kabla hatujaenda kumtafuta kokote hebu zungukeni vyumbami kwanza, mkimkosa ndipo tutajua tuanzie wapi kumsaka" Alisema hivyo kamanda Mudy. Pasipo kupoteza muda, Askari hao walianza kazi hiyo mara moja, wakiwa na mitutu yao mbavuni walikagua chumba kimoja baada ya kingine na hatimaye mmoja wao alimkuta Nyogoso akiwa peke yake chumbani amelala amejikunyata mithili ya mtu anayehisi baridi kali. Askari huyo aliyemuona Nyogoso amelala alikereka sana, hima alikunjua bakora yake iliyokuwa na kamba nyembamba isiyokatika kisha akamcharaza Nyogoso pale chini alipolala. Mfungwa huyo alistuka, kwa pupa alikurupuka kutoka usingizini muda huo huo akapigwa bakora nyingi mfululizo makalioni na mgongoni, kelele za maumivu huku akiomba msamaha alipasa Nyogoso huku akikimbilia nje hali yakuwa Askari huyo aliyekuwa akimcharaza akiendelea kumsindikiza kwa viboko mfululizo. "Nisamehe afande.. Nisamehe afande.. Mamaa nakufaaa nisamehe afande.." Alisema Nyogoso kwa sauti iliyoambatana na kilio cha maumivu. Lakini mwishowe Askari huyo alimuacha pindi alipojichanganya na wafungwa wenzake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Hey namba kumi na tano, hebu njoo hapa" Afande Mudy alimuita Nyogoso. Mfungwa Nyogoso akiwa na uso wenye huzuni alitoka katika lile kundi la wafungwa kwa unyonge huku machozi yakiendelea kumdondoka, machoni akitia huruma kwa namna nguo zake ziliivyokuwa zimechanwa hovyo hovyo alitii wito.

"Hivi unaweza kuniambia unamtatizo gani?.." Alihoji afande Mudy. Kamanda ambaye uso wake ulikuwa mkavu hata sekunde moja asionyeshe tabasamu. Swali alilouliza afande huyo Nyogoso hakuweza kulijibu zaidi alidondosha tu machozi huku akijaribu kuyafuta kwa kutumia jezi yake ambayo tayari ilikuwa imechanwa chanwa na bakora alizochapwa. Afande Mudy alimshangaa sana mfungwa huyo kisha mwishowe akamwambia.

"Ondoka ila kesho asubuhi mapema nitafute. Sawa sawa?.." Alisema Mudy wakati huo akandika taarifa fulani kwenye kitabu chake kidogo alichokuwa nacho. Muda huo Nyogoso alirejea kujichanganya na wafungwa wenzake kwenye mstari. Wasaa huo ulikuwa wa kupata uji kwa kila mfungwa ndipo waelekee mashambani kufanya kazi.

Nyogoso pamoja na wenzake waliendelea kujisogeza pole pole kwa mgawaji uji,ila ilipofika zamu yake ghafla Afande aliyekuwa kando kidogo ya mgawa uji alimzuia mgawaji asimpe. "Kamanda tunajali muda, lakini pia huyu naye anahaki ya kupata uji kama wenzake" Mgawaji ambaye naye vile ni Afande alisema hivyo kwa msisitizo. Daniel Afande huyo aliyetoa tamko juu ya Nyogoso kutopewa uji alijibu "Mimi nimeshasema usimpe uji namba kumi na tano, zaidi ya hapo sihitaji maswali" Hayo maneno yalimnyong'onyesha sana kamanda huyo aliyepo kwenye kitengo hicho cha kugawa uji, alimuonea huruma Nyogoso kwani alijua kijana huyo anakwenda kufanya kazi ngumu. Alijuliza maswali mengi ambayo hakuyapatia majibu ilihali muda huo huo Nyogoso aliinamisha paji la uso wake chini halafu akamtazama Afande Daniel kisha akatikisa kichwa ishara ya kusikitika wakati yeye Afande Daniel akiachia tabasamu pana huku moyoni akijisemea "Nilikwambia sana achana na msichana Mazoea ila hukutaka kunielewa. Sasa utaonja joto la jiwe pumbafu.." Maneno hayo Daniel alikuwa akijisemea Ndanda ya moyo wake hali ya kuwa Nyogoso baada kunyimwa haki ya kupewa uji kama ilivyokuwa kwa wafungwa wenzake, alimpisha wa nyuma yake kisha yeye akajichanganya na wale wafungwa ambao tayari wamekunywa uji.

Hayo ndio asilimia kubwa ya maisha ya Nyogoso tangu ahukumiwe jela, ni dhahili shahili alichukiwa mno na kamanda huyo aliyefahamika kwa jina Daniel, lakini mfungwa huyo kamwe hakudhubutu kurusha ngumi ama kumtupia matusi kamanda huyo. Aliishi kwa matuaini, siraha pakee aliyotegemea ni nidhamu na heshima gerezani humo.

Dakika arobaini na tano baadae zilikatika, punde kengere ililia. Amri kutoka kwa bwana jela ilitoka kupitia kipasa sauti. Sauti hiyo ilisema kwa msisitizo "Wote vikombe chini, haijalishi umemaliza kunywa uji ama hujamaliza. Afande Daniel, Afande Sure ongozeni kundi kuelekea shambani" Pasipo kupoteza muda makamanda hao walioteuliwa waliwaamuru wafungwa kupanda gari la magereza tayari kwa safari ya kuelekea shambani,muda huo alionekana mfungwa Nyogoso akijikongoja pole pole kulisogelea gari, ghafla alipigwa teke nyuma baada kuonyesha uzembe wa kutembea. Nyogoso akiwa na uso wenye huzuni aligeuka nyuma ili amtazame mtu aliyethubutu kumpiga. Alimuona yule yule mtemi wake wa kila siku, si mwingine Afande Daniel. Daniel akiwa amekunja uso wake alisema "Songa mbele mbwa wewe unamtazama nani?.." Nyogoso alikerwa sana na huo unyanyasaji ila ilimbidi awe mpole kwa sababu alijua dhahili shahili Daniel analindwa na mkono wa dola.

Baada ya masaa mawili gari kubwa mbili zilizokuwa zimejaza wafungwa na moja ndogo ziliwasili katika mashamba ya magereza,hivyo kwa vurugu kubwa wafungwa walitelemka kwenye zile gari huku Afande mmoja akiwa amesimama kando kidogo akitoa vitendea kazi kwenye gari ile ndogo. Dakika kadhaa mbele kila mfungwa alikuwa na kitendea kazi chake. Walifanya kazi pasipo kupumzika, ila mwishowe hali ikawa si shwari kwa mfungwa Nyogoso tumbo lake likaanza kuhisi njaa kwani siku hiyo hakupata kutia chochote mdomoni mwake, na ilipotimia saa nane mchana alipunguza kasi ya kufanya kazi kitendo ambacho kilimpelekea Nyampala (Kilanja) aliyekuwa akiwasimamia kumsogelea na kisha kumwambia "Mbona unategea? Ulijua huku kula kulala?.."

"Hapana sio hivyo brother, ila tu.."

"Ila nini?.. Kilanja alimkatisha Nyogoso, muda huo huo akampiga teke na ngumi huku akimsindikiza kwa matusi mabaya yaliyoweza kumuumiza Nyogoso moyoni mwake. Nyampala huyo hakuishia hapo tu, bali aliendelea kumpiga Nyogoso wakati huo makamanda wakiwa kwa mbali chini ya mti wakipiga zogo mbili tatu na hata wasijue kuwa kuna timbwili limezuka kwa wafungwa wao. Nyogoso aliomba msamaha akiahidi kufanya kazi kwa nguvu zake zote, ila bado Nyampala huyo hakuweza kumuelewa. Kipigo mfululizo alizidi kumtwisha Nyogoso lakini wakati Nyampala huyo alipokuwa akiendelea kumnyanyasa Nyogoso jinsi awezavyo mara ghafla alijitokeza mfungwa mmoja aitwae Bukulu. Mfungwa huyo alioneakana kujazia mwili huku macho yake nayo yakiwa yakionekana kuwa mekundu.

"Hey basi inatosha, sio vizuri kuwaonea wanyonge Bro wakati wababe unawaona" Aliongea Bukulu kwa sauti ya kujiamini kabisa. Nyampala aliposikia sauti hiyo aliachana na Nyogoso akageuka kumtazama Bukulu kisha akasema "Wewe unaongea hivyo kama nani?.."

"Mimi naongea kama Bukulu karibu kama unayaweza" Alijibu Bukulu. Punde wawili hao wakaanza kupigana, kila mmoja alionyesha umahili wa kurusha na kukwepa ngumi lakini mwishowe makamanda waliingilia kati kabla miamba hiyo haijatandabaisha nani mbabe.

Baada ugomvi huo kuamuliwa, punde si punde filimbi ililia kuashilia kuwa ni muda wa kupumzika. Na hiyo ndio ikawa nafasi ya wafungwa kwa wafungwa kukaa vikundi na kisha kuzungumza kuhusu maisha yao mbali mbali..ila hali hiyo ikawa tofauti kabisa kwa mfungwa Nyogoso, yeye alijitenga peke yake. Bukulu alipomuona alijisogeza kwake akaanza kwa kumsabahi "Habari yako ndugu" Muda huo Nyogoso alikuwa amejiinamia, mawazo yake yalikuwa yakiwaza mbali sana, kwahiyo mara baada kusikia sauti ya Bukulu alistuka akamtazama akaachia tabasamu kisha akamutikia salamu yake. "Safi tu.."

"Naona umejitenga swahiba, unaonekana ni mtu mwenye mawazo sana. Usiweze sana swahiba huu ni moja wa mtihani kwako cha msingi muombe Mungu sababu yeye hufanya njia pasipo na njia..hofu ondoa kabisa moyoni mwako, mimi nitamnyoosha mtu yoyote atakaye jitokeza kukunyapaa. " Bukulu alisema akimuasa Nyogoso ambaye muda mfupi uliopita alikuwa amejiinamia. Maneno hayo yalimfanya Nyogoso kuachia tabasamu kisha akajibu" Shukrani sana ndugu yangu Bukulu. Sasa natambua nini maana ya dunia tambala bovu,penzi limeniponza na pesa imepoteza haki yangu na ndio maana kuna wakati nafikiria kosa nililofanya hapo awali kwa sababu laiti kama ningeyasikiliza maneno ya mama leo mimi nisingeonekana mahali hapa.. "

" Kwanini unasema hivyo Swahiba? Ni kipi hasa ulichomkosea mama yako?. Vile vile unaweza kunisimulia japo kwa ufupi mkasa uliokupelekea kufungwa?.. " Alishusha pumzi ndefu Nyogoso mara baada kuyasikia maswali hayo ya Bukulu, machozi yalimtoka ila mwishowe aliyafuta kisha akaanza kumsimulia..



http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nyogoso alianza kwa kusema

"Bukulu, jina langu mimi naitwa Nyogoso Masumbuko. Ni mtoto pekee kwa mama na baba yangu mzazi. Tulizaliwa watoto tisa, mimi ni mtoto wa pili kutoka mwisho kati ya watoto hao tisa, lakini katika makuzi mimi pekee ndeye niliyopo wenzangu walishafariki kwa nyakati tofauti tofauti. Nimepitia mengi sana mpaka leo hii wanaona mahala hapa natumikia kifungo .. Ilikuwa hivi."

****

Asubuhi angavu kabisa, mvua ndogo ikinyesha iliyoambatana na ukungu mwingi kiasi kwamba mtu akiwa mbele yako hatua saba usingeliweza kumuona vizuri. Kwa mbali kabisa alionekana mama Nyogoso akiwa na mkongojo wake ilihali akiwa amejifunika kitenge ambacho alinunuliwa na marehemu mume wake manamo mwaka 1971 alivyotoka kwenye mkataba wake wa kukata mkonge (karani) Kinguruwila mkoani Morogoro. Mzee Masumbuko aliona zawadi pekee inayomfaa mkewe ni kitenge na si vinginevyo. Mama Nyogoso ambaye tayari umri ulikuwa umtaladadi alijongea kuelekea kwenye nyumba ya kijana wake wakuitwa Nyogoso kisha akagonga mlango, mlango ambao ulikuwa umetengenezwa kwa matete.

"Nyogoso.. Nyogoso mboni yangu" Alipasa sauti kikongwe huyo, naye Nyogoso baada kusikia sauti mama yake haraka sana alisukuma blanket yake kwa miguu akasimama kando ya kitanda chake cha kamba kilicho tengenezwa kwa nguzo nne fupi, punde akatungua bukta yake iliyojaaa viraka kila upande akavaa kisha akausogelea mlango akafungua wakati huo akijiuliza ni kitu gani kilichomfanya mama yake kumdamkia asubuhi ya mapema

"Karibu mama" Nyogoso kwa heshima na taadhima alimkaribisha mama yake ndani huku akimuwekea kigoda sawa. Kikongwe huyo alikikalia kigoda hicho pole pole huku akilalama kiuno na mgongo kuuma ila mwishowe aliketi kisha akamuuliza mwanaye "Umekaje?.."

"Nimeaka salama mama Shkamoo"

"Malakhabaa mwanangu!.." Aliitika mama Nyogoso kisha akakohoa kidogo, baada kumaliza akasema "Nyogoso mwanangu, mguu huu uliotoka si sawa na uliosimama sehemu moja. Pia naomba utambue maisha ya kizazi hiki chinu nyinyi na maisha ya zamani kizazi chetu tofauti kabisa my mwanangu. Siku hizi binadam hawapendani hata kidogo, hali ya kuwa hapo zamani mtu ulikuwa anahakikisha jirani yako halali njaa kama umejaliwa chakula, lakini dunia ya sasa si ajabu kumkuta mtu anakula huku mtoto wa jirani anamtazama tu wala asimkaribishe... Kwahiyo nakuomba mwanangu, jicho langu, furaha yangu wewe ndio pekee niliyebaki nawe kati ya watoto tisa niliowazaa. Nyogoso wewe ndio furaha yangu pekee niliyobaki nayo hivyo chunga usije ukaipoteza" Alisema mama Nyogoso kwa hisia kali huku machozi yakimtoka ingawa aliyastili kwa kujifuta kutumia kitambaa chake alichojifunga kichwani. Hapo alikaa kimya kidogo kisha muda mchache baadae alivunja ukimya akaendelea kumuhisia kijana wake duniani namna ilivyo. Maneno hayo mama Nyogoso aliyaongea pindi baada kusikia kuwa kijana wake anampango wa kusafiri kuelekea Jijini Dar es salam kutafuta maisha. Ni habari ambayo ilimstua kikongwe huyo, na ndio maana siku hiyo aliamua kusema naye kisha ahakikishe kama habari hiyo inaukweli ndani yake.

"Sasa basi naomba unithibitishie wewe mwenyewe mwanangu kwa kinywa chako. Je, ni kweli unataka kwenda Dar es salaam?.." Mama Nyogoso alimuuliza mwanaye huku kwikwi ikiwa tayari imempanda. Wakati huo Nyogoso aliposikia swali hilo la mama yake aliinamisha uso wake chini akitafakari jibu la kumpa mama yake lakini mwishowe aliinua paji la uso wake kisha akajibu huku akiogopa akionekana kuwa na wasi wasi.

"Eeeh..ndi..o..ndi..ndioooo mama. Ni kweli safari ipo, nimeona bora nikajaribu maisha mjini nione kama nitafanikiwa kwa sababu hapa kijijini sioni dalili yoyote ya mimi kabadilika kimaisha. Umri huu hata baiskeli sina? Tazama baba tangu mzee afariki mpaka leo hii bado nyumba ya matope juu imeezekwa nyasi, wakati yule mtoto wa mzee Swedi. Yendese aliondoka hapa kijijini akakaa huko Dar es salaam miezi michache tu amerudi amejenga nyumba ya kisasa, amenuna baiskeli. Mimi kama mtoto wa kiume mwenye uchu na maendeleo nimeumizwa sana na mafanikio ya Yendese, mwanakijiji gani asiyemjua Yendese kwa uvivu wake? Lakini cha ajabu katoka amerudi na mambo ya maana. Kwahiyo mama acha na mimi nikajaribu bahati yangu huko mjini" Aliongea kwa kirefu Nyogoso wakati huo mama yake akiwa ametulia kimya huku mikono yake ikiwa shavuni, Baada Nyogoso kukomea hapo,mama yake aliongeza kusema "Kweli kabisa mwanangu unathubutu kuniacha peke yangu? Najua kama unauchu wa maendeleo na ni jambo la heri kwako na kwangu pia, lakini geuka upende wa pili tazama sasa mimi ni kikongwe, Sina uwezo wa kulima istoshe nasumbuliwa na maradhi ya mara kwa mara. Je, utakapo ondoka nitabaki naishi maisha gani?.. "Nyogoso chonde chonde mwanangu usinifanye nijutie zao langu mwanangu" Maneno hayo mama Nyogoso aliyaongea huku akiangua kilio mbele ya mwanae, ajabu Nyogoso hakujali thamani ya chozi la mama yake zaidi alisisitiza kwa kusema "Mama iwe isiwe lazima niende Dar es salaam kutafuta maisha,hapa kijijini wachawi wengi bwana" Alisema hivyo Nyogoso kwa jeuri saa hali ya juu huku akidiliki kurusha mkono wake mfano wa mtu aliyedharau jambo au kitendo fulani.

Kikongwe mama Nyogoso alipoona mwanae kamwe hataki kumuelewa hima alijikusanya kisha akasimama, akamtazama mwanae mara mbili mbili kisha akaondoka zake na mkongojo wake huku akisema "Safari njema faraja yangu ila ipo siku utanikumbuka tu.." Alipokwisha kusema hayo mama Nyogoso aliishia zake akimuacha mwanae ndani akikusanya baadhi ya nguo ili aende mtoni kufua kwa niaba ya maandalizi ya safari ya kwenda Dar es salam. Nyogoso alidhamilia kweli kweli. Usiku ulipoingia kijana huyo alienda kula chakula kwa mama yake kama ilivyo ada. Alipomaliza kula alikumbushia uwepo wa safari yake kisha akamuaga mama yake, lakini kabla hajapiga hatua kuondoka, mama yake alisema "Hebu subiri kidogo.." Hima Kikongwe huyo alizama chumbani kwake punde akatoka na kikapu cha zamani sana alichotunzwa na marehemu mama yake, bibi wa Nyogoso pindi alipokuwa anaolewa na Masumbuko baba yake Nyogoso.. Ndani ya kikapu hicho mama Nyogoso alimuwekea mwanae viazi vitano vilivyo chemshwa pia na balauli mbili za karanga zilizo kaangwa halafu akamkabidhi kijana wake. "Haya chakula hiki kitakusaidia huko mbele ya safari, mimi nakutakia safari njema ingawa kunikuta hai majaliwa yake Mungu" Alisema mama Nyogoso kwa sauti ya upole iliyojaa huzuni ndani yake huku macho yake yakilengwa na machozi, moyo wake ukiwa umefura maumivu makali sana. Nyogoso aliondoka zake, na kabla hajalala alichukuwa barua aliyopewa na Yendese, barua ambayo ilielekeza mahali anapopatikana pindi Nyogoso atakapo ingia Jijini Dar es salam. Nyogoso alipoisoma barua hiyo mara mbili mbili alijikuta akiachia tabasamu pana kisha akaikunja akaiweka kwenye mfuko wa suruali maalumu ambayo aliianda kuivaa kesho siku ya safari. Usiku wa siku hiyo usingizi ulikuwa mgumu kuja, alijigalagaza huku na kule wakati huo mawazo yake yote yakiifikiria safari ya Dar es salaam,alijaribu kuunganisha picha mbali mbali ndani ya kichwa chake kipi atakifanya pindi maisha yatakapo mnyookea.. Usuku ulikuwa mrefu kwa Nyogoso aliona kama hapapambazuki lakini baada ya kuwaza kwa muda mrefu, mwishowe usingizi ulimpitia. Akiwa katika usingizi mzuri wenye furaha kwake, kuna ndoto mbaya aliota. Aliota kuwa baada Kufika Dar es salaam rafiki yake tegemezi kijana Yendese alimtaka wajiunge pamoja katika kazi ya kupora suala mbalo lilikuwa gumu upande wake "Yendese hii ndio kazi uliyoniita huku?.." Kwa hamaki kubwa Nyogoso alimuhoji Yendese. Yendese aliangua kicheko kisha akajibu "Nisikilize we boya, mimi sijasoma wala nini! Mchana nasukuma mkokoteni, usiku ni kuiba. Kwahiyo siwezi kubagua kazi. Kuwa msaka tonge ili utusue maisha na sio kukaa kibwebwege hapa mjini, kama hutaki shauri yako baki na hamsini zako Ebo". Maneno hayo Yendese aliyaongea akiwa amekunja uso. Punde si punde akajitokeza mtu wa pili aliyeonekana kujazia mwili wake. Mtu huyo akaongezea kusema "Kwanza umeshajua kazi yetu, dhahili shahili utaenda kututangaza kwahiyo hapa ulipo lazima ufe ili usije kuvuruga mipango yetu". Mtu huyo alipokwisha kusema hivyo alichomoa panga. Nyogoso alistuka akaogopa wakati huo huo mtu huyo alinyanyua panga juu kisha akamkata Nyogoso kichwani "Mama nakufaaa.." Nyogoso alipasa mayowe, akakurupuka kitandani akajikuta kuwa ni ndoto aliyokuwa akiota, muda Hu Jogoo aliwika kuashiria kuwa tayari kumekucha na niwasaa wa yeye kuanza safari sasa..



http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Pumzi ndefu alishusha Nyogoso mara baada kusikia sauti ya Jogoo aliyewika kuashilia kuwa tayari kumekucha, hofu na woga ulimjaa pindi alipoitafakari ndoto aliyoota lakini mwisho wa yote aliamini kuwa hiyo ni ndoto na sio lazima ndoto ikawa na maana hiyo hiyo. Haraka sana alijifunua blanket yake kisha akawasha kibatali, mwanga hafifu wa kuloboi ulijaa chumbani mwake, punde akapanga nguo zake kwenye mfuko wa shangazi kaja dhahili alijua muda wa kuianza safari umewadia.

Mara baada maandalizi kuwa sawa, kwa mara nyingine tena alikwenda kumuaga mama yake. Mama Nyogoso kwa shingo upande alimtakia mwanae safari njema ingawa moyoni mwake akiwa hajalidhia. Ndani ya basi la Mohamed Trans Nyogoso alipanda, safari ikawa imeanzia hapo. Safari sio kifo, salama salimini basi hilo lilitinga ndani ya stendi ya Ubungo mnamo saa kumi na mbili jioni. Abiria walishuka kunako basi hilo, wenye wanyeji wao walipokelewa kwa bashasha ya hali ya juu ilihali wale wasio na wenyeji nao wakionekana kuambaa kuelekea mahali lilipo geti la kutokea ndani. Kijana Nyogoso aliachia tabasamu pana baada kujiaminisha kuwa tayari yupo katika Jiji la Dar es salaam huku muonekano wake ukidhihilisha kuwa ni mgeni wa jiji, mshamba kupindukia. Mfuko wake wa nguo na kapu lake lenye viazi na karanga viliaminisha kuwa kijana huyo katoka kijijini.. Kijiji cha mbali kabisa ambacho huwenda hata mtandao wa simu kuupata mpaka ukwee juu kwenye mti. Macho ya kijana huyo muda wote yalikuwa yakitazama huku na kule, taa zilizokuwa zikiwaka zilimfurahisha sana na kujikuta kila mara akiachia tabasamu lakini mwishowe aliingiza mkono kwenye mfuko wa suruali yake, akatoa barua ile aliyopewa na rafiki yake aitwae Yendese. Kwa umakini Nyogoso alisoma maelezo yaliyoandikwa kwenye karatasi hiyo kisha akatoka nje akaelekea mahali palikuwa na jopo la abiria waliokuwa wamelala kungoja gari za mapema ziendazo mikoani. Hapo ndipo Nyogoso naye akawa amejichanganya na abiria hao kwa dhumuni la kulala ili kesho pakipambazuka aanze safari ya kuelekea mahali anapoishi Yendese. Alilala usingizi mzito Nyogoso yote shauri ya uchovu wa safari ndefu ya kutoka Mbeya mpaka Dar es salaam, aliamka asubuhi ambapo alistuka baada kutoliona kapu lake lenye vyakula. Alistaajabu huku akiupeleka mkono wake mfukoni, napo haukuwa na pesa wala ile karatasi iliyokuwa ikimuongoza. Nyogoso alipagawa, aliwaza ni namna gani ataweza kumpata rafiki yake Yendese ndani ya jiji la Dar es salaam ikiwa karatasi ambayo ingeliweza kumuongoza imeibiwa na wahuni. Machozi yalimlenga lenga na mwishowe yalianza kumtiririka mashavuni, kwa upole mfano wa twiga alithubutu kumuuliza kila abiria aliyekuwepo hapo stendi. "Samahani umenionea kikapu Changu?."

"Hapana sijamuona mtu aliyekuibia" Ndivyo Nyogoso alivyojibiwa kwa kila aliyemuuliza ambapo mwishowe alikata tamaa, aliamua kupotezea ingawa mapigo ya moyo wake yalikuwa yakimuenda mbio akihofia maisha magumu ambayo yatamtokea siku za usoni baada ramani yake kuibiwa vibaka waliomvizia akiwa amelala fo fo fo hajitambui. Hivyo pindi alipokuwa hana hili wala lile, asijue pa kuanzia wala pakuishia ghafla utumbo wake ulilindima kuashiria kuwa njaa tayari inajongea ikiwa mfukoni hakuwa na hata shilingi mia ya kununulia kitumbua. Akionekana kuwa wasi wasi juu ya mstakibali wa maisha yake alitoka eneo hilo la stendi akaingia mtaani kutafuta chakula chochote kile hatakama kilicho tupwa jalalani. Mungu siku zote hamtupi mja wake, hatimaye alipata kuona mkate kando kidogo ya dimbwi la maji mchafu. Tabasamu bashasha lilimjia kwenye paji la uso wake, aliamini kuwa tayari amepata tiba ya njaa...jambo ambalo lilimfanya akazane mwendo kuufuata mkate huo lakini kabla hajaikaribia ghafla alitokea Mwendawazimu, aliuchukua mkate huo na kisha kuishia kwenye moja ya uchochoro. Hicho kitendo kilimkera sana Nyogoso, aliaani sana huku hasira zikiwa zimetawala moyoni mwake, alimeza mate mfululizo ilihali akiangalia kwa hasira uchochoro ule alioishia yule Mwendawazimu aliyechukuwa mkate aliokuwa akiufuata ili apoze njaa kali aliyokuwa nayo. Lakini licha ya kuukosa mkate huo, kamwe hakuweza kukata tamaa. Akiwa na mfuko wake shangazi kaja wenye nguo zake aliambaa mtaa kwa mtaa, lakini mpaka jioni inaingia hajaambulia chochote.

"Eeh Mungu wangu nisaidie mja wako" Alijisemea maneno hayo Nyogoso akianza kwa kushusha pumzi ndefu. Muda huo alikuwa amelala chali kwenye valanda la duka saa ya usiku. Na kipindi alipokuwa katika hali ya mawazo ya hapa na pale, ghafla alionekana kijana mmoja ambaye kimuonekano alikuwa amechakaa mwili mzima huku akitokwa harufu ya jasho ilihali mbavuni mwake akiwa na box. Nyogoso alipomuona aliogopa sana lakini kijana huyo alimtoa hofu akamwambia "Usiniogope mimi ni mtu mwema brother" Baada kuyasikia maneno ya huyo kijana, alituliza munkali kisha zogo mbili tatu zikafuatia huku Nyogoso akionekana kudadisi sana Jiji la Dar es salaam namna maisha ya watu wanavyoishi.

"Unamuda gani ndani ya jiji hili?.." Kijana huyo alimuuliza Nyogoso.

"Kaka yangu yani ndio kwanza leo nimekanyaga hapa mjini, kwa kutumia ramani niliyopewa na rafiki yangu lakini bahati mbaya ilipotea katika mazingira pamoja na fedha nilizokuwa nazo. Kwahiyo hapa nilipo sielewi mwisho wangu.." Alijibu Nyogoso, maneno ambayo aliongea kwa sauti ya upole iliyojaa huzuni ndani yake.

" Laah! Pole sana bro,simulizi ya maisha yako na yangu hazijapishana sana ingawa mimi jamaa niliyemtegemea alizima simu baada kumtaarifu kwamba nimefika stendi Ubungo. Kwahiyo nikawa sina namna ya kuishi mjini hapa, ufinyu wa Elimu yangu ukanipelekea kujikita katika kazi ya kuokota makopo na kisha kwenda kuyauza. Kiukweli bro sio kwamba hii kazi niliipenda lahasha bali shida ndio iliyonifanya nijikite kwenye kazi hii ili walau nipate fedha japo ya kujikimu.. " Jamaa huyo aliyeonekana kuchakaa sana alimwambia hivyo Nyogoso huku akijifuta machozi. Nyogoso alimtuliza kwa kumpa pole na mwishowe akasema." Huu nao pia ni mtihani, hivyo naomba na mimi niungane nawe kwenye kazi yako ya kuokota makopo ndugu.. "

" Kazi ya kuokota makopo?.. Hapana heri ufanye kazi ya kuzoa takakata majumbani mwa watu kuliko kufanya kazi hii. Kazi hii haina chochote, hebu jaribu upande huo tuone mafanikio yake"





"Lakini pia kazi hii inahitaji uzoefu wa hali ya juu ambao moja wapo ni kuizoea mitaa ya kuzulula wakati wa kutafuta makopo ili usipotee" Kijana muokota makopo aliendelea kumshauri Nyogoso. Naye baada kusikia ushauri huo alikaa kimya kidogo kisha akasema "Sawa nitajitahidi kaka maana sina namna"

"Pole sana kijana, ukisikia Dar es salaam ndio hii. Piga moyo konde nina imani utaweza tu. Jina langu naitwa Jaluo mzaliwa wa Bunda mkoani Mara sijui mwenzangu unaitwa nani?.."

"Jina langu Nyogoso..Nimetokea Baliadi" Alijibu Nyogoso, wawili hao wakapata kufahamiana,punde mazungumzo mengine mbali mbali yakafuatia lakini mwishowe Jaluo kijana huyo muokota makopo alinyanyuka akaelekea dukani kununua maandazi na maji ya kandolo akampa Nyogoso ili apoze njaa aliyokuwa nayo. "Poza njaa uliyonayo bro kwa chakula hiki, haya ndio maisha yetu sisi wasaka tonge" Alisema Jaluo huku akimkabidhi Nyogoso maandazi na maji. Nyogoso alishukuru sana, akasema "Shukrani sana, maana umeniokoa" Alipokwisha kusema hivyo akaanza kula andazi moja baada ya jingine, kwa muda wa dakika mbili alimaliza maandazi yote sita aliyopewa. Jaluo ndani ya moyo wake akajisemea "Kweli mshikaji alikuwa na njaa kali" Muda huo huo Nyogoso naye akaishusha pumzi yake ndefu kisha akajisemea "Ama kweli Mungu hamtupi mja wake, laiti nisingeangukia mikononi mwa huyu bwana sidhani kama mpaka muda huu ningekuwa hai".

"Mungu akubariki sana bro.." Alisema Nyogoso akimshukuru Jaluo. Jaluo aliachia tabasamu halafu akajibu "Tupo pamoja,nafikiri huu ni wakati wa kupumzika". Wawili hao wakawa wamelala. Punde Jaluo akapitiwa na usingizi hali ya kuwa upande wa Nyogoso bado usingizi kwake ulikuwa kizungumkuti, hakuzoea kulala nje kitendo ambacho kilimpelekea kukosa lepe la usingizi. Lakini pia mbali na hilo, bado suala la kufanya kazi ya kuzoa takakata ilimfanya awaze sana. Mwisho wa mawazo hayo yaliyokuwa yakizunguka kichwani mwake,usingizi ukampitia akawa amesinzia.

Kesho yake asubuhi,Jaluo ndiye alikuwa wa kwanza kuamka. Tayari kumekucha na hivyo alihitaji kuelekea katika mizunguko yake ya kila siku lakini akaona sio vema kuondoka pasipo kumuaga Nyogoso. Hapo Nyogoso akaingiwa na wazo la ghafla, alimuomba Jaluo atembee naye kwenye mizunguko yake ili apate kuifahamu mitaa kadhaa, pindi atakapo anza kazi ya kuzoa takakata asipate tabu wakati wa kurudi nyumbani. Jaluo alimkubalia Nyogoso lakini kabla hawajaanza safari Jaluo akamuuliza "Je, utaweza kutembea kutwa nzima bila kupumzika?.."http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Bila kupumzika?.." Nyogoso alijiuliza mwenyewe ndani ya nafsi yake. Hilo ni zoezi zaidi ya mazoezi kutembea kutwa pasipo kupumzika ila kwa kuwa mtaka cha uvunguni sharti ainame, ilimbidi akubali ili aweze kupata ramani ya kurejea maskani kwao. "Ndio niko vizuri" Alijibu Nyogoso huku akiwa na wingi wa tabasamu hali ya kuwa moyoni akiwa na hofu dhofu lihali. "Uko vizuri? Yani unamaanisha kuwa unaweza kutembea kutwa pasipo kupumzika? Sio!.." Jaluo alihoji tena akionekana kutolielewa jibu la Nyogoso.

"Ndio namaanisha hivyo.." Alisisitiza Nyogoso. Jaluo baada kusikia vizuri jibu hilo alichukuwa gunia lake la kuwekea makopo kisha safari ikaanza. Vijana hao walizungukua huku na kule kutafuta makopo. Walianzia Magomeni walikwenda mpaka Kawe bila kupumzika zaidi ya kunywa maji ya shilingi mia kila mmoja. Nyogoso alijitahidi kuazana ingawa tayari alikuwa amechoka, njaa nayo iliukabili vema utumbo wake. Njaa hiyo ilichangia kuchoka zaidi kumlegeza ila hakuwa na budi kupiga moyo konde ingawa alijuta kwanini amekubali kutoka na Jaluo ambaye yeye kwa upande wake hakuonyesha dalili ya kuchoka. Aliona jua linachelewa kuzama, lakini kabla wakati akiwa kwenye hali hiyo ghafla kando yake aliona kitumbua chini, haraka sana akachuchumaa ili akiokote ili apoze njaa aliyokuwa nayo. Ila kabla hajakitia mdomoni mwake, Jaluo akamkanya kisha akamwambia "Nyogoso mtu wangu, hili ni jiji kijana. Chunga sana usijishushe thamani yako kisa huna kitu. Mimi ni muokota makopo naonekana kichaa mbele ya kadamnasi ilihali nina akili zangu timamu. Lakini licha ya kutazamwa kwa jicho hilo kamwe huwezi kunikuta naokota chakula kilicho tupwa, kwa sababu huwezi kujua huyo aliyekitupa anamaana gani! Na ndio maana asilimia kubwa ya sisi vijana tunao jihusisha na kazi hii na wale wazoa takataka wengi wao wameathirika kiakili, yote hayo husababishwa na kula kula hovyo vyakula vilivyo tupwa. Kwahiyo naomba tupa hicho kitumbua " Nyogoso kabla hajakitupa kitumbua hicho, akakitazama mara mbili mbili, mate yalimdondoka ila hakuwa na budi kukubaliana na takwa la mwenyeji wake. Safari iliendelea,japo kwa msoto lakini Nyogoso alivumilia mpaka pale mzigo ulipoenea wakapeleka kuuza kisha wakarejea maskani huku Nyogoso akiwa hoi bin'tabaani. Walinunua chakula kwa mama ntilie, na sasa wakalala ili kukusanya nguvu ya kesho. Ila kabla hawajasinzia Nyogoso alimwambia Jaluo kuwa kesho ataanza kibarua chake cha kuzoa takataka. Jaluo aliachia tabasamu kidogo kisha akasema "Safi sana bro. Haya maisha tu huwezi jua mwisho wako ni upi. Mjini kila mmoja huja na nyota yake, si ajabu ukafanikiwa mpaka ukashangaza ulimwengu"

"Ahahahah Hahaha.." Alicheka Nyogoso. Punde akaongeza kusema "Ni kweli yote hiyo ni mpango ya Mungu. Lakini pia mimi na wewe ni ndugu sasa, kwahiyo ukikwama nitakusaidia, na mimi nikikwama utanisaidia pia!?au vipi?.."

"Ndivyo ilivyo" Alijibu Jaluo huku akimpa tano Nyogoso, kisha wakalala.

Kesho yake asubuhi, Nyogoso alianza kazi rasmi ya kuzoa takataka majumbani. Alizunguka mtaa kwa mtaa huku mbavuni akiwa na gunia lake ambalo muda huo halikuwa na kitu. Siku hiyo ilikuwa siku ya njema kwake, alifanikiwa kupata takataka nyingi majumbani kana kwamba gunia lake lilionekana ndogo sana. Alibeba mzigo huo kwa dhumuni la kwenda kuzimwaga jalalani kisha arudi kuchukua takataka nyingine,lakini akajikuta akipata tabu baada kutofahamu mahali lilipo jalala. Akiwa na mzigo begani, Nyogoso alitembea huku na kule. Maji machafu yaliyokuwa yakitoa harufu mbaya yalichuruzika kwenye mwili wake hali ambayo ilipelekea kunuka mwili mzima. Alipoona kalikosa jalala hali ya kuwa mzigo tayari umemchosha, hatimaye aliamua kuubwaga mzigo huo kwenye uchochoro mdogo kabisa uliyopo kwenye moja ya mitaa Magomeni. Lakini wakati anafany tukio hilo, vijana wajiitao wajanja wa mjini. Vijana wasio pungua watano wakamfuata Nyogoso,wakamshambulia matusi kisha wakamtushwa mzigo wake wa takataka na mara moja wakaanza kumtembeza mtaa kwa mtaa huku wakimpiga bila hata lepe la huruma.

"Kumbe nyie ndio mnaotubwagia takataka, sasa subir tukukomeshe ili ukawaambie na mateja wenzako" Alisikika akisema hivyo moja ya vijana hao waliokuwa wakimuadhibu Nyogoso. Nyogoso alilia kilio cha mtu mzima wakati huo huo kijana mwingine akaongeza kusema "Unaambiwa weka jiji safi halafu wewe wakuja unatupa takataka hovyo! Ngoja tukuonyeshe sasa"

"Naombeni mnisamehe sitorudia tena, nipo chini ya miguu yenu ndugu zangu" Alijibu Nyogoso kwa sauti iliyoambatana na kilio. Ila vijana hao kamwe hawakujali msamaha wa Nyogoso,bado walimpiga na kumtukania mama yake. Alitia huruma, wala hakuna hata mtu aliyejitokeza kuwakemea vijana hao waliokuwa wakimtendea unyama huo. Baada kupigwa huku akitembezwa na mzigo mzito begani, hatimaye aliishiwa nguvu, akaanguka kando kidogo ya barabara itakayo Kawe kwenda Mbagala. Umati wa watu ulikusanyika kutazma tukio hilo, napo bado hakuna aliyejitokeza kumtetea Nyogoso. Bado aliendelea kupigwa bila huruma, damu ilimtoka kwa wingi mwilini wakati huo akilazimishwa kuanyanyuka ili aendelee na safari ilihali akisindikizwa kwa kipigo. Lakini pindi tukio hilo lilipokuwa liliendelea, hatua kadhaa kutoka mahali ulipokuwa umati huo wa watu inaonekana gari aina ya Hulux. Punde ndani ya gari hiyo anashuka msicahana mrembo mwenye kuvutia machoni pawatu. Anaitwa Mazoea, binti pekee kwa wazazi wake matajiri. Mazoea akiizungusha funguo ya gari kwenye kidole chake, akatembea mwendo wa madaha kuelekea kwenye umati ule wa watu waliokuwa wakimtazama Nyogoso akipigwa.

"Mungu wangu.." Mazoea akajikuta akitamaka maneno hayo kwa kushtuka baada kuona jinsi mtu anavyopigwa kama mnyama poli. Huruma ikamjia binti huyo,akapasa sauti kuwataka vijana hao wamuache Nyogoso.

"Sio vizur, acheni. Kuweni na roho ya huruma jamani" Alisema Mazoea. Ila kamwe sauti hiyo haikuweza kuwashawishi hao vijana kusitisha zoezi lao. Na hapo ndipo Mazoea alipouliza "Ni sababu gani inayowafanya mumuadhibu huyu mkaka kiasi hiki?.."

"Kauli mbiu ya hapa jijini,usitupe takataka hivyo. Huyu mjinga tumemkuta ameutupa mzigo wake wa takataka kwenye uchochoro. Tumeamua kumuadhibu sababu hana uwezo wa kulipa faini" Alijibu moja ya hao vijana waliokuwa wakimpiga Nyogoso.

"Kwahiyo hilo ndio tatizo!?." Akarudi kuhoji Mazoea, muda ho watu wakimtazama mara mbili mbili namna binti huyo alivyoumbika.

"Ndio maana yake, lazima ashike adabu take" Mazoea aliposika jibu hilo akamtazama Nyogoso pasipo kupepesa macho ilihali Nyogoso yeye akijifuta damu zilizokuwa zikimtoka kichwani alipoumizwa. Pumzi ndefu alishusha binti huyo kisha akawauliza hao vijana.

"Sawa ni kosa. Je, niwape kiasi gani ili mumuache aende zake?.." Vijana hao waliposikia swali hilo wakatazamana kisha wakaangua vicheko. Mmoja akasema "Huna pesa ya kutupatia wewe wakati gari yeyewe umehongwa na bwana wako". Maneno hayo ya dharau yalipenya vema masikioni mwa Mazoea, yalimchefua sana ambapo kwa hasira alifungua pochi yake akatoa kiasi cha fedha shilingi laki tatu akawapa halafu akasema "OK faini yake hii hapa, na nyingine itawasaidia. Muacheni tafadhali" Walistaajabu sana vijana hao baada kuona kiasi cha pesa alichotoa Mazoea. Ni pesa nyingi mno ambayo hawakutegemea. Kwa haibu mmoja wao alipokea kisha wakaondoka vichwa chini. Punde anaonekana Mazoea anachuchumaa akamtazama Nyogoso wakati huo akisikitika. Pumzi ndefu akashusha kisha akasema "Pole sana kaka, yakupasa kutii utaratibu wa mji. Lakini wasamehe bure sababu hawajui walitendalo" Maneno hayo ya Mazoea yalimpelekea Nyogoso kuitikia kwa kichwa huku akiendelea kujifuta damu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Pia chukua hii fedha kajitibie majeraha uliyo yapata" Akaongeza kusema Mazoea ilihali akimpatia Nyogoso pesa tasilimu. Nyogoso akastaajabu,akasita kupokea ila mwishowe akaipokea pesa hiyo kisha akajiuliza ndani ya nafsi yake kwanini binti huyo kawa mwepesi kumsaidia kiasi hicho? Lakini wakati Nyogoso anajiuliza swali hilo, upande wa pili mrembo Mazoea akaingia ndani ya gari akaondoka huku akijishangaa moyo wake kustuka mara alipomuona mzoa takataka Nyogoso.. Na hata usiku ilipo ingia Mazoea akajikuta akikosa lepe la usingizi,muda wote akawa anamfikiria mzoa takataka huyo ambaye kimuonekano amejaazia kifua,mrefu pia umbile lake likionekana kuwa kubwa kiasi chake. Ni muonekano ambao ulimvutia sana Mazoea hali ambayo ilimpelekea kumfikiria mara kwa mara huku tabasamu bashasha likitawala kinywani mwake.



ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog