Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

MY CLASSMATE - 1




IMEANDIKWA NA : HALFANI SUDY



*********************************************************************************



Simulizi : My Classmate

Sehemu Ya Kwanza (1)



Ilikuwa jumatatu tulivu.Siku iliyoanza kwa rasharasha za manyunyu ya mvua na radi kidogo katika Jiji la Arusha.



Kutokana na manyunyu yale ya mvua yaliongeza ubaridi mkali uliyofanya watu wengi kuyakumbuka makoti yao na kuyatia mwilini.



Mimi ilikuwa siku ya furaha sana kwangu.Siku ambayo Nilikuwa natimiza ndoto kubwa sana katika maisha yangu.Nilichaguliwa kujiunga na chuo cha Udaktari wa binadamu jijini Arusha.Na leo ndio Ilikuwa siku ya kuripoti pale chuoni.



Nilikuwa na furaha sana.Hata ile hali ya baridi haikunichukiza kabisa.Sikuwa naihisi kabisa.Mawazo yangu yote yalikuwa juu ya kutimiza ndoto hii kubwa sana katika maisha yangu.



Wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza tuliitwa katika ukumbi wa Chuo kwa ajiri ya usajiri.



Tulikuwa wanafunzi wengi sana.Wake kwa waume.Toka mikoa mbali mbali Tanzania Na Kuja jikoni Arusha kuisaka elimu.



Baada ya maelezo ya awali ya utambulisho,pale ukumbini,sasa ulifika muda wa kupanga foleni ili usajiri uanze.



Kila mtu alikuwa anagombea nafasi ya kukaa mbele ili angalau asisote sana kwenye foleni.Ilikuwa ni fujo hasa!



Mimi nilikaa kwenye kiti cha plastiki nikiangalia vurugu zile.Sikuwa na shaka nilijua maadamu nimechaguliwa nitasajiriwa tu.Baada ya fujo kutulia nami nilienda kujiunga kwenye foleni.Nilikuwa mtu wa mwisho katika foleni ile ya usajiri.



Nilikaa kwenye foleni huku nikiwaza safari yangu ya kielimu ilipotokea.Niliwaza jinsi nilivyosoma kwa shida shule ya Sekondari Bagamoyo.Wazazi wangu hawakuwa na uwezo wa kunisomesha.Hivyo nilipata shida sana kupata mtu mwenye moyo wa kunisomesha.Ilibidi mchana nisome jioni nifanye biashara ndogondogo ya kuuza karanga ili niweze kupata hela ya mahitaji madogomadogo ya shule.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Baba alikuwa mvuvi .Lakini pesa akizopata zilitosha kulisha familia tu.Hii ilitokana na kuwa na familia kubwa ya watoto kumi na mbili.Mama hakuwa na kazi zaidi ya kuchuuza mitaani samaki wa baba.Inamaana Baba na mama walikuwa wanafanya biashara moja.Baba anavua samaki,tena kwa zana dhaifu za uvuvi na mama anawauza kwa kuwatembeza barabarani.



Katika watoto wote kumi na mbili wa baba na mama.Mimi pekee ndio nilikuwa nasoma shule.Wengine wote hawakutaka hata kusikia neno shule.Hawakuona umuhimu wa kusoma.Waliona kaka yao nikivyoteseka kwa ajiri ya kusoma.Wote walikuwa wanashinda pwani wakijitafutia ridhiki.Hata hivyo hawakuwa wanapata vya kutosha.



Pamoja na shida zote hizo nilikumbuka nikivyojitahidi darasani ili nifanikiwe na kuisaidia familia yangu iliyotopea katika dimbwi la umaskini.



Ukweli nilikuwa nafanya vizuri sana shuleni.Siku zote nilikuwa naamini elimu ndio mkombozi wangu.Elimu ndio silaha pekee ya kuishika kwa maskini kama mimi.



Mungu hamtupi mja wake ! Nilifanikiwa kufaulu na kutakiwa kujiunga na masomo ya kidato cha sita.Pamoja na kuijua thamani ya elimu lakini hapo ndipo nilipoitambua thamani ya pesa.Kumbe pesa na elimu vilikuwa vinaenda sambamba.Sikuwa na pesa kabisa ya kwenda kusoma shule ya Sekondari Ndanda ambayo ndio nilichaguliwa kwenda kusoma.



Kwanza nauli kutoka Bagamoyo hadi Mtwara Ilikuwa mtihani.Hapo hujahesabia ada pamoja na vitu vingine vya shule.Ndoto yangu ya kusoma ilikomea hapo.Nilihisi siwezi tena kuendelea na kusoma .Hata wazazi wangu walinambia hivyo!



Baba Alikuwa na jukumu zito la kuhakikisha familia inakula.Mimi nilikuwa na akiba ya shilingi elfu kumi iliyotokana na biashara zangu za karanga.Kumbuka mimi ndiye nilikuwa mkubwa katika familia hii.Nilikuwa na ndugu kumi na moja nyuma,wote wakiniangalia mimi.



Lakini sikukata tamaa.Niliamini kukata tamaa ni dhambi kubwa sana katika maisha.Niliyakumbuka maneno ya mwalimu wangu wa Kiswahili wakati nasoma pale Bagamoyo sekondari "Usikate tamaa ukiwa bado unaishi" Ndio...sikukata tamaa.Niliapa lazima nisome kwa njia yoyote ile.



Nilikuwa najiona mwenye wajibu wa baadae kuwasaidia wazazi wangu.Kusaidia ndugu zangu.



"Lazima nisome !"



nilihisi nasema taratibu maneno hayo.Haikuwa hivyo yalisikiwa na mtu aliyopo mbele yangu katika foleni ya usajiri.



"unaonekana una mawazo sana kaka" Sauti nyororo ya dada aliyopo mbele yangu ilipenya kwenye masikio yangu.

"Hapana"

"Mbona unaongea peke yako sasa ?"

Sikujibu.

"Naitwa Mayasa"

"Naitwa Abdul"

"Tunaweza kuonana baadae sehemu tofauti na hapa"

"Bila shaka"

Tulibadirishana namba zetu za simu !





Zoezi la usajiri lilichukuwa saa tano.Hatimaye na mimi nikasajiriwa kama mwanafunzi wa udaktari katika chuo cha udaktari Arusha.



Kuwa daktari ilikuwa ndoto yangu ya siku nyingi sana.Nilikuwa najua masomo ya msingi ili uwe daktari.Nilikazana sana katika masomo hayo.Nilijitahidi sana katika somo la hesabu.Nilijitahidi sana katika somo la fizikia na Nilijitahidi pia katika somo la baiolojia.



Nakumbuka nilipata A katika masomo hayo matatu pale Bagamoyo Sekondari.Nilikuwa napenda niwe daktari ili nije kusaidia wananchi maskini wanaoteseka kwa kukosa hela za matibabu.



Siku zote nilikuwa najisemea mwenyewe. "Mimi ndiye daktari pekee nitakayekuwa mkombozi kwa maskini wote wanaoteseka kwa maradhi mbali mbali kwa kukosa pesa za matibabu"



Baada ya usajiri nikaenda hostel kupumzika.Nilikuwa nakaa hosteli za mule mule chuoni.Nilikaa kitandani huku nikikumbuka misukosuko ya safari yangu ya elimu.



Nilikumbuka nilivyoteseka kipindi kile natafuta hela ya ada pamoja na ya matumizi ili niende kusoma Ndanda Sekondari.



Nilienda kuomba selikalini lakini hawakunielewa.Nilienda kuomba kwa Mbunge nae hakunielewa.Sikupata hela ya ada,sikupata hela ya nauli.Bado nilikuwa na elfu kumi ndani chini ya mto wangu.



Ilikuwa bado wiki moja ili shule ifunguliwe.Na mimi nikaanze kidato cha tano.Sasa ndoto yangu ilikuwa inaanza kuyeyuka.Sikuwa na njia ya mkato ya kunipeleka shule.



"Hairuhusiwi kukata tamaa katika maisha ukiwa bado unaishi" Kauli ya mwalimu wangu ilijirudia katika kichwa changu.



"Sasa kwanini mimi naruhusu kukata tamaa.Nikiwa bado naishi.Tena na afya tele.Haiwezekani!Lazima niende Mtwara nikasome "



Usiku wa siku ile nilipata wazo.Wazo ambalo lilipewa baraka na kichwa changu.Ndio !

Niliamua kwenda Mtwara kwa miguu.Nilikuwa nimeamua hivyo.Usiku ule ule niliweka vitu vyangu sawa.Asubuhi nikawaambia wazazi.



"Baba na mama mimi leo naenda shule"

"Umepata ada mwanangu ?" Mama aliniuliza kwa sauti yake ya upole.

" Hapana"

"Sasa utaenda vipi shule?"Baba aliniuliza nae.

" kwa miguu"

"Miguu?"

"Ndio wazazi wangu.Lazima niende Mtwara kusoma.Na nimeamua kwenda Mtwara kwa miguu!" Nilisema nikiwa na uhakika tele.

"Hivi Abdul unakujua Mtwara?"l

"Sikujui lakini nitafika"

"Ni mbali sana Mtwara,huwezi kwenda kwa miguu Abdul!" Mama alinambia kwa sauti yake ya upole.

"Nimeshafunga kila kitu changu.Ilibaki kuwaaga nyinyi na ndugu zangu. Nakubali Mtwara ni mbali. Lakini bila elimu safari yetu ya kuelekea kwenye mafanikio inazidi kuwa mbali.Bora niumie kwa kutembea kwa miguu kuisaka elimu.Kuliko kuumia kwa umaskini huu uliotukuka.Umaskini umeweka kambi nyumbani kwetu.Na kitu pekee kinachoweza kuufukuza umaskini huu kipo Mtwara.Lazima niende Mtwara"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sawa utaenda Mtwara kwa miguu.Je hela ya ada utaitoa wapi?" Baba alinitupia swali zito.

Nilifikiria kidogo nikajibu.

"Nitajua huko huko.Lakini lazima nifike Mtwara kwanza.Mambo mengine yatajijibu huko huko."

Wazazi wangu hawakuwa na jinsi.Waliniruhusu niende Mtwara.

Mama Alikuwa analia machozi kwa kunionea huruma.Baba alikuwa ananihurumia pia.Mimi nilikuwa jasiri na imara katika msimamo wangu.Nilidhamiria kwenda kusoma kwa njia yoyote ile!



Baba aliwaita ndugu zangu wote.Akawaambia juu ya safari yangu ya kwenda shuleni Mtwara tena kwa miguu.



Ndugu zangu wote walisikitika sana.Kila mmoja aliingia ndani Na kutoa akiba aliyojiwekea na kunipa.



Nilianza safari yangu ya kutoka Bagamoyo kwenda Mtwara nikiwa na elfu ishirini.Familia mzima niliiacha kwenye majonzi makuu.Sikujari.Sikusikitika.Nilidhamiria kwenda kusoma.Nilidhamiria hasa kwenda Mtwara kwa miguu.



Nikiwa katikati ya mawazo simu yangu iliita.Nikaangalia kwenye kioo cha simu yangu,alikuwa Mayasa!

Niliipokea na kuanza kumsikiliza..!





Kwa Abdul Ramadhani.Mungu akulaze mahali pema peponi.Amean.

***********************



"Hallo"

"Mambo Abdul"

"Safi Mayasa, nambie"

"Nipo tu,nilikuwa na ombi moja Abdul"

"Nakusikiliza"

"Naomba tuwe wote kwa ajiri chakula cha usiku leo"

"Haina shida,wapi?"

"Tukutane Tengeru hotel saa mbili usiku"

"Sawa Mayasa"

Simu ikakatwa.



Aliponambia habari ya chakula cha usiku.Nilikumbuka kitu.Nilimkumbuka Raiya.Mwanamke niliyesoma nae shule ya Msingi kule Bagamoyo na kuja kukutana nae kama bahati mbaya jijini Dar es salaam.



Nilikutana nae kama bahati mbaya siku ile natoka Bagamoyo kuelekea Mtwara kwa miguu.Siku ile nilitembea kweli kwa miguu kutoka Bagamoyo hadi Dar es salaam.Nilipofika Mwenge ndipo nilikutana na Raiya akiwa anauza duka la simu pale Mwenge stendi.Ni yeye ndiye aliyeniona na kuniita.



"Mambo Abdul"

"Safi Raiya za Siku?"

"Nzuri,vipi mbona na begi unaenda wapi?"

"Mtwara"

"Mtwara utapata gari sahivi.Saa saba hii Abdul ?"

"Naenda kwa miguu"

"Miguu ?!!!"

"Ndiyo Raiya"



Nilimsimulia kila kitu Raiya kuhusu maisha yangu.Nilivyofika mwisho niliukuta uso wake hautamaniki.Umelowa kwa machozi.Alinionea huruma na kuahidi kunisaidia.



"Ngoja nikupe hela hii ukapumzike Hotelini.Halafu kesho nitakusafirisha Mtwara.Na pesa ya ada nitakupa mimi"

"Ahsante sana Raiya yaani sijui nikushukuru vipi dada yangu."

"Jioni nikifunga hapa nitakupigia simu tukapate chakula cha usiku"

"Sina simu Raiya'

Alitoa simu moja mpya dukani na kunikabidhi.Kwa siku ile nilimuona Mungu mtu Raiya.Nilimshukuru sana.



Nilienda kutafuta chumba cha kupumzika.Diva hoteli lilikuwa jibu langu.Nikaingia ndani na kukaa kitandani.Nikaitoa ile simu niliyopewa na Raiya na kuichaji.



Diva hotel ilikuwa hoteli nzuri ya kisasa yenye gharama nafuu iliyokuwa Kijitonyama.Ilikuwa na kila kitu ndani.Kwa mimi Ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kulala kwenye hoteli kubwa kama ile.Siku ile ilikuwa ni moja ya siku niliyokuwa na furaha sana.Ndoto yangu ya kusoma ilikuwa inaenda kutimia.Tena inatimizwa na mtu ambaye sikutegemea kabisa.Kweli usimdharau mtu yeyote duniani.Ingawa mimi na Raiya hatukuwa marafiki kipindi tunasoma lakini tulikuwa tunaheshimiana sana.Heshima ile bila shaka ilimpa moyo Raiya wa kunisaidia leo hii.



Saa moja kamili tulikutana na Raiya pale Diva hoteli.Kulikuwa na mgahawa mzuri wa kisasa mbele ya hotel ile. Tulikaa na kupata chakula cha usiku.



Wakati tunakula tuliongea mambo mengi sana na Raiya.Alinisimulia mambo mengi sana kuhusu maisha yake.Kumbe kwa sasa Raiya alikuwa mke wa mtu.Alinisimulia mateso anayoyapata toka kwa mumewe.Mumewe alikuwa mtu wa kisirani na mwingi wa wanawake. Pia hakuwa anampa vizuri haki yake ya ndoa .



Mimi nilibaki nimeduwaa.Kumbe unaweza kumuona mtu anaendesha Prado mjini.Ukamuonea gere.Kumbe ndani ya moyo wake anabubujikwa na machozi mazito huku anaendesha Prado.



" Sasa Abdul mimi nitakupa hela"

"Nitashukuru sana yaani dada yangu"

"Lakini kwa sharti moja"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Nipo tayari kufuata sharti lolote Raiya"

"Kweli ?"

"Kweli nakwambia"

"Nitakupa shilingi laki tano leo.Na nitakuwa nakutumia matumizi kila utakapohitaji.Lakini naomba twende chumbani ukaniridhishe Abdul.Ukaupe nafuu moyo wangu.Ukanipe vile nilivyovikosa tangu niolewe na mume wangu."

Na tutakuwa tunafanya hivyo kila nitakapokuwa nahitaji !

Nilihemewa sana..!





Nilipigwa na butwaa.Kwanza sikutegemea kupata msaada mkubwa kama ule kutoka kwa Raiya.Ulikuwa msaada mkubwa uliokuja wakati nikiouhitaji sana.Kwangu mimi laki tano Ilikuwa ni zaidi ya msaada.



Tatizo lilikuja katika sharti lake.Raiya alikuwa anataka kufanya mapenzi na mimi.Lilikuwa sharti gumu sana kwangu. Pesa nilikuwa nazitaka sana lakini kufanya mapenzi Na Raiya tena mke wa mtu nilikuwa sitaki kabisa !



"Umenielewa Abdul ?.

" Nimekuelewa Raiya,lakini wewe mke wa mtu"

"Kwahiyo"

"Utakuwa humtendei haki mumeo"

"Hizi laki tano ninazotaka kukupa wewe nimemuibia yeye.Je kumuibia hela zake ni kumtendea haki ?" Raiya aliongea huku akinionesha burungutu kubwa la pesa.

"Kama hutaki pesa nenda kwa miguu Mtwara"



Nilikuwa katika wakati mgumu sana wa kufanya maamuzi katika maisha yangu.Nilijikuta nikikubari kufanya mapenzi na Raiya siyo kwa kumpenda ila kwa kupenda kusoma.Niliamua kuutumia mwili wangu kwa manufaa ya maisha yangu ya baadae.Tulivunja amri ya sita ndani ya Diva hoteli !



Nilistuka na kuangalia saa yangu.Nikakumbuka nilikuwa na ahadi na Mayasa saa mbili usiku Tengeru.Na sasa Ilikuwa saa moja kamili.Nilijiandaa kwa ajiri ya kwenda kutekeleza ahadi hiyo.Nilioga.Nikavaa suruali yangu nzuri ya jeans pamoja na T-shirt nyeupe.Chini nilivaa raba nyeupe.Nilijupulizia pafyumu nilikuwa nanukia vizuri sana.Nikaenda Tengeru hoteli.



Nilifika hotelini saa mbili na dakika mbili.Nilimkuta Mayasa ameshawasiri.Mayasa alinilaki kwa furaha kubwa sana.

Tulikaa na Mayasa tukiongea mambo mbalimbali hadi saa nne usiku. Ndipo Mayasa alipotaka kujua sababu ya mimi kuwa na mawazo na kuongea peke yangu.



"Abdul"

"Naam"

"Kwanini unaonekana mtu mwenye mawazo sana ?"

"Niko sawa Mayasa"

"Hauko sawa Abdul,unafikia hatua ya kuongea peke yako Abdul "

"Kweli nina matatizo Mayasa, ila tutafute sehemu iliyotulia nitakueleza.Wewe ushakuwa rafiki yangu sasa sina budi kukwambia"

"Nitafurahi sana,sehemu gani unadhani itakuwa nzuri kwako"

"Popote patakapokuwa pametulia zaidi ya hapa"

"Sawa kesho jioni nitakupigia.Tutaenda Moshi.Kule kuna bustani moja nzuri sana kwa maongezi"

"Sawa Mayasa"

Tulikodi teksi pale Tengeru liyoturudisha hadi Arusha mjini.Aliniacha hosteli za Chuo,na yeye kuelekea kwao.



Kesho yake tulienda Moshi na Mayasa.Paradise garden ndipo aliponipeleka.Ilikuwa sehemu tulivu.Yenye maua mazuri na majani machache yaliyopandwa kwa ustadi mkubwa.Kulikuwa na meza zilizokaa mbali mbali.

Tulichagua meza moja .Tulikaa na Mayasa na nilianza kumsimulia historia ya maisha yangu.



Nilimsimulia Mayasa historia yangu kuanzia Bagamoyo .Magumu yote niliyopitia katika kusoma.Nilimsimulia jinsi nilivyokutana na Raiya.Na mkataba wa ngono nilioingia na Raiya.



Sasa Nilikuwa mtumwa wa Raiya.Kumpa penzi Raiya kila atakapojisikia,naye kunihudumia katika matatizo yangu yote.



"Ukweli sikuwa nampenda Raiya .Sikuwa napenda mkataba ule wa ngono.Niliuchukia sana.Lakini sikuwa na jinsi Mayasa Nilikuwa napenda kusoma.Ilibidi nifanye akivyotaka Raiya.

Naamini Raiya nae hakuwa ananipenda.Alinipenda mimi kwa ajili ya ngono tu .Alinifanya sex toy .Nilimaliza kidato cha sita kwa kusomeshwa na Raiya chini ya mkataba wa ngono.



Matokeo ya kidato cha sita yalipotoka nilifaulu vizuri .A ya baiolojia B ya fizikia na B ya Hesabu.Nilichaguliwa kuja kusomea udaktari. Katika Chuo cha udaktari hapa Arusha.Ambapo ndipo jana nilikutana na wewe."



"Daah pole sana Abdul.Hakika umepitia makuu.Umekuwa mtumwa wa mapenzi. Sasa una Mpango gani Abdul?"



"Natamani kujitoa katika utumwa huo.Lakini sina jinsi Mayasa.Elimu yangu inamtegemea Raiya.Maisha yangu yanamtegemea Raiya.Nitakapomaliza Chuo na kupata kazi hapo ndipo nitakuwa nimejivua utumwa..utumwa wa mapenzi kama ulivyouita".

" Nataka nikusaidie Abdul bila sharti lolote .Dhamira yangu ya ndani nimeamua kukusaidia.Nimependa harakati zako za kuitafuta elimu.Unaonesha unapenda kusoma,na una akili sana."

"Nilimshukuru sana Mayasa.Nilimwona ni mwanamke mwenye moyo wa ajabu sana.Tuliagana huku akikodi gari iliyoturejesha Arusha mjini.



Sasa nilihamia himaya mpya.Himaya ya Mayasa nilimkabidhi Kila kitu kuhusu maisha yangu kasoro moyo tu.Nilipunguza mawasiliano na Raiya na kuongeza mawasiliano na Mayasa.



Ilikuwa siku ya jumatano jioni.Nilikuwa na Mayasa tunajisomea darasani.Simu yangu ikaita.Alikuwa Raiya.



" Wewe unajifanya kiburi.Mimi nimekusomesha umefika Chuo unajifanya mjanja.Sasa kesho nakuja huko huko Arusha nione kinachokuzuzua.Ole wako nisikie una mwanamke.Ole wako"Bila salamu Raiya aliwaka kwenye simu.

Sikumjibu.Nilikata simu na kuizima kabisa.

Hamu ya kusoma iliniisha.Mayasa alisikia kila kitu alichosema Raiya.Raiya alikuwa ananikaripia kama Mtoto na kwa nguvu.Halafu Mimi na Mayasa tulikuwa karibu sana.Alinionea sana huruma.Hamu ya kusoma iliniisha.Nilimuaga Mayasa na kurudi hosteli.



Nilifika kitandani na kulala chali.Nilifikiria mustahabari wa maisha yangu.Nilijiona ni mtu mwenye mikosi.



Sikuwa naamini kama Raiya anaweza Kuja .Nilijua ni mkwara.

Niliulaumu umaskini wangu.Niliulaumu umaskini wa wazazi wangu.Machozi yalitoka yenyewe taratibu.



Nikauhisi mkono laini ukinifuta machozi.Nilifumbua macho yangu na kumwangalia.Alikuwa Mayasa..!



"Acha kulia Abdul.Nimejitoa kukusaidia kwa lolote kaka yangu.Naamini tutaushinda mtihani huu.Tutamshinda Raiya.Sitokubali ulie tena."

Mayasa alinibembeleza sana siku ile.Mwishowe nikamwelewa.Nikanyamaza.



Ilipita wiki moja tangu Raiya anipe vitisho vyake.Hakutokea Arusha wala hakunipigia simu.Nikajua labda amekata tamaa.Nikawa naishi maisha yangu kama kawaida.Furaha ikanirejea.Huku nikimtegemea Mayasa kwa kila kitu.Naye hakuchoka.Alinisaidia.



Upande wa darasani nilikuwa nafanya vizuri sana katika masomo.Nilikuwa na uwelewa mkubwa sana.Mayasa hakuwa mzuri sana darasani.Nilijitahidi kumsaidia kila nilipopata nafasi.Nilielewana sana na Mayasa.Sasa tukawa tunaitana Mate tukifupisha neno la kizungu classmate likiwa na maana mtu unayesoma nae darasa moja.Tulifatana muda wote. Tulijisomea pamoja.Tulikuwa mithili ya chanda na pete.



Kila mwishoni mwa wiki tulikuwa tunatoka nje ya jiji la Arusha kutembea na Mayasa.Nakumbuka jumamosi moja ilitukuta Same na Mayasa.Sasa tulikuwa marafiki tulioshibana.Nilikuwa najua mengi juu ya Mayasa.



Kumbe baba yake Mayasa alikuwa balozi Ally Hamisi.Makamu wa raisi wa Zanzibar.Baba yake alikuwa mtu mkubwa sana Serikalini lakini hakuna hata siku moja aliyenitamkia mdomoni mwake.Nilisikia tu kutoka kwa watu wa pembeni.



Nakumbuka siku ile tulirudi chuoni saa kumi na mbili jioni kutoka Same.Same Ilikuwa mbali kidogo na Jiji la Arusha.Mayasa alinirudisha kwanza mimi hosteli ili na yeye arudi kwao.Tulienda Same na gari lake siku ile.



Nilipofika karibu na chumba changu nje nilikutana na Justus.Kijana tuliokuwa tunakaa chumba kimoja pale hosteli.Na alikuwa rafiki yangu pia.



"Daah afadhali umerudi Abdul kuna mgeni wako ndani"

"Nani?"

"Simfahamu,ila amefika zamani sana"

"Sawa kaka"



Tuliingia ndani na Mayasa.Tukiwa hatuna wasiwasi hata kidogo.Tulipofungua mlango na kuingia ndani tulimwona msichana amelala kitandani kwangu.Nilistuka sana!

Nilipomwangalia kwa makini,alikuwa Raiya! Nilistuka zaidi sasa!



"Naitwa Raiya Mohamedi"Aliongea huku akimwangalia Mayasa.

"Naitwa Mayasa Ally"Mayasa nae alijibu kwa kujiamini.

"Wewe ndiye unajifanya unajua kutembea na wanaume wa watu ?"

"Sema kilichokuleta"

"Kilichonileta ndio hiki ninachoongea"

"Usione vyaelea dada......"

"Sina muda wa kuongea na wewe"

"Abdul?"

Sikuitika

"Umenisaliti kwa sababu ya hiki kikaragosi.

Nilikaa kimya namwangalia.

" Kumbuka nilipokutoa Abdul,Kumbuka Siku ile pale Mwenge,ningekuacha ungekutana na hiki kikaragosi leo ? "

Raiya aliongea maneno yaliyoniingia kidogo .

Pamoja na madhaifu yake kadhaa lakini Raiya alikuwa na mchango mkubwa sana katika maisha yangu hadi nilipofikia sasa.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sasa chagua moja Abdul.Utakuwa na mimi au huyu?"Raiya alishusha jazba sasa,alikuwa anaongea kwa upole.

Nilibaki njia panda.Raiya na Mayasa wote walikuwa na mchango mkubwa katika maisha yangu.Na wote wananiangalia mimi kusubiri jibu langu.



" Mayasa siyo mpenzi wangu"Nilijua nimetamka kwa sauti kumbe sauti haikutoka nje.Mdomo ulikuwa unatetemeka tu.



"Chagua Abdul"

"Achague nini,mimi Abdul siyo mpenzi wangu"

"Ni nani yako sasa?"

"Rafiki yangu tu"

"Hahaha siku zote mapenzi yanaanzia kwenye urafiki,

OK marafiki.Basi mimi ni mke wa Abdul. Nasema naomba muvuunje kabisa huo urafiki wenu. Siutaki siutaki,siutaki hata kuusikia.Mkewe nimesema !"

"Raiya wewe ni mke wa Abdul?"

"Hilo jibu uliza swali"

"Una hakika Raiya ?"

"Ndio"

"Na Salehe je,unamwitaje Raiya ?"



Swali hilo allouliza Mayasa lili mstua sana Raiya !







Swali hilo alilouliza Mayasa lilimstua sana Raiya..!

Hali sasa ilibadirika mule ndani !



"Mimi ni Mayasa Ally Hamisi,unanikumbuka?



Mumeo Salehe ni kaka yangu.Mtoto wa mama mdogo Fatma.Au nimpigie Salehe nimuulize kama kakuacha"?

Mayasa aliongea huku akitafuta namba za Salehe katika simu yake.



Raiya sasa alikuwa amechoka hoi.Hajui lipi aseme,lipi aache.Alikosa kauli kabisa.Ghafla alitoka nje ya hostel kwa ghadhabu mithili ya roketi, bila ya kuaga !



Niligundua kitu kimoja kuhusu Mayasa.Mayasa alikuwa msichana msiri sana.Alinificha cheo cha baba yake hadi sasa.



Pia kumbe alikuwa ananificha kama Raiya ni wifi yake, hakunambia kabla.Nilianza kumwangalia Mayasa kwa jicho la kumuogopa sasa.



" Usijari Mate.Raiya ni wifi yangu lakini yeye hakuwa ananijua.Tulionana na Raiya siku moja tu.Tena siku ya harusi yake na kaka Salehe.Hata wewe ulivyonisimulia historia ya maisha yako.Ulipotaja jina la Raiya sikujua kama Raiya wifi yangu,sikufikiria kabisa.

Leo nilivyomwona hapa ndio nimemkumbuka".

Mayasa alinijibu kitu ambacho nilikuwa nakifikiria.

"Sawa mate nimekuelewa"



Tulitoka nje na kumwangalia Raiya ameenda wapi?Hatukumuona.Hatukujua ameelekea wapi?Aliyeyuka mithili ya upepo !

Baadae Mayasa aliniaga na kuondoka kwao huku mimi nikibaki na wingi wa mawazo.



Nilisinzia nikiwa na mawazo yangu.Lakini kutokana na uchovu wa kutoka Same na ukijumlisha mawazo aliyoniletea Raiya ndio yalinichosha kabisa,nililala fofofo.



Saa kumi usiku simu yangu ilitoa mlio wa sauti nilioutega Kwa ajiri ya mwitikio wa ujumbe mfupi .Ikimaanisha kuna meseji mpya iliingia.



'Umeuchokoza moto.Niliacha zamani ukatili.Wewe unajitahidi kunirudisha huko. Nilikuwa katili sana zamani.Kama hupendi nirudie tabia zangu za zamani nakuomba achana na kikaragosi.Nitakuuwa, nitamuuwa pia !.Nakupa siku tatu za kufikiria juu ya suala hili.Mimi bado nipo Arusha.Namaanisha!"



Nilikaa kitandani na kuurudia kuusoma ujumbe ule Mara tano.Jasho lilikuwa linanitiririka kama maji.Nikamtumia ule ujumbe na Mayasa.Hakunijibu !Hajanijibu mpaka leo !



Asubuhi na mapema walikuja watu wanne nisiowafahamu.Walikuwa wamefuatana na kiongozi wa hosteli,Mshauri wa wanafunzi,na Raisi wa Chuo.Waliniita pembeni na kunambia.



"Sisi ni askari wa kituo kikuu cha Polisi Arusha.Unahitajika kituo cha Polisi kwa mahojiano kidogo"

"Nimefanya nini jamani ?"

"Utajua hukohuko kituoni !



Askari mmoja alininyanyua kwa nyuma suruali yangu na kupelekwa kituoni.Nilikuwa natembelea vidole sasa.Wanafunzi wenzangu walinionea sana huruma pale chuoni .

Sikujua nimefanya nini?Hawakujua nimefanya nini?



Baada ya kufika kituoni ndipo nilipoambiwa kosa langu.

Eti nilituhumiwa kwa kumuua Mayasa !

Na ujumbe wangu wa vitisho juu yake ulikutwa katika simu yake.Na ulitumika kama ushahidi !

Nilihemewa sana !Nililia sana!

Niliuona mwisho wa ndoto zangu umetimia.Nikajua nitaozea jela.Niliwekwa selo nikisubiri ushahidi ukamilike.



Nikiwa ndani ya selo niliwaza mambo mengi sana.Moja kwa moja nilijua kama kweli Mayasa ameuwawa basi Raiya ndiye mhusika mkuu wa kifo cha Mayasa.Lakini ujumbe ule niliomtumia Mayasa ulikuwa unaniweka mashakani mimi.Nilikuwa ninalia mithili ya kichanga.



Afande aliyekuwa anaitwa John ndiye alipewa jukumu la kupeleleza kesi ya kifo cha mtoto wa Makamu wa Raisi wa Zanzibar, Mayasa.Huku wapelelezi mahiri Tanzania wakiletwa Arusha kufumbua chanzo cha kifo hiki kisichoeleweka.



Afande John alianza kunihoji mimi kwanza.Mtuhumiwa wa kwanza wa mauaji yale.



" Unaitwa nani? "

"Abdul"

"Majina matatu !!"

"Abdul Ramadhani Washiro"

"Kabila"

"Msukuma"

"Nambie uhusiano wako na Mayasa"

"Alikuwa my classmate tu"

"Hamkuwa na uhusiano wa kimapenzi"

"Hapana,alikuwa ni rafiki yangu wa kawaida tu"

"Sasa kwanini uliamua kumuua rafiki yako ?"

"Sijamuua mimi afande"

"Soma huu ujumbe"

"Alinitumia Raiya,Mimi nilimfowadia tu Mayasa."

"Raiya ndio nani ?"



Nilimsimulia afande John kila kitu kuhusu ugomvi wetu mimi na Raiya.Nilirudishwa selo na afande John alikwenda kwa kina Raiya kumuhoji.Hakuwa anapajua ,na wala nilikuwa sipajui.Ila alisema atapajua tu !



Afande john alifanikiwa kufika nyumbani kwa dada yake Raiya.

Baada ya kumuonesha kitambulisho cha Polisi,Raiya alishangaa sana.



"Jamani,Wewe ni askari wa tatu kuja kunihoji leo !"

"Walikuja maaskari wengine hapa ?!"

" Ndio na mmoja katoka nusu saa iliyopita"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Walikuwa na vitambulisho?"

"Ndio walinionesha"

"Unayakumbuka majina yao"

"Nayakumbuka sana kwa kuwa majina yao yanafanana"

"Wanaitwaje?"

"Wote wanaitwa John"

Afande John alisikia kizunguzungu na mivumo isiyoeleweka masikioni mwake.Ilikuwa taarifa ya kushangaza sana !



"Itabidi nikakuhoji kituoni"

Afande John aliona pale siyo mahali salama pa kufanyia mahojiano.



Walifuatana na Raiya kuelekea kituoni....!







Walifuatana na Raiya kuelekea kituoni..!



Hapakuwa na umbali mkubwa sana toka nyumba aliyokuwa anakaa Raiya hadi kituo kikuu cha Polisi Arusha.Raiya alikuwa anakaa katika nyumba ya dada yake aliyokuja kukaa kwa muda mahsusi ili kutekeleza aliyoyakusudia,kutenganisha penzi la Abdul na Mayasa kama akivyoamini yeye kuwa walikuwa wapenzi.



"Raiya hebu nambie vizuri kuhusu hao askari waliokuja kukuhoji kwako."

" Ndiyo kama nilivyokwambia Afande.Walikuja askari wawili kunihoji.Mmoja alikuja asubuhi na mwingine alikuja muda mfupi kabla hujaja wewe.Na wote walitaka maelezo yangu kuhusu kifo cha Mayasa na uhusiano wangu na Mayasa na Abdul."

"Wewe uliwajibu nini?"

"Yule wa kwanza sikumjibu kitu.Maana aliniacha kwenye mstuko mkubwa sana baada ya kunambia Mayasa amefariki.Sikuamini kama Mayasa amefariki..nilikuwa nalia tu kila alichokuwa ananiuliza .Askari yule alifanya kazi ya kunibembeleza tu,akaondoka"

"Askari wa pili je?"

"Yule alinikuta nimetulia sasa.Nilimueleza kila kitu kuhusu ugomvi wetu mimi, Mayasa na Abdul."

"Alisemaje baada ya maelezo yako"

"Aliandika kwenye kitabu chake na kuondoka"

Afande John alishusha pumzi ndefu .Akajua ngoma sasa imekuwa mzito !



Akamfungia Raiya selo na kutoka nje kwenda kutafakari.Alikaa chini ya mwembe mrefu uliokuwepo pale nje ya kituo.Akiwaza na kuwazua.

Simu yake ikawa inaita.Namba ilikuwa ngeni.Zilitokea namba tu.Akaipokea na kuiweka sikioni.

"Hallo"

"Hallo nani mwenzangu?"

"Huna haja ya kulijua jina langu.Cha muhimu acha kuifatilia hiyo kesi utauwawa bure.Unahamu ya kumuweka eda mkeo?"

"Usinitishe kijana"

"Nitakuuwa!"

"Huna jeuri hiyo"

"Unajifanya kiburi"

"Nitawakamata wote wauaji waoga!'

" utaenda kutukamata kuzimu.."



Afande John alihisi amerukiwa na kitu cha maji maji utosini.Aligusa kwa mkono wake wa kulia.Aligusa yale maji.Sauti ya kwenye simu ilianza kucheka.

Ghafla ngozi ya afande John ilianza kuvuka.Afande John alitupa simu chini alisikia maumivu makali sana.Alikufa taratibu. Alikufa kifo sawa na alichokufa Mayasa !

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Sasa ilikuwa mshikemshike.Mauaji ya polisi kuuwawa nje ya kituo.ilizua mambo mengi.Mauaji haya ya pili yaliwafanya Polisi wafikirie nje ya boksi.Watuhumiwa wawili wapo ndani Lakini Afande John kauwawa akiwa nje.Bila shaka na wauaji walewale waliomuuwa Mayasa.



Mauaji ya Mayasa yalilitikisa Jiji la Arusha.Arusha iligeuzwa nje ndani kumtafuta muuaji au wauaji.Hawakupata fununu zozote.Polisi walibaki gizani.Giza totoro !



Mayasa alikuwa Mtoto wa mkubwa Serikalini.Serikali ilituma wapelelezi mahiri watatu.Kuja Arusha kumsaka muuaji !



Walikuja wapelelezi watano.Na kila mmoja alivuliwa ngozi kwa siku yake.Waliuwawa kwa maji yaleyale yaliyomuua Mayasa.



Mmoja alikutwa amekufa hotelini kwake,akiwa amelala.Ngozi ikiwa imejitenga na mwili wake !



Wapili alikutwa amekufa akiwa kwenye gari lake.Aina ileile ya kifo alichouwawa mwenzake.



Wa mwisho aliuwawa mgahawani.Akiwa anakula chakula cha usiku.



Siku tano zilitosha kuwavua ngozi wapelelezi watatu.Waliuwawa kwa maji yaleyale.Yaliyomuua mtoto wa makamu wa raisi.Maji yaleyale yaliyomuua Afande John !



Hali sasa ilitisha !



"Ndani ya selo hali yangu Ilikuwa mbaya sana.Polisi hawakuwa wamenipiga hata kidogo .Lakini nilikuwa nimechoka taabani.Nilichoka kimwili.Nilichoka kimawazo.



Kifo cha Mayasa kiliniumiza sana kichwa.Akilini mwangu nilijua Raiya anahusika kwa asilimia zote.Niliukumbuka sana wema wa Mayasa.Mayasa alikuwa malaika kwangu.Mayasa alikuwa mwanamke mwenye roho ya kipekee sana.Alinisaidia bila ya sharti lolote.Nilimkumbuka kila dakika mule selo.



Sasa nilimchukia sana Raiya.Chuki kwa Raiya ilianza taratibu.Sasa ilikuwa imeota mizizi.Nilimwona ni adui yangu namba moja duniani.Adui kwa kumuua Mayasa. Rafiki mwenye upendo wa kweli kwangu.



Wazazi wangu hawakuwa wanajua kama niko jela.Na wala sikutaka kuwaambia,maana hata ningewaambia isingesaidia lolote, maana hakuna atakayekuja.Wasingekuwa na nauli ya kuja Arusha.Nilikuwa naijua hali ya uchumi ya nyumbani.Niliacha kuwaambia nikihofia kuwapa presha za bure.



Wakati nikiwa nawaza hayo, mlango wa geti ulifunguliwa.Aliingia askari mmoja wa kike. Alikuwa na sura ya huzuni.Alikuja kunipa taarifa mbaya ya kifo. Taarifa ya kifo cha Afande John !



"Inamaana Raiya kamuua na Afande John?"

" Sidhani kama Raiya anahusika.Afande John amefariki wakati Raiya yuko selo"

"Unasema!"

"Ndio hivyo Abdul,hebu tuambie mtu mwengine unayehisi anaweza kuwa nyuma ya mauaji haya Abdul ?"

"Hakuna nilijualo Afande kweli sijui kitu afande"Nilisema huku machozi yananitoka .



Nilirudishwa selo baada ya mahojiano mafupi na askari yule wa kike.



Sasa nikaona uzito na ugumu wa kesi hii iliyokuwa inanikabiri.Nikaamua kuwaeleza wazazi wangu Bagamoyo kwa simu.Sikuwa na jinsi sasa.Nilikuwa nahitaji hekima za wakubwa.Nilikuwa nahitaji sana majaliwa ya Mungu.Kutoka katika mkasa huu mzito...!

***********""*****



Nilikuwa nahitaji sana hekima za wakubwa.Nilikuwa nahitaji sana majaliwa ya Mungu.

Ili kuokoka katika mkasa huu mzito..!



Niliwaomba askari wanipe simu ili niwapigie wazazi wangu.Niwataarifu juu ya kukamatwa kwangu.

Waliniruhusu.



Nilimueleza baba yangu mzazi, Mzee Washiro juu ya kukamatwa kwangu na Polisi na tuhuma za mauaji zinazonikabiri.Alisikitika sana baba.Kwa mara ya kwanza nilimsikia baba akilia.Tena kwenye simu.Nilipatwa na uchungu sana.



Mimi nilikuwa mtoto wake wa kwanza kati ya watoto kumi.Mimi ndiye nilikuwa tumaini hai la familia yangu.Mtoto niliyesoma zaidi ya wote katika familia yangu.



Habari ya kutuhumiwa kwangu kwa kesi ya mauaji,kwa baba ilikuwa mithili ya kuzimika ghafla kwa mshumaa pekee akioutegemea gizani.Pamoja na yote aliniahidi kitu.Aliniahidi lazima aje Arusha punde atakapopata pesa.



Nilijua hatokuja Arusha karibuni.Na pengine hatokuja kabisa.Na naweza kuozea jela Arusha bila kumuona ndugu yangu yeyote.Tulikuwa mafukara sana nyumbani.Lakini kidogo nilipata imani.Kwakuwa nyumbani walikuwa wanafahamu sasa kuwa mtoto wao nipo katika matatizo makubwa ugenini.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Kwa upande wa Polisi wa Arusha Ilikuwa hekaheka ndani ya Jiji.Walitafuta wachuna ngozi wale wasio na huruma bila mafanikio.Walimkamata kila waliyemuhisi,lakini hawakufanikiwa kumkamata muuaji halisi.Ilikuwa kama ametoweka ghafla Arusha.Jiji lilibaki likisubiri Muuaji yule katili ataibukia wapi ?



Baada ya wiki mbili yalitokea mauaji !. Safari hii katika Jiji la Mwanza .







ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog