Search This Blog

Tuesday 1 November 2022

KICHAA WA MTAA - 2

 






Simulizi : Kichaa Wa Mtaa
Sehemu Ya Pili (2)






Kichaa Nyogoso hakujua kama nyuma anafuatwa na mtu, aliendelea kutembea wakati huo Suzani akizidi kukazana mwendo kumfikia. Lakini kabla hajamkaribia, Nyogoso alivuka barabara. Barabara ambayo ilikua ikipitisha magari kwa wingi muda huo kiasi kwamba ilimlazimu Suzani kungojea yapungue ndipo avuke. Jambo hilo lilipotimia, tayari kichaa Nyogoso alikua ameshaishia zake sehemu ambayo Suzani hakuweza kufahamu. Hivyo basi mpango wake ukawa umegonga mwamba. Alilaani sana kitendo hicho, roho ilimuuma sana, alipiga miguu yake chini huku akitazama kila pande. Alitazama kulia na kushoto, mbele na nyuma kisha akajiuliza"Nina mkosi gani mimi?..", alipokwisha kujiuliza swali hilo machozi hayakua mbali kumtoka, punde yakimtiririka. Hiyo yote ikiwa ishara ya kuchukizwa ha kitendo kile cha kumkosa Nyogoso, ni kama alipokonywa tonge ambalo ingali ananjaa kali.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alirudi nyumbani akiwa mnyonge,bado hakuyaamini macho yake kama yalimuona Nyogoso. Usiku wa siku hiyo Suzani hakula chakula wala hakuweza kupata hata lepe la usingizi,nafsi yake ilishiba vile vile maumivu aliyokua akiyapata moyoni mwake yalimpelekea kuupoteza usingizi. Ikiwa sababu ni kichaa Nyogoso. Hali hiyo ya Suzani iliwaweka wazazi wake katika hali ya sintofahamu, ni mara kadhaa walikua wakistaajabishwa na mabadiliko aliyonayo binti yao.

"Unatakiwa ukae na binti yako, muulize kipi kinacho msibu", Mr Mbega, baba yake Suzani aliongea kwa msisitizo akimwambia mkewe. Ulikua usiku wa siku hiyo hiyo ambayo Suzani alisusa kula chakula pasipo kueleza kinacho msibu ilihali haikua kawaida yake. Mama Suzani alipoyasikia maneno hayo, alikunywa bunda moja la maji, akarejesha grasi kwenye meza kisha kajibu "Ni vizuri sana kama na wewe utakua umeliona hili suala, na ukae ukijua hii tabia hajaanza sio leo tu. Sasa basi hofu ondoa, nitakaa naye nimuulize halafu tutajua cha kufanya"

"Hapo nimekuelewa vilivyo", aliunga mkono Mr Mbega huku tabasamu bashasha likionekana usoni mwake wakati huo wakiendelea kula chakula. Walipomaliza kula, mama Suzani alielekea chumbani kwa binti yake. Alipoingia alimkuta Suzani kalala kifudifudi, na ndipo kwa sauti chini alimuita lakini Suzani hakuitika mpaka pale alipoitwa zaidi ya mara nne. Mama Suzani alistaajabu sana, akiwa ndani ya taharuki alisema "Suzi mwanangu! Unanini wewe? Mbona kila kitu unapata? Furahaia maisha binti yangu, kama ni pesa wazazi wako Zipo za kutosha. Haya nataka uniambie kipi kinacho kusumbua", Suzani hakusema neno lolote, alinyamanza kimya. Ila baada dakika kadhaa alimgeukia mama yake, uso wake ulionyesha kuchoshwa na chumvi ya machozi. Kwa sauti kwa sauti ya kilio alisema "Mama, nimekua mtumwa wa mawazo. Kila siku nazorota sababu ya yule mkaka mzoa takataka aliyeniokotea pochi iliyokua na vitu vya thamani,kiukweli kabisa mama kaka yule nilimkosea sana tena zaidi ya sana kumutukana na kumdharau. Sasa nafsi yangu inanisuta, roho nayo inaniuma sana tena zaidi ya sana ", alisema Suzani kwa sauti iliyoambatana na kilio. Mama Suzani aliyafuta machozi ya binti yake wakati huo akimtuliza aache kulia. Alipokatisha kilio ndipo akamwambia " Ni kweli ulifanya kosa kubwa sana mwanangu, nakuasa usije rudia tena kumdharau mtu yoyote hapa ulimwenguni kwa sababu hujui ni nani atakaye kusaidia. Lakini pia kwenye suala hili, shaka ondoa. Nina imani yule kijana tutampata tu, utamuomba radhi. Sawa mwanangu?. "

"Sawa mama", aliitika Suzani huku akiwa na wingi wa tabasamu. Mama yake aliahidi kumsaidia binti yake kumpata Nyogoso,wala hakujua dhamila ya binti yake pindi atakapo kutana na Nyogoso ingawa yeye alijua kuwa Suzani anahitaji kumuomba msamaha na sio kingine. Hatimaye alipata usingizini usiku huo, alilala akiwa na wingi wa tabasamu mwanana.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Siku iliyofuata, asubuhi panapambazuka. Ni asubuhi ambayo ilikua tulivu sana, anga karibia lote la jiji la Dar es salaam lilionekana nyeupe bila kuwa na hata lepe la wingu. Kichaa Nyogoso aliamka kutoka usingizini, kando ya jalala ambapo ndipo yalipo malazi yake. Alijinyoosha kisha akazipiga hatua kuingia jalalani kutafuta makombo yaliyotupwa. Mungu si Athumani, asubuhi hiyo Nyogoso alibahatika kupata mkate. Alifurahi sana, aliimba na kucheza. Lakini wakati yupo kwenye hali hiyo ya furaha, punde aliona chupa ndogo kando yake, jupa ambayo ndani ilikua na maji ya njano. Furaha ilizidi kwa kichaa Nyogoso, alijua fika kuwa maji hayo huwenda ni shurabati (Juice). Aliinama akifungua haraka haraka kisha akanywa.

"Loh! Kumbe mkojo?..", alilaani Nyogoso baada kunywa na kugundua kuwa sio shurabati. Alifadhaika sana moyoni mwake, ghafla akaanza kutapika. Alitapika sana mapaka akajihisi kizunguzungu,ambapo baada dakika kadhaa alianguka chini na hata asiweze kujinyanyua shauri ya kuishiwa nguvu ilihali harufu mbaya ya mkojo ikizidi kutamalaki puani mwake.

Masaa matatu baadaye harufu ile ya mkojo ilitoweka, alionekana kuwa hoi bin'taabani. Mwili wake haukua na nguvu, tumbo lake lilihisi njaa. Alipoutazama mkate wake hakuuona, ulichukuliwa na kichaa mwingine aliyekatiza eneo hilo wakati yeye alipokua kwenye dimbwi zito la usingizi uliompita pindi alipoanguka chini. Nyogoso alisafa, lakini muda mfupi baadaye alitokea mama ntilie. Mama ntilie huyo alionekana kushika ndoo ndogo mkononi, huku kichwani akiwa amebeba sufuria kubwa. Alizipiga hatua kuelekea jalalani, alipofika alitua chini sufuria lake ambalo ndali lilikua na ukoko na makombo mengineyo. Ila kabla hajaumwaga ukoko huo mchanganyiko na makombo, alistuka kumuona kichaa akiwa amelala katika jalala hilo. Mama ntilie huyo alisikitika sana kisha akajisemea "Ni kweli bora ukose mali kuliko kukosa akili, hivi kichaa huyu anaifurahia hii harufu mbaya? Mungu wasaidie watu kama hawa", alimaliza kwa dua mama ntilie kisha akaendela na shughuli iliyomfikisha hapo jalalani. Alipomaliza aliondoka zake ikiwa nyuma akimuacha kichaa Nyogoso akijivuta kwa nguvu za soda kuyakaribia makombo yale yaliyomwagwa na mama ntilie aliyeondoka hivi punde. Alipoyafikia aliyala haraka haraka,aliposhiba alitulia hapo hapo jalalani akingojea nguvu ikusanyike upya ndipo aingie mtaani. Hatimaye hali ikawa nzuri upande wake, alipata nguvu ya kunyanyuka pale jalalani. Alizipiga hatua kuufuata mzigo wake wenye mazagazaga, aliunyanyua akautupia mgongoni kisha akaingia mtaani. Alitembea huku na kule, punde alitoka mtaani sasa akaambaa barabani. Eneo la Kinomdoni studio, alionekana kichaa Nyogoso akitembea huku akiwa na mzigo wake wenye mazagazaga. Lakini wakati anatembea, ghafla ilionekana gari ndogo Rav4 nyeusi. Ndani ya gari hilo alikuwemo Suzani na mama yake,ambapo Suzani alistuka kumuona kwa mara nyingine tena Nyogoso kando. Macho yake hayakutaka kuamini mapema kama kweli aliyemuona ni Nyogoso au amemfananisha, na hivyo haraka sana alimwambia mama yake asimamishe gari. Mama Suzani alifanya alikubali, aliweka kando gari yake kisha akashuka pamoja na na binti yake hali ya kuwa muda huo huo ilionekana gari nyingine aina ya Hilux. Ndani ya gari hilo alikuwemo Mazoea alitaharuki sana kumuona Nyogoso. Hakuweza kuamini kwa haraka, alijua amemfananisha ingawa fikra zake zilimuaminisha kuwa huyo aliyemuona kando ya barabara akitembea ndio Nyogoso mzoa takataka kipenda roho chake. Hima alimwambia mama yake asimamishe gari, naye alifanya hivyo kisha akahoji "Kuna nini Mazoea?.."

"Mama huwezi amini nimemuona mzoa takataka", alijibu Mazoea huku akifungua mlango wa gari haraka haraka. Alitoka ndani gari na kisha kuzipiga hatua kumfuata Nyogoso wakati huo huo mama yake naye akimfuata nyuma kama ilivyo kwa Suzani na mama yake. Hivyo wazazi hao kila mmoja akiwa sambamba na mabinti yake walizipiga hatua kumfuata kichaa Nyogoso pasipo wao kujua kuwa wanamfuata mtu mmoja.



Suzani na mama yake, ndio walikua wa kwanza kumfikia kichaa Nyogoso. Kwa sauti ya mshangao mama Suzani akamuuliza binti yake "Mtu mwenyewe ndio huyu?."

"Ndio mama", Suzani alijibu wakati tayari amemsimamisha Nyogoso. Nyogoso aliishia kuwatazama na hata asijue kinacho endelea.

"Haya basi muombe radhi tuendelee na safari yetu", kwa msisitizo mama Suzani alimsihi binti yake. Suzani aliangua kicheko kisha akasema "Unajua mama, mbali na kumuomba msamaha. Pia huyu ndio anayeutesa moyo wangu"

"Unasemaje?", aling'aka mama Suzani.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Nasema huyu ndio kipenda roho changu, najua huwezi kunielewa kwa sasa", alijibu Suzani. Jibu ambalo lilileta mzozo mfupi wakati huo kichaa Nyogoso aliamua kuondoka zake baada kuona hakuna kipya kwa watu hao. Kichaa huyo alionekana akivuka barabara kuelekea upande wa pili. Haraka sana Suzani alipasa sauti kumuita kwa kutaja jina mzoa takataka. Lakini kwa hali aliyokua nayo Nyogoso, kamwe hakujua kama ni yeye anayeitwa. Kumbukumbu za kuwa aliwahi kufanya kazi ya kuzoa takataka zilimpotea kabisa. Alizidi kutembea kuelekea ng'ambo ya pili,muda huo Suzani akiendelea kupasa sauti yake kumuita. Punde aliguswa bega. Ni Mazoea ndiye aliyemgusa bega. Kwa hasira na ghabu kubwa Mazoea alimuuliza Suzani "Unamtambua vipi yule mkaka"

"Unaniuliza hivyo wewe kama nani?", alijibu Suzani kwa jeuri na nyodo wakati huo wazazi wao wakiwa kando. Jibu hilo lilimchefua Mazoea, punde akazua tafarani. Ugomvi uliibuka ila ugomvi huo ghafla ulitoweka baada kusikika mshindo kutoka barabarani huku zilisikika sauti zikipasa mayowe kwa kusema "Ajari.. Ajari..gari imeuwa", sauti ya kishindo na sauti ya mayowe kwa pamoja ziliwamfanya mabinti hao kugeuka kutazama barabarani. Wote hawakuamini kile walichokiona. Alionekana kichaa Nyogoso akiwa amelala chini, damu zikimvuja mithili ya maji kupitia puani na mdomoni. Kwa sauti iliyoambatana na kilio Mazoea alisema "Mama angalia barabarani mama", alipokwisha kusema hivyo alianguka chini akapoteza fahamu. Kipindi Mazoea amepoteza fahamu, Suzani yeye alikua akilia bila kukoma. Punde si punde alizipiga hatua kuelekea pale alipoangukia kichaa Nyogoso, wala hakutazama usalama wake hapo barabarani. Akili yake yote ilimfikiria Nyogoso,lakini kabla hajamfikia alishikwa mkono na mama yake kisha akarudishwa nyuma akapandishwa ndani ya gari wakaondoka mahali hapo huku nyuma wakimuacha mama Mazoea akijifuta machozi, aliomba msaada kwa watembea kwa miguu ili wamsaidie kumbeba Mazoea wamuingize ndani ya gari. Zoezi hilo lilifanyika haraka sana ila akajikuta akiishi wa nguvu pindi alipotazama kule barabarani alipoangukia kichaa Nyogoso baada kugongwa na gari. Muda huo huo huo Nyogoso alipatiwa msaada, wasamalia wema walimpakia kwenye taksi moja ambayo ilijitolea kutoa msaada. Nyogoso akapelekwa hospital. Pumzi ndefu alishusha mama Mazoea, ndani ya nafsi yake akajisemea "Mungu mjalie uzima kijana huyu ili mwanangu awe na furaha kwenye hii Dunia", kwa huzuni mama Mazoea alijisemea hivyo akianza kwa kushusha pumzi ndefu. Baada ya dakika kadhaa, mama Mazoea alipata ujasiri wa kuliendesha gari lake. Aliendesha kwa kasi kupeleka binti yake hospital lakini kabla hajamfikia, Mazoea alizinduka. Safari ikawa imekomea hapo, na sasa mama huyo aliendesha gari kuelekea nyumbani ilihali kadri muda ulivyozidi kwenda ndivyo kumbukumbu za Mazoea zilivyozidi kurejea kichwani. Hatimaye akili yake ilikaa sawa, alilia sana huku akimtaja Nyogoso kwani aliamini kuwa amefariki Dunia. Kilio cha Mazoea kilimsononosha sana mama yake, naye akajikuta akidondosha chozi la huruma juu ya binti yake aliye ama kwenye penzi nzito la mzoa takataka Nyogoso ambaye kwa wakati huo ni kichaa. Alipofuta chozi lake akajiuliza "Mzoa takataka. Hivi ulimpatia nini binti yangu mpaka ifikie hatua hii ya kushindwa kukusahau?.."

"Ama kweli nimeamini mapenzi ni uchizi, tayari binti yangu amekua kichaa wa mapenzi juu ya mtu", alisema mama Mazoea baada kujiuliza swali pasipo kupata jawabu. Akili yake inawaza mbali sasa, aliwaza mengi sana hasa kama Mazoea atajua Nyogoso kafariki. Hofu ilimjaa na kuamin kuwa siku hiyo hiyo ndio siku ya kumkosa binti yake,alisikitika sana ilihali kwa mara kadhaa akionekana kushusha pumzi na kujisonya. Lakini wakati amekumbwa na wingu nzito la mawazo, alisikia sauti ya Mazoea ikimuuliza juu ya uzima ww kichaa Nyogoso.

"Mama, hivi mzoa takataka atakua amepona kweli?"

"Mazoea, mimi na wewe tupo hapa kwahiyo hakuna anayejua", alijibu mama Mazoea. Jibu hilo lilimfanya Mazoea kuanza upya kaungua kilio chake huku akisema "Nitaishi vipi mimi mama yangu? Nampenda sana mzoa takataka wangu mama. Nampenda Nyogoso wangu mama.", alilia Mazoea.

"Mazoea, nyamanza mwanangu. Ngoja nifuatilie ili nijue hali yake. Sawa mama?.."

Maneno hayo yanampa faraja Mazoea, anakatisha kilio chake. Muda huo huo mama Mazoea anachukua funguo ya gari anaamua kumfuatilia kichaa Nyogoso ili kujua hali yake. Safari yake alianza kuelekea hospital ya muhimbili, alipofika alieleza aina ya mgonjwa jinsi muonekano wake ulivyo lakini akaambiwa kuwa hajapokelewa mgonjwa mwenye muonekano huo na wala hajapokelewa mgonjwa aliyepata ajari. Mama Mazoea alishusha pumzi ndefu, kijasho kilimtoka polepole. Hofu ilimjaa kwani aliamini uwepo wa kijana Nyogoso ndio uzima wa binti yake, mtoto pekee aliyemzaa kwa tabu sana akifanyiwa upasuaji.

"Hapana sikubali kumpoteza mwanangu, nitamtafuta kijana huyu popote pale alipo. Eeh Mungu nijalie nimpate akiwa mzima", alijisemea mama Mazoea wakati huo akiliwasha gari lake. Sasa aliamua kutembelea kila hospital aliyoifahamu ndani ya jiji la Dar es salaam kwa dhumuni la kumtafuta kichaa Nyogoso aliyeumbwa na janga la kugongwa na gari pindi alipokua akivuka barabara kuelekea ng'ambo ya pili.

Wakati mama Mazoea akiendelea kuhaha kumsaka kichaa Nyogoso, upande mwingine nako binti yake alijihisi mjamzito. Kila dalili ya mimba siku hiyo zilijizihilisha, ilihali tumbo lake nalo likionekana kuwa kubwa kidogo kuonyesha kuwa mimba hiyo inamiezi isiyopungua mitatu ingawaje muda wote yeye mwenye mama Mazoea hakutambua kuwa binti yake ni mjamzito. Mazoea alifurahi sana moyoni mwake, akajisemea "Maisha yangu yatakua ya furaha sana, natumai mwanangu nitakaye mzaa ndio atakua faraja yangu na kumbukumbu ya mpenzi wangu mzoa takataka Nyogoso", aliwaza Mazoea, jambo hilo lilimpelekea kuachia tabasamu pana. Punde tabasamu hilo lilipotea baada kuzinduka kutoka usingizini, ilikua ndoto. Ndoto ambayo aliota kwamba amenasa mimba ya Nyogoso,alisikitika sana Mazoea. Akajikuta akilaani ndoto hiyo ya mchana ilihali kwingeneko mama yake aliwasili hospital ya Mwananyamala. Mama Mazoea akiwa na hofu alieleza namna mgonjwa wake alivyo, wahusika walikubali kuletewa mgonjwa huyo lakini walimpa taarifa iliyomstua sana mpaka kupeleka mama mama Mazoea kudondosha machozi na hata asiamini kile alichokisikia..

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/





" Pole mama,hari ya mgonjwa ipo mahututi sana. Naweza kusema sio wa leo wala wa kesho "

"Mungu wangu", alitaharuki mama Mazoea. Ni taarifa ambayo ilimshtua sana, akajikuta akipigwa na butwa.

"Huna haja ya kuwaza sana, kinacho takiwa hapa wewe toa dau linalo eleweka ili mimi sisi tuanze haraka sana jitihada za kumuhudumia mgonjwa wako, kwa sababu ukungojea ifike zamu yake basi tambua utamkosa", aliongea daktari akihitaji rushwa kutoka kwa mama Mazoea. Suala la pesa upande wa mama Mazoea halikua jambo la kutatiza, kwa sauti ya kujiamini kabisa alimuuliza Daktari huyo kiasi cha pesa anacho hitaji kwani naye alijua fika Daktari huyo kipi anahitaji.

"Kiasi gani nikupatie, niambie nipo tayari kukupa ilimradi kijana wangu apone kwa haraka iwezekanavyo"

"Sawa laki sita zipo?..", akionekana kuwa na wingi wa wasi wasi, Daktari huyo alitaja kiasi hicho cha fedha. Ni pesa ambayo haikuweza kumstua mama Mazoea, alishusha pumzi ndefu kisha akamwambia "Ipo hiyo fedha, tena nitakuongeza laki mbili. Jumla itakua laki nane". Daktari huyo aliyefahamika kwa jina Luanda alijikuta kuwa na furaha baada kuyasikia maneno hayo ya mama Mazoea, haraka sana walikubalina mahali pakukutana ili wakamlishe kile walicho kubaliana. Luanda alisema "Ngoja nikupe siri moja ambayo huifahamu, wagonjwa wengi wanakufa kwa kukosa matibabu ya papo kwa hapo kwa sababu ya pesa. Maisha yamebadilika sana mama, kwa hiyo usitegemee mgonjwa wako atatibiwa wakati kuna mtu kaja anataka kukupa kiasi kikubwa cha pesa ili umuhudumie mgonjwa wake. Vile vile tukiachana na hayo. Ammh,nadhani unatambua kwamba hili jambo ni adui mkubwa wa maendeleo na kila siku serikali yetu inapiga vikari suala la rushwa. Kwa maana hiyo basi haipendezi kunipa pesa hiyo hapa kazini ila nakuomba vuta subira mgonjwa wako afanyiwe uchunguzi kisha utaambiwa ghalama zote za dawa na matibabu utalipia halafu hiyo laki nane sasa, nitakupigia simu nikwambie tukutane sehemu fulani unipatie "

" Sawa hakuna tatizo Dokta, jitahidi sana umrejeshe kwenye hali yake ", aliongea kwa kusikitika mama Mazoea. Daktari Luanda alimtia moyo kisha wakawa wameagana. Mama alionekana akizipiga hatua kuelekea mahali lilipo gari lake, alipolifikia alifungua mlango akaliwasha akaondoka zake pale Mwananyamala hospital. Furaha ilimpotea mama huyo, moyoni aliamini kuwa endapo kama ikitokea Nyogoso kaaga Dunia basi huwenda ikimpelekea kumkosa na binti yake kipenzi. Hivyo mama Mazoea ilimlazimu kumuombea dua kichaa Nyogoso ili arudi kwenye hali yake.

Hatimaye alifika nyumbani kwake, alipokelewa na binti yake kwa taba bashasha. Walipofika sebuleni, mama Mazoea alijitupa kwenye sofa huku akifuatia na kushusha pumzi ndefu jambo ambalo lilimchanganya Mazoea kuingiwa na hofu juu yake, ndipo kwa sauti ya chini iliyojaa taharuki ndani yake akamuuliza mama yake kuhusu Nyogoso.

"Mazoea mwanangu yani hata sijapumzika unaanza kuniuliza maswali?.", aling'aka mama Mazoea. Naye aligundua kuwa amemuudhi mama yake, haraka sana alimuomba msamaha. Mama yake hakusita kumsamehe ambapo baada ya msamaha akamuuliza "Umeshakula?.."

"Ndio nimekula.. Ammh labda wewe huko ulikotoka umekula umekula kweli?..", alijibu Mazoea na kisha kuacha swali kwa mama yake. Maneno hayo aliyaongea kwa sauti ya kudeka, akidiliki kudeka kwa mama yake.

"Hapana sijala, na wala sina hamu ya kula mwanangu", alijibu mama Mazoea huku akiwa ameshika tama.

"Kwanini mama?.", alistuka Mazoea.

"We acha tu"

"Hapana mama, mimi ndio mwanao pekee, kwahiyo hutakiwi kunificha mama"

"Ni kweli Mazoea lakini...", kabla mama Mazoea hajaendelea kuongea, alishusha pumzi kwanza kisha akaendelea kusema "Nimefika hospital kumfuatilia mzoa takataka wako, japo nimehangaika huku na kule lakini mwishowe nilimpa hospital ya Mwananyamala. Nimeonana na Daktari mkubwa tu wa pale hospital akaniambia hali ya mgonjwa wangu ni mbaya sana", alisema mama Mazoea kwa sauti ya majonzi. Mazoea alistuka sana kusikia taarifa hiyo lakini kabla hajaongeza chochote mama yake akaongeza kusema "Usiwe na hofu, tulia nitamwambia zaidi na zaidi ila nenda kwanza kamwambie Madenge anioshee gari pia ayamwgilie maua maji", haraka sana Mazoea alinyanyuka akaelekea nje kumwambia Madenge kile alichoambiwa na mama yake. Madenge ni mlinzi aliyechukua nafasi ya Jerome aliyefukuzwa kazi hapo awali. Hakika alikua na shauku kubwa ya kutaka kujua hali aliyonayo Nyogoso, hivyo alipokwisha kufikisha maagizo ya mama yake alirejea ndani ambapo ndipo mama yake kwa sauti ya upole alimueleza namna hali ilivyokua.

"Ila licha ya hari yake kuwa mbaya, lakini nimeweza kumshawishi Dokta mkuu aweze kupambania uhai wa mpenzi wako. Kwa uwezo wa Mungu na nguvu ya pesa zangu, tegemea mzoa takataka wako hali yake itatengemaa" , alisema mama Mazoea akimuasa binti yake. Mazoea alifurahi sana kusikia maneno hayo, machozi ya furaha yalimtoka huku akizidi kumuomba mama yake amsaidie.

"Usijali nipo mama yako, na sasa nenda chumbani kapumzike, kitakacho endelea nitakujuaza". Mazoea alinyanyuka kutoka kwenye sofa akaelekea chumbani kwake huku akijifuta machozi ya furaha yaliyokua yakimtiririka. Hakika ilikua habari njema kwa upande wake,wakati huo huo upande wa pili mama Suzani alionekana akimfokea binti yake. Alisema "Suzani, unamatatizo gani mpumbafu mkubwa wewe. Ulisema ukimuona utamuomba msamaha kwa kosa ulilomfanyia, sasa inakuwaje unaniambia kwamba umempenda? Hivi wewe kweli wa kumpenda mzoa takataka? Yule si nusu kichaa? Mbona unataka kunidhalilisha kenge wewe", aliwaka mama Suzani. Maneno hayo aliyaongea kwa hasira kali na ghadhabu ya hali ya juu. Lakini wakati mama huyo anayaongea maneno hayo, Suzani alikua kimya. Akili yake yote ikimfikiria mzoa takataka Nyogoso huku akiwa na sinto juu ya kile kilicho mpata. Suzani alipoa sana, punde si punde chozi lilimtiririka. Kitendo hicho kilimfanya mama yake kuzidi kukereka ambapo kwa sauti kali aliongeza kusema "Suzi, ukae ukijua sipo tayari kupoteza pesa zangu kukusomesha shule za ghalama ikiwa wewe huna mpango wa kusoma. Hivyo basi nahitaji jibu kutoka kwako. Unahitaji kusoma au hutaki"., swali hilo Suzani hakulijibu, aliendelea kukaa kimya. Mama yake alipoona binti yake hayupo naye hapo kimawazo, alimpiga kofi kuashiria kuwa hayupo tayari kuona binti yake akizama kwenye penzi la mzoa takataka Nyogoso ambaye kwa wakati huo ni mwendawazimu. Suzani aliangua kilio, kwa hasira haraka akanyanyuka kutoka kitandani chumbani kwake. Akaelekea jikoni, punde alitoka huko akiwa na kisu mkononi wakati huo huo akakutana na mama yake. Alikigeuza kisu kukielekeza kwenye tumbo lake, kwa sauti ya kilio akasema "Kwanini unaingilia hisia zangu mama? Tambua unapo fanya hivi unaukosea moyo wangu. Unaumia sana. Kosa langu ni nini hasa? Mimi kumpenda mzoa takataka? Kwani yeye sio mwanaume? Hafai kupendwa? Moyo haona macho lakini umetokea kumuona yeye. Mzoa takataka ndio furaha ya moyo wangu. Sasa najiuwa ili niyaepuke maumivu haya ", wakati Suzani anaongea maneno hayo kwa kilio, mama yake alikua amesimama mbele yake wala hata asiamini kama kweli mapenzi yangeliweza kumfanya mwanae akawa kichaa namna hiyo. Kijasho kilimtoka, akamuuliza" Suzi? Kweli unataka kujiuwa?.. "

" Ndio mama, kamwe siwezi kuvumilia maumivu ninayo yapata. Najiuwa mimi ", alijibu Suzani na kisha kujichoma kisu. Mama Sizani alipagawa, alipiga mayowe kumlilia binti yake wakati huo damu mithili ya maji zikimwagika kunako tumbo lake. Haraka sana mama Suzani alimuita mfanyakazi wake, kwa pamoja walishirikina kumbeba Suzani na kumuingiza ndani ya gari kisha safari ya kuelekea hospital ikaanza. Suzani alipelekwa hospital ya Mwananyamala, hospital ambayo amelazwa kichaa Nyogoso ambaye alikua akiendelea kupata matibabu chini ya uangalizi wa Dokta Luanda. Dokta mpenda rushwa.



Wodi aliyolazwa Suzani haikua mbali na wodi aliyolazwa kichaa Nyogoso, punde harakati za kumtibu Suzani ziliendelea kuokoa uhai wake wakati huo upande mwingine alionekana mama Mazoea akiwa ameketi kwenye sofa huku akiwa na wingi wa mawazo,na kila mara akishusha pumzi ndefu. Mama Mazoea aliwaza sana, alishindwa kuelewa ni kipi hasa kilichomvutia binti yake kwa Nyogoso kiasi kwamba ampende kwa dhati kuliko hata uhai wake. Lakini licha ya kuwaza sana, ila bado jibu alilotegemea lilimpiga chenga,ambapo alijikuta akishikwa na hasira. Kwa jazba alinyanyuka kutoka kwenye sofa akaingia chumbani. Akajitupa kitandani huku akionekana kuchoka sana. Kichwa chake kikiwa bado na kiza kinene kuhusu binti yake, hatimaye polepole usingizi ulimnyemelea. Haikuchukua muda mrefu akasinzia. Alilala fo fo fo, usingizi huo wa saa ya jioni ulimnogea vilivyo mama Mazoea hasa ukilinganisha dimbwi la mawazo lililokua limetwama kichwani mwake. Hali hiyo ilimpelekea kuota ndoto kadhaa wa kadhaa, lakini wakati yupo katika dangulo la njozi, ghafla simu yake ya mkononi iliita. Mama Mazoea akakurupuka kutoka usingizini, macho yake yakuwa bado na mawenge alinyanyuka akaupeleka mkono wake juu kwenye meza akaichukua simu akatazama jina la aliyempigia. Ilikua namba mpya,haraka sana akabofya kitufe cha kijani kisha akaweka simu skioni.

"Habari yako mama, ni mimi hapa Dokta Luanda. Ukowapi ili tukubidhiane makubaliano yetu", ilisikika ikisema hivyo sauti hiyo. Ilikua sauti ya Dokta Luanda. Jioni hiyo alipiga simu ili afanikishe kile walichokubaliana na mama Mazoea. Kwa sauti nzito, sauti ya mtu aliyetoka usingizini. Mama Mazoea akamuuliza Dokta Luanda. "Mimi nipo nyumbani kwangu, nikukute wapi? Na vipi kuhusu hali ya mgonjwa wangu?.."

"Hali yake sio mbaya kama awali, kwahiyo kuhusu hilo nikutake kabisa ondoa shaka. Lakini pia sehemu salama njoo Sophie Hotel", alijibu Luanda.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sawa naomba dakika kumi na tano nitakua nimewasili mahali hapo"

"Sawa", Wawili hao walipokwisha kukubaliana, mama Mazoea akakata simu kisha akavua nguo alizokua amevaa, akavaa taulo yake iliyoanzia kifuani mpaka kwenye magoti akaelekea bafuni kuoga ambapo huko hakuchukua muda mrefu akarejea chumbani akajiandaa haraka haraka kwa kupendeza nguo nzuri huku akinukia marashi. Punde safari ya kuelekea Sophie Hotel kwa niaba ya kuonana na Dokta Luanda ikaanza, lakini kabla hajaingia ndani ya gari alirudi ndani. Akaelekea chumbani kwa binti yake ili amuage. Alipokifikia chumba cha Mazoea, alibisha hodi ila Mazoea hakuitika. Alirudia tena na tena ila bado mambo yakawa yale yale ambapo mara ya mwisho alinyonga kitasa, mlango ukafunguka. Alimkuta binti yake amelala chali miguu ikining'inia upande wa kupandia kwenye kitanda wakati huo kichwa akikilaza kuelekea ukutani. Mama Mazoea alitikisa kichwa kwanza kisha akapasa sauti kumuita "Mazoea.. Mazoea.. Mazoea", aliita mama huyo huku akimtikisa. Punde si punde Mazoea alistuka kutoka usingizini, alinyanyuka kisha akaketi ilihali mkono wake wa kulia ukiyafikinya macho yake akiyaweka sawa ili amtazame vizuri mama yake.

"Unalala kama pono?.", alitania mama huyo. Mazoea aliachia tabasamu kisha akasema "Haya bwana mama"

"Punguza kulala. Haya nimekuja kukuaga. Narudi Hospital kumjulia hali mzoa takataka,kwahiyo baba yako akirudi akikuuliza nimekwenda wapi mwambie nimekwenda kumuona mama Zawadi anaumwa. Hili suala lazima liwe siri, sawa sawa?.."

"Sawa mama, nakutakia safari njema ila usisahau"

"Nisisahau nini?."

"Jamani mama hujui?.."

"Ndio, sasa ningekua najua ningekuuliza?.."

"Anhaa. Usisahau kuniletea matunda", aliongea Mazoea kwa tabasamu bashasha.

"Mmmh kumbe? Sasa ulivyokua unanizungusha? Haya mwanangu wala usijali. Lakini sitaki uendelee kulala, amka ukaoge utalalaje muda wote kama unamimba changa?..", alitania mama Mazoea. Mazoea aliangua kicheko akionekana kufurahishwa na utani wa mama yake. Punde Mazoea alishuka kitandani akaongozana na mama yake mpaka kwenye gari, aliingia ndani mlinzi Madenge akafungua geti. Mama huyo akaondoka zake huku Mazoea akimpungia mkono wa kwaheri ilihali akiwa na wingi wa tabasamu usoni mwake akiamini kuwa mama yake hatomungusha kuhusu penzi lake na mzoa takataka. Macho yake bado yalilikodolea gari la mama yake mpaka pale mlinzi alipofunga geti. "Mazoea, mrembo chuchu konzi. Hakika Mungu fundi amekuumba akiwa hana haraka", Mazoea alipokua akirudi ndani, nyuma yake alisikia sauti ya Madenge akimwambia maneno hayo. Alipoyasika hayo maneno aligeuka, akamtazama akacheka kisha akiendelea na safari yake.

"Kweli nimeamini huli jiji la Dar es salaam linamabinti wazuri sana. Mfano narudi kijijini kwetu na mrembo kama huyu, sinitarogwa!?. Na nafikiri watakao niroga ni wale mabinti wenye miguu iliyopauka kama miwa. Yule muhenga aliyesema tembea uone,wala hakukosea kwa sababu leo ndio naona maana harisi ya msemo huo. Laah! Hakika hii ndio Dar es salaam,warembo kama hawa wa jiji hili ukiwakuta kijijini basi yupo kwa bahati mbaya ", aliendelea kuongeza mlinzi Madenge, uzuri wa Mazoea ulimpagawisha sana.

Upande mwingine, mama Mazoea aliegesha gari lake kando ya barabara kisha akaelekea bank iliyokua hatua chache kutoka mahali alipoegesha gari. Alipokamilisha hitaji lake alirejea ndani ya gari lake akazungusha funguo, gari likawaka. Kwa kasi ya alielekea Sophie Hotel ambapo huko alimkuta Dokta Luanda akimsubiri. "Pole sana kwa kuvuta subira", aliongea mama Mazoea wakati huo akiwa ameshatelemka kwenye gari. Luanda alicheka kidogo kisha akajibu "Wala usijali, najua adha ya foleni ndani ya jiji hili. Imepelekea kuchelewa. Lakini pia wahenga walishasema. Subira yavuta heri, kweli hatimaye heri imewadia"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Haswaa. Eenhe kwahiyo tuingie ndani tupate japo kinywaji au unasemaje?.."

"Hapana, inatakiwa niende kupumzika ili kesho niwahi kwenye majukumu yangu",alikataa Dokta Luanda kuingia ndani. Baada kukacha suala hilo, mama Mazoea alifungua mkoba wake, akatoa bahasha ya kaki iliyokua imetuna akamkabidhi Luanda. Luanda aliachia tabasamu bashasha huku akiipokea bahasha hiyo wakati huo huo mama Mazoea akasema. "Dokta, usiwe na wasi wasi. Ingia ndani ya gari lako, haina haja ya kuhesabu. Siwezi kukufanyia uhuni mimi. Sina njaa hiyo"

"Anhaa sawa ahsante sana. Pia napenda kukuhakikishia kwamba kazi yako nitaifanya ipasavyo"

"Nakutegemea sana"

"Hofu ondoa kabisa, vile vile kesho saa nne asubuhi njoo umjulie hali mgonjwa wako"

"Sawa kwaheri nakutakia majukumu mema". Wawili hao baada kukamilisha mipango yao kila mmoja aliingia kwenye gari lake wakaondoka mahali hapo. Sophie Hotel.



*************





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog